Na
HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewaapisha Mahakimu Wakazi wapya wawili, Mhe.
Moonlight Martin Tupa na Mhe. Deus Philo Nyimbo na kuwataka Mahakimu hao
kuviishi viapo vyao huku wakizingatia mila na desturi za maeneo wanayofanyia
kazi.
Mhe.
Masaju ameyasema hayo leo tarehe 04 Machi, 2026 mara baada ya zoezi la uapisho wa Mahakimu hao lililofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
“Katiba
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua kiapo au viapo, na kuna viongozi
wanatajwa moja kwa moja kwamba wao kabla ya kuanza majukumu yao watalazimika
kula kiapo na moja ya wanaotajwa katika Katiba hiyo ni Majaji na Mahakimu,
tuliokwisha kula kiapo maneno haya ya kiapo tunayafahamu, wasiwasi wangu ni
kwamba kama tunayatilia maanani,” amesema Jaji Mkuu huku akiwasisitiza Mahakimu
hao kuendeleza tamaduni za maeneo husika.
Akizungumzia
kuhusu uadilifu, Mhe. Masaju amesema kuwa, uadilifu unaanzia kwenye kiapo
ambacho wametumia kuapa hivyo ni vema wakakiheshimu na kukitekeleza kwa
uadilifu ili wasiwe wamelitaja bure Jina la Mwenyezi Mungu na kuwa heshima
haitokani na cheo bali heshima inatokana na huduma.
“Uadilifu
unaanzia kwenye kiapo, juzi nilipoongea na wenzenu niliwaambia tusimchukulie
Mungu poa, Mungu mwenyewe anatamka, anaelekeza kwamba jina lake lisitamkwe
bure. Kwenye hicho kiapo mlipokuwa mnamaliza mmesema Eee Mwenyezi Mungu
nisaidie, uadilifu wenu unaanzia hapa kwenye kiapo kile,” amesisitiza Jaji
Mkuu.
Ameongeza
kwamba, Mahakama ina kiapo ambacho ikiwa watakikiuka watawajibishwa
wasipozingatia kiapo hicho Mungu atawaadhibu mwenyewe hapa duniani au baada ya
kufa ikiwa hawatatubu.
“Kwa
kawaida kiapo kina adhabu na sisi hapa tuna adhabu mbili, moja ukikiuka hicho
kiapo unaweza kushtakiwa kwa kosa la jinai ukawajibishwa, cha pili
unawajibishwa na Mwenyezi Mungu ambaye umeapa kwake na ndiye unayemuomba
akusaidie, na yeye ana namna nyingi ya kuwawajibisha, anaweza akakusubiri
wakati umeshakufa kama hukutubu akakuwajibisha huko huko, lakini mara nyingi
huwa naona wala rushwa na wale wanaokiuka maadili anawawajibisha hapa
hapa duniani kwanza, watambue wajibu wao wamrudie Mwenyezi Mungu” amesema Mhe.
Masaju.
Jaji
Mkuu ameeleza kuwa, kila anayehitaji kuheshimiwa anapaswa kuheshimika pia
kutambua kuwa jamii itamheshimu kwa namna anavyotenda na si kwa nguo anazovaa
na cheo alichonacho, akiongeza kuwa hawahitaji kujitutumua bali wawe
wanyenyekevu na kuwaheshimu watu wengine katika sehemu zao za kazi na jamii
yote kwa ujumla.
Akizungumza
kuhusu kutambua mila na desturi za jamii za Kitanzania, Mhe. Masaju amesema
kwamba, kila Hakimu anapaswa kuzingatia na kuziheshimu mila na desturi kama
ambavyo Katiba inazitambua na kuziheshimu Katiba za Kiislamu, akisisitiza kuwa
Mahakama za mwanzo zinalazimika kukaa na washauri wa Mahakama kwenye mashauri
yanayohisha sheria za kimila au Kiislamu.
“Katiba
inatambua hizi mila na desturi za Tanzania, inatambua viapo, sisi tutatakiwa
kufuata mila na desturi, na ndio maana tuna Mahakama hapa zinatambua hizi mila
na desturi, na Mahakama za Mwanzo mnapokuwa mnatekeleza majukumu yenu katika
yale mashauri yasiyokuwa ya jinai, ni pamoja na kuzingatia hizo mila, desturi
na sheria za Kiislamu,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Ameongeza
kuwa, si lazima mtu kufanya kazi katika sehemu aliyozaliwa na kwamba wapo
watakaoenda kufanya kazi mijini au vijijini hivyo ni lazima wazitambue mila na
desturi za mahali husika, ili waweze kutatua kwa haki migogoro mbalimbali
inayohusu mila na desturi au migogoro katika ndoa za kiislamu kulingana na mila
na desturi husika.
Aidha
Jaji Mkuu ameeleza kwamba, katika kutatua migogoro hiyo pale watakapoona
inafaa, watapaswa kukaa na washauri wa Mahakama ambao watawashauri kwa hekima
katika kuzingatia mila na desturi katika kutoa hukumu huku akishauri Uongozi wa
Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto kujumuisha masuala ya mila na
desturi ili zitambulike na kurahisisha wakati wa utoaji hukumu.
Ametaja
uhumimu wa Washauri wa Mahakama kuwa ni pamoja na kutoa ushauri ili kutoa
hukumu ya haki kwa kuzingatia jamii, kusaidia kutatua migogoro ya kijamii ya
kiislamu katika masuala ya ndoa pamoja na kutoa ushauri wa kimila kulingana na
mazingira, pia kuwashirikisha katika maamuzi pale Mahakama itakapoona kwa
maslahi ya haki inalazimu kufanya huvyo, au pale Mahakama itakapoombwa na mmoja
wapo wa wadaawa katika shauri husika.
Amesema
kuwa ikiwa Wazee wa mila na Machifu
watatungiwa sheria ya kuwatambua, pamoja na wajibu mwingine, wajibu wao
utakuwa ni ule ulioelezwa katika Ibara ya 19(3) na Ibara ya 30(2)(a) akiyataja
majukumu hayo kuwa ni usalama wa jamii, amani katika jamii na umoja wa kitaifa,
kadhalika watasaidia katika utatuzi wa migogoro ya ardhi, masuala ya ndoa,
ulinzi na utunzaji wa mazingira, huku
akitilia mkazo kuwa watu hao ni muhimu katika utatuzi wa migogoro kwa sababu
jamii inayowazunguka inawasikiliza na kuwaheshimu.
Katika
hatua nyingine, Mhe. Masaju ameeleza majukumu ya Serikali za Mitaa ambazo zina
wajibu wa kuhimiza utawala wa sheria katika jamii, amani katika jamii na umoja
wa kitaifa huku akieleza kuwa, Serikali za Mitaa pia zinapaswa kutekeleza
shughuli zake ipasavyo kwa kutumia demokrasia, kuhakikisha utekelezaji wa
sheria na ulinzi wa wananchi akirejea Ibara ya 146(1) pamoja na Ibara ya
146(2)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaeleza wazi
madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa.
Kadhalika,
Jaji Mkuu amesema kuwa, mategemeo ya Mahakama ni ya kwanza kutii kiapo kama
ambavyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan
anasisitiza juu ya kuishi viapo sambamba na kuziheshimu mila na desturi za
Tanzania, huku akiwakumbusha pia kuzingatia mila katika mavazi kwa wanawake
kujistiri kwa heshima na wanaume kuvaa mavazi yenye hadhi na heshima.
Akizungumza
kuhusu uwajibikaji, weledi na uadilifu, Mhe. Masaju amewahimiza kuwajibika
ipasavyo kama ambavyo imeelekezwa katika Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ambayo unahimiza kuhusu uwajibikaji na kuweka wazi kuwa
kila mtu ana wajibu wa kushiriki na kujituma kwa uaminifu katika kazi halali za
uzalishaji mali, kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya
uzalishaji mali ya binafsi na yale ya pamoja yaliyowekwa na sheria.
“Ibara
ya 25 inatukumbusha kuhusu uwajibikaji, Ibara ya 25(1) inasema kwamba kazi
pekee ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii, ndilo chimbuko la ustawi wa
Wananchi na kipimo cha Utu……...”
Ameongeza
kuwa kazi ya kuhukumu waliyopewa sio ya shuruti hivyo wanapaswa kujituma
wenyewe, kuwa na nidhamu ya kazi ili kufikia malengo na kuwa wazembe
watashauriwa ili kubadilika au kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.
“Hii
kazi ya kuhukumu tuliyopewa si ya shuruti, ndio maana tunataka muwajibike
mjitume ninyi wenyewe, muwe na nidhamu ya kazi, mfikie malengo, wale wazembe
tutajaribu kuwashurutisha kwa kuwashauri, lakini ikishindikana watawawajibishwa
kwa kushindwa kutekeleza wajibu wao na tunayo sheria inatuongoza,” amesisitiza
Jaji Mkuu.
Mhe.
Masaju amerejea Ibara ya 25(3)(d)(i)(ii)(iii) na kueleza kuwa, kazi ni majukumu
yoyote ambayo ni sehemu ya majukumu ya kawaida ya kuhakikisha ustawi wa jamii,
ujenzi wa Taifa kwa mujibu wa sheria pamoja na jitihada za kutumia uwezo wa
kila mtu kufanya kazi kwa ajili ya kuimarisha jamii na uchumi wa Taifa na
kuhakikisha maendeleo na tija ya Kitaifa.
Hafla
ya Uapisho huo imehudhuriwa na sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Tanzania pamoja
na Mahakimu Wakazi wengine 90 ambao walikuwa wakiendelea na mafunzo elekezi
baada ya uapisho wao tarehe 23 Februari, 2026.
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Mahakimu Wakazi wapya wawili aliowaapisha leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Katika hafla hiyo pia walikuwepo Mahakama Wakazi wapya 90 wanaoendelea na Mafunzo elekezi baada ya kuapishwa hivi karibuni.
Hakimu
Mkazi Mpya, Mhe. Moonlight Martin Tupa (wa kwanza kulia) akila kiapo cha uadilifu mbele ya Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele) leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wanaoshuhudia wa pili kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya na wa pili kulia ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert.
Mahakimu
Wakazi wapya walioapishwa wakisaini viapo vya uadilifu mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati wa hafla ya
uapisho iliyofanyika leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya
Tanzania jijini Dodoma.
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akisaini viapo vya Mahakimu
Wakazi aliowaapisha leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya
Tanzania jijini Dodoma.
Mahakimu Wakazi wapya waliokuwa wakiendelea na mafunzo elekezi pamoja na walioapishwa wakisikiliza kwa makini hotuba ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju
baada ya zoezi la kuwaapisha Mahakimu wapya wawili leo tarehe 04 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi wapya aliowaapisha leo tarehe 04 Machi, 2026. Kulia ni Mhe. Moonlight Martin Tupa na kushoto ni Mhe. Deus Philo Nyimbo.
Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto (wa kwanza kushoto), Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili
kushoto), Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Massabo (katikati), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma (wa pili
kulia) na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Kuu, Mhe Abdi Kagomba (wa kwanza kulia) wakifuatilia tukio la uapisho wa Mahakimu Wakazi wapya (hawapo katika picha).
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)