- Wasisitizwa pia kuzingatia matumizi ya Teknolojia na kujiendeleza kielimu
Na MICHAEL RITTE, Mahakama-Bukoba
Watumishi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wamehimizwa kuendelea kuboresha huduma kwa wateja, kutumia lugha nzuri
wanapohudumia wananchi pamoja na kujiendeleza kielimu ili kwenda sambamba na
kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani.
Wito huo umetolewa
na Viongozi kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania wakati
wa kikao cha utoaji wa elimu ya huduma kwa wateja kilichofanyika tarehe
26 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba.
Kikao hicho cha
mafunzo na majadiliano kililenga kuwakumbusha watumishi umuhimu wa huduma bora
kwa wananchi pamoja na matumizi sahihi ya mifumo ya kisasa ya utoaji huduma.
Akizungumza katika
kikao hicho, Mmoja kati ya Viongozi kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Aloyce
Katemana alisema, “Mahakama ya Tanzania imeendelea kuboresha mifumo yake
ya huduma kwa wananchi kupitia Kituo cha Huduma kwa Wateja kinachopatikana
kupitia namba maalum ya bure 0800 750 247 inayofanya kazi saa 24 kwa siku, siku
saba kwa wiki mwaka mzima.”
Aliendelea kueleza kuwa, Kituo hicho
kimeboreshwa kwa kutumia mfumo wa kisasa wa IVR (Interactive Voice Response) unaomuwezesha mwananchi kupata
maelekezo ya awali kwa njia ya simu, sambamba na matumizi ya WhatsApp ambayo
sasa yana uwezo wa kutoa baadhi ya majibu ya awali automatiki.
“Lengo letu ni
kuhakikisha mwananchi hapati shida ya kusafiri umbali mrefu kufuatilia
malalamiko, maoni, pongezi au maulizo yake. Tunataka huduma ziwe rahisi
kufikika kwa kila mtu,” alisema Mhe. Katemana.
Aidha, alibainisha
kuwa Kituo cha Huduma kwa Mteja kiko chini ya Idara ya Ukaguzi wa Mahakama,
Mrejesho kwa Umma na Maadili, ambapo kwa sasa mrejesho kutoka kwa wananchi
unahusisha maeneo manne ambayo ni maulizo,
maoni, pongezi na malalamiko.
Kwa upande wake, Kiongozi
wa Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania, Dkt. Evetha Mboya
ambaye alikuwa Muelimishaji katika kikao
hicho, alisema huduma bora huanzia mapokezi ya kwanza kabisa kwa mteja, huku
akisisitiza kuwa hata namna mteja anavyopokelewa getini inaweza kujenga au
kuharibu taswira ya Mahakama mbele ya wananchi.
Aliwapongeza
watumishi wa Mahakama Bukoba kwa mapokezi mazuri waliyoyatoa kwao, lakini pia aliwakumbusha
kuwa, bado kuna baadhi ya malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu ucheleweshaji
wa huduma na namna ya mawasiliano wanayopata kutoka kwa baadhi ya watumishi.
Alisisitiza kwa kusema kuwa, “Mteja anapokuja mahakamani mara nyingi tayari ana
changamoto zake. Wengine wanakuwa wamechoka, wamekasirika au wana mawazo mengi,
hivyo jukumu letu ni kumtuliza na kumfanya aone kuwa amesikilizwa.”
Katika mafunzo
hayo, Dkt
Evetha aliwahizimiza watumishi kutumia
lugha ya heshima kwa wananchi, kuwa wasikivu pamoja na kutoa maelezo kwa
utulivu hata kwa wateja wanaoonekana kuwa wagumu au wenye hasira.
Pia alikumbusha
umuhimu wa kuzingatia sera ya (Open Door Policy) inayosisitiza uwazi na
upatikanaji wa Viongozi au Watumishi kwa wananchi pale inapowezekana, ili
kuepusha hisia za kunyimwa haki au kubezwa.
Sambamba na hilo, Viongozi
hao
kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja walionya dhidi ya vitendo vya rushwa ndogondogo
vinavyoweza kujitokeza katika utoaji wa huduma, wakisema mazingira yoyote
yanayoweza kumfanya mwananchi ahisi analazimika kutoa fedha ili kupata huduma
hayapaswi kuvumiliwa.
Katika kuelezea
vigezo vya huduma bora kwa mteja, Mkufunzi
alitaja maeneo muhimu yakiwemo kujenga imani kwa wateja (assurance), kutoa huduma kwa haraka (responsiveness), muonekano mzuri wa watumishi na mazingira ya kazi (tangibility), kujali hali ya mteja (empathy), pamoja na kuhakikisha huduma
zinakuwa za kuaminika wakati wote (reliability).
Mafunzo hayo pia
yaligusia umuhimu wa watumishi kujiendeleza kielimu kutokana na kasi ya
maendeleo ya teknolojia, ikiwemo matumizi ya mifumo ya kidijitali, (biometric)
na Akili Unde (Artificial Intelligence) katika taasisi mbalimbali.
“Dunia inabadilika
sana, kama hatutaongeza ujuzi wetu, ipo siku mifumo itabadilika na tukajikuta
tumebaki nyuma,” alieleza Dkt Evetha.
Kwa upande wake,
Mhe. Hamza Marishi aliwasihi watumishi kuifahamu vizuri Taasisi yao pamoja na nyaraka
muhimu za Mahakama ya Tanzania ikiwemo Mpango Mkakati wa Mahakama na Mkataba wa
Huduma kwa Mteja.
Alisema nyaraka
hizo zinaeleza wajibu wa watumishi kwa wananchi pamoja na haki za wateja kupata
huduma bora, uwazi na ushirikishwaji.
Katika mjadala wa
wazi, baadhi ya watumishi walieleza changamoto wanazokutana nazo katika
kujiendeleza kielimu, hususan ucheleweshaji wa malipo ya ufadhili kwa watumishi
wanaopata nafasi za masomo.
Baadhi yao
waliomba Mahakama kuweka mfumo bora wa mawasiliano kati ya Mwajiri na Vyuo ili
wanafunzi wanaodhaminiwa wasipate usumbufu wanapowasili vyuoni.
Mmoja wa washiriki
ambaye ni Mlinzi alisema amenufaika na ufadhili wa Mwajiri kwa kupata nafasi ya
kusoma katika Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) lakini akaomba nafasi zaidi za
kujiendeleza zitolewe kwa Kada mbalimbali kutokana na mabadiliko ya teknolojia
na mifumo ya kazi.
Kikao hicho kilihitimishwa kwa watumishi kuaswa kuendelea kulinda taswira ya Mahakama ya Tanzania kwa kutoa huduma bora, kuwa waadilifu, kutumia teknolojia vizuri na kuendelea kujifunza ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
Picha ya pamoja. Kuanzia Kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Bw. Edward Mbara, wa pili kushotp ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe Said Mkasiwa, katikati ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzani, Mhe. Aloyce Katemana ambaye ni Mkufunzi katika kikao hicho, wa pili kulia ni Dkt. Evetha Mboya Kiongozi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja ambaye pia alikuwa Mkufunzi wa Kikao cha utoaji elimu kutoka Kituo hicho na wa kwanza kulia ni Bi. Monica Kalokola, Ofisa Utumishi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wakiwa katika ufunguzi wa kikao hicho na utambulishaji wa watumishi waliohudhuria.
Dkt. Evetha Mboya (aliyesimama) akitoa elimu ya utoaji wa huduma bora kwa wateja kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Bukoba. Walioketi katikati ni Bi Monica Kalokola, Ofisa Utumishi Mahakama Kuu Bukoba na kulia Bw. Rojas Rwanyumba, Ofisa Tawala Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Bukoba na nyuma yao ni baadhi ya watumishi wa Mahakama waliohudhuria wakisikiliza na kufuatilia kwa umakini mafunzo hayo.







































