Jumatano, 26 Februari 2025

JAJI MAGHIMBI AFUNGUA MAFUNZO YA KANUNI ZA MAADILI YA KIMAHAKAMA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi leo tarehe 26 Februari, 2025 amefungua mafunzo yanayohusu Kanuni za Maadili ya Kimahakama (Bangalore Principles) kwa Mahakimu Wakazi 30 wa Mahakama za Wilaya kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Mafunzo hayo ya siku tatu yanafanyika katika Hoteli ya Four Points by Sheraton jijini Dar es Salaam. Yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), kwa ufadhili wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Ujerumaini (GIZ), kupitia mradi wake wa Ukuzaji wa Utawala wa Sheria na Mahakama Barani Afrika (Promotion of Rule of Law and Judiciary in Africa-ProLA).

Wawezeshaji wa mafunzo hayo ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Bukoba, Mhe. Lilian Itemba.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Maghimbi amewahimiza watumishi wa Mahakama kuzingatia maadili na kuendelea kuwajibika kwa umma wakati wa kutekeleza majukumu ya utoaji haki.

Jaji Maghimbi amewaambia washiriki kwamba kanuni za Bangalore hutoa mfumo wa jumla unaosaidia Majaji na Mahakimu kukabiliana na changamoto za kimaadili kwa namna ambayo inahakikisha uhuru, kutopendelea na uwajibikaji.

“Kanuni hizi za uhuru wa kimahakama ni nguzo muhimu kwenye wajibu wetu kwani zinatuongoza kwenye matendo yetu ndani na nje ya Mahakama na kutusaidia kudumisha imani ya umma tunaohudumia,” amesema.

Jaji Maghimbi amebainisha kuwa katika ulimwengu wa kisasa unaoendelea kwa kasi, Majaji na Mahakimu wanakabiliwa na matatizo yanayoongezeka ya kimaadili, kuongezeka kwa mitandao ya kijamii na utata wa masuala ya kisasa ya kisheria, ambayo yote yanawahitaji kuwa makini zaidi kimaadili.

Kwa hivyo, amewaeleza washiriki kuwa mafunzo kama hayo yatawawezesha kubaini changamoto kama hizo na kubadilishana maarifa juu ya jinsi wanavyoweza kutumia kanuni za Bangalore kwa ufanisi katika mamlaka zao.

Jaji Maghimbi aliwakumbusha washiriki hao pia kuwa katika muda wa siku tatu za mafunzo hayo, wawezeshaji watawaelekeza jinsi maadili yao yanavyochangia kwenye kufanya maamuzi na nini wafanye ili kuhakikisha wanaendana na majukumu yao ya kikazi.

Naye Mshauri wa Kisheria GIZ Tanzania, Bi Neema Ndemno aliwaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa kama Maofisa wa Mahakama wana wajibu wa kipekee na muhimu wa kusimamia sheria na kulinda haki za watu wote wanaofika mbele yao.

Alieleza kuwa mienendo ya Maofisa wa Mahakama, kitaaluma na kibinafsi, ina mchango mkubwa katika kudumisha uadilifu na kuhakikisha haki inatolewa kwa haki na bila upendeleo.

Malengo ya mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo washiriki hao juu ya ufahamu wa kanuni hizo ili waendelee kutenda kazi zao za utoaji wa hukumu kwa uhuru, uadilifu, umahiri na bila upendeleo.

Kanuni za Bangalore ziliundwa mwaka 2002 na jopo la Majaji Wakuu na Majaji Waandamizi kutoka sehemu mbalimbali duniani kwa ushirikiano na Umoja wa Mataifa (UN) na zinatoa muongozo wa kanuni za maadili ya Kimahakama ili kuhakikisha taaluma hiyo inazingatia misingi ya uadilifu, uhuru, usawa, umahiri na bila upendeleo.

Mahakama ya Tanzania ina kanuni kama hizo za mienendo na maadili za mwaka 2020 kwa ajili ya Maafisa wake ambazo zilitungwa chini ya Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Namba 4 ya mwaka 2011. Kanuni hizi zinawataka maofisa wa Mahakama kuzingatia uadilifu, uhuru, ustaarabu, umahiri, bila upendeleo na usawa.

 


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji wa mafunzo hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Bukoba, Mhe. Liliani Itemba (kulia).


Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Maofisa kutoka GIZ Tanzania.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya wanaohudhuria mafunzo hayo. Picha chini ni sehemu ya Mahakimu Wakazi wanaoshiriki kwenye mafunzo.


Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu nyingine ya Mahakimu Wakazi wa Mahakama za Wilaya (juu na chini) wanaohudhuria mafunzo hayo.



Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Sekretariet. Picha chini ni Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni