Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma
Kaimu Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji
Hassan, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji
katika utoaji wa huduma za haki, akibainisha kuwa misingi hiyo ni nguzo kuu ya
utendaji wa Mahakama nchini.
Mhe. Hassan
ameyasema hayo leo tarehe 10 Aprili, 2026, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa
Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dodoma uliofanyika katika Ukumbi wa
Halmashauri ya Wilaya ya Bahi.
Amesema kuwa
kila mfanyakazi wa Mahakama ana nafasi muhimu katika kutekeleza jukumu la
kikatiba la utoaji haki, akirejea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya
mwaka 1977 inayoweka wajibu wa kuhakikisha Wananchi wanapata haki bila ubaguzi.
Aidha,
ameipongeza Menejimenti ya Mahakama kwa kuendelea kutekeleza matakwa ya
kisheria ya uendeshaji wa mabaraza ya wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na Tamko Na.
1 la mwaka 1970 na kanuni mbalimbali za utumishi wa umma zinazolenga
kuwashirikisha katika maamuzi ya kiutendaji.
Jaji huyo
amesisitiza kuwa mabaraza ya wafanyakazi yana jukumu la kuishauri Serikali
kuhusu usimamizi wa rasilimaliwatu, kuboresha mazingira ya kazi, kulinda haki
na wajibu wa Mwajiri na Mwajiriwa pamoja na kuimarisha ustawi wa Watumishi
mahali pa kazi.
Amepongeza Wafanyakazi
wa Mahakama kwa mchango wao katika utoaji wa haki na kutambua Wafanyakazi
hodari wa mwaka 2026, akisema hatua hiyo ni chachu ya kuongeza ari ya utendaji
kazi.
Kuhusu
maadili, amesisitiza kuwa Watumishi wa Mahakama wanapaswa kuzingatia kanuni za
maadili ya utumishi wa umma ili kuhakikisha utoaji wa huduma bora, akibainisha
kuwa Mahakama ni chombo kinachobeba dhamana ya haki kwa Wananchi wote bila
kujali hali, jinsia, dini au rangi.
Ameeleza
kuwa Dira ya Mahakama ni kuhakikisha haki inapatikana kwa wote kwa wakati,
akirejea misingi ya kikatiba inayolenga kulinda amani, usalama, maadili na
umoja wa kitaifa.
Katika
kuimarisha utendaji kazi, Jaji huyo amesisitiza matumizi ya Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano (TEHAMA), akibainisha kuwa Mahakama inaelekea katika
mfumo wa Mahakama Mtandao (e-Judiciary) utakaowezesha utoaji wa huduma za haki
kwa njia ya kidijitali.
Amewataka Viongozi
wa Mahakama ngazi zote kwenye Kanda hiyo kuhakikisha Watumishi wanapatiwa
mafunzo ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi, uwazi na kasi ya utoaji haki pamoja na
kupunguza mlundikano wa mashauri.
Aidha, Mhe.
Hassan amerejea maelekezo ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
yaliyotolewa Februari 2, 2026, akisisitiza umuhimu wa kuongeza matumizi ya
mifumo ya TEHAMA pamoja na kuzingatia uadilifu katika usimamizi wa sheria na
utoaji haki.
Pia ametoa
maelekezo kwa Viongozi katika Kanda hiyo kuhakikisha utekelezaji wa sera
mbalimbali za mafunzo ya utumishi wa umma na Mahakama pamoja na mipango mkakati
inayolenga kuboresha utendaji kazi.
Katika hatua
nyingine, amesisitiza umuhimu wa Watumishi kulinda na kutumia kwa uangalifu
rasilimali za Mahakama, akirejea wito uliotolewa kwa madereva wa Mahakama
kuhusu kuzingatia nidhamu, usalama na weledi katika utekelezaji wa majukumu
yao.
Amesema
Mahakama ina wajibu wa kuendelea kuwaelimisha Wananchi kuhusu taratibu na
huduma zinazotolewa ili kuongeza uelewa na upatikanaji wa haki kwa urahisi
zaidi.
Amehimiza Watumishi
kufanya kazi kwa bidii, kuzingatia maadili na kutoa huduma bora kwa wakati,
akisisitiza kuwa wao ni Waajiriwa wa Wananchi na wanapaswa kuwahudumia kwa
uadilifu na weledi wa hali ya juu.
Vilevile
katika baraza hilo kulikuwa na uchaguzi wa Viongozi ambao ni Katibu wa Baraza
la Wafanyakazi Kanda ya Dodoma, Mhe Dickson Tigalyoma, Naibu Katibu Baraza, Bi.
Irine Msafiri pamoja na Mjumbe wa Baraza Kuu Taifa Bi. Arapha Rusheke. Aidha
katika Mkutano huo Wafanyakazi Hodari wa Mkoa wa Dodoma waliweza kutambuliwa.
Kabla ya Kufungwa kwa kikao hicho cha Baraza wajumbe mbalimbali pamoja na waalikwa walitoa neno la shukrani kwa Viongozi kwa kufanikisha kikao hicho. Baada ya kikao hicho wajumbe wote walirejea katika sehemu zako za kazi.
Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan akisalimiana na wajumbe wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Mahakama ya Wilaya Bahi.
Kaimu
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan akisaini
kitabu cha wageni katika Ofisi ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya
Bahi.
Kaimu
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan, akifuatilia
kwa makini kikao cha Baraza la Wafanyakazi katika Ukumbi wa Halmashauri ya
Wilaya ya Bahi.
Meza kuu ikiongozwa na Kaimu Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan (katikati),
kulia kwake ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerald
Gamba na kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Tughe Mkoa wa Dodoma, Bw. Maulid
Kipeneku, wakiimba nyimbo ya mshikamano katika Baraza hilo lilofanyika katika
ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya Bahi.
Meza kuu ikiongozwa na Kaimu Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan (aliyesimama)
akisema neno wakati wa kikao hicho. Kulia
kwake ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dodoma Mhe Gerald Gamba na
kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Tughe Mkoa wa Dodoma Bw. Maulid Kipeneku,
wakiimba nyimbo ya mshikamano katika baraza hilo lilofanyika katika ukumbi wa
Halmashauri ya Wilaya Bahi.
Katibu anayemaliza muda wake, Mhe. Gerald Gamba (kulia)
akimkabidhi mkataba Katibu Mpya, Mhe Dickson Tigalyoma, mara baada ya uchaguzi
wakati wa kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya Wilaya ya
Bahi.
























