Jumatatu, 15 Desemba 2025

WAJUMBE WA TAASISI YA MAFUNZO YA UANASHERIA KWA VITENDO WAKUTANA NA JAJI MKUU

  • Wajadiliana juu ya utoaji wa elimu bora ya Sheria

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 15 Desemba, 2025 amekutana na kufanya mazungumzo na Wajumbe wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (LST), waliomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Jijini Dodoma.

Mazungumzo hayo yamelenga kuhakikisha utoaji wa elimu bora ya sheria, upatikanaji wa mikopo na upatikanaji wa fursa kwa vijana kusoma Shule ya Sheria kwa vitendo.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (LST) mara baada ya mazungumzo yaliyofanyika leo tarehe 15 Desemba, 2025, ofisini kwa Jaji Mkuu jijini Dodoma.
 
Sehemu nyingine ya wajumbe wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (LST) wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (wa nne kulia) mara baada ya mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwa Jaji Mkuu jijini Dodoma.  Wa tatu kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba, wa nne kushoto ni Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno (kushoto)  na wa kwanza kulia ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert. 

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akipokea nakala ya kitabu kutoka kwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno (kushoto). Kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza jambo wakati wa mazungumzo kati yake na Wajumbe wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo yaliyofanyika leo tarehe 15 Desemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.


Sehemu ya wajumbe wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo wakisikiliza kwa makini hoja zilizokuwa zikitolewa wakati wa mazungumzo kati ya Wajumbe wa Taasisi hiyo na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju yaliyofanyika leo tarehe 15 Desemba, 2025 kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akimsikiliza kwa makini Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba alipokuwa akichangia hoja wakati wa kikao cha mazungumzo na Wajumbe wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo yaliyofanyika Ofisini kwa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Picha na HABIBA MBARUKU & JEREMIA LUBANGO, Mahakama)


 

 

 

 

 



 

WITO MUHIMU WA AMIDI MAHAKAMA KUU TANZANIA KWA VIONGOZI WA MAHAKAMA, SERIKALI

  • Ashiriki maadhimisho jubilee miaka 20 Kanda ya Iringa, ahimiza uwajibikaji
  • Asema kuanzishwa Mahakama Kuu Iringa kumesogeza huduma za haki kwa umma

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa

Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ametoa wito kwa Majaji, Mahakimu na Watumishi wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, kuzingatia misingi ya maadili na kutumia teknolojia kwa ufanisi.

Mhe. Aboud ametoa wito huo leo tarehe 15 Desemba, 2025 kwenye maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa. Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama na Serikali na wananchi lukuki wa Mkoa wa Iringa.

Kadhalika, Kaimu Jaji Kiongozi amewasihi Wadau wote katika mnyororo wa utoaji haki na wananchi kwa ujumla, kushirikiana na Mahakama kupunguza ucheleweshaji wa mashauri na kuendelea kuwa sehemu ya uboreshai wa utoaji haki kwa kutoa mrejesho wa wazi.

Kwa upande wa Serikali, Mhe. Aboud amewasihi Viongozi katika ngazi mbalimbali kuhamasisha wananchi kutumia vyombo vya haki badala ya kujichukulia sheria mkononi.

Akizunguzia maadhimisho hayo, Amidi wa Mahakama Kuu ameeleza kuwa hatua hiyo ni kumbukumbu muhimu katika historia ya utoaji haki nchini, ni safari iliyojaa juhudi, changamoto na mafanikio ambayo kwa pamoja wameyaona na kuyaishi.

‘Mafanikio na changamoto tulizokutana nazo iwe ni fursa kwetu ya kubuni na kuweka mikakati thabiti katika kutekeleza wajibu wetu wa kikatiba wa utoaji haki kwa umma wa Watanzania…

“Ni wazi kuwa, safari ya utoaji wa huduma za haki kwa umma bado inaendelea, pamoja na mazingatio ya Katiba, Sheria na Kanuni katika utekelezaji wetu wa majukumu ya kila siku, tuendelee kuishi katika viapo vyetu vya kazi pamoja na salamu yetu ya Mahakama ambayo inasisitiza katika uadilifu, weledi na uwajibikaji,’ Mhe. Aboud amesema.

Amewapongeza na kuwashukuru watumishi wa ngazi zote wa Mahakama waliopitia Kanda hiyo tangu kuanzishwa kwake kwa jitihada na mchango wao katika kuijenga taswira nzuri ya Mahakama ya Tanzania.

Kaimu Jaji Kiongozi ameeleza kuwa kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa ilikuwa ni moja ya hatua muhimu katika kusogeza huduma za haki kwa umma wa Watanzania.

Ameeleza kuwa kabla ya kuanzishwa kwa Kanda hiyo, kulikuwepo na Mahakama Kuu Kanda ya Songea iliyoanzishwa mwaka 1992 na kuanzia mwaka hadi 1999, Kanda ya Songea ilijumuisha na kutoa huduma kupitia Mahakama zote za Mkoa wa Iringa.

‘Ilipofika mwaka 2000, Mahakama zote za Mkoa wa Iringa zilienguliwa kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Songea na kuwekwa chini ya Kanda ya Mbeya kwa tangazo la Serikali Na. 162/2000,’ amesema.

Mhe. Aboud amebainisha kuwa juhudi za dhati zilifanyika kufuatia changamoto walizokuwa wanapitia wananchi kutoka Mkoa wa Iringa waliokuwa wakitafuta haki zao mahakamani, ikiwemo kusafiri umbali mrefu kufuata huduma ya Mahakama sambamba na matumizi ya muda na gharama.

Ameeleza kuwa Serikali ilitoa majengo yaliyokuwa yakitumika kama kiwanda cha kuchakata Almasi (TUNCUT) Iringa, ambayo yalikarabatiwa na kuwa majengo ya kutolea huduma za Mahakama kwa ngazi tofauti, kwa maana ya Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya.

Majengo hayo yalizinduliwa tarehe 22 Novemba, 2005 na Rais wa Awamu ya tatu, Hayati Benjamin Mkapa. Shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Iringa zilianza rasmi mnamo mwaka 2006 baada ya Jaji Mfawidhi kutoka Kanda ya Dodoma kuhamishiwa Iringa pamoja na watumishi kutoka maeneo mbalimbali ya Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza kwenye maadhimisho hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru ameeleza kuwa Kanda hiyo ilianzishwa mwaka 2005, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Mahakama ya Tanzania wa kusogeza huduma karibu na wananchi ili kupunguza umbali na gharama za kufuata haki katika Mikoa ya Iringa na Njombe.

Amesema kuwa wakati inaanzishwa, kulikuwepo na Jaji mmoja na idadi ndogo ya watumishi wasiozidi 30 katika ngazi mbalimbali, jengo kuu lilikuwa dogo, lenye uwezo mdogo wa kuhudumia idadi kubwa ya wananchi, mashauri yaliyofunguliwa kwa mwaka yalikuwa wastani wa mashauri 250 hadi 300 na hapakuwa na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA] katika uendeshaji wa mashauri.

“Katika kipindi cha miaka 20 tumepiga hatua kubwa na zinazooneka kwa uwazi katika maeneo makuu mawili; miundombinu na huduma kwa wananchi na usikilizaji wa mashauri na maboresho ya mifumo ya utoaji haki,” Mhe. Ndunguru amesema.

Kuhusu miundombinu, Jaji Mfawidhi ameeleza kuwa katika miaka 20 wamejenga msingi imara wa miundombinu ya kimahakama na kufanya uboreshaji ili kusogeza huduma karibu na wananchi, pamoja na kufanya mazingira ya kazi kuwa rafiki kwa Wadau wa Mahakama.

Kupitia uboreshaji huo, jumla ya majengo 20 yamejengwa kwa kutumia fedha za ndani na ufadhili wa Benki ya Dunia na kwa kushirikiana na Wadau wa Mahakama Kanda ya Iringa, ikiwemo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Njombe ambacho ujenzi wake upo mbioni kukamilika.

Kuhusu TEHAMA, Jaji Mfawidhi ameeleza kuwa katika miaka 20, wameingia katika zama za matumizi ya TEHAMA kwani wamewezesha watumishi kumiliki mfumo wa usimamizi wa mashauri (JoT-eCMS) katika uendeshaji wa mashauri, mfumo wa usikilizaji mashauri kwa njia ya mtandao, ambao unasaidia mdau kusikiliza shauri hata akiwa ndani ya nchi ama nje ya nchi, mfumo tumizi wa Mahakama za Mwanzo na mifumo mingine mingi.

Aidha, Jaji Mfawidhi ameeleza kuwa kutokana na kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, kasi ya umalizaji wa mashauri imekuwa ikiongezeka siku hadi siku na hii ni kwa sababu huduma zinapatikakana karibu, watuishi wa Mahakama wanatoa huduma wakiwa hapa hapa Iringa kwa kutumia nguvu kazi iliyopo.

“Hii imethibitishwa na viwango tofauti tofauti vya mashauri yaliyokuwa yakifunguliwa na kumalizika tangu 2006 hadi Octoba, 2025. Kwa mfano kwa mwaka, 2006 mashauri yaliyofunguliwa Mahakama Kuu yalikuwa 37, yaliyoaamriwa yalikuwa saba. Kwa mwaka, 2005 Januari hadi octoba, 2025 yalifunguliwa 551 na yaliyoamriwa yalikuwa ni 454. Kwa mwaka, 2006 hadi 0ktoba, 2025 mashauri yalitofunguliwa Mahakama Kuu Kanda yalikuwa 4,953 na kati ya hayo mashauri 4,289 yamemalizika,” amesema.

Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud [juu na chini] akizungumza kwenye maadhimisho ya jubilei ya miaka 20 tangu kuanzisha kwa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku, akitambulisha wageni mbalimbali kwenye maadhimisho hayo.


Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, akiratibu matukio mbalimbali wakati wa maadhimisho hayo.


Meza Kuu inayoongzwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Mstaafu, waliohudhuria maadhimisho hayo. Picha chini ni Msajili wa Mahakama Kuu, Mtendaji wa Mahakama Kuu na Naibu Wasajili.


Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Dini na Mila wa Mkoa wa Iringa. Picha chini ni Watendaji na Wakuu wa Vitengo kutoka Mahakama mbalimbali na Makao Makuu.


Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili na Mahakimu wa Mahakama Kanda ya Iringa.

Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu nyingine ya Mahakimu wa Mahakama Kanda ya Iringa [juu na chini].


Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama [juu na chini].

Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na Mawakili wa Serikali [juu] na Mawakili wa Kujitegemea [chini].


Meza Kuu inayoongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama [juu na chini].



 

  

MAHAKAMA KUU KANDA YA IRINGA YAWEKA HISTORIA

  • Yaadhimisha Jubilei ya miaka 20 tangu kuanzishwa
  • Ndiyo Kanda ya kwanza kuweka historia hiyo ya Mahakama Tanzania

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, leo tarehe 15 Desemba, 2025 imeweka historia ya kipekee baada ya kuadhimisha jubilei ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwake mwaka 2005.

Tukio hilo linaifanya Mahakama Kuu Iringa kuwa ya kwanza kati ya Kanda 20 za Mahakama Kuu Tanzania kuadhimisha jubilei tangu zianzishwe. Hatua hiyo imepongezwa na Viongozi wengi waliohudhuria maadhimisho hayo, akiwemo Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud.

Kanda nyingine za Mahakama Kuu zilizopo kwa sasa ni Dar-es-Salaam, Morogoro, Temeke,Tanga, Moshi, Arusha, Manyara, Mwanza, Bukoba, Geita, Shinyanga, Dodoma, Tabora, Sumbawanga, Kigoma, Mbeya, Songea, Mtwara na Musoma.

Maadhimisho hayo yaliyofanyika kwenye viunga vya Mahakama hiyo, maarufu kama 'Uwanja wa Haki' yamehudhuriwa na Mhe. Aboud na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Kanda mbalimbali.

Viongozi wengine wa Mahakama waliohudhuria maadhimisho hayo ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, kwa niaba ya Msajili Mkuu na Mtendaji wa Mahakama Kuu, kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Majaji wastaafu, Naibu Wasajili, Watendaji wa Mahakama, Mahakimu na watumushi wengine wengi wa Mahakama Kanda ya Iringa.

Kwa upande wa Serikali alikuwepo Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama Mkoa na Mawakili wa Serikali. Wengine waliohudhuria maadhimisho hayo ni Wabunge, Madiwani, Viongozi wa Dini na wananchi kwa ujumla.

Viongozi mbalimbali walipata nafasi ya kutoa salamu kwenye maadhimisho hayo. Katika salamu zake, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James, amewapongeza watumishi wa Mahakama kwa kuadhimisha miaka 20 tangua kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa.

Amesema kuwa maadhimisho hayo yanawakumbusha umuhimu na wajibu wa kuzisimamia, kuzipigania na kuhakikisha haki za wananchi zinatolewa wakati wote.

“Sisi wote tunafahamu, umoja, mshikamano, amani na maendeleo yetu ni matunda ya haki. Kwa msingi huo, tunaendelea kuwajibika kama wananchi, viongozi na watumishi ndani ya Mkoa wa Iringa kuhakikisha Taasisi hii muhimu iliyopewa mamlaka ya kikatiba kutafsi na kutoa haki kwa wananchi tunailinda, tunaitetea na kuiwezesha kufanya wajibu huu wa msingi ili haki iweze kutamalaki katika jamii yetu,” amesema.

Mkuu wa Mkoa ametumia fursa hiyo kuwahimiza wananchi kuipa ushirikiano Mahakama pale kesi zinazopoanza ili wanapohitajika mahakamani kutoa ushahidi wajitokeze ili kurahisisha mchakato wa haki .

Naye Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika, Mkoa wa Iringa, Wakili Msomi Moses Ambindwile, amesema kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa imeandika na inaendelea kuandika historia ya kipekee katika utoaji haki na ujenzi wa uongozi wa Mahakama ya Tanzania.

Wakili Msomi Ambindwile amebainisha pia kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa imekuwa mithiri ya Chuo Kikuu cha Uongozi nchini kwa kutoa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Mkuye, Mhe. Rehema Kerefu, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi.

Kwa mujibu wa Wakili Msomi, wapo pia Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dunstan Ndunguru, Mhe. David Ngunyale, Mhe. Ruth Massam, Mhe. Isaya Arufani, Mhe. Augustine Rwizile, Mhe. Gladys Barthy, Mhe. Cyprian Mkeha, Mhe. Martha Mpaze na Mhe. Victoria Nongwa.

“Lakini pia imewahi kutoa Jaji Viongozi wawili, Mhe. Fakih Jundu na Mhe. Dkt. Feleshi na Wanasheria Wakuu wa Serikali wawili, Mhe. Fredrick Welema na Mhe. Dkt. Feleshi, ambao wamewahi kufanya kazi hapa Kanda ya Iringa,” amesema.

Ameeleza kuwa wao kama TLS wataendelea kusimama bega kwa bega na Mahakama kwa maslahi ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Wakati wa maadhimisho hayo kulifanyika uzinduzi wa Jarida la Mahakama Kanda ya Iringa linaloitwa, "Uwanja wa Haki " ambao ulifanywa na Mhe. Aboud. Jarida hilo limesheheni makala mbalimbali zinazoelezea historia ya Mahakama Kanda ya Iringa, shughuli za usikilizaji wa mashauri na utendaji kwa ujumla na andiko la kusisimua la chimbuko la Mahakama ya Mwanzo Kalenga iliyopo kwenye Makumbusho ya Taifa ya Kalenga ya Chifu Mkwawa.

Burudani za ngoma, bendi na kwaya ya Mahakama Kanda ya Iringa zimepamba maadhimisho hayo. Kikundi cha Ngoma Kibate kinachocheza na Nyoka aina ya Chatu kimekonga nyoyo za wananchi waliokuwa wamefurika kwenye viunga hivyo vya Mahakama. Kulifanyika pia igizo la mfano wa namna Mahakama inavyofanya kazi wakati wa kuendesha mashauri.

Kabla ya Mahakama Kuu Kanda ya Iringa kuanzishwa mwaka 2005, shughuli za kimahakama katika Mkoa wa Iringa na Njombe zilikuwa zinafanyika katika Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.

Meza Kuu ikiongozwa na Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud ikifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa maadhimisho ya jubilei ya miaka 20 tangu Mahakama Kuu Kanda ya Iringa kuanzishwa mwaka 2005. Picha chini ikiimba Wimbo wa Taifa na ule wa Afrika Mashariki.


 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James akiwasilisha salamu kwenye maadhimisho hayo. Picha chini ni Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika, Mkoa wa Iringa, Wakili Msomi Moses Ambindwile.


Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Jarida la Mahakama Kanda ya Iringa kwenye maadhimisho hayo. Picha chini akionesha kwa wananch Jarida hilo.



Kaimu Jaji Kiongozi na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud, akikata keki kwenye maadhimisho hayo.

Mahakimu wa ngazi mbalimbali wa Mahakama Kanda ya Iringa [juu na chini] wakifuatilia kilichokuwa kinajiri.



Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Iringa na wananchi wakiwa kwenye maadhimisho hayo.


Sehemu nyingine ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Iringa [juu na chini] wakiwa kwenye maadhimisho hayo.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Victoria Nongwa, akisakata ngoma kwenye maadhimisho hayo. Picha chini ni fundi wa kucheza na nyoka hatari, Chatu, kwenye ngoma mbalimbali.


Bendi ya Mahakama Kanda ya Iringa ikitumbuiza kwenye maadhimisho hayo.

Kwaya ya Mahakama Kanda ya Iringa [juu na chini] ikilishambulia jukwaa kwenye maadhimisho hayo.



Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Iringa wakionesha mfano namna Mahakama inavyoendesha shughuli za kusikiliza kesi.

Ijumaa, 12 Desemba 2025

MCHANGO WA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA BIASHARA KWENYE UKUAJI UCHUMI, UFANISI KIBIASHARA

  • Yarejesha kwenye mzunguko wa fedha bilioni 11 za Kitanzania kila mwezi

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, imefanikiwa kurejesha kwenye mzunguko wa fedha wastani wa kiasi cha Shilingi za Kitanzania bilioni 11 kila mwezi kwa mwaka wa 2025.

Hayo yamebainishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, kwenye hotuba iliyowasilishwa kwa niaba yake na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud, kwenye uzinduzi wa Mwongozo wa Uendeshaji wa Mashauri ya Biashara uliofanyika leo tarehe 12 Desemba, 2025 jijini Dar es Salaam.

‘Hizi fedha zinatokana na mashauri ambayo uamuzi wake umekamilika hadi utekelezaji. Ninaposema Mahakama ya Biashara ipo kwa ajili ya kuwezesha miamala ya kibiashara, itekelezwe kwa ufanisi ninamaanisha hiyo. Taarifa za Mahakama hii zinathibitisha eneo la ukuaji wa uchumi na ufanisi wa biashara nchini,’ Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kwenye hotuba yake.

Jaji Kiongozi ameeleza kuwa urejeshaji wa kiasi kikibwa cha fedha hizo kwenye mzunguko wa fedha ni tafsiri kuwa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara imechangia katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya mwaka 2025-2050 inayolenga kuboresha maisha ya wananchi pamoja na kuongeza imani ya wananchi, wafanyabiashara na wawekezaji kwa Mahakama ya Tanzania.

 Ameeleza kuwa anafahamu pia kuwa kuanzia katikati ya mwezi Octoba hadi Novemba, 2025, Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara ilikuwa na vikao maalum vya usikilizaji mashauri, ambapo jumla ya mashauri ya kibishara yaliyoamuliwa  ni 96 yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania 65,964,979,029/04, Dola za Kimarekani 10,195,592,01 na Euro 172,892.

‘Taarifa nilizozipokea kutoka kwa Jaji Mfawidhi ni kwamba mashauri haya yalisikilizwa kama yalivyopangwa kwa  zaidi ya asilimia 90,’ sehemu ya hotuba ya Jaji Kiongozi inaeleza.

Ameeleza kuwa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara imeamua kutoa mwongozo huo kwa kutambua kuwa mashauri ya kibiashara yanapaswa kusikilizwa na kuamriwa mapema ipasavyo na kuzingatia weledi unaoakisi kwa usahihi ujuzi kwenye eneo husika la mgogoro na kwa kutambua kuwa si wengi walio na maarifa sahihi kwenye ushughulikiaji wa mashauri ya kibiashara.

Kwa mujibu wa Jaji Kiongozi, licha ya mwongozo huo kushughulika na mashauri ya kibiashara, ni imani yake kuwa utanufaisha Wadau wengi, hata kwenye mashauri mengine ya madai kwa kuwa mashauri ya kibiashara ni mashauri ya madai pia.

‘Kwa sababu hiyo, taratibu za uendeshaji wa mashauri ya kibiashara zinashabihiana na taratibu za uendeshaji wa mashauri mengine ya madai, ingawa kuna tofauti za hapa na pale,’ Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Kwa upande mwingine, Jaji Kiongozi amesema kuwa Mwongozo huo utakuwa rejea nzuri kwa vijana waliopo kwenye Shule ya Sheria kwa Vitendo na Vyuo Vikuu kwa mambo mbalimbali wanayojifunza. Kadhalika, Wahadhiri na Watafiti mbalimbali wa ndani na nje ya nchi pia watanufaika na maarifa yaliyomo ndani ya Mwongozo huo.

Akizungumzia chimbuko la Mwongozo huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, ameeleza kuwa pamoja na uboreshaji ambao umefanyika kwenye maeneo mbalimbali, nyenzo na vitendea kazi vilivyopo kwa sasa katika eneo la haki madai haviwezeshi Maofisa Mahakama, Mawakili na Wadau wenye mashauri mahakamani hapo kufanya mambo kwa wepesi.

Amesema kuwa hali hiyo inatokana na upekee wa migogoro ya kibiashara ambao utatuzi wake wakati mwingine unaweza kuhitaji maarifa ya ziada yasiyopatikana kwenye vitendea kazi vilivyopo. Mhe. Mkeha ametaja sababu nyingine ni mabadiliko ya namna njia za ufanyaji biashara zinavyobadilika kwa kasi kutokana na kukua kwa teknolojia ulimwenguni.

Hivyo, Mhe. Mkeha ameishukuru Benki Kuu ya Tanzania, hususan Gavana wa Benki Kuu Emmanuel Tutuba kwa kufanikisha kwa kiasi kikubwa uandishi, uhariri na uzalishaji wan akala 100 za Mwongozo huo.

 Ameahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uaminifu na kasi itakayowezesha kurudi kwa fedha zinazoshikiliwa, kwa sababu ya uwepo wa mashauri katika Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, kwenye mzunguko wa uchumi.

‘Tutafanya hivyo kwa kuharakisha ukazaji wa tuzo tunazozitoa, eneo ambalo Benki imeliwekea pia mkazo katika fedha ambazo imezitoa kwa Divisheni ya Biashara katika mwaka huu wa fedha wa 2025/2026. Kwa kufanya hivyo, Mahakama itakuwa imechangia ukuaji wa uchumi na kuwa kivutio cha uwekezaji nchini,’ amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA] na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, akiwasilisha neno lake wakati wa uzinduzi huo, amepongeza ushirikiano kati ya Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara na Benki Kuu, ambao umefanikisha kupatikana kwa Mwongozo huo.

Ameeleza kuwa wao kama Chuo, ambao kazi yao ni kufundisha na kuwajengea weledi na uwezo Majaji na Majaji katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku, watautumia Mwongozo huo kama nyenzo ya kufundishia na ameahidi kuenedeleza ushirikiano uliopo kati ya IJA na Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara kwenye eneo la mafunzo.

Uzinduzi wa Mwongozo huo umehudhuriwa na Viongozi mbalimbali, wakiwemo Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu, Msajili wa Mahakama Kuu, Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni, Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama, Wahadhiri wa Vyuo, Mawakili wa Serikali na Kujitegemea, Wadau na watumishi wa Divisheni ya Biashara.

Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud, akiwasilisha hotuba kwa niaba ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, kwenye uzinduzi wa Mwongozo wa Uendeshaji wa Mashauri ya Biashara uliofanyika leo tarehe 12 Desemba, 2025 jijini Dar es Salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, akieleza kwa kifupi chimbuko la Mwongozo huo.

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA] na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa Mwongozo huo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Joyce Minde akitambulisha wageni mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo.

Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani. Picha chini ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria uzinduzi huo.


Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji na Viongozi Waandamizi wa Mahakama Kuu Divisnehi ya Biashara. Picha chini ni wajumbe wa kamati iliyofanikisha utayarishaji wa Mwongozo huo.


Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama kutoka Makao Makuu Dodoma. Picha chini Wadau waliohudhuria hafla hiyo.


Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama Kuu. Picha chini ni Mawakili na Wadau mbalimbali waliohudhuria uzinduzi huo.


Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara [juu na chini] waliohudhuria uzinduzi huo.