- Majaji na Mahakimu Wanawake Afrika wakubaliana kusimamia haki za kijinsia
Na Mary Gwera, Mahakama ya Tanzania, Accra-Ghana
Chama cha Majaji Wanawake Duniani (IAWJ) Ukanda wa Afrika kimehitimisha Mkutano wake huku kikitoka na maazimio kadhaa ikiwemo kuwataka Wanachama kutoka Ukanda huo kuhakikisha kuwa Sheria, Kanuni na desturi ndani za nchi zao zinawiana na Haki za Binadamu na dhamana za kikatiba.
Akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 18 wa Chama cha Majaji Wanawake Duniani (IAWJ) Ukanda wa Afrika katika Hoteli ya Labadi jijini Accra nchini Ghana, Rais wa Chama hicho tawi la Ghana, Mhe. Rita Agyeman-Budu aliwasisitiza washiriki wa mkutano huo kutekeleza yote waliyojadiliana na kukubaliana.
“Nachukua fursa hii kuwapongeza washiriki wote mliohudhuria katika mkutano huu, hivyo nawaomba tuungane sote kwa pamoja kuvunja tamaduni hasi na za kibaguzi ambazo zinasababisha ukiukwaji wa haki za binadamu,” alisema Mhe. Rita.
Mkutano huo ulioanza tarehe 13 Mei, 2024 ulihudhuriwa na Wanachama wa IAWJ kutoka Nchi takribani 14 ambazo ni pamoja na Tanzania, Nigeria, Kenya, Uganda, Afrika Kusini, Botswana, Senegal, Cote D’voire na nyingine.
Akisoma maazimio ya Mkutano huo, mmoja wa Sekretarieti ya Maandalizi, alieleza miongoni mwa maazimio hayo ni pamoja na ushirikishwaji wa Watawala wa kimila ili kuleta mabadiliko kwa kuwaelimisha juu ya haja ya wao kuepuka kuingilia Mchakato wa Mahakama hasa unapohusisha makosa ya kujamiiana na uhalifu dhidi ya watoto na wanawake.
Azimio lingine ni Viongozi wa Kimila wanapaswa kufunzwa kuwawezesha wanawake na walio katika Mazingira hatarishi katika jamii zao kwa kuwa wanaheshimiwa na kuchukuliwa kama Viongozi wa kutoa ushauri na maoni.
Maazimio mengine yaliyofikiwa katika Mkutano huo ni kila Nchi Wanachama kuwa na Rejesta ya Wahalifu wa Kujamiiana ambayo inapaswa kuhuishwa mara kwa mara ili kusaidia kufuatilia na kubadilishana taarifa miongoni mwa Nchi Wanachama ili kupambana na makosa ya kingono yanayohusiana nayo.
Majaji na Mahakimu hao wanawake wamekubaliana pia kuelimisha na kutoa mafunzo kwa waliotengwa na walio katika mazingira hatarishi juu ya Mifumo ya Kisheria ya Nchi Wanachama na upatikanaji wa haki.
Kadhalika, waliazimia kufuatilia na kuchambua hoja za Mahakama. Huku kila Nchi Mwanachama wa ‘IAWJ’ inapaswa kuwa macho katika kuhakikisha kuwa dhana potofu hazizuii upatikanaji wa haki kwa waathiriwa/wanusurika wa unyanyasaji wa kijinsia.
Maazimio hayo na mengine yote yalijielekeza katika mlengo wa Kaulimbiu ya Mkutano wa mwaka huu iliyosema; Nafasi ya Majaji Wanawake katika kupambana na mila potofu katika ulimwengu wa sasa.’ Kupitia Kaulimbiu hiyo Wanachama wa ‘IAWJ’ walisisitizwa kuendelea kuelimisha jamii kuhusu vitendo mbalimbali vinavyoakisi mila potofu.
Mada zilizotolewa katika Mkutano huo ni pamoja na ya Ukatili wa mtandao; je Watoto wetu wapo salama, umaskini na upatikanaji wa haki, kuondosha dhana hasi dhidi ya wanawake-wajibu wa Majaji, ushiriki wa wanawake katika Utawala wa Taasisi za Manispaa na kitaifa na nyingine.
Mkutano ujao wa Chama cha Majaji Wanawake Duniani (IAWJ) unatarajia kufanyika Aprili, 2025 nchini Afrika Kusini.
Jaji Mkuu wa Ghana, Mhe. Gertrude Sackey Torkornoo akitoa neno la shukrani kwa Washiriki wa Mkutano wa 18 wa Chama cha Majaji Duniani 'IAWJ' Ukanda Afrika (hawapo katika picha) uliofanyika jijini Accra nchini Ghana.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni