- Washiriki watakiwa kuimarisha maadili, matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa mashauri
Na HALIMA MNETE
& JAMES BUSANYA-Mahakama, Dodoma.
Msajili wa Mahakama Kuu
ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, leo tarehe 9 Machi 2026 amefungua mafunzo ya
kubadilishana uzoefu kati ya Maofisa wa Mahakama ya Tanzania na wenzao kutoka
Mahkama ya Zanzibar, yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini
Dodoma.
Akizungumza wakati wa
ufunguzi huo mbele ya washiriki kutoka Zanzibar wakiongozwa na Jaji wa Mahkama
Kuu Zanzibar, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim, Mhe. Tengwa alisema mafunzo hayo ni
sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kimfumo kati ya Taasisi hizo
mbili katika kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.
Alisema Mahakama ya
Tanzania na Mahakama ya Zanzibar zimeona umuhimu wa kuendelea kubadilishana
uzoefu ili kuimarisha weledi, uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa
Mahakama, hali itakayosaidia kuongeza imani ya wananchi kwa Mhimili wa utoaji
haki.
“Nawapongeza washiriki
wote kutoka Zanzibar kwa kufika Dodoma salama. Mafunzo haya ni fursa muhimu ya
kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uwezo wetu katika utoaji wa
huduma bora za Mahakama,” alisema Mhe. Tengwa.
Aliongeza kuwa uchaguzi
wa Dodoma kama eneo la kufanyia mafunzo hayo umezingatia mazingira yake tulivu
yanayofaa kwa kujifunza na kujadiliana masuala muhimu yanayolenga kuboresha
utendaji wa Mahakama.
Katika hotuba yake,
alieleza kuwa mafunzo hayo yatajadili mada mbalimbali muhimu ikiwemo ukaguzi wa
shughuli za Mahakama, utekelezaji wa majukumu ya msingi, maboresho ya huduma za
Mahakama, maadili na namna ya kushughulikia malalamiko ya kimaadili, usimamizi
wa mashauri, matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano katika usimamizi
wa mashauri pamoja na kuharakisha umalizaji wa mashauri.
Aidha, alisisitiza
umuhimu wa kuzingatia usawa wa kijinsia katika utoaji wa huduma za Mahakama,
akieleza kuwa Mahakama inapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha haki na
usawa vinazingatiwa kwa vitendo katika jamii.
Mhe. Tengwa alinukuu
kauli ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin William Mkapa,
aliyewahi kusema kuwa mtu hawezi kujua kama mama yake ni mpishi mzuri hadi pale
atakapoonja chakula kilichopikwa na mama mwingine, akieleza kuwa mfano huo
unaonesha umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wengine.
Alisema kuwa kupitia
mafunzo hayo washiriki wanatarajiwa kuwa mabalozi wa kuimarisha utatuzi wa
migogoro kwa wakati, kuboresha huduma za Mahakama kupitia ukaguzi pamoja na
kuimarisha maadili na usawa wa kijinsia katika utendaji wao.
Mafunzo hayo ya siku tano
yatahitimishwa tarehe 13 Machi, 2026, yakilenga kuongeza ufanisi katika
usimamizi na utoaji wa haki kwa wananchi.


































