· Yumo pia Mkuu wa Wilaya ya Kwimba
Na Lydia Churi-Tume ya Utumishi wa Mahakama, Magu Mwanza
Mkuu wa Wilaya ya Magu na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili
ya Maafisa Mahakama wilayani humo Mhe. Joshua Nassari ameahidi kuwaelimisha wananchi
kuhusu uwepo wa Kamati hizo ili waweze kuzitumia katika kuwasilisha malalamiko
yao yanayohusu ukiukwaji wa Maadili kwa Mahakimu.
Akizungumza wakati wa Utoaji wa Elimu kuhusu uwepo wa
Kamati hizo inayotolewa na Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama jana
wilayani Magu, Mkuu huyo wa wilaya pia amewashauri wakuu wa wilaya wengine
kufanya hivyo ili kuziimarisha Kamati hizo na kuwasaidia wananchi kupata haki.
’’Sisi Wakuu wa wilaya ndiyo Wenyeviti wa Kamati za
Maadili na kwa kuwa kazi zetu nyingi zinatukutanisha na wananchi, nitatumia nafasi hizo kuwaelimisha wananchi wetu ili wafahamu juu ya uwepo wa kamati hizi
na kuzitumia” , alisema.
Alisema ushirikiano kati ya Wajumbe wa Kamati hizo
utasaidia na kuziwezesha kutekeleza jukumu lake la kusimamia Maadili ya Maafisa
Mahakama kwa urahisi na kwa ufanisi.
Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Kwimba Mhe. Ng’wilabuzu
Ludigija amesema Kamati ya
Maadili wilayani Kwimba imekuwa ikishirikiana na Mahakama kwa karibu na hivyo
kupunguza mashauri ya kinidhamu.
Hata hivyo ameishauri Mahakama ya Tanzania kuwakumbusha Watumishi
wasio Maafisa Mahakama kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia weledi na kutoingilia
kazi za Mahakimu. Alisema wakati mwingine makosa ya ukiukwaji wa maadili
hufanywa na watumishi hao na lawama kuelekezwa kwa Mahakimu na hivyo kuchafua
taswira ya Mhimili wa Mahakama.
Kuhusu Elimu kwa wajumbe wa Kamati za Maadili, Mkuu huyo
wa wilaya ameishauri Tume kutenga fedha kwa ajili ya Watumishi wa Sekretariet ya Tume kupita kwenye maeneo mbalimbali nchini na kutoa elimu kwa kuwa wajumbe wa
Kamati hizo wamekua wakibadilika mara kwa mara.
Naye Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama
(Maadili na Nidhamu) Bi. Alesia Mbuya alisema Tume imeandaa Kanuni na Miongozo ya Uendeshaji wa Kamati hizo kwa
lengo la kuwarahisishia wajumbe wa Kamati kutekeleza jukumu lao la usimamizi wa
Maadili.
Watumishi wa Sekratariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama
wanaendelea na kazi ya utoaji wa Elimu kwa Kamati za Maadili ya Maafisa
Mahakama za Mikoa na Wilaya katika mikoa ya Mwanza na Mara pamoja na wilaya
zake.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni