Ijumaa, 17 Aprili 2026

MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO SIMIYU YASHIRIKI MAADHIMISHO YA WIKI YA USULUHISHI

  •   Yawaelimisha Wadau wa Mahakama umuhimu wa Usuluhishi kupitia Kongamano maalum

Na NAUMI SHEKILINDI, Mahakama-Simiyu

Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Simiyu nayo imeungana pamoja na Mahakama nyingine nchini kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi nchini ambayo iliyoanza tarehe 14 Aprili, 2026 na kufikia tamati tarehe leo tarehe 17 Aprili, 2026.

Katika Maadhimisho hayo, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu imefanikiwa kufanya kongamano la Usuluhishi tarehe 16 Aprili, 2026 likiongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Hussein Mtembwa pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo Watumishi wa Mahakama, Polisi, Taasisi za kibenki, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Uhamiaji, Wakala wa Vipimo, TUGHE, Viongozi wa dini na wananchi.

 Mhe. Mtembwa alifungua kongamano hilo na kueleza kuwa lengo la Wiki ya Usuluhishi ni kupunguza muda wa mashauri mahakamani, kupunguza gharama za mashauri na kuwezesha suluhu ya haraka na ya kirafiki, “Mfano benki wanapofanya usuluhishi baina ya benki na mteja inajenga mahusiano mema na ya kirafiki baina ya benki na mteja” amesisitiza Jaji Mtembwa.

Aidha, Mhe. Mtembwa aliongeza kwa kusema, “Haki sio tu kuhukumu bali pia kusuluhisha,” alieleza kuwa usuluhishi una mchango mkubwa katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwani amani, usalama na utulivu ndio msingi utakaojenga umoja ndani ya nchi, vilevile Mahakama imejipanga kukuza dhana ya usuluhishi kama ilivyo kwenye Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, (1977) na kwamba ana imani kongamano hilo litaleta tija kwa jamii.

Naye, Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Elimo Daniel Massawe alitoa mada juu ya usuluhishi wa migogoro ya Tanzania ambapo alieleza maana ya usuluhishi, lengo, faida zake pamoja na mbinu za kufanya usuluhishi.

Mhe. Massawe alieleza kwamba, usuluhishi ni sehemu rasmi ya mfumo wa sheria unaotambuliwa na taratibu za Mahakama nchini, pia ni utaratibu unaowapa wahusika nafasi ya kusuluhisha mgogoro wao kwa hiari na kwa msaada wa mtu wa kati asiye na upendeleo, lakini pia mpatanishi sio mtoa uamuzi bali wahusika ndio wenye mamlaka ya mwisho.

Wakati wa kuhitimisha kongamano hilo, Kaimu Jaji Mfawidhi alisema kuwa, kongamano hilo litakua chachu katika kuimarisha usuluhishi na kuwaomba wadau waende kuwa Mabalozi wa Usuluhishi  kabla ya wadaawa kufika Mahakamani.

   Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Hussein Mtembwa akifungua Kongamano la Usuluhishi kwa wadau waliohudhuria kongamano hilo lililofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 katika Mahakama hiyo.


Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Elimo Daniel Massawe akitoa mada juu ya Usuluhishi kwa wadau waliohudhuria Kongamano hilo.

   Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Simiyu, Mhe. Elimo Massawe (aliyesimama) akimkaribisha Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Hussein Salum Mtembwa (katikati) kuzungumza  na wadau wakati wa Kongamano hilo.

    Wadau mbalimbali waliohudhuria kongamano wakisikiliza mada kutoka kwa Mhe. Elimo Daniel Massawe, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Simiyu.

   Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Hussein Mtembwa (katikati mstari wa mbele ) akiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali aliohudhuria Kongamano la Usuluhishi katika Mahakama Kuu Masjala ndogo Simiyu.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara) 

Hitimisho Wiki ya Usuluhishi Dodoma

WATUMISHI IJC DODOMA WANUFAIKA NA MAFUNZO YA USULUHISHI

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma

Watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma wamepatiwa mafunzo maalum yanayohusu matumizi ya usuluhishi katika kushughulikia migogoro ya kiutawala na kikazi, ikiwa ni sehemu ya hitimisho la Wiki ya Usuluhishi kwenye Mahakama hiyo.

Mafunzo hayo yamefanyika leo tarehe 17 Aprili, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano, kuhitimisha Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi. Mafunzo hayo yalilenga kuimarisha ufanisi kazini na kujenga utamaduni wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo.

Mafunzo hayo yalisimamiwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ametoa elimu ya kina kuhusu dhana nzima ya usuluhishi na matumizi yake katika mazingira ya kazi.

Amesisitiza kuwa usuluhishi ni nyenzo muhimu katika kuongeza tija, kuimarisha mahusiano ya kikazi na kupunguza migogoro isiyo ya lazima katika Taasisi za umma.

Mafunzo hayo yaliwashirikisha pia Viongozi wa Dini ambao walitoa mchango mkubwa katika kuelezea nafasi ya usuluhishi kwa mtazamo wa kidini.

Kwa upande wa dini ya Kikristo, Bw. Ford Saileni alitoa mafundisho yaliyolenga kuhimiza amani, msamaha na maridhiano kama msingi wa kutatua migogoro.

Aidha, kwa upande wa dini ya Kiislamu, Ustadh Bwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma alieleza umuhimu wa suluhu (usuluhishi) kama sehemu ya mafundisho ya dini, akisisitiza haki, uvumilivu na maelewano katika jamii.

Mafunzo hayo hayakuwa ya kawaida, bali yalipambwa na shamrashamra mbalimbali zilizoongeza hamasa kwa washiriki. Vipengele vya maigizo vilivyowasilishwa na baadhi ya Watumishi pamoja na Wasanii walioalikwa vilionyesha kwa vitendo namna usuluhishi unavyoweza kutumika katika kutatua migogoro kwa njia ya kirafiki na yenye tija.

Watumishi walioshiriki walionesha kufurahishwa na mafunzo hayo, wakieleza kuwa yamewajengea uelewa mpana zaidi na kuwapa mbinu bora za kushughulikia changamoto za kikazi. Walibainisha kuwa elimu hiyo ina manufaa makubwa katika kuboresha utendaji wao pamoja na kuimarisha mshikamano kazini.

Kwa ujumla, mafunzo hayo yameacha alama chanya kwa Watumishi wa IJC Dodoma, yakionesha wazi umuhimu wa usuluhishi katika kujenga mazingira bora ya kazi na utoaji haki wenye ufanisi zaidi.

Ikumbukwe kuwa Wiki ya Usuluhishi nchini yalizinduliwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, tarehe 13 Aprili, 2026. Maadhimisho hayo yalienda sambamba na kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania.”

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (aliyesimama) akizungumza wakati wa kutoa mafunzo ya usuluhishi kwa Watumishi wa Mahakama IJC Dodoma.

Mchungaji Ford Saileni (aliyesimama) akiwasilisha mada ya usuluhishi kwa upande wa dini ya kikristo katika mafunzo ya watumishi wa IJC Dodoma.

 

Ustadhi Mbwana Haji akiwasilisha mada ya usuluhishi kwa upande wa Kiislamu wakati wa mafunzo ya usuluhishi kwa watumishi wa Mahakama wa IJC Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo kutoka Wizara ya Katiba na Sheria. Waliokaa kushoto kwake ni Ustadh Mbwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma na kulia kwake ni Mchungaji Ford Saileni.


 Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo ambao Maofisa Usafirishaji wa IJC Dodoma. Waliokaa kushoto kwake ni Ustadh Mbwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma na kulia kwake ni Mchngaji Ford Saileni.

 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki na wakufunzi wa mafunzo hayo ambao ni Mahakimu, Mawakili pamoja na Watumishi (waigizaji) waliopamba mafunzo hayo ya usuluhishi kwa watumishi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Wiki ya Usuluhishi Dodoma

WANAFUNZI UDOM WAPATA ELIMU KUHUSU USULUHISHI

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma.

Katika kuendelea kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi nchini, Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamepata fursa adhimu ya kupatiwa elimu muhimu ya usuluhishi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwaandaa vijana kuwa mabalozi wa amani na utatuzi wa migogoro katika jamii.

Elimu hiyo imetolewa jana tarehe 16 Aprili, 2026 katika moja ya kumbi za mikutano zilizopo ndani ya Chuo hicho, ambapo Wanafunzi walijitokeza kwa wingi kushiriki na kujifunza kwa kina kuhusu mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro, nje ya mfumo wa kawaida wa Mahakama.

Watoa mada katika mafunzo hayo walikuwa ni Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria, wakiwemo Mahakimu, Mawakili wa Serikali pamoja na Mawakili wa Kujitegemea. Wadau hao waliotoa uzoefu wao wa vitendo na kusisitiza umuhimu wa usuluhishi katika kuharakisha haki, kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani na kudumisha mahusiano mema katika jamii.

Mafunzo hayo yalisimamiwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan.  Kupitia usimamizi wake, zoezi hilo lilifanikiwa kwa kiwango cha juu, likiwaacha Wanafunzi na uelewa mpana pamoja na hamasa ya kujifunza zaidi kuhusu taaluma ya sheria na mbinu za kisasa za utatuzi wa migogoro.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mhe. Dkt Fatma   alisisitiza kuwa kuwafikia Wanafunzi ni uwekezaji muhimu kwa mustakabali wa Taifa, kwani wao ndio watakaobeba dhamana ya kusimamia haki na amani katika jamii siku zijazo.

Kwa upande wao, Wanafunzi walionesha mwamko mkubwa na shauku ya kujifunza, wakieleza kuwa elimu hiyo imewafungua macho na kuwapa mtazamo mpya juu ya namna bora ya kushughulikia migogoro bila migongano mikali.

Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi yanaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini, yakilenga kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro, badala ya kutegemea Mahakama pekee.

Kwa ujumla, utoaji wa elimu hiyo kwa Wanafunzi wa UDOM, ambao wanachukua taaluma ya sheria ni hatua muhimu katika kujenga kizazi chenye uelewa, busara na uwezo wa kuleta suluhu za kudumu katika jamii, ikiwa ni msingi imara wa amani na maendeleo ya Taifa.

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan, akiwa katika Ukumbi Chuo cha Udom pamoja na Wanafunzi wakisikiliza neno la ukaribisho kutoka kwa Mkufunzi, Dkt Gamba (hayupo pichani)).

 

Wanafunzi wa Sheria Chuoni cha UDOM wakisikiliza kwa makini elimu ya usuluhishi kutoka kwa watoa mada.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, akifafanua jambo wakati wa utoaji elimu ya usluhishi kwa Wanafunzi wanaosomea sheria UDOM.

 

Wakili wa Kujitegemea, B. Elias Macibya, akifafanua jambo kuhusu usuluhishi wakati wa mafunzo hayo.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (aliyevaa mtandio wa blue) akiwa katika picha ya pamoja na watoa mada pamoja na baadhi ya Wanafunzi mara baada ya mafunzo hayo.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

LINDI YAWASISITIZA WADAU KUIMARISHA USHIRIKIANO, KUBORESHA UTOAJI HAKI

Na. HILARI GDIYE NA WINIFRIDA KISAMO – Mahakama, Lindi

Wadau wa Sekta ya Haki mkoani Lindi wamehimizwa kuongeza na kuimarisha ushirikiano katika uendeshaji wa mashauri ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema ipasavyo na kwa ufanisi.

Akizungumza katika kikao cha wadau kilichofanyika hivi karibuni, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Sylester Kainda alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu miongoni mwa wadau wote wa Sekta ya haki ili kutotoa nafasi ya kuchelewesha mashauri yanapofunguliwa mahakamani.

Mhe. Kainda amesema kuwa, mafanikio ya Mahakama yanategemea mchango wa pamoja wa kila mdau. Alibainisha kuwa kikao hicho kililenga kuweka mkakati madhubuti wa namna bora ya kuendesha shughuli za Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Lindi kwa ufanisi, uwazi na kasi na kuhakikisha huduma za haki zinatolewa kwa wakati mapema ipasavyo na kwa viwango vinavyotarajiwa.

Aidha, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa, Mahakama haiwezi kusimama peke yake bila ushirikiano wa wadau wake, akiwataka wadau wote kutambua nafasi zao katika kuhakikisha mchakato wa haki unakuwa thabiti na wenye matokeo chanya kwa jamii.

Vilevile, Mhe. Kainda alisisitiza umuhimu wa kumaliza mashauri kwa wakati ili kuwawezesha wananchi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi bila ucheleweshaji usio wa lazima, kwa mujibu wa takwimu Mkoa wa Lindi una mashauri machache, hali inayotoa fursa kwa Mahakama kuhakikisha kesi zote zinakamilika kabla ya mwezi Disemba, 2026.

“Kwa idadi ndogo ya mashauri yaliyopo ni matarajio yetu kwamba, Mahakama zetu zifike hatua ya kumaliza kesi zote kwa wakati na hata kuwa, katika nafasi ya kusubiri mashauri mapya,” alisema Jaji Kainda.

Jaji Mfawidhi huyo, alifafanua kuwa, mfumo wa kimahakama hupima ufanisi kwa kuzingatia muda unaotumika kusikiliza na kumaliza mashauri, hivyo Mahakama zinapaswa kuepuka uwepo wa kesi za muda mrefu zinazoleta mlundikano wa mashauri.

Akizungumzia suala la mashahidi, Mhe. Kainda alisema kuwa, matumizi ya teknolojia yamerahisisha usikilizwaji wa mashahidi kwa njia ya mtandao (remote hearing), hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya umbali na gharama.

Hata hivyo, alionya kuwa baadhi ya mashauri huathirika kutokana na mapungufu katika uendeshaji wake, akiwataka Mahakimu na wadau kuongeza umakini katika maandalizi na usikilizwaji wa mashauri ili kulinda haki za wahusika wote katika shauri husika. Pia alikemea vitendo vya rushwa na ucheleweshaji wa majalada ya kesi, akisisitiza kuwa maadili na uadilifu vinapaswa kupewa kipaumbele katika utoaji wa haki.

Katika jitihada za kurahisisha huduma kwa wananchi, Jaji Kainda alieleza kuwa, utambulisho wa wadhamini unaweza kuthibitishwa kwa kutumia Kitambulisho cha Taifa (NIDA) pekee, bila ulazima wa kuwasilisha barua za utambulisho kutoka kwa viongozi wa vijiji au Serikali za mitaa.

Kwa upande wa maboresho ya mifumo kiteknolojia, Mhe. Kainda alisema kuwa, Mahakama Kuu Lindi na Mahakama zake za chini zimeshanza kutumia mfumo wa kielektroni (paperless), hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kupunguza matumizi ya karatasi.

Jaji Mfawidhi huyo, ameyahimiza mabaraza ya ardhi kuhakikisha yanatoa nakala za hukumu kwa wakati ili kuwawezesha wananchi kupata haki zao bila ucheleweshaji usio wa lazima.

Wadau walikubaliana juu ya umuhimu wa ushirikiano, uwajibikaji na matumizi ya teknolojia katika kuimarisha utoaji wa haki, hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi wa Mahakama katika utoaji wa haki kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi akiwasilisha Mada wakati wa Kikao na Wadau. Wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (kulia)

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.


Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (aliyesimama) akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.

Mdau wa Mahakama Kutoka Ofisi ya Huduma ya Uangalizi wa Jamii Bi. Wilhelmina Qambalo akitoa hoja wakati wa kikao hicho.

Wadau wakifuatilia kwa Makini Mada zilizokuwa zinawasilishwa wakati wa kikao.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Sylivester Kainda (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama) 



BARAZA LA WAFANYAKAZI DAR ES SALAAM LAKUTANA; JAJI MFAWIDHI AWAKUMBUSHA WAFANYAKAZI, WADAU KUWAJIBIKA IPASAVYO

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Mussa Maghimbi ametoa rai kwa wafanyakazi wa Mahakama na Wadau kwa ujumla kuwajibika ipasavyo ili kuhakikisha maono ya Mahakama ya Tanzania ifikapo 2050, iwe ya mfano duniani katika utoaji haki kama chombo huru chenye kuzingatia weledi, maadili, ufanisi na inayoaminiwa na wananchi katika jamii inayowazunguka.

Mhe. Maghimbi aliyasema hayo jana tarehe 16 Aprili, 2026 alipokuwa akiongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari jijini Dar es Salaam.

Katika hotuba yake Jaji Maghimbi, alisema maono hayo hayawezi kufikiwa kufikiwa bila kuwa na mikakati madhubuti katika utoaji haki ikiwa ni pamoja na kuimarisha upatikanaji wa haki, kuongeza imani kwa wananchi, kuimarisha uwezo wa rasilimali watu na kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Amesema kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 107A, Mhimili wa Mahakama ni Mamlaka yenye kauli ya mwisho katika Utoaji Haki katika Jamhuri ya Muungano, na Ibara ya 107B ya Katiba inatamka kuwa katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, Mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya Katiba na yale ya Sheria. “Ibara hizi zinatarajia watumishi kujipanga kimkakati na kuzingatia uadilifu, weledi, uwajibikaji na kwa kulenga matokeo makubwa,” amesisitiza.

Hali kadhalika, Jaji Maghimbi amewakumbusha wajumbe hao ahadi ambazo Mahakama imetoa kwa wananchi kwa wadau na kwa wanaofuata huduma mbalimbali mahakamani kuwa Maadhimisho ya Siku ya Sheria  kwa mwaka huu yaliongozwa na Kaulimbiu isemayo; “Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa,” ambapo waliahidi kuwa Viongozi na Wafanyakazi wa Mahakama  kutumia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kama kichocheo cha maboresho makubwa zaidi katika Mhimili wa Mahakama.

Akizungumzia kuhusu dhumuni ya Baraza la Wafanyakazi, Jaji Mfawidhi huyo na Mwenyekiti wa Kikao hicho alieleza kuwa ni kutoa fiursa kwa watumishi kupitia wawakilishi kujadili juu ya masuala ya msingi yanayohusu tija na ufanisi kwa upande mmoja na upande mwingine maslahi yao kama watumishi.

Aidha, Mhe. Maghimbi amesema kuwa, Wawakilishi wa Mabaraza ya Kanda wanatekeleza kwa vitendo takwa la kisheria linalotokana na Tamko la Rais (Tamko Na. 1 la Mwaka 1970) na Sheria nyingine za kazi zinazohimiza kuwakilisha wafanyakazi katika kufanya maamuzi mbalimbali kupitia Mabaraza ya Wafanyakazi.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti amesema, vikao vya Mabaraza ya Wafanyakazi viko kisheria na lengo la kuanzishwa kwa Mabaraza hayo ni kuwapa fursa watumishi ya kushauri Menejimenti, kuwaunganisha watumishi na menejimenti kusuluhisha  changamoto mbalimbali, kutoa shida zao za kiutumishi na maslahi, na wao kama Kanda wakishindwa zitawasilishwa Makao Makuu.

Amesema pia, Mabaraza hayo ni mahali pa kupata mrejesho wa mambo yanayofanyika ndani ya Kanda na mrejesho kwa ngazi ya Taifa.

Kabla ya kikao hicho kuanza kilitanguliwa na uchaguzi uliosimamiwa na Ofisa Kazi, Bi. Vaileth Ndeza wa kujaza nafasi zilizoachwa wazi baada ya Katibu kuhama Kanda ya Dar es Salaam na Katibu msaidizi kufariki dunia.

Wajumbe hao walimchagua Bw. Shadrack Mlomo kuwa Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dar es Salaam na Mhe. Juliana Nankoma kuwa Katibu Msaidizi na pia Wilky Kavunjika alichaguliwa kuwa Mjumbe.

Katika kikao hicho walikuwepo Maofisa kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) ambapo wameeleza faida za mifuko hiyo kwa watumishi wa umma.

Vikao hivyo vimekuwa vikifanyika kila mwaka na wajumbe kuwasilisha hoja zao na pia kushauri kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu utumishi na maslahi ya watumishi kwa ujumla.

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda ya Dar es Salaam wakiwa katika kikao cha baraza hilo jana tarehe 16 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari jijini Dar es Salaam.

 Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda ya Dar es Salaam wakiimbo wimbo wa wafanyakazi (solidarity forever).


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda hiyo, Mhe Salma Maghimbi (katikati) pamoja na Bw. Shadrack Mlomo (kushoto) ambaye ni Katibu wa Baraza hilo na Mhe. Juliana Nankoma (kulia) ambaye ni Katibu Msaidizi wa Baraza wakiimba wimbo wa wafanyakazi ujulikanao kwa jina la (solidarity forever) wakati wa Kikao hicho.


 Meza Kuu ikiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dar es Salaam. Katikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo, Mhe. Salma Mussa Maghimbi, kushoto ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana na kulia (aliyesimama) ni Mtendajiwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,  Bw. Sumera Manoti.

Ofisa Kazi, Bi. Vaileth Ndezi akitoa utaratibu wa kufanya uchaguzi wa Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe wakati wa kikao hicho. 

Bw.Wilcky Kavunjika akitoa shukurani kwa wajumbe baada ya kuchaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi Taifa.


Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana akitoa taarifa ya mashauri wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam. 

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti akitoa taarifa ya utawala wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam. 


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara)

 

 

MANYARA YAENDESHA MAFUNZO YA USULUHISHI KWA WADAU

Na. CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora amejumuika na wadau wa Mahakama katika kuendesha mafunzo ya Wiki ya Usuluhishi yakiwa na lengo la kuwajengea wadau wa haki madai uwezo wa kusuluhisha migogoro kwa njia za upatanishi, elimu hiyo ilitolewa katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mhe. Kamuzora alieleza kuwa, usuluhishi ni silaha ambayo inamaliza na kutatua migogoro na matatizo katika jamii kuliko hata kufika mahakamani na kusikiliza mashauri.

“Tukiachana na mashauri ya jinai yanayohusu makosa au uhalifu mkubwa, mashauri mengi ya madai yanaweza kwisha kwa kutumia Suluhu ambazo tunaweza kufanya wenyewe. Usuluhishi unasaidia sana katika kuokoa muda na gharama ambazo tunaweza kuzitumia wakati tumefungua mashauri mahakamani,” alieleza Mhe. Kamuzora.

Akitoa neno la utangulizi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo, aliwaasa watu wote kutumia muda wao kusikiliza elimu ambayo itatolewa kwa sababu ni ya msingi sana na ina tija katika kutatua migogoro mbalimbali katika jamii.

“Wananchi wengi mnafika mahakamani kwa ajili ya kutatua migogoro ambayo kimsingi mngeweza kuimaliza wenyewe kwa sababu mmekosa elimu hii ya usuluhishi. Hivyo, ninawasihi sana msikilize kwa makini yale ambayo yatakuwa yanafundishwa na wataalamu wetu,” alisema Mhe. Mpepo.

Naye, Wakili wa Kujitegemea Bw. Kuyengwa Ndonjekwa alisema kuwa, elimu hiyo ni muhimu sana kuendelea kutolewa mara kwa mara kwa sababu ina madhumuni ya kupunguza mzigo mkubwa kwa Mahakama wa kusikiliza mashauri na kuwafanya wananchi wapatane wenyewe kuliko kuendelea kuleta mashauri mahakamani hususan kwa masuala ambayo yanaweza kuzungumzika na suluhu ikapatikana.

Kwa upande wake mdau wa Mahakama Bw. Gwandu Nada ambaye ni mwananchi kutoka katika Wilaya ya Babati aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kufanya elimu hiyo ya upatanishi kuwa endelevu kwani itaisaidia jamii kuokoa muda wa kwenda mahakamani kutatua migogoro isiyokuwa na tija.

“Mafunzo haya ni mazuri kwa kuwa yamenifundisha kupatana na washtaki wangu mapema kabla ya kufikishana katika vyombo vya sheria na ninaahidi kwenda kupatana na wale ambao nimekosana nao kwa njia ya usuluhishi,” alisema Bw. Nada.

Waliohudhuria kupata elimu hiyo ni wadau wa Mahakama pamoja na wadaawa waliofika kwa ajili ya kupata mafunzo ya usuluhishi, Watumishi wa Mahakama Kuu Manyara, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Mwakilishi kutoka Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia, Ofisi ya Ustawi wa Jamii pamoja na baadhi ya wananchi.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora akitoa neno wakati wa utoaji elimu ya Usuluhishi iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu. Kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara Mhe. Mariam Lusewa.

Sehemu ya wananchi wakifuatilia mafunzo ya upatanishi 

Afisa Huduma kwa Jamii Mkoa wa Manyara Bw. Tumaini Moshi akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi waliofika Mahakama Kuu Manyara kupata elimu hiyo.

Mwananchi wa Wilaya ya Babati akitoa maoni yake wakati wa mafunzo elimu ya Wiki ya usuluhishi yaliyofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Kimario akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi waliofika Mahakama Kuu Manyara kupata elimu hiyo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo kushoto akizungumza na mmoja wa Wananchi waliofika kupata elimu ya upatanisho kwenye maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi. 

Sehemu ya wananchi waliohudhuria mafunzo ya wiki ya usuluhishi wakiwa katika picha ya Pamoja na Meza Kuu wakati wa utoaji elimu ya Wiki ya usuluhishi iliyofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Alhamisi, 16 Aprili 2026

WADAU WA SHERIA WANUFAIKA NA MAFUNZO MAALUM YA UTATUZI WA MIGOGORO

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu, Dodoma.

Mahakimu na Mawakili wa Mkoa wa Dodoma wameendelea kupatiwa elimu muhimu kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, hatua inayozidi kuimarisha mifumo ya haki na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kisheria nchini.

Mafunzo hayo yaliyofanyika jana tarehe 15 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dodoma kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) yamewakutanisha Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria.

Lengo la mafunzo hay oni kujengeana uelewa wa kina kuhusu matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR), njia inayozidi kupata nafasi kubwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka na kwa gharama nafuu.

Akitoa neno la ukaribisho, Naibu Msajili wa Mahakaa Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, aliwahimiza washiriki kutumia ipasavyo jukwaa hilo muhimu kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha weledi wao katika kushughulikia migogoro ya Wananchi.

Mafunzo hayo yaliendeshwa chini ya uratibu mahiri wa Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ameendelea kuonesha uongozi thabiti, weledi wa hali ya juu pamoja na dhamira ya dhati ya kuendeleza usuluhishi nchini.

Kupitia jitihada zake, Wadau wa Sheria wameendelea kunufaika na elimu yenye tija, huku akihamasisha kwa vitendo matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama suluhisho endelevu.

Mada mbalimbali ziliwasilishwa wakati wa mafunzo hayo na wataalamu wa sheria, akiwemo Mhe. Thurstone Kombe, Mhe. Sarah Mwalilino, Mhe. Judith Barigenge pamoja na wengine kutoka Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi nyingine kama CHRAGG.

Mada hizo zilieleza kwa kina umuhimu wa usuluhishi katika kupunguza migogoro, kuokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha mahusiano katika jamii.

Akisimamia majadiliano, Mhe.  Dkt. Khalfan alisisitiza kuwa usuluhishi si tu njia mbadala, bali ni nyenzo muhimu ya kujenga jamii yenye amani na mshikamano, huku akitoa wito kwa Wadau wa Sheria kuendelea kuipa kipaumbele.

Washiriki walipata nafasi ya kuuliza maswali na kuchangia hoja mbalimbali, hali iliyoonesha mwitikio mkubwa na uhitaji wa elimu hiyo katika jamii ya Wanasheria.

Akitoa neno la shukrani, Mhe. Zabibu Mpangule aliwashukuru waandaaji pamoja na washiriki wote kwa ushiriki wao, akibainisha kuwa mafunzo hayo yameongeza thamani kubwa katika utendaji wao wa kila siku.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa hotuba ya kufunga kutoka kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara ya Katiba na Sheria, aliyesisitiza umuhimu wa kuendeleza elimu ya usuluhishi ili kuhakikisha Wananchi wanapata haki kwa wakati, kwa ufanisi na kwa amani.

Kwa ujumla, tukio hili limeacha alama kubwa katika Mkoa wa Dodoma, likiwa ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za kuifanya Tanzania kuwa kinara wa matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati). Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


 

Mahakimu pamoja na Mawakili mbalimbali waliohudhuria elimu hiyo ya usuluhishi katika ukumbi uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo.

 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, akitoa neno la ukaribisho kwa wajumbe hao waliohudhuria elimu ya usuluhishi kwa Mahakimu na Mawakili.

 Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, akifuatilia kwa makini mada inayotolewa wakati wa utoaji wa elimu kwa Mahakimu na Mawakili.


 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu wa Dodoma walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi. Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watoa ujumbe maalumu kuhusu elimu ya usuluhish,i ambao pia ni Watumishi wa Mahakama Dodoma wakati wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.