Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.
George Masaju ametoa rai kwa Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA) kupigania haki za watu wote kwa usawa bila
kubagua baadhi ya makundi kwa kuwa kila raia wa Kitanzania ni sawa na ana haki
zinazotambulika kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mhe. Masaju alitoa rai hiyo tarehe 12 Septemba, 2025 alipokuwa akizungumza na Wanachama kutoka TAWLA waliomtembelea
ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Akitoa ufafanuzi kuhusu suala la usawa wa binadamu,
Jaji Mkuu alinukuu Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
ambayo inasema, ‘watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki bila ubaguzi
wowote kulindwa kupata haki sawa mbele ya sheria.” Hata waasisi wa Taifa
letu walipokuwa wakiandaa nembo ya taifa, walizangatia usawa ndio maana kuna
bibi na bwana na wote wawili ukiwaangalia kwenye nembo ile wanaonekana kushika
rasilimali za taifa pasipo ubaguzi.
Mhe. Masaju alisema huku akirejea Ibara ndogo
ya 4 ya Ibara ya 13 ya Katiba ambayo inasema, ‘ni marufuku kwa mtu yoyote kubaguliwa na mtu au
mamlaka yoyote inayotekeleza madaraka yake chini ya sheria yoyote katika
utekelezaji wa kazi au shughuli yoyote ya mamlaka hizo.’
Jaji Mkuu amenukuu, ‘Ibara ya 8 ya Katiba
pamoja na mengine inazungumza jinsi Serikali inavyopatikana na lengo kuu la
Serikali litakuwa ni ustawi wa wananchi na Serikali itawajibika kwa wananchi.’
Amesema wananchi wanaozungumziwa kwenye Ibara hiyo ni Raia wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ambao ni wanawake na wanaume na kwa tofauti za umri wao
ambapo kuna wazee, watoto, wavulana na wasichana na kwamba hao wote ni watu
ambao haki zao zinapaswa kuzingatiwa.
Mhe. Masaju aliongeza kuwa, ‘Ibara ya 9
pamoja na mengineyo inasema, mamlaka ya nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika
kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha kuwa; a) Utu
na haki nyinginezo zote za binadamu zinaheshimiwa na kuthaminiwa b) Sheria za
nchi zinalindwa na kutekelezwa.’
Aidha, Jaji Mkuu aliitaka TAWLA kuainisha
sheria na kanuni ambazo wanaona sio rafiki na zinazokiuka haki za binadamu ili
ziwezwe kuwasilishwa kwa Watoa Uamuzi ili ziweze kufanyiwa kazi.
“Kama kuna sheria au kanuni ambazo sio rafiki
au ni za kibaguzi kwa makundi mbalimbali ikiwemo wanawake, watoto mziainishe
kwa sababu Mahakama ndio imepewa jukumu la kulinda haki,” alisema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju alieleza kwamba, Mahakama
inatekeleza majukumu yake ipasavyo bila kujali aina ya mtu anayepewa huduma,
hivyo amesisitiza kwa kueleza kwamba, “kama
kuna mambo yanafanyika mahakamani ambayo yanaathiri labda kutekelezwa kwa haki
za wanawake au za watoto hayo yatakuwa ni madhaifu ya mhusika mmoja mmoja
binafsi lakini sio msingi wa Mahakama.”
Alisisitiza kuwa, Mahakama haitafanya
upendeleo wa aina yoyote kwa kundi lolote la watu bali itaendelea kutimiza
majukumu yake ya utoaji haki kwa mujibu wa Katiba na Sheria za nchi.
“TAWLA mna mchango mkubwa wa kuishauri
Mahakama, kwahiyo mnapokuja mahakamani, mnapaswa mjiandae vizuri kuishauri
Mahakama ili kufikia maamuzi sahihi,” alisisitiza Jaji Mkuu.
Kadhalika, Mhe. Masaju alikipongeza chama
hicho kwa kuendelea kutetea haki na kukitaka kuendelea kutoa elimu ya sheria
kwa wananchi na kutetea zaidi haki za binadamu. Aliwashauri
kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi
Maalum na vilevile Wizara nyingine katika kutekeleza malengo ya kuanzishwa kwa
TAWLA kwa ustawi wa Watanzania.
Akisoma taarifa mbele ya Jaji Mkuu kuhusu
Chama hicho, naye Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania
(TAWLA), Bi. Tike Mwambipile aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa uboreshaji wa
huduma za kiutendaji ikiwa ni pamoja na matumizi ya Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano (TEHAMA), maboresho ya Kanuni na Sheria, Uboreshaji wa Miundombinu,
Usuluhishi wa migogoro na kuondoa Mahabusu wa Mahakama za Mwanzo Magerezani.
“Tunachukua fursa hii kuipongeza Mahakama kwa
hatua kubwa zilizochukuliwa katika maboresho ya kiutendaji, imefanya maboresho
makubwa katika matumizi ya teknolojia, usikilizwaji wa mashauri ya njia ya
video/mtandao hatua ambayo imesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza malalamiko ya
wananchi na kurahisisha upatikanaji wa huduma za kimahakama,” alisema Bi. Tike.
Hata hivyo, Mkurugenzi huyo alitaja baadhi ya
changamoto wanazokabiliana nazo kuwa ni pamoja na utekelezaji wa mashauri
yaliyoamriwa na Mahakama kutoheshimika ambapo amesema, “kuna baadhi ya kesi
ambazo maamuzi ya Mahakama hayaheshimiwi na kutekelezwa kwa wakati jambo ambalo
linaweza kuathiri imani ya umma kwa mfumo wa haki na kupunguza ufanisi wa
vyombo vya utoaji haki.
Bi. Tike alieleza kuwa, changamoto nyingine
wanayokabiliana nayo ni katika Mfumo wa Kielektroniki wa Ufunguaji wa mashauri
(e-filling) hususani kwenye mashauri ya mirathi hasa kwa wateja wao wa msaada
wa kisheria, ukatili dhidi ya wanawake na Watoto, unyang’anyaji wa mali za
wanawake na wazee hususani vijijini.
“Tozo kwenye Mabaraza ya Ardhi kwa wateja wa
msaada wa kisheria, hii ni changamoto nyingine, tunaomba ushirikiano wako ili
kuangalia namna ya kuondoa tozo hizi kwa wateja wanaopata msaada wa kisheria na
kama inawezekana wajumuishwe kwenye orodha ya wanaosamehewa ada za Mahakama,” alisema
Mkurugenzi huyo.
Kadhalika, Chama hicho kimeiomba Mahakama
kukisaidia kupata vitendea kazi kama kompyuta na vinginevyo katika baadhi ya
Ofisi zake na katika Madawati ya Msaada wa Kisheria ambayo yapo katika baadhi
ya Mahakama.
Mara baada ya kupokea taarifa hiyo, Jaji Mkuu
alikiri kupokea pongezi na changamoto zilizowasilishwa na kuwataka kuandaa
taarifa ambayo itajumuisha yote waliyowasilisha na kuzungumza ili Mahakama ione
namna ya kuyafanyia kazi.
Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA) ni shirika lisilokuwa la kiserikali (NGO) lililoanzishwa mwaka 1989 kwa lengo la kutetea na kuendeleza haki za kisheria na kikatiba za wanawake. Dira ya TAWLA ni kuhamasisha jamii, kulinda na kutetea haki za wanawake.
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akizungumza na Wanachama wa Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania waliomtembelea tarehe 12 Septemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mazungumzo yakiendelea...
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA), Bi. Tike Mwambipile akizungumza jambo walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania tarehe 12 Septemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni