Alhamisi, 14 Mei 2026

JAJI MKUU GEORGE MASAJU AMSHUKURU RAIS SAMIA KUIWEZESHA MAHAKAMA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAKE IPASAVYO

·     Alishukuru pia Bunge la Tanzania kwa ushirikiano

·     Ni wakati akifunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama

·      Aipongeza Menejimenti ya Mahakama kwa usimamizi na utekelezaji thabiti wa majukumu

· Awataka watumishi wa Mahakama kuishi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana, kusaidiana.......

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania hususan katika kuuwezesha Mhimili huo kupata fedha za kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na miradi ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia (WB).

Mhe. Masaju ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania ameyasema hayo leo tarehe 14 Mei, 2026 alipokuwa akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

“Ninamshukuru Rais Samia, Mkuu wa Nchi hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania wanavyotafuta fedha hata za mikopo kuwezesha sisi kutekeleza majukumu yetu ikiwa ni pamoja na miradi hii ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia,” amesema Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema, wakati Rais Samia aliposhiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) pamoja na hotuba ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ya mwaka huu, 2026 alielekeza kwamba wataendelea kuboresha bajeti ya Mahakama na maslahi ya watumishi kwa kadri bajeti inavyoruhusu.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amelishukuru pia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Mhe. Masaju amesema, “Nalishukuru Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu, muda mfupi uliopita wamepitisha bajeti yetu ya Mahakama ya Tanzania, bajeti ilivyoenda kule haikuwa hivyo lakini kwa sababu ya Wabunge kutambua umuhimu wa Mhimili huu wakaongeza hizo bilioni 26 kwa hiyo nawashukuru sana Viongozi hayo wa Mihimili hiyo ya Serikali kwa ushirikiano wanaotoa kwa Mahakama ya Tanzania.”

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewapongeza washiriki wote wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama kwa ushiriki wao mzuri uliosheheni mijadala yenye tija, uwazi wa hoja pamoja na mapendekezo na mikakati mbalimbali inayolenga kuimarisha utendaji wa Mahakama ya Tanzania.

“Baraza hili si tukio la kawaida pekee, bali ni sehemu muhimu ya kujitathmini kama Taasisi, kusikilizana kama familia ya Mahakama na kupanga mustakabali wa utoaji haki hapa nchini kwa pamoja na kila mmoja wetu hapa ana wajibu na anawajibika,” amesema Mhe. Masaju huku pia akiwashukuru watoa mada wote kwa mada zao zenye kujenga na kuelimisha kwa maslahi ya watumishi wa Mahakama na Taifa kwa ujumla.

“Kama nilivyowaeleza katika hotuba yangu ya ufunguzi wa baraza hili jana, hii ni mara yangu ya kwanza kuongoza Baraza Kuu la Wafanyakazi na nililenga kujifunza zaidi na hivyo, nilijikita zaidi katika kujifunza na hakika nimejifunza mambo mengi sana kutoka kwenu wajumbe na pia kwa watoa mada wetu,” ameeleza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju ametoa pongezi za dhati kwa Menejimenti ya Mahakama kwa maandalizi mazuri ya mkutano huo, usimamizi mzuri wa shughuli wezeshi zinazowezesha Mahakama kutekeleza jukumu lake la kikatiba la utoaji haki, kuendelea kusimamia mageuzi mbalimbali ya kimfumo na kiutendaji.

“Vilevile, nawapongeza Menejimenti kwa kusimamia matumizi bora ya TEHAMA katika utoaji haki, kuimarisha mazingira ya kazi kwa watumishi wa Mahakama na kipekee kabisa nipongeze mpango wa suala la ‘Supplementary’ Bima ya Afya kwa watumishi wa Mahakama ambalo litaimarisha afya za watumishi na kuongeza ufanisi kazini,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumzia kuhusu bima hiyo, Mhe. Masaju amewaomba Watumishi wa Mahakama kutumia bima hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa yaani kuimarisha afya za Watumishi.

Vilevile, amewapongeza Viongozi wote wa Mahakama katika ngazi mbalimbali kwa usimamizi wa mashauri, ufuatiliaji wa utendaji kazi, usimamizi wa maadili ya watumishi sambamba na kuendeleza nidhamu na uwajibikaji.

“Mafanikio tunayoyaona leo ndani ya Mahakama yanatokana na mshikamano, uwajibikaji, uongozi wenye maono na ushirikiano baina ya watumishi wote,” amesema.

Mbali na Viongozi, Jaji Mkuu amewapongeza pia Watumishi wa Mahakama                        kwa              kazi                      kubwa wanayoendelea kuifanya kila siku hasa kwa kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri; kupunguza mlundikano wa mashauri, kuendelea kutekeleza majukumu yao hata katika mazingira magumu.

“Aidha, niwaombe watumishi wote kuendelea kutafuta suluhisho la changamoto mnazokabiliana nazo, na zile zilizoko nje ya uwezo wenu zileteni kwetu Makao Makuu ili tuzitafutie ufumbuzi,” ameeleza Mhe. Masaju huku akiwataka Viongozi wa Mahakama kutafuta suluhu ya changamoto na hoja mbalimbali zilizowasilishwa na watumishi wakati wa Mkutano huo.

“Tumesikia vilio vya wawakilishi wa watumishi hasa katika kada za chini kuwa ni maslahi duni na mazingira magumu ya kazi, niendelee kuwasisitiza viongozi wote (Menejimenti na Viongozi wa Kanda) kuendelea kuwa wabunifu ili kuboresha maslahi na mazingira ya watumishi wa Mahakama ili kuimarisha ustawi wao,” amesisitiza Jaji Mkuu.


Hali kadhalika amewakumbusha watumishi wote wa Mahakama kuzingatia Maadili na Uwajibikaji katika kazi, kutunza siri za kazi, kuwa waadilifu pamoja na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kushusha hadhi ya Mahakama.

Amewasisitiza watumishi kuendelea kufanya Kazi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana, kusaidiana na kujenga utamaduni wa uwajibikaji.

Kwa upande mwingine, Jaji Mkuu amezungumzia kuhusu umuhimu wa Viongozi kusikiliza Watumishi ambapo amesema, “moja       ya mafanikio makubwa        ya                        mabaraza     haya                    ni          kuwapa watumishi nafasi ya kutoa maoni; kueleza changamoto; kupendekeza maboresho; hivyo, ni muhimu sana kuhakikisha kuwa hoja zote zilizowasilishwa hazibaki kwenye makabrasha.”

Vilevile amewataka wajumbe wa Baraza walioshiriki Mkutano huo kutoa Mrejesho kwa Watumishi kuhusu maazimio ya mkutano huo; mikakati iliyokubaliwa pamoja na wajibu wa kila upande katika utekelezaji wake.


Kuhusu, Bajeti na Mpango Mkakati wa Mahakama, Mhe. Masaju amesema Taasisi yoyote yenye mafanikio lazima iwe na mipango; vipaumbele na matumizi yenye tija na kusisitiza kwa kusema kuwa, “kwakuwa tayari tulishapanga bajeti ya Mahakama kwa mwaka 2026/2027, tuelekeze matumizi ya bajeti hiyo kulingana na mipango yetu, utekelezaji wake uzingatie kufikia malengo na shabaha ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Na hapa niwakumbushe kuendelea kuisoma Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kuifahamu misingi mikuu ya dira hiyo.


Mkutano huo ulihitimishwa kwa maazimo yafuatayo; Fursa finyu za ufadhili wa masomo kwa watumishi; Mwajiri aweke utaratibu wa wazi katika utoaji wa fursa za mafunzo kwa udhamini wa Mahakama kwa watumishi wanaohitaji kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo vya miundo mbalimbali ya kiutumishi.


Mahakama kutoshiriki katika baadhi ya michezo kwenye mashindano mbalimbali; Mahakama iongeze idadi ya michezo itakayoshiriki katika mashindano mbalimbali ya ndani pamoja na yale yanayoshirikisha Taasisi zingine.


Mafunzo ya Matumizi ya Mifumo ya TEHAMA kutowafikia watumishi wa kada zote; Mafunzo ya matumizi ya mifumo TEHAMA yatolewe kwa watumishi wote ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.


Kutokubaliwa kwa maombi ya uhamisho kwa baadhi ya watumishi ndani ya taasisi; Mwajiri aweke .utaratibu wa kuwahamisha watumishi ambao wamekaa kwa muda mrefu katika eneo moja la kazi na walio mbali na familia zao, ili kuimarisha ustawi wao wa kiutumishi na kifamilia.


Upandishwaji vyeo kwa RMAs na MMOs walioajiriwa kwa sifa ya darasa la saba na kidato cha nne waliokwama kupanda cheo kwa kukosa sifa za kimuundo; Mwajiri awasilishe maombi ya kibali maalumu cha kulegezewa masharti ya kimuundo kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili watumishi husika wafikiriwe kupandishwa vyeo kwa mserereko.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto), Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bw. Victor Kategere pamoja na wajumbe wengine wa Baraza la Wafanyakazi wakiwa katika siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza.

Makundi mbalimbali ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza hilo uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa PSSSF jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiongoza Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026. Kushoto ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando na kulia ni Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.


Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama aliyoitoa leo wakati wa kufunga kikao hicho kilichofanyika kwa siku mbili tarehe 13 na 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.











 

 

HAKI MILIKI NGUZO YA MSINGI KATIKA KUKUZA UCHUMI MAENDELEO YA TEKNOLOJIA, UVUMBUZI...; JAJI MKEHA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Haki miliki imekuwa nguzo ya msingi katika kukuza uchumi, maendeleo ya teknolojia, uvumbuzi, biashara na msingi wa maendeleo ya viwanda  katika nchi.

Hayo yamebainishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa kwa Majaji na Naibu wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam na Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara.

Mhe. Mkeha amesema mafunzo hayo, yamekuwa na umuhimu mkubwa si tu kwa Mahakama ya Tanzania bali hata kwa Taifa kwa ujumla huku Tanzania ikiendelea kukumbatia  uchumi unaotokana na maarifa na uvumbuzi, hivyo ni jukumu la Mahakama kuhakikisha utekelezaji na ulinzi wa haki miliki unazidi kuwa muhimu.

Ameongeza kuwa, Dunia inazunguka kwa kasi kupitia teknolojia ya kidijitali, akili unde, biashara ya mtandaoni na muunganisho wa kimataifa. “Maendeleo haya yanapoendelea kupanuka, mizozo inayohusiana na alama za biashara, hataza, haki miliki, miundombinu ya viwanda, siri za biashara na haki zingine za uvumbuzi inazidi kuwa ngumu,” ameeleza.

Jaji Mfawidhi huyo amesema kuwa, katika kipindi chote cha mafunzo hayo washiriki wamepata fursa ya kuongeza ufahami katika sintofahamu zao katika maeneo muhimu ikiwa ni pamoja na misingi ya sheria ya haki miliki, mifumo ya usajili, uchambuzi wa ukiukaji, tathmini ya ushahidi wa kiufundi, masuluhisho ya mwingiliano wa habari, uharibifu na changamoto za kisiasa kama vile uharamia wa kidijitali.

Pia amesema Kikao cha Amri za Muda (Temporary injuction) maagizo ya Mareva (Mareva Injuction), uhifadhi wa ushahidi na hatua za utekelezaji wa mipaka zimekuwa muhimu sana katika kuimarisha mbinu za kimahakama za migogoro ya dharura na ngumu ya haki miliki.

Vivyo hivyo, Mhe. Mkeha amesema majadiliano juu ya tathmini ya ushahidi wa kitaalamu na ushahidi wa kiufundi yamesisitiza hitaji linaloongezeka la Maofisa wa Mahakama kuendelea kuonesha hali halisi ya kisheria na kiteknolojia inayoendelea.

Jaji Mkeha amesisitiza kuwa, mpango huo wa mafunzo haujazingatia tu nadharia za kisheria lakini masomo na mijadala ya vitendo, ushirikishwaji wa vitendo kama huo ni muhimu katika kukuza uthabiti, uwiano na kutabirika katika sheria ya haki miliki nchini Tanzania.

Aidha, amewaomba washiriki wa mafunzo hayo kuendelea kujihusisha na maendeleo yanayojitokeza katika Sheria ya Haki Miliki, kubadilishana uzoefu na Maofisa wenzao wa Mahakama katika mamlaka nyingine na kutumia ujuzi uliopatikana katika utoaji haki unaofaa na thabiti wa mashauri yaliyopo katika  Mahakama zao. 

Amewashukuru Waandaaji, Wawezeshaji, Taasisi zilizosaidia pamoja na Washiriki wote kwa ushirikiano na kujitolea kwa muda wote wa mafunzo hayo.

“Ninaamini kwamba ujuzi na uzoefu uliopatikana hapa utachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha maamuzi ya Mahakama na kuimarisha utekelezaji wa Haki Miliki nchini Tanzania,” alisema Mhe. Mkeha. 

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam, Mhe. Lumuli Mbuya akizungumza wakati akitoa neno la shukrani amemshukuru Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi kwa kuwezesha kufanikisha kufanyika kwa mafunzo hayo kwakuWa anapenda kuhakikisha kwamba wanasoma na kupata kupata mafunzo mbalimbali kwa ajili ya kuwajengea uwezo.

Mhe. Mbuya amewashukuru pia Sekretarieti kwa kuandaa mada nzuri na kuwachagua Wawezeshaji mahiri kwa kutoa mafunzo hayo.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliandaliwa na Mahakama ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam. Katika siku ya pili ya mafunzo hayo, mada zilizofundishwa ni pamoja na uthibitishaji wa ukiukwaji wa Haki Miliki (Element of Proving IP Infringement) na masuala yanayoibuka katika utekelezaji wa Haki Miliki (Emerging Issues in IP Enforcement) ambapo Profesa Saudin Mwakaje alifundisha na mada nyingine.

Mwisho wa mafunzo hayo Washiriki na Wakufunzi wa mafunzo hayo walipokea vyeti vya ushiriki.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha akitoa hotuba ya kufunga Mafunzo ya Miliki Bunifu tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.




Washiriki wa mafunzo ya Miliki Bunifu wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Mussa Maghimbi (kushoto) akipokea cheti cha ushiriki wa mafunzo ya Miliki Bunifu kutoka kwa Mhe. Cyprian Mkeha.


wakili Shehzada Walli akipokea cheti cha uwezeshaji wa mafunzo.

 Profesa Saudin Mwakaje akipokea cheti cha uwezeshaji wa mafunzo ya Haki Miliki.

Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Cleophace Morris Mwezeshaji wa Mafunzo ya Miliki Bunifu akifundisha wakati wa mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJIDHATITI KUBORESHA HUDUMA YA UTOAJI HAKI MAPEMA IPASAVYO

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imetunga jumla ya kanuni mpya tano (5) na kufanyia marekebisho kanuni nane (8) na hivyo kufanya uwepo wa jumla ya kanuni 13 za uendeshaji wa mashauri, lengo likiwa ni kurahisisha mchakato wa usikilizaji mashauri ili haki iweze kupatikana mapema ipasavyo.

Hayo yamebainishwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, alipokuwa akiwasilisha Taarifa kuhusu Kazi za Kimahakama za mwaka 2025 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama lililofunguliwa jana tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Mhe. Nkya ametaja Kanuni hizo kuwa ni pamoja na The Primary Courts-Administration of Estates) (Amendment) Rules 2025 GN No.  428 published on 11th July, 2025, The Civil Procedure Code (Amendment of the First Schedule) Rules, 2025 GN No. 569 published on 12th September, 2025.

Nyingine ni Judicature and Application of Laws (Electronic Filing) (Amendment) Rules, 2025 GN No. 39 published on 17th October, 2025, Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Madiwani za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na.433 la tarehe 11 Julai, 2025, Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Wabunge za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na.431 la tarehe 11 Julai, 2025, Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na. 430 la tarehe 11 Julai, 2025.

Kanuni za Marekebisho ya Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Wabunge za Mwaka 2025, Tangazo la Serikali Na 610 la tarehe 17 Oktoba, 2025, The Judiciary Administration Regulations (The Judiciary Administration (Judiciary Flag) (Amendment) Regulations, 2025, GN 608/2025 na nyingine.

Akizungumzia kuhusu mafanikio ya Mahakama yaliyopatikana, Msajili Mkuu ameeleza kuwa kumekuwa na ongezeko la usikilizaji mashauri kwa asilimia tatu sambamba na kupungua kwa wastani wa mzigo wa kazi toka 227 hadi 222.

Kadhalika, Msajili Mkuu ameeleza kuwa, kumekuwa na kasi ya kupungua kwa wastani wa muda wa kumaliza shauri kutoka siku 78 hadi 66.

Kadhalika, amebainisha kwamba, Mahakama imefanikiwa kufikia malengo ya kiashiria cha kiwango cha mashauri ya mlundikano kwa asilimia tano na usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (lengo lilikuwa 18,500 - 62,041).

“Mafanikio mengine yaliyopatikana ni pamoja na kuanzishwa kwa Masjala ndogo tano za Mahakama Kuu, kuanzishwa kwa Vituo vya Mahakama ya Mwanzo 15,” amesema Mhe. Nkya.

Kwa upande wa kiwango cha ukaguzi wa Mahakama na Magereza, Mahakama imefanikiwa kwa asilimia 1.6 na 11.6 mtawalia na kusababisha kupungua kwa mahabusu na wafungwa gerezani, huku Mahakama za Mwanzo kukiwa hakuna mahabusu.

Kwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, Mhe. Nkya amebainisha kuwa, zilikaguliwa kwa 100.

“Kuhusu ushughulikiaji wa mrejesho ulikuwa asilimia 99.9 ambapo jumla ya mirejesho 3,144 kati ya 3,149 (ikiwepo mitano “5” iliyobaki mwaka 2024) ilishughulikiwa,” ameeleza.

Amebainisha kuwa, kati ya mirejesho hiyo ushughulikiaji wa malalamiko ulikuwa ni asilimia 99.8 ambapo jumla ya malalamiko 1,609 kati ya 1,611 yaliyokuwepo (yakiwepo matano “5” yaliyobaki mwaka 2024) yalishughulikiwa.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya alipokuwa akiwasilisha Taarifa kuhusu Kazi za Kimahakama za mwaka 2025 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama lililofunguliwa jana tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.





Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia wasilisho la Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (hayupo katika picha).


Jumatano, 13 Mei 2026

JAJI MKUU ATAKA CHANGAMOTO ZA WATUMISHI KUTATULIWA BILA VIKWAZO

·       Awataka watumishi wa Mahakama kuendelea kutekeleza Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, 2026

·       Ataka mashauri yasikilizwe mapema ipasavyo ili kuchangia ustawi na maendeleo ya Taifa

·       Asisitiza ushirikiano, amani na kuthaminiana kwa Watumishi

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama nchini, amewataka Viongozi wa Mhimili huo kuwa wanyenyekevu sambamba na kufungua milango kwa ajili ya kuwasikiliza Watumishi walio chini yao ili kutatua changamoto wanazokabiliana nazo bila vikwazo.

Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania ikiwa ni mara yake ya kwanza kuendesha Mkutano Mkuu wa Baraza hilo tangu ateuliwe kushika wadhifa wa Jaji Mkuu takribani mwaka mmoja uliopita.

“Kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unakuwa mtumishi wa wote, sisi Viongozi ni Watumishi wa watu, tuwe na tabia ya kufungua milango tuwasikilize walio chini yetu, tusifunge milango,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema Viongozi pia wanawategemea Watumishi walio chini yao ambapo ameeleza kuwa, kwa kadri Kiongozi anavyozidi kupanda kimadaraka ni kwa kiwango hicho hicho anazidi kuwa tegemezi kwa watu wengine, na kwamba kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unapaswa kuwa mnyenyekevu ili uwafikie wanaokutegemea na wao wakufikie ili ujue changamoto zao na mafanikio yao.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema kuwa, Viongozi wasiwazuie wajumbe wa Baraza kuzungumza yale yanayowasibu, badala yake wawaache huru kusema yale wanayokabiliana nayo katika utekelezaji wa majukumu yao ili kupata ufumbuzi wa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mahakama.

