Jumatano, 27 Mei 2026

WATUMISHI WA MAHAKAMA BUKOBA WAKUMBUSHWA KUTOA HUDUMA BORA KWA WATEJA

  •  Wasisitizwa pia kuzingatia matumizi ya Teknolojia na kujiendeleza kielimu

Na MICHAEL RITTE, Mahakama-Bukoba

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wamehimizwa kuendelea kuboresha huduma kwa wateja, kutumia lugha nzuri wanapohudumia wananchi pamoja na kujiendeleza kielimu ili kwenda sambamba na kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani.

Wito huo umetolewa na Viongozi kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania wakati wa kikao cha utoaji wa elimu ya huduma kwa wateja kilichofanyika tarehe 26 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba.

Kikao hicho cha mafunzo na majadiliano kililenga kuwakumbusha watumishi umuhimu wa huduma bora kwa wananchi pamoja na matumizi sahihi ya mifumo ya kisasa ya utoaji huduma.

Akizungumza katika kikao hicho, Mmoja kati ya Viongozi kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Aloyce Katemana alisema, Mahakama ya Tanzania imeendelea kuboresha mifumo yake ya huduma kwa wananchi kupitia Kituo cha Huduma kwa Wateja kinachopatikana kupitia namba maalum ya bure 0800 750 247 inayofanya kazi saa 24 kwa siku, siku saba kwa wiki mwaka mzima.”

Aliendelea kueleza kuwa, Kituo hicho kimeboreshwa kwa kutumia mfumo wa kisasa wa IVR (Interactive Voice Response) unaomuwezesha mwananchi kupata maelekezo ya awali kwa njia ya simu, sambamba na matumizi ya WhatsApp ambayo sasa yana uwezo wa kutoa baadhi ya majibu ya awali automatiki.

“Lengo letu ni kuhakikisha mwananchi hapati shida ya kusafiri umbali mrefu kufuatilia malalamiko, maoni, pongezi au maulizo yake. Tunataka huduma ziwe rahisi kufikika kwa kila mtu,” alisema Mhe. Katemana.

Aidha, alibainisha kuwa Kituo cha Huduma kwa Mteja kiko chini ya Idara ya Ukaguzi wa Mahakama, Mrejesho kwa Umma na Maadili, ambapo kwa sasa mrejesho kutoka kwa wananchi unahusisha maeneo manne ambayo ni maulizo, maoni, pongezi na malalamiko.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania, Dkt. Evetha Mboya ambaye alikuwa Muelimishaji katika kikao hicho, alisema huduma bora huanzia mapokezi ya kwanza kabisa kwa mteja, huku akisisitiza kuwa hata namna mteja anavyopokelewa getini inaweza kujenga au kuharibu taswira ya Mahakama mbele ya wananchi.

Aliwapongeza watumishi wa Mahakama Bukoba kwa mapokezi mazuri waliyoyatoa kwao, lakini pia aliwakumbusha kuwa, bado kuna baadhi ya malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu ucheleweshaji wa huduma na namna ya mawasiliano wanayopata kutoka kwa baadhi ya watumishi.

Alisisitiza kwa kusema kuwa, “Mteja anapokuja mahakamani mara nyingi tayari ana changamoto zake. Wengine wanakuwa wamechoka, wamekasirika au wana mawazo mengi, hivyo jukumu letu ni kumtuliza na kumfanya aone kuwa amesikilizwa.”

Katika mafunzo hayo, Dkt Evetha aliwahizimiza watumishi kutumia lugha ya heshima kwa wananchi, kuwa wasikivu pamoja na kutoa maelezo kwa utulivu hata kwa wateja wanaoonekana kuwa wagumu au wenye hasira.

Pia alikumbusha umuhimu wa kuzingatia sera ya (Open Door Policy) inayosisitiza uwazi na upatikanaji wa Viongozi au Watumishi kwa wananchi pale inapowezekana, ili kuepusha hisia za kunyimwa haki au kubezwa.

Sambamba na hilo, Viongozi hao kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja  walionya dhidi ya vitendo vya rushwa ndogondogo vinavyoweza kujitokeza katika utoaji wa huduma, wakisema mazingira yoyote yanayoweza kumfanya mwananchi ahisi analazimika kutoa fedha ili kupata huduma hayapaswi kuvumiliwa.

Katika kuelezea vigezo vya huduma bora kwa mteja, Mkufunzi alitaja maeneo muhimu yakiwemo kujenga imani kwa wateja (assurance), kutoa huduma kwa haraka (responsiveness), muonekano mzuri wa watumishi na mazingira ya kazi (tangibility), kujali hali ya mteja (empathy), pamoja na kuhakikisha huduma zinakuwa za kuaminika wakati wote (reliability).

Mafunzo hayo pia yaligusia umuhimu wa watumishi kujiendeleza kielimu kutokana na kasi ya maendeleo ya teknolojia, ikiwemo matumizi ya mifumo ya kidijitali, (biometric) na Akili Unde (Artificial Intelligence) katika taasisi mbalimbali.

“Dunia inabadilika sana, kama hatutaongeza ujuzi wetu, ipo siku mifumo itabadilika na tukajikuta tumebaki nyuma,” alieleza Dkt Evetha.

Kwa upande wake, Mhe. Hamza Marishi aliwasihi watumishi kuifahamu vizuri Taasisi yao pamoja na nyaraka muhimu za Mahakama ya Tanzania ikiwemo Mpango Mkakati wa Mahakama na Mkataba wa Huduma kwa Mteja.

Alisema nyaraka hizo zinaeleza wajibu wa watumishi kwa wananchi pamoja na haki za wateja kupata huduma bora, uwazi na ushirikishwaji.

Katika mjadala wa wazi, baadhi ya watumishi walieleza changamoto wanazokutana nazo katika kujiendeleza kielimu, hususan ucheleweshaji wa malipo ya ufadhili kwa watumishi wanaopata nafasi za masomo.

Baadhi yao waliomba Mahakama kuweka mfumo bora wa mawasiliano kati ya Mwajiri na Vyuo ili wanafunzi wanaodhaminiwa wasipate usumbufu wanapowasili vyuoni.

Mmoja wa washiriki ambaye ni Mlinzi alisema amenufaika na ufadhili wa Mwajiri kwa kupata nafasi ya kusoma katika Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) lakini akaomba nafasi zaidi za kujiendeleza zitolewe kwa Kada mbalimbali kutokana na mabadiliko ya teknolojia na mifumo ya kazi.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa watumishi kuaswa kuendelea kulinda taswira ya Mahakama ya Tanzania kwa kutoa huduma bora, kuwa waadilifu, kutumia teknolojia vizuri na kuendelea kujifunza ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

 

Picha ya pamoja. Kuanzia Kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Bw. Edward Mbara, wa pili kushotp ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe Said Mkasiwa, katikati ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzani, Mhe. Aloyce Katemana ambaye ni Mkufunzi katika kikao hicho, wa pili kulia ni Dkt. Evetha Mboya Kiongozi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja ambaye pia alikuwa Mkufunzi wa Kikao cha utoaji elimu kutoka Kituo hicho na wa kwanza kulia ni Bi. Monica  Kalokola, Ofisa Utumishi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wakiwa katika ufunguzi wa kikao hicho na utambulishaji wa watumishi waliohudhuria.

Dkt. Evetha Mboya (aliyesimama) akitoa elimu ya utoaji wa huduma bora kwa wateja kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Bukoba. Walioketi katikati ni Bi Monica Kalokola, Ofisa Utumishi Mahakama Kuu Bukoba na kulia Bw. Rojas Rwanyumba, Ofisa Tawala Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Bukoba na nyuma yao  ni baadhi ya  watumishi wa Mahakama waliohudhuria wakisikiliza na kufuatilia kwa umakini mafunzo hayo.


 Elimu ya huduma kwa wateja ikiendelea kutolewa.Walioketi ni Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wakisikiliza kwa utulivu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

MAHAKAMA KIGOMA YAWAAGA WATUMISHI WALIOHAMA KITUO, WASTAAFU NA KUWAKARIBISHA WATUMISHI WAPYA

  • Jaji Mfawidhi awapongeza waliohama kwa kazi nzuri na kuwataka wakachape kazi Vituo walivyohamishiwa

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile amewaongoza watumishi na wadau wa Mahakama katika hafla ya kuwaaga watumishi waliohamishwa kutoka Mahakama hiyo.

Hafla ya kuwaaga watumishi hao ilifanyika tarehe 23 Mei, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Kigoma.

