Alhamisi, 19 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJADILI BAJETI YA MWAKA 2026/2027

  • Mtendaji Mkuu asema bajeti iakisi dira, kuimarisha msingi wa utoaji haki
  • Asisitiza nidhamu ya matumizi, ulinzi wa Mahakama za Mwanzo

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amesema maandalizi ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27 yanapaswa kwenda sambamba na mipango ya kimkakati ya Mahakama na kulenga kuimarisha utoaji wa haki kwa ufanisi zaidi.

Prof. Ole Gabriel alisema hayo wakati anafungua kikao cha mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 na uchambuzi wa maoteo ya bajeti ya 2026/27 kilichofanyika tarehe 16 Februari 2026 katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Alikumbusha kuwa Julai Mosi 2025, wakati utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 ulipoanza, alitoa waraka ulioelekeza masuala ya msingi ya kuzingatia, ikiwemo kudhibiti ulimbikizaji wa madeni, kuzingatia Sheria ya Bajeti Na. 11 ya Mwaka 2015 na kutohamisha fedha kutoka vifungu vya Mahakama za Mwanzo na Wilaya kwenda Mahakama za juu. Alisema maelekezo hayo yalilenga kuimarisha nidhamu ya matumizi na kuhakikisha rasilimali zinatumika kwa mujibu wa sheria.

“Kuna wakati unaweza kutamani kufanya malipo fulani, lakini kama ni nje ya utaratibu na nje ya sheria huwezi kufanya, kwa sababu itatuletea hoja za ukaguzi. Majukumu yetu tunapaswa kuyafanya kwa mujibu wa sheria na si vinginevyo,” alisema, akitoa shukrani kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Fedha na Uhasibu kwa mchango wao mkubwa katika kuhakikisha Mahakama inaendelea kuwa kinara wa Taasisi za umma zenye hati safi ya hesabu.

Alisema mafanikio hayo ni matokeo ya mipango madhubuti na usimamizi thabiti wa fedha, akisisitiza kuwa rasilimali fedha huwa hazitoshi, hivyo upangaji sahihi ni muhimu ili kufikia matarajio na Dira ya Mahakama. Alieleza kuwa mapitio ya nusu mwaka yanatoa fursa ya kujitathmini kama utekelezaji unaendana na mipango na kama Taasisi iko katika mwelekeo sahihi.

Akigusia suala la Mahakama za Mwanzo, Prof. Ole Gabriel alisema kuwa zaidi ya asilimia 70 ya mashauri huanzia katika ngazi hiyo, hivyo ni lazima zilindwe na kuimarishwa. Alibainisha kuwa katika bajeti ya sasa, Mahakama za Mwanzo zimeongezewa fedha kwa asilimia 100 kwa makusudi maalum, na akaelekeza fedha hizo ziende moja kwa moja katika ngazi hiyo.

“Haikuwa kwa bahati mbaya. Tulimaanisha kulinda Mahakama za Mwanzo kwa sababu ndizo msingi wa utoaji haki kwa wananchi wengi,” alisema.

Aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/27, Mahakama inapanga kuongeza uwekezaji katika ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama za Mwanzo ili kuboresha mazingira ya utoaji haki na kuongeza imani ya wananchi.

Kuhusu rasilimali watu, alisema Mahakama imeendelea kuiomba Serikali kuongeza watumishi kwa kuwa bila rasilimali watu ya kutosha, utoaji haki unaweza kukwama. Alieleza kuwa tayari kibali cha ajira 642 kimepatikana na mchakato wake umekamilika kupitia Tume ya Utumishi wa Mahakama, akiwashukuru watendaji wote waliohusika katika zoezi hilo.

Aidha, aliwahimiza washiriki kutoa ushiriki wa dhati katika maandalizi ya Mpango Mkakati wa Tatu wa Mahakama, akibainisha kuwa mafanikio ya mpango huo yatategemea tathmini ya mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mipango iliyopita na ushiriki wa pamoja katika kuweka mikakati mipya inayopimika.

Alieleza pia umuhimu wa kuunganisha udhibiti wa vihatarishi katika maandalizi na utekelezaji wa bajeti ili kuhakikisha mipango inayowekwa inatekelezeka bila kuathiri malengo makuu ya Taasisi.

Prof. Ole Gabriel aliwataka wasimamizi wa bajeti katika kanda na divisheni kuandaa bajeti zinazoakisi uhalisia wa mahitaji na kuongeza thamani katika utoaji wa haki.

“Jiulizeni kila wakati: Shughuli hii ninayoipangia fedha inatusaidiaje kufikia malengo yetu makuu. Tuwekeze kwenye maeneo yenye matokeo makubwa na yanayoakisi uhalisia,” alisisitiza.

Alisema maandalizi ya bajeti ni mchakato wa kimkakati unaobeba mustakabali wa Mahakama na kwamba uwajibikaji, ushirikiano na nidhamu ya matumizi ni nguzo muhimu za kuendelea kuimarisha Taasisi hiyo na kulinda imani ya wananchi.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, alisema bajeti ni nyenzo ya kimkakati inayopaswa kuakisi dira na dhamira ya Taasisi katika utoaji wa haki.

Alisisitiza kuwa maandalizi ya bajeti ya 2026/27 yanapaswa kuendana na maandalizi ya Mpango Mkakati wa Tatu wa Mahakama ili kuhakikisha mipango inayowekwa inatekelezeka na inapimika.

“Haki inapaswa kutolewa kwa wakati na kwa usawa. Hilo linahitaji mipango madhubuti na usimamizi makini wa rasilimali,” alisema.

Mhe. Nkya pia alisisitiza umuhimu wa kuendelea kupunguza mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama, pamoja na kuimarisha matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA] katika usimamizi wa mashauri ili kuongeza uwazi na ufanisi.

Kikao hicho kimeweka msingi wa mchakato wa upangaji wa rasilimali kwa mwaka wa fedha 2026/27, kikionesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuendelea kuimarisha utendaji, uwajibikaji na utoaji wa haki kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya Taifa.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akizungumza wakati anafungua kikao cha mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 na uchambuzi wa maoteo ya bajeti ya 2026/27 kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho.

Sehemu ya Watendaji na Naibu Wasajili kutoka Kanda na Divisheni [juu na picha mbili chini] wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa kikao hicho.



Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa kikao hicho [juu na chini].



 

 

Jumatano, 18 Februari 2026

WEKEZENI KWENYE WATAALAMU NA MIUNDOMBINU YA TEHAMA: PROF. OLE GABRIEL

 Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama, Arusha

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel  amewashauri wakuu wa Taasisi mbalimbali za Serikali na Mashirika ya Umma kuwekeza kwenye Wataalamu na Miundombinu ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuongeza tija na ufanisi katika kazi.

Akiwasilisha Mada kuhusu Mifumo ya Kielekitroniki ya Ubadilishanaji wa Taarifa kwa kutumia Akili Unde kwenye Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Serikali Mtandao leo tarehe 18 Februari, 2026 jijini Arusha, Prof. Ole Gabriel alisema kuwekeza kwenye Utaalam na miundombinu ya TEHAMA kutazisaidia Taasisi na Mashirika ya Umma kuongeza tija na ufanisi.

Prof. Ole Gabriel alisema kuwa  Mahakama ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika  matumizi ya mifumo mbalimbali ya Kielekitroniki ambayo imerahisisha kwa kiasi kikubwa shughuli za utoaji haki nchini na kutoa muda kwa wananchi kushiriki katika shughuli za kujiongezea kipato.

”Taasisi inapojikita kwenye matumizi ya mifumo ya Kielekitroniki husaidia kuokoa muda kwa kuwa wananchi watapatiwa huduma kwa haraka na kwenda kufanya shughuli za uzalishaji”, alisisitiza Mtendaji Mkuu.

Mkutano wa Sita wa mwaka wa Serikali Mtandao unafanyika jijini Arusha ambapo umewakutanisha Wataalam wa masuala ya TEHAMA na wataalamu wengine zaidi ya 1,000 kutoka Taasisi mbalimbali na mashirika ya Umma ili unajadili  jitihada za Serikali Mtandao, mafanikio pamoja na changamoto zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa jitihada hizo na namna ya kukabiliana nazo.

Aidha. Mkutano huo wa siku tatu unatarajiwa kumalizika kesho tarehe 19 Februari, 2026. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasilisha Mada kuhusu Mifumo ya Kielekitroniki ya Ubadilishanaji wa Taarifa kwa kutumia Akili Unde kwenye Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Serikali Mtandao leo tarehe 18 Februari, 2026 jijini Arusha,   
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa kwenye Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Serikali Mtandao leo tarehe 18 Februari, 2026 jijini Arusha.   
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akitoa ufafanuzi wa hoja wakati wa Majadiliano mara baada ya kuwasilisha Mada kuhusu Mifumo ya Kielekitroniki ya Ubadilishanaji wa Taarifa kwa kutumia Akili Unde kwenye Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Serikali Mtandao leo tarehe 18 Februari, 2026 jijini Arusha.   
Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Ajira) Bi. Enziel Mtei (wa kwanza kulia) akiwa kwenye Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Serikali Mtandao leo tarehe 18 Februari, 2026 jijini Arusha.   
Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Maadili na Nidhamu) Bi. Alesia Mbuya (katikati) akiwa kwenye Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Serikali Mtandao leo tarehe 18 Februari, 2026 jijini Arusha.   




TANZIA: HAKIMU MAHAKAMA YA MWANZO MIKESE AFARIKI DUNIA


Mhe. Asajile Joshua Mhando enzi za uhai wake.

Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen M. Magoiga, anasikitika kutangaza kifo cha Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Mwanzo Mikese, Mhe. Asajile Joshua Mhando, aliyefariki Dunia tarehe 17 Februari, 2026 saa 7.00 mchana katika Hospitali ya Platnum mjini Morogoro alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kujisikia vibaya akiwa kazini.

Taratibu za mazishi zinaendelea kuratibiwa, na mara baada ya kukamilika zitatolewa.

Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro unatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na watumishi wote kwa msiba huu mzito.

Bwana alitoa, Bwana ametwaa jina lake lihimidiwe.

 

Jumatatu, 16 Februari 2026

JAJI MFAWIDHI DAR ES SALAAM AONGOZA ZIARA YA UTOAJI MSAADA KWA WANAFUNZI WENYE UHITAJI PUGU

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi jana tarehe 15 Februari, 2026 aliwaongoza watumishi wanawake wa Kanda hiyo kutoa msaada wa vifaa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum wa Shule ya Sekondari Pugu iliyoko jijini Dar es Salaam.

Akizungumza akiwa ofisini kwa Mkuu wa Shule ya Sekondari Pugu, Mhe. Maghimbi alieleza dhumuni la wao kufika shuleni hapo kuwa ni matokeo ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika mwaka jana 2025 na wao kama wanawake watumishi wa Mahakama Kanda ya Dar es salaam walikuwa na vitu ambavyo wao waliwiwa kuvitoa kwa wanafunzi hao lakini baada ya kuvitoa waliomba wapewe mahitaji ya msingi yanayohitajika kwa wanafunzi hao.

Jaji Maghimbi alisema baada ya kupata mahitaji hayo, watumishi wanawake wa Mahakama Kanda ya Dar es Salaam walichanga pesa ili kufanikisha upatikanaji wa vifaa hivyo na pia waliwashirikisha baadhi ya wanaume ambao waliguswa nao walichangia na hivyo kuweza kupatikana kwa mahitaji yote yaliyohitajika.

Aliongeza kuwa, kama kinamama watumishi wa Mahakama Kanda ya Dar es salaam wameomba mahusiano ya karibu na shule hiyo na chochote kitakachotokea wameomba kuwasiliana ili kwa kile watakachoweza kusaidia wasaidie. 

Akizungumzia kuhusu taarifa ya Mwalimu Msuya, Mhe. Maghimbi alisema siku zote yeye amekuwa akifikiri kuwa ana msongo wa kazi anayoifanya lakini alipomsikiliza Mwalimu Msuya na kazi ya kuhudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum, alikiri kwamba amepata nguvu mpya ya kufanya kazi na ameona kazi yake haina msongo kama ilivyo ya walimu hao, “kama unafikiri una tatizo fikiri tena,” alisema Mhe. Maghimbi kwa msisitizo. 

Aidha, akizungumza na wanafunzi wenye mahitaji maalum, Jaji Maghimbi aliwaeleza dhumuni la safari hiyo na kusema kwamba baada ya kutembelea kwa mara ya kwanza waliona kwamba wanatakiwa kufanya nacho kazi kwa ukaribu kutokana na mioyo yao na wala sio mfumo wa kazi yao. 

Aidha, aliwapongeza wanafunzi hao kwa matokeo mazuri katika mitihani yao na kuwaambia kuwa wao wameonesha kuwa chochote kinawezekana kwa sababu wanao uwezo wa kufanya vitu, kwakuwa uwezo wa kufikiria na kuelewa kile kinachofanyika na kuwa makini na kuwasihi kuwa na moyo huo pasipo kuteteleka. 

Akizungumzia kuhusu Mchepuo mpya ulioanzishwa shuleni hapo wa Sanaa kwa Masomo ya Historia, Lugha ya Kiingereza na Jiografia, Mhe. Maghimbi aliwatia moyo kuwa, hayo sio masomo wa wanawake kama wanavyofikiria bali ni masomo yanasomwa na wanaume pia.

Aliongeza kuwa, kutokana na kuanzishwa kwa mchepuo huo kuna uwezekano mkubwa wa kuwapata Wanasheria, Majaji na Mahakimu na hivyo Mhe. Maghimbi ametoa mwaliko maalum kwa Wanafunzi wa masomo hayo kutembelea Mahakama na kuona shughuli za kimahakama zinavyoendeshwa.

Kabla ya kukabidhi vifaa hivyo, Jaji Maghimbi alipata wasaa wa kupata historia fupi ya Shule hiyo kutoka kwa Makamu Mkuu wa Shule Taaluma, Mwalimu Juma Msuya ambapo alisema shule hiyo ilianzishwa mwaka 1948 ikiitwa Mtakatifu Francis ikiwa chini ya Kanisa Katoliki na kwamba baada ya kupata uhuru ilibinafsishwa na kuitwa Pugu na ilianza na jumla ya Wanafunzi nane (8) na mpaka sasa shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 1000 wa Kidato cha Kwanza mpaka cha Sita.

Mwalimu Msuya alisema kati ya wanafunzi hao wapo Watoto wenye mahitaji maalum kuanzia mwaka 1990 Serikali ilipoingia Mkataba wa Elimu Jumuishi ndipo shule hiyo ilitakiwa kupokea Watoto wenye mahitaji maalum haswa wale wa viungo ingawa kwa sasa wanachukua mchanganyiko wale wenye uziwi hafifu, mgongo wazi hasa wale wenye vichwa vikubwa.

Mwalimu huyo aliongeza kuwa, mwanzo Watoto hao walikuwa hawafanyi vizuri darasani lakini kwa bahati nzuri Serikali imeajiri Walimu wenye elimu maalum ambao wamepambana mpaka sasa wamefanikiwa kufuta daraja sifuri (division zero) na hata daraja la nne (division four). Matokeo ya juzi kulikuwa na Watoto 24 lakini hakuna aliyetoka daraja la tatu wala la nne.

“Watoto utakapowaona na ukiangalia na mafanikio wanayoyafanya ndipo utakapoamini ‘disability is not inability’ kwamba kutokana na ulemavu alionao basi anashindwa kila kitu hapana ni pale wanapowezeshwa basi na wenyewe wanaweza,” alieleza Mwalimu Msuya.

Mwalimu huyo alisema kuwa, kuna baadhi ya Wanafunzi hao hawawezi kuandika hivyo wanapata usaidizi wa notisi na ndio maana wameomba mashine za kuchapia na kurudufu. Na kuna baadhi wanatumia kompyuta ambazo kuna baadhi wamepatiwa na Serikali.

Akizungumza wakati wa kutoa maoni na maombi ya mahitaji mengine Mwanafunzi aliyejulikana kwa jina maarufu Bangimoto alisema anachukizwa na tabia ya baadhi ya watu wenye ulemavu kukaa barabarani na kuomba badala ya kujishughulisha na kupata kipato halali.

Mwanafunzi huyo aliongea kwa uchungu na kuonyesha namna gani walemavu wanachukuliwa na jamii kutokana na wao mwenyewe kuubeba udhaifu.

Vitu vilivyokabidhiwa katika ziara hiyo ni pamoja na mashine mbili za kisasa cha kuchapa zenye skana na kurudufu, karatasi katoni  40, wino sita (6), flashi za hizo mashine, mashuka tisa, Madaftari (Counter books) seti mbili, ‘diapers’ katoni  mbili, sabuni za unga, kipande na za kuogea, mafuta kwa ajili ya watu wenye changamoto ya Ngozi (albino) na vitu vingine vingi pamoja na vinywaji baridi ambavyo vimegharimu jumla ya fedha za Kitanzania 5,564,000/=.

Katika ziara hiyo ya Jaji Mfawidhi, Mhe. Maghimbi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Ubungo, Mhe. Tumsifu Barnabas na Kigamboni Mhe. Mwanakombo Athuman, Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Lucy Tuikailize, Msaidizi wa Kumbukumbu, Mwandishi Mwendesha Ofisi pamoja na Madereva. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akikabidhi vifaa vya Shule kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum wa Shule ya Sekondari Pugu walipotembelea shule hiyo hivi karibu kwa lengo la kutoa msaada kwa wanafunzi hao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi  akisaini kitabu cha wageni katika Ofisi ya Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Pugu.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo (aliyevaa fulana ya bluu) akitoa utambulisho wa wageni waliongozana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi walipotembelea Shule ya Sekondari Pugu kwa ajili ya kutoa msaada kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo (kushoto), Makamu Mkuu wa Shule Utawala (kulia), Mwalimu Ndimwangwa Nzota.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi  (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Walimu wa Shule ya Sekondari Pugu na Watumishi wanawake wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

'USULUHISHI NI SUALA LINALOHITAJI UVUMILIVU NA USIKILIZAJI WA UMAKINI'

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma ametoa rai kwa Wasuluhishi nchini kuwa wavumilivu na kusikiliza kwa makini wakati wanapofanya usuluhishi.

Mhe. Maruma aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tatu ya Upatanishi kwa Mahakimu na Wasajili wa Kanda ya Dar es Salaam yaliyofanyika kuanzia tarehe 11 hadi 13, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Temeke.

Jaji Maruma alisema, endapo Msuluhishi ana haraka, hana uvumilivu na hana usikivu hawezi kufanya usuluhishi na kwamba kama Msuluhishi akiwa hana usikivu na uvumilivu hata wale anaowasuluhisha hawawezi kumuamini, wadaawa wakimuangalia msuluhishi wanajua tu kwamba anawajali na kuwasikiliza ama la.

Ameongeza kuwa, uvumilivu na utulivu unasababisha usuluhishi, hivyo kuwataka kuwa wavumilivu hata kama wadaawa watawashambulia kwa maneno makali wao wawe chanya na wavumilie hatua hiyo itasababisha wadaawa kurudi kwenye mstari, hivyo usuluhishi kuendelea na kufanikiwa.

Awali akifungua mafunzo hayo, Mhe. Maruma alieleza kuwa, mafunzo hayo ni mwendelezo wa juhudi za Mahakama katika kuwajengea uwezo watumishi wake ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Jaji Maruma alisema mafunzo hayo, yanafanyika wakati muafaka na muhimu sana wakati Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inahimiza usuluhishi kama nyenzo  muhimu ya msingi  mkuu katika kuleta amani, umoja na utulivu  katika Taifa letu.

“Hii inaendana na mikakati ya Mahakama  katika kukuza matumizi ya usuluhishi ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo  kama inavyosisitizwa  katika ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisisitiza.

Aidha Mhe. Maruma afafanua kwamba Mahakama zinaendelea kukabiliwa na ongezeko la mashauri ambayo mengi kati yake yanaweza kutatuliwa kwa haraka, kwa gharama nafuu na kwa maridhiano bila kupita mchakato mrefu wa mashauri ya shauri la kawaida hivyo kuokoa gharama na muda ambao utatumika katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Alisema kuwa, upatanishi wa Mahakama umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuwezesha migogoro kumalizika kwa haraka na kwa sasa ongezeko la upatanishi limezidi asilimia 50 tofauti na hali ilivyokuwa miaka minne nyuma.

“Hali hii inatupa matumaini na chachu ya kuendelea kuwajengea uwezo Mahakimu na wadau wa usuluhishi ili kuongeza ufanisi katika kutatua migogoro kupitia upatanishi na kufika malengo yaliyopo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ya kutumia njia hii katika kuleta  amani na utulivu katika jamii zetu,” alisema Jaji Maruma.

Aliongeza kwamba, mafunzo hayo ni maandalizi ya Wiki ya Usuluhishi ambayo imepangwa kufanyika mwezi Machi nchini kote na kusema kuwa mafunzo hayo ni mwanzo wa mafunzo ambayo yataendelea kutolewa kwa Majaji, Mahakimu na Wadau ili kujenga uwezo wa ufanisi wa kutekeleza njia ya upatanishi katika kuharakisha upatikanaji wa haki.

Kadhalika alisema kwamba, ushiriki wa Majaji, Mahakimu, Wasajili na wadau wa Taasisi nyingine unaonesha kuwa, usuluhishi si jukumu la mtu mmoja bali ni juhudi ya pamoja ya taasisi zote zinazohusika na utoaji haki. Majaji na Mahakimu ingawa si Wasuluhishi katika mashauri yao, ni wasimamizi na walezi wa mchakato wa usuluhishi, hivyo ni muhimu kuwa na uelewa wa kina wa msingi, taratibu na falsafa ya usuluhishi.

Naye Naibu Msajili ya Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi Mhe.Augustina Mmbando alisema, Usuluhishi huimarisha  upatikanaji wa haki mapema ipasavyo, kwa gharama nafuu na kwa kuzingatia mahusiano ya kijamii na kibiashara.

Mhe. Mmbando alisema usuluhishi sio mbadala wa Mahakama bali ni nyenzo inayosaidia Mahakama kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na kwa mtazamo unaomjali binadamu.

Akizungumzia kuhusu miongoni mwa Wadau waliohudhuria mafunzo hayo ambao ni Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Mhe. Mmbando alisema uwepo wa TIRA katika mafunzo hayo una umuhimu wa pekee kwa kuwa Sekta ya Bima ni miongoni mwa sekta zinazozalisha migogoro mingi ya kibiashara na kimikataba ambayo kwa asili yake inafaa kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi.

Aliongeza kuwa, ushirikiano kati ya Mahakama na Taasisi za Udhibiti kama TIRA ni nguzo muhimu katika kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haraka, haki na kwa namna inayohifadhi mahusiano na kuimarisha imani ya wadau katika mfumo wa haki.

Naye Mwezeshaji katika mafunzo hayo Mhe. Mhangwa Yunge alisema usuluhishi ni mzuri kwakuwa unaokoa muda na pia Wadaawa wanabaki na amani na kuongeza kuwa sio kila mgogoro unaweza kusuluhishwa bali kuna migogoro mingine wahusika wanakuwa hawako tayari kusuluhishwa.

Mafunzo hayo yaliwezeshwa na Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Angela Bahati na Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke, Mhe. Mhangwa Yunge.

Mafunzo hayo yalihudhuriwa na Naibu wasajili, Mahakimu, Wadau na Mtendaji wa Mahakamu Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa.

 Jaji  Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akifundisha mada wakati wa Mafunzo yaliyotolewa hivi karibuni kwa Wasuluhishi wa Mahakama.


Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo kwa Wasuluhishi wa Mahakama, Mhe. Mhangwa Yunge akiwaongoza washiriki wa mafunzo hayo kuimba wimbo uliotungwa wakati wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi na Mwezeshaji wa Mafunzo (kulia), Mhe. Angela Bahati Salema na Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Mhangwa Yunge wakisikiliza michango iliyokuwa ikitolewa na washiriki wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha usuluhishi na mwezeshaji wa mafunzo, Mhe. Angela Bahati Salema (kulia) akipokea cheti katika hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo ya Upatanishi, Mhe. Mhangwa Yunge akipokea cheti katika hafla ya kufunga mafunzo hayo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbado  akipokea cha ushiriki wa mafunzo katika hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 


 

MAHAKAMA KITUO CHA USULUHISHI YAENDESHA MAFUNZO YA UPATANISHI KWA MAHAKIMU, NAIBU WASAJILI

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], hivi karibuni kiliendesha mafunzo ya siku tatu yanayohusu ya upataniishi wa Mahakama ili kuimarisha uwezo wa kutumia njia ya upatanishi ambayo ni rafiki katika utatuzi wa migogoro.

Mafunzo hayo ya siku tatu yaliyoanza tarehe 11 Februari, 2026, yakiwaleta pamoja Mahakimu wa ngazi zote pamoja na Naibu Wasajili kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Divisheni, yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma.

Akizunzungumza kwenye ufunguzi huo, Mhe. Maruma alieleza kuwa mafunzo hayo yamefanyika katika wakati muafaka na muhimu wakati dira ya 2050 inahimiza usuluhishi kama nyenzo muhimu ya msingi mkuu katika kuleta amani, umoja na utulivu katika taifa letu.

‘Hii inaendana na mikakati ya Mahakama katika kukuza matumizi ya usuluhishi ili kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo kama inavyosistizwa katika ibara ya 107A (2) (d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,’ alisema.  

Jaji Mfawidhi alibainisha kuwa mafunzo hayo pia ni moja ya maandalizi ya Wiki ya Usuliuhishi ambayo imepangwa kufanyika mwezi Machi 2026 nchini kote, hivyo, ni mwanzo wa mafunzo ambayo yataendelewa kutolewa kwa Majaji, Mahakimu na Wadau ili kujenga uwezo wa ufanisi wa kutekeleza njia hiyo ya upatanishi katika kuharakisha upatikanaji wa haki.

Mhe. Maruma alibainisha kuwa Mahakama zinaendelea kukabiliwa na ongezeko la mashauri, ambayo mengi kati yake yanaweza kutatuliwa kwa haraka, kwa gharama nafuu, na kwa maridhiano, bila kupitia mchakato mrefu wa mashauri, hivyo kuokoa gharama na muda ambao utatumika katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Alieleza kuwa upatanishi wa Mahakama umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuwezesha migogoro kumalizika kwa haraka na kila mmoja ni mashuhuda wa ongozeko la migogoro inayomalizika katika hatua ya upatanishi ambayo kwa sasa inazidi asilimia 50, tofauti na hali ilivyokuwa miaka minne nyuma.

Hali hii inatupa matumaini na chachu ya kuendelea kuwajengea uwezo Mahakimu na Wadau wa usuluhishi ili kuongeza ufanisi katika kutatua migororo kupitia upatanishi na kufikia malengo yaliyopo katika dira ya 2050 ya kutumia njia hii katika kuleta amani na utulivi katika jamii zetu pamoja na kuchangia katika uchumi endelevu,’ alisema.    

Jaji Mfawidhi alieleza pia kuwa upatanishi unaofanyika nje na ndani ya Mahakama hauondoi mamlaka ya Mahakama, bali unaikamilisha na kusaidia upatikanaji wa haki, kuondoa mrundikano wa mashauri, kuokoa muda na rasilimali, kulinda mahusiano ya kijamii na kibiashara, na kuwapa wahusika nafasi ya kushiriki kikamilifu katika kupata suluhu ya migogoro.

Alisema kuwa mafunzo hayo, siyo ya kiutaratibu pekee, bali ni uwekezaji katika kujenga uwezo, maadili, na taaluma ya wapatanishi wa Mahakama na wadau wa usuluhishi.  

Mhe. Maruma alitumia fursa hiyo kutoa shukrani za dhati kwa chuo cha IJA kwa kubali ombi lao la kushirikiana nao katika kuendesha mafunzo hayo ambayo ni muendelezo wa juhudi za Mahakama katika kuwajengea uwezo wa watumishi wake ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Natambua kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mafunzo ya upatanishi tayari yameshafanyika kwa Majaji na Mahakimu zaidi ya mia moja na baadhi yao ndio wamekuwa wakufunzi wa mafunzo haya ambayo ni endelevu,’ alisema.

Jaji Mfawidhi alitumia fursa hiyo pia kuwashukuru Wadau muhimu kwa kushirikiana na Kituo katika kuwezesha mafunzo hayo bila kusita pale walipowafikia.

Alieleza kuwa hatua hiyo inaashiria mwanzo wa ushirikiano ambao utakuwa endelevu na kutaleta faida kubwa katika kukuza, kuongeza ufanisi na kuhamasisha si tu matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro bali hata katika kuibua changamoto zinazokwamisha na kuzifanyia kazi kwa pamoja.

Awali, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbando, alieleza kuwa ushiriki wa Majaji, Mahakimu, Naibu Wasajili na Wadau wa Taasisi nyingine unaonesha kuwa usuluhishi si jukumu la mtu mmoja, bali ni juhudi ya pamoja zinazohusika na utoaji haki.

‘Majaji na Mahakimu, ingawa si wasuluhishi katika mashauri yao, ni wasimamizi na walezi wa mchakato wa usuluhishi, na hivyo ni muhimu kuwa na uelewa wa kina wa misingi, taratibu na falsafa ya mediation.

Aidha, Mhe. Mmbando alielezea kutambua kwa heshima uwepo wa Mratibu wa Mafunzo kutoka IJA, ambaye mchango wake ni muhimu katika kujenga uwezo wa Mahakama kupitia mafunzo endelevu na ya vitendo.

Alieleza pia kuwa uwepo wa TIRA katika mafunzo hayo una umuhimu wa pekee kwani bima ni miongoni mwa sekta zinazozalisha migogoro mingi ya kibiashara na kimkataba, ambayo kwa asili yake inafaa kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi.

‘Ushirikiano kati ya Mahakama na taasisi za udhibiti kama TIRA ni nguzo muhimu katika kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haraka, haki, na kwa namna inayohifadhi mahusiano na kuimarisha imani ya wadau katika mfumo wa haki,’ alisema.

Picha ya Meza Kuu, katikati ni Mhe. Zahra Maruma, kulia ni Mhe. Angela Bahati na kushoto ni Bi. Magreth Magumi.

Mgeni Rasmi akifungua mafunzo.

Meza Kuu na Wakufunzi wa usuluhishi.

Meza Kuu na Naibu Wasajili.

Meza Kuu na Mahakimu wa ngazi zote [juu na chini].


Washiriki wote wakiwa kwenye mafunzo [juu na chini].


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma