Jumanne, 26 Mei 2026

RAIS SAMIA AAHIDI KUENDELEA KUIMARISHA UWEZO NA UFANISI WA MAHAKAMA YA TANZANIA

  •   Ni wakati akiwaapisha Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani
  •   Awataka Majaji hao kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, busara na hofu ya Mungu
  •     Awataka Majaji hao pia kulinda heshima na uhuru wa Mahakama

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa, kwa kutambua umuhimu wa suala la utoaji haki nchini, Serikali imeendelea na itaendelea kuchukua hatua stahiki za kuimarisha uwezo wa Mahakama ya Tanzania ili iweze kusimamia vizuri eneo hilo kwa ufanisi.

Rais Samia ameyasema hayo leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam katika Hafla ya Uapisho wa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani aliowateua tarehe 20 Mei mwaka huu.

“Kwa muktadha huo, uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Rufani ni sehemu ya jitihada hizo za kuongeza ufanisi katika Mhimili huu muhimu. Tumefanya mengine mengi na ninyi ni mashahidi kwamba Mahakama zimebadilika kwa kiasi kikubwa, zimeendelea kwa kiasi kikubwa sana katika miaka hii ya karibuni, kwahiyo sasa ni kuongeza watu wenye dhamira ya kufanya kazi, wenye uwezo wa kufanya kazi lakini wanaosimama kwenye mstari mzuri wa haki,” amesema Mhe. Dkt. Samia.

Rais Samia amesema kuwa, Mahakama ya Rufani ndio ngazi ya juu ya utoaji haki nchini Tanzania, kwahiyo kila uamuzi unaotolewa na Majaji katika Mahakama hiyo una uzito mkubwa si kwa wahusika wa shauri pekee bali pia kwa Taasisi, mwenendo wa jamii na tafsiri pana ya sheria nchini, yote yanawaangalia wao kama Wasimamizi wa Haki nchini.

“Hivyo basi nendeni mkalinde heshima na uhuru wa Mahakama lakini pia muendelee kuimarisha uwajibikaji, nidhamu na maadili ndani ya Mhimili huu muhimu, uhuru huu una umuhimu pale unapoenda sambamba na uadilifu, ufanisi na utendaji wenu unaoangalia uzalendo kwa nchi yenu, mnapotoa maamuzi Taifa kwanza, Nchi kwanza halafu ndio mtaenda kwenye mambo mengine,” ameeleza Mhe. Dkt. Samia.

Akizungumza na Majaji hao mara baada ya kuwaapisha, Mhe. Dkt. Samia amewapongeza Majaji hao kwa kuaminiwa na kuteuliwa kushika wadhifa huo na kuwasisitiza kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, busara na hofu ya Mungu kama viapo vyao vinavyowataka.

“Vilevile niwapongeze Majaji wote mlioapa leo, dhamana mliyopewa ni kubwa na ya heshima kwa Taifa letu katika kuwatumikia wananchi, hongereni sana. Uteuzi wenu unatokana na uzoefu, weledi na utumishi mliuonesha katika kutumikia nafasi zenu mbalimbali mlizotumikia, nazikumbuka sura nyingine hapa nilishaziapisha nadhani leo mara ya pili kama sio ya tatu, ina maana kipindi nilichokuwepo mimi ulishapanda, ukapanda, umepanda katika ngazi hii ya leo...” amesema Rais Samia.

Amesema pia, uteuzi wa Majaji hao ni ishara kwamba wamefanya kazi nzuri na Tume ya Utumishi wa Mahakama imetambua kazi yao na imewapendekeza kupandishwa katika ngazi hiyo, kwahiyo ana imani kwamba kwa heshima hiyo waliopewa Majaji hao, watafanya kazi wa bidii zaidi.

“Nendeni mkaongeze nguvu katika Mahakama ya Rufani, kwa kutambua umuhimu wa haki kama msingi wa amani, utulivu lakini pia maendeleo ya Taifa letu na ustawi wa wananchi kwa ujumla, haki ndio inashinda katika yote haya,” amesisitiza Mhe. Dkt. Samia.

Kadhalika, Rais Samia amewataka Majaji hao kuitumikia Nchi kwa uadilifu, weledi na uzalendo kama walivyoapa, huku akisisitiza kwa kusema kuwa, “mmeapa mtafanya kazi bila upendeleo, huba, chuki. Sasa bila upendeleo, bila upendeleo kwa sababu kazi yenu ina Kanuni zake, sasa kuna hili suala la huba na chuki, hicho ndio ninataka mkajitazame vizuri ndani yenu katika kutoa maamuzi ya hukumu zenu.”

Mkuu huo wa Nchi ameongeza kuwa, dhamana waliyopewa Majaji hao sio ya cheo tu bali pia ni wajibu wa kulinda haki za Watanzania katika maamuzi yote wanayofanya wakumbuke kuwa kwa kuwatumikia Wanadamu ni kumtumikia Mungu.

“Nimeshawaambia mara kadhaa kwamba kwa hapa duniani, ukiacha Mungu anayesimamia haki za wote, wengine ambao Mungu amewateua kusimamia haki za wenzenu ni ninyi Majaji, katika ngazi zenu tofauti tofauti. Kwahiyo mnafanya kazi kubwa na mna dhima kubwa kwa Nchi hii katika kutenda haki, kuhakikisha haki za wananchi zinapatikana lakini si tu za wananchi hata haki ya kusimamia Taifa lenu iko mikononi mwenu, kwahiyo wale wenzetu wanasema ‘the service to humanity is serving to God’ mnapohudumia wananchi kusimamia haki mnatumikia kazi ya Mungu pia,” amesisitiza Rais Samia.

Majaji walioapishwa ni Mhe. Imani Daudi Aboud, Mhe. Rabia Hussein Mohamed, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha, Mhe. Yohane Bokobora Masara, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba na Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim.

Kwa mujibu wa taarifa ya Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert, baada ya uapisho wa Majaji hao tisa (9), idadi ya Majaji wa Rufani imeongezeka kutoka 37 hadi 46 sawa na majopo 15.

Viongozi mbalimbali wamehudhuria katika hafla ya uapisho ambao ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera (Mb), Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Mhe. Daniel Sillo (MB), Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila na wengine.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Imani Daudi Aboud kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Imani Daudi Aboud akila kiapo mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Rabia Hussein Mohamed kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Rabia Hussein Mohamed akiapa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
 

Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina akiapa mbele ya Rais Samia kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Immaculata Kajetan Banzi kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
 
  Mhe. Immaculata Kajetan Banzi akiapa mbele ya Rais Samia kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe.Cyprian Phocas Mkeha kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
   
  Mhe. Cyprian Phocas Mkeha akiapa mbele ya Rais Samia kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

   Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Yohane Bokobora Masara kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Yohane Bokobora Masara akiapa mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.
   
   Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo akiapa mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Abdi Shaaban Kagomba 
kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini hati ya kiapo cha Jaji Kagomba baada ya kumuapisha yeye pamoja na wenzake nane kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimuapisha Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Ibrahim Mzee Ibhrahim akiapa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania mbele ya Rais Samia (hayupo katika picha) leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Makamu  wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi (wa kwanza kushoto), Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kushoto), Jaji Mkuu wa Zanzibar, 
Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah (wa pili kulia) na Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Mhe. Daniel Sillo (wa kwanza kulia) wakiwa katika Hafla ya Uapisho wa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Majaji na Watanzania kwa ujumla mara baada ya kuwaapisha Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Sehemu ya Viongozi mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria hafla ya Uapisho wa Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija, katikati ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani.

Majaji wapya tisa wa Mahakama ya Rufani walioapishwa leo tarehe 26 Mei, 2026 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Ikulu jijini Dar es Salaam.

Kamishna wa Maadili nchini Tanzania (Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma), Jaji Mstaafu Sivangilwa Sikalalilwa Mwangesi akiwaongoza Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani kula kiapo cha Maadili mara baada ya kuapishwa kushika wadhifa huo leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani wakila kiapo cha maadili ya utumishi wa umma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) pamoja na Viongozi wengine walioketi wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani mara baada ya kuapishwa kwao leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam. Wa tatu kushoto ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, wa tatu kulia ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, wa pili kushoto ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah, wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, wa pili kulia ni Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Mhe. Daniel Sillo (Mb) na wa kwanza kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera.

Meza Kuu katika picha ya pamoja na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya Majaji wengine wa Mahakama hiyo na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.


Meza kuu ikiongozwa na Rais Samia (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya Viongozi wa Mahakama waliohudhuria Hafla ya Uapisho wa Majaji hao leo tarehe 26 Mei, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Picha ya pamoja Meza Kuu, Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani na Viongozi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS).

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

































 

 


TMJA SONGEA YAFANYA MKUTANO WA ROBO YA KWANZA 2026

Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea

Chama cha Mahakimu na Majaji Songea tarehe 22 Mei 2026 kilifanya mkutano wa robo ya kwanza ya mwaka 2026, ikiwa ni kutekeleza matakwa ya Katiba yaliyowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mkutano huo uliofanyika kwenye ukumbi wa Heritage Cortage (Padogo Pazuri) ulioko Msamala Songea Mjini ulifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, ambaye ndiye mlezi wa chama hicho kwenye Mkoa wa Ruvuma.

Mkutano huo ulio hudhuliwa na Wanachama 58 kutoka Mahakama Kuu Songea (5), Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea (2), Mahakama ya Wilaya Songea (15), Mahakama ya Wilaya Mbinga (11), Mahakama ya Wilaya Namtumbo (10), Mahakama ya Wilaya Tunduru (10) na Mahakama ya Wilaya Nyasa (5).

Katika mkutano huo, Wanachama walijadili malengo ya TMJA Songea, ikiwemo kukuza uhuru wa Mahakama kama msingi wa kulinda haki za binadamu na uhuru, kukuza haki, maslahi na ustawi wa wanachama.

Malengo mengine ni kukuza na kulinda heshima ya ofisi ya Mahakimu na Majaji, kuongeza au kuimarisha ujuzi na uelewa wa Mahakimu na Majaji katika majukumu yao kwa kuendeleza tafiti na elimu (kuwajengea uwezo) na kutoa tuzo kwa Wilaya itakayofanya vizuri ili kuenzi kazi zao.

Katika mkutano huo, Katibu wa TMJA Songea, Mhe. Shughuli Mwapashe, alisoma tarifa fupi ya chama na kugusia vipengele mbalimbali kama mahusiano ya TMJA na Mwajili, mafunzo na semina kwa Wanachama, mafanikio pamoja na changamoto.

“Mafanikio ni pamoja na kuimarisha uhusiano uliobora kati ta TMJA na Mwajiri, kutoa elimu kwa umma kila jumatano katika kituo cha redio (selous fm) na kwenye viunga vya Mahakama, kabla ya kuanza kusikiliza mashauri na uanzishwaji wa kamati ya kuandaa majarida na elimu.

Alieleza changamoto zilizopo katika chama kama vile baadhi ya Wanachama kukosa hamasa ya chama pamoja na ufinyu wa bajeti, jambo ambalo limekuwa likisababisha Tawi kishindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu na kwa wakati.

Katibu huyo aliahidi kutimizaa kwa vitendo vigezo maalum vya kupima utendaji na ubora wa mfumo wa Mahakama kama ilivyoelekezwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, katika hotuba yake ya tarehe 13 Januari, 2026 wakati wa kufungua mkutano mkuu wa TMJA jijini Dodoma.

Vigezo hivyo ni uadilifu, uwezo wa kutekeleza majukumu kwa ufanisi, kuwiwa kuona haki inatendeka, ubunifu, uchukuaji wa hatua mapema, uzalendo na kuzingatia uhalisia wanapotekeleza majukumu yao.

Mgeni maalum katika mkutano huo, Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma, Bi. Marry Makondo, katika hotuba yake aliwapongeza Mahakamu na Majaji kwa kusaidia kwenye upatikanaji wa haki kwa wakati.

Katika hotuba yake, Mhe. Karayemaha aliwasisitiza wanachama kujitoa katika kushiriki matukio yanayohusiana na chama na kushirikiana kwa hali na mali.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha wakati wa kufungua mkutano wa TMJA Tawi la Songea.

Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe. (aliye simama).

Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma, Bi. Marry Makondo, akitoa hotuba kwa Wanachama wa TMJA Tawi la Songea.

Mwenyeki wa TMJA Tawi la Songea, Mhe. Saada tagalile,  wakati akitambulisha meza kuu.

Katibu wa TMJA Tawi la Songea, Mhe. Shughuli Mwampashe.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama Kuu Songea (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Songea (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Mbinga (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Nyasa (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Namtumbo (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Wanachama wa TMJA kutoka Mahakama ya Wilaya Tunduru (waliosimama) kwenye picha ya pamoja na meza kuu.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

Jumatatu, 25 Mei 2026

IDDI NASSIBU CHUMU APUMZISHWA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Dodoma

Aliyekuwa Dereva wa Mahakama ya Tanzania, Makao Makuu Dodoma, Iddi Nassibu Chumu, ambaye alifariki dunia tarehe 23 Mei, 2026, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma (General Hospital), amepumzishwa kwenye nyumba yake ya milele.

Marehemu Chumu amezikwa kwenye makaburi katika Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani, tukio lililohudhuriwa na mamia ya Wananchi, wakiwemo Watumishi w Mahakama ya Tanzania, na kuacha simanzi kubwa.

Ifuatayo ni sehemu ya matukio katika picha ya maziko hayo.