Alhamisi, 5 Februari 2026

HUDUMA YA MAHAKAMA INAYOTEMBEA KIGAMBONI YAANZISHWA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Dar es Salaam

Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia (IJC) Temeke kimeanza rasmi kutoa huduma ya Mahakama Inayotembe katika Wilaya ya Kigamboni, Mtaa wa Mjimwema zilipo Ofisi za Mtendaji Kata.

Kuanzishwa kwa huduma hiyo ya kimahakama kulitanguliwa na kipindi cha kumepambazuka kilichoendeshwa katika Mahakama hiyo, kikilenga kufikisha ujembe kwa wakazi wa Wilaya ya Kigamboni kuhusu kuanzishwa kwa shughuli za usikilizwaji wa mashauri ya mirathi, ndoa na talaka katika Mahakama Inayotembea ndani ya Wialaya hiyo.

Kipindi hicho kiliongozwa na Mtangazaji Abdalah Kulwa wa Radio One na Mzungumzaji akiwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo iliyopo ndani ya IJC Temeke, Mhe. Upendo Kapama.

Mhe. Kapama alifafanua kwamba Mahakama Inayotembea itatoa huduma za mashauri ya mirathi, ndoa na talaka yanayosikilizwa na Mahakama ya Mwanzo, na mpango huo unalenga kusogeza huduma kwa wananchi.

Aliendelea kusema kwamba sasa Wilaya ya Kigamboni, Mtaa wa Mjimwema patakuwa na Kituo kitakachotoa huduma kila siku ya Jumatano ili kuwaepushia wananchi adha ya kusafiri, muda na gharama za kutoka Kigamboni hadi Temeke.

Mhe. Kapama alieleza jinsi Mahakama Inayotembea inavyowasaidia Wananchi katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata elimu na huduma bora kwa haraka mtaani kwako. Huduma hii inatolewa katika Wilaya ya Kinondoni, Bunju A Ofisi za Mtendaji Kata, Wilaya ya Ubungo Kibamba zilipo Ofisi za Mkuu wa Wilaya na Wilaya ya Ilala Chanika Ofisi za Mtendaji Kata na sasa ni Kigamboni.

Alisisitiza huduma hii inaongeza ufunguaji wa mashauri katika maeneo hayo kwa sababubu wananchi wengi wanapata elimu kubwa ya masuala ya familia, mirathi na ndoa na wanarahisishiwa kwa kufuatwa walipo.

Pia Mhe. Kapama aliendelea kuonyesha jinsi gani Mahakama hiyo inavyowarahisishia wagonjwa kutoa ushahidi kwa kutokusafiri umbali mrefu, hivyo kupunguza gharama na muda.

Mhe. Kapama alisema matarajio ya kusogeza huduma hiyo Mjimwema Kigamboni ni kuondoa dhana ya watu kuishi kimazoea pindi wanapopoteza wapendwa wao na kufuata sheria kwa kufungua mirathi mapema ili kuondoa migogoro katika familia inayoweza kutokea, hivyo kwa kusogezewa Mahakama Inayotembea kutaondoa changamoto hizo.

Aidha, Mhe. Kapama aliwahimiza wakazi wa Kigamboni kujitokeza kwa wingi ili kupata elimu na kufungua mashauri kwa wale wenye uhitaji na mashauri yao yatasikilizwa hapo hapo ndani ya Mahakama Inayotembea kwa haraka, kwani mashauri huchukua siku 30 hadi kusomwa hukumu.



Mahakama Inayototembea ikiwa Wilaya ya Kigamboni, Mtaa wa Mjimwema. Picha chini, wadau wakiwa ndani ya Mahakama Inayotembea.


 

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo iliyopo ndani ya IJC TemekeMhe. Upendo Kapama akiwa ndani ya Mahakama Inayotembea.






MAHAKAMA DODOMA, WADAU WAKUTANA KUTATHMINI UTENDAJI

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama – Dodoma.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, hivi karibuni ilifanya kikao na wadau ili kutathmini utendaji kazi wa mwaka 2025 na kuweka mikakati ya kuboresha huduma za utoaji haki kwa mwaka 2026.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, kilifunguliwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo. Mhe. Dkt. Masabo alieleza kuwa kikao hicho ni sehemu ya utamaduni wa Mahakama kukutana na wadau wake ili kufanya tathmini ya pamoja na kubadilishana uzoefu wa namna bora ya kuboresha utoaji wa huduma.

Mhe. Dkt. Masabo alieleza kuwa lengo lingine ni kuangalia kwa pamoja utendaji kazi wa mwaka uliopita, kubaini mafanikio na changamoto zilizojitokeza, na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha maeneo yaliyohitaji uboreshaji.

Alisisitiza kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, inayojumuisha Mikoa ya Dodoma na Singida, ina wajibu mkubwa kutokana na Dodoma kuwa Makao Makuu yaNnchi, hivyo mabadiliko yanayoendelea yanahitaji kasi na ubora zaidi katika utoaji haki.

Aidha, alibainisha lengo jingine ni kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na wadau, ambao ni nguzo muhimu katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama. Kupitia vikao vya namna hiyo, wadau wamekuwa wakipanga pamoja na kutekeleza majukumu kwa pamoja, jambo lililochangia kuongeza ufanisi wa utendaji.

Akizungumzia mafanikio ya mwaka uliopita wa 2025, Mhe. Dkt. Masabo alisema Mahakama ilipokea mashauri zaidi ya 1,000 na pia kufanikiwa kumaliza mashauri zaidi ya 1,000. Alibainisha kuwa mafanikio hayo yametokana kwa kiasi kikubwa na ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Mabaraza ya Ardhi, Ofisi ya Kamishna wa Ardhi, Msajili wa Hati, pamoja na Taasisi nyingine zinazohusika na masuala ya kisheria na kiutawala.

Aliongeza kuwa mashauri mengi yaliyopokelewa na kumalizwa yalihusu masuala ya ardhi, jambo linaloonesha umuhimu wa ushirikiano wa karibu na taasisi zinazohusika na sekta hiyo.

Katika kikao hicho, wadau walipata pia fursa ya kujifunza mambo mbalimbali zitakazowasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akisoma taarifa ya mashauri katika kikao hicho, Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe Silivia Lushasi, alibainisha mikakati mbalimbali ya kuzuia mashauri kukaa muda mrefu mahakamani kwa mwaka 2026.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa inasikiliza kwa makini maoni na ushauri kutoka kwa wadau waliodhuria kikao hicho, aliyepo kulia kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Amir Mruma na aliyepo kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Silvia Lushasi.

Washiriki wa kikao wakiogozwa na Jaji Mfawdhi (hayupo pichani) wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Silivia Lushasi (hayupo pichani).

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Dodoma pamoja Viongozi kutoka Taasisi mbalimbali waliohudhuria kikao hicho, walioketi kulia kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Amir Mruma na aliyepo kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Silvia Lushasi.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu pamoja na wadau kutoka Taasisi mbalimbali waliohudhuria kikao hicho.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa katika picha ya pamoja na Si.ekretariet  

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

 

WATUMISHI WA MAHAKAMA KUU MUSOMA WATEMBELEA WATOTO WENYE MAHITAJI

Na FRANCISCA SWAI-Mahakama, Musoma

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, jana tarehe 04 Februari 2026, walitembelea Kituo cha Watoto wenye mahitaji maalum na kutoa msaada wa vitu mbalimbali muhimu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, aliwaongoza watumishi hao, ambao walitembelea Kituo cha Al-Jaziira Orphan Centre kilichopo Kijiji cha Mkirira, Kata ya Nyegina, Musoma Vijiji. Kituo hicho kinahudumia watoto wa kiume wenye umri wa miaka minne hadi 15.

Akitoa shukrani kwa watumishi wa Mahakama, Kaimu Meneja wa Kituo hicho, Bw. Said Masaka, alisema Kituo hicho kina mahitaji mengi, ikiwa ni pamoja na elimu ya ushauri wa kisheria kuhusu haki za motto, mafunzo ya sheria ya mtoto kwa walezi na watumishi, pamoja na msaada wa kusimamia sera ya ulinzi wa mtoto.

Ombi hilo lilipokelewa na uongozi wa Mahakama ambapo waliahidi kwenda kujipanga ili kuwapa elimu hiyo hivi karibuni.

Aidha, pamoja na tendo jema hilo, watumishi wa Mahakama walipata pia elimu kuhusiana na masuala ya kibenki na fedha kutoka kwa watumishi wa Benki ya NMB Musoma.

Mwenyekiti wa Kamati ya Tendo Jema, Bw. Musa Komba, akimkabidhi Kaimu Meneja wa Kituo cha Al-Jaziira Orphan Centre, Bw. Said Masaka, zawadi mbalimbali kutoka kwa watumishi wa Mahakama Musoma.

Watoto wa kituo cha Al-Jaziira Orphan Centre (waliosimama katikati) wakiongoza dua ya kuwashukuru na kuwaombea watumishi na Mahakama ya Tanzania.

Kaimu Meneja wa Kituo cha Al-Jaziira Orphan Centre, Bw. Said Masaka [wa kwanza kushoto] akisikiliza kwa makini salamu za Mahakama zinazotolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Tendo Jema, Bw. Musa Komba, [aliyesimama katikati].

Picha ya pamoja ya watumishi wa Mahakama Musoma, viongozi na walimu wa kituo cha Al-Jaziira Orphan Centre.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (wa pili kushoto) pamoja na watumishi wa Benki ya NMB waliotoa elimu ya masuala ya kifedha kwa watumishi wa Mahakama Musoma.

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

 

MAHAKAMA KUU MWANZA YAADHIMISHA MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA NCHINI

Na. Rehema Awet – Mahakama, Mwanza

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Nimilwa Kilekamajenga amesema kuwa, Siku ya Sheria ni fursa muhimu ya kutathmini na kutafakari upya dhamira ya Mahakama katika kulinda haki za wananchi na kusimamia utawala wa sheria nchini. Aliongeza kuwa Mahakama ina nafasi ya kipekee katika kujenga jamii yenye haki, amani na maendeleo endelevu.

Aidha, alibainisha maeneo makuu ya mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya taifa kuwa ni pamoja na ulinzi wa haki za binadamu na kuimarisha utawala wa sheria, kuchochea ukuaji wa uchumi na uwekezaji, pamoja na kudumisha amani na utulivu wa kijamii.

Mhe. Kilekamajenga, alibainisha kuwa, maeneo mengine kuwa ni kuimarisha Demokrasia, mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi. Pia alieleza kuwa maboresho ya miundombinu na matumizi ya TEHAMA katika usikilizwaji na uendeshaji wa mashauri, jambo ambalo limeongeza ufanisi na uwazi katika utoaji wa haki.

Kwa upande wake, Bw. Kabyemela S. Lushagara akizungumza kwa niaba ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, alisema Mahakama ni Mhimili muhimu wa Dola unaochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia ulinzi wa haki, utawala wa sheria na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji. Alioneza kuwa, Mahakama huru, yenye weledi na uadilifu huongeza imani ya wananchi na wawekezaji, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Aidha, mwakilishi huyo kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali alisema, mafanikio mbalimbali yaliyopatikana katika sekta ya haki, ikiwemo kupungua kwa msongamano wa mashauri, ongezeko la Majaji na Mahakimu, matumizi ya mifumo ya TEHAMA kama e-filing, pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama na Taasisi za utoaji haki. Pia alisisitiza kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji mfumo imara wa utoaji haki unaofanya kazi kwa ufanisi na kwa wakati

Akizungumza kwa niaba ya Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Kanda ya Mwanza, Wakili Erick Mutta alisisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa uhuru wa Mahakama na ulinzi wa Mawakili wa Kujitegemea kama nguzo ya Utawala wa Sheria. Wakili Mutta alieleza kuwa Mahakama inayofanya kazi kwa haki na bila upendeleo hujenga imani ya wananchi na kuleta utulivu wa kijamii na kisiasa unaohitajika kwa maendeleo endelevu.

Chama cha Mawakili wa Kujitegemea kanda ya Mwanza ilitumia jukwaa hilo kueleza mchango wake katika utoaji wa msaada wa kisheria kwa wananchi wasio na uwezo, elimu ya kisheria kwa umma, pamoja na ushiriki wake katika utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala nje ya Mahakama.

Mgeni rasmi ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi Kanda ya Mwanza Mhe. Kilekamajenga alihitimisha kwa kutoa wito kwa wadau wote wa haki kushirikiana kwa karibu na Mahakama ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati kwa usawa na kwa mujibu wa sheria, kwa lengo la kuimarisha ustawi wa wananchi na maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Maadhimisho hayo ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika mkoani Mwanza kwa yakibeba kauli mbiu isemayo “Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.” yalihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali, vyombo vya Dola, wataalamu wa sheria pamoja na wananchi.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akiwa tayari kwa ukaguzi wa Gwaride maalum kuashiria uzinduzi wa mwaka mpya wa shughuli za kimahakama kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026. Waliosimama nyuma ni Majaji, Mawakili na sehemu ya Wadau wengine wa Mahakama Kanda ya Mwanza.

Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe.Dkt Ntemi Kilekamajenga wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kanda ya Mwanza.

Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe.Dkt Ntemi Kilekamajenga wakiwa katika picha ya pamoja na mawakili wa serikali na wa kujitegemea.

Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe.Dkt. Ntemi Kilekamajenga (katikati), Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda (wa tatu kushoto) na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akihutubia wananchi katika  viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kanda ya Mwanza  kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Ntanda akihutubia katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza kwenye  maadhimisho ya siku ya sheria nchini.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt  Ntemi Kilekamajenga akikagua Gwaride maalum lililoandaliwa kuashiria kuanza kwa mwaka mpya wa Mahakama, 2026.

Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe.Dkt. Ntemi Kilekamajenga wakiwa anapokea heshima kutoka kwa kiongozi wa gwaride maalum la heshima siku ya maadhimisho ya siku ya sheria nchini. 

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

Jumatano, 4 Februari 2026

TEHAMA YAONDOA MLUNDIKANO WA MASHAURI MAHAKAMANI GEITA

Na DOTTO MKAJA-Mahakama, Geita

Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yameiwezesha Mahakama Kuu Kanda ya Geita kuondoa mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama kwa mwaka 2025.

Hayo yamebainishwa jana Februari 2, 2026 na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, wakati akitoa hotuba yake katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini yaliyofanyika katika Uwanja wa Kituo Jumuishi Geita (Jengo Jipya).

Mhe. Mhina alisema Mahakama ni chombo muhimu katika kuchochea ukuaji wa uchumi na kulinda amani ya wananchi, akibainisha kuwa bila uwepo wa Mahakama, vyombo vya ulinzi na usalama, Magereza na Serikali, hata siku moja haviwezi kupita bila kutokea uvunjifu mkubwa wa amani.

Akizungumza kuhusu utendaji wa Mahakama Kanda ya Geita, alisema kuwa kwa mwaka 2025 Mahakama zote zilifanikiwa kumaliza mashauri kwa wakati, huku wastani wa umalizaji wa mashauri katika Mahakama za Wilaya tano ukiwa siku 35.

Aliongeza kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita ilikuwa na wastani wa siku 60, Mahakama Kuu siku 46 na Mahakama za Mwanzo siku 15. Alisema kuwa wastani wa muda wa usikilizaji mashauri kwa mwaka 2025 umepanda kulinganisha na mwaka 2024.

Akifafanua mafanikio hayo, alisema yameleta ongezeko la ufanisi katika usikilizwaji wa mashauri, kupungua kwa muda wa mashauri kusikilizwa na kuamuliwa, pamoja na kuondolewa kabisa kwa mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama Kanda ya Geita.

Aidha, alisema Mahakama ilisikiliza na kumaliza mashauri yote ya kimkakati yaliyokuwa yameshikilia uchumi, hali iliyosababisha fedha zilizokuwa zimezuiwa kurejeshwa katika mzunguko wa uchumi na kuhamasisha uwekezaji.

Mhe. Mhina alisema mafanikio hayo yametokana na matumizi ya TEHAMA, akieleza kuwa teknolojia hiyo imeongeza uwazi kwa wadau wa haki na kuimarisha ushirikiano kati ya Taasisi mbalimbali kupitia mifumo inayosomana, ikiwemo NIDA, RITA, Magereza na taasisi nyingine.

Aliwasihi wadau wa sheria kuendelea kufanya kazi kwa kuzingatia uadilifu, weledi na ushirikiano.

Kwa upande wake, Mgeni Mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, aliipongeza Mahakama Kuu Kanda ya Geita kwa kumaliza mashauri kwa wakati na kwa haki, akisema hali hiyo imepunguza kwa kiasi kikubwa malalamiko kutoka kwa wananchi.

“Sipokei malalamiko kutoka mahakamani, jambo linaloonesha kuwa haki inatendeka kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji,” alisema Mhe. Shigela.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akitoa hutuba Siku ya Sheria katika uwanja wa Mahakama Kuu Geita (Jengo Jipya).

Mchungaji kutokKanisa la KKKT akitoa maombi ya kufungua Maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Uwanja wa Kituo Jumuishi Geita (IJC - Geita).

Meza kuu katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria iliyofanyika katika kituo Jumuishi Geita (IJC – Geita).

Mahakimu wakikiwa katika picha ya pamoja Siku ya Sheria nchini katika uwanja wa Kituo Jumuishi Geita(IJC - Geita).

Maofisa kutoka ofisi ya Mwendasha Mashitaka wakiwa katika picha ya pamoja.

Mawakili wa Kujitegemea wakiwa katika picha ya pamoja na meza kuu kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Kevin Mhina, akikagua gwalide Siku ya Sheria katika uwanja wa kituo Jumuishi Geita.

 

Watumishi wanawake Mahakama Kuu Geita na Mahakama ya Wilaya Geita katika picha ya pamoja wakiadhisha Siku ya Sheria 2026 katika Kituo Jumuishi Geita.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma