Alhamisi, 16 Mei 2024

WATUMISHI, WAJUMBE WA BARAZA IJA WAMUAGA MWENYEKITI WA BARAZA LA CHUO

Na Mwandishi Wetu


Watumishi pamoja na Wajumbe wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa  Mahakama Lushoto (IJA) wamemuaga mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo hicho ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika baada ya kumaliza kipindi chake cha miaka sita ya  kulitumikia Baraza hilo.

 

Hafla ya kumuaga Mhe. Dkt. Ndika imefanyika tarehe 13/05/2024 katika ukumbi wa mafunzo wa Ibrahim Hamis Juma hapa Chuoni Lushoto mkoani Tanga.

 

Mhe. Dkt. Ndika aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Marehemu Dkt John Magufuli tarehe 17/06/2018 kushika wadhifa huo akichukua nafasi iliyoachwa wazi na Jaji mstaafu wa Mahakama ya Rufani Mhe. John Mrosso ambae alikuwa amemaliza muda wake wa kulitumikia Baraza hilo kwa kipindi cha miaka sita. 

 

Watumishi wa IJA pamoja na Wajumbe hao wa Baraza walimuaga Mwenyekiti huyo kwa kumpatia zawadi mbalimbali zikiwemo za  tarakilishi mpakato (laptop) na tuzo maalumu ikiwa ni kuuenzi mchango wake katika kulitumikia Baraza hilo la Uongozi wa Chuo kwa mafanikio makubwa.

 

Katika nasaha zake, Mhe. Dkt. Ndika amesema kuwa ni fahari kubwa kwake kuliongoza Baraza hilo na kwamba mafanikio yaliyopatikana chini ya Uongozi wake ni ya watu wote wakiwemo watumishi pamoja na wajumbe wa Baraza.

 

Aidha, amesema kuwa katika kipindi chake, Chuo kimepiga hatua katika kuendesha mafunzo ya Kimahakama, kufanya utafiti na kutoa ushauri elekezi.

 

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Katibu wa Baraza hilo Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo amebainisha mafanikio makubwa yaliyopatikana chini ya uongozi wa Mhe. Jaji Ndika kuwa ni mabadiliko ya sheria ya Chuo ya mwaka 1998 yaliyofanyika mwaka jana ambayo yanampa mamlaka mbalimbali Jaji Mkuu wa Tanzania ikiwemo kuteua wajumbe wa Baraza la Uongozi wa Chuo pamoja na Muundo mpya wa Uongozi wa Chuo ambao umeanzisha Kurugenzi ya Mafunzo ya Kimahakama ikiwa ni mara ya kwanza tangu Chuo hicho kianzishwe zaidi ya miaka 20 iliyopita.

Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa  Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika akionesha zawadi aliyopatiwa na Watumishi wa pamoja na Wajumbe wa Baraza la Uongozi IJA baada ya kumaliza kipindi chake cha miaka sita ya  kulitumikia Baraza hilo.


Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Katibu wa Baraza hilo Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akimkabidhi tuzo maalumu Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa  Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika Chuo baada ya kumaliza kipindi chake cha miaka sita ya  kulitumikia Baraza hilo.


Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa  Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa Menejimenti na wa Baraza la Chuo. Wa kwanza kushoto waliyokaa ni  Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Katibu wa Baraza hilo Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo na wa pili Makamu mwenyekiti wa Baraza ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Jaji Fauz Twaib.


Makamu mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la IJA ambaye pia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Jaji Fauz Twaib akifafanua jambo katika hafla hiyo.

Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa  Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika akiwa anaonyesha zawadi ya tarakilishi mpakato (laptop) aliyokabidhiwa na watumishi wa IJA na tuzo maalumu ikiwa ni kuuenzi mchango wake katika kulitumikia Baraza hilo la Uongozi wa Chuo kwa mafanikio makubwa.


Mkuu wa Chuo cha IJA ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Katibu wa Baraza hilo Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akitoa neno wakati wa hafla hiyo.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni