Na
MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewasihi Majaji wa
Mahakama ya Rufani wapya kuwa huru kutoa maoni au misimamo ya kisheria wanayoamini
ni sahihi bila hofu yoyote, kwani kwa kufanya hivyo, watakuwa wanaboresha
maamuzi ya Mahakama ya Rufani ambayo ndiyo inategemewa kutoa kauli ya mwisho
kwa mashauri yanayofika mbele yake.
Mhe.
Masaju amesisitiza hilo kupitia Hotuba yake ya Kufunga Mafunzo Elekezi kwa
Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya iliyosomwa na Mwakilishi wake Jaji wa
Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe.
Jacobs Mwambegele leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
“Nawasihi muwe huru kutoa maoni au
misimamo ya kisheria mnayoamini ni sahihi bila hofu yoyote, kwani kwa kufanya
hivyo ndiyo mtakuwa mnaboresha maamuzi ya Mahakama ya Rufani ambayo ndiyo
inategemewa kutoa kauli ya mwisho kwa mashauri yanayofika mbele yake lakini
ndiyo inayotoa mwongozo wa tafsiri ya sheria unaopaswa kufuatwa na Mahakama
zote za chini yake na kujenga au kuendeleza misingi ya kisheria (jurisprudence)
nchini,” amesema Mhe. Masaju kupitia hotuba hiyo.
Jaji Mkuu amesema kuwa, moja kati ya Mada
waliyojifunza Majaji hao inahusu Ushirikiano katika Mahakama ya Rufani (Collegiality
at the Court of Appeal), hivyo, amewaomba pia kujenga utamaduni wa
kushirikiana, kusikilizana, kuheshimiana na kujenga maamuzi bora kupitia
majadiliano ya kitaaluma. Na kwamba hiyo haimaanishi kukubali tu msimamo wa
Majaji wengine hata kama dhamiri na utaalamu wao vinaelekeza vinginevyo.
Aidha, Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, katika
mada ya Haki ya Msingi dhidi ya Masharti ya Kiufundi ambapo amesema, “mada hii
inatutaka kuamua mashauri kwa kubainisha haki na wajibu wa kila mdaawa, ambalo
ndilo jukumu la msingi la Mahakama, kuliko kuamua mashauri kwa kutumia masharti
ya kiufundi ambayo hayatatui mgogoro uliopo baina ya wadaawa. Na kama ambavyo
mmeona, hili lina msingi wake kuanzia kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ambayo mmeapa kuizingatia, hivyo nawasihi sana mkalitekeleze hilo.”
Amesema kuwa, mada hiyo msingi wake umeanzia
kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo wameapa kuizingatia,
hivyo amewasisitiza wakalitekeleze hilo ipasavyo. Na kwamba wanapaswa kulitekeleza
vema zaidi kwa kutumia hekima na akili kama alivyosema siku ya ufunguzi wa
mafunzo hayo, kwani hekima na akili walizobarikiwa na Mwenyezi Mungu
zitawawezesha kuwapa upeo wa ziada wa kupata ufumbuzi wa masuala magumu na
yanayohitaji ubunifu na kujiongeza (creativity and proactiveness).
Akizungumzia kuhusu umuhimu wa Mafunzo
Elekezi, Jaji Mkuu amesema, Mafunzo hayo yalilenga kuwaandaa washiriki kuanza
kutekeleza majukumu ya Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa weledi, kujiamini zaidi
na kwa ufanisi zaidi.
“Kama tunavyofahamu, Mahakama ya
Rufani ndiyo chombo chenye kauli ya mwisho katika mfumo wa utoaji haki nchini,
hivyo ni muhimu Majaji wapya wakaandaliwa kuanza kazi hiyo wakiwa wamepigwa
msasa ili kuelewa vizuri zaidi Sheria, Kanuni na taratibu zinazotumika katika
Mahakama hii licha ya ukweli kuwa ninyi tayari ni wataalam wa Sheria,” imeeleza
hotuba hiyo iliyosomwa na Mhe. Mwambegele.
Kadhalika, Mhe. Masaju amesema mafunzo
hayo yasiwe mwisho wa kujifunza na kuwataka Majaji hao kuendelea kujifunza hata
baada ya mafunzo hayo.
Akizungumzia Wawezeshaji na Mtindo wa
Uwasilishaji mada, amesema, “Kama nilivyosema siku ya ufunguzi, wawezeshaji
waliowezesha katika mafunzo haya ni wabobezi na wana uzoefu mkubwa wa utendaji
kazi katika Mahakama ya Rufani. Waheshimiwa Majaji Wastaafu Mhe. Msoffe na Mhe.
Rutakangwa wamehudumu katika Mahakama hii kwa muda mrefu na hukumu zao
zimeendelea kutumika kama rejea na mwongozo katika maamuzi yetu mpaka sasa.”
Ameongeza kuwa, wakati mafunzo hayo
yakiendelea alipata fursa ya kufika mara kadhaa, na alishuhudia mtindo mzuri wa
uwasilishaji ambapo alishuhudia mafunzo hayo yakitolewa kwa mtindo wa
majadiliano ya pamoja kama jopo na ushirikishwaji wa kila mmoja badala ya
mhadhara wa upande mmoja.
“Mtindo huu unawajenga kufikiri,
kuchambua na kufanya kazi kwa pamoja kama ulivyo mtindo wa ufanyaji kazi katika
Mahakama ya Rufani,” ameeleza.
Vilevile, Jaji Mkuu amekipongeza Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kuandaa mafunzo hayo,
Wawezeshaji wote wa mafunzo sambamba na kuwapongeza Majaji hao kwa kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo na kuwatakia kila la heri kwenye utekelezaji wa majukumu yao huku akiwakumbusha kila
mmoja kukiishi kiapo chake na kuzingatia dhamana kubwa waliyopewa na Taifa na matarajio ya
wananchi kwao.
Katika hatua nyingine, naye Jaji Mwambegele amewashauri
Majaji hao kusoma hukumu za Majaji Wastaafu, Mhe. Msoffe na Mhe. Rutakangwa na
nyingine ili kuongeza maarifa zaidi katika utekelezaji wa jukumu la msingi la
utoaji haki.
“Someni hukumu zao tangu wakiwa Majaji wa Mahakama Kuu mpaka Majaji
wa Mahakama ya Rufani. Nina uhakika hamtajutia, Mimi nimekuwa msomaji wa hukumu
za hawa Wawezeshaji tangu nikiwa Wakili wa Serikali, mpaka nikawa Jaji wa
Mahakama Kuu, na sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani. Kama alivyosema Mheshimiwa
Jaji Mkuu hapa, ni kwamba hawa Wawezeshaji wana uwezo mkubwa, ninachotaka
kuwasihi katika kuchomekea kwangu hapa ni kwamba, mpate muda wa kusoma hukumu
zao. Uwezo wao sio wa kawaida. Mtakapokuwa mnasoma hukumu zao, mtagundua kwamba
ni kwa nini Mahakama bado inawatumia mpaka leo,” amesisitiza Jaji Mwambegele.
Akizungumzia jinsi Mahakama ya Rufani inavyofanya maamuzi, Mhe.
Mwambegele amesema maamuzi ya Mahakama hiyo ni maamuzi ya jopo la Majaji watatu,
na maamuzi ya Majaji watano au kuendelea kwa (full bench), ambapo amesema, “Na
jinsi ya kufanya, tunafanya maamuzi kwa kujadiliana, tukiongozwa na sheria.
Pamoja na mlivyofundishwa, nawasihi pia mkasome hukumu ya Ahmadi Chali dhidi ya
Jamhuri, imekuwa ‘reported’ katika mwaka 2006 TLR 313. Hukumu hii inaonesha ni
jinsi gani hukumu ya Mahakama ya Rufani inaandikwa.”
Ameongeza kuwa, kupitia hukumu hiyo watapata habari ya ziada
kuhusiana na nini kifanyike endapo mmoja wa jopo anashindwa kutekeleza jukumu
lake, ama kwa sababu ya kiafya, au kwa kufariki na mambo mengine kama hayo. “Mtajua
kwamba hukumu ya Mahakama ya Rufani inafanywa kwa pamoja, ‘this is a collegial Court’,” amesisitiza.
Hali kadhalika, Jaji Mwambegele amewasisitiza Majaji hao kuwa
na Ushirikiano na Uadilifu wanapotekeleza majukumu yao.
Akitoa neno kwa niaba ya Majaji wenzake wakati wa hafla ya kufunga mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Aboud ameishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto chini ya Mkuu wa Chuo hicho ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo kwa kuandaa mafunzo hayo muhimu.
Kadhalika, Mhe. Aboud amewashukuru Wawezeshaji wote wa Mafunzo hayo wakiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju na Majaji Wastaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. January Msoffe na Mhe. Edward Rutakangwa.
Majaji hao tisa waliopatiwa mafunzo elekezi ambao ni Mhe.
Imani Daudi Aboud, Mhe. Rabia Hussein Mohamed, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina,
Mhe. Immaculata Kajetan Banzi, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha, Mhe. Yohane Bokobora
Masara, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba na Mhe.
Ibrahim Mzee Ibrahim wote kwa pamoja
wamepatiwa vyeti vya kuhitimu Mafunzo hayo muhimu ambayo ni moja ya maandalizi ya
kuanza kazi rasmi kazi katika Mahakama ya Rufani ambayo ndio ngazi ya juu
katika mfumo wa utoaji haki nchini.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa (waliosimama) waliohitimu Mafunzo Elekezi leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akitoa hotuba ya kutoka Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya pamoja na baadhi ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama na IJA wakisikiliza Hotuba ya Jaji Mkuu ya Kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya iliyokuwa ikitolewa na Mwakilishi wake Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (hayupo katika picha) leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Daudi Aboud ambaye ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rabia Hussein Mohamed ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Yohane Bokobora Masara ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba ameshiriki mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati wa hafla ya kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mahakama (waliosimama) waliohudhuria hafla ya ufungaji wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti ya maandalizi ya Mafunzo hayo (waliosimama). Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.
(Picha na MARY GWERA & FAUSTINE KAPAMA, Mahakama)