Jumamosi, 7 Februari 2026

WATUMISHI WA MAHAKAMA MBEYA WATEMBELEA KITUO CHA KULEA WATOTO YATIMA CHA NURU

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa, wamefanya ziara ya kutembelea Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru. Ziara hiyo imefanyika tarehe 30/01/2026 na kuhusisha watumishi kutoka Mahakama Kuu Mbeya, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mahakama ya Wilaya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama za Mwanzo mkoani Mbeya. Aidha, ziara hiyo pia ilihudhuriwa na wadau wengine katika mnyororo wa utoaji haki, wakiwemo Jeshi la Polisi na Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya.

Watumishi hao walipokelewa na Meneja wa Kituo hicho, Bi. Mary Kassim Himiri, ambaye alitoa maelezo ya utangulizi kwa kuelezea historia fupi ya Kituo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2005 hadi sasa, pamoja na hali ya Kituo kwa sasa. Alieleza kuwa kwa sasa kituo kina watoto arobaini (40), ambapo wanne (04) kati yao wamehitimu elimu ya Sekondari Kidato cha Nne mwaka 2025. Aliongeza kuwa baadhi ya watoto wamechukuliwa na watu waliokuwa na nia ya kuwalea, kwa kufuata taratibu zilizowekwa na Kituo hicho kwa kushirikiana na Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya.

Aidha, Bi. Mary Himiri alizungumzia suala la ufadhili, ambapo alisema kuwa kwa sasa kituo hakina mfadhili wa kudumu na kinategemea misaada midogo midogo kutoka kwa watu binafsi au Taasisi zinazojitolea kusaidia pale inapohitajika.

“Hapo awali tulipata ufadhili kutoka Ubalozi wa Japan ambao walitujengea majengo mawili. Hata hivyo, tangu mwaka 2016, baada ya mwanzilishi wa kituo kufariki, hatuna tena ufadhili wa kudumu. Kwa sasa, tunategemea msaada wa watu binafsi wanaoguswa na hali ya Kituo na kujitolea kusaidia,” alisema Bi. Mary Kassim Himiri, Meneja wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru.

Kwa upande wake, Mhe. Victoria Nongwa akizungumza machache baada ya kukabidhi zawadi walizokwenda nazo kituoni hapo, ambapo alitoa shukrani na pongezi kwa uongozi wa kituo kwa kazi kubwa wanayoifanya.

“Tunatambua mchango mkubwa wa asasi hizi katika malezi ya watoto yatima na wenye mahitaji maalum. Tunatoa pongezi za dhati kwa uongozi na walezi wote wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru kwa jitihada mnazozifanya. Kwa niaba ya wenzangu wote, tunawashukuru kwa kila hatua mnayopiga, Mwenyezi Mungu awabariki sana,” alisema Mheshimiwa Nongwa.

Ziara hiyo pia ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, akiwemo Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu; Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mbeya Mjini, Mhe. Ayubu Shelimo, pamoja na viongozi wengine wa Mahakama Mkoa wa Mbeya.

Ziara hiyo ilihitimishwa kwa kutembelea miundombinu ya Kituo hicho na kufanya mazungumzo ya pamoja na watoto na walezi wao, ikiwa ni ishara na dhamira ya Mahakama amabayo siyo tu katika utoaji wa haki, bali pia katika kushiriki kikamilifu katika ustawi wa jamii.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa, akizungumza machache wakati wa ziara hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu (aliyeketi katikati) akiwa sehemu ya watu walioshiriki matatendo ya huruma katika ziara hiyo.

Meneja wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru Orphans Centre, Bi. Mary Himiri (aliyesimama katikati), akitoa neno la shukrani baada ya kupokea zawadi.

Sehemu ya watumishi waliotembelea kituoni hapo.

Sehemu ya watumishi walipotembelea kituo cha Nuru Orphans Centre; kutoka kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer; anayefuatia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu, akikabidhi zawadi walizokwenda nazo kituoni hapo.


Watumishi wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na walezi wa kituo, wapili kushoto ni Meneja wa kituo, na wa nne kushoto ni mlezi mkuu wa kituo hicho.


Watumishi wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na walezi wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru Orphans Centre.


Watumishi wa Mahakama wakiwa mbele ya Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru (Nuru Orphans Centre) Mbeya wakati wa ziara hiyo, (kushoto) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba, (wa pili kushoto) ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu na wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa.

MAHAKAMA KUU MBEYA YAADHIMISHA SIKU YA SHERIA NCHINI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, amewaongoza watumishi wa Mahakama Kuu ya Kanda hiyo pamoja na wananchi wa Mbeya katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa mwaka 2026.

Mhe. Tiganga, ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo, aliambatana na Mgeni Maalum, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Wakili Beno Marisa. Sherehe hizo zilifanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya.

Akitoa salamu za Mkuu wa Mkoa, Mgeni Maalum ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda, aliipongeza Mahakama Kuu ya Mbeya kwa maandalizi mazuri ya maadhimisho hayo. Aidha, aliwahimiza watumishi wa Mahakama kuendelea kusimamia utoaji wa haki kwa wakati na kwa wote, akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni kujiwekea hazina ya kudumu mbinguni mbele ya Mwenyezi Mungu.

Kwa upande wake, Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, katika hotuba yake alieleza kuhusu maboresho ya kanuni ngumu yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania kwa lengo la kurahisisha wananchi kupata huduma za Mahakama na kufanikisha upatikanaji wa haki kwa wote kwa wakati.

Mhe. Tiganga aliongeza kuwa Mahakama ina mpango wa kuimarisha na kuongeza matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kurahisisha utoaji wa haki kwa wakati, kupunguza muda wa wananchi kukaa Mahakamani, na kuwezesha usikilizwaji wa mashauri kwa njia ya mtandao pale inapowezekana. Aidha, aliwahabarisha wadau na watumishi wa Mahakama kuwa, kutokana na maboresho hayo, Mheshimiwa Jaji Mkuu anasisitiza kuwa dira ya Mahakama kwa sasa ni “Utoaji wa haki kwa wote na kwa wakati zaidi iwezekanavyo.”

Kwa upande wao, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Mawakili wa Kujitegemea, wote walisisitiza kuwa kaulimbiu ya Siku ya Sheria kwa mwaka 2026 inaakisi ukweli kwamba hakuna maendeleo ya kweli bila kuzingatia misingi ya haki, usawa na uadilifu katika jamii.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na watumishi wa Mahakama, viongozi wa dini na jadi, pamoja na wadau kutoka taasisi mbalimbali wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mbeya, Mawakili wa Kujitegemea, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya, Jeshi la Polisi, Idara ya Uhamiaji, na wananchi kwa ujumla.

Mgeni Rasmi na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, akisoma hotuba katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Mahakama Kuu Mbeya.

Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Mbeya.

Watumishi na wadau mbalimbali waliokaa mbele ni Mahakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya na Mahakama ya Wilaya, wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya.

Kwaya ya Mahakama Mbeya ikitumbuiza wakati wa maadhimisho hayo.

Mgeni Rasmi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, akikagua gwaride maalum la kuashiria kuanza kwa mpya wa kimahakama 2026.


Mgeni Rasmi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, akikagua gwaride maalum la kuashiria kuanza kwa mpya wa kimahakama 2026.

Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Mahakama na Serikali, (wa kwanza kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo, (wa pili kushoto) ni Heshima, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda (wa kwanza kulia) ni Wakili wa Serikali Mkuu, Bw. Iddi Mgeni na (wa pili kulia) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa.

Mgeni Rasmi ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mbeya, Wengine (kutoka kushoto walioketi) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa (wa pili kulia) na Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mbeya. 

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

WATUMISHI SUMBAWANGA WAPATA MAFUNZO KUHUSU MAADILI KATIKA UTUMISHI WA UMMA

Na. Fredrick Mahava- Mahakama, Sumbawanga

Watumishi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wamepata mafunzo juu ya Maadili katika utumishi wa Umma na mambo ya mchaka wa mtu mwenye uzoefu na maarifa kumsaidia mtu mwenye uzoefu mdogo kwa kumpa ushauri, muongozo, maarifa na msaada ili akue kielimu, kikazi au kimaisha (Mentorship) ambayo yalitolewa kwa njia mbili yaani uso kwa uso kwa waliokuwepo ukumbini na kwa njia ya Mtandao kwa waliokuwa mbali.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Manyanda jana tarehe 06 Februari 2026 ambayo yalifanyika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Sumbawanga.

Akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo Mhe. Manyanda alisema, Kanda ya Sumbawanga imejiwekea utaratibu wa kufanya mafunzo kila Mwezi kwa watumishi ili kuwajengea uwezo na kuwafanya kuwa wabunifu zaidi katika kazi zao za kila siku.

Mafunzo hayo yalitolewa na wawezeshaji watatu ambao ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Sumbawanga Mhe, Joseph Luambano, Afisa Utumishi Mwandamizi Mahakama Kuu Sumbawanga Bi. Irene T. Mlangwa na Afisa Tawala Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Bi. Sarah C. Mwasomola ambao wasifu wao ulisomwa na msimamizi wa Mafunzo hayo Mhe. Elisha Mwasomola.

Mada ya Kwanza kuhusu Mentorship programu iliwasilishwa na Naibu Msajili Mahakama Kuu Sumbawanga Mhe. Joseph Luambano ambaye aliwataka watumishi wote wenye uzoefu wa kutosha kazini kuwa washauri (mentor) kwa wale ambao ndiyo wameajiriwa na hawana uzoefu kazini. Pia alielezea kuhusu misingi ya Maadili katika utumishi wa Umma na mambo ya mchaka wa mtu mwenye uzoefu na maarifa kumsaidia mtu mwenye uzoefu mdogo kwa kumpa ushauri, muongozo, maarifa na msaada ili akue kielimu, kikazi au kimaisha (Mentorship) kwa Maafisa wa Mahakama kwamba njia za kufanya Mentorship na Miongozo mbalimbali ya kufanya Mentorship.

Kwa upande wake, wakilishi wa mada ya pili Afisa Utumishi Mwandamizi Mahakama Kuu Sumbawanga Bi. Mlangwa na Afisa Tawala Mwandamizi Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Bi. Sarah ambao walifundisha kuhusu Maadili katika Utumishi wa Umma walisema ni muhimu kuzingatia miongozo, kanuni na taratibu zote za utumishi wa umma pale mtumishi unakuwa unamuhudumumia mwananchi ili kuondoa dukuduku la na aweze kupata majibu sahihi ya shida yake.

Aidha, Mhe. Manyanda wakati akichangi kuhusu mada zilizofundishwa alisema, suala la Mentorship sio tu kutoka kwa mkubwa kwenda kwa mdogo bali pia linaweza kuwa kutoka kwa mdogo kwenda kwa mkubwa.

Naye, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi alisema kwenye suala ya Mentorship uhuru wa kujieleza unatakiwa kuwepo na utakuwa huru zaidi kama unafanya mambo yako kwa usahihi na hapo ndipo suala la maadili linapozingatiwa.

Wakati wa mafunzo hayo watumishi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga walipata wasaa wa kuuliza maswali mbalimbali kuhusu mada zilizowasilishwa na kupewa majibu ambayo yaliwasadia kuelewa zaidi.

Jaji mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Fredrick Manyanda akifungua mafunzo kwa watumishi wa Mahakama Kanda ya sumbawanga juu ya Maadili katika utumishi wa Umma na Mentorship Programu

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi akizungumza wakati wa mafunzo hayo

Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe. Joseph Luambano akiwasilisha Mada wakati wa Mafunzo.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wakifuatilia kwa makini mafunzo yanayotolewa.

Afisa Tawala Mwandamizi Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Bi. Sarah C. Mwasomola akiwasilisha Mada wakati wa Mafunzo.

Afisa Utumishi Mwandamizi Mahakama Kuu Sumbawanga Bi. Irene T. Mlangwa akiwasilisha Mada wakati wa Mafunzo.

Mheshimiwa Elisha Mwasomola akitoa mwongozo wa Mafunzo kwa Watumishi Kanda ya Sumbawanga







KIKAO CHA MENEJIMENTI MBEYA CHA KETI NA KUSISITIZA MAADILI KWA WATUMISHI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga amewaasa wajumbe kuhusiana na suala la kuzingatia maadili kwa watumishi wote wa Mahakama na kusema suala la maadili siyo la Mahakimu pekee bali linahusu watumishi wote hata wasio Mahakimu.

Akifungua kikao hicho cha menejimenti Mkoa wa Mbeya kilichofanyika tarehe 04 February, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Tiganga alisema “tuyaishi maadili kwa kadiri kazi zetu zinavyotutaka kwa kuzingatia sheria na kanuni za kiutumishi na si vinginevyo ili kujenga imani ya wananchi tunaowahudumia tunapokuwa kwenye majukumu yetu ya kila siku,”

Aidha, Mhe. Tiganga alisistiza kwamba, suala la maadili siyo kwa Mahakimu pekee ni kwa watumishi wote hata watumishi wasio Mahakimu, nawasisitiza ninyi kama viongozi nanyi mkawasisitize watumishi walio chini yenu kuzingatia maadili ya kiutumishi ili kuboresha utendaji kazi wa Mahakama.

Mhe. Tiganga aliongeza kuwa Mahakimu wote katika Vituo vyao kuweka mikakati imara ya kumaliza mashauri kwa wakati na kuhakikisha kuwa wanamaliza kabisa mashauri ya mlundikano mapema iwezekanavyo hasa katika Mahakama za mwanzo.

“Tuendelee kuchapa kazi na tuongeze bidii kwenye usikilizaji wa mashauri na tuhakikishe kuwa katika masijala zetu tumemaliza kabisa mashauri ya mrundikano,”alisema Mhe. Tiganga

Vilevile, kikao hicho kilitumika kujadili mapitio ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027. Akiwasilisha taarifa hiyo Afisa Bajeti ambaye ni Afisa Rasilimali Watu Mahakama Kuu Mbeya Bi. Sarah Lossi katika mapitio hayo ya bajeti alizungumzia kuhusu hali ya rasilimali watu, fedha, hali ya majengo na hali ya bajeti ya Mwaka wa fedha 2025/2026.

Aidha, Bi. Sarah aliongeza kuwa, changamoto katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 ni nyingi ambazo zinatakiwa kukabiliwa, mikakati na muelekeo wa bajeti ya mwaka 2026/2027 ambapo alieleza juu ya majukumu na vipaumbele yaliyopangwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027

Kikao hicho pia kilijadili taarifa ya utendaji kazi kwa robo ya pili ya mwaka 2025/2026 Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, katika taarifa iliyowasilishwa na Afisa Utumishi Mahakama Kuu Mbeya Bw. Moses Luoga alitoa taarifa ya rasilimali watu, usimamizi wa rasilimali fedha, hali ya mashauri, taarifa ya matumizi ya mifumo ya TEHAMA, Utoaji wa elimu kwa umma na hali ya majengo mbalimbali ya Mahakama mkoa wa Mbeya.

Vilevile, kulitolewa mrejesho kuhusu taarifa za Mirathi kutoka katika kila Wilaya za Mkoa wa Mbeya, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama zote za Wilaya waliwasilisha taarifa za mirathi kutoka katika Wilaya zao.

Akiwasilisha taarifa za Mirathi Mjumbe kutoka Wilaya ya kyela Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. James Mhanusi alisema kuwa, mikakati iliyowekwa ili kupunguza na kumaliza kabisa bakaa ya fedha katika akaunti ya mirathi wilayani Kyela.

“Tumefanya jitihada kubwa kupambana na bakaa ya fedha ya mirathi katika Mahakama zetu kwa kufanya vipindi redioni na tumepata fursa kwenye redio kufanya kipindi kimoja kila wiki kutoa elimu kwa wananchi kuhusu elimu ya mirathi na kuwaomba wananchi kufuatilia mirathi yao mahakamani,” alinukuliwa Mhe. Mhanusi

Aidha kikao hicho pia kilijadili kuhusu taarifa ya upatikanaji na upimaji wa viwanja, Pamoja na hatua iliyofikiwa katika kulinda mipaka ya Mahakama ili kufikia lengo la Mahakama ya Tanzania lililokusudia kupeleka huduma ya Mahakama hadi kwenye ngazi ya kata

 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (Katikati) akiongoza kikao cha menejimenti Mkoa wa Mbeya, kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti wakiwa kwenye kikao hicho.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (Katikati) akiongoza kikao cha menejimenti Mkoa wa Mbeya, kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti wakiwa kwenye kikao hicho.

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Mmoja wa wajumbe akizungumza jambo katika kikao hicho (aliyesimama) Afisa utumishi Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Odilia Mapunda

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho.


Alhamisi, 5 Februari 2026

HUDUMA YA MAHAKAMA INAYOTEMBEA KIGAMBONI YAANZISHWA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Dar es Salaam

Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia (IJC) Temeke kimeanza rasmi kutoa huduma ya Mahakama Inayotembe katika Wilaya ya Kigamboni, Mtaa wa Mjimwema zilipo Ofisi za Mtendaji Kata.

Kuanzishwa kwa huduma hiyo ya kimahakama kulitanguliwa na kipindi cha kumepambazuka kilichoendeshwa katika Mahakama hiyo, kikilenga kufikisha ujembe kwa wakazi wa Wilaya ya Kigamboni kuhusu kuanzishwa kwa shughuli za usikilizwaji wa mashauri ya mirathi, ndoa na talaka katika Mahakama Inayotembea ndani ya Wialaya hiyo.

Kipindi hicho kiliongozwa na Mtangazaji Abdalah Kulwa wa Radio One na Mzungumzaji akiwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo iliyopo ndani ya IJC Temeke, Mhe. Upendo Kapama.

Mhe. Kapama alifafanua kwamba Mahakama Inayotembea itatoa huduma za mashauri ya mirathi, ndoa na talaka yanayosikilizwa na Mahakama ya Mwanzo, na mpango huo unalenga kusogeza huduma kwa wananchi.

Aliendelea kusema kwamba sasa Wilaya ya Kigamboni, Mtaa wa Mjimwema patakuwa na Kituo kitakachotoa huduma kila siku ya Jumatano ili kuwaepushia wananchi adha ya kusafiri, muda na gharama za kutoka Kigamboni hadi Temeke.

Mhe. Kapama alieleza jinsi Mahakama Inayotembea inavyowasaidia Wananchi katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata elimu na huduma bora kwa haraka mtaani kwako. Huduma hii inatolewa katika Wilaya ya Kinondoni, Bunju A Ofisi za Mtendaji Kata, Wilaya ya Ubungo Kibamba zilipo Ofisi za Mkuu wa Wilaya na Wilaya ya Ilala Chanika Ofisi za Mtendaji Kata na sasa ni Kigamboni.

Alisisitiza huduma hii inaongeza ufunguaji wa mashauri katika maeneo hayo kwa sababubu wananchi wengi wanapata elimu kubwa ya masuala ya familia, mirathi na ndoa na wanarahisishiwa kwa kufuatwa walipo.

Pia Mhe. Kapama aliendelea kuonyesha jinsi gani Mahakama hiyo inavyowarahisishia wagonjwa kutoa ushahidi kwa kutokusafiri umbali mrefu, hivyo kupunguza gharama na muda.

Mhe. Kapama alisema matarajio ya kusogeza huduma hiyo Mjimwema Kigamboni ni kuondoa dhana ya watu kuishi kimazoea pindi wanapopoteza wapendwa wao na kufuata sheria kwa kufungua mirathi mapema ili kuondoa migogoro katika familia inayoweza kutokea, hivyo kwa kusogezewa Mahakama Inayotembea kutaondoa changamoto hizo.

Aidha, Mhe. Kapama aliwahimiza wakazi wa Kigamboni kujitokeza kwa wingi ili kupata elimu na kufungua mashauri kwa wale wenye uhitaji na mashauri yao yatasikilizwa hapo hapo ndani ya Mahakama Inayotembea kwa haraka, kwani mashauri huchukua siku 30 hadi kusomwa hukumu.



Mahakama Inayototembea ikiwa Wilaya ya Kigamboni, Mtaa wa Mjimwema. Picha chini, wadau wakiwa ndani ya Mahakama Inayotembea.


 

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo iliyopo ndani ya IJC TemekeMhe. Upendo Kapama akiwa ndani ya Mahakama Inayotembea.






MAHAKAMA DODOMA, WADAU WAKUTANA KUTATHMINI UTENDAJI

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama – Dodoma.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, hivi karibuni ilifanya kikao na wadau ili kutathmini utendaji kazi wa mwaka 2025 na kuweka mikakati ya kuboresha huduma za utoaji haki kwa mwaka 2026.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, kilifunguliwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo. Mhe. Dkt. Masabo alieleza kuwa kikao hicho ni sehemu ya utamaduni wa Mahakama kukutana na wadau wake ili kufanya tathmini ya pamoja na kubadilishana uzoefu wa namna bora ya kuboresha utoaji wa huduma.

Mhe. Dkt. Masabo alieleza kuwa lengo lingine ni kuangalia kwa pamoja utendaji kazi wa mwaka uliopita, kubaini mafanikio na changamoto zilizojitokeza, na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha maeneo yaliyohitaji uboreshaji.

Alisisitiza kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, inayojumuisha Mikoa ya Dodoma na Singida, ina wajibu mkubwa kutokana na Dodoma kuwa Makao Makuu yaNnchi, hivyo mabadiliko yanayoendelea yanahitaji kasi na ubora zaidi katika utoaji haki.

Aidha, alibainisha lengo jingine ni kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na wadau, ambao ni nguzo muhimu katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama. Kupitia vikao vya namna hiyo, wadau wamekuwa wakipanga pamoja na kutekeleza majukumu kwa pamoja, jambo lililochangia kuongeza ufanisi wa utendaji.

Akizungumzia mafanikio ya mwaka uliopita wa 2025, Mhe. Dkt. Masabo alisema Mahakama ilipokea mashauri zaidi ya 1,000 na pia kufanikiwa kumaliza mashauri zaidi ya 1,000. Alibainisha kuwa mafanikio hayo yametokana kwa kiasi kikubwa na ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Mabaraza ya Ardhi, Ofisi ya Kamishna wa Ardhi, Msajili wa Hati, pamoja na Taasisi nyingine zinazohusika na masuala ya kisheria na kiutawala.

Aliongeza kuwa mashauri mengi yaliyopokelewa na kumalizwa yalihusu masuala ya ardhi, jambo linaloonesha umuhimu wa ushirikiano wa karibu na taasisi zinazohusika na sekta hiyo.

Katika kikao hicho, wadau walipata pia fursa ya kujifunza mambo mbalimbali zitakazowasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akisoma taarifa ya mashauri katika kikao hicho, Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe Silivia Lushasi, alibainisha mikakati mbalimbali ya kuzuia mashauri kukaa muda mrefu mahakamani kwa mwaka 2026.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa inasikiliza kwa makini maoni na ushauri kutoka kwa wadau waliodhuria kikao hicho, aliyepo kulia kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Amir Mruma na aliyepo kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Silvia Lushasi.

Washiriki wa kikao wakiogozwa na Jaji Mfawdhi (hayupo pichani) wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Silivia Lushasi (hayupo pichani).

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Dodoma pamoja Viongozi kutoka Taasisi mbalimbali waliohudhuria kikao hicho, walioketi kulia kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Amir Mruma na aliyepo kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Silvia Lushasi.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu pamoja na wadau kutoka Taasisi mbalimbali waliohudhuria kikao hicho.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo [aliyepo katikati] ikiwa katika picha ya pamoja na Si.ekretariet  

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.