Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Geita
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, tarehe 15 Julai, 2026 alipokea ugeni kutoka Mahakama Kuu Songwe, kwa lengo la kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji wa huduma za Mahakama.
Ziara
ya Viongozi kutoka Mahakama Songwe iliongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu
ya Tanzania, Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Joyce Minde, akiwa ameambatana na
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, Afisa Utumishi pamoja
na watumishi wengine wa Mahakama hiyo.
Akifungua
kikao hicho, Mhe. Kahyoza alisema kuwa kubadilishana uzoefu ni fursa muhimu ya
kujifunza mbinu bora zinazoweza kuboresha utendaji kazi na kuimarisha utoaji wa
huduma za haki kwa ufanisi, kwa wakati na kwa kuzingatia matumizi ya
teknolojia.
Aliwahimiza
watumishi wa Mahakama Kuu Geita kuitumia kikamilifu fursa hiyo kwa kujifunza
kutoka kwa wenzao wa Songwe na kushiriki kikamilifu katika mijadala.
"Kama
una jambo la kuchangia au kuuliza, usisite kulisema. Lengo letu ni kujifunza
kutoka kwa kila mmoja ili kuboresha huduma zetu," alisema Jaji Kahyoza.
Akizungumzia
Mkoa wa Geita, Mhe. Kahyoza alisema kuwa licha ya kuwa ni Mkoa mchanga, una
mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kupitia shughuli za uchimbaji madini,
kilimo, uvuvi na ufugaji. Aidha, alisema Mkoa huo umejaliwa vivutio mbalimbali
vya utalii, ikiwemo Ziwa Victoria, Hifadhi ya Kigosi pamoja na urithi wa
utamaduni.
Kuhusu
matumizi ya TEHAMA mahakamani, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa ni takwa la kisheria
na kwamba Mahakama Kuu Geita ilianza rasmi kutekeleza mfumo wa Mahakama kidijiti
tangu ilipoanzishwa tarehe 23 Desemba, 2023, kufuatia maelekezo ya Jaji Mkuu wa
Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wakati wa uzinduzi wa masjala hiyo.
Alisema
Jaji Mkuu alielekeza Mahakama Kuu Geita kuanza shughuli zake kama Mahakama ya
kidijiti (purely digital), bila kutumia karatasi. Aliongeza kuwa
kufuatia maelekezo hayo, Masjala iliweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha
matumizi ya TEHAMA yanatekelezwa kikamilifu.
Mikakati
hiyo ilijumuisha kuendesha mafunzo ya ndani kwa watumishi, kufanya mikutano na
wadau wa Mahakama, Viongozi wa Serikali pamoja na wananchi ili kuwajengea
uelewa kuhusu umuhimu wa kuondokana na matumizi ya karatasi katika utoaji wa
huduma za Mahakama.
Kwa
upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita,
Mhe. Fredrick Lukuna, aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya Mfumo wa
Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (ECMS), akieleza namna mfumo huo
unavyowezesha uendeshaji wa mashauri bila matumizi ya karatasi.
Alisema
mfumo huo umeongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri kwa kuwezesha
ufuatiliaji wa mwenendo wa kesi, kupunguza mlundikano wa mashauri, kuharakisha
utoaji wa haki na kuimarisha uwazi katika shughuli za Mahakama.
Aidha,
alieleza kuwa matumizi ya TEHAMA yameboresha utunzaji wa kumbukumbu za mashauri
kwa kuondoa changamoto ya upotevu wa mafaili, kurahisisha upatikanaji wa hukumu
na maamuzi kupitia hifadhidata, kuboresha usahihi wa takwimu za Mahakama pamoja
na kupunguza muda na gharama za uendeshaji kupitia matumizi ya Mahakama pepe.
Akizungumza
kuhusu mafanikio ya Taasisi, Mhe. Lukuna alisema kuwa ni muhimu kuwa na malengo
yaliyo wazi na yanayopimika, kujenga timu yenye nidhamu, kusimamia muda kwa
ufanisi na kuendelea kuwajengea uwezo watumishi kupitia mafunzo endelevu.
"Ni
muhimu kudumisha mahusiano mazuri kazini, kujifunza kutokana na makosa
yaliyopita, kubaini changamoto zinazochelewesha utendaji, kuhakikisha
rasilimali muhimu zinapatikana na kuwa tayari kufanya maamuzi yatakayochochea
mafanikio ya pamoja," alisema.
Naye
Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, alieleza namna masjala hiyo
ilivyoondokana na matumizi ya karatasi kwa kutumia mifumo ya kidijitali katika
mawasiliano na utunzaji wa nyaraka.
Alisema
hatua hiyo imeongeza ufanisi wa kazi, kupunguza gharama za ununuzi wa mafaili
na vifaa vya kuhifadhia nyaraka, kuimarisha usalama wa taarifa kwa kupunguza
hatari ya uvujaji wa taarifa, kurahisisha utoaji wa huduma kwa wateja na
kuongeza ubunifu katika utendaji kazi.
Bi.
Kisasila aliwashauri washiriki kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mara kwa mara
wa mifumo ya TEHAMA, kutoa motisha kwa watumishi na kuendelea kuendesha mafunzo
ya ndani ili kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.
Kwa
niaba ya ujumbe kutoka Songwe, Mhe. Minde, alitoa shukrani kwa uongozi wa
Mahakama Kuu ya Geita kwa mapokezi mazuri na mafunzo yenye tija yaliyotolewa
wakati wa ziara hiyo.
Alimshukuru
Jaji Mfawidhi, Naibu Msajili, Mtendaji pamoja na watumishi wote wa Mahakama Kuu
ya Geita kwa ushirikiano waliouonyesha licha ya taarifa ya ujio wa ujumbe huo
kutolewa kwa muda mfupi. Aidha, aliahidi kuwa maarifa na uzoefu walioupata
vitatekelezwa na kusambazwa katika vituo vyao vya kazi ili kuboresha utoaji wa
huduma za Mahakama.






























