Jumamosi, 1 Februari 2025

WANAFUNZI WANUFAIKA NA ZOEZI LA UTOAJI ELIMU YA SHERIA SONGWE

Na IMAN PATSON MZUMBWE- Mahakama, Songwe

Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe pamoja na wadau wa Mahakama Mkoani humo wamefanikiwa kutembelea shule za Sekondari na Msingi katika kipindi cha maadhimisho ya wiki ya sheria mwaka 2025, kwa lengo la kutoa elimu juu ya Ukatili wa kijinsia, Rushwa, Wosia, Mirathi, Muundo wa Mahakama ya Tanzania pamoja na Nafasi ya Mahakama ya Tanzania katika kufanikisha dira ya maendeleo ya Taifa 2050.

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Wilaya ya Mbozi Mhe. Vitalis Changwe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu Mkoa aliongoza zoezi hilo la utoaji elimu alisema kuwa, elimu hiyo itasaidia kupunguza matukio na matendo yasiyokuwa ya kiungwana katika jamii zetu kwani wanafunzi hao wataweza kusaidia kueneza na kuwaelimisha wazazi, watoto wengine katika jamii zinazowazunguka.

Aidha, Maafisa kutoka Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe walitoa mada juu ya namna ambavyo vitendo vya ukatili vinavyoweza kusababisha watoto wengi kutofikia malengo yao kwenye jamii. Watoto wengi wanafanyiwa vitendo hivyo vya ukatili lakini hawatoi taarifa popote matokeo yake yanaleta madhara kwa jamii mfano; mimba za utotoni, magonjwa na kufanyishwa kazi ambazo hawazisitahili bira ridhaa yao.

Aidha, Vitendo hivyo, vinafanyika kwa sababu wengi wao hawana elimu juu ya ukatili. Ni wakati sahihi kuwaelimisha wanafunzi nini maana ya ukatili na kuwasisitiza kuwa wasisite kutoa  taarifa pale wanapofanyiwa au kuona vitendo hivyo vinafanyika kwani kufanya hivyo kunaweza kusababisha wanafunzi hao kutofikia malengo yao, lakini pia waliwasihi wanafunzi hao kuwa waende kuwa mabalozi kwa wengeni katika jamii kwani kwa kufanya vitendo vya ukatili ni kosa kisheria na adhabu ni kifungo jela.

Wakati huohuo, Maafisa kutoka TAKUKURU Mkoa wa Songwe wametoa elimu kuhusu rushwa na madhara yake wanafunzi hao kwa nyakati tofauti wakieleza kuwa, vitendo vya rushwa ni adui namba moja wa haki katika jamii kwasababu inaweza kusababisha mwenye haki asiipate haki yake anayoitafuta. Rushwa inaweza kusababisha migogoro baina ya pande mbili na inaweza kufifisha maendeleo katika jamii.

Vilevile, wamewaelimisha na kuwahimiza wanafunzi hao kuwa  waende kuwaelimisha wengine ikiwa pamoja na wazazi, marafiki na watu wengine juu ya madhara ya rushwa ikiwa ni pamoja na kutotoa au kutopokea rushwa, kwani kwa kufanya hivyo ni kosa  la kijinai na adhabu yake ni kifungo au faini ama adhabu zote mbili kwa wakati mmjo.

Kamati  hiyo ya utoaji elimu imejumuisha  wadau kutoka Taasisi mbalimbali kama vile TAKUKURU, Ofisi ya mashtaka Taifa Mkoa wa Songwe, Jeshi la polisi Mkoa, Ustawi jamii, Huduma kwa jamii, mwakilishi kutoka Ofisi ya Mkurugenzi Wilaya ya Mbozi  na Mawakili wa kujitegemea Mkoa wa Songwe.

Afisa wa TAKUKURU akiwaelimisha wanafunzi wa Shule ya Msingi Ephata juu ya madhara yatokanayo na Rushwa katika jamii.

Mmoja ya mwanafunzi wa shule ya msingi Ephata akitoa neno la shukurani kwa niaba ya wanafunzi wengine.

Wanafunzi wa Shule ya Msingi Oswe Girls wakipewa elimu ya ukatili wa kijinsia.

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lwati wakipata elimu juu ya Nafasi ya Mahakama ya Tanzania katika kufanikisha dira ya maendeleo ya Taifa 2050.
Afisa kutoka Jeshi la Police Bi. Gradness Aaron akitoa elimu kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Insani.

Afisa wa Jeshi la Police Bi. Merina Method akitoa elimu kwa wanafunzi wa shule Msingi Sasenga.

Wanafunzi wa shule ya Sekondari Insani walionufaika na elimu ya sheria wakimsikiliza kwa makini mtoa elimu hiyo hayupo pichani.


 Kamati ya Elimu Mkoa wa Songwe ikiongozwa na Mwenyekiti wake Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Wilaya ya Mbozi Mhe. Vitalis Changwe (aliyepakatia laptop) wakiwa kwenye picha ya pamoja katika zoezi la kutoa elimu ya sheria.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni