Jumamosi, 13 Juni 2026

JENGO LA MAHAKAMA YA MWANZO MASUMBWE LAZINDULIWA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, tarehe 11 Juni, 2026, alizindua Jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe baada ya ujenzi wake kukamilika, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma za haki kwa Wananchi wa Wilaya ya Mbogwe na maeneo jirani.

Uzinduzi huo ulipokelewa kwa shangwe na Wananchi wa Masumbwe kutokana na kusogezwa karibu kwa huduma za Mahakama ambazo kwa muda mrefu zilikuwa zikitolewa katika jengo la Ofisi ya Tarafa.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, Jaji wa Mahakama Kuu  Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya, Watumishi wa Mahakama, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mbogwe, Viongozi wa Taasisi mbalimbali pamoja na Wananchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mhina alimshukuru Jaji Kahyoza kwa kushiriki uzinduzi huo na kueleza kuwa ushiriki wake unaakisi historia ya usimamizi wa shughuli za Mahakama katika eneo hilo, ambalo hapo awali lilikuwa chini ya Wilaya ya Kahama kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Geita.

Alisema kuwa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe ilianzishwa mwaka 1998 wakati eneo hilo likiwa chini ya Wilaya ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga, na imeendelea kutoa huduma za haki licha ya kukosa jengo rasmi kwa kipindi kirefu.

“Kwa miaka mingi, Mahakimu na Watumishi wa Mahakama walifanya kazi katika mazingira yasiyokuwa rasmi, huku Wananchi wakipata huduma katika maeneo yenye changamoto za miundombinu. Hata hivyo, hali hiyo haikuwazuia kutekeleza wajibu wao wa msingi wa kusimamia haki,” alisema Jaji Mhina.

Alisisitiza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya Mahakama ni msingi wa kuimarisha amani, utulivu na maendeleo ya Taifa, akieleza kuwa haki ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo ya jamii.

Aidha, alieleza kuwa ujenzi wa jengo hilo uliwezeshwa kwa kiasi kikubwa na uzalendo wa aliyekuwa Diwani wa Kata ya Masumbwe, Mhe. Shimo Kasheto, ambaye alitoa eneo la ekari mbili kwa ajili ya mradi huo. Pia aliwapongeza Evarist Gervas na wadau wengine waliochangia hatua za awali za ujenzi.

Kwa mujibu wa Jaji Mhina, juhudi za kukamilisha ujenzi ziliongezeka baada ya kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Geita mwaka 2023, ambapo uongozi wa Mahakama ulianza kutenga sehemu ya fedha za uendeshaji wa ofisi kwa ajili ya kukamilisha mradi huo.

Katika hafla hiyo, pia ulizinduliwa mfumo wa kidijitali wa kuhifadhi taarifa na majalada ya Mahakama za Mwanzo unaojulikana kama GEITA Repository Database, ambao sasa umeanza kutumika katika Mahakama zote za Mwanzo zilizopo Kanda ya Geita.

Jaji Mhina alisema mfumo huo ulifanyiwa majaribio katika Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu na kuthibitishwa kuwa tayari kwa matumizi rasmi. Alifafanua kuwa mfumo huo utasaidia kuhifadhi taarifa za mashauri, kuzuia upotevu wa majalada na kupunguza ucheleweshaji wa mashauri unaotokana na kusubiri kumbukumbu za mahakama.

Kwa upande wake, Jaji Kahyoza aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Geita pamoja na Wananchi wa Masumbwe kwa ushirikiano uliowezesha kukamilika kwa mradi huo.

Aliahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama na Wananchi ili kuboresha huduma za Mahakama na kutatua changamoto zilizopo katika Mahakama za Mwanzo.

Naye mMakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe alisema Serikali imefanikisha ujenzi wa barabara inayofika katika Mahakama hiyo na kuahidi kusimamia utekelezaji wa mradi wa umeme katika mwaka wa fedha 2026/2027 ili eneo la Mahakama pamoja na makazi ya jirani yaweze kupata huduma ya umeme.

Alieleza kuwa upatikanaji wa umeme utarahisisha utoaji wa huduma za Mahakama na kuchochea maendeleo ya Wananchi wa eneo hilo.

Wananchi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuridhishwa na ubora wa jengo hilo la kisasa na kuomba Serikali pamoja na Mahakama kuendelea kujenga majengo ya Mahakama yenye gharama nafuu katika maeneo ya vijijini na maeneo yenye changamoto za miundombinu ili kusogeza huduma za haki karibu zaidi na Wananchi.

Uzinduzi wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe unaonekana kuwa hatua muhimu katika kuimarisha upatikanaji wa haki, kuboresha mazingira ya kazi kwa Watumishi wa Mahakama na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za ki,ahakama katika Mkoa wa Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe Kevin Mhina, akikata utepe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, wakifungua Jiwe la Msingi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, akiutangazia Umma juu ya kuanza kutumika kwa jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, akitoa shukurani kwa uongozi Mahakama Kuu Geita na Wananchi wa Masumbwe kwa kushirikiana kikamilisha mradi huo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akiwakaribisha wageni katika hafla hiyo.

Wananchi wa Masumbwe wakiongonzwa na ugeni katika zoezi la kukagua mradi wa jengo hilo.

Picha ya pamoja katika Jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe, wakatikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Kevin Mhina, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa MahaKama Kuu Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama kuu Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje.

Picha ya pamoja katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe ngoma ya jadi na wageni katika hafla hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

 

 

Ijumaa, 12 Juni 2026

JAJI MKUU AWATAKA WADAU WA HAKI JINAI KUIMARISHA UMAKINI KATIKA UPELELEZI

 ·       Awataka pia wazingatie matakwa ya Kifungu cha 134 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai na Kanuni za Jaji Mkuu

·       Asisitiza Polisi kutoa dhamana kwa watuhumiwa kwa mujibu wa sheria

·       Amtaka kila mdau kusimama ipasavyo katika eneo lake kuboresha Haki Jinai

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Wadau wa Haki Jinai nchini kuendelea kuimarisha umakini katika upelelezi wa mashauri ya Jinai ya aina zote na uendeshaji wa mashauri ya jinai Mahakamani kwa kuzingatia Katiba na Sheria ipasavyo.

Mhe. Masaju aliyasema hayo jana tarehe 11 Juni, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu amesema kuwa, “miongoni mwa Taasisi ambazo zinaongoza kufanya/kushiriki Mafunzo ya ndani na nje ya Nchi ni Taasisi zinazohusika na upelelezi, hivyo tunataka kuona matunda yake na matokeo yake kazini.”

Jaji Mkuu amesema, zoezi la upelelezi liendane na Kifungu cha 134 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kinachotaka mashauri yafunguliwe Mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika isipokuwa kwa makosa ambayo ni makubwa na yale ambayo yanasikilizwa na Mahakama Kuu kama ilivyotajwa katika kifungu cha 134(4).

Aidha, amempongeza Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kwa kuweka Mwongozo ambao ni Sheria ambayo hata katika mashauri makubwa, upelelezi uwe umekamilika ndani ya siku 90 ili shauri lianze kusikilizwa.

“Yazingatieni hayo, lakini pia endeleeni kuzingatia na kanuni zilizotolewa na Jaji Mkuu kuhusu watuhumiwa kupata maelezo ya ushahidi dhidi yao, kabla ya kusomewa mashtaka kwa mara ya kwanza (Preliminary hearing) na kesi kuanza kusikilizwa ili kesi zinaposikilizwa wawe wanafamu ushahidi dhidi yao kama ilivyo kawaida katika Mahakama Kuu, hapo ndipo kutakuwa na usikilizwaji kikamilifu ile (fair trial) inayozungumzwa katika Katiba Ibara ya 13(6),” amesema Mhe. Masaju.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amesema kuwa, kuna changamoto ya dhamana kwa upande wa Polisi ambapo amesema, “niwaombe Polisi, mmepewa mamlaka chini ya kifungu namba 65 mpaka 70 vya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai na bahati mbaya sisi tunawafamu ninyi Polisi peke yenu, lakini kuna Taasisi nyingine ambazo zinakamata watu zinaleta kwenye vituo vyenu. Vituo vyenu unakuta vimejaa, sasa sijui kama mna fedha za kutosha au ni vikubwa kiasi gani, hii yenyewe ni sababu ya msingi kwa makosa yale ambayo yanadhaminika kuwapa dhamana,” ameeleza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amewashauri Polisi kutoa dhamana kwakuwa kifungu namba 65 mpaka 70 vya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kimeeleza vizuri. “Wapeni dhamana itatupunguzia pia na hizi tuhuma nyingine zisizokuwa na sababu mtu anaweza akajidhamini au anaweza akadhaminiwa na mtu, mpeni dhamana, msipoweka utaratibu wa kuwa dhamana watajaa mahabusu na kusababisha magonjwa ya mlipuko hata wengine wanaweza wakafia Mahabusu ikawa shida, kwahiyo hakuna sababu ya kuogopa kuwapa dhamana kama umewakamata kwa usahihi kabisa wapeni dhamana,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, Sheria inaelekeza kuhusu mtuhumiwa kutakiwa kufikishwa Mahakamani ndani ya saa 24 tangu alipokamatwa, hii itasaidia na kwa upande wa makosa ya uhujumu Uchumi wanatakiwa kufikishwa Mahakama ya Wilaya iliyo jirani na alipokamatwa ndani ya saa 48.

