Jumatano, 18 Machi 2026

HAKIMU MKAZI MFAWIDHI PWANI AWATAKA WAKRISTO NA WAISLAMU KUWA KITU KIMOJA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi amewataka Wakristo na Waislam kuwa wamoja maana hata vitabu vya Mungu vinasema watu wote ni sawa.

Mhe. Mkhoi aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa hafla ya Iftar iliyoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani.

Amesema hata wakiangalia kwa sasa, Waislamu wamefunga na Wakristo nao wako Kwaresma, ameeleza, “hii haitokei kwa bahati mbaya ni jinsi tu Mungu anavyoendela kutuonesha kuwa, sisi ni kitu kimoja tunatakiwa kuishi kwa kupendana, kushirikiana lakini pia tudumishe ushirikiano kama ambavyo vile tumeweza kuyadumisha.”

Akizungumza wakati wa Iftar hiyo, Ustadhi Mohamed alisema, kuna watu kila siku kazi zao kuingiza huzuni kwenye mioyo ya wenzao, huku akimpongeza Mhe. Mkhoi kwa kuandaa kitu cha kuwakutaniasha watu. 

“Katika mkusanyiko huu kuna watu inawezekana walikuwa na tofauti zao lakini kupitia mkusanyiko huu inawezekana tofauti zao zikaisha  lakini pia kupitia mkusanyiko huu tunaweza kupata marafiki wengi  watu wakabadilishana mawasiliano lakini mwisho wa siku wakatengeneza amani zaidi na upendo na mshikamano kwa sababu tu iliyosababishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani,” amesisitiza Ustadhi Mohamed. 

Iftar hiyo iliyoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani iliwajumuisha watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mahakama ya Wilaya Kisarawe.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi  ( wa kwanza kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama hiyo baada ya kushiri Iftar hivi karibuni.

Sehemu ya watumishi na waalikwa katika hafla ya iftar iliyofanyika katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)

 

 

 

 

 

Jumanne, 17 Machi 2026

JAJI MKUU ASHIRIKI KUMBUKIZI MIAKA MITANO YA HAYATI DKT. JOHN POMBE MAGUFULI

  •   Asema Hayati Dkt. Magufuli alikuwa mnyenyekevu, mwenye huruma na mchapakazi

  • Apongeza Kanisa kwa kuhimiza usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii, umoja wa kitaifa na maslahi ya Taifa

Na MARY GWERA, Mahakama-Chato

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Viongozi wengine wa Serikali, Wanafamilia na Watanzania kwa ujumla leo tarehe 17 Machi, 2026 kwa pamoja wameungana na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi, kuadhimisha miaka mitano ya Kumbukizi ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  

Katika Kumbukizi hiyo, Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Nchimbi amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan huku Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa Mgeni Maalum.

Ibada Maalum ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Kifo cha Hayati Dkt. Magufuli imefanyika katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.

Aidha, shughuli za Maadhimisho hayo zilianza majira ya saa 3:30 Asubuhi kwa Adhimisho la Ibada Takatifu iliyoongozwa na Maaskofu mbalimbali wakiongozwa na Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki la Rulenge-Ngara.

Mara baada ya ibada kukamilika, Viongozi mbalimbali walipata wasaa wa kutoa neno miongoni mwao akiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju ambaye ameishukuru familia ya Hayati Magufuli kwa mwaliko wa kushiriki katika Kumbukizi hiyo.

“Nashukuru Mama Janeth kwa ukarimu wako na kutualika, hii ni fursa ambayo inatukutanisha, lakini yatosha tu kusema kwamba nikushukuru Mhashamu Baba Askofu kwa ibada kubwa hii na muhimu uliyoifanya, ninawashukuru Kanisa kwa kuendelea kuhimiza usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii, umoja wa kitaifa na maslahi ya Taifa,” amesema Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, alimfahamu Hayati Magufuli wakati akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alipokuja kusoma Shahada ya Pili wakati yeye (Mhe. Masaju) akiwa anasoma Shahada ya kwanza.

Aidha, Mhe. Masaju amesema kuwa, baadaye mwaka 2015, Hayati Magufuli alimteua kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali mara baada ya kuwa ametumika kama Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa uteuzi wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Jaji Mkuu ameongeza kuwa, alifanya kazi na Hayati Dkt. Magufuli kwa miaka miwili katika nafasi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na baadaye alimteua kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na hatimaye Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akamteua kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania Juni, 2025.

“Ninawashukuru sana Viongozi hawa, Rais Kikwete, Rais Magufuli, Rais Samia, Rais Mwinyi ‘Senior’ na Rais Mkapa wana mchango mkubwa sana katika utumishi wangu,” ameeleza Mhe. Masaju.

Kadhalika, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, Hayati Magufuli alikuwa na huruma, mnyenyekevu na mchapakazi.

“Hayati Magufuli alikuwa mchapakazi na uchapakazi ule ndio maana tunayashuhudia haya aliyoyafanya na ambaye mrithi wake ambaye mimi naamini ilikuwa timu nzuri ameyakamilisha na mengine ameendelea kuyaibua na kuyafanya. Huu ni utaratibu mzuri kwa Taifa letu,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu alitumia nafasi hiyo pia kuitakia heri familia ya Hayati Magufuli kuendelea kwa kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu kuwabariki katika maisha yao, katika utumishi wao na katika shughuli zao.

“Tunajua hili ni pengo, Mwanadamu yeyote anapofariki anaacha pengo kubwa ambalo halizibiki lakini pia linaloumiza kwa sababu pia kila mwanadamu ana utambulisho wake, faraja yangu mimi kwenu ni kwamba Mungu yupo pamoja na ninyi,” amesema Mhe. Masaju huku akimsihi Mama Janeth Magufuli kuendelea kuwa imara katika kuisimamia familia huku akimtanguliza Mungu.  

Viongozi mbalimbali waliopata nafasi ya kuzungumza wakiongozwa na Makamu wa Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Nchimbi wamemuelezea Hayati Magufuli kwa mema aliyoyafanya enzi za uhai wake na kutoa rai kwa Watanzania kuyaenzi yote mema aliyoyafanya.

Wakati wa kumbukizi hiyo, Makamu wa Rais ameendesha Harambee maalum ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Parokia ya Mlimani-Chato ambayo ilikuwa ndoto ya Hayati Magufuli ambapo imepatikana Ahadi za jumla ya Shilingi 474,000,000/=.

Shughuli ya Kumbukizi imehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Mawaziri, Viongozi Waastafu, Wanafamilia na Wananchi kwa ujumla.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa neno wakati wa Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 17 Machi, 2026 katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.



Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi (katikati) aliyemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na viongozi wengine wa Serikali wakiwa katika Maadhimisho ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Viongozi wa dini wakiingia tayari kwa ajili ya kuendesha Ibada maalum ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi akizungumza kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 17 Machi, 2026 katika maadhimisho ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Picha za makundi mbalimbali ya Viongozi wa Serikali, wa Dini, Wanafamilia pamoja na Wananchi kwa ujumla wakiwa katika Maadhimisho ya Kumbukizi ya Miaka Mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Maadhimisho hayo yamefanyika leo tarehe 17 Machi, 2026 katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje wakiwa katika Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiweka shada la ua katika kaburi la Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ikiwa ni ishara ya kumkumbuka na kumuenzi.  Kulia kwa Jaji Mkuu ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi na baadhi ya Viongozi wengine.


(Picha na Jeremia Lubango, Mahakama)


UADILIFU MTAJI WA IMANI YA UMMA KWA MAHAKAMA: JAJI KIONGOZI

 Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama, Lushoto

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama Mhe. Dkt. Mustapher Siyani amesema maadili, uwazi na uwajibikaji ni mambo ya muhimu yatakayoimarisha imani ya Umma kwa Mhimili wa Mahakama.   

Akifungua Mafunzo ya siku mbili ya Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama leo tarehe 16 Machi, 2026 katika Wilaya ya Lushoto Mkoa wa Tanga, Jaji Kiongozi amesema miongoni mwa mambo ya kipaumbele kwa Mahakama ni kuhakikisha inaendelea kujenga na kuimarisha imani ya umma kwa muhimili huo wenye kauli ya mwisho katika utoaji wa haki nchini.

Alisema lengo kubwa la juhudi za Mahakama katika kuimarisha imani ya umma ni kuifanya Mahakama kuwa Taasisi ya watu na inayowajibika kwa umma (Citizen Centric Judiciary).

“Imani ndio mtaji wa taasisi yoyote inayotoa haki. Ili kuwa na Mahakama inayoaminiwa na umma, masuala ya maadili, uwazi na uwajibikaji ni ya muhimu na hayawezi kuwekwa kando. Kwa ujumla wake, watumishi wa Mahakama, wanayo dhima ya kwanza ya kuwa waadilifu”, alisema Jaji Kiongozi.

Mwenyekiti huyo alisema kuwa imani ya watumiaji wa huduma za Mahakama haijengwi kwa uamuzi wa haki peke yake  bali pia kwa tabia nzuri na mwenendo usiotiliwa shaka wa watumishi wa Mahakama wakiwemo Majaji na Mahakimu.

Alisema matarajio ya umma kwa Maafisa Mahakama (Majaji na Mahakimu) ni kuona kuwa wao swanakuwa ni mfano au tafsiri sahihi ya uadilifu, weledi na uwajibikaji.

“Vitu hivi vitatu, vinajenga kwa pamoja dhana nzima ya maadili. Kwa hiyo, ni muhimu Maafisa Mahakama kuwa na kiwango cha juu cha uadilifu kwani huo ndio mtaji wa imani yetu kwa umma”, alisisitiza.

Alisema ili kulinda na kuimarisha maadili kwa Maafisa Mahakama, Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama haina budi kusimamia na kufuatilia mienendo na tabia za Maafisa hao na pia kuchunguza kwa umakini na weledi wa hali ya juu wao wa utoaji wa uamuzi.

Aliwataka wajumbe hao kujifunza na kuelewa mambo ya msingi ya kazi yao ili waweze kusimamia kikamilifu nidhamu na maadili ya Maafisa Mahakama. Aliongeza kuwa mafanikio yao yatategemea weledi na ufanisi katika uzingatiaji wa taratibu za kupokea malalamiko, kuchunguza tuhuma, kusikiliza na kutoa uamuzi.

Alisema kuwa mafunzo haya ni muhimu kwa wajumbe wa Kamati, kwani yatawajengea uwezo katika utekelezaji wa majukumu yao, na hivyo kuboresha utendaji kazi wa Kamati.

Alisisitiza kuwa jukumu la Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama si kutoa adhabu pekee, Kamati hii inapaswa pia kuwa, kichocheo cha uadilifu na uwazi ili kuimarisha imani ya umma kwa Mahakama.

Aidha, Jaji Kiongozi ameipongeza Tume ya Utumishi wa Mahakama kwa kuona umuhimu wa kufanyika kwa mafunzo haya na kutaka yawe endelevu na kujumuisha watumishi wote.

Tume ya Utumishi wa Mahakama imeandaa mafunzo ya siku mbili ya Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama ili kuwajengea uwezo wajumbe hao na kuimarisha utendaji kazi wa Kamati hiyo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama Mhe. Dkt. Mustapher Siyani akifungua Mafunzo ya Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama yanayofanyika Katika Chuo cha Uongozi wa Mahamaka (IJA) Lushoto, Tanga. Tume ya Utumishi wa Mahakama imeandaa Mafunzo hayo kwa lengo la kuwajengea uwezo wajumbe hao na kuimarisha utendajai kazi wa Kamati hiyo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto Mhe. Dkt. Paul Kihwelo (kulia) pamoja na Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa kwenye Mafunzo ya Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama jana tarehe 16 Machi, 2026. 

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama Mhe. Dkt. Mustapher Siyani akiwa na Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama (waliosimama) mara baada ya kufungua Mafunzo yao jana wilayani Lushoto. Aliyekaa kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Tanga Mhe. Katarina Mteule na kushoto ni Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Maadili na Nidhamu) Bi. Alesia Mbuya. 

Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Maadili na Nidhamu) Bi. Alesia Mbuya akizungumza Neno la Utangulizi wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama jana tarehe 16 Machi, 2026 wilayani
Lushoto.
Sehemu ya Manaibu Wasajili wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye Mafunzo ya Wajumbe wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama yaliyoanza jana tarehe 16 Machi, 2026 wilayani Lushoto.
 


Jumatatu, 16 Machi 2026

WANAFUNZI BULONGE KIGOMA WAJIFUNZA MCHANGO WA MAHAKAMA KATIKA KUKUZA SIASA, UTAWALA WA SHERIA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma 

Wanafunzi wapatao 19 wa kidato cha sita kutoka Shule ya Sekondari Bulonge mkoani Kigoma wametembelea Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma ili kupata fursa ya kujifunza masuala mbalimbali ya kisheria, mchango wa Mahakama katika kukuza siasa na Utawala wa Sheria nchini.

Akitoa elimu kuhusu namna Mahakama nchini inavyofanya kazi tarehe 13 Machi, 2026 kwenye ukumbi Mahakama ya wazi wa Mahakama Kuu Kigoma, Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola aliwaeleza wanafunzi hao kuhusu majukumu ya Mahakama katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na namna Mhimili huo unavyoshiriki kutoa haki katika mashauri mbalimbali ya uchaguzi na kutoa haki na amri mbalimbali zinazolinda na kuleta amani na ustawi wa Nchi. 

Aidha, wanafunzi hao walisisitizwa kufuatilia hotuba mbalimbali za Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, hususani ya tarehe 31 Julai, 2025 jijini Dodoma wakati akitoa salamu kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliokuwa wakishiriki katika Mafunzo ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi yaliyofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court).

Kadhalika, Mhe. Msola aliwafundisha ni kwa jinsi gani Mahakama inatoa fursa kwa mgombea wa chama chochote ambaye hajaridhika na matokeo ya uchaguzi kuja Mahakama ya Wilaya husika kufungua shauri katika ngazi fulani ya uchaguzi, hata hivyo  anaweza kukata rufaa kwenda Mahakama Kuu au  ya Mahakama ya Rufani asiporidhishwa na hukumu ya Mahakama ya chini. 

Alisema kuwa, kwa Mahakama za Mwanzo zote, rufaa zake hupelekwa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Wilaya rufaa zake hupelekwa Mahakama Kuu ya Tanzania na vilevile Mahakama Kuu rufaa zake huwasilishwa Mahakama ya Rufani ili kutoa haki iliyokosekana kutolewa kwa Mahakama za chini. 

“Kupitia mlolongo huo, mwananchi/wanasiasa wanayo fursa kubwa ya kutafuta haki aliyonyimwa na Tume ya Uchaguzi, kwa namna hiyo Mahakama inashiriki kikamilifu katika kukuza siasa na haki nchini,” alisisitiza Mhe. Msola. 

Aidha, aliwaasa wanafunzi hao kusoma kwa bidii na kujituma huku wakikua katika maadili ya kuwa viongozi wasomi katika kada mbalimbali wanazopenda kusomea. 

Hata hivyo, aliwakaribisha katika tasnia ya sheria kwani ni miongoni mwa tasnia mahsusi katika kulinda na kutetea haki za kisiasa na masuala mbalimbali ya kijamii na kiuchumi, na kuwasisitiza kusoma na kufaulu vizuri ili kuweza kupata fursa ya kufika elimu ya juu katika masomo yao ili kuja kuwa viongozi wenye tija kwa jamii na Taifa kwa ujumla.

Akizungumza juu ya nia yao ya kujifunza kupitia Kazi Mradi (School Project), Kiongozi wa Wanafunzi hao, Bw. Sefu Hamis alibainisha kiu waliyokuwa nayo kujifunza masuala ya kisheria hususani sheria za siasa  ambapo alisema, “tunapenda kufahamu mchango wa Mahakama kukuza siasa na taratibu za kusikiliza mashauri hayo ili kulinda haki za wanasiasa.” 

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola akisisitiza jambo fulani alipokuwa akitoa elimu kwa wanafunzi wa kidato cha sita Shule ya Sekondari Bulonge juu ya utaratibu wa usikilizwaji wa mashauri ya uchaguzi.

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola akifundisha kwa vitendo wanafunzi wa kidato cha Sita Shule ya Sekondari Buronge namna ambavyo Mahakama huketi kusikiliza mashauri mbalimbali ikiwemo ya uchaguzi.

Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Bulonge  Kidato cha Sita, Bi. Elizabeth Elifasi akisoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 107 inayoainisha uanzishwaji wa Mahakama ya Tanzania wakati wakipatiwa elimu na Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola (hayupo katika picha).

Wanafunzi wapatao 19 wa Kidato cha Sita kutoka Shule ya Sekondari Bulonge wakisikiliza kwa makini mtoa elimu  Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola alipokuwa akitoa mada wakati walipotembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Picha ya pamoja ya Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na  Wanafunzi wapatao 19 wa kidato cha sita Shule ya Sekondari Bulonge mara baada ya kupatiwa elimu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)

 

 

JAJI MAGHIMBI ATOA WITO KWA VIONGOZI WANAWAKE NGAZI MBALIMBALI KUWA WALEZI, WALIMU

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi ametoa wito kwa viongozi wanawake ngazi mbalimbali kuwa walezi na walimu kwa kuwaongoza wanawake wenye nia na bidii katika kuleta maendeleo kwa taasisi na taifa kupitia majukumu ya kazi wanazozifanya.

Mhe. Maghimbi alitoa wito huo tarehe 13 Machi 2026 wakati wa kutaniko la wanawake watumishi wa Mahakama wa Dar es Salaam lililofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF Golden Jubilee Tower.

Alieleza kuwa, chanzo cha Maadhimisho ya Siku ya Wanamke Duniani yalianza 1911 ambapo lengo lilikuwa ni kuikumbusha jamii kuhusu nafasi, haki  na mchango wa mwanamke katika maendeleo ya jamii, ambapo alisema, “katika maadhimisho haya wanawake wamekuwa wakikutana kufanya majadiliano ya kutafuta ufumbuzi wa changamoto wanazokabiliana nazo pamoja na kuelimishana kuhusu namna bora ya kujikomboa kiuchumi.”

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo alisema anayo furaha kushiriki maadhimisho ya siku hiyo muhimu ambapo imebebwa na Kauli mbiu isemayo, ‘Haki na usawa kwa wanawake na wasichana; msingi jumuishi kufikia Dira 2050.’

Alisema kuwa, kaulimbiu hiyo inawakumbusha kwamba  wanawake na wasichana wanalo jukumu la kujifunza zaidi katika maeneo  wanayofanyia  kazi kama vile sheria, TEHAMA, utawala na kadhalika ili waweze kuongeza ujuzi wao na hatimaye  kuongeza tija na ufanisi katika kutenda haki kwenye majukumu yao ya kila siku wanayofanya.

Ameeleza kuwa, takwimu zinaonesha Mahakama ya Tanzania ina jumla ya watumishi 6,959 ambapo wanaume ni 3,549 na wanawake 3,410 sawa na asilimia 49, hiyo inaonesha kwamba dhana ya haki na usawa inatekelezwa kwa kiwango kikubwa ndani ya Mahakama ya Tanzania.

Aliongeza kwamba, mwaka 1979 Mahakama ya Rufani Tanzania ilikuwa na Majaji watano wote wanaume lakini kwa sasa Mahakama ya Rufani ina Majaji 37 ambapo wanaume ni 25 na wanawake ni 12 sawa na asilimia 32. Mahakama Kuu ina jumla ya Majaji 104 ambapo wanaume ni 65 na wanawake ni 39 sawa na asilimia 37, kwa upande wa Wasajili, Msajili Mkuu ni mmoja na ni mwanamke, Naibu Wasajili wapo 82 ambapo wanaume ni 40 na wanawake ni 42 sawa na asilimia 51.

Kwa upande wa Watendaji wa Mahakama, jumla wapo 40 ambapo wanaume wapo 28 na wanawake 12 sawa na asilimia 30, pia idadi ya Mahakimu wa Mahakama za Hakimu Mkazi, Wilaya na Mwanzo ni 1,623 ambapo  wanaume ni 857 na wanawake ni 766 sawa na asilimia 47.

Mhe. Maghimbi alisema katika Mahakama za Wilaya 12 za Kanda ya Dar es Salaam, Mahakimu Wafawidhi 12 kati yao 11 ni wanawake ambapo ameeleza kwamba hiyo ni hatua kubwa wanayojivunia kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi huyo amewakumbusha wanawake na wasichana hao kuwa, mwanamke anayo nguvu ya asili katika malezi na uongozi kwa jamii na Taifa kwa ujumla, hivyo wanapotekeleza majukumu yao ya ofisi wakumbuke pia wana wajibu katika jamii ikiwemo malezi ya familia zao kama Mama, Dada, Shangazi na kadhalika kwa kufanya hivyo itasaidia kuwa na Taifa lenye maendeleo jumuishi ifikapo 2050.

Mhe. Maghimbi alitoa wito kwa wanawake na wasichana  kuwa na moyo wa kujituma na kujiendeleza kitaaluma, ambapo ujuzi watakaoupata utawasaidia kuongeza maarifa kazini na kwa mazingira yanayowazunguka kwa ujumla katika hatua ya kuelekea kuweka msingi jumuishi kwa maendeleo kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katika hatua nyingine, Jaji Maghimbi alitoa wito kwa Majaji Wafawidhi kuanzisha programu ya kuwafundisha watumishi wanawake katika vituo vyao kuhusu Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ili waielewe.

Kadhalika Jaji Mfawidhi huyo ametoa rai kwa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania kuendelea kuwapa ushirikiano, kuwaamini na kuwapa fursa nyingi za kazi ikiwemo nafasi za utoaji haki kwa jamii.

Hafla hiyo ilipambwa na mdahalo ulioongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma na wachangia mada walitoka katika kada mbalimbali tofauti na kada ya sheria kutoka Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara na Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia- Temeke.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na watumishi wanawake wa Kanda ya Dar es Salaam kutoka Mahakama Kuu Divisheni zote na Mahakama za chini.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi  akizungumza hivi karibuni katika hafla ya Siku ya Wanamke Duniani iliyohusisha watumishi wanawake wa Mahakama Mkoa wa Dar es Salaam.

 Majaji waliohudhuria hafla ya Siku ya Wanamke Duniani iliyofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF Golden Jubilee jijini Dar es Salaam (katikati) ni 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi aliyekuwa mgeni rasmi, kushoto ni  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Angela Bahati Salema.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wanawake kutoa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara.
   
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam (katikati) wakiwa katika picha ya pamojana watumishi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi. 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wanawake kutoka Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wanawake wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke.

 Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wanawake kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Meza kuu katika picha ya pamoja na watumishi wanawake kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam-Kisutu.

 


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi,  Mhe. Zahra Maruma (kushoto) akiongoza mdahalo katika hafla hiyo. Anayefuata  ni Bi. Joyce Ndosi kutoka Mahakama ya Biashara, Bi. Christina Nchimbi kutoka Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Bernadina Tayali kutoka Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia- Temeke na Bi. Anitha Kabwogi kutoka Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)

KAZI YA UHAKIMU NI ADILIFU NA WITO KATIKA JAMII: JAJI RWIZILE

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka Mahakimu Wakazi wapya wa Mahakama za Mwanzo kuzingatia utu, uadilifu na tabia njema katika kutimiza majukumu yao ya uhakimu huku wakimtanguliza Mungu mbele katika kuenenda vema.

Mhe. Rwizile alitoa wito huo tarehe 13 Marchi, 2026 mara baada ya kuwapokea Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama za Mwanzo wakati wa mazungumzo yaliyofanyika katika ofisi yake.

“Ninyi ambao mmepangiwa kufanya kazi Kanda hii mmependelewa sana kwakuwa Kigoma tunafanya tofauti hivyo dhamana ya utoaji haki ni jukumu zito linalohitaji nidhamu, uaminifu, weledi na tabia njema ya kiwango cha juu na tunaamini kazi hiyo ni adilifu na wito kwenu na ndio matarajio ya jamii, kwani kazi ya uhakimu ni tofauti na kazi zingine,” alisisitiza Jaji Rwizile.

Katika hatua nyingine, Jaji Mfawidhi huyo, alimshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju kwa kuongeza nguvukazi na kuwafunda kwa kiasi cha kutosha Mahakimu hao wapya.

Mhe. Rwizile amewasisitiza Mahakimu hao kuyaishi maelekezo aliyoyatoa Jaji Mkuu tarehe 23 Februari, 2026 mara baada ya kuwaapisha.

Kadhalika Jaji Mfawidhi huyo, amewataka Mahakimu hao kutofungwa na masharti ya kiufundi, kelele za mamlaka au  maneno ya mitandaoni, msukumo wa kihisia, upendeleo wa wazi na kutoa hukumu bila kuzingatia haki itadhoofisha utendaji kazi wao huku akiwasisitiza kwamba wana wajibu wa kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujiamini.

Sambamba na hayo, Mhe. Rwizile amewaasa Mahakimu hao kutumia vizuri muda wao kusoma na kuongeza ujuzi, weledi juu ya kazi yao, huku wakifanya tafiti mbalimbali kabla ya kufanya maamuzi katika kazi zao.

Naye, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, amewapongeza Mahakimu hao kupata kazi na amewasisitiza kuhusu umuhimu wa kuwa  waadilifu pamoja na kuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, kwakuwa, wananchi wanatarajia kuona mashauri yakisikilizwa na kuamuliwa mapema ipasavyo bila ucheleweshaji usio wa lazima huku akiweka wazi kuwa kuchelewa kwa haki kunaweza kuathiri imani ya wananchi kwa Mahakama na kusababisha mlundikano wa kesi mahakamani.

kwa upande wake Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza amewataka Mahakimu hao kujenga umoja na mshikamano katika maeneo yao ya kazi na kuwahimiza kujifunza kwa watumishi watakaowakuta katika maeneo watakayopangiwa kazi, huku akisisitiza kuwa wajifunze kutoka Kanda mbalimbali kwakuwa nguvu ya Mahakama ipo katika ushirikiano, uwajibikaji na kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Ameongeza kuwa, kila Hakimu anapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii kwa matendo na maamuzi mbalimbali, huku wakitumia maarifa na uzoefu wao katika kuchambua masuala na kutoa maamuzi sahihi kwa kuzingatia sheria kwakuwa kazi ya uhakimu ni wito.

Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga ambao wote kwa nyakati tofauti wamewasisitiza Mahakimu hao kujifunza kwa haraka matumizi ya mifumo ya Mahakama ili kwenda na kasi ya Mahakama katika Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akisisitiza jambo alipokuwa akifanya mazungumzo na Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama za Mwanzo. Mazungumzo hayo yalifanyika katika ofisi yake ya Mahakama Kuu Kigoma.

Mahakimu Wakazi wa Mahakama za Mwanzo wapya wanne wakisikiliza kwa makini maelekezo mbalimbali waliyokuwa wakitoa  Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma wakati wa mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John  Nkwabi akisisitiza jambo wakati akitoa nasaha kwa Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama ya Mwanzo waliopangiwa mkoani Kigoma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza akizungumza jambo na  Mahakimu Wakazi wapya wanne wa Mahakama ya Mwanzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (kulia) akifanya utambulisho wa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo wapya wanne mbele ya Majaji.  Kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)





 

 

'VIKAO VYA USUKUMAJI WA MASHAURI VINALETA TIJA KATIKA UMALIZAJI WA MASHAURI'

 Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Kibaha

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi amesema Vikao vya Kusukuma Mashauri vinaleta tija katika umalizaji wa mashauri,hayo.

Mhe. Mkhoi aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akiongoza kikao cha robo ya kwanza cha Kusuma Mashauri katika Mkoa wa Pwani kilichohudhuriwa na Wadau wa Haki jinai na Haki Madai.

Katika kikao hicho, Mhe. Mkhoi alisema maazimio yanayofikiwa yanafanyiwa kazi kwa wakati na ndio maana malengo yanatimia ya kumaliza mashauri kwa wakati uliokubaliwa kwenye vikao.

Aidha, Mfawidhi huyo ametoa mbinu mbadala ya kupatikana kwa mashahidi kuwa, ni kuharakisha kuwaita waathirika kwanza kutoa ushahidi akiwa bado ana uchungu wa kufanyiwa tukio, kwa kuwa upelelezi unakuwa umekamilika wakati shauri linafikishwa mahakamani siku ya kusomewa shtaka mtuhumiwa asomewe na maelezo ya awali ili tarehe inayofuata mashahidi waitwe na shahidi wa kwanza awe mwathirika wa tukio.

“Mbinu hii imetokana na maelezo ya Mwakilishi wa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Pwani, Mkaguzi wa Polisi Erick Lubuva kusema kwamba mashahidi wamekuwa wagumu kuifika Mahakama kutokana na ndugu wa watuhumiwa kuwatafuta na kuongea nao na kukubaliana kuwalipa hivyo wanakataa kufika mahakamani mpaka wengine wanapeleka hati za kukatwa na hata wakifika hawatoi ushirikiano,” alisema Mhe. Mkhoi.

Sambamba na kikao hicho ilifanyika ziara katika Gereza la Mahabusu Mkuza ambapo Wadau wa Haki Jinai walifika kusikiliza kero zinazowakabili mahabusu hao. Kabla ya kuzungumza na mahabusu hao, Mkuu wa Gereza la Mahabusu Mkuza, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza (SSP) Ibrahim Nyamka alitoa taarifa ya Mahabusu na wafungwa waliomo ndani ya gereza hilo ambapo alisema kwa sasa wana idadi ya Wafungwa ambao ni Watanzania 44, wafungwa ambao ni Raia wa Burundi watatu (03),mfungwa mmoja Raia wa Uganda, Mahabusu ambao ni Watanzania 51, Mahabusu wawili Raia wa China na Mzuiwa mmoja Raia wa Ethiopia na kufanya jumla yao kuwa 102 na kwamba Gereza hilo kwa sasa halina msongamano.

 Akijibu hoja ya mahabusu kuhusu changamoto ya watuhumiwa kuachiwa na Mahakama na kukamatwa tena katika maeneo ya Mahakama, Mkuu wa Mashtaka Mfawidhi wa Mkoa wa Pwani, Bi. Fajara George alisema kuwa, ameshafanyia kazi suala hilo la kukamatwa na kuachiwa siku hizi limepunguzwa kwa kiasi kikubwa na kama ikitokea mtu kaachiwa na kukamatwa ni pale tu panapokuwa na ulazima na anaendelea kushughulikia hoja hiyo ili kupunguza msongamano wa kuwa na mashauri yasiyo na ulazima kwani kuachiwa pia ni haki ya Mshtakiwa.

Katika kikao kilichopita cha tarehe 10 Oktoba, 2025 maazimio yalikuwa ni kumaliza mashauri matatu yalikuwa yamepita muda wake na katika hayo mashauri mawili yalimalizika, limebaki moja ambapo wameweka maazimio kufikia mwezi Juni liwe limemalizika na hivyo kufanikiwa kwa asilimia 80.

Katika ziara hiyo, Wadau wa haki jinai walitembelea pia jengo litakalotumika kama Mahakama matandao ambapo jengo hilo limefika hatua za mwisho kukamilika.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe Joyce Mkhoi (kulia) ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kikao cha kusukuma mashauri akiwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Bi. Anna Chimpaye ambaye alikuwa Katibu wa kikao hicho wakiwa katika kikao cha Kusukuma Mashauri kilichofanyika hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi (kushoto) akiwa na Mkuu wa Gereza la Mahabusu Mkuza, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza, Ibrahim Nyamka (katikati) na Hakimu Mkazi, Mhe. Fredrick Shayo walipokuwa wakikagua jengo litakalotumika kwa shughuli za Mahakama Mtandao.


Wadau wa haki jinai wakiwa katika kikao cha kusukuma mashauri.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)