Jumamosi, 1 Machi 2025

WADAU WASISITIZWA USHIRIKIANO KUISAIDIA MAHAKAMA KUMALIZA MASHAURI KWA WAKATI

Na Christopher Msagati- Mahakama, Manyara

Wadau wa Mahakama Mkoa wa Manyara wamesisitizwa kuendelea kutoa ushirikiano wa karibu kwa Mahakama ili kuboresha na kuisaidia Mahakama kumaliza mashauri kwa wakati kumwezesha mwananchi kupata muda wa kutosha kuzalisha mali na kujenga uchumi kwa ustawi wa Taifa.

Hayo yamesemwa jana tarehe 28 Februari, 2025 na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora wakati wa kikao kilichofanyika katika Ukumbi wa Wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Kikao hicho kiliwashirikisha wadau mbalimbali wa Mahakama Mkoa wa Manyara wakimo Ofisi ya Mashtaka, TAKUKURU, Ofisi ya Uhamiaji, Ofisi ya Magereza, Ofisi ya Kamanda wa Polisi, Ofisi ya Ustawi wa Jamii, Madalali wa Mahakama, Ofisi ya Wakili wa Serikali, Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba wa Wilaya ya Babati, Mawakili wa Kujitegema pamoja na Mahakimu waliopo Wilayani Babati.

Aidha, kikao hicho kilichoandaliwa mahsusi kwa ajili ya kujadili mafanikio ya mwaka 2024 pamoja na kujiwekea malengo ya Mwaka 2025. Mhe. Kamuzora aliwasisitiza wajumbe wa kikao kuhakikisha kuwa wanaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuisaidia Mahakama Kanda ya Manyara kumaliza mashauri mapema ili wananchi wapate haki zao kwa wakati.

“Tumefanikiwa kumaliza mwaka 2024 bila ya kuwa na mashauri ya Mlundikano, kwa hili inabidi tuwashukuru sana wadau wetu kwa kuwa ushirikiano wenu kwetu ndiyo uliofanikisha haya yote. Kila mmoja humu ndani amekuwa na mchango mkubwa katika suala zima la kumaliza mashauri, tunaomba pia kwa mwaka huu 2025 muendelee hivyo hivyo na tena kwa bidii zaidi ili tuweze kuwasaidia wananchi tunaowahudumia wapate haki zao kwa wakati,” alisema Mhe. Kamuzora.

Katika taarifa ya Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara inayohusu mashauri iliyosomwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo ilisisitiza wadau kuendeleza kasi ya matumizi ya TEHAMA na mabadiliko yake yanayotokea mara kwa mara mahakamani.

“Huduma zetu kwa sasa zinapatikana kwa njia ya mtandao, kuanzia kufungua shauri, kuliendesha na hadi kulitolea hukumu, wadau wetu tunawasihi muendelee kujifunza na kuifahamu mifumo hii kwa sababu licha ya kupunguza gharama na matumizi ya karatasi, pia mifumo hii inasaidia kufikisha huduma haraka na kwa uhakika zaidi kwa wananchi,” ilinukuliwa sehemu ya taarifa hiyo.

Akichangia mada katika kikao hicho, Mkuu wa Uhamiaji Mkoa wa Manyara Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Philon P. Kyetema alisema kuwa, Ofisi yake itaendelea kushirikiana na Mahakama katika mnyonyoro wa Utoaji Haki na itaendelea kujitahidi kutafuta mbinu za kukabiliana na changamoto ya wafungwa ambao ni wahamiaji haramu wanaokaa gerezani kwa muda mrefu na kusababisha changamoto ya kuwa na mlundikano katika magereza.

“tunajua kuwa wafungwa wengi wa makosa ya uhamiaji haramu wanakaa katika magereza yetu kwa muda mrefu bila ya kurudishwa makwao. Hii yote inasababishwa na sababu za kiuchumi na kibajeti. Tumeanza kubuni mbinu za kuwasiliana na ndugu zao pia ili nao waweze kufanya taratibu za kuwarudisha makwao,” alisema Kamishna Msaidizi Kyetema.

Akichangia katika kikao hicho Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Bw. Lisungu. M. Cosmo kwa niaba ya Jeshi la Magereza wameipongeza Mahakama kwa juhudi wanazozifanya za kuhakikisha kuwa Nakala za Hukumu na Mienendo ya mashauri zinatoka mapema na mara nyingi siku hukumu inaposomwa.

“kwa kuwa jitihada za Mahakama za kutoa nyaraka zimeonekana, sisi Jeshi la Magereza tutaendelea kuendana na kesi hii ya TEHAMA ili tuweze kuhakikisha mahabusu na wafungwa wanapata mawasiliano ya mara kwa mara, kuanzia usikilizwaji wa mashauri na hata Rufaa zao,” alisema Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Lisungu. M. Cosmo.

Mahakama Kuu Kanda ya Manyara imeweka utaratibu wa kukutana na wadau wake mara kwa mara na kuweka mikakati mbalimbali ambayo yote ina lengo la kuongeza ushirikiano miongoni mwa wadau lakini pia kukiwa na lengo la Kumaliza mapema mashauri yanayofunguliwa Mahakamani ili kuendana na malengo ya Mahakama ambayo yamewekwa Kitaifa na Kikanda.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora akizungumza katika kikao cha Mahakama na Wadau wa Mahakama kilichofanyika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Manyara jana tarehe 28 Februari, 2025. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemedi. 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo akitoa taarifa yake katika kikao na wadau wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.

Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Mkoa wa Manyara Lisungu M. Cosmo akichangia mada katika kikao cha wadau wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.

Sehemu ya wajumbe wakifuatilia mada zilizokuwa zikichangiwa katika kikao cha wadau wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.

Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Philon P. Kyetema akichangia mada katika kikao cha wadau wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Magugu Mhe. Kuruthumu Mkundawantu akichangia mada katika kikao cha wadau wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni