- Ashiriki maadhimisho
jubilee miaka 20 Kanda ya Iringa, ahimiza uwajibikaji
- Asema kuanzishwa Mahakama
Kuu Iringa kumesogeza huduma za haki kwa umma
Na FAUSTINE
KAPAMA-Mahakama, Iringa
Kaimu Jaji Kiongozi na
Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ametoa wito kwa Majaji,
Mahakimu na Watumishi wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa kujituma,
kuzingatia misingi ya maadili na kutumia teknolojia kwa ufanisi.
Mhe. Aboud ametoa wito
huo leo tarehe 15 Desemba, 2025 kwenye maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 20 tangu
kuanzishwa kwa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa. Maadhimisho hayo
yamehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama na Serikali na wananchi lukuki
wa Mkoa wa Iringa.
Kadhalika, Kaimu Jaji
Kiongozi amewasihi Wadau wote katika mnyororo wa utoaji haki na wananchi kwa
ujumla, kushirikiana na Mahakama kupunguza ucheleweshaji wa mashauri na
kuendelea kuwa sehemu ya uboreshai wa utoaji haki kwa kutoa mrejesho wa wazi.
Kwa upande wa Serikali,
Mhe. Aboud amewasihi Viongozi katika ngazi mbalimbali kuhamasisha wananchi
kutumia vyombo vya haki badala ya kujichukulia sheria mkononi.
Akizunguzia maadhimisho
hayo, Amidi wa Mahakama Kuu ameeleza kuwa hatua hiyo ni kumbukumbu muhimu
katika historia ya utoaji haki nchini, ni safari iliyojaa juhudi, changamoto na
mafanikio ambayo kwa pamoja wameyaona na kuyaishi.
‘Mafanikio na changamoto
tulizokutana nazo iwe ni fursa kwetu ya kubuni na kuweka mikakati thabiti
katika kutekeleza wajibu wetu wa kikatiba wa utoaji haki kwa umma wa
Watanzania…
“Ni wazi kuwa, safari ya
utoaji wa huduma za haki kwa umma bado inaendelea, pamoja na mazingatio ya
Katiba, Sheria na Kanuni katika utekelezaji wetu wa majukumu ya kila siku,
tuendelee kuishi katika viapo vyetu vya kazi pamoja na salamu yetu ya Mahakama
ambayo inasisitiza katika uadilifu, weledi na uwajibikaji,’ Mhe. Aboud amesema.
Amewapongeza na
kuwashukuru watumishi wa ngazi zote wa Mahakama waliopitia Kanda hiyo tangu
kuanzishwa kwake kwa jitihada na mchango wao katika kuijenga taswira nzuri ya
Mahakama ya Tanzania.
Kaimu Jaji Kiongozi
ameeleza kuwa kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa ilikuwa ni moja ya
hatua muhimu katika kusogeza huduma za haki kwa umma wa Watanzania.
Ameeleza kuwa kabla ya
kuanzishwa kwa Kanda hiyo, kulikuwepo na Mahakama Kuu Kanda ya Songea
iliyoanzishwa mwaka 1992 na kuanzia mwaka hadi 1999, Kanda ya Songea
ilijumuisha na kutoa huduma kupitia Mahakama zote za Mkoa wa Iringa.
‘Ilipofika mwaka 2000,
Mahakama zote za Mkoa wa Iringa zilienguliwa kutoka Mahakama Kuu Kanda ya
Songea na kuwekwa chini ya Kanda ya Mbeya kwa tangazo la Serikali Na.
162/2000,’ amesema.
Mhe. Aboud amebainisha
kuwa juhudi za dhati zilifanyika kufuatia changamoto walizokuwa wanapitia
wananchi kutoka Mkoa wa Iringa waliokuwa wakitafuta haki zao mahakamani,
ikiwemo kusafiri umbali mrefu kufuata huduma ya Mahakama sambamba na matumizi
ya muda na gharama.
Ameeleza kuwa Serikali
ilitoa majengo yaliyokuwa yakitumika kama kiwanda cha kuchakata Almasi (TUNCUT)
Iringa, ambayo yalikarabatiwa na kuwa majengo ya kutolea huduma za Mahakama kwa
ngazi tofauti, kwa maana ya Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama
ya Wilaya.
Majengo hayo
yalizinduliwa tarehe 22 Novemba, 2005 na Rais wa Awamu ya tatu, Hayati Benjamin
Mkapa. Shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Iringa zilianza rasmi mnamo mwaka 2006
baada ya Jaji Mfawidhi kutoka Kanda ya Dodoma kuhamishiwa Iringa pamoja na
watumishi kutoka maeneo mbalimbali ya Mahakama ya Tanzania.
Akizungumza kwenye
maadhimisho hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe.
Dunstan Ndunguru ameeleza kuwa Kanda hiyo ilianzishwa mwaka 2005, ikiwa ni
sehemu ya mpango wa Mahakama ya Tanzania wa kusogeza huduma karibu na wananchi
ili kupunguza umbali na gharama za kufuata haki katika Mikoa ya Iringa na
Njombe.
Amesema kuwa wakati
inaanzishwa, kulikuwepo na Jaji mmoja na idadi ndogo ya watumishi wasiozidi 30
katika ngazi mbalimbali, jengo kuu lilikuwa dogo, lenye uwezo mdogo wa
kuhudumia idadi kubwa ya wananchi, mashauri yaliyofunguliwa kwa mwaka yalikuwa
wastani wa mashauri 250 hadi 300 na hapakuwa na matumizi ya Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano [TEHAMA] katika uendeshaji wa mashauri.
“Katika kipindi cha miaka
20 tumepiga hatua kubwa na zinazooneka kwa uwazi katika maeneo makuu mawili;
miundombinu na huduma kwa wananchi na usikilizaji wa mashauri na maboresho ya
mifumo ya utoaji haki,” Mhe. Ndunguru amesema.
Kuhusu miundombinu, Jaji
Mfawidhi ameeleza kuwa katika miaka 20 wamejenga msingi imara wa miundombinu ya
kimahakama na kufanya uboreshaji ili kusogeza huduma karibu na wananchi, pamoja
na kufanya mazingira ya kazi kuwa rafiki kwa Wadau wa Mahakama.
Kupitia uboreshaji huo,
jumla ya majengo 20 yamejengwa kwa kutumia fedha za ndani na ufadhili wa Benki
ya Dunia na kwa kushirikiana na Wadau wa Mahakama Kanda ya Iringa, ikiwemo
Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Njombe ambacho ujenzi wake upo mbioni kukamilika.
Kuhusu TEHAMA, Jaji
Mfawidhi ameeleza kuwa katika miaka 20, wameingia katika zama za matumizi ya
TEHAMA kwani wamewezesha watumishi kumiliki mfumo wa usimamizi wa mashauri
(JoT-eCMS) katika uendeshaji wa mashauri, mfumo wa usikilizaji mashauri kwa
njia ya mtandao, ambao unasaidia mdau kusikiliza shauri hata akiwa ndani ya
nchi ama nje ya nchi, mfumo tumizi wa Mahakama za Mwanzo na mifumo mingine
mingi.
Aidha, Jaji Mfawidhi
ameeleza kuwa kutokana na kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, kasi ya
umalizaji wa mashauri imekuwa ikiongezeka siku hadi siku na hii ni kwa sababu
huduma zinapatikakana karibu, watuishi wa Mahakama wanatoa huduma wakiwa hapa
hapa Iringa kwa kutumia nguvu kazi iliyopo.
“Hii imethibitishwa na
viwango tofauti tofauti vya mashauri yaliyokuwa yakifunguliwa na kumalizika
tangu 2006 hadi Octoba, 2025. Kwa mfano kwa mwaka, 2006 mashauri
yaliyofunguliwa Mahakama Kuu yalikuwa 37, yaliyoaamriwa yalikuwa saba. Kwa
mwaka, 2005 Januari hadi octoba, 2025 yalifunguliwa 551 na yaliyoamriwa
yalikuwa ni 454. Kwa mwaka, 2006 hadi 0ktoba, 2025 mashauri yalitofunguliwa
Mahakama Kuu Kanda yalikuwa 4,953 na kati ya hayo mashauri 4,289 yamemalizika,”
amesema.
Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud [juu na chini] akizungumza kwenye maadhimisho ya jubilei ya miaka 20 tangu kuanzisha kwa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku, akitambulisha wageni mbalimbali kwenye maadhimisho hayo.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, akiratibu matukio mbalimbali wakati wa maadhimisho hayo.
Meza Kuu inayoongzwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Mstaafu, waliohudhuria maadhimisho hayo. Picha chini ni Msajili wa Mahakama Kuu, Mtendaji wa Mahakama Kuu na Naibu Wasajili.
Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Dini na Mila wa Mkoa wa Iringa. Picha chini ni Watendaji na Wakuu wa Vitengo kutoka Mahakama mbalimbali na Makao Makuu.
Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili na Mahakimu wa Mahakama Kanda ya Iringa.
Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu nyingine ya Mahakimu wa Mahakama Kanda ya Iringa [juu na chini].
Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama [juu na chini].
Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Mawakili wa Serikali [juu] na Mawakili wa Kujitegemea [chini].
Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama [juu na chini].