Jumatano, 8 Oktoba 2025

LINDENI NA KUENDELEZA IMANI YA WANANCHI WALIYONAYO KWA MAHAKAMA; JAJI KIONGOZI

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewataka Mahakimu Wakazi Wapya kufanya kazi kwa kuzingatia misingi ya uadilifu huku akisisitiza kuwa uadilifu ndio msingi wa kujenga na kuendeleza imani ya wananchi kwa Mahakama.

Akizungumza jana tarehe 07 Oktoba, 2025 wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Mahakimu Wakazi Wapya 89 iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Dkt. Siyani alisema kuwa, uadilifu unajenga na kukuza imani ya Umma kwa Mahakama na katika kuhakikisha hilo amewataka kuwa waadilifu, kuishi kiapo walichoapa ili waendelee kuwa Mahakimu wenye weledi kwa kufanya kazi kwa kuzingatia haki bila upendeleo.

"Sifa ya Hakimu pamoja na uwezo wa kufanya kazi ni uadilifu, hakimu mzuri ni yule ambaye anaweza kufanya kazi yake ya uhakimu lakini ni muadilifu na uadilifu wa Hakimu una faida nyingi pamoja na kukupa baraka, lakini uadilifu unajenga na kukuza imani ya Umma kwa Mahakama," alisema Jaji Kiongozi.

Mhe. Dkt. Siyani aliwahimiza Mahakimu hao kuwa watakapofika kwenye vituo vyao vya kazi kila mmoja atoe mchango wake katika kutekeleza na kulinda imani ya Umma kwa Mahakama kwa lengo la kuhakikisha wanakuwa sehemu ya kulinda heshima na hadhi ya Mahakama nchini.

"Mimi niwaase sana kila mmoja wetu atakapokwenda kwenye kituo atakachopangiwa siyo tu kuhakikisha kwamba anajenga na kukuza hiyo Imani bali anaiendeleza hiyo imani ambayo ipo lakini pia anajiuliza kila wakati haya ninayoyafanya, yanaiweka Mahakama katika taswira ipi, hilo ni jambo la muhimu sana, jipimeni mchango wenu katika kujenga, kukuza na kuendeleza imani ya Umma kwa Mahakama," alisema Jaji Kiongozi.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani aliwakumbusha Mahakimu hao kuwa Tanzania ni nchi inayoongozwa kwa mujibu wa Katiba, Sheria na maelekezo ya viongozi, hivyo ni lazima kila mmoja afanye kazi kwa kuzingatia misingi hiyo bila kuingiliwa na ushawishi wa kisiasa au kikundi chochote na kuwaasa wasigeuze Mahakama kuwa chombo cha  kisiasa na wasijiunge na vikundi vya uaharakati na kueleza kuwa ziko namna za kufikisha kero  na changamoto  hivyo ni vyema Mahakimu wakatumia njia hizo.

“Msigeuze Mahakama kuwa chombo cha kisiasa, msigeuze Mahakama kuwa sehemu ya kufanyia harakati zozote zile, tunazo sheria na tunao utamaduni, usijiunge kwenye vikundi vya harakati ziko namna za kufikisha kero na manung'uniko yetu zitumieni," alisema Jaji Kiongozi.

Mafunzo hayo yanaendeshwa kwa lengo la kuwajengea Mahakimu wapya uwezo wa kiutendaji, kimaadili na kisheria kabla ya kuanza kazi rasmi katika vituo mbalimbali vya kazi nchini.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akitoa neno la utangulizi wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Mahakimu Wakazi wapya jana tarehe 07 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

 Sehemu ya Mahakimu Wakazi wapya wakifuatilia kinachojiri wakati wa ufunguzi wa Mafunzo Elekezi yanayotolewa kwao baada ya kula kiapo cha kufanya kazi hiyo.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania walioshiriki kwenye hafla ya ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Mahakimu Wakazi wapya jana tarehe 07 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wa kwanza kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu ambaye pia ni Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Imani Aboud, wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, anayefuatia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba

Sehemu ya Mahakimu Wakazi wapya wakifuatilia kinachojiri wakati wa hafla ya Mafunzo Elekezi yanayotolewa kwao baada ya kuapishwa rasmi kushika wadhifa huo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni