Jumatatu, 23 Februari 2026

ZINGATIENI USALAMA, MAADILI, AMANI, UMOJA KATIKA JAMII: JAJI MKUU

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Mahakimu Wakazi wapya wa Mahakama za Mwanzo kuzingatia usalama, maadili na umoja katika kutimiza majukumu yao huku wakimtanguliza Mungu mbele kama walivyoapa katika viapo vyao.

Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 23 Februari, 2026 mara baada ya kuwaapisha Mahakimu Wakazi wa Mahakama za Mwanzo wapya 90 katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Ninyi ambao mmeapishwa leo hamkuapa mbele yangu mimi, mlikuwa mnaapa kwa Mwenyezi Mungu, nimeona huwa mmebeba hivyo vitabu wengine walishikilia Biblia wengine Quran Takatifu, mlivyokuwa mnaapa sikusikia mkisema eee Jaji Mkuu nisaidie, kila mmoja alisema Ee Mwenyezi Mungu nisaidie kwa kadri mlivyokula hivyo viapo njooni mviishi, yale maneno mliyokuwa mnakula yapo kwenye Ibara ya 107A (1) na Ibara ndogo ya kwanza na Ibara ndogo ya pili a na b lakini yapo pia katika Ibara ya 107B nendeni mkayaishi,”amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumza baada ya zoezi la uapisho, Mhe. Masaju amesisitiza kuwa dhamana ya utoaji haki ni jukumu zito linalohitaji nidhamu, uaminifu na weledi wa hali ya juu na kueleza kuwa Mahakimu hao wanapaswa kufanya kazi kwa kuzingatia misingi ya sheria, kuepuka upendeleo na kuhakikisha kuwa yale wanayotaka kutendewa nao wawatendee wengine vivyo hivyo.

Akizungumza kuhusu uadilifu katika kazi, Mhe. Masaju amewaasa Mahakimu hao kutopokea wala kutoa rushwa kwa sababu rushwa huchangia kwa kiasi kikubwa kuporomosha maadili ya utumishi na kwamba sifa kubwa ya Mahakimu hao inapaswa kuwa unyenyekevu na kuongeza kuwa kadri wanapokuwa na ukubwa wa madaraka ndivyo hivyohivyo kiwango chao cha unyenyekevu kinapaswa kuongezeka na wawe watumishi wa watu wote.

“Kwenye Quran Tukufu Sura ya pili Aya ya 188 inasema hivi wala msiliane mali zenu kwa batili kinyume cha haki na kuzipeleka kwa Mahakimu ili mpate kula sehemu ya mali ya watu kwa shamba na hali mnajua, amesisitiza Jaji Mkuu.”

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju ameweka wazi kuwa, watumishi wanapaswa kuwa mfano kwa watu wengine hasa kwa kukiishi kiapo cha maadili ya kazi na kwamba yeyote atakayekiuka maadili na sheria za kazi Mahakama haitasita kumchukulia sheria na kumuwajibisha Mahakamani huku akieleza wazi kuwa, sifa ya Mahakama inaharibika pale tu watumishi wanapokiuka maadili ya utumishi na wanaposhiriki katika vitendo vya rushwa hivyo wajue kuwa Serikali inawatazama lakini Mungu pia anawatazama.

Kadhalika Jaji Mkuu amewataka Mahakimu hao kutofungwa na Masharti ya kiufundi kupita kiasi hali ambayo itadhoofisha utendaji wao wa kazi huku akiwasisitiza kwamba wana wajibu wa kutekeleza majukumu yao kama nguzo ya kutoa haki kwa jamii inayowatazama na kuwategemea.

Sambamba na hayo, Mhe. Masaju amewaasa Mahakimu hao kutotumia vibaya uhuru wa Mahakama kwa kuingiza uzembe na kukiuka Katiba na Sheria huku akiwataka wafanye tafiti za kutosha kabla ya kufanya maamuzi.

Kuhusu suala la mlundikano wa mahabusu, Jaji Mkuu ameeleza kuwa mshtakiwa ana haki ya kupata dhamana hivyo mtu anaweza kupata dhamana kwa kudhaminiwa au kujidhamini mwenyewe.

Aidha Jaji Mkuu amebainisha kwamba, Mahakama ni Mhimili muhimu wa Dola unaosimamia haki na kudumisha amani katika jamii, hivyo kila Hakimu ana wajibu wa kulinda heshima, hadhi na taswira ya Mahakama mbele ya wananchi.

Katika hatua nyingine Mhe. Masaju amewataka Mahakimu hao kujenga umoja na mshikamano katika maeneo yao ya kazi na kuwahimiza kujifunza kwa watumishi watakaowakuta katika maeneo watakayopangiwa kazi, huku akisisitiza kuwa nguvu ya Mahakama ipo katika ushirikiano, uwajibikaji na kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni na taratibu zilizowekwa.

Ameongeza kuwa, kila Hakimu anapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii kwa matendo na maamuzi yake, huku akitumia maarifa na uzoefu wake katika kuchambua masuala na kutoa maamuzi sahihi kwa kuzingatia sheria.

Akisisitiza kuhusu utumiaji wa Mahakama, Jaji Mkuu amewashauri Mahakimu hao kutoruhusu Mahakama kutumia vibaya wala kukubali mahairisho ya kesi yasiyo na msingi, pia wahakikishe mashauri yaliyo mbele yao yanahitimishwa mapema ipasavyo kwa kuzingatia sheria.

“Sasa nina ushauri mwingine ninapoenda kumaliza moja msiruhusu Mahakama zitumike vibaya kupitia mashauri yaliyopo mbele yenu, mbili msikubali mahairisho ambayo hayana msingi yasiyokuwa na sababu za msingi, tatu hitimisheni mashauri yaliyoko mbele yenu mapema iwezekanavyo kwa kuzingatia Katiba na sheria sio kulipua” amesisitiza.

Mhe. Masaju amezungumzia pia kuhusu watu wa makundi maalumu katika jamii kama watoto, wajane na yatima katika jamii. Pamoja na hayo ameeleza kuwa, katika kupunguza urasimu kwenye masuala ya mirathi, kuleta uwazi na kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za mirathi na kuweka udhibiti dhidi ya wasimamizi wa mirathi wenye dhamira ya kutumia vibaya fedha na mali za marehemu, kunahitajika kinga mahsusi kuhusu makundi hayo.

“Katika kanuni ya tano katika kesi za makundi maalum tumetunga kanuni hapo… tumeweka mwongozo unaosimamia mashauri haya yanayowahusu watu wenye mahitaji maalumu ni yatima, ni mjane hana mtetezi, ni watoto ni wanawake katika jamii nyingine ambayo wanawake wanapuuzwa, Jaji au Hakimu anayesikiliza shauri linalohusiana na hao watu katika makundi hayo katika hatua zote anapokuwa anasikiliza mashauri hayo ikijumuisha wakati wa usajili wa shauri lake wakati wa kusikiliza na kuliamua anapaswa ayape kipaumbele mashauri ya aina hii na hata sisi tunafanya hivyo,” amesisitiza.

Aidha, Jaji Mkuu amewasisitiza Mahakimu hao kuhusu umuhimu wa kuwa na uadilifu pamoja na kuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu kwa ufanisi, akieleza kuwa, wananchi wanatarajia kuona mashauri yakisikilizwa na kuamuliwa mapema ipasavyo bila ucheleweshaji usio wa lazima huku akiweka wazi kuwa kuchelewa kwa haki kunaweza kuathiri imani ya wananchi kwa Mahakama.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo, wakila kiapo cha uaminifu mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati wa hafla ya uapisho wao iliyofanyika leo tarehe 23 Februari, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo, wakisaini viapo vyao vya uadilifu mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati wa hafla ya uapisho iliyofanyika leo tarehe 23 Februari, 2026 katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

 


 Mahakimu Wakazi wapya wakila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto). Aliyesimama katika ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya na kushoto kwake ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akisaini viapo vya Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo, aliowaapisha leo tarehe 23 Februari, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Jijini Dodoma. Aliyesimama kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

 


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo mara baada ya kuwaapisha leo tarehe 23 Februari, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo mara baada ya zoezi la uapisho lililofanyika leo tarehe 23 Februari, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wa pili kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher, Mohamed Siyani, wa tatu kushoto wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Imani Abood, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa pili kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya na wa kwanza kulia ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wazazi na walezi waliohudhuria katika Hafla ya Uapisho wa Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo iliyofanyika leo tarehe 23 Februari 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Dini waliohudhuria katika hafla ya uapisho wa Mahakimu Wakazi wapya wa Mahakama za Mwanzo iliyofanyika leo tarehe 23 Februari, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

Sehemu nyingine ya Mahakimu Wakazi Wapya wa Mahakama za Mwanzo wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele katikati) mara baada ya zoezi la uapisho lililofanyika leo tarehe 23 Februari, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

JAJI MKUU APONGEZA USHIRIKIANO WA WADAU KATIKA UONDOSHAJI MASHAURI YA BIASHARA, UCHUMI...

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewapongeza Wadau wa Mahakama kwa ushirikiano wa dhati waliotoa uliouwezesha Mhimili huo kuondosha jumla ya mashauri 2,973 yanayohusu biashara, uchumi na kodi na kufanikiwa kuokoa Shilingi za Kitanzania Trioni 13.1 katika kipindi kifupi.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 23 Februari, 2026 wakati wa Mkutano wa Utekelezaji wa Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Wadau Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara uliofanyika kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

“Natambua na kuthamini mchango wa kila mmoja,” amesema Jaji Mkuu huku akiwataka Wadau hao kila mmoja kwa nafasi yake kuifanyia kazi mikakati waliokubaliana katika kikao hicho.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewasisitiza Wadau wa Mahakama kuendelea kudumisha Utawala wa Sheria, na kutoa angalizo kwamba bila kufanya hivyo migogoro itazidi.

Mhe. Masaju ameeleza kuwa, Mahakama inaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha huduma ya utoaji haki inatolewa mapema ipasavyo ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua ya kugatua madaraka ya Mahakama ya Rufani.

“Mpango wa kugatua Mahakama ya Rufani bado upo palepale, matarajio yaliyopo ni kwamba usikilizaji wa mashauri utaongezeka baada ya ugatuzi wa Mahakama ya Rufani,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju amesema kwamba, katika kuhakikisha kuwa Mahakama inaendelea kutoka haki mapema ipasavyo kama ambavyo Dira yake inataka, imepanga pia kusikiliza mashauri ya ardhi katikati ya mwezi Machi mwaka huu.

Kwa upande mwingine, Jaji Mkuu ameipongeza Benki ya Tanzania kwa kuandaa Waraka unaotoa mwongozo kwa Taasisi za Kibenki. Vilevile amewataka Madalali wa Mahakama kuwa na maadili katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mkakati wa Uondoshaji wa Mashauri yanayohusu biashara, uchumi na kodi uliofanyika kuanzia tarehe 03 Novemba, 2025 hadi tarehe 15 Desemba, 2025, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya amesema mkakati huyo umekuwa wa mafanikio makubwa.

“Tuliweza kumaliza mashauri 2,973, sawa na zaidi ya asilimia 93 ya mashauri tuliyokuwa tumepanga kuyasikiliza. Hili ni jambo la kujivunia kwa Mahakama na Wadau wote walioshiriki,” amesema Mhe. Nkya.

Msajili Mkuu ameeleza kuwa, usikilizaji wa mashauri ulifanyika kupitia vikao maalum pamoja na utaratibu wa kawaida wa Mahakama na kwamba kutokana na baadhi ya mashauri kumalizika mapema, Mahakama ilipata fursa ya kuongeza mashauri mengine 1,068, yakiwemo 256 yaliyohusu masuala ya hifadhi ya jamii na kufanya jumla ya mashauri yaliyosikilizwa kufikia 3,196.

Ameongeza kwamba, thamani ya fedha iliyohusika katika mashauri yaliyomalizika ilifikia shilingi trilioni 13.1, kiwango ambacho ni kikubwa zaidi ya kile kilichokuwepo awali.

Katika kuimarisha utatuzi wa migogoro, Msajili Mkuu ameeleza kuwa Mahakama pia ilitumia njia ya usuluhishi ambapo mashauri 18 yalimalizika kupitia utaratibu huo, huku mashauri 25 yakiombwa na Wadaawa kupelekwa kwenye usuluhishi nje ya Mahakama.

Kadhalika, Mhe. Nkya amesema kuwa, vikao maalum vya Wadau vimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza mlundikano wa mashauri, ambapo hadi kufikia mwisho wa mwaka 2025, mashauri yaliyokuwa yamelundikana yalikuwa asilimia tano ya mashauri yote.

Katika Mkutano huo Wadau mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria wamepata fursa ya kuwasilisha kwa kueleza kuhusu utekelezaji wa uondoshaji wa mashauri hayo ambao kwa ujumla wamepongeza jitihada zilizofanywa na Mahakama kufuatia uondoshaji wa mashauri hayo.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

Wadau wengine waliyowasilisha taarifa za utekelezaji wa mikakati ni pamoja na Baraza la Ushindani, Benki Kuu ya Tanzania, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Chama cha Madalali wa Mahakama, TISEZA na wengine.

Mkutano huo wa Wadau uliofanyika leo ni mwendelezo wa kikao kilichofanyika tarehe 08 Oktoba, 2025, ambapo pamoja na mambo mengine Wadau hao pamoja na Mahakama walikubaliana kukutana mara nne kwa mwaka ili kufuatilia utekelezaji wa mikakati waliyojiwekea.

Mikakati waliokubaliana katika kikao hicho kilichofanyika leo ni pamoja na Ushirikiano unaotolewa katika usikilizwaji wa mashauri ya ardhi, biashara, mabenki na ushindani wa kibiashara utolewe pia katika utekelezaji (execution) wa hukumu.

Mahakama na wadau wa mnyororo wa haki waimarishe mawasiliano na mahusiano miongoni mwao, kwa lengo la kuchukua hatua za haraka pale changamoto zinazoathiri upatikanaji haki mapema zinapojitokeza.

Wadau wa mnyororo wa haki wapatiwe elimu kuhusu sheria, kanuni na taratibu zinazoratibu uendeshaji wa mashauri ya ardhi, biashara, ushindani wa kibiashara, kodi na mabenki na uwekezaji ili kupata uelewa wa pamoja.

Kila taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki Mahakamani iwajibike ipasavyo kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia Katiba, sheria na maadili ya utumishi wa taasisi husika.

Mkakati mwingine ni Wadau wote wa Mahakama wenye mashauri mbele ya Mahakama wanapaswa kuhudhuria na kuyaendesha mashauri yao kikamilifu ili kuwezesha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Mwingine ni Kila taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki iimarishe ufuatiliaji wa mashauri na uwajibikaji kwa kutoa taarifa sahihi na za mara kwa mara kuhusu utekelezaji wa mikakati tuliojiwekea na kutumia mifumo inayosomana ili kuimarisha mawasiliano na mahusiano.

Aidha, Mkakati mwingine ni kila taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki Mahakamani iweke utaratibu mahususi wa ndani ya taasisi utakaofanikisha utekelezaji wa mikakati tunayojiwekea na kadhalika.

Wadau waliohudhuria katika Mkutano huo ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Fedha, Benki Kuu, Tume ya Mipango, Baraza la Ushindani, Baraza la Rufani la Kodi, Umoja wa Mabenki, Chemba ya Taifa ya Biashara, Mamlaka ya Uwekezaji wa Maeneo Maalum ya Kiuchumi, Chama cha Wanasheria Tanganyika, pamoja na Wadau wengine wanaohusika na masuala ya kiuchumi na biashara.

 

MAHAKAMA TANZANIA YAJIVUNIA MAFANIKIO YA USIKILIZAJI MASHAURI

  • Zaidi ya asilimia 93 ya mashauri yaliyopangwa yamalizwa
  • Yarejesha kwenye mzunguko wa fedha trioni 13 kwa muda mfupi

 Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dodoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, leo tarehe 23 Februari, 2026, amekutana na Waandishi wa Habari katika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma na kuelezea mafanikio makubwa yaliyopatikana, ikiwemo kumaliza mashauri ya kimkakati yanayohusu biashara, uchumi na kodi yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania Trioni 13.1 katika kipindi kifupi.

Mhe. Nkya amebainisha kuwa mashauri hayo 2,973 yalisikilizwa katika ngazi mbalimbali za Mahakama kuanzia tarehe 3 Novemba hadi 15 Desemba, 2025. Amekumbusha kuwa Oktoba 8, 2025, Mahakama iliitisha kikao maalum cha wadau wa masuala ya biashara na uchumi kwa lengo la kuweka mikakati ya kusikiliza mashauri 2,128 ya kiuchumi yaliyokuwa tayari kwa usikilizaji katika ngazi mbalimbali za mahakama.

Kwa mujibu wa Msajili Mkuu, wakati huo Mahakama ya Rufani ilikuwa na mashauri 405, Mahakama Kuu mashauri 1,673, Mahakama za Hakimu Mkazi mashauri 17 na Mahakama za Wilaya mashauri 33. Jumla ya mashauri hayo yalikuwa yameshikilia kiasi cha shilingi trilioni 4.4 za kitanzania.

Amefafanua kuwa usikilizaji wa mashauri hayo ulianza Novemba 3 hadi Desemba 15, 2025, kupitia vikao maalum pamoja na utaratibu wa kawaida wa Mahakama. Kutokana na baadhi ya mashauri kumalizika mapema, Mahakama ilipata fursa ya kuongeza mashauri mengine 1,068, yakiwemo 256 yaliyohusu masuala ya hifadhi ya jamii na kufanya jumla ya mashauri yaliyosikilizwa kufikia 3,196.

“Tuliweza kumaliza mashauri 2,973, sawa na zaidi ya asilimia 93 ya mashauri tuliyokuwa tumepanga kuyasikiliza. Hili ni jambo la kujivunia kwa Mahakama na Wadau wote walioshiriki,” amesema Mhe. Nkya.

Alieleza kuwa thamani ya fedha iliyohusika katika mashauri yaliyomalizika ilifikia shilingi trilioni 13.1, kiwango ambacho ni kikubwa zaidi ya kile kilichokuwepo awali. Mafanikio hayo, yanaendana na kaulimbiu ya Siku ya Sheria ya mwaka 2026 iliyosisitiza mchango wa Mahakama katika ustawi wa jamii na maendeleo ya nchi.

Katika kuimarisha utatuzi wa migogoro, Msajili Mkuu ameeleza kuwa Mahakama pia ilitumia njia ya usuluhishi ambapo mashauri 18 yalimalizika kupitia utaratibu huo, huku mashauri 25 yakiombwa na Wadaawa kupelekwa kwenye usuluhishi nje ya Mahakama.

Mhe. Nkya alibainisha kuwa vikao maalum vya Wadau vimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza mlundikano wa mashauri, ambapo hadi kufikia mwisho wa mwaka 2025, mashauri yaliyokuwa yamelundikana yalikuwa asilimia tano ya mashauri yote. Aidha, amesema kuwa wastani wa muda wa usikilizaji ulipungua kutoka siku 96 hadi 30 katika Mahakama za Mwanzo, ambazo hushughulikia zaidi ya asilimia 70 ya mashauri yote.

Alieleza kuwa vikao hivyo hushirikisha Taasisi mbalimbali za kiserikali na binafsi zikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Fedha, Benki Kuu, Tume ya Mipango, Baraza la Ushindani, Baraza la Rufani la Kodi, Umoja wa Mabenki, Chemba ya Taifa ya Biashara, Mamlaka ya Uwekezaji wa Maeneo Maalum ya Kiuchumi, Chama cha Wanasheria Tanganyika, pamoja na Wadau wengine wanaohusika na masuala ya kiuchumi na biashara.

Msajili Mkuu ameeleza kuwa mkutano wa leo wa Wadau hao ni mwendelezo wa kikao kilichofanyika tarehe 8 Oktoba, 2025, ambapo walikubaliana kukutana mara nne kwa mwaka ili kufuatilia utekelezaji wa mikakati waliyojiwekea.

Aliongeza kuwa mbali na mashauri ya kiuchumi na biashara, Mahakama pia inaendelea kufanya tathmini ya mashauri ya haki jinai, na kikao kingine cha Wadau wa sekta hiyo kinatarajiwa kufanyika ili kupima mafanikio ya mikakati iliyowekwa awali.

Kwa ujumla, Mahakama imeonesha dhamira ya kuendelea kuboresha utoaji haki kwa wakati, kupunguza gharama kwa Wadaawa na kuimarisha mchango wake katika kukuza uchumi na maendeleo ya Taifa.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya [juu na chini] akizungumza na Waandishi wa Habari leo tarehe 23 Februari, 2026, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Katibu wa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Jovin Binshanga [kushoto] pamoja na sehemu ya Waandhi wa Bari [juu na chini] wakichukua kumbukumbu muhimu wakati wa mkutano huo. 




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

TAARIFA YA KITAALAAM YA MAFUNZO KUHUSU FIDIA KWA WAFANYAKAZI YAANDALIWA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, pamoja na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), wanakutana mjini Kibaha kuandaa taarifa ya kitaalaam ya mafunzo awamu ya kwanza kuhusu fidia kwa Wafanyakazi yaliyofanyika nchi nzima kwa nyakati tofauti.

Mafunzo hayo yalifanyika mfululizo Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia Bagamoyo tarehe 09-10 Juni 2023, Mwanza tarehe 15-16 Agosti 2023, Arusha tarehe 01-02 Desemba 2023, Songea tarehe 09-12 Februari 2024, Kigoma tarehe 19-20 April 2024, Zanzibar tarehe 19-20 Julai 2024 na Arusha tarehe 07-08 Oktoba 2024.

Akizungumza wakati anafungua kikao kazi hicho cha siku nne leo tarehe 23 Februari, 2026, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, amesema kuwa mafunzo hayo yamekuwa chachu ya kuongeza uelewa miongoni mwa Majaji, Naibu Wasajili, Wasuluhishi, Waamuzi, Watendaji wa Mahakama na Maofisa wengine wa Mahakama nchi nzima, kuhusu namna bora ya kushughulikia masuala ya fidia kwa wafanyakazi kwa mujibu wa sheria.

Huku akinukuu Wanazuoni mbalimbali, Jaji Mfawidhi amebainisha kuwa kukusanya elimu na kuiweka katika mfumo wa compendium si jambo la kawaida, bali ni jukumu la kitaaluma na la hali ya juu na kwamba ni mahali pa kupata taarifa kuhakikisha kuwa Hakimu, Mwanasheria, au mtoa huduma hafanyi kazi kwa njia ya makisio, bali ana rejea thabiti.

Miongoni mwa Wanazuoni hao ni James Boswell katika kitabu cha The Life of Samuel Johnson, Oxford World’s Classics, Ukurasa wa 1071, Blaise Pascal katika Kitabu cha The Provincial Letters, letter 16 na Francis Bacon aliandika katika kitabu cha The Essays of Counsel, Civil and Moral Studies Uk. 50.

‘Naamini itatumika kama rejea mahakamani, kwenye shughuli za WCF na Wizara kwa ajili ya mabadiliko ya sera na sheria, Vyuo na Vyuo Vikuu mbalimbali, Shule ya Sheria, Kikanda ikiwa ni pamoja na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Shirika la Kazi Duniani (ILO) na sehemu mbalimbali Duniani kama chachu ya mabadiliko ya sheria,’ Mhe. Dkt. Mlyambina amesema.

Jaji Mfawidhi amebainisha kuwa kuwa juhudi hii ya kuandaa compendium ni sehemu ya kuwapa silaha watumishi wa sheria, wakiwemo Majaji, Manaibu Wasajili, Wasuluhishi, Waamuzi na Watendaji ili waweze kubadilisha dunia ya kazi na kutoa haki kwa ufanisi zaidi kwa wafanyakazi wanaopata madhira au magonjwa wakiwa kazini.

Amemnukuu Rais wa Afrika Kusini na Mshindi wa Tuzo ya Nobel, kwa sasa Marehemu Nelson Mandela kama alivusema: 'Education is the most powerful weapon which you can use to change the world.' (Elimu ni silaha kali unayoweza kuitumia kubadilisha dunia).

Mhe. Dkt. Mlyambina amewakumbusha maneno ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliyeasisi umuhimu wa kuandika vitabu kwa ajili ya uhifadhi wa ukweli. Mwalimu alisema: 'What is written is permanent; it can be referred to, ‘akimaanisha kuwa; ‘Kilichoandikwa ni cha kudumu; kinaweza kurejelewa).

‘Kupitia compendium hii, tunajenga uhakika kwamba mafunzo yetu ya fidia hayatapotea kwenye mawazo ya muda mfupi, bali yatakuwa kumbukumbu ya kudumu itakayowalinda wafanyakazi na kuongoza watoa haki kwa miaka ijayo,’ amesema.

Ameendelea kumnukuu Mwalimu Nyerere alipokuwa anaelezea kwa nini aliamua kukusanya na kuichapisha hotuba zake za awali (1952–1965) aliwahi kusema katika kitabu chake cha Freedom and Unity: katika utangulizi (Preface), toleo la Oxford University Press (1966), ukurasa wa xvii.

Mwalimu alisema, "I have put these speeches together... primarily because I want to leave a record of the growth of our nationalist movement... We must write our own history. If we don't, others will write it for us..."

Kwa tafsiri isiyo rasmi ni; ‘Nimekusanya hotuba hizi... hasa kwa sababu nataka kuacha rekodi ya ukuaji wa harakati zetu za kitaifa... Tunapaswa kuandika historia yetu wenyewe. Kama hatutaandika, wengine wataandika kwa ajili yetu...’

‘Kwa msingi huo, kikao hiki kinabeba umuhimu mkubwa katika kuunganisha fikra, uzoefu na ushahidi wa wahanga walioshiriki katika vikao kazi, ili tuweze kuandaa rejea ya kitaalamu yenye ubora, inayostahili hadhi ya Mahakama na WCF kama Taasisi tegemeo katika utoaji wa haki na ustawi wa wafanyakazi nchini,’ Jaji Mfawidhi amesema.

Ameeleza kuwa compendium hiyo itaweka vema kumbukumbu juu ya yote yaliyojiri kabla ya mafunzo (msimamo wa sheria kufika Juni 09-10, 2023), wakati wa mafunzo (mapendekezo ya washiriki ama maamuzi ya kesi mbalimbali yaliyopelekea mabadiliko ya sheria ama kanuni wakati mafunzo yanaendelea) na nini wanapendekeza.

Mhe. Dkt. Mlyambina, kwa niaba ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ametoa shukrani za dhati kwa WCF kwa ufadhili na ushirikiano thabiti uliowezesha kufanyika kwa mafunzo hayo na sasa kikao hiki cha kuandaa compendium.

Amesema kuwa wataanza na compendium ya Kingereza kisha kuaitafsiri kwa Kiswahili kama alivyoagiza Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania wakati anafungua Kikao Kazi kati ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mfuko wa Fidia uliofanyika jijini Arusha ili Watanzania wote waweze kufaidika nayo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akizungumza wakati anafungua kikao kazi hicho.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina [katikati] akiwa katika picha ya pamoja na Mtalaam Mwelekezi, Dkt. Cornel Mtaki [kushoto] na Ofisa Sheria Mwandamizi, Bi Francisca Kweka.

Meza Kuu ikiwa kawenye picha ya pamoja na Timu ya watalaam wa kazi husika, Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Enock Matembele [wa tatu kulia], Kaimu Mtendaji, Bi. Joyce Mulugu [katikati], Naibu Msajili, Mhe. Mary Mrio [wa pili kushoto], Naibu Msajili, Mhe. Rita Tarimo [wa tatu kushoto] na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji, Mhe. Jane Masua, Mhe. Baraka Mahenge na Mhe. Suzana Mwiguru.



Kikao kazi kikiendelea [juu na chini].


 




Ijumaa, 20 Februari 2026

MAHAKAMA KUU GEITA YAFANYA BONANZA LA MICHEZO KUFUNGUA MWAKA 2026

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Timu ya Mpira wa Miguu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita, hivi karibuni ilimenyana vikali na Timu ya Polisi Mkoa wa Geita katika mchezo uliovutia hisia za mashabiki wengi, licha ya kupoteza kwa mabao 4-2.

Mchezo huo wa kirafiki ulifanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Waja uliopo eneo la Magogo, mkoani Geita. Kuanzia dakika za mwanzo, timu ya Mahakama ilionyesha kiwango cha juu cha mchezo kwa kushambulia kwa kasi na nidhamu kubwa.

Kipindi cha kwanza kilitawaliwa na Mahakama ambapo walifanikiwa kufunga magoli mawili safi yaliyoamsha shangwe kwa mashabiki wao. Ushirikiano mzuri kati ya safu ya kiungo na ushambuliaji uliwapa nafasi nyingi za kufunga, huku safu ya ulinzi ikidhibiti vyema mashambulizi ya wapinzani.

Hata hivyo, kipindi cha pili kilileta ushindani mpya baada ya Polisi Mkoa wa Geita kurejea uwanjani wakiwa na ari na mikakati mipya. Walifanikiwa kusawazisha kwa kufunga magoli mawili ya haraka na kurejesha matumaini yao. Baada ya kusawazisha, waliendelea kushambulia kwa nguvu na kuongeza magoli mengine mawili, na kufanya jumla ya magoli yao kufikia manne.

Mchezo huo ulimalizika kwa Polisi Mkoa wa Geita kuibuka na ushindi wa magoli 4–2 dhidi ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita. Licha ya matokeo hayo, Mahakama Kuu Kanda ya Geita wanastahili pongezi kwa kiwango bora walichoonesha hasa katika kipindi cha kwanza, wakidhihirisha ushindani na umoja mkubwa.

Baada ya mashindano hayo, watumishi na wadau wote walikutana kwa ajili ya kufungua mwaka. Waliohudhuria ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina na Jaji wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Giffin Mwakapeje.

Wengine ni Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Waendesha Mashtaka wa Mkoa wa Geita pamoja na Polisi Mkoa wa Geita, wakiongozwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita Safia Jongo.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna akitoa maelekezo kwa wachezaji katika Timu ya Mahakama Kanda ya Geita.

Wachezaji kutoka Polisi Geita wakijiandaa kuanza mashindano na Timu ya Mahakama Geita.

Timu ya Mahakama Kanda ya Geita ikiwa katika picha ya pamoja kabla ya kuanza mchuano na Timu ya Polisi Geita.

Innocent Mwandoje wa Timu ya Mahakama akichuana na mchezaji kutoka Polisi Mkoa Geita.

Kiungo mshambuliaji wa Timu ya Mahakama Abel Lucas Bunzali akiwa kasi kuelekea lango la Police Geita. 

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Fredrick Lukuna akiwakilibisha wageni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Kevin Mhina, akiwahimiza wadau wa Mahakama kuongeza umoja na mshikamano ili kuongeza kasi ya kutoa haki mapema ipasavyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.


Alhamisi, 19 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJADILI BAJETI YA MWAKA 2026/2027

  • Mtendaji Mkuu asema bajeti iakisi dira, kuimarisha msingi wa utoaji haki
  • Asisitiza nidhamu ya matumizi, ulinzi wa Mahakama za Mwanzo

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amesema maandalizi ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27 yanapaswa kwenda sambamba na mipango ya kimkakati ya Mahakama na kulenga kuimarisha utoaji wa haki kwa ufanisi zaidi.

Prof. Ole Gabriel alisema hayo wakati anafungua kikao cha mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 na uchambuzi wa maoteo ya bajeti ya 2026/27 kilichofanyika tarehe 16 Februari 2026 katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Alikumbusha kuwa Julai Mosi 2025, wakati utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 ulipoanza, alitoa waraka ulioelekeza masuala ya msingi ya kuzingatia, ikiwemo kudhibiti ulimbikizaji wa madeni, kuzingatia Sheria ya Bajeti Na. 11 ya Mwaka 2015 na kutohamisha fedha kutoka vifungu vya Mahakama za Mwanzo na Wilaya kwenda Mahakama za juu. Alisema maelekezo hayo yalilenga kuimarisha nidhamu ya matumizi na kuhakikisha rasilimali zinatumika kwa mujibu wa sheria.

“Kuna wakati unaweza kutamani kufanya malipo fulani, lakini kama ni nje ya utaratibu na nje ya sheria huwezi kufanya, kwa sababu itatuletea hoja za ukaguzi. Majukumu yetu tunapaswa kuyafanya kwa mujibu wa sheria na si vinginevyo,” alisema, akitoa shukrani kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Fedha na Uhasibu kwa mchango wao mkubwa katika kuhakikisha Mahakama inaendelea kuwa kinara wa Taasisi za umma zenye hati safi ya hesabu.

Alisema mafanikio hayo ni matokeo ya mipango madhubuti na usimamizi thabiti wa fedha, akisisitiza kuwa rasilimali fedha huwa hazitoshi, hivyo upangaji sahihi ni muhimu ili kufikia matarajio na Dira ya Mahakama. Alieleza kuwa mapitio ya nusu mwaka yanatoa fursa ya kujitathmini kama utekelezaji unaendana na mipango na kama Taasisi iko katika mwelekeo sahihi.

Akigusia suala la Mahakama za Mwanzo, Prof. Ole Gabriel alisema kuwa zaidi ya asilimia 70 ya mashauri huanzia katika ngazi hiyo, hivyo ni lazima zilindwe na kuimarishwa. Alibainisha kuwa katika bajeti ya sasa, Mahakama za Mwanzo zimeongezewa fedha kwa asilimia 100 kwa makusudi maalum, na akaelekeza fedha hizo ziende moja kwa moja katika ngazi hiyo.

“Haikuwa kwa bahati mbaya. Tulimaanisha kulinda Mahakama za Mwanzo kwa sababu ndizo msingi wa utoaji haki kwa wananchi wengi,” alisema.

Aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/27, Mahakama inapanga kuongeza uwekezaji katika ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama za Mwanzo ili kuboresha mazingira ya utoaji haki na kuongeza imani ya wananchi.

Kuhusu rasilimali watu, alisema Mahakama imeendelea kuiomba Serikali kuongeza watumishi kwa kuwa bila rasilimali watu ya kutosha, utoaji haki unaweza kukwama. Alieleza kuwa tayari kibali cha ajira 642 kimepatikana na mchakato wake umekamilika kupitia Tume ya Utumishi wa Mahakama, akiwashukuru watendaji wote waliohusika katika zoezi hilo.

Aidha, aliwahimiza washiriki kutoa ushiriki wa dhati katika maandalizi ya Mpango Mkakati wa Tatu wa Mahakama, akibainisha kuwa mafanikio ya mpango huo yatategemea tathmini ya mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mipango iliyopita na ushiriki wa pamoja katika kuweka mikakati mipya inayopimika.

Alieleza pia umuhimu wa kuunganisha udhibiti wa vihatarishi katika maandalizi na utekelezaji wa bajeti ili kuhakikisha mipango inayowekwa inatekelezeka bila kuathiri malengo makuu ya Taasisi.

Prof. Ole Gabriel aliwataka wasimamizi wa bajeti katika kanda na divisheni kuandaa bajeti zinazoakisi uhalisia wa mahitaji na kuongeza thamani katika utoaji wa haki.

“Jiulizeni kila wakati: Shughuli hii ninayoipangia fedha inatusaidiaje kufikia malengo yetu makuu. Tuwekeze kwenye maeneo yenye matokeo makubwa na yanayoakisi uhalisia,” alisisitiza.

Alisema maandalizi ya bajeti ni mchakato wa kimkakati unaobeba mustakabali wa Mahakama na kwamba uwajibikaji, ushirikiano na nidhamu ya matumizi ni nguzo muhimu za kuendelea kuimarisha Taasisi hiyo na kulinda imani ya wananchi.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, alisema bajeti ni nyenzo ya kimkakati inayopaswa kuakisi dira na dhamira ya Taasisi katika utoaji wa haki.

Alisisitiza kuwa maandalizi ya bajeti ya 2026/27 yanapaswa kuendana na maandalizi ya Mpango Mkakati wa Tatu wa Mahakama ili kuhakikisha mipango inayowekwa inatekelezeka na inapimika.

“Haki inapaswa kutolewa kwa wakati na kwa usawa. Hilo linahitaji mipango madhubuti na usimamizi makini wa rasilimali,” alisema.

Mhe. Nkya pia alisisitiza umuhimu wa kuendelea kupunguza mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama, pamoja na kuimarisha matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA] katika usimamizi wa mashauri ili kuongeza uwazi na ufanisi.

Kikao hicho kimeweka msingi wa mchakato wa upangaji wa rasilimali kwa mwaka wa fedha 2026/27, kikionesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuendelea kuimarisha utendaji, uwajibikaji na utoaji wa haki kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya Taifa.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akizungumza wakati anafungua kikao cha mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 na uchambuzi wa maoteo ya bajeti ya 2026/27 kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho.

Sehemu ya Watendaji na Naibu Wasajili kutoka Kanda na Divisheni [juu na picha mbili chini] wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa kikao hicho.



Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa kikao hicho [juu na chini].