Ijumaa, 12 Juni 2026

JAJI MKUU AWATAKA WADAU WA HAKI JINAI KUIMARISHA UMAKINI KATIKA UPELELEZI

 ·       Awataka pia wazingatie matakwa ya Kifungu cha 134 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai na Kanuni za Jaji Mkuu

·       Asisitiza Polisi kutoa dhamana kwa watuhumiwa kwa mujibu wa sheria

·       Amtaka kila mdau kusimama ipasavyo katika eneo lake kuboresha Haki Jinai

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Wadau wa Haki Jinai nchini kuendelea kuimarisha umakini katika upelelezi wa mashauri ya Jinai ya aina zote na uendeshaji wa mashauri ya jinai Mahakamani kwa kuzingatia Katiba na Sheria ipasavyo.

Mhe. Masaju aliyasema hayo jana tarehe 11 Juni, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu amesema kuwa, “miongoni mwa Taasisi ambazo zinaongoza kufanya/kushiriki Mafunzo ya ndani na nje ya Nchi ni Taasisi zinazohusika na upelelezi, hivyo tunataka kuona matunda yake na matokeo yake kazini.”

Jaji Mkuu amesema, zoezi la upelelezi liendane na Kifungu cha 134 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kinachotaka mashauri yafunguliwe Mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika isipokuwa kwa makosa ambayo ni makubwa na yale ambayo yanasikilizwa na Mahakama Kuu kama ilivyotajwa katika kifungu cha 134(4).

Aidha, amempongeza Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kwa kuweka Mwongozo ambao ni Sheria ambayo hata katika mashauri makubwa, upelelezi uwe umekamilika ndani ya siku 90 ili shauri lianze kusikilizwa.

“Yazingatieni hayo, lakini pia endeleeni kuzingatia na kanuni zilizotolewa na Jaji Mkuu kuhusu watuhumiwa kupata maelezo ya ushahidi dhidi yao, kabla ya kusomewa mashtaka kwa mara ya kwanza (Preliminary hearing) na kesi kuanza kusikilizwa ili kesi zinaposikilizwa wawe wanafamu ushahidi dhidi yao kama ilivyo kawaida katika Mahakama Kuu, hapo ndipo kutakuwa na usikilizwaji kikamilifu ile (fair trial) inayozungumzwa katika Katiba Ibara ya 13(6),” amesema Mhe. Masaju.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amesema kuwa, kuna changamoto ya dhamana kwa upande wa Polisi ambapo amesema, “niwaombe Polisi, mmepewa mamlaka chini ya kifungu namba 65 mpaka 70 vya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai na bahati mbaya sisi tunawafamu ninyi Polisi peke yenu, lakini kuna Taasisi nyingine ambazo zinakamata watu zinaleta kwenye vituo vyenu. Vituo vyenu unakuta vimejaa, sasa sijui kama mna fedha za kutosha au ni vikubwa kiasi gani, hii yenyewe ni sababu ya msingi kwa makosa yale ambayo yanadhaminika kuwapa dhamana,” ameeleza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amewashauri Polisi kutoa dhamana kwakuwa kifungu namba 65 mpaka 70 vya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kimeeleza vizuri. “Wapeni dhamana itatupunguzia pia na hizi tuhuma nyingine zisizokuwa na sababu mtu anaweza akajidhamini au anaweza akadhaminiwa na mtu, mpeni dhamana, msipoweka utaratibu wa kuwa dhamana watajaa mahabusu na kusababisha magonjwa ya mlipuko hata wengine wanaweza wakafia Mahabusu ikawa shida, kwahiyo hakuna sababu ya kuogopa kuwapa dhamana kama umewakamata kwa usahihi kabisa wapeni dhamana,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, Sheria inaelekeza kuhusu mtuhumiwa kutakiwa kufikishwa Mahakamani ndani ya saa 24 tangu alipokamatwa, hii itasaidia na kwa upande wa makosa ya uhujumu Uchumi wanatakiwa kufikishwa Mahakama ya Wilaya iliyo jirani na alipokamatwa ndani ya saa 48.

Kadhalika, amewataka kuzingatia masharti ya Kifungu cha 34 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kinachowataka Mkuu wa Kituo cha Polisi kutoa taarifa ya kila Mtuhumiwa aliyekamatwa bila kibali cha Mahakama (Warrant of Arrest) na ambao wako ndani ya Vituo vya Polisi na wale waliopata dhamana. “Hili ni takwa la kisheria, zingatieni haya masharti, faida zake ni nyingi na tumezitafakari hapa wote, hapa hakutakuwa na cha Mswalia Mtume, zingatieni hayo masharti ili twende kwa sababu hata tusiposema hayo mengine ni vizuri tukayazingatia yote haya,” amesisitiza.

“Kwa upande wa Mahakama, wajibu wetu tuutekeleze ipasavyo bila kutumia madaraka yetu vibaya,” amesema Jaji Mkuu huku akiwaahidi Wadau hao kuwa, Mahakama itaendelea kuwa makini kwa kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa Ibara ya 107A(1)(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) kwa sababu ndio Wasimamizi wa Sheria hizo kwa sababu kuna changamoto katika eneo la upelelezi.

“Lakini wajibu wetu wa kuandaa vitabu vya Rufaa kwa Wafungwa wanaotoka Mahakama Kuu kuja Mahakama ya Rufani, tuviandae na kuvikamilisha hivi vitabu na kuwapatia wahusika ili waweze kukamilisha sababu zao za Rufaa, hivyo hivyo Mahakama tuwapatie wengine wanaotaka kukata rufaa labda kutoka Mahakama ya Wilaya au Hakimu Mkazi kuja Mahakama Kuu, wanaotaka nakala za hukumu, wanaotaka mwenendo wa mashauri tuwapatie mapema ipasavyo ili waweze kuandaa rufaa zao,” amesema Mhe. Masaju huku akisisitiza yote ambayo yamesemwa kuhusu Mahakama yatekelezwe na kila mdau wa mkutano huo atekeleze majukumu yake ipasavyo ili kushughulikia changamoto.

Jaji Mkuu amewataka Wadau hao wa Haki Jinai wakiwemo Magereza, Polisi, TLS na Wadau wengine kama kuna changamoto zozote zinazokwamisha upatikanaji haki wasisite kutoa taarifa Mahakama badala ya kusubiri siku ya vikao tu.

“Mahakama ina nafasi kubwa sana katika ustawi na maendeleo ya Taifa letu, bila na kuwa na amani na utengamano katika Taifa, maendeleo gani yatatoka katika Taifa hilo, watu hawatafanya siasi, watu hawatafanya shughuli zao za kiuchumi, hawatafanya shughuli zao za kijamii ikiwa ni pamoja na shughuli za siasa na kufunga ndoa na kushiriki katika matamasha, kwahiyo tuna dhamana kubwa katika hili ili Taifa hili lidumu kuwa la udugu kama ilivyokuwa zamani tunaitana ndugu. Amani na udugu ndivyo vinavyohimizwa katika Katiba kupitia Ibara ya 9, hivyo simamieni utekelezaji wa sheria kwa ufanisi ipasavyo,” amesema.

Aidha, Jaji Mkuu amesema kuwa, katika hotuba yake ya Siku ya Sheria nchini mwaka huu alieleza mambo ambayo Mahakama inafanya katika kuchangia ustawi na maendeleo ya Taifa. Amesema, “Kaulimbiu yetu ya Mahakama kwa mwaka huu 2026 ni; Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.”

Ameeleza kuwa, Mahakama na wadau wake ni watu muhimu katika kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ambayo msingi wake mkuu ni Utawala, Amani, Usalama na Utulivu na vipaumbele vinne ambao ni Utawala Bora na Haki, Serikali za Mitaa Imara na zenye ufanisi, Utumishi wa Umma unaowajibika na Amani, Usalama na Utulivu ambapo kila mdau anahusika.

Amesema kuwa, pamoja na kwamba, Mahakama inatekeleza wajibu wake, inajikita kuangalia ni kwa namna gani Mhimili huo unachangia katika ustawi na maendeleo ya Taifa. “Sasa moja tunajua umuhimu wa Mahakama katika jamii, sasa katika kipindi hiki tangu tulivyokutana tarehe 02 Machi, 2026 mwaka huu Mahakama Kuu sita ambazo ni Njombe, Singida, Lindi, Simiyu, Songwe na Katavi zimezinduliwa na kufanya kazi na Mahakama za Mwanzo 15 nazo zimezinduliwa na kuanza kufanya kazi. Amesema kwa Tanzania Bara umebaki Mkoa mmoja pekee ambao hauna Masjala ya Mahakama Kuu ambao ni Pwani.

“Tumesogeza huduma zetu za Mahakama kwa watu ili haki ipatikane, kuwepo na amani na utulivu watu waweze kushiriki shughuli zao za kiuchumi, za kisiasa na kijamii kwa ufanisi ipasavyo. Kwa hiyo wenzetu mnaohusika na huduma za upelelezi mjue sasa kuna huduma za Mahakama Kuu katika hiyo Mikoa,” amesema Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, Ibara ya 25(1) ya Katiba inasema; Kazi pekee ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii, ndilo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha Utu. Na kila mtu anao wajibu wa: - a) kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji mali na b) kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji mali ya binafsi na yale malengo ya pamoja yanayotakiwa au yaliyowekwa na sheria.

Kadhalika, Jaji Mkuu amewakumusha Wadau hao kuhusu mikakati waliyokubaliana ambayo ni endelevu, ambapo mkakati wa kwanza unasema, kila Taasisi ambayo ni Mdau wa Mnyororo wa Utendaji Haki Mahakamani iwajibike ipasavyo kwa kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia Katiba, Sheria na maadili ya utumishi yanayosimamia Taasisi ipasavyo.

Na Mkakati wa pili ni kwamba Wadau wote Waheshimu na kulinda hadhi ya Mahakama, aidha Mahakama kwa upande wake, isimamie sheria na kanuni zilizopo ikiwemo sheria inayohusu kosa la kuidharau Mahakama yaani ‘Contempt of Court’ ili kulinda hadhi na ukuu wake.

Amesema kuwa, Sharti hilo ni la Kikatiba na lipo kwenye Ibara ya 30 (1) na ya (2d) kulinda hadhi, heshima na uhuru wa Mahakama, si kama sisi tunataka kuheshimiwa tu hapa, hili ni takwa la Kikatiba.

Mkakati wa tatu ni; Mahakama na Wadau wa mnyororo wa haki waimarisha mahusiano miongoni mwao kwa lengo la kuchukua hatua haraka ili kutatua changamoto za utoaji haki zitakapojitokeza.

Mwingine ni, Mahakama na Wadau wote watambue nafasi ya kila mmoja, wadumishe heshima, nidhamu ya kazi na wazingatie sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza utendaji kazi wa majukumu ya kila mdau.

Taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki, iimarishe ufuatiliaji mashauri na uwajibikaji kwa kutoa taarifa sahihi na za mara kwa mara kuhusu utekelezaji wa mikakati iliyowekwa na kutumia mifumo inayosomana ili kurahisisha mawasiliano.

Wadau wanaokiuka maadili wachukuliwe hatua ipasavyo kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazosimamiwa na kila mdau husika.

“Mkakati wa saba, Mahakama iongeze na kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali (Virtual Court) katika kuendesha mashauri yanayohusu watuhumiwa waliohamishiwa katika Magereza mbalimbali kutoka kwenye Wilaya zisizo na Magereza na ili upatikanaji wa haki uwe wa haraka na wa gharama nafuu.

Mkakati mwingine ni Vikao kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa jukumu la utoaji haki mahakamani vifanyike angalau mara nne kwa mwaka ilikujadili changamoto na kufuatilia utekelezaji wa mikakati hiyo. Mkakati wa tisa ni kila Taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa utoaji haki Mahakamani iweke utaratibu madhubuti wa ndani ya Taasisi utakaofanikisha utekelezaji wa mikakati hiyo.

Aidha, katika Mkutano huo uliofanyika jana uliongezeka mkakati mwingine mpya unaosema kwamba, migogoro yote inayopaswa kwa mujibu wa sheria kutatuliwa kwanza katika ngazi mbalimbali kwa njia ya kimadai au kiutawala ishughulikiwe na kukamilishwa katika hatua na ngazi zote husika badala ya kufunguliwa kama jinai moja kwa moja na hili ni sharti la kisheria.

Jaji Mkuu amesema kwamba, mikakati hiyo ikitekelezwa yatasaidia kuboresha mfumo wa haki jinai na haki itakuwa inapatikana mapema, kwa changamoto ambazo zinatatulika kwa urahisi.

“Huu mkakati wa mwisho pia ni wa kisheria, katika kifungu cha 4 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai ndipo kinapopatikana....., mikakati yote tuliyoiweka ni mikakati ya kisheria ipo kwenye sheria hakuna kitu hapa ambacho hakipo kwenye sheria na ndio maana tunaweka mikakati, kilichopo kwenye sheria lazima kinapaswa kitekelezwa, hatuwezi kuwekewa maazimio kwahiyo kwenye vikao vyetu sisi tumeshakataa maazimio huwezi kuazimia kutekeleza au kutotekeleza sheria, sheria ni lazima uitekeleze vinginevyo utaivunja na ukiivunja unawajibika. Kwahiyo tuna wajibu wa kutekeleza haya yote, tuna wajibu wa kutekeleza hii mikakati ambayo ni ya kisheria, vinginevyo tutawajibika,” ameeleza Mhe. Masaju.

Amesema, kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba inayoweka Utawala wa Sheria, inasema kila mtu ana wajibu wa kufuata na kutii Katiba hii na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara 26(2) inasema kila mtu ana haki kwa kufuata utaratibu uliowekwa na Sheria kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na Sheria za Nchi.

“Hata mikutano yetu hii, ni katika hatua tunazochukua kuhakikisha kwamba Katiba na Sheria za nchi zinatekelezwa ipasavyo na Ibara ya 25 inatutaka kila mmoja awajibike kwenye hili, na sisi wote tunafanya kazi sasa kwa nafasi mbalimbali, wengine ni Majaji, wengine ni Majaji Wakuu, wengine ni Wakurugenzi, wengine ni Maofisa wa Polisi, wengine Ofisi ya Magereza, wengine Ofisi ya PCCB, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, watumishi wote wa Taasisi zilizowakilishwa hapa tuna majibu tuonafanya kazi hizi,” amesema Jaji Mkuu.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wadau wa Haki Jinai alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 11 Juni, 2026.


Wadau wa Mahakama wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipokuwa akifunga 
 Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Mwenyekiti wa Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani  akizungumza jambo wakati wa mkutano huo uliofanyika tarehe 11 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Baadhi ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania walioshiriki katika 
Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

JAJI MFAWIDHI SONGWE AZINDUA MAHAKAMA YA MWANZO MSANGANO

Na. ELIUD ANDREW KIWANGA – Mahakama, Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata aongoza hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano iliyopo Kata ya Msangano Wilaya ya Momba Mkoa wa Songwe na kufanyika katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Msangano

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata aliishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuwezesha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano,

Aidha, aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuiwezesha Mahakama ya Tanzania na kuhakikisha inakuwa na miundombinu ya kisasa. Vilevile aliishukuru Mahakama ya Tanzania chini ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Geoge M. Masaju kwa kuendelea kubuni miradi mbalimbali ya uboreshaji wa Miundombinu ya Mahakama.

Mhe. Malata alisema kuwa, ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano ni ishara ya Serikali ya awamu ya sita kuwathamini  na kuwajali wananchi wa Msangano na maeneo jirani kwa kuwasogezea huduma ya upatikanaji wa haki na kuwa tofauti zozote za kisiasa, kijamii, kiuchumi, kiitikadi zisiwe sababu ya kuharibu miundombinu ya Mahakama ya Mwanzo Msangano.

“Hivyo wananchi wote kwa pamoja wanao wajibu wa kulinda na kutunza miundombinu ya Mahakama hiyo kwasababu ni mali ya umma na imejengwa kwa kodi za wananchi wenyewe. Wananchi wa Msangano wamepata bahati kujengewa Jengo la kisasa la Mahakama mapema ikilinganishwa na maeneo mengine. Nawaasa wananchi wa Msangano kuishi wa amani na upendo ili kuepuka migogoro kwani migogoro hurudisha nyuma maendeleo ya jamii,” alisisitiza Jaji Mfawidhi Malata.

Mhe. Malata aliwashukuru wanachi wote wa Msangano na maeneo jirani kwa kuwa walipa kodi wazuri na kufika katika hafla ya uzinduzi katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Msangano na pia aliushukuru uongozi wa Wilaya ya Momba  kwa kuupokea mradi, kuusimamia na kuulinda mpaka ulipokamilika.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo alianza kwa kuwaomba wananchi kuepuka tabia ya kujichukulia sheria mkononi kwani kwa kufanya hivo ni kinyume na sheria na pia alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwezesha ujenzi wa miundombinu ya Mahakama maeneo mbalimbali nchini.

Mhe. Daniel Mwandobo aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuendelea kutumia mifumo ya kidigitali kwani kwa kufanya hivyo kumepunguza gharama, muda wa ufatiliaji na pia imeimarisha mifumo ya utoaji wa haki.

Vile vile aliwaasa wananchi wasiiogope Mahakama bali wailinde na kuitunza na pia siyo mashauri yote yanapaswa kwenda mahakamani bali watumie pia njia za usuluhishi kutatua baadhi ya migogoro miongoni mwao. Aidha, aliipongeza Serikali na Mahakama ya Tanzania kwa kuanza kwa mchakato wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Momba inayotarajiwa kujengwa katika mji mdogo wa Chapwa.

Naye, Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Momba Bw. Kataba Sukuru aliishukuru Serikali ya awamu ya sita na Mahakama ya Tanzania kwa kuwezesha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Bw. Sakuru aliahidi kuendelea kushirikiana na uongozi wa Wilaya ya Momba na Mahakama ya Tanzania ili kuhakikisha huduma za msingi ikiwemo huduma ya Haki inapatikana kwa wananchi wa Kata ya Msangano pamoja na  wa Wilaya ya Momba kwa ujumla.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na sehemu ya viongozi wa ngazi ya Wilaya wakiwemo Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma Bw. Salumu Kyambi, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Momba Bw. Paul Sheyo, Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raymond Kaswaga, Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Momba Bw. Sukuru Kataba pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata akihotubia wakati wa uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia) akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano, (wa kwanza kulia) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Songwe Mhe. Francis Kishenyi, (wa tatu kulia) ni Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo, (wanne kulia) ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Tunduma Bw. Salumu Kyambi na Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Momba Bw. Paul Sheyo wakifuatilia hafla hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo katika zoezi la kukata utepe.

Sehemu ya wageni waalikwa waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja ya viongozi wa Mahakama Mkoa wa Songwe pamoja na Viongozi mbalimbali wa ngazi ya Wilaya ya Momba nje ya jengo la Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Momba Bw. Sukuru Kataba akitoa neno akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo akitoa neno katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.


Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo akipanda mti wa kivuli katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Msangano.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama) 



Alhamisi, 11 Juni 2026

JAJI MKUU ATETA NA WADAU WA HAKI JINAI

  • Awataka kuwa huru kutoa michango yenye kuboresha mnyororo wa Haki Jinai
  • Asema ushirikiano wa wadau kwa Mahakama ni muhimu katika kufikia azma hiyo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Wadau wa Haki Jinai nchini kuwa huru na wakweli katika kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yanayoukabili mnyonyoro wa Haki Jinai.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 11 Juni, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

"Kama changamoto zipo Mahakamani semeni, kama changamoto zipo ili mradi tuwe wakweli sio kusingiziana na tutasema hapa kwa kuheshimiana hatujaja kusutana, tumekuja kushauriana ni wapi kuna tatizo turekebishe na ni wapi tunafanya vizuri kwa hiyo vikao hivi ni vya muhimu," amesema Mhe. Masaju. 

Jaji Mkuu amewaeleza Wadau hao kuwa, wao ni watu muhimu katika kusukuma mbele na kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki Mahakamani.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Mahakama itaendeleza utaratibu wa kufanya vikao hivyo na wadau, ambapo amesema jana tarehe 10 Juni, 2026 kulikuwa na mkutano na wadau wa Haki Madai.

"Leo tunafanya mkutano na Wadau wa Haki Jinai, sasa kama mnavyofahamu sisi utaratibu huu tutauendeleza, kumekuwa na tatizo kubwa hata katika mfumo wa haki jinai na jinsi tunavyofanya kazi katika Taifa hili, ndio maana Rais aliunda Tume, moja ya Tume za kwanza kabisa alizoziunda ilikuwa ni Tume ya Haki Jinai iliyoongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman ikiwa imesheheni na wajumbe wengine wengi maarufu mpaka Inspekta Jenerali wa Polisi, walikuwepo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali alikuwepo na watu wengine maarufu," ameeleza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kwamba, uundwaji wa Tume hiyo uliashiria kwamba bado kuna changamoto kubwa katika utekelezaji wa haki jinai katika Taifa. "Na ile Tume ilikuja na mapendekezo na mimi nilivyoteuliwa na Mhe. Rais kuwa Jaji Mkuu siku ananiapisha tarehe 15 Juni, 2025 alinielekeza pamoja na mengineyo kutekeleza mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai, sasa yale sisi hatuwezi kuyatekeleza peke yetu, lazima tuyatekeleze kwa kushirikiana na Wadau wa Mahakama waliopo kwenye mnyororo wa haki jinai,'" amesisitiza.

Kadhalika, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, "Mahakamani huwa hatukai peke yetu huwa tunakuwepo sisi Mahakama na watu wenye mashauri Mahakamani, watu wenye mashauri mahakamani wanaweza kuwa ni watu binafsi na Taasisi binafsi, miongoni mwao lakini pia wanaweza kuwa baina ya Taasisi za Serikali na watu na mashirika binafsi."

Kupitia ukweli huo, amesema ndipo unaona nafasi ya kwa mfano Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka wakiwakilisha Taasisi za Serikali kwenye mashauri mbalimbali ama wao wenyewe kama Washtaki na Wadai au Washtakiwa na Wadaiwa na ziko na Taasisi nyingine nyingi.

"Kwahiyo ndio maana tunakuwa na utaratibu huu wa kuwashirikisheni ninyi katika shughuli za Mahakama si kwa maana kwamba kwenye masuala ya ushirikishaji wa mashauri, tunashirikisha kwenye hizi shughuli kwa maana kujadili kwa pamoja changamoto zinazotukabili katika utoaji haki na ndio maana tumeanzisha hicho kitu kinachoitwa Haki Jinai," amesema Mhe. Masaju.

Mhe. Masaju ametoa kuwa, uwepo wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) wanawakilisha watu wanaoshtakiwa Mahakamani wenye makosa ya jinai lakini na hata wao wenyewe wanapoamua kushtaki mahakamani (private prosecution), lakini Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Katiba na Sheria ambaye naye amehudhuria kikao hicho ni muhimu ili Wizara hiyo ijue ni kitu gani kinaendelea ndani ya Mahakama ili wanaporatibu masuala ya kisera wajue hali ya Mahakama kwa maana ya mafanikio na changamoto zinazoukabili Mhimili huo.

Aidha, Jaji Mkuu amesema, hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokuwa akiwaapisha Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani, pamoja na mambo mengine alisema Haki ndio Msingi wa Amani.

"Na jana (tarehe 10 Juni, 2026) nilisema haki ni nini, nilisema haki ni uamuzi unaofanywa na Mahakama huru kwa kuzingatia Katiba na Sheria za Nchi hii kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa Mahakamani, hiyo ndio haki. Kwahiyo niwaalike wote kwa dhati tushiriki katika mkutano huu, hapa leo hatuko Mahakamani tupo katika mkutano kwahiyo tuwe wazi, tushauriane," amesisitiza Mhe. 

Katika Mkutano huo Mahakama na Wadau wametoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati waliojiwekea katika vikao viwili vilivyofanyika nyuma. Kupitia taarifa hizo, kila mdau ataeleza amefanya nini na kubaini maeneo waliyofanikiwa na walipokwama na kuweka mikakati zaidi ya kujikwamua ili kwenda pamoja.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akizungumza alipokuwa akifungua Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. Wa kwanza kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na kulia ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga.

Wadau mbalimbali walioshiriki katika Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Mikakati kutoka Mahakama ya Tanzania wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. 

Sehemu ya Viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika Mkutano wa Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. 

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)













JAJI MKUU ASHAURI KUFANYIKA KWA MAREKEBISHO YA SHERIA ZA MAHAKAMA ZA MAHAKIMU

·       Asema Mahakama imetunga Kanuni kuruhusu matumizi ya Ushahidi wa kieletroniki katika Mahakama za Mwanzo

·       Ahimiza matumizi ya Usuluhishi wa migogoro kwa kufuata mila na desturi za Kitanzania

·       Awataka Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea kujiandaa vema kabla ya kuja Mahakamani

·       Azishauri Wizara za Kisekta kusimamia uboreshaji wa sheria zenye mapungufu ili kuwezesha ufanisi wa utoaji haki

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ameishauri Serikali na hasa Wizara ya Katiba na Sheria inayohusika na Sheria za Mahakama za Mahakimu (The Magistrate’s Court Act) kufanya mabadiliko ili kuongeza mamlaka ya Mahakama za Mwanzo ya kifedha kwa mashauri yanayofunguliwa katika Mahakama hizo. 

Mhe. Masaju ametoa ushauri huo jana tarehe 10 Juni, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Tumezungumza hapa juu ya Uchumi wa Kidijitali (Digital Economy), siku hizi miamala mingi inafanyika kwa njia ya mtandao, mikataba inafungwa ya kielektroniki, kuna miamala ya kifedha inafanyika kwa njia ya mtandao na mambo ya aina hiyo, na sisi tunahimiza matumizi ya TEHAMA katika kufanikisha kitu hiki. Na ndio maana pia tumetunga kanuni hivi karibuni tarehe 04 Juni, 2026 za matumizi ya Ushahidi wa kielektroniki katika Mahakama za Mwanzo na ndio maana sasa tunaishauri Serikali na hasa Wizara ya Katiba na Sheria kufanya mabadiliko katika Sheria ya Mahakama za Mahakimu kuongeza mamlaka ya Mahakama za Mwanzo....,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema, kutokana na ukweli kwamba watu wengi wanatumia simu, imeleta msukumo wa kushauri kuwa matumizi makubwa ya Ushahidi wa kielektroniki. Amesema, “Katika kufanikisha suala hilo ndio maana Mahakama ya Tanzania inahimiza matumizi ya TEHAMA na hivi karibuni tarehe 04 Juni, 2026 tumetunga Kanuni za matumizi ya Ushahidi wa kielekitroniki katika Mahakama za Mwanzo ili kuziwezesha Mahakama hizo ambazo ziko nyingi ziweze kusikiliza mashauri mengi zaidi kuliko kwenda Mahakama ya Wilaya ambayo iko moja tu kila Wilaya.”

Kadhalika, Jaji Mkuu amewaeleza wajumbe wa mkutano huo kwamba, katika jitihada za kutekeleza wajibu wa utoaji haki, kuna mambo mengine ambayo Mahakama inafanya yenyewe na yale ambayo wanaona hayawezi kutekelezwa na Mahakama pekee huwashirikisha wadau kwa njia mbalimbali ikiwemo kupitia vikao.

Aidha, Mhe. Masaju amewajulisha wajumbe wa Mkutano huo kuwa, tarehe 30 Machi, 2026 jumla ya Mahakama za Mwanzo mpya 15 zimefunguliwa na kupeleka huduma za Mahakama karibu zaidi na wananchi kwa kufunguliwa jumla ya Masjala ndogo sita za Mahakama Kuu katika Mikoa ya Singida, Lindi, Njombe, Songwe, Katavi na Simiyu.

“Jitihada hizi ukiziangalia sana zipo katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050, kwa ule msingi mkuu wa Dira na vile vipaumbele vyake vinne vyote vinahusu Utawala wa Sheria na kama Taifa ili tuweze kwenda lazima utawala wa sheria uzingatiwe kwa sababu kila kitu kinatawaliwa na kuongozwa na sheria,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema kuwa, katika kuendelea kuimarisha Utawala wa Sheria, Mahakama imefanya mafunzo kuhusu Sheria za Kiislamu ili Mahakama za Mwanzo ambazo zinahudumia asilimia 70 ya wananchi, Sheria inasema watatumia Sheria za Kimila na Sheria za Kiislamu.

“Na katika viapo vyetu pia (sisi Majaji na Mahakimu), tunaambiwa kuzingatia Katiba, Mila, Desturi na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema Jaji Mkuu huku akisisitiza kuwa ni vyema kuzingatia mila na desturi za Tanzania katika utatuzi wa migogoro mbalimbali (ya madai, jinai au migogoro ya ndoa) badala ya kujikita katika mila za Kizungu.

Amesisitiza kuwa ni vyema kutumia na kuenzi mila na desturi za kitanzania kwa kuwa zina sifa ya watu kuishi bila kubaguana, kuzingatia usalama wa jamii, amani katika jamii, umoja wa kitaifa pamoja na kupunguza migogoro.

Mhe. Masaju ameikumbusha Mahakama ya Tanzania kutoa haki ipasavyo bila kufungwa na masharti ya kiufundi kupita kiasi yanayoweza kuzuia haki kutendeka.

“Majaji na Mahakimu niwaombe sana, muwe makini mnapoamua haki za watu kwa mujibu wa ushahidi. Ukishakuwa Jaji au Hakimu lazima uwe tayari kupokea malalamiko, Sisi wajibu wetu ni kutekeleza haki kwa mujibu wa Katiba na Sheria,” amesema Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju amesema akirejea Ibara ya 26(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) inayosema; Kila mtu ana wajibu wa kuifuata na kuitii Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ameongeza kuwa, “Ibara 26(2) inasema kila mtu ana haki kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria, kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na Sheria za Nchi’, kwa hiyo tuzifuate sheria kwakuwa zimeweka utaratibu wa kutatua migogoro na huku mahakamani migogoro itapungua lakini gharama zitakuwa nafuu sana kwa wadau wanapoenda kule kutatua migogoro yao kwa kuanzia kule kule kuja Mahakamani moja kwa moja ndio maana tunahimiza hili jambo.”

Mhe. Masaju amesema kwamba, "linapozungumziwa suala la uchumi, unazungumzia matumizi ya ardhi, kwa sababu kwenye ardhi ndipo mazao yanalimwa ni biashara hiyo, kwenye ardhi kuna maji ni biashara, kwenye ardhi kuna madini, kuna petroli ni biashara, uchumi wote siku zote ni ardhi."

Ameeleza kuwa, mashauri ya migogoro ya ardhi yamewekewa utaratibu mzuri kwenye Sheria ya Ardhi (The Land Registration Act) ili kuwezesha migogoro kutatulika kwa ufanisi na kupunguza gharama 

Jaji Mkuu amekitaka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kusaidia kuwashauri Wadaawa badala ya kwenda Mahakamani waanze kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi na ikishindikana ndio waende Mahakamani kama rufaa, hatua hiyo itasaidia kutatua migogoro ya wananchi haraka zaidi.

Sambamba na hilo, Mhe. Masaju amewataka Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea kuja Mahakamani wakiwa wamejiandaa na kuweka sawa nyaraka za mashauri ili kuepukana na uahirishaji wa mashauri usio na sababu za msingi. Na vilevile, amewaonya Mawakili kutoka TLS kusimamia vema nafasi yao na majukumu yao ipasavyo, kuwa imara na kuwajibika ipasavyo kuishauri Serikali badala ya kuwa kama chama cha siasa.

Mhe. Masaju amesema kuwa, hivi karibuni Mahakama itarekebisha Kanuni ya 96(7) ya Kanuni za Mahakama ya Rufani ambayo inatumiwa vibaya na Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea inafikia mwisho, "Tunafanya mabadiliko ya hizo kanuni, niwashauri kuzingatia umuhimu wa kuwasilisha Mahakamani kumbukumbu za rufaa zilizokamilika kwakuwa imekuwa ni kawaida sasa kuwasilisha mahakama kumbukumbu ambazo hazijatimia aidha kwa uzembe au kukusudia ili kuchelewa kesi.

Jaji Mkuu amewaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa, Mahakama imepokea pia ushauri wa kurekebisha Kanuni za (Remote proceedings) umepokelewa na watafanya mabadiliko. Ameongeza kwa kuwaomba wadau hao kuwasilisha maoni ya kanuni ambazo zimekaa vibaya au zina changamoto wasisite kusema au hata kwa maandishi ili zifanyiwe marekebisho na kuleta ufanisi.

Katika hatua nyingine, wajumbe wa mkutano huo wameshauri kuwa, zitungwe sheria zinazoziba mianya ya kisheria ya kukwepa kulipa kodi ili kuwezesha Serikali kupata mapato. “Huo ni ushauri mzuri, sisi kesi ikija mahakamani tutaamua kwa mujibu wa sheria zilizopo lakini ukweli ni kwamba kama kuna mianya hii inatengeneza migogoro inakuja huku mahakamani, sisi tunashauri kama sheria za namna hiyo zipo zirekebishwe zizibe mianya ili kuwezesha Serikali kupata mapato lakini itapunguza migogoro,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu kuboresha sheria, kama zipo ziboreshwe mapema, zile Wizara za Kisekta zinazohusika zichukue hatua mapema na pia kuoanisha sheria zinazogongana ili kuboresha ufanisi wa utoaji haki Mahakamani. Amesema lisipofanyika hilo msingi mkuu wa Dira hautatekelezeka, uchumi hautakua na hata wakiteuliwa Majaji wengi, kiwango cha migogoro kama kinaendelea kuongeza bado shida itakuwa palepale.

Mhe. Masaju ametoa rai kwa watumishi wa Serikali kwa ujumla kujituma na kusimamia utawala wa sheria ipasavyo ili kupunguza migogoro kwakuwa migogoro mingine inakuja kutokana na kukiuka sheria.

"Njia mojawapo ya kupunguza hii migogoro ni watumishi wa Serikali wote tufanye na kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia Katiba na Sheria za Nchi, ukishazingatia hivyo migogoro inatoka wapi? hakuna jambo katika nchi hii ambalo halisimamiwi na sheria, ukitaka kufunga ndoa kuna sheria, masuala ya ibada yana sheria, ukitaka kuwa Mganga wa Tiba za Asili kuna sheria, ukitaka kuandika habari kuna sheria, ukitaka kilimo, ufugaji uvuvi kuna sheria hakuna jambo la umma ambalo halisimamiwi na sheria. Sasa kama tunafanya kwa namna ya kukiuka sheria tunatengeneza migogoro," ameeleza Jaji Mkuu.

Kwa upande mwingine, Jaji Mkuu ametoa wito kwa Wadau hao kutenga muda wa kuhudhuria vikao hivyo muhimu ambavyo pamoja na mambo mengine vinalenga kuboresha ufanisi wa Mahakama na Sekta ya Sheria kwa ujumla.

“Wananchi wanatutegemea sisi katika ustawi na maendeleo ya Taifa letu, zile Taasisi ambazo zinalegalega tutawaacha nyuma,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Katika kikao hicho cha Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji, wajumbe wameweka mkakati mpya unaosema kuwa, ushirikiano unaotolewa katika usikilizwaji wa mashauri ya ardhi, biashara, kodi, mabenki, ushindani wa kibiashara na uwekezaji utolewe pia katika utekelezaji (execution) wa hukumu.

Mikakati mingine iliyowekwa na Wajumbe hao wakati wa mikutano miwili iliyofanyika awali ni pamoja na Mahakama na wadau wa   mnyororo   wa   haki waimarishe mawasiliano na mahusiano miongoni mwao, kwa lengo la kuchukua hatua   za   haraka   pale changamoto   zinazoathiri upatikanaji haki mapema zinapojitokeza.

Mkakati mwingine ni Wadau wa mnyororo wa haki wapatiwe elimu kuhusu sheria, kanuni na taratibu zinazoratibu uendeshaji wa mashauri ya ardhi, biashara, ushindani wa kibiashara, kodi, mabenki na uwekezaji ili kupata uelewa wa pamoja.

Kila taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki Mahakamani iwajibike ipasavyo kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia Katiba, sheria na maadili ya utumishi wa taasisi husika.

Mwingine ni Wadau wote   wa   Mahakama wenye   mashauri  mbele ya Mahakama wanapaswa kuhudhuria na kuyaendesha mashauri yaokikamilifu ili kuwezesha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo. Mahakama haitakuwa tayari kuahirisha shauri isipokuwa kama kutakuwa na sababu za msingi kufanya hivyo mingine mitano.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wadau wa Haki Jinai jana tarehe 10 Juni, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Wajumbe wa Mkutano huo wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele) alipokuwa akifunga Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.  

Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.