Na. HABIBA MBARUKU & INNOCENT KANSHA - Mahakama
Mtendaji
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka madereva
kuongeza umakini wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao ili kupunguza ajali
zisizokuwa za lazima pamoja na kupunguza uharibifu wa vyombo vya usafiri na
kulinda afya za wateja wao.
Pro. Ole Gabriel ameyasema hayo wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa
Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama
Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama
ya Tanzania jijini Dodoma.
Aidha,
Prof. Ole Gabriel, amesema mafunzo hayo maalum kwa madereva wote wa Mahakama,
yamelenga kuimarisha huduma kwa mteja, kuzingatia maadili ya kazi na kuongeza
usalama barabarani, mafunzo hayo yaliyoandaliwa chini ya mada ya Huduma kwa
Mteja kwa kada ya madereva au maafisa usafirishaji yamesisitiza nafasi muhimu
ya dereva katika mnyororo wa huduma za utoaji haki ndani ya taasisi, huku akibainisha
kuwa kila mtumishi ana mchango wa moja kwa moja katika taswira na ufanisi wa
Mahakama.
“Kuna
mambo mengi yanachangia utulivu wa mawazo na kufanya kazi kwa timu kama vile
kupata stahiki bora ni msingi wa mafanikio katika taasisi yoyote, uzembe wa
kada moja unaweza kuathiri kada nyingine, hivyo ni muhimu kila mmoja kutimiza
wajibu wake kwa umakini na weledi,” amesisitiza Prof. Ole Gabriel.
Akizungumzia
dhana ya mteja, Mtendaji Mkuu huyo amefafanua kuwa, mteja ni yeyote
anayenufaika na huduma inayotolewa, akiwemo kiongozi anayeendeshwa, watumishi
wa Mahakama pamoja na wadau wengine barabarani. Amesisitiza kuwa utoaji wa
huduma haupimwi tu kwa kutekeleza jukumu, bali kwa namna huduma hiyo
inavyotolewa.
Vilevile
katika mada ya matarajio ya mteja, madereva wamekumbushwa kuzingatia mambo kumi
muhimu ikiwemo usahihi na umahiri katika kazi, usafi wa gari na muonekano
binafsi, kutunza muda, usalama, utulivu barabarani na kutunza siri za kikazi na
binafsi za viongozi wanaowahudumia.
Kadhalika,
Prof. Ole Gabriel ameainisha sehemu ya changamoto zinazowakabili maafisa
usafirishaji wa Mahakama nchi nzima, zikiwemo usimamizi wa bajeti binafsi,
msongo wa mawazo ya kifamilia, bajeti finyu za matengenezo ya magari na wakati
mwingine kukosa heshima kutoka kwa baadhi ya viongozi. Hata hivyo, amewataka
madereva hao kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi licha ya changamoto
hizo.
Prof.
Ole Gabriel ameongeza kuwa, katika kuimarisha maadili ya kazi, Itifaki ya
Dereva Bora, inajumuisha mavazi ya heshima, kuepuka kupiga honi ili kumuita
kiongozi badala yake dereva anaweza kuwasiliana na kiongozi wake kwa
njia ya ujumbe mfupi wa maandishi au kumpigia simu baada ya dakika kumi
ikiwa ujumbe hautajibiwa, kuweka simu katika hali ya ukimya wanapoendesha,
kutoingia katika mabishano barabarani, kufika mapema kabla ya muda wa safari walau
dakika kumi kabla ya safari na kuepuka matumizi ya pombekabla ya safari na
wakati wa safari.
Akizungumza
kuhusu usalama, Mtendaji Mkuu amewakumbusha kuwa dereva anakabidhiwa chombo cha
thamani kubwa pamoja na uhai wa abiria na uhai wake mwenyewe, hivyo ni lazima
kuhakikisha gari liko katika hali nzuri kabla ya safari, dereva asikubali
kuendesha gari bovu lisilokaguliwa kabla ya safari, ahakikishe yuko kwenye afya
njema ili kuepuka uzembe unaoweza kusababisha ajali na kuleta hasara kubwa kwa
taasisi.
Mafunzo
hayo pia yaligusia tabia tano za kuepuka ili kutoleta usumbufu kwa kiongozi,
zikiwemo kuanza safari bila kukagua gari, kubishana na kiongozi, uzembe katika
mapokezi, kutoa taarifa za siri na kufokeana na wadau wengine wa barabara.
Aidha,
Prof. Gabriel amesisitiza kuwa, mteja ndiye sababu ya ajira ya mtumishi, hivyo
madereva wanapaswa kushirikiana kwa pamoja, kuepuka majungu na kuweka
kipaumbele katika utunzaji wa magari pamoja na maisha ya wanaowahudumia.
Mafunzo
hayo ni juhudi za Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utendaji kazi na
kuhakikisha huduma zinazotolewa kwa umma zinazingatia viwango vya juu vya
taaluma na maadili.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.














