Jumatano, 11 Machi 2026

JAJI MKUU, MHE. GEORGE MASAJU AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA KATIBU MKUU UMOJA WA MATAIFA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 11 Machi, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Bw. Parfait Onanga-Anyanga,  Mjumbe Maalum  wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. António Guterres.

Bw. Onanga-Anyanga na ujumbe alioambatana nao waliwasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma majira ya Asubuhi na kupokelewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert.

Mjumbe huyo Maalum amefanya ziara nchini Tanzania kwa lengo la kuonana na Viongozi mbalimbali wa Serikali kwa lengo la kujadili masuala yanayohusu amani, uimarishaji wa demokrasia na utawala wa sheria kwa ujumla.

Bw. Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania pia kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali na kutathmini hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kitaifa na kuendeleza misingi ya utawala wa sheria kufuatia matukio ya uvunjifu wa amani ya kabla na wakati wa Uchaguzi Mkuu tarehe 29 Oktoba, 2025.

Aidha, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa hatua inayoendelea kuchukua kufuatia matukio ya uvunjivu wa amani wakati na baada ya uchaguzi wa tarehe 29 Oktoba, 2025. Ameeleza kuwa hatua hizo ni pamoja na; kuunda Tume Huru ya Uchunguzi ya Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025, dhamira ya kufanya mazungumzo jumuishi na mchakato wa mabadiliko ya Katiba.

Bw. Onanga–Anyanga ameeleza kuwa Umoja wa Mataifa unaendelea kuitambua Tanzania kama nchi yenye historia ya muda mrefu ya amani na pia wanatambua umuhimu wa kuwa na taasisi imara mfano Mahakama kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Kwa upande wake Mhe. Jaji Mkuu amemshukuru Mjumbe huyo Maalum kwa kutambua juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania.

Aidha, Mhe. Masaju amemueleza Bw. Onanga-Anyanga kwamba, Mahakama ya Tanzania imeendelea kuwa huru na kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba mashauri yaliyofunguliwa kuhusiana na mchakato wa uchaguzi na pia baada ya uchaguzi yameshughuliwa ipasavyo.

Katika ziara hiyo Bw. Onanga-Anyang mbali na wajumbe wengine ameambatana pia na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Bw. Shigeki Komatsubara.

Picha mbalimbali za ziara ya Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa (UN) katika Umoja wa Afrika, Bw. Parfait Onanga-Anyanga Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika, Bw. Parfait Onanga-Anyanga leo tarehe 11 Machi, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati alipomtembelea Jaji Mkuu. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akimpokea Bw. Parfait Onanga-Anyanga, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati yeye na ujumbe alioambatana nao walipowasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma kwa lengo la kuonana na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) pamoja na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert wakiongoza Ujumbe wa Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulipowasili Makao Makuu ya Mahakama kuonana na kufanya mazungumzo na Jaji Mkuu.


Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Parfait Onanga-Anyanga akisaini kitabu cha wageni alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 11 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mazungumzo kati ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Ujumbe maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na sehemu ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakiendelea na mazungumzo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimpatia zawadi 
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Parfait Onanga-Anyanga.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimpatia zawadi Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Bw. Shigeki Komatsubara.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa zawadi kwa wajumbe walioambatana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa waliomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Machi, 2026.







UADILIFU NDIO NGUZO KUU YA UTENDAJI; PROF. NDALICHAKO

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako amewaeleza Majaji na Mahakimu Wanawake wa Tanzania kuwa, weledi na uadilifu ndizo nguzo kuu na muhimu za utendaji hivyo hawana budi kuzizingatia wakati wanapotimiza wajibu wao.

Prof. Ndalichako aliyasema hayo jana tarehe 10 Machi, 2026 alipokuwa akifunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake, lililofanyika katika ukumbi wa New Generation Hall Kisasa jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa kufunga Kongamano hilo, Prof. Ndalichako amesema kuwa, ameridhishwa na mjadala wenye afya na nia ya dhati ya kujenga na kuimarisha haki na usawa wa kijinsia, pamoja na maazimio yaliyowekwa ambayo watakwenda kuyatekeleza.

Aliongeza kuwa, lengo la kuanzishwa kwa TAWJA ni kutambua mchango wa Majaji Wanawake duniani na kuhimiza usawa wa kijinsia katika Mhimili wa Mahakama, hivyo kongamano hilo ni tukio muhimu la kubadilishana maarifa kuonesha uongozi, ujasiri na dira ya mabadiliko pia ni mwanga unaoangaza nuru na kazi kubwa wanayoifanya ambayo inaakisiwa hadi nje na si ndani ya kumbi za Mahakama pekee bali katika jamii nzima.

Prof. Ndalichako amesisitiza kuwa uadilifu ni nguzo kuu ya utendaji, hivyo ni vema Majaji na Mahakimu Wanawake kuendelea kuzingatia uadilifu katika masuala ya haki, huku akinukuu maneno ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati alipokuwa akiwaapisha Majaji ambapo alisema, “uzoefu umeonesha kuwa Majaji wanawake huwazidi wenzao wa kiume katika utendaji unaozingatia masuala ya uadilifu.”

Aliongeza kuwa, anavutiwa na weledi, mshikamano na kujitoa kwa Majaji na Mahakimu wanawake hali inayoleta mabadiliko ya kijamii kwa kuzingatia utawala wa haki unaoleta usawa wa kijinsia.

Aidha, amesema kuwa haki haitoshi kutolewa bali inapaswa ieleweke na iguse mioyo ya watu pamoja na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama, hivyo Majaji na Mahakimu Wanawake wana nafasi muhimu katika kuhakikisha sheria inazungumza kwa haki na uadilifu.

Katika hatua nyingine, Prof. Ndalichako alizungumzia kuhusu umuhimu wa kuimarisha mifumo ya Taasisii ili kulinda afya ya kisaikolojia ya Mahakimu ambapo ameeleza kuwa mtu hawezi kuponya wengine ikiwa yeye mwenyewe ana maumivu, hivyo ni vema kulinda afya ya akili ili kuimarisha utendaji.

“Mmesisitizwa pia kuhusu umuhimu wa kulinda mifumo ya Taasisi ili kulinda afya ya kisaikolojia ya Mahakimu, huwezi kuponya jamii wakati wewe mwenyewe unaumia kimyakimya, ni vema kuendelea kuhakikisha kwamba tunalinda afya za akili ndani ya Makahama ili iendelee kutoa haki endelevu,” alisisitiza Mwenyekiti huyo.

Kadhalika, alisema kuwa, ni vema kuepuka kuwajeruhi upya wahanga na manusura wa ukatili wa kijinsia na kusisitiza kuwa, manusura wanastahili kujisikia salama na kuheshimiwa, hivyo haki lazima irejeshe utu na si kufungua tena majeraha.

Alieleza kwamba, teknolojia inakua kwa kasi hivyo ni vema itumike katika kuwalinda waathirika wa masuala ya ukatili wa kijinsia hasa ukatili wa mitandaoni, hivyo ubunifu ni lazima uendelee kutumika ili kuimarisha ulinzi wa waathirika na kuongeza uwajibikaji kwa kutumia Mahakama mtandao.

Alisema kuwa, yeye kama Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake anawahakikishia kuwa, Bunge pamoja na Wabunge wengine wataendelea kushirikiana katika kuimarisha sheria zinazolinda wanawake na watoto, hivyo ujumbe alioubeba katika mijadala ya leo utatumika ili kuendelea kukuza usawa wa kijinsia. 

Katika hatua nyingine, Prof. Ndalichako ameeleza kuwa mojawapo ya mafanikio makubwa kwa Mahakama na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA) ni kufikia usawa wa asilimia 50 kwa 50 kwa Majaji jambo ambalo ni la msingi katika kukuza imani kwa wananchi.

Kama Kaulimbiu ya mwaka huu inavyokumbusha, amewataka Majaji na Mahakimu hao wanawake kutoka mahakamani na kwenda kwenye jamii wakitoa haki kwa uadilifu huku wakijihusisha kikamilifu katika shughuli za uelimishaji hususan kupitia vyombo vya habari, kuzalisha maarifa na kujengeana uwezo jambo litalaojenga uaminifu kwa jamii ya watoto wa kike kuwa ndoto zao ni halali na matarajio yanawezekana na mustakabali wa maisha yake hauna mashaka.

Kauli mbiu ya Kongamano hilo kwa mwaka huu ni “Kutoka mahakamani kuifikia jamii: Majaji na Mahakimu wanawake mstari wa mbele kuongoza mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Awali, kongamano hilo lilifunguliwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Juma Homera, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi. Kongamano hilo lilihudhuriwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, UN Women, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka na wageni wengine waalikwa.


Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako akizungumza alipokuwa mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. 


Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) baada ya kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. Aliyekaa kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winifrida Korosso. 


Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) baada ya kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. Aliyekaa kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winifrida Korosso. 


Mgeni rasmi Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (kushoto) akifuatilia kinachojiri wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake. Kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Kongamano hilo, Mhe. Winifrida Korosso.

Mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Majaji Wanaume waliohudhuria katika Kongamano hilo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

UJENZI WA MAHAKAMA ZA MWANZO TATU MKOANI RUVUMA WAKAMILIKA

Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea

Mahakama ya Tanzania imekamilisha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo tatu, Lilolndo, Likuyusekamaganga na Nalasi, zilizopo katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, mkoani Ruvuma.

Mahakama za Mwanzo Lilondo ipo Wilaya ya Songea katika Halimashauri ya Madaba, Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga ipo katika Wilaya ya Namtumbo na Mahakama ya Mwanzo Nalasi ipo katika Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma.

Ujenzi huo uliokuwa unatekelezwa na Mkandalasi Mkuu (Pivotech), akisaidiana na Mkadalasi Msaidizi(Cadson) na majengo hayo matatu ya Mahakama yamegharimu jumla ya Shilingi za Kitanzania 2,954,059,829.18.

Mahakama ya Mwanzo Lilondo imegharimu 985,625,739/=, Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga imegharimu 961,400,162/= na Mahakama ya Mwanzo Nalasi imegharimu 1,007,033,928.18/=.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele, alikabidhiwa majengo hayo hivi karibuni kwa nyakati tofauti na  Mkandarasi Arqes Africa Architects and Interior Designers Ltd. 

Alitoa shukrani kwa wananchi wa maeneo hayo kwa ushirikiano waliouonyesha tangu kuanza hadi kumalizika kwa miradi hiyo.

Alieleza kuwa uzinduzi wa Mahakama hizo umepangwa kufanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Lilondo, kama  kuashiria kuanza kwa huduma za kimahakama zitakazoanza kutolewa katika majengo hayo mapya yaliyokamilika.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Lilondo.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Nalasi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa pili kulia) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Lilondo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa katikati) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (kushoto) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Nalasi.

Wananchi na wakazi wa Nalasi wakiwa katika eneo la tukio wakishuhudia makabidhiano hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

  

WIKI YA USULUHISHI


 

Jumanne, 10 Machi 2026

MAJAJI NA MAHAKIMU WANAWAKE WAUNGANA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA

     Wajadili nafasi ya wanamke katika kuimarisha utoaji haki na kuifikia jamii

Na HALIMA MENETE, Mahakama-Dodoma

Kongamano maalumu la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake limefanyika leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New Generation jijini Dodoma, likiwakutanisha Viongozi wa Serikali, Mahakama ya Tanzania pamoja na wadau wa maendeleo kujadili nafasi ya Majaji na Mahakimu wanawake katika kupambana na ukatili wa kijinsia.

Kongamano hilo lililobeba Kauli mbiu, “Kutoka Mahakamani Kuifikia Jamii: Majaji na Mahakimu Wanawake Mstari wa Mbele Kuongoza Mapambano Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia” lilihudhuriwa na mgeni rasmi Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Majaji na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania bara na visiwani pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo UN Women, RITA, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka.

Katika kongamano hilo pia, kulikuwa na nafasi ya utoaji mada mbalimbali, ambapo moja wa mada ilihusu “Nafasi ya Mwanamke kama Kiongozi katika Kuleta Mabadiliko kwenye Jamii kupitia Utoaji wa Haki unaozingatia Masuala ya Kijinsia.”

Mada hiyo iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Joseph Kerefu huku ikiendeshwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Magimbi, na ilijadiliwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Moshi Mhe. Dkt Lilian Mongela, Naibu Msajiri Mhe. Upendo Ngitiri na Hakimu Mkazi, Mhe. Juliana Mvungi.

Akifafanua kwa kina mada hiyo, Mhe. Kerefu amesema kuwa, katika juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia katika utoaji wa haki, tayari kuna misingi na nyenzo mbalimbali zilizowekwa kimataifa na kitaifa ambazo zinaweza kusaidia katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Amesema miongoni mwa nyenzo hizo ni pamoja na maandiko ya kitaaluma kama kitabu kilichoandikwa na Kosana Beker kinachojadili Gender and Diversity in the Judiciary, ambacho kinaeleza kwa kina umuhimu wa kuzingatia masuala ya kijinsia na utofauti katika mfumo wa utoaji haki.

Kwa mujibu wa Jaji Kerefu, uwepo wa vitendea kazi hivyo unaonesha wazi kuwa, kuna uwanja mpana wa kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa ipasavyo na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.

Hata hivyo, ameeleza kuwa, pamoja na uwepo wa misingi hiyo imara ya kisheria na kitaaluma bado kuna changamoto zinazotokana na baadhi ya mila, desturi na tamaduni katika jamii ambazo wakati mwingine zimekuwa zikikwamisha juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia.

Amesema baadhi ya mila na desturi hizo zimejikita katika mfumo dume, hali ambayo wakati mwingine imekuwa ikiweka vikwazo kwa watoa haki katika kuhakikisha misingi ya usawa wa kijinsia kama ilivyoainishwa katika mikataba ya kimataifa, Katiba ya nchi na sheria mbalimbali zinazozingatia masuala ya kijinsia zinatekelezwa kikamilifu.

Aidha, amesema licha ya maendeleo yaliyopatikana katika kuimarisha haki za wanawake, bado kuna changamoto mbalimbali zinazoendelea kujitokeza katika jamii ikiwemo ongezeko la mashauri ya ubakaji, unyanyasaji wa kingono, ukatili wa majumbani pamoja na ndoa za utotoni.

Ameongeza kuwa, hata katika masuala ya umiliki wa mali na mirathi bado kuna changamoto zinazowakabili wanawake katika jamii, huku baadhi ya sheria zilizopo zikionekana kutokidhi kikamilifu matakwa ya usawa wa kijinsia.

Ametolea mfano wa ‘Customary Law Declaration Order’ ya mwaka 1963 pamoja na baadhi ya vipengele vya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ambavyo bado vinaibua mjadala kutokana na kuwepo kwa vipengele vinavyohusishwa na ruhusa ya ndoa za utotoni.

Kwa upande mwingine, washiriki wa mada hiyo walieleza kuwa, changamoto hizo zinapaswa kuwa chachu kwa wadau wa sekta ya sheria, hususan majaji na Mahakimu wanawake, kuendelea kutumia elimu yao ya sheria pamoja na misingi iliyowekwa kuhakikisha vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.

Vilevile ilielezwa kuwa mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia yanahitaji ushirikiano mpana wa taasisi mbalimbali, ikiwemo Mahakama, Serikali, Wadau wa maendeleo pamoja na jamii kwa ujumla.

Akizungumzia uwakilishi wa wanawake katika Sekta ya Mahakama duniani, Mhe. Kerefu alieleza kuwa baadhi ya nchi zimepiga hatua kubwa katika kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi za kimahakama, akitolea mfano wa Italia ambapo wanawake wanawakilisha zaidi ya asilimia 52.9 ya Majaji.

Hata hivyo, alisema bado kuna nchi ambazo uwakilishi wa wanawake katika Mahakama uko chini, akitolea mfano wa Iraq yenye takribani asilimia 7.6 na Nepal yenye asilimia 3.8.

Kwa upande wa Tanzania, washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa, kumekuwa na mafanikio makubwa katika kuongeza uwakilishi wa wanawake katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

Imeelezwa kuwa Mahakama ya Rufani tangu ilipoanzishwa mwaka 1979 ilianza na Majaji watano wote wakiwa wanaume, lakini kwa sasa idadi hiyo imeongezeka na kufikia Majaji 37, ambapo wanaume ni 25 na wanawake ni 12, idadi inayozidi asilimia 30 ya uwakilishi wa wanawake.

Aidha, katika Mahakama Kuu kuna jumla ya Majaji 104 ambapo wanaume ni 65 na wanawake 39, wakati Mahakama za Hakimu Mkazi zina jumla ya Mahakimu 1,434 ambapo wanaume ni 746 na wanawake 688 sawa na takribani asilimia 48.

Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo, kuna Mahakimu 189 ambapo wanaume ni 111 na wanawake 78 sawa na asilimia 41.

Kwa upande wa Zanzibar, Mahakama Kuu ina jumla ya majaji 14 ambapo wanaume ni tisa na wanawake watano sawa na asilimia 35, huku katika ngazi ya mahakimu kukiwa na jumla ya Mahakimu 66 ambapo wanawake ni 23 na wanaume 43.

Washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa takwimu hizo zinaonesha wazi juhudi za Serikali katika kuhakikisha wanawake wanapata nafasi katika ngazi mbalimbali za uongozi ndani ya Mhimili wa Mahakama.

Hata hivyo, walisisitiza kuwa pamoja na ongezeko hilo la uwakilishi wa wanawake, bado kuna umuhimu wa kuhakikisha kuwa nafasi hizo zinatumika ipasavyo kuimarisha utoaji wa haki na kuchangia kikamilifu katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Rehema Kerefu (wa kwanza kulia) akiongoza mada isemayo, “Nafasi ya Mwanamke kama Kiongozi katika Kuleta Mabadiliko kwenye Jamii kupitia Utoaji wa Haki unaozingatia Masuala ya Kijinsia," wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake ambayo huadhimishwa tarehe 10 Machi kila mwaka.


Baadhi ya washiriki wa Kongamano maalum la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake ambalo limefanyika  leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New Generation jijini Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

SUALA YA KUTOKOMEZA VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA LISHUGHULIKIWE KWA KUSHIRIKIANA; DKT. HOMERA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (MB) amesema kuwa, Ukatili wa Kijinsia (GBV) si tu ukiukaji wa kisheria bali ni jeraha la kijamii linalokua kwa ukimya, hofu, pamoja na mila na desturi hatarishi kama vile ukeketaji hivyo ni jukumu la Majaji, Mahakimu wanawake na kila mmoja katika jamii kutokomeza vitendo hivyo na kuhakikisha haki inapatikana.

Akizungumza leo tarehe 10 Machi, 2026 wakati akifungua Kongamano Maalum la Kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake katika ukumbi wa ‘New Generation’ jijini Dodoma, Mhe. Dkt. Homera amesema kuwa Majaji na Mahakimu Wanawake si tu watekelezaji wa sheria, bali pia ni walinzi wa amani ya jamii na watetezi wa haki za binadamu.

Waziri huyo amesema, wakati waathirika wanapofika Mahakamani, wanabeba maumivu, aibu na mara nyingine kutokuwa na imani na wale wanaowazunguka, hivyo ameeleza, ninyi kama Majaji wanawake, uwepo wenu katika tasnia ya utoaji haki unatoa unatia faraja na kuleta tumaini la upatikanaji wa haki wanawake wengine walio tendewa vibaya.

Kwa upande wa Tanzania, Kaulimbiu ya maadhimisho hayo inasema, “Kutoka katika kuta za Mahakama hadi katika Jamii: Majaji Wanawake Wakiongoza Mapambano Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia,” Mhe. Dkt. Homera amesema kauli mbiu hiyo inaendana na kaulimbiu ya kimataifa inayosema: “Majaji Wanawake Ndani na Nje ya Mahakama: Wakilinda Upatikanaji wa Haki,”  

Waziri huyo amekipongeza Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kwa kuipa uzito Siku ya Kimataifa ya Majaji Wanawake tangu mwaka 2023 baada ya Azimio la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lililopitishwa tarehe 26 Aprili 2021 huko Doha nchini Qatar.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Homera ameupongeza uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa hatua kubwa ya mafanikio iliyopiga katika uboreshaji wa huduma za utoaji haki nchini.

‘Hapa napenda kutoa pongezi kwa Mahakama ya Tanzania chini ya uongozi wa Mheshimiwa George M. Masaju, Jaji Mkuu wa Tanzania, kwa mabadiliko makubwa yaliyoimarisha upatikanaji wa haki,’ amesema Waziri huyo.

Ameongeza kuwa, katika muda wangu mfupi tangu aanze majukumu yake Wizara Katiba na Sheria amevutiwa na maendeleo ya Mahakama katika suala zima la matumizi ya teknolojia katika utoaji wa haki ambapo amesema Mahakama imejizatiti kwa ajenda ya kisasa na mpango wa usikilizaji mashauri kwa njia ya Mahakama mtandao, ikitoka katika matumizi ya karatasi na kuelekea mfumo wa kidijitali.

Ametaja miongoni mwa mabadiliko yenye athari chanya kuwa ni pamoja na Mfumo wa kielektroniki wa kusajili na kuendesha Mashauri (JoT-eCMS) ambao umesaidia kuondoa ucheleweshaji wa usikilizwaji wa mashauri, kuongeza uwazi na kuimarisha usimamizi wa mashauri ya familia na ukatili wa kijinsia.

Waziri huyo amesema mabadiliko mengine ni uwepo wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJCs), ambapo ameeleza hadi sasa kuna vituo jumuishi zaidi ya tisa nchi nzima vilivyokwisha jengwa na vinavyoendelea kujengwa.

Ameongeza kwamba, Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia  kilichopo Temeke mkoani Dar es Salaam kimetoa mafanikio makubwa ikiwa ni ushahidi wa maono ya Serikali kwa kushirikiana na Mahakama. Kwa mwaka 2025, Mahakama hiyo ilishughulikia mashauri zaidi ya 9,200, yakiwemo ya ukatili wa kijinsia na familia, lakini pia iliwezesha asilimia 61 ya wanawake kupata msaada wa kisheria jambo linaloonyesha wazi kuwa, zinapounganishwa huduma za Mahakama, Polisi, na Ustawi wa Jamii katika eneo moja, vizuizi vya upatikanaji wa haki kwa wanawake vinaanza kupungua.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Homera ameongeza mafanikio mengine ya Mahakam ani pamoja na kuwepo kwa Uwajibikaji Unaotegemea Takwimu kupitia mfumo wa kanzi data (Data Hub), Mahakama inaonesha jinsi inavyoshughulikia mashauri nyeti ya ukatili wa kijinsia (GBV) kwa wakati halisi na kuhakikisha mashauri hayo muhimu yanatatuliwa haraka.

Hata hivyo, Waziri huyo ametoa rai kwa Mahakama kuwa, panapo mafanikio hapakosi changamoto hivyo ni lazima iwe makini na changamoto zilizopo.

“Mnapaswa kushughulikia ubaguzi wa kidijitali, mnatakiwa kuipeleka haki hii hasa ya matumizi ya teknolojia katika hatua nyingine kwa kuhakikisha huduma hii si kwa watu wa mijini tu bali pamoja na watu walio pembezoni, vilevile ni muhimu kuhifadhi kumbukumbu nyeti za Mahakama kwa viwango vya juu vya ulinzi wa kanzi data ili kuepuka kuvujisha siri za waathirika,” ameeleza.

Ameihakikishia Mahakama kuwa, Wizara itaendelea kushirikiana kwa karibu na Mhimili huo kuhakikisha mifumo ya kisheria inaendana na ulinzi wa athari za teknolojia.

Kadhalika, Waziri huyo ameipongeza TAWJA na kuahidi kuendelea kuipa ushirikiano, kwa kuwa sehemu ya mabadiliko haya ya kidijitali kuwa ni mabadiliko yenye tija katika kutoa haki ya kijinsia.

“Mmepeleka sheria kutoka kwenye viunga vya Mahakama hadi kwenye jamii kwa kufanya yafuatayo, kuchangia katika uundaji na marekebisho ya sheria zinazolinda wanawake na watoto dhidi ya Ukatili wa Kijinsia (GBV), kuhakikisha sheria zetu ni za haki, jumuishi, na zinawalinda walioko hatarini,” amesema.

Jitihada nyingine zilizofanywa na Chama hicho ni pamoja na kupinga ubaguzi katika mali za ndoa na faragha kupitia sayansi ya sheria yenye msingi wa jinsia; kuwajengea uwezo wasichana na kuonesha kwamba uongozi katika tanuru la haki kupitia Mahakama unawezekana na kuandaa shughuli za jamii ili kuhakikisha Mahakama mtandao inafika hadi maeneo ya pembezoni ambayo ni maeneo ya vijijini.

Akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa Kongamano hilo, Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel amesema hii ni mara ya tatu tangu Chama hicho kianze kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.


Aidha, Mhe. Sehel ameshukuru kwa ushirikiano ambao wanapata kutoka Serikalini. Na vilevile alichukua fursa hiyo kumueleza Mhe. Dkt. Homera kuhusu Chama hicho na namna kinavyofanya kazi kwa kuwa ni mara yake ya kwanza kushiriki katika shughuli ya TAWJA.


"TAWJA ni Taasisi ya Kitaaluma isiyo ya Kiserikali na wala hatujihusishi na masuala ya siasa, yenyewe inawaleta pamoja Mahakimu na Majaji Wanawake kwa pande zote mbili Tanzania Bara na Visiwani Zanzibar na wanachama wake wanatoka katika ngazi zote za Mahakama kuanzia Mahakama za Mwanzo mpaka Mahakama ya Rufani na lengo kuu la Chama chetu  ni kukuza utawala wa sheria, kulinda haki za binadamu, kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa makundi yote...," amesema Mwenyekiti huyo.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewapongeza Wanachama cha TAWJA na kusema kuwa anajivunia wanachama hao kwa kuwa ni watu makini.


"Pamoja na Ujaji na Uhakimu wenu, ninyi ni akina Mama, kila mwanadamu amezaliwa na mwanamke, mnafanya kazi kubwa sana," amesema Prof. Ole Gabriel.

Ameongeza kuwa, asilimia 80 ya tabia za watu zinatokana na wazazi, na kati ya asilimia hizo, Mama ana asilimia 64 ya kutengeneza tabia ya mtoto, hivyo mwanamke ni mtu muhimu katika ustawi wa jamii.

Kongamano hilo limehudhuriwa na Washiriki mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wanachama wa TAWJA kutoka matawi mbalimbali, Wjumbe Waalikwa wa TAWJA, Washirika wa Maendeleo na Wawakilishi wa Jamii ya Kiraia.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (MB) akitoa hotuba wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu wanawake (TAWJA) leo tarehe 10 Machi, 2026 katika ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) akitoa hotuba wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe.Barke Sehel akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake  leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa salamu za Mahakama ya Tanzania wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake kwa upande wa TAWJA leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu waliohudhuria sherehe ya Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA). Wa pili kulia ni Mhe. Joachim Tiganga, wa pili kushoto ni Mhe.Wilbert Martin Chuma na wa kwanza kushoto ni Mhe.Dkt Yose Joseph Mlyambina wakifuatilia mdahalo kwenye kongamano hilo.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa salamu za Mahakama ya Tanzania wakati wa ufunguzi wa kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 katika ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.


Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu wanawake (TAWJA) leo tarehe 10 Machi, 2026 katika ukumbi wa New Generation hall uliopo kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu waliohudhuria sherehe ya Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake. katikati ni Mhe. Joachim Tiganga, wa pili kushoto ni Mhe.Wilbert Martin Chuma na kushoto ni Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina wakifuatilia mdahalo kwenye kongamano hilo.


Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (wa pili kulia) akipokea zawadi kutoka kwa Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe.Barke Sehel (wa pili kushoto) wakati wa hafla hiyo. 

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na sheria Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa TAWJA ambao ni Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania waliohudhuria kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wanachama wa TAWJA ambao ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.
Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji Wafawidhi ambao ni walezi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) waliohudhuria kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa TAWJA waliohudhuria kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.

(Picha na INNOCENT KANSHA - Mahakama)