Alhamisi, 26 Machi 2026

SONGWE YAJIVUA RASMI KUTOKA MAHAKAMA KUU KANDA YA MBEYA

Na. IMAN PATSON – Mahakama, Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga jana tarehe 25 Machi, 2026 alikabidhi rasmi eneo jipya la kiutawala la Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kanda ya Songwe kwa Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo Mhe. Gabriel Malata, katika hafla iliyofanyika katika Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe.

Aidha, Mhe. Tiganga alifanya ukaguzi wa jengo hilo jipya ambapo alipitia miundombinu ya jengo na vifaa vya Ofisi na kisha kufanya makabidhi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songwe Mhe. Malata.

Mhe. Tiganga alipongeza wakandarasi wa Jengo hilo kwa kazi nzuri waliofanya na pia aliwasihi wafanyakazi wa jengo hilo kumalizia kazi iliyobakia kwa muda mfupi ili kazi zingine za kimahakama ziweze kuendelea.

Aidha, baada ukaguzi huo Mhe, Tiganga alifanya kikao cha kuagana na watumishi wa Mahakama Kanda ya Songwe na kuwashukuru kwa ushiriakiano alioupata kutoka kwao na aliwaahidi kuwa ataendelea kutoa ushirikiano wakati wote atakapo hitajika. Vilevile, aliwakumbusha umuhimu wa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi Mhe. Malata aliwasisitiza watumishi kuhusu suala la nidhamu, kuthaminiana, upendo, ulinzi wa miundombinu, vitendea kazi wa vya Ofisi na utendaji wa kazi mzuri kwa watumishi wote ili kuwezesha kutoa huduma bora ya haki kwa wananchi.

Mhe. Malata Uongozi wa Mahakama kwa kumteua kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songwe na kuahidi kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha haki inatolewa kwa wananchi kwa wakati mapema ipasavyo.

Kufuatia makabidhiano hayo, Mhe. Tiganga aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mavis Miti.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (kulia) akifanya makabidhiano na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (kushoto) kuashiria shughuli rasmi za Mahakama Kuu, Kanda ya Songwe.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kanda ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa kwanza kushoto) akionesha hati ya makabidhiano.

Muonekano wa Jengo la Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kanda ya Songwe lilipofikia.

Mhandisi wa jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji haki Kanda Songwe Bw. Victor akielezea maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo lilipofikia na akiahidi kuwa kufikia Aprili 1, 2026 jengo hilo litakua lipo tayari kwa matumizi.

Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe mara baada ya makabidhiano, wa tatu kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa tatu kulia), Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (wa pili kushoto), Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Mhe. Joyce Minde (wa pili kulia), Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Bw. Sostenes Mayoka (wa kwanza

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




JAJI MFAWIDHI MBEYA AFUNGUA MAFUNZO YA USULUHISHI KWA NAIBU WASAJILI, MAHAKIMU WAKAZI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga amefungua mafunzo maalum ya Usihi na Usuluhishi kwa Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi kutoka katika Kanda mbalimbali za Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Iringa, Njombe, Sumbawanga, Songwe na Katavi.

Mafunzo hayo yaliyofunguliwa tarehe 24 Machi, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya. Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Tiganga alisema kuwa usuluhishi unalenga kuimarisha upatikananaji wa haki mapema ipasavyo na kwa gharama nafuu.

“Usuluhishi ni nguzo muhimu sana katika utoaji haki, kwani hupunguza migogoro baina ya wanajamii na kupunguza gharama kwa wadaawa katika kutatua migogoro yao,” alisema Mhe. Tiganga.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mafunzo hayo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Mhe. Gloria Shuma akizungumza na washiriki alisema kuwa, mafunzo hayo yatakayodumu kwa muda wa siku tatu yana lengo mahususi la kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani na kupunguza athari za upatikanaji wa vidonda na makovu ambayo ni matokeo ya migogoro katika jamii.

Aidha, washiriki walieleza kuwa matarajio yao katika mafunzo hayo ni kujifunza kwa kubadilishana uzoefu baina yao namna ya kufanya usihi na usuluhishi, kujifunza namna ya kuwa wasuluhishi bora na kubaini changamoto mbalimbali zinazojitokeza wakati wa usuluhishi na namna ya kuzitatua kwa pamoja.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mafunzo ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2013, Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania pamoja na sera ya Mafunzo ya Mahakama ya Tanzania ya mwaka 2019.

    Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Waheshimiwa Naibu Wasajili na Waheshimiwa Mahakimu Wakazi kutoka katika Kanda mbalimbali za Nyanda za Juu Kusini wanaoshiriki mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi ambao ni Naibu Wasajili wanaoshiriki Mafunzo ya Usuluhishi kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.


Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (aliyesimama kwenye podium) akifungua mafunzo hayo maalum kwa Waheshimiwa Naibu Wasajili na Waheshimiwa Mahakimu Wakazi.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto) akiwa sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba ambaye pia ni mwezeshaji Mhe. Raymond Kaswaga akitoa mada kwenye mafunzo hayo ya Usuluhishi

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.


Mratibu wa mafunzo hayo Mhe. Gloria Shuma (kulia) kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) akifuatilia mafunzo hayo, kushoto ni Hakimu Mkazi Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Franco Msuja


Jumatano, 25 Machi 2026

TMJA TAWI LA KILIMAJARO YANOGESHA MASHINDANO YA KILIMANJARO MARATHON 2026

  • Watumia jukwaa hilo kutoa elimu ya sheria kwa umma
  • Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo awapongeza

Na PAUL MUSHI- Mahakama, Moshi

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu (TMJA) Tawi la Kilimanajaro, wakiongozwa na Mlezi wao, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lilian Mongella, hivi karibuni walishiriki kikamilifu kwenye mbio za urefu wa Kilomita 42, 21 na 5 katika kwenye tamasha kubwa la michezo la International Kilimanjaro Marathon.

Tamasha hilo lililofanyika kuanzia tarehe 19 hadi tarehe 22 Machi, 2026 liliongozwa na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda na kushirikisha Wadau wa michezo wa ndani ya nchi na mataifa mbalimbali duniani. Mhe. Makonda pia alitoa zawadi kwa washindi katika mbio za aina tofauti.

Baada ya kutoa zawadi hizo, Waziri Makonda alitembelea na kukagua mabanda yaliyokuwa yanatoa huduma mbalimbali, likiwemo la TMJA lililokuwa linatoa elimu ya masuala ya kisheria kwa Wananchi.

Akiwa kwenye banda hilo, Mhe. Makonda aliwapongeza Majaji na Mahakimu  kwa kutumia jukwaa hilo kuimarisha afya zao na kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya kisheria.

“Nilipata taarifa ya uwepo wenu katika tamasha hili, kwakweli sikutegemea kama mngekuwepo. Nawapongeza sana kwa kazi kubwa mliyoifanya, hasa ya kutoa elimu katika siku hizi zote toka siku ya ufunguzi. Niwaombe muendelee na awamu zijazo ili muwafikie watu wengi zaidi kwa elimu hii mnayotoa,” alisema Waziri Makonda.

Naye Mhe. Dkt. Mongella aliwapongeza washiriki kwa kujitoa kwao katika hali na mali kushiriki katika tamasha hilo kwa lengo la kuimarisha afya zao na kutoa elimu kwa watu wenye uhitaji kwenye masuala ya kisheria.

“Nawapongeza sana viongozi wa Tawi letu la TMJA Kilimanjaro kwa kuona umuhimu kwa kushiriki tamasha hili kubwa. Hili si tu kwamba ni muhimu katika kujenga afya zetu, bali pia jambo la kutoa elimu ni kubwa zaidi, hasa kwa kuzingatia uwingi wa watu katika tamasha,” alisema.

Katika hatua nyingine, Rais wa TMJA, Mhe, Elimo Massawe, aliyeambatana na Katibu wa Chama hicho, alipata fursa ya kutembelea na kuona shughuli zilizofanyika wakati wa tamasha hilo.

Mhe. Masawe naye aliwapongeza wanachama wa Tawi hilo kwa kazi kubwa waliyofanya na kuwapa shime ya kuendelea kuwa wabunifu na kufanya zaidi kwa siku zijazo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lilian Mongella akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kutembelea banda la maonyesho katika viwanja vya ushirika Moshi yalipofanyikia mashindano ya Kilimanjaro Marathon 2026.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, (wa kwanza kushoto mwenye fulana ya njano) akikabidhiwa zawadi na Mjumbe wa Baraza Tendaji Taifa wa Chama cha Majaji na Mahakimu, Mhe. James Kapele, kwa niaba ya mlezi wa Tawi, baada ya kutembelea banda la chama hicho.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi wakitoa elimu kwa Wananchi waliofika katika banda la Mahakama katika viwanja vya ushirika Moshi yalipofanyikia mashindano ya Kill Marathon 2026.

Rais wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania, Mhe. Elimo Massawe, alipotembelea banda la TMJA Tawi la Kilimanjaro wakati wa tamasha la Kilimanjaro Marathon 2026.

Baadhi ya Watumishi wa Mahakama walioshiriki mbio wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumaliza mbio za Kill marathon 2026.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

 

Jumanne, 24 Machi 2026

MBEYA YAZINDUA MAHAKAMA TATU ZA MWANZO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga ameongoza hafla ya uzinduzi wa Majengo Mapya Matatu (3) ya Mahakama za Mwanzo. Majengo hayo matatu yaliyozinduliwa ni pamoja na Mahakama ya Mwanzo Lupatingatinga wilayani Chunya, Mahakama ya Mwanzo Ndobo Wilaya ya Kyela na Mahakama ya Mwanzo Madibila Wilaya ya Mbarali.

Hafla hiyo ilifanyika tarehe 23 Machi, 2026 katika Viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Lupatingatinga wilayani Chunya. Uzinduzi wa Mahakama hizo unalenga kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wananchi, kupunguza umbali wa kufuata huduma za kimahakama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa wakati mapema ipasavyo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Tiganga, aligusia dhima ya Mahakama katika kutoa haki kwa wakati unaostahili bila kuchelewesha huduma hizo za msingi kwa wananchi.

“Haki ndiyo msingi wa ustawi wa amani na usalama wa wananchi, na sisi kama Mahakama tumejidhatiti katika utoaji wa haki kwa watu wote na tuko tayari kufanya hivyo mapema ipasavyo,” alisema Mhe. Tiganga.

Vilevile, Mhe. Tiganga aliwaasa watumishi wa Mahakama katika Vituo hivyo kuhakikisha huduma zitakazotolewa zinaakisi hadhi ya Majengo hayo, na kusisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora kwa haki na weledi kwa kuzingatia uadilifu na misingi ya utumishi wa umma.

Aidha, aliuomba uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chunya kusaidia upatikanaji wa viwanja katika kila kata ili kufikia lengo la Mahakama ya Tanzania la kusogeza huduma za Mahakama karibu zaidi na wananchi.

Kwa upande wake, mgeni maalum katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mhe. Alhaj Baraka Batenga, aliwaasa wananchi kuyatunza na kuyahifadhi Majengo hayo kwani ni kwa ajili ya kulinda msingi wa amani na kudumisha ustawi wa utoaji haki kwa wananchi.

“Mahakama ni mali ya wananchi, hivyo ni wajibu wetu sote kuyalinda na kuyatunza majengo ya Mahakama zetu pamoja na miundombinu yake kwa ujumla,” alisema Mhe. Batenga.

Naye, Mbunge wa Jimbo la Lupa, Mhe. Masache Kasaka, alitoa shukrani kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuwezesha kukamilika kwa Majengo hayo ya kisasa, ambayo yatasogeza huduma za Mahakama karibu na wananchi.

“Suala la utoaji haki kwa wananchi mapema ipasavyo linaendana sambamba na ukaribu wa upatikanaji wa huduma za kimahakama,” alisema Mhe. Kasaka.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu, Kanda za Mbeya na Songwe, akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Songwe, Mhe. Gabriel Malata, Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Songwe Mhe. Joyce Minde.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Bi. Mavis Miti, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Songwe Bw. Sostenes Mayoka na Mahakimu Wakazi wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer.

Aidha, Uongozi wa Wilaya ya Chunya uliongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mhe. Alhaj Baraka Batenga, pamoja na Mbunge wa Jimbo la Lupa, Mhe. Masache Kasaka na viongozi wengine.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akihutubia wakati wa hafla ya uzinduzi wa Majengo Mapya Matatu (3) ya Mahakama za Mwanzo za Lupatingatinga wilayani Chunya, Mahakama ya Mwanzo Ndobo Wilaya ya Kyela na Mahakama ya Mwanzo Madibila Wilaya ya Mbarali, tarehe 23 Machi, 2026 katika Viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Lupatingatinga wilayani Chunya.

Sehemu ya wananchi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya na Mkoa wa Mbeya waliohudhuria hafla hiyo ya uzinduzi waliosimama mbele wakiongoza na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (watatu kulia)


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, wengine ni Mbunge wa Jimbo la Lupa Mhe. Masache Kasaka (kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Chunya Mhe. Alhaj Baraka Batenga (wa pili kushoto).




Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Wananchi waliohudhuria hafla hiyo, wengine ni Mbunge wa Jimbo la Lupa Mhe. Masache Kasaka (kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Chunya Mhe. Alhaj Baraka Batenga (wa pili kushoto).

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama waliohudhuria hafla hiyo, wengine ni Mbunge wa Jimbo la Lupa Mhe. Masache Kasaka (kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Chunya Mhe. Alhaj Baraka Batenga (wa pili kushoto).

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama waliohudhuria hafla hiyo, wengine ni Mbunge wa Jimbo la Lupa Mhe. Masache Kasaka (kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Chunya Mhe. Alhaj Baraka Batenga (wa pili kushoto).
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Mkoa wa Mbeya waliohudhuria hafla hiyo, wengine ni Mbunge wa Jimbo la Lupa Mhe. Masache Kasaka (kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Chunya Mhe. Alhaj Baraka Batenga (wa pili kushoto).

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akipanda Mti wa Matunda katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Lupatingatinga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (kulia) akikabidhi kibao cha Ufunguzi wa Mahakama ya Mwanzo Madibila kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbarali Mhe. Emily Mwambapa.



Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (kulia) akikabidhi kibao cha Ufunguzi wa Mahakama ya Mwanzo Ndobo kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Rosta Mofuga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi Jengo la Mahakama ya Mwanzo Lupatingatinga pamoja na majengo mengine mawili ya Mahakama za Mwanzo Ndobo na Madibila.

Kikundi cha ngoma za asili “Dedede” wakitumbuiza katika hafla hiyo.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama waliohudhuria katika hafla hiyo.


Sehemu ya watumishi wa Mahakama waliohudhuria katika hafla hiyo.


JAJI NKWABI APONGEZA WATUMISHI KWA KUTEKELEZA MAELEKEZO YA VIONGOZI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi amewapongeza watumishi wa Mahakama za Wilaya Kanda ya Kigoma kwa kuzingatia majukumu yao na kutekeleza maelekezo mbalimbali yanayotolewa na viongozi wa ngazi mbalimbali za Mahakama hususani ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Mhe. Nkwabi aliyasema hayo hivi karibuni katika ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Wilaya na Magereza, huku akisisitiza kuwa, maelekezo ya Viongozi yanapaswa kuzingatiwa kwakuwa ndio mwelekeo wa kasi ya shughuli za Mahakama ili kuhakikisha usikilizwaji wa mashauri unafikiwa kwa viwango vya juu. 

Ameongeza kuwa, maelekezo yanayotolewa na Viongozi ndio kichocheo cha utendaji wa Mahakama na hivyo kuwa katika nafasi ya juu katika usikilizwaji na umalizwaji wa mashauri Mahakamani kwa mwaka 2025-2026.

Aidha, ametoa rai kwa Viongozi wa Mahakama hizo kusimamia vema mashauri ya mirathi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha fedha za mirathi haziendelei kuonekana katika akaunti ya Mahakama badala yake walipwe wanufaika na Mahakama ihakikishe msimamizi anawajibika kuisaidia Mahakama kufunga mirathi mara baada ya kugawa mirathi kwa wanufaika wa mirathi husika.

Alisema kwamba, hatua hiyo itasaidia kupunguza msongamano wa fedha na malalamiko mahakamani lakini pia amewataka watendaji kufuatilia vema malipo ya mirathi kwani ndio wanaohusika na ulipwaji wa fedha za mirathi, hivyo ni vema kuwa na mawasiliano ya karibu kati ya Hakimu husika na jalada la shauri pamoja na Maafisa Masuhuli wanaoendelea kufanya malipo ya fedha za wanufaika hao kupitia nyaraka halisi za Mahakamani.

Jaji Nkwabi na Viongozi wa Kanda ya Kigoma na Wilaya Kasulu walitembelea ujenzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Heru Juu na kukagua maeneo ya mipaka ya Mahakama hiyo ambayo ujenzi upo zaidi ya asilimia 76 ikiwa ni utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama wa kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

“Mkizingatia taratibu zote za usimamizi wa mashauri ya mirathi hakika fedha za mirathi zaidi ya shilingi za Kitanzania 201,868,074.66 iliyopo kwenye akaunti ya mirathi ya Kigoma itaisha na haitaongezeka tena na suala hilo litabaki historia kwa Kanda ya Kigoma, hivyo nashauri Maafisa wapitie jalada kwa jalada ili kubaini wanufaika hatimaye fedha hiyo ilipwe mapema kwa wadau hao,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kigoma   Bw. Filbert Matotay wote katika nyakati tofauti walisisitiza umuhimu wa kuzingatia ufungaji wa mirathi kwa mujibu wa taratibu pamoja na kufuatilia kwa karibu wasimamizi wa mashauri hayo ili kuondoa sintofahamu katika hatua ya ufungaji wa Mirathi.

Vilevile, waliweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha zoezi hilo la ufungaji wa mirathi linafanyika kwa ufanisi na ndani ya muda waliojipangia ndani ya Kanda ili kuendana na muda wa maelekezo ya Viongozi wa juu wa Mahakama.

Mahakama zilizokaguliwa kwanzia tarehe 16 hadi 20 mwezi 03, 2026 ni Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mahakama ya Wilaya Kigoma, Kasulu, Kibondo, Uvinza, Buhigwe, Kakonko na Gereza la Kilimo Kwitanga.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma , Mhe. John  Nkwabi akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kakonko alipoanzia ziara yake ya ukaguzi wa Mahakama za Wilaya hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigoma, Mhe. Eva  Mushi akitoa ufafanuzi wa moja ya mambo aliyokuwa akiulizwa na
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, alipokuwa akikaguliwa hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi-Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo akifanya utambulisho wa watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma kwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi (hayupo katika picha) wakati wa ukaguzi wa Mahakama hiyo.

Ukaguzi ukiendelea.....

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na ni Maofisa Waandamizi wa Magereza (wa pili na wa tatu kutoka kulia na wa tatu kushoto), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma,  Mhe. Fadhili Mbelwa (wa pili kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya  Kigoma, Bw. Filbert Matotay mara baaada ya ukaguzi wa Gereza la Kilimo Kwitanga.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma,  Mhe. Fadhili Mbelwa (wa pili kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya  Kigoma, Bw. Filbert Matotay  (wa pili kulia)Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kakonko, Mhe. Ambikile Kyamba (wa kwanza kushoto), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Kakonko (wa kwanza kulia) na waliosimama ni sehemu ya watumishi wa Mahakama hiyo mara baaada ya ukaguzi.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi  (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama hiyo ya Wilaya Kasulu (waliosimama) mara baada ya ukaguzi. Wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,  Mhe. Fadhili Mbelwa, wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya  Kigoma, Bw. Filbert Matotay, wa pili kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Kasulu, Mhe. Imani Batenzi, na wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya wilaya  Kasulu.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya-Uvinza. Wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya  Kigoma, Bw. Filbert Matotay, wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Mhe. Misana Majula  na wa kwanza kulia ni Afisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Bw. Tumaini Panga.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)

 

 

 

 

 

 

Jumatatu, 23 Machi 2026

JAJI MFAWIDHI GEITA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI WA MAHAKAMA ZA WILAYA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, amefanya ziara ya ukaguzi katika Mahakama za Wilaya za Bukombe, Mbogwe na Nyang’hwale, kwa lengo la kujionea hali halisi ya uendeshaji wa mashauri pamoja na nidhamu ya Watumishi.

Katika ziara hiyo, Jaji Mhina aliwapongeza Watumishi wa Mahakama hizo kwa kutekeleza maelekezo ya kuhakikisha kasi ya usikilizaji wa mashauri kwa mwaka 2026 inaongezeka.

Aliwasisitiza kuwa wahakikishe wanavuka mwaka 2026 bila kuwa na mashauri kwa Mahakama za Mwanzo kama walivyofanya mwaka 2025 kwa kumaliza mwaka wakiwa wamemaliza mashauri yote yaliyokuwa yamefunguliwa. Aidha, alisifu hatua ya kutokuwepo kwa malalamiko ya ukiukwaji wa maadili katika usikilizaji wa mashauri.

Pamoja na pongezi hizo, Jaji Mhina alisisitiza umuhimu wa kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa viwanja pamoja na nyumba za Mahakama zisizotumika ili kuzuia uvamizi na upotevu wa mali za Taasisi. Aliwahimiza Viongozi na Watumishi kutafuta matumizi mbadala ya viwanja vilivyo wazi ili kuongeza tija na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Vilevile, aliwataka Viongozi wa Mahakama kuendelea kujadili masuala ya maadili katika vikao vya ndani ili kuimarisha utendaji kazi na kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza wakati wa uendeshaji wa mashauri.

Katika ziara hiyo, Jaji Mhina aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Fredrick Lukuna, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mhe. Cleofas Waane na Maofisa wengine.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Bi. Masalu Kisasila, aliwataka watumishi kuendelea kuzingatia taratibu za ununuzi wa Serikali kupitia mfumo wa kielektroniki wa ununuzi (NeST) ili kuhakikisha uwazi na ufanisi katika matumizi ya rasilimali za umma.

Jaji Mhina na wajumbe wake walitembelea pia mradi wa ujenzi wa jengo jipya la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe kwa lengo la kukagua maendeleo yake.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Jaji Mhina alisema kuwa jengo hilo linatarajiwa kuanza kutumika kabla ya Juni 2026. Alibainisha kuwa kwa sasa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe inafanya kazi katika mazingira finyu yasiyokidhi mahitaji, hali inayowaweka Watumishi katika mazingira magumu na hatarishi kiafya na kiutendaji.

Kwa sasa, ujenzi wa jengo hilo umefikia hatua ya mwisho ya umaliziaji, ukiwa katika hatua ya upakaji rangi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akisaini kitabu cha wageni katika Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe, Mhe. Mashaka Msonogone, akitoa taarifa ya usikilizaji wa mashauri na ikama ya Watumishi Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.

Mtendaji wa Mahakama Geita akisisitiza Watumishi kufuata taratibu za ununuzi kupitia Mfumo nunuzi (NeST) ili kuongeza uwazi na ufasi kwa rasilimali za umma.

Hakamu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bukombe, Mhe. Zawald Nyekelela, akitoa taarifa ya mashauri Mahakama ya Wilaya ya Bukombe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Kevin Mhina, akijadiliana na Mtendaji wa Mahakama Geita, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbogwe namna ya kuweka uzio kwenye jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.

    Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.