Mhe. Rwizile amewapongeza Jaji Projestus Kahyoza na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Singida, Bw. Filbert Matotay kwa uchapakazi wao ulioacha alama kubwa walipokuwa katika Kituo cha Kigoma, alisema kuwa, Viongozi hao ni taa popote walipo maana wanayo maono na ari kubwa ya kutenda kazi kwa ubunifu na weledi mkubwa.

Jaji Rwizilea, alitumia nafasi hiyo kuwapongeza pia jumla ya watumishi sit awa Mahakama hiyo waliostaafu wa utumishi wa Mahakama kwa mujibu wa sheria ambao nao wameagwa katika sherehe hiyo.

“Tunawapongeza sana kufikia umri wa kustaafu utumishi wenu hakika Mahakama Kigoma itauenzi na kuukumbuka utumishi wenu uliotukuka wa kujitoa kwa nguvu zenu, weledi na kujituma mlipokuwa mkitimiza majukumu yenu na hatimaye kustaafu mkiwa na afya njema, muendelee kujishughulisha na kazi zenu binafsi ili muendelee kustawi katika maisha yenu huko muendako,” alisema Mhe. Rwizile.

Ameongeza kwa kuwakaribisha, watumishi walioajiriwa hivi karibuni na kupangiwa katika Kituo cha Mahakama Kigoma.

“Karibuni sana Kigoma tunafanya tofauti, hivyo tunayo imani na matarajio makubwa kwenu mtafanya kazi nasi kwa ushirikiano kupitia maarifa yenu mbalimbali tutasonga mbele zaidi katika shughuli zetu za kila siku,” amesema Jaji Mfawidhi huyo.

Kwa upande wake Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza alimshukuru Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kigoma, kwa kuwa msaada mkubwa katika kusimamia shughuli za Mahakama hiyo, ambapo amesema kupitia usimamizi wake mzuri ulimfanya kazi zake kuwa rahisi na kujisikia kwamba Kigoma kuwa kituo pekee ambacho amewahi kuhudumu chenye upekee.

Hata hivyo, aliwashukuru watumishi wa Mahakama hiyo kwa upendo na ushirikiano wao, ingawa hana budi kwenda kutumikia kituo kingine, amewataka kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, weledi na uwajibikaji ili Kigoma iendelee kuwa na sifa yake njema. 

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Filbert Matotay, aliwashukuru watumishi wote wa Mahakama Kigoma kwa ushirikiano waliompatia alipokuwa Mtendaji wa Mahakama hiyo kwa muda wa miaka miwili, ambayo amehudumu katika Kituo hicho.

Hata hivyo, amesema Kigoma ni kituo cha kwanza kuhudumu kwa nafasi ya Mtendaji hivyo, amejifunza mengi kutoka kwa Viongozi na Watumishi wote, na kuwaomba watumishi wampe ushirikiano Mtendaji mpya ya Mahakama hiyo ili aweze kutumika kuanzia pale alipoishia yeye.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na wadau mbalimbali Mahakama na Serikali, watu binafsi, Mashirika, Taasisi binafsi na za Serikali, watumishi kutoka Mahakama za Wilaya sita, kadhalika kulikuwa na bendi ya muziki kwa ajili ya burudani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akitoa cheti kwa mmoja kati ya watumishi wastaafu aliyekuwa akihudumu kwa cheo cha Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Lucas Gervas aliyestaafu utumishi hivi karibuni, Kituo cha Mahakama ya Wilaya Kibondo.

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza (kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Bw. Filbert Matotay na Msaidizi wa Kumbukumbu, Bi. Christina Simoni kwa pamoja wakikata keki ikiwa ni ishara ya kuagana na Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza (wa pili kulia), Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Singida, Bw. Filbert Matotay (wa kwanza kulia) na Mke wa Jaji Rwizile kwa pamoja wakifurahia jambo wakati wa hafla hiyo iliyofanyika tarehe 23 Mei, 2026.

 Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusufu Kasuka (kushoto) pamoja na Mahakimu wapya wa Mahakama za Mwanzo wakikata keki ikiwa ni ishara ya ukaribisho katika Mahakama hiyo.

Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA), Tawi la Kigoma wakimuaga mwenzao Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Projestus Kahyoza nakumtakia kila la kheri katika kituo chake kipya.


Sehemu ya Watumishi na Wadau wa Mahakama waliojitokeza katika hafla ya kuwaaga watumishi na kuwakaribisha watumishi wapya na kuwapongeza watumishi waliostaafu utumishi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma) 

 



Jumanne, 26 Mei 2026

RAIS SAMIA AAHIDI KUENDELEA KUIMARISHA UWEZO NA UFANISI WA MAHAKAMA YA TANZANIA

  •   Ni wakati akiwaapisha Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani
  •   Awataka Majaji hao kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, busara na hofu ya Mungu
  •     Awataka Majaji hao pia kulinda heshima na uhuru wa Mahakama

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa, kwa kutambua umuhimu wa suala la utoaji haki nchini, Serikali imeendelea na itaendelea kuchukua hatua stahiki za kuimarisha uwezo wa Mahakama ya Tanzania ili iweze kusimamia vizuri eneo hilo kwa ufanisi.

Rais Samia ameyasema hayo leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam katika Hafla ya Uapisho wa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani aliowateua tarehe 20 Mei mwaka huu.

“Kwa muktadha huo, uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Rufani ni sehemu ya jitihada hizo za kuongeza ufanisi katika Mhimili huu muhimu. Tumefanya mengine mengi na ninyi ni mashahidi kwamba Mahakama zimebadilika kwa kiasi kikubwa, zimeendelea kwa kiasi kikubwa sana katika miaka hii ya karibuni, kwahiyo sasa ni kuongeza watu wenye dhamira ya kufanya kazi, wenye uwezo wa kufanya kazi lakini wanaosimama kwenye mstari mzuri wa haki,” amesema Mhe. Dkt. Samia.

Rais Samia amesema kuwa, Mahakama ya Rufani ndio ngazi ya juu ya utoaji haki nchini Tanzania, kwahiyo kila uamuzi unaotolewa na Majaji katika Mahakama hiyo una uzito mkubwa si kwa wahusika wa shauri pekee bali pia kwa Taasisi, mwenendo wa jamii na tafsiri pana ya sheria nchini, yote yanawaangalia wao kama Wasimamizi wa Haki nchini.

“Hivyo basi nendeni mkalinde heshima na uhuru wa Mahakama lakini pia muendelee kuimarisha uwajibikaji, nidhamu na maadili ndani ya Mhimili huu muhimu, uhuru huu una umuhimu pale unapoenda sambamba na uadilifu, ufanisi na utendaji wenu unaoangalia uzalendo kwa nchi yenu, mnapotoa maamuzi Taifa kwanza, Nchi kwanza halafu ndio mtaenda kwenye mambo mengine,” ameeleza Mhe. Dkt. Samia.

Akizungumza na Majaji hao mara baada ya kuwaapisha, Mhe. Dkt. Samia amewapongeza Majaji hao kwa kuaminiwa na kuteuliwa kushika wadhifa huo na kuwasisitiza kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, busara na hofu ya Mungu kama viapo vyao vinavyowataka.

“Vilevile niwapongeze Majaji wote mlioapa leo, dhamana mliyopewa ni kubwa na ya heshima kwa Taifa letu katika kuwatumikia wananchi, hongereni sana. Uteuzi wenu unatokana na uzoefu, weledi na utumishi mliuonesha katika kutumikia nafasi zenu mbalimbali mlizotumikia, nazikumbuka sura nyingine hapa nilishaziapisha nadhani leo mara ya pili kama sio ya tatu, ina maana kipindi nilichokuwepo mimi ulishapanda, ukapanda, umepanda katika ngazi hii ya leo...” amesema Rais Samia.

Amesema pia, uteuzi wa Majaji hao ni ishara kwamba wamefanya kazi nzuri na Tume ya Utumishi wa Mahakama imetambua kazi yao na imewapendekeza kupandishwa katika ngazi hiyo, kwahiyo ana imani kwamba kwa heshima hiyo waliopewa Majaji hao, watafanya kazi wa bidii zaidi.

“Nendeni mkaongeze nguvu katika Mahakama ya Rufani, kwa kutambua umuhimu wa haki kama msingi wa amani, utulivu lakini pia maendeleo ya Taifa letu na ustawi wa wananchi kwa ujumla, haki ndio inashinda katika yote haya,” amesisitiza Mhe. Dkt. Samia.

Kadhalika, Rais Samia amewataka Majaji hao kuitumikia Nchi kwa uadilifu, weledi na uzalendo kama walivyoapa, huku akisisitiza kwa kusema kuwa, “mmeapa mtafanya kazi bila upendeleo, huba, chuki. Sasa bila upendeleo, bila upendeleo kwa sababu kazi yenu ina Kanuni zake, sasa kuna hili suala la huba na chuki, hicho ndio ninataka mkajitazame vizuri ndani yenu katika kutoa maamuzi ya hukumu zenu.”

Mkuu huo wa Nchi ameongeza kuwa, dhamana waliyopewa Majaji hao sio ya cheo tu bali pia ni wajibu wa kulinda haki za Watanzania katika maamuzi yote wanayofanya wakumbuke kuwa kwa kuwatumikia Wanadamu ni kumtumikia Mungu.

“Nimeshawaambia mara kadhaa kwamba kwa hapa duniani, ukiacha Mungu anayesimamia haki za wote, wengine ambao Mungu amewateua kusimamia haki za wenzenu ni ninyi Majaji, katika ngazi zenu tofauti tofauti. Kwahiyo mnafanya kazi kubwa na mna dhima kubwa kwa Nchi hii katika kutenda haki, kuhakikisha haki za wananchi zinapatikana lakini si tu za wananchi hata haki ya kusimamia Taifa lenu iko mikononi mwenu, kwahiyo wale wenzetu wanasema ‘the service to humanity is serving to God’ mnapohudumia wananchi kusimamia haki mnatumikia kazi ya Mungu pia,” amesisitiza Rais Samia.

Majaji walioapishwa ni Mhe. Imani Daudi Aboud, Mhe. Rabia Hussein Mohamed, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha, Mhe. Yohane Bokobora Masara, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba na Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim.

Kwa mujibu wa taarifa ya Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert, baada ya uapisho wa Majaji hao tisa (9), idadi ya Majaji wa Rufani imeongezeka kutoka 37 hadi 46 sawa na majopo 15.

Viongozi mbalimbali wamehudhuria katika hafla ya uapisho ambao ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera (Mb), Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Mhe. Daniel Sillo (MB), Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila na wengine.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Imani Daudi Aboud kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Imani Daudi Aboud akila kiapo mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Rabia Hussein Mohamed kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Rabia Hussein Mohamed akiapa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
 

Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina akiapa mbele ya Rais Samia kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Immaculata Kajetan Banzi kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
 
  Mhe. Immaculata Kajetan Banzi akiapa mbele ya Rais Samia kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe.Cyprian Phocas Mkeha kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
   
  Mhe. Cyprian Phocas Mkeha akiapa mbele ya Rais Samia kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

   Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Yohane Bokobora Masara kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Yohane Bokobora Masara akiapa mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
   
   Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo akiapa mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Abdi Shaaban Kagomba 
kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini hati ya kiapo cha Jaji Kagomba baada ya kumuapisha yeye pamoja na wenzake nane kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Ibrahim Mzee Ibhrahim akiapa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Makamu  wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi (wa kwanza kushoto), Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kushoto), Jaji Mkuu wa Zanzibar, 
Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah (wa pili kulia) na Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Mhe. Daniel Sillo (wa kwanza kulia) wakiwa katika Hafla ya Uapisho wa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Majaji na Watanzania kwa ujumla mara baada ya kuwaapisha Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Sehemu ya Viongozi mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria hafla ya Uapisho wa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija, katikati ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani walioapishwa leo tarehe 26 Mei, 2026 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Ikulu jijini Dar es Salaam.

Kamishna wa Maadili nchini Tanzania (Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma), Jaji Mstaafu Sivangilwa Sikalalilwa Mwangesi akiwaongoza Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani kula kiapo cha Maadili mara baada ya kuapishwa kushika wadhifa huo leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani wakila kiapo cha maadili ya utumishi wa umma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) pamoja na Viongozi wengine walioketi wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani mara baada ya kuapishwa kwao leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam. Wa tatu kushoto ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, wa tatu kulia ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, wa pili kushoto ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah, wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, wa pili kulia ni Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Mhe. Daniel Sillo (Mb) na wa kwanza kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera.

Meza Kuu katika picha ya pamoja na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya Majaji wengine wa Mahakama hiyo na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.


Meza kuu ikiongozwa na Rais Samia (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya Viongozi wa Mahakama waliohudhuria Hafla ya Uapisho wa Majaji hao leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Picha ya pamoja Meza Kuu, Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na Viongozi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS).

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

































 

 


TMJA SONGEA YAFANYA MKUTANO WA ROBO YA KWANZA 2026

Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea

Chama cha Mahakimu na Majaji Songea tarehe 22 Mei 2026 kilifanya mkutano wa robo ya kwanza ya mwaka 2026, ikiwa ni kutekeleza matakwa ya Katiba yaliyowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mkutano huo uliofanyika kwenye ukumbi wa Heritage Cortage (Padogo Pazuri) ulioko Msamala Songea Mjini ulifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, ambaye ndiye mlezi wa chama hicho kwenye Mkoa wa Ruvuma.

Mkutano huo ulio hudhuliwa na Wanachama 58 kutoka Mahakama Kuu Songea (5), Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea (2), Mahakama ya Wilaya Songea (15), Mahakama ya Wilaya Mbinga (11), Mahakama ya Wilaya Namtumbo (10), Mahakama ya Wilaya Tunduru (10) na Mahakama ya Wilaya Nyasa (5).

Katika mkutano huo, Wanachama walijadili malengo ya TMJA Songea, ikiwemo kukuza uhuru wa Mahakama kama msingi wa kulinda haki za binadamu na uhuru, kukuza haki, maslahi na ustawi wa wanachama.

Malengo mengine ni kukuza na kulinda heshima ya ofisi ya Mahakimu na Majaji, kuongeza au kuimarisha ujuzi na uelewa wa Mahakimu na Majaji katika majukumu yao kwa kuendeleza tafiti na elimu (kuwajengea uwezo) na kutoa tuzo kwa Wilaya itakayofanya vizuri ili kuenzi kazi zao.

Katika mkutano huo, Katibu wa TMJA Songea, Mhe. Shughuli Mwapashe, alisoma tarifa fupi ya chama na kugusia vipengele mbalimbali kama mahusiano ya TMJA na Mwajili, mafunzo na semina kwa Wanachama, mafanikio pamoja na changamoto.

“Mafanikio ni pamoja na kuimarisha uhusiano uliobora kati ta TMJA na Mwajiri, kutoa elimu kwa umma kila jumatano katika kituo cha redio (selous fm) na kwenye viunga vya Mahakama, kabla ya kuanza kusikiliza mashauri na uanzishwaji wa kamati ya kuandaa majarida na elimu.

Alieleza changamoto zilizopo katika chama kama vile baadhi ya Wanachama kukosa hamasa ya chama pamoja na ufinyu wa bajeti, jambo ambalo limekuwa likisababisha Tawi kishindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu na kwa wakati.

Katibu huyo aliahidi kutimizaa kwa vitendo vigezo maalum vya kupima utendaji na ubora wa mfumo wa Mahakama kama ilivyoelekezwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, katika hotuba yake ya tarehe 13 Januari, 2026 wakati wa kufungua mkutano mkuu wa TMJA jijini Dodoma.

Vigezo hivyo ni uadilifu, uwezo wa kutekeleza majukumu kwa ufanisi, kuwiwa kuona haki inatendeka, ubunifu, uchukuaji wa hatua mapema, uzalendo na kuzingatia uhalisia wanapotekeleza majukumu yao.

Mgeni maalum katika mkutano huo, Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma, Bi. Marry Makondo, katika hotuba yake aliwapongeza Mahakamu na Majaji kwa kusaidia kwenye upatikanaji wa haki kwa wakati.

Katika hotuba yake, Mhe. Karayemaha aliwasisitiza wanachama kujitoa katika kushiriki matukio yanayohusiana na chama na kushirikiana kwa hali na mali.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha wakati wa kufungua mkutano wa TMJA Tawi la Songea.

Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe. (aliye simama).

Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma, Bi. Marry Makondo, akitoa hotuba kwa Wanachama wa TMJA Tawi la Songea.

Mwenyeki wa TMJA Tawi la Songea, Mhe. Saada tagalile,  wakati akitambulisha meza kuu.

Katibu wa TMJA Tawi la Songea, Mhe. Shughuli Mwampashe.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama Kuu Songea (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Songea (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Mbinga (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Nyasa (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Namtumbo (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Tunduru (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.