Jumatatu, 11 Agosti 2025

WATUMISHI 59 WA MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA WATEMBELEA JENGO LA MAKAO MAKUU

 Na. Innocent Kansha, Mahakama

Watumishi wapatao 59 wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma Mhe. Fahamu Mtulya walifanya ziara ya kutembelea Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma ili kujionea uzuri wa jengo hilo ambalo ni la sita Dunia kwa majengo ya kimahakama.

Katika ziara hiyo ya kimafunzo iliyofanyika tarehe 10 Agosti, 2025 ilitanguliwa na ziara ya watumishi hao iliyofanyika Zanzibar mnamo tarehe 8 Agosti, 2025, kisha Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam na kuhitimisha katika jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Watumishi hao walipata wasaa wa kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo historia ya Mahakama namna ya uendeshaji wa shughuli mbalimbali za Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu Masijala Kuu na zile za Makao Makuu ya Mahakama.

Aidha, watumishi walipata wasaa wa kuona na kujifunza shughuli mbalimbali zinazofanyika katika chumba cha mifumo ya kutolea taarifa muhimu za Mahakama (Judiciary Situation Room). Taarifa mbalimbali za Mahakama ambazo husaidia moja kwa moja mipango na mikakati ya namna bora ya kuboresha huduma kwa wananchi katika mchakato wa upatikanaji haki kwa ujumla.

Chumba hicho maalumu kinahusika kitaalumu kuzalisha, kuchambua, kuchakata, kusimamia na kutoa taarifa mbalimbali maalumu kwa ajili ya kuonesha na kutoa taarifa ya shughuli zinazoendelea moja kwa Mahakama zote nchini.

Vilevile, chumba hicho kinasimamia kuendesha na kuhakikisha usalama na upatikanaji wa mtandao wa Mahakama sambamba na ufuatiliaji wa miundombinu ya mawasiliano kwa ajili ya usimamizi mzuri wa rasilimali za TEHEMA, alisema Afisa TEHAMA Bw. Razaro Sanga.

Watumishi hao walihitimisha ziara yao kwa kutembelea Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania na kupokea maelezo ya jinsi kituo hicho kinavyotoa huduma kwa wananchi kwa muda wa masaa 24 kwa siku saba za wiki na kuchakata taarifa mbalimbali za wateja.

Kituo kinapokea taarifa mbalimbali ikiwemo malalamiko, pongezi, maswali mbalimbali ya huduma zinazotolewa mahakamani na hata nje ya Mahakama na kuzitolea ufafanuzi ili kumpa mwananchi au mdau uelewa mpana wa taratibu mbalimbali na njia sahihi za kufuata kutatua kero kwa wakati.     












































Hakuna maoni:

Chapisha Maoni