Jumanne, 21 Aprili 2026

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA KITUO JUMUISHI TEMEKE YAFANYA KIKAO

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, hivi karibuni ilifanya kikao cha menejimenti kujadili mambo mbalimbali ya kiuntendaji.  

Kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho kilihusisha uongozi wa Mahakama pamoja na watumishi wa vitengo mbalimbali kwa lengo la kupokea na kujadili taarifa za utekelezaji wa majukumu, kupima mafanikio, kuchambua changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji wa mahakama.

Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sarah Mwaipopo, aliongoza kikao hicho kusisitiza umuhimu wa uwajibikaji, ushirikiano na uadilifu katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya utoaji haki.

Katika kikao hicho, wajumbe walipokea taarifa ya kipindi cha Januari hadi Machi 2026 kutoka kwa Ofisa Utumishi wa Mahakama, Bi. Jennifer Malisa, aliyekuwa mjumbe wa kikao hicho.

Alieleza kuwa Mahakama katika Kituo Jumuishi Temeke imeendelea kufanya kazi kwa ufanisi katika maeneo mbalimbali ya utoaji huduma kwa wateja wanaofika mahakamani hapo, hivyo kuelezea mafanikio, changamoto na mikakati iliyofanywa katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita.

Moja ya mafanikio makubwa ni kuendelea kuboreshwa kwa huduma za usikilizaji wa mashauri kwa kutumia teknolojia na huduma za Mahakama Inayotembea zilizoanzishwa katika Wilaya zote kwa Dar es salaam, hali iliyosaidia kupunguza gharama na muda kwa wahusika walioko mbali na Kituo.

“Mifumo ni jjambo endelevu  na lenye tafsiri pana, ambapo bado tunaendelea kufanyia kazi katika kubuni ili kurahisisha ufanisi wa kazi,” aliongeza Bw. Fredrick Kachenje, katika kuelezea mafanikio na umuhimu wa TEHAMA katika jukumu zima la kutoa haki kwa Watanzania.

Pamoja na hayo, Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samsoni Mashalla, alileza juhudi wanazozifanya katika kupeleka wataalamu wa TEHAMA kupata mafunzo kwa Mahakama nyingine, ikiwemo matumizi yasiyo na karatasi ili kuchukua ujuzi.

Aidha, Mahakama imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kiutawala na usimamizi wa mashauri kwa kuongeza ufanisi katika utendaji wa kila siku. Watumishi wameendelea kupatiwa mafunzo mbalimbali ya kujenga uwezo na kuboresha utoaji huduma ndani nan je ya kituo.

Halikadhalika, Mtendaji alieleza juu ya mafunzo yanayotolewa kwa wateja nje na na ndani ya kituo kwa ajili ya kuogeza uelewa juu ya haki zao na upatikanaji wa haki unaotolewa kituoni hapo.

Katika upande wa miundombinu, baadhi ya marekebisho ya vitendea kazi na majengo yamefanyika, pamoja na ukarabati wa vyombo vya usafiri na vifaa vya ofisi, huku jitihada za kuboresha mazingira ya kazi zikiendelea.

Licha ya mafanikio yaliyopatikana, kikao kilibaini changamoto mbalimbali zinazoathiri ufanisi wa utoaji huduma za Mahakama. Changamoto kubwa ni upungufu wa Watumishi na vitendea kazi, hali inayoathiri mazingira ya kazi na ufanisi wa Watumishi.

Mtendaji alieleza pia ufinyu wa bajeti ambao umeathiri utekelezaji wa baadhi ya shughuli muhimu ikiwemo matengenezo ya vifaa, ununuzi wa vitendea kazi na kuboresha miundombinu ya ofisi.

Changamoto nyingine ni katika usimamizi wa mirathi ambapo baadhi ya mirathi hazifungwi kwa wakati, pamoja na changamoto za usimamizi wa fedha zake katika akaunti ya mirathi iliyoko mahakamani hapo kuendelea kupokea fedha.

Kaimu Jaji Mfawihidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo akiongoza kikao cha menejimenti.

 

Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, aliyekuwa Katibu katika kikao hicho akifafanua jambo.

Ofisa TEHAMA, Bw. Fredrick Kachenje, akifanya wasilisho juu ya mafanikio ya mifumo ya TEHAMA katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka katika kikao hicho.

 

Wajumbe wa menejiment wakisikiliza mawasilisho katika hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

JAJI MWAIPOPO AONGOZA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI IJC TEMEKE

  • Wajumbe wadhamiria mifumo ya Mahakama, Wadau kusomana kupunguza udanganyifu

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, hivi karibuni aliwaongoza Mahakimu na Wadau mbalimbali wa Mahakama katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai.

Kikao hicho (Bench Bar Meeting) kilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano katika kituo hicho na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbalimbali wa Mahakama, akiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Frank Moshi, aliyekuwa Katibu wa Kikao.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuisgi Temeke, Bw. Samson Mashalla, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Watoto, Mhe. Mwamini Kazema, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya, Mhe. John Msafiri na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Upendo Kapama.

Walikuwepo pia Wajumbe wa Sekretarieti kutoka IJC Temeke pamoja na Wadau mbalimbali wa huduma za kimahakama kutoka PSSSF, RITA, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hati, Mwakilishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, Mwakilishi kutoka Benki ya CRDB na wawakilishi kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).

Akizungumza katika ufunguzi wa Kikao hicho, Mhe. Mwaipopo alisema kuwa ni jukumu la Mahakama kushirikiana kwa karibu na Wadau katika utekelezaji wa majukumu.

“Katika kusimamia mpango mkakati wake wa kumaliza mashauri ya mlundikano, Mahakama katika Kituo Jumuishi Temeke inatambua umuhimu mkubwa wa Wadau kwenye utekelezaji wa majukumu yetu. Tunawaalika Wahusika na Wadau wote ambao majukumu yao yanaathiri utendaji wa kazi tushirikiane ili kupunguza au kumaliza kabisa mashauri mlundikano,” aliongeza Mhe. Mwaipopo.

Aidha, katika kikao hicho, Wadau walipata taarifa katik ya robo ya tatu ya mwaka iliyowasilishwa na Katibu, ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Frank Moshi, na kuona takwimu za hali ya mashauri kutoka Mahakama Kuu, Mahakama ya Watoto, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo.

Wakati wa wasilisho hilo, wajumbe pia waliweza kufahamu sababu zilizochangia kutokumalizika kwa wakati mashauri katika Mahakama zote na walipata nafasi ya kutoa maoni yao.

Naibu Msajili alieleza changamoto kubwa upande wa mirathi kuwa na muda mrefu wa kufuatilia mashauri hayo pamoja na kuchelewa kufunga mirathi kwa wakati.

Aidha, alieleza changamoto kubwa ya utekelezaji kuwa ni muda mrefu wa upatikanaji wa wanunuzi wa mali za ndoa pamoja na utathimini wa thamani wa mali husika.

Wajumbe wa kikao walijadili mambo mbalimbali, ikiwemo tatizo la uhamishaji wa hati za umiliki kwenda kwa warithi pamoja na uhamishaji wa hisa na vipande kutoka kwenye Taasisi za Waadau.

Suluhisho lililotolewa ni kuomba uboreshaji wa mifumo ya Mahakama na Wadau wake kusomana, lakini pia kuongeza uelewa kwa wateja wanohudumiwa juu  ya ufuatiliaji wa stahiki hizo.

Pia kulikuwepo na majadiliano kuhusu kuchelewa kufunga mashauri kutoka Mahakama ya Watoto, ambapo sababu iliyobainishwa ni kuchelewa kwa majibu ya vinasaba (DNA) kutoka ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, huku upande wa Mahakama Kuu, sababu iliyotolewa ni kuwepo kwa amri ya Mahakama ya kufungua shauri upya baada ya makosa kufanyika.

Kulikuwepo pia na  changamoto ya suala la kubadilisha majina ya umiliki wa ardhi iliyobainishwa, jambo linalosababisha kupita muda wa kusikiliza mashauri uliowekwa kwenye kadi kipimo, ambayo ni siku 60 kwa Mahakama ya Mwanzo na Watoto, Siku 90 kwa Mahakama ya Wilaya na Siku 120 kwa Mahakama Kuu.

Ofisa Sheria kutoka RITA, Bi.Janeth Mandawa, aliongeza kuwa kuna changamoto ya wateja kuvutana juu ya nani kupata mali zisizohamishika na zinazoamishika kutokana na usheleweshaji katika uhamishaji wa umilik wa ardhi.

