Jumatatu, 29 Juni 2026

MENEJIMENTI MASJALA NDOGO MBEYA YAFANYA TATHMINI YA UTENDAJI KAZI ROBO YA NNE

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Menejimenti ya Mahakama Masjala Ndogo ya Mbeya hivi karibuni ilifanya kikao cha tathmini ya utendaji kazi kwa robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026, kwa lengo la kupitia utekelezaji wa majukumu ya kimahakama, kiutawala pamoja na kuweka mikakati ya kuendelea kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, na kuwakutanisha Majaji, viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya za Masjala Ndogo ya Mbeya pamoja na Maafisa mbalimbali kutoka katika Mahakama hizo.

Aidha, kila Mahakama iliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu yake kwa robo ya nne, zikijumuisha usimamizi wa rasilimali watu, matumizi ya fedha, manunuzi na ugavi, hali ya mashauri, upimaji wa utendaji kazi pamoja na utoaji wa motisha kwa watumishi.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Mtulya alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usawa katika kuwathamini watumishi ili kuongeza ari ya kazi na kuimarisha utendaji katika Mahakama zote za Masjala hiyo.

“Katika kuboresha utendaji kazi, nasisitiza kuwepo na usawa wa utoaji wa stahiki na motisha kwa watumishi wa mahakama zote katika Masjala nzima ya Mbeya, kuanzia Mahakama Kuu hadi Mahakama za Mwanzo,” alisema Mhe. Mtulya.

Taarifa zilizowasilishwa zilionesha mafanikio mbalimbali mathalani kusikiliza na umalizaji wa mashauri yaliyopangwa, matumizi bora ya fedha kwa kuzingatia vipaumbele vya ofisi, kupunguza msongamano wa wafungwa na Mahabusu magerezani kupitia usikilizaji wa mashauri na kuendelea kudumisha ushirikiano mzuri na wadau wa Mahakama,

Aidha, kikao hicho pia kilibaini changamoto mbalimbali zinazohitaji kufanyiwa kazi, miongoni mwa changamoto hizo ni uchakavu wa vyombo vya usafiri unaosababisha kuongezeka kwa gharama za matengenezo, uchakavu wa majengo hususan Mahakama za Mwanzo, ufinyu wa bajeti pamoja na upungufu wa watumishi.

Mwenyekiti alisisitiza umuhimu wa kuendeleza usimamizi madhubuti wa rasilimali zilizopo, kuimarisha uwajibikaji na kuendelea kushirikiana katika kutafuta suluhisho la changamoto zilizojitokeza ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za Mahakama na kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiongoza kikao hicho cha menejimenti, wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (kulia) na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti.

Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer akiwasilisha taarifa ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya.

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Odilia Mapunda (katikati) akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi kwa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo. 






KAMPENI YA KUPANDA MITI YASHIKA KASI MAHAKAMA ZA MWANZO KIGOMA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa hivi karibuni aliwaongoza watumishi wa Masjala hiyo na Mahakama ya Mwanzo Bangwe kupanda miti ya kivuli na matunda katika maeneo ya wazi yaliyopo katika Mahakama hiyo mpya iliyofunguliwa na kuanza kazi.

Upandaji miti huo ni Kampeni inayosimamiwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile, ambaye mara kadhaa katika ziara zake amekuwa akipanda miti katika Mahakama husika anapotembelea, hata hivyo amekuwa akisisitiza kuwa miti hutunza uoto wa asili, kutunza miundombinu ya majengo ya Mahakama pamoja na kulinda mipaka ya maeneo ya Mahakama hizo sambamba na kuvutia kwa mandhari nzuri iliyopambwa na miti hiyo.

Aidha, Mhe. Rwizile amenukuliwa mara kadha katika vikao vya watumishi akisema, “tumekuwa na maeneo ya Mahakama zetu ambayo yapo wazi sana, hivyo tusipoweka mikakati ya makusudi ya  kuyalinda maeneo hayo, basi tunaweza kuyapoteza kwa watu wengine kuyatumia, maana hatuna alama zinazolinda maeneo hayo, ni rai yangu Uongozi wa Mahakama za Wilaya zote, kuandaa utaratibu wa kupanda miti katika maeneo hayo kuanzia Mahakama za Mwanzo sambamba na viwanja vipya vya Mahakama za Kata na nyumba za Mahakimu, hasa ambavyo vimepatikana na upimaji umefanyika na kukabidhiwa viwanja hivyo.”

Vilevile, watumishi wametumia muda wa asubuhi kabla ya shughuli za Mahakama kuanza, ili kutekeleza jukumu hilo, ambapo wamepanda miti hiyo na kuahidi kuitunza hususan katika kipindi hiki cha kiangazi ambapo miti hiyo inahitaji maji ya kutosha ili kustawi vizuri.

Kampeni hiyo pia ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama ikiwa ni pamoja na maelekezo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050, inayotaka kuwa na Tanzania ya kijani, hivyo, Mahakama Kuu Kigoma imeendelea kuhakikisha maeneo yote ya Mahakama yanavutia kwa miti mizuri inayopandwa kwa mpangilio mzuri na wenye kuleta mvuto wa mazingira ya Mahakama zote Mkoani humo.

Zoezi hilo la kupanda miti lilihudhuriwa na Viongozi wa Mahakama Kigoma akiwemo Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bw. Yusuph Kasuka, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya mwanzo Bangwe, Mhe. Florence Ikorongo pamoja na Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Valerian Msola, Ofisa Utumishi Mwandamizi, Bw. Festo Sanga na Watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma na Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akipanda Mti wa Mpapai katika eneo la wazi lililoandaliwa kupandwa miti Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Mtendaji  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka akipanda mti wa kivuli katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Bangwe, Mhe. Florence Ikorongo akipanda Mti wa Kivuli katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya  Kigoma,  Mhe. Valerian Msola akipanda Mti wa Mpapai katika eneo la wazi liloandaliwa kupandwa miti Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Ofisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Festo Sanga akipanda Mti wa Kivuli katika eneo la wazi liloandaliwa kupandwa miti Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Kigoma walioshiriki kupanda miti hivi karibuni katika eneo la wazi liloandaliwa kupandwa miti katika Mahakama ya Mwanzo Bangwe.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

MASJALA NDOGO MBEYA YAKUTANA NA WADAU WA HAKI MADAI

 Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, hivi karibuni ilifanya kikao cha kusukuma mashauri ya madai (Bench-Bar Meeting) kwa lengo la kutathmini mwenendo wa mashauri ya madai na kuweka mikakati ya kuhakikisha mashauri hayo yanamalizika kwa wakati, kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya na kuhudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer pamoja na wadau wengine wa haki madai.

Katika kikao hicho, wajumbe walipokea taarifa kuhusu hali ya mashauri ya madai, ikiwemo mashauri yaliyomalizika, yaliyobaki, mashauri yaliyoitishwa kutoka mabaraza mbalimbali pamoja na mashauri ya mlundikano.

Aidha, wajumbe wa kikao hicho, walijadili mikakati ya kuhakikisha mashauri ya mlundikano na yale yanayokaribia kuwa ya mlundikano yanashughulikiwa na kukamilishwa kwa wakati ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa haki kwa wakati mapema ipasavyo.

Vilevile, miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa ni changamoto ya baadhi ya mawakili kutokuzingatia ratiba na taratibu zilizowekwa na Mahakama katika uendeshaji wa mashauri, hali inayochangia ucheleweshaji wa usikilizwaji wa baadhi ya mashauri.

Kwa upande wao, Mawakili wa Kujitegemea kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (Tanganyika Law Society - TLS) walipendekeza kuwa pale ambapo Jaji au Hakimu hatakuwa na uwezo wa kuendelea na usikilizaji wa shauri kwa siku iliyopangwa, taarifa itolewe mapema kwa mawakili ili kuwawezesha kupanga ratiba zao nyingine na kutumia muda wao kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Mtulya alihitimisha kwa kusisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama na wadau wote wa sekta ya sheria katika kuhakikisha mashauri ya madai yanasikilizwa na kuamuliwa kwa wakati, sambamba na kuendelea kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (kushoto) akiongoza kikao cha kusukuma Mashauri ya Madai, kulia nia Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo.

Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer (kushoto) akiwasilisha taarifa ya mashauri ya haki madai wakati wa kikao hicho.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Paul Rupia akiwasilisha Taarifa ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya katika kikao hicho.

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).








TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA YA TANZANIA-SIMIYU, BI. ANGELA MTESIGWA AFARIKI DUNIA

Marehemu Angela Angelus Mtesigwa enzi za uhai wake.

TANZIA

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake, Bi. Angela Angelus Mtesigwa aliyekuwa akihudumu Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu kama Mwandishi Mwendesha Ofisi.

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Simiyu, Bw. Gasto Kanyairita marehemu Angela alifikwa na umauti Alfajiri ya tarehe 26 Juni, 2026 katika Hospitali ya Bugando mkoani Mwanza alipokuwa akipatiwa matibabu. 

Bw. Kanyairita amesema, mazishi yanatarajiwa kufanyika leo tarehe 29 Juni, 2026 Wilaya ya Kisarawe Mkoani Pwani.

Mahakama ya Tanzania inaungana na Ndugu, Jamaa na Marafiki kuomboleza msiba huo mzito wa kuondokewa na Mpendwa wetu.

BWANA ALITOA, BWANA AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE.

JAJI MFAWIDHI MTWARA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI WA MAHAKAMA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, hivi karibuni amefanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Mkoa wa Mtwara ili kujionea utendaji kazi ili kuhakikisha huduma ya utoaji haki inaendelea kufanya vyema.

Miongoni mwa Mahakama zilizokaguliwa ni Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya Tandahimba, Newala, Nanyumbu, Masasi na Mahakama za Mwanzo Litehu, Mnyambe, Nakopi, Chiungutwa.

Ziara hiyo pia ilijumuisha mazungumzo ya pamoja na Watumishi wa Mahakama alizopita kwa ajili ya ukaguzi. Aliweza kupata taarifa za utendaji kazi, mafanikio, changamoto, mapato na matumizi.

Mhe. Mteule aliwapongeza Mahakimu na Watumishi wa Mahakama kwa utendaji bora na mzuri, hasa kumaliza mashauri kwa wakati, kutokuwa na mlundikano.

Katika ukaguzi huo pia, Jaji Mfawidhi aliwapongeza Watumishi wa Mahakama katika matumizi wa mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo inawezesha kufuatilia na kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao. Aliwasisitiza kuendelea kuwaelewesha Wananchi kwenye matumizi ya mifumo hiyo ili kupunguza gharama za kila mara.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga na Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi, Mhe. Stella Shindika.

Jaji Mfawidhi pia alitembelea na kukagua Mahakama ya Wilaya Masasi iliyopo katika ujenzi na kusisitiza ufanyike kwa kuzingatia ubora na kwenda kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule akisalimiana na Mahakimu na Watumishi katika Mahakama ya Wilaya Newala.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, akipanda mti wa ukumbusho katika Mahakama ya Wilaya Newala.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule akiwa katika ukaguzi wa eneo la Mahakama ya Mwanzo Mnyambe iliyopo Wilaya ya Newala.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule akisalimiana na Mahakimu, Watumishi na Wadau baada ya kuwasili katika Mahakama ya Wilaya Nanyumbu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (kushoto mbele) akiwa kwenye ukaguzi wa eneo la Mahakama ya Mwanzo Litehu.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (kulia) akiwa kwenye ukaguzi wa jengo jipya la Mahakama ya Wilaya Masasi lililopo kwenye ujenzi unaondelea.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwasikiliza Watumishi katika kikao kilichifanyika Mahakama ya Wilaya Tandahimba.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akipata picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Chiungutwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Litehu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Nakopi.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Newala.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tandahimba.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Masasi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.


Jumapili, 28 Juni 2026

JAJI MFAWIDHI BUKOBA AFANYA ZIARA MAHAKAMA YA WILAYA KYERWA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Bukoba

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. David Ngunyale, hivi karibuni alifanya ziara katika Mahakama ya Wilaya Kyerwa kwa lengo la kujitambulisha.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Ngunyale aliwataka Watumishi wa Mahakama hiyo kuendelea kukumbatia maendeleo yaliyopatikana katika utoaji haki na kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi ili kuweza kuwafikia wananchi wengi zaidi kutoa huduma iliyo bora.

Jaji Ngunyale amekumbushia umuhimu kujiendeleza kielimu ili kuongeza ufanisi katika majukumu ya utoaji haki. Amesisitiza utoaji haki uendane na ubora unaohitajika kuweza kufikia malengo ya Mahakama.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. David Ngunyale (katikati) akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kyerwa. Kulia kwakwe ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Bukoba, Mhe. Saidi Mkasiwa na kushoto kwakwe ni Kaimu Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Kyerwa, Mhe. Allen Ifunya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. David Ngunyale na Naibu Msajili Mahakama Kuu Bukoba, Mhe. Saidi Mkasiwa wakifatilia taarifa ya utekelezaji wa majukumu iliyokuwa inasomwa na Kaimu Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Kyerwa, Mhe. Allen Ifunya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. David Ngunyale (katikati aliyekaa) akiwa katika picha ya pamoja na Watumsihi wa Mahakama ya Wilaya Kyerwa. Wengine waliokaa kuanzia kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Bukona, Mhe. Saidi Mkasiwa na Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilya Kwerw, Mhe. Allen Ifunya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. David Ngunyale akionyeshwa maeneo mbalimbali ya Mahakama ya Wilaya Kyerwa.

 

 

 

ZIARA YA UKAGUZI WA GEREZA KUU LILUNGU MTWARA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, hivi karibuni amefanya ziara ya ukaguzi na kutembelea Gereza Kuu la Lilungu katika Mkoa wa Mtwara, ili kujionea utendaji kazi wa Gereza hilo.

Ziara hiyo ilijumuisha pia mazungumzo ya pamoja na Askari Magereza na kufanya ukaguzi wa mazingira na kupata taarifa za utendaji kazi, mafanikio na changamoto.

Aidha, Jaji Mfawidhi pia alizungumza na kusikiliza changamoto za Wafungwa, mawazo na maoni kutoka kwa Watumishi kutoka kwa Wadau.

Mhe. Mteule aliahidi kujibu changamoto ambazo zilizokuwa katika meza yake kwa upande wa Mahakama, na kuwaomba kila mmoja kuweza kushiriki utendaji kazi bora katika maeneo yanayohusu Magereza.

Aliwasisitiza matumizi ya TEHAMA kwa wale ambao mashauri yao bado kwenye kusikilizwa na kuhakikisha kunakuwa na uwezekano wa kupunguza gharama za kila mara.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga na Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi, Mhe. Stella Shindika.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, akipokelewa na Askari Magereza wakati wa ziara yake.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, akipata picha ya pamoja na Askari Magereza pamoja na Wadau mbalimbali.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, (katikati) akipata picha ya pamoja baada ya kumaliza ziara ya ukaguzi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.

MAFUNZO YA UKATILI WA KIJINSIA YAHITIMISHWA

  • Jaji Kihwelo asisitiza uadilifu

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, amehitimisha mafunzo ya siku tatu yaliyolenga kuimarisha uwezo wa Mahakimu katika kushughulikia mashauri ya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia kwa kuzingatia utu, heshima na ustawi wa waathirika.

Akifunga mafunzo hayo tarehe 24 Juni, 2026 yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, Mhe. Dkt. Kihwelo alisisitiza umuhimu wa Mahakimu kuzingatia uadilifu, weledi na misingi ya haki wakati wa kushughulikia mashauri ya ukatili wa kijinsia ili kuhakikisha waathirika wanapata haki bila kuongeza maumivu ya kisaikolojia.

Jaji Kihwelo alisema mafunzo hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uelewa wa namna bora ya kuhudumia waathirika wanaofika mahakamani kutafuta haki. Aliwataka washiriki kutumia maarifa waliyojifunza katika utendaji wao wa kila siku ili kuendelea kujenga imani ya wananchi kwa mhimili wa Mahakama.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, aliwashukuru wawezeshaji na washiriki kwa ushiriki wao mzuri na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza mafunzo ya aina hiyo ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa ugawaji wa vyeti kwa washiriki, zoezi lililoongozwa na Jaji Kihwelo, kabla ya Viongozi na washiriki kupiga picha ya pamoja kuashiria kufungwa rasmi kwa mafunzo hayo.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha utoaji wa haki unaozingatia utu wa binadamu, kuongeza uadilifu na weledi katika usikilizaji wa mashauri ya ukatili wa kijinsia, pamoja na kuimarisha ulinzi wa haki za waathirika ndani ya mfumo wa Mahakama.

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt Paul Kihwelo, akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya unyanyasaji wa kijinsia. .

 

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe, Dkt Paul Kihwelo, (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wakufunzi wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Joachim Tiganga. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Upendo Ngitiri.


 

Meza kuu ikiongozwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe, Dkt Paul Kihwelo (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki. wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri.


 

 Baadhi ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo ya ukatili wa kijinsia wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo.

Meza kuu ikiongozwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe, Dkt Paul Kihwelo, (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Joachim Tiganga, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.


JAJI MFAWIDHI DODOMA ATETA NA WATUMISHI

  • Asisitiza uadilifu, weledi, uwajibikaji

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, ameanza rasmi majukumu yake kwa kukutana na Watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mara baada ya kuripoti katika kituo hicho.

Katika ziara hiyo aliyoifanya tarehe 22 Juni, 2026, Mhe. Tiganga alitembelea kila ofisi ya mtumishi ili kujionea mazingira ya kazi na kufahamu kwa karibu shughuli zinazotekelezwa na watumishi.

Baadaye, Mhe. Tiganga alifanya kikao na wawakilishi wa watumishi pamoja na wakuu wa vitengo mbalimbali vya Mahakama katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma.

Katika kikao hicho, alieleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha utendaji kazi, ushirikiano na utatuzi wa changamoto zinazoweza kujitokeza katika mazingira ya kazi.

Aidha, Jaji Mfawidhi alisikiliza maoni, ushauri na hoja mbalimbali kutoka kwa watumishi, akisisitiza umuhimu wa mawasiliano ya wazi, uwajibikaji na mshikamano ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Akihitimisha kikao hicho, aliwahimiza watumishi kuendelea kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na kujituma, huku akiahidi kushirikiana nao katika kutafuta suluhisho la changamoto mbalimbali kwa lengo la kuimarisha utendaji wa Mahakama na huduma kwa umma.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (aliyekaa katikati) akisema neno wakati wa kikao chake na watumishi waliopo IJC Dodoma, kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Bw.Bedson Mariba.

 

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma waliohudhuria kikao hicho.


 

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma waliohudhuria kikao hicho.


 

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma waliohudhuria kikao hicho.


 

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma waliohudhuria kikao hicho.