Jumatano, 1 Julai 2026

KITUO JUMUISHI TEMEKE, MFUKO WA FIDIA KWA WAFANYAKAZI WABADILISHANA UZOEFU

  • Waweka mikakati kuboresha utoaji haki kwenye mashauri ya mirathi, madai ya fidia

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Temeke

Mahakama Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke hivi karibuni kilishiriki mafunzo ya kubadilishana uzoefu na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) ili kuongeza ufanisi katika kuwahudumia wananchi, hasa katika utoaji wa haki zinazohusu fidia katika mashauri ya mirathi.

Mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Destiny Hall ulioko Kibaha katika Mkoa wa Pwani yalifunguliwa rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mhe. Mwanabaraka alisisitiza kuwa lengo la mafunzo hayo ni kutatua changamoto za ucheleweshaji wa haki kwa warithi na kuimarisha ushirikiano wa kiutendaji kati ya Taasisi hizo mbili. 

Katika Kikao hicho, mada ziliwasilishwa kuhusu Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi, Taratibu na changamoto za madai ya fidia kwa wafanyakazi pamoja na taratibu za ufunguaji na uendeshaji wa mashauri ya mirathi.

Bw. Deo Victor Ngowi kutoka Idara ya Huduma za Sheria WCF, akiwasilisha mada kuhusu sheria inayoongoza fidia kazini, alitoa ufafanuzi kuwa fidia hutolewa na WCF kutokana na ajali au vifo kazini na hivyo haiwezi kudaiwa kama sehemu ya mirathi na wasimamizi wa mirathi.

Alieleza pia kuwa fedha hizo hazilipwi kwenye akaunti ya mirathi, bali huenda moja kwa moja kwenye akaunti binafsi za wanufaika sahihi.  Bw. Ngowi alichambua makundi muhimu yanayolipwa na WCF ambayo ni wenza na watoto wenye umri chini ya miaka 18.

Aidha, alieleza kuwa madai yote ya fidia ni lazima yawasilishwe WCF ndani ya miezi 12 tangu kutokea kwa ajali au kifo kwa mnufaika wa WCF.

Bw. Ngowi aliwaelimisha washiriki pia juu ya nani hufaa kuwa wanafaika wa WCF kwa kusema kuwa, “WCF haihusiki na wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi kama mikataba ya chini ya siku 30, wafanyakazi wa kujitolea, pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama.”

Meneja Msimamizi wa Ulipaji Fidia, Bi. Rehema Mwakabongo, alipokuwa akiwasilisha mada, alieleza faida mbalimbali zitolewazo na mfuko huo, ikiwemo gharama za matibabu ya ulemavu wa muda au wa kudumu, msaada wa matibabu nje ya nchi, na fao la mazishi.

Alieleza changamoto zinazojitokeza katika ulipaji wa fidia kama udanganyifu kutoka kwa wanufaika, ikiwemo uwepo wa nyaraka zaidi ya moja ya cheti cha kifo, changamoto ya utofauti wa majina ya walipwaji, hivyo kusababisha uwepo wa ‘deed poll’ za udanganyifu.

Bi. Rehema alielezea pia changamoto ya waajiri na waajiriwa kuchelewa kuwasilisha nyaraka muhimu kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wakati, hivyo kuomba ushirikiano mkubwa na Mahakama pale inapohitajika.

Katika kikao hicho, mada kuhusu utaratibu wa ufunguaji mashauri ya mirathi, uendeshaji hadi kufungwa zilitolewa na  Mahakimu, Mhe. Stephanie Kagaruki Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Mwanzo, kwa kushirikiana na Mhe. Mhangwa Yunge, Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya.

Mahakimu hao walifafanua mada juu ya taratibu za ufunguaji na uendeshaji wa mashauri ya  mirathi, taratibu na mamlaka za Mahakama kulingana na ngazi zake.

Mahakama za Mwanzo husikiliza mirathi ya kiislamu na ile ya mila na desturi, Mahakama za Wilaya na Mahakama Kuu husikiliza mirathi ya kikristo na asili ya kiasia.

Pia watoa mada walieleza juu ya nyaraka zinazoweza kutumika ili WCF itoe malipo, nyaraka za Mahakama kama vile fomu namba 80 kwa Mahakama Kuu na Wilaya pamoja na Fomu No.5 kwa Mhakama ya Mwanzo zinazoonyesha orodha ya mali za marehemu.

Fomu No.81 kwa Mahakama Kuu na Wilaya pamoja na Fomu No. 6 kwa Mahakama ya Mwanzo zinazoonyesha hesabu za mali ya marehemu ikiwaonyesha wanufaika na walichopewa.

Watoa mada walisema muhtasari wa kikao cha familia sio takwa la kisheria bali hutumika kama utaratibu wa kujiridhisha. Walieleza pia hukumu inaweza kuwa nyaraka muhimu, lakini sio inayowataja warithi halisi, hivyo ni muhimu kuthibitisha wanaostahili kulipwa.

Watoa mada walieleza kuwa hakuna haja ya msimamizi wa mirathi kuagizwa hati ya kiapo cha uthibitisho kwa kuwa hati ya usimamizi wa mirathi kutoka mahakamani ni uthibitisho tosha kuwa ameteuliwa na Mahakama.

Washiriki wa mafunzo hayo walipata nafasi ya kujadili juu ya mada zilizowasilishwa na kuibua maswali muhimu kama vile stahiki za watoto waliozidi miaka 18 wenye changamoto maalumu za kuwafanya kuwa chini ya uangalizi wa wazazi wao.

Mfuko wa WCF uliahidi kuifanyia kazi changamoto hiyo kwa kuwa kwa sasa watoto wa kuanzio umri huo sio wanufaika wa mfuko.

Kuhusu maboresho ya sheria, washiriki waliishauri WCF kuona namna ya kurahisisha michakato, ikiwemo kuheshimu nyaraka za Mahakama bila kuweka ulazima mkubwa wa cheti cha kifo pale ambapo Mahakama imeshathibitisha vifo hivyo.

Kikao kazi hicho kilifungwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Gladys Barthy, ambaye aliishukuru WCF kwa fursa hiyo ya kujengeana uwezo. Ili kuhakikisha makubaliano hayo yanafanyiwa kazi kwa vitendo, Mahakama imeahidi kuteua mtu maalum (focal person) atakayekuwa kiunganishi cha haraka kati ya Mahakama Kituo Jumuishi Temeke na WCF ili kuharakisha huduma kwa wananchi.

Jaji Mfawidhiwa Mahakama Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, akifungua mafunzo ya kubadilishana ujuzi katika ukumbi wa Destiny Hall Kibaha Pwani.

Washiriki wa mafunzo hayo wakisikiliza hotuba kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu Wa WCF, Bw. Abrahamu Siyovelwa.

Majaji Kutoka Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke walioshiriki katika kikao mafunzo wakifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa.

Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Mhe. Stephani Kagaruki,  akitoa mada juu ya taratibu za ufunguaji wa mirathi Mahakama za Mwanzo  katika kutoa haki kwa wananchi.

Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Mhangwa Yunge, akitoa ufafanuzi juu ya mada za Usimamizi wa mashauri ya mirathi katika Mahakama ya Wilaya na Mahakama Kuu Temeke.

Meneja Malipo toka WCF, Bi Rehema Kabongo, akitoa mada kuhusu taratibu za fidia kwa wafanyakazi.

Jaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Gladies Barthy akihitimisha rasmi mafunzo hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.


WADAU WA HAKI JINAI SONGWE WAKUTANA KUPANGA MIKAKATI YA UONDOSHAJI MASHAURI

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe

Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe, hivi karibuni ilifanya kikao cha kusukuma Mashauri ya Jinai, kikilenga kutathimni na kuimarisha usimamizi na ufanisi wa utoaji wa haki katika Masjala ya Songwe.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe na kuongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha na kuhudhuriwa na wadau wa Haki Jinai kutoka Taasisi mbalimbali Mkoa wa Songwe.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde alisoma taarifa ya mwenendo wa Mashauri ya Haki Jinai Masjala ya Songwe kuanzia tarehe 30, Machi, 2026 mpaka tarehe 26 Juni, 2026 kwa kuainisha mashauri yote yaliyofunguliwa, mashauri yaliyomalizika na mashauri yaliyoendelea kusikilizwa.

Mhe. Minde aliaainisha changamoto zinazoathiri usikilizwa wa mashauri ya jinai na baadae zilipatiwa ufumbuzi. “Tunaomba ushirikiano wa wenu kwa Mahakama na sisi tunajitahidi kadri tunavyoweza ili kuhakikisha mashauri aliyosalia yanamalizika kwa wakati,” alisistiza.

Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Malata alisisitiza kwamba, kikao hicho kinajikita katika mikakati ya kuhakikisha mashauri ya jinai kwa ngazi ya Mahakama Kuu yanasikilizwa haraka ili kuepuka mlundikano wa Mashauri huku tukiendelea kuwahimiza wadau kila mmoja wetu kutimiza wajibu wake katika mnyororo wa haki jinai ili kusaidia Mahakama kutekeleza jukumu lake la msingi ipasavyo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Tawi la Songwe, Bw. Moses Mwampashi amesema, idadi ya Mawakili mkoani Songwe haitoshi ukilinganisha na uhitaji wa wananchi katika uwakilishi wa Mawakili mahakamani Songwe, aliendelea kubainisha kuwa uhitaji wa Mawakili ni mkubwa ukilinganisha na idadi ya mashauri yaliyopo mkoani humo.

Wakili huyo, ameliomba jukwaa la Haki Jinai Mkoa wa Songwe kusaidia ongezeko la Mawakili ili kutoa huduma ya kisheria na uwakilishi mzuri wa wananchi mahakamani kwa wakati, hatua hiyo itaiwezesha Mahakama kumaliza mashauri mapema ipasavyo.

Katika kikao hicho, Wadau wa Haki Jinai pamoja Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe waliazimia kuwa Wafungwa na Mahabusu wafikishwe kwa wakati, Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea wafike mahakamani saa moja kabla ya muda ulioandikwa kwenye Summons, kujiridhisha kwa kina juu ya mashahidi wanaofika kutoa ushahidi mahakamani.

Vilevile, wadau waliazimia kwamba, ikiwa wakili atashindwa kuendelea kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wake arudishe doc brief ili wakili mwingine aweze kupangiwa shauri hilo, pia uongozi wa TLS uwakumbushe mawakili majukumu yao kisheria ikiwemo kuwatembelea mahabusu kabla ya kuletwa mahakamani, Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea kujiandaa ipasavyo kabla ya kuingia mahakamani. Vyombo vya haki jinai kuzingatia taratibu za kisheria zinazosimamia masuala yote ya haki jinai.

Mhe. Malata aliwashukuru wadau wote waliofika katika kikao hicho na kuwasisitiza kutimiza na kutekeleza maazimio yote waliyokubaliana kwa kuzingatia sheria za haki jinai zinavyotaka, aliomba ushirikiano ili kuboresha utoaji wa haki jinai kwa wananchi.

Kikao hicho cha Wadau wa Haki Jinai Songwe kilihudhuriwa na wajumbe kutoka Ofisi ya Mkuu wa Magereza, Polisi, Ofisi ya Upelelezi Mkoa, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Ustawi wa Jamii, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Ofisi ya Uangalizi Mkoa wa Songwe na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala, Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha (kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde (kulia) wakiwa kwenye kikao cha kusukuma mashauri ya jinai.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Stephano Minja akifuatilia kikao hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha (kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde (kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama mara baada ya kuhitimisha kikao cha kusukuma mashauri ya jinai.

Sehemu ya wawakilishi wa baadhi ya Taasisi zilizoalikwa za haki jinai mkoani Songwe.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Bw. Mohamed Kimungu Rajabu akifuatilia kikao hicho.

Sehemu ya Wadau wa Mahakama waliohudhuria kikao hicho akiwemo Bi.Tea Mshana, Bi. Maria Sanga kutoka NPS-Songwe pamoja na Bi. Geladina Theobard kutoka Ofisi ya Uangalizi-Songwe.



JESHI LA MAGEREZA LAIPONGEZA MAHAKAMA PWANI KWA KUFANYA KAZI KWA BIDII

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Jeshi la Magereza Mkoa wa Pwani wameipongeza Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani humo pamoja na Mahakama ya Wilaya Kibaha kwa kufanya kazi kwa bidii na kuondoa msongamano gerezani.

Akitoa pongezi hizo wakati wa Kikao cha Kusukuma Mashauri kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Pwani tarehe 30 Juni, 2026, Mrakibu Msaidizi wa Magereza, Basili Kiwone amesema wamebakiwa na Mahabusu 21 tu tofauti na kipindi cha nyuma ambapo Mahabusu walikuwa wengi kuliko wafungwa.

Katika kikao hicho cha kusukuma mashauri kilichoongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi amesema kwa sasa Mahakama ya Hakimu Mkazi inayo mashauri mawili tu na bado hayazidi miezi sita na Mashahidi wanakuja.

Kikao hicho kimeazimia kwamba upande wa Mashtaka kuhakikisha Mashahidi wanafika Mahakamani kwa wakati, hilo ni azimio endelevu na pia kuhakikisha upelelezi unakamilika mapema ipasavyo. 

Aidha, Mhe. Mkhoi amesisitiza kuwa, upande wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mashahidi wafike kwa wakati ili mashauri hayo yasivuke miezi sita.

Akizungumza wakati wa kuwakaribisha Wadau wa Haki Jinai, Kaimu Mkuu wa Gereza la Mkuza, Mrakibu Msaidizi wa Magereza, Eliatosha Yamakili alisema, siku ya jana (tarehe 30 Juni, 2026) walikuwa na Mahabusu 21 tu na Wafungwa 54 wa Kitanzania na Wafungwa Raia wa Burundi watatu, mfungwa mmoja Raia wa Ethiopia na Mzuiwa mmoja Raia wa Ethiopia, hivyo jumla yao wote wako 80 ingawa Gereza hilo lina uwezo wa kubeba Wahalifu 140.

Akieleza utekelezaji Mrakibu Msaidizi, Yamakili amesema kwa sasa wanaendelea na ujenzi wa jiko la kisasa ambalo litatumika kuandaa chakula cha Wahalifu na kwa sasa mfumo wa gesi umeshafungwa kilichobaki ni hatua ya umaliziaji tu.

Vilevile, ameeleza kwamba, Gereza hilo linafanya ukarabati wa Selo za Kike ambapo wameanza kwa kuweka sakafu mpya na kupaka rangi kwenye Selo moja, kujenga sehemu ya chakula na kupumzika.

Katika hatua ya kutekeleza dhana nzima ya urekebu Gereza hilo la Mahabusu Mkuza lilipokea ugeni wa Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Mashariki kwa madhumuni ya kuona shughuli zote za kujifunza na kuona namna bora ya kuandaa upimaji wa Wanafunzi kwa lengo la kutoa vyeti kwa watakaohitimu na kufaulu.

Naye, Mahabusu Simon Marekani akisoma risala kwa niaba ya Mahabusu na Wafungwa wenzake amewashukuru Wadau wa Haki Jinai kwa maboresho wanayoyafanya gerezani hapo licha ya kuwa zipo changamoto mbalimbali ambazo waliomba kuwasilisha kwa timu hiyo ambazo ni pamoja na upande wa mashtaka  kutopeleka mashahidi kwa wakati mpaka wapate msukumo wa Hakimu ndipo walete Mashahidi na wakati mwingine hawafiki kwa wakati ukizingatia mashauri mengi mashahidi ni Askari Polisi wa Mkoa wa Pwani.

Changamoto nyingine walizielekeza kwa Jeshi la Polisi kwa Watuhumiwa kukaa muda mrefu Kituo cha Polisi zaidi ya mwezi mmoja bila kufikishwa Mahakamani, Watuhumiwa kubadilishiwa vielelezo,  kulazimishwa kuweka saini kwa Dole Gumba kwenye maelezo wasiyoyatambua na pia Watuhumiwa kudhulumiwa mali zao hasa wakiwa Kituo cha Polisi mfano Simu, Pesa, Viatu na vitu vingine.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Haki Jinai mara baada ya kukagua Gereza la Mkuza. Wa pili kushoto ni  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha Mhe.  Emmael Lukumai, wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mkuza, Mhe. Leah Mkono, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mlandizi na wa pili kulia ni Mrakibu Msaidizi wa Magereza,Eliatosha Yamakili.



Wadau wa Haki Jinai wakiendelea na Kikao cha Kusukuma Mashauri kilichofanyika tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani.

 Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi (kushoto) akiongoza Kikao cha Kusukuma Mashauri. Kulia ni Katibu wa kikao hicho ambaye ni Wakili wa Serikali, Bi. Laura Kimaro.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

MAHAKAMA PWANI YAFANYA ZIARA YA KITALII VISIWANI ZANZIBAR

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Zanzibar

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani wakiongozwa na Naibu Msajili ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Joyce Mkhoi na Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bw. Nestory Mujunangoma wamefanya ziara ya kitalii visiwani Zanzibar mwishoni mwa wiki iliyopita ikiwa ni ziara ya kujifunza pamoja na kuburudika na kufurahi kwa pamoja ili kujiweka sawa kiroho, kimwili na kiakili baada ya kazi.

Akizungumza baada ya kuhitimisha utalii huo, Mhe. Mkhoi alisema anatumaini kila mtumishi amefurahia utalii huo na kwamba baada ya hapo deni lililobaki ni kwa watumishi pindi warudipo katika Vituoni kufanya kazi kwa bidii na kwa ari mpya.

Naye Mtendaji wa Mahakama Pwani, Bw. Mujunangoma alisema dhumuni la ziara hiyo ni kupumzisha akili kutokana na kazi na vilevile kujifunza historia mbalimbali Visiwani humo.

Akitoa shukrani kwa niaba ya Watumishi wote, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Mkuranga, Mhe. Sameera Suleiman alisema wamefurahia utalii huo maana imewapa fursa nzuri ya kufahamiana Wilaya moja na nyingine lakini pia wamepata fursa ya kutengeneza kumbukumbu kubwa katika maisha. 

Ziara hiyo ilijumuisha maeneo ya Msitu wa Jozani (Jozani Forest) ambapo watumishi hao walipata wasaa wa kubadilisha mandhari ya mjini na msituni ambapo waliweza kuona ngedere wekundu na pia kuona uwekezaji katika msitu huo.

Hali kadhalika waliweza kutembelea Shamba la Viungo (Spice Farm) ambapo walijifunza namna viungo vinavyotumika pamoja na ulimwaji, utunzwaji hadi kuvunwa kwake.

Pia walitembelea sehemu maarufu ya Forodhani na kushuhudia mandhari nzuri ya Bahari, kuzama kwa jua (Sun Set) na Mchezo maarufu wa Makachu.

Aidha, katika utalii huo walitembelea Mji maarufu wa Nungwi na kufanya utalii wa ndani ya maji kwa kutumia Jahazi linaloongozwa na upepo na pia kutembelea Makazi ya Kasa na kupata wasaa wa kuwalisha Kasa hao, pia kupata historia ya kuzaliwa, ukuaji wao na namna ya kuwatunza.   

Ziara hiyo ya siku tatu ilianza tarehe 26-28 Juni, 2026 ikihusisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mahakama za Wilaya za Kibaha, Kisarawe, Mkuranga, Mafia na Rufiji. 

Watumishi wa Mahakama Pwani wakicheza Mchezo wa Makachu Forodhani Zanzibar walipofanya ziara Visiwani humo hivi karibuni.


Baadhi ya Watumishi wa Mahakama Pwani wakilisha Kasa

Baadhi ya Watumishi wa Mahakama Pwani wakisikiliza maelezo ya Mtunza Shamba la Viungo (hayupo pichani) walipotembelea shamba hilo na Msitu wa Jozani wakati wa Ziara yao ya Utalii waliyofanya hivi karibuni.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi (katikati) akiwa na baadhi ya watumishi wa Mahakama Pwani wakiwa katika Ziara ya Utalii Visiwani Zanzibar.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma) 

 

 

 

 

Jumanne, 30 Juni 2026

JAJI MKUU AKEMEA VIKALI VITENDO VYA KUINGILIA AMRI NA MAAMUZI YA MAHAKAMA

·       Awataka Madalali na Wasambaza Nyaraka za Mahakama kusimama ipasavyo katika utendaji kazi wao

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amekemea vikali vitendo vya baadhi ya Viongozi wa Serikali na wa Kisiasa kuingilia utendaji wa shughuli za Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kwa kisingizio kwamba wao ni Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 30 Juni, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Hizo sheria zinazowapa madaraka hazikuwapa mamlaka ya kuingilia utekelezaji wa amri na maamuzi ya Mahakama. Wachukulieni hatua. Haiwezekani Mahakama imeshatoa amri halafu mtu mwingine anazuia, hiyo inakuwa ni Mahakama au ni kitu gani? Ni lazima tutofautishe shughuli za kisiasa na shughuli za kutoa haki zinazofanywa na Mahakama,” amesema Jaji Mkuu.

Akizungumzia kuhusu Changamoto na Usimamizi wa Sheria, Jaji Mkuu amewaeleza, Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kuwa nao wana changamoto ndio maana wanaruhusu wanasiasa kuingilia utendaji kazi wao bila kuwachukulia hatua.

“Hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria na hata mimi Jaji Mkuu siko juu ya sheria. Na kwanza hata mimi kwa kiapo changu na Majaji wote hapa na Mahakimu wote, na hata Wasajili tunaapa tunapotekeleza majukumu yetu kuzingatia Katiba, mila na desturi, na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bila hofu, upendeleo, wala chuki,” amesema Mhe. Masaju. 

Aidha, Jaji Mkuu amewataka Madalali na Wanasheria wao kuchukua hatua kali za kisheria, ikiwa ni pamoja na kuzuiliwa kinyume cha sheria (false imprisonment) au uzuiaji wa utekelezaji wa amri halali, Maofisa wa Polisi au Viongozi wanaokiuka Sheria kwa majina yao binafsi, kwani Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameshafafanua kuwa wavunja Sheria watagharamia makosa yao wenyewe.

Mhe. Masaju amesema kuwa, katika kipindi hiki ambacho Tanzania inatekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, msingi Mkuu wa Dira hiyo inahusu Utawala Bora na Haki, hivyo, hakuwezi kuwa na ‘Utawala Bora na Haki’ kama maamuzi ya Mahakama yanaingiliwa na watu wengine bila sababu za msingi.

Amesisitiza kuwa Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatamka wazi kuwa, kila mtu ana wajibu wa kuitii Sheria za pamoja na haki ya kulinda na kusimamia Katiba.

“Ili kufikia malengo haya, Mhimili wa Mahakama lazima ubaki na hadhi na heshima yake na pande zote zitekeleze wajibu wao kwa usafi na uadilifu ili kuzuia mianya ya kuingiliwa,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Aidha, Jaji Mkuu amewakumbusha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kuwa, kama wanataka wasiingiliwe nao wanapaswa kuwa wasafi kwa kutekeleza wajibu wao kwa mujibu wa Katiba, Sheria, Maadili na Kanuni zilizowekwa ili kutotoa fursa kwa watu wengine kuwaingilia katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kadhalika, amewataka wadau hao muhimu wa Mahakama kuwa na uwezo wa kumudu majukumu yao kwa ufanisi unaotakiwa. Akiwasisitizia jambo hilo, ameeleza: “Mmeshukuru hapa kwamba Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kinatoa mafunzo yanayowasaidia; lakini moja ya masharti ya kupewa kazi hizi ni kuwa na uwezo wa kumudu majukumu husika. Masharti yanasema wazi kuwa mnatakiwa muwe watu mnaojua taratibu za mambo mnayoyasimamia. Sasa kama mlikuwa hamyajui, mlipataje hizi nafasi ? Tutawanyang’anya hizi leseni.”

“Mmewekewa utaratibu ambao lazima ninyi wenyewe muuheshimu mnapokuwa mnatekeleza majukumu yenu, utaratibu huu umetajwa katika Sheria, yale maadili yenu, ningependa niwarejeshe hapa katika hayo maadili myazingatie, haya yatawafanya basi mkiyatekeleza na kuyaishi muwe na sifa sasa ya kuwa Maofisa wa Mahakama. Mkishindwa kuyaishi haya na kuyatekeleza hata kama sisi nia yetu ingetaka ninyi muwe Maofisa wa Mahakama,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amebainisha kuwa, Misingi ya kimaadili kwa Madalali na Wasambaza Nyaraka imebainishwa katika Nyongeza ya Pili na ya Tatu, mtawalia ya Kanuni za Madalali na Wasambaza Nyaraka (Uteuzi, Malipo na Nidhamu), Tangazo la Serikali Na. 363 la 2017 kama ilivyorekebishwa na Tangazo la Serikali Na. 106 la 2019.

Aidha, ametaja sifa za Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kuwa ni pamoja na Uadilifu ambapo amesema suala la kuwa na uadilifu ni jambo la msingi na wanatakiwa kulidumisha.

“Mtakuwa Waadilifu kwa kutekeleza Sheria za Nchi na Katiba, lakini mtakuwa waadilifu kuyaishi maadili ya utumishi wenu na mtakuwa waadilifu wakati wa kutekeleza majukumu yenu, myatekeleze kwa uadilifu ipasavyo,” amesisitiza.

Jaji Mkuu ametaja sifa nyingine wanayopaswa kuwa nayo kuwa ni kuwa Waaminifu kwa kile ambacho wanakifanya kwa kutekeleza sheria kwa uaminifu bila kutumia vibaya mamlaka yao sambamba na kufanya kila hatua kwa uaminifu.

“Tulianza shughuli hii kwa dua na sala, Mungu hadhihakiwi unachopanda ndicho unachovuna, hatuwezi kutumia fursa hii kujinufaisha na kuonea watu, kimsingi wanaotumia hii vibaya watawajibishwa na Mungu, nendeni msome Zaburi 37 muone inasema nini. Hatuwezi kuwa wakati wote tunalitaja jina la Mungu, lazima tuishi hilo kauli Mungu hadhihakiwi, huwezi kulichukulia jina la Mwenyezi Mungu bure kama jina langu mimi. Kuna amri inasema usilitaje jina la Mungu wako bure yaani unalichukulia poa na unamchukulia poa,” amesema.

Mhe. Masaju amesema, Mahakama haipaswi kuwa na sifa mbaya na kwamba ikiwa na sifa mbaya, itakosa uhalali wa kuwa Mahakama ya kufanya maamuzi, hivyo amewataka kutoshiriki kuchafua sifa ya Mhimili huo.

Ameongeza kwa kusema kuwa, kama Mahakama imeamua sahihi, halafu wao wanapofanya tofauti na kilichoamriwa wanakosea na maana yake ni kupotosha uamuzi wa Mahakama hali inayosababisha Mahakama iwe na sifa mbaya.

Aidha, amewataka Wadau hao muhimu wa Mahakama kufanya kazi kwa uadilifu na uaminifu na wawe na uwezo wa kumudu majukumu yao kwa ufanisi ipasavyo. Amesema, kutokufanya hivyo kutaleta migogoro isiyoisha Mahakamani.

Ameongeza kuwa, sifa nyingine ni pamoja na Usiri (Confidentiality), kutovujisha siri za mchakato wa maamuzi ya Mahakama kabla hayajatamkwa rasmi na kutoa Huduma Bora (Quality Service) zenye viwango vinavyoacha picha chanya kwa jamii.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema Madalali ni Nguzo Muhimu ya Haki, ambapo amewatambua kama Maofisa muhimu wanaotekeleza majukumu ya ukamilishwaji wa maamuzi ya kisheria.

"Ninyi ni watu muhimu sana. Vinginevyo, kwenye mashauri ya madai, maamuzi ya Mahakama yasingekuwa yanatekelezwa. Na kama maamuzi hayatekelezwi, Mahakama itadhulika, na hatma yake ni uvunjifu wa amani na kupotea kwa uhuru wa Mahakama," amesema Mhe. Masaju.

Aidha, amewakumbusha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kuhusu kuwa na hofu ya Mungu, Jaji Mkuu amewataka kusoma Zaburi ya 37 na kuacha tabia ya kulitaja jina la Mungu bure huku matendo yao yakiwa ya kidhalimu.

“Sheria inawataka Madalali kutambua makundi maalum yenye uhitaji na kutoa huduma kwa uangalifu mkubwa bila kuwaletea fedheha au majonzi zaidi. Makundi hayo ni pamoja na Watu wazima, Walemavu, Wagonjwa sana, Waliogubikwa na majonzi ya kufiwa, Wanawake wajawazito,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, kila Dalali wa Mahakama ana wajibu wa kuheshimu utu, faragha na staha ya mwanamke. Ambapo amesisitiza, hawa watu wengine ni wajane, msiende kuwanyang'anya mali zao na kuwaongezea majonzi."

Kanuni ya 7 ya Kanuni za Madalali na Wasambaza Nyaraka zinabainisha jukumu kuu la Madalali wa Mahakama kuwa ni kutekeleza amri au maamuzi ya Mahakama zilizo ndani ya mamlaka yake, na itajumuisha majukumu mengine kama; kukamata na kuuza mali ya mdaiwa kwa ajili ya kutekeleza amri au maamuzi ya Mahakama kama ilivyoelekezwa kwenye Amri ya 21 ya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai na Sheria Nyinginezo Pamoja na kutekeleza amri za kuwaondoa/kufukuza wadaiwa (eviction orders). 

Majukumu mengine ni kutekeleza amri nyingine yoyote iliyotolewa na Mahakama;kuandaa na kuwasilisha Mahakamani taarifa au mrejesho namna utekelezaji ulivyofanyika; na kutekeleza maelekezo mengine yoyote yaliyotolewa na Mahakama. 

Aidha, Kanuni ya 8 ya Kanuni za Madalali na Wasambaza Nyaraka zinabainisha jukumu kuu la Wasambaza Nyaraka kuwa ni kufikisha nyaraka za kimahakama na zile zisizo za kimahakama, na itajumuisha kufikisha; Wito wa Mahakamani (summonses), notisi, nakala za hukumu, uamuzi (rulings), amri za Mahakama (decree or orders), notisi za uteuzi kwa madalali wa Mahakama na nyaraka nyingine zozote zinazotolewa na Mahakama.

Kwa mujibu wa Orodha ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kwa mwaka 2026/2027 iliyotolewa na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa idadi yao ni 99.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mhe. George Masaju akitoa hotuba yake ya akifungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania leo tarehe 30 Juni, 2026  kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Baadhi ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania walioshiriki katika Mkutano Mkuu wakimsikiliza na kufuatilia hotuba ya Jaji Mkuu (hayupo katika) alipokuwa akifungua Mkutano huo leo 
tarehe 30 Juni, 2026  kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mkutano huo iliyokuwa ikitolewa na Mgeni Rasmi Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 30 Juni, 2026  kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga ambaye pia ni Mwezeshaji katika Mkutano huo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika hafla ya Ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania leo tarehe 30 Juni, 2026 Makao Makuu ya Mahakama-Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Mwenyekiti wa Chama hicho, Bi. Mwamvua Kigulu

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama walioudhuria katika Mkutano Mkuu wa Chama hicho 
leo tarehe 30 Juni, 2026 Makao Makuu ya Mahakama-Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Mwenyekiti wa Chama hicho, Bi. Mwamvua Kigulu.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



MADALALI, WASAMBAZA NYARAKA WA MAHAKAMA WAASWA KUWA WAADILIFU

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma amewaasa Madalali wa Mahakama na Wasambaza Nyaraka   kufanya kazi zao kwa kuzingatia Uadilifu wa hali ya juu na Sheria.

Mhe. Mruma ametoa rai hiyo leo tarehe 30 Juni, 2026 alipokuwa akitoa neno kwa niaba ya Jaji Kiongozi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

"Mkikosa uadilifu katika hilo, mnatengeneza mazingira rahisi kwa watu wa Mihimili mingine kuingilia Mhimili wa Mahakama na kuhalalisha uingiliaji wao," amesema Jaji Mruma.

Akizungumza kwa niaba ya Jaji Kiongozi ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Uteuzi na Nidhamu ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama, Mhe. Mruma amebainisha kuwa, utekelezaji wa hukumu za madai unategemea kwa kiasi kikubwa utendaji wa Madalali hao, na kwamba bila wao, mnyororo wa utoaji haki unakuwa haujakamilika.

Jaji Mruma amesema, katika miaka ya karibuni, kumeonekana kuwepo kwa changamoto kubwa ya Viongozi wa Kisiasa—hasa wanaotumia nyadhifa zao kama Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama—kuingilia utekelezaji wa amri za Mahakama.

Akieleza jinsi ya kukabiliana na hali hiyo, amewataka Madalali kujiamini na kutumia sheria kuchukua hatua dhidi ya yeyote anayewakwamisha.

"Sheria inawaruhusu kuwachukulia hatua watu wanaoingilia utendaji wenu kwa njia ya dharau kwa Mahakama (contempt of court). Kumzuia Ofisa yeyote wa Mahakama kutekeleza amri halali ni kosa, na tunategemea mchukue hatua za kisheria ili kukomesha hali hii mara moja na kwa mara zote," amesisitiza.

Pamoja na kuwataka Madalali hao kuwa wajasiri, Mhe. Mruma ameeleza kuwa, uhuru wao wa kufanya kazi na ulinzi wa kisheria unaweza tu kulindwa ikiwa wao wenyewe wataonesha uadilifu wa hali ya juu.

Ametaja maeneo yanayolalamikiwa zaidi kuwa ni pamoja na: Ukamataji na Uhifadhi wa Mali ambapo Mali kukamatwa na kutofikishwa kwenye yadi za Madalali, na wakati mwingine kupotea.

Kaimu Jaji Kiongozi huyo ametaja eneo lingine linalolalamikiwa kuwa ni Uuzaji wa Mali chini ya Kiwango: Mali kuuzwa kwa bei isiyo ya soko au isiyozingatia tathmini halisi.

“Ukiukwaji wa Taratibu za Uondoaji, baadhi ya madalali wasio waadilifu kufunga nyumba au kutoa watu nje bila kuwa na amri maalum ya uondoaji badala ya kuweka tu tangazo la zuio la Mahakama,” amesema.

Ameongeza kuwa, ili kuimarisha usalama na hadhi ya Madalali hao, Mahakama inaangalia uwezekano wa Kisheria wa kuwatambua rasmi watendaji hao kama Maofisa kamili wa Mahakama ili wapate ulinzi thabiti wa kisheria wakati wa kutekeleza majukumu yao.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama Tanzania uliofanyika leo tarehe 30 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Baadhi ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama wakimsikiliza Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma (hayupo katika picha) alipokuwa akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama hicho leo tarehe 30 Juni, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)