Jumatatu, 11 Agosti 2025

WATUMISHI MAHAKAMA MOROGORO WATEMBELEA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA DODOMA

Na ARAPHA RUSHEKE –Mahakama, Dodoma

Jumla ya Watumishi 100 wa Mahakama Kanda ya Morogoro jana tarehe 10 Agosti, 2025 walitembelea jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania  jijini Dodoma ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa utendaji kazi na uboreshaji wa huduma ya utoaji haki.

Watumishi hao waliambatana nabaadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, akiwemo Jaji Mfawidhi, Mhe. Rose Ebrahimu. Baada ya kuwasili katika jengo hilo, watumishi hao walipata fursa ya kuona maeneo mbalimbali ya Makao Makuu ya Mahakama na kuona vitu mbalimbali vilivyomo katika jengo hilo.

Akizungumza mara baada ya kujionea mandhari mbalimbali ya jengo hilo, Mhe. Ebrahimu alisema, “Niliona ni fahari kwamba watumishi wote wa Morogoro waje kushuhudia sehemu hii na kupata moyo na ari ya kuijua na kuielezea historia ya Mahakama pamoja na mapinduzi makubwa ya uboreshaji uliofanyika.’’ 

Alisema pia kuwa ni vema watumishi pia wakafahamu tulipotoka, tupo wapi na tunakoelekea na kwanini tunatakiwa kufanya kazi kwa bidii na kwa uadilifu ili kuendana na kasi ya Mahakama kwa sasa ya Mahakama mtandao.

Jaji Mfawidhi alitoa rai kwa watumishi wengine kutembelea Makoa Makuu hayo ya Mahakama kwani kuna vitu vingi vya kujifunza na kufahamu kwa undani zaidi.

Naye Jaji wa Mahakama Kuu Morogoro, Mhe Aisha Ally Sinda alionesha kufurahishwa na mabadiriko  hayo na ameshauri watumishi wengine kwenda kujionea nini kinaendelea katika Makao Makuu hayo ya Mahakama.

Ziara hiyo ililenga kujifunza kuhusu utekelezaji wa majukumu ya kimahakama, mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA, uboreshaji mbalimbali wa huduma kwa wananchi pamoja na kubadilishana uzoefu katika utendaji kazi wa kila siku.

Baada ya ziara yao, watumishi hao walionesha kufurahishwa na uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama na kuipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kufanikisha kazi hiyo.

Waliahidi kutumia maarifa waliyoyapata kuboresha huduma kwa wananchi wa Morogoro kupitia Mahakama zao.

Watumishi wa Mahakama Kuuya Tanzania, Kanda ya Morogoro wakiongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Rose Ebrahimu (katikati mstari wa mbele) wakiwa katika picha ya pamoja walipotembelea Makao Makuu ya Mahakama yaliyopojJijini Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahimu [aliyevaa kofia nyekundu] akifurahia jambo wakati walipotembelea Makao Makuu ya Mahakama Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahimu akiongea jambo wakati wa ziara hiyo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakiwa katika picha ya pamoja.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahimu (wa kwanza kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro Mhe Aisha Ally Sinda walipotembelea Makao Mkuu ya Mahakama Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni