- Azungumza na Watumishi
- Afurahishwa na nidhamu ya Wafungwa, Mahabusu
Na FAUSTINE KAPAMA
na Noel Daud-Mahakama, Songea
Jaji Kiongozi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, leo tarehe 22
Juni, 2026, ametembelea Mahakama ya Wilaya Nyasa na Gereza la Wilaya ya Mbinga,
na kuzungumza na Watumishi, Mahabusu na Wafungwa.
Akiwa katika
Mahakama ya Wilaya, Mhe. Dkt. Siyani
amepokea taarifa ya utendaji wa Mahakama hiyo, iliyowasilishwa na Hakimu Mkazi
Mfawidhi, Mhe. Osmund Ngatunga.
Kabla ya
kuzungumza na Watumishi, Jaji Kiongozi alipokea pia changamoto zao na kuzitolea
ufafanuzi na majawabu, ikiwepo upatikanani wa miundombinu ya majengo ya
Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo.
Akizungumza na
Watumishi hao, Mhe. Dkt. Siyani aliwakumbusha kuendelea kutekeleza majukumu yao
kwa bidii na uaminifu Kadiri inavyowezekana na kuzingatia maadili, huku matendo
yao yakiakisi salamu ya Mahakama kuhusu uadilifu, weledi na uwajibikaji.
“Katika zama zetu
hizi, kufanya kazi kwa haki ni njia mojawapo ya kulinda miundo mbinu yetu. Watu
wasiporidhika na hukumu zenu, ndiyo matukio ya ajabu ajabu wakati mwingine
yanatokea,” Jaji Kiongozi amesema.
Mhe. Dkt. Siyani
amewataka pia Watumishi hao kutoa huduma kwa Wananchi kwa ufanisi zaidi ili
kuongeza imani kwa Mahakama na kushughulikia kero zao zinazoletwa mahakamani mapema
ipasavyo, kwani Mahakama ina mchango katika kutunza amani na usalama nchini.
“Hakuna sababu kwa
Wananchi kuwa na wasiwasi na Mahakama yetu. Shughulikieni kero za Wananchi.
Wananchi wanaleta kero mahakamani kwa njia nyingi, wengine kwa Mkuu wa Wilaya.
Mtu ana dai nakala ya hukumu, mtu ana mirathi yake anazungushwa. Kila mmoja
wetu ana wajibu wa kusaidia Mtanzania,” amesema.
Katika taarifa
yake, Mhe. Ngatunga alieleza kuwa hapakuwepo na mashauri yaliyobaki kwa mwaka
2025, yaliyofunguliwa Januari hadi Juni, 2026 yalikuwa 208 na mashauri ambayo
yamesikilizwa na kumalizika ni 200, yanayoendelea n inane.
Akizungumzia
mashauri ya mirathi, ameeleza kuwa kwa kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi
Juni, 2026, Mahakama za Mwanzo zimefungua, kusikiliza na kufunga mashauri 11,
huku katika Mahakama ya Wilaya yamefunguliwa mashauri ya mirathi 11, yamesikilizwa
tisa na mashauri mawili bado kusikilizwa.
“Mashauri yote
hayajafungwa kwa sababu muda wake wa kufunga bado. Ili kuhakikisha wasimamizi
wa mirathi wanatekeleza wajibu wao kwa kufuata sheria, baada ya kuteuliwa kwao,
tunawapangia kila mwisho wa mwezi wafike mahakamani kuelekeza namna
wanavyoedelea na ukusanyaji na kugawa mali za marahemu,” amesema.
Akiwa kwenye
Gereza la Wilaya, Jaji Kiongozi alipokea taarifa kutoka kwa Mkuu wa Gereza,
Mrakibu Mwandamizi wa Magereza, Afande Benjamin Masika, ambaye alionesha hali
ya Gereza, idadi ya Mahabusu na Wafungwa.
Afande Masika pia
alimwelezea Mhe. Dkt. Siyani miradi
mbalimbali inayotekelezwa na Gereza hilo, ikiwemo ufugaji wa samaki na ujenzi
wa zahanati.
Baada ya kupokea
taarifa hiyo, Jaji Kiongozi amewapongeza Mahakama katika Wilaya ya Mbinga na
Nyasa pamoja na upande wa Mashataka kwa kazi nzuri ya kutekeleza sheria,
ikiwemo kutozalisha Mahabusu wanaotoka Mahakama za Mwanzo.
Mhe. Dkt. Siyani
pia amepongeza ubunifu unaofanywa na Gereza hilo katika maeneo mbalimbali na
kushauri kuruhusu ushirikiano na Wadau, jambo litakalosaidia kuchochea
maendeleo na kuondoa changamoto zilizopo.
Baada ya
mazungumzo hayo, Jaji Kiongozi alikagua miradi hiyo na mazingira ya Gereza na
baadaye kuzungumza na Mahabusu na Magereza na kisha kupokea changamoto zao na
kuzitolea ufafanuzi na ufumbuzi.
Mhe. Dkt. Siyani
ameonesha kufurahishwa na ukweli na nidhamu ya hali ya juu iliyooneshwa na
vijana hao wakati wa mazungumzo hayo.
Jaji Kiongozi
ataendelea na ziara yake ya kimahakama mkoani Ruvuma kwa kutembelea Magereza
mawili ya Mkwaya na Kitai, yote yakiwa katika Wilaya ya Mbinga.
Katika ziara hiyo,
Jaji Kiongozi ameambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala
Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel
Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na Naibu
Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.
Wengine ni
Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Mahakimu Wakazi Wfawidhi wa
Mahakama za Wilaya ya Nyasa na Mbinga Songea na Watumishi wengine wa Mahakama
Songea.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (aliyesimama) akitoa utambulisho wa wageni mbalimbali walioambatana na Jaji Kiongozi. Aliyekaa ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela.


















