Ijumaa, 17 Aprili 2026

BARAZA LA WAFANYAKAZI DAR ES SALAAM LAKUTANA; JAJI MFAWIDHI AWAKUMBUSHA WAFANYAKAZI, WADAU KUWAJIBIKA IPASAVYO

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Mussa Maghimbi ametoa rai kwa wafanyakazi wa Mahakama na Wadau kwa ujumla kuwajibika ipasavyo ili kuhakikisha maono ya Mahakama ya Tanzania ifikapo 2050, iwe ya mfano duniani katika utoaji haki kama chombo huru chenye kuzingatia weledi, maadili, ufanisi na inayoaminiwa na wananchi katika jamii inayowazunguka.

Mhe. Maghimbi aliyasema hayo jana tarehe 16 Aprili, 2026 alipokuwa akiongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari jijini Dar es Salaam.

Katika hotuba yake Jaji Maghimbi, alisema maono hayo hayawezi kufikiwa kufikiwa bila kuwa na mikakati madhubuti katika utoaji haki ikiwa ni pamoja na kuimarisha upatikanaji wa haki, kuongeza imani kwa wananchi, kuimarisha uwezo wa rasilimali watu na kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Amesema kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 107A, Mhimili wa Mahakama ni Mamlaka yenye kauli ya mwisho katika Utoaji Haki katika Jamhuri ya Muungano, na Ibara ya 107B ya Katiba inatamka kuwa katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, Mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya Katiba na yale ya Sheria. “Ibara hizi zinatarajia watumishi kujipanga kimkakati na kuzingatia uadilifu, weledi, uwajibikaji na kwa kulenga matokeo makubwa,” amesisitiza.

Hali kadhalika, Jaji Maghimbi amewakumbusha wajumbe hao ahadi ambazo Mahakama imetoa kwa wananchi kwa wadau na kwa wanaofuata huduma mbalimbali mahakamani kuwa Maadhimisho ya Siku ya Sheria  kwa mwaka huu yaliongozwa na Kaulimbiu isemayo; “Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa,” ambapo waliahidi kuwa Viongozi na Wafanyakazi wa Mahakama  kutumia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kama kichocheo cha maboresho makubwa zaidi katika Mhimili wa Mahakama.

Akizungumzia kuhusu dhumuni ya Baraza la Wafanyakazi, Jaji Mfawidhi huyo na Mwenyekiti wa Kikao hicho alieleza kuwa ni kutoa fiursa kwa watumishi kupitia wawakilishi kujadili juu ya masuala ya msingi yanayohusu tija na ufanisi kwa upande mmoja na upande mwingine maslahi yao kama watumishi.

Aidha, Mhe. Maghimbi amesema kuwa, Wawakilishi wa Mabaraza ya Kanda wanatekeleza kwa vitendo takwa la kisheria linalotokana na Tamko la Rais (Tamko Na. 1 la Mwaka 1970) na Sheria nyingine za kazi zinazohimiza kuwakilisha wafanyakazi katika kufanya maamuzi mbalimbali kupitia Mabaraza ya Wafanyakazi.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti amesema, vikao vya Mabaraza ya Wafanyakazi viko kisheria na lengo la kuanzishwa kwa Mabaraza hayo ni kuwapa fursa watumishi ya kushauri Menejimenti, kuwaunganisha watumishi na menejimenti kusuluhisha  changamoto mbalimbali, kutoa shida zao za kiutumishi na maslahi, na wao kama Kanda wakishindwa zitawasilishwa Makao Makuu.

Amesema pia, Mabaraza hayo ni mahali pa kupata mrejesho wa mambo yanayofanyika ndani ya Kanda na mrejesho kwa ngazi ya Taifa.

Kabla ya kikao hicho kuanza kilitanguliwa na uchaguzi uliosimamiwa na Ofisa Kazi, Bi. Vaileth Ndeza wa kujaza nafasi zilizoachwa wazi baada ya Katibu kuhama Kanda ya Dar es Salaam na Katibu msaidizi kufariki dunia.

Wajumbe hao walimchagua Bw. Shadrack Mlomo kuwa Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dar es Salaam na Mhe. Juliana Nankoma kuwa Katibu Msaidizi na pia Wilky Kavunjika alichaguliwa kuwa Mjumbe.

Katika kikao hicho walikuwepo Maofisa kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) ambapo wameeleza faida za mifuko hiyo kwa watumishi wa umma.

Vikao hivyo vimekuwa vikifanyika kila mwaka na wajumbe kuwasilisha hoja zao na pia kushauri kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu utumishi na maslahi ya watumishi kwa ujumla.

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda ya Dar es Salaam wakiwa katika kikao cha baraza hilo jana tarehe 16 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari jijini Dar es Salaam.

 Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda ya Dar es Salaam wakiimbo wimbo wa wafanyakazi (solidarity forever).


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda hiyo, Mhe Salma Maghimbi (katikati) pamoja na Bw. Shadrack Mlomo (kushoto) ambaye ni Katibu wa Baraza hilo na Mhe. Juliana Nankoma (kulia) ambaye ni Katibu Msaidizi wa Baraza wakiimba wimbo wa wafanyakazi ujulikanao kwa jina la (solidarity forever) wakati wa Kikao hicho.


 Meza Kuu ikiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dar es Salaam. Katikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo, Mhe. Salma Mussa Maghimbi, kushoto ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana na kulia (aliyesimama) ni Mtendajiwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,  Bw. Sumera Manoti.

Ofisa Kazi, Bi. Vaileth Ndezi akitoa utaratibu wa kufanya uchaguzi wa Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe wakati wa kikao hicho. 

Bw.Wilcky Kavunjika akitoa shukurani kwa wajumbe baada ya kuchaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi Taifa.


Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana akitoa taarifa ya mashauri wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam. 

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti akitoa taarifa ya utawala wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam. 


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara)

 

 

MANYARA YAENDESHA MAFUNZO YA USULUHISHI KWA WADAU

Na. CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora amejumuika na wadau wa Mahakama katika kuendesha mafunzo ya Wiki ya Usuluhishi yakiwa na lengo la kuwajengea wadau wa haki madai uwezo wa kusuluhisha migogoro kwa njia za upatanishi, elimu hiyo ilitolewa katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mhe. Kamuzora alieleza kuwa, usuluhishi ni silaha ambayo inamaliza na kutatua migogoro na matatizo katika jamii kuliko hata kufika mahakamani na kusikiliza mashauri.

“Tukiachana na mashauri ya jinai yanayohusu makosa au uhalifu mkubwa, mashauri mengi ya madai yanaweza kwisha kwa kutumia Suluhu ambazo tunaweza kufanya wenyewe. Usuluhishi unasaidia sana katika kuokoa muda na gharama ambazo tunaweza kuzitumia wakati tumefungua mashauri mahakamani,” alieleza Mhe. Kamuzora.

Akitoa neno la utangulizi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo, aliwaasa watu wote kutumia muda wao kusikiliza elimu ambayo itatolewa kwa sababu ni ya msingi sana na ina tija katika kutatua migogoro mbalimbali katika jamii.

“Wananchi wengi mnafika mahakamani kwa ajili ya kutatua migogoro ambayo kimsingi mngeweza kuimaliza wenyewe kwa sababu mmekosa elimu hii ya usuluhishi. Hivyo, ninawasihi sana msikilize kwa makini yale ambayo yatakuwa yanafundishwa na wataalamu wetu,” alisema Mhe. Mpepo.

Naye, Wakili wa Kujitegemea Bw. Kuyengwa Ndonjekwa alisema kuwa, elimu hiyo ni muhimu sana kuendelea kutolewa mara kwa mara kwa sababu ina madhumuni ya kupunguza mzigo mkubwa kwa Mahakama wa kusikiliza mashauri na kuwafanya wananchi wapatane wenyewe kuliko kuendelea kuleta mashauri mahakamani hususan kwa masuala ambayo yanaweza kuzungumzika na suluhu ikapatikana.

Kwa upande wake mdau wa Mahakama Bw. Gwandu Nada ambaye ni mwananchi kutoka katika Wilaya ya Babati aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kufanya elimu hiyo ya upatanishi kuwa endelevu kwani itaisaidia jamii kuokoa muda wa kwenda mahakamani kutatua migogoro isiyokuwa na tija.

“Mafunzo haya ni mazuri kwa kuwa yamenifundisha kupatana na washtaki wangu mapema kabla ya kufikishana katika vyombo vya sheria na ninaahidi kwenda kupatana na wale ambao nimekosana nao kwa njia ya usuluhishi,” alisema Bw. Nada.

Waliohudhuria kupata elimu hiyo ni wadau wa Mahakama pamoja na wadaawa waliofika kwa ajili ya kupata mafunzo ya usuluhishi, Watumishi wa Mahakama Kuu Manyara, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Mwakilishi kutoka Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia, Ofisi ya Ustawi wa Jamii pamoja na baadhi ya wananchi.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora akitoa neno wakati wa utoaji elimu ya Usuluhishi iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu. Kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara Mhe. Mariam Lusewa.

Sehemu ya wananchi wakifuatilia mafunzo ya upatanishi 

Afisa Huduma kwa Jamii Mkoa wa Manyara Bw. Tumaini Moshi akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi waliofika Mahakama Kuu Manyara kupata elimu hiyo.

Mwananchi wa Wilaya ya Babati akitoa maoni yake wakati wa mafunzo elimu ya Wiki ya usuluhishi yaliyofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Kimario akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi waliofika Mahakama Kuu Manyara kupata elimu hiyo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo kushoto akizungumza na mmoja wa Wananchi waliofika kupata elimu ya upatanisho kwenye maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi. 

Sehemu ya wananchi waliohudhuria mafunzo ya wiki ya usuluhishi wakiwa katika picha ya Pamoja na Meza Kuu wakati wa utoaji elimu ya Wiki ya usuluhishi iliyofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Alhamisi, 16 Aprili 2026

WADAU WA SHERIA WANUFAIKA NA MAFUNZO MAALUM YA UTATUZI WA MIGOGORO

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu, Dodoma.

Mahakimu na Mawakili wa Mkoa wa Dodoma wameendelea kupatiwa elimu muhimu kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, hatua inayozidi kuimarisha mifumo ya haki na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kisheria nchini.

Mafunzo hayo yaliyofanyika jana tarehe 15 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dodoma kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) yamewakutanisha Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria.

Lengo la mafunzo hay oni kujengeana uelewa wa kina kuhusu matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR), njia inayozidi kupata nafasi kubwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka na kwa gharama nafuu.

Akitoa neno la ukaribisho, Naibu Msajili wa Mahakaa Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, aliwahimiza washiriki kutumia ipasavyo jukwaa hilo muhimu kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha weledi wao katika kushughulikia migogoro ya Wananchi.

Mafunzo hayo yaliendeshwa chini ya uratibu mahiri wa Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ameendelea kuonesha uongozi thabiti, weledi wa hali ya juu pamoja na dhamira ya dhati ya kuendeleza usuluhishi nchini.

Kupitia jitihada zake, Wadau wa Sheria wameendelea kunufaika na elimu yenye tija, huku akihamasisha kwa vitendo matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama suluhisho endelevu.

Mada mbalimbali ziliwasilishwa wakati wa mafunzo hayo na wataalamu wa sheria, akiwemo Mhe. Thurstone Kombe, Mhe. Sarah Mwalilino, Mhe. Judith Barigenge pamoja na wengine kutoka Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi nyingine kama CHRAGG.

Mada hizo zilieleza kwa kina umuhimu wa usuluhishi katika kupunguza migogoro, kuokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha mahusiano katika jamii.

Akisimamia majadiliano, Mhe.  Dkt. Khalfan alisisitiza kuwa usuluhishi si tu njia mbadala, bali ni nyenzo muhimu ya kujenga jamii yenye amani na mshikamano, huku akitoa wito kwa Wadau wa Sheria kuendelea kuipa kipaumbele.

Washiriki walipata nafasi ya kuuliza maswali na kuchangia hoja mbalimbali, hali iliyoonesha mwitikio mkubwa na uhitaji wa elimu hiyo katika jamii ya Wanasheria.

Akitoa neno la shukrani, Mhe. Zabibu Mpangule aliwashukuru waandaaji pamoja na washiriki wote kwa ushiriki wao, akibainisha kuwa mafunzo hayo yameongeza thamani kubwa katika utendaji wao wa kila siku.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa hotuba ya kufunga kutoka kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara ya Katiba na Sheria, aliyesisitiza umuhimu wa kuendeleza elimu ya usuluhishi ili kuhakikisha Wananchi wanapata haki kwa wakati, kwa ufanisi na kwa amani.

Kwa ujumla, tukio hili limeacha alama kubwa katika Mkoa wa Dodoma, likiwa ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za kuifanya Tanzania kuwa kinara wa matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati). Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


 

Mahakimu pamoja na Mawakili mbalimbali waliohudhuria elimu hiyo ya usuluhishi katika ukumbi uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo.

 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, akitoa neno la ukaribisho kwa wajumbe hao waliohudhuria elimu ya usuluhishi kwa Mahakimu na Mawakili.

 Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, akifuatilia kwa makini mada inayotolewa wakati wa utoaji wa elimu kwa Mahakimu na Mawakili.


 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu wa Dodoma walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi. Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watoa ujumbe maalumu kuhusu elimu ya usuluhish,i ambao pia ni Watumishi wa Mahakama Dodoma wakati wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

MAHAKAMA MOROGORO YAFANYA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI YA JINAI, MADAI

Na ASHA JUMA -Mahakama, Morogoro

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, imefanya kikao cha robo ya kwanza ya mwaka 2026, chenye lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kazi, hususan katika kusukuma mashauri ya jinai na madai.

Kikao hicho kilichofanyika jana tarehe 15 Aprili, 2026, katika ukumbi mkubwa wa mikutano uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro ni sehemu ya vikao vya kitaasisi vinavyolenga kuongeza ufanisi wa utoaji haki na kupunguza ucheleweshaji wa mashauri mahakamani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, aliongoza kikao hicho kiichowahusisha Wadau mbalimbali wa mnyororo wa haki, wakiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Amiri Msumi, Mtendaji wa Mahakama Kuu Morogoro, Bw. Ahmed Ng’eni na Mahakimu.

Wengine walitoka Ofisi ya Mawakili wa Serikali, Chama cha Wanasheria wa Kujitegemea, Ofisi ya Baraza la Ardhi na Nyumba, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Wasaidizi wa Sheria wa Majaji pamoja na Ofisi za Madalali.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Msumi alipongeza juhudi za Mahakama na Wadau wote kwa ushirikiano wao katika kutekeleza majukumu ya kila siku.

Alieleza hali ya mashauri kwa robo ya kwanza ya mwaka 2026, akisisitiza kuwa bado kuna haja ya kuongeza juhudi zaidi, hususan katika mashauri ya rufaa za madai ambayo yanahitaji msukumo wa ziada.

Mhe. Msumi alibainisha baadhi ya changamoto zinazosababisha ucheleweshaji wa mashauri, ikiwemo kuchelewa kuwasilishwa kwa kumbukumbu kutoka Mahakama za chini, hasa Baraza la Ardhi na Nyumba.

Alieleza kuwa hali hiyo hupunguza kasi ya usikilizaji wa mashauri na hivyo kuathiri utoaji wa haki kwa wakati.

Ili kukabiliana na changamoto hizo, Mhe. Msumi aliainisha mikakati mbalimbali, ikiwemo kusimamia kwa ukaribu hatua zote za awali za maandalizi ya mashauri, kuhakikisha zinazingatia muda uliowekwa kisheria, pamoja na kupanga na kuamua maombi na mapingamizi kwa wakati.

Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha mawasiliano na Mahakama ya Rufani ili kusaidia kusikiliza na kumaliza mashauri kwa ufanisi, pamoja na kuhakikisha ufuatiliaji wa karibu wa mashauri yote.

“Mikakati hii pamoja na changamoto hizi inabidi tuzifanyie kazi haraka iwezekanavyo kwa sababu tunashughulika na haki za watu,” alisisitiza Mhe. Msumi.

Kwa upande wao, Wadau waliohudhuria kikao hicho waliipongeza Mahakama kwa hatua ya kutumia mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa mashauri, wakieleza kuwa hatua hiyo imeongeza kasi na uwazi katika utoaji wa huduma za haki.

Baadhi ya Taasisi pia zimeanza kutumia mifumo hiyo ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia yanayoletwa na Mahakama.

Akihitimisha kikao hicho, Jaji Mfawidhi alipendekeza kuwepo kwa mafunzo ya muda mfupi kati ya Mahakama na Wadau wa sekta ya haki ili kusaidia kuongeza ufanisi katika utoaji haki, kuboresha ubora wa maamuzi, kuimarisha ushirikiano, pamoja na kupunguza makosa ya kisheria.

“Elimu hii itasaidia kung’amua vitu gani tunaweza kusaidiana na kujadiliana pamoja na kubadilishana ujuzi,” alisema Mhe. Ebrahim.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeweka msingi imara wa kuboresha utendaji wa Mahakama Kuu Morogoro kwa kushirikiana na Wadau wake, kwa lengo la kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati na kwa ufanisi zaidi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, akiongoza kikao hicho.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Amiri Msumi, akisoma taarifa yake katika kikao hicho.

Picha mbalimbali za wajumbe katika kikao hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.