Jumanne, 31 Machi 2026

KITUO JUMUISHI CHA MASUALA YA FAMILIATEMEKE CHATOA MAFUNZO KWA WAJANE

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam

Kituo Jumuishi cha Masuala ya FamiliaTemeke tarehe 28 Machi, 2026 kiliendesha mafunzo maalum kwa wajane wa Wilaya ya Temeke kwa lengo la kuwajengea uelewa kwenye haki zao za kisheria, hususan katika masuala ya urithi na mirathi.

Halikadhalika, washiriki wa mafunzo hayo walipatiwa elimu ya kisheria itakayowasaidia kulinda haki zao na za watoto wao, kusimamia mali za marehemu kwa mujibu wa sheria na kuepuka migogoro ya mirathi katika familia na jamii

Mafunzo hayo yalifunguliwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, ambaye alisisitiza umuhimu wa wajane kufahamu haki zao, kufungua mirathi kwa wakati na kutumia mifumo ya kisheria ili kuepusha migogoro ya kifamilia.

Mtandao wa Mashirika yanayotoa Msaada wa Sheria Tanzania (TANLAP), uliowakilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa TANLAP, Wakili Fransisca Silaya, ndiyo uliofadhili mafunzo hayo.

Wakili Silaya, akizungumza wakati wa mafunzo hayo, alionesha dhamira ya Taasisi hiyo kuendelea kuunga mkono juhudi za utoaji wa elimu ya kisheria kwa makundi maalum katika jamii.

Mafunzo hayo yalijumuisha mada kuu nne zilizowasilishwa na wakufunzi wenye uzoefu, ikiwemo Urithi na Mirathi na Sheria za Urithi Tanzania zilizowasilishwa na Mhe. Magdalena Malaba.

Nyingine ni Kufungua Mirathi na Nyaraka Muhimu na Wosia na Ulinzi wa Haki zilizowasilishwa na Mhe. Edna Mollel.

Katika mada hizo, washiriki walipata uelewa wa kina kuhusu taratibu za mirathi, haki zao za kisheria, umuhimu wa nyaraka sahihi pamoja na namna ya kuandika wosia na kulinda haki zao.

Mafunzo yalihusisha wajane kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Temeke, wakiwemo wanachama wa vikundi vya kijamii, hususan kikundi cha VIWOTA Women Group. Washiriki walionesha hamasa kubwa ya kujifunza na kuchangia mijadala.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, alifunga mafunzo hayo na kuwasihi washiriki wote kutumia maarifa waliyoyapata maarifa kwenye maisha yao na kuwafikishia wengine elimu hiyo kwani ni nyenzo ya kujikomboa dhidi ya dhuluma na kuhakikisha haki inatendeka.

“Napenda pia kuwakumbusha kuwa taasisi zetu za haki, ikiwemo Kituo Jumuishi Temeke, zipo kwa ajili yenu. Msisite kufika pale mnapohitaji msaada wa kisheria au ushauri,” alisema.

Bw. Mashalla alitumia fursa hiyo kuushukuru Mtandao wa Asasi za Msaada wa Sheria Tanzania (TANLAP) kwa mchango wao katika kufanikisha mafunzo hayo, kwani mchango wao umeleta mabadiliko chanya katika maisha ya washiriki.

Aliwashukuru pia wakufunzi kwa kujitolea kutoa maarifa na kwa uvumilivu wao katika kuhakikisha kila mshiriki anaelewa mada zilizowasilishwa. “Mafunzo haya yamekuwa ya manufaa makubwa na yamegusa moja kwa moja maisha yetu ya kila siku,” alisema.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo (Picha na Maktaba).

Kaimu Mkurugenzi wa Mtandao wa Asasi za Msaada wa Sheria Tanzania (TANLAP), Bi. Fransisca Silaya.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya kwenye Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Magdalena Malaba, akiwsilisha mada kwenye mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo kwenye Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Moleli, akiwasilisha mada kwenye mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo wakifuatilia kilichokuwa kinajiri.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, akizungumza wakati anahitimisha mafunzo hayo.

