Jumapili, 10 Agosti 2025

JAJI MKUU ASHIRIKI IBADA YA KUMUAGA SPIKA MSTAAFU HAYATI JOB NDUGAI

·       Amuelezea Hayati Ndugai kuwa mpenda haki

 Na MARY GWERA, Mahakama - Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju leo tarehe 10 Agosti, 2025 ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson na Watanzania kwa ujumla katika ibada ya kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge, Hayati Mhe. Job Yustino Ndugai aliyefariki dunia tarehe 06 Agosti mwaka huu.

Ibada ya kumuaga Hayati Ndugai imefanyika katika Viwanja vya Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania jijini Dodoma huku ikihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali na wananchi.

Kabla ya kuanza kwa ibada ya kuaga mwili wa Hayati Job Yustino Ndugai ilitanguliwa na ratiba ya kuwasili kwa Waombolezaji, Viongozi katika viwanja hivyo na baadaye kufuatiwa na nyimbo za maombolezo kutoka Wasanii na Vikundi mbalimbali wakiwemo Vijana wa Kigogo, Mrisho Mpoto, Peter Msechu, Starah Thomas, Linah Sanga, Kwaya ya Bunge na Kwaya ya Kanisa la Anglikana.

Mara baada ya Rais Samia kuwasili katika Viwanja vya Bunge, mwili wa Hayati Job Ndugai uliingizwa katika eneo ambalo lilikuwa limeandaliwa kwa ajili ya ibada ya kumuaga.

Mara baada ya kumalizika kwa ibada kumalizika Viongozi mbalimbali walitoa salamu za rambirambi akiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju ambapo amesema kuwa, kwa upande wa Mahakama Hayati Ndugai atakumbukwa kwa sifa yake ya kuwa mpenda haki.

“Nimepata fursa ya kumtambua Spika Ndugai nilipokuwa Katibu Binafsi wa Waziri wa Katiba na Sheria wa wakati huo Hayati Mhe. Bakari Mwapachu na sababu ya kumfahamu alihitaji sana kujengwa kwa Mahakama pale Kongwa, kwahiyo akawa anakuja na Waziri kuomba Mahakama ya Wilaya ijengwe katika Kongwa badala ya wananchi kwenda Mpwapwa na baadaye Mahakama hiyo ilijengwa,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema kuwa, alishirikiana pia na Hayati Ndugai katika uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kibaigwa na baadaye katika tukio la kuzinduliwa kwa Mahakama ya Wilaya Kondoa wakati huo Jaji Mkuu akiwa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma.

“Kwetu sisi Mahakama, tutaendelea kumuenzi Hayati Ndugai kwa sababu ya mchango wake wa kupenda sana haki, vilevile nitamkumbuka Mhe. Ndugai pamoja Mhe. Anne Makinda kwa ushirikiano walionipatia nilipokuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali,” ameeleza Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu ameongeza kuwa, wakati wa uzinduzi wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050, moja ya vitu ambavyo Rais Samia alisema kuhusu Mahakama ya Tanzania ni kwamba Mhimili huo uendelee kutenda haki kwa kuzingatia viapo bila hofu, upendeleo, huba wala chuki.

“Kama mtakavyokumbuka moja ya vipaumbele vya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Tanzania 2050 ni haki, nawashukuru watumishi wa Mungu kwa kutuombea na kutambua mchango wetu sisi Mahakimu na Waamuzi kwamba tuendelee kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia viapo vyetu,” amesema Mhe. Masaju.

Aidha, Jaji Mkuu amewapa neno la faraja familia ya Hayati Ndugai na waombolezaji kwa ujumla kuwa, kila binadamu anapoondoka anaacha pengo na pigo ambalo halizibiki kwa kuwa kila mtu ni wa kipekee na ana utambulisho wake, hivyo ni vyema kuendelea kuishi kwa kutokuumia zaidi kwakuwa kuna maisha baada ya kifo kama wasemavyo viongozi wa dini.

Viongozi wengine walioambatana na Jaji Mkuu ni pamoja na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Amour Said Khamis, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Manyara, Mhe. Nenelwa Mwihambi na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Mbali na Jaji Mkuu, Viongozi wengine waliohudhuria katika ibada hiyo ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango, Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Doto Mashaka Biteko, Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Bunge, Mhe. William Lukuvi, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule na viongozi wengine.

Hayati Job Yustino Ndugai anatarajiwa kupumzishwa kwenye makazi yake ya milele kesho tarehe 11 Agosti, 2025 wilayani Kongwa.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akisaini Kitabu cha Maombolezo alipowasili katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma leo tarehe 10 Agosti, 2025 kwa ajili ya kushiriki kwenye ibada ya kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (wa sita kulia) pamoja na Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwa katika Ibada ya kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai. Wa pili kulia ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akitoa salamu za rambirambi wakati wa Ibada ya Kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai leo tarehe 10 Agosti, 2025 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitoa neno wakati wa Ibada ya Kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai leo tarehe 10 Agosti, 2025 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Viongozi wa Dini ya Anglikana wakiongoza Ibada ya Kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai leo tarehe 10 Agosti, 2025 katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.


Picha mbalimbali za waombolezaji walioshiriki kwenye ibada ya kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai iliyofanyika leo tarehe 10 Agosti, 2025 kwenye Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisaini Kitabu cha Maombolezo alipowasili katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma leo tarehe 10 Agosti, 2025 kwa ajili ya kushiriki kwenye ibada ya kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel 
akisaini Kitabu cha Maombolezo alipowasili katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma leo tarehe 10 Agosti, 2025 kwa ajili ya kushiriki kwenye ibada ya kumuaga Spika Mstaafu wa Bunge la Tanzania, Hayati Job Yustino Ndugai.









 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni