Jumanne, 12 Mei 2026

JAJI SEHEL, MWENYEKITI KAMATI YA JAJI MKUU UFUATILIAJI NA TATHMINI AFANYA ZIARA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel hivi karibuni alifanya ziara ya kikazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe lengo likiwa ni kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa shughuli za Mahakama.

 

Mhe. Sehel ambaye pia ni na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) alianza ziara yake tarehe 07 Mei, 2026 ambapo alipokelewa na mwenyeji wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA pamoja na Viongozi na watumishi watumishi wa Mahakama Njombe.

 

Jaji Sehel alipata wasaa wa kuzungumza na watumishi wa Mahakama Njombe ambapo alisikiliza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo ikiwemo ukosefu wa huduma ya usafiri wa basi la Mahakama linaloweza kuwapeleka ofisini kutokana na umbali mkubwa wa kutoka maeneo wanayoishi mpaka mahali pa kazi.

 

Aidha, Mwenyekiti huyo alipata fursa ya kutembelea jengo la Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Njombe (IJC) ambalo lipo kwenye hatua za mwisho kwa asilimia 97 na baadhi ya viongozi na watumishi tayari wameanza kuhamia kwenye jengo hilo.

 

Katika ziara hiyo Mwenyekiti alifanya ukaguzi wa shughuli za kimahakama katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mahakama ya Wilaya ya Njombe na Makete pamoja na Mahakama ya Mwanzo Njombe.

 

 Vilevile, katika ziara hiyo Mhe. Sehel alipata fursa ya kuzungumza mambo mbalimbali ya TAWJA Njombe katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wake pamoja na kuhuisha uanachama  wa TAWJA na IAWJ.

 

 

Akiendelea na kikao hicho huku wanachama wengine wakishiriki kwa njia ya mkutano mtandao (Video Conference) walio nje ya Wilaya ya Njombe, Mhe. Sehel  alisisitiza mshikamano pamoja na kushirikiana kikamilifu katika shughuli za Chama hicho, Tawi la Njombe ikiwa ni pamoja na kujitolea katika majukumu mbalimbali bila kujali malipo pamoja na kutoa elimu na kuhudhuria mikutano ya ndani.

 

 

Mwenyekiti huyo wa TAWJA alisisitiza kuwa Chama hicho ni jukwaa linalowawezesha kung’ara kitaifa na kimataifa kwa kazi zinazofanyika, ambapo aliwatakia wanachama wa TAWJA Njombe majukumu mema ya ujenzi wa Taifa huku akisisitiza uadilifu, weledi na uwajibikaji kama ambavyo Kaulimbiu ya Mahakama inasema.

 

Mhe, Sehel pamoja na wanachama wa TAWJA Njombe walipata fursa ya kukata keki na kufungua champeni pamoja na Makamu Mwenyekiti Mhe. Victoria Nongwa kama ishara ya mwanzo mpya wa TAWJA mkoani Njombe.

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani  ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi mbele katikati) akizungumza na Watumishi wa Mahakama Njombe alipotembelea Masjala hiyo hivi karibuni. Kushoto ni  Jaji Mfawidhi wa  Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndono ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Victoria Nongwa na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge. Aliyesimama upande wa kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama.  

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Njombe mbele ya jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe wakati walipofanya ziara hivi karibuni. 


 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel akipatiwa maelezo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe (wa kwanza kushoto). Wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA akizungumza hivi karibuni na baadhi ya Wanachama wa Chama hicho wa mkoani Njombe.

Jaji Sehel akiwa katika maandalizi ya kukata keki maalum ikiwa ni ishara ya kuanza kwa Tawi mpya la TAWJA Mahakama Njombe.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa  TAWJA, Mhe.  Victoria Nongwa (kulia) akimpatia zawadi Jaji Sehel.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




 

 

 

 

 

 

 

 


MTENDAJI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA VIONGOZI WA TUGHE WA MAHAKAMA YA TANZANIA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel leo tarehe 12 Mei, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.

Kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kuhudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick pamoja na Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.

Lengo la kikao hicho ambacho hufanyika kila mwaka kabla ya Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ni kujadili pamoja kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu watumishi wa Mahakama sambamba na kujadili hoja za Mabaraza ya Kanda na Divisheni za Mahakama Kuu kwa upana zaidi kabla ya kufanyika kwa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

Aidha, Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania kinatarajiwa kufanyika kesho tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake ambaye ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Yafuatayo ni matukio katika picha ya Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania (hawapo katika picha) leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kulia ni Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick na kushoto ni Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.


Picha mbalimbali za Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza nao leo tarehe 12 Mei, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick akiwa katika kikao hicho.

Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.


Viongozi mbalimbali wa TUGHE Mahakama wakichangia juu ya masuala mbalimbali ya Watumishi wa Mhimili huo wakati wa Kikao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kilichofanyika leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ikisikiliza na kurekodi hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 jijini Dodoma.


Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiandika hoja na michango mbalimbali iliyokuwa ikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania wakati wa kikao.

(Picha na MARY GWERA & ARAFA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma)








MAJAJI KANDA YA DAR ES SALAAM, DIVISHENI YA BIASHARA WANOLEWA KUHUSU MILIKI BUNIFU

 Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood amefungua mafunzo ya Miliki Bunifu yanayowahusisha Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Mahakama ya Kuu Divisheni ya Biashara lengo likiwa ni kuwapa uelewa zaidi juu ya jambo hilo.

Akifungua mafunzo hayo jana tarehe 11 Mei, 2026 kwenye Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Jaji Kiongozi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Mhe. Aboud alisema katika uchumi wa dunia ya leo hati miliki imekua moja ya mali ya thamani zaidi kuendesha uvumbuzi, ukuaji wa viwanda, ubunifu na biashara za kimataifa.

Jaji Abood alisema pia Nchi zinazoongoza kwa uchumi duniani hazijengwi juu ya rasilimali asili tu bali pia mawazo, uvumbuzi chapa, kazi za kisanii miundo na teknolojia za kidijitali ambazo huchangia ushindani na ustawi wa Taifa.

Aliongeza kuwa, kwa Tanzania ulinzi madhubuti na utekelezaji wa haki miliki unaendana moja kwa moja na lengo pana chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 na msukumo unaoendelea kuelekea ukuaji wa viwanda, uvumbuzi na uchumi unaotegemea maarifa.

Amesema, Mahakama inasimama katikati ya utekelezaji wa hati miliki wakati Mashirika kama vile Tume ya Ushindani (FCC), BRELA, TIRDO na COSOTA hushugulikia masuala ya utawala, Mahakama zinahakikisha kwamba haki inapatikana na kuheshimiwa kikamilifu.

Akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Abood alisema kuwa, yeye amemwakilisha Jaji Kiongozi ambaye ndiye alitakiwa kuwepo ila kutokana na majukumu mengine aliyonayo hakuweza kushiriki.

Amesema mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam wakishirikiana na Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara pamoja na Wadau wengine wa Mahakama kama Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Ofisi ya Haki Miliki Tanzania (COSOTA), Tume ya Ushindani (FCC) na wengine ambao wapo mahsusi kwa ajili kuwawezesha Majaji kupata elimu zaidi na pia kubadilishana uzoefu kuhusu Miliki Bunifu. Ameongeza, “kama unavyojua maendeleo kuchelewa sana inategemea na ubunifu.”

“Mahakama kama Watafsiri wa Sheria zinazohusu hayo na kuhakikisha kunakuwa na utekelezaji inabidi kuelewa kwa undani mchakato mzima na nini maana ya Miliki Bunifu wameona ni muhimu sana kupata mafunzo hayo ya siku mbili kwa sababu maamuzi yao sio tu kwamba yatatumika ndani ya nchi bali pia yamechaguliwa kuwekwa kwenye kanzidata (database) ambapo nchi nyingine wanasoma na wanaweza kuyatumia pia,” ameeleza Jaji Abood.

Ameongeza kuwa, mtu anaweza kubuni mradi wake wa kusuka nywele tu na ukachukuliwa na watu wengine wakanufaika wakati yeye ndiye mnufaika wa kwanza. Pia ilielezwa kuwa, kuna watu wanatumia taswira za watu kubuni katika Makampuni mbalimbali na watu wakapelekea shauri na kulalamika kwa hiyo ikaonekana ni ngumu kwa Majaji na Mahakimu kama watoa haki ambao wanatafsiri sheria kutoa hukumu na kuhakikisha zinatekelezeka waelewe kiundani.

Jaji Abood amemnukuu Jaji Kiongozi kuwa, “huu ni mwanzo tu mafunzo haya yataendelea kuwezesha na baadae kuwapata Majaji na Mahakimu wataalam kwenye eneo hili la miliki bunifu. Na kama ikiendelea hivyo watu watahakikisha kwamba hizo miliki bunifu zinalindwa na wawekezaji pia watakaribishwa.”

Amesema, kwa hatua hiyo watu wataamua kuanzisha bidhaa mbalimbali ambazo watabuni pamoja na kumiliki miradi mbalimbali. Hatua hiyo itachochea ukuaji wa uchumi wa nchi na kuhakikisha kwamba wanatimiza lengo la Dira ya Taifa ya Maendeleo.

Akijibu swali aliloulizwa na Mwandishi wa Azam Media kuhusu idadi ya Majaji wenye utaalam wa Miliki Bunifu, Mhe. Abood amesema hana uhakika ni wangapi wana utaalam huo japo amesema wameona shida ni kubwa ndio maana wameona kuna umuhimu na haja ya kufanya  mafunzo hayo na wameanza na Dar es Salaam lakini mpango mkakati ni kwamba Majaji wote nchi nzima waweze kupata mafunzo hayo.

Akimkaribisha Jaji Abood, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Salma Maghimbi amesema wizi halisi wa haki miliki sio tu kutoa nakala bali pia ni unyang’anyi wa haki za ubunifu.

Mhe. Maghimbi amesema, kwa sasa Mahakama zinashughulikia mashauri yanayohusisha alama za biashara, haki miliki, usanifu wa viwanda, viashiria vya kijiografia na siri za biashara. Changamoto mpya kama ukiukaji mitandaoni, uharamia wa kidijitali, maudhui ya akili unde na utekelezaji wa sheria mipakani hizi zinachanganya michakato ya Mahakama licha ya kuwepo mfumo wa kisheria. 

“Maofisa wa Mahakama bado wanakabiliwa na mapungufu ya uwezo wa kusimamia, ufundi, kiutaratibu na ushahidi na vipengele vya utekelezaji wa miliki bunifu, hii imewapa nguvu ya kuendesha mafunzo hayo,” amesema Jaji Maghimbi. 

Ameeleza kwamba, mpango huo utatoa mwelekeo wa vitendo na wa Mahakama juu ya mada ya haki miliki, taratibu za usajili na athari zake katika mashauri, kuthibitisha ukiukwaji, tathmini ya ushahidi wa kiufundi, muingiliano wa nafuu, changamoto ya kisiasa katika utekelezaji wa haki miliki.

Naye Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Cleophas Moriss amesema, mafunzo hayo yatawasaidia kuelewa kwa sababu mada zimepangwa katika mtiririko ambao utawapatia nafasi ya pekee kuongeza ujuzi kwakuwa mada zimepangwa kumuwezesha mtu kufahamu kuanzia chanzo na chimbuko la haki hiyo na maendeleo yake kitaifa na kimataifa.

Mhe. Morris amesema wataangalia jinsi kanuni zinavyozidi kukua katika tasnia husika na kwa nchi na kimataifa na pia wanaangalia sheria za nchi zimepangwa vipi au zimetengenezwa kwa mtindo gani katika kuleta uwiano wa kikanuni wa kitaifa na kimataifa.

Naye, Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa amesema sio mara ya kwanza wao kutoa mafunzo hayo, wameshawahi kutoa kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani.

“Lengo la kutoa mafunzo haya ni kuwapa elimu Majaji uelewa kuhusu masuala mazima ya miliki ubunifu kwa sababu eneo hili ni geni  kidogo hapa nchini na baada ya kuangalia hukumu kadhaa ambazo zimekuwa zikitolewa na Majaji wakaona kuna umuhimu sasa wa kupeana elimu hiyo ili wawe pamoja,” ameeleza Bw. Nyaisa.

Amesema katika maamuzi ya Majaji huwa wanagusa maslahi ya Nchi katika eneo la miliki ubunifu na kwamba zipo hukumu kadhaa ambazo zimetolewa na Majaji zimewasaidia sana katika utendaji wa majukumu yao.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani, Bi. Khadija Ngasongwa amesema wameungana na Mahakama kutoa mafunzo ya miliki bunifu ambazo katika sehemu ya sheria alama ya bidhaa wao ni kama Polisi au Wasimamizi wa kulinda miliki bunifu nchini hasa katika upande wa alama za bidhaa (IPR) imeelezewa katika sheria ambayo kwa sasa wanaifanyia marekebisho.

Amesema katika uzalishaji wa kusajili alama ya bidhaa au nembo inayofanywa na wakala wa BRELA wao kazi yao wanazirekodi ili waweze kuzitambua sokoni bidhaa halisi ni ipi na ambayo sio halisi.

Mafunzo hayo ya siku mbili baada ya kufunguliwa wameanza kwa masomo ya muhtasari wa Haki Miliki, Mfumo wa Kisheria wa Taasisi wa Haki Miliki nchini Tanzania, uamuzi na utekelezaji wa haki miliki na umuhimu wa kisheria wa hatua za usajili katika madai. Masomo hayo yamefundishwa na Mkufunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. Saudine Mwakaje na Wakili Mshirika  wa ‘Next Law Advocates’, Bw.  Seka Kasera na Msajili Msaidizi/Meneja wa Alama za Biashara na Huduma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood akitoa hotuba  ya ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu jana tarehe 11 Mei, 2026 kwa niaba ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani. 


Sehemu ya washiriki wa mafunzo Miliki Bunifu wakifuatailia hotuba ya mgeni rasmi (hayupo katika picha).

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akitoa neno fupi wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana akifanya utambulisho wa washiriki wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu.

Mtendaji  Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa akitoa salam wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu jana tarehe 11 Mei, 2026 jijini Dar es Salaam.


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa akitoa salamu wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wanaoshiriki katika Mafunzo ya Miliki Bunifu (waliosimama baadhi). Walioketi wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi,  wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa na wa kwanza kulia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa.

Meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na Wawezeshaji wa Mafunzo ya Miliki Bunifu. Walioketi katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi,  wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa na wa kwanza kulia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


Jumapili, 10 Mei 2026

JAJI MKUU AWATAKA VIJANA WA KITANZANIA KUTUMIA VIPAJI VYAO KWA MANUFAA YA TAIFA

  • Ni wakati akizindua Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu
  • Ampongeza Wakili huyo kwa uandishi Kitabu hicho
  • Asisitiza juu ya umuhimu na faida za kuwa na Shukrani katika nyakati zote za maisha

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa wito kwa vijana wa Kitanzania waliopo katika fani mbalimbali kutumia vipaji vyao kuandika vitabu vitakavyotumika kwa manufaa ya Taifa.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 10 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Kitabu kiitwacho SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu. 

“Vijana msisubiri mpaka muwe na kila kitu ili muweze kutumia vipaji vyenu, hivyo natoa wito kwa vijana wa Tanzania; kuandika, kusoma, kutafakari na kuchangia Taifa letu kwa vipaji vyenu. Taifa linalowapa vijana nafasi ya kuandika na kubuni hujenga urithi wa maarifa na mshikamano wa vizazi,” amesema Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju ametoa rai kwa wananchi kuona wajibu wa kuunga mkono Waandishi wa Tanzania kwa kusoma kazi zao, kununua vitabu vyao, kuwapa mrejesho, kuwapa nafasi katika majukwaa ya mijadala na Vyombo vya Habari.

Akizungumzia kuhusu Kitabu hicho cha SING GRATITUDE ambacho amekizindua, Mhe. Masaju amempongeza Wakili Aisha kwa kukiandika na kusema kuwa, Kitabu hicho kina viwango na hadhi ya Kimataifa.

“Napenda kutumia fursa hii kumpongeza Wakili Aisha Saidi Kingu kwa ujasiri wa kuandika. Kuandika si kazi ndogo, inahitaji nidhamu, uvumilivu, kujitafakari na kukubali kubeba ujumbe ambao wengine wanaweza kuusoma, kuuchambua na kuuhoji. Ninampongeza pia kwa kuonesha kuwa kijana anaweza kuchangia ujenzi wa Taifa kwa njia nyingi. Mtu anaweza kuwa, Mwanasheria, Mshairi, Mwanadiplomasia, Msomaji na Mwandishi, kama alivyo Wakili Aisha,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Vitabu vya fasihi vina nafasi kubwa sana katika maendeleo ya jamii kwa sababu husaidia kufundisha, kuelimisha na kuburudisha watu. 

“Kwanza, vitabu vya fasihi hutoa elimu kwa jamii. Kupitia hadithi, riwaya, tamthilia na mashairi, watu hujifunza maadili mema kama vile uaminifu, heshima, uvumilivu na mshikamano. Fasihi pia huwafundisha watu kuhusu historia, mila na desturi za jamii mbalimbali, pili, fasihi huburudisha jamii. Wasomaji hupata furaha na kupunguza mawazo wanaposoma vitabu vya fasihi…,” ameeleza Jaji Mkuu.

Ameeleza Kuandika vitabu vya fasihi ni jambo muhimu sana katika jamii kwa sababu huelimisha, huburudisha, hukemea maovu, huhifadhi utamaduni na kukuza lugha. Hivyo, jamii inapaswa kuwahamasisha waandishi wa fasihi ili waendelee kuandika vitabu vitakavyosaidia kujenga taifa lenye maadili mema na maendeleo.

Kuhusu umuhimu wa kuwa na Shukrani ambapo amesema kuwa, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, ina faida lukuki kwa upande wa Kisaikolojia na Kimaisha, husaidia kupunguza msongo wa Mawazo, husaidia mtu kuona mema hata katika changamoto, na hivyo kupunguza wasiwasi na huzuni.

Mhe. Masaju amesema pia, shukrani huongeza furaha ya mtu binafsi, ambapo amesema, “Watu wanaoshukuru huishi maisha yenye matumaini na amani ya ndani.”

Ameongeza kuwa, manufaa mengine ya kuwa na Shukrani ni pamoja na kuimarisha afya ya akili ambapo Tafiti zinaonesha kuwa, shukrani hupunguza hisia za hasira na wivu na kuongeza kuridhika na maisha.

“Kwa upande wa Kijamii na Kiutamaduni, Shukrani huimarisha mshikamano wa kijamii: Jamii yenye shukrani hujenga uhusiano wa heshima na mshikamano, kwani watu wanapohisi kuthaminiwa, hujitolea zaidi kushirikiana, hujenga maadili ya uwajibikaji: Shukrani ni kiashiria cha kutambua mchango wa wengine, na hivyo kuimarisha utamaduni wa kuheshimiana na kusaidiana,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema, Shukrani hujenga maadili ya uwajibikaji: Shukrani ni kiashiria cha kutambua mchango wa wengine, na hivyo kuimarisha utamaduni wa kuheshimiana na kusaidiana, uendeleza utamaduni wa amani.

Katika upande wa Kidini na Kiroho, Jaji Mkuu amesema, ni tendo la imani: Katika dini nyingi, shukrani ni ibada na ishara ya kutambua ukuu wa Mungu. Mfano, “Shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu” (1 Wathesalonike 5:18).

“Shukrani huimarisha maadili ya kiroho, Shukrani hujenga moyo wa unyenyekevu na kutambua neema za Mungu katika maisha ya kila siku na kwa upande wa Kiuchumi na Kimaendeleo, huongeza tija kazini: Wafanyakazi wanaothaminiwa huonyesha bidii na uaminifu zaidi, huimarisha uongozi bora: Viongozi wanaoshukuru mchango wa wananchi hujenga imani na mshikamano wa kitaifa, huendeleza mshikamano wa kizazi kipya,” ameeleza.

Kwa upande mwingine, Mhe. Masaju amesema, kukosa shukrani kuna hatari kadhaa ikiwa ni pamoja na kujenga malalamiko na chuki, kupoteza mshikamano wa kijamii, kudhoofisha maadili ya kiroho na kitaifa:

“Kukosa shukrani ni ishara ya kutokubali uongozi wa Mungu na kupuuza mchango wa wengine. Shukrani si neno dogo bali ni nguzo ya maadili, mshikamano na maendeleo ya kijamii. Jamii inayojenga moyo wa shukrani huimarisha furaha ya watu wake, hujenga mshikamano wa kitaifa, na kuendeleza maadili ya uwajibikaji,” amesisitiza.

Akiwa katika mahojiano maalum wakati wa hafla hiyo, Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha amesema wazo la kuandika kitabu hicho lilianzia kwenye neno lisemalo ‘Muujiza upo katika asante’ (The Miracle is in the thank you).

Wakili Aisha amesema, njia kuu mojawapo ya shukrani ni kutambua na kuelewa uwepo wa sasa ambapo amesema, “kuchagua kushukuru kunakufanya usonge mbele, kushukuru kwenye udogo ndipo kuna ukubwa…..”

Ameongeza kuwa, ana ndoto ya kuona vijana wanakuwa katika maadili mema ya Kitanzania, pamoja na kuendelea kuandika kuhusu masuala mbalimbali ya kuelimisha jamii ya Kitanzania.

Wakizungumzia umuhimu wa shukrani nao Viongozi wa Dini ya Kiislamu na Kikristo, Sheikh Issa Issa pamoja na Padri Faustine Furaha, kwa pamoja wamesema neno Shukrani limesisitizwa pia hata katika vitabu vya dini hizo. Mfano katika Biblia 1 Watheselonike 5:18 inasema; Shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu. Na Katika Quran Tukufu- Surah Ibrahim 14:7 inasema, Mkinishukuru, hakika nitawazidishia.

“Tujenge utamaduni wa kumshukuru Mungu, Zaburi 136:1, nitamshukuru Bwana kwa ajili ya Haki yake na nitaliimbia.........Kwa muda mrefu sana dhana ya shukrani imepuuzwa, kuhesabu baraka huongeza nyingine,” amesema Padri Furaha.

Amesema, kushukuru ni kuangalia tulicho nacho na sio kile ambacho hatuna na kwamba shukrani ni tunda la uvumilivu na kwamba yatupasa kushukuru kabla ya kumuomba Mungu kwa kuwa moyo usiokuwa na shukrani hukausha mema yote.

Naye Sheikh Issa amesema, kushukuriwa na kupendwa ni miongoni mwa mahitaji ya binadamu.

Kwa upande wao Mchambuzi wa Kitabu, Bw. Joram Nkumbi pamoja na Mhariri wa Kitabu hicho, Dkt. Ishmail Mwambapa kwa pamoja wamempongeza Wakili Aisha na kusema kuwa, kitabu kilichoandikwa kwa mfumo wa mashairi kinaelimisha na kusisitiza juu ya umuhimu wa kuwa na shukrani katika hali yoyote katika maisha.

Bw. Nkumbi amesema, Kitabu kinaonyesha moyo wa Shukrani na kwamba muujiza mkubwa upo katika neno Asante, amesema “shukrani ni kama kuomba ten, ruhusu moyo wa shukrani uingie moyoni mwako, kitabu pia kinasisitiza mambo ya maadili.”

Katika kitabu hicho cha SING GRATITUDE kinamfundisha mtu kusema ahsante kwa mambo mema na makubwa, na pia kwa mambo madogo ambayo mara nyingi hupita bila kutambuliwa kirahisi.

Uzinduzi wa kitabu hicho ni ushahidi kuwa taifa letu lina hazina kubwa ya fikra na vipaji. Vijana kama Wakili Aisha wanapochukua kalamu na kuandika, wanajenga msingi wa leo na kesho yenye maarifa na matumaini.

Hafla hiyo imehudhuriwa pia na baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Majaji Wastaafu wa Mahakama Kuu, Mabalozi, Wazazi pamoja na ndugu jamaa na marafiki wa familia ya Aisha Saidi Kingu.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akizindua Kitabu kiitwacho SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Msomi Aisha Saidi Kingu. Hafla ya uzinduzi wa Kitabu hicho imefanyika leo tarehe 10 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mwandishi wa Kitabu hicho, Wakili Aisha Saidi Kingu.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiteta jambo na Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha Saidi Kingu mara baada ya kukizindua kitabu hicho.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu (wa tatu kushoto).

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba yake wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu kiitwacho SING GRATITUDE kilichoandaliwa na Wakili Aisha Saidi Kingu.

Picha za makundi mbalimbali ya wageni waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu.

Baba Mzazi wa Wakili Aisha Saidi Kingu, Dkt. Saidi Kingu Mtemi akizungumza wakati wa hafla hiyo. Kulia ni Mama Mzazi wa Wakili huyo.

Kiongozi wa Dini ya Kiislamu, Sheikh Issa Issa akizungumza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu. 

Padri Faustine Furaha akizungumza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu. 

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha Saidi Kingu (kushoto) na kulia ni Mchambuzi wa Kitabu, Bw. Joram Nkumbi.

Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha Saidi Kingu (kushoto) akifanyiwa mahojiano kuhusu Kitabu hicho leo tarehe 10 Mei, 2026 wakati wa uzinduzi wa kitabu hicho.

(Picha na BAKARI MTAULLAH)