Jumatatu, 13 Aprili 2026

MBEYA YAZIDI KUIMARISHA UTENDAJI KAZI KWA NJIA YA TEHAMA

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga amekutana na wasaidizi wa kumbukumbu wa Mahakama Mkoa wa Mbeya na kufanya nao mazungumzo kuhusu masuala muhimu ya kazi ikiwemo nidhamu, uadilifu, matumizi ya mfumo mpya wa kusajili mashauri pamoja na utunzaji wa vielelezo.

Ameyasema hayo wakati wa kikao kazi hicho kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya. Mhe Tiganga alisisitiza kuwa, maadili ya utumishi wa umma na nidhamu kazini ndiyo msingi wa kazi za Mahakama. Aliongeza kuwa, utunzaji sahihi wa nyaraka na vielelezo ni jambo la msingi katika kuhakikisha haki inatolewa kwa wananchi bila vikwazo.

“Ni vizuri kuusoma mfumo wa kusajili mashauri na kuufanyia kazi, lakini pia tuongeze nidhamu na maadili kazini. Tunapaswa kuhakikisha tunatunza kumbukumbu vizuri pamoja na vielelezo ili kutokwamisha zoezi zima la utoaji haki kwa wananchi.” alisema Mhe. Tiganga

Naye, Hakimu Mkazi Mkuu kutoka Kurungenzi ya usimamizi, ukaguzi, Maadili na ufuatiliaji wa huduma za kimahakama kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Mhe. Mohamed Siliti alipata fursa ya kuongea na watumishi hao kwa njia ya mtandao.

Akitoa elimu juu ya utunzaji wa kumbukumbu za Mahakama Mhe. Mohamed Siliti aliwaasa watunza kumbukumbu hao kutimiza wajibu wao na kuepuka kutumia lugha zisizo za staha na nzuri kwa wateja.

Kupitia kikao kazi hicho kiliweka maazimio na kukubaliana kufanya kazi kwa ushirikiano na weledi mkubwa huku wakizingatia maadili na nidhamu kufuatia kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Aziza Temu, Mtendaji wa Mahakama Bi Mavis Miti, Maafisa Utumishi pamoja na wasaidizi wa kumbukumbu Mahakama Mkoa wa Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (katikati) akiongoza kikao kazi hicho cha wasaidizi wa kumbukumbu na nyaraka (kulia) ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Bi. Marvis Miti.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akitolea ufafanuzi sehemu ya mambo yaliyojadiliwa kwenye kikao hicho.

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Mmoja wa wajumbe akizungumza jambo katika kikao hicho Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama Kuu Mbeya Bi. Isabela Osiah

Mmoja wa wajumbe akizungumza jambo katika kikao hicho Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya wilaya Mbeya Bi. Queen Mapunda.

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho
Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Sehemu ya Maafisa Utumishi Mahakama Mbeya walioshiriki kikao kazi hicho.



 

WIKI YA USULUHISHI YAANZA KUADHIMISHWA MKOANI MBEYA

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Katika kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi nchini Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya imeungana na Kanda zingine nchini kuadhimisha wiki ya Usuluhishi kuanzia tarehe 13 Aprili, 2026 hadi tarehe 17 Aprili, 2026 yenye kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania”.

Katika maadhimisho hayo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga, Naibu Wasajili pamoja na Mahakimu wameweka mkakati wa kupokea na kusajili migogoro mbalimbali ihusuyo ardhi, ndoa na madai ya kawaida na kuwapangia wasuluhishi wenye nyenzo za usuluhishi kwa ajili ya kuitatua migogoro hiyo.

Mbali na hilo Uongozi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya umeweka dawati maalumu la kupokea migogoro katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya pamoja na kuandaa vyumba maalumu vitakavyotumika kufanya usuluhishi.

 Wananchi wote waliokuwa wamejitokeza walianza kwa kupatiwa elimu ya usuluhishi na misingi yake, ambapo wananchi walipata nafasi ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi wa kina juu ya masuala mbalimbali ya kisheria yanayohusu usuluhishi wa migogoro.

Sehemu ya watumishi na Mawakili wa Serikali wanaoshiriki katika maadhimisho hayo


Sehemu ya watumishi na Mawakili wa Serikali wanaoshiriki katika maadhimisho hayo

 Hakimu Mkazi Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Adriano Mtafya akitoa elimu ihusuyo usuluhishi na misingi yake kwa wananchi (hawapo pichani)

Wananchi waliofika mahakamani wakipatiwa elimu aliyesimama ni Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Paul Rupia.

Wananchi waliofika mahakamani wakipatiwa elimu ya usuluhishi inayoadhimishwa Kanda ya Mbeya.


CHAMA CHA MAJAJI NA MAHAKIMU MUSOMA CHAFANYA MKUTANO

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma.

Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma, kilifanya mkutano wake tarehe 10 Aprili, 2026 kujadiliana masuala ya kiutendaji na kuweka mikakati mbalimbali kuhakikisha suala la utoaji wa haki linatekelezwa kama inavyokusudiwa bila mkwamo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, alisistiza umuhimu wa Mahakimu kuhudhuria mikutano, kwani ndio sehemu pekee wanapopata nafasi ya kukutana kwa wingi na kujadiliana mambo mbalimbali.

“Kanda inavyo vikao mbalimbali ikiwemo cha menejimenti, kusukuma mashauri, vikao vya Mawakili na Madalali na vingine vingi, ila huko kote Mahakimu hawaingii kwa pamoja, isipokuwa katika mkutano wa TMJA ambao ndio jukwaa pekee linalowawezesha Mahakimu kwa umoja wao kukukutana na kujadili masuala yanayowahusu,” alisema Mhe. Mtulya.

Pamoja na kuwasisitiza umuhimu wa mkutano huo, Jaji Mfawidhi aliwahimiza kuzingatia na kutekeleza maelekezo ya Viongozi mbalimbali, ikiwemo kusimamia utekelezaji wa malengo yanapangwa na Menejimenti ya Kanda, kwani yanasaidia kuboresha utendaji wa kazi na kuwezesha Kanda ya Musoma kushika nafasi ya pili kitaifa kwa kasi nzuri ya usikilizaji wa mashauri.

Aidha, katika mkutano huo mada mbalimbali zilizijadiliwa ikiwa ni pamoja na ushughulikiwaji wa mashauri ya mirathi. Wajumbe wa mkutano huo walikumbushana maelekezo mbalimbali ya Viongozi kuhusu utekelezaji wa masuala ya mirathi, changamoto wanazokutana nazo katika kushughulikia masuala hayo pamoja na namna bora ya kuyashughulikia.

Vilevile, wajumbe wa mkutano huo kwa pamoja walishiriki mafunzo yaliyotolewa kwa njia ya mtandao kuhusu matumizi ya Sheria ya Kiislam katika Mahakama za Mwanzo. Mafunzo hayo yaliyotolewa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania.

Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA), Kanda ya Musoma, Mhe. Hadija Masala (aliyesimama) akitoa neno la utangulizi wakati wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma.

Wajumbe wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma wakiwa wamesimama kwa ajili ya kutoa heshima zao na kuwakumbuka watumishi wa Kanda ya Musoma waliofariki katika kipindi cha mwaka 2025/2026, akiwemo aliyekuwa Hakimu Mahakama ya Mwanzo Bunda Mjini, Mhe. Patrick Masenge na aliyekuwa Dereva Mahakama ya Wilaya Bunda, Bw. Abriel Lazaro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama) akitoa neno la ufunguzi wakati wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musom,a Mhe. Oscar Lyimo (aliyesimama) akiwasilisha mada kuhusu ushughulikiwaji wa mashauri ya mirathi wakati wa mkutano huo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (wa pili kushoto), akisisitiza jambo wakati wa mkutano huo.

Wajumbe wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma, ambao pia ni Majaji wa Mahakama Kuu Musoma, wakifurahia jambo wakati wa mkutano huo, wa kwanza kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Marline Komba na wa kwanza kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Kamazima Kafanabo.

Wajumbe wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma wakifuatilia kwa makini mafunzo yaliyotolewa kwa njia ya mtandao kuhusu matumizi ya Sheria ya Kiislam katika Mahakama za Mwanzo.

Sehemu ya wajumbe wa mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Kanda ya Musoma wakiwa katika picha ya pamoja.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

TUMIENI UJUZI MTAKAOUPATA KUPUNGUZA MLUNDIKANO WA MASHAURI MAHAKAMANI: JAJI RWIZILE

Na FESTO SANGA, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile amewataka washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi kwa Maofisa wa Mahakama wa Kanda za Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza kutumia ujuzi watakaoupata kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani.

Mhe. Rwizile ameyasema hayo leo tarehe 13 Aprili, 2026 mkoani Kigoma wakati akifungua mafunzo ya usuluhishi yatakayoendeshwa kwa siku tano na kuhudhuriwa na washiriki 16. 

“Tumieni mbinu za usuluhishi kama njia ya utatuzi wa migogoro ili kuongeza ufanisi, kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani, na kuboresha upatikanaji wa haki kwa wananchi” alisema Jaji Rwizile

Aliongeza kuwa, mafunzo hayo ni mwendelezo wa Mafunzo ya Msingi ya Usuluhishi na Mafunzo ya Wakufunzi (ToT) yaliyofanyika mwaka 2025, yaliyowawezesha Maofisa Mahakama kupata mafunzo ya kina kutoka kwa wataalamu wa usuluhishi kutoka Ujerumani kwa lengo la kuandaa wakufunzi wa ndani watakaosambaza ujuzi huo.

Alibainisha kuwa, mafunzo kama hayo tayari yamefanyika Arusha, Dodoma, Dar es Salaam na Mbeya, huku Kigoma ikiwa hatua ya mwisho ya utekelezaji wa awamu hii, inayotarajiwa kuwafikia takribani washiriki 80.

Aidha, alifafanua kwamba, mafunzo hayo yanafanyika sambamba na Wiki ya Usuluhishi Kitaifa, na kueleza kufurahishwa na ushiriki wa washiriki katika Wiki ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala, akisisitiza kuwa fursa hiyo itaongeza uelewa wa vitendo, kuimarisha upatikanaji wa haki na kuchangia moja kwa moja katika kuongeza ufanisi wa Mahakama, sambamba na kuakisi dhamira ya Mahakama katika kuendeleza mifumo ya utatuzi wa migogoro na kuboresha huduma za haki kwa wananchi.

Naye Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna Rweikiza  akizungumza kwa niaba ya Mhe.Dkt. Paul Kihwelo, Jaji wa Rufani na Mkuu wa Chuo alibainisha dhamira thabiti ya Chuo hicho katika kujenga na kuendeleza uwezo wa Maofisa wa Mahakama katika maeneo mbalimbali, ikiwemo usuluhishi, kama sehemu ya juhudi za kuimarisha ufanisi na upatikanaji wa haki.

Kwa upande wake, Bi. Rose Nyatega kutoka Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania) alieleza kuwa, mafunzo hayo yanaendeleza mpango ulioanzishwa mwaka 2025, ambapo kundi la Majaji na Mahakimu waliopatiwa mafunzo liliundwa kupitia ufadhili wa GIZ Tanzania chini ya mradi wa PROLA, pamoja na kuendelea kuimarisha ushirikiano na IJA pamoja na Mahakama ya Tanzania katika kuboresha mifumo ya utoaji haki kupitia programu za mafunzo na matumizi ya mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania), Wawezeshaji wa Mafunzo hayo ya Usuluhishi ni Mhe. Rwizile ,Jaji Mfawidhi Kigoma na Mhe. Fadhili Yohana Mbelwa, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akifungua mafunzo ya Usuluhishi leo tarehe 13 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kigoma.

Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna Rweikiza akifurahia jambo na washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi (hawapo katika picha). 

Sehemu ya washiriki wa Mafunzo wakimsikiliza kwa makini Mgeni Rasmi ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (hayupo katika picha).

Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ  Tanzania), Bi. Rose Nyatega akielezea mpango wa mafunzo ya Usuluhishi.

Washiriki wa mafunzo wakiwa katika majadiliano ya mbinu za Usuluhishi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi.  Wa pili kushoto ni Naibu Msajili Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigomawa pili kushoto ni Bi. Rose Nyatega kutoka Shirika la Maendeleo la Ujerumani, wa kwanza kulia ni Mhe Aristrida Tarimo  na wa kwanza  kushoto ni Mhe. Husna Rweikiza, Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka IJA.

(Habari hii imehaririwa na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

MBEYA YAENDESHA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ambaye ni Mweneyekiti Baraza la wafanyakazi Mahakama Kuu aliongoza watumishi wa Kanda hiyo kuendesha baraza hilo katika kujadili mambo mbalimbali yanayohusu watumishi ili kuendelea kujenga umoja, maadili na mshikamano mahali pa kazi.

Akiongea katika kikao hicho kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Mbeya. Mwenyekiti huyo wa Baraza alisema, umuhimu wa kikao hicho ni kujadili dira ya taasisi kimkoa, kikanda na kuelezea muelekeo wa utekelezaji wa majukumu kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

“Nawaomba wajumbe kuwa wawazi katika kutoa Mawazo ya kujenga taasisi, mkikumbuka kwamba mnawawakilisha watumishi zaidi ya 300 katika kikao hiki lakini pia mkawe mabalozi wa kuwasilisha yale yote yaliyojadiliwa hapa,” alisema Mhe. Tiganga,

Kikao hiki kulihudhuriwa na Maafisa wawili kutoka TUGHE na wajumbe mbalimbali kutoka Mahakama kwa mujibu wa Mkataba mpya wa Baraza la wafanyakazi wa Mahakama.

Aidha katika kikao hicho pia kulifanyika uchaguzi wa kuwachagua Viongozi ambao ni Katibu na Katibu Msaidizi wa Baraza la wafanyakazi wa Mahakama Mkoa wa Mbeya na uchaguzi wa wajumbe wawakilishi wawili wa baraza kuu Taifa kufuatia wale waliokuwepo muda wao kuisha.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (kushoto) akiongoza kikao hicho cha Baraza na kulia ni Katibu wa Baraza la wafanyakazi Mahakama Mkoa wa Mbeya Bw. Alintula Ngalile.

Katibu wa Baraza la wafanyakazi Mahakama Mkoa wa Mbeya Bw. Alintula Ngalile akielezea jambo katika kikao hicho.


Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (katikati) kulia ni Afisa kutoka Tughe (aliyesimama) kushoto ni Katibu wa Baraza la wafanyakazi Mahakama Mkoa wa Mbeya Bw. Alintula Ngalile.



WATUMISHI MANYARA WAFANYA UTALII HIFADHI YA TAIFA TARANGIRE

Na. CHRISTOPHER MSAGATI–Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. Ilvin Claud Mugeta, amewaongoza watumishi wa Mahakama Kanda hiyo, kufanya ziara ya utalii wa ndani iliyofanyika mnamo tarehe 10, Aprili 2026 katika Hifadhi ya Taifa Tarangire mkoani Manyara.

Akizungumza na watumishi kwa nyakati tofauti wakati wa maandalizi na hitimisho la ziara hiyo, Mhe. Mugeta alieleleza lengo la ziara hiyo ni kutambua maeneo mapya ambayo watumishi wengi hawajawahi kuyafikia, kupata furaha na kuimarisha afya ya akili.

“Muda mrefu tunakaa ofisini tukiwa tunashughulika na majukumu ya usikilizwaji wa mashauri bila kupata fursa ya kufahamu masuala mengine mengi ambayo tunapaswa kuyafahamu. Hili jambo linaweza kupunguza ufanisi wa utendaji kazi kama tunakosa muda wa kuwaza masuala mengine nje ya kazi, ziara hii ya Tarangire ituwezeshe kuwa na mtazamo mpya lakini pia kuyafahamu maeneo ambayo yanatuzunguka,” alisema Mhe Mugeta.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora aliwapongeza watumishi wote waliofanikiwa kushiriki ziara hiyo na kuwashauri watumishi kuendelea kushirikiana katika masuala kama hayo yanapojitokeza kwa kuwa pia yanaongeza upeo wa ufahamu ambao unaimarisha utendaji kazi.

“Nawapongeza watumishi wote ambao no watalii wenzangu waliofanikiwa kusafiri kwa ajili ya utalii wa ndani, nawashauri siku nyingine ziara kama hii ikitokea tuungane sote kwa pamoja kwa kuwa tutakuwa tumeongeza kitu kikubwa sana katika upeo na ufahamu wetu na kuboresha ufanisi wa kazi,” alisema Mhe. Jaji Kamuzora.

Katika hatua nyingine, watumishi ambao walikuwa wamepanda basi walikwama kwenye matope ambayo yamesababishwa na mvua ambazo zinaendelea kunyesha nchi nzima jambo liliwafanya watumishi hao kushuka kwenye basi na kuanza kulisukuma. Hata hivyo walijulishwa na waongoza watalii kuwa hayo ni mambo ya kawaida kutokea katika mbuga na pia ni sehemu ya masuala ambayo yanafanya ziara ipendeze zaidi.

Watumishi 112 wa kada mbalimbali kutoka Mahakama za ngazi mbalimbali wakiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mahakimu Wakazi wafawidhi wa Wilaya zilizopo katika Kanda ya Manyara, Mahakimu na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara walishiriki ziara hiyo ikiwa ni muendelezo wa kutambua vivutio vya asili vilivyo ndani na nje ya Mkoa wa Manyara pamoja na kuwafanya watumishi kuendelea kuishi kwa umoja na ushirikiano.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara wakati wa ziara ya kuona Wanyama katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta (wa nne kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi ambao wameajiriwa siku za hivi karibuni katika ziara ya kuona Wanyama Tarangire.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara wakiwa wanasukuma basi lililokwama kwenye matope wakati wa Ziara ya kuona Wanyama katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.

Kundi la Swala wakiwa wanaonekana wakila majani katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.

Tembo akiwa anaonekana akila majani katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyama Tarangire.

Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora (aliyesimama) mbele, akitoa neno kwa watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara kabla ya kuanza safari ya kuelekea Tarangire.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara wakiwa katika picha ya pamoja mbele ya jengo la Mahakama Kuu Manyara wakati wakijiandaa kuelekea Tarangire.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


 

TANZIA: OPERETA WA KOMPYUTA MKUU MAHAKAMA KUU MOSHI AFARIKI DUNIA

 

Marehemu Lukio Ezekiel Mrutu enzi za uhai wake.

TANZIA

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake, Bw. Lukio Ezekiel Mrutu aliyekuwa Opereta wa Kompyuta Mkuu aliyekuwa akihudumu Mahakama Kuu Kanda ya Moshi.

Kwa mujibu wa Mtendaji Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Bi. Maria Francis Itala marehemu Lukio amefariki dunia saa 8 usiku wa kuamkia leo tarehe 13 Aprili, 2026 katika Hospitali ya Rabininsia iliyopo Tegeta jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.

Bi. Itala amesema, taratibu za mazishi zinaendelea kuratibiwa na mara baada ya kukamilika taarifa za mazishi zitatolewa.

Uongozi wa Mahakama ya Tanzania unatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki na watumishi wote kufuatia msiba huu mkubwa wa kuondokewa na mpendwa wetu.

BWANA ALITOA, BWANA AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE.

BARAZA LA WAFANYAKAZI KANDA YA ARUSHA LAKETI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda hiyo, Mhe. Frank Mahimbali ameongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo na kuwataka wajumbe wa Kikao hicho kutumia fursa ya uwepo wa baraza hilo kama eneo muhimu la kujadili na kutoa mapendekezo juu ya kuboresha mazingira ya kazi.

Akifungua kikao cha Kikao cha Baraza hilo kilichofanyika tarehe 09 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha, Mhe. Mahimbali alisema kuwa, umuhimu wa mabaraza ya wafanyakazi ni mkubwa katika kulinda haki na maslahi ya wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kuleta amani na utulivu mahali pa kazi kwa kutatua migogoro kwa njia ya mazungumzo.

“Hivyo, ni matarajio yangu kuwa kila mjumbe katika kikao hiki atashiriki kikamilifu kwa kutoa michango huru ya mawazo na pia kwa pamoja tuweze kuibua na kujadili hoja za kuwasilisha Makao Makuu kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi au ufafanuzi zaidi,” alisema Jaji Mahimbali.

Aliongeza kuwa, Vikao vya Baraza la Wafanyakazi vinasaidia katika kuongeza uelewa wa wafanyakazi kuhusu sheria za kazi, usalama kazini na majukumu yao kwa waajiri.

Jaji Mfawidhi huyo aliwahamasisha wajumbe wa Baraza hilo kwamba watumie fursa ya uwepo wa baraza hilo ili kuendelea kuwa na weledi katika kutekeleza shughuli za Mahakama na ujenzi wa Taifa kwa ujumla.

Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Arusha kilifanya uchaguzi wa Viongozi wa Baraza hususan katika nafasi za Katibu na Katibu Msaidizi, ikiwa ni pamoja na Mwakilishi wa watumishi katika Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ambapo Bi. Therezia Shetui ambae ni Msaidizi wa Kumbukumbu alichaguliwa kuwa Katibu wa Baraza la Wafanyakazi.

Aidha, Bw. Raphael Magoha ambae ni Ofisa Hesabu alichaguliwa kuwa Katibu Msaidizi na kwa upande wa nafasi ya Mwakilishi wa Wafanyakazi katika Baraza Kuu la Wafanyakazi, Msaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Arusha, Bi. Felister Bisangwa alichaguliwa katika nafasi hiyo. Viongozi hao waliochaguliwa watahudumu kwa kipindi cha miaka miatatu ijayo.

Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Arusha kilihudhuriwa na wajumbe mbalimbali wakiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Sophia Massati, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama, Ofisa Kazi Mfawidhi wa Mkoa wa Arusha, Bw. Goodluck Luginga na Katibu wa TUGHE Mkoa wa Arusha aliyewakilishwa na Bi. Christina Ngatunga.

Wengine ni Mahakimu Wakazi Wafawidhi na Maofisa Tawala na Utumishi wa Mahakama pamoja na watumishi wa kada nyingine walioalikwa katika kikao hicho kutoka Wilaya zote za Mkoa wa Arusha.

Uwepo wa Mabaraza ya Wafanyakazi ni kwa mujibu wa Sheria na Agizo Na. 1 la mwaka 1970 ambalo linaelekeza utaratibu wa kuundwa kwa Mabaraza katika Taasisi na Ofisi za Umma kwa kuzingatia sheria mbalimbali za Kimataifa ikiwemo zile za Shirika la Kazi Dunia (ILO), na imesaidia kwa kiasi kikubwa kuleta haki, usalama na ustawi mahali pa kazi na hatimaye kuleta maendeleo kwa mfanyakazi, mwajiri na uchumi wa Tanzania kwa ujumla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha na Mwenyekiti wa Baraza la Wanyakazi wa Mahakama mkoani Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akiongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama kilichofanyika tarehe 09 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Ofisa Kazi Mfawidhi Mkoa wa Arusha, Bw. Goodluck Luginga akitoa ufafanuzi wa jambo fulani wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Arusha kilichofanyika tarehe 09 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Arusha wakifuatilia kwa makini kilichokuwa kikijiri katika Kikao cha Baraza hilo kilichofanyika tarehe 09 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

 (Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

Jumapili, 12 Aprili 2026

MAHAKAMA NI ZA WANANCHI KWA AJILI YA WANANCHI; JAJI MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amesema kuwa, Mahakama ni mali ya wananchi na kwamba Mahakama hizo zipo kwa ajili kuwahudumia wananchi.

Mhe. Mahimbali ambaye alikuwa Mgeni Rasmi wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya tatu za Ketembeine, Makuyuni na Terrat zilizopo mkoani Arusha uliofanyika tarehe 10 Aprili 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli. 

Jaji Mfawidhi huyo alisisitiza kuwa, tukio hilo la uzinduzi na urasimishaji wa Mahakama hizo ni hatua muhimu katika kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi wote wa Tanzania na ujenzi wa Mahakama hizo ni matunda ya dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa, wananchi wote wanapata haki mapema ipasavyo na kwa gharama nafuu.

“Kwa muda mrefu, wananchi wa maeneo hayo wamekuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata huduma za Mahakama, kwa mfano; wananchi wa Kata za Makuyuni, Mswakini, Esiraeli na Nanja walikuwa wakisafiri umbali wa kilomita 36 kwenda katika Mahakama ya Mwanzo Mto wa Mbu au kusafiri kilomita takribani 70 kwenda katika Mahakama ya Mwanzo Kisongo iliyopo Monduli mjini ili kupata huduma, hivyo ujenzi wa Mahakama hizi umesogeza huduma kwa wananchi hao,” alisema Jaji Mahimbali.

Vilevile Mhe. Mahimbali aliongeza kuwa, kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za Mahakama kulisababisha baadhi ya wananchi kukata tamaa na kuacha kufuatilia mashauri yao na hivyo kupoteza haki zao. Pia wananchi wengine walikuwa wakiamua kujichukulia sheria mkononi mwao, hivyo Mahakama hizo zinazozinduliwa zinakwenda kuhudumia jamii zinazozizunguka Mahakama hizo kwa kusogeza huduma karibu na makazi yao na hivyo kurahisisha upatikanaji wa haki na kupunguza muda wa kupata haki, hivyo kutumia muda wao mwingi katika shughuli za kiuchumi na kujiongezea kipato.

Jaji Mahimbali amewashukuru wadau wa Mahakama hususan Halmashauri za Wilaya Arusha, Monduli na Longido wa kushiriki kikamilifu kufanikisha ujenzi wa Mahakama hizo mpya na kuongeza kuwa, ushirikiano huo ni kielelezo cha dhana ya kwamba ‘Mahakama ni ya Wananchi na kwa Wananchi.’ Amesisitiza kuwa huduma zitakazopatikana katika majengo hayo ya Mahakama ziwe ni kwa ajili ya maslahi mapana ya wananchi na si vinginevyo.

Aidha, ameongeza kwa kuwataka wananchi na watumishi wa Mahakama kutumia Mahakama hizo kwa malengo yaliyokusudiwa, huku akiwasisitiza wananchi kuwa, wanao wajibu wa kutambua kuwa majengo hayo ni mali yao na kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku na kuyalinda ikiwa ni pamoja na kuyaheshimu.

Kwa upande mwingine, Jaji Mfawidhi huyo amewasisitiza watumishi wa Mahakama hususan Mahakimu kwamba wanapaswa kuyatumia majengo hayo kama nyenzo ya kuimarisha imani ya wananchi kwa mfumo wa utoaji haki nchini.

Akiwasilisha taarifa fupi ya ujenzi wa Mahakama hizo, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama alisema kuwa, ujenzi wa Mahakama hizo ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa kwanza na wa pili wa Mahakama uliolenga kuboresha upatikananji na utoaji haki mapema ipasavyo kupitia uboreshaji wa Miundombinu ya Majengo na Mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mijini na vijijini.

Bi. Kapama aliongeza kuwa jumla ya miradi minne ya ujenzi ilitekelezwa, yaani ujenzi wa Mahakama za mwanzo Maji ya Chai, Terat, Makuyuni na Ketumbeine. Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine ilijengwa kwa fedha za ndani wakati mahakama hizo nyingine zilijengwa kwa fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia.

Bi. Kapama alisema kuwa, ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni na Terrat ulianza tarehe 06 Julai, 2024 na kukamilika tarehe 31 Mei, 2025. Ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine ulianza 01 Juni, 2024 na kukamilika 06 Oktoba, 2025. 

Mahakama za Mwanzo Makuyuni na Terrat zimeanza kutoa huduma kwa wananchi mnamo mwezi Agosti, 2025 na Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine ilianza kutoa huduma kwa wananchi tarehe 22 Oktoba, 2025. 

Naye Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Groliana Kimathi alisema kuwa, Serikali itaendelea kuhakikisha kuna amani na usalama ili kuwezesha shughuli mbalimbali za Kiserikali na wananchi kufanyika katika hali tulivu. Ameishukuru Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo zilizozinduliwa  na kuongeza kuwa, ujenzi wa Mahakama hizo ni ishara ya dhati ya Serikali kuwajengea mazingira mazuri watumishi wa Mahakama katika kutekeleza majukumu yao na kutoa huduma kwa wananchi.

Aidha, amewasihi watumishi wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa weledi na kujiepusha na vitendo vya rushwa ambavyo vinaweza kutia doa Mhimili wa Mahakama.

Mkuu huyo wa Wilaya ameahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Mahakama katika kutekeleza majukumu yote ambayo yapo kwa mujibu wa taratibu zilizopo. Aidha, ameiomba Mahakama kuendelea kutenga siku maalum ya kutoa elimu ya sheria kwa wananchi kwani itasaidia kupunguza ukiukwaji wa sheria miongoni mwa wananchi na hatimaye kuwa na jamii iliyostaarabika.

Akizungumza katika hafla hiyo, Diwani wa Kata ya Makuyuni, Mhe. Ngayok Mollel ameishukuru Serikali kwa kuwaletea Mahakama katika Kata yao na kuongeza kuwa, wananchi wa Kata yake katika vijiji vya Makuyuni, Mbuyuni na Naiti ikiwa ni pamoja na Kata za jirani wanafurahia kupata huduma katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni kwani ni karibu na makazi yao.

Uzinduzi wa Mahakama hizo unafanya jumla ya Mahakama za Mwanzo zinazofanya kazi mkoani Arusha kufikia 22 na hivyo kupanua wigo na kusogeza karibu utoaji wa huduma za Mahakama kwa wananchi katika Wilaya ya Arusha, wananchi wa Kata za Murieti, Terrat, Sombetini, Mbauda, Eleroi, Sokoni 1 na Olasiti ambao walikuwa  wakisafiri umbali wa takribani kilomita 19 hadi 23 kufuata huduma katika Mahakama za Mwanzo Arusha Mjini na Themi, sasa wamesogezewa huduma karibu yao kwa kujengewa Mahakama ya Mwanzo Terrat.

Pia, Katika Wilaya ya Longido, wananchi wa Kata za Ketumbeine, Lang’atabash, Elerininto, Nondoto, Gelarirumbwa na Gelarimerugwe walikuwa wakisafiri umbali wa Kilomita 50 kufuata huduma za Mahakama ya Mwanzo Longido Mjini, kwa sasa wanapata huduma hizo katika Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine.

Hafla hiyo ya uzinduzi rasmi wa Mahakama za Mwanzo mpya mkoani Arusha imehudhuriwa na Viongozi na Wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo Majaji na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Arusha, Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mahakimu, Viongozi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Diwani wa Kata ya Makuyuni, Viongozi wa Dini, Viongozi wa Kimila na wananchi kwa ujumla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akizungumza na wananchi pamoja na wadau waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama mpya za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni iliyopo wilayani Monduli.


Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Gloriana Kimath akitoa salamu kwa wananchi na wadau waliofika katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama akisoma historia fupi ya ujenzi wa Mahakama hizo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama (kushoto) akikabidhi taarifa fupi ya historia ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali (kushoto picha ya chini) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli. Picha ya juu akiwa na viongozi mbalimbali walioalikwa katika hafla hiyo. 


Wananchi na wadau mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akipanda mti ikiwa ni ishara ya kumbukumbu na sehemu ya kuboresha mazingira ya Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat iliyofanyika tarehe 10 Aprili, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali (katika) pamoja na Majaji wengine wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Gloriana Kimathi (wa pili kushoto mstari wa mbele) wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni Monduli. Waliosimama nyuma ni kulia Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Dkt. Kassian Mshomba na kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama.

 Majaji wa Mahakama Kuu Arusha wakiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi rasmi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni Monduli. 

Diwani wa Kata ya Makuyuni, Mhe. Ngayok Mollel akitoa salamu za wananchi wa Kata ya Makuyuni wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026  Makuyuni Monduli.

Kiongozi wa Mila wa Kabila la Maasai Monduli, Bw. Samwel Laiza akisoma dua wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026  Makuyuni Monduli.

Kikundi cha Burudani cha Kabila la Wamaasai kutoka Makuyuni Juu kiitwacho Nashpai Eko kikitumbuiza wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026  Makuyuni Monduli.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Makuyuni moja kati majengo ya Mahakama za Mwanzo mpya tatu zilizozinduliwa.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)