Jumanne, 5 Mei 2026

JAJI NONGWA AHITIMISHA MICHEZO NJOMBE KWA WANA MAHAKAMA SPORTS

·        Mahakama Sports yashinda Makombe manne Njombe mashindano ya michezo Mei Mosi

·       Asisitiza umuhimu wa Michezo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amewasisitiza Wanamichezo wa Mahakama Sports na Watumishi wengine Mahakama juu ya umuhimu wa Michezo na kusema kuwa ina faida nyingi ikiwemo kulinda afya ya mwili, pia ni ajira, vilevile huleta furaha pamoja na ushirikiano.

 

Mhe. Nongwa aliyasema hayo hivi karibuni alipohudhuria hafla ya usiku ya kuhitimisha michezo Mkoani Njombe iliyofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya ‘Agreement’ mkoani Njombe.

 

Katika hafla hiyo, alikuwepo pia Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Martine Mushi, Makamu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Maria Mayalla na Wanamichezo wa Mahakama Sports.

 

Naye, Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Donald Tende aliwasilisha taarifa aliyoisoma mbele ya Mhe. Nongwa pamoja na Wanamichezo ambapo alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwalinda na kuwajaalia afya njema na kuwakinga na maradhi na majeraha mbalimbali wakati wote wa mashindano.

 

“Pili, naushukuru Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kutupatia ruhusa na uwezeshaji wa rasilimali fedha wa kutuwezesha kushiriki kikamilifu katika mashindano ya Mei Mosi, 2026,” alisema Bw. Tende.

 

Vilevile, aliwashukuru Wachezaji wa Mahakama Sports walioshiriki mazoezi na mashindano kwa kujituma na kujitoa kwao katika kipindi chote kwa manufaa ya Timu ya Mahakama ya Tanzania.

 

Katibu huyo wa Mahakama Sports aliendelea kusema kuwa, “Wafanyakazi wanaoshiriki michezo ni kundi mojawapo la wafanyakazi wanaotegemewa na Taifa kiuchumi, kijamii na huduma mbalimbali kwa umma.” 

Bw. Tende aliongeza kuwa, Timu ya Michezo ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ilishiriki kikamilifu katika Mashindano ya Mei mosi yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe kuanzia tarehe 13 Aprili, 2026 hadi 01 Mei, 2026.

Alisema kuwa, Mashindano hayo yalifunguliwa rasmi tarehe 20 Aprili, 2022 na Mgeni Rasmi aliyekuwa Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo.

 Mashindano ya Mei Mosi yamelenga kusherehesha Sikukuu ya Wafanyakazi ili kuboresha mahusiano baina ya watumishi wa umma,  kutoka Wizara, Mashirika, Taasisi na Idara mbalimbali za Serikali, pamoja na jamii lengo likiwa ni kuboresha na kulinda afya za watumishi na kuimarisha nguvu kazi katika utumishi wa umma. 

Bw. Tende alibainisha kupitia taarifa yake kuwa katika michezo hiyo jumla ya Wizara, Idara, Taasisi za Umma, Mashirika ya Umma 61   walishiriki mashindano hayo ikiwemo Mahakama ya Tanzania.

Alieleza kuwa, Timu ya Mahakama ilijumuisha washiriki 84 na Timu ya ‘Mahakama Sports Club’ ilishiriki jumla ya michezo saba ambapo  iliweza kunyakua jumla ya Makombe manne ambayo ni Kamba mshindi wa tatu, Karata mshindi wa kwanza, Baiskeli mshindi wa pili na Mchezo wa Bao ni mshindi wa pili.

Wanamichezo wa Mahakama Sports ni watumishi kutoka katika Mahakama mbalimbali zilizopo nchini Tanzania ambapo wanamichezo hao wamejikita katika michezo  kama vile Mpira wa Miguu, Netiboli, Kamba Wanawake, Kamba Wanaume, Riadha, Kurusha Tufe, Drafti Karata, Baiskeli na Bao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wana Mahakama Sports. Wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, wa pili kushoto ni  Mwenyekiti wa Michezo Mahakama Sports, Mhe. Martine Mushi, wa kwanza kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Maria Mayalla na wa kwanza kushoto ni Katibu wa Michezo Mahakama Sports, Bw. Robert  Tende. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (aliyesimama) akizungumza na Wana Mahakama Sports kuhusu umuhimu wa michezo na kutoa hongera kwa wana michezo hao. Kushoto ni Mwenyekiti wa Michezo wa Mahakama Sports Mhe. Martine Mushi.

Katibu wa Mahakama Sports Club,  Bw. Robert  Tende akisoma taarifa ya michezo tangu walipoanza mpaka walipomaliza na mashindano ya michezo ya Mei Mosi, 2026.



Sehemu ya wageni waalikwa na wanamichezo waliohudhuria kwenye hafla hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

 

 

 

 

 

 

 


ENDELEZENI UZALENDO KATIKA UTENDAJI KAZI WENU; JAJI MSTAAFU, MHE. DKT. STEVEN BWANA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana ametoa rai kwa watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma kufanya kazi kwa uzalendo ili kujenga Mahakama yenye sifa njema katika Taifa lenye umoja na uzalendo wa kweli katika utumishi wa umma.

Akizungumza katika kikao kifupi na watumishi wa Mahakama hiyo jana tarehe 04 Mei, 2026 alipotembelea Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Bwana alisema, “Nimeambiwa mnafanya vizuri Kigoma, ni rai yangu kwenu kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, uzalendo wa kweli kwa Taifa na bila kuangalia utapata nini kesho, maana kazi zako zitakupa kukua, kuaminiwa na kutengeneza nafasi kubwa zaidi katika utumishi wenu.”

Jaji Mstaafu huyo amewaeleza watumishi hao kukumbuka kuwa shughuli zao za kila siku ndio msingi na kichocheo cha maendeleo ya Taifa na kusisitiza kuwa, “Wastaafu tulifanya sehemu yetu, ambapo teknolojia katika Mahakama kipindi hicho ilikuwa kidogo sana lakini tulifanya kwa uzalendo na kujituma na shughuli za kusikiliza mashauri na utawala zilifanyika vema.”

Aidha, Mhe. Dkt. Bwana alisema kuwa, ni mara yake ya kwanza kufika mkoani Kigoma, hivyo ni vema kuacha alama ya zawadi ya kitabu chake kiitwacho, ‘Maisha yangu, Utumishi wangu” chenye Tawasifu yake, ili kiwekwe kwenye Maktaba ya Mahakama hiyo hatimaye watumishi waweze kusoma maudhui ya kitabu hicho na kuongeza weledi wa kizalendo katika eneo la maisha ya utumishi wa umma.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile alipata wasaa wa kumzungumzia walau kwa kifupi Jaji Mstaafu, Mhe. Dkt. Steven Bwana kupitia kitabu chake kuwa ni moja ya Majaji wa Rufani ambaye alihudumu kwa weledi, kujituma kwa uzalendo mkubwa wakati wa kipindi chake, hivyo kufika kwake Kigoma ni jambo la muhimu na kuigwa na watumishi wa sasa hasa kwa umakini wake na utumishi uliotukuka katika kuwahudumia wananchi katika nafasi mbalimbali alizowahi kuaminiwa na Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, alitoa neno la shukrani kwa Jaji Mstaafu, Mhe. Dkt. Bwana aliyeambatana na Mkewe kutembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Aidha, Mhe. Mbelwa alimuomba Jaji huyo kupanda mti ili kuacha alama ya ujio wake wa kutembea kituo hicho, hata hivyo Jaji Mstaafu huyo aliridhia kupanda mti kama kumbukumbu ya ujio wake Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kulia) akimkabidhi Kitabu cha wasifu wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Karichuba Rwizile wakati Jaji Mstaafu huyo alipotembelea Mahakama Kuu Kigoma jana tarehe 04 Mei, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile akisoma Kitabu alichokabidhiwa na Jaji msatafu wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dr. Steven Bwana kwa ajili ya watumishi kusoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile (katikati) akimkaribisha Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kulia) alipowasili katika viunga vya Mahakama Kuu Kigoma jana tarehe 04 Mei, 2026. Aliyesimama kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Steven Bwana (hayupo katika picha), na mkewe kwa niaba ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana, na  Mkewe wakikata keki maalum ya upendo iliyoandaliwa kwa ajili yao walipotembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana akipanda mti katika eneo la mbele ya jengo la Mahakama Kuu Kigoma alipotembelea Mahakama hiyo jana tarehe 04 Mei, 2026.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na 
Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kushoto) na mkewe, Mama Steven Bwana.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

 

 

 

JAJI MFAWIDHI SINGIDA ASISITIZA WATUMISHI KUIISHI KWA VITENDO SALAMU YA MAHAKAMA

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda amewasisitiza watumishi kuiishi salamu ya Mahakama ya Tanzania isemayo ‘Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji.’

Mhe. Mwenda amewasisitiza watumishi hao hivi karibuni akiwa katika ziara yake ya kwanza ya ukaguzi iliyofanyika kuanzia tarehe 28 Aprili 2026 hadi 30 Aprili 2026 katika Wilaya za Iramba, Manyoni na Singida Mjini.

Katika ziara hiyo aliwakumbusha watumishi kuwa kazi ya kutoa haki sio jambo dogo hivyo watumishi wasijiingize katika vitendo viovu ambapo alisema, “ndugu watumishi nasisitiza kuwa waadilifu kwa kuwa ndio msingi mkubwa wa kutoa haki hivyo, muwe na tabia njema kazini na nje ya kazi.”

Aidha, Jaji Mwenda aliwapongeza watumishi wote kwa ujumla kwa kazi nzuri inayofanyika hususan ya usikilizwaji wa mashauri kwani katika taarifa zote zilizowasilishwa mashauri yote yanayofunguliwa yanaisha kwa wakati.

Kadhalika, amesisitiza kila mmoja kufanya kazi kwa bidii na kwamba asitokee mtu wa kumkwamisha mwingine, kuheshimiana, kufanya kazi kwa umoja na kufanya majukumu zaidi ya mengine pasipo kuangalia kada ili kuongeza ufanisi. Vilevile aliwashauri watumishi kuongeza maarifa kwa kujibidiisha kwenye mafunzo mbalimbali ili kuimarisha taaluma.

Katika ukaguzi huo alitembelea pia Gereza la Wilaya Manyoni na kujionea hali halisi na alipongeza ushirikiano uliopo kati ya Mahakama na Wadau wa Haki Jinai kwani katika Gereza hilo hakukuwa na msongamano wa Mahabusu hivyo akasisitiza kuendeleza ushirikiano huo ili kuhakikisha Magereza yanakuwa na nafasi ili yaweze kujiendesha.

Katika ziara hiyo, Viongozi walipanda miti ya matunda kusisitiza utunzwaji wa mazingira katika maeneo yote ya Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Iramba (waliosimama). Wa pili kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi, wa pili kulia ni Mtendaji Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Bw. Filbert Matotay, wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi- Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe.Allu Nzowa na wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Iramba, Mhe.Luzango Khamsini.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Manyoni, Mhe.Alisile Mwankejela (aliyesimama) akiwasilisha taarifa fupi ya utekelezaji mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyeketi mbele katikati) wakati alipofanya ziara ya kikazi. Aliyeketi kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi na kulia ni Mtendaji Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Bw. Filbert Matotay.

 Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akiwa na wadau wa Haki Jinai alipotembelea Gereza la Wilaya Manyoni.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akipanda mti wa Matunda katika Mahakama ya Wilaya Manyoni.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi akipanda mtu wa matunda Mahakama ya Wilaya Manyoni.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Bw.Filbert Matotay akipanda mti wa matunda Mahakama ya Wilaya Manyoni.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

TMJA MOROGORO YAADHIMISHA SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI KWA MAFUNZO

  • Yafanya pia uchaguzi wa Viongozi

Na ASHA JUMA-Mahakama Morogoro

Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Mkoa wa Morogoro hivi karibuni kiliungana na Wafanyakazi wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani inayofanyika kila mwaka tarehe 1 Mei, kwa kufanya mkutano maalum uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Kongamoyo mkoani Morogoro.

Maadhimisho hayo yalilenga kuwakutanisha pamoja Majaji na Mahakimu kwa ajili ya kusherehekea siku hiyo muhimu kwa  kubadilishana uzoefu, pamoja na kujengeana uwezo kupitia mafunzo mbalimbali ya kitaaluma yanayohusu utendaji kazi wa Mhimili wa Mahakama.

Miongoni mwa mada zilizotolewa ni Muhtasari wa Utamaduni wa Mahakama (Judicial Culture) nchini Tanzania, ambapo washiriki walipata fursa ya kujifunza kuhusu misingi, maadili, mila na taratibu zinazoongoza utendaji kazi wa vyombo vya utoaji haki.

Ilielezwa kuwa utamaduni wa Mahakama unajengwa juu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sheria mbalimbali pamoja na kanuni na miongozo ya Mahakama.

Msingi huo ni muhimu katika kuhakikisha haki inatendeka kwa usawa na ufanisi. Mada hii iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga.

Aidha, mada nyingine iliyowasilishwa ni Muhtasari wa Sifa na Tabia Muhimu za Uongozi katika Mhimili wa Mahakama (Overview on Judicial Leadership Attributes), iliyolenga kuwajengea washiriki uelewa kuhusu sifa zinazopaswa kuzingatiwa na Viongozi wa Mahakama.

Baadhi ya sifa hizo ni pamoja na uadilifu, hekima na busara katika kufanya maamuzi, uwazi na uwajibikaji, uwezo wa kusimamia haki kwa usawa, pamoja na kuwa na uongozi wenye maadili na mfano bora kwa wengine. Mada hii ilitolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim.

Baada ya mafunzo hayo, wajumbe walipata nafasi ya kufanya uchaguzi wa Viongozi mbalimbali wa TMJA kwa Mkoa wa Morogoro. Katika uchaguzi huo, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Aisha Sinda, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti na Mhe. Mbaraka Mchopa akachaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti. Nafasi ya Katibu ilichukuliwa na Mhe. Joseph Ngwega, Mhe. David Luvanga akachaguliwa kuwa Mwakilishi wa Taifa, na Mhe. Latifa Kassim Mohammed kuchukua nafasi ya Mhazini.

Kwa ujumla, maadhimisho hayo yamekuwa na mafanikio makubwa kwa kuimarisha mshikamano miongoni mwa wanachama wa TMJA, kuongeza uelewa wa kitaaluma na kuweka msingi imara wa uongozi bora ndani ya Mhimili wa mahakama mkoani Morogoro.

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Aisha Sinda aliye chaguliwa kuwa Mwenyekiti TMJA Morogoro.

Mhe. Mbaraka Mchopa aliye chaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti.

Mhe. Joseph Ngwega  aliye chaguliwa kuwa Katibu.

Mhe. David Luvanga aliye chaguliwa kuwa Mwakilishi wa Taifa.

Mhe. Latifa Kassim Mohammed aliyechukua nafasi ya Mhazini.

Mahakimu pamoja na Majaji wakiwa katika viwanja vya Kongamoyo.

HABARI HII IMEHARIRIWA NA FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Jumatatu, 4 Mei 2026

LL.M. STUDENT ANIPHA ABASS MWINGIRA ATTENDS THE 70th SESSION OF THE UN COMMISSION ON THE STATUS OF WOMEN IN NEW YORK

Published: May 04, 2026

A woman in a black suit, white headscarf, and a blue, green, black "TANZANIA" scarf stands before a UN emblem and flag.
LL.M. student Anipha Abass Mwingira at the United Nations Headquarters in New York

Anipha Abass Mwingira, an LL.M. Student in the International Human Rights Law program at Notre Dame Law School, is from Tanzania and brings more than two decades of experience in the Judiciary and Human Rights Sectors. She recently attended the 70th Session of the UN Commission on the Status of Women at the United Nations Headquarters in New York. Bringing both the perspective of a seasoned Magistrate and a global Legal Scholar, she engaged in critical conversations on advancing gender equality through law and accountability. In this Q&A, she reflects on the insights she gained, the global connections she formed, and how the experience will shape her continued work championing women’s rights in Africa and beyond.

What drew you to attend the 70th Session of the UN Commission on the Status of Women? What were your expectations going into the experience?

As a woman Magistrate, I was drawn to attend this event for its timely focus on achieving gender equality and empowering all women and girls. This year's theme resonates deeply with my work and commitment to advancing women's rights in Africa. I expected to engage with global leaders, experts, and activists to share best practices, challenges, and innovative solutions for promoting gender equality. I was eager to learn about new strategies and frameworks that could enhance our work in Tanzania and contribute to the broader African context. I also expected to highlight the struggles women face and explore ways to address these challenges collectively.

Two women in headphones sit focused at a conference table. One wears a red jacket and black head covering, writing.

Were there any particular discussions, panels, or moments during the session that left a lasting impression on you? What made them stand out?

Yes, one that stood out was the emphasis on the ECOWAS Gender Barometer as a tool to hold State Parties accountable for their gender equality commitments. The discussion highlighted the importance of data-driven advocacy to drive policy changes and secure resources to address gender disparities. A panelist noted that the barometer would provide a clear snapshot of progress and gaps, enabling civil society and governments to work together more effectively. The launch underscored the need for regional cooperation and ECOWAS's role in promoting gender equality across member states. The commitment from ECOWAS officials to support the implementation of the barometer's recommendations was also a significant takeaway, suggesting a potential shift toward more transparent and accountable governance in the region.

How did your background in human rights and your perspective as an LL.M. student at Notre Dame Law School shape the way you engaged with the conversations at the event?

My background in human rights and my experience as an LL.M. student at Notre Dame Law School, particularly through the Global Human Rights Clinic, gave me a nuanced understanding of international frameworks and advocacy strategies, enabling me to engage critically with the discussions. The clinic's focus on the practical application of human rights law allowed me to contribute effectively. My studies at Notre Dame emphasized the importance of leveraging international law to drive national change, shaping my perspective on the role of regional tools, such as the Gender Barometer, in advancing gender equality.

Twelve smiling women in professional attire stand before a line of colorful national flags. Several wear sashes reading "Tanzania".

In what ways did attending the session deepen or challenge your understanding of global gender equality and the role of law in advancing it? What was your biggest takeaway?

Attending the session deepened my understanding of global gender equality by showing how regional tools, such as the ECOWAS Gender Barometer, can turn treaty commitments into measurable accountability. It challenged me to think beyond national frameworks and to view law not only as legislation but also as a mechanism for data-driven monitoring and cross-border advocacy. My biggest takeaway was that real progress on gender equality requires linking international legal obligations to concrete, region-specific accountability tools. As Magistrates and Lawyers, we have a direct role in making those tools effective on the ground.

How do you hope to carry and implement what you learned at the session into your future work in human rights or legal practice?

My experience at the ECOWAS Gender Barometer session, combined with my background as a Magistrate, Human Rights Lawyer, and LL.M. candidate at Notre Dame Law School, has deepened my understanding of women's rights through both judicial and justiciable lenses. Moving forward, I aim to amplify my advocacy beyond Tanzania to the broader African continent and globally. I'll leverage these insights to strengthen regional accountability mechanisms for women's rights; support data-driven advocacy using tools such as the Gender Barometer; collaborate with Judges, Lawyers, and Civil Society to make women's rights more justiciable; and expand my work with women's associations and human rights organizations. I'm committed to intensifying my efforts to promote women's rights and to ensure they receive the attention they deserve. The global stage is next.

WANA-TAWJA KANDA YA DAR ES SALAAM WAKUTANA KIGAMBONI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Kanda ya Dar es Salaam wamekutana kwa ajili ya kubadilishana mawazo na kufurahi kwa pamoja sambamba na kufanya uchaguzi wa Mratibu wa Chama hicho katika Kanda hiyo.

Hafla hiyo ilifanyika tarehe 01 Mei, 2026 katika Kijiji cha Mwasonga-Kigamboni jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mlezi wa TAWJA Kanda ya Dar es Salaam ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi alisema kwamba, TAWJA ni yao na hawawezi kuikwepa huku akinukuu maneno ya Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Sharmillah Sarwatt aliyeomba hafla hizo zifanyike mara mbili kwa mwaka na wajumbe waliridhia na hivyo akamuomba Mhe. Sarwatt awe Muandaaji Mkuu wa shughuli hizo.

Wakati wa mtoko huo, Mhe. Maghimbi alimteua Mhe. Zenas Tarimo kutoka Mahakama ya Mwanzo Ilala kuwa Mratibu wa sherehe zote za TAWJA na Mhe. Irene Maganga kutoka Mahakama ya Mwanzo Kimara kuwa Mratibu Msaidizi wa sherehe.

Akizungumza baada ya uteuzi huo, Mhe. Tarimo amewaomba WanaTAWJA wa Kanda ya Dar es Salaam kumuunga mkono ili kumuwezesha kufanya kazi hiyo maana bila mkono wa shirika yeye peke yake hataweza.

Naye Mratibu Msaidizi, Mhe. Irene Maganga amemshukuru Jaji Maghimbi  kwa kumteua kuwa Mratibu Msaidizi na kukiri kuwa amefurahi  japo hakuwahi kuwaza lakini ameahidi kumsaidia vema Mratibu Mkuu.

Katika hafla hiyo, kulikuwa na burudani mbalimbali na mashindano ya michezo ya karata, kucheza ngoma kuimba, kuogelea na kombolela ambapo washindi walipewa zawadi.

Hafla waliiita jina la “Sneakers & Jeans Day” ambapo wanachama waliohudhuria walivaa ‘jeans’ na raba.

Wana TAWJA wa Mkoa wa Dar es Salaam wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa hafla yao iliyofanyika tarehe 01 Mei, 2026 Kigamboni jijini Dar es Salaam.


 Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya Kanda ya Dar es Salaam wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mlezi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Salma Maghimbi wakati wa hafla ya Wanachama wa TAWJA Kanda ya Dar es Salaam iliyofanyika tarehe 01 Mei, 2026 Kigamboni jijini Dar es Salaam.

Wanachama cha Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mkoa wa Pwani wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa hafla iliyowakutanisha Wana-TAWJA Kanda ya Dar es Salaam tarehe 01 Mei, 2026.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam  na Mlezi wa TAWJA  Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwasili kwenye hafla ya Wanachama hao akiwa katika vazi maalum la siku hiyo 'Sneaker' na 'Jeans.' 

Sehemu ya Majaji Wanawake Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ambao ni Wanachama wa TAWJA wa Kanda hiyo. Katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Butamo Phillip, kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Monica Otaro na kushoto ni Jaji  wa Mahakama Kuu  ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe.Sharmila Sarwatt kwa pamoja wakiwasili katika eneo la tukio wakiwa katika mavazi rasmi ya siku hiyo.

Baadhi ya Wana TAWJA Mkoa wa Dar es Salaam wakicheza karata. 


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Modesta Opiyo (wa nne kushoto) akiwaongoza wana TAWJA kukata keki wakati wa hafla ya Wana-TAWJA Kanda ya Dar es Salaam iliyofanyika tarehe 01 Mei, 2026 Kigamboni jijini Dar es Salaam.

Kamati ya Maandalizi ya hafla ya TAWJA Mkoa wa Dar es Salaam wakiwa katika picha ya pamoja. Kushoto ni Mhe. Aziza Mbadjo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, katikati ni Mhe. Zenas Tarimo, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Ilala na kulia ni Mhe. Scola Odeyo. 

Keki maalum iliyoandaliwa kuashiria upendo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

Ijumaa, 1 Mei 2026

SERIKALI ITAENDELEA KUBORESHA MASLAHI, MAZINGIRA YA KAZI KWA WAFANYAKAZI; MHE. SENYAMULE

Na. INNOCENT KANSHA & JAMES BUSANYA - Mahakama

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma leo tarehe Mosi Mei, 2026 wameungana na wafanyakazi wa Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi kuadhimisha Siku ya wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) katika Kiwanja cha michezo cha Jamhuri jijini Dodoma.

Maadhimisho hayo yalianza kwa Taasisi mbalimbali kushiriki kwenye maandamano huku wakiwa wamebeba Mabango yenye kaulimbiu ya maadhimisho hayo isemayo “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050” matembezi hayo yaliyoanzia kwenye viwanja vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuhitimishwa kiwanjani Jamhuri na kupokelewa na Mgeni Rasmi ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, mgeni rasmi ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amelishukuru Shirikisho la Vyama vya wafanyakazi TUCTA kwa kumualika kushiriki katika kilele cha maadhimisho hayo, huku akimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuhimiza uwajibikaji na bidii kazini miongoni mwa wafanyakazi.

Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha mazingira ya kazi kwa wafanyakazi nchini ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kufikia malengo ya maendeleo ya Dira ya Taifa ifikapo mwaka 2050.

Mhe. Senyamule amesema kuwa, katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, Serikali imefanikiwa kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi, huku ikiendelea kuboresha miundombinu muhimu ya kurahisisha mfanyakazi kutoa huduma bora kwa jamii kama vile upatikanaji wa umeme, ujenzi wa miundombinu ya majengo pamoja na kuimarisha mawasiliano ya simu na intaneti.

“Serikali inaendelea kuweka mazingira bora ya kazi ili kuwasaidia wafanyakazi kufanya kazi kwa urahisi na ufanisi zaidi ili kuongeza tabasamu kwa wananchi,” alisema Mkuu wa Mkoa huyo.

Aidha, alitoa wito kwa wafanyakazi kushirikiana na Serikali kwa kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, huku akisisitiza umuhimu wa Sekta binafsi kufuata taratibu na sheria zilizowekwa ili kuboresha maslahi ya wafanyakazi.

Mhe. Senyamule akigusia maelekezo ya Rais Samia amesema kuwa, alielekeza kuwapa tabasamu wananchi nanyi Viongozi muwape tabasamu watumishi ili wafanyaka wawape tabasamu wananchi wanaowahudumia kuendelea kuimarisha ustawi wa wananchi kwa kuhakikisha huduma bora zinatolewa kwa usawa na kuepuka rushwa.

Aidha, Mhe. Senyamule amesema kwamba, Mkoa wa Dodoma umetajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayonufaika na uwekezaji wa Serikali hususan Vyuo vya elimu ya Juu. Mkuu wa Mkoa ametoa wito kwa wafanyazi kujiendeleza kielimu kutokana na fursa hiyo.

Katika hatua nyingine, wafanyakazi wametakiwa kuepuka vitendo vya rushwa na badala yake kuzingatia uadilifu katika utoaji wa huduma kwa wananchi. Pia wamehimizwa kutenga siku maalum za kusikiliza kero za wananchi ili kuboresha huduma.

Mkuu wa Mkoa huyo aliwatakia wafanyakazi wote mkoani Dodoma maadhimisho mema ya Siku ya Wafanyakazi Duniani na kuwataka kuendelea kushirikiana kwa ngazi zote kitaasisi katika kujenga Taifa lenye maendeleo na ustawi.

Kwa upande wake, Katibu wa Shirikisho la Vyama vya wafanyakazi Mkoa wa Dodoma Bw. Albert Stanslaus akisoma risala ya wafanyakazi mbele ya Mgeni rasmi amesema kuwa, licha ya juhudi za Serikali kuboresha maslahi ya wafanyakazi nchini, bado kuna changamoto zinazoikumba Sekta ya ajira ambazo zimeendelea kujitokeza, hususan katika sekta binafsi, ambapo wafanyakazi wanalalamikia ukiukwaji wa haki zao za msingi.

Risala hiyo ya wafanyakazi imebainisha mambo mbalimbali yaliyotajwa na wadau kwamba licha ya hatua stahiki zilizochukuliwa na Serikali kutatua changamoto za wafanyakazi lakini bado kuna matatizo yanayohitaji ufumbuzi wa haraka.

Bw. Stanslaus ameongeza kuwa, kupitia risala hiyo wafanyakazi wanakumbwa na ucheleweshaji wa malipo ya malimbikizo mbalimbali kama vile likizo, kupanda madaraja, huku wengine wakidai kutokuwa na mikataba rasmi ya ajira, hali inayowafanya kukosa uhakika wa ajira zao. Aidha, ilibainika kuwa kuna waajiri wanaolipa mishahara midogo isiyokidhi viwango vinavyokubalika kisheria.

Changamoto nyingine iliyotajwa ni kutowasilishwa kwa michango ya wafanyakazi kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii kwa wakati, jambo linalosababisha usumbufu mkubwa wanapohitaji mafao yao pindi wanapostaafu au wanapopata matatizo.

Pamoja na hayo, washiriki wa maadhimisho hayo walitoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake katika kuboresha mazingira ya kazi, ikiwa ni pamoja na kupandisha mishahara kwa mwaka 2025, kupandisha watumishi madaraja na kulipa madeni ya muda mrefu ya wafanyakazi.

Kupitia risala hiyo Katibu huyo alisisitiza kuwa juhudi zaidi zinahitajika ili kuhakikisha haki za wafanyakazi zinalindwa kikamilifu, hasa kwa kuimarisha usimamizi wa sheria za kazi na kuwawajibisha waajiri wanaokiuka taratibu.


Mkuu wa Mkoa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule akihutubia alaiki ya wafanyakazi wa Taasisi mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi katika Siku ya Maadhimisho ya Wafanyakazi Duniani leo tarehe Mei, Mosi, 2026 katika kiwanja cha michezo cha Jamhuri jijini Dodoma.




Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa tayari kwa ajili ya matembezi ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani leo tarehe Mosi Mei, 2026 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa tayari kwa ajili ya matembezi ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani leo tarehe Mosi Mei, 2026 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanashiriki matembezi na Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi ikiwa ni ishara ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanashiriki matembezi na Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi ikiwa ni ishara ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani.
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanashiriki matembezi na Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi ikiwa ni ishara ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani
Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kuhitimisha matembezi 

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanapita mbele ya Mgeni Rasmi kwa mbwembwe na bashasha wakati wanaingia uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.