- Awataka pia kuheshimu utawala wa sheria, kuendeleza ushirikiano na Wadau
Na
FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Jaji
wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, amewahimiza Watumishi
wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kuendelea kulinda uhuru wa Mahakama,
kuheshimu utawala wa sheria na kuendeleza ushirikiano baina ya Mahakama,
Taasisi na Wadau wa Haki Kazi nchini.
Mhe.
Dkt. Mlyambina alitoa wito huo usiku wa kuamkia Jana tarehe 18 Juylai, 2026
kwenye hafla ya kumuaga iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirika la Hifadhi
ya Jamii PSSSF Mwenge jijini Dar es Salaam baada ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa
Jaji wa Mahakama ya Rufani hivi karibuni
na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Haki
inapotekelezwa kwa wakati na kwa usawa, hujenga amani mahali pa kazi, huongeza
imani ya wananchi kwa Taasisi za umma na huimarisha maendeleo ya Taifa,”
alisema huku akinukuu maneno ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere
ambaye alisema, “Haki ndiyo msingi wa amani, na amani ndiyo msingi wa
maendeleo.”
Mhe.
Dkt. Mlyambina alimshukuru kila mmoja kwa ushirikiano, heshima, urafiki na
msaada waliompa katika kipindi chote alichohudumu kama Jaji Mfawidhi wa
Mahakama ya Kazi na kwamba ataendelea kuyathamini mahusiano hayo na popote atakapokuwa
ataendelea kuwa balozi mwema wa Mahakama ya Kazi.
Jaji
Mlyambina alieleza kuwa anajivunia kuwa sehemu ya safari ya kuendelea
kuimarisha Mahakama ya Kazi, kwani ameshuhudia maendeleo katika usimamizi wa
mashauri, matumizi ya teknolojia, uboreshaji wa huduma kwa wananchi, na
kuimarika kwa ushirikiano na wadau mbalimbali.
“Mafanikio
haya hayakuwa ya mtu mmoja, ni matokeo ya kazi ya pamoja. Tulifanya kazi kama
timu moja. Timu yetu haikuwa kikundi cha watu wanaofanya kazi pamoja, ilikuwa
kikundi cha wau wanaoaminiana kila mmoja. Nimebahatika kufanya kazi na timu
yenye uwezo mkubwa, inayojali haki na inayoweka mbele maslahi ya wananchi. Kila
mmoja wenu amechangia mafanikio yaliyopatikana,” alisema na kuwashukuru kwa
dhati Majaji wenzake, Wasajili, Mahakimu na watumishi wote wa Mahakama ya Kazi.
Aidha,
Mhe. Dkt. Mlyambina alieleza kuwa akiwa Jaji Mfawidhi alipata nafasi ya
kujifunza, kufundishwa na kushirikiana na watu wenye weledi mkubwa na kujifunza
kuwa uongozi si mamlaka bali ni dhamana; si nafasi ya kutawala bali ni wajibu
wa kutumikia wengine kwa haki, busara na unyenyekevu.
Alimnukuu
Mwandishi Simon Sinek katika kitabu chake ‘Find your why’ uk. 157, ambaye
anasema, “The greatest contribution of a leader is to make other leaders” kwa
tafsiri isiyorasmi kwa Kiswahili anasema, “Mchango mkubwa wa Kiongozi ni kuwafanya
wengine kuwa Viongozi.”
“Naamini
nimetekeleza hili kwa kadri nilivyoweza. Zaidi ya yote kila iitwayo leo kwa
ushirikiano tulioujenga niliona kila mtumishi anatamani kuendelea kufanya kazi
Mahakama ya Kazi” Mhe. Dkt. Mlyambina alisema.
Halikadhalika,
aliwapitisha washiriki wa hafla hiyo kwenye nukuu nyingine ya Mwandishi Simon
Sinek katika utangulizi wa kitabu chake cha Find your why anaposema:
“Fulfilment
is a right and not a privilege. Every single one of us is entitled to feel
fulfilled by the work we do, to wake up feeling inspired to go to work, to feel
safe when we’re there and to return home with a sense that we contributed to
something larger than ourselves. Fulfilment is not a lottery. It is not a
feeling reserved for lucky few who get to say, ‘‘I love what I do’’
Kwa
Kiswahili kisicho rasmi anasema, “Kuridhika ni haki, si upendeleo. Kila mmoja
wetu ana haki ya kupata utoshevu kutokana na kazi anayoifanya; kuamka kila siku
akiwa na hamasa ya kwenda kazini; kujisikia salama akiwa mahali pa kazi; na
kurejea nyumbani akiwa na hisia kwamba ametoa mchango katika jambo kubwa zaidi
kuliko maslahi yake binafsi. kuridhika si bahati nasibu inayowakuta wachache,
bali ni haki inayomstahili kila mfanyakazi.”
Jaji
Mlyambina ana imani kuwa Mahakama ya Kazi itaendelea kuwa nguzo muhimu katika
kulinda haki za wafanyakazi na waajiri, kuimarisha mazingira bora ya kazi na
kuchangia maendeleo ya uchumi wa Taifa kupitia utoaji wa haki wenye ufanisi na
unaoaminika.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, akizungumza kwenye hafla ya kumuaga iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirika la Hifadhi ya Jamii PSSSF Mwenge jijini Dar es Salaam.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, akizungumza kwenye hafla hiyo.











