Ijumaa, 6 Septemba 2024

MAHAKAMA YAPONGEZWA KWA JITIHADA ZA KUSOGEZA HUDUMA KARIBU NA WANANCHI

  •    Pongezi hizo zinatokana na Mahakama Kuu Jijini Mbeya kupokea Mahakama Inayotembea

 Na Daniel Sichula – Mahakama, Mbeya 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa jitihada kubwa za kuboresha huduma za kimahakama ili kuhakikisha huduma za utoaji haki zinaendelea kumlenga mwananchi wa kawaida.

Akizungumza hivi karibuni katika hafla fupi ya kupokea gari maalum litakalotumika kama Mahakama Inayotembea ‘Mobile Court’, hafla iliyojumuisha na mafunzo kwa watumishi ya namna ya kutoa huduma kwa mteja katika Mahakama Inayotembea. Mhe. Tiganga alisema Mahakama hiyo itakuwa msaada mkubwa wa kuhakikisha huduma bora za kimahakama zinaendea kutolewa kwa wepesi na haraka bila kuathiri taratibu za utoaji haki kwa wananchi mahali popote walipo na kupunguza gharama za kuitafuta haki. 

“Nitumie nafasi hii kuipongeza Mahakama ya Tanzania kwa jitihada kubwa inayoweka katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma iliyo bora na tunaahidi kuendelea kutoa huduma iliyotukuka kwa wananchi kwa kuzingatia ufanisi na weledi mkubwa” alisema Mhe. Tiganga 

Mapokezi hayo ya Mahakama Inayotembea yaliambatana na mafunzo ya namna ya uendeshaji wa huduma katika Mahakama hiyo, ambapo washiriki walikua ni Mahakimu wa Mahakama za Wilaya na Mwanzo, Maafisa usafirishaji, Maafisa Kumbukumbu pamoja na Afisa TEHAMA. 

Aidha, wahusika wote katika mafunzo hayo walipewa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania unaotekeleza shughuli za Mahakama ikiwemo zile za Mahakama Inayotembea, ikiwa ni pamoja na Utawala, uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali, upatikanaji na utoaji huduma kwa wakati, kuimarisha Imani ya Umma na kushirikisha wadau wakiwemo Viongozi wa Serikali za Mitaa, Polisi, Magereza pamoja na jamii kwa ujumla. 

Naye, Mkufunzi wa mafunzo hayo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe.  Moses Ndelwa akifafanua juu ya nguzo zinazosimamia Mahakama Inayotembea alisema kuwa, lengo ni kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na jamiii, kuongeza ufanisi na weledi katika utoaji haki na usikilizwaji wa mashauri mbalimbali na pia kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi kwa kutumia Mahakama Inayotembea itapunguza gharama za wananchi kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za kimahakama na kuokoa muda.

“Ni muhimu kwa watoa hudumu katika Mahakama Inayotembea kuepuka kujihusisha na vitendo vya rushwa ili kuongeza imani kwa wananchi. Aidha kupitia mpango huu wa Mahakama Inayotembea Tanzania imepata sifa kubwa sana kimataifa, mpaka kupelekea baadhi ya mataifa ya Afrika kuja kujifunza jinsi ya uendeshaji wa Mahakama hizi, baadhi ya mataifa hayo ni Ethiopia, Uganda na Malawi na Zimbabwe,” alisisitiza Mhe. Ndelwa

Aidha, shabaha kubwa ya Mahakama Inayotembea inalenga kuongeza wigo wa kutoa huduma za haki kwa wananchi kwa kuwafikia watu 5,833 kwa mwaka na kusikikiliza mashauri kwa wakati, kwa muda usiozidi siku thelathini (30) kwa shauri lililosajiliwa, kutoa huduma zenye ubora, kutoa ratiba za vikao, kutoa elimu kwa umma, kukuza matumizi ya teknolojia na kutoa taarifa mbalimbali za mashauri yaliyoamuliwa kwenye Mahakama Inayotembea kwa haki na kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (wa saba kutoka kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kanda ya mbeya wakati wa hafla ya kupokea Mahakama Inayotembea jijini Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga akishuka ndani gari maalum lijulikanalo kama Mahakama Inayotembea kwa kutumia ngazi ya watu wenye mahitaji maalum huki akishudiwa na Mratibu wa Mahakama Inayotembea nchini Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mhe. Moses Ndelwa wakati wa hafla ya kukabidhi gari hilo maalum.

Mratibu wa Mahakama Inayotembea nchini Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mhe. Moses Ndelwa (mwenye tai nyeusi) akionesha matumizi ya ngazi ya kupandia na kushuka kwa wateja wenye mahitaji maalum watakofika kuhudumiwa katika Mahakama Inayotembea. Kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga.



Mratibu wa Mahakama Inayotembea nchini Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mhe. Moses Ndelwa (mwenye tai nyeusi) akionesha matumizi ya vifaa mbalimbali vinavyotumika ndani ya Mahakama Inayotembea kwa watumishi na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga.



Sehemu ya Maafisa Usafirishaji waliopata mafunzo ya kuihudumia Mahakama Inayotembea.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha- Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni