Ijumaa, 16 Januari 2026

MAHAKAMA GEITA YANG’ARA UTOAJI TUZO ZA TMJA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, imeibuka kinara kwenye Tuzo 16 zilizoandaliwa na kutolewa na Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [TMJA] jana tarehe 15 Januari, 2026 kwa matawi mbalimbali ya Mahakama ya Tanzania.

Tuzo hizo zilitolewa kwa washindi kwenye chakula cha jioni kilichoandaliwa na TMJA kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma, baada ya kutambua mchango waliouonesha kwa Chama hicho kwa mwaka 2024 na 2025.

Mahakama Kanda ya Geita iling’ara kwenye tukio hilo baada ya kuzoa jumla ya Tuzo nne, ikiwemo ya Mlezi Bora, ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina.

Tuzo ya kwanza Kanda hiyo kunyakua ilihusu utambuzi wa kuwa Mahakama ya mfano na ya kwanza Tanzania kwa kuachana na matumizi ya karatasi [paperless court] kwenye shughuli zote za kimahakama.

Aidha, Kanda ya Geita ilikabidhiwa pia Tuzo ya tawi bora katika michezo, nyingine ya tawi bunifu kwa ujumla na Tuzo ya tawi bora zaidi kwa mwaka 2025.

Kwa upande mwingine, Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, nayo ilikabidhiwa Tuzo maalum kwa ubunifu wa kuendesha mafunzo mengi nchi nzima kupitia ufadhiri wa wadau mbalimbali.

Tunzo nyingine zilizotolewa na matawi ya Mahakama kwenye mabano ni tawi bora katika mafunzo [Mbeya], tawi bora katika ubunifu wa vyanzo vya fedha [Arusha] na tawi bora katika utalii [Morogoro].

Utoji wa Tuzo hizo kwa matawi hayo ulitanguliwa na Tuzo maalum zilizotolewa kwa Viongozi Wakuu wa Mahakama ya Tanzania. Tuzo ya kwanza katika kundi hilo maalum ilitolewa kwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.

Tuzo ya pili ilitolewa kwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, ya tatu kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Tuzo ya nne ikatolewa kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Wakati wa hafla hiyo, zilitolewa pia Tuzo za mwaka 2024, Songwe kama tawi bora bunifu vyanzo vya fedha, Mtwara na Lindi kama tawi bora katika mafunzo na Mahakama ya Rufani na Masjala Kuu kama tawi bora katika michezo.

Utoaji wa Tuzo hizo ulikuwa sehemu ya Mkutano Mkuu wa Mwaka wa TMJA uliokuwa unafanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkutano huo ulifunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 13 Januari, 2026. Jumla ya wanachama wa TMJA 1,200 walihudhuria Mkutano huo, ambao ni wa pili kufunguliwa na Mkuu wa Nchi tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 1984. 

Chama cha JMTA ni cha kitaaluma chenye malengo mbalimbali, ikiwemo kukuza na kulinda uhuru wa Mahakama kama sharti la msingi na la lazima la utekelezaji wa majukumu ya kimahakama.

Malengo mengine ni kukuza maslahi na ustawi wa wanachama, kudumisha hadhi, heshima na tamaduni za Majaji na Mahakimu, kuongeza na kuendeleza ujuzi, maarifa na uelewa wa Majaji na Mahakimu kuhusu majukumu yao ya kimahakama kupitia tafiti endelevu na elimu ya kitaaluma.

Mengine ni kutoa taarifa na machapisho mbalimbali kuhusu masuala yenye maslahi au yanayowahusu wanachama, kuandaa makongamano na mikutano ya wanachama na kudumisha mahusiano ya karibu kadri inavyowezekana miongoni mwa wananchama na kushirikiana, na inapobidi, kujiunga na vyama au Taasisi nyingine zenye malengo yanayofanana.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju [kulia] akimkabidhi Tuzo ya tawi bora zaidi kwa mwaka 2025 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina.

Shangwe likitawala baada ya Mahakama Kanda ya Geita kutangazwa washindi wa Tuzo ya tawi bora kwa mwaka 2025.

Picha ya pamoja baada ya kutangazwa tawi bora kwa mwaka 2025.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju [kushoto] akipokea Tuzo yake kutoka kwa Rais wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania, Mhe. Elimo Masawe.  

Picha chini akionesha Tuzo yake.
  

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani [kushoto] akipokea Tuzo yake.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akionesha Tuzo yake.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani [kulia] akimkabidhi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina Tuzo baada ya kutangazwa Mlezi Bora. 


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina [kushoto] akipokea Tuzo 
kwa ubunifu wa kuendesha mafunzo mengi nchi nzima kupitia ufadhiri wa wadau mbalimbali. 

Picha chini zinaonesha matukio mbalimbali wakati wa utoaji wa Tuzo hizo.










Maoni 1 :

  1. Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [TMJA] je! Chama cha wasio mahakimu na Weshimiwa Majaji kinaiteje???
    yaani namanisha Non-Judiciary

    JibuFuta