Alisisitiza kuwa ni muhimu ujumbe wa vikao kama hivyo kufika katika ofisi zote zinazohusika na taratibu za uhamishaji wa umiliki wa ardhi.

Hakukuwepo na mjumbe kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu ili kuleta majibu katika hoja ya miongozo inayohitajika kwa ajili ya upimaji wa vinasaba (DNA) kutokana na udhuru wa kuomba muda kwa ajili ya taratibu ya kuandaa orodha itakayotumika kwa nchi nzima.

 Akijibu hoja hiyo, Mjumbe wa Halmashauri ya Kigamboni alieleza kuwa ,“Sisi bado tupo kwenye majadiliano na pia tumeanzisha mradi wa kutengeneza hati miliki kwa awamu na kuendelea na zoezi la upimaji wa ardhi kwa maeneo ambayo hayajapimwa.

“…tumewasiliana na Ofisi ya Ardhi na tayari hoja hii imepelekwa katika Baraza la Madiwani ili kujadili namna bora ya kutoa uhakiki wa taarifa maalum za umiliki ili kutatua changamoto hii.”

Mjumbe huyo aliongeza kuwa ni muhimu kuwepo na mfumo unaosomana ili kuwezesha kesi zilizopo mahakamani na zenye kuhitaji uhamishaji wa umiliki ardhi zitumwe na Mahakama katika mfumo husika ili kufanyiwa kazi kwa haraka na kuepusha mashauri kukaa muda mrefu bila kumalizika.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, akitoa neno la ufunguzi wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai kilichofanyika hivi karibuni. Kulia ni Katibu wa Kikao na Naibu Msajili, Mhe. Frank Moshi na kushoto ni Mtendaji, Bw. Samson Mashalla.

Katibu wa Kikao na Naibu Msajili, Mhe. Frank Moshi, akitoo ufafanuzi katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai.

Ofisa kutoka Banki Kuu ya Tanzania akitoa ufafanunuzi juu ya orodha ya mahitaji ili kuhamisha umiliki wa hisa au vipande kutoka kwa marehemu kuja kwa warithi.

Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai ambao ni wadau wa Mahakama kutoka Taasisi mbalimbali wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili na Katibu wa Kikao, Mhe. Frank Moshi (hayupo pichani).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

KIKAO CHA BARAZA LA WANYAKAZI KITUO JUMUISHI TEMEKE CHAFANYIKA

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke limefanyika hivi karibuni kujadili ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita, pamoja na kupanga mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.

Kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho kilikuwa jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi kati ya uongozi na Watumishi, kikilenga kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji katika masuala ya kiutumishi.

Kikao hicho kiliongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sarah Mwaipopo. Katika hotuba yake ya ufunguzi, alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha mahusiano kazini.

Mhe. Mwaipopo alieleza kuwa, “Baraza hili ni jukwaa la kujenga Taasisi yetu kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho tunayoyahitaji.

Katika kikao hicho, kulikuwepo pia na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza. Hivyo aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita, Bi. Fatuma Jumbe, aliyekuwa Katibu na Bw. David Mbago, aliyekuwa Katibu Msaidizi.

Zoezi la uchaguzi lilisimamiwa na Ofisa Kazi, Bw. Hussein Mwamba, ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi na shirikishi kwa wajumbe kwa mujibu wa Mkataba. 

Baada ya wajumbe kupiga kura, Bw. David Mbago alichaguliwa kuwa Katibu mpya wa Baraza, huku Bi. Fatuma Jumbe akawa Katibu Msaidizi. Bi.Doroth Ndunguru alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE.

Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa chanya zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa Watumishi na ufanisi wa utendaji kazi.

Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, Baraza lilibaini kuwepo kwa changamoto kadhaa zinazoendelea kuathiri utekelezaji wa maazimio na ufanisi wa kazi kwa ujumla. Changamoto hizo zinahitaji kushughulikiwa kwa umakini ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika mjadala, ilisisitizwa kuwa Watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo. Aidha, wajumbe walisisitiza umuhimu wa kutoa elimu kuhusu Miundo ya Utumishi ili kuondoa mkanganyiko.

Baraza linasisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana huku likichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia changamoto zilizobainika.

Katikati ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi. Kushoto ni aliyekua Katibu wa Baraza, Bi. Fatuma Jumbe na kulia ni aliyekua Katibu Msaidizi, Bw. David Mbago.

 Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Hamisi Some, akichangia Hoja katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi.

Bw. David Mbago aliyekuwa Katibu Msaidizi akiwashukuru wajumbe kwa nafasi ya kuwatumikia.

Katibu na Katibu Msaidizi wakiwashukuru wajumbe kwa kuwapigia kura za kuwachagua katika awamu nyingine ya uongozi.

Bwana Hussein Mwamba, mjumbe kutoka Baraza Kuu la Wafanyakazi katika kusimamia zoezi la uchaguzi wa Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe Mwakilishi katika Baraza la TUGHE.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi waliohudhuria.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

JAJI MANYANDA ASISITIZA UTOAJI HAKI USIYOTONESHA MAJERAHA YA UKATILI WA KIJINSIA

Na. SHARIFU MOKIWA-Mahakama, Sumbawanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda amewataka washiriki wa Mafunzo ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia ambao ni Mahakimu wa Mahakama za Wilaya, Waendesha Mashtaka wa Serikali pamoja na Maafisa wa Ustawi wa Jamii kutoka mikoa ya Rukwa na Katavi kuongeza umakini wanaposhughulikia mashauri ya aina hiyo ili kuwajengea imani waathirika wanapofika mahakamani.

Mhe. Manyanda alisema hayo wakati akifungua Mafunzo ya siku tatu kuhusu namna ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia (Sexual and Gender Based Violance-SGBV) Mafunzo hayo yameanza jana tarehe 20 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga.

Mhe. Manyanda ameongeza kuwa, mafunzo hayo yanalenga kuwasaidia washiriki kuhakikisha wanaepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

“Mafunzo haya yakatumike kuhakikisha kuwa tunaepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, tutumie lugha ya staha, tuzingatie weledi na tujenge mazingira ambayo waathirika wanaweza kuwa huru kutoa ushahidi bila kuathiri kumbukumbu zao,” alisema Mhe. Manyanda

Aidha, Jaji Manyanda aliongeza kuwa, utoaji wa haki unapaswa kuzingatia utu, usalama na mazingira rafiki kwa waathirika ili kusaidia upatikanaji wa haki bila kuongeza maumivu ya kihisia na kisaikolojia.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa  Irishi Rule of Law International pamoja na kushirikiana na Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga.

Vilevile, Mafunzo hayo yanawezeshwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo kwa kushirikiana na Hakimu Mkazi Mkuu Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 22 Aprili, 2026 huku yakilenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa haki na kuimalisha ulinzi kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia katika jamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda akifungua mafunzo ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia

Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo wakifuatilia kwa umakini mada mbalimbali zinazoendelea kutolewa na wawezeshaji

Washiriki wa Mafunzo hayo wakiwa kwenye majadiliano ya pamoja wakati wa Mafunzo 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo (aliyesimama) akiwasilisha mada wakati wa mafunzo hayo. 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa Mafunzo hayo. 

Hakimu Mkazi Mkuu Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga (aliyesimama) akiwasilisha mada wakati wa mafunzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga



WATUMISHI SONGWE WAMUAGA MTUMISHI MSTAAFU

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe wamemuaga Mtumishi mwenzao Bw. Sigula Simfukwe ambaye alikuwa ni Mlinzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kishenyi alimpongeza Bw. Sigula Simfukwe kwa kutimiza umri wa kustaafu akiwa na afya njema na alimtakia kila la kheri kwenye maisha yake mapya na pia alimsihi aendelee kuishi kwa upendo na ushirikiano kama alivyokuwa akiishi na Watumishi wenzake mahakamani hapo.

Naye, Mtumishi mwenzake aliyefanya kazi kwa muda mrefu na Bw. Simfukwe mahakamani Bi. Jenitha Sheyo alimpongeza Bw. Simfukwe kwa hatua hiyo na kushukuru kwa ushirikiano wake na kumtakia kila la kheri kwenye maisha yake mapya ya nje ya utumishi wa umma.

Kwa upande wake, Mtoto wa Mstaafu huyo Bw. Joshua Simfukwe alimpongeza baba yake kwa kufikisha umri wa kustaafu akiwa na afya nzuri pia aliwashukuru Watumishi wa Mahakama kwa kumfanyia baba yake hafla hiyo, aliongeza kuwa, hiyo inaonesha baba yake alikuwa akiishi kwa upendo na ushirikiano na Watumishi wenzake mahakamani hapo.

Bw. Sigula Simfukwe aliwashukuru Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe kwa kumfanyia hafla hiyo ya kumuaga, aliwatakia utumishi mwema watumishi wote wanaobaki mahakamani hapo na kwamba hatasahau nyakati zote nzuri alizopitia mahakamani hapo pia aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano wakati wowote utakapohitajika.

Hafla hiyo iliyohudhuriwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Mhe. Nemes Chami na baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbozi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, Mhe. Francis Kishenyi (kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Nemes Chami (kulia) akifungua hafla ya kumuaga Mtumishi Mstaafu Bw. Sigula Simfukwe.

Mtumishi Mstaafu wa Mahakama Songwe Bw. Sigula Simfukwe akitoa neno katika hafla ya kuagwa kwake.

Hakimu Mkazi Mwandamizi Mhe. Vitalis Changwe (kushoto) akimkabidhi Bw. Sigula Simfukwe zawadi ya jezi ya Kilabu ya Simba.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Mhe. Nemes Chami (kushoto), akimkabidhi zawadi Bw. Sigula Simfukwe.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbozi wakiwa katika hafla ya kumuaga Mtumishi Mstaafu Bw. Sigula Simfukwe.






 

Jumatatu, 20 Aprili 2026

WANANCHI KIGOMA WAPATIWA ELIMU YA USULUHISHI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Veronica John ametoa elimu kwa wananchi kuhusu kutumia njia ya usuluhishi katika utatuzi wa migogoro mingi inayojitokeza katika jamii akieleza kuwa inaleta amani, utengamano wa kijamii na kudumisha udugu miongoni mwa jamii.

Bi. Veronica amesisitiza hayo hivi karibuni wakati akitoa elimu kwa wananchi waliokuwa wakisubiri kupata huduma mbalimbali Mahakama Kuu Kigoma.

Aidha, aliwajulisha wananchi hao kuwa, zipo njia nyingi za kutatua migogoro katika jamii ikiwemo njia ya Usuluhishi, amesema, “njia hii inapendelewa kwa kuwa inaleta maridhiano ya pamoja kwa amani bila kuathiri haki ya mtu katika mgogoro husika.”

Bi. Veronica amewaeleza wananchi hao kuwa, njia ya usuluhishi ina faida nyingi kuliko njia nyingine za utatuzi wa migogoro katika jamii, ambapo amesema kuwa, usuluhishi unadumisha udugu na ushirikiano wa jamii kuliko njia nyingine, upatikanaji haki kwa njia ya kirafiki na kucheka na kuendelea kushirikiana kwenye mambo kadhaa, kupunguza gharama za wananchi katika kuendesha mashauri Mahakamani kwakuwa  usuluhishi hauhitaji Wakili wala gharama za vikao kwa msuluhishi kwani Mahakama inao utajiri wa wasuluhishi kutoka ndani na nje ya Mahakama.

Kwa upande wake Bw. Bakari Abdallah Mfaume, Mkazi wa Gungu, ameishauri Mahakama kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili wananchi kufahamu zaidi faida za usuluhishi ili kuleta amani zaidi katika migogoro ya Ardhi, ikiwa ni pamoja na kuona eneo la mgogoro ili kuweza kung’amua kiini cha mgogoro na kuutatua kwa njia ya amani.

Elimu ya usuluhishi iliyoanza tarehe 13, Aprili 2026 hadi tarehe 17 Aprili, 2026 ilitolewa vema katika Vituo vya Mahakama Kuu Kigoma, Mahakama za Wilaya Kigoma, Kibondo, Kasulu, Uvinza, Kakonko na Buhigwe ikienda na sambamba na utoaji elimu kupitia Redio ambapo Wilaya hizo zilishiriki kuwahabarisha wananchi kuhusu Wiki ya Usuluhishi iliyofanyika katika Mahakam azote nchini.

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Bi. Veronica John akifafanua jambo hivi karibuni alipokuwa akitoa elimu ya Usuluhishi kwa wananchi Mahakama Kuu Kigoma.

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bi. Veronica John akisisitiza jambo alipokuwa akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi Mahakama Kuu Kigoma hivi karibuni.


Mwananchi Mkazi wa Gungu-Kigoma, Bw. Bakari Abdallah Mfaume (katikati) akitoa neno la kuishauri Mahakama baada ya kupewa elimu juu ya faida za Usuluhishi katika jamii.

Sehemu ya wananchi wakisikiliza kwa makini elimu iliyokuwa ikitolewa na Wakili Veronica John, Mahakama Kuu Kigoma.

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bi. Veronica John akisikiliza kwa makini swali alilokuwa akiulizwa na mmoja wa wananchi wakati alipokuwa akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi hao hivi karibuni.

 (Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

'TUMIENI UJUZI WA USULUHISHI MLIOUPATA KUISAIDIA JAMII KUMALIZA MIGOGORO KWA AMANI'

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa amewataka washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi ambao ni Mahakimu kutoka Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza kutumia ujuzi walioupata kuisaidia jamii kumaliza migogoro yao kwa amani na utengamano.

Mhe. Mbelwa aliyasema hayo hivi karibuni mkoani Kigoma wakati akifunga mafunzo ya Usuluhishi yaliyoendeshwa kwa siku tano na kuhudhuriwa na washiriki 16. 

“Tumieni ujuzi huu wa usuluhishi kuisaidia jamii kutatua migogoro kwa njia ya amani ili kuleta utengamano wa kijamii ili kupunguza utitiri wa migogoro katika Mahakama zetu na hii itaboresha upatikanaji haki kwa wananchi,” alisema Mbelwa.

Alibainisha kuwa, mafunzo hayo yamefanikiwa kwani washiriki wamepewa mbinu zote muhimu za usuluhishi, hivyo ni matarajio ya Mahakama na Jamii kwa ujumla wake kuona wanatumia vema ujuzi na weledi walioupata kuleta tija katika utatuzi wa migogoro Mahakamani ili kupunguza mashauri.

Aidha, alifafanua kuwa, mafunzo hayo yamefanyika sambamba na Wiki ya Usuluhishi Kitaifa, huku akitoa pongezi kwa washiriki ambavyo wameshiriki vema Wiki ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi, ambapo wametumia weledi walioupata kufanya usuluhishi na umeleta tija kwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma kwa mashauri waliyosimamia ambayo usuluhishi wake umefanikiwa.

Aidha, alimshukuru Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju kukubali mafunzo hayo yafanyike Kigoma na washiriki kutoka maeneo tajwa walioshiriki katika mafunzo hayo.

Vilevile alimshukuru Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo kwa kuridhia Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa kuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo ya Usuluhishi.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nyamagana, Mhe. Ramla Shehagilo alitoa shukrani kwa niaba ya washiriki, ambapo aliwashukuru Wakufunzi wa Mafunzo hayo sambamba na Waandaaji wa mafunzo hayo ambao ni Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) pamoja na Mahakama ya Tanzania kwa kuwachagua wao kuwa washiriki wa mafunzo ya usuluhishi katika Wiki ya Kitaifa ya Usuluhishi.

Naye, Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna Rweikiza akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Chuo IJA, Mhe. Dkt. Kihwelo alibainisha kuwa washiriki wamejifunza mbinu zote za usuluhishi hivyo, malengo ya mafunzo hayo yamefikiwa, na kubainisha kuwa wasuluhishi hao watakuwa na tija katika kuongeza juhudi za kuimarisha ufanisi na upatikanaji wa haki Mahakamani.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania).


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa hotuba ya kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyika kwa siku tano Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi Mahakama Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akitoa neno kwa washiriki siku ya mwisho wa Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyika kwa siku tano mkoani Kigoma. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na kushoto ni Bi. Rose Nyatega kutoka Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania).

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa  Mahakama ya Wilaya Nyamagana, Mhe. Ramla Shehagilo akitoa neno la shukrani kwa niaba ya washiriki wote wakati wa kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyikia Mahakama Kuu Kigoma.

Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna Rweikiza akitoa neno kwa niaba ya Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto wakati wa kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyotolewa kwa washiriki 16 kutoka Mahakama Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (kulia) akitoa cheti kwa moja ya washiriki wa Mafunzo ya Usuluhishi wakati wa kufunga mafunzo hayo yaliyowahusisha washiriki 16 kutoka 
Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.

Picha ya pamoja baada ya kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyika Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)