Alhamisi, 2 Mei 2024

UJENZI WA KITUO JUMUISHI LINDI WAIVA

Na Hilaly Lorry – Mahakama, Lindi

Mkandarasi kutoka kampuni ya Rizvi Engineering Ltd amekabidhiwa eneo kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Mradi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Lindi.

Makabidhiano hayo yalifanyika hivi karibuni huku yakushuhudiwa na Mkuu wa Kitengo cha Majengo cha Mahakama ya Tanzania Mhandisi Moses Lwiva na Mkandarasi Mshauri Mhandisi Bw. Amri Mumba kutoka kampuni ya Usanifu wa Majengo ya Y & P (T) Ltd na viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi.

Mwenyekiti wa kikao hicho Bw. Amri Mumba alieleza kuwa ujenzi wa mradi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Lindi utachukua miezi tisa (9) hadi kukamilika na unatarajiwa kuanza rasmi tarehe 09 Mei, 2024 na kukamilika 08 Februari 2025.

Aidha, Bw.  Mumba alisisitiza mambo mbalimbali ikiwemo jinsi ya kuratibu taka zinazozalishwa wakati wa zoezi la ujenzi na kuwataka kutafuta namna bora yakuweza kuziharibu taka hizo ili zisilete madhara kwa watu wanaozunguka eneo hilo la mradi.

Kwa upande wake, Mhandisi Moses Lwiva alimtaka Mkandarasi kujisajili kwa wakala wa usalama na afya mahala pa kazi (OSHA).Vilevile kuzingatia sheria zote za usalama kwa mafundi na watu watakao fika eneo la mradi kwani mradi huo ni wa Benki ya Dunia huku akiwapa angalizo kuwa Benki ya Dunia wanazingatia  usalama mahali pa kazi zaidi.

 Mhandisi Mshauri, Mkandarasi na timu nzima walikubaliana kufanya kazi  kwa ushirikiano usiku na mchana kwa lengo la kuhakikisha kuwa zoeli la ujenzi linakamilika kwa muda waliopewa  ili kuwapunguzia gharama wananchi mkoani Lindi  kufuata huduma za kimahakama hasa Mahakama kuu nje ya Mkoa wao.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela na Hakimu mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Singano pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe. Maria Batulaine waliahidi kutoa ushirikiano wa karibu na kufanya mawasiliano na pande zote zinahusika na ujenzi huo kwa lengo la kuhakikisha ujenzi wa mradi huo unakamilika bila mkwamo wowote.

Makabidhiano ya mkataba kwa ajili ya ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Lindi kati ya Mkandarasi kutoka Kampuni ya Rizvi Engineering Ltd Bw.Ali Rivzi na Mkuu wa Kitengo cha Majengo Mahakama ya Tanzania Mhandisi Moses Lwiva kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Mkandarasi kutoka kampuni ya Rizvi Engineering Ltd   akionyeshwa eneo la ujenzi na mipaka yake.

Mkandarasi kutoka kampuni ya Rizvi Engineering Ltd   akionyeshwa eneo la ujenzi na mipaka yake.

Wajumbe wa kikao cha makabadhiano wakifuatia kwa Makini wakati wa kikao.

Mtendji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela (aliyevaa shati jeupe) wakitoa neno la ukaribisho wakati wa kikao cha makabidhiano ya eneo la mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Lindi.


Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Singano (aliyevaa gauni jeusi), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe.Maria Batulaine (aliyevaa suti) wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kikao hicho

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha -Mahakama) 


Jumatano, 1 Mei 2024

WATUMISHI WA MAHAKAMA YA TANZANIA DODOMA WASHIRIKI MAADHIMISHO YA MEI MOSI 2024

Na Arapha Rusheke , Mahakama Kuu Dodoma 

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dodoma na Watumishi wa Makao Makuu ya Mahakama leo tarehe 1 Mei, 2024 wameungana na Watanzania wengine kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi, inayojulikana kama Mei Mosi, inayosherekewa kote duniani.

Maadhimisho hayo ambayo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, yamefanyika katika Uwanja wa Jamhuri katika  Jiji la  Dodoma na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi.

Pilikapilika za maadhimisho hayo zilianza mapema asubuhi ambapo watumishi wa Mahakama waliojitokeza kwa wingi waliungana na wananchi wengine katika eneo la viwanja vya Bunge na baadaye kushiriki kwenye maandamano hadi kwenye Uwanja wa Jamhuri.

Maandamano hayo yaliyoongozwa na Bendi ya Jeshi la Magereza yalipita katika barabara ya Bunge kupitia wimpy  baadaye Uwanja wa Jamhuri na kupokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule.

Mbali na watumishi kupita mbele ya mgeni rasmi kwenye maandamano hayo, magari nayo kutoka taasisi na mashirika mbalimbali ambayo yalipita mbele yake na kupamba sherehe hizo.

Baada ya maandamano hayo, ratiba ya maadhimisho hayo iliendelea, ikiwemo viongozi mbalimbali wa Chama cha Wafanyakazi (TUCTA) na Serikali ya Mkoa walipata nafasi ya kutoa salamu.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mhe. Senyamule amewapongeza wafanyakaizi wote kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye maadhimisho hayo ambayo kwa mwaka huu wa 2024 yamebeba kauli mbiu inayosema, “Nyongeza ya mishahara ni msingi wa mafao bora na kinga dhidi ya hali ngumu ya Maisha.


Sehemu ya watumishi wa Mahakama wa  makao makuu na watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma wakiwa katika maandamano ya Meimosi yaliyofanyika katika uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

 

Sehemu ya watumishi wa Mahakama wa  makao makuu na watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma wakiingia uwanjani Jamhuri Dodoma na kupita jukwaa kuu  katika maandamano ya Meimosi yaliyofanyika Ki Mkoa katika uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

Baadhi ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi bora wa Mahakama Kuu kanda ya Dodoma.


(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam) 

 

 

WATUMISHI MAHAKAMA DAR ES SALAAM WASHIRIKI MAADHIMISHO MEI MOSI 2024

Na FAUSTINE KAPAMA -Mahakama, Dar es Salaam


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam, leo tarehe1Mei, 2024 wameungana na Watanzania wengine kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi, inayojulikana kama Mei Mosi, inayosherekewa kote duniani.

 

Maadhimisho hayo ambayo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila yamefanyika katika Uwanja vya Uhuru jijini hapo na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi.

 

Pilikapilika za maadhimisho hayo zilianza mapema asubuhi ambapo watumishi wa Mahakama waliojitokeza kwa wingi waliungana na wananchi wengine katika eneo la Mnazi Mmoja na baadaye kushiriki kwenye maandamano hadi kwenye Uwanja wa Uhuru.

 

Maandamano hayo yaliyoongozwa na Bendi ya Jeshi la Magereza yalipita katika barabara ya Nyerere, Keko na baadaye Uwanja wa Uhuru na kupokelewa na Mkuu wa Mkoa.

 

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania ndiyo waliokuwa wa kwanza kuingia katika Uwanja wa Uhuru na kushangiliwa kwa nguvu na wananchi waliofurika uwanjani hapo kufuatia kazi nzuri wanayoifanya katika muktadha mzima wa utoaji haki nchini.

 

Mhe. Chalamila aliongoza jukwaa kuu kuwashangilia watumishi wa Mahakama walipokuwa wanapita mbele yake na kupokewa na wananchi wengine waliokuwa wamesimama muda wote.

 

Mbali na watumishi kupita mbele ya mgeni rasmi kwenye maandamano hayo, magari ya Mahakama nayo yalikuwa miongoni kutoka Taasisi na mashirika mbalimbali ambayo yalipita mbele yake, likiwemo gari la Mahakama Inayotembea, ‘Mobile Court’, ambalo lilikuwa kivutio kikubwa kwa wananchi.

 

Baada ya maandamano hayo, ratiba ya maadhimisho hayo iliendelea, ikiwemo viongozi mbalimbali wa Chama cha Wafanyakazi (TUCTA) na Serikali ya Mkoa walipata nafasi ya kutoa salamu.

 

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mhe. Chalamila amewapongeza wafanyakaizi wote kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye maadhimisho hayo ambayo kwa mwaka huu wa 2024 yamebeba kauli mbiu inayosema, “Nyongeza ya mishahara ni msingi wa mafao bora na kinda dhidi yahali ngumu ya maisha.”

 


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam wakijiandaa kushiriki katika maandamano kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani.


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam wakiingia kwenye Uwanja wa Uhuru kushiriki katika maandamano kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani.


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam (juu na chini) wakipita mbele ya jukwa kuu, likiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, Mei Mosi, leo tarehe 1 Mei, 2024 kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.


Jukwa Kuu, likiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila likiwapungia mkono watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam walipokuwa wanapita mbele yake katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ya Tanzania nao hawakubaki nyuma kushiriki kwenye maadhimisho hayo.

Bendi ya Jeshi la Magereza iliyoongoza maandamano hayo ikipita mbele ya mgeni rasmi kwenye Uwanja wa Uhuru.

Sehemu ya magari ya Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam (juu na picha mbili chini) ikipita ndani ya Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kwenye maadhimisho ya Mei Mosi.

 


Sehemu ya Wananchi wa Mkoa wa Dar-es-Salaam (juu na chini) waliojitokeza  kwenye maadhimisho ya Mei Mosi.  

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Dar es Salaam wakiwa katika picha ya pamoja (juu na chini) kabla ya kupanda magari kuelekea kwwenye maadhimisho ya Mei Mosi.



Safari ndiyo inaanza. 

 




 


 


 


 


 


 

Safari kuelekea katika maeneo ya Mnazi Mmoja ndiyo inaanza kushiriki katika maandamano ya kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani.

 

Sehemu ya magari ya Mahakama ya Tanzania yakiwa yamefurika watumishi yakiwasili katika maeneo ya Mnazi Mmoja kabla ya kuanza maandamano hayo.

 

Maandamano yameanzia sasa.

 

Maandamano yamekolea....

 


 

 

Wananchi wakiimba wimbo wa mshikamano katika Uwanja wa Uhuru baada ya maandamano.

 

 

Jumanne, 30 Aprili 2024

MAHAKAMA KUU SONGEA YATOA MAFUNZO YA NDANI KWA WATUMISHI

Na Hasani Haufi- Mahakama, Songea

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, jana tarehe 29 Aprili, 2024 wamepatiwa mafunzo ya ndani kuwajengea uelewa wa mambo mbalimbali, ikiwemo miongozo, kanuni na sheria, stahiki zao  na maadili kwa ujumla.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhe. Nyembele aliwahimiza watumishi wote katika Kanda hiyo kuzingatia yale watakayofundishwa na watoa mada mbalimbali ili kuwa na uelewa wa pamoja.

Watoa mada walikuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea, Mhe. Japhet Manyama, Afisa Utumishi Mahakama Kuu Songea, Bi. Paulina Kapinga, Afisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Bi. Catherine Okum na Afisa Tawala Mahakama ya Wilaya Tunduru, Bw Alex Hotay.

Akiwasilisha mada yake, Mhe. Manyama alihimiza washiriki kama watumishi wa umma kuwa na maadili yanayokubalika kwani Taasisi yoyote huchafuka ikiwa na watu ambao hawana nidhamu.

Sambamba na hilo alieleza kuhusu sheria ya maadili ya Viongozi wa umma, mwongozo wa uendeshaji wa kamati za maadili na kuwapitisha kuhusu Tume ya Utumishi wa Mahakama inavotekeleza majukumu yake.

Naye Bi. Kapinga alitoa mada kuhusiana na ushughulikiaji wa upandishwaji vyeo kwa watumishi, ambapo alieleza sifa zinazoweza kupelekea mtumishi akapanda cheo, muundo wa cheo cha mtumishi husika na mambo mengine.

Kwa upande wake, Bw. Hotay aliwapitisha washiriki kwenye utaratibu wa uombaji wa likizo na ruhusa, aina za likizo na hutolewa kwa wakati na misingi gani ili kwenda na matakwa ya sheria ya za utumishi wa umma.

Bi. Catherine yeye alisisitiza usalama wa data, taarifa na nyaraka na vifaa vya ofisi na usalama wa taasisi kwa ujumla kwa kuzingatia taratibu za kiusalama wa mifumo. 

Mafunzo hayo yalihusisha watumishi wote wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea huku watumishi kutoka Mahakama za Wilaya Nyasa, Mbinga, Namtumbo na Tunduru na wengine walishiriki kupitia njia ya mtandao.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea, Mhe. Japhet Manyama akiwasilisha mada.

Afisa Utumishi, Mahakama Kuu Songea, Bi. Paulina Kapinga, akiwasilisha mada.

Afisa Tawala Mahakama ya Wilaya Tunduru, Bw Alex Hotay akiwasilisha mada kupitia mtandao.


Sehemu ya watumishi (juu na chini) wakifuatilia kwa karibu watoa mada. 

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Bw. Epaphras Tenganamba, akitoa neno kwa washiriki kabla ya kuhitimisha mafunzo hayo. 

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

WATUMISHI WAHIMIZWA KUWA WAMOJA

 

Na. Francisca Swai, Mahakama – Musoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma wahimizwa kuwa wamoja katika utendaji kazi wao kwa kuwa  umoja ndio msingi wa mafanikio katika maeneo ya kazi. 

Hayo yamebainishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya pamoja na Katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara Bw. Hamis Mwisa katika Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo uliofanyika hivi karibuni.

Akifungua mkutano huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya aliwaasa watumishi kutumia nafazi hiyo  kwa umoja wao kusema kwa uwazi changamoto wanazokutana nazo katika kazi ili zifikishwe kwa mwajiri kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi. 

‘‘Miaka ya zamani, nafasi hizi hazikuwepo, mfanyakazi alikuwa hapati nafasi ya kuoongea na mwajiri. Hivyo tutumie fursa hii kufikisha hoja zetu kwa mwajiri, tuongee changamoto na mafanikio yetu kwa umoja na kwa uwazi kuliko kuongelea pembeni. Vikao hivi ndio nafasi ya pekee ya uhuru inayomkutanisha mwajiri na mwajiriwa kwa pamoja ili kujadili masuala mbalimbali ya kuboresha mazingira ya kazi na utendaji kazi kwa ujumla,’’ alisema Mhe. Jaji Mtulya.

Naye Katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara Bw. Hamis Mwisa, alitoa elimu juu ya umuhimu wa vyama vya wafanyakazi, mabaraza ya wafanyakazi na haki na wajibu wa mwajiri na mwajiriwa. Ambapo kupitia elimu hiyo amewaasa watumishi kujiunga na TUGHE kwa wingi ili kuendelea kukipa chama hicho nguvu ya kuwasilisha masuala mbalimbali ya watumishi kwa mwajiri na Serikali kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya watumishi.

Aidha, Mwisa, ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa maboresho makubwa ya mazingira ya kazi hususani miundombinu ya majengo ya Mahakama. Alisema watumishi hawawezi kufanya kazi kwa moyo au kuwa na utendaji kazi mzuri kama hata mazingira ya kazi ni magumu. 

Pamoja na pongezi hizo, Bw. Mwisa, amepongeza pia salamu ya Mahakama isemayo uadilifu, weledi na uwajibikaji. Amewaasa watumishi kuzingatia salamu hiyo kwani imejitosheleza na kila mmoja akiizingatia basi hatutakuwa na migogoro kazini, tutaishi kwa umoja na upendo.

Nao viongozi wa Kanda ya Musoma walioshiriki katika baraza hilo wakiwemo Naibu Wasajili Mhe. Salome Mshasha na Mhe. Monica Ndyekobora pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Leonard Maufi waliwasisitiza watumishi kuzingatia na kutekeleza yaliyojadiliwa na kukubaliana kwa pamoja ili kuboresha utendaji kazi wa Kanda hiyo.

Katika mkutano huo mengi yalijadiliwa. wajumbe walishiriki kikamilifu katika kujadili hoja mbalimbali za kuwasilisha kwa mwajiri pamoja na kusisitiza umoja kati ya watumishi wote.

 Watumishi wakiimba kwa pamoja wimbo wa mshikamano daima wakati wa kufungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma akisema neno la ufunguzi wa baraza hilo na kuwakaribisha wajumbe.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Musoma Bw. Leonard Maufi, akisisitiza jambo wakati wa mkutano huo wa baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.

 Katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara Bw. Hamis Mwisa akiongea akitoa elimu ya vyama vya wafanyakazi, mabaraza ya wafanyakazi pamoja na kujibu hoja mbalimbali katika mkutano wa baraza la wafanyakazi Kanda ya Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma na mwenyekiti wa baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akisisitiza jambo wakati wa baraza hilo. (Kushoto) ni Katibu wa baraza hilo Bw. Kandana Lucas na (kulia) ni Katibu Msaidizi Bi. Farajaa Barakazi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma Mhe. Salome Mshasha akizungumza na kusisitiza jambo wakati wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.



Picha juu na chini ni  baadhi wa wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma wakiongea na kuwasilisha hoja zao katika baraza hilo.


(Habari hii imehaririwa na Magreth Kinabo - Mahakama)


BUNGE LAIDHINISHA BILIONI 441.3 BAJETI YA WIZARA YA KATIBA NA SHERIA NA TAASISI ZAKE

  •    Wabunge waipongeza Mahakama kwa maboresho ikiwemo matumizi ya TTS
  • Wapongeza Uanzishwaji wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki ‘IJCs’

Na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jana tarehe 29 Aprili, 2024 lilipitisha jumla ya fedha za Kitanzania Bilioni 441.3 ikiwa ni bajeti ya Mwaka wa Fedha 2024/2025 ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali ikiwemo Miradi ya Maendeleo ya Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi zilizopo chini yake.  

Akizungumza wakati akiwasilisha Hotuba ya Mipango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hiyo kwa Mwaka wa Fedha 2024/ 2025 katika Mkutano wa 15 wa Bunge unaoendelea jijini Dodoma, Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Mhe. Dkt. Pindi Chana (MB) alisema Wizara hiyo imeendelea kusimamia na kuratibu utekelezaji wa mipango inayolenga kufanikisha jukumu la kuimarisha mifumo ya utoaji haki kwa kuweka mazingira yanayohakikisha usawa kwa wote na kwa wakati.

Mhe. Dkt. Chana alisema Serikali kupitia Wizara imejikita kushughulikia masuala manne muhimu ili haki ipatikane kwa wote na kwa wakati ambayo ni pamoja na kufanya mapitio ya mfumo wa Haki Jinai na kuandaa mpango wa marekebisho ya Sheria ambazo zinatoa mianya ya ama kuchelewesha upatikanaji wa haki au ukandamizaji katika upatikanaji wa haki.

“Katika kuendelea kusimamia upatikanaji wa haki kwa wananchi, Mahakama imeendelea na mpango wa kupunguza mrundikano wa mashauri mahakamani, katika kipindi cha Julai, 2023 hadi Aprili, 2024 Mahakama imeshughulikia jumla ya mashauri 196,592,” alisema Mhe. Dkt. Chana.

Alieleza kuwa, kati ya mashauri hayo, mashauri 133,82 yamesikilizwa na kuhitimishwa na mashauri 62,769 yaliyobaki yanaendelea kusikilizwa.

Aliongeza kwamba, katika mashauri yanayoendelea kusikilizwa, mashauri ya umri mrefu ni 2,087 pekee sawa na asilimia tatu (3) ya mashauri
yote yaliyobaki Mahakamani.

Akizungumzia kuhusu, utekelezaji wa Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Mahakama katika ngazi mbalimbali, hadi kufikia Aprili, 2024, Miradi ya Ujenzi iliyokamilishwa ni Mahakama za Wilaya ya Ulanga, Kwimba na Liwale; Ukarabati wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya
Maswa.

Ujenzi wa Majengo ya Mahakama za Mwanzo Usevya Mlele, Nyakibimbili Bukoba, Mahenge (Kilolo), Newala Mjini, Madale Dar es Salaam, Kinesi Rorya na Luilo Ludewa.

"Majengo ya Mahakama yanayoendelea ama kujengwa au kukarabatiwa ni kama Ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita vya Katavi, Songea Ruvuma, Songwe, Njombe, Simiyu na Geita," alieleza Balozi Mhe. Dkt. Chana.

Waziri huyo alisema ujenzi wa majengo ya Mahakama za Mwanzo tatu ambazo ni Ilangala (Ukerewe), Mbalizi (Mbeya) na Machame (Kilimanjaro).

Miradi mingine ni ujenzi wa majengo ya Mahakama za Wilaya sita (6) ambazo ni Kibiti Pwani, Nachingwea Lindi, Simanjiro Manyara, Hanan’g Manyara, Mbulu Manyara na Tunduru Ruvuma pamoja na Ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Korogwe ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 61, ujenzi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Ubungo ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 98 na ukarabati wa jengo la zamani la Mahakama Kuu Dodoma ambapo ukarabati wake umefikia asilimia 49.

Kadhalika, Waziri huyo alizungumzia kuhusu ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania ambapo hadi sasa umefikia asilimia 97.3 huku akiongeza kuwa, ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kabanga-Ngara unaendelea na kwa sasa upo asilimia 97, ujenzi wa nyumba 48 za Majaji eneo la Iyumbu Dodoma ambao umefikia asilimia 98 na kuendelea kwa ujenzi wa nyumba ya Jaji Mkuu jijini Dodoma ambapo ujenzi umefikia asilimia 53.

Kwa upande mwingine, Waziri Mhe Dkt. Chana alisema katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali imesajili jumla ya watoa huduma 46 walioomba kuthibitishwa kama Watoa Huduma za Utatuzi wa Migogoro kwa njia mbadala, ambapo Waendesha Maridhiano ni watatu (3), Watoa Huduma za Majadiliano watatu (3), Wapatanishi 13 na Wasuluhishi 27.

”Hadi kufikia Aprili, 2024 wapo Watatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala 576, kati ya hao, Waendesha Maridhiano 38, Watoa Huduma za Majadiliano 60, Wapatanishi 185 na Wasuluhishi 293,” alisema Waziri Chana.

Aliongeza kwamba, Serikali inaendelea na taratibu za kuanzisha Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania (Tanzania International Arbitration Centre), Taasisi hiyo itakuwa na Kituo Dar es Salaam ambapo tayari jengo kwa ajili ya kuanzisha Kituo hicho limepatikana.

Akizungumza wakati akichangia bajeti hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu wa Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa matumizi ya Mfumo wa Unukuzi na Tafsiri (TTS).

“Napenda kuipongeza Mahakama kwa hatua kubwa ya kuanza matumizi ya Mfumo wa Unukuzi na Tafsiri (TTS), nipende kuishauri Mahakama kufunga Mfumo huu katika Mahakama zote nchini ili kurahisisha upatikanaji wa Haki,” alisema Mhe. Dkt. Mhagama.

Wabunge mbalimbali wamepata nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria iliyowasilishwa; miongoni mwa maoni na pongezi zilizotolewa ni pamoja na pongezi kwa Mahakama juu ya uanzishwaji wa Vituo Jumuishi vya utoaji Haki (IJCs), uwepo wa Mahakama zinazotembelea (Mobile Courts).

Kati ya Shilingi 441,260,152,000 zilizopitishwa na Bunge, jumla ya fedha za Kitanzania Bilioni 241.6 ni bajeti ya Mfuko wa Mahakama fungu 40. Baadhi ya Taasisi ambazo bajeti yake imesomwa na Wizara ni pamoja na Tume ya Utumishi wa Mahakama, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Mahakama, Tume ya Kurekebisha Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka. 

Katika mwaka wa fedha 2023/2024, Wizara iliidhinishiwa na Bunge jumla ya Shilingi 383,619,511,000 (bilioni 383.62) kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Miradi ya Maendeleo. Kati ya fedha hizo Shilingi 97,815,618,000 (bilioni 97.82) ni kwa ajili ya mishahara ya Watumishi, Shilingi 176,148,324,000 (bilioni 176.15) ni kwa ajili ya matumizi mengineyo na Shilingi 109,655,569,000 (bilioni 109.66) ni kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kati ya fedha za maendeleo Shilingi 44,112,800,000 (bilioni 44.11) ni fedha za ndani na Shilingi 65,542,769,000 (bilioni 65.54) ni fedha za nje.

 

Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Mhe. Dkt. Pindi Chana (MB) akisoma Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi zake tarehe 29 Aprili, 2024 Bungeni jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe., Eva Nkya wakimsikiliza Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Mhe. Dkt. Pindi Chana (MB) akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi zake tarehe 29 Aprili, 2024 jijini Dodoma
Sehemu ya Viongozi wa Wizara ya KJatiba na Sheria pamoja na Taasisi zake wakimsikiliza Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Mhe. Dkt. Pindi Chana (MB) akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi zake tarehe 29 Aprili, 2024 jijini Dodoma

Sehemu ya Viongozi wa Wizara ya KJatiba na Sheria pamoja na Taasisi zake wakimsikiliza Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Mhe. Dkt. Pindi Chana (MB) akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi zake tarehe 29 Aprili, 2024 jijini Dodoma