Alhamisi, 23 Aprili 2026

MAHAKAMA MOROGORO YATOA MAFUNZO KUHUSU MFUMO WA KUHIFADHI MWENENDO MAHAKAMA ZA MWANZO

Na ASHA JUMA- Mahakama Morogoro.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, imeendesha mafunzo maalumu kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo pamoja na Makarani kuhusu matumizi ya mfumo wa kuhifadhi mienendo, vielelezo na hukumu ikiwa ni sehemu ya kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji haki.

Mafunzo hayo yalifanyika jana tarehe 22 Aprili, 2026, katika Ukumbi wa Mikutano uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro, sambamba na njia ya mtandao (online) ili kuwezesha ushiriki mpana.

Mafunzo hayo yaliendeshwa na kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Morogoro, kikiongozwa na Mkuu wa Kitengo hicho pamoja na Mwanzilishi wa mfumo huo, Bw. Justine Kemhe. Aidha, mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Amiri Msumi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Msumi alikishukuru kitengo cha TEHAMA kwa ubunifu wao katika kuanzisha mfumo huo unaoitwa unaoitwa Primary Court Depository, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuboresha utendaji kazi wa Mahakama. Pia aliwahimiza washiriki kutoa ushirikiano wa kutosha pale changamoto zitakapojitokeza ili kuhakikisha mfumo unaboreshwa zaidi.

“Hongereni sana kwa kutafsiri mawazo ya watu na kuyaweka katika utekelezaji. Nawasihi Mahakimu na watumiaji wote wa mfumo huu kuwasilisha changamoto na maoni yao ili kuboresha mfumo huu,” alisema Mhe. Msumi.

Mfumo wa Primary Court Depository ni sehemu ya jitihada za kuendeleza matumizi ya TEHAMA katika Mahakama ya Tanzania. Mfumo huu unasaidia kurahisisha upatikanaji wa mienendo ya mashauri kutoka Mahakama za Mwanzo pamoja na kuhifadhi kumbukumbu hizo kidijitali, hivyo kupunguza usumbufu wa kutafuta nyaraka kwa njia za kawaida.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA alibainisha umuhimu wa kuongeza vifaa vya TEHAMA kama kompyuta na skana ili kuhakikisha mfumo huo unafanya kazi kwa ufanisi zaidi. Aliongeza kuwa mfumo huo tayari umeanza kutumika katika baadhi ya Masjala nyingine, zikiwemo Simiyu na Geita.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi  wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage, alisisitiza umuhimu wa washiriki kuzingatia maelekezo waliyopewa wakati wa mafunzo hayo, akieleza kuwa mfumo huo utarahisisha kazi na kuondoa changamoto ya upatikanaji wa mienendo ya mashauri.

Mafunzo haya yanatarajiwa kuleta mabadiliko chanya katika utendaji kazi wa Mahakama za Mwanzo kwa kuongeza ufanisi, uwazi na uhifadhi bora wa kumbukumbu za mashauri kwa njia ya kisasa (kidijitali).

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe.Amiri Msumi, akifungua mafunzo hayo.

Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA pamoja na Mwanzilishi wa mfumo huo, Bw. Justine Kemhe, akitoa mafunzo juu ya mfumo wa Primary Court Depository.

Mahakimu  pamoja na Makarani wakifuatilia mafunzo hayo kwa njia  ya mtandao na njia ya kawaida.


Habari hii imehririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


 


 


 

  

Jumatano, 22 Aprili 2026

JAJI NONGWA AANZISHA TAWI LA TAWJA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe,Mhe. Victoria Nongwa   ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) ameanzisha Tawi la Chama hicho Mahakama Kuu Njombe kinachowajumuisha Mahakimu na Majaji Wanawake.

Tawi hilo limeanzishwa kupitia alichofanya Mhe. Nongwa tarehe 20 Aprili, 2026 na Mahakimu wanawake waliopo Mkoa wa Njombe pamoja na Mahakimu waliopo Wilaya za Makete, Ludewa na Wanging’ombe kwa kutumia mkutano mtandao (Video Conference).,

Aidha, Jaji Nongwa alizungumza pia na Mahakimu wanawake wa Mahakama za Mwanzo ambapo alianza kuwaambia Mahakimu hao wampendekeze Kiongozi ambaye atakuwa Mratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Kanda ya Njombe ambaye alipendekezwa, Mhe. Matilda Kayombo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Njombe aliyepigiwa kura nyingi

Baada ya Mhe. Kayombo kuteuliwa kuwa Mratibu wa TAWJA aliwashukuru Mahakimu wanawake wenzake kwa kupewa nafasi hiyo ya kuwa Mratibu kwa Kanda ya Njombe na kuomba ushirikiano pamoja na kuongoza vikao vyote vitakavyoendelea itakapobidi.

 Kwa upande wake, Mhe. Nongwa baada ya uchaguzi wa kumpata Mratibu wa TAWJA Njombe, aliwasisitiza umuhimu wa ushirikishwaji wa Taasisi na Idara mbalimbali kwa lengo la kutoa elimu katika Mashirika na Taasisi mbalimbali mkoani humo. 

Mahakimu wanawake wa Mahakama Kanda ya Njombe walishukuru kwa kuanzishwa kwa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tawi la Njombe na kufahamu umuhimu wa kujiunga na Chama hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe na Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na  Mahakimu wanawake (TAWJA) , Mhe. Victoria Nongwa akizungumza na Mahakimu wanawake tarehe 20 Aprili, 2026 lengo likiwa ni uanzishwa wa Tawi la TAWJA Mahakama-Njombe.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Victoria Nongwa akiwa katika kikao na sehemu ya Mahakimu wanawake wa Mahakama Njombe. Dhumuni la kikao hicho ni kuanzisha Tawi la Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Njombe.

Sehemu ya Mahakimu Wanawake wa Mahakama Njombe walioshiriki katika kikao hicho wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (hayupo katika picha). Kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe. Matilda Kayombo katikati ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini,  Mhe.Lisa Abel na kulia ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini, Mhe. Maria Kiduge (hayupo katika picha).

  Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini, Mhe. Maria Kiduge akimsikiliza kwa umakini Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (hayupo katika picha).


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 

MAHAKIMU, WADAU WA HAKI WAPATIWA MAFUNZO JINSI YA KUWAHUDUMIA WAATHIRIKA WA UKATILI WA KINGONO

Na MICHAEL RITTE, Mahakama-Bukoba

Mahakimu, Waendesha Mashtaka na Maofisa Ustawi wa Jamii kutoka Mikoa ya Kagera, Geita, Rukwa na Katavi wameanza kupatiwa mafunzo maalum ya siku tatu yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kingono wakati wa mchakato wa utoaji haki.

Mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 20 Aprili, 2026 yalifunguliwa na yamefunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Immaculata Banzi kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba.

Akizungumza wakati wa ufunguzi hayo, Mhe. Banzi alisisitiza umuhimu wa wataalamu wa sheria kuwa makini wanaposhughulikia mashauri ya ukatili wa kingono huku akibainisha kuwa ukatili huo huacha madhara makubwa ya kihisia na kisaikolojia kwa waathirika.

“Unyanyasaji wa kingono na ukatili wa kijinsia huacha majeraha makubwa ya kihisia na kisaikolojia kwa waathirika. Tusipokuwa waangalifu hata mchakato wa kisheria unaweza kuwaongezea maumivu manusura,” alisema Jaji Mfawidhi huyo.

Ameongeza kwa kusema kuwa, “Tusipokuwa waangalifu, mchakato wa kisheria wenyewe unaweza kuwaongezea maumivu manusura wa ukatili wa kingono. Hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha wanajisikia vizuri, wanasikilizwa na kuheshimiwa.”

Sambamba na hilo, mafunzo kama hayo yanafanyika pia Sumbawanga ambapo yamefunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Manyanda.

Kwa upande wake, Mhe. Manyanda alieleza kuwa, mazingira yasiyo rafiki pamoja na maswali yasiyo na staha wakati wa usikilizwaji wa mashauri yanaweza kuwaumiza zaidi manusura wa ukatili wa kingono.

Alisisitiza kuwa, wahusika wa mifumo ya haki wana wajibu mkubwa wa kulinda utu na ustawi wa waathirika katika hatua zote za shauri.

Kwa mujibu wa Mratibu wa Mafunzo, Mhe. Gloria Shuma amesema  kwamba, washiriki watapatiwa maarifa na mbinu za kitaalamu ikiwemo matumizi ya lugha yenye huruma na staha pamoja na namna ya kujenga mazingira rafiki ya kimahakama kwa waathirika wa ukatili wa kingono.

Lengo kuu la mafunzo hayo ni kuhakikisha kuwa waathirika wanapatiwa mazingira salama yenye kuheshimu utu wao na yanayowawezesha kutoa ushahidi bila hofu wala shinikizo la kisaikolojia.

Mafunzo ya aina hiyo tayari yameshafanyika katika mikoa mbalimbali ikiwemo Tanga, Dodoma, Dar es Salaam, Kigoma, Mtwara, Mbeya, Mwanza, Morogoro, Arusha, Musoma na Songea.

Jitihada hizi ni sehemu ya mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa kuimarisha utoaji haki kwa kuzingatia misingi ya huruma, usawa na ujumuishi, hususan kwa makundi maalum kama waathirika wa ukatili wa kijinsia.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto kwa kushirikiana na Taasisi ya Kimataifa ya ‘Irish Rule of Law International’ (IRLI) kupitia ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania. Hii ni sehemu ya awamu ya tano ya mafunzo hayo yanayoendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali nchini.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu yaTanzania Masjala Ngodo ya  Bukoba, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi akitoa neno tarehe 20 Aprili, 2026 wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu yenye lengo la kuwajengea uwezo Mahakimu na Wadau wa Haki jinsi ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kingono.


Hakimu Mkazi ambaye ni Mratibu wa Mafunzo ya Mahakama, kutoka Chuo cha Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Gloria Shuma akitoa neno la utangulizi wakati wa Ufunguzi wa mafunzo kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba.

Sehemu ya washiriki/ wawakilishi katika mafunzo hayo. Wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Missenyi, Mhe. Nelson Bagenda,  na wadau mbalimabali kutoka Ofisi ya Taifa ya Mshataka (NPS) na Ofisi ya Ustawi wa Jamii wakiwa katika mafunzo hayo yanayoendeshwa kwenye Ukumbi wa Mahakama Kuu Bukoba.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Immaculata Banzi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Lilian Itemba (kushoto),  Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba,  Mhe Ferdinand Kiwonde (kulia). Waliosimama nyuma kulia ni  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Said Mkasiwa katikati ni Naibu Msajili kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu Dodoma, Mhe Mwajabu Mvungi na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma ambaye pia Mwezeshaji wa Mafunzo, Mhe Fadhili Mbelwa.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Immaculata Banzi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Lilian Itemba (kushoto),  Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba,  Mhe Ferdinand Kiwonde (kulia). Waliosimama ni Wawakilishi kutoka Ofisi ya Mashtaka, Bw. Robert Neophitus (kushoto) na Scholastica Teffe.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 



Jumanne, 21 Aprili 2026

SERIKALI YAENDELEA KUBORESHA MAJENGO YA MAHAKAMA NCHINI

  • Ujenzi, ukarabati kufanyika kwa awamu kusogeza huduma za haki karibu na wananchi

Na HALIMA MNETE- MAHAKAMA DODOMA.

Serikali imesema inaendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama nchini ili kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa Wananchi.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 21 Aprili, 2025 jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, wakati akijibu maswali ya Wabunge katika kikao cha Bunge la Kumi na Tatu jijini Dodoma kuhusu hali ya miundombinu ya Mahakama.

Amesema kuwa Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza ujenzi na ukarabati wa majengo kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026, kufuatia kuwepo kwa uhaba wa majeng,o hususan Mahakama za Mwanzo katika maeneo mbalimbali nchini.

Naibu Waziri ameeleza kuwa utekelezaji huo unafanyika kwa awamu, ambapo kwa sasa Serikali inakamilisha maandalizi ya awamu ya tatu ya mpango huo wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya mahakama.

Katika swali la msingi, Mbunge wa Nanyamba, Abdallah Chikota, alihoji kuhusu mpango wa Serikali kujenga Mahakama ya Mwanzo katika Wilaya hiyo, huku akishauri pia kujengwa kwa nyumba za Watumishi wa Mahakama ili kuboresha mazingira ya kazi.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri alisema kuwa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo wilayani Nanyamba utazingatiwa katika mpango wa awamu ya tatu.

Aidha, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, Ado Shaibu Ado, aliuliza swali la nyongeza akitaka kufahamu sababu za kusimama kwa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya hiyo kwa takribani miezi mitano na ni lini utakamilika.

Katika majibu yake, Mhe. Katimba alisema kuwa mradi huo upo katika awamu ya pili ya utekelezaji na tayari mkandarasi yupo eneo la kazi akiendelea na ujenzi, huku Serikali ikiwa na dhamira ya kuhakikisha Wananchi wanapata majengo ya kisasa yatakayowezesha upatikanaji bora wa haki.

Kwa upande wake, Mbunge wa Muleba Kaskazini, Mhe. Adonis Alfred Bitegeko, alihoji lini jengo la Mahakama ya Wilaya hiyo litaboreshwa kutokana na changamoto ya uchakavu na ufinyu wa nafasi.

Akijibu, Naibu Waziri alisema kuwa Serikali ina mpango wa kuboresha jengo hilo ili Wananchi wa Muleba waweze kupata huduma za mahakama katika mazingira bora zaidi.

Naye Mbunge wa Kiteto, Mhe. Edward Ole Lekaita, aliitaka Serikali kueleza lini ujenzi wa Mahakama ya kisasa katika Wilaya hiyo utaanza.

Katika majibu yake, Mhe. Katimba alisema kuwa tayari mchakato wa kumpata mkandarasi umeanza baada ya kutangazwa kwa zabuni, na hatua zilizopo sasa ni za majadiliano ya mkataba ili kuruhusu kuanza kwa ujenzi huo.

Serikali imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha inaboresha miundombinu ya Mahakama nchini ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki na kupunguza changamoto zinazowakabili Wananchi katika kupata huduma hiyo muhimu.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, akisisitiza jambo wakati anajibu maswali ya Wabunge katika kikao cha Bunge la Kumi na Tatu jijini Dodoma.



Bunge la Kumi na Tatu likiendelea na shughuli zake jijini Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA KITUO JUMUISHI TEMEKE YAFANYA KIKAO

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, hivi karibuni ilifanya kikao cha menejimenti kujadili mambo mbalimbali ya kiuntendaji.  

Kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho kilihusisha uongozi wa Mahakama pamoja na watumishi wa vitengo mbalimbali kwa lengo la kupokea na kujadili taarifa za utekelezaji wa majukumu, kupima mafanikio, kuchambua changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji wa mahakama.

Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sarah Mwaipopo, aliongoza kikao hicho kusisitiza umuhimu wa uwajibikaji, ushirikiano na uadilifu katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya utoaji haki.

Katika kikao hicho, wajumbe walipokea taarifa ya kipindi cha Januari hadi Machi 2026 kutoka kwa Ofisa Utumishi wa Mahakama, Bi. Jennifer Malisa, aliyekuwa mjumbe wa kikao hicho.

Alieleza kuwa Mahakama katika Kituo Jumuishi Temeke imeendelea kufanya kazi kwa ufanisi katika maeneo mbalimbali ya utoaji huduma kwa wateja wanaofika mahakamani hapo, hivyo kuelezea mafanikio, changamoto na mikakati iliyofanywa katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita.

Moja ya mafanikio makubwa ni kuendelea kuboreshwa kwa huduma za usikilizaji wa mashauri kwa kutumia teknolojia na huduma za Mahakama Inayotembea zilizoanzishwa katika Wilaya zote kwa Dar es salaam, hali iliyosaidia kupunguza gharama na muda kwa wahusika walioko mbali na Kituo.

“Mifumo ni jjambo endelevu  na lenye tafsiri pana, ambapo bado tunaendelea kufanyia kazi katika kubuni ili kurahisisha ufanisi wa kazi,” aliongeza Bw. Fredrick Kachenje, katika kuelezea mafanikio na umuhimu wa TEHAMA katika jukumu zima la kutoa haki kwa Watanzania.

Pamoja na hayo, Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samsoni Mashalla, alileza juhudi wanazozifanya katika kupeleka wataalamu wa TEHAMA kupata mafunzo kwa Mahakama nyingine, ikiwemo matumizi yasiyo na karatasi ili kuchukua ujuzi.

Aidha, Mahakama imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kiutawala na usimamizi wa mashauri kwa kuongeza ufanisi katika utendaji wa kila siku. Watumishi wameendelea kupatiwa mafunzo mbalimbali ya kujenga uwezo na kuboresha utoaji huduma ndani nan je ya kituo.

Halikadhalika, Mtendaji alieleza juu ya mafunzo yanayotolewa kwa wateja nje na na ndani ya kituo kwa ajili ya kuogeza uelewa juu ya haki zao na upatikanaji wa haki unaotolewa kituoni hapo.

Katika upande wa miundombinu, baadhi ya marekebisho ya vitendea kazi na majengo yamefanyika, pamoja na ukarabati wa vyombo vya usafiri na vifaa vya ofisi, huku jitihada za kuboresha mazingira ya kazi zikiendelea.

Licha ya mafanikio yaliyopatikana, kikao kilibaini changamoto mbalimbali zinazoathiri ufanisi wa utoaji huduma za Mahakama. Changamoto kubwa ni upungufu wa Watumishi na vitendea kazi, hali inayoathiri mazingira ya kazi na ufanisi wa Watumishi.

Mtendaji alieleza pia ufinyu wa bajeti ambao umeathiri utekelezaji wa baadhi ya shughuli muhimu ikiwemo matengenezo ya vifaa, ununuzi wa vitendea kazi na kuboresha miundombinu ya ofisi.

Changamoto nyingine ni katika usimamizi wa mirathi ambapo baadhi ya mirathi hazifungwi kwa wakati, pamoja na changamoto za usimamizi wa fedha zake katika akaunti ya mirathi iliyoko mahakamani hapo kuendelea kupokea fedha.

Kaimu Jaji Mfawihidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo akiongoza kikao cha menejimenti.

 

Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, aliyekuwa Katibu katika kikao hicho akifafanua jambo.

Ofisa TEHAMA, Bw. Fredrick Kachenje, akifanya wasilisho juu ya mafanikio ya mifumo ya TEHAMA katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka katika kikao hicho.

 

Wajumbe wa menejiment wakisikiliza mawasilisho katika hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

JAJI MWAIPOPO AONGOZA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI IJC TEMEKE

  • Wajumbe wadhamiria mifumo ya Mahakama, Wadau kusomana kupunguza udanganyifu

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, hivi karibuni aliwaongoza Mahakimu na Wadau mbalimbali wa Mahakama katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai.

Kikao hicho (Bench Bar Meeting) kilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano katika kituo hicho na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbalimbali wa Mahakama, akiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Frank Moshi, aliyekuwa Katibu wa Kikao.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Kituo Jumuisgi Temeke, Bw. Samson Mashalla, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Watoto, Mhe. Mwamini Kazema, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya, Mhe. John Msafiri na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Upendo Kapama.

Walikuwepo pia Wajumbe wa Sekretarieti kutoka IJC Temeke pamoja na Wadau mbalimbali wa huduma za kimahakama kutoka PSSSF, RITA, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hati, Mwakilishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, Mwakilishi kutoka Benki ya CRDB na wawakilishi kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).

Akizungumza katika ufunguzi wa Kikao hicho, Mhe. Mwaipopo alisema kuwa ni jukumu la Mahakama kushirikiana kwa karibu na Wadau katika utekelezaji wa majukumu.

“Katika kusimamia mpango mkakati wake wa kumaliza mashauri ya mlundikano, Mahakama katika Kituo Jumuishi Temeke inatambua umuhimu mkubwa wa Wadau kwenye utekelezaji wa majukumu yetu. Tunawaalika Wahusika na Wadau wote ambao majukumu yao yanaathiri utendaji wa kazi tushirikiane ili kupunguza au kumaliza kabisa mashauri mlundikano,” aliongeza Mhe. Mwaipopo.

Aidha, katika kikao hicho, Wadau walipata taarifa katik ya robo ya tatu ya mwaka iliyowasilishwa na Katibu, ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Frank Moshi, na kuona takwimu za hali ya mashauri kutoka Mahakama Kuu, Mahakama ya Watoto, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo.

Wakati wa wasilisho hilo, wajumbe pia waliweza kufahamu sababu zilizochangia kutokumalizika kwa wakati mashauri katika Mahakama zote na walipata nafasi ya kutoa maoni yao.

Naibu Msajili alieleza changamoto kubwa upande wa mirathi kuwa na muda mrefu wa kufuatilia mashauri hayo pamoja na kuchelewa kufunga mirathi kwa wakati.

Aidha, alieleza changamoto kubwa ya utekelezaji kuwa ni muda mrefu wa upatikanaji wa wanunuzi wa mali za ndoa pamoja na utathimini wa thamani wa mali husika.

Wajumbe wa kikao walijadili mambo mbalimbali, ikiwemo tatizo la uhamishaji wa hati za umiliki kwenda kwa warithi pamoja na uhamishaji wa hisa na vipande kutoka kwenye Taasisi za Waadau.

Suluhisho lililotolewa ni kuomba uboreshaji wa mifumo ya Mahakama na Wadau wake kusomana, lakini pia kuongeza uelewa kwa wateja wanohudumiwa juu  ya ufuatiliaji wa stahiki hizo.

Pia kulikuwepo na majadiliano kuhusu kuchelewa kufunga mashauri kutoka Mahakama ya Watoto, ambapo sababu iliyobainishwa ni kuchelewa kwa majibu ya vinasaba (DNA) kutoka ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, huku upande wa Mahakama Kuu, sababu iliyotolewa ni kuwepo kwa amri ya Mahakama ya kufungua shauri upya baada ya makosa kufanyika.

Kulikuwepo pia na  changamoto ya suala la kubadilisha majina ya umiliki wa ardhi iliyobainishwa, jambo linalosababisha kupita muda wa kusikiliza mashauri uliowekwa kwenye kadi kipimo, ambayo ni siku 60 kwa Mahakama ya Mwanzo na Watoto, Siku 90 kwa Mahakama ya Wilaya na Siku 120 kwa Mahakama Kuu.

Ofisa Sheria kutoka RITA, Bi.Janeth Mandawa, aliongeza kuwa kuna changamoto ya wateja kuvutana juu ya nani kupata mali zisizohamishika na zinazoamishika kutokana na usheleweshaji katika uhamishaji wa umilik wa ardhi.

Alisisitiza kuwa ni muhimu ujumbe wa vikao kama hivyo kufika katika ofisi zote zinazohusika na taratibu za uhamishaji wa umiliki wa ardhi.

Hakukuwepo na mjumbe kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu ili kuleta majibu katika hoja ya miongozo inayohitajika kwa ajili ya upimaji wa vinasaba (DNA) kutokana na udhuru wa kuomba muda kwa ajili ya taratibu ya kuandaa orodha itakayotumika kwa nchi nzima.

 Akijibu hoja hiyo, Mjumbe wa Halmashauri ya Kigamboni alieleza kuwa ,“Sisi bado tupo kwenye majadiliano na pia tumeanzisha mradi wa kutengeneza hati miliki kwa awamu na kuendelea na zoezi la upimaji wa ardhi kwa maeneo ambayo hayajapimwa.

“…tumewasiliana na Ofisi ya Ardhi na tayari hoja hii imepelekwa katika Baraza la Madiwani ili kujadili namna bora ya kutoa uhakiki wa taarifa maalum za umiliki ili kutatua changamoto hii.”

Mjumbe huyo aliongeza kuwa ni muhimu kuwepo na mfumo unaosomana ili kuwezesha kesi zilizopo mahakamani na zenye kuhitaji uhamishaji wa umiliki ardhi zitumwe na Mahakama katika mfumo husika ili kufanyiwa kazi kwa haraka na kuepusha mashauri kukaa muda mrefu bila kumalizika.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, akitoa neno la ufunguzi wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai kilichofanyika hivi karibuni. Kulia ni Katibu wa Kikao na Naibu Msajili, Mhe. Frank Moshi na kushoto ni Mtendaji, Bw. Samson Mashalla.

Katibu wa Kikao na Naibu Msajili, Mhe. Frank Moshi, akitoo ufafanuzi katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai.

Ofisa kutoka Banki Kuu ya Tanzania akitoa ufafanunuzi juu ya orodha ya mahitaji ili kuhamisha umiliki wa hisa au vipande kutoka kwa marehemu kuja kwa warithi.

Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai ambao ni wadau wa Mahakama kutoka Taasisi mbalimbali wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili na Katibu wa Kikao, Mhe. Frank Moshi (hayupo pichani).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

KIKAO CHA BARAZA LA WANYAKAZI KITUO JUMUISHI TEMEKE CHAFANYIKA

Na HIGHNESS TERRY-Kituo Jumuishi cha Masuala Familia,Temeke

Kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke limefanyika hivi karibuni kujadili ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita, pamoja na kupanga mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.

Kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo hicho kilikuwa jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi kati ya uongozi na Watumishi, kikilenga kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji katika masuala ya kiutumishi.

Kikao hicho kiliongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sarah Mwaipopo. Katika hotuba yake ya ufunguzi, alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha mahusiano kazini.

Mhe. Mwaipopo alieleza kuwa, “Baraza hili ni jukwaa la kujenga Taasisi yetu kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho tunayoyahitaji.

Katika kikao hicho, kulikuwepo pia na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza. Hivyo aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita, Bi. Fatuma Jumbe, aliyekuwa Katibu na Bw. David Mbago, aliyekuwa Katibu Msaidizi.

Zoezi la uchaguzi lilisimamiwa na Ofisa Kazi, Bw. Hussein Mwamba, ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi na shirikishi kwa wajumbe kwa mujibu wa Mkataba. 

Baada ya wajumbe kupiga kura, Bw. David Mbago alichaguliwa kuwa Katibu mpya wa Baraza, huku Bi. Fatuma Jumbe akawa Katibu Msaidizi. Bi.Doroth Ndunguru alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE.

Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa chanya zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa Watumishi na ufanisi wa utendaji kazi.

Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, Baraza lilibaini kuwepo kwa changamoto kadhaa zinazoendelea kuathiri utekelezaji wa maazimio na ufanisi wa kazi kwa ujumla. Changamoto hizo zinahitaji kushughulikiwa kwa umakini ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika mjadala, ilisisitizwa kuwa Watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo. Aidha, wajumbe walisisitiza umuhimu wa kutoa elimu kuhusu Miundo ya Utumishi ili kuondoa mkanganyiko.

Baraza linasisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana huku likichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia changamoto zilizobainika.

Katikati ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Sara Mwaipopo, aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi. Kushoto ni aliyekua Katibu wa Baraza, Bi. Fatuma Jumbe na kulia ni aliyekua Katibu Msaidizi, Bw. David Mbago.

 Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Hamisi Some, akichangia Hoja katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi.

Bw. David Mbago aliyekuwa Katibu Msaidizi akiwashukuru wajumbe kwa nafasi ya kuwatumikia.

Katibu na Katibu Msaidizi wakiwashukuru wajumbe kwa kuwapigia kura za kuwachagua katika awamu nyingine ya uongozi.

Bwana Hussein Mwamba, mjumbe kutoka Baraza Kuu la Wafanyakazi katika kusimamia zoezi la uchaguzi wa Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe Mwakilishi katika Baraza la TUGHE.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi waliohudhuria.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.