Jumanne, 11 Agosti 2026

MAJAJI, MAHAKIMU MBEYA WANOLEWA JINSI YA KUKABILIANA NA MSONGO WA MAWAZO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Majaji, Naibu Wasajili na Mahakimu wa Mahakama Masjala Ndogo ya Mbeya wametakiwa kutambua, kudhibiti na kukabiliana na msongo wa mawazo kwa wakati, wakizingatia kuwa afya njema ya akili ni msingi muhimu wa kufanya maamuzi yenye umakini, weledi na ya haki katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wito huo umetolewa katika mafunzo maalumu yaliyowakutanisha Majaji na Mahakimu wa Masjala Ndogo ya Mbeya, yaliyofanyika hivi karibuni katika Hoteli ya Lake Nyasa, iliyopo katika fukwe za Ziwa Nyasa, Wilaya ya Kyela, ambapo washiriki walipata elimu kuhusu chanzo, madhara na namna bora ya kukabiliana na msongo wa mawazo katika maisha na mazingira ya kazi.

Mafunzo hayo yaliendeshwa na mtaalamu wa afya ya akili kutoka Hospitali ya Kilutheri ya Matema, Wilaya ya Kyela, Dkt. Ebenezer Richard Minja, ambaye aliwaeleza washiriki kuwa msongo wa mawazo ni hali inayoweza kumpata mtu kutokana na changamoto mbalimbali za maisha na mabadiliko ya mazingira au mtindo wa maisha na kwamba hali hiyo inapopuuzwa inaweza kuleta madhara makubwa kwa afya ya mtu.

Dkt. Minja alisisitiza umuhimu wa mtu kutambua mambo yanayoweza kumletea msongo wa mawazo na kuchukua hatua stahiki mapema, akiwataka washiriki kuzingatia ulaji unaofaa, kufanya mazoezi mepesi mara kwa mara na kuepuka tabia ya kujilinganisha na watu wengine.

Aidha, alieleza kuwa kufanya ibada ni miongoni mwa njia zinazoweza kumsaidia mtu kupata utulivu wa akili, kwa kuwa humwezesha mtu kujenga imani na kumweleza Mungu changamoto anazokabiliana nazo.

Kwa mujibu wa Dkt. Minja, msongo wa mawazo unapokomaa unaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa afya ya mtu na kusababisha matatizo mbalimbali, yakiwemo shinikizo la juu la damu, magonjwa ya moyo, kupoteza kumbukumbu, kupungua uzito na kushuka kwa kinga ya mwili, hali inayoweza kuongeza hatari ya kupata magonjwa mengine kama kisukari.

“Ukihisi mambo yanaenda mrama, tafuta msaada mapema. Njiti moja ya kiberiti inaweza kuangamiza msitu mzima, hivyo chukua hatua mapema kupambana na msongo wa mawazo kabla matatizo makubwa hayajajitokeza,” alisema Dkt. Minja, huku akisisitiza umuhimu wa kutafuta msaada mapema pale mtu anapohisi kuzongwa na msongo wa Mawazo.

Akizungumzia suala hilo kwa mtazamo wa mazingira ya kazi za Mahakama, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya alisema kuwa, majukumu ya kimahakama yanaweza kuwa miongoni mwa vyanzo vya msongo wa mawazo kutokana na mlundikano wa mashauri, uzito wa maamuzi yanayofanywa pamoja na mazingira mbalimbali yanayowazunguka watendaji hao.

Bw. Chonya aliongeza kuwa, changamoto hizo zinahitaji usimamizi mzuri wa muda, kutenganisha majukumu ya kikazi na maisha ya nyumbani pamoja na kutafuta ushauri wa kitaalamu pale mtu anapohisi amelemewa.

“Akili iliyochoka inashindwa kuchuja ukweli na uwongo kwa wakati, hivyo tujitahidi kudhibiti msongo wa mawazo. Kwani afya ya watendaji wa Mahakama ina uhusiano wa moja kwa moja na uwezo wao wa kutekeleza wajibu wa kutoa haki kwa jamii,” alisema Bw. Chonya.

“Ili uweze kutoa haki kwa jamii ni lazima ujitendee haki mwenyewe kwa kulinda afya ya mwili na akili. Jamii inatuhitaji tukiwa na afya njema na akili timamu,” alisema Mtendaji Chonya

Katika mafunzo hayo pia washiriki walijifunza umuhimu wa kuzuia changamoto kabla hazijawa kubwa kwa kujadili umuhimu wa mpango wa malezi kwa mahakimu “mentorship programe”

Akizungumzia suala hilo, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, alisema ‘Mentorship Programme’ ni muhimu katika kuwasaidia Mahakimu kukua kitaaluma, kuboresha utendaji wao na kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza katika safari yao ya kiutumishi.

Mhe. Mtulya alisema kuwa, malezi ya kitaaluma yanaweza kuwa nyenzo muhimu ya kumsaidia Hakimu kupata ushauri mapema kabla changamoto anazokabiliana nazo hazijawa kubwa na kuathiri utendaji wake au kufikia hatua ya kushughulikiwa na Kamati za Maadili.

“Mahakimu wengi wanaharibikiwa kwa kutopata mlezi wa kumsaidia kabla changamoto haijawa kubwa hadi kufikia kwenye Kamati ya Maadili,” alisema Mhe. Mtulya.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, alisisitiza umuhimu wa kuwa na viongozi, walezi na wasimamizi wanaoweza kuwasaidia watendaji kukabiliana na changamoto za kazi na maisha kwa wakati.

“Kazi zetu ni ngumu sana na ukipata mtu wa kumtolea mambo au changamoto zako ni jambo kubwa sana, hivyo ni muhimu kupata kiongozi, mlezi na msimamizi wa kukusimamia,” alisisitiza Mhe. Mlimba

Mafunzo hayo yameweka wazi kuwa mjadala kuhusu afya ya akili kwa Majaji na Mahakimu haupaswi kuangaliwa kama suala binafsi pekee, bali kama sehemu ya kujenga mazingira bora ya utoaji wa haki.

Majukumu ya kimahakama yanahitaji umakini mkubwa, uwezo wa kuchambua hoja kwa kina na kufanya maamuzi kwa usawa na bila kuyumbishwa. Kwa msingi huo, kulinda afya ya akili na mwili, kusimamia muda, kutafuta msaada pale inapohitajika na kuwa na mfumo imara wa malezi na ushauri wa kitaaluma ni miongoni mwa hatua zinazoweza kuimarisha ustawi wa watendaji na ufanisi wa kazi za Mahakama.

Hatua hiyo pia inalinda dhamira ya kujenga Mahakama yenye watendaji wenye weledi, maadili na utayari wa kutekeleza wajibu wao kwa uadilifu. Afya ya akili ya watendaji wa Mahakama ni uwekezaji katika haki na kulinda akili iliyo imara ni sehemu ya kulinda haki ya mwananchi.

Mtaalamu wa afya ya akili kutoka Hospitali ya Kilutheri ya Matema, Wilaya ya Kyela Dkt. Ebenezer Richard Minja (aliyesimama) akitoa mafunzo ya kukabiliana na Msongo wa Mawazo kwa Waheshimiwa Majaji na Mahakimu (hawapo pichani).

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Mahakimu ambao walioshiriki katika mafunzo hayo ambao ni wananchama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Ndogo ya Mbeya wakifanya zoezi kwa vitendo.

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo ambao ni Mahakamu wananchama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia mafunzo hayo kwa makini.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Roster Mofuga akichangia jambo katika mafunzo hayo, (katikati) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba na (kushoto) ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer.

Jaji wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (aliyesimama) akizungumza jambo katika mafunzo hayo, kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa katika mafunzo hayo (wa kwanza kushoto) ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (katikati) ni Jaji wa Mahakama kuu masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo na Jaji wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kulia)

(Habari Hii Imehaririwa na INNOCENT KANSHA - Mahakama)




TMJA MBEYA WAHIMIZWA KUIMARISHA WELEDI, MAADILI NA MSHIKAMANO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Majaji na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, wametakiwa kuendelea kudumisha weledi, maadili, mshikamano na mahusiano mema katika utendaji wa kazi, huku wakihimizwa kuongeza maarifa na kufanya tafiti za kitaalamu kwa ajili ya kuimarisha weledi katika utoaji haki.

Wito huo umetolewa katika kikao cha Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Masjala Ndogo ya Mbeya, kilichofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 7 hadi 9 Agosti 2026, katika fukwe za Ziwa Nyasa, Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.

Akizungumza katika kikao hicho, Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, amewakumbusha wanachama kuzingatia malengo ya chama hicho, hususan kudumisha hadhi na heshima baina ya Majaji na Mahakimu, pamoja na kuimarisha maarifa, uelewa na uwezo wao katika kufanya tafiti za kitaalamu.

“Miongoni mwa malengo ya TMJA Mbeya ni pamoja na kudumisha hadhi na heshima baina ya Majaji na Mahakimu na kuimarisha zaidi maarifa, uelewa na uwezo wetu katika kufanya tafiti za kitaaluma. Hivyo, tupo hapa ikiwa ni sehemu ya kutekeleza malengo hayo. Tuwe tayari kuzingatia na kujifunza ili tukitoka hapa tuwe Mahakimu wenye weledi zaidi,” alisema Mhe. Mtulya.

Mhe. Mtulya pia alisisitiza umuhimu wa kuthaminiana, kujaliana, kuheshimu viongozi, kuzingatia nidhamu na kuepuka ubaguzi, huku akiwataka wanachama kuendelea kushikamana kupitia vikundi vilivyoanzishwa kwa ajili ya kusaidiana wakati wa shida na raha.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, alisisitiza umuhimu wa maadili, mawasiliano na mahusiano mazuri katika mazingira ya kazi.

“Ili uwe na utendaji kazi mzuri, ni lazima muwe na mahusiano na mawasiliano mazuri na viongozi wenu,” amesema Mhe. Mpepo, akiongeza kuwa ni muhimu kujenga mahusiano mazuri kati ya Majaji, Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama ili kuboresha utendaji kazi.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, amewataka watumishi kuepuka ubinafsi, kuzingatia taratibu na itifaki, pamoja na kujenga utamaduni wa upendo, kujali na kusaidiana, kadhalika amewataka watumishi kuendelea kumuunga mkono Jaji Mfawidhi katika utekelezaji wa majukumu yake ya kiuongozi.

Aidha, Mwenyekiti wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Asha Njovu, amewashukuru wanachama wanaotekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji, akiwahimiza kuendelea kudumisha viwango hivyo katika utumishi wao.

Kikao hicho pia kiliambatana na mafunzo kuhusu mbinu za kukabiliana na msongo wa mawazo pamoja na umuhimu wa malezi ya kitaaluma kwa Mahakimu (Mentorship Programme) yaliyolenga kuimarisha uwezo na ustawi wa kitaaluma wa washiriki.

Mbali na kikao na mafunzo hayo, wanachama walipata fursa ya kuburudika na kushiriki shughuli za utalii katika fukwe za Ziwa Nyasa, hatua iliyosaidia kuimarisha zaidi mahusiano na mshikamano miongoni mwa wanachama.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya katika kuimarisha weledi, maadili, mshikamano na uwezo wa kitaaluma wa Majaji na Mahakimu, kwa lengo la kuendelea kuboresha utoaji wa haki na huduma kwa wananchi.

Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa kwenye kwenye picha ya Pamoja na viongozi na wanachama wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya wakati wa mafunzo na kikao hicho.

Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye kikao kilichoambatana na mafunzo ya Mentorship Programme


Sehemu Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika Kikao hicho cha TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya. 

Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye kikao kilichoambatana na mafunzo ya Mentorship Programme

Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wa pili kushoto) akiwa na viongozi wengine wa Mahakama  wakiwa kwenye picha ya pamoja na wanachama wapya wa TMJA Mbeya

Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wapili kushoto) akiwa na viongozi wengine wakikata keki kwa pamoja kuwakaribisha wanachama wapya wa TMJA Masjala hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho (katikati) ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho, kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Roster Mofuga na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer.

Mwenyekiti wa TMJA Mbeya Mhe. Asha Njovu (aliyesimama wapili kushoto) akifungua kikao hicho, (wa kwanza kushoto) ni katibu wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angela Byera na Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (Katikati)

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)

 

Jumatatu, 10 Agosti 2026

JAJI KIONGOZI ATEMBELEA NA KUFANYA UKAGUZI MAHAKAMA YA WILAYA CHAMWINO

Na ARAPHA RUSHEKE & JAMES BUSANYA - Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amefanya ziara katika Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo, huku akitoa maelekezo mbalimbali yanayolenga kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 10 Agosti 2026 wakati alipotembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino iliyoanza kutoa huduma rasmi kuanzia tarehe 24 Julai 2026, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania za kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi. Kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama hiyo, huduma za kimahakama kwa wananchi wa Wilaya ya Chamwino zilikuwa zikitolewa na Mahakama ya Wilaya Dodoma mjini.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani alikagua jengo na miundombinu ya Mahakama hiyo pamoja na kuzungumza na watumishi, ambapo alieleza kufurahishwa na jengo hilo na kuwapongeza waliokuwa wakisimamia ujenzi wake.

Nimefurahi leo tuna jengo zuri lenye viwango. Nawapongeza waliokuwa wanasimamia ujenzi huu. Tumesogeza huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Chamwino. Mahakama hii itawaletea nafuu, kuwaokolea muda na gharama,” alisema Jaji Kiongozi.

Alisema kuanzishwa kwa Mahakama hiyo ni hatua muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki karibu na maeneo yao, akiwataka viongozi wa Mahakama kuendelea kufikiria namna ya kusogeza huduma kwa wananchi bila kuathiriwa na mipaka ya kijiografia.

Jaji Kiongozi aliutaka Uongozi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kushirikiana na viongozi wa Kata katika maeneo yanayohudumiwa na Mahakama hiyo, ili kuhakikisha wananchi wanapata taarifa kuhusu huduma zinazotolewa na Mahakama, ikiwemo kupitia njia za mtandao nakufanya vipindi kwa njia ya Radio.

Aidha, alisisitiza matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma za Mahakama, akieleza kuwa teknolojia inaweza kusaidia kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wananchi na kupunguza utegemezi wa matumizi ya makaratasi.

Katika kusisitiza matumizi ya TEHAMA, Mhe. Dkt. Siyani aliagiza timu ya wataalum kuhakikisha huduma za mtandao ziunganishwe haraka katika Mahakama hiyo ili ziweze kusadifu ubora wa jengo na huduma za kimahakama kwa wananchi, akieleza kuwa uwepo wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ni fursa inayopaswa kutumika kikamilifu katika kuboresha huduma za Mahakama.

Alibainisha pia kuwa, ushahidi unaweza kutolewa katika Mahakama kwa njia ya Mahakama Mtandao, pale ambapo utaratibu huo unaruhusiwa kisheria, hatua ambayo inaweza kusaidia kurahisisha mwenendo wa mashauri na kupunguza usumbufu kwa wananchi.

Katika hatua nyingine, Jaji Kiongozi alisisitiza umuhimu wa Mahakama kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wananchi wanaofika kupata huduma, akionya watumishi dhidi ya kuweka vikwazo visivyo vya lazima, hivyo mwananchi anapofika mahakamani anapaswa kuhudumiwa kwa wakati.

Mhe. Dkt. Siyani pia alitoa maelekezo kuhusu utunzaji wa vielelezo na kuvirejesha kwa wahusika mara baada ya mashauri kukamilika mahakamani, akitaka kuwepo kwa utaratibu maalum wa kuhakikisha vielelezo hivyo vinatunzwa kwa usalama na kwamba wenye mali wanarejeshewa kwa kufuata sheria na taratibu zinazokubalika.

Akizungumzia utunzaji wa mazingira, Jaji Kiongozi alisisitiza kuwa, majengo ya Mahakama yanapaswa kwenda sambamba na mazingira safi na yanayovutia, akiwataka watumishi kupanda miti na maua pamoja na kuhakikisha uchafu unaondolewa katika maeneo ya Mahakama.

Tusikubali jengo letu na miundombinu yetu ichakae kwa wepesi. Watumishi tushirikiane kulitunza jengo letu na kulifanyia usafi. Mazingira yetu ya ndani na nje ya Mahakama yawe vizuri,” alisema Dkt Siyani.

Aliagiza uongozi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kusimamia utekelezaji wa mpango wa utunzaji mazingira na upandaji miti katika maeneo ya Mahakama, akieleza kuwa taasisi jirani zinapaswa kuvutiwa na mazingira bora yatakayowekwa na Mahakama hiyo.

Katika kuimarisha utendaji kazi, Jaji Kiongozi aliwataka watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kuwa na utamaduni wa kujifunza, kukumbushana na kufundishana, akisema kuwa mafanikio yanahitaji watumishi wenye utayari wa kujifunza mambo mapya kila wakati.

Kama mnataka mafanikio muwe na utaratibu wa kukumbushana kwa kufundishana. Watu bora ni wale wanaojifunza. Msibweteke na mnachokijua, vipo vingine hamvijui. Mnaweza kufundishana wenyewe mambo mengi na muhimu,” alisema Jaji Kiongozi

Akihitimisha ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani aliwataka watumishi kujitathmini mara kwa mara kuhusu namna wanavyowahudumia wananchi na kuhakikisha kila anayefika mahakamani anapata huduma kwa heshima, weledi, uadilifu na kwa wakati.

Mahakama ya Wilaya Chamwino inahudumia wananchi wapatao 486,176, Wilaya hiyo inayoundwa na tarafa tano (5), Kata 36, Vijiji 107 na Vitongoji 814. Kuanzishwa kwa Mahakama hiyo ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi, kuwaokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha imani ya wananchi katika mfumo wa utoaji haki nchini.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (aliyeketi kiti cha mbele), akipokea taarifa fupi ya Mahakama ya Wilaya ya Chamwino Kutoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (wa pili kulia) wakati wa ziara ya kutembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo leo tarehe 10 Agosti, 2026.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kulia) akitete jambo na Waendesha Mashitaka wa Serikali wakati alipotembelea Ofisi hiyo ya wadau wanaotoa huduma mahakamani hapo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto), akikagua sehemu ya miundombinu jengo la Mahakama ya wilaya Chamwino huku akiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (kulia aliyenyoosha mkono) wakati wa ziara ya kutembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto) akizungumza na kupata maelekezo kutoka kwa mtumishi wa mahakama hiyo kwenye dirisha la Mapokezi.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino wakikagua sehemu ya miundombinu ya jengo la Mahakama ya wilaya Chamwino huku akiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga. 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (aliyenyoosha mkono) akimuonesha eneo la vielelezo Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama wakati wa ziara hiyo.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma Bw. Bedson Mariba (wa kwanza kushoto) akimuonesha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani eneo la mipaka ya Mahakama ya Wilaya Chamwino wakati alipokuwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama wakati wa ziara hiyo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (aliyenyoosha mkono) akitoa maelekezo kwa Viongozi wa Mahakama juu ya utunzaji wa mazingira ya Mahakama ya Wilaya Chamwino.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati), akisisitiza jambo wakati alipokuwa akiongea na watumishi na viongozi wa Mahakama (hawapo pichani) wakati wa ziara ya kutembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo. Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya wa kwanza kulia.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino mara baada ya ziara ya ukaguzi wa jengo hilo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania alioambatana nao katika  ziara ya ukaguzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.

Muonekano wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.

Muonekano wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)



 

WATUMISHI WA MAHAKAMA KIGOMA WAKUMBUSHWA MADHARA YA RUSHWA MAHALI PA-KAZI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewasisitiza watumishi wa Mahakama hiyo juu ya umuhimu wa kuzingatia maadili ya kazi zao na kuepuka vitendo vyote vya rushwa vinavyoweza kuharibu sifa ya Mhimili wa Mahakama na kukosesha haki kwa wananchi wanaowafuata huduma.

Mhe. Rwizile aliyasema hayo tarehe 07 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma alipokuwa akifungua mafunzo ya siku moja yaliyolenga kuwajengea uelewa watumishi wa Mahakama hiyo kuhusu elimu ya kuzuia na kupambana na rushwa mahali pa kazi sambamba na kuimarisha misingi ya uadilifu, uwazi, na uwajibikaji katika utoaji wa haki kwa wananchi.

"Rushwa ni adui wa haki; watumishi wa Mahakama tunapaswa kuwa mstari wa mbele katika kulinda na kusimamia maadili ya utumishi wa umma ili wananchi waendelee kuamini mfumo wetu wa utoaji haki usioacha shaka ili haki hiyo ipatikane mapema ipasavyo," alisisitiza Jaji Mfawidhi huyo.

Aidha, Mhe. Jaji Rwizile aliwasisitiza zaidi watumishi hao kuwa uadilifu ni nguzo kuu katika kusimamia sheria na kwamba Mahakama inapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii.

Mada kuu za mafunzo hayo ziliwasilishwa na Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kigoma, Bi. Asha Kwaliko.

Katika uwasilishaji wake, Bi. Kwaliko aliwafahamisha watumishi hao kuhusu aina mbalimbali za rushwa, madhara yake kisheria na kijamii, pamoja na mbinu za kujikinga na vishawishi kazini.

Bi. Kwaliko alieleza kwa kina wajibu wa kila mtumishi katika kutoa taarifa za vitendo vya rushwa na kueleza sheria mbalimbali zinazowalinda watoa taarifa (whistleblowers).

Aidha, aliwakumbusha watumishi hao kuwa TAKUKURU itaendelea kushirikiana kwa karibu na Mahakama Kuu Kigoma katika kutoa elimu endelevu na kuchukua hatua kali dhidi ya yoyote atakayebainika kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Kwa upande wake Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Kigoma, Bw. John Mgallah, alisema kuwa, rushwa inaweza kutafsiriwa kama kitu chochote cha thamani kinachotolewa au kupokelewa na mtu yeyote kinyume na sheria ili kupata huduma au kutoa huduma na vilevile rushwa ni utumiaji mbaya wa madaraka ili kujinufaisha au kumnufaisha mtu mwingine kwa kupindisha sheria, kanuni au taratibu za nchi.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka aliwashukuru Viongozi hao wa TAKUKURU na kusema kuwa  Mafunzo waliyotoa yataleta tija kubwa katika kuongeza ufanisi wa kazi kwa watumishi, kupunguza mianya ya rushwa na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama katika Mkoa huo.

Hata hivyo, Bw. Kasuka alibainisha kuwa mafunzo hayo yalifanyika katika Mahakama za Wilaya sita ambazo ni Kibondo, Uvinza, Buhigwe, Kakonko, Kasulu na Kigoma pamoja na Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma pamoja na watumishi wa Mahakama za Mwanzo na kadhalika.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kigoma wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikiendelea kutolewa hivi karibuni na Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kigoma, Bi. Asha Kwaliko (aliyesimama) wakati wa Mafunzo kuhusu madhara ya Rushwa kwa Watumishi wa Mahakama yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa neno kwa msisitizo alipokuwa akifungua Mafunzo kuhusu madhara ya Rushwa kwa Watumishi wa Mahakama yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kigoma, Bi. Asha Kwaliko akifafanua jambo kwa msisitizo wakati wa Mafunzo kuhusu madhara ya Rushwa kwa Watumishi wa Mahakama yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Mtendaji wa Mahakama Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka akitoa neno la shukrani kwa viongozi wa TAKUKURU Mkoa wa Kigoma kwa kukubali kutoa mafunzo kwa watumishi wa Mahakama juu ya athari za rushwa mahali pa-kazi.

Naibu Mkuu wa TAKUKURU (M) Kigoma, Bw. John Mgalla (aliyesimama) akiwasilisha mada ya maadili na wajibu wa watumishi wa Mahakama katika mapambano dhidi ya rushwa.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma na Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji wa Mahakama Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka (wa pili kulia), Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kigoma, Bi. Asha Kwaliko (wa pili kushoto),  Naibu Mkuu wa TAKUKURU (M) Kigoma, Bw. John Isaac Mgallaha (wa kwanza kushoto), Hakimu Mkazi wa Wilaya Kigoma, Mhe. Anna Kahungu na waliosimama nyuma ni sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kigoma na Mahakama zake za Mwanzo.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

Ijumaa, 7 Agosti 2026

MAZOEZI YA KUJENGA AFYA YA MWILI NA AKILI YASHIKA KASI MBEYA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Uongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya wameendeleza dhamira yao ya dhati ya kujenga afya bora ya mwili na akili kupitia programu ya mazoezi ya pamoja inayofanyika kila Jumanne na Ijumaa ya kila wiki katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala hiyo.

Mazoezi hayo yanawakutanisha viongozi, wadau na watumishi wa kada mbalimbali katika mazingira yanayosaidia kukuza mshikamano, ushirikiano na ustawi wa afya, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utamaduni wa kujali afya mahali pa kazi.

Ushiriki wa Viongozi na Watumishi hao umeendelea kuwa chachu ya kuwahamasisha watumishi wengine kujitokeza kwa wingi katika zoezi hilo, jambo linalosisitiza kwamba, uwepo wa afya njema ni msingi muhimu wa kuongeza ufanisi, tija na ubora wa utoaji huduma za haki kwa wananchi.

Mbali na kuimarisha afya ya mwili, mazoezi hayo yamekuwa yakisaidia kupunguza msongo wa mawazo, kuongeza nguvu ya kiutendaji na kuimarisha mahusiano ya kikazi miongoni mwa watumishi wa Mahakama.

Nayo, timu ya mpira wa miguu ya Mahakama “Mbeya Mahakama sports” inayoundwa na wachezaji kutoka Mahakama zilizopo Mbeya Mjini imeendelea kufanya mazoezi yake katika viwanja mbalimbali huku ikiwa na mwendelezo mzuri wa kupata matokeo uwanjani.

Timu hiyo hivi karibuni imecheza mechi za kirafiki na baadhi ya timu za mpira wa miguu za taasisi na timu za wanachi huku wakiibuka na ushindi kwa mechi tatu mfululizo na kupata sare kwa mechi moja pekee iliyochezwa hivi karibuni na timu ya mpira wa miguu ya watumishi wa Hospitali ya Mkoa wa Mbeya.

Mwamko huo wa kufanya mazoezi kwa watumishi unaendelea kujenga taswira inayotambua kuwa mtumishi mwenye afya bora ni nguzo muhimu katika utoaji wa haki kwa wakati na kwa ubora unaostahili.

Aidha, kupitia utaratibu huo wa mazoezi ya kila wiki, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya inaendelea kuonesha mfano kwamba uwekezaji katika afya ya watumishi ni uwekezaji katika huduma bora kwa wananchi. Vilevile ushiriki wa pamoja kati ya watumishi wa Mahakama na wananchi katika michezo mbalimbali ni chachu ya kuisaidia Mahakama kuongeza imani ya Mahakama kwa wananchi.

Sehemu ya viongozi, wadau na watumishi Mahakama wa Kada mbalimbali wakiwa kwenye mazoezi ya pamoja yaliyowakutanisha kwa ajili ya kujenga afya ya mwili na akili ili kurejesha utimamu wa mwili katika mahala pa kazi, mazoezi hayo yanafanyika katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya. 

Sehemu ya matukio katika mazoezi mbalimbali yanayoendelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya apo.

Sehemu ya matukio katika mazoezi mbalimbali yanayoendelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya apo.

Sehemu ya matukio katika mazoezi mbalimbali yanayoendelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya apo.

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Mbeya ikiendelea na mazoezi yake katika uwanja cha shule ya msingi Nzovwe Mbeya kujiandaa na mechi zinazoendelea za kirafiki. 

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (kushoto) akiwa katika mazoezi pamoja na sehemu ya watumishi alioshiriki na mazoezi hayo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (Kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (kulia) wakiendelea kufanya mazoezi katika viunga vya Mahakama Kuu jijini Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (wa kwanza kulia) akizungumza machache wakati wa kufunga mazoezi. (wa kwanza kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (wanne kulia)

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (watano kutoka kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa kada mbalimbali baada ya mazoezi ya pamoja katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Alhamisi, 6 Agosti 2026

JAJI MAMBI ATETA NA KATIBU MKUU WA TUGHE TAIFA

Na CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi ametembelewa na Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Bw. Henry Mkunda ofisini kwake jana tarehe 05 Agosti, 2026 mjini Babati.

Akimkaribisha Katibu Mkuu huyo wa TUGHE, Jaji Mfawidhi Mhe. Dkt. Mambi alimueleza Bw. Mkunda kuwa, ujio wake ni muhimu sana katika kujadili maslahi mapana ya ushirikiano miongoni mwa watumishi wa Umma wanaounda Shirikisho hilo la wafanyakazi kutoka Taasisi mbalimbali.

“Katibu Mkuu ninakukaribisha sana Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara na tumefurahi umefika kwa kuwa ujio wako ni chachu ya kuongeza ushirikiano ambao unapaswa kuwepo miongoni mwetu sisi watumishi wa Umma. Ninaomba pia muendelee kutoa elimu kwa watumishi kuhusu umuhimu wa kujiunga kwenye vyama vya wafanyakazi,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora akitoa salamu alimshukuru Katibu huyo wa TUGHE kwa kufika mahakamani hapo na kumueleza kuwa, watumishi wa Mahakama wanapaswa kujua majukumu yanayofanywa na Vyama vya Wafanyakazi hivyo waendelee kufundishwa na kueleweshwa.

“Pamoja na jukumu kubwa tulilopewa la kusikiliza na kuamua mashauri, watumishi wetu wanastahili kupata nafasi ya kueleweshwa majukumu ya Vyama hivi vya wafanyakazi kwa sababu vyama hivi vinawasaidia sana kujua haki na wajibu wao wanapokuwa kazini kama watumishi wa umma,” ameongeza Mhe. Kamuzora.

Naye, Bw. Mkunda, aliushukuru Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ukaribisho aliopewa na kuahidi kuongeza ushirikiano miongoni mwa watumishi wa Mahakama katika kutekeleza majukumu yake ya kitaasisi kwani Chama kinategemea wanachama kwa kiasi kukubwa ili kuendesha programu zake.

“Mhe. Jaji Mfawidhi ninakushukuru sana kwa kunikaribisha ofisini kwako, nami ninaahidi kuendelea kutoa ushirikiano katika ofisi yako ili kazi zetu tunazozifanya ziende kwa ufasaha lakini pia ili tuwawezeshe watumishi wote waweze kujua haki na wajibu wao wa kila siku wanapokuwa katika mazingira ya kazi,” alisema Bw. Mkunda.

Aidha, Bw. Mkunda aliipongeza Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kuweza kumpata na kuchaguliwa Bw. Shadrack Aron ambaye ni mtumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara ambaye alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Manyara katika uchaguzi uliofanyika hivi karibuni.

Katika ziara hiyo, Mwenyekiti huyo Bw. Mkunda aliambatana na Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Manyara Bw. Shadrack Aron pamoja na Katibu wa TUGHE Mkoa wa Manyara Bw. Maulidi Kasimba.

Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara wakiwa kwenye mazungumzo yaliyokuwa yanaendelea katika ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (kiti cha mbele) wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda (aliyevalia kofia).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea ofisini kwake mara baada ya kutembelewa na Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wageni waliomtembelea ofisini kwake wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda. 

Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Manyara Bw. Shadrack Aron akifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea mara baada ya kutembelewa na Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda.

Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda akimsikiliza na kufuatilia ujumbe mahususi wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (hayupo pichani) wakati alipomtembelea ofisini kwake.


Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Devotha Kamuzora (kulia) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu hiyo Mhe. Charles Mnzava (kushoto) wakifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea katika ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi walipotembelewa na Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda (hayupo pichani).

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)