Na Mary Gwera, Mahakama
Mahakama ya Tanzania
inaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha kuwa inatekeleza ipasavyo
jukumu lake la msingi la utoaji haki sambamba na kufikia kwa vitendo Dira yake
ya Utoaji Haki Sawa kwa wote na kwa wakati.
Jitihada hizi zinadhihirishwa
na kasi ya uondoshaji wa mashauri katika ngazi mbalimbali za Mahakama nchini ikiwemo Divisheni za Mahakama Kuu ya
Tanzania mojawapo ikiwa ni Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi.
Katika kikao cha Watumishi wa
Divisheni hiyo kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa Shule ya Sheria ‘Law
School’ jijini Dar es Salaam, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi,
Mhe. Agnes Mgeyekwa amewapongeza watumishi wa Divisheni hiyo kwa kufanya kazi
kwa bidii na ushirikiano ulioiwezesha Mahakama hiyo kuondosha jumla ya mashauri
2249 kwa kipindi cha mwezi Februari 2022 hadi Oktoba mwaka huu.
Akizungumza na Watumishi wa
Divisheni hiyo, Mhe. Mgeyekwa alisema kuwa idadi hiyo inajumuisha jumla ya
mashauri ya mlundikano 167 yaliyovuka mwaka 2021.
“Kila mtumishi amekuwa na
mchango mkubwa sana kwa sababu kazi ya kuondosha mashauri sio kwa Majaji peke
yao, bali kila mtumishi. Hivyo, pongezi za takwimu nzuri za uondoshaji mashauri
zinakwenda kwa kila mtumishi wa Divisheni hii,’ alisema.
Anaeleza kuwa, katika kipindi
hicho cha Februari hadi Oktoba mwaka huu mashauri yaliyofunguliwa yalikuwa 1684,
yaliyoamuliwa 2249 na yanayoendelea (pending) ni 1014.
Aidha; Mhe. Mgeyekwa anabainisha
kuwa, hadi kufikia tarehe 04 Novemba, 2022 mashauri ya mlundikano yaliyosalia
katika Divisheni hiyo ni 46 pekee huku 12 kati ya hayo yapo nje ya uwezo wa
Mahakama hiyo kwa sababu kuna mashauri ya rufaa yanaendelea Mahakama ya Rufani na sababu nyingine ni kutolewa
kwa amri za kutoendelea kuyasikiliza kutoka Mahakama ya Rufani. Ameongeza kuwa,
“mkakati uliopo ni kumaliza mashauri 34 kabla ya mwisho wa mwaka huu.”
Jaji Mfawidhi huyo anaongeza kwamba, Divisheni
ya Ardhi imefanya jitihada mbalimbali zenye lengo la kuondosha mashauri
mojawapo ikiwa ni pamoja na kutumia vikao maalum vya kuendesha mashauri ‘sessions’
ambapo mashauri 59 yalipangiwa mbele ya Majaji watano (5) kutoka nje ya Kituo,
kati ya hayo mashauri 51 yalimalizika, saba (7) yanaendelea kusikilizwa na
shauri moja (1) linasubiri hukumu.
“Divisheni imeweka kipaumbele cha
kibajeti kwenye kuondosha mashauri hasa ya mlundikano ili kufikia malengo iliyojiwekea
ambapo walilazimika kualika Majaji na Naibu Wasajili kutoka vituo vingine ili kuongeza
nguvu zaidi ya kuondosha mashauri hayo,” anasisitiza Jaji Mfawidhi.
“Mbinu hii yenye matokeo
chanya huongeza matumizi ya bajeti, kwa kuwa mashauri ndiyo jukumu la msingi la
Mahakama, Menejimenti imeona ni busara kujikita kwenye matumizi hayo, ambapo tulialika
Majaji na Naibu Wasajili walioendesha vikao vya Mahakama ‘session’ na
kuiwezesha Divisheni kung’ara na hivyo watumishi wote mnastahili kujipongeza na
kuona fahari,” alisisitiza Mhe. Mgeyekwa.
Katika kikao hicho kilichohudhuriwa
na Majaji na Watumishi wote wa Divisheni hiyo, mada mbalimbali ziliwasilishwa
ikiwemo Mpango Mkakati wa Mahakama wa 2020/2021 hadi 2024/2025. Katika mada hii
watumishi watatu (3) wa Divisheni hii Bw. Ukani, Mlinzi, Bi. Carolina Mambo, Msaidizi wa Kumbukumbu na Bi. Radhia Mpinga, Mwandishi Mwendesha Ofisi walifanya mawasilisho kwa umahiri mkubwa na kuonesha namna ambavyo Mpango
Mkakati umeeleweka kwa watumishi wa kada zote.
Aidha, Mtaalam Mwezeshaji wa
mada hii alikuwa Bw. Kisingi Mhando, Mchumi kutoka Makao Makuu ya Mahakama
ambaye alitoa ufafanuzi wa kina kuhusu vipengele muhimu vya Mpango Mkakati huo na
hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wake.
Mada nyingine iliyowasilishwa na
Mwezeshaji, Bi. Betty Jones almaarufu kama ‘BJ’ ilihusu Mbinu za Kukabiliana na
Msongo wa Mawazo (Stress Management) katika maisha ya kila siku nje na mahali
pa kazi ili kuwajengea watumishi uwezo na mbinu za kumudu msongo ‘stress’ na
kutimiza malengo ya Taasisi.
Kadhalika, Mada nyingine
iliyowasilishwa ilihusu Mpango wa Bajeti ya Divisheni, Usimamizi na Matumizi
yake kwa Mwaka 2022/23 iliwasilishwa na Bw. Peter Mbaguli, Afisa Tawala
akishirikiana na Bibi. Hawa Wanguvu, Afisa Hesabu Mwandamizi.
Katika majadiliano ya pamoja
watumishi walitoa hoja zilizolenga kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa
kuongeza idadi ya watumishi, vitendea kazi, vikao vya watumishi wote pamoja na kuboresha
masilahi ya watumishi ili kuwapunguzia ukali wa maisha.
Katika ufafanuzi wa hoja hizo,
Mtendaji wa Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi, Bw. Anatory Kagaruki alisema kuwa
masuala yote yanazingatiwa kikamilifu huku na kuongeza kuwa, uwezo na mipango
ya kibajeti katika ngazi ya Taasisi na Divisheni ndiyo unaotoa dira ya namna ya
kutimiza mahitaji hayo. Alifafanua kuwa ipo mipango na mikakati ya
kimenejimenti ya ndani ya Divisheni na ile ya kitaasisi ya kuboresha mazingira
ya kazi. Alitoa mfano wa Programu ya Kuboresha Maslahi ya Watumishi wa Mahakama
inayotekelezwa na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Mtendaji
Mkuu.
Pamoja na kuwapongeza watumishi
kwa kuchapa kazi kwa bidii, Bw. Kagaruki pia aliwasihi watumishi hao kuendelea kuwa
wavumilivu, kufanya kazi kwa juhudi na maarifa ili kutoa huduma kwa kiwango
kinachotarajiwa na wananchi, Serikali na Viongozi wa Mahakama.
"Nichukue nafasi hii kuwapongeza Watumishi wenzangu kwa kuchapa kazi, hata hivyo tusisahau vipaumbele vyetu ambavyo ni kuendelea na matumizi ya TEHAMA, kuimarisha ushirikiano na wadau na nidhamu kwa watumishi," alisema Bw. Kagaruki.
Kikao hicho kilichosheheni
matukio mbalimbali kilihitimishwa kwa kuwapongeza na kuwakaribisha Majaji
wageni walioteuliwa Mwezi Agosti 2022 na kupangiwa Divisheni ya Ardhi. Katika
tukio, Jaji mpya wa Divisheni hiyo, Mhe. Kevin Mhina alizungumza kwa niaba ya Jaji
mwenzake Mhe. Jaji Hemed Lusungu kuwa wanaahidi kufanya kazi kwa ushirikiano na
kuahidi kwamba wanaungana na Timu ya Divisheni ya Ardhi kutimiza malengo
yaliyopo.
Zoezi lingine lililofanyika lilikuwa ni la utoaji wa zawadi kwa mfanyakazi bora wa Divisheni hiyo Bw. Nkotya Muro, Mlinzi ambaye alipongezwa na Jaji Mfawidhi kwa kuchaguliwa na wafanyakazi na kuwasihi watumishi wengine hasa vijana kuiga mfano huo.
Akitoa neno la kufunga kikao kwa niaba ya Jaji Mfawidhi, Jaji wa Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi, Mhe. Isaya Arufani alipongeza uongozi wa Divisheni hiyo kwa kuandaa kikao hicho na matukio yote ambayo yamewaunganisha pamoja. Akiongeza kwamba, tukio hilo limesisimua ari na morali ya watumishi wote na kwamba ufanisi na tija ya kazi itaongezeka maradufu.
Watumishi walionesha kufurahishwa na kikao hicho na kushauri vikao na matukio ya aina hiyo yafanyike mara kwa mara kwa sababu
yanaimarisha umoja na upendo miongoni mwa watumishi. Mtumishi mmoja alisema
kuwa kukaa pamoja na Majaji ambao ni viongozi adimu kukutana nao tena nje ya
mazingira ya ofisi ni suala la kupongeza na kuendelezwa kwa kuwa inafanya watumishi
kuwafahamu zaidi viongozi wao na hata kujifunza mambo mengi kutoka kwao.
Katika kuhakikisha kwamba,
azma ya Mahakama ya kuongeza kasi ya usikilizaji wa Mashauri na kuondoa
mlundikano, Mahakama iliweka idadi ya mashauri yanayopaswa kumalizwa na Maafisa
wa Mahakama (Majaji na Mahakimu) ambapo Hakimu wa Mahakama za Mwanzo anapaswa
kumaliza mashauri 260 kwa mwaka, mashauri 250 kwa Mahakama za Hakimu Mkazi na mashauri
220 kwa ngazi ya Mahakama Kuu.
Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Benhajj Masoud (aliyesimama) akizungumza jambo wakati wa kikao cha Watumishi wa Divisheni hiyo. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Agnes Mgeyekwa.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Bw. Anatory Kagaruki akijibu hoja mbalimbali zilizoibuliwa katika kikao cha Watumishi wa Divisheni hiyo kilichofanyika hivi karibuni. Kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Crisencia Kisongo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni