Jumapili, 21 Juni 2026

WATUMISHI WA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA ARDHI WAPATIWA MAFUNZO

Na DHILLON UISSO-Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Dar es Salaam

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, hivi karibuni walipatiwa mafunzo ili kuwakumbusha kuhusu mambo mbalimbali, ikiwemo maadili ya utumishi wa umma.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoanza tarehe 18 Juni, 2026, yalijikita pia kuwakumbusha Watumishi hao kuhusu uwekezaj, afya ya kansa ya mlango wa kizazi, uelewa wa mifuko ya jamii na bima ya afya.

Akifungua mafunzo hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda, aliwashukuru walioandaa mafunzo hayo na kusema mafunzo hayo ni muhimu kwa Watumishi.

Mhe. Luvanda alisema kuwa fursa hiyo siyo tu kufundishana, bali pia ni jambo la kukumbushana kwakuwa mambo hayo yana zungumzwa mara kwa mara. Pia alizishukuru Taasisi zilizofadhili na kutoa mada  katika mafunzo hayo.

Maada ya maadili ilwasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Eliamani Laltaika, ambapo alisisitiza umuhimu wa maadili kwa Watumishi wa Umma katika kutenda haki kwa Wadau na Wadaawa wa Mahakama kwa ujumla.

Katika kuelezea suala la maadili, Watumishi walipata fursa ya kujifunza maana ya maadili, matawi na umuhimu wa maadili katika utumishi wa umma. Mhe. Dkt. Laltaika pia alifundisha mambo muhimu ya kuzingatia ili kutokuvunja maadili kwa Watumishi wa umma kwa maongezi, vitendo, mavazi na utendaji wa kazi kwa ujumla.

Katika mafunzo hayo, Watumishi pia walipata mafunzo juu ya umuhimu wa kupima afya zao mara kwa mara, hususani kupima saratani ya mlango wa kizazi kwa wanawake.

Mafunzo hayo pia yalihusisha maafisa kutoka UTT, PSSSF na NHIF, ambao kwa ujumla wao walielezea muhimu wa uwekezaji, fao la uzeeni na bima ya afya kwa Watumishi.

Mafunzo hayo yalihitimishwa na Kaimu Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Mohamed Gwae, ambaye aliwashukuru waandaaji kwa kufanikisha mafunzo hayo.

Alieleza kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwakuwa yanajenga mahusiano bora katika kazi. Mhe. Gwae aliwataka Watumishi kuzingatia maadili ya utumishi wa umma kama walivyo fundishwa.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda, (wa pili kushoto), wengine ni Majaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Dkt. Thedora Mwenegoha, Mhe. Dkt. Eliamani Laltaika na Mhe. Monica Otaru.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Eliamani Laltaika, akiwasilisha mada kuhusu maadili kwa utumishi wa umma.

 Watumishi wa Mahakama (juu na chini) wakiwa kwenye mafunzo hayo.

 

Picha za pamoja baada ya kuhitimishwa mafunzo hayo. Katikati waliokaa ni Kaimu Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Mohamed Gwae.

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Songea.

JAJI MFAWIDHI MPYA MUSOMA AKABIDHIWA OFISI

Na KANDANA LUCAS-Mahakama Kuu, Musoma

Makabidhiano ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Musoma, yamefanyika hivi karibuni, kufuatia uhamisho wa mtangulizi wake, Mhe. Fahamu Mtulya kwenda Mahakama Kuu Mbeya.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mhe. Mtulya aliwashukuru Watumishi wa Mahakama Musoma kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi cha utumishi wake.  Alisema mafanikio yaliyopatikana yametokana na ushirikiano mzuri kati ya Viongozi na Watumishi, kujituma na uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao.

Aidha, Mhe. Mtulya aliwaasa Watumishi kuendeleza kudumisha mshikamano na kumpatia ushirikiano Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Edwin Kakolaki, ili kuhakikisha huduma za kimahakama zinaendelea kutolewa kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Mhe. Kakolaki aliahidi kuendeleza mazuri yaliyoanzishwa na mtangulizi wake pamoja na kushirikiana na Watumishi wote katika shughuli za utoaji haki kwa Wananchi.

Vilevile Mhe, Jaji Mfawidhi mpya aliwahimiza Viongozi wote na Watumishi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu, weledi na kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma.

Makabidhiano hayo yalihusisha taarifa za utendaji kazi, hali ya mashauri, vifaa vya kazi pamoja na mikakati mbalimbali inayotekelezwa na Mahakama Musoma.

 

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya Pamoja na Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Edwini Kakolaki, wakipeana taarifa ya makabidhiano ya ofisi. Waliosimama nyuma ni Majaji wa Mahakama Kuu, Naibu Wasajili na Mtendaji wa Mahakama Musoma.

Majaji Wafawidhi wakisaini hati ya makabidhiano ya Ofisi ambapo upande wa kushoto ni Mhe. Fahamu Mtulya, kulia ni Mhe. Edwin Kalokola. Waliosimama kutoka kulia ni Majaji wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Marlin Komba na Mhe. Kamazima Idd na Naibu Msajili, Mhe. Omari Kingwele, ambao wanashuhudia utiaji wa saini katika hati ya makabidhiano.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki, akisalimiana na Watumishi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma baada ya kuwasili kushiriki makabidhiano ya ofisi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Songea.

JAJI MFAWIDHI MPYA DODOMA ATAMBULISHWA KWA MKUU WA MKOA

Na ARAPHA RUSHEKE- Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, tarehe 19 Juni 2026, alimtembelea Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, kwa ajili ya kutambulisha.

Ziara hiyo imefanyika ikiwa ni siku moja tu tangu Mhe. Tiganga aliporipoti rasmi katika kituo chake kipya cha kazi baada ya kuhamishwa kutoka Mahakama Kuu Mbeya.

Katika ziara hiyo, Mhe. Tiganga aliambatana na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Masabo. Mhe. Dkt.Masabo akitumia fursa hiyo kumuaga Mkuu wa Mkoa.

Pande hizo mbili zilijadiliana masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya Mahakama na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa katika kuhakikisha huduma za haki zinaendelea kutolewa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Wananchi.

Mkuu Mkoa alimkaribisha Mhe. Tiganga na kumtakia mafanikio mema katika majukumu yake mapya, huku akiahidi kuendeleza ushirikiano uliopo kati ya Taasisi hizo muhimu.


Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt Juliana Masabo, akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.


 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.


 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe, Rosemary Senyamule (aliyepo katikati) akizungumza na wageni kutoka Mahakama ya Tanzania mara baada ya kuwasili katika Ofisi yake Jijini Dodoma.


 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe, Rosemary Senyamule (aliyepo katikati)akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi kutoka Mahakama mara baada ya kumtembelea ofisini kwake. Kulia kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt Juliana Masabo na aliyepo kulia kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma Mhe Joachim Tiganga.

 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe, Rosemary Senyamule (aliyesimama katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi kutoka Mahakama pamoja na Watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, wa tatu kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Masabo na wa tano kutoka kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, wa sita kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe/ Upendo Ngitiri na wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma Bw. Bedson Mariba.

 

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Songea.

JAJI KIONGOZI ZIARANI MKOANI RUVUMA

  • Kukagua Mahakama, Magereza
  • Kuteta na Mkuu wa Mkoa, kuzungumza na Watumishi

Na FAUSTINE KAPAMA na Noel Daud-Mahakama, Songea

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewasili mkoani Ruvuma leo tarehe 21 Juni, 2026, kufanya ziara ya kimahakama ya siku tano, kukagua Mahakama na Magereza.

Mhe. Dkt. Siyani amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Songea majira ya saa 5.00 asubuhi akiwa ameambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, na kupokelewa na Viongozi wa Mahakama.

Viongozi waliokuwa Uwanja wa Ndege kumpokea Jaji Kiongozi ni Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Dkt. Emmanuel Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Songea, Mhe. Lilian Rugarabamu, Mahakimu na Watumishi wengine wa Mahakama Songea.

Ratiba iliyotolewa mjini hapa inaonesha kuwa JaJi Kiongozi ataanza ziara yake kwa kutembelea Mahakama ya Wilaya Nyasa na kufanya kikao na Watumishi, kabla ya kuelekea Wilaya ya Mbinga na kuongea na Watumishi na kukagua Gereza la Wilaya ya Mbinga.

Kesho yake, kwa mujibu wa ratiba hiyo, Mhe. Dkt. Siyani ataelekea kwenye Gereza la Mkwaya kufanya ukaguzi na baadaye kugagua Gereza lingine la Kitai, yote yakiwa katika Wilaya ya Mbinga.

Siku ya tatu, Jaji Kiongozi atamtembelea Mkuu wa Mkoa, Mhe. Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, na kufanya naye mazungumzo mafupi na baadaye kufanya ukaguzi katika Gereza Kuu Songea.

Siku hiyo hiyo, Mhe. Dkt. Siyani atatembelea Mahakama Kuu Songea na kufanya mazungumzo mafupi na Jaji Mfawidhi na kisha kuongea na Watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama ya Wilaya pamoja na Mahakama zote za Mwanzo Songea mjini.

Siku ya nne, Jaji Kiongozi atatemebelea Mahakama ya Wilaya Namtumbo na kuzungumza na Watumishi na kisha kuelekea Wilaya ya Tunduru kufanya ukaguzi kwenye Gereza la Tundura, kabla ya kufanya kikao na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tunduru na Mahakama za Mwanzo katika Wilaya hiyo.

Siku ya tano, Mhe. Dkt. Siyani atafanya kikao cha majumuisho ya ziara katika Mahakama ya Wilaya Tunduru, kikihusisha Watumishi wote kutoka maeneo tofauti mkoani Ruvuma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisalimiana na Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Dkt. Emmanuel Kawishe, baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege Songea kuanza ziara ya kimahakama mkoani Ruvuma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisalimiana na Meja Jenerali wa Jeshi la Wananchi Tanzania, Kamanda Brigedi ya Kusini, Charles Feruzi, walipokutana uwanjani hapo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisamiana na Naibu Msajili, Mhe. Asha Waziri.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisalimiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Songea, Mhe. Lilian Rugarabamu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha akisalimiana na Viongozi mbalimbali wa Mahakama kwenye Uwanja wa Ndege Songea.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, akisalimiana na Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisaini kitabu cha wageni kwenye Chumba cha Wageni Mashuhuri kwenye Uwanja wa Ndege Songea. Picha chini akiwa kwenye mapumziko uwanjani hapo.


Picha na Noel Daud-Mahaama, Songea.

 

CHAMA CHA MAHAKIMU NA MAJAJI TAWI LA KILIMANJARO WAKUTANA

  • Wafanya Mafunzo na Kikao Kazi
  •       Jaji Mongela asisitiza utaratibu wa mafunzo ya mara kwa mara

Na JAMES KAPELE, Mahakama-Moshi

Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Kilimanjaro kimefanya kikao kazi cha robo ya kwanza tarehe 19 Juni 2026 kilichoongozwa na Mwenyekiti wa Tawi hilo Mhe,  Elibahati Petro kwa kujumuisha wanachama kutoka katika Wilaya zote za Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Moshi kwa kufanya mafunzo na kikao kwa lengo la kujijengea uwezo katika masuala ya kisheria na kubuni mikakati mbalimbali ya kimaendeleo katika Tawi hilo.

Awali akifungua mafunzo hayo, Mlezi wa Tawi hilo ambaye pia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Moshi,  Mhe. Dkt. Lillian Mongella aliwapongeza Wanachama na Viongozi wa Tawi hilo kwa kazi kubwa wanayofanya ya kujitolea kulijenga Tawi lao na kuwa na utaratibu wa kukutana kufanya mafunzo ya kujijengea uwezo katika majukumu ya utoaji haki.

“Nawapongeza sana Viongozi wetu wa Tawi pamoja na Wanachama wote kwa umoja wenu, Tawi hili ni letu mambo tunayopanga lazima tuyatekeleze kwa pamoja, tukifanya hivyo Tawi letu litazidi kuwa imara zaidi. Mmefanya vizuri sana kufanya kufanya kikao kwa kuanza na mafunzo nitafurahi kama mtajenga utaratibu wa kukutana mara kwa mara kujijengea uwezo katika masuala mbalimbali ya kisheria,” alisema Jaji Mongella.

Kikao hicho kilitanguliwa na  Mafunzo yaliyohusishwa mada mbalimbali ikiwemo utoaji wa adhabu mbadala katika mashauri ya jinai, utekelezaji wa amri za Mahakama katika mashauri ya madai pamoja na namna bora ya kupokea ushahidi wa kielektroniki katika Mahakama za Mwanzo.  

Akifunga kikao hicho, Jaji wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Moshi, Mhe. Adrian Kilimi aliwapongeza Wanachama na Watoa Mada kwa kushiriki kikao hicho na kufanya mafunzo ya kujijengea uwezo.

Mhe. Kilimi aliwasisitiza Washiriki kujenga utamaduni wa kufanya hivyo mara kwa mara kwa kuwa, jambo hilo linawajenga katika shughuli zao kila siku pamoja na kupata muda wa kujumuika pamoja.

Alitoa rai kwa Wanachama kupenda kushiriki katika michezo mbalimbali ili kuimarisha afya zao pamoja na kujenga utaratibu wa kujumuika pamoja kwa lengo la kuongeza ufanisi katika majukumu yao ya kila siku. 

Mafunzo na kikao hicho vilihitimishwa kwa tafrija fupi ya kuwapongeza Waheshimiwa Ally Mkama na Jasmin Athuman ambao wameteuliwa hivi karibuni kuwa Naibu Wasajili.

 


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Moshi na Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Kilimanjaro, Mhe.Dkt. Lillian Mongella  (aliyesimama) akifungua mafunzo na kikao hicho kilichofanyika tarehe 19 Juni, 2026. 


Picha ya pamoja ya Wanachama wa Tawi la Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Kilimanjaro.

Katika picha ni sehemu ya washiriki wakiendelea na majadiliano katika mafunzo hayo. Aliyesimama ni Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Kilimanjaro, Mhe. Elibahati Petro akichangia hoja katika kikao hicho.

Wakili wa Kujitegemea Desderius Hekwe aliyealikwa kutoa mafunzo kuhusu Ushahidi wa Kielektroniki katika mafunzo hayo.

Aliyeketi kulia ni Mhe. Aden Kanje, Hakimu Mkazi aliyewasilisha Mada ya Matumizi ya Adhabu Mbadala katika mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Moshi, Mhe. Adrian Kilimi  (aliyesimama) akifunga kikao hicho.


 (Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 

 

 

 

 

'MAENDELEO YA TEKNOLOJIA YAMEWEZESHA SHUGHULI NYINGI ZA KIJAMII, KIUCHUMI NA KISHERIA'

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Lumuli Mbuya amesema maendeleo ya Teknolojia yamesababisha shughuli  nyingi za kijamii, kiuchumi na kisheria kufanyika kwa njia kielektroniki.

Mhe. Mbuya aliyasema hayo tarehe 19 Juni, 2026 alipokuwa akitoa mafunzo ya Namna ya Kupokea Ushahidi wa kielekroniki kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya Ilala na Mahakama za Mwanzo za Wilaya hiyo.

Mhe. Mbuya, alisema  mawasiliano ya WhatsApp, sms, baruapepe (email), mitandao ya kijamii, miamala ya fedha kwa simu, picha za kidijitali, video na sauti za kurekodiwa sasa ni sehemu ya maisha ya kila siku ya wananchi na kutokana na hali hiyo, sheria imefanyiwa marekebisho kwa kuongeza kifungu cha 8A katika kanuni za Ushahidi za Mahakama za Mwanzo.

Amesema marekebisho hayo yameondoa shaka iliyokuwepo hapo awali kuhusu uwezo wa Mahakama ya Mwanzo kupokea ushahidi wa kieletroniki na kwamba Mahakama za Mwanzo sasa zina mamlaka kamili ya kupokea, kuchunguza na kutathmini ushahidi huo kwa kuongozwa na kifungu cha 19 cha Sheria ya Miamala ya Kieletroniki na kifungu cha 70 cha Sheria ya Ushahidi.

Akieleza misingi minne ya Sheria ya chini ya Kifungu cha 19(2), Mhe. Mbuya alisema, Sheria ya Miamala ya Kieletroniki inaelekeza Mahakama kuzingatia mambo manne muhimu wakati wa kutathmini ushahidi wa kieletroniki kwamba uaminifu wa namna ya taarifa iliyotengenezwa, kuhifadhiwa au kutumwa.

Ameongeza kuwa, msingi wa pili ni uaminifu wa namna uhalisia wa taarifa iliyohifadhiwa na namna aliyetoa au kuanzisha taarifa (originator) aliyetambulika na nne jambo lolote lingine linaloweza kusaidia Mahakama kuamua uzito wa ushahidi huo.

Amesema kuwa, mambo hayo manne ndiyo msingi mkuu wa kazi ya Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo katika kutathmini ushahidi wa kielektroniki.

Kadhalika, Naibu Msajili huyo amesema ataandaa mwongozo huo vizuri ili kuwawezesha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kufanya kazi kwa ufanisi na uhakika wa kile wanachokifanya katika kupima na uzito wa ushahidi na kupokea ushahidi wa kieletroniki.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Ilala, Mhe. Herrieth Mwailolo aliwashukuru Mahakimu hao kwa kuhudhuria mafunzo hayo.

Akieleza madhumuni ya mafunzo hayo, Mhe. Mwailolo amesema kutokana na Sheria ya Miamala ya kielektoniki kwa Mahakama za Mwanzo wameona vema wapate mafunzo mafupi ili kuongeza ujuzi na pia kwa Mahakama ya Wilaya wamekuwa wakitumia sheria hiyo lakini wameona vema kuwa na uelewa wa pamoja katika mashauri yanayohusu Sheria za Miamala ya Kieletroniki.

“Kwahiyo tumeona umuhimu wa kukaa pamoja na kwamba Mahakama ya Wilaya tumekuwa tukifanya kesi za aina hiyo, lakini kwa namna moja ama nyingine  wakikaa wawili au watatu  huwa jambo linakuwa jema zaidi pengine hata sisi tulikuwa tunakosea kwa majadiliano hayo tutafika mahali wote tutakuwa na uelewa mmoja,” alisema Mhe. Mwailolo.

Naye Ofisa Upelelezi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wakili Emmanuel  Cheneko amesema kodi ni sheria, kodi ni madai na kodi ni jinai na kwamba kodi ikiwa madai lazima ianzie kwa Kamshina Mkuu  na pale unapoona hujaridhishwa na maamuzi ya Kamishna Mkuu kwa muktadha wa madai, hatua ya kwanza unatakiwa kwenda kwenye Bodi halafu Baraza la Rufaa la Kodi na mwisho Mahakama ya Rufani.

Bw. Cheneko amesema kuwa, wakati kodi inapokuwa jinai ndipo Mahakama za kawaida zinahusishwa. Amesema katika kesi hizo ushahidi mwingi ni wa kieletroniki.

Akifafanua zaidi amesema, kesi za madai za kodi zinaenda kwenye Mabaraza na Jinai zinaenda kwenye Mahakama za kawaida na malalamiko yanaenda kwenye Baraza la Uchunguzi (Ombudsman).

Wakati huohuo, kulikuwa na kikao kazi kilichofanyika kabla ya mafunzo kuanza ambapo Hakimu Mkazi Mfawidhi aliwapongeza Mahakimu hao kwa kufanya kazi kwa bidii na kusema kuwa, hakuna kesi za mlundikano pamoja na Mahakama za Mwanzo kusajili mashauri kwenye mfumo na kuyahuisha kwa wakati.

Katika kikao hicho waliweka mpango mkakati wa kukutana kila robo ya mwaka ili kutathmini utendaji kazi wao ikiwa ni pamoja na kuweka maazimo, lakini pia katika vikao hivyo vinne kimojawapo kitahusisha watumishi wote na wale wasio Mahakimu maana ni sehemu ya uwezeshaji wa kufanisi utendaji kazi wa Mahakimu. 

Mafunzo hayo ya siku moja yalifanyika Kinyerezi na baada ya mafunzo na kikao waliweza kubadilishana mawazo na kufurahi pamoja.


 Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Lumuli Mbuya (kushoto) akitoa mafunzo ya Namna ya Kupokea Ushahidi wa kielekroniki kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya Ilala na Mahakama za Mwanzo za Wilaya hiyo tarehe 19 Juni, 2026. Kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Ilala, Mhe. Herrieth Mwailolo.

 Washiriki wa Mafumo ya Namna Bora ya Kupokea Ushahidi wa Kieletroniki wakiwa katika picha ya pamoja na Mwezeshaji wa mafunzo hayo Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Lumuli Mbuya (aliyekaa katikati). Kushoto ni Mhe. Herrieth Mwailolo na kulia Mhe. Mohamed Burhan.

Baadhi ya Washiriki ambao ni Mahakimu wakishiriki mafunzo ya namna ya kupokea Ushahidi wa Kieletroniki.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Ilala, Mhe. Herrieth Mwailolo akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Namna Bora ya Kupokea Ushahidi wa Kieletroniki.

Ofisa Upelelezi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wakili Emmanuel Cheneko akifundisha Sheria za Kodi kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya Ilala na Mahakama za Mwanzo za Wilaya hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 

 

 

 

 

JAJI RWIZILE AFUNGUA MAHAKAMA ZA MWANZO TATU KIGOMA

Na AIDAN ROBERT-Mahakama Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile ameongoza hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Bangwe, Wilaya ya Kigoma, Manyovu iliyopo Wilaya Buhigwe na Heru Juu iliyopo Wilaya ya Kasulu.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika tarehe 19 Juni, 2026, Mhe. Rwizile amesisitiza kuwa, “tunachokishuhudia leo ni maono ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju, aliwahi kusema, alipokuwa anahutubia Mkutano wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tarehe 13 Mwezi Januari, 2026 Dodoma, ninamnukuu; - "Ujenzi wa majengo ya Mahakama, uwezeshaji wa rasilimali watu na fedha, pamoja na kuboresha mazingira ya kazi kwa Majaji, Mahakimu, na watumishi wa Mahakama ni nguzo muhimu zinazowezesha uhuru wa Mahakama kuwa halisi, unaoonekana na unaotekelezeka kwa ustawi wa wananchi na utawala wa sheria kwa ujumla."

Jaji Rwizile amesema, maneno hayo ya Kiongozi Mkuu wa Mhimili wa Mahakama, yanasadifu haja ya watu kupata haki katika maeneo ambayo si tu haki inakuwa imetendeka bali pia inaonekana kutendeka kwa kuzingatia unadhifu wa watoa haki, ubora wa haki yenyewe na mazingira mazuri ya mahali ambapo haki hiyo hutolewa.

“Kupitia maono hayo ya viongozi wetu wakuu wa Mahakama na Serikali, leo hii tunafurahia uzinduzi wa majengo haya tukitambua kuwa, kinachozinduliwa hapa si Majengo wala Samani au Nakshi zinazopendezesha majengo haya, Bali ni dhana thabiti ya Mahakama kama chombo pekee cha utoaji haki kwa vitendo kwa wananchi wetu,” amesema Mhe. Rwizile.

Aidha, ameongeza kuwa, Mahakama hizo tayari wameshazipangia watumishi mahsusi wa kutoa huduma zilizo bora kuendana na ubora wa majengo yenyewe, amesema, “leo hii baada ya ufunguzi, mashauri yataanza kusajiliwa hapa Bangwe na pale Heru Juu na Manyovu kadhalika wataendelea kupatiwa huduma kwa kadri ya mahitaji yao,” amebainisha Jaji Mfawidhi huyo.

“Nitoe Wito kwa Mahakimu na Watumishi wa Mahakama hizi mpya, pamoja na Wengine kwa ujumla, ninyi ndio nguzo kuu ya usimamiaji haki katika ngazi hii. Tendeni kazi kwa mujibu wa viapo vyenu kwani kiapo chetu ni kizuri kinasema bila ya Huba, Woga, Chuki wala upendeleo wa aina yoyote, mnapaswa kuendelea kulinda imani ya wananchi kwa Mahakama kwa kutoa maamuzi yasiyokuwa na upendeleo, hila au ushawishi wa aina yoyote,” amesisitiza Jaji Mfawidhi huyo.

Kadhalika, amesema kuwa, ni muhimu kutoa maamuzi yenye rejea thabiti katika sheria na misingi iliyowekwa na Mahakama za ngazi za juu, “hii inawataka muwe wa kisasa, wenye kujiongezea maarifa na kufuatilia mabadiliko katika maeneo mbalimbali ya kisheria mtakayokuwa mkiyafanyia kazi,” alisema Jaji Rwizile.

“Majengo haya mapya ni mwendelezo wa utatuzi wa changamoto za muda mrefu za kijiografia katika Mkoa wa Kigoma, hakuna shaka kwamba kipindi cha nyuma wakazi wengi walilazimika kusafiri umbali mrefu na kuingia gharama kubwa kufuata huduma katika Mahakama za Mwanzo zilizokuwa mbali na makazi yao kiasi cha kupoteza muda mwingi kwenye mashauri na sio shughuli za kiuchumi na kijamii,” alieleza Mhe. Rwizile.

Aliongeza kuwa, kupitia maboresho hayo ya ujenzi wa Mahakama mpya za Mwanzo, wananchi wataendelea kufikiwa na huduma hizo na kuokoaa muda na gharama.

“Sote tunakubalina kuwa, umbali wa kutoka Bangwe, Kigoma Mjini, Katonga, Gungu, Kibirizi, Mwanga Kusini na Mwanga Kaskazini, Katubuka na maeneo mengine jirani, haikuwa rahisi kutembea na kufuata huduma Mwandiga au Ujiji ambako Mahakama zinapatikana. Kwa sasa uwepo wa Mahakama ya Mwanzo Bangwe ni faraja na majibu ya wengi katika kufuata haki. Inakadiriwa takribani watu 62,582 watanufaika na huduma hii,” alisema Jaji Rwizile.

Kadhalika alisema kwamba, kwa Mahakama za Mwanzo Heru Juu na Manyovu; Wananchi wa Maeneo ya jirani na Mahakama hizo wataondolewa adha ya kusafiri umbali mrefu kuitafuta haki huku shughuli zao binafsi zikikwama, wanufaika wa huduma hiyo inakadiriwa kuwa watu 24,242 kwa kuzingatia Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, pia huduma ya Mahakama ya Mwanzo Manyovu hapo awali ilikuwa inapatikana Tarafa ya Munanila, na baadae kutokana na uchakavu wa jengo la awali kushindwa kuwa salama kwa matumizi ya binadamu  huduma ikahamia kwa muda katika Ofisi za Serikali ya Kijiji.

Hata hivyo, Mhe. Rwizile alibainisha kuwa, kwa sasa Mahakama imesogezwa karibu na mpaka wa Tarafa mbili yaani Manyovu na Mnanila, Tarafa ambazo zina idadi kubwa ya watu, ambapo Tarafa ya Manyovu ina wastani wa watu 131,298 wakati Tarafa ya Munanila ina wastani wa watu 15,273 kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022.

“Kumbe uwepo wa Jengo hili kwa sasa litatoa huduma Kata za Munzeze, Janda, Rusaba, Muhinda, Mwayaya, Mkatanga, Mubanga, Kinazi, Kibwigwa na Bukuba, wakati huohuo Kata za Munanila na Nyakimwe nazo zikipata huduma za Mahakama katika jengo hilo jipya,” alieleza Jaji Rwizile.

Kwa upande wake Mgeni wa Heshima katika hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro, alisema kuwa, uzinduzi wa majengo hayo mapya ni kielelezo tosha kuwa Mahakama imedhamiria kwa dhati kuhakikisha kuwa wananchi hawapati tu haki, bali wanaipata katika mazingira yenye staha, hadhi na usalama.

“Ujenzi na uzinduzi wa miundombinu hii ya kisasa sio jambo la bahati mbaya ni taswira halisi ya utambuzi wa kina na dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita, kupitia Wizara ya Katiba na Sheria, maboresho haya makubwa ya miundombinu ni tafsiri ya maono ya kimkakati ya Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha tunaimarisha, tunakuza na kulinda kikamilifu Uhuru wa Mahakama ikiwa ni utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” alisema Balozi Mhe. Sirro.

Hafla hiyo iliyofanyika katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Bangwe ilihudhuriwa na Viongozi wa ngazi ya Wilaya na Mkoa wa Kigoma pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusufu Kasuka.

Wageni wengine ni Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa na Wilaya, Wakuu wa Wilaya za Kasulu na Buhigwe, pamoja Mahakamu wafawidhi wa Wilaya za Buhigwe, Kigoma, Kasulu, Kibondo, Kakonko na Uvinza, sambamba na wadau wa Mahakama na wananchi pamoja na vikundi vya burudani.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akikata utepe kuashiria ufunguzi wa Mahakama za Mwanzo tatu za Bangwe, Manyovu na Heru Juu uliofanyika tarehe 19 Juni, 2026. Wanaoshuhudia kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi na kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Kigoma Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro (kushoto) kwa pamoja wakifungua kitambaa cha jiwe la msingi la Jengo hilo ikiwa ni ishara ya kufunguliwa kwa Mahakama.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mahakama za Mwanzo tatu katika hafla iliyofanyikia katika Viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro akitoa salamu za Serikali katika ufunguzi wa Mahakama za Mwanzo tatu katika hafla iliyofanyikia katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe ikiwa ni ishara ya alama na historia katika Mahakama hiyo ya Mwanzo Bangwe mara baada ya kufunguliwa.

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe ikiwa ni ishara ya alama na historia katika Mahakama hiyo ya mwanzo hiyo mara baada ya kufunguliwa.

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe ikiwa ni ishara ya alama na historia katika Mahakama hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (kushoto), Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro (kulia). Waliosimama ni Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)