Alhamisi, 16 Aprili 2026

WADAU WA SHERIA WANUFAIKA NA MAFUNZO MAALUM YA UTATUZI WA MIGOGORO

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu, Dodoma.

Mahakimu na Mawakili wa Mkoa wa Dodoma wameendelea kupatiwa elimu muhimu kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, hatua inayozidi kuimarisha mifumo ya haki na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kisheria nchini.

Mafunzo hayo yaliyofanyika jana tarehe 15 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dodoma kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) yamewakutanisha Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria.

Lengo la mafunzo hay oni kujengeana uelewa wa kina kuhusu matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR), njia inayozidi kupata nafasi kubwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka na kwa gharama nafuu.

Akitoa neno la ukaribisho, Naibu Msajili wa Mahakaa Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, aliwahimiza washiriki kutumia ipasavyo jukwaa hilo muhimu kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha weledi wao katika kushughulikia migogoro ya Wananchi.

Mafunzo hayo yaliendeshwa chini ya uratibu mahiri wa Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ameendelea kuonesha uongozi thabiti, weledi wa hali ya juu pamoja na dhamira ya dhati ya kuendeleza usuluhishi nchini.

Kupitia jitihada zake, Wadau wa Sheria wameendelea kunufaika na elimu yenye tija, huku akihamasisha kwa vitendo matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama suluhisho endelevu.

Mada mbalimbali ziliwasilishwa wakati wa mafunzo hayo na wataalamu wa sheria, akiwemo Mhe. Thurstone Kombe, Mhe. Sarah Mwalilino, Mhe. Judith Barigenge pamoja na wengine kutoka Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi nyingine kama CHRAGG.

Mada hizo zilieleza kwa kina umuhimu wa usuluhishi katika kupunguza migogoro, kuokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha mahusiano katika jamii.

Akisimamia majadiliano, Mhe.  Dkt. Khalfan alisisitiza kuwa usuluhishi si tu njia mbadala, bali ni nyenzo muhimu ya kujenga jamii yenye amani na mshikamano, huku akitoa wito kwa Wadau wa Sheria kuendelea kuipa kipaumbele.

Washiriki walipata nafasi ya kuuliza maswali na kuchangia hoja mbalimbali, hali iliyoonesha mwitikio mkubwa na uhitaji wa elimu hiyo katika jamii ya Wanasheria.

Akitoa neno la shukrani, Mhe. Zabibu Mpangule aliwashukuru waandaaji pamoja na washiriki wote kwa ushiriki wao, akibainisha kuwa mafunzo hayo yameongeza thamani kubwa katika utendaji wao wa kila siku.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa hotuba ya kufunga kutoka kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara ya Katiba na Sheria, aliyesisitiza umuhimu wa kuendeleza elimu ya usuluhishi ili kuhakikisha Wananchi wanapata haki kwa wakati, kwa ufanisi na kwa amani.

Kwa ujumla, tukio hili limeacha alama kubwa katika Mkoa wa Dodoma, likiwa ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za kuifanya Tanzania kuwa kinara wa matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati). Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


 

Mahakimu pamoja na Mawakili mbalimbali waliohudhuria elimu hiyo ya usuluhishi katika ukumbi uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo.

 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, akitoa neno la ukaribisho kwa wajumbe hao waliohudhuria elimu ya usuluhishi kwa Mahakimu na Mawakili.

 Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, akifuatilia kwa makini mada inayotolewa wakati wa utoaji wa elimu kwa Mahakimu na Mawakili.


 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu wa Dodoma walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi. Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watoa ujumbe maalumu kuhusu elimu ya usuluhish,i ambao pia ni Watumishi wa Mahakama Dodoma wakati wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

MAHAKAMA MOROGORO YAFANYA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI YA JINAI, MADAI

Na ASHA JUMA -Mahakama, Morogoro

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, imefanya kikao cha robo ya kwanza ya mwaka 2026, chenye lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kazi, hususan katika kusukuma mashauri ya jinai na madai.

Kikao hicho kilichofanyika jana tarehe 15 Aprili, 2026, katika ukumbi mkubwa wa mikutano uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro ni sehemu ya vikao vya kitaasisi vinavyolenga kuongeza ufanisi wa utoaji haki na kupunguza ucheleweshaji wa mashauri mahakamani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, aliongoza kikao hicho kiichowahusisha Wadau mbalimbali wa mnyororo wa haki, wakiwemo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Amiri Msumi, Mtendaji wa Mahakama Kuu Morogoro, Bw. Ahmed Ng’eni na Mahakimu.

Wengine walitoka Ofisi ya Mawakili wa Serikali, Chama cha Wanasheria wa Kujitegemea, Ofisi ya Baraza la Ardhi na Nyumba, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Wasaidizi wa Sheria wa Majaji pamoja na Ofisi za Madalali.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Msumi alipongeza juhudi za Mahakama na Wadau wote kwa ushirikiano wao katika kutekeleza majukumu ya kila siku.

Alieleza hali ya mashauri kwa robo ya kwanza ya mwaka 2026, akisisitiza kuwa bado kuna haja ya kuongeza juhudi zaidi, hususan katika mashauri ya rufaa za madai ambayo yanahitaji msukumo wa ziada.

Mhe. Msumi alibainisha baadhi ya changamoto zinazosababisha ucheleweshaji wa mashauri, ikiwemo kuchelewa kuwasilishwa kwa kumbukumbu kutoka Mahakama za chini, hasa Baraza la Ardhi na Nyumba.

Alieleza kuwa hali hiyo hupunguza kasi ya usikilizaji wa mashauri na hivyo kuathiri utoaji wa haki kwa wakati.

Ili kukabiliana na changamoto hizo, Mhe. Msumi aliainisha mikakati mbalimbali, ikiwemo kusimamia kwa ukaribu hatua zote za awali za maandalizi ya mashauri, kuhakikisha zinazingatia muda uliowekwa kisheria, pamoja na kupanga na kuamua maombi na mapingamizi kwa wakati.

Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha mawasiliano na Mahakama ya Rufani ili kusaidia kusikiliza na kumaliza mashauri kwa ufanisi, pamoja na kuhakikisha ufuatiliaji wa karibu wa mashauri yote.

“Mikakati hii pamoja na changamoto hizi inabidi tuzifanyie kazi haraka iwezekanavyo kwa sababu tunashughulika na haki za watu,” alisisitiza Mhe. Msumi.

Kwa upande wao, Wadau waliohudhuria kikao hicho waliipongeza Mahakama kwa hatua ya kutumia mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa mashauri, wakieleza kuwa hatua hiyo imeongeza kasi na uwazi katika utoaji wa huduma za haki.

Baadhi ya Taasisi pia zimeanza kutumia mifumo hiyo ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia yanayoletwa na Mahakama.

Akihitimisha kikao hicho, Jaji Mfawidhi alipendekeza kuwepo kwa mafunzo ya muda mfupi kati ya Mahakama na Wadau wa sekta ya haki ili kusaidia kuongeza ufanisi katika utoaji haki, kuboresha ubora wa maamuzi, kuimarisha ushirikiano, pamoja na kupunguza makosa ya kisheria.

“Elimu hii itasaidia kung’amua vitu gani tunaweza kusaidiana na kujadiliana pamoja na kubadilishana ujuzi,” alisema Mhe. Ebrahim.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeweka msingi imara wa kuboresha utendaji wa Mahakama Kuu Morogoro kwa kushirikiana na Wadau wake, kwa lengo la kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati na kwa ufanisi zaidi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, akiongoza kikao hicho.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Amiri Msumi, akisoma taarifa yake katika kikao hicho.

Picha mbalimbali za wajumbe katika kikao hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


WANANCHI SUMBAWANGA WAHAMASISHWA KUTUMIA UPATANISHI KUTATUA MIGOGORO

Na. SHARIFU MOKIWA-Mahakama, Sumbawanga

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga imeungana na Masjala nyingine nchini kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi iliyoanza tarehe 13 Aprili, 2026 kwa kutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea mabanda yaliyowekwa Mahakama Kuu Sumbawanga na Ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi  Sumbawanga ili kupata elimu ya utatuzi   wa migogoro kwa njia ya upatanishi ikiwa ni sehemu ya kuimarisha utoaji wa haki.

Aidha, wiki usuluhishi inatumia kaulimbiu isemayo “kutumia njia mbadala ya utatuzi wa migogoro kama mbinu inayo pendelewa ya kutatua migogoro nchini Tanzania” kaulimbiu hiyo inasisitiza dhamira ya Mahakama kuhamasisha jamii kutumia njia za usuluhishi katika kutatua migogoro kwa amani.

Akitoa elimu ya usuluhishi Jaji Mfawidhi wa Mahakama wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe.Frederick Manyanda akizungumzia umuhimu wa usuluhishi alisisitiza kuwa ni vyema kufanya usuluhishi kwa sababu unaweza kupoteza kila kitu kwa hoja za kiutaratibu na kisheria lakini ni faida zaidi pale unapokubali kumaliza mgogoro nje ya Mahakama kwa upatanishi.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo aliwahakikishia wananchi kuhusu nguvu ya kisheria ya makubaliano ya usuluhishi baina ya pande zenye mgogoro.

“Tuwatoe hofu kuwa, makubaliano ya usuluhishi yana nguvu ya kisheria na yanaweza kutekelezwa kama ilivyo kwa uamuzi wa Mahakama hivyo yale mtakayokubaliana yana thamani na uhalali wa kisheria,” alisisitiza Mhe. Mazengo

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Mhe. Kisasila Saguda akitoa elimu hiyo alisema kuwa, usuluhishi hutoa fursa ya kumaliza mgogoro kwa amani bila kuwepo mshindi au mshindwa, “usuluhishi husaidia kumaliza jambo kwa amani bila kuwa na mshindi wala mshindwa wote mnakuwa washindi kwasababu mmemaliza mgogoro wenu kwa maelewano,” alisema.

Akifafanua sehemu ya mambo Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Sumbawanga Mhe. Yusuph Sakara alisisitiza umuhimu wa usuluhishi katika kujenga maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii ili kuboresha ustawi wa wananchi.

“Tunataka jamii ipige hatua kimaendeleo, hatuwezi kupiga hatua hiyo kama tunahudhuria mahakamani siku nzima, hatuwezi kuwa na maendeleo tukiwaza tumerundika mashauri mahakamani. Usuluhishi ni jambo jema ukifanyika kwa haraka watu wanapata muda wa kwenda kufanya shughuli nyingine za kimaendeleo,” amesema Mhe. Sankara

Hivyo Mahakama inawahimiza wananchi kujitokeza kushiriki katika wiki ya usuluhishi ili kutatua migogoro kwa njia ya upatanishi, amani na kwa wakati hali itayakayo chochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Katika zoezi hilo Wasuluhishi na Wapatanishi walioteuliwa walipata wasaa wa kushughulikia sehemu ya migogoro iliyowasilishwa na wadau baada ya kupata elimu miongoni mwa migogoro iliyoshughulikiwa ni pamoja na migogoro ya kifamilia, kama vile ndoa ambapo pande husika zilipata fursa ya kusikilizana na kuelekezwa namna ya kufikia makubaliano bila ya kuendelea na mchakato wa kesi mahakamani.

Vilevile zoezi la kutoa elimu ya usuluhishi linaendelea katika Mahakama ya Wilaya Kalambo na Mahakama ya Wilaya Nkasi zilizopo Mkoa wa Rukwa.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Manyanda akieleza umuhimu wa usuluhishi wakati akitoa elimu kwa wananchi wakati wa kuadhimisha wiki ya usuluhishi nchini.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo akizungumza na wananchi waliojitokeza kupata elimu ya usuluhishi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa Mhe. Kisasila Saguda akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi.

Wananchi wakisikiliza kwa makini elimu ya usuluhishi iliyokuwa inatolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Rukwa Mhe. Kisasila Saguda (hayupo pichani)

Msaidizi wa Kumbukumbu Bw. Fredrick Mushi akisulusha wananchi walioamua kumaliza mgogoro wao kwa njia ya usuluhishi.

Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Sumbawanga Mjini Mhe.Yusuph Sakara akitoa elimu kuhusu umuhimu wa usuluhishi katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa


Wananchi wakisikiliza kwa makini elimu ya usuluhishi iliyokuwa inatolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Rukwa Mhe. Kisasila Saguda







 

JAJI MFAWIDHI SONGWE ATOA ELIMU YA USUHUHISHI KWA WADAU

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata, ametoa elimu ya usuhuhishi kwa wadau mbalimbali wa Mahakama katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe ikiwa ni siku ya kwanza ya kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi nchini.

Mhe. Malata alisema kuwa, katika pande mbili zenye migogoro husuluhishwa na upande wa tatu wa mtu anayejulikana kama msuluhishi ambapo msuluhishi huyo anaweza kuwa mtu yeyote, Mchungaji, Sheikh, Baraza la Wazee, Baraza la Kata, au Chombo kingine chochote cha usuluhishi.

Mhe. Malata aliongeza kuwa, usuluhishi unapaswa kutumika kama njia mbadala ili kutatua migogogoro katika familia, migogoro ya kibiashara, migogoro mahali pa kazi na migogoro ya kijamii na pia njia hii imerasimishwa kikatiba, kisheria kikanuni, kimila na desturi, na kwamba siyo Tanzania pekee, usuluhishi pia hutumika kutatua migogoro mbalimbali ya kimataifa. 

Aidha, Mhe. Malata alieleza faida za kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi na kusema kupitia usuluhishi unaokoa gharama na muda kwani usuluhishi huchukua mda mfupi kuliko kesi mahakamani na pia gharama zake ni ndogo ukilinganisha na ada za mahakamani na mawakili.

Vilevile, usuluhishi humaliza migogoro mapema bila kuchelewa hivyo kupunguza msongamano wa kesi mahakamani na kupitia usuluhishi wahusika huzungumza kwa amani na kuelewana hivyo husaidia kudumisha urafiki, undugu na ushirikiano.

Mhe. Malata alisisitiza suala la msamaha kwani kusamehe ni agizo kutoka kwa Mungu, kuto kufanya hivyo ni kwenda kinyume na agizo la Mungu, kwani migogoro haipendezi katika jamii na sio lazima kila mgogoro umalizwe na msuluhishi au kupelekwa kwenye vyombo vya sheria kwa kufanya hivyo huongeza gharama zisizo na misingi.

Mhe. Malata aliwasisitiza viongozi wa Dini waendelee kudumisha upendo, umoja na mshikamano baina ya waumini wao ili waishi kwa upendo na pia aliwakumbusha viongozi hao kuwa wana wajibu wa kuchunga kondoo wao vizuri kwani hilo ni jukumu lao walilopewa na Mungu ili kuepusha migogoro ambayo inaweza kutokea katika jamii.

Aidha, aliwaasa wadau wa usuluhishi kuwa waipokee njia ya usuluhishi na kutoa elimu kwa wanajamii wote kuhusu usuluhishi kama njia mbadala ya kutatua migogoro baina ya pande mbili na pia jamii itambue kuwa usuluhishi au upatanishi ni jambo ambalo lipo kwa mujibu wa dini zetu, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kisheria na pia hata katika mila na desturi zetu.

Mhe. Malata aliwashukuru wajumbe kwa kuhudhuria kikao hicho na pia aliwashukuru kwa michango yao mizuri yenye kujenga amani, upendeo na ushirikiano katika jamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata, akitoa elimu ya usuhuhishi kwa wadau mbalimbali wa Mahakama (hawapo pichani) ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha wiki ya usuluhishi nchini.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Bw. Sostenes Mayoka (kulia) akiwa katika kikao hicho cha wiki ya usuluhishi nchini.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde akifuatilia elimu ya Usuluhishi.

Sehemu ya Wadau waalikwa wakisikiliza kwa makini wakati Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (hayupo pichani) akitoa elimu ya usuluhishi.


Sehemu ya Wadau waalikwa wakisikiliza kwa makini wakati Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (hayupo pichani) akitoa elimu ya usuluhishi.

(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Jumatano, 15 Aprili 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAPOKEA KOMPYUTA MPAKATO 150

·       Ni kutoka Wizara ya Katiba na Sheria

·       Wizara hiyo yaipatia pia Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Magari Matano na Kompyuta Mpakato 30

·       Mahakama na Tume… waishukuru Wizara ya Katiba na Sheria kwa vitendea kazi hivyo

Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Mahakama ya Tanzania leo tarehe 15 Aprili, 2026 imekabidhiwa jumla ya Kompyuta Mpakato 150 kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, vifaa ambavyo vimekabidhiwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Dkt. Juma Homera (MB) ikiwa ni jitihada za Serikali za za kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuimarisha utoaji  haki kwa ufanisi.

Hafla ya kukabidhi Kompyuta hizo iliyofanyika katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma imeenda sambamba na kukabidhi jumla ya magari Matano na Kompyuta mpakato 30 vifaa ambavyo wamepatiwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi, Mhe. Dkt. Homera amesema tukio hilo linathibitisha dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuendelea kuimarisha Sekta ya Sheria ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wananchi wote na kwa wakati bila ya ubaguzi wa aina yoyote.

“Serikali chini ya uongozi mahiri wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeweka kipaumbele katika kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa kuhimiza kutumia fursa iliyopo ya maendeleo ya TEHAMA nchini katika kuimarisha mifumo ya kitaasisi ya utoaji wa huduma kwa umma kwa njia za kielekroniki. Fursa ya maendeleo ya TEHAMA iliyopo ni kichocheo kikuu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Hivyo, kwa upande wa Sekta ya Sheria, matumizi ya TEHAMA siyo ya hiari tena, bali ni hitaji la msingi katika kujenga Mfumo wa Haki unaokwenda sambamba na mahitaji ya karne ya 21,” amesema Mhe. Dkt. Homera.

Waziri huyo amesema kuwa, katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara hiyo yenye dhamana ya kusimamia masuala ya Katiba na Sheria, wameendelea kushirikiana na Taasisi zake katika kutekeleza majukumu yake, hususan kuimarisha mifumo ya utoaji haki na usimamizi wa haki nchini. Ametaja Taasisi hizo ni pamoja na Mahakama ya Tanzania ambayo imepewa jukumu la utoaji haki chini ya Ibara ya 1 07A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977; na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inayohamasisha hifadhi ya haki za binadamu, kwa kufanya uchunguzi na kupokea malalamiko ya uvunjaji wa haki za binadamu chini ya Ibara ya 1 29 na 1 30 ya Katiba.

Mhe. Dkt. Homera ameongeza kuwa, katika kutekeleza majukumu yake, Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora zinakutana na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta hivyo kushindwa kufikia malengo waliyojiwekea kiutendaji.

Hivyo, katika kutumia fursa hizo Wizara imekuwa ikitafuta na kuingia makubaliano na wadau mbalimbali wa maendeleo kutekeleza miradi na afua mbalimbali zinazolenga kuimarisha utendaji wa Sekta ya Sheria. Katika hili, Wizara kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) imeona ni vyema kuziwezesha taasisi hizi kwa kuzipatia vitendea kazi vichache ili kuimarisha uwezo wa kitaasisi katika kuhudumia watanzania,” ameeleza.

Amesema, ana imani kwamba, vitendea kazi hivyo vitaenda kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa majukumu na kuleta matokeo chanya na hatimaye kuwezesha Sekta ya Sheria kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

Aidha, Waziri huyo amebainisha kuwa, lengo la upatikanaji na utumiaji wa vifaa hivyo ni kutekeleza kwa vitendo Sera ya Serikali ya kujenga Mfumo Jumuishi, shirikishi na unaotumia teknolojia katika utoaji wa huduma za kisheria.

Mhe. Dkt. Homera ametoa rai kwa wanufaika wa magari na vifaa hivyo kuhakikisha vinatunzwa na kutumiwa vizuri ili kufanikisha malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amesema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha utendaji kazi wa Mahakama, hususan katika matumizi ya mifumo ya kielektroniki.

Ameeleza kuwa, kompyuta hizo zitachangia kurahisisha usajili wa mashauri, usimamizi wa kumbukumbu pamoja na uendeshaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (video conference), hatua itakayopunguza mlundikano wa kesi na kuongeza uwazi katika utoaji wa haki.

Aidha, amebainisha kuwa, matumizi ya TEHAMA ni nyenzo muhimu katika kuongeza kasi na ufanisi wa utoaji wa huduma za Mahakama nchini.

Kwa mujibu wa Msajili Mkuu, hatua hiyo pia itawezesha wananchi kupata huduma za Mahakama kwa urahisi zaidi bila kulazimika kufika mahakamani, ikiwemo kufungua mashauri, kufanya malipo na kufuatilia mwenendo wa mashauri.

Ameongeza kwamba, maboresho ya kimahakama yamechangia kupungua kwa muda wa usikilizwaji wa mashauri. Aidha, amebainisha kuwa tayari maboresho ya kimahakama yameanza kuleta matokeo chanya, ambapo muda wa wastani wa kusikiliza na kuamua mashauri umepungua hadi siku 68 mwaka 2025 kutoka viwango vya mwaka 2015.

Amesema kuwa, katika Mahakama za Mwanzo, ambazo hushughulikia zaidi ya asilimia 70 ya mashauri yote, muda wa usikilizwaji umepungua hadi wastani wa siku 30, hali inayoonesha kuongezeka kwa ufanisi katika utoaji wa haki.

Katika hafla hiyo, Msajili Mkuu aliambatana na baadhi ya Viongozi na Maofisa kutoka Makao Makuu ya Mahakama. Viongozi wengine walioshiriki ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mhe. Franklin Rwezimula, Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bw. Patience Ntwina, Viongozi na watumishi wengine wa Wizara hiyo pamoja na watumishi wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.



Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Dkt. Juma Homera (MB) (kushoto) akikabidhi Kompyuta Mpakato kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma wakati wa hafla ya kukabidhi magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama walioambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya wakati wa hafla ya Kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Sehemu ya Watumishi wa Wizara ya Katiba na Sheria waliohudhuria katika hafla ya Kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (MB) akizungumza jambo wakati wa 
hafla ya Kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa neno la shukrani wakati wa  
hafla ya kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (MB) (katikati). Wa pili kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mhe. Franklin Rwezimula, wa pili kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, wa kwanza kushoto ni Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bw. Patience Ntwina na wa kwanza ni kulia ni Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania, Bw. Shigeki Komatsubara wakiwa katika .


Meza kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mahakama walioambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa pili kulia) wakati wa 
hafla ya kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.




Picha za pamoja wakati wa 
hafla ya kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Magari matano yaliyokabidhiwa kwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.




Picha ya magari matano waliyokabidhiwa ume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Wizara ya Katiba na Sheria.