- Afurahishwa na ushiriki wa dhati na mijadala yenye tija ya Majaji Wafawidhi na Wadau wa haki madai
Na MARY GWERA, Mahakama-Arusha
Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) Ukanda wa Afrika Mashariki, Bi. Caroline Mugala amekiri kufurahishwa na Ushirikiano uliopo kati ya Shirika la Kazi Duniani na Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Tanzania huku akionesha furaha yake kufuatia mafanikio yaliyopatikana katika Kikao cha Haki Kazi baina ya Shirika hilo na Majaji Wafawidhi na wadau wa haki kazi.
Bi. Mugala amebainisha hayo leo tarehe 16 Mei, 2025 alipokuwa
akifunga kikao kazi cha siku mbili kilichohusisha Majaji Wafawidhi pamoja na
Wadau wa haki kazi kilichofanyika katika Hoteli ya ‘Corrridor Springs’
jijini Arusha.
“Mafunzo haya ni hatua nyingine
muhimu katika ushirikiano wa Shirika la Kazi Duniani na Mahakama ya Tanzania
katika kuimarisha haki za kazi na kuendeleza kazi zenye staha kwa maadili ya
uongozi hadi mageuzi ya kidijitali kutoka viwango vya kimataifa vya kazi hadi
mijadala ya kijamii,” amesema Mkurugenzi huyo.
Bi. Mugala
amesema kuwa, amefurahishwa hasa na wingi wa mitazamo na madhumuni madhubuti iliyowasilishwa na kujadiliwa wakati wote wa kikao kazi hicho na
kwamba ana imani elimu hiyo ya pamoja itaendelea kuunda Mahakama ya Kazi yenye
ufanisi zaidi na yenye kuzingatia haki.
Ameongeza
kwa kuahidi kuwa, Shirika la Kazi Duniani litaendelea kutoa ushirikiano kwa
Mahakama ya Tanzania hususani Divisheni ya Kazi ili kuendelea kuboresha haki
kazi.
Kadhalika,
ametoa shukrani zake kwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt.
Mustapher Mohamed Siyani kwa kufungua kikao kazi hicho pamoja na uongozi wa Mahakama
ya Kuu Divisheni ya Kazi chini ya Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina kwa kufanikisha
uratibu wa kikao hicho.
Awali akizungumza wakati akitoa
majumuisho ya Kikao Kazi hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni
ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina amelishukuru kwa dhati Shirika la Kazi Duniani
(ILO) kwa ushirikiano wanaoendelea kuutoa kwa Mahakama hiyo unaolenga kuboresha
haki kazi.
Mhe. Mlyambina amewakumbusha washiriki wa kikao kazi hicho kuwa ni muhimu kuzingatia kaulimbiu ya kikao hicho isemayo; ‘Uboreshaji wa Uongozi kwa Ufanisi na Tija katika Utoaji wa Haki Kazi’.
Kadhalika, amewakumbusha pia yaliyosisitizwa
na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed
Siyani wakati wa ufunguzi wa kikao hicho ambapo alisisitiza juu ya kuhakikisha
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yanaimarishwa ili
kuboresha huduma, kuongeza uwazi na uwajibikaji katika kushughulikia mashauri yote,
yakiwemo yanayohusu migogoro ya kazi mahakamani.
Aidha, Mhe. Dkt. Mlyambina aliwadokeza washiriki
wa kikao hicho kuhusu mada zilizowasilishwa na Wawezeshaji na kuzielezea kwa
ufupi kila moja. Miongoni mwa mada zilizotolewa ni pamoja na Uongozi (Leadership); Motisha kwa watumishi na kujenga
ujasiri (motivating employees and building confidence); Kanuni za Maadili za
uongozi na Uadilifu (Leadership Code of ethics and Integrity); Utatuzi Mbadala
wa Migogoro ADR, kupitia Upatanishi, na Usuluhishi (ADR, through Mediation, and
Arbitration) na kadhalika.
Aidha, Majaji Wafawidhi pamoja na wadau wa haki kazi walioshiriki katika kikao hicho walipatiwa vyeti ikiwa ni ishara ya kushiriki ipasavyo katika kikao kazi hicho.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni