Alhamisi, 14 Mei 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJIDHATITI KUBORESHA HUDUMA YA UTOAJI HAKI MAPEMA IPASAVYO

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imetunga jumla ya kanuni mpya tano (5) na kufanyia marekebisho kanuni nane (8) na hivyo kufanya uwepo wa jumla ya kanuni 13 za uendeshaji wa mashauri, lengo likiwa ni kurahisisha mchakato wa usikilizaji mashauri ili haki iweze kupatikana mapema ipasavyo.

Hayo yamebainishwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, alipokuwa akiwasilisha Taarifa kuhusu Kazi za Kimahakama za mwaka 2025 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama lililofunguliwa jana tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Mhe. Nkya ametaja Kanuni hizo kuwa ni pamoja na The Primary Courts-Administration of Estates) (Amendment) Rules 2025 GN No.  428 published on 11th July, 2025, The Civil Procedure Code (Amendment of the First Schedule) Rules, 2025 GN No. 569 published on 12th September, 2025.

Nyingine ni Judicature and Application of Laws (Electronic Filing) (Amendment) Rules, 2025 GN No. 39 published on 17th October, 2025, Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Madiwani za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na.433 la tarehe 11 Julai, 2025, Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Wabunge za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na.431 la tarehe 11 Julai, 2025, Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na. 430 la tarehe 11 Julai, 2025.

Kanuni za Marekebisho ya Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Wabunge za Mwaka 2025, Tangazo la Serikali Na 610 la tarehe 17 Oktoba, 2025, The Judiciary Administration Regulations (The Judiciary Administration (Judiciary Flag) (Amendment) Regulations, 2025, GN 608/2025 na nyingine.

Akizungumzia kuhusu mafanikio ya Mahakama yaliyopatikana, Msajili Mkuu ameeleza kuwa kumekuwa na ongezeko la usikilizaji mashauri kwa asilimia tatu sambamba na kupungua kwa wastani wa mzigo wa kazi toka 227 hadi 222.

Kadhalika, Msajili Mkuu ameeleza kuwa, kumekuwa na kasi ya kupungua kwa wastani wa muda wa kumaliza shauri kutoka siku 78 hadi 66.

Kadhalika, amebainisha kwamba, Mahakama imefanikiwa kufikia malengo ya kiashiria cha kiwango cha mashauri ya mlundikano kwa asilimia tano na usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (lengo lilikuwa 18,500 - 62,041).

“Mafanikio mengine yaliyopatikana ni pamoja na kuanzishwa kwa Masjala ndogo tano za Mahakama Kuu, kuanzishwa kwa Vituo vya Mahakama ya Mwanzo 15,” amesema Mhe. Nkya.

Kwa upande wa kiwango cha ukaguzi wa Mahakama na Magereza, Mahakama imefanikiwa kwa asilimia 1.6 na 11.6 mtawalia na kusababisha kupungua kwa mahabusu na wafungwa gerezani, huku Mahakama za Mwanzo kukiwa hakuna mahabusu.

Kwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, Mhe. Nkya amebainisha kuwa, zilikaguliwa kwa 100.

“Kuhusu ushughulikiaji wa mrejesho ulikuwa asilimia 99.9 ambapo jumla ya mirejesho 3,144 kati ya 3,149 (ikiwepo mitano “5” iliyobaki mwaka 2024) ilishughulikiwa,” ameeleza.

Amebainisha kuwa, kati ya mirejesho hiyo ushughulikiaji wa malalamiko ulikuwa ni asilimia 99.8 ambapo jumla ya malalamiko 1,609 kati ya 1,611 yaliyokuwepo (yakiwepo matano “5” yaliyobaki mwaka 2024) yalishughulikiwa.

Jumatano, 13 Mei 2026

JAJI MKUU ATAKA CHANGAMOTO ZA WATUMISHI KUTATULIWA BILA VIKWAZO

·       Awataka watumishi wa Mahakama kuendelea kutekeleza Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, 2026

·       Ataka mashauri yasikilizwe mapema ipasavyo ili kuchangia ustawi na maendeleo ya Taifa

·       Asisitiza ushirikiano, amani na kuthaminiana kwa Watumishi

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama nchini, amewataka Viongozi wa Mhimili huo kuwa wanyenyekevu sambamba na kufungua milango kwa ajili ya kuwasikiliza Watumishi walio chini yao ili kutatua changamoto wanazokabiliana nazo bila vikwazo.

Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania ikiwa ni mara yake ya kwanza kuendesha Mkutano Mkuu wa Baraza hilo tangu ateuliwe kushika wadhifa wa Jaji Mkuu takribani mwaka mmoja uliopita.

“Kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unakuwa mtumishi wa wote, sisi Viongozi ni Watumishi wa watu, tuwe na tabia ya kufungua milango tuwasikilize walio chini yetu, tusifunge milango,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema Viongozi pia wanawategemea Watumishi walio chini yao ambapo ameeleza kuwa, kwa kadri Kiongozi anavyozidi kupanda kimadaraka ni kwa kiwango hicho hicho anazidi kuwa tegemezi kwa watu wengine, na kwamba kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unapaswa kuwa mnyenyekevu ili uwafikie wanaokutegemea na wao wakufikie ili ujue changamoto zao na mafanikio yao.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema kuwa, Viongozi wasiwazuie wajumbe wa Baraza kuzungumza yale yanayowasibu, badala yake wawaache huru kusema yale wanayokabiliana nayo katika utekelezaji wa majukumu yao ili kupata ufumbuzi wa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mahakama.

Ameongeza kuwa, hata Viongozi wanapotembelea Mahakama mikoani Viongozi wa Mahakama husika wanapaswa kuwaacha watumishi wazungumze na Viongozi ili wajue Mahakama imepiga hatua gani katika maendeleo, wajue changamoto  zilizopo ili tutatue changamoto hizo na kupiga hatua ili hatimaye vikao vya Baraza viwe vya furaha.

Aidha, Jaji Mkuu amewapongeza watumishi wa Mahakama wa Kada zote kwa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mhimili huo kwa ufanisi ipasavyo.

“Kwanza natambua mchango wenu, kila mmoja wetu katika utendaji wa Mahakama ya Tanzania, mmefanya kazi kubwa sana, miaka iliyopita na mimi tangu nimekuja kushirikiana na ninyi mmefanya kazi kubwa sana ya kutekeleza majukumu yenu na wakati fulani katika mazingira magumu mimi naelewa katika utumishi wangu mimi nimeanzia chini sana nikiwa Wakili wa Serikali Daraja la tatu, kwahiyo ninafahamu na wakati mwingine

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju amewakumbusha Viongozi na watumishi wote wa Mahakama kwa ujumla kuendelea na utekelezaji wa Kaulimbiu ya Siku ya Sheria Nchini ya mwaka huu 2026 isemayo; ‘Mchango wa Mahakama ya Tanzania katika Maendeleo na Ustawi na Maendeleo ya Taifa.’

“Mahakama ina mchango mkubwa sana, mnaweza kurejea hotuba yangu ya Siku ya Sheria, nimeeleza yote, hii haiwezi kuwa ni Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, hii tunaiishi mwaka huu wote wa 2026, kwahiyo tunapofanya kazi yatupasa tujue tuna mchango katika ustawi na maendeleo ya Taifa la Tanzania. Wajibu wetu Mahakama ni kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi ipasavyo na tunapaswa kuendelea kuwa wabunifu,” amesema Jaji Mkuu.

“Kwenye Kanda mtaangalia mnapopanga mashauri mjue kuna kitu tunafanya, kwahiyo mnatakiwa kuangalia ustawi na maendeleo ya Taifa, tunahusika hata sisi katika maendeleo kwa sababu amani ni msingi mkubwa unaoleta ustawi na maendeleo ya Taifa,” amesema Mhe. Masaju.

Ameeleza kuwa, kwa msingi huo ndio maana wa mfano kuna mashauri ya jinai, mashauri ya madai, mashauri ya uchaguzi na kila aina ya mashauri yanashughulikiwa na kumalizika watu wanapiga hatua mapema.

“Mpaka sasa kwa mfano yale mashauri ya uchaguzi yaliyofunguliwa, limebaki shauri moja tu, mengine yote yameshaisha, kuna mashauri ya kila aina ya mirathi, ya ndoa, ya uhujumu uchumi. Sisi kama Mahakama wajibu wetu ni upi? najua tunazo changamoto pengine hatupati ushirikiano mzuri sana lakini sisi hatuwezi kukata tamaa ndio wajibu wetu, tukiharibu tunawajibishwa sisi, sisi ndio tunaosemwa na tunapaswa tuendelee kuwa wabunifu katika maeneo yetu ya kazi kuhakikisha kwamba mchango wa Mahakama ya Tanzania katika ustawi na maendeleo ya Taifa unazidi kuimarika,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Amesema, tunaishi katika nchi inayozingatia Utawala wa Sheria, hivyo, Mahakama ina nafasi kuwa katika ustawi na maendeleo ya Taifa na kwa sababu ni muhimu mashauri yanapopangwa yapangwe kimkakati na hayatakiwi kucheleweshwa bila sababu za msingi, lakini pia inabidi kuwa ni mikakati ya kubaini mashauri yenye kero yanayoleta sintofahamu katika jamii yashughulikiwe.

“Uchumi ni Ardhi wala hata sio kitu kingine, kwahiyo tuna mikakati ya kumaliza haya mashauri ya Ardhi tangu mwaka jana tumekuwa na hiyo mikakati, na Mahakama Kuu wamefanya vizuri sana kwa sababu mashauri ya ardhi kwa Mahakamani yanaanzia Mahakama Kuu, yanakwenda Mahakama Rufaa mengine kwenye ‘originial jurisdiction’ tunafanya vizuri japo bado ni mengi kwa sababu migogoro inazalishwa mingi na sehemu fulani tumeshauri kwa mfano ukisoma Sheria ya Usajili wa Ardhi (Land Registration Act) kuna mtu pale anaitwa ‘The Registrar of Titles) ana mamlaka makubwa sana  mashauri mengine hata yasingekuwa yanakuja mahakamani yangekuwa yanaenda pale kama kuna migogoro wakishindwa kutatua upande ambao hauridhiki unakuja Mahakama ya Rufani,” ameeleza.

Kwa upande wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Masaju amesema kuna mashauri mengi ya jinai, hivyo wameweka mkakati wa kushughulikia mashauri hayo ambayo walianza kusikiliza katika Vikao vya Mahakama ya Rufani (COA Session) ya mwezi Februari ambapo walichanganya na mashauri ya mirathi ili watu wawe na amani kwenye familia zao na wengine wajue hatma yao.

“Majaji hawa wa Mahakama ya Rufani wamefanya kazi nyuma, mashauri mengi yameenda, kama wengine hawasema sisi wenyewe tujisemee, mimi nawapongeza sana Mahakama ya Rufani,” amesema Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Mwezi Aprili walipanga mashauri ya kazi na ndoa ambayo kikao chake kimekamilika tarehe 08 Mei, 2026 na wengine wanaendelea, jitihada hizo ni katika wajibu wa kutekeleza mchango wa Mahakama katika maendeleo na ustawi wa Taifa.

Kadhalika, amesema katika Vikao vinavyofanyika Juni na Agosti, 2026 mashauri ya ardhi yatashughulikiwa tena ili kuyapunguza. Ameeleza kuwa, katika vikao hivyo wataweka pia mashauri machache ya jinai na kabla ya Desemba pia watakuwa na mashauri ya jinai.

Amebainisha kuwa, ili Mahakama ifanikiwe inahitaji ushirikiano kutoka Mihimili mingine ili kutekeleza jukumu la utoaji haki kwa ufanisi ipasavyo.

Kwa upande wa Mahakama Kuu, Mhe. Masaju amesema, wamekamilisha vikao vya kusikiliza mashauri ya ardhi ikiwa ni mwendelezo wa zoezi ambalo lilianza mwaka jana, ambapo amesema kwa sasa hatatoa takwimu kwakuwa zinaandaliwa na Msajili wa Mahakama Kuu na zitatangazwa kwa wananchi kile ambacho Mahakama imefanya.

Amesema pia kulikuwa ni shida kubwa za mashauri ya baadhi ya waajiri kutowasilisha michango ya mafao ya watumishi wao katika mifuko ya hifadhi za jamii ambapo amesema wamefanya mabadiliko ya kanuni na kwamba katika usikilizaji wa mashauri hayo Majaji na Mahakimu wamefanya vizuri kwakuwa mashauri hayo mengi yameisha na yameisha kwa njia ya usuluhishi.

“Sisi Mahakama nia yetu ni kwamba wafanyakazi wapate stahili zao sio wanakatwa halafu mwisho wa siku hawapewi stahili zao,” ameeleza.

Kadhalika Jaji Mkuu amewataka watumishi wote wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, umoja na kuthaminiana katika utekelezaji wa majukumu.

 Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando akizungumza jambo wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama leo tarehe 13 Mei, 2026.


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Muu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 13 Mei, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama jijini Dodoma.

Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa pili kushoto) wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama nchini ulioanza leo tarehe 13 Mei, 2026. Mkutano huo unatarajiwa kuhitimishwa kesho tarehe 14 Mei, 2026.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija (wa pili kushoto), Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (wa kwanza kushoto) na Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, Mhe. Christina Mlilwo.


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Muu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 13 Mei, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama jijini Dodoma.

Wimbo wa Mshikamano Daima (Solidarity Forever) ukiimbwa na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasilisha taarifa ya Mahakama wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akiwasilisha taarifa wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma.

Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Sekretarieti ya Maandalizi ya Mkutano huo.

(Picha na Mary Gwera-Mahakama)

MAHAKAMA YAENDELEA KUIMARISHA UTOAJI HAKI

  • Yataja mafanikio ya utumishi, TEHAMA na Miradi ya Ujenzi
  • Mtendaji Mkuu aeleza mafanikio ya ajira, ustawi wa Watumishi

Na HALIMA MNETE- Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amesema kuwa Mahakama inaendelea kuimarisha utoaji wa huduma za haki nchini kupitia maboresho mbalimbali ya kiutumishi, matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) pamoja na utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa majengo katika maeneo tofauti ya nchini.

Prof. Ole Gabriel amesema hayo leo tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma wakati akiwasilisha taarifa ya mwaka wa fedha 2025/2026 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania 2026 unaofanyika katika ukumbi wa PSSSF Makole, chini ya uenyekiti wa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.

Akizungumza katika mkutano huo utakaohitimishwa kesho tarehe 14 Mei, 2026, Prof. Ole Gabriel amesema Mahakama imeendelea kutekeleza Mpango Mkakati wake wenye lengo la kuendeleza maboresho ya utoaji huduma, huku mafanikio yaliyopatikana yakitokana na juhudi za Watumishi wa Mahakama nchini kote.

Amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, Mahakama imefanikiwa kuajiri Watumishi wapya 1,121, wakiwemo Mahakimu 173, hatua ambayo imeongeza nguvu kazi katika utoaji wa huduma za haki nchini. Hata hivyo, amesema bado Mahakama inakabiliwa na upungufu wa Watumishi ambapo hadi Aprili 30, 2026 idadi ya watumishi waliopo ni 6,976 dhidi ya mahitaji ya watumishi 12,121.

“Tumekuwa na kikao kizuri na Viongozi wa TUGHE Mahakama, ambapo hoja nyingi zimejadiliwa na baadhi yake zimepatiwa ufumbuzi,” amesema Prof. Ole Gabriel.

Katika masuala ya ustawi wa watumishi, amesema Mahakama imetenga zaidi ya shilingi milioni 900 kwa ajili ya kuanzisha kifurushi maalum cha bima ya afya kwa Watumishi wake ili kusaidia huduma za ziada za matibabu.

Kuhusu miundombinu. Prof. Gabriel amesema Mahakama inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi, ikiwemo ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama Dodoma ambao umefikia asilimia 99.

Amesema pia Mahakama imeendelea kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama katika Mikoa mbalimbali, huku baadhi ya majengo mapya ya Mahakama Kuu yanayoitwa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tayari yakianza kutumika katika Mikoa mbalimbali.

Kwa upande wa TEHAMA, Prof. Ole Gabriel amesema Mahakama itaendelea kuimarisha mifumo mbalimbali pamoja na mfumo wa Mahakama Mtandao (Virtual Court) ili kuongeza ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa Wananchi.

Amesisitiza kuwa matumizi ya TEHAMA yanapaswa kuendelea kuwa sehemu ya utamaduni wa Mahakama ili kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia duniani.

Katika hitimisho lake, Prof. Ole Gabriel ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuipa Mahakama kipaumbele katika utoaji wa bajeti na kuwataka Watumishi kuendelea kushirikiana katika kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza Kuu la Wafanyakazi Mahakama ya Tanzania 2026. Picha chini ni sehemu ya wajumbe kutoka Masjala mbalimbali wanaohudhuria Mkutano huo.












Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.



 

Jumanne, 12 Mei 2026

JAJI SEHEL, MWENYEKITI KAMATI YA JAJI MKUU UFUATILIAJI NA TATHMINI AFANYA ZIARA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel hivi karibuni alifanya ziara ya kikazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe lengo likiwa ni kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa shughuli za Mahakama.

 

Mhe. Sehel ambaye pia ni na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) alianza ziara yake tarehe 07 Mei, 2026 ambapo alipokelewa na mwenyeji wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA pamoja na Viongozi na watumishi watumishi wa Mahakama Njombe.

 

Jaji Sehel alipata wasaa wa kuzungumza na watumishi wa Mahakama Njombe ambapo alisikiliza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo ikiwemo ukosefu wa huduma ya usafiri wa basi la Mahakama linaloweza kuwapeleka ofisini kutokana na umbali mkubwa wa kutoka maeneo wanayoishi mpaka mahali pa kazi.

 

Aidha, Mwenyekiti huyo alipata fursa ya kutembelea jengo la Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Njombe (IJC) ambalo lipo kwenye hatua za mwisho kwa asilimia 97 na baadhi ya viongozi na watumishi tayari wameanza kuhamia kwenye jengo hilo.

 

Katika ziara hiyo Mwenyekiti alifanya ukaguzi wa shughuli za kimahakama katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mahakama ya Wilaya ya Njombe na Makete pamoja na Mahakama ya Mwanzo Njombe.

 

 Vilevile, katika ziara hiyo Mhe. Sehel alipata fursa ya kuzungumza mambo mbalimbali ya TAWJA Njombe katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wake pamoja na kuhuisha uanachama  wa TAWJA na IAWJ.

 

 

Akiendelea na kikao hicho huku wanachama wengine wakishiriki kwa njia ya mkutano mtandao (Video Conference) walio nje ya Wilaya ya Njombe, Mhe. Sehel  alisisitiza mshikamano pamoja na kushirikiana kikamilifu katika shughuli za Chama hicho, Tawi la Njombe ikiwa ni pamoja na kujitolea katika majukumu mbalimbali bila kujali malipo pamoja na kutoa elimu na kuhudhuria mikutano ya ndani.

 

 

Mwenyekiti huyo wa TAWJA alisisitiza kuwa Chama hicho ni jukwaa linalowawezesha kung’ara kitaifa na kimataifa kwa kazi zinazofanyika, ambapo aliwatakia wanachama wa TAWJA Njombe majukumu mema ya ujenzi wa Taifa huku akisisitiza uadilifu, weledi na uwajibikaji kama ambavyo Kaulimbiu ya Mahakama inasema.

 

Mhe, Sehel pamoja na wanachama wa TAWJA Njombe walipata fursa ya kukata keki na kufungua champeni pamoja na Makamu Mwenyekiti Mhe. Victoria Nongwa kama ishara ya mwanzo mpya wa TAWJA mkoani Njombe.

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani  ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi mbele katikati) akizungumza na Watumishi wa Mahakama Njombe alipotembelea Masjala hiyo hivi karibuni. Kushoto ni  Jaji Mfawidhi wa  Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndono ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Victoria Nongwa na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge. Aliyesimama upande wa kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama.  

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Njombe mbele ya jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe wakati walipofanya ziara hivi karibuni. 


 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel akipatiwa maelezo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe (wa kwanza kushoto). Wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA akizungumza hivi karibuni na baadhi ya Wanachama wa Chama hicho wa mkoani Njombe.

Jaji Sehel akiwa katika maandalizi ya kukata keki maalum ikiwa ni ishara ya kuanza kwa Tawi mpya la TAWJA Mahakama Njombe.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa  TAWJA, Mhe.  Victoria Nongwa (kulia) akimpatia zawadi Jaji Sehel.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




 

 

 

 

 

 

 

 


MTENDAJI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA VIONGOZI WA TUGHE WA MAHAKAMA YA TANZANIA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel leo tarehe 12 Mei, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.

Kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kuhudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick pamoja na Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.

Lengo la kikao hicho ambacho hufanyika kila mwaka kabla ya Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ni kujadili pamoja kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu watumishi wa Mahakama sambamba na kujadili hoja za Mabaraza ya Kanda na Divisheni za Mahakama Kuu kwa upana zaidi kabla ya kufanyika kwa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

Aidha, Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania kinatarajiwa kufanyika kesho tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake ambaye ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Yafuatayo ni matukio katika picha ya Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania (hawapo katika picha) leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kulia ni Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick na kushoto ni Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.


Picha mbalimbali za Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza nao leo tarehe 12 Mei, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick akiwa katika kikao hicho.

Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.


Viongozi mbalimbali wa TUGHE Mahakama wakichangia juu ya masuala mbalimbali ya Watumishi wa Mhimili huo wakati wa Kikao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kilichofanyika leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ikisikiliza na kurekodi hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 jijini Dodoma.


Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiandika hoja na michango mbalimbali iliyokuwa ikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania wakati wa kikao.

(Picha na MARY GWERA & ARAFA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma)