Jumapili, 26 Aprili 2026

JAJI MKUU MASAJU AHUDHURIA IBADA YA SHUKRANI KUMBUKIZI YA KUZALIWA BI. LOYCE NYALALI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 26 Aprili, 2026 amehudhuria Ibada maalum ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.

Ibada hiyo maalum ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai imefanyika katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro Oysterbay jijini Dar es Salaam ikiongozwa na Paroko wa Kanisa hilo, Padri Bartholomew Mrosso na Padri mwenzake.

Katika mahubiri yake wakati wa ibada hiyo, Padri Mrosso ametoa rai kwa Waumini kumshukuru Mungu kwa uzima kwa kuwa uzima ni zawadi kubwa ambayo kwayo yatupasa kumshukuru Mungu. Amesisitiza kwa kusema, “tumshukuru Mungu kwa uzima kwanza halafu vingine ndio vifuate.”

Kadhalika Padri huyo, amewakumbusha Viongozi kusimamia haki, na kutenda mema kwa walio chini yao na wanaowaongoza.

“Katika Injili ya Jumapili ya leo ya Mchungaji Mwema msingi wake ni Uongozi, namna fulani ya Uongozi ambao Kristo anaudhihirisha kupitia matendo yake mema,” ameeleza.

Ameongeza kuwa, Kiongozi anapaswa kusimama kwa ajili ya wale anaowaongoza hivyo, Uongozi usichukuliwe kama ajira bali kujitoa na kuwajali watu waliopo chini.

Ibada hiyo imehudhuriwa pia na baadhi ya Viongozi wakiwemo Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba, Majaji Wastaafu wa Mahakama Rufani na Mahakama Kuu, Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakili Tom Nyanduga, Wenza wa Majaji Wakuu Wastaafu akiwemo Mama Marina Juma, Mama Sada Chande pamoja na ndugu, jamaa na marafiki na wageni wengine waalikwa.

Baada ya ibada hiyo, imefanyika sherehe maalum ya kumpongeza Bi. Loye Nyalali iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Kadinali Rugambwa uliopo pembeni ya Kanisa la Mt. Petro jijini Dar es Salaam.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kushoto mwenye tai nyekundu) akiwa katika misa ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, marehemu Francis Nyalali. Ibada hiyo imefanyika leo tarehe 26 Aprili, 2026 katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro jijini Dar es Salaam. Kulia kwa Jaji Mkuu ni Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba na aliyeketi mbele ni Mama Loyce Nyalali anayeadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimsalimia na kumpongeza Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.
 
Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiingia ndani ya Kanisa Katoliki la Mtakatifa Petro lililopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya ibada maalum ya kumshukuru Mungu kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiwa katika uso wa furaha ikiwa ni siku yake maalum ya kuadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Stephen Bwana (kushoto) pamoja na mwenza wake (katikati) na wengine wakiwa katika ibada ya shukrani maalum kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Paroko wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro, Padri Bartholomew Mrosso akiongoza ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Mama Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.


Picha mbalimbali za matukio ya Ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

WATUMISHI WA MAHAKAMA KIGOMA WAKUMBUSHWA KUZINGATIA MATUMIZI YA OFISI MTANDAO

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mkurugenzi wa Kumbukumbu na Nyaraka Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula amewasisitiza Watumishi wa Mahakama Kigoma juu ya matumizi ya Ofisi mtandao na kuongeza weledi wa matumizi ya mfumo huo ili kuendana na kasi ya maboresho ya Mahakama. 

Bw. Manyambula alisema hayo tarehe 23 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Kigoma akiwa katika ziara yake ya ukaguzi wa Masjala za Mahakama katika eneo la utunzaji wa kumbukumbu, nyaraka na taarifa zinazozalishwa kila siku katika shughuli zote za Mahakama.

“Watumishi wenzangu nipo kwenye ukaguzi wa kawaida kufahamu changamoto zenu na kuwapongeza pale panapostahili kupongezwa na zaidi kuwasisitiza kuendelea kutumia mifumo hii kwa ufasaha ili kuweza kuhifadhi nyaraka zetu katika mifumo yetu bila kufanya shughuli zetu nje ya mifumo yetu, hata hivyo Kanda ya Kigoma mnafanya vizuri muendelee kufanya hivyo ili mbaki vinara wa matumizi mazuri ya Ofisi mtandao,” alisema Mkurugenzi huyo.

Alieleza kuwa, Kurugenzi ya Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka Mahakama ya Tanzania inaendelea na usimamizi mzuri wa Ofisi mtandao kuhakikisha Idara zote zilizopo Mahakamani zinatunza kumbukumbu na nyaraka katika mifumo na mpangilio uliokubalika katika viwango vya utunzaji wa nyaraka pamoja na maelekezo yanayoelekezwa katika miongozo mbalimbali ya utunzaji wa kumbukumbu katika Masjala.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Mhoja alimshukuru Mkurugenzi huyo kwa niaba ya watumishi wa Kanda ya Kigoma, kwa ukaguzi wake kwani ndio unaoleta chachu ya kuwa bora zaidi na maelekezo aliyoyatoa ameahidi kuyasimamia ili Mahakama Kuu Kigoma iendelee kuwa kinara katika matumizi bora na sahihi ya Ofisi Mtandao (e-Office).

Aidha, wajumbe waliohudhuria kikao cha kuhitimisha ukaguzi wa utunzaji wa kumbukumbu katika Mahakama hiyo ni Maofisa na Wakuu wa Vitengo pamoja watumishi wanaotumia mfumo huo pamoja na Watunza Kumbukumbu na Nyaraka wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma.

Mkurugenzi wa Kumbukumbu na Nyaraka Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula akisisitiza jambo kwa watumishi wa Mahakama Kuu Kigoma alipokuwa akitoa tathmini fupi ya ukaguzi wake.


Mkurugenzi wa Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka- Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula akisaini katika kitabu cha wageni  alipowasili katika Ofisi ya Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo.


Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo(katikati) akiwa katika maongezi na mgeni wake Mkurugenzi wa Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula (wa pili kushoto). Kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Mhoja na wa kwanza kushoto ni Ofisa Kumbukumbu kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Bw. Kelvin Mayala wakiwa katika mazungumzo mara baada ya kuwasili Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.
Sehemu ya watumishi waliohudhuria kikao cha tathmini ya ukaguzi wa Mfumo wa Ofisi mtandao ya Mahakama wakimsikiliza kwa makini Mkurugenzi wa Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula (aliyesimama).

 Mkurugenzi wa 
Idara ya Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Ofisa Utumishi Mwandamizi, Bw. Festo Sanga (kulia) na Ofisa Kumbukumbu,  Bw. Kelvin Mayala.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 

BENKI YA DUNIA WAKIPONGEZA KITENGO CHA MABORESHO YA MAHAKAMA

  • Ni kufuatia usimamizi mzuri wa Miradi ya Ujenzi wa Mahakama 

Na AIDAN ROBERT, Mahakama -Kigoma

Ujumbe wa Benki ya Dunia (WB) ukiongozwa na Kiongozi wa ujumbe huo, Bi. Christina Owuor umempongeza Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania (JDU), Mhe. Dkt. Angelo Rumisha baada ya kujionea maendeleo ya Miradi ya Ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Bangwe, Heru juu na Manyovu walipoitembelea miradi hiyo hivi karibuni.

Ujumbe huo uliongozwa na Mhe. Dkt. Rumisha kufanya ukaguzi wa Ujenzi wa Miradi ya Mahakama za Mwanzo tatu (3) zinazojengwa mkoani Kigoma ili kuona maendeleo ya miradi hiyo.

Akitoa pongezi hizo, Kiongozi wa Ujumbe huo, Bi. Christina Owuor aliipongeza Mahakama ya Tanzania kupitia Kitengo cha Maboresho (JDU) kwa usimamizi mzuri wa ujenzi wa Mahakama za Mwanzo tatu zinazojengwa Kanda ya Kigoma.

“Mhe. Rumisha (Jaji), hongereni kwa ujenzi huu wa Mahakama hizi, nawapongeza sana kwa kuwa mmehakikisha ubora wa vifaa vya ujenzi vilivyotumika kujenga majengo haya ni vya kiwango kizuri sana na kwa kupitia ubora wa miradi hii, nadhani tutafikiria kuendelea kutoa miradi mingine kwenu maana mmeonesha thamani ya fedha imeonekana katika miradi hii ya Kanda ya Kigoma,” alisema Bi. Owuor.

Naye Jaji Rumisha alisema, “napokea pongezi hizi kubwa mlizotupatia kwa usimamizi bora wa ujenzi wa miradi hii mitatu, hakika tunashukuru kwa pongezi hizi kwani usimamizi wa miradi hii una weledi mkubwa wa watalaam wetu kusimamia kila hatua na ndio matokeo ya ufanisi huu wa miradi hii, aidha, nami niwapongeze wataalam wetu kwa kutumia vema utalaamu wao kwa tija ya Taasisi yetu.”  

Kwa upande wake, Mkandarasi Mshauri Mwelekezi, Bw. Norman & Dawbarn aliwasilisha taarifa yake kuwa, ujenzi huo umefikia asilimia 98 kwa Mahakama zote tatu (3) na kwamba kwa sasa zinasubiriwa samani za ofisi ili majengo hayo yaweze kuanza kutoa huduma haraka iwezekanavyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Kigoma,  Bw. Yusuph Mhoja alitoa shukrani zake kwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kitengo cha Maboresho, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha na kwa ujumbe wa Benki ya Dunia kufika mkoani humo kukagua maendeleo ya ujenzi wa miradi hiyo kwani tegemeo la wananchi wa Mkoa wa Kigoma ni kupata huduma karibu ili kuwapunguzia baadhi ya gharama za usafiri wanazozitumia kwa sasa kwenda kupata haki zao mahakamani.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania (JDU),  Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (wa kwanza kulia) akitoa maelekezo kwa Mkandarasi kumaliza haraka ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Bangwe Kigoma. Wa kwanza kushoto ni Kiongozi wa ujumbe kutoka Benki ya Dunia (WB), Bi. Christina Owuor.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania (JDU),  Mhe. Dkt. Angelo Rumisha akitoa maelekezo kadhaa ya kiukaguzi kwa Wakandarasi katika umaliziwaji wa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Heru Juu, akiwa na Wajumbe wa Benki ya Dunia pamoja na sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kasulu.

Ukaguzi Mahakama ya Mwanzo Heru Juu-Kigoma

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (aliyenyoosha mkono) akisema neno baada ya kupokea pongezi kutoka kwa Kiongozi wa Ujumbe wa Benki ya Dunia kufuatia ubora wa ujenzi uliofanyika kwenye miradi yote ya  Mahakama Mwanzo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania (JDU),  Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (mbele)  Viongozi kutoka Benki ya Dunia pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kigoma Bw. Yusufu Mhoja (aliyevaa koti la rangi la kijivu) na watumishi wa Mahakama hiyo wakikagua Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Heru Juu.

Picha ya pamoja katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania (JDU),  Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (katikati). Wa pili kulia ni Kiongozi wa Ujumbe kutoka Benki ya Dunia (WB), Bi. christina Owuor, wa pili kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka, wa kwanza kushoto ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kasulu, Mhe. Imakulata Shuli, na wengine ni Viongozi na wajumbe kutoka Benki ya Dunia pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Heru Juu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 

 

Ijumaa, 24 Aprili 2026

‘USIKILIZAJI, UMALIZAJI HARAKA WA MASHAURI UNA MCHANGO MKUBWA KWA TAIFA KIUCHUMI, KIJAMII’

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, amesema leo tarehe 24 Aprili, 2026 kuwa, usikilizaji na umalizaji wa haraka wa mashauri yaliyopo mahakamani una mchango mkubwa kwa Taifa kiuchumi na kijamii

Akiwasilisha bungeni Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mhe. Dkt. Homela ameeleza pia kuwa suala la kuharakisha usikilizaji wa mashauri mahakamani ni moja ya vipaumbele muhimu vya Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha kuwa Wananchi wote wanapata haki kwa wakati.

Ameliambia Bunge kuwa katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026, kulikuwa na jumla ya mashauri 205,038 mahakamani na kati ya hayo, 45,187 yalianza mwaka 2024/ 2025, yaani yalikuwepo kabla ya tarehe 30 Juni, 2025, na mashauri 159,851 yalifunguliwa katika mwaka wa fedha 2025/2026.

“Kati ya mashauri 205,038 yaliyokuwepo, mashauri 166,553 yalisikilizwa na kuhitimishwa na mashauri 38,485 yanaendelea katika hatua mbalimbali. Aidha, mashauri yenye umri mrefu mahakamani ni 3,675,” Waziri Homela amesema.

Amebainisha kuwa katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, kasi ya uondoshaji wa mashauri mahakamani (case clearance rate) ni asilimia 104, huku uwezo wa umalizaji wa mashauri (disposal rate) ni asilimia 81.

Akizungumzia mchango wa usikilizaji na umalizaji wa haraka wa mashauri mahakamani kwa Taifa kiuchumi na kijamii, Waziri Homela ameeleza kuwa katika zoezi maalum la kusikiliza mashauri ya kiuchumi na kibiashara lililofanywa na Mahakama Oktoba na Novemba, 2025 lilifanikisha umalizaji wa mashauri 2,973.

“Kuhitimishwa kwa mashauri hayo kuliwezesha kuachilia jumla ya shilingi za Kitanzania trilioni 13.1 zilizokuwa zimeshikiliwa na mashauri hayo kuingia kwenye mzunguko wa uchumi,” amesema.

Akizungumzia ukaguzi na usimamizi wa shughuli za kimahakama katika ngazi ya Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo kwa Masjala Ndogo 20 za kimahakama, Mhe. Dkt. Homela amesema kuwa zoezi hilo limefanyika kwa asilimia 100.

“Matokeo ya ukaguzi huo yamewezesha kuongeza kasi ya umalizaji mashauri mahakamani kwa kuwa huambatana na ukaguzi wa jalada moja baada ya jingine,” Waziri Homela ameliambia Bunge wakati anawasilisha hotuba yake.

Ameeleza vilevile kuwa Magereza 129 kati ya 130 yaliyopo yalikaguliwa, sawa na asilimia 98.8 ikilinganishwa na ukaguzi wa kipindi kama hiki katika mwaka 2024/2025 uliofanyika kwa asilimia 80.2.

Waziri pia ameeleza kuwa katika mwaka 2025/2026, Mahakama ya Tanzania imeendelea kushirikiana na Wadau wake katika mnyororo wa haki jinai ili kuhakikisha mashauri yanamalizika kwa wakati.

Amebainisha kuwa tarehe 12 na 13 Machi, 2026 Mahakama iliitisha kikao kazi cha pamoja kilichohusisha Wadau kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

Waziri Homela ametaja Wadau wengine waliohudhuria kikao kazi hicho kama Chama cha Wanasheria Tanganyika, Idara ya Ustawi wa Jamii, Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza pamoja na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya.

“Kupitia kikao hicho, wajumbe walijadili taarifa ya hali ya mashauri ya mlundikano hadi kufikia Desemba, 2025, hali ya mahabusi magerezani na mikakati ya kupunguza mlundikano pamoja na kuongeza matumizi ya TEHAMA kwenye usikilizaji wa rufaa na maombi,” amesema.

Kwa mujibu wa Mhe. Dkt. Homela, kikao hiki kimesaidia kupata ufumbuzi wa pamoja wa changamoto mbalimbali, ikiwemo kuongeza kasi ya umalizaji wa 36 mashauri mahakamani, na kila mdau kutekeleza wajibu wake kwa wakati.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, akiwasilisha bungeni jijini Dodoma Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027.


Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia uwasilishaji wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria bungeni kuhusu mpango na makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

 

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania likiendelea na shughuli zake jijini Dodoma.

MAGEUZI YA SEKTA YA SHERIA KUIMARISHA MAHAKAMA, IJA LUSHOTO

Na HALIMA MNETE- Mahakama, Dodoma

Serikali imeendelea kuimarisha Mhimili wa Mahakama pamoja na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, katika jitihada za kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati, kwa usawa na kwa kuzingatia misingi ya utawala wa sheria.

Akiwasilisha bungeni mpango na makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2026/2027 leo tarehe 24 Aprili, 2026, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera, amesema mageuzi yanayoendelea yanalenga kuifanya Mahakama kuwa Mhimili imara unaochochea maendeleo ya Taifa.

Aidha, Waziri Homela amelieleza Bunge jijini Dodoma kuwa katika jitihada za kuimarisha mifumo ya utoaji haki, Serikali pia imeendelea kuboresha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kupitia mifumo kama Mahakama Mtandao na e-CMS, ambayo imerahisisha usikilizaji wa mashauri na upatikanaji wa nyaraka kwa wakati.

Kwa upande wa elimu na mafunzo, amesema kuwa IJA imeendelea kuwa kitovu muhimu cha kujenga uwezo wa watendaji wa Mahakama. Kupitia chuo hicho, mafunzo ya kitaaluma na kiutawala yamekuwa yakitolewa ili kuongeza ufanisi, maadili na weledi katika utoaji haki.

Aidha, Waziri Homela ameeleza kuwa IJA imeendelea kushiriki katika utoaji wa huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali za kusogeza huduma za haki karibu na jamii, hususan kwa makundi yenye uhitaji.

Sambamba na hayo, Serikali imeendelea kuhimiza matumizi ya mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR) ili kupunguza mzigo wa mashauri mahakamani na kuharakisha upatikanaji wa haki bila urasimu mrefu.

Katika hotuba hiyo, Waziri Homera alitoa shukrani za kipekee kwa uongozi wa Mhimili wa Mahakama kwa mchango wao katika kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Aidha, amempongeza Mhe. George Masaju kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania. Uteuzi wake unadhihirisha umahiri na uzoefu alionao katika Sekta ya Sheria kwa ujumla, ikiwemo Mhimili wa Mahakama.

Katika hotuba hiyo, Mhe. Homera ametoa pia shukrani za kipekee kwa uongozi wa mhimili wa Mahakama kwa mchango wao katika kuimarisha utoaji wa haki nchini. Amewataja Viongozi wengine wa juu wa Mahakama akiwemo Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha IJA, Mhe. Dkt. Paul Faustine Kihwelo, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel, na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Mhe. Homera alisisitiza kuwa uongozi huo umeendelea kuwa nguzo muhimu katika mageuzi ya kimfumo ndani ya sekta ya sheria na kuongeza imani ya Wananchi kwa vyombo vya utoaji haki. “Sekta ya Sheria siyo tu msimamizi wa sheria pekee, bali ni injini ya uthabiti wa Taifa na kichocheo cha maendeleo ya uchumi katika kufikia malengo ya DIRA 2050.”

Waziri Homera alieleza kuwa uongozi huo umekuwa mstari wa mbele kusukuma mageuzi ya kimfumo ndani ya Mahakama, hususan katika kuongeza matumizi ya teknolojia, kuboresha usimamizi wa mashauri na kuimarisha uwajibikaji.

Alisisitiza kuwa mchango wa viongozi hao umeendelea kujenga imani ya Wananchi katika Mhimili wa Mahakama na kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kwa usawa.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha Mahakama pamoja na Taasisi zake ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wote, kwa wakati na kwa usawa, ikiwa ni msingi muhimu wa amani, utulivu na maendeleo ya Taifa.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera akionesha mpango na makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2026/2027. Picha chini, akisoma hotuba ya bungeni Dodoma kuhusu mpango na makadirio hayo.


Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia uwasilishaji wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria bungeni kuhusu 
mpango na makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Alhamisi, 23 Aprili 2026

MAHAKAMA MOROGORO YATOA MAFUNZO KUHUSU MFUMO WA KUHIFADHI MWENENDO MAHAKAMA ZA MWANZO

Na ASHA JUMA- Mahakama Morogoro.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, imeendesha mafunzo maalumu kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo pamoja na Makarani kuhusu matumizi ya mfumo wa kuhifadhi mienendo, vielelezo na hukumu ikiwa ni sehemu ya kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji haki.

Mafunzo hayo yalifanyika jana tarehe 22 Aprili, 2026, katika Ukumbi wa Mikutano uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro, sambamba na njia ya mtandao (online) ili kuwezesha ushiriki mpana.

Mafunzo hayo yaliendeshwa na kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Morogoro, kikiongozwa na Mkuu wa Kitengo hicho pamoja na Mwanzilishi wa mfumo huo, Bw. Justine Kemhe. Aidha, mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Amiri Msumi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Msumi alikishukuru kitengo cha TEHAMA kwa ubunifu wao katika kuanzisha mfumo huo unaoitwa unaoitwa Primary Court Depository, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuboresha utendaji kazi wa Mahakama. Pia aliwahimiza washiriki kutoa ushirikiano wa kutosha pale changamoto zitakapojitokeza ili kuhakikisha mfumo unaboreshwa zaidi.

“Hongereni sana kwa kutafsiri mawazo ya watu na kuyaweka katika utekelezaji. Nawasihi Mahakimu na watumiaji wote wa mfumo huu kuwasilisha changamoto na maoni yao ili kuboresha mfumo huu,” alisema Mhe. Msumi.

Mfumo wa Primary Court Depository ni sehemu ya jitihada za kuendeleza matumizi ya TEHAMA katika Mahakama ya Tanzania. Mfumo huu unasaidia kurahisisha upatikanaji wa mienendo ya mashauri kutoka Mahakama za Mwanzo pamoja na kuhifadhi kumbukumbu hizo kidijitali, hivyo kupunguza usumbufu wa kutafuta nyaraka kwa njia za kawaida.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA alibainisha umuhimu wa kuongeza vifaa vya TEHAMA kama kompyuta na skana ili kuhakikisha mfumo huo unafanya kazi kwa ufanisi zaidi. Aliongeza kuwa mfumo huo tayari umeanza kutumika katika baadhi ya Masjala nyingine, zikiwemo Simiyu na Geita.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi  wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage, alisisitiza umuhimu wa washiriki kuzingatia maelekezo waliyopewa wakati wa mafunzo hayo, akieleza kuwa mfumo huo utarahisisha kazi na kuondoa changamoto ya upatikanaji wa mienendo ya mashauri.

Mafunzo haya yanatarajiwa kuleta mabadiliko chanya katika utendaji kazi wa Mahakama za Mwanzo kwa kuongeza ufanisi, uwazi na uhifadhi bora wa kumbukumbu za mashauri kwa njia ya kisasa (kidijitali).

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe.Amiri Msumi, akifungua mafunzo hayo.

Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA pamoja na Mwanzilishi wa mfumo huo, Bw. Justine Kemhe, akitoa mafunzo juu ya mfumo wa Primary Court Depository.

Mahakimu  pamoja na Makarani wakifuatilia mafunzo hayo kwa njia  ya mtandao na njia ya kawaida.


Habari hii imehririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.