Jumatano, 13 Mei 2026

JAJI MKUU ATAKA CHANGAMOTO ZA WATUMISHI KUTATULIWA BILA VIKWAZO

·       Awataka watumishi wa Mahakama kuendelea kutekeleza Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, 2026

·       Ataka mashauri yasikilizwe mapema ipasavyo ili kuchangia ustawi na maendeleo ya Taifa

·       Asisitiza ushirikiano, amani na kuthaminiana kwa Watumishi

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, amewataka Viongozi wa Mahakama kuwa wanyenyekevu sambamba na kufungua milango kwa ajili ya kuwasikiliza Watumishi walio chini yao ili kutatua changamoto wanazokabiliana nazo bila vikwazo.

Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

“Kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unakuwa mtumishi wa wote, sisi Viongozi ni Watumishi wa watu, tuwe na tabia ya kufungua milango tuwasikilize walio chini yetu, tusifunge milango,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema Viongozi pia wanawategemea Watumishi walio chini yao ambapo ameeleza kuwa, kwa kadri Kiongozi anavyozidi kupanda kimadaraka ni kwa kiwango hicho hicho anazidi kuwa tegemezi kwa watu wengine, na kwamba kadri unavyokuwa na Madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho unapaswa kuwa mnyenyekevu ili uwafikie wanaokutegemea na wao wakufikie ili ujue changamoto zao na mafanikio yao.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema kuwa, Viongozi wasiwazuie wajumbe wa Baraza kuzungumza yale yanayowasibu, badala yake wawaache huru kusema yale wanayokabiliana nayo katika utekelezaji wa majukumu yao ili kupata ufumbuzi wa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mahakama.

Ameongeza kuwa, hata Viongozi wanapotembelea Mahakama mikoani Viongozi wa Mahakama husika wanapaswa kuwaacha watumishi wazungumze na Viongozi ili wajue Mahakama imepiga hatua gani katika maendeleo, wajue changamoto  zilizopo ili tutatue changamoto hizo na kupiga hatua ili hatimaye vikao vya Baraza viwe vya furaha.

Aidha, Jaji Mkuu amewapongeza watumishi wa Mahakama wa Kada zote kwa utekelezaji mzuri wa majukumu ya Mhimili huo kwa ufanisi ipasavyo.

“Kwanza natambua mchango wenu, kila mmoja wetu katika utendaji wa Mahakama ya Tanzania, mmefanya kazi kubwa sana, miaka iliyopita na mimi tangu nimekuja kushirikiana na ninyi mmefanya kazi kubwa sana ya kutekeleza majukumu yenu na wakati fulani katika mazingira magumu mimi naelewa katika utumishi wangu mimi nimeanzia chini sana nikiwa Wakili wa Serikali Daraja la tatu, kwahiyo ninafahamu na wakati mwingine

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju amewakumbusha Viongozi na watumishi wote wa Mahakama kwa ujumla kuendelea na utekelezaji wa Kaulimbiu ya Siku ya Sheria Nchini ya mwaka huu 2026 isemayo; ‘Mchango wa Mahakama ya Tanzania katika Maendeleo na Ustawi na Maendeleo ya Taifa.’

“Mahakama ina mchango mkubwa sana, mnaweza kurejea hotuba yangu ya Siku ya Sheria, nimeeleza yote, hii haiwezi kuwa ni Kaulimbiu ya Siku ya Sheria, hii tunaiishi mwaka huu wote wa 2026, kwahiyo tunapofanya kazi yatupasa tujue tuna mchango katika ustawi na maendeleo ya Taifa la Tanzania. Wajibu wetu Mahakama ni kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi ipasavyo na tunapaswa kuendelea kuwa wabunifu,” amesema Jaji Mkuu.

“Kwenye Kanda mtaangalia mnapopanga mashauri mjue kuna kitu tunafanya, kwahiyo mnatakiwa kuangalia ustawi na maendeleo ya Taifa, tunahusika hata sisi katika maendeleo kwa sababu amani ni msingi mkubwa unaoleta ustawi na maendeleo ya Taifa,” amesema Mhe. Masaju.

Ameeleza kuwa, kwa msingi huo ndio maana wa mfano kuna mashauri ya jinai, mashauri ya madai, mashauri ya uchaguzi na kila aina ya mashauri yanashughulikiwa na kumalizika watu wanapiga hatua mapema.