Picha ya pamoja ya washiriki wakati wa mafunzo hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA YAFANYA KIKAO CHA MENEJIMENTI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, amewapogeza Watumishi wa Mahakama Kanda ya Musoma kwa uwajibikaji mzuri uliowezesha Mahakama hiyo kuwa ya pili kitaifa kwa kasi nzuri ya umalizaji wa mashauri.

Mhe. Mtulya alitoa pongezi hizo katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma kilichofanyika hivi karibuni wilayani Serengeti katika ukumbi wa Ofisi ya Mashtaka.

Alisisitiza umuhimu wa vikao vya menejimenti ambavyo vinatumika kuweka mikakati mbalimbali ya kiutendaji pamoja na kusisitiza utekelezaji wa maelekezo ya Viongozi wa juu, jambo lililodhihirishwa kwa matokea mazuri ya usikilizaji na umalizaji wa mashauri.

Aidha, katika kikao hicho kinachoundwa na wajumbe kutoka Mahakama Kuu Musoma, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma na Mahakama za Wilaya za Musoma, Butiama, Bunda, Serengeti, Tarime na Rorya, ziliwasilishwa taarifa mbalimbali za utendaji kazi kwa robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26.

Kuliwasilishwa pia taarifa za Mkaguzi wa Ndani, Ofisa TEHAMA, miradi inayoendelea ndani ya Kanda na ushiriki katika matukio ya kijamii.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, alisisitiza utekelezaji wa maelekezo ya Viongozi wa Mahakama, ikiwemo ufungaji wa mirathi, kuendelea na utoaji wa adhabu mbadala pamoja na usikilizaji wa mashauri kwa wakati ili kuepuka kuzalisha mlundikano.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Leonard Maufi, alielezea mikakati mbalimbali ya Kanda, ikiwemo uboreshaji wa miundombinu. Alisema kwa mwaka wa fedha, Kanda inaendelea na ukarabati mkubwa wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Nyaburongo iliyoko Wilayani Rorya kwa kutumia fedha za ndani.

Pia alielezea hatua iliyofikiwa katika miradi inayoendelea ya ujenzi wa Mahakama za Wilaya Serengeti na Tarime. Aidha, aliwaasa Watumishi kuendelea kuzingatia kanuni, taratibu na miongozo ya utumishi wa umma.

Akihitimisha kikao hicho, Mhe. Mtulya aliwakumbusha wajumbe mafanikio yaliyopatikana ndani ya Kanda, ikiwemo kutovuka mwaka na mashauri mlundikano kwa miaka mitatu mfululizo na ukarabati wa majengo ya Mahakama, hasa za Mwanzo.

Alitaja mafanikio mengine kama ulinzi wa mipaka ya maeneo ya Mahakama, upatikanaji wa hati, umoja na ushirikiano wa kikanda kwenye kazi na matukio ya kijamii kma kushiriki matukio ya huzuni na furaha.

Hivyo aliwaasa wajumbe hao kwenda kuwasimamia vyema Watumishi katika maeneo yao ili, kwa pamoja waweze kufikia malengo ya Kanda yaliyowekwa.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Leonard Maufi (kushoto), wakichambua kwa makini baadhi ya taarifa zilizowasilishwa na wajumbe wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Wajumbe wa kikao cha Menejiment Kanda ya Musoma kutoka Wilaya mbalimbali wakiwasilisha taarifa za utendaji kazi katika vituo vyao vya kazi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mhe. Veronica Mugendi (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa kituo chake katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Kandana Lucas (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na taarifa ya miradi inayotekelezwa ndani, huku wajumbe wakifuatilia kwa makini taarifa hiyo wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Mkaguzi wa Ndani wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Andala Odock (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya ukaguzi katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Afisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Japhet Mnyetta (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya hali ya miundombinu na matumizi ya TEHAMA ilivyo ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, akiwasilisha taarifa ya hali ya mashauri ilivyo ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Leonard Maufi (aliyesimama), akifafanua jambo wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa kamati ya utalii (matukio ya kijamii) ambaye ni Mhasibu wa Mahakama Kuu Musoma, Bi. Samira Nkya (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya ushiriki katika matukio ya kijamii ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), akisisitiza jambo kwa wajumbe wa kikao cha Mnenejimenti Kanda ya Musoma wakati wa kikao hicho.

Picha ya pamoja ya wajumbe wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma walipotembelea mmoja ya miradi inayoendelea ndani ya Kanda hiyo, ambayo ni ujenzi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Serengeti, mara baada ya kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma kilichofanyika Wilayani Serengeti. 

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

JAJI RWIZILE AWASISITIZA VIONGOZI WA MAHAKAMA KIGOMA KUZINGATIA MAMBO SITA MUHIMU

Na AIDAN ROBERT - Mahakama Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka Mahakimu pamoja na Viongozi  wengine wa Mahakama Kigoma kufanya kazi kwa kuzingatia mambo sita muhimu ya maadili ambayo ni Uadilifu, kuwa viongozi bora kwa wengine, kujali stahili za watumishi, Ubunifu katika kazi, Mahusiano mazuri kazini na mawasiliano ya karibu katika utendaji wa shughuli za kiutawala.

Mhe. Rwizile aliyasema hayo tarehe 28 Machi 2026 wakati akifungua Kikao cha Uongozi kwa robo ya tatu ya mwaka kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe ambapo alitumia fursa hiyo kuwakumbusha kuhusu majukumu ya kila siku na kubaini mapungufu, changamoto na kuona mapendekezo na njia sahihi za kutatua changamoto hizo.

“Fanyeni kazi kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma na nidhamu kama Sheria ya  Utawala wa Mahakama inavyotutaka katika ibara (237), ambapo Sheria hii ina maboresho yake imeeleza wazi utendaji wa Viongozi wa Mahakama katika mnyororo wa haki na hasa fungu la (11) ambapo linaeleza wazi jinsi ambavyo utawala katika muhimili wa Mahakama unapaswa kuwa, ni vema mkaisoma vizuri ili kuongeza weledi katika eneo la utawala,” alisema Jaji Rwizile.

Aidha, alisisitiza pia kifungu cha (65) cha sheria hiyo kinachotoa namna ambavyo watendaji wanafanya kazi wakishirikiana na Ofisi ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, ikiwataka kushirikiana kwa karibu ili kuhakikisha shughuli za kiutawala zinasimamiwa vema kwa ajili ya kuhakikisha mnyororo wa usikilizwaji wa mashauri katika Mahakama zote haukwami kwa namna yeyote.

Hata hivyo, aliwasisitiza viongozi hao kuongeza kasi katika umalizaji wa mashauri kwa kuzingatia lengo mama la Mahakama ya Tanzania ambalo ni kusikiliza mashauri na kuyatolea uamuzi mapema ipasavyo. Vilevile Mhe.Rwizile aliwaasa Viongozi kuendelea kudumisha ushirikiano mzuri uliopo eneo la kazi.

Sambamba na hayo Jaji Rwizile, alizindua chumba cha Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Kasulu Mjini kilichokarabatiwa kwa fedha ya ndani ili kusaidia kusogeza huduma na kuongeza kasi ya usikilizwaji wa mashauri kwa Mahakama za Mwanzo.

Aidha, wajumbe wa kikao hicho walipata fursa ya kupanda miti ya matunda katika eneo la wazi lililopo katika Mahakama ya Wilaya Buhigwe.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma Mhe. John Francis Nkwabi, alitoa pongezi kwa Viongozi wa Mahakama za Wilaya Kanda ya Kigoma kwa jinsi wanavyoshirikiana kwa karibu na watumishi wa kada zote kuhakikisha usikilizwaji wa mashauri na kutunza miundombinu ya Majengo na TEHAMA inaendelea kuboreshwa ili utendaji wa kazi za watumishi uendelee kuwa rahisi, sambamba na ubunifu unaoleta tija katika shughuli za kila siku.

Katika ziara hiyo iliyoambatana na Kikao cha Uongozi, Jaji Mfawidhi, Mhe. Rwizile aliambatana na Viongozi wengine wa Mahakama akiwemo Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza, Naibu Msajili Mahakama Kuu, Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka na Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Singida, Bw.Filbert Matotay, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo, Mahakimu Wakazi Wafawidhi kutoka Wilaya za Kigoma, Kasulu, Kibondo, Uvinza, Buhigwe na Kakongo pamoja na Wakuu wa Vitengo wa Mahakama Kuu Kigoma.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine  Rwizile akisisitiza jambo wakati alipokuwa akifungua Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kanda ya Kigoma kilichofanyika tarehe 28 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Kigoma, Mhe.Augustine
 Rwizile akikata utepe kuashiria ufunguzi wa Ofisi ya Hakimu. Pamoja naye wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi, wa kwanza kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza na wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kasulu na walisimama nyuma wakishuhudia ufunguzi huo viongozi wengine wa Mahakama pamoja na watumishi wa Mahakama Kasulu. 

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi na Wakuu wa Vitengo Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma. Wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza, wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu-Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Mhoja.

Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Wilaya Buhigwe mara baada ya Kikao cha Uongozi kumalizika.

 
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,  Mhe. John Nkwabi akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Wilaya Buhigwe mara baada ya kikao cha uongozi kumalizika.

  
Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Wilaya Buhigwe.
 
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Mhoja akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Wilaya Buhigwe.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Kasulu (waliosimama) mara baada ya uzinduzi wa chumba cha Hakimu. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 


Jumatatu, 30 Machi 2026

JAJI MFAWIDHI MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO SINGIDA AWASILI KITUONI

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda leo tarehe 30 Machi, 2026 amewasili mkoani Singida ikiwa ni mara ya kwanza baada ya kupata uteuzi huo hivi karibuni wa kuiongoza Kanda hiyo mpya ya Mahakama Kuu.

Akiwa katika hafla ya ukaribisho wake alipata nafasi ya kusikiliza taarifa fupi ya utekelezaji iliyosomwa na Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Bi. Eva James Leshange. 

Mara baada ya kupokea taarifa hiyo, Mhe. Mwenda amewapongeza Viongozi na watumishi wote wa Mahakama Mkoa wa Singida kwa kazi nzuri wanayoifanya hasa katika usikilizwaji wa mashauri kwani hadi kufikia tarehe 27 Machi, 2026 Mkoa wa Singida haukuwa na shauri la mlundikano.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo amewashukuru watumishi kwa mapokezi mazuri na kuona watumishi wana ari na nguvu ya kufanikisha malengo ya Mpango Mkakati wa Mahakama.

“Nawashukuru sana viongozi na watumishi kwa ujumla kwa mapokezi mazuri na hongereni sana kwa kufanya kazi kwa bidii na ushiriano mkubwa hususan katika usikilizwaji wa mashauri ni kiashiria watu wanafanya kazi kwa ushirikiano,” amesema.

Vilevile amewasisitiza watumishi kuendela kuwa na nidhamu kwani, Mahakama inapokea wateja ambao wameumizwa na wanahitaji msaada hivyo wasaidiwe kuhudumiwa kwa heshima, pia amesisitiza kufanya kazi katika timu pasipo kuangalia vyeo ili kusiwe na mkwamo katika kutekeleza majukumu ya kila siku.

Baada ya kuzungumza na watumishi alipata wasaa wa kwenda kutembelea jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Singida na kufanya ukaguzi wa vyumba vya ofisi na kuona hatua ilipofikiwa.

 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (wa kwanza kushoto) akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida alipowasili ofisini hapo leo tarehe 30 Machi, 2026.

Afisa Utumishi Mwandamizi Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Bi. Eva Leshange akiwasilisha taarifa ya utekelezaji majukumu mbele ya Mhe. Ayoub Mwenda, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda Ya Singida (hayupo katika picha) leo tarehe 30 Machi, 2026 alipowasili katika Mahakama hiyo.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria hafla fupi ya ukaribisho wa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda mpya ya Singida.


Sehemu ya watumishi ajira mpya wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyeketi katikati) . Aliyeketi kushoto ni Naibu Msajili, Mhe. Evodia Kyaruzi na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Singida, Bw. Filbert Matotay. 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akikagua jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Singida.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

MTENDAJI WA MAHAKAMA PWANI AWATAKA WATUMISHI WA KANDA YA DAR ES SALAAM KUITHAMINI MICHEZO

  • Asema michezo ni haki ya msingi kwa ustawi na ufanisi katika utendaji kazi
Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestory Mujunangoma amewataka watumishi wa Mahakama Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani kuifanya michezo kuwa haki kwa kila mtumishi.

Bw. Mujunangoma aliyasema hayo tarehe 28 Machi, 2026 wakati akifungua Bonanza lililofanyika katika viwanja vya Zimamoto Kibaha Mkoa wa Pwani. Bonanza hilo lililoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani ambalo liliwashirikisha watumishi wa Mahakama Mkoa wa Dar es Salaam ambao wanaunda Kanda ya Dar es Salaam.

Alisema kuwa, kushiriki katika michezo ni haki ya kila mtu na kwamba michezo ni furaha, inaleta umoja na mshikamano na ndio maana wako pamoja, hivyo ni amewasisitiza kuongeza bidii kushiriki katika michezo kwakuwa michezo ni haki yao. 

Aidha, akifafanua kauli hiyo alisema kila mtumishi wa Mahakama aione michezo kama haki yake na kwamba ana uhakika kama watashiriki kwa wingi na kwa umoja huo licha ya kuimarisha afya zao, furaha zao na mshikamano wao hata utendaji kazi wao utakuwa na ufanisi zaidi maana wakiwa na michezo akili zitakuwa vizuri.

“Kadhalika umoja utakuwepo mipango itapangika na watakuwa karibu na Viongozi wao na watakachokipanga kitaeleweka na kitafanyiwa kazi kinachotakiwa ni kupata ufanisi wa kazi katika Taasisi,” ameeleza Mtendaji huyo. 

Kadhalika aliwapongeza Viongozi wa Kitaifa wa Mahakama Sports Club kwa kujumuika katika Bonanza hilo na kusema kwamba, uwepo wa Viongozi wa michezo kitaifa inaonesha kuwa shughuli hiyo haitaishia hapo bali itakuwa endelevu.

Alisema pia, kwa Mkoa wa Pwani, imekuwa ni heshima kubwa kwa kufanya bonanza hilo na pia ameomba ushirikiano huo waliouonesha Dar es Salaam na Pwani uendelee.

Amewaomba Uongozi wa Kitaifa kushirikiana na Uongozi wa Pwani na Dar es Salaam kufanya kitu kikubwa zaidi na kitu kitakachofahamika zaidi na kuitangaza Mahakama kwa upana  mkubwa Zaidi. “Sasa tujiandae kutakapokuwa na Bonanza linalofuata  maana yake tuwe na timu nyingine za Taasisi nyingine kwa hiyo lazima tuwe na maandalizi makubwa zaidi,” alisema Bw. Mujunangoma.

Bonanza hilo lilihusisha mchezo wa mpira wa miguu ambapo mpaka dakika zote 90 walitoka kwa sare ya kufungana goli moja kwa moja na walipoenda kwenye matuta Pwani walipata penati sita wakati Dar es Salaam walipata penati saba hivyo Dar es Salaam kupata ushindi kwa upande wa mpira wa miguu.

Kwa upande wa Mpira wa Pete Pwani waliibuka kidedea kwa kuwafunga Dar es Salaam magoli 10 kwa nane, wakati mchezo wa kuvutana kwa kwamba wanaume na wanawake Dar es salaam waliibuka kidedea.

Mchezo wa riadha kwa wanaume Dar es Salaam wameibuka kidedea wakati upande wa wanawake Pwani wameibuka kidedea na mchezo wa kufukuza kuku wanawake na wanaume Dar es Salaam wamefanikiwa kuchukua kuku wote wawili.


Mgeni rasmi Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestor Mjunangoma  (aliyesimama) akizungumza wakati wa ufunguzi wa Bonanza tarehe 28 Machi, 2026 katika viwanja vya Zimamoto Kibaha Mkoa wa Pwani. Kulia ni Mwenyekiti wa Mahakama Sports Club, Mhe. Martin Mushi na kushoto ni Naibu Katibu, Mahakama Sports Club, Bi. Eva Mapunda.

 Mgeni rasmi Mtendaji wa Mahakama Pwani,  Bw. Nestory Mujunangoma  akikagua kikosi cha Mpira wa Miguu cha Pwani. Kushoto ni Nahodha wa Kikosi hicho ni Bw. Isihaka Mgude.

Mgeni rasmi Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestory Mujunangoma (mwenye kofia)  akikagua kikosi cha Mpira wa Miguu cha Dar es Salaam. Kulia kwake ni Nahodha wa Kikosi hicho, Abdi Sasamalo.

Washindi wa kukimbiza kuku, kulia ni Stanley Sirikwa na kushoto ni Bi. Patricia Patrick.

 Kikosi cha Kamba Wanaume Dar es Salaam wakijiandaa na pambano.

Vikosi vya Kamba Wanawake Pwani na Dar es Salaam wakisikiliza maelekezo kabla ya pambano.

Matukio katika picha Bonanza la Michezo lililoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

WATUMISHI WANAWAKE WA MAHAKAMA KANDA GEITA WAFANYA MATENDO YA HURUMA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama Kuu, Geita

Wanawake wa Mahakama Kanda ya Geita kutoka Mahakama Kuu Geita, Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mahakama ya Wilaya ya Geita na Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, tarehe 28 Machi  2026 walitembelea Wodi ya Wajawazito na Wazazi katika Kituo cha Afya Kasamwa.

Lengo la ziara hiyo ni kufanya matendo ya huruma ikiwa ni utaratibu waliojiwekea kila mwaka wanapoadhimisha kilele cha Siku ya Wanawake Duniani.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kasamwa, Dkt. Emmanuel Zillagera, pamoja na Watumishi wengine wa Kituo hicho waliwaongoza Wanawake wa Mahakama katika wodi hizo na kutoa zawadi mbalimbali.

Watumishi hao wa Mahakama walitoa vifaa na mahitaji kwa Wajawazito na Wazazi ambavyo ni sukari, sabuni za unga, mafuta ya kujipaka, pampers na vingine.

Akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo, Dkt. Zillagera aliwashukuru Wanawake wa Mahakama kwa matendo ya huruma waliyotoa. Pia aliwaomba kurudi kipindi kingine kwa ajili ya hiyo mara watakapopata nafasi.

Naye Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, aliwashukuru Viongozi pamoja na Watumishi wa Kituo hicho kwa kuwakubalia kufika na kufanya matendo ya huruma.

"Kila mwaka Wanawake wa Kanda ya Geita wanapokuwa wanaelekea kilele cha Siku ya Wanawake Duniani, hufanya matendo ya huruma kwa kupeleka vifaa ambavyo ni mahitaji mbalimbali. Kitendo hiki ni sadaka yetu kama Wanawake kwa Wazazi pamoja na Wajawazito,” alisema.

Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Masalu Kisasila, akikabidhi sabuni, pampers na vitu vingine kwa Muuguzi Mkunga Sr. Joyce wa Kituo cha Afya Kasamwa.

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufika katika Kituo cha Afya Kasamwa.

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Kituo cha Afya Kasamwa (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

NAIBU WASAJILI NA MAHAKIMU WAKAZI WANOLEWA MBINU ZA USULUHISHI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) imeendesha mafunzo maalum ya Usihi na Usuluhishi kwa Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi toka katika Mahakama mbalimbali za mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Iringa, Njombe, Sumbawanga, Songwe, Songea na Katavi.

Mafunzo hayo ya siku tatu yalianza tarehe 24 Machi, 2026 hadi tarehe 26 Machi 2026 katika ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya yakiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ambaye pia ni alikuwa mwezeshaji akishirikiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raymond Kaswaga pamoja na Mhe. Gloria Shuma kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA).

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo Mhe. Tiganga alitoa shukrani zake za dhati kwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi Dar Es Salaam, Mhe. Zahara Maruma kwa kuandaa na kuratibu Mafunzo hayo. Vilevile, aliwaasa washiriki kuwa chachu ya mabadiliko katika kutatua migogoro mingi kwa njia ya usuluhishi.

“Kwa mafunzo haya mliyoyapata mkawe sababu ya mabadiliko katika kutatua migogoro mingi kwa njia ya usuluhishi na kuwa walimu wazuri kwa kuwapa wengine kile mlichojifunza kwa ambao hawakupata bahati ya kuwa sehemu ya mafunzo haya. Natamani mashauri mengi katika masjala zetu yaishe kwa njia ya Usuluhishi” alisema Mhe. Tiganga.’’ alisema Mhe. Tiganga.

Mafunzo hayo yanaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na Mpango Mkakati wa Mahakama unaosisitiza umuhimu wa kutumia njia mbadala ya utatuzi wa migogoro (usuluhishi) ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Na pia ni utekelezaji wa Ibara ya 107 A (2) (d) ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977. Mafunzo hayo yalilenga pia maandalizi ya Wiki ya Usulujishi itakayozinduliwa tarehe 9 Aprili 2026 katika Ukumbi wa Golden Jubilee PSSSF Tower Dar Es Salaam na kufuatiwa na Wiki ya Usuluhishi itakayofanyika Nchi nzima kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba alitoa shukurani kwa waandaaji na wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa kufanikisha mafunzo hayo na kuahidi kuwa watayafanyia kazi yale waliyofundishwa na watakuwa walimu wazuri kwa wengine ambao hawakupata bahati ya kuwa sehemu ya mafunzo hayo.

Sehemu ya mada zilizofundishwa ni pamoja na dhana ya Usuluhishi, sheria na kanuni za usuluhishi, mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa usuluhishi, nafasi ya sheria na mawakili katika usuluhishi, vikwazo na changamoto katika usuluhishi na pia mafunzo hayo yaliambatana na mazoezi ya vitendo (Practical sessions) yaliyowasaidia washiriki kuelewa kwa kina namna ya kuendesha vikao vya usuluhishi kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Mbeya wakiwa Meza Kuu wakati wa kufunga mafunzo ya Usuluhishi Nyanda za Juu Kusini katikati ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto) na Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (kulia)

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akikabidhiwa cheti na Jaji Mfawidhi Mahakama kuu kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga kwa kuwa sehemu ya mafunzo hayo.

Mhe. Raimond Kaswaga akikabidhiwa cheti na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga kwa kuwa sehemu ya wawezeshaji katika mafunzo hayo.

Washiriki katika mafunzo hayo wakiwa katika mazoezi ya vitendo (Practical session) ya namna ya kuendesha vikao vya usuluhishi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akikabidhiwa cheti na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Songea Mhe. Elizabeth Nyembele kwa kuwa sehemu ya wawezeshaji katika mafunzo hayo.

Mwezeshaji katika mafunzo hayo ambaye ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, akimwaga madini wakati wa mafunzo hayo.

Mwezeshaji katika mafunzo hayo ambaye ni Hakimu mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raimond Kaswaga akifundisha wakati wa mafunzo hayo

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba akitoa neno la shukurani kwa waandaaji na wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa niaba ya washiriki wa mafunzo.

Mhe. Gloria Shuma kutoka Chuo Cha Uongozi wa mahakama (IJA) akitoa neno la shukurani katika Ufungaji wa mafunzo hayo