Jumatano, 26 Februari 2025

WATUMISHI MAHAKAMA MOROGORO WAPIGWA MSASA MATUMIZI YA MIFUMO

Na ASHA JUMA - Mahakama Morogoro

Kufuatia maboresho makubwa ya Mahakama katika matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), tarehe 24 Februari, 2025 Watumishi wa Mahakama Kanda ya Morogoro walipatiwa mafunzo ya matumizi ya mifumo mbalimbali.

Akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo, Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga aliwataka Watumishi wote kushiriki kikamilifu kwani yana tija katika majukumu yao ya kazi za kila siku.

“Mafunzo haya yana umuhimu kwetu sote, hivyo ninaagiza kila Kiongozi kwenye eneo lake ndani ya Mahakama kwenye Kanda ya Morogoro ahakikishe Watumishi walio chini yake wanashiriki kikamilifu, lazima wote twende kwa pamoja na maboresho makubwa yanayofanywa na Mahakama,” alisisitiza Mhe. Magoiga.

Aidha, Mhe. Magoiga alitoa rai kwa Watumishi ambao wanaujuzi na masuala yeyote ambayo yatasaidia kufanikisha utendaji kazi kwa ufanisi zaidi wawasilishe mawazo yao kwenye uongozi ambao utayapitia na kujiridhisha ili kuandaa mafunzo ya ndani kwa ajili ya kushirikishana uzoefu.

“Niseme tu kama kuna mtu ana ujuzi wa jambo lolote ambalo litatusaidia kutekeleza majukumu yetu, asisite kuja kutushirikisha nasi tutaandaa mafunzo ya ndani ili wote tupate uelewa wa pamoja, lengo ni kuhakikisha kazi inafanyika kwa ubora,” alieleza Mhe. Magoiga.

Mafunzo hayo yanayotolewa na Wawezeshaji kutoka Kitengo cha TEHAMA ndani ya Kanda ya Morogoro yanategemewa kuhitimishwa kesho tarehe 27 Februari, 2025.

Miongoni mwa mada zitakazotolewa ni pamoja na matumizi na maboresho ya mifumo, matumizi sahihi ya mitandao na usalama wake yanayotumika katika shughuli mbalimbali za kimahakama.

Mafunzo hayo pia yamelenga kuwafikia Watumishi wa ngazi zote ndani ya Kanda ya Morogoro.  Watumishi waliopo wilayani wanapokea mafunzo hayo kwa njia ya mtandao.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga akifungua mafunzo ya ndani ya matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro, Mhe. Susan Kihawa akifuatilia hotuba ya ufunguzi toka kwa Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Stephen Magoiga (hayupo pichani).

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe.  Janeth Kinyage (kushoto), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo (kulia) wakifuatilia mafunzo.

Watumishi wa Mahakama kutoka kada tofauti (juu na chini) akifuatilia mafunzo.


Ofisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano toka Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Bw. Justine Khemuhe akiwawezesha watumishi wakati wa mafunzo hayo.


 Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga (kulia) pamoja na Naibu Msajili, Mhe. Susan Kihawa (kushoto) wakifuatilia mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni