Ijumaa, 6 Machi 2026

HUDUMA ZA MAHAKAMA KUU KATAVI KUANZA WAKATI WOWOTE KUANZIA SASA

Na. Ally Ramadhani - Katavi

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mkoa wa Katavi Mhe. Silivia S. Lushasi tarehe 5 Machi, 2026 amefanya kikao na wadau wa Mahakama cha maandalizi ya uanzishaji wa masjala ndogo ya Mahakama Kuu, Kanda ya Katavi na kuwapongeza wadau kwa ushiriki wao kwa kuhakikisha masjala hiyo inaanza kuwatumikia wananchi.

Akizungumza katika kikao, Mhe. Lushasi amesema, taarifa itatolewa kwa wananchi muda wowote ya kuanza kupata huduma za Mahakama Kuu Mara tu itakapokuwa imetangazwa rasmi kwenye Tangazo la Serikali.

Naibu Msajili huyo amesema, Mahakama Kuu itakapoanza mkoani Katavi, mashauri yote yaliyo sajiliwa Mahakama Kuu Sumbawanga yataendelea huko huko ila yale mapya yatasikiliziwa masjala mpya ya Katavi na kuongeza kuwa, dira ya Mahakama ya Tanzania ni kutoa haki kwa wakati na mapema kadri iwezekanavyo.

Aidha, Mhe. Lushasi aliongeza kuwa, wadau waliopo kwenye mnyororo wa haki Jinai inabidi kuendana na kasi ya Mahakama kidijitali kwa kuboresha na kuimarisha miundombinu.

Mhe. Lushasi ameongeza kuwa, nguzo ya pili ya Mpango Mkakakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania inasisitiza utoaji haki kwa wakati. Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huo kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hiyo.

Kwa upande wake, Mwakilishi kutokea TANESCO Mhandisi Victor Ng’wigulu alisema, kwa sasa Taasisi zote za umma ikiwemo Mahakama tumeziweka kwenye kipaumbele cha kwanza katika kuhakikisha zinapata nishati ya umeme.

“Tuliwashauri Mahakama ya Tanzania Mkoa wa Katavi wapate kangavuke (Standby Generator) na nitumie nafasi hii kuwashukuru kwa kupata kangavuke zuri na la kisasa tumeliona lipo, hivyo ikitokea changamoto za umeme wa TANESCO naamini shughuli za kimahakama zitaendelea ila tumejipanga vizuri kama TANESCO Mkoa kuendelea kutoa huduma bora kwa Taasisi zote.

Wadau wa Mahakama waliohuduria kwenye kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi ni pamoja na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Takukuru, Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali Sumbawanga, Ofisi ya Magereza Katavi, Chama cha wanasheria Tanganyika (TLS) Katavi, Baraza la Ardhi na Nyumba, Hifadhi ya Taifa Katavi, Afisa Ustawi wa Jamaii Katavi, Mahakimu Wafawidhi, Tanesco, Tume ya Usuluhishi na Upatanishi (CMA) Katavi, Ofisi ya Mganga Mkuu Katavi, Mwanasheria wa Halmashauri za Mpanda, Mlele na Tanganyika.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Silivia S. Lushasi (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama ya Tanzania mkoa wa Katavi mara baada ya kikao cha wadau wa Mahakama.

Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Katavi Bi. Flavia F. Shiyo akichangia hoja wakati wa Kikao cha Wadau wa Mahakama Katavi.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Silivia S. Lushasi (katikati waliokaa mbele) akiongea na Wadau wa Mahakama ya Tanzania mkoa wa Katavi kwenye kikao cha wadau wa Mahakama.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


Alhamisi, 5 Machi 2026

TANZIA

Bi. Lightness Elia Kiula wakati wa uhai wake.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam Kisutu inasikitika kutangaza kifo cha Ofisa Tawala Mwandamizi, Bi. Lightness Elia Kiula, aliyekuwa akihudumu katika Mahakama ya Wilaya Kigamboni.

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Bi. Athanasia Kabuyanja, kifo hicho kimetokea tarehe 04 Machi, 2026 katika Hospitali ya Moyo ya Jakaya (JKCI) iliyopo Upanga Dar es Salaam.

Bwana ametoa, Bwana ametwaa, Jina Lake lihimidiwe. Amen.

MWANANCHI MKOA WA GEITA WAPATIWA ELIMU KUHUSU UTEKELEZAJI WA AMRI ZA MAHAKAMA

Wananchi wa Mkoa wa Geita wamenufaika na mpango wa utoaji elimu kwa Umma ulioratibiwa na Mahakama Kuu Masjala ya Geita.

Utoaji huo wa elimu ulifanyika tarehe 03 Machi, 2026 katika Ukumbi wa Elimu kwa Umma, Kituo Jumuishi (IJC) Geita.

Mada iliyowasilishwa ilikuwa Utekelezaji wa Amri za Mahakama, ikiwa na lengo la kuwajengea wananchi uelewa kuhusu taratibu za kisheria baada ya hukumu kutolewa.

Elimu hiyo ilitolewa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, ambaye alieleza kwa kina hatua zinazofuatwa katika utekelezaji wa amri za Mahakama mara baada ya hukumu kutolewa.

Katika mafunzo hayo, Mhe. Muchunguzi alifafanua kuwa utekelezaji wa amri za Mahakama hufanyika kwa njia mbalimbali, ikiwemo kukamata na kuuza mali za mdaiwa, kuamrisha jambo fulani litendeke ili kumpatia mdai haki yake, au utekelezaji wa kifungo cha madai pale inapobidi. Alieleza kuwa taratibu zote hufuata misingi ya kisheria ili kuhakikisha haki inatendeka kwa pande zote zinazohusika.

Aidha, wananchi walipata fursa ya kuuliza maswali kuhusu migogoro ya ardhi, zuio litolewalo na Mahakama na masuala ya dhamana katika mikopo ya benki.

Akijibu hoja hizo, Mhe. Muchunguzi alisisitiza kuwa endapo mali itauzwa kwa thamani kubwa kuliko deni, kiasi kinachozidi hurudishwa kwa mdaiwa.

Aliongeza kuwa migogoro ya ardhi inapaswa kuanzia Baraza la Ardhi la Kata kwa usuluhishi na baadaye kama hawajaelewana kupeleka mgogoro wa ardhi kwenye Baraza la Ardhi Nyumba na Makazi Wilaya kwa mujibu wa sheria.

Alisema kwamba ni kosa la kukaidi amri ya Mahakama, ambapo anayekiuka zuio halali anaweza kuchukuliwa hatua za kisheria.

Wananchi walieleza kufurahishwa na elimu hiyo, wakisema imewasaidia kuelewa haki na wajibu wao katika masuala ya kisheria. Mahakama imeueleza Umma huo kuwa itaendelea kutoa elimu kama hiyo mara kwa mara ili kuongeza uelewa wa sheria na kuimarisha upatikanaji wa haki kwa jamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akiwahutubia na kuwasalimia wananchi, huku akiwaalika wale wote wenye changamoto au wanaohitaji msaada wa kisheria kujitokeza ili wasikilizwe na kupatiwa msaada stahiki.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilayya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi akiendelea kutoa elimu kwa wananchi Mkoa wa Geita.

Wananchi Mkoa wa Geita wakiendelea kupata mafunzo katika ukumbi wa mafunzo wa Mahakama Kuu Geita.

Hakimu Mfawidhi, Mhe. Mujuni Muchunguzi akiwa katika picha ya pamoja na Wananchi baada ya mafunzo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

FANYENI KAGUZI ZENYE TIJA NA TATHMINI YA UTENDAJI KAZI; JAJI MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amewaagiza Viongozi wa ngazi mbalimbali za Mahakama katika Kanda  hiyo kuhakikisha wanafanya kaguzi zenye tija katika Mahakama zilizo chini yao ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya utendaji kazi katika vituo hivyo lengo likiwa ni kuongeza ufanisi wa kazi za Mahakama.

Mhe. Mahimbali aliyasema hayo katika Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Kanda ya Arusha kilichoketi hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha ambapo aliwaambia wajumbe wa kikao hicho kuwa ni lazima juhudi zao zijikite katika kuibua mikakati bunifu inayolenga kufanikisha malengo ya Mahakama ya kutoa haki kwa wananchi mapema ipasavyo na kwa ubora unaotakiwa.

“Tunapokagua Mahakama zetu, lazima tubainishe mafanikio, changamoto, njia au mbinu za kuondokana na changamoto hizo na kutoa mapendekezo ya namna ya kuboresha utendaji kazi katika mahakama zetu. Ni kwa kufanya kazi namna hiyo ndio tutafikia malengo ya kuondokana na mashauri ya mlundikano yasiyo na sababu za msingi,” alisisitiza Jaji Mahimbali.

Mhe. Mahimbali aliongeza kuwa, kwa kufanya hivyo kutasaidia na kusukuma usikilizaji wa mashauri unaojikita katika kumaliza idadi kubwa ya mashauri kuliko mashauri yanayosajiliwa.

Akiwasilisha Taarifa ya hali ya mashauri katika Kanda ya Arusha, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati aliwaeleza wajumbe kuwa, kasi ya usikilizaji wa mashauri ni nzuri na kwamba wameweza kumaliza kiasi kikubwa cha mashauri ya mlundikano na mikakati madhubuti imewekwa kuhakikisha kasi ya umalizaji mashauri inaongezeka na hivyo kudhibiti kiasi cha mashauri mlundikano mapya.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa na Mhe. Massati, hadi kufikia tarehe 26 Februari, 2026, Mahakama Kuu Arusha ilikuwa imebakiwa na mashauri mlundikano sita tu, na Kanda nzima ya Arusha zikiwemo Mahakama za chini kulikuwa na mashauri mlundikano 15 pekee. 

Aliongeza kuwa, idadi hiyo ya mashauri mlundikano inatarajiwa kupungua kutokana na mikakati iliyowekwa na Kanda ya Arusha kumaliza mashauri kwa wakati.

Naye Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama aliwasilisha taarifa ya utendaji ambayo kwa kiasi kikubwa ilionesha mafanikio makubwa katika kuweka mazingira wezeshi kuwezesha usikilizaji mashauri kufanyika katika mazingira mazuri na rafiki zaidi.

Bi. Kapama alibainisha baadhi ya mafanikio hayo kuwa ni pamoja na ukarabati wa Mahakama za Mwanzo Likamba na Nkoanrua zilizopo wilayani Arumeru zilizokuwa zimefungwa kwa kipindi kirefu na hatimaye kufanikiwa kuzifufua na mpaka sasa zinafanya kazi.

Aidha, katika kikao hicho Wajumbe wamesisitizwa kuwa wabunifu zaidi katika usimamizi wa vituo vyao vya kazi na kuhakikisha huduma za Mahakama kwa wananchi zinakuwa bora zaidi na kutolewa mapema ipasavyo.

Kikao hicho cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilihudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka Mahakama Kanda ya Arusha ikiwemo wajumbe wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya Arumeru, Longido, Karatu, Monduli na Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akiongoza Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati (aliyesimama) akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha. Walioketi kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Dkt. Kassian Mshomba na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mhe. Erasto Philly.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama akiwasilisha Taarifa ya Utendaji wakati wa Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilichoketi hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Wajumbe mbalimbali waliohudhuria Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha wakifuatilia kinachojiri katika kikao hicho.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)

 

 

 

 

 



Jumatano, 4 Machi 2026

ENDELEENI KUISHI VIAPO VYENU MKIZINGATIA MILA NA DESTURI; JAJI MKUU

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewaapisha Mahakimu Wakazi wapya wawili, Mhe. Moonlight Martin Tupa na Mhe. Deus Philo Nyimbo na kuwataka Mahakimu hao kuviishi viapo vyao huku wakizingatia mila na desturi za maeneo wanayofanyia kazi.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 04 Machi, 2026 mara baada ya zoezi la uapisho wa Mahakimu hao lililofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua kiapo au viapo, na kuna viongozi wanatajwa moja kwa moja kwamba wao kabla ya kuanza majukumu yao watalazimika kula kiapo na moja ya wanaotajwa katika Katiba hiyo ni Majaji na Mahakimu, tuliokwisha kula kiapo maneno haya ya kiapo tunayafahamu, wasiwasi wangu ni kwamba kama tunayatilia maanani,” amesema Jaji Mkuu huku akiwasisitiza Mahakimu hao kuendeleza tamaduni za maeneo husika.

Akizungumzia kuhusu uadilifu, Mhe. Masaju amesema kuwa, uadilifu unaanzia kwenye kiapo ambacho wametumia kuapa hivyo ni vema wakakiheshimu na kukitekeleza kwa uadilifu ili wasiwe wamelitaja bure Jina la Mwenyezi Mungu na kuwa heshima haitokani na cheo bali heshima inatokana na huduma.

“Uadilifu unaanzia kwenye kiapo, juzi nilipoongea na wenzenu niliwaambia tusimchukulie Mungu poa, Mungu mwenyewe anatamka, anaelekeza kwamba jina lake lisitamkwe bure. Kwenye hicho kiapo mlipokuwa mnamaliza mmesema Eee Mwenyezi Mungu nisaidie, uadilifu wenu unaanzia hapa kwenye kiapo kile,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameongeza kwamba, Mahakama ina kiapo ambacho ikiwa watakikiuka watawajibishwa wasipozingatia kiapo hicho Mungu atawaadhibu mwenyewe hapa duniani au baada ya kufa ikiwa hawatatubu.

“Kwa kawaida kiapo kina adhabu na sisi hapa tuna adhabu mbili, moja ukikiuka hicho kiapo unaweza kushtakiwa kwa kosa la jinai ukawajibishwa, cha pili unawajibishwa na Mwenyezi Mungu ambaye umeapa kwake na ndiye unayemuomba akusaidie, na yeye ana namna nyingi ya kuwawajibisha, anaweza akakusubiri wakati umeshakufa kama hukutubu akakuwajibisha huko huko, lakini mara  nyingi  huwa naona wala rushwa na wale wanaokiuka maadili anawawajibisha hapa hapa duniani kwanza, watambue wajibu wao wamrudie Mwenyezi Mungu” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, kila anayehitaji kuheshimiwa anapaswa kuheshimika pia kutambua kuwa jamii itamheshimu kwa namna anavyotenda na si kwa nguo anazovaa na cheo alichonacho, akiongeza kuwa hawahitaji kujitutumua bali wawe wanyenyekevu na kuwaheshimu watu wengine katika sehemu zao za kazi na jamii yote kwa ujumla.

Akizungumza kuhusu kutambua mila na desturi za jamii za Kitanzania, Mhe. Masaju amesema kwamba, kila Hakimu anapaswa kuzingatia na kuziheshimu mila na desturi kama ambavyo Katiba inazitambua na kuziheshimu Katiba za Kiislamu, akisisitiza kuwa Mahakama za mwanzo zinalazimika kukaa na washauri wa Mahakama kwenye mashauri yanayohisha sheria za kimila au Kiislamu.

“Katiba inatambua hizi mila na desturi za Tanzania, inatambua viapo, sisi tutatakiwa kufuata mila na desturi, na ndio maana tuna Mahakama hapa zinatambua hizi mila na desturi, na Mahakama za Mwanzo mnapokuwa mnatekeleza majukumu yenu katika yale mashauri yasiyokuwa ya jinai, ni pamoja na kuzingatia hizo mila, desturi na sheria za Kiislamu,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, si lazima mtu kufanya kazi katika sehemu aliyozaliwa na kwamba wapo watakaoenda kufanya kazi mijini au vijijini hivyo ni lazima wazitambue mila na desturi za mahali husika, ili waweze kutatua kwa haki migogoro mbalimbali inayohusu mila na desturi au migogoro katika ndoa za kiislamu kulingana na mila na desturi husika.

Aidha Jaji Mkuu ameeleza kwamba, katika kutatua migogoro hiyo pale watakapoona inafaa, watapaswa kukaa na washauri wa Mahakama ambao watawashauri kwa hekima katika kuzingatia mila na desturi katika kutoa hukumu huku akishauri Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto kujumuisha masuala ya mila na desturi ili zitambulike na kurahisisha wakati wa utoaji hukumu.

Ametaja uhumimu wa Washauri wa Mahakama kuwa ni pamoja na kutoa ushauri ili kutoa hukumu ya haki kwa kuzingatia jamii, kusaidia kutatua migogoro ya kijamii ya kiislamu katika masuala ya ndoa pamoja na kutoa ushauri wa kimila kulingana na mazingira, pia kuwashirikisha katika maamuzi pale Mahakama itakapoona kwa maslahi ya haki inalazimu kufanya huvyo, au pale Mahakama itakapoombwa na mmoja wapo wa wadaawa katika shauri husika.

Amesema kuwa ikiwa Wazee wa mila na Machifu  watatungiwa sheria ya kuwatambua, pamoja na wajibu mwingine, wajibu wao utakuwa ni ule ulioelezwa katika Ibara ya 19(3) na Ibara ya 30(2)(a) akiyataja majukumu hayo kuwa ni usalama wa jamii, amani katika jamii na umoja wa kitaifa, kadhalika watasaidia katika utatuzi wa migogoro ya ardhi, masuala ya ndoa, ulinzi na utunzaji wa  mazingira, huku akitilia mkazo kuwa watu hao ni muhimu katika utatuzi wa migogoro kwa sababu jamii inayowazunguka inawasikiliza na kuwaheshimu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju ameeleza majukumu ya Serikali za Mitaa ambazo zina wajibu wa kuhimiza utawala wa sheria katika jamii, amani katika jamii na umoja wa kitaifa huku akieleza kuwa, Serikali za Mitaa pia zinapaswa kutekeleza shughuli zake ipasavyo kwa kutumia demokrasia, kuhakikisha utekelezaji wa sheria na ulinzi wa wananchi akirejea Ibara ya 146(1) pamoja na Ibara ya 146(2)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaeleza wazi madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa.

Kadhalika, Jaji Mkuu amesema kuwa, mategemeo ya Mahakama ni ya kwanza kutii kiapo kama ambavyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anasisitiza juu ya kuishi viapo sambamba na kuziheshimu mila na desturi za Tanzania, huku akiwakumbusha pia kuzingatia mila katika mavazi kwa wanawake kujistiri kwa heshima na wanaume kuvaa mavazi yenye hadhi na heshima.

Akizungumza kuhusu uwajibikaji, weledi na uadilifu, Mhe. Masaju amewahimiza kuwajibika ipasavyo kama ambavyo imeelekezwa katika Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo unahimiza kuhusu uwajibikaji na kuweka wazi kuwa kila mtu ana wajibu wa kushiriki na kujituma kwa uaminifu katika kazi halali za uzalishaji mali, kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji mali ya binafsi na yale ya pamoja yaliyowekwa na sheria.

“Ibara ya 25 inatukumbusha kuhusu uwajibikaji, Ibara ya 25(1) inasema kwamba kazi pekee ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii, ndilo chimbuko la ustawi wa Wananchi na kipimo cha Utu……...”

Ameongeza kuwa kazi ya kuhukumu waliyopewa sio ya shuruti hivyo wanapaswa kujituma wenyewe, kuwa na nidhamu ya kazi ili kufikia malengo na kuwa wazembe watashauriwa ili kubadilika au kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

“Hii kazi ya kuhukumu tuliyopewa si ya shuruti, ndio maana tunataka muwajibike mjitume ninyi wenyewe, muwe na nidhamu ya kazi, mfikie malengo, wale wazembe tutajaribu kuwashurutisha kwa kuwashauri, lakini ikishindikana watawawajibishwa kwa kushindwa kutekeleza wajibu wao na tunayo sheria inatuongoza,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amerejea Ibara ya 25(3)(d)(i)(ii)(iii) na kueleza kuwa, kazi ni majukumu yoyote ambayo ni sehemu ya majukumu ya kawaida ya kuhakikisha ustawi wa jamii, ujenzi wa Taifa kwa mujibu wa sheria pamoja na jitihada za kutumia uwezo wa kila mtu kufanya kazi kwa ajili ya kuimarisha jamii na uchumi wa Taifa na kuhakikisha maendeleo na tija ya Kitaifa.

Hafla ya Uapisho huo imehudhuriwa na sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Tanzania pamoja na Mahakimu Wakazi wengine 90 ambao walikuwa wakiendelea na mafunzo elekezi baada ya uapisho wao tarehe 23 Februari, 2026.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Mahakimu Wakazi wapya wawili aliowaapisha leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Katika hafla hiyo pia walikuwepo Mahakama Wakazi wapya 90 wanaoendelea na Mafunzo elekezi baada ya kuapishwa hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mpya, Mhe. Moonlight Martin Tupa (wa kwanza kulia) akila kiapo cha uadilifu mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele) leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wanaoshuhudia wa pili kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya na wa pili kulia ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert.



Mahakimu Wakazi wapya walioapishwa wakisaini viapo vya uadilifu mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati wa hafla ya uapisho iliyofanyika leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akisaini viapo vya Mahakimu Wakazi aliowaapisha leo tarehe 04 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mahakimu Wakazi wapya waliokuwa wakiendelea na mafunzo elekezi pamoja na walioapishwa wakisikiliza kwa makini hotuba ya Jaji Mkuu wa  Tanzania, Mhe. George Masaju baada ya zoezi la kuwaapisha Mahakimu wapya wawili leo tarehe 04 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi wapya aliowaapisha leo tarehe 04 Machi, 2026. Kulia ni Mhe. Moonlight Martin Tupa na kushoto ni Mhe. Deus Philo Nyimbo.


Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto (wa kwanza kushoto), Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto),  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Massabo (katikati), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma (wa pili kulia) na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Kuu, Mhe Abdi Kagomba (wa kwanza kulia) wakifuatilia tukio la uapisho wa Mahakimu Wakazi wapya (hawapo katika picha).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)

JAJI KIONGOZI ASISITIZA UADILIFU, UELEDI NA UWAJIBIKAJI KWA MAHAKIMU

        Awakumbusha maneno ya Hayati Benjamin William Mkapa kuhusu bidii, maarifa na kufanya kazi kwa matokeo

Na. Halima Mnete – Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewataka Mahakimu kote nchini kuzingatia misingi ya uadilifu, ueledi na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao, akisisitiza kuwa bila kuzingatia nguzo hizo, haki haiwezi kutendeka kwa ufanisi.

Akizungumza mapema leo tarehe 4 Machi, 2026 katika hafla ya kuapishwa kwa Mahakimu Wakazi wawili (2) iliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma, ambapo kiapo hicho kilisimamiwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Mhe. Dkt. Siyani awakumbusha maneno ya Hayati Benjamin William Mkapa kuhusu bidii, maarifa na kufanya kazi kwa matokeo.

Akizungumza mara baada ya kuapishwa kwa mahakimu hao, Mhe. Dkt. Siyani alisema kazi ya uhakimu si ya mazoea bali ni dhamana kubwa kwa umma, inayohitaji mtu mwenye maadili thabiti na uwezo wa kitaaluma.

“Sasa mambo haya yanabeba msingi kwa kazi mnayoenda kuifanya. Mtumishi yeyote wa Mahakama au wa Umma, hususani Hakimu au Jaji, anapaswa kuyachukua na kuyazingatia mambo haya matatu kama sehemu ya maisha yake. Kazi ya uhakimu bila uadilifu hautofika popote, bila ueledi na kuwajibika hamtafika popote,” alisema Mhe. Dkt. Siyani.

Aliongeza kuwa, Mahakimu hao wameomba wenyewe nafasi hiyo na kwa mapenzi ya Mungu wamefanikiwa kuipata, hivyo wanapaswa kuitumikia kwa moyo wa kujituma na kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao.

Katika kuimarisha msisitizo wake, Jaji Kiongozi alinukuu maneno ya Rais wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Benjamin William Mkapa, aliyewahi kusema kuwa njia ya maendeleo imejaa jasho na vumbi, na kusisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii, maarifa, ubunifu na kujituma.

Aidha, Jaji Kiongozi alikumbusha kauli ya hayati Mkapa kwamba kilicho muhimu si muda anaotumia mfanyakazi kazini, bali ni kiasi cha kazi anachoweza kuifanya katika muda aliopewa. Alisema kauli hiyo ina umuhimu mkubwa hata kwa Mahakama ya Tanzania, hasa katika kuhakikisha mashauri yanamalizika kwa wakati na kwa ubora unaotarajiwa.

“Katika kuwajibika, si tu kufanya kazi kwa bidii, lazima mfanye kazi kwa ufanisi. Matokeo yanapatikana kwa kufanya kazi kwa weledi na kwa akili. Unaweza kufanya kazi usiku na mchana lakini usimalize kesi kama haufanyi kazi kwa mpangilio na kwa ufanisi,” alisisitiza.

Mhe.Dkt. Siyani aliwakaribisha rasmi Mahakimu hao katika utumishi wa Mahakama ya Tanzania na kuwahakikishia kuwa, licha ya kutopata fursa ya kukutana nao wakati wa mafunzo yao, watakutana katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku wakiwa sehemu ya taasisi inayosimamia haki na ustawi wa jamii.

Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akitoa nasaha kwa Mahakimu Wakazi Wapya walioapishwa leo tarehe 04 Machi, 2026 jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. George Masaju (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu Wapya walioapishwa leo tarehe 04 Machi, 2026. Wengine ni Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa kwanza kushoto) na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Cho cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).

Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Cho cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) (wa kwanza kushoto), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma Mhe. Dkt Juliana Massabo (katikati), Jaji Mfawidhi wa Kituo cha Usuluhishi cha Mahakama ya Tanzania Mhe. Zahra Maruma (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Kuu Mhe Abdi Kagomba (wa kwanza kulia). wakifuatilia tukio la uapisho wa Mahakimu Wakazi (hawapo pichani).



Sehemu ya Mahakimu Wakazi wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. George Masaju (hayupo pichani)

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



 

WATUMISHI KUPATA HUDUMA BORA ZA KIBENKI NA MIKOPO YA RIBA NAFUU

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya.

Afisa wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Bi. Agatha Masao kutoka Makao Makuu ya benki hiyo amefanya kikao na watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya na kusema kuwa, benki hiyo imejipanga kuwahudumia watumishi wa Mahakama kwa kutoa huduma bora za kifedha pamoja na mikopo yenye riba nafuu.

Kikao hicho kilifanyika tarehe 02 Machi 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya, chini ya Mwenyekiti ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga.

Bi. Agatha Masao aligusia kuhusu makubaliano ya kibiashara na uwekezaji yaliyoingiwa kati ya Mahakama ya Tanzania na Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), yenye lengo la kuimarisha ushirikiano na kuboresha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa watumishi wa Mahakama.

Aidha, alifafanua kuwa makubaliano hayo yanawawezesha watumishi kupata mikopo yenye riba nafuu pamoja na unafuu wa huduma za kifedha, hususani kwa watumishi watakaopitisha mishahara yao kupitia benki hiyo. Pia alibainisha uwepo wa huduma ya mikopo ya haraka kupitia simu za mkononi (salary advance) inayofikia hadi asilimia 50 ya mshahara.

Vilevile, Bi. Agatha alitoa elimu kuhusu bidhaa nyingine zinazotolewa na Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), ikiwemo uwezeshaji wa watumishi wa Mahakama kununua hatifungani za Serikali, ambapo mtumishi hulipia asilimia 25 pekee, huku asilimia iliyobaki ikifadhiliwa na benki hiyo.“Matatizo yako mwachie NBC, wewe songa na maisha.” Alisisitiza Bi. Agatha

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, alitoa shukrani zake za dhati kwa ujio wa maafisa hao kutoka NBC kwa elimu waliyoitoa kwa watumishi.

“Ninawashukuru sana kwa ujio wenu. Bidhaa zenu ni nzuri, na nina imani mna lengo jema. Ni matumaini yangu kuwa watumishi wetu watanufaika zaidi na huduma mnazotoa,” alisema Mhe. Tiganga.

Aidha, kikao hicho kilihusisha watumishi kutoka Mahakama Kuu Mbeya, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mahakama ya Wilaya Mbeya, pamoja na Mahakama za Mwanzo zilizopo Mbeya Mjini.

Kwa upande mwingine, kikao hicho pia kilitumika kuwakaribisha watumishi wa ajira mpya waliopangiwa vituo mbalimbali mkoani Mbeya katika kada tofauti, zikiwemo maafisa ugavi, wapishi, wasaidizi wa ofisi, madereva na walinzi.

Katika hafla hiyo ya ukaribisho, watumishi walikata keki kwa pamoja kuonesha umoja na mshikamano miongoni mwa watumishi wa kada zote. Pia, pongezi zilitolewa kwa watumishi waliokuwa na siku za kuzaliwa katika miezi ya Januari na Februari, kama ilivyo desturi ya Kanda hiyo kila inapofika mwisho wa mwezi.

Ugeni huo wa maafisa wa NBC uliongozwa na Afisa Utumishi wa Mahakama ya Tanzania kutoka Makao Makuu, Bi. Viviene Kishembo, aliyeambatana na Meneja wa NBC Tawi la Mbeya, Bw. Asumisye Edward; Meneja wa NBC Tawi la Mwanjela, Bw. Khalid Omary; Afisa Mikopo kutoka NBC Tawi la Mbeya, Bw. Alex Elias; pamoja na maafisa wengine.

Sehemu ya Maofisa kutoka Benki ya Taifa ya Biashara NBC waliokwenda kutoa elimu ya masuala ya kifedha kwa watumishi wa Mahakama Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe, Joachim Tiganga (watatu kulia) akitoa neno la shukurani kwa Maofisa wa NBC katika kikao hicho, wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (wa kwanza kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa pili kulia), wanne kulia ni Mtendaji wa Mahakama kuu kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti.

Afisa Utumishi Mahakama ya Tanzania Makao Makuu Bi. Viviene Kishembo (aliyesimama) akitambulisha ugani aliokuja nao.

Sehemu ya watumishi katika kikao hicho.

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika kikao hicho.


Sehemu ya watumishi walioshiriki katika kikao hicho.

Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo akilishwa keki kwa niaba ya Majaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akimlisha keki mmoja wa watumishi waliozaliwa kati ya mwezi Januari na Februari ambaye ni Mwandishi mwendesha ofisi Mahakama ya Wilaya Mbeya.

Watumishi wa Mahakama waliozaliwa mwezi Januari na Februari wakikata keki ya pamoja

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


JAJI MFAWIDHI MBEYA ASHIRIKI MAZISHI YA MTUMISHI WA MAHAKAMA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga ameshiriki mazishi ya aliyekuwa Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese, Kanda ya Morogoro, Mhe. Asajile Joshua Mhando. Mazishi hayo yamefanyika tarehe 20 Februari 2026 katika Kijiji cha Vwawa, Wilaya ya Mbozi, Mkoa wa Songwe, ambako ndiko nyumbani kwa familia ya marehemu Asajile Mhando.

Awali, mwili wa marehemu uliagwa na viongozi pamoja na watumishi mbalimbali wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya katika viunga vya Mahakama hiyo, wakiwemo Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania waliokuwa wakiendelea na vikao vya mashauri ya rufani katika Kanda hiyo na baadaye mwili wa marehemu ulisafirishwa kwenda Kijiji cha Vwawa, Mkoa wa Songwe, kwa ajili ya kupumzishwa kwenye nyumba yake ya milele.

Akizungumza wakati wa mazishi hayo, Mhe. Tiganga, alitoa salamu za pole kwa mjane, familia na ndugu wa marehemu, pamoja na kutoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro na Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe kwa mchango wao mkubwa katika kufanikisha kumpumzisha aliyekuwa mtumishi hodari wa Mahakama ya Tanzania.

“Ninafahamu hiki ni kipindi kigumu kwa mjane, familia na hata watumishi wenzake, lakini hatuna budi kukubali kwani ni mapenzi ya Mwenyezi Mungu; aliyemtoa ndiye aliyemtwaa. Wajibu wetu sisi ni kumuombea ili Mwenyezi Mungu ampumzishe kwa amani,” alisema Mhe. Tiganga.

Aidha, Mhe. Tiganga aliwasisitiza wanafamilia kufuatilia stahiki za marehemu kutoka kwa mwajiri mara baada ya kumaliza msiba, ikiwemo kukaa kikao cha familia na kumteua msimamizi na mfuatiliaji wa stahiki hizo.

Kwa upande wa Uongozi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Morogoro ulitoa shukrani zao kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, pamoja na Uongozi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, kwa ushirikiano mkubwa waliouonesha katika kumpumzisha aliyekuwa mtumishi mwenzao kutoka Kanda ya Morogoro.

Mhe. Asajile Joshua Mhando alifariki Dunia mchana wa tarehe 17 Februari 2026 katika Hospitali ya Platinum, mjini Morogoro, alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kujisikia vibaya akiwa kazini. Marehemu atakumbukwa kwa ucheshi wake, busara, unyenyekevu na ari ya kuchapa kazi, kwani hadi umauti unamfikia hakuwa na shauri lolote la mlundikano; alikamilisha mashauri yote aliyopangiwa kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akizungumza machache katika mazishi hayo.

Viongozi, Majaji wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya wakitoa pole kwa wafiwa na kuaga mwili wa Marehemu Mhe. Asajile Mhando katika viunga vya Mahakama Kuu Kanda Mbeya walipopita katika Kanda hiyo wakitokea Mkoani Morogoro

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika Mazishi hayo.


Mwili wa aliyekuwa hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese Kanda ya Morogoro Mhe. Asajile Joshua Mhando ukiagwa huko kijijini kwao Vwawa wilaya ya Mbozi mkoa wa Songwe.


Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama kutoka Morogoro, Mbeya na Songwe walioshiriki mazishi hayo wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wapili kushoto waliosimama mbele)

Sehemu ya waombolezaji katika mazishi hayo.




Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama kutoka Morogoro, Mbeya na Songwe walioshiriki mazishi hayo wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wapili kushoto kwa waliokaa mbele)

Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya wakitoa pole kwa wafiwa na kuaga mwili wa Marehemu Mhe. Asajile Mhando katika viunga vya Mahakama Kuu Kanda Mbeya walipopita katika Kanda hiyo wakitokea Mkoani Morogoro






Mwili wa aliyekuwa hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese Kanda ya Morogoro Mhe. Asajile Joshua Mhando ukiagwa huko kijijini kwao Vwawa wilaya ya Mbozi mkoa wa Songwe.