Na PAUL PASCAL-Mahakama, Moshi
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian
Mongella, tarehe 18 Machi, 2026 alifanya ziara kwa ajili ya kuzungumza na Viongozi
wa Serikali na Wananchi wa Kata ya Kwakoa juu ya ombi lao kuhusu kupatiwa
huduma ya Mahakama katika eneo lao.
Katika
ziara hiyo, Mhe. Dkt. Mongela aliambatana na Viongozi wa Mahakama Kuu Moshi na
Mahakama ya Wilaya Mwanga, kufuti ombi la Wananchi hao kutoka Kijiji cha Ngulu
kilichoko Kata ya Kwakoa, Wilayani Mwanga, Mkoa wa Kilimanjaro.
Kwenye
ombi hilo waliloliwasilisha kwenye Ofisi ya Jaji Mfawidhi, wananchi walieleza hitaji
la kupata huduma za kimahakama kutokana na adha wanayoipata kwa kufuata huduma
hiyo umbali wa zaidi ya kilometa 40.
Akisoma
taarifa fupi ya Kata ya Kwakoa, Diwani wa eneo hilo, ambae pia ni Mwenyekiti wa
Kamati ya Maendeleo ya Kata, Mhe. Kiende Mvungi, alieleza kuwa kwenye Kata nne
zinazounda ukanda kwenye eneo lao hakuna hata moja yenye huduma ya kimahakama.
“Naomba
nikufahamishe kuwa Kata yetu ya Kwakoa inaundwa na Vijiji viwili; Kijiji cha Kwakoa
na Kijiji cha Ngulu. Ukanda huu umeundwa na Kata nne; Toroa, Kigonigoni, Jipe na
Kwakoa na katika Kata zote, hakuna yenye Mahakama ya Mwanzo. Wananchi wote wa Kta
hizi wanafuata huduma za kimahakama katika Mahakama ya Mwanzo Lembeni, ambayo
iko zaidi ya kilometa 40 kutoka hapa,” alisema Mhe. Kiende.
Diwani
huyo alibainisha kuwa katika kata yao wana Kituo cha Polisi, lakini mnyororo wa
utoaji haki hauwezi kukamilika pasipo kuwepo kwa Mahakama ambayo ndiyo yenye
jukumu la kutafsiri sheria za nchi na kwa kuliona hilo Serikali ya Kata ya
Kwakoa ikawasilisha ombi la kuanzishwa Mahakama ya Mwanzo Kwakoa ili iweze
kuhudumia Kata zote nne katika ukanda huo.
“Tumetenga
eneo lenye ukubwa wa ekari nne kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Mahakama na
makazi ya Watumishi kwa mpango wetu wa muda mfupi, tunaomba tuwakibidhi jengo
la kuanzia kutoa huduma za kimahakama katika eneo hili, wakati michakato ya
muda mrefu wa ujenzi ukiendelea ili nasi tupate huduma tuliyoikosa katika eneo
letu tangu tulipopata uhuru,” lisema Mhe. Kiende.
Kwa
upande wake, Jaji Mfawidhi aliwashukuru Wananchi na Viongozi wa Kata ya Kwakoa
kwa kutambua na kuwa na imani na Mahakama. Alipongeza juhudi katika kuhakikisha
huduma zote muhimu zinapatikana ndani ya Kata pasipo kuzifuata mbali.
“Tumefurahishwa
na jitihada zote mlizofanya ili muweze kupata huduma ya Mahakama katika eneo
lenu, niwaahidi kwa juhudi hizi jambo lenu linakwenda kukamilika, tunakwenda
kutekeleza matakwa ya kisheria ya uanzishaji wa Mahakama ya Mwanzo ndani ya
miezi mitatu. Tutahakikisha michakato yote inakamilika na huduma za kimahakama
katika Kata hii zinaanza,” alisema.
Katika ziara hiyo, Jaji Mongella aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje, Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Moshi, Bi. Maria Itala na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mwanga, Mhe. Marium Mfanga.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian
Mongella akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika katika Kata ya Kwakoa
wilayani Mwanga.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian
Mongella akisalimiana na Mwenyekiti wa Kijiji cha Ngulu, Kata ya Kwakoa, Bw.
Said Mvungi mara baada yakuwasili katika ziara yake.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian
Mongella akizungumza na Wananchi wa Kata ya Kwakoa wilayani Mwanga (hawako
pichani) wakati wa ziara yake.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian
Mongella akiongozana na Viongozi wa Serikali ya Kata ya Kwakoa kukagua jengo
kwa ajili ya kutolea huduma za Mahakama
ya Mwanzo.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian
Mongella (aliyesimama mbele katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi
wa Kata ya kwakoa mbele ya jengo linalotazamiwa kutumika kutolea huduma za Mahakama
ya Mwanzo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma




























.jpeg)


.jpg)