Ameongeza kuwa, hata Viongozi wanapotembelea Mahakama mikoani Viongozi wa Mahakama husika wanapaswa kuwaacha watumishi wazungumze na Viongozi ili wajue Mahakama imepiga hatua gani katika maendeleo, wajue changamoto  zilizopo ili tutatue changamoto hizo na kupiga hatua ili hatimaye vikao vya Baraza viwe vya furaha.

Aidha, Jaji Mkuu amewapongeza watumishi wa Mahakama wa Kada zote kwa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mhimili huo kwa ufanisi ipasavyo.

“Kwanza natambua mchango wenu, kila mmoja wetu katika utendaji wa Mahakama ya Tanzania, mmefanya kazi kubwa sana, miaka iliyopita na mimi tangu nimekuja kushirikiana na ninyi mmefanya kazi kubwa sana ya kutekeleza majukumu yenu na wakati fulani katika mazingira magumu mimi naelewa katika utumishi wangu mimi nimeanzia chini sana nikiwa Wakili wa Serikali Daraja la tatu, kwahiyo ninafahamu na wakati mwingine

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju amewakumbusha Viongozi na watumishi wote wa Mahakama kwa ujumla kuendelea na utekelezaji wa Kaulimbiu ya Siku ya Sheria Nchini ya mwaka huu 2026 isemayo; ‘Mchango wa Mahakama ya Tanzania katika Maendeleo na Ustawi na Maendeleo ya Taifa.’

“Mahakama ina mchango mkubwa sana, mnaweza kurejea hotuba yangu ya Siku ya Sheria, nimeeleza yote, hii haiwezi kuwa ni Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, hii tunaiishi mwaka huu wote wa 2026, kwahiyo tunapofanya kazi yatupasa tujue tuna mchango katika ustawi na maendeleo ya Taifa la Tanzania. Wajibu wetu Mahakama ni kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi ipasavyo na tunapaswa kuendelea kuwa wabunifu,” amesema Jaji Mkuu.

“Kwenye Kanda mtaangalia mnapopanga mashauri mjue kuna kitu tunafanya, kwahiyo mnatakiwa kuangalia ustawi na maendeleo ya Taifa, tunahusika hata sisi katika maendeleo kwa sababu amani ni msingi mkubwa unaoleta ustawi na maendeleo ya Taifa,” amesema Mhe. Masaju.

Ameeleza kuwa, kwa msingi huo ndio maana wa mfano kuna mashauri ya jinai, mashauri ya madai, mashauri ya uchaguzi na kila aina ya mashauri yanashughulikiwa na kumalizika watu wanapiga hatua mapema.

“Mpaka sasa kwa mfano yale mashauri ya uchaguzi yaliyofunguliwa, limebaki shauri moja tu, mengine yote yameshaisha, kuna mashauri ya kila aina ya mirathi, ya ndoa, ya uhujumu uchumi. Sisi kama Mahakama wajibu wetu ni upi? najua tunazo changamoto pengine hatupati ushirikiano mzuri sana lakini sisi hatuwezi kukata tamaa ndio wajibu wetu, tukiharibu tunawajibishwa sisi, sisi ndio tunaosemwa na tunapaswa tuendelee kuwa wabunifu katika maeneo yetu ya kazi kuhakikisha kwamba mchango wa Mahakama ya Tanzania katika ustawi na maendeleo ya Taifa unazidi kuimarika,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Amesema, tunaishi katika nchi inayozingatia Utawala wa Sheria, hivyo, Mahakama ina nafasi kuwa katika ustawi na maendeleo ya Taifa na kwa sababu ni muhimu mashauri yanapopangwa yapangwe kimkakati na hayatakiwi kucheleweshwa bila sababu za msingi, lakini pia inabidi kuwa ni mikakati ya kubaini mashauri yenye kero yanayoleta sintofahamu katika jamii yashughulikiwe.

“Uchumi ni Ardhi wala hata sio kitu kingine, kwahiyo tuna mikakati ya kumaliza haya mashauri ya Ardhi tangu mwaka jana tumekuwa na hiyo mikakati, na Mahakama Kuu wamefanya vizuri sana kwa sababu mashauri ya ardhi kwa Mahakamani yanaanzia Mahakama Kuu, yanakwenda Mahakama Rufaa mengine kwenye ‘originial jurisdiction’ tunafanya vizuri japo bado ni mengi kwa sababu migogoro inazalishwa mingi na sehemu fulani tumeshauri kwa mfano ukisoma Sheria ya Usajili wa Ardhi (Land Registration Act) kuna mtu pale anaitwa ‘The Registrar of Titles) ana mamlaka makubwa sana  mashauri mengine hata yasingekuwa yanakuja mahakamani yangekuwa yanaenda pale kama kuna migogoro wakishindwa kutatua upande ambao hauridhiki unakuja Mahakama ya Rufani,” ameeleza.

Kwa upande wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Masaju amesema kuna mashauri mengi ya jinai, hivyo wameweka mkakati wa kushughulikia mashauri hayo ambayo walianza kusikiliza katika Vikao vya Mahakama ya Rufani (COA Session) ya mwezi Februari ambapo walichanganya na mashauri ya mirathi ili watu wawe na amani kwenye familia zao na wengine wajue hatma yao.

“Majaji hawa wa Mahakama ya Rufani wamefanya kazi nyuma, mashauri mengi yameenda, kama wengine hawasema sisi wenyewe tujisemee, mimi nawapongeza sana Mahakama ya Rufani,” amesema Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Mwezi Aprili walipanga mashauri ya kazi na ndoa ambayo kikao chake kimekamilika tarehe 08 Mei, 2026 na wengine wanaendelea, jitihada hizo ni katika wajibu wa kutekeleza mchango wa Mahakama katika maendeleo na ustawi wa Taifa.

Kadhalika, amesema katika Vikao vinavyofanyika Juni na Agosti, 2026 mashauri ya ardhi yatashughulikiwa tena ili kuyapunguza. Ameeleza kuwa, katika vikao hivyo wataweka pia mashauri machache ya jinai na kabla ya Desemba pia watakuwa na mashauri ya jinai.

Amebainisha kuwa, ili Mahakama ifanikiwe inahitaji ushirikiano kutoka Mihimili mingine ili kutekeleza jukumu la utoaji haki kwa ufanisi ipasavyo.

Kwa upande wa Mahakama Kuu, Mhe. Masaju amesema, wamekamilisha vikao vya kusikiliza mashauri ya ardhi ikiwa ni mwendelezo wa zoezi ambalo lilianza mwaka jana, ambapo amesema kwa sasa hatatoa takwimu kwakuwa zinaandaliwa na Msajili wa Mahakama Kuu na zitatangazwa kwa wananchi kile ambacho Mahakama imefanya.

Amesema pia kulikuwa ni shida kubwa za mashauri ya baadhi ya waajiri kutowasilisha michango ya mafao ya watumishi wao katika mifuko ya hifadhi za jamii ambapo amesema wamefanya mabadiliko ya kanuni na kwamba katika usikilizaji wa mashauri hayo Majaji na Mahakimu wamefanya vizuri kwakuwa mashauri hayo mengi yameisha na yameisha kwa njia ya usuluhishi.

“Sisi Mahakama nia yetu ni kwamba wafanyakazi wapate stahili zao sio wanakatwa halafu mwisho wa siku hawapewi stahili zao,” ameeleza.

Kadhalika Jaji Mkuu amewataka watumishi wote wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, umoja na kuthaminiana katika utekelezaji wa majukumu.

 Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando akizungumza jambo wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama leo tarehe 13 Mei, 2026.


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Muu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 13 Mei, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama jijini Dodoma.

Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa pili kushoto) wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama nchini ulioanza leo tarehe 13 Mei, 2026. Mkutano huo unatarajiwa kuhitimishwa kesho tarehe 14 Mei, 2026.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija (wa pili kushoto), Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (wa kwanza kushoto) na Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama, Mhe. Christina Mlilwo.


Wajumbe mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Muu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 13 Mei, 2026 alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama jijini Dodoma.

Wimbo wa Mshikamano Daima (Solidarity Forever) ukiimbwa na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasilisha taarifa ya Mahakama wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akiwasilisha taarifa wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma.

Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Sekretarieti ya Maandalizi ya Mkutano huo.

(Picha na Mary Gwera-Mahakama)