Kadhalika, amewataka kuzingatia masharti ya Kifungu cha 34 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kinachowataka Mkuu wa Kituo cha Polisi kutoa taarifa ya kila Mtuhumiwa aliyekamatwa bila kibali cha Mahakama (Warrant of Arrest) na ambao wako ndani ya Vituo vya Polisi na wale waliopata dhamana. “Hili ni takwa la kisheria, zingatieni haya masharti, faida zake ni nyingi na tumezitafakari hapa wote, hapa hakutakuwa na cha Mswalia Mtume, zingatieni hayo masharti ili twende kwa sababu hata tusiposema hayo mengine ni vizuri tukayazingatia yote haya,” amesisitiza.

“Kwa upande wa Mahakama, wajibu wetu tuutekeleze ipasavyo bila kutumia madaraka yetu vibaya,” amesema Jaji Mkuu huku akiwaahidi Wadau hao kuwa, Mahakama itaendelea kuwa makini kwa kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa Ibara ya 107A(1)(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) kwa sababu ndio Wasimamizi wa Sheria hizo kwa sababu kuna changamoto katika eneo la upelelezi.

“Lakini wajibu wetu wa kuandaa vitabu vya Rufaa kwa Wafungwa wanaotoka Mahakama Kuu kuja Mahakama ya Rufani, tuviandae na kuvikamilisha hivi vitabu na kuwapatia wahusika ili waweze kukamilisha sababu zao za Rufaa, hivyo hivyo Mahakama tuwapatie wengine wanaotaka kukata rufaa labda kutoka Mahakama ya Wilaya au Hakimu Mkazi kuja Mahakama Kuu, wanaotaka nakala za hukumu, wanaotaka mwenendo wa mashauri tuwapatie mapema ipasavyo ili waweze kuandaa rufaa zao,” amesema Mhe. Masaju huku akisisitiza yote ambayo yamesemwa kuhusu Mahakama yatekelezwe na kila mdau wa mkutano huo atekeleze majukumu yake ipasavyo ili kushughulikia changamoto.

Jaji Mkuu amewataka Wadau hao wa Haki Jinai wakiwemo Magereza, Polisi, TLS na Wadau wengine kama kuna changamoto zozote zinazokwamisha upatikanaji haki wasisite kutoa taarifa Mahakama badala ya kusubiri siku ya vikao tu.

“Mahakama ina nafasi kubwa sana katika ustawi na maendeleo ya Taifa letu, bila na kuwa na amani na utengamano katika Taifa, maendeleo gani yatatoka katika Taifa hilo, watu hawatafanya siasi, watu hawatafanya shughuli zao za kiuchumi, hawatafanya shughuli zao za kijamii ikiwa ni pamoja na shughuli za siasa na kufunga ndoa na kushiriki katika matamasha, kwahiyo tuna dhamana kubwa katika hili ili Taifa hili lidumu kuwa la udugu kama ilivyokuwa zamani tunaitana ndugu. Amani na udugu ndivyo vinavyohimizwa katika Katiba kupitia Ibara ya 9, hivyo simamieni utekelezaji wa sheria kwa ufanisi ipasavyo,” amesema.

Aidha, Jaji Mkuu amesema kuwa, katika hotuba yake ya Siku ya Sheria nchini mwaka huu alieleza mambo ambayo Mahakama inafanya katika kuchangia ustawi na maendeleo ya Taifa. Amesema, “Kaulimbiu yetu ya Mahakama kwa mwaka huu 2026 ni; Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.”

Ameeleza kuwa, Mahakama na wadau wake ni watu muhimu katika kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ambayo msingi wake mkuu ni Utawala, Amani, Usalama na Utulivu na vipaumbele vinne ambao ni Utawala Bora na Haki, Serikali za Mitaa Imara na zenye ufanisi, Utumishi wa Umma unaowajibika na Amani, Usalama na Utulivu ambapo kila mdau anahusika.

Amesema kuwa, pamoja na kwamba, Mahakama inatekeleza wajibu wake, inajikita kuangalia ni kwa namna gani Mhimili huo unachangia katika ustawi na maendeleo ya Taifa. “Sasa moja tunajua umuhimu wa Mahakama katika jamii, sasa katika kipindi hiki tangu tulivyokutana tarehe 02 Machi, 2026 mwaka huu Mahakama Kuu sita ambazo ni Njombe, Singida, Lindi, Simiyu, Songwe na Katavi zimezinduliwa na kufanya kazi na Mahakama za Mwanzo 15 nazo zimezinduliwa na kuanza kufanya kazi. Amesema kwa Tanzania Bara umebaki Mkoa mmoja pekee ambao hauna Masjala ya Mahakama Kuu ambao ni Pwani.

“Tumesogeza huduma zetu za Mahakama kwa watu ili haki ipatikane, kuwepo na amani na utulivu watu waweze kushiriki shughuli zao za kiuchumi, za kisiasa na kijamii kwa ufanisi ipasavyo. Kwa hiyo wenzetu mnaohusika na huduma za upelelezi mjue sasa kuna huduma za Mahakama Kuu katika hiyo Mikoa,” amesema Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, Ibara ya 25(1) ya Katiba inasema; Kazi pekee ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii, ndilo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha Utu. Na kila mtu anao wajibu wa: - a) kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji mali na b) kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji mali ya binafsi na yale malengo ya pamoja yanayotakiwa au yaliyowekwa na sheria.

Kadhalika, Jaji Mkuu amewakumusha Wadau hao kuhusu mikakati waliyokubaliana ambayo ni endelevu, ambapo mkakati wa kwanza unasema, kila Taasisi ambayo ni Mdau wa Mnyororo wa Utendaji Haki Mahakamani iwajibike ipasavyo kwa kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia Katiba, Sheria na maadili ya utumishi yanayosimamia Taasisi ipasavyo.

Na Mkakati wa pili ni kwamba Wadau wote Waheshimu na kulinda hadhi ya Mahakama, aidha Mahakama kwa upande wake, isimamie sheria na kanuni zilizopo ikiwemo sheria inayohusu kosa la kuidharau Mahakama yaani ‘Contempt of Court’ ili kulinda hadhi na ukuu wake.

Amesema kuwa, Sharti hilo ni la Kikatiba na lipo kwenye Ibara ya 30 (1) na ya (2d) kulinda hadhi, heshima na uhuru wa Mahakama, si kama sisi tunataka kuheshimiwa tu hapa, hili ni takwa la Kikatiba.

Mkakati wa tatu ni; Mahakama na Wadau wa mnyororo wa haki waimarisha mahusiano miongoni mwao kwa lengo la kuchukua hatua haraka ili kutatua changamoto za utoaji haki zitakapojitokeza.

Mwingine ni, Mahakama na Wadau wote watambue nafasi ya kila mmoja, wadumishe heshima, nidhamu ya kazi na wazingatie sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza utendaji kazi wa majukumu ya kila mdau.

Taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki, iimarishe ufuatiliaji mashauri na uwajibikaji kwa kutoa taarifa sahihi na za mara kwa mara kuhusu utekelezaji wa mikakati iliyowekwa na kutumia mifumo inayosomana ili kurahisisha mawasiliano.

Wadau wanaokiuka maadili wachukuliwe hatua ipasavyo kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazosimamiwa na kila mdau husika.

“Mkakati wa saba, Mahakama iongeze na kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali (Virtual Court) katika kuendesha mashauri yanayohusu watuhumiwa waliohamishiwa katika Magereza mbalimbali kutoka kwenye Wilaya zisizo na Magereza na ili upatikanaji wa haki uwe wa haraka na wa gharama nafuu.

Mkakati mwingine ni Vikao kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa jukumu la utoaji haki mahakamani vifanyike angalau mara nne kwa mwaka ilikujadili changamoto na kufuatilia utekelezaji wa mikakati hiyo. Mkakati wa tisa ni kila Taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa utoaji haki Mahakamani iweke utaratibu madhubuti wa ndani ya Taasisi utakaofanikisha utekelezaji wa mikakati hiyo.

Aidha, katika Mkutano huo uliofanyika jana uliongezeka mkakati mwingine mpya unaosema kwamba, migogoro yote inayopaswa kwa mujibu wa sheria kutatuliwa kwanza katika ngazi mbalimbali kwa njia ya kimadai au kiutawala ishughulikiwe na kukamilishwa katika hatua na ngazi zote husika badala ya kufunguliwa kama jinai moja kwa moja na hili ni sharti la kisheria.

Jaji Mkuu amesema kwamba, mikakati hiyo ikitekelezwa yatasaidia kuboresha mfumo wa haki jinai na haki itakuwa inapatikana mapema, kwa changamoto ambazo zinatatulika kwa urahisi.

“Huu mkakati wa mwisho pia ni wa kisheria, katika kifungu cha 4 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai ndipo kinapopatikana....., mikakati yote tuliyoiweka ni mikakati ya kisheria ipo kwenye sheria hakuna kitu hapa ambacho hakipo kwenye sheria na ndio maana tunaweka mikakati, kilichopo kwenye sheria lazima kinapaswa kitekelezwa, hatuwezi kuwekewa maazimio kwahiyo kwenye vikao vyetu sisi tumeshakataa maazimio huwezi kuazimia kutekeleza au kutotekeleza sheria, sheria ni lazima uitekeleze vinginevyo utaivunja na ukiivunja unawajibika. Kwahiyo tuna wajibu wa kutekeleza haya yote, tuna wajibu wa kutekeleza hii mikakati ambayo ni ya kisheria, vinginevyo tutawajibika,” ameeleza Mhe. Masaju.

Amesema, kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba inayoweka Utawala wa Sheria, inasema kila mtu ana wajibu wa kufuata na kutii Katiba hii na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara 26(2) inasema kila mtu ana haki kwa kufuata utaratibu uliowekwa na Sheria kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na Sheria za Nchi.

“Hata mikutano yetu hii, ni katika hatua tunazochukua kuhakikisha kwamba Katiba na Sheria za nchi zinatekelezwa ipasavyo na Ibara ya 25 inatutaka kila mmoja awajibike kwenye hili, na sisi wote tunafanya kazi sasa kwa nafasi mbalimbali, wengine ni Majaji, wengine ni Majaji Wakuu, wengine ni Wakurugenzi, wengine ni Maofisa wa Polisi, wengine Ofisi ya Magereza, wengine Ofisi ya PCCB, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, watumishi wote wa Taasisi zilizowakilishwa hapa tuna majibu tuonafanya kazi hizi,” amesema Jaji Mkuu.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wadau wa Haki Jinai alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 11 Juni, 2026.


Wadau wa Mahakama wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipokuwa akifunga 
 Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Mwenyekiti wa Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani  akizungumza jambo wakati wa mkutano huo uliofanyika tarehe 11 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Baadhi ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania walioshiriki katika 
Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

JAJI MFAWIDHI SONGWE AZINDUA MAHAKAMA YA MWANZO MSANGANO

Na. ELIUD ANDREW KIWANGA – Mahakama, Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata aongoza hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano iliyopo Kata ya Msangano Wilaya ya Momba Mkoa wa Songwe na kufanyika katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Msangano

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata aliishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuwezesha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano,

Aidha, aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuiwezesha Mahakama ya Tanzania na kuhakikisha inakuwa na miundombinu ya kisasa. Vilevile aliishukuru Mahakama ya Tanzania chini ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Geoge M. Masaju kwa kuendelea kubuni miradi mbalimbali ya uboreshaji wa Miundombinu ya Mahakama.

Mhe. Malata alisema kuwa, ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano ni ishara ya Serikali ya awamu ya sita kuwathamini  na kuwajali wananchi wa Msangano na maeneo jirani kwa kuwasogezea huduma ya upatikanaji wa haki na kuwa tofauti zozote za kisiasa, kijamii, kiuchumi, kiitikadi zisiwe sababu ya kuharibu miundombinu ya Mahakama ya Mwanzo Msangano.

“Hivyo wananchi wote kwa pamoja wanao wajibu wa kulinda na kutunza miundombinu ya Mahakama hiyo kwasababu ni mali ya umma na imejengwa kwa kodi za wananchi wenyewe. Wananchi wa Msangano wamepata bahati kujengewa Jengo la kisasa la Mahakama mapema ikilinganishwa na maeneo mengine. Nawaasa wananchi wa Msangano kuishi wa amani na upendo ili kuepuka migogoro kwani migogoro hurudisha nyuma maendeleo ya jamii,” alisisitiza Jaji Mfawidhi Malata.

Mhe. Malata aliwashukuru wanachi wote wa Msangano na maeneo jirani kwa kuwa walipa kodi wazuri na kufika katika hafla ya uzinduzi katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Msangano na pia aliushukuru uongozi wa Wilaya ya Momba  kwa kuupokea mradi, kuusimamia na kuulinda mpaka ulipokamilika.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo alianza kwa kuwaomba wananchi kuepuka tabia ya kujichukulia sheria mkononi kwani kwa kufanya hivo ni kinyume na sheria na pia alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwezesha ujenzi wa miundombinu ya Mahakama maeneo mbalimbali nchini.

Mhe. Daniel Mwandobo aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuendelea kutumia mifumo ya kidigitali kwani kwa kufanya hivyo kumepunguza gharama, muda wa ufatiliaji na pia imeimarisha mifumo ya utoaji wa haki.

Vile vile aliwaasa wananchi wasiiogope Mahakama bali wailinde na kuitunza na pia siyo mashauri yote yanapaswa kwenda mahakamani bali watumie pia njia za usuluhishi kutatua baadhi ya migogoro miongoni mwao. Aidha, aliipongeza Serikali na Mahakama ya Tanzania kwa kuanza kwa mchakato wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Momba inayotarajiwa kujengwa katika mji mdogo wa Chapwa.

Naye, Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Momba Bw. Kataba Sukuru aliishukuru Serikali ya awamu ya sita na Mahakama ya Tanzania kwa kuwezesha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Bw. Sakuru aliahidi kuendelea kushirikiana na uongozi wa Wilaya ya Momba na Mahakama ya Tanzania ili kuhakikisha huduma za msingi ikiwemo huduma ya Haki inapatikana kwa wananchi wa Kata ya Msangano pamoja na  wa Wilaya ya Momba kwa ujumla.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na sehemu ya viongozi wa ngazi ya Wilaya wakiwemo Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma Bw. Salumu Kyambi, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Momba Bw. Paul Sheyo, Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raymond Kaswaga, Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Momba Bw. Sukuru Kataba pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata akihotubia wakati wa uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kulia) akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano, (wa kwanza kulia) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Songwe Mhe. Francis Kishenyi, (wa tatu kulia) ni Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo, (wanne kulia) ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Tunduma Bw. Salumu Kyambi na Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Momba Bw. Paul Sheyo wakifuatilia hafla hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo katika zoezi la kukata utepe.

Sehemu ya wageni waalikwa waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja ya viongozi wa Mahakama Mkoa wa Songwe pamoja na Viongozi mbalimbali wa ngazi ya Wilaya ya Momba nje ya jengo la Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Momba Bw. Sukuru Kataba akitoa neno akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.

Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo akitoa neno katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msangano.


Mkuu wa Wilaya ya Momba Mhe. Elius Daniel Mwandobo akipanda mti wa kivuli katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Msangano.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama) 



Alhamisi, 11 Juni 2026

JAJI MKUU ATETA NA WADAU WA HAKI JINAI

  • Awataka kuwa huru kutoa michango yenye kuboresha mnyororo wa Haki Jinai
  • Asema ushirikiano wa wadau kwa Mahakama ni muhimu katika kufikia azma hiyo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Wadau wa Haki Jinai nchini kuwa huru na wakweli katika kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yanayoukabili mnyonyoro wa Haki Jinai.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 11 Juni, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

"Kama changamoto zipo Mahakamani semeni, kama changamoto zipo ili mradi tuwe wakweli sio kusingiziana na tutasema hapa kwa kuheshimiana hatujaja kusutana, tumekuja kushauriana ni wapi kuna tatizo turekebishe na ni wapi tunafanya vizuri kwa hiyo vikao hivi ni vya muhimu," amesema Mhe. Masaju. 

Jaji Mkuu amewaeleza Wadau hao kuwa, wao ni watu muhimu katika kusukuma mbele na kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki Mahakamani.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Mahakama itaendeleza utaratibu wa kufanya vikao hivyo na wadau, ambapo amesema jana tarehe 10 Juni, 2026 kulikuwa na mkutano na wadau wa Haki Madai.

"Leo tunafanya mkutano na Wadau wa Haki Jinai, sasa kama mnavyofahamu sisi utaratibu huu tutauendeleza, kumekuwa na tatizo kubwa hata katika mfumo wa haki jinai na jinsi tunavyofanya kazi katika Taifa hili, ndio maana Rais aliunda Tume, moja ya Tume za kwanza kabisa alizoziunda ilikuwa ni Tume ya Haki Jinai iliyoongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman ikiwa imesheheni na wajumbe wengine wengi maarufu mpaka Inspekta Jenerali wa Polisi, walikuwepo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali alikuwepo na watu wengine maarufu," ameeleza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kwamba, uundwaji wa Tume hiyo uliashiria kwamba bado kuna changamoto kubwa katika utekelezaji wa haki jinai katika Taifa. "Na ile Tume ilikuja na mapendekezo na mimi nilivyoteuliwa na Mhe. Rais kuwa Jaji Mkuu siku ananiapisha tarehe 15 Juni, 2025 alinielekeza pamoja na mengineyo kutekeleza mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai, sasa yale sisi hatuwezi kuyatekeleza peke yetu, lazima tuyatekeleze kwa kushirikiana na Wadau wa Mahakama waliopo kwenye mnyororo wa haki jinai,'" amesisitiza.

Kadhalika, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, "Mahakamani huwa hatukai peke yetu huwa tunakuwepo sisi Mahakama na watu wenye mashauri Mahakamani, watu wenye mashauri mahakamani wanaweza kuwa ni watu binafsi na Taasisi binafsi, miongoni mwao lakini pia wanaweza kuwa baina ya Taasisi za Serikali na watu na mashirika binafsi."

Kupitia ukweli huo, amesema ndipo unaona nafasi ya kwa mfano Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka wakiwakilisha Taasisi za Serikali kwenye mashauri mbalimbali ama wao wenyewe kama Washtaki na Wadai au Washtakiwa na Wadaiwa na ziko na Taasisi nyingine nyingi.

"Kwahiyo ndio maana tunakuwa na utaratibu huu wa kuwashirikisheni ninyi katika shughuli za Mahakama si kwa maana kwamba kwenye masuala ya ushirikishaji wa mashauri, tunashirikisha kwenye hizi shughuli kwa maana kujadili kwa pamoja changamoto zinazotukabili katika utoaji haki na ndio maana tumeanzisha hicho kitu kinachoitwa Haki Jinai," amesema Mhe. Masaju.

Mhe. Masaju ametoa kuwa, uwepo wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) wanawakilisha watu wanaoshtakiwa Mahakamani wenye makosa ya jinai lakini na hata wao wenyewe wanapoamua kushtaki mahakamani (private prosecution), lakini Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Katiba na Sheria ambaye naye amehudhuria kikao hicho ni muhimu ili Wizara hiyo ijue ni kitu gani kinaendelea ndani ya Mahakama ili wanaporatibu masuala ya kisera wajue hali ya Mahakama kwa maana ya mafanikio na changamoto zinazoukabili Mhimili huo.

Aidha, Jaji Mkuu amesema, hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokuwa akiwaapisha Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani, pamoja na mambo mengine alisema Haki ndio Msingi wa Amani.

"Na jana (tarehe 10 Juni, 2026) nilisema haki ni nini, nilisema haki ni uamuzi unaofanywa na Mahakama huru kwa kuzingatia Katiba na Sheria za Nchi hii kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa Mahakamani, hiyo ndio haki. Kwahiyo niwaalike wote kwa dhati tushiriki katika mkutano huu, hapa leo hatuko Mahakamani tupo katika mkutano kwahiyo tuwe wazi, tushauriane," amesisitiza Mhe. 

Katika Mkutano huo Mahakama na Wadau wametoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati waliojiwekea katika vikao viwili vilivyofanyika nyuma. Kupitia taarifa hizo, kila mdau ataeleza amefanya nini na kubaini maeneo waliyofanikiwa na walipokwama na kuweka mikakati zaidi ya kujikwamua ili kwenda pamoja.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akizungumza alipokuwa akifungua Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. Wa kwanza kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na kulia ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga.

Wadau mbalimbali walioshiriki katika Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Mikakati kutoka Mahakama ya Tanzania wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. 

Sehemu ya Viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika Mkutano wa Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Juni, 2026. 

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)