Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Mussa Maghimbi ametoa rai kwa wafanyakazi wa Mahakama na Wadau kwa ujumla kuwajibika ipasavyo ili kuhakikisha maono ya Mahakama ya Tanzania ifikapo 2050, iwe ya mfano duniani katika utoaji haki kama chombo huru chenye kuzingatia weledi, maadili, ufanisi na inayoaminiwa na wananchi katika jamii inayowazunguka.
Mhe. Maghimbi aliyasema hayo jana tarehe 16 Aprili, 2026 alipokuwa akiongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari jijini Dar es Salaam.
Katika hotuba yake Jaji Maghimbi, alisema maono hayo hayawezi kufikiwa kufikiwa bila kuwa na mikakati madhubuti katika utoaji haki ikiwa ni pamoja na kuimarisha upatikanaji wa haki, kuongeza imani kwa wananchi, kuimarisha uwezo wa rasilimali watu na kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.
Amesema kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 107A, Mhimili wa Mahakama ni Mamlaka yenye kauli ya mwisho katika Utoaji Haki katika Jamhuri ya Muungano, na Ibara ya 107B ya Katiba inatamka kuwa katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, Mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya Katiba na yale ya Sheria. “Ibara hizi zinatarajia watumishi kujipanga kimkakati na kuzingatia uadilifu, weledi, uwajibikaji na kwa kulenga matokeo makubwa,” amesisitiza.
Hali kadhalika, Jaji Maghimbi amewakumbusha wajumbe hao ahadi ambazo Mahakama imetoa kwa wananchi kwa wadau na kwa wanaofuata huduma mbalimbali mahakamani kuwa Maadhimisho ya Siku ya Sheria kwa mwaka huu yaliongozwa na Kaulimbiu isemayo; “Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa,” ambapo waliahidi kuwa Viongozi na Wafanyakazi wa Mahakama kutumia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kama kichocheo cha maboresho makubwa zaidi katika Mhimili wa Mahakama.
Akizungumzia kuhusu dhumuni ya Baraza la Wafanyakazi, Jaji Mfawidhi huyo na Mwenyekiti wa Kikao hicho alieleza kuwa ni kutoa fiursa kwa watumishi kupitia wawakilishi kujadili juu ya masuala ya msingi yanayohusu tija na ufanisi kwa upande mmoja na upande mwingine maslahi yao kama watumishi.
Aidha, Mhe. Maghimbi amesema kuwa, Wawakilishi wa Mabaraza ya Kanda wanatekeleza kwa vitendo takwa la kisheria linalotokana na Tamko la Rais (Tamko Na. 1 la Mwaka 1970) na Sheria nyingine za kazi zinazohimiza kuwakilisha wafanyakazi katika kufanya maamuzi mbalimbali kupitia Mabaraza ya Wafanyakazi.
Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti
amesema, vikao vya Mabaraza ya Wafanyakazi viko kisheria na lengo la kuanzishwa
kwa Mabaraza hayo ni kuwapa fursa watumishi ya kushauri Menejimenti,
kuwaunganisha watumishi na menejimenti kusuluhisha changamoto mbalimbali, kutoa shida zao za kiutumishi
na maslahi, na wao kama Kanda wakishindwa zitawasilishwa Makao Makuu.
Amesema pia, Mabaraza hayo ni mahali pa kupata mrejesho wa mambo yanayofanyika ndani ya Kanda na mrejesho kwa ngazi ya Taifa.
Kabla ya kikao hicho kuanza kilitanguliwa na uchaguzi uliosimamiwa na Ofisa Kazi, Bi. Vaileth Ndeza wa kujaza nafasi zilizoachwa wazi baada ya Katibu kuhama Kanda ya Dar es Salaam na Katibu msaidizi kufariki dunia.
Wajumbe hao walimchagua Bw. Shadrack Mlomo kuwa Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dar es Salaam na Mhe. Juliana Nankoma kuwa Katibu Msaidizi na pia Wilky Kavunjika alichaguliwa kuwa Mjumbe.
Katika kikao hicho walikuwepo Maofisa kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) ambapo wameeleza faida za mifuko hiyo kwa watumishi wa umma.
Vikao hivyo vimekuwa vikifanyika kila mwaka na wajumbe kuwasilisha hoja zao na pia kushauri kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu utumishi na maslahi ya watumishi kwa ujumla.
Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kanda ya Dar es Salaam wakiimbo wimbo wa wafanyakazi (solidarity forever).
Ofisa Kazi, Bi. Vaileth Ndezi akitoa utaratibu wa kufanya uchaguzi wa Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe wakati wa kikao hicho.
Bw.Wilcky Kavunjika akitoa
shukurani kwa wajumbe baada ya kuchaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi Taifa.
Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana akitoa taarifa ya mashauri wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti akitoa taarifa ya utawala wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara)











.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)