Jumanne, 3 Machi 2026

KAZI KUPATA KAZI, ITUNZENI KAZI ILI MUWE WATUMISHI WENYE TIJA MAHAKAMANI; JAJI RWIZILE

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka watumishi wapya wa Mahakama hiyo kuzingatia maadili na umoja katika kutimiza majukumu yao huku wakitanguliza mbele uwajibikaji wa kiwango cha juu katika utumishi wao.

Mhe. Rwizile ametoa wito huo leo tarehe 03 Machi, 2026 ofisini kwake katika mazungumzo aliyofanya na watumishi hao wapya tis awa kada mbalimbali mara baada ya kupokelewa.

“Ninyi ambao mmepata kazi leo mmeona ilivyo kazi kupata kazi, hivyo itunzeni kazi kwa maadili ya hali ya juu, mkiwa kielelezo kazini na mtaani ambapo jamii inatarajia kuona mtumishi wa Mahakama mwenye maadili mazuri na mfano kwa watu wengine,” amesema Mhe. Rwizile.

 Jaji Mfawidhi huyo amesisitiza kuwa, mtumishi yoyote wa Mahakama anayo dhamana katika mnyororo wa utoaji haki, ambalo ni jukumu zito linalohitaji nidhamu, uaminifu na weledi wa hali ya juu, na kuwa watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa kuzingatia misingi ya sheria, kuepuka tabia zisizofaa kwa mtumishi wa umma.

Aidha, amewataka pia watumishi hao kujenga umoja na mshikamano na kuwahimiza kujifunza kwa watumishi watakaowakuta katika vituo watakavyopangiwa kazi, huku akisisitiza kuwa nguvu ya Mahakama ipo katika ushirikiano, uwajibikaji na kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni na taratibu zilizowekwa.

Kwa upande wake Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay amewahakikishia watumishi hao mazingira wezeshi ya kazi ikiwemo vifaa na miundombinu itakayowawezesha katika utendaji kazi wao pahala pa kazi.

Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Yohana Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay na Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile  akizungumza na watumishi wapya wa Mahakama wa Kada mbalimbali walioajiriwa hivi karibuni na kupangiwa Mahakama Kigoma (hawapo katika picha).

Sehemu ya Watumishi wapya wa Mahakama waliopangiwa Kigoma wakifuatilia kwa makini maelekezo aliyokuwa akiyatoa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (hayupo katika picha).

Mtumishi mpya wa Mahakama Kanda ya Kigoma wa Kada ya Udereva, 
Bw. Azizi Saburi Gilla akijitambulisha kwa Viongozi wa Kanda hiyo.

Sehemu ya watumishi wapya tisa wakifuatilia maelekezo ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (hayupo katika picha).

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay (kulia) akiteta jambo  na Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga wakati wa mazungumzo na watumishi wapya wa Mahakama Kanda hiyo leo tarehe 03 Machi, 2026.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



 

SUMBAWANGA WASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

Na. Fredrick Mahava- Mahakama, Sumbawanga

Watumishi Wanawake wa Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga wameshiriki katika Maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani kwa kushiriki katika shughuli mbalimbali kama vile kufanya matendo ya huruma na kushiriki mafunzo ya ujasiriamali.

 Maadhimisho hayo ya mwaka 2026 yanafanyika na kuadhimishwa kuanzia ngazi ya Kata. Kwa upande wa Kata ya Katandala maadhimsho hayo yamefanyika tarehe 2 Machi 2026 yakiongozwa na Diwani wa Kata hiyo Mhe. Edwin Misasi.

Maadhimisho hayo yalianza kwa Maandamano yaliyoanzia Ofisi ya Kata ya Katandala kuelekea katika kituo cha kulelea watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi cha Bethania ambapo mahitaji mbalimbali ya watoto yalitolewa.

Kwa upande wake Mhe. Deontinta Kashaija ambaye alikuwa Mkuu wa Msafara wa Watumishi wanawake wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wakati anakabidhi mahitaji kwa watoto alisema, walichanga pesa ili kufanikisha upatikanaji wa mahitaji hayo na pia waliwashirikisha baadhi ya wanaume ambao waliguswa na kuchangia na hivyo kuweza kupatikana kwa mahitaji hayo.

Naye, Mkurugenzi wa Kituo cha Bethania aliwashukuru wanawake wote kwa kuwaletea watoto hao mahitaji muhimu ambayo yatawasaidia. Vilevile aliwaomba wawe wanakuja kuwatembelea watoto hao mara kwa mara kwani watoto hao wanafarijika wanapotembelewa na watu mbalimbali.

Aidha, alieleza kuwa wana Vituo viwili vya watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu yaani kile cha watoto wadogo wa chini ya miaka 10 na kile cha watoto kuanzia miaka 10 na kuendelea.

Baada kumaliza kutoa mahitaji kwa watoto wa kituo cha Bethania maandamano hayo yalielekea katika Ofisi ya Tarafa ya Lwiche ili kuendana na kauli mbiu ya mwaka isemayo “Haki kwa wanawake na wasichana: msingi wa Maendeleo Jumuishi kufikia Dira 2050” Wanawake walikusanyika katika ukumbi uliopo ofisi ya taarafa ya Lwiche na kupewa mafunzo mbalimabali kuhusu ujasiliamali, elimu kuhusu malezi na makuzi ya watoto na elimu kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika maeneo jamii.

Vilevile Taasisi za kifedha kama NMB walipata fursa ya kutoa elimu kwa wanawake kuhusu mikopo ya masharti nafuu inayotolewa kwa vikundi mbalimbali na namna gani wanawake wanaweza kunufaika na fursa hizo. Pia walipata wasaa wa kujua fursa ya mikopo inayotolewa na Serikali na kusimamiwa na benki ya NMB ambayo kipaumbele chake wanapewa wanawake.

Nao Jeshi ya Zimatoto na Uokoaji walitumia jukwaa hilo kutoa elimu kwa wanawake kuhusu mambo mbalimbali yanayohusu namna ya kupambana na majanga ya moto kuanzia ngazi ya familia na kuelezea huduma muhimu zinazotolewa na Jeshi hilo  ikiwa ni pamoja namna ya kutoa taarifa kwa Jeshi hilo pindi unapopata majanga ya Moto.

Aidha, wakati wa Mafunzo hayo wanawake walipata wasaa wa kuuliza maswali mbalimbali kwa kila mada iliyofundishwa na wawezeshaji walitoa ufafanuzi ili kuongeza uelewa kwa washiriki wa mafunzo hayo. Baada  ya mafunzo wanawake walihimizwa kushiriki kilele cha siku ya wanawake duniani itayofanyika tarehe 08 Machi 2026.

Picha ya watumishi wanawake wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wakati wa maadhimisho ya siku ya wanawake katika Kata ya Katandala Sumbawanga Mjini.

Afisa kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji akitoa elimu kuhusu namna ya kupambana na majanga ya moto wakati wa sherehe ya siku ya wanawake kwa Kata ya Katandala Sumbawanga.

Picha ya Pamoja kati ya viongozi wa Kata ya Katandala na wanawake waliohudhuria katika siku ya wanawake.

Picha ya pamoja kati ya Watoto wa kituo cha Bethania na wanawake waliopeleka mahitaji mbalimbali kwa watoto hao.

Afisa Maendeleo ya Jamii Bi. Shukrani Sijaona akitoa mafunzo kuhusu ujasiliamali kwa wanawake waliohudhuria katika sherehe ya siku ya wanawake katika kata ya Katandala Sumbawanga

Diwani wa Kata ya Katandala Mhe. Edwin Misasi akifungua mafunzo kwa wanawake waliohudhuria katika sherehe ya siku ya wanawake katika kata ya Katandala Sumbawanga.

Mheshimiwa Deontina Kashaija akizungumza kwaniaba ya wanawake wakati wanakabidhi  mahitaji kwa watoto wa kituo cha bethania.


WATUMISHI WASHAURIWA KUKOPA NBC KWAKUWA INA MASHARTI NAFUU

Na. Hilary Lorry – Mahakama, Lindi

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi wameombwa kuchukua mikopo katika Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa sababu benki hiyo imeingia Mkataba maalumu na Mahakama ya Tanzania kutoa mikopo hiyo kwa riba nafuu.

Taarifa hiyo ilitolewa hivi karibuni wakati wa Mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi baina ya wataalam kutoka Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Lindi.

Akizungumza wakati wa Ufunguzi wa kikao hicho Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe. Consolata Peter Singano alisema kuwa, Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imeingia mkataba maalum na Mahakama ya Tanzania juu ya utoaji wa Mikopo yenye masharti nafuu kwa watumishi wa Mahakama ya Tanzania.

Mhe.Singano aliwataka watumishi wa Mahakama hizo kuchangamkie fursa hiyo ya mikopo yenye masharti nafuu kwaajili ya kufanyia shughuli za maendeleo, kuliko kuchukua mikopo kwenye taasisi za fedha zenye riba kubwa.

Naye, Meneja wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Tawi la Lindi, Bw. Iovan Mapunda wakati wa uwasilishaji wa mada katika mkutano huo alisema kwamba Benki hiyo ilianzishwa rasmi Mnamo mwaka 1967 huku akipambanua kuwa benki hiyo ina hazina kubwa ya historia katika upande wa utoaji wa huduma bora za kibenki hapa Tanzania, pia akieleza kuwa benki hiyo ina bidhaa (products) nyingi za huduma kwa wateja wake.

Aidha, Meneja huyo alisisitiza kuwa endapo Mtumishi wa Mahakama ataamua ku pitisha mshahara wake benki ya NBC atapata Mkopo kwa asilimia 14 badala ya asilimia 17 ambazo zimezoeleka na zinazoonekana katika mfumo wa watumishi portal (ess),vilevile alieleza kuwa mkopo huo unaenda hadi miaka 65 kwa watumishi wa kawaida na miaka 80 kwa Majaji  na yote hayo ni kutokana na Mkataba maalum ulioingiwa kati ya benki hiyo na Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande wake, Afisa Uhusiano kutoka Makao Makuu ya Beki hiyo Bw. Peter Mwasomola, aliongeza kuwa benki hiyo inatoa mikopo maalum kwa kuwakopesha watumishi wa Mahakama fedha kwa ajili ya kununua hati fungani za Serikali.

Vilevile, aliongeza kuwa, benki hiyo inatoa mikopo ya haraka (Chap chap loan) kupitia simu ya Mkononi yaani Salary Advance hadi asilimia 50 ya mshahara wako na kikubwa zaidi unaweza kuchukua mkopo huo kwa muda wa hadi miezi 12.

 Bw. Mwasomola aliwataka watumishi wa Mahakama ya Tanzania kufika katika ofisi za NBC kuchukua mikopo hasa ya muda mrefu ili kuitumia katika shughuli zao za maendeleo. “Kukopa siyo kubaya ila kukopa bila malengo ndiyo kubaya” alisistiza Bw. Mwasomola.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano (aliyefunga kilemba katikati) akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Mkutano huo.

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Lindi wakifuatilia mada zilizowasilishwa na wataalamu wa fedha kutoka benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa umakini Mkubwa.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Godfrey Mbeyela akitoa neo la utangulizi na ukaribisho kwa wataalamu kutoka Benki ya Taifa ya Biashara na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Lindi.

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Lindi wakifuatilia mada zilizowasilishwa na wataalamu wa fedha kutoka benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa umakini Mkubwa.

Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe. Khalfan O. Khalfan  akichangia mada katika mkutano huo.

Meneja wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) tawi la Lindi  Bw. Iovan Mapunda aliyenyoosha mkono akifafanua jambo wakati wa mkutano uliowakutanisha benki ya NBC na watumishi wa Mahakama ya Lindi.



WADAU WAWEKA MKAKATI MPYA KUIMARISHA UTOAJI HAKI 2026

  • Jaji Mkuu asema uwajibikaji, mageuzi ya kiutendaji ili kulinda imani ya wananchi

Na HALIMA MNETE &  JAMES BUSANYA-Mahakama,  Dodoma

Mkutano wa kwanza wa mwaka 2026 kati ya Mahakama ya Tanzania na Wadau wa sekta ya haki jinai umefanyika jana tarehe 2 Machi, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania jijini Dodoma.

Lengo la mkutano huo ni kupitisha tathmini ya utekelezaji wa mikakati iliyokubaliwa hapo awali na kuweka mwelekeo wa pamoja katika kuimarisha ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani.

Mkutano huo uliongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, huku Mgeni Rasmi akiwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Akifungua mkutano huo, Jaji Mkuu alisisitiza kuwa uimara wa mnyororo wa haki jinai unategemea kwa kiasi kikubwa uwajibikaji wa kila Taasisi katika kutekeleza wajibu wake kwa wakati, kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi.

Alieleza kuwa haki inapocheleweshwa huathiri si wahusika wa shauri pekee, bali pia hupunguza imani ya wananchi kwa mfumo mzima wa utoaji haki.

Katika kikao hicho, Wadau mbalimbali waliwasilisha taarifa za utekelezaji wa majukumu yao pamoja na changamoto wanazokutana nazo katika utekelezaji wa mkakati wa haki jinai.

Bi. Singwa Mokiwa, aliyemwakilisha Kamishna Mkuu wa Uhamiaji, alieleza kuwa Taasisi ya Uhamiaji imeendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria na maadili ya utumishi wa umma.

Alisema Taasisi hiyo inahakikisha watuhumiwa wanafikishwa mahakamani kwa wakati, vielelezo vinawasilishwa ipasavyo na amri za Mahakama zinatekelezwa bila kuchelewa.

Hata hivyo, alibainisha changamoto zikiwemo ucheleweshaji wa usajili wa majalada katika baadhi ya maeneo, upungufu wa wakalimani na ucheleweshaji wa upatikanaji wa mashahidi, hali inayoweza kusababisha watuhumiwa kukaa mahabusu kwa muda mrefu zaidi.

Kwa upande wake, Bi. Alice Mtulo kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali aliwasilisha tathmini ya mashauri ya kikatiba na haki za binadamu yenye viashiria vya jinai yanayosimamiwa na ofisi hiyo. Alieleza kuwa katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2025, ofisi ilisajili mashauri 1,693 ya madai, ambapo 216 yalikuwa mashauri ya kikatiba na haki za binadamu, yakiwemo mashauri ya uchaguzi.

Bi Alice pia alibainisha kuwa changamoto kubwa ni ucheleweshaji wa upatikanaji wa taarifa kutoka Taasisi mbalimbali za Serikali wakati wa kuandaa majibu ya utetezi, pamoja na ufinyu wa muda wa siku 14 uliowekwa kwa mujibu wa kanuni za mashauri ya kikatiba na haki za binadamu.

Aidha, alieleza changamoto ya matumizi ya hati za dharura katika baadhi ya mashauri bila kuwepo utaratibu madhubuti wa kuthibitisha udharura wake, jambo linaloweza kuathiri maandalizi ya kina ya utetezi wa Serikali.

Ofisi hiyo imeweka mikakati ya kuimarisha mafunzo kwa Mawakili wa Serikali, kuboresha mawasiliano kupitia mfumo wa usimamizi wa mashauri (CMIS) na kuanzisha mifumo ya kupata taarifa za mashauri kwa njia ya simu za kiganjani.

Vilevile, Mkurugenzi Divisheni ya Uaimamizi wa Kesi na Uratibu wa Upelelezi, Bw. Siraji Iboru, alisema kikao hicho kilipitia na kuthibitisha utekelezaji wa mikakati minane iliyokubaliwa katika kikao kilichopita.

Alieleza kuwa ofisi hiyo hufanya vikao vya kila Wiki kwa ajili ya tathmini ya utendaji na utoaji wa maelekezo kwa watumishi wake. Alibainisha kuwa mlundikano wa kesi umepungua na kiwango cha ushindi wa kesi kimeongezeka na kufikia asilimia 84.

Hata hivyo, alieleza kuwa bado kuna changamoto ikiwemo baadhi ya Wilaya kukosa Magereza na uhaba wa Waendesha Mashtaka katika maeneo kadhaa.

Naye Kamishna wa Jeshi la Magereza, Afande Nicodemus Tenga, alieleza   kuwa Jeshi limeendelea kuimarisha uwajibikaji kwa kuingiza maudhui ya uwajibikaji katika mitaala ya mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi kwa Askari na Maofisa wake.

Aidha, vituo 181 vya Magereza tayari vimeunganishwa na Mahakama kwa njia ya mtandao, hatua inayorahisisha ufuatiliaji wa mashauri na upatikanaji wa taarifa kwa wakati.

Jeshi hilo pia linaendelea kusimika mfumo wa taarifa za Wafungwa unaounganishwa na Taasisi mbalimbali, ikiwemo NIDA, NECTA, Mahakama na Jeshi la Polisi. Pamoja na jitihada hizo, changamoto ya ukosefu wa Magereza katika baadhi ya Wilaya imeelezwa kuongeza gharama za usafirishaji wa Wafungwa.

Kwa upande wake, Bw. Joseph Kisusi, ambaye ni Kamishna Msaidizi Kanda ya Kati Dodoma na Mwakilishi wa Kamishna Jenerali, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, alisema ofisi hiyo imeendelea kuwajengea uwezo watumishi wake na kuimarisha maadili katika utekelezaji wa majukumu.

Alieleza kuwa kamati maalum zimeanzishwa kwa ajili ya kufuatilia na kusimamia maadili ya watumishi, huku wakisisitizwa kuheshimu hadhi na mamlaka ya Mahakama wanapotekeleza majukumu yao.

Katika mkutano huo pia, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bonaventure Mwabukusi, alisema chama hicho kimeendelea kusimamia kwa ukali maadili ya taaluma ya uwakili, hususan kwa Mawakili wanaochukua fedha za wateja bila kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa makubaliano.

Alieleza kuwa TLS imekuwa ikiwalazimisha Mawakili watakaobainika kukiuka maadili kurejesha fedha kwa wateja wao pamoja na kuchukuliwa hatua stahiki za kinidhamu kwa mujibu wa Katiba na kanuni za chama. Alisisitiza kuwa chama hicho hakitavumilia vitendo vinavyodhalilisha taaluma ya uwakili na kuathiri imani ya wananchi kwa mfumo wa haki.

Aidha, alisema TLS inaendelea kutoa elimu ya maadili kwa Mawakili ili kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Katiba, sheria na kanuni za taaluma, pamoja na kuheshimu ukuu na hadhi ya Mahakama.

Alibainisha kuwa chama hicho kimeimarisha ushirikiano na Wadau wa mnyororo wa haki jinai, kinaendelea kutoa mafunzo ya maadili kwa Mawakili wapya na kusisitiza umuhimu wa msaada wa kisheria kwa wasiojiweza ili kuendeleza dhana ya usawa mbele ya sheria.

Wakili Mwabukusi pia alisema TLS inakaribia kukamilisha matumizi ya mifumo ya kidijitali itakayowezesha mawasiliano na ushirikiano wa karibu zaidi na Wadau wa sekta ya haki jinai.

Hata hivyo, alitaja changamoto zinazoikabili taaluma hiyo kuwa ni pamoja na vitisho dhidi ya Mawakili, masuala ya ulinzi na uhuru wa taaluma ya uwakili. Alisisitiza kuwa Wakili anapomtetea mteja mahakamani haimaanishi anahusika na kosa analodaiwa mteja wake, bali anatekeleza wajibu wake wa kisheria wa kuhakikisha haki inapatikana kwa mujibu wa sheria.

Kwa ujumla, mkutano huo umeonesha dhamira ya pamoja ya kuimarisha uwajibikaji, maadili na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Taasisi zote za mnyororo wa haki jinai.

Wadau walikubaliana kuwa ushirikiano wa karibu, mawasiliano ya wazi na utekelezaji wa majukumu kwa weledi ndivyo vitakavyoendelea kuimarisha utoaji haki na kulinda imani ya wananchi kwa mfumo wa Mahakama nchini

Mkutano huo umehitimishwa kwa msisitizo kwamba utoaji haki ni dhamana ya pamoja ya Taasisi zote katika mnyororo wa haki jinai, na kwamba uwajibikaji, maadili na ushirikiano wa karibu ndivyo vitakavyoendelea kuimarisha imani ya wananchi kwa mfumo wa Mahakama nchini.

Bi. Singwa Mokiwa, aliyemwakilisha Kamishna Mkuu wa Uhamiaji.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Bw. Crispin Chalamila.

Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo.

Kamishna wa Jeshi la Magereza, Afande Nicodemus Tenga.

Kamishna Msaidizi Kanda ya Kati Dodoma na Mwakilishi wa Kamishna Jenerali, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Bw. Joseph Kisusi. 

Mkurugenzi Divisheni ya Usimamizi wa Kesi na Uratibu wa Upelelezi, Bw. Siraji Iboru.


Wadau wakichukua kumbukumbu kwenye mkutano huo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.



 

 

MAHAKAMA YA TANZANIA YAANZA MWAKA 2026 KWA KUIMARISHA USHIRIKIANO NA WADAU

  • Msajili Mkuu asema ushirikiano, mahusiano imara ni msingi wa utoaji haki

Na Halima Mnete-Mahakama, Dodoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, jana tarehe 2 Machi, 2026 amezungumza na Waandishi wa Habari kuhusu mkutano wa kwanza wa mwaka 2026 kati ya Mahakama na Wadau wa haki jinai, uliolenga kuimarisha ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani.

Akizungumza katika mkutano huo katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Nkya alisema kuwa kikao hicho ni mwendelezo wa makubaliano yaliyofikiwa tarehe 24 Septemba, 2025. Katika kikao hicho, Mahakama na Wadau walikubaliana kuweka mikakati tisa ya pamoja, ikiwemo kufanya vikao mara nne kwa mwaka ili kuimarisha uratibu na mawasiliano katika mnyororo wa haki jinai.

Alisema kuwa mkutano huo wa kwanza kwa mwaka 2026 umejikita katika tathmini ya utekelezaji wa mikakati iliyowekwa pamoja na kuweka mwelekeo wa pamoja kwa mwaka, kwa lengo la kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa ufanisi na kwa wakati.

“Utoaji haki ni jukumu la pamoja, Mahakama haiwezi kufanya kazi peke yake bila ushirikiano madhubuti wa Wadau wote katika sekta ya haki jinai. Mahusiano yetu ya kikazi ndiyo msingi wa kuongeza ufanisi na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama,” alisema.

Akiwasilisha mafanikio yaliyopatikana kupitia ushirikiano huo, Msajili Mkuu alieleza kuwa katika kipindi cha Septemba hadi Desemba 2025, mashauri 30,076 yalifunguliwa huku mashauri 38,639 yakimalizika, sawa na asilimia 128 ya mashauri yaliyofunguliwa katika kipindi hicho.

Kwa mwaka mzima wa 2025, mashauri ya jinai 138,368 yalifunguliwa katika ngazi zote za Mahakama na mashauri 145,467 yalimalizika, sawa na asilimia 105 ya mashauri yaliyofunguliwa. Kutokana na hali hiyo, Mahakama ilifunga mwaka ikiwa na mashauri 14,172 pekee yanayoendelea, ambapo asilimia 75 ya mashauri hayo yana umri usiozidi miezi sita.

Aidha, Mhe. Nkya alieleza kuwa ushirikiano huo umeimarisha matumizi ya mifumo ya kidigitali, hususan mfumo wa JOT-eCMs ambao umeunganishwa na mifumo ya Wadau mbalimbali ili kurahisisha usimamizi na ufuatiliaji wa mashauri. Kupitia mfumo wa Mahakama Mtandao, mashauri 24,662 yalisikilizwa katika kipindi cha Januari hadi Desemba 2025.

Vilevile, aligusia kutungwa kwa Kanuni katika Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, ambazo zimempa haki mshtakiwa kupewa ushahidi wa upande wa mashtaka mapema, hatua ambayo imeongeza uwazi na kuharakisha usikilizaji wa mashauri.

Akihitimisha, Msajili Mkuu alisisitiza kuwa Mahakama itaendelea kuimarisha mahusiano ya kikazi na Wadau wake kwa mwaka 2026, kwa lengo la kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati, kwa uwazi na kwa kuzingatia misingi ya sheria, huku akiipongeza vyombo vya habari kwa mchango wao katika kuhabarisha umma kuhusu masuala ya haki na sheria.


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo kwenye picha).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.



Jumatatu, 2 Machi 2026

JAJI MKUU ASISITIZA UTAWALA WA SHERIA NA USHIRIKIANO WA KIKATIBA

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amezitaka Taasisi za Haki Jinai kudumisha ushirikiano katika kutekeleza mikakati ya Haki Jinai ili kuendelea kufanikisha upatikanaji wa Haki kwa haraka katika jamii sambamba na kudumisha utawala wa sheria na ushirikiano wa kikatiba ili kuleta amani, ustawi na maendeleo katika Taifa.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 02 Machi, 2026 alipokuwa akifungua na kufunga mkutano wa kwanza kwa Mwaka 2026 wa Wadau wa Haki Jinai, uliofanyika katika ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, ushirikiano uliopo umejengwa katika wajibu wa kila Taasisi na kwamba wajibu wa Kikatiba na Kisheria wa kila Mdau wa Haki Jinai ndio unaozalisha ushirikiano huo, huku akirejea Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa uzinduzi wa Bunge la 13 mnamo tarehe 14 Novemba, 2025 ambapo Rais Samia  alisema kwamba, "msingi wa mafanikio yote ya nchi unategemea utawala wa sheria ikiwa ni pamoja na kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili haki ipatikane kwa wote mapema ipasavyo."

“Ushirikiano huu tulionao pia umejengwa katika wajibu wetu, wote hapa wajibu wetu ni wa kikatiba na kisheria, utekelezaji wa Sheria au Katiba unazalisha ushirikiano, lakini pia tunashukuru kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye kwa mujibu wa Katiba pia ndiye Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu amekuwa akisistiza juu ya ushirikiano huu wa Mahakama na Wadau wake,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Kadhalika, Jaji Mkuu ameendelea kuutambua mchango wa Jukwaa la Haki Jinai katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu kama ambavyo Mhe. Dkt. Samia alivyosisitiza katika hotuba yake ya kufungua Bunge kuhusu umuhimu wa jukwaa la Haki Jinai ambapo alisema kwamba, Serikali itaendelea kufanya mageuzi na maboresho katika Taasisi zote zinazoshughulikia masuala ya Haki Jinai ili ziweze kukabiliana na vitendo vya uhalifu jambo linaloonesha umuhimu wa Taasisi hizi katika utekelezaji wa Utawala wa Sheria ambao umewekwa kwenye Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, Mahakama iko tayari kuendelea kushughulikia changamoto ambazo zimeonekana kukwamisha utekelezaji wa mikakati iliyowekwa, kwa kuzingatia mikakati iliyowekwa ili kushughulikia changamoto hizo na kila Taaasisi inahusika kuzirekebisha changamoto hizo mapema ipasavyo.

“Tutaendelea kuwa tayari kushughulikia zile changamoto ambazo tulikuwa tunaziona zinatukwamisha lakini kwa kuzingatia ile mikakati ambayo tumeiweka ya kushughulikia hizo changamoto kwa hiyo hizo changamoto zinazojitokeza kila Taasisi inayohusika twende tukazirekebishe mapema ipasavyo na matokeo au tija yaanze kuonekana mapema,”ameeleza Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, kila mtu katika jamii anao wajibu wa kuifuata na kuitii Katiba na Sheria za nchi, kwa kufuata utaratibu uliowekwa, kadhalika kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na Sheria za nchi, huku akiwataka Mawakili wa Kujitegemea wanapowakilisha watu fulani, wasichukuliwe kama wahusika wa tuhuma, bali wapewe ushirikiano ili na wao waweze kutimiza majukumu yao ya kikatiba.

Akirejea hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa mwaka 2026 tarehe 02 Februari mwaka huu alisisitiza kuhusu wadau kushirikiana na Mahakama katika suala la utoaji haki, huku akizitaja faida zake kuwa ni, kuongeza kasi ya utoaji haki, kulinda uhuru na ukuu wa Mahakama na heshima yake, kupunguza migogoro ya kiutendaji ambayo waathirika ni wananchi, kuimarisha imani ya umma kwa mfumo wa utoaji haki, kukuza Utawala wa Sheria, kuzuia migogoro ya kimaslahi.

Faida nyingine alizozitaja ni pamoja na kurahisisha utekelezaji wa maamuzi ya Mahakama ambapo lengo kuu ni ustawi wa wananchi kama ambavyo inaelezwa vizuri katika Ibara ya 8(1)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasema lengo kuu la Serikali ni ustawi wa wananchi, huku ripoti ya Msajili Mkuu ya utendaji wa shughuli za kazi za Mahakama kwa mwaka 2025 ikithibitisha faida zilizoletwa na mahusiano na ushirikiano mzuri baina ya Mahakama na Wadau katika kuyafikia mafanikio.

Aidha, Mhe. Masaju ameongeza kuwa, ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu si jambo la hisani wala maelewano ya kirafiki bali ni takwa la kikatiba, kisheria na kisera hivyo wadau wote watenge muda wao kuhudhuria katika vikao, isipokuwa kwa sababu za msingi za kutohudhuria na ikitokea hivyo watume wawakilishi kwa sababu katika vikao ndipo changamoto za utekelezaji na mafanikio ya kila Taasisi yanapoonekana.

Akizungumza kuhusu maana ya haki, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, Haki ni uamuzi unaofanywa na Mahakama kwa kuzingatia na kutekeleza masharti ya Katiba na Sheria kwa mujibu wa ushahidi ulioletwa mahakamani huku akisisitiza Taasisi zinazohusika kujitahidi ushahidi uwe unaojitosheleza.

“Kwa maana hiyo, basi tujitahidi kwa Taasisi zinazohusika zinapokusanya ushahidi, ushahidi uwe ule unaotosheleza kufanya kesi iende mahakamani na Mahakama inapofanya maamuzi kama mtu hakuridhika akate rufaa vinginevyo Mahakama ndio ina jukumu la kutamka hiyo haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akisisitiza kuhusu ushirikiano, Mhe. Masaju amesema kwamba, majukumu ya utoaji haki hayaihusu Mahakama peke yake, hivyo kila Taasisi inapaswa kutekeleza wajibu wake akirejea hotuba ya Rais Samia katika Siku ya Sheria mwaka 2026 ambapo alisema na kuagiza kutoa haki kwa kuzingatia masharti yaliyoainishwa katika Ibara ya 107A(2)(a)(e) na 107B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuheshimu na kuulinda uhuru wa Mahakama bila kuutumia vibaya, kutotumia uhuru huo kama kichaka cha kuficha uzembe na vitendo visivyo vya haki.

Pia kutenda kwa uadilifu na kwa uwazi, kuendeleza suala la usimamizi wa dhamana ili kuhakikisha kuwa, watuhumiwa wenye stahili ya kupata dhamana wanapata dhamana kwa mujibu wa sheria, pia wadau wote wa Mahakama katika suala la dhamana kuunga mkono jitihada za Mahakama katika suala la dhamana.

Kadhalika kuendeleza kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia, pia wadau wa haki kuendelea kushirikiana na Serikali na Mahakama katika utoaji wa msaada wa kisheria kwa wasioweza kumudu gharama, kuimarisha ushirikiano kwa utoaji huduma za kisheria mapema ipasavyo na kwa ufanisi, pia kuendelea kushirikiana na Mahakama katika kuimarisha Utawala wa Sheria pamoja na Taasisi za Haki Jinai kutekeleza mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Haki Jinai.

Kadhalika, Jaji Mkuu amewashauri wadau wengine kurejea mapendekezo mbalimbali ya Mhe. Dkt. Samia kuhusu utoaji haki na kujiridhisha endapo wameshayatekeleza na kuchukua hatua kwa sababu jukumu hilo ni jukumu mtambuka, jukumu jumuishi, la pamoja ambalo haliwezi kuwa jukumu la Mahakama peke yake.

Ameongeza kuwa, kila jamii yoyote lazima iwe na Viongozi kwa ajili ya kusimamia Utawala wa Sheria na mambo mengine, "kwa hiyo ni vyema kuwa tayari na hasa sisi watumishi wa umma kuwa tunafuatilia kunasemwa nini kwenye sekta yetu lakini na Viongozi Wakuu wa Serikali ngazi ya Taifa wanasema nini."

Amesema kuwa, masuala ya jinai yanapodhibitiwa kwa ufanisi ipasavyo yanawezesha wananchi kushiriki shughuli zao za kiuchumi, kisiasa na kijamii ipasavyo na hivyo kuimarisha uwepo wa ustawi  na maendeleo ya Taifa, jambo linalodhihirisha mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa kama ilivyo kaulimbiu ya Mahakama kwa mwaka huu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju ameeleza kuwa, msingi mkuu wa Dira ya Maendeleo 2050 ni Utawala, Amani, Usalama na Utulivu ambapo ndipo umuhimu wa Sekta ya Sheria unaonekana, Mahakama na Wadau wake wa Haki Jinai, kwa sababu kama huo ndio msingi mkuu unaowezesha mengine yote kutekelezwa.

Aidha, amefafanua kuwa, katika hotuba ya Rais, Mhe. Dkt. Samia  ya Siku ya Sheria mwaka 2026 alieleza kuwa, Mahakama ina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 na kuelekeza mambo kadhaa yafanyike ikiwa ni pamoja na  kuendelea kulinda haki na misingi ya Katiba, ambapo alihimiza  Mahakama isitoke katika misingi yake na jukumu lake, kuhakikisha migogoro ya kiuchumi, kibiashara na kijamii inatatuliwa kwa haraka na kwa haki, kujenga imani ya wananchi na wawekezaji katika mfumo wa kisheria wa nchi, kukuza uwajibikaji  na nidhamu katika utumishi wa umma na wa sekta binafsi.

Vilevile, kudumisha amani na mshikamano wa kitaifa ambao ni msingi wa maendeleo endelevu, kuwezesha mazingira bora ya uwekezaji na ukuaji  wa uchumi kwa kuhakikisha Utawala wa Sheria unazingatiwa, kulinda haki za makundi maalumu wakiwemo Wanawake, Watoto na watu wenye mahitaji maalumu, kuzuia migogoro inayoweza kuwa chanzo cha mgawanyiko wa kijamii au kisiasa.

Pia, kuharakisha utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo kwa kutoa tafsiri ya kisheria iliyo wazi na thabiti, kujenga na kuimarisha utamaduni wa kuheshimu sheria, haki na taasisi za umma, kuchangia katika mapambano dhidi ya rushwa na matumzizi mabaya ya madaraka kwa kutoa haki bila upendeleo pamoja na kuwezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwa kuwahakikishia ulinzi wa haki zao za kisheria.

Mhe. Masaju amebainisha kuwa, Mahakama inaendelea kusogeza huduma zake karibu zaidi na wananchi, pamoja na kufanya  ugatuzi wa Mahakama ya Rufani, ambapo mwezi Aprili Mahakama zinazoanzishwa katika Kanda za Arusha, Dar es Salaam, Mbeya, Mwanza na Tabora pamoja na Makao Makuu Dodoma zitaanza kufanya kazi.

"Sambamba na hilo, Kanda za Mahakama Kuu nazo zinafunguliwa mapema mwezi huu ambazo ni Mahakama Kuu Singida, Mahakama Kuu Songwe, Mahakama Kuu Katavi, Mahakama Kuu Njombe na Mahakama Kuu Lindi, hii ikiwa ni hatua kubwa inayopigwa na Mahakama katika kutambua umuhimu wa utawala wa sheria katika ustawi na maendeleo ya taifa letu," ameeleza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amehitimisha kwa kushauri na kuhimiza kuwa, mikutano itapimwa kwa utekelezaji wa majukumu ipasavyo na si kwa idadi na wingi wa mikakati.

“Niwashauri na kuwahimiza kuwa mikutano yetu hii itapimwa si kwa idadi ya wingi wa mikakati bali kwa ufanisi wa utekelezaji wa majukumu yetu ipasavyo hususan katika jukumu la utoaji haki mapema ipasavyo, kila aliye na wajibu wa kutekeleza atekeleze,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na  Wadau wa Utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki Mahakamani uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Jaji Mkuu- Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika Mkutano wa Wadau wa Utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai. Aliyeketi kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amiri Mruma. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akizungumza jambo na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakati wa mawasilisho ya Utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai kwa Wadau na Taasisi zinazohusika, katika mkutano wa kwanza kwa mwaka 2026 uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba akifuatilia mawasilisho ya utekelezaji wa mikakati ya Haki Jinai wakati wa mkutano huo uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akifuatilia kwa makini mawasilisho kutoka kwa Wadau wa Mnyororo wa Haki Jinai katika mkutano uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu- Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Wadau wa mnyororo wa utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai walioshiriki katika mkutano huo.

 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akifuatilia mawasilisho katika mkutano huo.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)