Jumatano, 18 Februari 2026

TANZIA: HAKIMU MAHAKAMA YA MWANZO MIKESE AFARIKI DUNIA


Mhe. Asajile Joshua Mhando enzi za uhai wake.

Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen M. Magoiga, anasikitika kutangaza kifo cha Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese, Mhe. Asajile Joshua Mhando, aliyefariki Dunia tarehe 17 Februari, 2026 saa 7.00 mchana katika Hospitali ya Platnum mjini Morogoro alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kujisikia vibaya akiwa kazini.

Taratibu za mazishi zinaendelea kuratibiwa, na mara baada ya kukamilika zitatolewa.

Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro unatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na watumishi wote kwa msiba huu mzito.

Bwana alitoa, Bwana ametwaa jina lake lihimidiwe.

 

Jumatatu, 16 Februari 2026

JAJI MFAWIDHI DAR ES SALAAM AONGOZA ZIARA YA UTOAJI MSAADA KWA WANAFUNZI WENYE UHITAJI PUGU

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi jana tarehe 15 Februari, 2026 aliwaongoza watumishi wanawake wa Kanda hiyo kutoa msaada wa vifaa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum wa Shule ya Sekondari Pugu iliyoko jijini Dar es Salaam.

Akizungumza akiwa ofisini kwa Mkuu wa Shule ya Sekondari Pugu, Mhe. Maghimbi alieleza dhumuni la wao kufika shuleni hapo kuwa ni matokeo ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika mwaka jana 2025 na wao kama wanawake watumishi wa Mahakama Kanda ya Dar es salaam walikuwa na vitu ambavyo wao waliwiwa kuvitoa kwa wanafunzi hao lakini baada ya kuvitoa waliomba wapewe mahitaji ya msingi yanayohitajika kwa wanafunzi hao.

Jaji Maghimbi alisema baada ya kupata mahitaji hayo, watumishi wanawake wa Mahakama Kanda ya Dar es Salaam walichanga pesa ili kufanikisha upatikanaji wa vifaa hivyo na pia waliwashirikisha baadhi ya wanaume ambao waliguswa nao walichangia na hivyo kuweza kupatikana kwa mahitaji yote yaliyohitajika.

Aliongeza kuwa, kama kinamama watumishi wa Mahakama Kanda ya Dar es salaam wameomba mahusiano ya karibu na shule hiyo na chochote kitakachotokea wameomba kuwasiliana ili kwa kile watakachoweza kusaidia wasaidie. 

Akizungumzia kuhusu taarifa ya Mwalimu Msuya, Mhe. Maghimbi alisema siku zote yeye amekuwa akifikiri kuwa ana msongo wa kazi anayoifanya lakini alipomsikiliza Mwalimu Msuya na kazi ya kuhudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum, alikiri kwamba amepata nguvu mpya ya kufanya kazi na ameona kazi yake haina msongo kama ilivyo ya walimu hao, “kama unafikiri una tatizo fikiri tena,” alisema Mhe. Maghimbi kwa msisitizo. 

Aidha, akizungumza na wanafunzi wenye mahitaji maalum, Jaji Maghimbi aliwaeleza dhumuni la safari hiyo na kusema kwamba baada ya kutembelea kwa mara ya kwanza waliona kwamba wanatakiwa kufanya nacho kazi kwa ukaribu kutokana na mioyo yao na wala sio mfumo wa kazi yao. 

Aidha, aliwapongeza wanafunzi hao kwa matokeo mazuri katika mitihani yao na kuwaambia kuwa wao wameonesha kuwa chochote kinawezekana kwa sababu wanao uwezo wa kufanya vitu, kwakuwa uwezo wa kufikiria na kuelewa kile kinachofanyika na kuwa makini na kuwasihi kuwa na moyo huo pasipo kuteteleka. 

Akizungumzia kuhusu Mchepuo mpya ulioanzishwa shuleni hapo wa Sanaa kwa Masomo ya Historia, Lugha ya Kiingereza na Jiografia, Mhe. Maghimbi aliwatia moyo kuwa, hayo sio masomo wa wanawake kama wanavyofikiria bali ni masomo yanasomwa na wanaume pia.

Aliongeza kuwa, kutokana na kuanzishwa kwa mchepuo huo kuna uwezekano mkubwa wa kuwapata Wanasheria, Majaji na Mahakimu na hivyo Mhe. Maghimbi ametoa mwaliko maalum kwa Wanafunzi wa masomo hayo kutembelea Mahakama na kuona shughuli za kimahakama zinavyoendeshwa.

Kabla ya kukabidhi vifaa hivyo, Jaji Maghimbi alipata wasaa wa kupata historia fupi ya Shule hiyo kutoka kwa Makamu Mkuu wa Shule Taaluma, Mwalimu Juma Msuya ambapo alisema shule hiyo ilianzishwa mwaka 1948 ikiitwa Mtakatifu Francis ikiwa chini ya Kanisa Katoliki na kwamba baada ya kupata uhuru ilibinafsishwa na kuitwa Pugu na ilianza na jumla ya Wanafunzi nane (8) na mpaka sasa shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 1000 wa Kidato cha Kwanza mpaka cha Sita.

Mwalimu Msuya alisema kati ya wanafunzi hao wapo Watoto wenye mahitaji maalum kuanzia mwaka 1990 Serikali ilipoingia Mkataba wa Elimu Jumuishi ndipo shule hiyo ilitakiwa kupokea Watoto wenye mahitaji maalum haswa wale wa viungo ingawa kwa sasa wanachukua mchanganyiko wale wenye uziwi hafifu, mgongo wazi hasa wale wenye vichwa vikubwa.

Mwalimu huyo aliongeza kuwa, mwanzo Watoto hao walikuwa hawafanyi vizuri darasani lakini kwa bahati nzuri Serikali imeajiri Walimu wenye elimu maalum ambao wamepambana mpaka sasa wamefanikiwa kufuta daraja sifuri (division zero) na hata daraja la nne (division four). Matokeo ya juzi kulikuwa na Watoto 24 lakini hakuna aliyetoka daraja la tatu wala la nne.

“Watoto utakapowaona na ukiangalia na mafanikio wanayoyafanya ndipo utakapoamini ‘disability is not inability’ kwamba kutokana na ulemavu alionao basi anashindwa kila kitu hapana ni pale wanapowezeshwa basi na wenyewe wanaweza,” alieleza Mwalimu Msuya.

Mwalimu huyo alisema kuwa, kuna baadhi ya Wanafunzi hao hawawezi kuandika hivyo wanapata usaidizi wa notisi na ndio maana wameomba mashine za kuchapia na kurudufu. Na kuna baadhi wanatumia kompyuta ambazo kuna baadhi wamepatiwa na Serikali.

Akizungumza wakati wa kutoa maoni na maombi ya mahitaji mengine Mwanafunzi aliyejulikana kwa jina maarufu Bangimoto alisema anachukizwa na tabia ya baadhi ya watu wenye ulemavu kukaa barabarani na kuomba badala ya kujishughulisha na kupata kipato halali.

Mwanafunzi huyo aliongea kwa uchungu na kuonyesha namna gani walemavu wanachukuliwa na jamii kutokana na wao mwenyewe kuubeba udhaifu.

Vitu vilivyokabidhiwa katika ziara hiyo ni pamoja na mashine mbili za kisasa cha kuchapa zenye skana na kurudufu, karatasi katoni  40, wino sita (6), flashi za hizo mashine, mashuka tisa, Madaftari (Counter books) seti mbili, ‘diapers’ katoni  mbili, sabuni za unga, kipande na za kuogea, mafuta kwa ajili ya watu wenye changamoto ya Ngozi (albino) na vitu vingine vingi pamoja na vinywaji baridi ambavyo vimegharimu jumla ya fedha za Kitanzania 5,564,000/=.

Katika ziara hiyo ya Jaji Mfawidhi, Mhe. Maghimbi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Ubungo, Mhe. Tumsifu Barnabas na Kigamboni Mhe. Mwanakombo Athuman, Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Lucy Tuikailize, Msaidizi wa Kumbukumbu, Mwandishi Mwendesha Ofisi pamoja na Madereva. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akikabidhi vifaa vya Shule kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum wa Shule ya Sekondari Pugu walipotembelea shule hiyo hivi karibu kwa lengo la kutoa msaada kwa wanafunzi hao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi  akisaini kitabu cha wageni katika Ofisi ya Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Pugu.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo (aliyevaa fulana ya bluu) akitoa utambulisho wa wageni waliongozana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi walipotembelea Shule ya Sekondari Pugu kwa ajili ya kutoa msaada kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo (kushoto), Makamu Mkuu wa Shule Utawala (kulia), Mwalimu Ndimwangwa Nzota.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi  (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Walimu wa Shule ya Sekondari Pugu na Watumishi wanawake wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

'USULUHISHI NI SUALA LINALOHITAJI UVUMILIVU NA USIKILIZAJI WA UMAKINI'

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma ametoa rai kwa Wasuluhishi nchini kuwa wavumilivu na kusikiliza kwa makini wakati wanapofanya usuluhishi.

Mhe. Maruma aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tatu ya Upatanishi kwa Mahakimu na Wasajili wa Kanda ya Dar es Salaam yaliyofanyika kuanzia tarehe 11 hadi 13, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Temeke.

Jaji Maruma alisema, endapo Msuluhishi ana haraka, hana uvumilivu na hana usikivu hawezi kufanya usuluhishi na kwamba kama Msuluhishi akiwa hana usikivu na uvumilivu hata wale anaowasuluhisha hawawezi kumuamini, wadaawa wakimuangalia msuluhishi wanajua tu kwamba anawajali na kuwasikiliza ama la.

Ameongeza kuwa, uvumilivu na utulivu unasababisha usuluhishi, hivyo kuwataka kuwa wavumilivu hata kama wadaawa watawashambulia kwa maneno makali wao wawe chanya na wavumilie hatua hiyo itasababisha wadaawa kurudi kwenye mstari, hivyo usuluhishi kuendelea na kufanikiwa.

Awali akifungua mafunzo hayo, Mhe. Maruma alieleza kuwa, mafunzo hayo ni mwendelezo wa juhudi za Mahakama katika kuwajengea uwezo watumishi wake ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Jaji Maruma alisema mafunzo hayo, yanafanyika wakati muafaka na muhimu sana wakati Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inahimiza usuluhishi kama nyenzo  muhimu ya msingi  mkuu katika kuleta amani, umoja na utulivu  katika Taifa letu.

“Hii inaendana na mikakati ya Mahakama  katika kukuza matumizi ya usuluhishi ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo  kama inavyosisitizwa  katika ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisisitiza.

Aidha Mhe. Maruma afafanua kwamba Mahakama zinaendelea kukabiliwa na ongezeko la mashauri ambayo mengi kati yake yanaweza kutatuliwa kwa haraka, kwa gharama nafuu na kwa maridhiano bila kupita mchakato mrefu wa mashauri ya shauri la kawaida hivyo kuokoa gharama na muda ambao utatumika katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Alisema kuwa, upatanishi wa Mahakama umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuwezesha migogoro kumalizika kwa haraka na kwa sasa ongezeko la upatanishi limezidi asilimia 50 tofauti na hali ilivyokuwa miaka minne nyuma.

“Hali hii inatupa matumaini na chachu ya kuendelea kuwajengea uwezo Mahakimu na wadau wa usuluhishi ili kuongeza ufanisi katika kutatua migogoro kupitia upatanishi na kufika malengo yaliyopo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ya kutumia njia hii katika kuleta  amani na utulivu katika jamii zetu,” alisema Jaji Maruma.

Aliongeza kwamba, mafunzo hayo ni maandalizi ya Wiki ya Usuluhishi ambayo imepangwa kufanyika mwezi Machi nchini kote na kusema kuwa mafunzo hayo ni mwanzo wa mafunzo ambayo yataendelea kutolewa kwa Majaji, Mahakimu na Wadau ili kujenga uwezo wa ufanisi wa kutekeleza njia ya upatanishi katika kuharakisha upatikanaji wa haki.

Kadhalika alisema kwamba, ushiriki wa Majaji, Mahakimu, Wasajili na wadau wa Taasisi nyingine unaonesha kuwa, usuluhishi si jukumu la mtu mmoja bali ni juhudi ya pamoja ya taasisi zote zinazohusika na utoaji haki. Majaji na Mahakimu ingawa si Wasuluhishi katika mashauri yao, ni wasimamizi na walezi wa mchakato wa usuluhishi, hivyo ni muhimu kuwa na uelewa wa kina wa msingi, taratibu na falsafa ya usuluhishi.

Naye Naibu Msajili ya Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi Mhe.Augustina Mmbando alisema, Usuluhishi huimarisha  upatikanaji wa haki mapema ipasavyo, kwa gharama nafuu na kwa kuzingatia mahusiano ya kijamii na kibiashara.

Mhe. Mmbando alisema usuluhishi sio mbadala wa Mahakama bali ni nyenzo inayosaidia Mahakama kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na kwa mtazamo unaomjali binadamu.

Akizungumzia kuhusu miongoni mwa Wadau waliohudhuria mafunzo hayo ambao ni Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Mhe. Mmbando alisema uwepo wa TIRA katika mafunzo hayo una umuhimu wa pekee kwa kuwa Sekta ya Bima ni miongoni mwa sekta zinazozalisha migogoro mingi ya kibiashara na kimikataba ambayo kwa asili yake inafaa kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi.

Aliongeza kuwa, ushirikiano kati ya Mahakama na Taasisi za Udhibiti kama TIRA ni nguzo muhimu katika kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haraka, haki na kwa namna inayohifadhi mahusiano na kuimarisha imani ya wadau katika mfumo wa haki.

Naye Mwezeshaji katika mafunzo hayo Mhe. Mhangwa Yunge alisema usuluhishi ni mzuri kwakuwa unaokoa muda na pia Wadaawa wanabaki na amani na kuongeza kuwa sio kila mgogoro unaweza kusuluhishwa bali kuna migogoro mingine wahusika wanakuwa hawako tayari kusuluhishwa.

Mafunzo hayo yaliwezeshwa na Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Angela Bahati na Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke, Mhe. Mhangwa Yunge.

Mafunzo hayo yalihudhuriwa na Naibu wasajili, Mahakimu, Wadau na Mtendaji wa Mahakamu Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa.

 Jaji  Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akifundisha mada wakati wa Mafunzo yaliyotolewa hivi karibuni kwa Wasuluhishi wa Mahakama.


Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo kwa Wasuluhishi wa Mahakama, Mhe. Mhangwa Yunge akiwaongoza washiriki wa mafunzo hayo kuimba wimbo uliotungwa wakati wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi na Mwezeshaji wa Mafunzo (kulia), Mhe. Angela Bahati Salema na Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Mhangwa Yunge wakisikiliza michango iliyokuwa ikitolewa na washiriki wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha usuluhishi na mwezeshaji wa mafunzo, Mhe. Angela Bahati Salema (kulia) akipokea cheti katika hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo ya Upatanishi, Mhe. Mhangwa Yunge akipokea cheti katika hafla ya kufunga mafunzo hayo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbado  akipokea cha ushiriki wa mafunzo katika hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 


 

MAHAKAMA KITUO CHA USULUHISHI YAENDESHA MAFUNZO YA UPATANISHI KWA MAHAKIMU, NAIBU WASAJILI

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], hivi karibuni kiliendesha mafunzo ya siku tatu yanayohusu ya upataniishi wa Mahakama ili kuimarisha uwezo wa kutumia njia ya upatanishi ambayo ni rafiki katika utatuzi wa migogoro.

Mafunzo hayo ya siku tatu yaliyoanza tarehe 11 Februari, 2026, yakiwaleta pamoja Mahakimu wa ngazi zote pamoja na Naibu Wasajili kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Divisheni, yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma.

Akizunzungumza kwenye ufunguzi huo, Mhe. Maruma alieleza kuwa mafunzo hayo yamefanyika katika wakati muafaka na muhimu wakati dira ya 2050 inahimiza usuluhishi kama nyenzo muhimu ya msingi mkuu katika kuleta amani, umoja na utulivu katika taifa letu.

‘Hii inaendana na mikakati ya Mahakama katika kukuza matumizi ya usuluhishi ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo kama inavyosistizwa katika ibara ya 107A (2) (d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,’ alisema.  

Jaji Mfawidhi alibainisha kuwa mafunzo hayo pia ni moja ya maandalizi ya Wiki ya Usuliuhishi ambayo imepangwa kufanyika mwezi Machi 2026 nchini kote, hivyo, ni mwanzo wa mafunzo ambayo yataendelewa kutolewa kwa Majaji, Mahakimu na Wadau ili kujenga uwezo wa ufanisi wa kutekeleza njia hiyo ya upatanishi katika kuharakisha upatikanaji wa haki.

Mhe. Maruma alibainisha kuwa Mahakama zinaendelea kukabiliwa na ongezeko la mashauri, ambayo mengi kati yake yanaweza kutatuliwa kwa haraka, kwa gharama nafuu, na kwa maridhiano, bila kupitia mchakato mrefu wa mashauri, hivyo kuokoa gharama na muda ambao utatumika katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Alieleza kuwa upatanishi wa Mahakama umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuwezesha migogoro kumalizika kwa haraka na kila mmoja ni mashuhuda wa ongozeko la migogoro inayomalizika katika hatua ya upatanishi ambayo kwa sasa inazidi asilimia 50, tofauti na hali ilivyokuwa miaka minne nyuma.

Hali hii inatupa matumaini na chachu ya kuendelea kuwajengea uwezo Mahakimu na Wadau wa usuluhishi ili kuongeza ufanisi katika kutatua migororo kupitia upatanishi na kufikia malengo yaliyopo katika dira ya 2050 ya kutumia njia hii katika kuleta amani na utulivi katika jamii zetu pamoja na kuchangia katika uchumi endelevu,’ alisema.    

Jaji Mfawidhi alieleza pia kuwa upatanishi unaofanyika nje na ndani ya Mahakama hauondoi mamlaka ya Mahakama, bali unaikamilisha na kusaidia upatikanaji wa haki, kuondoa mrundikano wa mashauri, kuokoa muda na rasilimali, kulinda mahusiano ya kijamii na kibiashara, na kuwapa wahusika nafasi ya kushiriki kikamilifu katika kupata suluhu ya migogoro.

Alisema kuwa mafunzo hayo, siyo ya kiutaratibu pekee, bali ni uwekezaji katika kujenga uwezo, maadili, na taaluma ya wapatanishi wa Mahakama na wadau wa usuluhishi.  

Mhe. Maruma alitumia fursa hiyo kutoa shukrani za dhati kwa chuo cha IJA kwa kubali ombi lao la kushirikiana nao katika kuendesha mafunzo hayo ambayo ni muendelezo wa juhudi za Mahakama katika kuwajengea uwezo wa watumishi wake ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Natambua kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mafunzo ya upatanishi tayari yameshafanyika kwa Majaji na Mahakimu zaidi ya mia moja na baadhi yao ndio wamekuwa wakufunzi wa mafunzo haya ambayo ni endelevu,’ alisema.

Jaji Mfawidhi alitumia fursa hiyo pia kuwashukuru Wadau muhimu kwa kushirikiana na Kituo katika kuwezesha mafunzo hayo bila kusita pale walipowafikia.

Alieleza kuwa hatua hiyo inaashiria mwanzo wa ushirikiano ambao utakuwa endelevu na kutaleta faida kubwa katika kukuza, kuongeza ufanisi na kuhamasisha si tu matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro bali hata katika kuibua changamoto zinazokwamisha na kuzifanyia kazi kwa pamoja.

Awali, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbando, alieleza kuwa ushiriki wa Majaji, Mahakimu, Naibu Wasajili na Wadau wa Taasisi nyingine unaonesha kuwa usuluhishi si jukumu la mtu mmoja, bali ni juhudi ya pamoja zinazohusika na utoaji haki.

‘Majaji na Mahakimu, ingawa si wasuluhishi katika mashauri yao, ni wasimamizi na walezi wa mchakato wa usuluhishi, na hivyo ni muhimu kuwa na uelewa wa kina wa misingi, taratibu na falsafa ya mediation.

Aidha, Mhe. Mmbando alielezea kutambua kwa heshima uwepo wa Mratibu wa Mafunzo kutoka IJA, ambaye mchango wake ni muhimu katika kujenga uwezo wa Mahakama kupitia mafunzo endelevu na ya vitendo.

Alieleza pia kuwa uwepo wa TIRA katika mafunzo hayo una umuhimu wa pekee kwani bima ni miongoni mwa sekta zinazozalisha migogoro mingi ya kibiashara na kimkataba, ambayo kwa asili yake inafaa kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi.

‘Ushirikiano kati ya Mahakama na taasisi za udhibiti kama TIRA ni nguzo muhimu katika kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haraka, haki, na kwa namna inayohifadhi mahusiano na kuimarisha imani ya wadau katika mfumo wa haki,’ alisema.

Picha ya Meza Kuu, katikati ni Mhe. Zahra Maruma, kulia ni Mhe. Angela Bahati na kushoto ni Bi. Magreth Magumi.

Mgeni Rasmi akifungua mafunzo.

Meza Kuu na Wakufunzi wa usuluhishi.

Meza Kuu na Naibu Wasajili.

Meza Kuu na Mahakimu wa ngazi zote [juu na chini].


Washiriki wote wakiwa kwenye mafunzo [juu na chini].


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma







 

 

 

Ijumaa, 13 Februari 2026

TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA AFARIKI DUNIA


TANZIA

Bi. Happiness Amos Majule enzi za uhai wake.

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake Bi. Happiness Amos Majule, aliyekuwa akifanya kazi katika kituo cha Mahakama ya Wilaya ya Meatu.

Kifo hicho kilichotokea mnamo tarehe 09 Februari, 2026 siku ya Jumatatu katika hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza alipokuwa amelazwa kwa matibabu.

Marehemu Bi.happiness A. Majule alizaliwa tarehe 11 April, 1969 na aliajiriwa na Mahakama ya Tanzania tarehe 04 Juni 1992 katika nafasi ya Msaidizi wa Ofisi.

Hadi umauti unamkuta, Bi happiness alikuwa akihudumu katika Mahakama ya Mwanzo Kisesa.

Aidha, Bi. Happyness Amos Majule anatarajiwa kupumzishwa kwenye nyumba yake ya milele mnamo tarehe 13 Februari, 2026 huko mkoani Singida Wilaya ya Iramba Kijiji cha Ulemo.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA JINA LA BWANA LIHIMIDIWE.

Alhamisi, 12 Februari 2026

MTENDAJI MKUU AMETOA WITO KWA MAAFISA USAFIRIRSHAJI KUONGEZA UMAKINI WANAPOTEKELEZA MAJUKUMU YAO

Na. HABIBA MBARUKU & INNOCENT KANSHA - Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka madereva kuongeza umakini wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao ili kupunguza ajali zisizokuwa za lazima pamoja na kupunguza uharibifu wa vyombo vya usafiri na kulinda afya za wateja wao.

Pro. Ole Gabriel ameyasema hayo wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Aidha, Prof. Ole Gabriel, amesema mafunzo hayo maalum kwa madereva wote wa Mahakama, yamelenga kuimarisha huduma kwa mteja, kuzingatia maadili ya kazi na kuongeza usalama barabarani, mafunzo hayo yaliyoandaliwa chini ya mada ya Huduma kwa Mteja kwa kada ya madereva au maafisa usafirishaji yamesisitiza nafasi muhimu ya dereva katika mnyororo wa huduma za utoaji haki ndani ya taasisi, huku akibainisha kuwa kila mtumishi ana mchango wa moja kwa moja katika taswira na ufanisi wa Mahakama.

“Kuna mambo mengi yanachangia utulivu wa mawazo na kufanya kazi kwa timu kama vile kupata stahiki bora ni msingi wa mafanikio katika taasisi yoyote, uzembe wa kada moja unaweza kuathiri kada nyingine, hivyo ni muhimu kila mmoja kutimiza wajibu wake kwa umakini na weledi,” amesisitiza Prof. Ole Gabriel.

Akizungumzia dhana ya mteja, Mtendaji Mkuu huyo amefafanua kuwa, mteja ni yeyote anayenufaika na huduma inayotolewa, akiwemo kiongozi anayeendeshwa, watumishi wa Mahakama pamoja na wadau wengine barabarani. Amesisitiza kuwa utoaji wa huduma haupimwi tu kwa kutekeleza jukumu, bali kwa namna huduma hiyo inavyotolewa.

Vilevile katika mada ya matarajio ya mteja, madereva wamekumbushwa kuzingatia mambo kumi muhimu ikiwemo usahihi na umahiri katika kazi, usafi wa gari na muonekano binafsi, kutunza muda, usalama, utulivu barabarani na kutunza siri za kikazi na binafsi za viongozi wanaowahudumia.

Kadhalika, Prof. Ole Gabriel ameainisha sehemu ya changamoto zinazowakabili maafisa usafirishaji wa Mahakama nchi nzima, zikiwemo usimamizi wa bajeti binafsi, msongo wa mawazo ya kifamilia, bajeti finyu za matengenezo ya magari na wakati mwingine kukosa heshima kutoka kwa baadhi ya viongozi. Hata hivyo, amewataka madereva hao kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi licha ya changamoto hizo.

Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa, katika kuimarisha maadili ya kazi, Itifaki ya Dereva Bora, inajumuisha mavazi ya heshima, kuepuka kupiga honi ili kumuita kiongozi badala yake dereva anaweza kuwasiliana na kiongozi  wake kwa  njia ya ujumbe mfupi wa maandishi au kumpigia simu baada ya dakika kumi ikiwa ujumbe hautajibiwa, kuweka simu katika hali ya ukimya wanapoendesha, kutoingia katika mabishano barabarani, kufika mapema kabla ya muda wa safari walau dakika kumi kabla ya safari na kuepuka matumizi ya pombekabla ya safari na wakati wa safari.

Akizungumza kuhusu usalama, Mtendaji Mkuu amewakumbusha kuwa dereva anakabidhiwa chombo cha thamani kubwa pamoja na uhai wa abiria na uhai wake mwenyewe, hivyo ni lazima kuhakikisha gari liko katika hali nzuri kabla ya safari, dereva asikubali kuendesha gari bovu lisilokaguliwa kabla ya safari, ahakikishe yuko kwenye afya njema ili kuepuka uzembe unaoweza kusababisha ajali na kuleta hasara kubwa kwa taasisi.

Mafunzo hayo pia yaligusia tabia tano za kuepuka ili kutoleta usumbufu kwa kiongozi, zikiwemo kuanza safari bila kukagua gari, kubishana na kiongozi, uzembe katika mapokezi, kutoa taarifa za siri na kufokeana na wadau wengine wa barabara.

Aidha, Prof. Gabriel amesisitiza kuwa, mteja ndiye sababu ya ajira ya mtumishi, hivyo madereva wanapaswa kushirikiana kwa pamoja, kuepuka majungu na kuweka kipaumbele katika utunzaji wa magari pamoja na maisha ya wanaowahudumia.

Mafunzo hayo ni juhudi za Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utendaji kazi na kuhakikisha huduma zinazotolewa kwa umma zinazingatia viwango vya juu vya taaluma na maadili.

 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (katika mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Maafisa Usafirisha wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya mafunzo elekezi kwa huduma kwa mteja.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (katika mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Maafisa Usafirisha wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya mafunzo elekezi kwa huduma kwa mteja.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiteta jambo na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick (kushoto) wakati wa mafunzo hayo elekezi kwa Maafisa Usafirishaji (hawapo pichani) 

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia mafunzo hayo.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia mafunzo hayo.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

 

 

 

MAAFISA USAFIRISHAJI WA MAHAKAMA WATAKIWA KUZINGATIA TAHADHARI, USALAMA WA VYOMBO VYA MOTO

Na. Halima Mnete & James Busanya - Mahakama

Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania nchini wamehimizwa kuongeza umakini, nidhamu na kuzingatia kwa kina misingi ya udereva wa kujihami ili kupunguza ajali zinazotokea wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ya kimahakama.

Wito huo umetolewa leo tarehe 12 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodma katika kikao maalum kilichowakutanisha madereva hao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, kilicholenga kujadili masuala ya usalama barabarani, ustawi wa madereva pamoja na changamoto wanazokumbana nazo katika utendaji wa kazi zao za kila siku.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Kitengo cha Usafirishaji cha Mahakama ya Tanzania , Bw. Shedrack Bambaganya, amesema kuwa, katika kipindi cha hivi karibuni kumekuwepo na ajali kadhaa zilizowakumba madereva wa Mahakama wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hali iliyosababisha madhara ya kibinadamu pamoja na uharibifu mkubwa wa magari ya Taasisi.

Ameeleza kuwa, ajali hizo zimeongeza gharama kubwa kwa Mahakama, zikiwemo gharama za matengenezo ya magari, ucheleweshaji wa ratiba za shughuli za kimahakama na hatari ya kupoteza maisha ya watumishi pamoja na wananchi wanaohudumiwa.

“Haya ni matukio ya bahati mbaya, lakini ni wajibu wetu kuongeza tahadhari zaidi barabarani. Tunapaswa kuzingatia kanuni za usalama, kutumia udereva kwa kujihami na kuwa makini muda wote tunapokuwa barabarani. Usalama wa maisha ya wateja wetu na watumiaji wengine wa barabara ni kipaumbele,” amesisitiza Bw. Bambaganya.

Aidha, ameongeza kuwa, zipo changamoto ambazo madereva hukutana nazo, zikiwemo ajali zinazosababishwa na uzembe au mwendo kasi wa madereva wa Taasisi nyingine na watumiaji wengine wa barabara. Akitolea mfano; ajali iliyotokea Nzega mkoani Tabora katika msafara wa Jaji Kiongozi, alisema kuwa msafara huo ulikuwa katika upande sahihi wa barabara, lakini dereva wa Taasisi nyingine ya Umma aliendesha kwa mwendo kasi bila kuchukua tahadhari, hali iliyomfanya ashindwe kudhibiti gari na kusababisha ajali.

Aidha, Bw. Bambaganya amefafanua kuwa, kutokana na umakini, uzoefu na ustadi wa dereva wa Jaji Kiongozi, aliweza kulidhibiti gari kwa haraka na kuokoa maisha ya waliokuwamo ndani ya gari hilo, licha ya gari kuharibika vibaya na kuhitaji matengenezo ya gharama kubwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick aliwashukuru madereva kwa kuitikia wito wa kikao hicho na kutoa maoni yao kwa uwazi na pia kuwasilisha changamoto mbalimbali wanazokutana nazo kazini. Mkurungenzi huyo ameahidi kuwa, uongozi wa Mahakama unatambua mchango mkubwa wa madereva katika kuhakikisha shughuli za kimahakama zinafanyika kwa wakati na kwa usalama.

Vilevile, miongoni mwa changamoto zilizotajwa na madereva ni suala la kupanda vyeo kwa waliopo katika madaraja ya chini, pamoja na uhitaji wa mafunzo ya mara kwa mara ya usalama barabarani. Bi. Beatrice aliahidi kuwa uongozi utayafanyia kazi masuala hayo kwa kushirikiana na kitengo cha ndani cha malalamiko cha kuwahudumia watumishi (Judiciary Internal Customer Services) ili kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza motisha kwa madereva hao.

Kikao hicho kimetajwa kuwa hatua muhimu ya kuimarisha mawasiliano na ushirikiano kati ya uongozi na madereva kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuboresha usalama barabarani, kulinda rasilimali za Mahakama na kuhakikisha utekelezaji wa majukumu ya kimahakama unafanyika kwa ufanisi, uwajibikaji na weledi.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick akijibu baadhi ya hoja zilizowasilishwa na Maafisa Usafirishaji kwenye mafunzo elekezi yaliyoendeshwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani)

Mkuu wa Kitengo cha Usafirishaji cha Mahakama ya Tanzania Bw. Shedrack Bambaganya akifafanua jambo wakati wa mafunzo elekezi kwa Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.
Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.


Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya mafunzo hayo elekezi yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha)

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)