Jumapili, 19 Julai 2026

JAJI MLYAMBINA AHIMIZA WATUMISHI WA MAHAKAMA YA KAZI KULINDA UHURU WA MAHAKAMA

  • Awataka pia kuheshimu utawala wa sheria, kuendeleza ushirikiano na Wadau

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, amewahimiza Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kuendelea kulinda uhuru wa Mahakama, kuheshimu utawala wa sheria na kuendeleza ushirikiano baina ya Mahakama, Taasisi na Wadau wa Haki Kazi nchini.

Mhe. Dkt. Mlyambina alitoa wito huo usiku wa kuamkia Jana tarehe 18 Juylai, 2026 kwenye hafla ya kumuaga iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirika la Hifadhi ya Jamii PSSSF Mwenge jijini Dar es Salaam baada ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani  hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Haki inapotekelezwa kwa wakati na kwa usawa, hujenga amani mahali pa kazi, huongeza imani ya wananchi kwa Taasisi za umma na huimarisha maendeleo ya Taifa,” alisema huku akinukuu maneno ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye alisema, “Haki ndiyo msingi wa amani, na amani ndiyo msingi wa maendeleo.”

Mhe. Dkt. Mlyambina alimshukuru kila mmoja kwa ushirikiano, heshima, urafiki na msaada waliompa katika kipindi chote alichohudumu kama Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Kazi na kwamba ataendelea kuyathamini mahusiano hayo na popote atakapokuwa ataendelea kuwa balozi mwema wa Mahakama ya Kazi.

Jaji Mlyambina alieleza kuwa anajivunia kuwa sehemu ya safari ya kuendelea kuimarisha Mahakama ya Kazi, kwani ameshuhudia maendeleo katika usimamizi wa mashauri, matumizi ya teknolojia, uboreshaji wa huduma kwa wananchi, na kuimarika kwa ushirikiano na wadau mbalimbali.

“Mafanikio haya hayakuwa ya mtu mmoja, ni matokeo ya kazi ya pamoja. Tulifanya kazi kama timu moja. Timu yetu haikuwa kikundi cha watu wanaofanya kazi pamoja, ilikuwa kikundi cha wau wanaoaminiana kila mmoja. Nimebahatika kufanya kazi na timu yenye uwezo mkubwa, inayojali haki na inayoweka mbele maslahi ya wananchi. Kila mmoja wenu amechangia mafanikio yaliyopatikana,” alisema na kuwashukuru kwa dhati Majaji wenzake, Wasajili, Mahakimu na watumishi wote wa Mahakama ya Kazi.

Aidha, Mhe. Dkt. Mlyambina alieleza kuwa akiwa Jaji Mfawidhi alipata nafasi ya kujifunza, kufundishwa na kushirikiana na watu wenye weledi mkubwa na kujifunza kuwa uongozi si mamlaka bali ni dhamana; si nafasi ya kutawala bali ni wajibu wa kutumikia wengine kwa haki, busara na unyenyekevu.

Alimnukuu Mwandishi Simon Sinek katika kitabu chake ‘Find your why’ uk. 157, ambaye anasema, “The greatest contribution of a leader is to make other leaders” kwa tafsiri isiyorasmi kwa Kiswahili anasema, “Mchango mkubwa wa Kiongozi ni kuwafanya wengine kuwa Viongozi.”

“Naamini nimetekeleza hili kwa kadri nilivyoweza. Zaidi ya yote kila iitwayo leo kwa ushirikiano tulioujenga niliona kila mtumishi anatamani kuendelea kufanya kazi Mahakama ya Kazi” Mhe. Dkt. Mlyambina alisema.

Halikadhalika, aliwapitisha washiriki wa hafla hiyo kwenye nukuu nyingine ya Mwandishi Simon Sinek katika utangulizi wa kitabu chake cha Find your why anaposema:

“Fulfilment is a right and not a privilege. Every single one of us is entitled to feel fulfilled by the work we do, to wake up feeling inspired to go to work, to feel safe when we’re there and to return home with a sense that we contributed to something larger than ourselves. Fulfilment is not a lottery. It is not a feeling reserved for lucky few who get to say, ‘‘I love what I do’’

Kwa Kiswahili kisicho rasmi anasema, “Kuridhika ni haki, si upendeleo. Kila mmoja wetu ana haki ya kupata utoshevu kutokana na kazi anayoifanya; kuamka kila siku akiwa na hamasa ya kwenda kazini; kujisikia salama akiwa mahali pa kazi; na kurejea nyumbani akiwa na hisia kwamba ametoa mchango katika jambo kubwa zaidi kuliko maslahi yake binafsi. kuridhika si bahati nasibu inayowakuta wachache, bali ni haki inayomstahili kila mfanyakazi.”

Jaji Mlyambina ana imani kuwa Mahakama ya Kazi itaendelea kuwa nguzo muhimu katika kulinda haki za wafanyakazi na waajiri, kuimarisha mazingira bora ya kazi na kuchangia maendeleo ya uchumi wa Taifa kupitia utoaji wa haki wenye ufanisi na unaoaminika.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, akizungumza kwenye hafla ya kumuaga iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirika la Hifadhi ya Jamii PSSSF Mwenge jijini Dar es Salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, akizungumza kwenye hafla hiyo.

Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Enock Matembele, akitoa utambulisho wa wageni mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo. Picha chini ni matukio ya picha za Wadau na Watumishi wa Mahakama kwenye hafla hiyo.












Picha na Bakari Mtaullah-Dar es Salaam.


 

MAHAKAMA YA KAZI, WADAU WAMUAGA JAJI MLYAMBINA

  • Wampongeza kwa uongozi uliotukuka
  • Wamzawadia tuzo, zawadi mbalimbali
  • Yeye asema haki kazi haiwezi kujengwa na Mahakama peke yake

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, ameagwa na Watumishi wa Mahakama hiyo pamoja na Wadau wa Haki Kazi baada ya kuapishwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Hafla ya kumuaga Mhe. Dkt. Mlyambina ilifanyika usiku wa kuamkia jana tarehe 18 Julai, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Shirika la Hifadhi ya Jamii (PSSSF) Mwenge jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali, akiwemo Majaji wa Mahakama Kuu.

Wengine ni Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Mahusiano), Bi. Zuhura Yunus Abdallah, Kamishna wa Kazi Bara na Wawakilishi kutoka Wadau mbalimbali wa Haki Kazi, wakiwemo Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA),

Walikuwepo pia Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Mamlaka ya Usalama Kazini (OSHA), Mahirika ya Hifadhiy a Jamii ya PSSF na NSSF, Vyama vya Wafabyajazi, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wawakilishi Binafsi na Watumishi wa Mahakama ya Kazi.

Hafla hiyo ilipambwa na shamra shamra za utoaji Tuzo na Zawadi mbalimbali pamoja na muziki uliotumbuizwa na vijana kutoka Mahakama ya Kazi uliobeba ujumbe murua wa kumtakia heri Mhe. Dkt. Mlyambina kwenye majukumu yake mapya.

Salamu mbalimbali ziliwasilishwa na washiriki kwenye hafla hiyo, akiwemo Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo pamoja na Naibu Katibu Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira na Mahusiano.

Katika salamu zake, Mhe. Dkt. Opiyo, pamoja na mambo mengne, alimwelezea Jaji Mlyambina kama Kiongozi asiyependa makuu na asiye mbinabinafsi, bali ni mtu anayependa kuwamshirikisha kila mtu kwenye majukumu mbalimbali ya kiutendaji, hivyo kuwa mfano bora katika uongozi.

“Tunakushukuru sana kwa uongozi uliotukuka, ni vigumu sana kukuelezea kutokana na makubwa uliyofanya, sisi tuliokuwa Mahakama ya Kazi tumejifunza (mengi), umekuwa mama, siyo baba katika uongozi...

“…Tumejifunza sana kwako kwa uongozi shirikishi. Hatukujisikia unyonge kuwa pamoja nawe, ulitushirikisha kwenye mambo mbalimbali. Hatutasahau kamati mbalimbali ulizozianzisha na kutojilimbikizia majukumu,” alisema.

Jaji Opiyo alimwelezea pia Mhe. Dkt. Mlyambina kama Kiongozi mfuatiliaji anayependa ndoto aliyonayo itimie na kile anachokiamini na kupanga kitokee, hivyo ni mtu anayefanikisha matokeo.

Aidha, Mhe. Dkt. Opiyo alimwelezea Jaji Mlyambina kama Kiongozi aliyejaa upendo anayetamani kila mtumishi apate kile kidogo kinachopatikana, kwani anaamini ufanizi kazini huongezeka pale Mtumishi anapofurahi.

Kwa upande wake, Bi. Zuhura alimpongeza Jaji Mlyambina kwa uimarisha uhusiano mzuri kati ya Mahakama, Serikali, Waajiri na Wafanyakazi na kwa kusimamia haki na usawa kwa wafanyakazi kwa Waajiri kwa weledi wa hali ya juu.

Aliemwelezea kuwa Ofisi yake haikuwa tu kwa ajili ya kutoa maamuzi ya kisheria bali pia ilikuwa chamichemi ya ushauri na hekima kwa Wadau wote wa sekta ya haki nchini.

Alieleza kuwa kuteuliwa kwake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani halikuwa jambo la bahati mbaya, bali ni matokeo ya utendaji uliotukuka, uadilifu na uwezo wake.

Naibu Katibu Mkuu alitumia fursa hiyo kumkaribisha Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi mpya, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, na kuahidi kuendeleza ushirikiano uliokuwa wakati akitekeleza majukumu yake.

Akihitimisha hafla hiyo, Mhe. Dkt. Mlyambina alieleza kuwa Ofisi ya Kamishna wa Kazi imeendelea kuwa msimamizi muhimu wa utekelezaji wa sheria za kazi, upatanishi wa migogoro na kukuza mazungumzo ya kijamii, hivyo kusaidia migogoro mingi kutatuliwa kabla haijafika mahakamani.

Alisema kuwa WCF imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuhakikisha wafanyakazi wanaopata madhara wanapata fidia stahiki kwa mujibu wa sheria, jambo linaloimarisha haki na ustawi wa wafanyakazi na kupunguza migogoro Mahakamani.

Mhe. Dkt. Mlyambina alieleza pia kuwa OSHA imechangia kwa kiasi kikubwa kujenga utamaduni wa usalama na afya mahali pa kazi, hivyo kupunguza ajali na magonjwa yatokanayo na kazi na kuimarisha heshima kwa utu wa mfanyakazi.

Alisema kuwa CMA nayo amekuwa mdau muhimu wa huduma za upatanishi na usuluhishi wa migogoro ya kikazi, na kwa kufanya hivyo imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza migogoro inayofika Mahakama na kuhimiza utatuzi wa migogoro kwa njia za amani.

Kwa mjibu wa Mhe. Dkt. Mlyambina, PSSF na NSSF zimeendelea kutoa mchango mkubwa katika kuhakikisha wafanyakazi wanapata hifadhi ya jamii, jambo ambalo si tu linawapa usalama wa kiuchumi, bali pia linachangia ustawi wa jamii na uthabiti wa mahusiano ya kazi.

Alielezea pia upande wa vyama vya wafanyakazi TUCTA, TUGHE, TUICO na vingine ambavyo vimeendelea kuwa sauti muhimu ya wafanyakazi kwa kutetea haki zao, kukuza mazungumzo ya pamoja na kuhamasisha uhusiano wa kazi unaozingatia sheria, usawa na heshima.

“Kwa pamoja, kila mmoja wenu amekuwa mshirika wa karibu wa Mahakama ya Kazi katika kuhakikisha kuwa mfumo wa haki za kazi unafanya kazi kwa ufanisi,” alisema na kuongeza…

“Ingawa wakati mwingine tumekutana katika nafasi tofauti kutokana na majukumu yetu ya kisheria, tumekuwa tukiongozwa na lengo moja kuhakikisha haki inatendeka kwa mujibu wa sheria, migogoro inatatuliwa kwa haki na kwa wakati, na mazingira ya kazi nchini yanaendelea kuwa ya amani, tija na yenye kuheshimu utu wa binadamu.”

Jaji Mlyambina alibainisha pia kuwa katika kipindi chake cha uongozi kama Jaji Mfawidhi, amejifunza kuwa haki kazi haiwezi kujengwa na Mahakama peke yake, bali inahitaji waajiri wanaoheshimu sheria na wafanyakazi wanaotekeleza wajibu wao kwa uaminifu.

Alieleza pia kuwa inahitaji vyama vya wafanyakazi na waajiri vinavyotanguliza mazungumzo ya kijamii, pamoja na taasisi za Serikali zinazotekeleza majukumu yao kwa weledi.

Mhe. Dkt. Mlyambina alisema pia kuwa Mahakama imekuwa kiungo muhimu katika kuhakikisha kuwa tofauti zinapotokea zinatatuliwa kwa haki, kwa mujibu wa sheria na bila upendeleo.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akipokea tuzo kutoka kwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Mahusiano), Bi. Zuhura Yunus Abdallah, kwenye hafla ya kumuaga iliyofanyika Mwenge jijini Dar es Salaam.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akipokea zawadi kutoka kwa Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (kulia) akipongezwa na Majaji na Watumishi wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga (kushoto) akizungumza wakati wa hafla hiyo. Kulia ni sehemu ya watumishi wa Mahakama hiyo.

Meza Kuu inayoongozwa na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati).

Meza Kuu inayoongozwa na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) ikiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu na Wadau mbalimbali (juu na picha mbili chini).




Sehemu ya Wageni mbalimbali wakiwa kwenye hafla hiyo.


Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Mahusiano), Bi. Zuhura Yunus Abdallah akizungumza wakati wa hafla hiyo.


Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akizungumza wakati wa hafla hiyo.
Vijana kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi (juu) na  Bendi ya Muziki (chini) wakitumbuiza wakati wa hafla hiyo.


Picha na Bakari Mtaullah-Dar es Salaam.

Jumamosi, 18 Julai 2026

TUMIENI UJUZI NA TAALUMA MLIZONAZO KUTATUA CHANGAMOTO; JAJI RWIZILE

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile hivi karibuni alifanya ziara ya Ukaguzi wa Mahakama za Wilaya mkoani humo na kuwataka Watumishi wa Mahakama hizo kutumia vema taaluma na ujuzi walionao ili kutatua changamoto mbalimbali katika maeneo yao ya kazi.

Mhe. Rwizile alifanya ziara hiyo kwa lengo la kuangalia maendeleo ya shughuli za Mahakama katika maeneo ya mashauri, miundombinu pamoja na watumishi.

“Tumieni vema taaluma mbalimbali mlizonazo kutatua changamoto mbalimbali katika maeneo yenu ya kazi, nafahamu wapo watumishi wameajiriwa mkiwa na taaluma tofauti na ajira zenu, hivyo ni fursa kwenu kuonesha uwezo katika kusaidia shughuli zetu pale tunapokwama, hata hivyo tukishirikiana vema tutaongeza ufanisi na tija katika shughuli za Mahakama,” alisema Mhe. Rwizile.

Hata hivyo, Jaji Mfawidhi huyo alitoa pongezi kwa Mtumishi, Mlinzi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe, Bw. George Kato ambapo alisema, “nimepokea taarifa yenu imeonesha huyu bwana ametatua tatizo la ki-Tehama kwa kutumia taaluma yake, ambapo imesaidia shughuli za mashauri kutokwama, anastahili pongezi kubwa na kutambuliwa, nasi tumeona. Ni rai yangu kuwa, kila mtumishi mwenye taaluma tofauti na ajira/kada yake aitumie vema kama sehemu ya ubunifu na weledi wa kusaidia shughuli zetu.”

Vilevile, alitoa wito kwa watumishi wote wa Mahakama Kanda ya Kigoma kuwasilisha changamoto kwa Viongozi wao ili zitatuliwe kabla ya kuleta madhara katika mnyororo wa utoaji haki mapema ipasavyo.

Aidha, alisema kuwa, watumishi waendelee kushirikiana katika mipango wanayopanga na kukubaliana na kuitekeleza kwa pamoja ili kufikia malengo yenye kiwango kinachokubalika na Mwajiri, sambamba na utunzaji wa mazingira na miundombinu mbalimbali ya Mahakama.

Kwa upande wake Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa alisema kuwa, atasimamia maelekezo na maono ya Mwajiri ili kuhakikisha shughuli za Mahakama zinatolewa kwa mapema ipasavyo katika kila kituo.

“Nawapongeza watumishi wa Mahakama zote Kigoma kwa uchapakazi wenu, hasa katika eneo la mashauri,” alisema Mhe. Mbwelwa na kukiri kuwa anaridhishwa na usikilizwaji na umalizaji wa mashauri kwa Mahakama zote, ambapo hakuna mashauri mlundikano.

Hata hivyo, Naibu Msajili huyo aliwataka Watumishi kuendelea na kasi hiyo ili Mahakama Kigoma iendelee kuwa bora na tofauti katika maeneo yote ya kiutendaji.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka alisema kuwa, atasimamia maagizo yote katika kutekeleza Mpango Mkakati wa Mahakama pamoja na maelekezo yote ya Viongozi wa juu wa Mahakama ya Tanzania ili kufikia lengo na tija katika utoaji haki mapema ipasavyo. Hata hivyo, alimuhakikishia Jaji Mfawidhi kuwa utunzaji wa miundombinu ya Mahakama na vitendea kazi, unakwenda.

Mahakama zilizokaguliwa ni Mahakama za Wilaya za Kigoma, Kasulu, Buhigwe, Kibondo na Uvinza pamoja Mahakama za Mwanzo Kasanda na Manyovu, zilizopo Wilaya ya Buhigwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile kikagua Mahakama ya Mwanzo Manyovu alipofanya ziara ya kikazi katika Mahakama hiyo hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akisalimiana na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe alipofanya ukaguzi hivi karibuni. Anayesalimiana naye ni Bw. George Ilunga Kato, Mlinzi wa Mahakama ya Wilaya hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma,  Mhe. Augustine K. Rwizile (katikati) akizungumza jambo wakati wa ziara yake Mahakama ya Wilaya Buhigwe.  Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na kushoto Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe, Mhe. Katoke Mwakitalu.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile akigusa mti uliopandwa na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora wa kipindi hicho mwaka 2001, Jaji Mstaafu, Mhe. Edward Rutakangwa, wakati wa ziara ya ukaguzi wa Mahakama Kibondo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akikagua orodha ya mashauri katika ubao wa matangazo, uliopo katika eneo la wateja kusubiria  Mahakama ya Wilaya Uvinza. Pamoja naye kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na katikati  ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya uvinza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (wa pili kulia) akipokea taarifa ya ukarabati wa Mahakama ya Mwanzo Kasanda kutoka kwa Ofisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Kakonko, Bw. Nehemiah Makoko, (kulia) wengine ni Viongozi Waandamizi wa Mahakama Kuu Kigoma walioambatana katika msafara wa Jaji Mfawidhi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Haki Jinai alioambatana nao kukagua Gereza la Mahakama ya Wilaya Kasulu.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibondo mara baada ya ukaguzi wake katika Mahakama hiyo.

 Picha ya pamoja. Katikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati), wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka, wa pili kushoto ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kakonko, Mhe. Magreth Rweyemamu wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Kasanda Mhe. Jonas Kilimba.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka, (kulia) ni Mwendesha Mashtaka Mfawidhi wa Wilaya Uvinza, Bi. Edina Mkala na waliosimama ni Watumishi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka wa Wilaya hiyo mara baada ya kuzulu katika ofisi hiyo.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Ijumaa, 17 Julai 2026

MAHAKAMA GEITA, SONGWE WABADILISHANA UZOEFU KWENYE MATUMIZI YA TEHAMA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, tarehe 15 Julai, 2026 alipokea ugeni kutoka Mahakama Kuu Songwe, kwa lengo la kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji wa huduma za Mahakama.

Ziara ya Viongozi kutoka Mahakama Songwe iliongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Joyce Minde, akiwa ameambatana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, Afisa Utumishi pamoja na watumishi wengine wa Mahakama hiyo.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Kahyoza alisema kuwa kubadilishana uzoefu ni fursa muhimu ya kujifunza mbinu bora zinazoweza kuboresha utendaji kazi na kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa ufanisi, kwa wakati na kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia.

Aliwahimiza watumishi wa Mahakama Kuu Geita kuitumia kikamilifu fursa hiyo kwa kujifunza kutoka kwa wenzao wa Songwe na kushiriki kikamilifu katika mijadala.

"Kama una jambo la kuchangia au kuuliza, usisite kulisema. Lengo letu ni kujifunza kutoka kwa kila mmoja ili kuboresha huduma zetu," alisema Jaji Kahyoza.

Akizungumzia Mkoa wa Geita, Mhe. Kahyoza alisema kuwa licha ya kuwa ni Mkoa mchanga, una mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kupitia shughuli za uchimbaji madini, kilimo, uvuvi na ufugaji. Aidha, alisema Mkoa huo umejaliwa vivutio mbalimbali vya utalii, ikiwemo Ziwa Victoria, Hifadhi ya Kigosi pamoja na urithi wa utamaduni.

Kuhusu matumizi ya TEHAMA mahakamani, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa ni takwa la kisheria na kwamba Mahakama Kuu Geita ilianza rasmi kutekeleza mfumo wa Mahakama kidijiti tangu ilipoanzishwa tarehe 23 Desemba, 2023, kufuatia maelekezo ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wakati wa uzinduzi wa masjala hiyo.

Alisema Jaji Mkuu alielekeza Mahakama Kuu Geita kuanza shughuli zake kama Mahakama ya kidijiti (purely digital), bila kutumia karatasi. Aliongeza kuwa kufuatia maelekezo hayo, Masjala iliweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha matumizi ya TEHAMA yanatekelezwa kikamilifu.

Mikakati hiyo ilijumuisha kuendesha mafunzo ya ndani kwa watumishi, kufanya mikutano na wadau wa Mahakama, Viongozi wa Serikali pamoja na wananchi ili kuwajengea uelewa kuhusu umuhimu wa kuondokana na matumizi ya karatasi katika utoaji wa huduma za Mahakama.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (ECMS), akieleza namna mfumo huo unavyowezesha uendeshaji wa mashauri bila matumizi ya karatasi.

Alisema mfumo huo umeongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri kwa kuwezesha ufuatiliaji wa mwenendo wa kesi, kupunguza mlundikano wa mashauri, kuharakisha utoaji wa haki na kuimarisha uwazi katika shughuli za Mahakama.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya TEHAMA yameboresha utunzaji wa kumbukumbu za mashauri kwa kuondoa changamoto ya upotevu wa mafaili, kurahisisha upatikanaji wa hukumu na maamuzi kupitia hifadhidata, kuboresha usahihi wa takwimu za Mahakama pamoja na kupunguza muda na gharama za uendeshaji kupitia matumizi ya Mahakama pepe.

Akizungumza kuhusu mafanikio ya Taasisi, Mhe. Lukuna alisema kuwa ni muhimu kuwa na malengo yaliyo wazi na yanayopimika, kujenga timu yenye nidhamu, kusimamia muda kwa ufanisi na kuendelea kuwajengea uwezo watumishi kupitia mafunzo endelevu.

"Ni muhimu kudumisha mahusiano mazuri kazini, kujifunza kutokana na makosa yaliyopita, kubaini changamoto zinazochelewesha utendaji, kuhakikisha rasilimali muhimu zinapatikana na kuwa tayari kufanya maamuzi yatakayochochea mafanikio ya pamoja," alisema.

Naye Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, alieleza namna masjala hiyo ilivyoondokana na matumizi ya karatasi kwa kutumia mifumo ya kidijitali katika mawasiliano na utunzaji wa nyaraka.

Alisema hatua hiyo imeongeza ufanisi wa kazi, kupunguza gharama za ununuzi wa mafaili na vifaa vya kuhifadhia nyaraka, kuimarisha usalama wa taarifa kwa kupunguza hatari ya uvujaji wa taarifa, kurahisisha utoaji wa huduma kwa wateja na kuongeza ubunifu katika utendaji kazi.

Bi. Kisasila aliwashauri washiriki kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mara kwa mara wa mifumo ya TEHAMA, kutoa motisha kwa watumishi na kuendelea kuendesha mafunzo ya ndani ili kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.

Kwa niaba ya ujumbe kutoka Songwe, Mhe. Minde, alitoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu ya Geita kwa mapokezi mazuri na mafunzo yenye tija yaliyotolewa wakati wa ziara hiyo.

Alimshukuru Jaji Mfawidhi, Naibu Msajili, Mtendaji pamoja na watumishi wote wa Mahakama Kuu ya Geita kwa ushirikiano waliouonyesha licha ya taarifa ya ujio wa ujumbe huo kutolewa kwa muda mfupi. Aidha, aliahidi kuwa maarifa na uzoefu walioupata vitatekelezwa na kusambazwa katika vituo vyao vya kazi ili kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, akiwakaribisha watumishi kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe.


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi (wa katikati) akihimiza kushiriki kikamirifu katika mafunzo ya kubadilishana uzoefu, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Songwe, Mhe. Joyce Minde.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akitoa mada kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (ECMS) bila matumizi ya karatasi.

Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, akieleza mafanikio ya matumizi ya TEHAMA katika eneo la utawala.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, akiwezesha mafunzo juu ya matumizi ya TEHAMA kwa upande mashauri na utawala katika ngazi ya Wilaya pasipo kutumia karatasi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, akiwezesha mafunzo juu ya mfumo wa Mahakama ya Mwanzo unaotumika Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (wa pili kushoto) akiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Songwe, Mhe. Joyce Minde na watumishi wa Mahakama Songwe.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.


 

Alhamisi, 16 Julai 2026

WATUMISHI MBEYA WAMUAGA MSTAAFU BW. CHARLES MAPUNDA CHITEKETELA KWA HESHIMA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya jana tarehe 15 Julai, 2026 walishiriki katika hafla ya kumuaga aliyekuwa mtumishi Mahakama mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela, ambaye alikuwa akihudumu kama Msaidizi wa Kumbukumbu na Msimamizi wa Kitengo cha mashauri ya Madai, anayestaafu utumishi wa umma baada ya kuitumikia Mahakama kwa weledi, uadilifu na kujituma kwa muda wa miongo kadhaa.

Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya na kuhudhuriwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, viongozi mbalimbali wa vitengo pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Wilaya Mbeya.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Mpepo alimpongeza Bw. Mapunda kwa utumishi wake uliotukuka na mchango mkubwa alioutoa katika kuimarisha utendaji wa Mahakama. Alieleza kuwa mstaafu huyo amekuwa mfano wa uwajibikaji, uaminifu na uzalendo katika kutekeleza majukumu yake.

“Tunakupongeza sana Bw. Mapunda, umekuwa mtumishi uliyeitumikia Mahakama kwa utumishi uliotukuka. Tunazijua na kuzithamini kazi ulizozifanya na kwa juhudi zako uliendelea kujiendeleza hadi kufika hapo ulipo, kwa hakika uliipenda na kuiheshimu kazi yako Mungu akubariki katika maisha yako mapya,” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, mstaafu huyo Bw. Chiteketela alitoa shukrani kwa viongozi na watumishi wote aliobahatika kufanya nao kazi kwa kipindi chote cha utumishi wake. Alisema ushirikiano, upendo na mshikamano alioupata kutoka kwa wenzake umechangia mafanikio yake katika kazi.

“Napenda kuwashukuru watumishi wenzangu ambao tumefanya kazi pamoja kwa ushirikiano mkubwa bila kuchoka na bila kubaguana. Nawashukuru pia viongozi wangu kwa kunilea na kuniongoza vyema hadi kufikia hatua hii, Mungu awabariki sana.”

Aidha, Bw. Chiteketela aliwaasa watumishi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, bidii na uaminifu, akisisitiza kuwa mafanikio katika utumishi yanatokana na kuipenda kazi na kutimiza wajibu kwa moyo wa kujituma.

“Ukifanya kazi kwa weledi na kujituma haikupi shida kuifanikisha kazi yako. Nawausia kuipenda kazi yenu na kujituma katika majukumu yote mnayopangiwa na viongozi, kwani huo ndiyo msingi wa mafanikio,” alisisitiza Bw. Chiteketela

Bw. Mapunda aliwahimiza watumishi kudumisha umoja na ushirikiano mahali pa kazi ili kuendelea kujenga mazingira bora ya utendaji na kuimarisha mahusiano ya kikazi.

“Nawasihi muwe na umoja na ushirikiano baina yenu, kwa kuwa kufanya hivyo kutaboresha utendaji kazi na kujenga undugu imara baina yenu.”

Hafla hiyo imeendelea kudhihirisha utamaduni wa Mahakama wa kuthamini na kuenzi mchango wa watumishi wake waliotumikia taasisi kwa uaminifu, uadilifu na kujituma.

Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) akizungumza machache na kutoa neno la shukrani katika hafla hiyo.


Bw. Charles Mapunda Chiteketela (watatu kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na Mahakimu Mbalimbali wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba (watatu kushoto)

Bw. Charles Mapunda Chiteketela (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa kitengo cha madai ambacho Bw. Charles Mapunda Chiteketela alikuwa msimamizi wa kitengo hicho

Bw. Charles Mapunda Chiteketela (wapili kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na maafisa Utumishi/Tawala (wa kwanza kushoto) ni Afisa Utumishi Mahakama ya Watoto Mbeya Bw. Ibrahim Mgallah, (wa pili kushoto) ni Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Odilia Mapunda, (wa kwanza kulia) ni  Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bi. Sarah Lossi a aliyesimamama nyuma ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Alintula Ngalile.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akikabidhi sehemu ya zawadi zilizoandaliwa kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akikabidhi sehemu ya zawadi zilizoandaliwa kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akimlisha keki kuonesha ishara ya pongezi kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.