Jumamosi, 7 Februari 2026

KIKAO CHA MENEJIMENTI MBEYA CHA KETI NA KUSISITIZA MAADILI KWA WATUMISHI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga amewaasa wajumbe kuhusiana na suala la kuzingatia maadili kwa watumishi wote wa Mahakama na kusema suala la maadili siyo la Mahakimu pekee bali linahusu watumishi wote hata wasio Mahakimu.

Akifungua kikao hicho cha menejimenti Mkoa wa Mbeya kilichofanyika tarehe 04 February, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Tiganga alisema “tuyaishi maadili kwa kadiri kazi zetu zinavyotutaka kwa kuzingatia sheria na kanuni za kiutumishi na si vinginevyo ili kujenga imani ya wananchi tunaowahudumia tunapokuwa kwenye majukumu yetu ya kila siku,”

Aidha, Mhe. Tiganga alisistiza kwamba, suala la maadili siyo kwa Mahakimu pekee ni kwa watumishi wote hata watumishi wasio Mahakimu, nawasisitiza ninyi kama viongozi nanyi mkawasisitize watumishi walio chini yenu kuzingatia maadili ya kiutumishi ili kuboresha utendaji kazi wa Mahakama.

Mhe. Tiganga aliongeza kuwa Mahakimu wote katika Vituo vyao kuweka mikakati imara ya kumaliza mashauri kwa wakati na kuhakikisha kuwa wanamaliza kabisa mashauri ya mlundikano mapema iwezekanavyo hasa katika Mahakama za mwanzo.

“Tuendelee kuchapa kazi na tuongeze bidii kwenye usikilizaji wa mashauri na tuhakikishe kuwa katika masijala zetu tumemaliza kabisa mashauri ya mrundikano,”alisema Mhe. Tiganga

Vilevile, kikao hicho kilitumika kujadili mapitio ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027. Akiwasilisha taarifa hiyo Afisa Bajeti ambaye ni Afisa Rasilimali Watu Mahakama Kuu Mbeya Bi. Sarah Lossi katika mapitio hayo ya bajeti alizungumzia kuhusu hali ya rasilimali watu, fedha, hali ya majengo na hali ya bajeti ya Mwaka wa fedha 2025/2026.

Aidha, Bi. Sarah aliongeza kuwa, changamoto katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 ni nyingi ambazo zinatakiwa kukabiliwa, mikakati na muelekeo wa bajeti ya mwaka 2026/2027 ambapo alieleza juu ya majukumu na vipaumbele yaliyopangwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027

Kikao hicho pia kilijadili taarifa ya utendaji kazi kwa robo ya pili ya mwaka 2025/2026 Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, katika taarifa iliyowasilishwa na Afisa Utumishi Mahakama Kuu Mbeya Bw. Moses Luoga alitoa taarifa ya rasilimali watu, usimamizi wa rasilimali fedha, hali ya mashauri, taarifa ya matumizi ya mifumo ya TEHAMA, Utoaji wa elimu kwa umma na hali ya majengo mbalimbali ya Mahakama mkoa wa Mbeya.

Vilevile, kulitolewa mrejesho kuhusu taarifa za Mirathi kutoka katika kila Wilaya za Mkoa wa Mbeya, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama zote za Wilaya waliwasilisha taarifa za mirathi kutoka katika Wilaya zao.

Akiwasilisha taarifa za Mirathi Mjumbe kutoka Wilaya ya kyela Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. James Mhanusi alisema kuwa, mikakati iliyowekwa ili kupunguza na kumaliza kabisa bakaa ya fedha katika akaunti ya mirathi wilayani Kyela.

“Tumefanya jitihada kubwa kupambana na bakaa ya fedha ya mirathi katika Mahakama zetu kwa kufanya vipindi redioni na tumepata fursa kwenye redio kufanya kipindi kimoja kila wiki kutoa elimu kwa wananchi kuhusu elimu ya mirathi na kuwaomba wananchi kufuatilia mirathi yao mahakamani,” alinukuliwa Mhe. Mhanusi

Aidha kikao hicho pia kilijadili kuhusu taarifa ya upatikanaji na upimaji wa viwanja, Pamoja na hatua iliyofikiwa katika kulinda mipaka ya Mahakama ili kufikia lengo la Mahakama ya Tanzania lililokusudia kupeleka huduma ya Mahakama hadi kwenye ngazi ya kata

 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (Katikati) akiongoza kikao cha menejimenti Mkoa wa Mbeya, kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti wakiwa kwenye kikao hicho.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (Katikati) akiongoza kikao cha menejimenti Mkoa wa Mbeya, kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti wakiwa kwenye kikao hicho.

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Mmoja wa wajumbe akizungumza jambo katika kikao hicho (aliyesimama) Afisa utumishi Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Odilia Mapunda

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni