Alhamisi, 15 Aprili 2021

KAMATI ZA MAADILI ZATAKIWA KUWAELIMISHA WANANCHI MABORESHO YANAYOFANYWA NA MAHAKAMA

 Na Lydia Churi-Mahakama, Arusha        

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewaomba wajumbe wa kamati za Maadili za Mkoa na Wilaya zilizopo mkoani Arusha kufuatilia kwa karibu maboresho yanayofanywa na Mahakama ya Tanzania ili waweze kuwaelimisha wananchi.

Jaji Mkuu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ameyasema hayo alipokuwa akifungua kikao kati ya Tume hiyo na wajumbe wa Kamati za Maadili za Mkoa wa Arusha pamoja na wilaya zake kilichofanyika katika ukumbi wa Hazina Ndogo mjini humo.

“Mahakama imeboresha mambo mengi ambayo wananchi walio wengi hawajapata fursa ya kuwafahamu hivyo mkiwa karibu na Mahakama mtafahamu mengi na kuwaelimisha wananchi”, alisema Jaji Mkuu.

Aliwataka wajumbe wa Kamati za Maadili za mkoa huo na wilaya zake kusoma taarifa mbalimbali zinazohusu maboresho ya Mahakama kupitia machapisho Tovuti ya Mhimili huo pamoja na machapisho mbalimbali yanayotolewa kwa lengo la kutoa elimu ili kuwaongezea ufahamu zaidi wa shughuli za Mahakama hatua itakayowasaidia kutekeleza wajibu wao kwa urahisi na ufasaha.

“Wananchi wengi hawafahamu majukumu ya Tume pamoja na kamati zake na wakati mwingine hujikuta wakiwasilisha malalamiko yanayotakiwa kushughulikiwa na katika mfumo wa kimahakama hivyo wajumbe mkifahamu mipaka ya kazi zenu  mtakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuwaelimisha waelewe na kutofautisha masuala ya kinidhamu nay a kimahakama”, alisisitiza.

Alisema Mahakama imeandaa miongozi kadhaa kwa lugha ya Kiswahili itakayosaidia katika utekelezaji wa majukumu yake, baadhi ya miongozo hiyo ni  mwongozo unaohusu masuala ya Dhamana, wajibu wa Madalali, Utekelezaji wa amri za Mahakama pamoja na ule wa Watumiaji wa huduma za Mahakama.  

Wakati huo huo, Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Iddi Hassan Kimanta amesema mkoa amewashauri wajumbe wa Kamati za Maadili za wilaya mkoani humo kuhakikisha wanajisomea nyaraka mbalimbali za Mahakama zinazohusu majukumu ya kamati zao ili wawe na uelewa mpana na kuwaeleimisha wananchi majukumu ya kamati hizo na namna bora ya kuwasilisha malalamiko yao.

Awali, akizungumza na Jaji Mkuu alipotembelewa na Kiongozi huyo wa Mhimili wa Mahakama ofisini kwake, Mkuu wa mkoa wa Arusha alisema kuwa  migogoro ya kazi imeongezeka mkoani humo na imetokana na athari za ugonjwa wa Covid 19 ambao kwa kiasi kikubwa umeathiri sekta ya Utalii.

Katika hatua nyingine, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye pia ni Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama amesema Mahakama inahuisha Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa majengo yake ili kuweza kuanza ujenzi kwenye maeneo yenye changamoto kubwa zaidi ya  miundombinu ya majengo.

Alisema Mahakama imekamilisha ujenzi wa miradi ya majengo ya Mahakama katika maeneo ya Longido na Ngorongoro na itatoa kipaumbele kwa mkoa huo kutokana na changamoto zilizopo.

Alisema zaidi ya majengo 10 ya Mahakama mkoani huo yanahitaji kujengwa na mengine kufanyiwa ukarabati ili kupunguza gharama za uendeshaji kwani baadhi ya maeneo wanachi wanalazimika kufuata huduma hizo kwa umbali mrefu.

Naye Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Bibi. Enziel Mtei amewashauri wajumbe wa kamati za Maadili kutumia elimu waliyoipata kuhusu uendeshaji wa kamati hizo kuwaelimisha wananchi.

Alitoa wito kwa wajumbe hao kutoa kipaumbele katika suala zima la uendeshaji wa kamati hizo kwa kutenga bajeti kwa ajili ya kuendesha kamati za Maadili kwenye maeneo yao.

Tume ya Utumishi wa Mahakama inafanya ziara katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara kwa lengo la kuitangaza na kutoa elimu kwa wadau wa Mahakama wakiwemo wajumbe wa kamati za Maadili za Mikoa na Wilaya zinazowajumuisha wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya.

Tume ya Utumishi ya Mahakama imeundwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 113 kwa lengo la kusimamia mambo muhimu yanayohusu Mhimili wa Mahakama. Wajumbe wa Tume hiyo ni pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania (Mwenyekiti), Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji moja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, na wajumbe wengine wawili wanaoteuliwa na Rais.

 Baadhi ya kazi za Tume hiyo ni pamoja na kumshauri Mhe. Rais katika uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu, kumshauri Rais kuhusu masuala ya nidhamu, mishahara na maslahi ya Majaji, na kushauri kuhusu ajira za Mahakimu na kusimamia nidhamu yao.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Arusha ofisini kwake. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika na Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa ArushaMhe. Iddi Hassan Kimanta

 

Mkuu wa Mkoa wa ArushaMhe. Iddi Hassan Kimanta akizungumza


Wajumbe wa Kamati za Maadili za Mkoa wa Arusha na wilaya zake pamoja na baadhi ya watumishi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Chuma akizungumza kwenye Mkutano huo. 

Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Bibi. Enziel Mtei akizungumza wakati wa Mkutano huo. 


Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa ArushaMhe. Iddi Hassan Kimanta (wa tatu kushoto), Viongozi wa Mahakama pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Arusha wakati Jaji Mkuu alipomtembelea Mkuu huyo wa Mkoa. 

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma Mhe. Ilvin Mugeta akitoa mada kwenye Mkutano huo. 

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Muro akizungumza wakati wa Mkutano huo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni