Jumatano, 24 Juni 2026

JAJI MTULYA ATETA NA WADAU WA MAHAKAMA MASJALA NDOGO YA MBEYA

 Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya amefanya mazungumza na wadau wa haki jinai na madai wa Masjala Ndogo ya Mbeya kwa lengo la kujitambulisha na kutambuana baina ya wadau hao kufuatia mabadiliko ya uongozi katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika jana tarehe 23 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Mtulya aliwaasa wadau kudumisha ushirikiano uliopo baina yao na Mahakama mbali na masuala ya kiofisi hata katika mambo mbalimbali ya kijamii ikiwemo michezo.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu alitumia nafasi hiyo kuwaaga wadau hao kufuatia uhamisho wake wa kwenda Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam huku akiwashukuru wadau hao kwa kuwa kinara wa kuhakikisha kuwa mashauri yanayamalizika mahakamani mapema ipasavyo kupitia ushirikiano wao wa karibu na Mahakama.

Naye, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo alitoa pongezi zake kwa wadau hao kwa namna walivyokuwa na ushirikiano mzuri kwa Mahakama na kutumia nafasi hiyo pia kuwaaga kufuatia uhamisho wake wa kuhamia Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Morogoro.

Nao wadau wa Mahakama waliahidi kudumisha ushirikiano uliopo baina yao na kueleza matumaini yao juu ya usimamizi thabiti kutoka kwa viongozi wa Mahakama huku wakitoa shukrani zao kwa Waheshimiwa Naibu Wasajili kwa muda wote walioshirikiana kwa pamoja katika shughuli mbalimbali za kiofisi na kijamii hadi kufikia uhamisho wao kwenda kwenye vituo vyao vipya vya kazi.

Aidha Mhe. Mtulya alihitimisha kikao hicho kwa kuahidi kushughulikia changamoto zote zilizowasilishwa na kuahidi kuwa mlezi bora kwa kuwajenga na kuwaweka katika mstari mnyoofu ili kufanikisha malengo ya kutoa haki kwa wakati mapema ipasavyo ili kukidhi matamanio ya wananchi wanaowahudumia.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama) akifafanua jambo wakati wa kikao chake na Wadau wa Mahakama wa haki jinai na madai, kikao kilichofanyika jana tarehe 23 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo.

Sehemu ya wadau  wa haki jinai na madai waliohudhuria wakifuatilia kwa makini hoja mbalimbali katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau  wa haki jinai na madai waliohudhuria wakifuatilia kwa makini hoja mbalimbali katika kikao hicho.

Mmoja wa wadau akizungumza na kuchangia mada kuhusu eneo lake la kazi katika kikao hicho.


Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu  (aliyesimama) akitoa neno wakati wa majadiliano na wadau hao wa Mahakama Masjala Ndogo ya Mbeya.

Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

JAJI MUGETA AKABIDHI OFISI RASMI KWA JAJI DKT. MAMBI

Na. Christopher Msagati – Mahakama, Manyara

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Ilvin C. Mugeta amekabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi leo tarehe 24 Juni, 2026 ikiwa ni baada ya Mhe. Mugeta kuhamishwa kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora.

Mhe. Dkt. Mambi ambaye kabla ya kuja Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Tabora. Katika hafla ya makabidhiano, Majaji hao walipata wasaa wa kuzungumza na watumishi pamoja na wadau wa Mahakama, ambapo Mhe. Mugeta alitumia nafasi hiyo kuagana na wanamanyara, huku Mhe. Dkt Mambi akitumia wasaa huo kujitambulisha na kuwatambua watumishi wa Mahakama katika Masjala hiyo.

Akitoa shukrani wakati wa kuagana na watumishi Mhe. Mugeta alisema kuwa, ushirikiano alioupata toka Masjala Ndogo ya Manyara usiishie hapo mara baada ya kuondoka kwake bali uendelee kwa Kiongozi huyo mpya na hata Viongozi wengine watakaoendelea kuja kwenye Masjala hiyo.

“Leo ni siku yangu ya pekee ambayo imechanganyikana na hisia za furaha pamoja na huzuni, nalazimika kuagana na watumishi niliokuwa nao tangu mwaka 2025 nilipohamia Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara nikitokea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha, watumishi hawa wamenipa heshima kubwa sana…

 …Viongozi hawawezi kufanya kazi peke yao isipokuwa kwa ushirikiano na umoja wetu. Mhe Jaji Mambi, ninakuachia watumishi hodari ambao wana moyo wa kufanya kazi kwa bidii pasipo kushurutishwa au kusimamiwa kwa nguvu,” alisema Mhe. Mugeta.

Naye, Mhe. Dkt. Mambi alipokea kwa mikono miwili ukaribisho aliyoupata kwa watumishi wa Masjala hiyo, huku akisisitiza kuwa ofisi yake ipo wazi kwa yeyote mwenye mawazo ya kuboresha. Alisisitiza kuwa yeye ni mtu wa kazi na anavutiwa zaidi na wachapa kazi.

“Nashukuru kwa uongozi wa Mahakama kwa kuona kuwa mimi naweza kuendeleza kazi njema ambayo ameifanya Mhe Jaji Mugeta katika Masjala hii ya Manyara, kasi ya utendaji kazi iliyokuwepo naamini tutaiendeleza na kushirikiana vema ili tuweze kuwahudumia wananchi kwa namna ambayo inastahili,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Katika hafla hiyo, watumishi wa Kada mbalimbali waliweza kutoa maneno ya kumkaribisha na kumpokea Mhe. Dkt. Mambi anayehamia Manyara na pia kumuaga Mhe. Mugeta.

Miongoni mwao alikuwa ni Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Thobias Kavishe John alisema kuwa, wataendelea kutoa ushirikiano kwa Mhe. Dkt. Mambi ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa. Pia Mhe. John alimtakia majukumu mema Mhe. Mugeta katika majukumu yake mapya anayokwenda kuyaanza katika Kituo chake Kipya cha Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora.

Naye, Msaidizi wa Hesabu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Bw. Sixbert Hongoli aliahidi kuendeleza ushirikiano kutoka kwa watumishi wa Kada nyingine ambao wote kwa ujumla wao wameonesha nia na utayari wa kuyapokea maelekezo toka kwa Kiongozi huyo mgeni aliyeripoti Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.

Kwa namna ya pekee wanamanyara watamkumbuka Mhe. Mugeta kwa kuwa ndiye Jaji Mfawidhi wa pili tangu kuanzishwa kwa huduma za Mahakama Kuu katika Masjala Ndogo ya Manyara mnamo Mwezi Novemba mwaka 2022.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Mahakama Kuu Tabora Mhe. Ilvin Mugeta (kulia) na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe Jaji Dkt. Adam Mambi wakiwa katika tukio la kupeana hati ya makabidhiano ya Ofisi ya Ufawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.

Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akitoa neno la shukrani kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa mapokezi waliyompatia mara baada ya kuwasili kituoni hapo. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Ilvin Mugeta akitoa neno la shukrani kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kumuuga vizuri.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Ilvin Mugeta (kulia) na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati) wakionesha hati za makabidhiano kwa watumishi waliofika kushuhudia tukio hilo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemedi akimkabidhi Zawadi ya ua Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Masjala Ndogo ya Tabora, Mhe. Ilvin Mugeta ikiwa ni Ishara ya kumuaga kutoka kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara wakiendelea na zoezi la kujitambulisha wakati wa zoezi la Makabidhiano ya Ofisi kati ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayeondoka Mhe. Ilvin Mugeta na Jaji Mfawidhi mpya Mhe Dkt Adam Mambi.

Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akisaini vitabu vya wageni katika Ofisi yake mpya mara baada ya kuripoti kituoni hapo.


Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akisalimiana na baadhi ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara mara baada ya kuripoti kituoni hapo.

Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akipokea Zawadi ya ua ikiwa ni Ishara ya Ukaribisho kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


JAJI MKUU AMUAPISHA HAKIMU MKAZI MPYA WA MAHAKAMA YA MWANZO

Na MARY GWERA & HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma

·       Jaji Mruma ampa Wasia Hakimu huyo kutoa maamuzi yanayozingatia Mila na Desturi za Jamii husika

·       Naye Jaji Tiganga amtaka kutoa haki kwa kuzingatia misingi ya Katiba, Sheria za Nchi

Katika jitihada za kuendelea kuimarisha utoaji haki nchini kupitia kuongezwa kwa watumishi wenye weledi na uadilifu, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 24 Juni, 2026 amemuapisha Mhe. Rose Baltazar Ngero kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo.

Uapisho huo umefanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, katika hafla iliyobeba uzito wa kiutumishi na kisheria, ikionesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania ya kuendelea kuimarisha Mhimili wa utoaji haki kuanzia ngazi za chini kabisa zinazogusa wananchi moja kwa moja.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali Waandamizi wa Mahakama akiwemo Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, baadhi ya Naibu Wasajili, watendaji pamoja na watumishi wengine wa Mahakama.

Akitoa wasia kwa Hakimu huyo mpya mara baada ya uapisho, Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma amemsisitiza juu ya umuhimu wa kuzingatia sheria sambamba na mila na desturi za jamii husika katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama.

“Katika kiapo chako umeahidi kusimamia sheria, mila na desturi. Ni muhimu kuelewa kwamba mashauri mengi katika Mahakama ya Mwanzo yanahusu maisha halisi ya jamii, hivyo uelewe mazingira na desturi za watu unaowaamria,” amesema Mhe. Mruma.

Jaji Mruma amesema mashauri mengi yanayofikishwa katika Mahakama za Mwanzo huhusisha masuala ya kijamii kama mirathi, talaka na migogoro ya kifamilia ambayo mara nyingi huongozwa na mila na desturi za jamii husika, hivyo ni muhimu kwa Hakimu kuwa na uelewa mpana wa mazingira anayofanyia kazi ili kutoa uamuzi wenye haki na unaokubalika kijamii.

Mhe. Mruma amebainisha kuwa, uwezo wa Hakimu kuelewa na kutafsiri Sheria za Kimila kwa usahihi unaweza kusaidia Mahakama kutoa maamuzi yanayozingatia haki huku yakibaki karibu na uhalisia wa jamii, jambo linaloongeza imani ya wananchi kwa mhimili wa Mahakama.

“Wakati mwingine suluhisho la mgogoro haliishii kwenye vifungu vya sheria pekee, bali linahitaji pia uelewa wa historia, utamaduni na namna jamii husika inavyoendesha maisha yake. Hapo ndipo busara ya hakimu inapokuwa muhimu,” amesisitiza.

Aidha, Mhe. Mruma amemtaka Hakimu huyo kuzingatia maadili ya kazi na kulinda heshima ya taaluma ya sheria.

“Jiepushe na mazingira au mienendo inayoweza kushusha hadhi ya kazi yako. Uadilifu wako binafsi ndio msingi wa wananchi kuendelea kuiamini Mahakama,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, amesema kazi ya utoaji haki ni dhamana kubwa inayopaswa kutekelezwa kwa kuzingatia misingi ya Katiba, Sheria za Nchi pamoja na maadili ya Viongozi wa Mahakama.

Amesema, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka wazi mamlaka ya Mahakama kama Mhimili huru wenye jukumu la kutafsiri sheria na kusimamia utoaji haki kwa usawa kwa wananchi wote.

“Kazi ya uamuzi si kazi ya kawaida; ni kazi inayogusa maisha ya watu moja kwa moja. Katiba imeweka mamlaka huru ya Mahakama kutafsiri sheria, hivyo kila uamuzi unaofanya unapaswa kuzingatia haki, sheria na maslahi mapana ya taifa,” amesema Mhe. Tiganga.

Mhe. Tiganga ameongeza kuwa, pamoja na kuongozwa na sheria, mtumishi wa Mahakama anapaswa kuwa na uadilifu, hofu ya Mungu na kujiepusha na tamaa zinazoweza kuathiri utoaji haki.

“Hii ni kazi ya Kimungu. Fedha isikuharibu wala tamaa isikupoteze, unapaswa kuwa na hofu ya Mungu kwa sababu wakati mwingine maamuzi yako yanaweza kubadili maisha ya mtu milele,” amesema.

Sambamba na hilo, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano, nidhamu ya kiutumishi na kuheshimu mamlaka ndani ya Taasisi ya Mahakama, huku akibainisha kuwa, hata wale walio na umri mdogo lakini wakabeba dhamana za kiuongozi wanastahili kupewa heshima inayostahili.

“Mahakama inajengwa kwa ushirikiano. Waheshimu wenzako, shirikiana nao na jifunze kila siku. Maarifa yapo mengi, hata kupitia Katiba, miongozo na hotuba mbalimbali zinazopatikana katika tovuti za Mahakama,” amesisitiza.

Uapisho wa Mhe. Rose Baltazar Ngero unaongeza nguvu katika jitihada zinazoendelea za Mahakama ya Tanzania za kujenga mfumo wa utoaji haki ulio karibu zaidi na wananchi, wenye ufanisi, unaozingatia maadili na unaoendelea kujenga imani ya umma kwa mhimili wa Mahakama. Kupitia watumishi wenye weledi, uadilifu na utayari wa kulitumikia taifa, Mahakama inaendelea kutekeleza wajibu wake wa msingi wa kusimamia haki na kulinda utawala wa sheria nchini.

Dhamira ya Mahakama ya Tanzania ni kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma za kimahakama mapema ipasavyo, kwa weledi na kwa kuzingatia misingi ya sheria, haki na usawa. Mahakama za Mwanzo zina nafasi muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini kwa kuwa ndizo ngazi za mwanzo zinazopokea na kusikiliza mashauri mengi yanayohusu maisha ya kila siku ya wananchi, hususan migogoro ya kifamilia, ardhi, mirathi na masuala mengine ya kijamii.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimuapisha Mhe. Rose Baltazar Ngero kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo leo tarehe 24 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mhe. Rose Baltazar Ngero akila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo leo tarehe 24 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mhe. Rose Baltazar Ngero akisaini hati ya kiapo mara baada ya kuapa kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo leo tarehe 24 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Viongozi mbalimbali wa Mahakama walioshiriki hafla fupi ya uapisho wa Hakimu Mkazi mpya wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Rose Baltazar Ngero aliyeapishwa leo na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza jambo baada ya kumuapisha Mhe. Rose Baltazar Ngero kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo leo tarehe 24 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa wasia kwa Mhe. Rose Baltazar Ngero, Hakimu Mkazi mpya wa Mahakama ya Mwanzo aliyeapishwa leo tarehe 24 Juni, 2026 na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga akitoa neno kwa Mhe. Rose Baltazar Ngero, Hakimu Mkazi mpya wa Mahakama ya Mwanzo aliyeapishwa leo tarehe 24 Juni, 2026 na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mkazi mpya wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Rose Baltazar Ngero (aliyesimama) aliyeapishwa leo tarehe 24 Juni, 2026 na Jaji Mkuu. Kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika hafla ya uapisho wa Hakimu Mkazi mpya aliyeapishwa leo tarehe 24 Juni, 2026 na Jaji Mkuu. Kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Naibu Wasajili wa Mahakama walioshiriki katika hafla ya uapisho wa Hakimu Mkazi mpya aliyeapishwa leo tarehe 24 Juni, 2026 na Jaji Mkuu. Kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)











 

CHAMA CHA MAJAJI NA MAHAKIMU MKOANI SONGWE CHAKUTANA

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe

Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Mkoa Songwe wamefanya kikao cha kutathmini utendaji kazi pamoja na kukuza malezi ya kitaaluma, kubadilishana uzoefu na kuwakaribisha wananchama wapya, kikao kazi hicho kilifanyika katika ukumbi wa Simple Palace uliopo mji wa Vwawa wilayani Mbozi.

Katika kikao hicho, Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele alimkaribisha Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata ambaye alitambulishwa kama mlezi wa Chama cha TMJA Mkoa wa Songwe kwani Katiba ya TMJA inamtambua Jaji Mfawidhi kama mlezi wa matawi yote yaliyo chini ya Masjala husika.

Sambamba na hilo, Mwenyekiti huyo alimkaribisha Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde pamoja na wanachama wengine wapya TMJA Mkoa wa Songwe.

Akiwasilisha taarifa ya Chama ya mwaka 2025/2026 Naibu Katibu wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Ian Mnyigumba alisema Chama kilifanikiwa kufanya safari za kitalii katika maporomoko ya Kalambo Mkoa wa Rukwa na Beach ya Kasanga na baada ya safari hizo walifanikiwa kuchagua viongozi wa TMJA Mkoa wa Songwe.

Aidha, Chama kilifanikiwa kutoa elimu kwa shule za Msingi na Sekondari zikiwemo, Shule ya Msingi Nungwi iliyopo Wilaya ya Mbozi na Shule ya Sekondari Tunduma iliyopo Halmashauri ya Mji wa Tunduma.

Vilevile, wanachama wa TMJA Mkoa Songwe walishiriki kutoa Elimu ya usuluhishi wakati wa wiki ya suluhishi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Songwe.

Mnamo Juni, 2025 TMJA Mkoa wa Songwe walishiriki mafunzo ya utafiti wa Sheria “Legal Research” chini ya aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga, sambamba na hayo wanachama walifanikiwa kufanya bonanza la michezo mbali mbali ikiwemo drafti na karata.

Vilevile, Chama cha TMJA Mkoa wa Songwe kilifanya matendo ya huruma ikiwa ni pamoja na kutembelea Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma na kutoa misaada mbali mbali kwa wagonjwa, Pia waliweza kutoa misaada kwa mahabusu na wafungwa katika baadhi ya magereza yaliyopo Mkoa wa Songwe.

Kuhusu ada ya uanachama Naibu Katibu Mhe. Ian Mnyigumba alisema kuwa, michango hiyo hutumika kuendesha Chama cha TMJA Mkoa wa Songwe ikiwa ni pamoja na kufarijiana pale mwanachama anapougua, anapofiwa, anapouguliwa na kupongezana katika nyakati za furaha, aliendelea kusema kuwa ada ya uanachama hutumika pia kama mtaji wa kuendesha miradi mbalimbali ya Chama kama vile kutengeneza T-shirt, Kofia na Vikombe.

Mhe. Mnyigumba alisisitiza kuwa, wateja wakubwa wa miradi hiyo yote ni wanachama wa TJMA Mkoa wa Songwe, pia alihimiza wanachama kuendelea kununua bidhaa zinazotokana na miradi hiyo ili kukuza mfuko wa chama hicho.

Aidha, kuhusu idadi ya wanachama Mhe. Mnyigumba alisema kuwa, TMJA Mkoa wa Songwe ina jumla ya wanachama 32 wakiwemo Majaji wawili, Naibu Msajili na Mahakimu wa ngazi mbali mbali.

Katibu wa chama TMJA Songwe alimuomba mlezi wa chama hicho awasaidie katika kuhimiza wanachama kulipa ada zao kwa wakati kwasababu ada ya uanachama ndio mapato pekee na pia ni mtaji wa kuendesha miradi mbalimbali ya Chama.

Akielezea kuhusu mafanikio ya ubunifu wa miradi wa chama cha TMJA Mkoa wa Songwe walifanikiwa kupata tuzo ya ubunifu bora wa miradi kutoka TJMA Taifa kwenye mkutano uliofanyika Dodoma mwezi Junuari, 2025.

Akiwasilisha taarifa ya fedha na miradi mweka hazina wa chama TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Martha Malima alisema kuwa, ada za uanachama ziliwezesha miradi ya T-shirt, Kofia, Vikombe na Badge vyote vikiwa na nembo za TMJA.

Mhazini wa Chama alisoma gharama na faida walizozipata kutokana na  miradi hiyo, pia alitaja bidhaa zilizosalia na wanachama kwa pamoja walikubaliana kuzitoa baadhi ya bidhaa kama zawadi kwa mlezi wa Chama ambaye ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Songwe, Mhe. Gabriel Pascal Malata, Jaji wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde.

Mhe. Martha Malima mhazini wa Chama TMJA Mkoa wa Songwe alikabidhi tuzo ya ubunifu bora wa miradi waliyoipata mwezi Januari, 2025 kwa mlezi wa chama TMJA Songwe.

Kwa upande mwingine wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe kupitia kikao hicho waliridhia kufanya marekebisho ya katiba kutokana na mapungufu waliyoyabaini kwenye katiba iliyopo. Wanachama walimchagua Mhe. Raymond Kaswaga kama mjumbe wa kamati ya maboresho ya katiba ya chama cha TMJA Mkoa wa Songwe na kila Wilaya ilichagua mjumbe mmoja ili kukusanya maoni ya katiba mpya.

Wajumbe kwa pamoja walikubaliana kuwa, mapendekezo hayo yatawasilishwa meza kuu mwezi Agosti 2026, wajumbe wataamua kama wameyakubali mabadiliko hayo ili mabadiliko ya katiba yaweze kwenda sanjari na hali ya sasa.

Mwenyekiti wa TMJA Mhe. Magreth Kannonyele na Mhe. Abubakar Mrisha aliwashauri wajumbe waliochaguliwa kuisoma vyema na kuielewa vizuri katiba iliyopo kabla ya kuanza zoezi la ukusanyaji wa maoni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata alitoa elimu kuhusu Applicability of Electronic Evidence in Primary Court, aliwasisitiza wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe kuendana na teknolojia kwasababu Mahakama Kuu ya Tanzania imeruhusu electronic evidence kutumika mahakamani, ambapo kwa mara ya kwanza Commercial Court ilikubali matumizi ya electronic evidence na sasa imeruhusiwa pia kutumika katika Mahakama za Mwanzo.

“Sisi kama kama Mahakimu na Majaji tunalazimika kusoma na kuielewa vilivyo sheria ya kimtandao Electronic Transaction Act ya 2015 ili itusaidie katika kufanya maamuzi sahihi ya mashauri ya aina hiyo,” alisisitiza Mhe. Malata.

Mhe. Malata aliwashauri wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe watambue kuwa, kwa sasa Songwe imepewa mamlaka kamili hivyo ni wajibu wa kila mmoja kutimiza majukumu yake ipasavyo.

Kwa upande wa Chama, Mhe. Malata alisisitiza kuwa, kila mwanachama ana wajibu wa kutekeleza majukumu ya chama ikiwa ni pamoja na kulipa ada za uanachama kwa wakati, kushiriki kikamilifu shughuli zote za chama na kununua bidhaa za chama ili kuboresha mfuko wa chama.

Wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe, Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kanonyele (katikati), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kushoto), Jaji wa Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha ( wa pili kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kikao hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (kushoto) na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha wakiteta jambo wakiwa kwenye kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe.


Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele (kushoto) mara baada ya kukabidhi tuzo ya ubunifu bora wa miradi kwa mlezi wa TMJA Mkoa wa Songwe ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata.

Sehemu ya wanachama waliohudhuria kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe.

Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele akipeana mkono  na Jaji wa Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha wakati wa kumkabidhi zawadi.

Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele (kushoto) akimkabidhi zawadi Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde (kulia).

Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele (aliyesimama) akifafanua jambo kwenye kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi akiwa katika kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe akifuatilia mawasilisho. 


Viongozi wa TMJA Mkoa wa Songwe wakiongozwa na Mwenyekiti Mhe. Magreth Kannonyele (wa pili kushoto), Makamu Mwenyekiti Mhe. Machumu G. Pamba (katikati), Mhazini wa Chama Mhe. Martha Malima (wa pili kulia), Mwakilishi TMJA Taifa Mhe. Linah Okello (wa kwanza kulia), na Kaimu Katibu wa chama Mhe. Ian Mnyigumba (wa kwanza kushoto)wakiwa kwenye kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




Jumanne, 23 Juni 2026

MAHAKAMA IENDANE NA KASI YA KUKUA KWA UCHUMI: JAJI KIONGOZI

  • Ataka huduma kutolewa kwa haraka

Na FAUSTINE KAPAMA na Noel Daud-Mahakama, Songea

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewahimiza Watumishi wa Mahakama ya Tanzania kwenda na kasi ya maendelea na kukua kwa shughuli za kiuchumi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mhe. Dkt. Siyani ametoa wito huo leo tarehe 23 Juni, 2026 mjini Mbinga, alipokuwa anazungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga katika siku ya pili ya ziara yake ya kimahakama, kukagua Mahakama na Magereza mkoani Ruvuma.

“Shughuli za kiuchumi zinapokuwa kubwa kama kwenye Mji wa Mbinga, mashauri kama ya mirathi, ardhi ambayo ni mengi, shughuli za kibiashara na mikataba, yatakuja mahakamani. Mahakama lazima iendane na kasi hiyo ya kukua kwa uchumi,” amesema.

Amewaambia Watumishi hao kuwa ili kuendana na kasi ya maendeleo ambayo Wananchi wanajifanyia na Serikali inawezesha, kuna mambo ambayo uongozi wa Mahakama unaweza kufanya kama kuboresha maslahi na miundombinu, hivyo wao kama watoa huduma hawatakiwi kuachwa nyuma.

“Kwa hiyo, ni waombe inapowezekana, sisi tutagulie. Siyo tu tuende na kasi ya kukua kwa uchumi na shughuli za watu, ikiwezekana sisi tutangulie mbele, tusiwe tunafukuza maendeleo,” Jaji Kiongozi amesema.

Amesisitiza kuwa Mahakama inatakiwa kuwa kinara wa kuonesha njia, ili watu wakifika mahakamani waone, pamoja na uchakavu wa miundombinu iliyopo, wasiwakute Watumishi wakiwa wanyonge, bali wapate huduma na waondoke wakiwa wameridhika.

“Huduma zitolewe haraka, mashauri yasichukue muda mrefu mahakamani, kwa kadri inanyowezekana tutoe haki mapema na tuweke mazingira ya kuwa na wepesi wa kupatikana huduma zenyewe,” Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Aidha, Jaji Kiongozi amewataka Watumishi wa Mahakama kutokuwa kikwazo kwa watu kuja mahakamani na pia wanapaswa kujiuliza ni kwa namna gani kila mmoja anapokea Wananchi wanaokuja mahakamani na jinsi gani anavyotoa huduma bila kuwa na upendeleo.

Amebainisha kuwa Watumishi wa Mahakama wanapaswa kutambua kuwa wao ni sehemu ya Mahakama, kwani wakitoa huduma vizuri Mahakama na wao binafsi watapata sifa, tofauti na hivyo Mahakama itachafuka.

“Kila Mtumishi anatakiwa kujua kuwa anao mchango anaopaswa kuutoa ili kuboresha huduma za Mahakama na hivyo kujenga imani ya umma kwa Mahakama. Msipofanya hivyo, watu hawatawaheshimu na Mahakama haitapewa hadhi inayostahiki,” amesisitiza.

Akizungumzia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Jaji Kiongozi amewaeleza Watumishi hao kuwa pamoja na ugumu wa miundombinu na mazingira yaliyopo, Mahakama haiwezi kurudi nyuma.

Mhe. Dkt. Siyani amewapongeza Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga kwa kazi nzuri wanaoifanya, kwani taarifa ya utendaji iliyowasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Lome Mwapemela, imeonesha kutokuwa na mlundikano wa mashauri na Wananchi wa Mbinga wanaendelea kupata huduma za haki.

Kwenye taarifa yake, Mhe. Mwapemela ameeleza kuwa mashauri yaliyobaki Desemba, 2025 katika ngazi ya Mahakama ya Wilaya yalikuwa 30, yaliyofunguliwa kati ya Januari 2026 hadi Juni 19, 2026, yalikuwa 77 na yaliyoamuriwa kwa kipindi hicho ni 84.

Kwa mujibu wa taaarifa hiyo, hapakuwepo na mashauri yaliyovuka mwaka 2025 katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo na mashauri yaliyofunguliwa kati ya Januari na Juni 19, 2026 yalikuwa 425 na yaliyoamuriwa ni 376.

Hakimu Mfawidhi ameeleza pia kuwa, kwa kipindi cha Januari hadi Juni 19, 2026, mashauri ya mirathi sita yamefungwa kati ya mashauri 14 ambayo uteuzi wa msimamizi wa mirathi umefanyika. Amebanisha kuwa kati ya mashauri hayo, mawili ni ya Mahakama za Mwanzo na mashauri nne ni Mahakama ya Wilaya.

“Mashauri ambayo hayajafungwa bado Wasimamizi wapo ndani ya muda wa kutekeleza majukumu yao. Tumekuwa tukichukua namba za simu za Msimamizi wa Mirathi na za watu wao wa karibu ili kuhakikisha wanapatikana baada ya kuteuliwa,” ameeleza.

Katika siku hiyo ya pili ya ziara yake, Jaji Kiongozi pia ametembelea Magereza mawili ya Mkwaya na Kitai, yote yakiwa katika Wilaya ya Mbinga. Akiwa kwenye Magereza hayo, Jaji Kiongozi amepokea changamoto mbalimbali za Wafungwa, ambazo amezipatia ufunguzi papo kwa papo.

Aidha, Jaji Kiongozi ametumia fursa hiyo kuwaomba Wafungwa watakaobahatika kutoka wawe raia wema, kwani kukaa kwao gerezni hakuna faida kwa nchi.

Katika ziara hiyo, Jaji Kiongozi ameambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya ya Nyasa na Mbinga Songea na Watumishi wengine wa Mahakama Songea.

Kesho tarehe 24 Juni, 2026, Jaji kiongozi anatarajia kuendelea na ziara yake kwa kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mhe. Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, na baadaye kufanya ukaguzi katika Gereza Kuu Songea na kisha kutembelea Mahakama Kuu Songea na kuongea na Watumishi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga (hawapo kwenye picha.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga, Mhe. Lome Mwapemela, akiwasilisha taarifa ya utendaji wakati wa kikao hicho.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele, akitoa utambulisho wa Viongozi mbalimbali wakati wa kikao hicho. 

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama kutoka Makao Makuu Dodoma (juu) na Viongozi kutoka Mahakama Kuu Songea (picha chini) wakiwa kwenye kikao hicho.


Sehemu ya Watumishi wa Mahakama (juu na chini) ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi. Picha chini ni sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu nyingine ya Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbinga (juu na chini).


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akipokea salamu baada ya kuwasili kwenye Gereza la Kilimo Kitai. Picha chini ni sehemu ya Maofisa Magereza, Wadau na Watumishi baaada ya ukaguzi wa Gereza hilo kufanyika.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwasili kwenye Gereza la Mkwaya kufanya ukaguzi na kuzungumza na Wafungwa.