Jumatano, 15 Aprili 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAPOKEA KOMPYUTA MPAKATO 150

·       Ni kutoka Wizara ya Katiba na Sheria

·       Wizara hiyo yaipatia pia Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Magari Matano na Kompyuta Mpakato 30

·       Mahakama na Tume… waishukuru Wizara ya Katiba na Sheria kwa vitendea kazi hivyo

Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Mahakama ya Tanzania leo tarehe 15 Aprili, 2026 imekabidhiwa jumla ya Kompyuta Mpakato 150 kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, vifaa ambavyo vimekabidhiwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Dkt. Juma Homera (MB) ikiwa ni jitihada za Serikali za za kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuimarisha utoaji  haki kwa ufanisi.

Hafla ya kukabidhi Kompyuta hizo iliyofanyika katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma imeenda sambamba na kukabidhi jumla ya magari Matano na Kompyuta mpakato 30 vifaa ambavyo wamepatiwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi, Mhe. Dkt. Homera amesema tukio hilo linathibitisha dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuendelea kuimarisha Sekta ya Sheria ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wananchi wote na kwa wakati bila ya ubaguzi wa aina yoyote.

“Serikali chini ya uongozi mahiri wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeweka kipaumbele katika kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa kuhimiza kutumia fursa iliyopo ya maendeleo ya TEHAMA nchini katika kuimarisha mifumo ya kitaasisi ya utoaji wa huduma kwa umma kwa njia za kielekroniki. Fursa ya maendeleo ya TEHAMA iliyopo ni kichocheo kikuu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Hivyo, kwa upande wa Sekta ya Sheria, matumizi ya TEHAMA siyo ya hiari tena, bali ni hitaji la msingi katika kujenga Mfumo wa Haki unaokwenda sambamba na mahitaji ya karne ya 21,” amesema Mhe. Dkt. Homera.

Waziri huyo amesema kuwa, katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara hiyo yenye dhamana ya kusimamia masuala ya Katiba na Sheria, wameendelea kushirikiana na Taasisi zake katika kutekeleza majukumu yake, hususan kuimarisha mifumo ya utoaji haki na usimamizi wa haki nchini. Ametaja Taasisi hizo ni pamoja na Mahakama ya Tanzania ambayo imepewa jukumu la utoaji haki chini ya Ibara ya 1 07A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977; na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inayohamasisha hifadhi ya haki za binadamu, kwa kufanya uchunguzi na kupokea malalamiko ya uvunjaji wa haki za binadamu chini ya Ibara ya 1 29 na 1 30 ya Katiba.

Mhe. Dkt. Homera ameongeza kuwa, katika kutekeleza majukumu yake, Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora zinakutana na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta hivyo kushindwa kufikia malengo waliyojiwekea kiutendaji.

Hivyo, katika kutumia fursa hizo Wizara imekuwa ikitafuta na kuingia makubaliano na wadau mbalimbali wa maendeleo kutekeleza miradi na afua mbalimbali zinazolenga kuimarisha utendaji wa Sekta ya Sheria. Katika hili, Wizara kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) imeona ni vyema kuziwezesha taasisi hizi kwa kuzipatia vitendea kazi vichache ili kuimarisha uwezo wa kitaasisi katika kuhudumia watanzania,” ameeleza.

Amesema, ana imani kwamba, vitendea kazi hivyo vitaenda kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa majukumu na kuleta matokeo chanya na hatimaye kuwezesha Sekta ya Sheria kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

Aidha, Waziri huyo amebainisha kuwa, lengo la upatikanaji na utumiaji wa vifaa hivyo ni kutekeleza kwa vitendo Sera ya Serikali ya kujenga Mfumo Jumuishi, shirikishi na unaotumia teknolojia katika utoaji wa huduma za kisheria.

Mhe. Dkt. Homera ametoa rai kwa wanufaika wa magari na vifaa hivyo kuhakikisha vinatunzwa na kutumiwa vizuri ili kufanikisha malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amesema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha utendaji kazi wa Mahakama, hususan katika matumizi ya mifumo ya kielektroniki.

Ameeleza kuwa, kompyuta hizo zitachangia kurahisisha usajili wa mashauri, usimamizi wa kumbukumbu pamoja na uendeshaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (video conference), hatua itakayopunguza mlundikano wa kesi na kuongeza uwazi katika utoaji wa haki.

Aidha, amebainisha kuwa, matumizi ya TEHAMA ni nyenzo muhimu katika kuongeza kasi na ufanisi wa utoaji wa huduma za Mahakama nchini.

Kwa mujibu wa Msajili Mkuu, hatua hiyo pia itawezesha wananchi kupata huduma za Mahakama kwa urahisi zaidi bila kulazimika kufika mahakamani, ikiwemo kufungua mashauri, kufanya malipo na kufuatilia mwenendo wa mashauri.

Ameongeza kwamba, maboresho ya kimahakama yamechangia kupungua kwa muda wa usikilizwaji wa mashauri. Aidha, amebainisha kuwa tayari maboresho ya kimahakama yameanza kuleta matokeo chanya, ambapo muda wa wastani wa kusikiliza na kuamua mashauri umepungua hadi siku 68 mwaka 2025 kutoka viwango vya mwaka 2015.

Amesema kuwa, katika Mahakama za Mwanzo, ambazo hushughulikia zaidi ya asilimia 70 ya mashauri yote, muda wa usikilizwaji umepungua hadi wastani wa siku 30, hali inayoonesha kuongezeka kwa ufanisi katika utoaji wa haki.

Katika hafla hiyo, Msajili Mkuu aliambatana na baadhi ya Viongozi na Maofisa kutoka Makao Makuu ya Mahakama. Viongozi wengine walioshiriki ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mhe. Franklin Rwezimula, Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bw. Patience Ntwina, Viongozi na watumishi wengine wa Wizara hiyo pamoja na watumishi wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.



Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Dkt. Juma Homera (MB) (kushoto) akikabidhi Kompyuta Mpakato kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma wakati wa hafla ya kukabidhi magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama walioambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya wakati wa hafla ya Kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Sehemu ya Watumishi wa Wizara ya Katiba na Sheria waliohudhuria katika hafla ya Kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (MB) akizungumza jambo wakati wa 
hafla ya Kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa neno la shukrani wakati wa  
hafla ya kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (MB) (katikati). Wa pili kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mhe. Franklin Rwezimula, wa pili kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, wa kwanza kushoto ni Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bw. Patience Ntwina na wa kwanza ni kulia ni Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania, Bw. Shigeki Komatsubara wakiwa katika .


Meza kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mahakama walioambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa pili kulia) wakati wa 
hafla ya kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.




Picha za pamoja wakati wa 
hafla ya kukabidhi Magari na Vitendea Kazi kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi  Homera akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Magari matano yaliyokabidhiwa kwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyofanyika leo tarehe 15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.




Picha ya magari matano waliyokabidhiwa ume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Wizara ya Katiba na Sheria.



Wiki ya Usuluhishi Dodoma

WANANCHI WAMIMINIKA MAHAKAMA KUU KUPATA ELIMU

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma

Wananchi kutoka viunga mbalimbali jijini Dodoma, jana tarehe 14 Aprili 2026, walijitokeza kwa wingi kushiriki na kujifunza kuhusu njia mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Katika mwendelezo huo, wananchi, wanasheria na watumishi kutoka Taasisi tofauti wameonekana kuguswa na umuhimu wa usuluhishi, wakionesha hamasa kubwa ya kufahamu namna bora ya kutatua migogoro kwa njia ya maelewano badala ya kutumia njia ya kawaida, ambayo ni ndefu mahakamani.

Watoa elimu wameweka wazi kuwa usuluhishi si tu unapunguza muda na gharama, bali pia hujenga mahusiano bora kati ya wahusika, hali inayochangia kudumisha amani katika jamii. Aidha, Usuluhishi unasaidia kupunguza msongamano wa mashauri mahakamani na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Baadhi ya washiriki wamesema elimu hiyo imekuwa chachu ya mabadiliko ya fikra, wakiahidi kuwa mabalozi wa kueneza uelewa wa usuluhishi katika maeneo yao, ili jamii iweze kunufaika zaidi na fursa hii muhimu.

Kwa mtazamo mpana, juhudi hizi zinaakisi dhamira ya dhati ya Mahakama ya Tanzania ya kuhakikisha haki haitafutwi kwa gharama kubwa au kwa muda mrefu, bali inapatikana kwa njia rahisi, ya haraka na yenye kuzingatia utu.

Kwa kasi hii, ni wazi kuwa usuluhishi si mbadala tena bali ni suluhisho halisi la migogoro katika jamii ya sasa.

Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi yanayoendelea kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026 kwenye maeneo mbalimbali nchini. Maadhimisho hayo yanaenda sambamba na kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania.”


Wananchi kutoka sehemu mbalimbali Mkoa wa Dodoma na Mikoa Jirani wakimsikiliza kwa makini mtoa mada ya usuluhishi, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe. Thurston Kombe, wakati wa kutoa elimu ya usuluhishi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma (IJC).

 



Mkazi wa Dodoma, Bi. Ashura Salumu, akiuliza swali wakati wa utoaji wa elimu ya usuluhishi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

 Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kongwa, Mhe. Sarah Mwalilino (aliyesimama) akitoa elimu kwa Wananchi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


USULUHISHI UNAJENGA JAMII YENYE AMANI NA UTENGAMANO; JAJI MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amesema kuwa, usuluhishi wa migogoro ya kijamii ni njia bora ya utatuzi na kujenga jamii bora yenye amani, utengamano na maendeleo ya kudumu.

Mhe. Mahimbali aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa uzinduzi rasmi wa Wiki ya Usuluhishi nchini uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Akizungumza na umati wa wananchi na wadau mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria uzinduzi huo, Jaji Mahimbali alisema kuwa, Mahakama ya Tanzania imezindua rasmi Wiki ya Usuluhishi ambayo itafanyika kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026 ambapo tayari Mahakama imefanya uchambuzi wa mashauri yote yanayofaa kufanyiwa usuluhishi na kwamba wadaawa wote wanaohusika na mashauri hayo wamepewa taarifa na wako tayari kwa usuluhishi.

“Moja ya malengo yetu ni kuwajengea uelewa wananchi kwamba si lazima mashauri yaliyoletwa Mahakamani yaishe kwa uamuzi wa Mahakama, hivyo mashauri yote yanayofaa kufanyiwa usuluhishi yatafanyiwa hivyo, kwahiyo wadau wa Usuluhishi hususan pande mbili zinazohusika katika migogoro wanapaswa kuwa tayari kwa majadiliano” aliongeza Jaji Mfawidhi huyo.

Vilevile Mhe. Mahimbali aliainisha kwamba, malengo yanayotarajiwa kufikiwa baada ya kukamilika kwa Wiki ya Usuluhishi kuwa ni pamoja na: Kujenga uelewa na umuhimu wa usuluhishi katika utatuzi wa migogoro, kuelimisha umma juu ya umuhimu na fursa zinazotokana na matumizi ya njia ya usuluhishi, kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo na kuongezeka kwa wigo wa usuluhishi wa migogoro iliyopo katika hatua mbalimbali mahakamani.

Malengo mengine ya Wiki ya Usuluhishi katika Kanda ya Arusha ni kupunguza msongamano wa migogoro ambayo inaweza kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi na kuweka misingi ya maridhiano ya kudumu, kwamba usuluhishi lazima ujikite katika makubaliano ya pande zote mbili.

Yapo manufaa mengi yanayopatikana pale migogoro ya wananchi inapotatuliwa kwa njia ya usuluhishi. Manufaa hayo ni pamoja na ongezeko la uwajibikaji wa watoa huduma za usuluhishi na wenye migogoro kwa lengo la kumaliza kwa haraka, kwa njia ya amani na utulivu. Pia, kuongezeka kwa soko la ajira kupitia kutambulika kwa wasuluhishi binafsi ambao ni watu wasio Mahakimu au Majaji lakini wana maarifa na weledi wa kutosha katika kutatua migogoro katika jamii.

Kwa Kanda ya Arusha, Wiki ya Usuluhishi itasaidia kuchochea mazingira wezeshi ili kuokoa na kufungua rasilimali zilizoshikiliwa kutokana na uwepo wa migogoro kama vile mashauri ya kibenki na migogoro ya kibiashara. Pia, usuluhishi wa haraka wa migogoro utawawezesha wananchi kutumia muda mchache mahakamani na kupata muda mwingi wa kushiriki kazi za kiuchumi, kuvutia wawekezaji na kuharakisha maendeleo ya watu na Taifa kwa ujumla.

Hali kadhalika, moja ya faida kubwa inayopatikana kwa kutatua migogoro ya kijamii kwa njia ya usuluhishi ni kuongezeka kwa imani ya wananchi kwa mfumo wa utoaji haki nchini. Wananchi wanapoona migogoro yao inatatuliwa kwa haraka, kwa haki na kwa njia ya amani, imani yao kwa Mahakama na Mfumo mzima wa Utoaji Haki inaongezeka kwa kiasi kikubwa.

Aidha, uwepo wa Wiki ya Usuluhishi nchini ni kutekeleza jukumu la Kikatiba chini ya Ibara ya 107 A (2) (d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) ambapo kupitia Wiki ya Usuluhishi, Mahakama inatekeleza jukumu lake la kukuza na kuendesha usuluhishi nchini.                              


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akizungumza na umati wa wananchi na wadau mbalimbali waliohudhuria uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi nchini uliofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Dkt. Kassian Mshomba akifafanua jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi katika Kanda ya Arusha uliofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mkoa wa Arusha, Wakili Msomi Hamisi Mkindi akichangia jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi katika Kanda ya Arusha uliofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Mmoja wa Wakazi wa Arusha aliyehudhuria uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi Arusha, Bw. Mustafa Kiago akichangia jambo wakati wa uzinduzi rasmi wa Wiki ya Usuluhishi uliofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Umati wa wananchi na Wadau mbalimbali waliofika kwenye uzinduzi rasmi wa Wiki ya Usuluhishi  Kanda ya Arusha uliofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Jumanne, 14 Aprili 2026

WASHIRIKI WA MAFUNZO KIGOMA WAPITISHWA KWENYE SHERIA, KANUNI NA MIONGOZO YA USULUHISHI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile amewapitisha washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi kuhusu sheria, kanuni na miongozo ya usuluhishi inayotoa mwelekeo wa utatuzi na  utambuzi wa kiini cha mgogoro inayofikishwa Mahakamani.

Mhe. Rwizile ametoa mada hiyo leo tarehe 14 Aprili, 2026 mkoani Kigoma kwa washiriki 16 wa mafunzo ya  usuluhishi wa migogoro yanayoendelea Mahakama Kuu Kigoma. 

“Tunazo sheria, kanuni na miongozo ya usuluhishi inayotoa welekeo wa utatuzi na utambuzi wa kiini cha mgogoro inayofikishwa Mahakamani, hata hivyo zipo hatua nne muhimu za usuluhishi zikifuatwa na kuzingatiwa na msuluhishi yeyote basi mgogoro uliopo mbele ya msuluhishi utaleta matokeo mazuri,” amesema Jaji Rwizile.

Ameongeza kuwa, ni muhimu kwa Msuluhishi kuwa na ufahamu mkubwa wa kanuni za usuluhishi ili kufikia makubaliano ya usuluhisi wa mgogoro, na kwamba wasifungwe na uelewa mbalimbali unaotokana na kanuni, sheria na miongozo mingine inayotumika katika usuluhishi wa migogoro kutoka nchi mbalimbali duniani bali wajielekeze kwenye utatuzi wa mgogoro husika.

Kwa upande wake Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa amewasilisha mada juu ya utambuzi wa kiini cha mgogoro, ikiwa ni kuwasikiliza walengwa wa mgogoro, nini wanahitaji kila mmoja katika mgogoro huo, kisha kuwapa nafasi kila mdau kuweza kutoa mawazo ya kile anachohitaji katika kusuluhisha mgogoro huo, kuwapatia kila mmoja kile ambacho ataridhika nacho ili kumaliza migogoro iliyopo mahakamani.

Aidha, alifafanua mbinu mbalimbali wanazopaswa kutumia wasuluhishi hao ili kuendelea kuwa bora katika usuluhishi, hasa kutengeneza mazingira rafiki kwa walengwa wa mgogoro, mpangilio wa kuketi katika chumba cha usuluhishi, utoaji wa taarifa juu ya kila kitu kitakachofanyika katika usuluhishi, kuwaeleza malengo ya usuluhishi huo na jukumu lao la msingi katika usuluhishi, kuwatambua wadau wenye mgogoro husika bila upendeleo wala ubaguzi ikiwa ni sambamba na matarajio yao kupitia usuluhishi huo, kuwapa muda sawa wa kuzungumza, kujieleza na uwazi usio na mashaka.

Leo ni siku ya pili ya mafunzo kwa washiriki hao, wakiendelea kunolewa kwa ufasaha ili waje kuwa Wasuluhishi maridadi wa kutatua migogoro iliyopo hapa nchini.

Washiriki wa mafunzo hayo ni Mahakimu wa Kanda za Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.



Sehemu ya washiriki wa mafunzo  ya Usuluhishi wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikiwasilishwa na moja ya Mkufunzi wa mafunzo ya usuluhishi leo tarehe 14, Aprili 2026 Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akiwasilisha mada leo tarehe 14 Aprili, 2026 katika Mafunzo ya Usuluhishi yanayoendelea kufanyika Mahakama Kuu Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akisisitiza jambo wakati akiwasilisha mada kwa washiriki wa Mafunzo ya Usuluhishi leo tarehe 14 Aprili, 2026.

Washiriki wa mafunzo wakitoa mfano halisi wa jinsi Msuluhishi na Mdau wanaweza kukaa na kuzungumza juu ya jambo fulani linalohitaji usuluhishi.


Moja ya picha inayotumika na wakufunzi katika chumba cha kutolea mafunzo ya usuluhishi Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

JAJI MKUU AKUTANA NA RAIS MSTAAFU WA JAMHURI YA MALAWI

Na WAANDISHI WETU-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, leo tarehe 14 Aprili, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Malawi na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Dkt. Lazarus Chakwera, kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
















MAHAKAMA DODOMA YAANZA MAADHIMISHO YA WIKI YA USULUHISHI

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu, Dodoma

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, imeanza rasmi maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi yanayoendelea kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026, sambamba na Kanda nyingine nchini.

Maadhimisho hayo yanaenda sambamba na kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania.”

Katika kipindi hiki, uongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, ukiongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, kwa kushirikiana na Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, umejipanga kikamilifu kuhakikisha Wananchi wanapata huduma kwa urahisi, haraka na kwa ufanisi zaidi.

Kwa upande mwingine, dawati maalumu la huduma limeanzishwa katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma kwa ajili ya kupokea malalamiko na kutoa mwongozo kwa Wananchi, huku mazingira maalumu yakiandaliwa ili kuhakikisha usuluhishi unafanyika kwa ufanisi na faragha.

Katika kuifikia jamii kwa upana zaidi, Mahakama pia imeendesha kampeni ya utoaji elimu kwa umma kupitia vyombo vya habari, ikiwemo Radio Mwangaza na Radio Family FM, ambapo Wananchi wameelimishwa juu ya umuhimu wa kuchagua usuluhishi kama njia ya haraka, nafuu na yenye tija katika kutatua migogoro.

Wananchi waliojitokeza kushiriki maadhimisho hayo wamepata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu dhana ya usuluhishi, kuuliza maswali na kupata majibu ya kitaalamu kuhusu masuala ya kisheria yanayohusu utatuzi wa migogoro nje ya mfumo wa kawaida wa Mahakama.

Kwa ujumla, Wiki ya Usuluhishi siyo tu jukwaa la kutoa elimu, bali ni fursa muhimu kwa jamii kubadili mtazamo kuhusu namna bora ya kushughulikia migogoro yao. Kupitia njia ya usuluhishi, Wananchi wanahimizwa kuchagua amani, maelewano na suluhisho la haraka badala ya migogoro mirefu inayoweza kuleta madhara kwa pande zote.

Mahakama ina matarajio kuwa Wananchi wataendelea kujitokeza kwa wingi kutumia fursa hii adhimu, siyo tu wakati wa maadhimisho haya, bali hata baada yake, kwa lengo la kujenga jamii yenye mshikamano, haki na ustawi wa kudumu.

Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiwa katika picha ya pamoja pamoja na Viongozi wa Dodoma baada ya kutembelea dawati maalumu lililowekwa kwa ajili ya Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.  Katikati ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Kirefu, anaefuatia kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe Abraham Mwampashi, anaefuatia wa kwanza kulia kwake Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe Mustafa Ismail, wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo, wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, wa tatu kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Agatha Chugulu na wa nne kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitili.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe. Judith Baligenge akiwa katika studio za Radio Mwangaza iliyopo Jijini Dodoma akitoa elimu kuhusu usuluhishi.

 Wakili wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Mwita Mohere, akiwa katika studio za Radio Mwangaza iliyopo Jijini Dodoma akitoa elimu kuhusu usuluhishi.


 

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kongwa, Mhe. Sarah Mwalilino (wa kwanza kulia) akiwa ameambatana na Wakili wa Serikali Mwandamizi Wizara ya Katiba na Sheria, Bi Zerafina Gotora wakiwa katika Studio za Family Fm zilizopo Ilazo Jijini Dodoma wakitoa elimu kuhusu usuluhishi.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) na kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule na kushoto kwake ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe. Thurston Kombe, wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa Wiki ya usuluhishi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.