Alhamisi, 4 Desemba 2025

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA KANDA YA IRINGA YAKETI

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Menejimenti ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa imefanya kikao kwa njia ya Video ili kutathmini utendaji kazi wa masuala mbalimbali ya Mahakama katika Kanda hiyo.

Mkutano huo ulifanyika jana tarehe 03 Desemba, 2025 na kuhudhuriwa Wajumbe kutoka Mahakama Kuu Iringa, Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe ambapo Mwenyekiti wa kikao hicho alikuwa ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Ndunguru aliwasisitiza Mahakimu wa Kanda hiyo kubaini mashauri ya Mlundikano huku akiwataka Mahakimu wapange mikakati ya kumaliza mashauri hayo pamoja na kuainisha sababu za kwanini mashauri hayo yamekuwa ya mlundikano.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi huyo alisisitiza umuhimu wa kutumia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) hasa kwa upandishaji wa Mashauri ya Majaji kwenye mfumo wa TanzLII ambapo alisema, “huu ni mwezi wa mwisho wa mwaka inatakiwa mashauri   yote yaliyosomwa hukumu yapandishwe kwenye Mfumo wa TanzLII.”

Pamoja na hilo, Jaji Ndunguru alizungumzia kuhusu suala la uthibiti wa  vitu vitakavyoleta hatari ambapo ni mchakato wa kutambua, kutathmini na kuchukua hatua ili kupunguza au kuthibiti hatari zinazoweza kuathiri utendaji kazi.

Kadhalika, Mwenyekiti wa Kikao hicho, Mhe. Ndunguru aligusia suala la mashauri ya Mahakama ya Rufani kwa kuyafanyia kazi haraka pindi taarifa ya kusudio la kufungua rufaa litakapowasilishwa Mahakamani.

 Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa alizungumzia tukio la Maadhimisho ya miaka 20 ya Mahakama Kuu Kanda ya Iringa ambalo maandalizi yake yanaendelea kufanyika pamoja na uwepo midahalo ya elimu ya sheria kuanzia tarehe 08 -12 Desemba, 2025 kwa njia ya Redio na Vyombo mbalimbali vya Habari.

Amesema kilele cha maadhimisho hayo itakuwa tarehe 15 Desemba, 2025 ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt.  Mustapher Mohamed Siyani.

Katika kikao hicho taarifa mbalimbali za utekelezaji wa majukumu ziliwasilishwa, taarifa hizo ni pamoja na taarifa ya Mkoa Njombe iliyosomwa na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Bw. Richard Mbambe, taarifa ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa iliyosomwa na Afisa Utumishi wa Mahakama hiyo, Bw. Noel Shayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan  Ndunguru (katikati) akizungumza na wajumbe waliohudhuria kwenye kikao cha Menejimenti ya Kanda hiyo (hawapo katika picha) kilichofanyika jana tarehe 03 Desemba, 2025. Kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan  Ndunguru  (aliyeketi mbele kushoto) pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa  wakisikiliza hoja zilizokuwa zinaibuliwa na wajumbe wakati wa kikao cha Menejimenti ya Mahakama Kanda ya Iringa kilichofanyika jana tarehe 03 Desemba, 2025.

 Mtendaji wa Mahakama ya Mkoa Njombe, Bw. Richard Mbambe (aliyeketi mbele kushoto) karibu na video akisoma taarifa ya utekelezaji wa kazi za Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe. Walioketi pamoja naye ni Wajumbe walioshiriki katika kikao hicho wakisikiliza taarifa hiyo.

 Picha ya juu na chini ni wajumbe wa Kikao cha Menejimenti kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Iringa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa  Njombe wakiwa kwenye kikao hicho wakijadiliana mambo mbalimbali kwa kutumia mfumo wa TEHAMA yaani njia ya Mkutano mtandao (Video Conference) katika kuwasilisha hoja mbalimbali zilizokuwa zinatolewa.

 (Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni