Jumamosi, 18 Julai 2026

TUMIENI UJUZI NA TAALUMA MLIZONAZO KUTATUA CHANGAMOTO; JAJI RWIZILE

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile hivi karibuni alifanya ziara ya Ukaguzi wa Mahakama za Wilaya mkoani humo na kuwataka Watumishi wa Mahakama hizo kutumia vema taaluma na ujuzi walionao ili kutatua changamoto mbalimbali katika maeneo yao ya kazi.

Mhe. Rwizile alifanya ziara hiyo kwa lengo la kuangalia maendeleo ya shughuli za Mahakama katika maeneo ya mashauri, miundombinu pamoja na watumishi.

“Tumieni vema taaluma mbalimbali mlizonazo kutatua changamoto mbalimbali katika maeneo yenu ya kazi, nafahamu wapo watumishi wameajiriwa mkiwa na taaluma tofauti na ajira zenu, hivyo ni fursa kwenu kuonesha uwezo katika kusaidia shughuli zetu pale tunapokwama, hata hivyo tukishirikiana vema tutaongeza ufanisi na tija katika shughuli za Mahakama,” alisema Mhe. Rwizile.

Hata hivyo, Jaji Mfawidhi huyo alitoa pongezi kwa Mtumishi, Mlinzi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe, Bw. George Kato ambapo alisema, “nimepokea taarifa yenu imeonesha huyu bwana ametatua tatizo la ki-Tehama kwa kutumia taaluma yake, ambapo imesaidia shughuli za mashauri kutokwama, anastahili pongezi kubwa na kutambuliwa, nasi tumeona. Ni rai yangu kuwa, kila mtumishi mwenye taaluma tofauti na ajira/kada yake aitumie vema kama sehemu ya ubunifu na weledi wa kusaidia shughuli zetu.”

Vilevile, alitoa wito kwa watumishi wote wa Mahakama Kanda ya Kigoma kuwasilisha changamoto kwa Viongozi wao ili zitatuliwe kabla ya kuleta madhara katika mnyororo wa utoaji haki mapema ipasavyo.

Aidha, alisema kuwa, watumishi waendelee kushirikiana katika mipango wanayopanga na kukubaliana na kuitekeleza kwa pamoja ili kufikia malengo yenye kiwango kinachokubalika na Mwajiri, sambamba na utunzaji wa mazingira na miundombinu mbalimbali ya Mahakama.

Kwa upande wake Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa alisema kuwa, atasimamia maelekezo na maono ya Mwajiri ili kuhakikisha shughuli za Mahakama zinatolewa kwa mapema ipasavyo katika kila kituo.

“Nawapongeza watumishi wa Mahakama zote Kigoma kwa uchapakazi wenu, hasa katika eneo la mashauri,” alisema Mhe. Mbwelwa na kukiri kuwa anaridhishwa na usikilizwaji na umalizaji wa mashauri kwa Mahakama zote, ambapo hakuna mashauri mlundikano.

Hata hivyo, Naibu Msajili huyo aliwataka Watumishi kuendelea na kasi hiyo ili Mahakama Kigoma iendelee kuwa bora na tofauti katika maeneo yote ya kiutendaji.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka alisema kuwa, atasimamia maagizo yote katika kutekeleza Mpango Mkakati wa Mahakama pamoja na maelekezo yote ya Viongozi wa juu wa Mahakama ya Tanzania ili kufikia lengo na tija katika utoaji haki mapema ipasavyo. Hata hivyo, alimuhakikishia Jaji Mfawidhi kuwa utunzaji wa miundombinu ya Mahakama na vitendea kazi, unakwenda.

Mahakama zilizokaguliwa ni Mahakama za Wilaya za Kigoma, Kasulu, Buhigwe, Kibondo na Uvinza pamoja Mahakama za Mwanzo Kasanda na Manyovu, zilizopo Wilaya ya Buhigwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile kikagua Mahakama ya Mwanzo Manyovu alipofanya ziara ya kikazi katika Mahakama hiyo hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akisalimiana na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe alipofanya ukaguzi hivi karibuni. Anayesalimiana naye ni Bw. George Ilunga Kato, Mlinzi wa Mahakama ya Wilaya hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma,  Mhe. Augustine K. Rwizile (katikati) akizungumza jambo wakati wa ziara yake Mahakama ya Wilaya Buhigwe.  Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na kushoto Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe, Mhe. Katoke Mwakitalu.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma,  Mhe. Augustine Rwizile akigusa mti uliopandwa na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora wa kipindi hicho mwaka 2001, Jaji Mstaafu, Mhe. Edward Rutakangwa, wakati wa ziara ya ukaguzi wa Mahakama Kibondo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akikagua orodha ya mashauri katika ubao wa matangazo, uliopo katika eneo la wateja kusubiria  Mahakama ya Wilaya Uvinza. Pamoja naye kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na katikati  ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya uvinza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (wa pili kulia) akipokea taarifa ya ukarabati wa Mahakama ya Mwanzo Kasanda kutoka kwa Ofisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Kakonko, Bw. Nehemiah Makoko, (kulia) wengine ni Viongozi Waandamizi wa Mahakama Kuu Kigoma walioambatana katika msafara wa Jaji Mfawidhi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Haki Jinai alioambatana nao kukagua Gereza la Mahakama ya Wilaya Kasulu.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibondo mara baada ya ukaguzi wake katika Mahakama hiyo.

 Picha ya pamoja. Katikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati), wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka, wa pili kushoto ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kakonko, Mhe. Magreth Rweyemamu wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Kasanda Mhe. Jonas Kilimba.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka, (kulia) ni Mwendesha Mashtaka Mfawidhi wa Wilaya Uvinza, Bi. Edina Mkala na waliosimama ni Watumishi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka wa Wilaya hiyo mara baada ya kuzulu katika ofisi hiyo.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Ijumaa, 17 Julai 2026

MAHAKAMA GEITA, SONGWE WABADILISHANA UZOEFU KWENYE MATUMIZI YA TEHAMA

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, tarehe 15 Julai, 2026 alipokea ugeni kutoka Mahakama Kuu Songwe, kwa lengo la kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji wa huduma za Mahakama.

Ziara ya Viongozi kutoka Mahakama Songwe iliongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Joyce Minde, akiwa ameambatana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, Afisa Utumishi pamoja na watumishi wengine wa Mahakama hiyo.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Kahyoza alisema kuwa kubadilishana uzoefu ni fursa muhimu ya kujifunza mbinu bora zinazoweza kuboresha utendaji kazi na kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa ufanisi, kwa wakati na kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia.

Aliwahimiza watumishi wa Mahakama Kuu Geita kuitumia kikamilifu fursa hiyo kwa kujifunza kutoka kwa wenzao wa Songwe na kushiriki kikamilifu katika mijadala.

"Kama una jambo la kuchangia au kuuliza, usisite kulisema. Lengo letu ni kujifunza kutoka kwa kila mmoja ili kuboresha huduma zetu," alisema Jaji Kahyoza.

Akizungumzia Mkoa wa Geita, Mhe. Kahyoza alisema kuwa licha ya kuwa ni Mkoa mchanga, una mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kupitia shughuli za uchimbaji madini, kilimo, uvuvi na ufugaji. Aidha, alisema Mkoa huo umejaliwa vivutio mbalimbali vya utalii, ikiwemo Ziwa Victoria, Hifadhi ya Kigosi pamoja na urithi wa utamaduni.

Kuhusu matumizi ya TEHAMA mahakamani, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa ni takwa la kisheria na kwamba Mahakama Kuu Geita ilianza rasmi kutekeleza mfumo wa Mahakama kidijiti tangu ilipoanzishwa tarehe 23 Desemba, 2023, kufuatia maelekezo ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wakati wa uzinduzi wa masjala hiyo.

Alisema Jaji Mkuu alielekeza Mahakama Kuu Geita kuanza shughuli zake kama Mahakama ya kidijiti (purely digital), bila kutumia karatasi. Aliongeza kuwa kufuatia maelekezo hayo, Masjala iliweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha matumizi ya TEHAMA yanatekelezwa kikamilifu.

Mikakati hiyo ilijumuisha kuendesha mafunzo ya ndani kwa watumishi, kufanya mikutano na wadau wa Mahakama, Viongozi wa Serikali pamoja na wananchi ili kuwajengea uelewa kuhusu umuhimu wa kuondokana na matumizi ya karatasi katika utoaji wa huduma za Mahakama.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (ECMS), akieleza namna mfumo huo unavyowezesha uendeshaji wa mashauri bila matumizi ya karatasi.

Alisema mfumo huo umeongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri kwa kuwezesha ufuatiliaji wa mwenendo wa kesi, kupunguza mlundikano wa mashauri, kuharakisha utoaji wa haki na kuimarisha uwazi katika shughuli za Mahakama.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya TEHAMA yameboresha utunzaji wa kumbukumbu za mashauri kwa kuondoa changamoto ya upotevu wa mafaili, kurahisisha upatikanaji wa hukumu na maamuzi kupitia hifadhidata, kuboresha usahihi wa takwimu za Mahakama pamoja na kupunguza muda na gharama za uendeshaji kupitia matumizi ya Mahakama pepe.

Akizungumza kuhusu mafanikio ya Taasisi, Mhe. Lukuna alisema kuwa ni muhimu kuwa na malengo yaliyo wazi na yanayopimika, kujenga timu yenye nidhamu, kusimamia muda kwa ufanisi na kuendelea kuwajengea uwezo watumishi kupitia mafunzo endelevu.

"Ni muhimu kudumisha mahusiano mazuri kazini, kujifunza kutokana na makosa yaliyopita, kubaini changamoto zinazochelewesha utendaji, kuhakikisha rasilimali muhimu zinapatikana na kuwa tayari kufanya maamuzi yatakayochochea mafanikio ya pamoja," alisema.

Naye Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, alieleza namna masjala hiyo ilivyoondokana na matumizi ya karatasi kwa kutumia mifumo ya kidijitali katika mawasiliano na utunzaji wa nyaraka.

Alisema hatua hiyo imeongeza ufanisi wa kazi, kupunguza gharama za ununuzi wa mafaili na vifaa vya kuhifadhia nyaraka, kuimarisha usalama wa taarifa kwa kupunguza hatari ya uvujaji wa taarifa, kurahisisha utoaji wa huduma kwa wateja na kuongeza ubunifu katika utendaji kazi.

Bi. Kisasila aliwashauri washiriki kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mara kwa mara wa mifumo ya TEHAMA, kutoa motisha kwa watumishi na kuendelea kuendesha mafunzo ya ndani ili kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.

Kwa niaba ya ujumbe kutoka Songwe, Mhe. Minde, alitoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu ya Geita kwa mapokezi mazuri na mafunzo yenye tija yaliyotolewa wakati wa ziara hiyo.

Alimshukuru Jaji Mfawidhi, Naibu Msajili, Mtendaji pamoja na watumishi wote wa Mahakama Kuu ya Geita kwa ushirikiano waliouonyesha licha ya taarifa ya ujio wa ujumbe huo kutolewa kwa muda mfupi. Aidha, aliahidi kuwa maarifa na uzoefu walioupata vitatekelezwa na kusambazwa katika vituo vyao vya kazi ili kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, akiwakaribisha watumishi kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe.


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi (wa katikati) akihimiza kushiriki kikamirifu katika mafunzo ya kubadilishana uzoefu, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Songwe, Mhe. Joyce Minde.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akitoa mada kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (ECMS) bila matumizi ya karatasi.

Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, akieleza mafanikio ya matumizi ya TEHAMA katika eneo la utawala.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, akiwezesha mafunzo juu ya matumizi ya TEHAMA kwa upande mashauri na utawala katika ngazi ya Wilaya pasipo kutumia karatasi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, akiwezesha mafunzo juu ya mfumo wa Mahakama ya Mwanzo unaotumika Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (wa pili kushoto) akiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Songwe, Mhe. Joyce Minde na watumishi wa Mahakama Songwe.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.


 

Alhamisi, 16 Julai 2026

WATUMISHI MBEYA WAMUAGA MSTAAFU BW. CHARLES MAPUNDA CHITEKETELA KWA HESHIMA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya jana tarehe 15 Julai, 2026 walishiriki katika hafla ya kumuaga aliyekuwa mtumishi Mahakama mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela, ambaye alikuwa akihudumu kama Msaidizi wa Kumbukumbu na Msimamizi wa Kitengo cha mashauri ya Madai, anayestaafu utumishi wa umma baada ya kuitumikia Mahakama kwa weledi, uadilifu na kujituma kwa muda wa miongo kadhaa.

Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya na kuhudhuriwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, viongozi mbalimbali wa vitengo pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Wilaya Mbeya.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Mpepo alimpongeza Bw. Mapunda kwa utumishi wake uliotukuka na mchango mkubwa alioutoa katika kuimarisha utendaji wa Mahakama. Alieleza kuwa mstaafu huyo amekuwa mfano wa uwajibikaji, uaminifu na uzalendo katika kutekeleza majukumu yake.

“Tunakupongeza sana Bw. Mapunda, umekuwa mtumishi uliyeitumikia Mahakama kwa utumishi uliotukuka. Tunazijua na kuzithamini kazi ulizozifanya na kwa juhudi zako uliendelea kujiendeleza hadi kufika hapo ulipo, kwa hakika uliipenda na kuiheshimu kazi yako Mungu akubariki katika maisha yako mapya,” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, mstaafu huyo Bw. Chiteketela alitoa shukrani kwa viongozi na watumishi wote aliobahatika kufanya nao kazi kwa kipindi chote cha utumishi wake. Alisema ushirikiano, upendo na mshikamano alioupata kutoka kwa wenzake umechangia mafanikio yake katika kazi.

“Napenda kuwashukuru watumishi wenzangu ambao tumefanya kazi pamoja kwa ushirikiano mkubwa bila kuchoka na bila kubaguana. Nawashukuru pia viongozi wangu kwa kunilea na kuniongoza vyema hadi kufikia hatua hii, Mungu awabariki sana.”

Aidha, Bw. Chiteketela aliwaasa watumishi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, bidii na uaminifu, akisisitiza kuwa mafanikio katika utumishi yanatokana na kuipenda kazi na kutimiza wajibu kwa moyo wa kujituma.

“Ukifanya kazi kwa weledi na kujituma haikupi shida kuifanikisha kazi yako. Nawausia kuipenda kazi yenu na kujituma katika majukumu yote mnayopangiwa na viongozi, kwani huo ndiyo msingi wa mafanikio,” alisisitiza Bw. Chiteketela

Bw. Mapunda aliwahimiza watumishi kudumisha umoja na ushirikiano mahali pa kazi ili kuendelea kujenga mazingira bora ya utendaji na kuimarisha mahusiano ya kikazi.

“Nawasihi muwe na umoja na ushirikiano baina yenu, kwa kuwa kufanya hivyo kutaboresha utendaji kazi na kujenga undugu imara baina yenu.”

Hafla hiyo imeendelea kudhihirisha utamaduni wa Mahakama wa kuthamini na kuenzi mchango wa watumishi wake waliotumikia taasisi kwa uaminifu, uadilifu na kujituma.

Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) akizungumza machache na kutoa neno la shukrani katika hafla hiyo.


Bw. Charles Mapunda Chiteketela (watatu kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na Mahakimu Mbalimbali wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba (watatu kushoto)

Bw. Charles Mapunda Chiteketela (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa kitengo cha madai ambacho Bw. Charles Mapunda Chiteketela alikuwa msimamizi wa kitengo hicho

Bw. Charles Mapunda Chiteketela (wapili kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na maafisa Utumishi/Tawala (wa kwanza kushoto) ni Afisa Utumishi Mahakama ya Watoto Mbeya Bw. Ibrahim Mgallah, (wa pili kushoto) ni Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Odilia Mapunda, (wa kwanza kulia) ni  Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bi. Sarah Lossi a aliyesimamama nyuma ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Alintula Ngalile.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akikabidhi sehemu ya zawadi zilizoandaliwa kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akikabidhi sehemu ya zawadi zilizoandaliwa kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akimlisha keki kuonesha ishara ya pongezi kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

ZIARA YA MAHAKAMA LINDI YAANGAZIA MAFANIKIO YA KITUO JUMUISHI CHA UTOAJI HAKI

  •  Timu ya Habari, Elimu na Mawasiliano yajionea matokeo ya Mradi wa Awamu ya Pili wa Maboresho ya Mahakama
  • Uwepo wa Mahakama Kuu Lindi watajwa kufurahiwa na Wananchi wa Mkoa huo
  • Wapunguza aza ya wananchi kusafiri umbali mrefu kusaka huduma za Mahakama Kuu

Na HALIMA MNETE, Mahakama- Lindi

Timu ya Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano cha Mahakama ya Tanzania imefanya ziara katika Mkoa wa Lindi tarehe 15 Julai, 2026 kwa kutembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (Integrated Justice Centre – IJC), kwa lengo la kujionea mafanikio ya utekelezaji wa Mradi wa Awamu ya Pili wa Maboresho ya Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Katika ziara hiyo, timu ilipata fursa ya kufanya mahojiano na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Lindi, Mhe. Sylvester Kainda, Mtendaji wa Mahakama Kuu Lindi, Bi. Quip Mbeyela pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama hiyo, Mhe. Elia Mrema ambao kwa pamoja walieleza mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Lindi na namna ilivyoleta mageuzi makubwa katika upatikanaji wa huduma za kimahakama.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Kainda alisema, kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Lindi imekuwa hatua muhimu katika kusogeza huduma za haki karibu na wananchi na kupunguza changamoto zilizokuwa zikiwakabili wananchi wa Mkoa huo kwa muda mrefu.

"Kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Lindi ni hatua kubwa katika kuboresha upatikanaji wa haki. Wananchi waliokuwa wakisafiri umbali mrefu kwenda Mtwara sasa wanapata huduma karibu na maeneo yao. Hii imepunguza muda wa usikilizaji wa mashauri, gharama kwa wananchi na kuongeza imani yao kwa Mahakama," alisema.

Kwa upande wake, Bi.Quip Mbeyela alisema mradi huo umeleta manufaa makubwa kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi na Wilaya zake kwa kuwa umeondoa aza ya safari ndefu zilizokuwa zikifanyika kufuata huduma za Mahakama Kuu.

"Wananchi wameupokea mradi huu kwa furaha kubwa, zamani walitumia muda mwingi na fedha nyingi kusafiri kwenda Mtwara kutafuta haki. Leo hii huduma zinapatikana hapa Lindi, jambo ambalo limewawezesha kuendelea na shughuli zao za kijamii na kiuchumi bila usumbufu mkubwa," alisema Mtendaji huyo.

Naye Naibu Msajili, Mhe. Mrema, alisema uwepo wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Lindi umeongeza ufanisi katika utendaji wa Mahakama kupitia matumizi ya mifumo ya TEHAMA na uendeshaji wa huduma kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia.

"Mradi huu umeimarisha uendeshaji wa mashauri kwa kuwezesha matumizi ya nyaraka za kidijitali na utekelezaji wa utaratibu wa kufanya kazi bila matumizi ya karatasi (paperless). Hali hii imeongeza ufanisi katika utoaji wa huduma, imeharakisha uchakataji wa mashauri na kupunguza gharama za uendeshaji," alisema Mhe. Mrema.

Taarifa zilizowasilishwa wakati wa ziara hiyo zinaonesha kuwa kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Lindi kupitia Tangazo la Serikali Na. 76 la mwaka 2026, wananchi kutoka Wilaya za Kilwa, Liwale, Nachingwea na Ruangwa walilazimika kusafiri zaidi ya kilomita 300 kwenda Mtwara kufuata huduma za Mahakama Kuu. Hali hiyo ilisababisha matumizi makubwa ya muda na fedha, huku ikiathiri shughuli zao za uzalishaji.

Hata hivyo, kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Lindi kumeondoa changamoto hiyo kwa kusogeza huduma karibu na wananchi, hatua iliyochangia kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri, kupunguza gharama za kutafuta haki na kuimarisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Aidha, Watumishi wa Mahakama hiyo wameeleza kuwa, matumizi ya mifumo ya kidijitali na uendeshaji wa ofisi bila karatasi yameongeza ufanisi katika utoaji wa huduma, kupunguza gharama za uendeshaji na kuimarisha usimamizi wa mashauri.

Ziara hiyo imeiwezesha Timu ya Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano kujionea kwa karibu matokeo ya utekelezaji wa Mradi wa Awamu ya Pili wa Maboresho ya Mahakama, unaoendelea kuimarisha miundombinu ya kimahakama na kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi.

Mafanikio hayo yanaendelea kudhihirisha dhamira ya Mahakama ya Tanzania ya kutoa huduma bora za haki mapema ipasavyo, kwa ufanisi na kwa kuzingatia misingi ya Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji.


Jengo la Kituo Jumishi cha Utoaji Haki (IJC) Lindi, likiwa ni moja kati ya majengo ya Mahakama yaliyojengwa ikiwa ni utelelezaji wa Mradi wa Awamu ya Pili wa Maboresho ya Mahakama ya Tanzania.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Lindi, Mhe. Sylvester Kainda.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Lindi, Mhe. Elia Mrema.


Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Lindi, Bi. Quip Mbeyela.

Mahojiano yakiendelea.

Picha ya pamoja, wa tatu kulia ni 
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Lindi, Mhe. Elia Mrema, wa tatu kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Lindi, Bi. Quip Mbeyela, wa pili kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano (HIECU), Bw. Gerard Chami na sehemu ya Maofisa Habari wa Mahakama.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 

Jumatano, 15 Julai 2026

JAJI MFAWIDHI MANYARA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI WA MAHAKAMA

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi amefanya ziara ya Ukaguzi katika Mahakama zilizopo Wilayani Mbulu na Hanang’ na kuwasisitiza watumishi kufanya kazi kwa uadilifu, ueledi na uwajibikaji ili kuhakikisha malengo ya Mahakama yanatimia ipasavyo.

Hii ni ziara ya kwanza ya ukaguzi kwa Mhe. Dkt. Mambi tangu ahamie Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kama Jaji Mfawidhi akitokea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora ambapo pia alikuwa Jaji Mfawidhi.

Akizungumza na watumishi katika Mahakama ya Wilaya ya Mbulu, Mhe. Dkt. Mambi aliwaasa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na nidhamu wanapokuwa ofisini na hata wanapokuwa nje ya Ofisi.

“sisi watumishi wa Mahakama tunapaswa kuishi kwa nidhamu kuanzia ofisini na hata tunapokuwa nje ya Ofisi zetu, tunatarajiwa kuwa vioo vya jamii kwa wadaawa wetu na watu wote tunaowahudumia. Kwa misingi hii, maadili na nidhamu lazima vitutawale popote tutakapokuwa”, alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Akizungumza kwa nyakati tofauti na Mahakimu wa vituo vilivyokaguliwa, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava aliwasisitiza Mahakimu kuhakikisha kuwa wanahuisha taarifa za mashauri yao kwenye mfumo kila siku bila kukosa na kuhakikisha kuwa wanatoa nakala za Hukumu ipasavyo.

“Katika kipindi hiki cha matumizi makubwa ya TEHAMA, hatutarajii kuona kuwa tuna madeni ya kuhuisha mashauri katika mfumo rasmi uliowekwa hivyo ninawasihi mlichukulie suala hili kwa uzito wa hali ya juu. Vilevile hatutarajii tukifika katika magereza yetu tukutane na mfungwa ambaye analalamika kukosa nakala ya hukumu katika zama hizi”, alisema Mhe. Mnzava.

Kwa upande wa Wilaya ya Mbulu, Mahakama zilizokaguliwa ni Mahakama ya Wilaya Mbulu, Mahakama za Mwanzo Daudi, Dongobesh, Haydom na Gereza lililopo wilayani Mbulu.

Kwa upande wa Wilaya ya Hanang, Mahakama ambazo zilikaguliwa ni Mahakama ya Wilaya ya Hanang, Mahakama za Mwanzo Katesh, Bassotu na Endasak pamoja na mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Hanang ambao unaendelea kwa sasa.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mambi alifanikiwa kufika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mbulu na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu pamoja na kamati ya Wilaya ya Ulinzi na usalama, ambapo Mkuu wa Wilaya huyo aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Mahakama hususan kusaidia upatikanaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama na upatikanaji wa hati za viwanja hivyo.

Aidha, Mhe. Dkt. Mambi alitumia pia ziara hiyo kutambulisha viongozi wapya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara ambao ni yeye mwenyewe pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava ambaye awali alikuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara.

Pia katika ziara hiyo, viongozi wengine walioambatana nao ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu anayehudumu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara Mhe. Mariam Lusewa pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemedi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama) akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbulu (hawapo pichani) katika ziara ya Ukaguzi iliyofanyika wilayani hapo, kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava na kulia ni Naibu Msajili anayehudumu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara Mhe Mariam Lusewa.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa kwanza kulia) akifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, aliyekaa mbele ni Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa tatu kushoto) akiendelea na zoezi la ukaguzi katika Mradi wa Ujenzi katika Mahakama ya Wilaya ya Hanang.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Hanang mara baada ya kufika kituoni hapo kwa ajili ya Ukaguzi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akiongoza zoezi la ukaguzi katika Mahakama ya Mwanzo Bassotu wilayani Hanang.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Haydom iliyopo Wilayani Mbulu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wanne kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara pamoja na viongozi waandamizi wa Gereza la Wilaya ya Mbulu mara baaada ya kufanya Ukaguzi Gerezani hapo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa tatu kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Hanang.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Charles Mnzava (aliyesimama) akichangia neno wakati walipo mtemebelea Ofisini Mkuu wa Wilaya ya Mbulu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Dongobesh wilayani Mbulu.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)

 

KATIBU MKUU WIZARA YA KATIBA NA SHERIA AJITAMBULISHA RASMI KWA JAJI MKUU

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, leo tarehe 15 Julai, 2026 amepokea ugeni wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, aliyefika ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma kwa ajili ya kujitambulisha.

Dkt. Shekalaghe amesema kuwa lengo la kukutana na Jaji Mkuu ni kujitambulisha rasmi kwake, kufuatia kuteuliwa kwake hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kushika nafasi hiyo. 

"Mhe. Jaji Mkuu, nimefika kujitambulisha kwako rasmi kwa nafasi yako kama Kiongozi Mkuu katika Mhimili huu wa Mahakama. Lakini pia kama kuna lolote niweze kupokea maelekezo. Ndilo lengo hasa kubwa kwa nini nimefika hapa," ameeleza Katibu Mkuu huyo.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe (aliyesimama) akijitambulisha mbele ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 15 Julai, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji
 
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo (kulia) akizungumza jambo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe aliyemtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 15 Julai, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akizungumza jambo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe (wa kwanza kulia kwa Jaji Mkuu) wakati alipomtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 15 Julai, 2026 kwa lengo la kujitambulia. Wa kwanza kushoto kwa Jaji Mkuu ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, kushoto kwa Jaji Kiongozi ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, anayefuatia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi, anayefuatia ni Katibu wa Jaji Kiongozi, Mhe. Mussa Hamza .

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto), Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (katikati) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi wakifuatilia mazungumzo wakati Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (wa kwanza kushoto) akiwa pamoja na 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 15 Julai, 2026.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimuonesha Dkt. Shekalaghe (katikati) picha za ukutani za Majaji Wakuu waliopita (hawapo katika picha) wakati Katibu Mkuu huyo alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe  alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 15 Julai, 2026.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa kwanza kushoto), Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (wa pili kulia), Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya na wa pili kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimuaga Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe mara baada ya kujitambulisha kwa Jaji Mkuu leo tarehe 15 Julai, 2026.