Jumatano, 26 Agosti 2026

TRAB YATEMBELEA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA YA TANZANIA

Na HABIBA MBARUKU-Mahakama, Dodoma

Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania (Tanzania Revenue Appeals Board-TRAB) leo tarehe 26 Agosti, 2026 wametembelea Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania ili kujifunza kwa vitendo jinsi mifumo mbalimbali ya Mahakama, hususan Mfumo wa Kielektronki wa Usimamamizi wa Mashauri (e-CMS) inavyofanya kazi.

Ziara hiyo inalenga kuimarisha uelewa wa namna mifumo ya Mahakama kwenye utoaji haki inavyotekeleza majukumu yake kwa kutumia teknolojia za kisasa.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Richard Kabate, pamoja na Wataalamu wa TEHAMA wa Mahakama, walieleza kwa vitendo namna mfumo wa e-CMS wa Mahakama unavyofanya kazi zake za kusimamia mashauri katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

Wajumbe hao walipata fursa ya kuuliza maswali kuhusu mfumo huo, na baadaye kutembelea Chumba Maalumu cha Usimamizi wa Taarifa za Mahakama (Judiciary Situation Room) pamoja na Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre).

Ugeni huo uliongozwa na Mwenyekiti Msaidizi wa TRAB, huku Wajumbe wengine wakiwa Katibu Mtendaji wa TRAB, Mkurugenzi wa Sheria wa TRAB, Maofisa kutoka Wizara ya Fedha pamoja na wengine.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Richard Kabate, akitoa wasilisho kwa Menejimenti, Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania pamoja na Maofisa kutoka Wizara ya Fedha namna Mfumo wa Kielektronki wa Usimamamizi wa Mashauri unavyofanya kazi leo tarehe 26 Agosti, 2026, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Sheria wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania, Bi. Sekela Mwabukusi akisikiliza wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Richard Kabeta (hayupo pichani).

Katibu Mtendaji Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania, Bi. Bahati Ndoserua, akisikiliza wasilisho.

Menejiment na Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania wakifuatilia maelekezo ya namna Mahakama inavyofuatilia mwenendo wa shughuli zake kupitia Chumba Maalumu cha Usimamizi wa Taarifa za Mahakama (Judiciary Situation Room).

Picha ya pamoja ya Menejiment, Wajumbe wa TRAB na Watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania, walipotembelea Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha Mahakama ya Tanzania.

Picha nyingine ya pamoja ikijumuisha Menejiment, Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania na Watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania baada ya kumaliza ziara yao Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Picha ya Meza Kuu, kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Richard Kabate, na kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania, Bw. Christopher David.

WATUMISHI WANAOFANYA MAJUKUMU YA ZIADA SINGIDA WAJENGEWA UWEZO

Na EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama- Singida

Watumishi wanaofanya majukumu ya ziada Mkoani Singida wamepatiwa mafunzo yaliyosheheni mada mbalimbali kwa ajili ya kuwajengea uwezo ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi.

Watumishi hao 14 wanaonufanika na mafunzo hayo ni Wasaidizi wa Ofisi na Walinzi kutoka Wilaya ya Singida, Manyoni na Iramba ambao mbali na kufanya majukumu ya Kada walizoajiriwa nazo ambazo ni ulinzi na Usaidizi wa Ofisi lakini wamekuwa wakifanya kazi za usaidizi wa kumbukumbu na kuingia Mahakamani.

Akifungua mafunzo hayo tarehe 21 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Singida, Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi aliwapongeza watumishi hao kwa kuwa tayari kufanya majukumu hayo katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa watumishi.

“Watumishi wenzangu kipekee kabisa niwashukuru kwa utayari mliouonesha na kuwa wabunifu kuhakikisha shughuli za kila siku za Mahakama hazikwami, hivyo basi kwa umuhimu tumeona kuandaa mafunzo haya ya kuwajengea uwezo ili kuhakikisha mnatoa huduma bora zaidi kwa wateja na kuhakikisha tunafikia malengo ya taasisi,” alisema Mhe. Kyaruzi.

Aidha, Naibu Msajili huyo aliwasisitiza washiriki kuwa huru wakati wa kuchangia mada na kubainisha maeneo ambayo yanahitaji kuboreshwa kwani Menejimenti inaamini baada ya mafunzo hayo kutakuwa na mabadiliko makubwa katika utendaji kazi.

Mada zilizotolewa ni pamoja na Majukumu ya kila siku katika Masjala za Mahakama za Mwanzo, Masuala ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na matumizi sahihi ya Mashine za kufanyia (POS) na Masuala ya uhasibu hususani kwenye kuandaa taarifa za maduhuli na ujazwaji wa vitabu.

Watoaji wa mada hizo walikuwa ni Bw. Paul Ndonde, Msaidizi wa Kumbukumbu, Bi. Elizabeth Bwaila, Ofisa Hesabu Msaidizi na Bi.Valentina Nkullanga, Ofisa TEHAMA.

Nao washiriki wa mafunzo hayo walishukuru kwa fursa hiyo adhimu ya kupewa nafasi ya kuhuduria mafunzo hayo kwani wamepata uelewa wa mambo mengi na kuhaidi kuacha kufanya kazi kwa mazoea  na kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na weledi.


Watumishi waliohudhuria Mafunzo kutoka Mahakama za Mwanzo zilizopo Wilaya ya Singida, Iramba, na Manyoni. Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 21 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Singida.

 Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi (aliyesimama) akifungua  Mafunzo ya kujengeana uwezo kwa Watumishi wa Mahakama (hawapo katika picha) wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo tarehe 21 Agosti, 2026. Kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu Mahakama Singida, Mhe. Aloyce Masua, kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.
 

Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Utemini, Bw. Paul Ndonde akielekeza jambo kwa watumishi waliohudhuria mafunzo hayo (hawapo katika picha).


Ofisa TEHAMA-Mahakama Kuu SingidaBi. Valentina Nkullanga akielezea  jambo kwa watumishi waliohudhuria mafunzo (hawapo katika picha).


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Jumatatu, 24 Agosti 2026

JAJI MAGHIMBI AWASIHI WATUMISHI, WADAU WA MAHAKAMA KUENDELEA KUFANYA MAZOEZI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amewataka Wadau wa Mahakama na watumishi wa Mahakama kuendelea kufanya mazoezi, kushiriki michezo na kuendelea kuhamasishana katika kulinda afya.

Mhe. Maghimbi aliyasema hayo tarehe 22 Agosti 2026 katika Viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua Bonanza la Michezo lililoandaliwa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na Mahakama Kuu Divisheni za Biashara, Kazi, Ardhi, Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Kituo cha Usuluhishi.

Bonanza hilo limehusisha Kanda nzima ya Dar es Salaam yaani Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani likiongozwa na Kaulimbiu isemayo ‘Afya bora kwa watumishi ni chachu ya Uwajibikaji.’

Akizungumza wakati akitoa hotuba ya ufunguzi wa Bonanza hilo, Jaji Maghimbi alisema angependa bonanza hilo lisibaki kuwa tukio la siku moja tu bali anatamani kuona utamaduni wa michezo na mazoezi ukiendelea.

“Ningependa bonanza hili lisibaki kuwa tukio la siku moja, ningependa kuona utamaduni wa michezo na mazoezi ukiendelezwa katika vituo vyetu mbalimbali vya kazi nchini. Kila mmoja wetu ana wajibu wa kutenga muda kwa ajili ya afya yake. Mahakama inahitaji watumishi wenye afya njema, ari na nguvu za utekelezaji wajibu wao kwa wananchi,” alisema Mhe. Maghimbi. 

Akizungumzia Kaulimbiu ya mwaka huu ya Bonanza Mhe. Maghimbi amesema kaulimbiu hiyo ni muhimu kwa sababu inawakumbusha kuwa, mafanikio ya Taasisi yoyote hayawezi kupatikana bila kujali afya na ustawi wa watumishi wake kwa maana mtumishi ndiye anayebeba majukumu ya Taasisi. Hivyo, wanapowekeza kwenye afya za watumishi wanawekeza katika tija, ufanisi na mafanikio ya taasisi.

Aliongeza kuwa, watumishi wenye afya bora wana uwezo wa kufanya kazi kwa umakini, ari na ufanisi, pia wanaweza kukabiliana na changamoto za kazi, kushirikiana vizuri na kutekeleza majukumu yao kwa wakati.

“Afya isipotiliwa maanani inaweza kuathiri mahudhurio kazini, uzalishaji, ubora wa huduma na hatimaye utendaji wa taasisi kwa ujumla,” alisema Jaji Mfawidhi huyo huku akiwasisitiza watumishi wote walichukulie suala la afya kama sehemu ya chachu ya uwajibikaji wao wa kila siku.

Jaji Maghimbi alisema, Bonanza limewapa fursa ya kufanya mazoezi, lakini pia limewakumbusha umuhimu wa kuwa na utamaduni wa michezo na mazoezi katika Maisha yao ya kila siku, michezo husaidia kuimarisha mwili kupunguza msongo wa mawazo na kujenga afya ya akili. Vilevile hujenga nidhamu, uvumilivu, ushirikiano na uwezo wa kufanya kazi kama timu moja. Amesema hizo ni tunu zinazohitajika kwa kiwango kikubwa katika maeneo yao ya kazi.

Vilevile, Mhe Maghimbi aliwasihi watumishi wasiishie kushiriki michezo wakati wa bonanza hilo pekee bali wajenge utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara na kuzingatia mtindo bora wa maisha kama kuzingatia ulaji bora wa chakula na kupima afya kila mara.

Aliongeza kwamba, Bonanza ni darasa la umoja na ushirikiano na kusisitiza kuwa bonanza hilo si mashindano ya michezo pekee bali ni jukwaa muhimu la kujenga umoja na kuimarisha mahusino kati ya Taasisi  na Taasisi kuleta picha nzuri ya umuhimu wa kufanya kazi kwa kushirikiana, bila kuathiri mipaka yao ya utendaji kazi.

Kuhusu uwajibikaji na utumishi wa umma, Jaji Maghimbi alisema inahusisha moja kwa moja suala la uwajibikaji na kwamba uwajibikaji unahitaji mtumishi mwenye afya ya mwili na akili.

Mhe. Maghimbi alitoa ujumbe kwa washiriki wa bonanza kuwa, siku hiyo imekuwa muhimu kwakuwa imewakutanisha pamoja kama ndugu, wameshiriki mazoezi kwa wiki nzima na siku hiyo wamekutana pamoja kama familia katika kilele cha siku ya bonanza kubwa.

Aliwasihi kushiriki michezo kwakuwa inaleta furaha, nidhamu na kuheshimiana huku akisema kuwa, “tushindane kwa nguvu zote lakini tushindane kwa kuzingatia kanuni na moyo wa kiungwana.”

Alihitimisha kwa kuwatakia watumishi/washiriki bonanza jema kwa kusema, “mshindi wa kweli wa bonanza hilo ni yule atakayemaliza siku akiwa na afya bora, furaha mpya na rafiki mpya kutoka taasisi nyingine.”

Akitoa neno la utangulizi katika bonanza hilo, Jaji wa Mahakama Kuu ambaye pia ni mwenyekiti wa michezo wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Arnold Kirekiano alisema kufanyika kwa bonanza hilo ni matokeo ya bonanza la tarehe 04 Oktoba, 2025 ambapo Jaji Mfawidhi aliagiza Kamati ya Bonanza hilo iandae bonanza lingine na mpaka sasa kamati imefanikiwa kuandaa bonanza hilo.

Katika bonanza hilo ilifanyika michezo mbalimbali kama Kukimbia na Yai, Mbio za Mita 100, Kukimbia na Gunia, Kuvuta Kamba, Rede, ‘Pool Table’, Kukuna Nazi, Kuendesha Baiskeli kwa Mwendo wa Polepole, Mashindano ya Kula, Kujaza Maji kwenye Chupa kwa Kutumia Sponji, Kuweka Mrija kwenye Chupa kwa Kutumia sehemu ya Pua, mpira wa pete, Mpira wa Kikapu, Mpira wa Miguu, Kucheza Bao, Kucheza Drafti, Kucheza Karata, Kukimbiza Kuku, Kucheza kwenye viti ‘Chair Dance  na ‘Golf’.

Washindi katika bonanza hilo wamepatiwa zawadi mbalimbali ikiwemo, vikombe, medali, kuku na pesa taslimu.  

Bonanza hilo lilianza kwa mazoezi ya viungo na kupambwa na burudani mbalimbali za muziki (live band) na muziki wa asili. 

Wadau wengine walioshiriki katika Bonanza hilo walitoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Tanzania (DCEA), Taasisi ya Kuzui ana Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), PSSF, NSSF, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Jeshi la Polisi, Magereza, Ofisi ya Uhamiaji, Chama cha Madalali na Wasambaza Nyaraka Tanzania, Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, Benki ya NMB.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma  Maghimbi akitoa hotuba ya ufunguzi wa  Tamasha la Michezo 'Bonanza' tarehe 22 Agosti, 2026. 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Michezo wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam Mhe. Arnold Kirekiano akitoa neno la utangulizi na kumkaribisha Jaji Mfawidhi ili kufungua tamasha hilo.

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Dkt. Cleoface Morris akisalimia na Timu ya Mpira wa Miguu ya Mahakama.

Washiriki wa shindano la kukuna nazi  kwa wanaume na wanawake  wakiendelea na shindano hilo.

Timu ya Kamba Wanaume  na Wanawake Mahakama wakitekeleza jukumu la kuvutana na kuibuka kidedea.

Mashindano ya kukimbia na gunia yakiendelea...

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro akifanya mazoezi ya viungo wakati wa Bonanza hilo lililofanyika tarehe 22 Agosti, 2026 katika Viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam.


Timu ya Mpira wa Miguu kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) walipofanikiwa kutetea kikombe hicho kwa miaka miwili mfululizo.
Mazoezi ya viungo yakiendelea..

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 


 

 

Jumapili, 23 Agosti 2026

MAOFISA MAGEREZA MKOA WA NJOMBE WAPATIWA MAFUNZO YA MFUMO WA e-CMS

  •  Wafundishwa jinsi ya kupakua Nakala za Hukumu....
  • Wasisitizwa juu ya matumizi ya TEHAMA
Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Maofisa Magereza Mkoa wa Njombe wamepatiwa Mafunzo ya Mfumo wa Ki-elektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyolenga kuwaelekeza juu ya upakuaji wa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri mahakamani.

Mafunzo hayo yaliyofanyika tarehe 19 Agosti, 2026 katika Gereza la Wilaya Njombe pamoja na Gereza la Wilaya Ludewa yalifunguliwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano ambapo washiriki walihudhuria mafunzo hayo kupitia Mkutano Mtandao (Video Conference) na tarehe 20 Agosti, 2026 mafunzo hayo yaliendelea kwa Maofisa wa Gereza la Wilaya Makete katika kumbi za Mahakama ya Wilaya Makete.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Luambano alisisitiza juu ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya kusaidia upatikanaji wa nakala za hukumu kwa haraka na kwa unafuu kupitia Mfumo wa e-CMS ili kuepuka malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa Mahabusu au Wafungwa.

“Kupakua hukumu na mienendo ya mashauri kunasaidia kuepusha muda na malalamiko yasiyo ya lazima juu ya upatikanaji wa nakala za hukumu kwa kuwa nakala za hukumu zinapatikana kupitia kwenye akaunti zenu za Magereza baada ya shauri kuwa limeshafanyiwa uamuzi,’’ alisema Naibu Msajili huyo.

Aliongeza kuwa, mfumo huo unaosimamia Mashauri Mahakamani    unalenga kuimarisha utoaji haki mapema ipasavyo na kwamba kupitia mfumo huo  kwa upande wa Mahakama Kuu Njombe kwa sasa  haitumii karatasi kupata nakala za hukumu bali zinapatikana kupitia kwenye mfumo.

Vilevile, Mhe. Luambano alibainisha kwa, mafunzo hayo yametokana na ziara ya Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Jinai katika Gereza la Butimba jijini Mwanza ambapo baada ya kuwasilisha taarifa ya ziara hiyo kwa Jaji Kiongozi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani alitoa maelekezo kwa Naibu Wasajili pamoja na Maofisa TEHAMA kwa kila Mahakama Kuu kutoa mafunzo kwa Maofisa Magereza juu ya kupakua  nakala za hukumu na mienendo kwenye Mfumo wa Kielektroniki wa Mahakama wa Usimamizi wa Mashauri (JoT e-CMS).

Mafunzo hayo yalihudhuriwa na Maofisa Magereza ya Njombe, Ludewa na Makete mkoani Njombe.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano akisisitiza jambo kwa Maofisa Magereza wa Gereza la Wilaya ya Makete wakati wa Mafunzo ya Mfumo wa Ki-elektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyolenga kuwaelekeza juu ya upakuaji wa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri mahakamani yaliyofanyika hivi karibuni.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano akizungumza jambo na Maofisa Magereza (hawapo katika picha) wakati wa mafunzo hayo.

Maofisa kutoka Gereza la Wilaya ya Makete. Kutoka kushoto ni SGT. Noah Mtofole, anayefuata ni SGT. Harid Katundu 
na kulia ni WRD. Jonathan Masele wakimsikiliza kwa umakini Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano.

 SGT.Ezekia Kalenga (aliyesimama) akijifunza kwa vitendo wakati wa mafunzo hayo. Walioketi kushoto ni WDR’S. Jamila Maulid anayefata ni SGT. Frank Nkosi wakielekezwa na Ofisa TEHAMA (hayupo katika picha).

Mafunzo kwa vitendo yakiendelea..






 

 

 

Jumamosi, 22 Agosti 2026

TLS DODOMA YAIMARISHA USHIRIKIANO NA MAHAKAMA

Na ARAPHA RUSHEKE -Mahakama Kuu Dodoma.

Uongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika, Dodoma Chapter, ukiongozwa Bi. Mary Munissi, tarehe 21 Agosti,2026 umemtembelea Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, katika ofisi yake iliyopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Katika kikao hicho, pande hizo zimezungumzia mambo mbalimbali ikiwemo changamoto zinazowakabili, pamoja na namna bora ya kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na Wanasheria ili kuhakikisha huduma za utoaji haki kwa wananchi zinaendelea kutolewa kwa ufanisi na kwa wakati.

Kikao hicho pia kimekuwa sehemu ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kitaaluma kwa lengo la kuboresha zaidi huduma za haki katika eneo la Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akisalimiana na wageni kutoka TLS Dodoma mara baada ya kuwasili katika ofisi yake kwa mazungumzo.


 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Upendo Ngitiri (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho mara baada ya kuwasili kwa wageni hao.


 

Mwenyekiti wa TLS Dodoma, Bi Mary Munissi (wa kwanza kushoto) akimsikiliza kwa umakini kilichokuwa kinajiri.


 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (aliyepo katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa TLS Dodoma, Bi. Mary Munissi (aliyepo kulia kwake) na aliyepo kushoto kwake ni Makamu Mwenyekiti wa TLS Dodoma, Bw, Anselm Mwampoma.


 

Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Joachim Tiganga (wa nne kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya uongozi wa TLS Dodoma mara baada ya kumtembelea ofisini kwake.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

TUGHE TAWI LA MAHAKAMA KUU DODOMA LAKUTANA

Na ARAPHA RUSHEKE -Mahakama Kuu Dodoma.

Tawi la Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) la Mahakama Kuu Dodoma limefanya mkutano wa wanachama uliojaa furaha, mshikamano na hamasa, ukiambatana na kujadili masuala mbalimbali ya ustawi wa wafanyakazi pamoja na kuwaaga wafanyakazi wastaafu na wanaokaribia kustaafu.

Mkutano huo ulifanyika katika ukumbi wa Mahakama uliopo Kituo Jumuishi cha uUoaji Haki (IJC) tarehe 21 Agosti,2026.

Mkutano huo uliongozwa na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye ni Jaji Mfawidhi, Mhe. Joachim Tiganga. Mhe. Tiganga aliwapongeza wanachama kushiriki katika mkutano huo na kusisitiza umuhimu wa umoja na mshikamano miongoni mwa wafanyakazi.

Jaji Tiganga alisema kuwa anaamini kikao hicho kitakuwa na manufaa kwa wanachama, akieleza kuwa TUGHE ni chama cha hiari kinacholenga kuwaleta pamoja wafanyakazi na kuwawezesha kushirikiana katika kujenga na kulinda maslahi yao.

Alitoa wito kwa wafanyakazi ambao bado hawajajiunga na TUGHE kujiunga kwa kadri watakavyoweza, akisisitiza kuwa nguvu ya wafanyakazi inatokana na kuwa na umoja na sauti moja.

Aidha, Jaji Mfawidhi alisisitiza ujumbe wa mshikamano unaosisitizwa kupitia wimbo wa TUGHE, akieleza kuwa wafanyakazi wanapaswa kuungana kwani kujitenga kunaweza kudhoofisha uwezo wao wa kusimamia masuala yao kwa pamoja.

Katika mkutano huo pia kulijadiliwa suala la afya ya akili, ambapo mada hiyo iliwasilishwa na Daktari kutoka Hospitali ya Mirembe, kwa lengo la kuongeza uelewa miongoni mwa wafanyakazi kuhusu umuhimu wa afya ya akili katika maisha na mazingira ya kazi.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa furaha na bashasha, ambapo wafanyakazi wastaafu pamoja na wanaokaribia kustaafu walikabidhiwa zawadi kama ishara ya kuthamini mchango wao katika utumishi wa Mahakama.

Shamrashamra ziliendelea kwa kukatwa kwa keki na kusherehekea pamoja, huku zawadi maalumu zikitolewa kwa Jaji Mfawidhi na Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Bw. Bedson Mariba, hali iliyoongeza furaha na kuufanya mkutano huo kuwa wa kipekee.

Mkutano huo umeendelea kuonesha umuhimu wa umoja, mshikamano na kujali ustawi wa wafanyakazi ndani ya Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, wakati akiwasilisha hotuba yake wakati wa kikao hicho.


 

Sehemu ya wajumbe wa Tawi la TUGHE Mahakama Kuu Dodoma wakiimba wimbo wa mshikamano mara baada ya ufunguzi wa kikao.


 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga akifurahishwa kwa bashasha na zawadi aliyopewa na wajumbe wakati wa kikao hicho.


 

Sehemu ya wajumbe wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma wakifurahia jambo wakati wa kikao hicho.


 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto) pamoja na Mtendaji wa Mahakama Dodoma, Bw. Bedson Mariba wakifurahishwa kwa bashasha na zawadi waliyopewa na wajumbe wakati wa kikao hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Ijumaa, 21 Agosti 2026

WATUMISHI MBEYA WAPITISHWA KWENYE RASIMU YA MPANGO MKAKATI WA MAHAKAMA 2026/27–2030/31

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, ameongoza mafunzo ya rasimu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa mwaka 2026/27–2030/31 kwa watumishi wa Mahakama Kuu kwa lengo la kuwajengea uelewa wa pamoja ili kila mtumishi aweze kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na kuchangia katika kufikia malengo ya Taasisi.

Mafunzo hayo yamefanyika jana Agosti 20, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, yakijumuisha watumishi wa Mahakama kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya na sehemu ya watumishi hao walishiriki mafunzo hayo kwa njia ya mkutano mtandao.

Akifungua mafunzo hayo, Mhe. Mtulya, alisisitiza umuhimu wa kila mtumishi kuuelewa kwa kina Mpango Mkakati wa Mahakama, akieleza kuwa, uelewa huo ni msingi muhimu wa utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Kila mtumishi wa Mahakama kwa ngazi zote anatakiwa afahamu kwa kina juu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ili kufanikisha malengo ya Taasisi, kwani kwa kufanya hivyo itatujengea ufanisi wa kutekeleza majukumu ili kulifikia lengo mama la Mahakama ya Tanzania la kutoa haki kwa wakati mapema ipasavyo,” alisema Mhe. Mtulya.

Jaji Mtulya ameongeza kuwa, uwasilishaji wa rasimu hiyo kwa watumishi wote unalenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mwelekeo wa Mahakama katika kipindi kijacho, hasa kutokana na changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa Mpango Mkakati uliopita wa mwaka 2021/22-2024/25, ambapo watumishi wengi hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu Mpango Mkakati huo.

Watumishi hao walipitishwa kwenye utekelezaji wa Mpango Mkakati uliopita, ikiwa ni pamoja na mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizojitokeza pamoja na mafunzo yaliyopatikana yanayopaswa kuzingatiwa katika kuandaa na kutekeleza Mpango Mkakati mpya.

Akifafanua umuhimu wa kuweka vipaumbele vinavyotekelezeka na vyenye tija, Mhe. Mtulya alisema: “Tunatakiwa kuwa na vipaumbele muhimu na vyenye tija na kuhakikisha bajeti iliyopo inaendana na vipaumbele vyetu,”

Amesisitiza kuwa, utekelezaji wenye mafanikio wa Mpango Mkakati wa Mahakama hautategemea mpango huo pekee, bali pia utayari, uwajibikaji na ushiriki wa kila mtumishi katika kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia mwelekeo na vipaumbele vya Taasisi.

Aidha, Jaji Mtulya alieleza kwa kina nguzo za kimkakati na maeneo ya msingi ya matokeo yaliyoainishwa katika rasimu hiyo, akifafanua namna malengo ya Taasisi yanavyoweza kufikiwa kupitia utekelezaji madhubuti wa majukumu ya kila mtumishi.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, alisisitiza umuhimu wa kuwa na Mpango Mkakati ambao siyo kwa Taasisi pekee bali hata katika maisha ya mtu mmoja mmoja, akihusianisha umuhimu wa kupanga, kuweka malengo kuyafanyia kazi na utekelezaji wake.

Naye, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, alitoa shukrani kwa Jaji Mfawidhi kwa uwezeshaji wa mafunzo hayo, huku akisisitiza umuhimu wa kila mtumishi kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia nguzo za kimkakati za Mahakama.

“Wote tunahusika katika kuhakikisha kuwa, nguzo hizo za kimkakati zinakuwa msingi wa utekelezaji wa majukumu yetu,” alisema Mhe. Laizer.

Katika hatua nyingine, watumishi walipata fursa ya kutoa maoni, ushauri na mapendekezo kuhusu maboresho ya vipengele mbalimbali vya rasimu hiyo, hatua iliyolenga kuhakikisha kuwa maoni ya watumishi yanazingatiwa katika kuboresha rasimu kabla ya kukamilishwa.

Jaji Mfawidhi, aliwashukuru watumishi kwa kushiriki katika mafunzo hayo na kuwataka kutambua thamani ya nafasi waliyonayo kama watumishi wa umma. Aidha, amewasisitiza kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kuzingatia misingi ya utumishi wa umma katika kutekeleza majukumu yao.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (Katikati), akiwasilisha rasimu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania kwa watumishi ya mwaka 2026/27–2030/31, Kulia ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer na (kushoto) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (aliyesimama) akizungumzia rasimu pendekezwa ya Mpango Mkakati wa Mahakama katika kikao hicho.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Paul Dandi Ntumo akitoa maoni yake ya kuboresha katika rasimu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (katikati) akichangia jambo katika Mafunzo hayo ya watumishi wa Masjala Ndogo ya Mbeya. 

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)