Jumatatu, 30 Machi 2026

JAJI MFAWIDHI MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO SINGIDA AWASILI KITUONI

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda leo tarehe 30 Machi, 2026 amewasili mkoani Singida ikiwa ni mara ya kwanza baada ya kupata uteuzi huo hivi karibuni wa kuiongoza Kanda hiyo mpya ya Mahakama Kuu.

Akiwa katika hafla ya ukaribisho wake alipata nafasi ya kusikiliza taarifa fupi ya utekelezaji iliyosomwa na Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Bi. Eva James Leshange. 

Mara baada ya kupokea taarifa hiyo, Mhe. Mwenda amewapongeza Viongozi na watumishi wote wa Mahakama Mkoa wa Singida kwa kazi nzuri wanayoifanya hasa katika usikilizwaji wa mashauri kwani hadi kufikia tarehe 27 Machi, 2026 Mkoa wa Singida haukuwa na shauri la mlundikano.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo amewashukuru watumishi kwa mapokezi mazuri na kuona watumishi wana ari na nguvu ya kufanikisha malengo ya Mpango Mkakati wa Mahakama.

“Nawashukuru sana viongozi na watumishi kwa ujumla kwa mapokezi mazuri na hongereni sana kwa kufanya kazi kwa bidii na ushiriano mkubwa hususan katika usikilizwaji wa mashauri ni kiashiria watu wanafanya kazi kwa ushirikiano,” amesema.

Vilevile amewasisitiza watumishi kuendela kuwa na nidhamu kwani, Mahakama inapokea wateja ambao wameumizwa na wanahitaji msaada hivyo wasaidiwe kuhudumiwa kwa heshima, pia amesisitiza kufanya kazi katika timu pasipo kuangalia vyeo ili kusiwe na mkwamo katika kutekeleza majukumu ya kila siku.

Baada ya kuzungumza na watumishi alipata wasaa wa kwenda kutembelea jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Singida na kufanya ukaguzi wa vyumba vya ofisi na kuona hatua ilipofikiwa.

 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (wa kwanza kushoto) akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida alipowasili ofisini hapo leo tarehe 30 Machi, 2026.

Afisa Utumishi Mwandamizi Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Bi. Eva Leshange akiwasilisha taarifa ya utekelezaji majukumu mbele ya Mhe. Ayoub Mwenda, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda Ya Singida (hayupo katika picha) leo tarehe 30 Machi, 2026 alipowasili katika Mahakama hiyo.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria hafla fupi ya ukaribisho wa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda mpya ya Singida.


Sehemu ya watumishi ajira mpya wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyeketi katikati) . Aliyeketi kushoto ni Naibu Msajili, Mhe. Evodia Kyaruzi na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Singida, Bw. Filbert Matotay. 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akikagua jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Singida.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

MTENDAJI WA MAHAKAMA PWANI AWATAKA WATUMISHI WA KANDA YA DAR ES SALAAM KUITHAMINI MICHEZO

  • Asema michezo ni haki ya msingi kwa ustawi na ufanisi katika utendaji kazi
Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestory Mujunangoma amewataka watumishi wa Mahakama Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani kuifanya michezo kuwa haki kwa kila mtumishi.

Bw. Mujunangoma aliyasema hayo tarehe 28 Machi, 2026 wakati akifungua Bonanza lililofanyika katika viwanja vya Zimamoto Kibaha Mkoa wa Pwani. Bonanza hilo lililoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani ambalo liliwashirikisha watumishi wa Mahakama Mkoa wa Dar es Salaam ambao wanaunda Kanda ya Dar es Salaam.

Alisema kuwa, kushiriki katika michezo ni haki ya kila mtu na kwamba michezo ni furaha, inaleta umoja na mshikamano na ndio maana wako pamoja, hivyo ni amewasisitiza kuongeza bidii kushiriki katika michezo kwakuwa michezo ni haki yao. 

Aidha, akifafanua kauli hiyo alisema kila mtumishi wa Mahakama aione michezo kama haki yake na kwamba ana uhakika kama watashiriki kwa wingi na kwa umoja huo licha ya kuimarisha afya zao, furaha zao na mshikamano wao hata utendaji kazi wao utakuwa na ufanisi zaidi maana wakiwa na michezo akili zitakuwa vizuri.

“Kadhalika umoja utakuwepo mipango itapangika na watakuwa karibu na Viongozi wao na watakachokipanga kitaeleweka na kitafanyiwa kazi kinachotakiwa ni kupata ufanisi wa kazi katika Taasisi,” ameeleza Mtendaji huyo. 

Kadhalika aliwapongeza Viongozi wa Kitaifa wa Mahakama Sports Club kwa kujumuika katika Bonanza hilo na kusema kwamba, uwepo wa Viongozi wa michezo kitaifa inaonesha kuwa shughuli hiyo haitaishia hapo bali itakuwa endelevu.

Alisema pia, kwa Mkoa wa Pwani, imekuwa ni heshima kubwa kwa kufanya bonanza hilo na pia ameomba ushirikiano huo waliouonesha Dar es Salaam na Pwani uendelee.

Amewaomba Uongozi wa Kitaifa kushirikiana na Uongozi wa Pwani na Dar es Salaam kufanya kitu kikubwa zaidi na kitu kitakachofahamika zaidi na kuitangaza Mahakama kwa upana  mkubwa Zaidi. “Sasa tujiandae kutakapokuwa na Bonanza linalofuata  maana yake tuwe na timu nyingine za Taasisi nyingine kwa hiyo lazima tuwe na maandalizi makubwa zaidi,” alisema Bw. Mujunangoma.

Bonanza hilo lilihusisha mchezo wa mpira wa miguu ambapo mpaka dakika zote 90 walitoka kwa sare ya kufungana goli moja kwa moja na walipoenda kwenye matuta Pwani walipata penati sita wakati Dar es Salaam walipata penati saba hivyo Dar es Salaam kupata ushindi kwa upande wa mpira wa miguu.

Kwa upande wa Mpira wa Pete Pwani waliibuka kidedea kwa kuwafunga Dar es Salaam magoli 10 kwa nane, wakati mchezo wa kuvutana kwa kwamba wanaume na wanawake Dar es salaam waliibuka kidedea.

Mchezo wa riadha kwa wanaume Dar es Salaam wameibuka kidedea wakati upande wa wanawake Pwani wameibuka kidedea na mchezo wa kufukuza kuku wanawake na wanaume Dar es Salaam wamefanikiwa kuchukua kuku wote wawili.


Mgeni rasmi Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestor Mjunangoma  (aliyesimama) akizungumza wakati wa ufunguzi wa Bonanza tarehe 28 Machi, 2026 katika viwanja vya Zimamoto Kibaha Mkoa wa Pwani. Kulia ni Mwenyekiti wa Mahakama Sports Club, Mhe. Martin Mushi na kushoto ni Naibu Katibu, Mahakama Sports Club, Bi. Eva Mapunda.

 Mgeni rasmi Mtendaji wa Mahakama Pwani,  Bw. Nestory Mujunangoma  akikagua kikosi cha Mpira wa Miguu cha Pwani. Kushoto ni Nahodha wa Kikosi hicho ni Bw. Isihaka Mgude.

Mgeni rasmi Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestory Mujunangoma (mwenye kofia)  akikagua kikosi cha Mpira wa Miguu cha Dar es Salaam. Kulia kwake ni Nahodha wa Kikosi hicho, Abdi Sasamalo.

Washindi wa kukimbiza kuku, kulia ni Stanley Sirikwa na kushoto ni Bi. Patricia Patrick.

 Kikosi cha Kamba Wanaume Dar es Salaam wakijiandaa na pambano.

Vikosi vya Kamba Wanawake Pwani na Dar es Salaam wakisikiliza maelekezo kabla ya pambano.

Matukio katika picha Bonanza la Michezo lililoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

WATUMISHI WANAWAKE WA MAHAKAMA KANDA GEITA WAFANYA MATENDO YA HURUMA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama Kuu, Geita

Wanawake wa Mahakama Kanda ya Geita kutoka Mahakama Kuu Geita, Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mahakama ya Wilaya ya Geita na Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, tarehe 28 Machi  2026 walitembelea Wodi ya Wajawazito na Wazazi katika Kituo cha Afya Kasamwa.

Lengo la ziara hiyo ni kufanya matendo ya huruma ikiwa ni utaratibu waliojiwekea kila mwaka wanapoadhimisha kilele cha Siku ya Wanawake Duniani.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kasamwa, Dkt. Emmanuel Zillagera, pamoja na Watumishi wengine wa Kituo hicho waliwaongoza Wanawake wa Mahakama katika wodi hizo na kutoa zawadi mbalimbali.

Watumishi hao wa Mahakama walitoa vifaa na mahitaji kwa Wajawazito na Wazazi ambavyo ni sukari, sabuni za unga, mafuta ya kujipaka, pampers na vingine.

Akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo, Dkt. Zillagera aliwashukuru Wanawake wa Mahakama kwa matendo ya huruma waliyotoa. Pia aliwaomba kurudi kipindi kingine kwa ajili ya hiyo mara watakapopata nafasi.

Naye Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, aliwashukuru Viongozi pamoja na Watumishi wa Kituo hicho kwa kuwakubalia kufika na kufanya matendo ya huruma.

"Kila mwaka Wanawake wa Kanda ya Geita wanapokuwa wanaelekea kilele cha Siku ya Wanawake Duniani, hufanya matendo ya huruma kwa kupeleka vifaa ambavyo ni mahitaji mbalimbali. Kitendo hiki ni sadaka yetu kama Wanawake kwa Wazazi pamoja na Wajawazito,” alisema.

Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Masalu Kisasila, akikabidhi sabuni, pampers na vitu vingine kwa Muuguzi Mkunga Sr. Joyce wa Kituo cha Afya Kasamwa.

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufika katika Kituo cha Afya Kasamwa.

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Kituo cha Afya Kasamwa (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

NAIBU WASAJILI NA MAHAKIMU WAKAZI WANOLEWA MBINU ZA USULUHISHI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) imeendesha mafunzo maalum ya Usihi na Usuluhishi kwa Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi toka katika Mahakama mbalimbali za mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Iringa, Njombe, Sumbawanga, Songwe, Songea na Katavi.

Mafunzo hayo ya siku tatu yalianza tarehe 24 Machi, 2026 hadi tarehe 26 Machi 2026 katika ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya yakiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ambaye pia ni alikuwa mwezeshaji akishirikiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raymond Kaswaga pamoja na Mhe. Gloria Shuma kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA).

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo Mhe. Tiganga alitoa shukrani zake za dhati kwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi Dar Es Salaam, Mhe. Zahara Maruma kwa kuandaa na kuratibu Mafunzo hayo. Vilevile, aliwaasa washiriki kuwa chachu ya mabadiliko katika kutatua migogoro mingi kwa njia ya usuluhishi.

“Kwa mafunzo haya mliyoyapata mkawe sababu ya mabadiliko katika kutatua migogoro mingi kwa njia ya usuluhishi na kuwa walimu wazuri kwa kuwapa wengine kile mlichojifunza kwa ambao hawakupata bahati ya kuwa sehemu ya mafunzo haya. Natamani mashauri mengi katika masjala zetu yaishe kwa njia ya Usuluhishi” alisema Mhe. Tiganga.’’ alisema Mhe. Tiganga.

Mafunzo hayo yanaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na Mpango Mkakati wa Mahakama unaosisitiza umuhimu wa kutumia njia mbadala ya utatuzi wa migogoro (usuluhishi) ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Na pia ni utekelezaji wa Ibara ya 107 A (2) (d) ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977. Mafunzo hayo yalilenga pia maandalizi ya Wiki ya Usulujishi itakayozinduliwa tarehe 9 Aprili 2026 katika Ukumbi wa Golden Jubilee PSSSF Tower Dar Es Salaam na kufuatiwa na Wiki ya Usuluhishi itakayofanyika Nchi nzima kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba alitoa shukurani kwa waandaaji na wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa kufanikisha mafunzo hayo na kuahidi kuwa watayafanyia kazi yale waliyofundishwa na watakuwa walimu wazuri kwa wengine ambao hawakupata bahati ya kuwa sehemu ya mafunzo hayo.

Sehemu ya mada zilizofundishwa ni pamoja na dhana ya Usuluhishi, sheria na kanuni za usuluhishi, mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa usuluhishi, nafasi ya sheria na mawakili katika usuluhishi, vikwazo na changamoto katika usuluhishi na pia mafunzo hayo yaliambatana na mazoezi ya vitendo (Practical sessions) yaliyowasaidia washiriki kuelewa kwa kina namna ya kuendesha vikao vya usuluhishi kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Mbeya wakiwa Meza Kuu wakati wa kufunga mafunzo ya Usuluhishi Nyanda za Juu Kusini katikati ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto) na Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (kulia)

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akikabidhiwa cheti na Jaji Mfawidhi Mahakama kuu kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga kwa kuwa sehemu ya mafunzo hayo.

Mhe. Raimond Kaswaga akikabidhiwa cheti na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga kwa kuwa sehemu ya wawezeshaji katika mafunzo hayo.

Washiriki katika mafunzo hayo wakiwa katika mazoezi ya vitendo (Practical session) ya namna ya kuendesha vikao vya usuluhishi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akikabidhiwa cheti na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Songea Mhe. Elizabeth Nyembele kwa kuwa sehemu ya wawezeshaji katika mafunzo hayo.

Mwezeshaji katika mafunzo hayo ambaye ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, akimwaga madini wakati wa mafunzo hayo.

Mwezeshaji katika mafunzo hayo ambaye ni Hakimu mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raimond Kaswaga akifundisha wakati wa mafunzo hayo

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba akitoa neno la shukurani kwa waandaaji na wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa niaba ya washiriki wa mafunzo.

Mhe. Gloria Shuma kutoka Chuo Cha Uongozi wa mahakama (IJA) akitoa neno la shukurani katika Ufungaji wa mafunzo hayo





MENEJIMENTI YA MAHAKAMA SONGEA YAFANYA KIKAO CHA ROBO YA TATU YA MWAKA

Na NOEL SYLIVESTER – Mahakama, Songea

Menejimenti ya Mahakama, Kanda ya Songea, tarehe 26 Machi 2026 ilifanya kikao cha tathmini ya utendaji kazi kwa kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026.

Kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa  Saint Vicent, wilayani Nyasa na kilifunguliwa rasmi na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha, ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa kikao hicho.

Katika kikao hicho, taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama kwa kipindi cha Januari hadi Machi, 2026 iliwasilishwa na Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Songea, Bw. Allan Mwela, ambaye alihudumu pia kama Katibu wa kikao.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Bw. Mwela alieleza masuala mbalimbali ikiwemo utawala bora, uwajibikaji pamoja na usimamizi wa rasilimali. Aligusia pia nguzo ya kwanza inayohusu utawala na usimamizi wa uendeshaji wa shughuli za Mahakama.

Naye Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya  Songea, Mhe. Lilian Rugalabamu, aliwasilisha taarifa inayohusu utoaji wa haki kwa wakati ambayo iligusia masuala ya usimamizi wa mashauri na usimamizi wa mashauri kwa njia ya mtandao (VC).

Kwa upande mwingine, Afisa Rasilimaliwatu wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Bi. Paulina Kapinga, aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama kwa kipindi cha Januari hadi Machi, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha.

Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Lilian Rugalabamu.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Songea, Bw. Allan Mwela.

Afisa rasilimaliwatu, Bi.Paulina Kapinga (aliyesimama).

Habari hii imehaririwa na FAUSTNE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


 

 

 

 

 

 

 

 

WADAU WA HAKI JINAI KIBAHA WAPEANA KAZI YA KUFANYA UTAFITI SHERIA YA USHAHIDI WA KIELEKRONIKI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Wadau wa Haki Jinai wa Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani wamepeana jukumu la kufanya utafiti kuhusu Sheria ya Ushahidi ya Kieletroniki kwa Mahakama za Mwanzo kwakuwa kumekua na sintofahamu wakati mashauri yenye ushahidi wa kielekroniki yanapofikishwa katika Mahakama za Mwanzo kujua kama sheria imekataza ama iko kimya.

Hayo yaliazimiwa katika kikao cha kusukuma mashauri cha Mahakama ya Wilaya Kibaha kilichofanyika tarehe 28 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa wazi wa Mahakama hiyo.

Wadau hao wamekuwa na sintofahamu wakati mashauri yenye ushahidi wa kielekroniki yanapofikishwa katika Mahakama za Mwanzo na kupitia maamuzi ya mashauri mbalimbali wamegundua kuwa, sheria haijakataza Mahakama za Mwanzo kutopokea mashauri yenye ushahidi wa kielekroniki, na ndipo kufikia maazimio kwamba kila mdau afanye utafiti kusoma sheria na kuitafsiri vizuri na pia kupitia mashauri yaliyoamriwa na Mahakama za juu kuhusiana na sheria hiyo.

Akizungumza wakati wa majadiliano hayo, Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Fredrick Shayo alisema Sheria ya Ushahidi wa Kielektroniki imetokana na shauri ambalo Jaji Massam alizungumzia wakati wa uamuzi wa shauri la rufaa kutoka Mahakama ya Mwanzo yenye ubishani kuhusu Ushahidi wa Kielekroniki rufaa namba 3076 ya mwaka 2025 kati ya Hussein Haji Miraji na Isack Elias Kiganga katika Mahakama Kuu masjala ndogo ya Shinyanga.

Mhe. Massam alisema, “hata hivyo hakuna kifungu katika Sheria ya Ushahidi ya Kielekroniki au Tangazo la Serikali na. 22/1964 inakataza ushahidi wa kielekroniki Mahakama za Mwanzo.”

Katika kikao hicho hoja mbalimbali zilijadiliwa lengo likiwa ni kupata namna bora ya kumaliza mashauri pasipo kuwa na mashauri ya mlundikano. 

Akitoa mchango wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Amos Sura alisema kuwa, ni bora mashauri yakasikilizwa siku moja ili kuepuka kubaki na majalada ya washtakiwa walioruka dhamana kwa kuzingatia mwongozo wa Jaji Mkuu wa kuzuia Mahabusu wa Mahakama za Mwanzo.

Akijibu lalamiko la Mawakili kuchelewesha mashauri kwa kigezo cha kuwa na mashauri Mahakama za juu Wakili Sura amemuomba Hakimu Mkazi Mfawidhi Kibaha na Mahakimu wengine wa Wilaya kutumia Mahakama Mtandao (Virtual Court) ili kuepuka kuchelewesha mashauri na Mawakili ambao wamekuwa wakitumia kisingizio cha kuwa na mashauri Mahakama za juu.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai alisema anatamani ifike kipindi katika vikao hivyo wafike na kupongeza tu, kwakuwa hakuna shida katika usikilizaji mashauri.

Mhe. Lukumai amewataka upande wa Polisi kuwa, wakati wanapopeleka mashauri ya Mahakama za Mwanzo wanatakiwa wawe na uhakika kuwa mlalamikaji yupo na siku hiyo hiyo shauri lisikilizwe kwakuwa mashauri ya Mahakama za Mwanzo hayana ufundi hivyo yanaweza kusikilizwa na kumalizika siku hiyo na kusema kuwa, hatua hiyo litaepuka washtakiwa kuruka dhamana.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha ambaye ni Mwenyekiti wa Kikao cha Kusukuma Mashauri Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai (kulia) akiwa na Wakili wa Serikali Said Seif  Katibu wa kikao hicho  kwa pamoja wakiongoza Kikao cha Kusukuma Mashauri kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama ya Wazi uliopo katika Mahakama hiyo.

 Baadhi ya Wajumbe wa Kikao cha Kusukuma Mashauri cha Mahakama ya Wilaya Kibaha wakiwa katika kikao hicho.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

KATAVI YAJIONDOA RASMI KUTOKA MAHAKAMA KUU KANDA YA SUMBAWANGA

Na. Ally Ramadhani – Mahakama, Katavi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda tarehe 27 Machi, 2026 alikabidhi rasmi eneo jipya la kiutawala la masjala ndogo ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi kwa Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo Mhe. Godfrey Ntemi Isaya, katika hafla iliyofanyika katika Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi.

Aidha, Mhe. Manyanda alifanikiwa kutembelea jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi na kufanya ukaguzi wa vifaa vya ofisi kisha kufanya makabidhiano kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya.

Baada ukaguzi huo Mhe. Manyanda alifanya kikao cha kuagana na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Katavi na kuwashukuru kwa ushiriakiano alioupata kutoka kwao na kuahidi kuwa ataendelea kutoa ushirikiano wakati wote atakapo hitajika. Vilevile, aliwakumbusha umuhimu wa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Kabla ya mwaka 2005, wakazi wa Sumbawanga na Katavi walikua wanapata Huduma za Mahakama Kuu kutoka Kanda ya Mbeya ila mwaka 2005 nasi tukapata Huduma za Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga na leo hii mwaka 2026 nina furaha kubwa sana kuwa kwenye historia ya tukio hili la kukabidhi eneo jipya la kiutawala la Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Katavi,” alisema Mhe. Manyanda.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya, aliwasisitiza watumishi kuhusu suala la nidhamu, kuthaminiana, upendo, ulinzi wa miundombinu, vitendea kazi wa vya Ofisi na utendaji wa kazi mzuri kwa watumishi wote ili kuwezesha kutoa huduma bora ya haki kwa wananchi.

Vilevile, Mhe. Isaya ameupongeza Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha mazingira ya utoaji haki kwa kusogeza huduma za utoaji haki kwa wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri.

Kufuatia makabidhiano hayo, Mhe. Manyanda aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Pamela S. Mazengo pamoja na Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Bi. Irene Mlangwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda (Katikati) akimkabidhi Hati ya makabidhiano Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (kushoto) kuashiria shughuli rasmi za Mahakama Kuu, Kanda ya Katavi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (wa kwanza kushoto) akionesha hati ya makabidhiano.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Thadeo M. Mwenempazi (wa Kwanza Kushoto) akikabidhi zawadi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Mhe Fredrick Kapela Manyanda (wa Kwanza Kulia), iliyo andaliwa na Uongoz wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda akionesha tuzo (Troph) aliyozawadia na Uongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Katavi kupitia Mhe Thadeo M.  Mwenempazi Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Sumbawanga.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Pamela S. Mazengo akilishwa keki na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya.


Uongozi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo Kanda ya Katavi ilipotembelea  jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji haki Kanda Katavi 






JAJI NDUNGURU AIKABIDHI KANDA YA NJOMBE KWA JAJI VICTORIA NONGWA

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji mfawidhi wa mahakama kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru amekabidhi ofisi ya Mahakama Kuu Kanda mpya ya Njombe kwa Jaji Victoria Mlonganile Nongwa ambaye ameteuliwa kuwa Jaji Mfawidhi.

Makabidhiano ya Masjala ndogo ya Mahakama Kuu Njombe  ambayo itaanza kutoa huduma zake rasmi kuanzia tarehe 30 Machi, 2026 yalifanyika Ijumaa tarehe 27 Machi, 2026 mbele ya watumishi wote  w Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe na Wilaya nne (4) ambazo ni Ludewa, Wanging’ombe, Makete pamoja na Makambako.                                                                                                     

Aidha akiwa katika kikao cha makabidhiano, Mhe. Ndunguru  alimpongeza Mhe. Jaji Nongwa kwa kuteuliwa kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe huku akishukuru kwa kupunguziwa majukumu ya mashauri ya rufaa ambazo zilikuwa zikitokea Njombe kwenda Mahakama Kuu Iringa.

Pamoja na hayo alizungumza na watumishi wote wa Mahakama za Mkoa wa Njombe kupitia mfumo wa mkutano mtandao (Video Conference) kwa ambao hawakuweza kufika katika kikao hicho cha makabidhiano hayo.

Kadhalika, Jaji Ndunguru alitoa pongezi kwa watumishi wote hususani kwa ushirikiano mkubwa  waliompa kwa kipindi chote alichokuwa akihudumu kwa Mahakama zote za Mkoa wa Njombe na Wilaya zake na kuwaomba ushirikiano waliompa yeye kwa kipindi chote wampe pia na Jaji Nongwa ambaye ameteuliwa kuwa Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Mlonganile Nongwa alimpongeza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa pamoja na kuwashukuru watumishi wote wa Mahakama za Mkoa wa Njombe kwa kumpa ushirikiano Jaji Ndunguru ambaye amehudumu kwa kipindi chote ambacho amekuwa akisimamia Mahakama za Mkoa wa Njombe ambaye kwa sasa atahudumu Mahakama Kuu Kanda ya Iringa pekee.

 Aidha, Mhe. Nongwa aliwasisitiza na kuwaomba watumishi wote wa Mahakama mkoani Njombe kumpa ushirikiano pamoja na kusisitiza watumishi watumie mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuachana na matumizi ya peni na karatasi katika utendaji kazi pamoja na kuwahudumia wananchi vizuri hasa makundi maalum mfano walemavu na akina mama wajawazito.

Tukio la makabidhiano ya Kituo cha Mahakama Kuu Njombe lilihudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama pamoja na Afisa Bajeti wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe na Wilaya zake, Bw. Juma Nyenzi.

Aidha, Viongozi hao walitoa neno la shukrani kwa pamoja wakati wa makabidhiano hayo mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa.

Awali Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe pamoja na Wilaya zake zote zilikuwa chini ya Mahakama Kuu Kanda ya Iringa. Mahakama inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za uboreshaji huduma ikiwemo ujenzi wa majengo ya Mahakama ili kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania  kanda ya Iringa,  Mhe. Dunstan Ndunguru (kushoto) akikabidhi kitabu cha makabidhiano ya Mahakama Kuu Masjala ndogo mpya ya Iringa kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe Mhe. Victoria Mlonganile Nongwa.

 Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania  Kanda ya Iringa,  Mhe. Dunstan Ndunguru akisaini kitabu cha wageni wakati  alipofika Mahakama ya  Hakimu Mkazi Njombe kabla ya makabidhiano  ya Kituo cha Masjala ndogo ya Mahakama Kuu Njombe.

 Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania  Kanda mpya ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa akisaini kitabu cha wageni  alipofika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe.

Kutoka  kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, katikati ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa na  anayefuata upande wa kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku wakiwa kwenye kikao cha makabidhiano ya Mahakama Kuu Kanda mpya ya Njombe.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda mpya ya Njombe,  Bw. Richard Mbambe akisoma taarifa pamoja na ratiba ya kikao hicho pamoja na  kuwakaribisha Majaji Wafawidhi mkoani Njombe.

 Watumishi wa Mahakama ya  Hakimu Mkazi  Njombe pamoja na Wilaya zake wakifuatilia kilichokuwa kinajiri kwenye kikao cha pamoja cha  makabidhiano ya Kituo cha Mahakama Kuu Kanda ya Njombe.

Meza Kuu ikiongozwa na 
Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania  Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu pamoja na watumishi wa kada mbalimbali baada ya kumalizika kikao cha makabidhiano ya Kituo cha Mahakama Kuu Kanda ya Njombe. Wa tatu kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe,  Mhe. Victoria Nongwa, wa tatu kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku, wa pili kulia ni  Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama, wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Mhe. Joseph Luambano, wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)