Na INNOCENT KANSHA - Mahakama
Mtendaji Mkuu wa Mahakama
ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amelihakikishia Baraza la Uongozi la
Chuo cha Uongozi wa Mahakama – Lushoto (IJA) kuwa Mahakama ya Tanzania,
itaendelea kutoa ushirikiano katika kuhakikisha Chuo hicho kinaendelea kuwa
kisima cha maarifa ili kizidi kuisaidia jamii.
Akizungumza na Baraza
hilo la Uongozi mapema leo tarehe 03 Juni, 2025 Ofisini kwake Makao Makuu ya
Mahakama Jijini Dodoma, Prof. Ole Gabriel amesisitiza kuendeleza ushirikiano uliopo
baina ya Tasisi zote mbili yaani Mahakama na Chuo kwa kuwa kwa kufanya hivyo
kutatoa msukumo mkubwa katika utendaji kazi.
“Nitoe rai kwamba kama
Chuo lazima kitekeleze majukumu yake kimkakati kwa kuwa na maono na malengo ya
muda mrefu na kutafuta ufumbuzi wa kutatua kero na changamoto zilizopo
zinazoweza kutatuliwa na pia wataalam wa Taasisi zote kushirikiana inapobidi
ili kuja na mikakati ya maboresho mbalimbali ya kimifumo,” amesema Mtendaji
Mkuu.
Aidha, Prof. Ole Gabriel
ameshauri Uongozi kupanua wigo na kufiria kuongeza matawi ya Chuo kwenye majiji
kama vile Dar es salaam, Mbeya na Dodoma ili kuwezesha Chuo kuongeza mapato ya
ndani. Vilevile kuanzisha mkakati wa kuanza kufundisha kwa njia ya masafa
(e-Classes) ili watu wengi zaidi wapate nafasi ya kupata maarifa kwa kujifunza
kwa njia ya mtandao.
Matumizi ya TEHAMA yana mchango
mkubwa katika kuboresha utendaji kazi, Mathalani Mahakama ya Tanzania kwa sasa ni kinara
wa Matumizi ya TEHAMA nchini. Hivyo basi Chuo ili kiweze kufundisha kwa njia ya
masafa kinatakiwa kuboresha mifumo na matumizi ya TEHAMA ili kuimarisha utoaji
wa elimu kwa njia hiyo.
Mtendaji Mkuu ameongeza kwa
kusema kuwa, Mahakama inamtandao nchi nzima na Majengo ya kisasa hivyo Chuo
kikishapanua wigo wa kufundisha masomo kwa njia ya masafa kila inapofika mwisho
wa muhula wa kimasomo wanafunzi wanaotakiwa kufanya mitihani wanaweza kutumia
majengo ya Mahakama na kufanya mitihani huko huko waliko, mitihani kama ile ile
inayofanywa na Wanafunzi kwenye kampasi Kuu na pia wanaweza kuwatumia Maafisa
Mahakama kusimamia na kuwapa motisha na maisha yakazidi kutamalaki.
Vilevile, Prof. Ole
Gabriel akaushauri Baraza la Uongozi kuanza kufikiria kutoa huduma kimataifa
kwani Chuo kinafanya mambo mazuri wako watanzania wengi wanaishi nje ya nchi
wangepeda kusoma IJA wawekewe utaratibu mzuri wa kujiunga na Chuo ili waweze
kujiunga na kupata elimu inayotolewa na Chuo. Kupitia Katibu Mkuu Wizara ya
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anaweza kusaidia hilo
likawezekana.
“Chuo kinatakiwa kuendelea
kulinda na kuheshimu itifaki za kiserikali na IJA hususani Waheshima Majaji
kuna mahali pengine hawawezi kwenda kutekeleza kazi za Chuo basi watumike
wawakilishi. Aidha kwa wale watumishi wa Chuo ambao siyo Maafisa Mahakama
wafikiriwe kwa karibu ili kuongeza tija katika utendaji kazi,” amesema Prof.
Ole Gabriel.
Kwa upande wake,
Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama – Lushoto (IJA)
ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mary Caroline
Levira ameushurukuru Uongozi wa Mahakama kwa niaba ya Baraza la Uongozi wa Chuo
kwa ushirikiano wanaopatiwa na Mahakama katika kutekeleza majukumu yao kama
washauri wa Chuo.
“Mjadala wetu umekuwa wa
manufaa makubwa kuna mambo mengi tumejifunza na tumepata uelewa wa pamoja ambao
utatusaidia kwenda kutekeleza mipango kabambe ambayo tumejiwekea ya
kukiendeleza na kuhakikisha IJA inafanya vizuri na tunasonga mbele,” amesisitiza
Mwenyekiti huyo.
Aidha, Mhe. Dkt. Levira ameongeza
kuwa, ni ari ya kila mwana IJA kuona kwamba anatimiza wajibu wake ili kuleta matokeo
chanya na yakupigiwa mfano. Vilevile hoja nyingi zimefafanuliwa vizuri na kutoa
muelekeo mpya tofauti na mtazamo wa Uongozi wa Baraza tuliokuwa nao awali kabla
hatujafika hapa, hivyo basi Baraza la Uongozi litatoka hapa na taswira chanya
juu ya hoja zilizojadiliwa kwa kina na kwa ufasaha mkubwa ili kuleta matokeo
yaliyokusudiwa.
Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama – Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mary Caroline Levira akiongoza kikao baina ya Viongozi Waandamizi wa Mahakama na Baraza la Uongozi la Chuo cha Uongozi wa Mahakama – Lushoto (IJA) leo tarehe 3 Juni, 2025 ofisini kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel jijini Dodoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni