Na Mwandishi Wetu- Mahakama, Momba
Kamati
ya Mafunzo ya kimahakama, Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya hivi karibuni iliratibu na
kuendesha mafunzo maalum ya utekelezaji wa hukumu kwa Mahakimu wa Mahakama za
Mwanzo wa Kanda hiyo ambayo inajumuisha Mikoa ya Mbeya na Songwe. 
Mafunzo
hayo yaliyoendeshwa mnamo tarehe 13 Machi, 2025 yalilenga kuboresha Utekelezaji wa Hukumu katika Mahakama
za Mwanzo na yalifanyika kwa njia ya mtandao kupitia jukwaa la Mahakama
Mtandao (Virtual Court Platform).
Akifungua
Mafunzo hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe.
Joachim Tiganga aliwasisitiza washiriki wa mafunzo hayo umuhimu wa
uelewa wa kina wa taratibu za utekelezaji wa hukumu ili kuhakikisha haki
inatendeka kwa ufanisi na weledi na kwa kuzingatia sheria. 
Mhe.
Tiganga alisema kuwa, utekelezaji wa hukumu ni hatua muhimu katika kuhakikisha
haki inapatikana kwa walioshinda mashauri yao, na kwamba kucheleweshwa kwa utekelezaji
huo kunaweza kupunguza imani ya wananchi kwa Mahakama lakini pia kufanya
ushindi katika kesi kuwa ni kama pambo tu.
Mhe.
Tiganga aliwataka washiriki wa mafunzo haya kutumia fursa hiyo kujifunza na
kubadilishana uzoefu ili kuboresha utendaji wao wa kazi kila siku. 
“Nipongeza
mwamko wenu wa ushiriki mkubwa wa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo katika mafunzo
haya na kuwataka kuhakikisha kuwa wanatumia maarifa watakayoyapata kuboresha
utoaji wa huduma za Mahakama,” alisistiza Jaji Tiganga.
Kwa
upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, Mhe.
Francis Kishenyi akihitimisha mafunzo hayo aliwapongeza washiriki kwa ushiriki
mzuri na kujituma katika kujifunza mbinu bora za utekelezaji wa hukumu. 
“Utekelezaji
wa hukumu ni hatua muhimu inayohakikisha kuwa haki inayotolewa na Mahakama
inatekelezwa kwa ufanisi na kwamba kutofuata taratibu sahihi kunaweza kuathiri
uaminifu wa Mhimili wa Mahakama kwa wananchi,” alisisitiza Mhe. Kishenyi.
Vilevile,
aliwaasa washiriki kuzingatia sheria na taratibu zote za utekelezaji wa hukumu
ili kuepuka ucheleweshaji au changamoto zinazoweza kusababisha malalamiko kutoka
kwa wadaawa. Aidha, aliwahimiza Wafawidhi wa Vituo vya Mahakama kuhakikisha
kuwa utekelezaji wa hukumu unafanyika kwa uadilifu na kuzingatia maadili ya
kimahakama. 
Aidha,
alikumbusha Mahakimu hao kuwa, ukaguzi wa mara kwa mara katika Mahakama
unapaswa pia kuelekeza macho katika eneo hilo la utekezaji wa hukumu ili
kubaini changamoto zinazoweza kujitokeza na kuzitafutia suluhisho mapema.
Mhe.
Kishenyi alisisitiza umuhimu wa kujifunza mara kwa mara na kuendelea kuhamasishana
na kushirikiana katika kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa hukumu. Aliwahakikishia
kuwa mafunzo kwa njia ya mtandao yataendelea kulingana na kadri muda
unavyoruhusu, hivyo akawataka washiriki kuwa tayari kujifunza na kushiriki
kikamilifu wakati wowote inapojitokeza fursa hiyo.
Mhe.
Kishenyi aliwataka washiriki kutekeleza yale yote waliyojifunza, huku
akiwahimiza kuendelea kupanua maarifa na kushirikiana kwa lengo la kuboresha
utoaji wa haki nchini.
Washiriki
wa mafunzo hayo walikuwa ni Mahakimu
Wafawidhi wa Mahakama za Mwanzo na pia yalihudhuriwa na viongozi
mbalimbali wa Mahakama akiwemo Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mashaka Said Kalunde Mhe. Victoria Nongwa ambaye pia ni Mwenyekiti
wa Kamati ya Mafunzo Kanda ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo na Naibu
Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu.
Aidha,
katika Mafunzo hayo yaliwezeshwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu
Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer pamoja
na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Momba Mhe. Raymond Venance Kaswaga 
Vilevile,
Mafunzo hayo yaliratibiwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Uyole Mhe.
Ayubu M. Shellimo yalihusisha mada mbalimbali zenye lengo la kuboresha utendaji
kazi wa Mahakama za Mwanzo katika kanda hiyo kwenye utekelezaji wa hukumu.
Aidha, mada zilizotolewa zilikuwa kama vile, taratibu sahihi za kukamata na kuuza mali, jukumu la madalali wa Mahakama na watoa huduma za mchakato wa utekelezaji wa hukumu, mbinu bora za uhamishaji wa tuzo za Mahakama, utunzaji wa kumbukumbu za utekelezaji wa hukumu na taratibu za kushughulikia mapingamizi.
Mafunzo
hayo ni mwendelezo wa utoaji wa mafunzo endelevu yanayotolewa na Mahakama ya
Tanzania kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ambacho ni kitovu cha
mafunzo na maarifa ya Mahakama ya Tanzania, kwa lengo la kuwajengea uwezo
watendaji wa Mahakama katika nyanja mbalimbali za utoaji haki na ni sehemu ya
utekelezaji Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania na Sera ya Mafunzo ya
Kimahakama.
 




 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni