Jumanne, 24 Septemba 2024

JAJI PROJESTUS KAHYOZA ASISITIZA MATUMIZI YA MFUMO WA e-CMS UVINZA- KIGOMA

Afanya ziara ya ukaguzi Uvinza, Gereza la Wilaya Kigoma

Apongeza kazi nzuri ya uondoshaji mashauri Uvinza

Na AIDAN ROBERT, Mahakama –Kigoma

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza amesema Mahakama ya Tanzania kupitia Mfumo wa Uratibu na Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) imeweka wazi juu ya hatua mbalimbali za mashauri kwa kila Jaji na Hakimu katika kituo chake, hivyo ni wazi kuwa mashauri mlundikano hayakubaliki Mahakamani.

Mhe. Kahyoza aliyasema hayo jana tarehe 23 Septemba 2024, alipokuwa akifanya ukaguzi wa kawaida wa Mahakama ya Wilaya Uvinza na Magereza ya Wilaya Kigoma ikiwa ni katika kutekeleza Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania.

Alisema ni vyema kushughulikia changamoto kabla ya kuzalisha mashauri ya mlundikano katika Kituo na kusisitiza kuwa, Mahakama za Mwanzo mbili ya Mgambo na Kalya ambazo hazitoi huduma ziangaliwe kwa jicho la umuhimu ili wananchi wanaoishi katika maeneo hayo ambayo ni kilometa 71 kutoka ilipo Mahakama ya Wilaya Uvinza wasogezewe huduma.

“Kwa umuhimu wa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ni vyema Mahakama hizi tukaona ni kwa jinsi gani Mahakama hizi za Mwanzo Mgambo na Kalya zinaweza kufanya kazi ili kuwapunguzia gharama wananchi wa maeneo hayo ambao wanakosa haki yao ya msingi ya kupata huduma za kimahakama,” alisema Jaji Kahyoza.

Aidha, alisema pamoja na uchache wa watumishi wa Mahakama ya Wilaya hiyo ambayo pia ina Hakimu mmoja pekee, ameona kazi nzuri wanayofanya na kuwapongeza kwa takwimu nzuri za kumaliza mashauri 161 kwa miezi tisa.

Pamoja na mambo mengine, Mhe. Kahyoza alisisitiza weledi, uadilifu na uchapakazi kwa watumishi hao ikiwa ni pamoja na kusoma Mkataba wa Huduma kwa Mteja wa Mahakama ili kuendelea kujikumbusha wajibu katika kutoa huduma stahiki kwa wananchi hasa wanaofika katika Ofisi za Mahakama.

Kwa upande wake Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya Uvinza, Mhe Misana Majula, akitoa taarifa ya utendaji kwa Jaji Kahyoza alisema kwamba, Mahakama ya Wilaya Uvinza ni moja ya Mahakama mkoani Kigoma yenye mashauri mengi yanayoskilizwa na Hakimu mmoja tu. 

Mhe. Majula alisema kuwa, jumla ya mashauri 134 yamesajiliwa kutoka Januari mpaka Septemba mwaka huu na kati ya hayo 161 yameamuliwa na kubaki mashauri 66 ambayo yanaendelea kusikilizwa mahakamani hapo.

Katika ziara hiyo ya ukaguzi, Jaji Kahyoza vilevile alipata fursa ya kuambatana na Wadau wa Haki Jinai kutembelea Gereza la Wilaya ya Kigoma kwa ajili ya ukaguzi wa kawaida wa Gereza hilo ili kujionea na kutatua changamoto walizo nazo wafungwa zinazohusiana na mwenendo wa mashauri yao mahakamani.

“Mahakama na Wadau wake tutaendelea kutatua changamoto zenu kwa karibu ili haki zenu za msingi zisichelewe, ndio sababu tuna utaratibu wa kuja kutembelea Magereza ili kufahamu na kupokea changamoto hizo na kuzitatua,” alisema Mhe. Kahyoza. 

Hata hivyo, Jaji huyo alisisitiza matumizi ya Mfumo  wa e-CMS   kwa Wadau wake ili kuwa na uelewa sawa katika kushughulikia mashauri ya wafungwa na mahabusu waliopo katika Gereza hilo la Bangwe sambamba na kuwafahamisha wadau wote juu ya Mahakama kupunguza matumizi ya karatasi na kutumia mifumo kusikiliza mashauri pamoja na kutoa nakala laini kwa wadau wa mashauri yanayoendelea mahakamani kwa ujumla wake.  

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Gereza hilo, Inspekta Geofrey Bitalisha aliishukuru Mahakama na Wadau wake waliofika gerezani hapo kwa ajili ya kusikiliza na kutatua changamoto za wafungwa na Mahabusu walipo katika Gereza hilo na kuongeza kuwa, maelekezo yote yaliyotolewa na Jaji Kahyoza yatafanyiwa kazi ili kwenda na kasi ya Mahakama katika kutoa haki kwa wafungwa na Mahabusu waliopo katika Gereza hilo. 

Katika ziara hiyo ya ukaguzi, Mhe. Jaji Kahyoza aliambatana na Hakimu Mkazi  Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Mtotay, Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Kigoma, Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Uvinza na kwa upande wa Wadau aliambatana na Afisa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Kigoma, Mkuu wa Ofisi ya Mashtaka Mkoa Kigoma na Afisa Uhamiaji Msaidizi wa Mkoa wa Kigoma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika katika Mahakama ya Wilaya Uvinza kwa ajili ya ukaguzi wa Mahakama za Wilaya hiyo jana tarehe 23 Septemba, 2024.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza (kushoto) akisalimiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya Kigoma, Mhe. Majula Misana mara baada ya kuwasili kwa ukaguzi Mahakama ya Wilaya Uvinza.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza (hawapo katika picha).

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza, (aliyesimama wa kwanza kulia)  akisalimiana na wananchi waliofika Mahakama ya Wilaya Uvinza kwa ajili ya kupata huduma katika Mahakama hiyo. Kulia kwa Jaji Kahyoza ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay. Aliyesimama wa kwamnza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo, wa pili kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Mhe. Majula Misana.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza (wa pili kulia)  pamoja na  Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay (wa kwanza kulia) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo (wa kwanza kushoto) wakipokea maelezo kutoka kwa Afisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Bw. Tumaini Panga.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Uvinza. Walioketi kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya Uvinza, Mhe. Majula Misana.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus R. Kahyoza (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi na wadau wa Mahakama. Wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo, wa pili kushoto ni Afisa Uhamiaji Msaidizi wa Mkoa wa Kigoma, Mrakibu wa Jeshi la Uhamiaji Mkoa Kigoma  Dominick Kibuga, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Mhe. Majula Misana akifuatiwa na Mpelelezi Mkuu wa Makosa ya Jinai wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Alfred Kasoro.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni