Jumanne, 10 Machi 2026

MAJAJI NA MAHAKIMU WANAWAKE WAUNGANA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA

     Wajadili nafasi ya wanamke katika kuimarisha utoaji haki na kuifikia jamii

Na HALIMA MENETE, Mahakama-Dodoma

Kongamano maalumu la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake limefanyika leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New Generation jijini Dodoma, likiwakutanisha Viongozi wa Serikali, Mahakama ya Tanzania pamoja na wadau wa maendeleo kujadili nafasi ya Majaji na Mahakimu wanawake katika kupambana na ukatili wa kijinsia.

Kongamano hilo lililobeba Kauli mbiu, “Kutoka Mahakamani Kuifikia Jamii: Majaji na Mahakimu Wanawake Mstari wa Mbele Kuongoza Mapambano Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia” lilihudhuriwa na mgeni rasmi Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Majaji na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania bara na visiwani pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo UN Women, RITA, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka.

Katika kongamano hilo pia, kulikuwa na nafasi ya utoaji mada mbalimbali, ambapo moja wa mada ilihusu “Nafasi ya Mwanamke kama Kiongozi katika Kuleta Mabadiliko kwenye Jamii kupitia Utoaji wa Haki unaozingatia Masuala ya Kijinsia.”

Mada hiyo iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Joseph Kerefu huku ikiendeshwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Magimbi, na ilijadiliwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Moshi Mhe. Dkt Lilian Mongela, Naibu Msajiri Mhe. Upendo Ngitiri na Hakimu Mkazi, Mhe. Juliana Mvungi.

Akifafanua kwa kina mada hiyo, Mhe. Kerefu amesema kuwa, katika juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia katika utoaji wa haki, tayari kuna misingi na nyenzo mbalimbali zilizowekwa kimataifa na kitaifa ambazo zinaweza kusaidia katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Amesema miongoni mwa nyenzo hizo ni pamoja na maandiko ya kitaaluma kama kitabu kilichoandikwa na Kosana Beker kinachojadili Gender and Diversity in the Judiciary, ambacho kinaeleza kwa kina umuhimu wa kuzingatia masuala ya kijinsia na utofauti katika mfumo wa utoaji haki.

Kwa mujibu wa Jaji Kerefu, uwepo wa vitendea kazi hivyo unaonesha wazi kuwa, kuna uwanja mpana wa kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa ipasavyo na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.

Hata hivyo, ameeleza kuwa, pamoja na uwepo wa misingi hiyo imara ya kisheria na kitaaluma bado kuna changamoto zinazotokana na baadhi ya mila, desturi na tamaduni katika jamii ambazo wakati mwingine zimekuwa zikikwamisha juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia.

Amesema baadhi ya mila na desturi hizo zimejikita katika mfumo dume, hali ambayo wakati mwingine imekuwa ikiweka vikwazo kwa watoa haki katika kuhakikisha misingi ya usawa wa kijinsia kama ilivyoainishwa katika mikataba ya kimataifa, Katiba ya nchi na sheria mbalimbali zinazozingatia masuala ya kijinsia zinatekelezwa kikamilifu.

Aidha, amesema licha ya maendeleo yaliyopatikana katika kuimarisha haki za wanawake, bado kuna changamoto mbalimbali zinazoendelea kujitokeza katika jamii ikiwemo ongezeko la mashauri ya ubakaji, unyanyasaji wa kingono, ukatili wa majumbani pamoja na ndoa za utotoni.

Ameongeza kuwa, hata katika masuala ya umiliki wa mali na mirathi bado kuna changamoto zinazowakabili wanawake katika jamii, huku baadhi ya sheria zilizopo zikionekana kutokidhi kikamilifu matakwa ya usawa wa kijinsia.

Ametolea mfano wa ‘Customary Law Declaration Order’ ya mwaka 1963 pamoja na baadhi ya vipengele vya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ambavyo bado vinaibua mjadala kutokana na kuwepo kwa vipengele vinavyohusishwa na ruhusa ya ndoa za utotoni.

Kwa upande mwingine, washiriki wa mada hiyo walieleza kuwa, changamoto hizo zinapaswa kuwa chachu kwa wadau wa sekta ya sheria, hususan majaji na Mahakimu wanawake, kuendelea kutumia elimu yao ya sheria pamoja na misingi iliyowekwa kuhakikisha vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.

Vilevile ilielezwa kuwa mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia yanahitaji ushirikiano mpana wa taasisi mbalimbali, ikiwemo Mahakama, Serikali, Wadau wa maendeleo pamoja na jamii kwa ujumla.

Akizungumzia uwakilishi wa wanawake katika Sekta ya Mahakama duniani, Mhe. Kerefu alieleza kuwa baadhi ya nchi zimepiga hatua kubwa katika kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi za kimahakama, akitolea mfano wa Italia ambapo wanawake wanawakilisha zaidi ya asilimia 52.9 ya Majaji.

Hata hivyo, alisema bado kuna nchi ambazo uwakilishi wa wanawake katika Mahakama uko chini, akitolea mfano wa Iraq yenye takribani asilimia 7.6 na Nepal yenye asilimia 3.8.

Kwa upande wa Tanzania, washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa, kumekuwa na mafanikio makubwa katika kuongeza uwakilishi wa wanawake katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

Imeelezwa kuwa Mahakama ya Rufani tangu ilipoanzishwa mwaka 1979 ilianza na Majaji watano wote wakiwa wanaume, lakini kwa sasa idadi hiyo imeongezeka na kufikia Majaji 37, ambapo wanaume ni 25 na wanawake ni 12, idadi inayozidi asilimia 30 ya uwakilishi wa wanawake.

Aidha, katika Mahakama Kuu kuna jumla ya Majaji 104 ambapo wanaume ni 65 na wanawake 39, wakati Mahakama za Hakimu Mkazi zina jumla ya Mahakimu 1,434 ambapo wanaume ni 746 na wanawake 688 sawa na takribani asilimia 48.

Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo, kuna Mahakimu 189 ambapo wanaume ni 111 na wanawake 78 sawa na asilimia 41.

Kwa upande wa Zanzibar, Mahakama Kuu ina jumla ya majaji 14 ambapo wanaume ni tisa na wanawake watano sawa na asilimia 35, huku katika ngazi ya mahakimu kukiwa na jumla ya Mahakimu 66 ambapo wanawake ni 23 na wanaume 43.

Washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa takwimu hizo zinaonesha wazi juhudi za Serikali katika kuhakikisha wanawake wanapata nafasi katika ngazi mbalimbali za uongozi ndani ya Mhimili wa Mahakama.

Hata hivyo, walisisitiza kuwa pamoja na ongezeko hilo la uwakilishi wa wanawake, bado kuna umuhimu wa kuhakikisha kuwa nafasi hizo zinatumika ipasavyo kuimarisha utoaji wa haki na kuchangia kikamilifu katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.


Baadhi ya washiriki wa Kongamano maalum la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake ambalo limefanyika  leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New Generation jijini Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

SUALA YA KUTOKOMEZA VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA LISHUGHULIKIWE KWA KUSHIRIKIANA; DKT. HOMERA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (MB) amesema kuwa, Ukatili wa Kijinsia (GBV) si tu ukiukaji wa kisheria bali ni jeraha la kijamii linalokua kwa ukimya, hofu, pamoja na mila na desturi hatarishi kama vile ukeketaji hivyo ni jukumu la Majaji, Mahakimu wanawake na kila mmoja katika jamii kutokomeza vitendo hivyo na kuhakikisha haki inapatikana.

Akizungumza leo tarehe 10 Machi, 2026 wakati akifungua Kongamano Maalum la Kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake katika ukumbi wa ‘New Generation’ jijini Dodoma, Mhe. Dkt. Homera amesema kuwa Majaji na Mahakimu Wanawake si tu watekelezaji wa sheria, bali pia ni walinzi wa amani ya jamii na watetezi wa haki za binadamu.

Waziri huyo amesema, wakati waathirika wanapofika Mahakamani, wanabeba maumivu, aibu na mara nyingine kutokuwa na imani na wale wanaowazunguka, hivyo ameeleza, ninyi kama Majaji wanawake, uwepo wenu katika tasnia ya utoaji haki unatoa unatia faraja na kuleta tumaini la upatikanaji wa haki wanawake wengine walio tendewa vibaya.

Kwa upande wa Tanzania, Kaulimbiu ya maadhimisho hayo inasema, “Kutoka katika kuta za Mahakama hadi katika Jamii: Majaji Wanawake Wakiongoza Mapambano Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia,” Mhe. Dkt. Homera amesema kauli mbiu hiyo inaendana na kaulimbiu ya kimataifa inayosema: “Majaji Wanawake Ndani na Nje ya Mahakama: Wakilinda Upatikanaji wa Haki,”  

Waziri huyo amekipongeza Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kwa kuipa uzito Siku ya Kimataifa ya Majaji Wanawake tangu mwaka 2023 baada ya Azimio la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lililopitishwa tarehe 26 Aprili 2021 huko Doha nchini Qatar.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Homera ameupongeza uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa hatua kubwa ya mafanikio iliyopiga katika uboreshaji wa huduma za utoaji haki nchini.

‘Hapa napenda kutoa pongezi kwa Mahakama ya Tanzania chini ya uongozi wa Mheshimiwa George M. Masaju, Jaji Mkuu wa Tanzania, kwa mabadiliko makubwa yaliyoimarisha upatikanaji wa haki,’ amesema Waziri huyo.

Ameongeza kuwa, katika muda wangu mfupi tangu aanze majukumu yake Wizara Katiba na Sheria amevutiwa na maendeleo ya Mahakama katika suala zima la matumizi ya teknolojia katika utoaji wa haki ambapo amesema Mahakama imejizatiti kwa ajenda ya kisasa na mpango wa usikilizaji mashauri kwa njia ya Mahakama mtandao, ikitoka katika matumizi ya karatasi na kuelekea mfumo wa kidijitali.

Ametaja miongoni mwa mabadiliko yenye athari chanya kuwa ni pamoja na Mfumo wa kielektroniki wa kusajili na kuendesha Mashauri (JoT-eCMS) ambao umesaidia kuondoa ucheleweshaji wa usikilizwaji wa mashauri, kuongeza uwazi na kuimarisha usimamizi wa mashauri ya familia na ukatili wa kijinsia.

Waziri huyo amesema mabadiliko mengine ni uwepo wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJCs), ambapo ameeleza hadi sasa kuna vituo jumuishi zaidi ya tisa nchi nzima vilivyokwisha jengwa na vinavyoendelea kujengwa.

Ameongeza kwamba, Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia  kilichopo Temeke mkoani Dar es Salaam kimetoa mafanikio makubwa ikiwa ni ushahidi wa maono ya Serikali kwa kushirikiana na Mahakama. Kwa mwaka 2025, Mahakama hiyo ilishughulikia mashauri zaidi ya 9,200, yakiwemo ya ukatili wa kijinsia na familia, lakini pia iliwezesha asilimia 61 ya wanawake kupata msaada wa kisheria jambo linaloonyesha wazi kuwa, zinapounganishwa huduma za Mahakama, Polisi, na Ustawi wa Jamii katika eneo moja, vizuizi vya upatikanaji wa haki kwa wanawake vinaanza kupungua.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Homera ameongeza mafanikio mengine ya Mahakam ani pamoja na kuwepo kwa Uwajibikaji Unaotegemea Takwimu kupitia mfumo wa kanzi data (Data Hub), Mahakama inaonesha jinsi inavyoshughulikia mashauri nyeti ya ukatili wa kijinsia (GBV) kwa wakati halisi na kuhakikisha mashauri hayo muhimu yanatatuliwa haraka.

Hata hivyo, Waziri huyo ametoa rai kwa Mahakama kuwa, panapo mafanikio hapakosi changamoto hivyo ni lazima iwe makini na changamoto zilizopo.

“Mnapaswa kushughulikia ubaguzi wa kidijitali, mnatakiwa kuipeleka haki hii hasa ya matumizi ya teknolojia katika hatua nyingine kwa kuhakikisha huduma hii si kwa watu wa mijini tu bali pamoja na watu walio pembezoni, vilevile ni muhimu kuhifadhi kumbukumbu nyeti za Mahakama kwa viwango vya juu vya ulinzi wa kanzi data ili kuepuka kuvujisha siri za waathirika,” ameeleza.

Ameihakikishia Mahakama kuwa, Wizara itaendelea kushirikiana kwa karibu na Mhimili huo kuhakikisha mifumo ya kisheria inaendana na ulinzi wa athari za teknolojia.

Kadhalika, Waziri huyo ameipongeza TAWJA na kuahidi kuendelea kuipa ushirikiano, kwa kuwa sehemu ya mabadiliko haya ya kidijitali kuwa ni mabadiliko yenye tija katika kutoa haki ya kijinsia.

“Mmepeleka sheria kutoka kwenye viunga vya Mahakama hadi kwenye jamii kwa kufanya yafuatayo, kuchangia katika uundaji na marekebisho ya sheria zinazolinda wanawake na watoto dhidi ya Ukatili wa Kijinsia (GBV), kuhakikisha sheria zetu ni za haki, jumuishi, na zinawalinda walioko hatarini,” amesema.

Jitihada nyingine zilizofanywa na Chama hicho ni pamoja na kupinga ubaguzi katika mali za ndoa na faragha kupitia sayansi ya sheria yenye msingi wa jinsia; kuwajengea uwezo wasichana na kuonesha kwamba uongozi katika tanuru la haki kupitia Mahakama unawezekana na kuandaa shughuli za jamii ili kuhakikisha Mahakama mtandao inafika hadi maeneo ya pembezoni ambayo ni maeneo ya vijijini.

Akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa Kongamano hilo, Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel amesema hii ni mara ya tatu tangu Chama hicho kianze kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.


Aidha, Mhe. Sehel ameshukuru kwa ushirikiano ambao wanapata kutoka Serikalini. Na vilevile alichukua fursa hiyo kumueleza Mhe. Dkt. Homera kuhusu Chama hicho na namna kinavyofanya kazi kwa kuwa ni mara yake ya kwanza kushiriki katika shughuli ya TAWJA.


"TAWJA ni Taasisi ya Kitaaluma isiyo ya Kiserikali na wala hatujihusishi na masuala ya siasa, yenyewe inawaleta pamoja Mahakimu na Majaji Wanawake kwa pande zote mbili Tanzania Bara na Visiwani Zanzibar na wanachama wake wanatoka katika ngazi zote za Mahakama kuanzia Mahakama za Mwanzo mpaka Mahakama ya Rufani na lengo kuu la Chama chetu  ni kukuza utawala wa sheria, kulinda haki za binadamu, kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa makundi yote...," amesema Mwenyekiti huyo.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewapongeza Wanachama cha TAWJA na kusema kuwa anajivunia wanachama hao kwa kuwa ni watu makini.


"Pamoja na Ujaji na Uhakimu wenu, ninyi ni akina Mama, kila mwanadamu amezaliwa na mwanamke, mnafanya kazi kubwa sana," amesema Prof. Ole Gabriel.

Ameongeza kuwa, asilimia 80 ya tabia za watu zinatokana na wazazi, na kati ya asilimia hizo, Mama ana asilimia 64 ya kutengeneza tabia ya mtoto, hivyo mwanamke ni mtu muhimu katika ustawi wa jamii.

Kongamano hilo limehudhuriwa na Washiriki mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wanachama wa TAWJA kutoka matawi mbalimbali, Wjumbe Waalikwa wa TAWJA, Washirika wa Maendeleo na Wawakilishi wa Jamii ya Kiraia.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (MB) akitoa hotuba wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu wanawake (TAWJA) leo tarehe 10 Machi, 2026 katika ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) akitoa hotuba wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe.Barke Sehel akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake  leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa salamu za Mahakama ya Tanzania wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake kwa upande wa TAWJA leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu waliohudhuria sherehe ya Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA). Wa pili kulia ni Mhe. Joachim Tiganga, wa pili kushoto ni Mhe.Wilbert Martin Chuma na wa kwanza kushoto ni Mhe.Dkt Yose Joseph Mlyambina wakifuatilia mdahalo kwenye kongamano hilo.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa salamu za Mahakama ya Tanzania wakati wa ufunguzi wa kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 katika ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.


Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake leo tarehe 10 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa New Generation hall uliopo Kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakiwa wanafuatilia matukio mbalimbali ya ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea siku ya kimataifa ya Majaji na Mahakimu wanawake (TAWJA) leo tarehe 10 Machi, 2026 katika ukumbi wa New Generation hall uliopo kisasa jijini Dodoma.

Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu waliohudhuria sherehe ya Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa ufunguzi wa kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake. katikati ni Mhe. Joachim Tiganga, wa pili kushoto ni Mhe.Wilbert Martin Chuma na kushoto ni Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina wakifuatilia mdahalo kwenye kongamano hilo.


Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (wa pili kulia) akipokea zawadi kutoka kwa Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe.Barke Sehel (wa pili kushoto) wakati wa hafla hiyo. 

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na sheria Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa TAWJA ambao ni Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania waliohudhuria kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wanachama wa TAWJA ambao ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.
Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji Wafawidhi ambao ni walezi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) waliohudhuria kongamano maalumu la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera (Mb) (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa TAWJA waliohudhuria kongamano maalum la kusherehekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake.

(Picha na INNOCENT KANSHA - Mahakama)

 
















WATUMISHI WANAWAKE KIGOMA WASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

  • Wanawake mkoani humo waaswa kuchangamkia fursa zilizopo kuboresha uchumi wa familia na taifa letu

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo aliwaongoza wanawake wa Mahakama Kanda ya Kigoma kujumuika na wanawake wenzao waliojitokeza wilayani Kakonko kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo kimkoa ilifanyika katika Wilaya hiyo. 

Mgeni Rasmi katika sherehe hizo zilizofanyika tarehe 08 Machi, 2026 alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mhe. Dinah Mathamani aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro.

Akizungumza na wanawake waliofika katika viwanja hivyo, Mhe. Mathamani, alisema kuwa, kupitia Kauli mbiu yam waka huu ya Siku ya Wanawake Duniani isemayo, "Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050," Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira rafiki yanayowawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo, uchumi na uongozi kupitia sera, programu na fursa mbalimbali za uwezeshaji.

Amewahimiza wanawake kwamba, wanao wajibu mkubwa wa kusimamia maadili ya familia na kulea kizazi kijacho na kwamba Serikali inaendelea kufungua fursa za kiuchumi na kuboresha miundombinu muhimu ya Afya, Elimu, Kilimo, Biashara na Uchukuzi katika kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Alieleza kuwa, uboreshaji wa huduma ya afya kutoka Hospitali za Wilaya na Halmashauri tatu, na kufikia tarehe 08 Machi zilikuwa nane sawa na asilimia 166.6, na Vituo vya Afya kutoka 34 mpaka kufikia 53 sawa asilimia 55.8, na kwa upande Shule za Sekondari awali zilikuwa 194 na sasa zipo 256 sawa na asilimia 31.9, ambapo shule za msingi awali zilikuwa 664 na sasa zimejengwa na kufikia 742 sawa asilimia 11.7.

“Hatua zote hizo zimeenda sambamba na ujenzi wa madarasa ya Shule za Sekondari kutoka 1,900 mpaka 3288 sawa na asilimia 70 na kwa Shule za Msingi vyumba vilikuwa 5401 na sasa tunaongea vyumba 6057 sawa na asilimia 12.1,” alisema Mkuu wa Wilaya huyo.

Aidha, aliongeza kwamba, kupitia Sera ya Taifa ya haki kwa wanawake na watoto wa kike inasisitiza umuhimu wa kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kama njia ya kukuza usawa wa kijinsia na haki za wanawake hivyo maadhimisho hayo yanalenga kuongeza uelewa kuhusu changamoto zinazowakuta wanawake na wasichana kama vile unyanyasaji wa maneno, ukatili wa kijinsia, na ukosefu wa usawa wa kiuchumi.

Kadhalika maadhimisho hayo yanatambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii na kukuza ushirikiano kati ya wanawake na wanaume katika kufikia usawa wa kijinsia na Wanawake wametakiwa kusimama imara katika kutetea haki na usawa wao na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukuza haki za wanawake na wasichana.

Naye, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Bi. Zainabu Buyogela alisema kuwa, wanawake wanatakiwa kuchangamka na asiwepo hata mmoja anayekosa shughuli inayompatia kipato ili watoe mchango wao katika uongozi na ujasiriamali unaojitokeza katika maeneo yao, na kuwaonya wasichana wasiache kazi kwa ajili ya kulinda ndoa au mahusiano.

Bi. Zainabu alitumia fursa hiyo kumshukuru mwanamke nambari moja Tanzania ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuongoza nchi kwa haki na usawa wa kijinsia.

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Hassan Abbas Rugwa, alisema kuwa, Mkoa huo unaendelea kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo inayolenga kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuhakikisha wanapata fursa sawa katika uongozi, uamuzi na kushiriki shughuli za maendeleo.

Hata hivyo, Bw. Rugwa aliwahimiza wanawake kuwa wabunifu, kujiamini na kutumia maarifa waliyonayo ili kunufaika na fursa za mikopo, mafunzo ya ujasiriamali pamoja na nafasi za uongozi zinazopatikana katika jamii wanazotoka ili nao kuwa sehemu ya mafanikio katika nafasi hizo.

Aidha, aliwapongeza wanawake na kuishukuru Serikali kuendelea kuweka sera na mikakati mbalimbali inayolenga kuwainua wanawake kiuchumi, kijamii na kisiasa hatua inayochangia kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya Taifa.


Watumishi Wanawake  wa Mahakama Kanda ya Kigoma wakiwa katika picha ya pamoja tayari kwa ajili ya kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika tarehe 08 Machi, 2026 katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda Wilayani Kakonko.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Valerian Tarimo (aliyevaa sare ya kitenge) akiwa pamoja na Viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Kigoma katika sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanamke Duniani iliyofanyika Wilaya ya Kakonko katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda.

Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mhe. Dinah Mathamani akitoa hotuba yake wakati wa Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani zilizofanyika tarehe 08 Machi, 2026 katika viwanja vya ofisi ya kata ya Kasanda.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Abbas Rungwe akitoa neno katika  hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda Wilaya ya Kakonko.

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania Mkoani Kigoma (UWT), Bi. Zainabu Buyogela akitoa neno wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda  Wilaya ya Kakonko.

Wanafunzi wa Kidato cha Tano wa Shule ya Sekondari Mtendeli iliyopo Kata ya Kasanda wakitumbuiza mbele ya Mgeni Rasmi Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mhe. Dinah Mathamani (hayupo katika picha) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Kasanda Wilaya ya Kakonko.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

Jumatatu, 9 Machi 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA, ZANZIBAR WAANZA MAFUNZO YA KUBADILISHANA UZOEFU DODOMA

  • Washiriki watakiwa kuimarisha maadili, matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa mashauri

Na HALIMA MNETE & JAMES BUSANYA-Mahakama, Dodoma.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, leo tarehe 9 Machi 2026 amefungua mafunzo ya kubadilishana uzoefu kati ya Maofisa wa Mahakama ya Tanzania na wenzao kutoka Mahkama ya Zanzibar, yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo mbele ya washiriki kutoka Zanzibar wakiongozwa na Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim, Mhe. Tengwa alisema mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kimfumo kati ya Taasisi hizo mbili katika kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.

Alisema Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Zanzibar zimeona umuhimu wa kuendelea kubadilishana uzoefu ili kuimarisha weledi, uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa Mahakama, hali itakayosaidia kuongeza imani ya wananchi kwa Mhimili wa utoaji haki.

“Nawapongeza washiriki wote kutoka Zanzibar kwa kufika Dodoma salama. Mafunzo haya ni fursa muhimu ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uwezo wetu katika utoaji wa huduma bora za Mahakama,” alisema Mhe. Tengwa.

Aliongeza kuwa uchaguzi wa Dodoma kama eneo la kufanyia mafunzo hayo umezingatia mazingira yake tulivu yanayofaa kwa kujifunza na kujadiliana masuala muhimu yanayolenga kuboresha utendaji wa Mahakama.

Katika hotuba yake, alieleza kuwa mafunzo hayo yatajadili mada mbalimbali muhimu ikiwemo ukaguzi wa shughuli za Mahakama, utekelezaji wa majukumu ya msingi, maboresho ya huduma za Mahakama, maadili na namna ya kushughulikia malalamiko ya kimaadili, usimamizi wa mashauri, matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano katika usimamizi wa mashauri pamoja na kuharakisha umalizaji wa mashauri.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usawa wa kijinsia katika utoaji wa huduma za Mahakama, akieleza kuwa Mahakama inapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha haki na usawa vinazingatiwa kwa vitendo katika jamii.

Mhe. Tengwa alinukuu kauli ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin William Mkapa, aliyewahi kusema kuwa mtu hawezi kujua kama mama yake ni mpishi mzuri hadi pale atakapoonja chakula kilichopikwa na mama mwingine, akieleza kuwa mfano huo unaonesha umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wengine.

Alisema kuwa kupitia mafunzo hayo washiriki wanatarajiwa kuwa mabalozi wa kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa wakati, kuboresha huduma za Mahakama kupitia ukaguzi pamoja na kuimarisha maadili na usawa wa kijinsia katika utendaji wao.

Mafunzo hayo ya siku tano yatahitimishwa tarehe 13 Machi, 2026, yakilenga kuongeza ufanisi katika usimamizi na utoaji wa haki kwa wananchi.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, akizungumza wakatia anafungua mafunzo hayo. Picha chini ni washiriki wa mafunzo yanayofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

WATUMISHI SUMBAWANGA WAPATIWA MAFUNZO KUHUSU MAFAO & KUSTAAFU

Na. Sharifu Mokiwa - Mahakama, Sumbawanga

Watumishi  wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wamepata mafunzo maalumu kuhusu mafao na maandalizi ya kuustaafu ambayo yalitolewa kwa njia mbili yaani uso kwa uso kwa waliokuwepo ukumbini na kwa njia ya Mtandao kwa waliokuwa  mbali.

Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 6 Machi 2026, katika ukumbi wa Mahakama Kuu  Sumbawanga na yalifunguliwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu  Sumbawanga  Bw. Machumu Essaba, kabla ya kuanza kuwasilishwa kwa mada na Afisa  kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi (PSSF) Bw. Eribariki Nsulau

Akizungumza wakati wa kuwasilisha mada Bw. Nsulau alitoa elimu kuhusu huduma na mafao yanayo tolewa na PSS, alifafanua jinsi ya kujisajili kwenye portal ya PSSF kuangalia michango, kuandikisha michango mipya, nakupata mafao mbalimbali, mafao hayo ni pamoja na fao la mishahara miwili endapo mfanyakazi atapoteza ajira ,fao la uzazi ndani ya siku 90 na malipo ya pensheni kuanzia tarehe 21- 23 au 21-25 ya mwezi, yanayolipwa pia kwa wategemezi wa mstaafu. Mafunzo hayo pia yalisisitiza umuhimu wa uhakiki wa kila mwaka kwa wastaafu na wategemezi ili malipo ya pensheni yaendelee bila usumbufu.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu Sumbawanga, Mhe. Abubakari Mrisha alitoa mwongozo wa kitaalamu kuhusu maandalizi ya kustaafu na alisisitiza kuwa maandalizi ya kustaafu yanapaswa kuanza mapema mara tu mtumishi anapopata cheki namba, kwani namba hiyo inaonesha muda unaotarajiwa wa kustaafu.

Alieleza kuwa ni muhimu kwa watumishi kupanga maisha yao ya baadae  mapema ili kuepuka changamoto pindi wanapo staafu.

Aidha, watumishi walipata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusu mafao, pensheni, mirathi, na namna ya kujiandaa kustaafu ambapo, mafunzo hayo yamewasaidia kuongeza uelewa na uwajibikaji wa watumishi katika kupanga mustakabali wao wa kifedha, huku wakiongezwa ujuzi muhimu kuhusu hifadhi ya jamii na usimamizi wa michango.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda, Sumbawanga Bw. Machumu Essaba akifungua rasmi mafunzo kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu kwa watumishi wa Mahakama tarehe 6 Machi, 2026.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda, Sumbawanga Mhe. Abubakari Mrisha (aliyenyanyua mkono) akisisitiza umuhimu wa maandalizi mapema ya kustaafu kwa watumishi wa Mahakama Sumbawanga.

Hakimu Mkazi Mhe. Willington Rwabinyasi akiuliza swali kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu wakati wa mafunzo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Sumbawanga wakisikiliza mafunzo kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu.

Afisa kutoka PSSF Bw. Elibariki Nsulau akipokea maswali kwa kuyaandika kutoka kwa watumishi wa Mahakama ya Sumbawanga kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu

Afisa kutoka PSSSF Bw. Elibariki Nsulau (aliyesimama) akieleza jinsi ya kujisajili, kuangalia michango nakufahamu mafao kupitia portal ya PSSF.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




MAHAKAMA KUU KANDA YA MOROGORO YAWAFARIJI WANAWAKE WA GEREZA LA KINGOLWIRA

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, imeungana na wanawake wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kwa kufanya ziara ya kijamii katika Gereza Kuu la Wanawake Kingolwira.

Maadhimisho hayo  ambayo hufanyika tarehe 8 Machi kila mwaka yalianza kwa watumishi wa Mahakama Kuu kushiriki pamoja na wanawake wengine katika siku hiyo muhimu inayolenga kutambua mchango wa wanawake katika jamii.

Maadhimisho hayo yalibeba na kauli mbiu inayosema, “Haki kwa wanawake na wasichana msingi wa maendeleo jumuishi kufikia dirĂ¡ 2050.”

Baada ya kushiriki katika maadhimisho hayo, watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro walifanya ziara maalum ya kutembelea Gereza la Wanawake Kingolwira lililopo mkoani Morogoro.

Ziara hiyo iliongozwa na Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage, ikiwa na lengo la kuwafariji wanawake waliopo gerezani hapo pamoja na kutoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia katika maisha yao ya kila siku wakiwa gerezani.

Watumishi hao walipata fursa ya kujumuika na wanawake waliopo gerezani hapo, kushirikiana nao katika mazungumzo ya faraja pamoja na kuonesha upendo na mshikamano kama sehemu ya kuadhimisha siku hiyo ya wanawake duniani.

Ziara hiyo pia ilikuwa na lengo la kuwapa moyo na matumaini wanawake hao kuwa bado wana nafasi ya kujifunza, kujirekebisha na kuendelea na maisha baada ya kumaliza vifungo vyao.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza ambaye pia ni Mkuu wa Gereza la Wanawake Kingolwira, Afande Nimwindael Mzirai, aliwashukuru watumishi wa Mahakama kwa moyo wao wa kujali na kuwafikia wanawake waliopo gerezani.

Alisema kuwa ujio huo umeleta faraja kubwa kwa wafungwa hao na umeonesha mshikamano wa kijamii kwa wanawake wote bila kujali hali walizonazo.

Aidha, alitoa wito kwa watumishi wa umma pamoja na wananchi kwa ujumla kuendelea kuheshimu sheria za nchi na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kusababisha kuvunja sheria na hatimaye kujikuta wakitumikia vifungo gerezani.

Aliongeza kuwa gereza hilo pia ni sehemu ya kujifunza na kujenga upya maisha, ambapo wanawake waliopo hapo hupatiwa mafunzo mbalimbali ya stadi za maisha kama vile kilimo, ushonaji wa cherehani pamoja na shughuli nyingine za uzalishaji ili kuwa na ujuzi utakaowasaidia wanaporejea katika jamii.

 Akizungumza wakati wa kuhitimisha ziara hiyo, Mhe. Kinyage aliwahimiza wanawake waliopo gerezani kuwa na uvumilivu, nidhamu pamoja na matumaini katika kipindi chote cha kifungo chao. Aliwaasa kutumia muda wao wakiwa gerezani kujifunza mambo yatakayowasaidia kujenga maisha mapya pindi watakapomaliza vifungo vyao.

“Msijisikie wanyonge kwa kuwa hapa, kwani kila changamoto ina mwisho wake. Muhimu ni kujifunza, kuwa na nidhamu na kujiandaa kwa maisha bora baada ya kutoka hapa,” alisema Mhe.Kinyage

Maadhimisho hayo pamoja na ziara hiyo yameonesha mshikamano, upendo na kujali kwa watumishi wa Mahakama kwa wanawake wote katika jamii, ikiwemo wale waliopo katika mazingira ya kifungo, huku yakilenga kuhamasisha matumaini, marekebisho na mshikamano wa kijamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, akiwasalimia wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake yakiyofanyika kimkoa Morogoro.

Watumishi wanawake wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakifanya maandamano katika serehe hiyo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakiwa katika Gereza Kuu la Wanawake Kingolwira.

Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage akikabidhi baadhi ya vifaa kwa Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza ambaye pia ni Mkuu wa Gereza la Wanawake Kingolwira, Afande Nimwindael Mzirai.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.