Jumatatu, 6 Julai 2026

MAJAJI WAPYA WA RUFANI WAPIGWA MSASA: WAHIMIZWA KUZINGATIA MAADILI, HEKIMA KATIKA UTOAJI HAKI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamehimizwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya haki, hekima na huruma, badala ya kufungwa na masharti ya kiufundi ya kisheria yanayoweza kukwamisha utoaji haki, hasa kwa wananchi wanyonge.

Wito huo umetolewa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 06 Julai, 2026 alipokuwa akifungua Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

Akizungumza katika ufunguzi huo, Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, Ibara ya 107A(1) na (2)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaelekeza wazi kuweka mbele maslahi ya haki (interest of justice).

Amesema, kwa kuwa Mahakama ya Rufani ndiyo ngazi ya mwisho katika mfumo wa utoaji haki nchini Tanzania, hivyo inabeba dhamana kubwa ya kijamii na kiungu. "Sisi tukiwa waamuzi na uamuzi wetu ukiwa wa mwisho, ninawashauri tuendelee kutenda haki tukiwa huru kwa kuzingatia Katiba na Sheria... kwa namna ambayo masharti ya kiufundi hayatatukwamisha haki kutendeka ipasavyo," ameeleza Jaji Mkuu.

Ameongeza kwa kusema kwamba, “Na kwa sababu sisi tunafanya maamuzi tukiwa huru, tumepewa madaraka makubwa, tunakuwa huru. Sasa mtu anayefanya maamuzi akiwa huru ana masharti mawili ya kuzingatia. Moja, azingatie Katiba na Sheria za Nchi. Lakini pia kwenye kiapo chetu kile tunahimizwa kuzingatia katiba, mila, desturi, na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tukiwa huru bila hofu, huba, chuki, wala upendeleo. Kila mtu aliye huru anapotekeleza madaraka yake, pale ambapo katiba au sheria imetamka utakuwa huru kama sisi. Kubwa la kwanza ni kuzingatia katiba na sheria za nchi.”

Aidha, Mhe. Masaju amewasisitiza Majaji hao juu ya umuhimu wa Kuzingatia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, ambapo amesema, Majaji na Mahakimu wametajwa bayana chini ya Kifungu cha 4 cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kama Viongozi wa umma. “Chini ya Kifungu cha 6(1)(a), Viongozi hawa wanatakiwa kuwa waaminifu (honest), wenye utu na huruma (compassion), na kufanya maamuzi kwa uhalisia na bila upendeleo (objectivity). Kadhalika, Jaji Mkuu amewataka kujituma na kuwa wepesi wa kujiongeza katika kazi (Proactive and Active).

Amesema; Majaji hawatakiwi kuwa watazamaji tu (passive) pale ambapo kumbukumbu za mashauri zinaonesha uwepo wa mapungufu yaliyo wazi. “Kwa kuwa sisi tuna kauli ya mwisho, ndio maana naomba kuwashauri Wahe. Majaji kwamba tuendelee kuwa ‘proactive’ na ‘active’, tusiwe 'passive'. Hatua yoyote, sisi ndio tuna hilo jukumu na ndio tunawajibika. Na ikiwa kuna lawama zozote, lawama zile hazitaenda kwa Mawakili, zitaenda kwetu Mahakama. Wakati fulani wanatuita wazee, lakini kwa sasa tunafanya vizuri. Mimi ninaomba kuwahimiza tu kwamba tudumishe huo utaratibu, tabia hiyo ni njema,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Vilevile, Jaji Mkuu amewataka Majaji hao kulinda haki ya wanyonge hususan wananchi wanaojitetea wenyewe bila Mawakili au wale ambao mashauri yao yamechukua miaka mingi tangu kuanzia Mahakama za Mwanzo.

Mbali na maslahi ya haki, Mhe. Masaju ameongeza pia kwa kuwataka Majaji hao kuzingatia maslahi ya umma pamoja na maslahi ya Taifa ambapo amesema kwenye Katiba, pamoja na kutajwa kwingineko, yametajwa pia katika Ibara ya 30(2). 

"Lakini kwa urahisi sana, kila kitu kilichokuwa kimewekwa kwenye Sheria kina maslahi ya umma, kina maslahi ya Taifa. Na ndio maana kikawekwa pale. Kwa hiyo katika mazingira kama hayo, mimi ninawaamini ninyi Waheshimiwa. Kwanza mna sifa zote za kuwa Majaji na Majaji wa Mahakama ya Rufani, mna hekima mna akili. Mtaendelea kulisaidia Taifa hili kufanya haki iendelee kutendeka katika taifa hili kwa ufanisi ipasavyo. Yazingatieni haya mafunzo," amesisitiza Jaji Mkuu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju amewasisitiza Majaji hao kujenga falsafa ya sheria za ndani (Local Jurisprudence); ambapo ameeleza kuwa, Tanzania ina miaka mingi ya uhuru na ina uwezo wa kutosha wa kisheria na ukweli wa mazingira wa kujenga misingi yake yenyewe ya kisheria, hivyo amewashauri Majaji kuacha tabia ya kukimbilia kunukuu maamuzi ya nchi za nje kama Uingereza au India na badala yake wachague kuendeleza maamuzi mazuri yaliyotolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania ili kuweka vigezo imara vya nchi.

“Sisi tunafanya maamuzi yanayoenda kutumika katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hatufanyi maamuzi yatakayoenda kutumika huko India au kwingineko. Sisemi kwamba hamuwezi mkayasoma huko au hatuwezi tukayasoma yale lakini wakati fulani mimi naona tunarejea huko, lakini unaangalia mbona hata hii Mahakama ya kwetu hapa ilishaamua kitu kama hiki?” ameeleza Jaji Mkuu.

Ameongeza kwa kuwakumbusha juu ya Matumizi ya Hekima na Akili; ambapo amesema kuwa, ingawa utaalamu wa sheria ni muhimu, matumizi ya akili ya kuzaliwa na hekima ni vitu vya thamani zaidi vinavyomsaidia Jaji kutoa uamuzi wa haki bila hofu, huba, chuki, wala upendeleo.

Vilevile, Jaji Mkuu amewakumbusha Majaji hao kuwa wao ni watumishi wa Mungu, hivyo wawe na amani ambapo amesisitiza kwa kusema, “hamuwezi mkasema ninyi si watumishi wa Mungu wakati mnafanya kazi ya Mungu. Ninyi ni sehemu ya Serikali, ni watumishi wa Mungu na hata hivyo mnafanya kazi zake. Hata kama ninyi sio Mungu. Kwa hiyo hamuwezi mkasema kwamba ninyi si watumishi wa Mungu. Sasa kama si watumishi wa Mungu mnataka kuwa watumishi wa mashetani? Na tukishakuwa watumishi wa mashetani hizo kazi tutazitenda? Ninavyozungumza kuwa watumishi wa Mungu ni katika muktadha wa kwamba mnafanya kazi za Mwenyezi Mungu. Na tunaofanya kazi ya Mwenyezi Mungu, moja lazima tuwe wanyenyekevu sana.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju ametoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa jitihada zake endelevu za kuimarisha Mhimili huo kupitia uboreshaji wa miundombinu, vitendea kazi, na kuongeza rasilimaliwatu (Majaji na watumishi wa Kada nyingine huku akibainisha kuwa Rais Samia anaiishi kwa vitendo kauli yake ya kutaka kuifikisha Mahakama ya Tanzania katika hadhi ya Kimataifa.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amekishukuru Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto chini ya Mkuu wa Chuo hicho, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo-Jaji wa Mahakama ya Rufani, amemshukuru Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Viongozi wote wa kada ya Utawala na sheria kwa ushirikiano wao katika kufanikisha mafunzo hayo yanayoendeshwa kwa njia shirikishi na kirafiki.

Mafunzo hayo yaliyosheheni mada mbalimbali yamewakusanya pamoja Majaji hao wapya wa Mahakama ya Rufani kwa lengo la kuwaandaa kuanza kutekeleza majukumu yao katika ngazi hiyo ya juu ya utoaji haki.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 06 Julai, 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 06 Julai, 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto kwa Jaji  Mkuu ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.


Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani wakisikiliza hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo Elekezi iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 06 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Viongozi na Watumishi wengine wa Mahakama na IJA walioshiriki katika ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo hayo leo tarehe 06 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani (waliosimama). Aliyeketi kushoto ni 
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania (waliosimama) walioshiriki kwenye ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 06 Julai, 2026. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania na wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto (waliosimama) walioshiriki kwenye ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 06 Julai, 2026. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)


























MAFUNZO ELEKEZI YANAWAJENGEA MAJAJI WA RUFANI UWEZO WA KUTOA HAKI KWA UFANISI; JAJI KIHWELO

·       Yanawaandaa pia Majaji wapya kutekeleza majukumu yao kwa weledi, kujiamini na kuzingatia misingi ya utoaji haki

Na HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma.

Majaji wa Mahakama ya Rufani wametakiwa kutumia mafunzo elekezi wanayopatiwa kama fursa ya kujenga uwezo, kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuimarisha utoaji haki unaozingatia misingi ya Katiba, sheria na maslahi ya wananchi.

Hayo yameelezwa leo tarehe 06 Julai, 2026 na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA)-Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo alipokuwa akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye Ukumbi wa miktano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mafunzo hayo yamefunguliwa rasmi na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju na yamewaleta pamoja Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani kwa lengo la kuwaandaa kuanza kutekeleza majukumu yao katika ngazi hiyo ya juu ya utoaji haki.

Akitoa salamu zake, Mhe.Dkt. Kihwelo amemshukuru Mungu kwa kuwezesha kufanyika kwa mafunzo hayo na Jaji Mkuu kwa kuridhia kufanyika kwa mafunzo hayo, kushiriki katika ufunguzi wake pamoja na kukubali kuwa mmoja wa Wawezeshaji wa mafunzo hayo licha ya majukumu yake mengi ya kiuongozi.

Amesema ushiriki wa Jaji Mkuu kama Mwezeshaji ni ishara ya namna ambavyo Uongozi wa Mahakama ya Tanzania unavyoweka kipaumbele katika maendeleo ya taaluma na kuwajengea uwezo Majaji ili waendelee kutekeleza majukumu yao kwa viwango vya juu vya weledi.

Mhe.Dkt. Kihwelo pia amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuiamini Mahakama ya Tanzania kupitia uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Rufani, akisema kwamba, hatua hiyo imeendelea kuimarisha uwezo wa Taasisi hiyo katika utoaji haki.

Sambamba na hilo, amewapongeza Majaji tisa walioteuliwa hivi karibuni kujiunga na Mahakama ya Rufani, akiwakaribisha rasmi katika ngazi hiyo ya juu ya Mhimili wa utoaji haki na kuwahimiza kutumia mafunzo hayo kama msingi wa safari yao mpya ya utumishi.

Akizungumza kuhusu umuhimu wa mafunzo hayo, Mhe. Dkt. Kihwelo amesema jukumu kuu la Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ni kuwajengea uwezo watumishi wa Mahakama ili kuboresha utendaji wao katika utoaji haki, akibainisha kuwa, mafunzo hayo yanatekeleza Sera ya Mafunzo ya Mahakama ya mwaka 2019 pamoja na Sera ya Mafunzo ya Taifa.

Ameongeza kuwa, Mahakama imeendelea kujenga utamaduni wa kuhakikisha Viongozi wote wanaoteuliwa katika nafasi mpya wanapatiwa mafunzo elekezi kabla ya kuanza rasmi majukumu yao, hatua ambayo imechangia kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa kazi za Mahakama.

"Dhamira yetu ni kuhakikisha kila Kiongozi anayepata nafasi mpya anaingia akiwa ameandaliwa ipasavyo ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa weledi na kujiamini," amesema.

Aidha, ameeleza kuwa, mafunzo hayo ni ya tano kufanyika kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani tangu programu hiyo ilipoanzishwa mwaka 2019, jambo linaloonesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania ya kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya rasilimali watu.

Kwa mujibu wa Mhe. Dkt. Kihwelo, washiriki watapata mafunzo kutoka kwa Wawezeshaji wenye uzoefu mkubwa katika masuala ya Mahakama ya Rufani, wakiwemo Majaji Waandamizi na Wastaafu, ambao watashirikiana nao kupitia majadiliano ya kitaaluma yanayojikita katika uzoefu wa kazi za kila siku.

Amesema, mada zitakazowasilishwa zimeandaliwa mahsusi kuwasaidia Majaji hao kuelewa kwa kina majukumu yao mapya, ikiwemo misingi ya utoaji haki, masuala ya utawala wa Mahakama ya Rufani, mwenendo wa mashauri yanayosikilizwa mbele ya Jaji mmoja na yale yanayosikilizwa na jopo la Majaji, maombi ya mapitio (Revision) pamoja na tofauti za kiutendaji kati ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani.

Aidha, Jaji Kihwelo amesisitiza kuwa, mafunzo hayo pia yatawakumbusha Majaji umuhimu wa kuzingatia lengo kuu la Mahakama ambalo ni kutenda haki kwa wananchi, akieleza kuwa masharti ya kiufundi hayapaswi kuwa sababu ya kuchelewesha au kunyima haki pale mazingira ya kisheria yanaporuhusu haki kutendeka.

"Lengo kubwa la Mahakama ni kuamua migogoro na kuhakikisha haki inapatikana kwa mujibu wa Katiba na sheria. Tunapaswa kujikita zaidi katika kutatua migogoro kuliko kushikilia masharti ya kiufundi yanayoweza kuathiri upatikanaji wa haki," amesema.

Mbali na mada za kisheria, amesema washiriki watapata mafunzo kuhusu afya ya akili na namna ya kukabiliana na msongo wa mawazo, akibainisha kuwa afya njema ya Jaji ni msingi muhimu wa utoaji wa maamuzi yenye ubora.

Aidha, amesema mafunzo hayo yataendeshwa kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia, ambapo washiriki watapatiwa nyenzo zote za mafunzo kupitia mfumo wa ‘QR Code’, utakaowawezesha kupata maudhui yote ya sasa pamoja na mafunzo yaliyotolewa katika programu zilizopita kwa urahisi.

Mhe.Dkt. Kihwelo ameeleza kuwa, mfumo huo wa kidijitali unapunguza matumizi ya karatasi huku ukiwapa washiriki fursa ya kurejea nyenzo hizo wakati wowote wanapozihitaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akizungumzia mbinu ya ufundishaji, amesema mafunzo hayo yameandaliwa kwa mfumo wa majadiliano na kubadilishana uzoefu badala ya mihadhara ya kawaida, ili kuwawezesha washiriki kujifunza kupitia uzoefu wa vitendo kutoka kwa Majaji waliobobea katika kazi za Mahakama ya Rufani.

Alisema uzoefu wa mafunzo yaliyopita umeonesha kuwa mfumo huo umekuwa na mchango mkubwa katika kuwaandaa majaji wapya na kuongeza kujiamini kwao wanapoanza kutekeleza majukumu yao.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe.Dkt. Kihwelo aliishukuru Sekretarieti ya Mahakama ya Tanzania, hususan Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, pamoja na Sekretarieti ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), kwa maandalizi na ushirikiano uliowezesha kufanyika kwa mafunzo hayo.

Amesema ushirikiano huo unaendelea kuimarisha juhudi za Mahakama ya Tanzania katika kujenga mfumo endelevu wa maendeleo ya kitaaluma kwa Majaji na watumishi wake, hatua inayochangia kuimarisha utoaji haki nchini.



Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA)-Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akitoa neno la utangulizi leo tarehe 06 Julai, 2026 wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania na wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto wakisikiliza neno kutoka kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha IJA, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo leo tarehe 06 Julai, 2026 wakati wa ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani.

Meza Kuu ikipongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju. Kushoto ni 
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA)-Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani kwa pamoja wakiwa katika hafla ya ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 06 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani wanaopatiwa mafunzo elekezi. Katikati ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA)-Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO DODOMA YAWEKA MIKAKATI KUZUIA MLUNDIKANO WA MASHAURI

Na ARAPHA- RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma imeendelea kuimarisha usimamizi wa mashauri ya jinai na kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati, ambapo hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2026 haikuwa na shauri lolote la mlundikano.

Hali hiyo ilibainishwa tarehe 03 Julai,2026 katika kikao cha Usimamizi wa Mwenendo wa Mashauri ya Jinai (Case Flow Management) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano uliopo kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).

Kikao hicho kilifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, ambaye alikuwa mgeni rasmi  na kuhudhuriwa na Viongozi na wawakilishi wa Taasisi mbalimbali za mnyororo wa haki jinai, wakiwemo  Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), TAKUKURU, Idara ya Uhamiaji Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Ofisi ya Ustawi wa Jamii na Idara ya Uangalizi.

Viongozi wa Mahakama pamoja na Wadau wa mnyororo wa haki jinai walikutana kwenye kikao hicho kwa lengo la kutathmini mwenendo wa mashauri, kujadili changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuharakisha utoaji wa haki.

Akiwasilisha taarifa ya mashauri, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, alisema katika kipindi cha Januari hadi Juni 2026, Mahakama ilisajili mashauri mapya 499 na kusikiliza mashauri 519.

Kwa upande wa mashauri ya jinai, mashauri mapya 203 yalipokelewa na 187 yakisikilizwa, huku kiwango cha kumaliza mashauri kikiongezeka.

Alisema mafanikio ya kutokuwa na mashauri ya jinai ya mlundikano yametokana na utekelezaji wa mikakati mbalimbali ambayo Mahakama Kuu imejiwekea, ikiwemo kufanya mapitio ya mashauri na kubaini yale yanayoweza kukamilika katika hatua za awali.

Mikakati mingine ni kufanya vikao vya mara kwa mara vya mashauri ya jinai  na vikao Maalum”Clean up Sessions” na kuongeza  matumizi ya Mahakama Mtandao katika usikilizaji wa rufaa na maombi ya jinai.

Mhe. Ngitiri alieleza kuwa, pamoja na mafanikio hayo, Mahakama imebaini mashauri   nane ya jinai yanayoweza kuwa ya mlundikano  ifikapo Desemba 2026, huku mikakati mahsusi ikiwa tayari imewekwa ili kuhakikisha yanakamilishwa mapema iwezekanavyo.

Katika kikao hicho, Wadau walichangia hoja mbalimbali na walipitisha maazimio kadhaa, yakiwemo kuendelea kutekeleza mikakati ya Jaji Mkuu ya kuharakisha utoaji wa haki, kuyapa kipaumbele mashauri yanayokaribia kuwa ya mlundikano na kuimarisha ushirikiano katika kushughulikia mashauri yanayoweza kumalizika katika hatua za awali.

Aidha, Wadau hao walikubaliana kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya makosa ya mauaji kwa kushirikiana na Viongozi wa dini na Serikali ili kuimarisha kinga dhidi ya uhalifu.

Mhe. Tiganga alisisitiza  kuwa usimamizi madhubuti wa mashauri na ushirikiano wa Wadau wa sekta ya haki jinai ni msingi muhimu wa kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mhimili  wa Mahakama.

Meza kuu waliokaa ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, kulia kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kushoto kwake ni Kaimu Mkuu wa Mashtaka kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Dodoma, Bi Bertha Kulwa wakiwa katika kikako.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, ambae pia ni mgeni rasmi akifurahia jambo wakati wa kikao hicho.


 

Meza kuu waliokaa ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Joachim Tiganga, (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa kikao hicho kutoka ofisi mbalimbali. Kulia kwake waliokaa ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Kaimu Mkuu wa Mashtaka,Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Dodoma, Bi. Bertha Benedict.


 Meza kuu waliokaa ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Joachim Tiganga, (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa kikao hicho kutoka ofisi mbalimbali. Kulia kwake waliokaa ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Kaimu Mkuu wa Mashtaka, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Dodoma, Bi. Bertha Benedict.

 Sehemu ya wajumbe wa kikao hicho wakifuatilia kwa umakini kikao hicho.

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

Jumamosi, 4 Julai 2026

MAHAKIMU WA WILAYA NA MWANZO KIBAHA WAPIGWA MSASA KUHUSU MIRATHI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Kibaha

Mahakama ya Wilaya Kibaha imetoa mafunzo ya Mirathi kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo za Wilaya hiyo yakilenga katika maeneo muhimu kuanzia ufunguaji hadi ufungaji wa mashauri ya aina hiyo.

Mafunzo hayo ya siku moja yalifanyika tarehe 03 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Akizungumza wakati akimkaribisha Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha Mhe Emmael Lukumai amesema kutokana na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo Mahakimu katika usikilizaji wa mashauri ya mirathi,wameona ni vyema wapate mafunzo ambayo yatawaweka sawa ili kutatua changamoto wanazokutana nazo.

Mwezeshaji wa mafunzo hayo ambaye ni Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe.Simon Swai amewaeleza Mahakimu hao kuwa, anapoteuliwa Msimamizi wa Mirathi wamueleze taratibu zote kuepuka usumbufu huku akiwataka Mahakimu kuangalia uhalisia wa mali za marehemu ili waweze kutoa muda wa kufanya hesabu kutokana na wingi au uchache wa mali hizo.

"Mfano marehemu alikuwa na mali NSSF tu haihitaji muda mrefu sana wiki tatu tu zinatosha," alisema Mhe. Swai huku akiongeza kuwa, miongoni mwa maeneo hayo ni pamoja na kutambua kama hayo ni maombi ya Mirathi au ni maombi ya barua ya kusimamaia mirathi pamoja fomu zake, Mamlaka ya Mahakama kusikiliza shauri hilo, mchakato wa mapingamizi wakati wa uteuzi wa Msimamizi wa mirathi, uteuzi, uwasilishaji wa hesabu za mali za marehemu, usikilizwaji wa mapingamizi, akaunti maalum ya mirathi, kuhamisha umiliki wa mali za marehemu kwenda kwa warithi na ufungaji wa mirathi.

Aidha, Mhe. Lukumai amemshukuru Mhe. Swai kwa kukubali mwaliko huo wa kufika Mahakamani hapo kutoa mafunzo hayo na kukiri kwamba wamefurahi kwakuwa kulikuwa na changamoto wanazokumbana nazo na wameweza kupata ufumbuzi.

Hakimu Mkazi kutoka Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Simon Swai akiwafundisha Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na wa Mwanzo Kibaha namna bora ya usikilizwaji wa mashauri ya mirathi tarehe 03 Julai, 2026 kwenye  ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha.


 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho kwa Mwezeshaji wa Mafunzo ya Mirathi, Mhe.Simon Swai ambaye ni Hakimu Mkazi kutoka Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke.

Baadhi ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo na za Wilaya ya Kibaha wakifuatilia mafunzo ya namna bora ya usikilizwaji wa Mashauri ya Mirathi.

Hakimu Mkazi- Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-TemekeMhe.Simon Swai (kulia) akieleza yaliyomo katika Kitabu chake cha FAMILIA. Kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai.

Hakimu Mkazi- Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe.Simon Swai (kulia) akikabidhi kitabu cha FAMILIA kwa Mahakama ya Wilaya Kibaha kama zawadi. Kushoto ni Mhe. Emmael Lukumai akipokea kitabu hicho kwa niaba ya Mahakama ya Wilaya Kibaha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 


Ijumaa, 3 Julai 2026

MAHAKAMA MDAU MUHIMU KATIKA KUSIMAMIA USALAMA NA AFYA KAZINI; MTENDAJI MKUU OSHA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda amesema kwamba Mahakama ni mdau muhimu katika kusimamia masuala ya usalama na afya mahala pa kazi kwa kuwa Ofisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Mhimili huo katika kuhamasisha uwepo na uzingatiaji wa sheria, taratibu na kanuni mahala pa kazi.

Bi. Mwenda alieleza hayo jana tarehe 02 Julai, 2026 akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Mafunzo haya si tu kwamba ni kwa wafanyakazi kwa kuwa ninyi ni wafanyakazi wa ndani ya Mahakama, lakini vilevile tunatambua kazi yenu kubwa ya kufanya maamuzi. Kwa hiyo kuifahamu Sheria ya Usalama na Afya, majukumu yake... Tunafahamu mnafahamu ipo, lakini inavyotekeleza majukumu yake na mafunzo yatakayotolewa hapa basi hata katika kutoa maamuzi mna inakuwa wepesi, lakini tunategemea sana Mhimili huu wa Mahakama na Wahe. Majaji ninyi muweze kuwa msaada mkubwa sana kwetu katika kuhakikisha kwamba maeneo ya kazi yanazingatia sheria,” amesema Mtendaji Mkuu huyo.

Amesema kuwa, suala hilo pia inakutokana na kwamba Sheria ya Usalama na Afya imekuwa ni haki na kanuni ya msingi mahali pa kazi. Kwa hiyo kutozingatia Sheria ya Usalama na Afya maanake ni kutozingatia haki za binadamu.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo wa OSHA, amebainisha kuwa, uzingatiaji wa masuala ya usalama na afya mahala pa kazi ni sehemu ya haki za msingi za binadamu, kama ilivyopitishwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwaka 2022 kupitia Mikataba Namba 155 na 187.

Ameongeza kwa kusema kuwa, Majaji wana uwezo wa kusaidia kutoa mwongozo wa namna gani ambavyo pia Nchi inaendelea kuwa salama katika uzingatiaji wa haki za binadamu mahali pa kazi.

Kadhalika Bi. Mwenda amemshukuru Jaji Mkuu kwa kuruhusu mafunzo hayo kufanyikia katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma. Amewapongeza pia Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani walioteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia kwa kuaminiwa na kupewa dhamana hiyo kubwa.

"Sheria ya Usalama na Afya ya mwaka 2003 inatutaka kulinda nguvu kazi ya Taifa ili kuhakikisha uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kwa watumishi unaleta tija. Tunataka Majaji wetu wafanye kazi kwa miaka yote waliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu wakiwa na afya njema na salama," alisema Kiongozi huyo wa OSHA.

Ameongeza kwamba, kupitia mafunzo hayo, Majaji hao watapata uelewa wa kina wa jinsi OSHA inavyofanya kazi, hatua zinazofuatwa kuthibitisha magonjwa yanayotokana na kazi (work-related diseases), jambo litakalorahisisha utoaji wa maamuzi na utendaji wa haki pale ambapo mashauri ya namna hiyo yanapofikishwa Mahakamani.

Katika mafunzo hayo ya siku mbili, Wataalam wa OSHA na Madaktari Bingwa watatoa elimu kuhusu vihatarishi vya kemikali, biolojia, na vihatarishi vya ki-ergonomia vinavyotokana na uhusiano wa mfanyakazi na mazingira yake.

Mbali na mafunzo hayo, OSHA imeweka kambi maalum ya Madaktari Bingwa wa Mifupa, Mgongo na Macho kwa ajili ya kuwafanyia uchunguzi wa afya na kutoa ushauri wa kitiba kwa Viongozi na watumishi wa Mahakama, pamoja na kutoa mafunzo ya vitendo ya Uokoaji na Huduma ya Kwanza.

OSHA imesisitiza utayari wake wa kuendelea kushirikiana na Mhimili wa Mahakama, ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mazingira ya kazi katika majengo mbalimbali ya Mahakama nchini ili kuhakikisha yanakuwa salama wakati wote.

Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) ni Taasisi ya Serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) yenye jukumu la kusimamia Sheria Namba 5 ya Mwaka 2003 (Sura namba 297) ili kuzuia ajali, magonjwa na vifo vinavyotokana na mazingira ya kazi nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani, Kaimu Jaji Kiongozi, pamoja na Viongozi na Watendaji wakuu wa Mahakama na OSHA. 


Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda akitoa neno wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Baadhi ya Viongozi na Watumishi mbalimbali wa Mahakama na OSHA wakiwa katika hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akimkabidhi zawadi ya Saa Bi. Khadija Mwenda, Mtendaji Mkuu wa OSHA wakati wa Hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akipokea zawadi ya (First Aid Tool Box) kutoka kwa Bi. Khadija Mwenda, Mtendaji Mkuu wa OSHA wakati wa Hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa OSHA walioshiriki ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Alhamisi, 2 Julai 2026

‘USALAMA NA AFYA MAHALI PA KAZI; MSINGI WA UTAWALA BORA NA UTOAJI HAKI’

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina amesema kuwa, masuala ya usalama na afya si jambo la hiyari bali ni sehemu muhimu ya utawala bora na utoaji haki wenye ufanisi.

Jaji Mlyambina ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Rufani ameyasema hayo leo tarehe 02 Julai, 2026 alipokuwa akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

"Tumekuza utamaduni wa usalama na afya mahala pa kazi ndani ya Mhimili wa Mahakama. Kupitia ushirikiano huu thabiti na OSHA, tumeshaendesha mafunzo kwa Majaji, Wasajili, Mahakimu, watumishi wa kada za utendaji, na hata watumishi wenye ulemavu. Msisitizo wetu ni kwamba usalama na afya ni haki ya kila mfanyakazi bila ubaguzi," amesema Jaji Mlyambina.

Mratibu huyo ameeleza juu ya mafanikio ya mafunzo ya aina yake yaliyofanyika mwaka jana (2025) jijini Mwanza (Malaika Hoteli) ambapo teknolojia ya kisasa ilitumika kuunganisha kumbi mbili tofauti ili Viongozi na Kada saidizi (Majaji na Madereva) wapate mafunzo yanayoendana na majukumu yao kwa wakati mmoja.

Mhe. Dkt. Mlyambina amesema baada ya mafunzo hayo, walitembelea katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ambapo waliendelea kujifunza kuhusu haki kazi katika mazingira ya mbugani, ambapo walidhihirisha kwamba usalama na afya mahala pa kazi ni suala ambalo linahusu kila eneo la kazi na kila mazingira ya utendaji.

Aidha, Mhe. Dkt. Mlyambina amesema kwa awamu hii, mafunzo yanalenga kujenga uwezo wa Majaji wa Rufani wapya na viongozi waandamizi, kutekeleza Sheria ya OSHA, inayomtaka kila mwajiri kuweka mazingira salama ya kazi, kuhimili changamoto za kisaikolojia, hasa kukabiliana na msongo wa mawazo (stress) na madhara ya kisaikolojia yanayotokana na kazi za utoaji haki (vicarious trauma) na kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Mwaka, 2050 kupitia watumishi wenye afya bora na tija kubwa.

Ameongeza kwamba, lengo ni kuwafikia Viongozi na Watumishi wote wa Mahakama kwa awamu ili kila mmoja, popote alipo, apate uelewa na ujuzi wa kujilinda na kulinda wenzake mahala pa kazi.

“Tunamini kwamba Mahakama yenye Viongozi na Watumishi wanaozingatia usalama na afya mahala pa kazi ndio inayoweza kutoa haki kwa ufanisi zaidi na kuchangia maendeleo endelevu ya taifa, na hasa katika kutekeleza Dira ya Taifa ya mwaka 2050,” ameeleza Jaji Mlyambina.

Kadhalika, Jaji Mlyambina ameongeza kuwa, ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na OSHA unaendelea kuwa mfano wa kuigwa katika Taasisi za umma, ukionesha namna utekelezaji wa Sheria za Usalama kazini unavyoweza kuongeza ufanisi, kulinda nguvu kazi ya Taifa na kuhakikisha haki inatendeka katika mazingira salama na yenye staha.

“Mhe. Jaji Mkuu, kwangu binafsi, mafunzo haya yana maana ya kipekee. Mbali na kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, ninayo heshima ya kuwa Mratibu wa mafunzo haya. Katika kipindi nilichohudumu kama Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mahakama imejenga na kuimarisha ushirikiano wa karibu na Wadau wa haki kazi, ikiwemo pamoja na OSHA Tanzania,” ameeleza Mhe. Dkt. Mlyambina.

Aidha, Jaji Mlyambina amempongeza Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, kwa utendaji kazi wake uliotukuka na wa kizalendo, ikiwa ni pamoja na kufadhili mafunzo hayo na kutoa vifaa kinga ili kuboresha mazingira ya utendaji kazi wa Majaji.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mlyambina ametumia jukwaa hilo kumpongeza Dkt. John Anthony Jingu kufuatia kuteuliwa kwake na Rais wa Jamhuri ya Munungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania.

Mafunzo hayo yamebeba Kaulimbiu isemayo, "Nafasi ya Haki Kazi, Afya na Usalama Mahala pa Kazi kwa Maendeleo Endelevu."


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina akitoa neno leo tarehe 02 Julai, 2026 wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Washiriki wa mafunzo pamoja na baadhi ya Viongozi waalikwaJaji  kutoka Mahakama wakimsikiliza Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina alipokuwa akitoa neno leo tarehe 02 Julai, 2026 wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.