“Mpaka sasa kwa mfano yale mashauri ya uchaguzi yaliyofunguliwa, limebaki shauri moja tu, mengine yote yameshaisha, kuna mashauri ya kila aina ya mirathi, ya ndoa, ya uhujumu uchumi. Sisi kama Mahakama wajibu wetu ni upi? najua tunazo changamoto pengine hatupati ushirikiano mzuri sana lakini sisi hatuwezi kukata tamaa ndio wajibu wetu, tukiharibu tunawajibishwa sisi, sisi ndio tunaosemwa na tunapaswa tuendelee kuwa wabunifu katika maeneo yetu ya kazi kuhakikisha kwamba mchango wa Mahakama ya Tanzania katika ustawi na maendeleo ya Taifa unazidi kuimarika,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Amesema, tunaishi katika nchi inayozingatia Utawala wa Sheria, hivyo, Mahakama ina nafasi kuwa katika ustawi na maendeleo ya Taifa na kwa sababu ni muhimu mashauri yanapopangwa yapangwe kimkakati na hayatakiwi kucheleweshwa bila sababu za msingi, lakini pia inabidi kuwa ni mikakati ya kubaini mashauri yenye kero yanayoleta sintofahamu katika jamii yashughulikiwe.

“Uchumi ni Ardhi wala hata sio kitu kingine, kwahiyo tuna mikakati ya kumaliza haya mashauri ya Ardhi tangu mwaka jana tumekuwa na hiyo mikakati, na Mahakama Kuu wamefanya vizuri sana kwa sababu mashauri ya ardhi kwa Mahakamani yanaanzia Mahakama Kuu, yanakwenda Mahakama Rufaa mengine kwenye ‘originial jurisdiction’ tunafanya vizuri japo bado ni mengi kwa sababu migogoro inazalishwa mingi na sehemu fulani tumeshauri kwa mfano ukisoma Sheria ya Usajili wa Ardhi (Land Registration Act) kuna mtu pale anaitwa ‘The Registrar of Titles) ana mamlaka makubwa sana  mashauri mengine hata yasingekuwa yanakuja mahakamani yangekuwa yanaenda pale kama kuna migogoro wakishindwa kutatua upande ambao hauridhiki unakuja Mahakama ya Rufani,” ameeleza.

Kwa upande wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Masaju amesema kuna mashauri mengi ya jinai, hivyo wameweka mkakati wa kushughulikia mashauri hayo ambayo walianza kusikiliza katika Vikao vya Mahakama ya Rufani (COA Session) ya mwezi Februari ambapo walichanganya na mashauri ya mirathi ili watu wawe na amani kwenye familia zao na wengine wajue hatma yao.

“Majaji hawa wa Mahakama ya Rufani wamefanya kazi nyuma, mashauri mengi yameenda, kama wengine hawasema sisi wenyewe tujisemee, mimi nawapongeza sana Mahakama ya Rufani,” amesema Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Mwezi Aprili walipanga mashauri ya kazi na ndoa ambayo kikao chake kimekamilika tarehe 08 Mei, 2026 na wengine wanaendelea, jitihada hizo ni katika wajibu wa kutekeleza mchango wa Mahakama katika maendeleo na ustawi wa Taifa.

Kadhalika, amesema katika Vikao vinavyofanyika Juni na Agosti, 2026 mashauri ya ardhi yatashughulikiwa tena ili kuyapunguza. Ameeleza kuwa, katika vikao hivyo wataweka pia mashauri machache ya jinai na kabla ya Desemba pia watakuwa na mashauri ya jinai.

Amebainisha kuwa, ili Mahakama ifanikiwe inahitaji ushirikiano kutoka Mihimili mingine ili kutekeleza jukumu la utoaji haki kwa ufanisi ipasavyo.

Kwa upande wa Mahakama Kuu, Mhe. Masaju amesema, wamekamilisha vikao vya kusikiliza mashauri ya ardhi ikiwa ni mwendelezo wa zoezi ambalo lilianza mwaka jana, ambapo amesema kwa sasa hatatoa takwimu kwakuwa zinaandaliwa na Msajili wa Mahakama Kuu na zitatangazwa kwa wananchi kile ambacho Mahakama imefanya.

Amesema pia kulikuwa ni shida kubwa za mashauri ya baadhi ya waajiri kutowasilisha michango ya mafao ya watumishi wao katika mifuko ya hifadhi za jamii ambapo amesema wamefanya mabadiliko ya kanuni na kwamba katika usikilizaji wa mashauri hayo Majaji na Mahakimu wamefanya vizuri kwakuwa mashauri hayo mengi yameisha na yameisha kwa njia ya usuluhishi.

“Sisi Mahakama nia yetu ni kwamba wafanyakazi wapate stahili zao sio wanakatwa halafu mwisho wa siku hawapewi stahili zao,” ameeleza.

Kadhalika Jaji Mkuu amewataka watumishi wote wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, umoja na kuthaminiana katika utekelezaji wa majukumu.

 Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

MAHAKAMA YAENDELEA KUIMARISHA UTOAJI HAKI

  • Yataja mafanikio ya utumishi, TEHAMA na Miradi ya Ujenzi
  • Mtendaji Mkuu aeleza mafanikio ya ajira, ustawi wa Watumishi

Na HALIMA MNETE- Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amesema kuwa Mahakama inaendelea kuimarisha utoaji wa huduma za haki nchini kupitia maboresho mbalimbali ya kiutumishi, matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) pamoja na utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa majengo katika maeneo tofauti ya nchini.

Prof. Ole Gabriel amesema hayo leo tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma wakati akiwasilisha taarifa ya mwaka wa fedha 2025/2026 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania 2026 unaofanyika katika ukumbi wa PSSSF Makole, chini ya uenyekiti wa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.

Akizungumza katika mkutano huo utakaohitimishwa kesho tarehe 14 Mei, 2026, Prof. Ole Gabriel amesema Mahakama imeendelea kutekeleza Mpango Mkakati wake wenye lengo la kuendeleza maboresho ya utoaji huduma, huku mafanikio yaliyopatikana yakitokana na juhudi za Watumishi wa Mahakama nchini kote.

Amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, Mahakama imefanikiwa kuajiri Watumishi wapya 1,121, wakiwemo Mahakimu 173, hatua ambayo imeongeza nguvu kazi katika utoaji wa huduma za haki nchini. Hata hivyo, amesema bado Mahakama inakabiliwa na upungufu wa Watumishi ambapo hadi Aprili 30, 2026 idadi ya watumishi waliopo ni 6,976 dhidi ya mahitaji ya watumishi 12,121.

“Tumekuwa na kikao kizuri na Viongozi wa TUGHE Mahakama, ambapo hoja nyingi zimejadiliwa na baadhi yake zimepatiwa ufumbuzi,” amesema Prof. Ole Gabriel.

Katika masuala ya ustawi wa watumishi, amesema Mahakama imetenga zaidi ya shilingi milioni 900 kwa ajili ya kuanzisha kifurushi maalum cha bima ya afya kwa Watumishi wake ili kusaidia huduma za ziada za matibabu.

Kuhusu miundombinu. Prof. Gabriel amesema Mahakama inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi, ikiwemo ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama Dodoma ambao umefikia asilimia 99.

Amesema pia Mahakama imeendelea kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama katika Mikoa mbalimbali, huku baadhi ya majengo mapya ya Mahakama Kuu yanayoitwa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tayari yakianza kutumika katika Mikoa mbalimbali.

Kwa upande wa TEHAMA, Prof. Ole Gabriel amesema Mahakama itaendelea kuimarisha mifumo mbalimbali pamoja na mfumo wa Mahakama Mtandao (Virtual Court) ili kuongeza ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa Wananchi.

Amesisitiza kuwa matumizi ya TEHAMA yanapaswa kuendelea kuwa sehemu ya utamaduni wa Mahakama ili kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia duniani.

Katika hitimisho lake, Prof. Ole Gabriel ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuipa Mahakama kipaumbele katika utoaji wa bajeti na kuwataka Watumishi kuendelea kushirikiana katika kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza Kuu la Wafanyakazi Mahakama ya Tanzania 2026. Picha chini ni sehemu ya wajumbe kutoka Masjala mbalimbali wanaohudhuria Mkutano huo.












Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.



 

Jumanne, 12 Mei 2026

JAJI SEHEL, MWENYEKITI KAMATI YA JAJI MKUU UFUATILIAJI NA TATHMINI AFANYA ZIARA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel hivi karibuni alifanya ziara ya kikazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe lengo likiwa ni kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa shughuli za Mahakama.

 

Mhe. Sehel ambaye pia ni na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) alianza ziara yake tarehe 07 Mei, 2026 ambapo alipokelewa na mwenyeji wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA pamoja na Viongozi na watumishi watumishi wa Mahakama Njombe.

 

Jaji Sehel alipata wasaa wa kuzungumza na watumishi wa Mahakama Njombe ambapo alisikiliza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo ikiwemo ukosefu wa huduma ya usafiri wa basi la Mahakama linaloweza kuwapeleka ofisini kutokana na umbali mkubwa wa kutoka maeneo wanayoishi mpaka mahali pa kazi.

 

Aidha, Mwenyekiti huyo alipata fursa ya kutembelea jengo la Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Njombe (IJC) ambalo lipo kwenye hatua za mwisho kwa asilimia 97 na baadhi ya viongozi na watumishi tayari wameanza kuhamia kwenye jengo hilo.

 

Katika ziara hiyo Mwenyekiti alifanya ukaguzi wa shughuli za kimahakama katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mahakama ya Wilaya ya Njombe na Makete pamoja na Mahakama ya Mwanzo Njombe.

 

 Vilevile, katika ziara hiyo Mhe. Sehel alipata fursa ya kuzungumza mambo mbalimbali ya TAWJA Njombe katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wake pamoja na kuhuisha uanachama  wa TAWJA na IAWJ.

 

 

Akiendelea na kikao hicho huku wanachama wengine wakishiriki kwa njia ya mkutano mtandao (Video Conference) walio nje ya Wilaya ya Njombe, Mhe. Sehel  alisisitiza mshikamano pamoja na kushirikiana kikamilifu katika shughuli za Chama hicho, Tawi la Njombe ikiwa ni pamoja na kujitolea katika majukumu mbalimbali bila kujali malipo pamoja na kutoa elimu na kuhudhuria mikutano ya ndani.

 

 

Mwenyekiti huyo wa TAWJA alisisitiza kuwa Chama hicho ni jukwaa linalowawezesha kung’ara kitaifa na kimataifa kwa kazi zinazofanyika, ambapo aliwatakia wanachama wa TAWJA Njombe majukumu mema ya ujenzi wa Taifa huku akisisitiza uadilifu, weledi na uwajibikaji kama ambavyo Kaulimbiu ya Mahakama inasema.

 

Mhe, Sehel pamoja na wanachama wa TAWJA Njombe walipata fursa ya kukata keki na kufungua champeni pamoja na Makamu Mwenyekiti Mhe. Victoria Nongwa kama ishara ya mwanzo mpya wa TAWJA mkoani Njombe.

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani  ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi mbele katikati) akizungumza na Watumishi wa Mahakama Njombe alipotembelea Masjala hiyo hivi karibuni. Kushoto ni  Jaji Mfawidhi wa  Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndono ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Victoria Nongwa na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge. Aliyesimama upande wa kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama.  

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa  Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Njombe mbele ya jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe wakati walipofanya ziara hivi karibuni. 


 Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na  Tathmini, Mhe. Barke Sehel akipatiwa maelezo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe (wa kwanza kushoto). Wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA akizungumza hivi karibuni na baadhi ya Wanachama wa Chama hicho wa mkoani Njombe.

Jaji Sehel akiwa katika maandalizi ya kukata keki maalum ikiwa ni ishara ya kuanza kwa Tawi mpya la TAWJA Mahakama Njombe.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa  TAWJA, Mhe.  Victoria Nongwa (kulia) akimpatia zawadi Jaji Sehel.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




 

 

 

 

 

 

 

 


MTENDAJI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA VIONGOZI WA TUGHE WA MAHAKAMA YA TANZANIA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel leo tarehe 12 Mei, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.

Kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kuhudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick pamoja na Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.

Lengo la kikao hicho ambacho hufanyika kila mwaka kabla ya Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ni kujadili pamoja kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu watumishi wa Mahakama sambamba na kujadili hoja za Mabaraza ya Kanda na Divisheni za Mahakama Kuu kwa upana zaidi kabla ya kufanyika kwa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

Aidha, Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania kinatarajiwa kufanyika kesho tarehe 13 Mei, 2026 jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake ambaye ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Yafuatayo ni matukio katika picha ya Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania (hawapo katika picha) leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kulia ni Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick na kushoto ni Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule.


Picha mbalimbali za Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wa Mahakama ya Tanzania wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza nao leo tarehe 12 Mei, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick akiwa katika kikao hicho.

Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Mahakama ya Tanzania, Bi. Alice Haule akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.


Viongozi mbalimbali wa TUGHE Mahakama wakichangia juu ya masuala mbalimbali ya Watumishi wa Mhimili huo wakati wa Kikao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kilichofanyika leo tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ikisikiliza na kurekodi hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania leo tarehe 12 Mei, 2026 jijini Dodoma.


Meza kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiandika hoja na michango mbalimbali iliyokuwa ikitolewa na Viongozi wa TUGHE-Mahakama ya Tanzania wakati wa kikao.

(Picha na MARY GWERA & ARAFA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma)








MAJAJI KANDA YA DAR ES SALAAM, DIVISHENI YA BIASHARA WANOLEWA KUHUSU MILIKI BUNIFU

 Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood amefungua mafunzo ya Miliki Bunifu yanayowahusisha Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Mahakama ya Kuu Divisheni ya Biashara lengo likiwa ni kuwapa uelewa zaidi juu ya jambo hilo.

Akifungua mafunzo hayo jana tarehe 11 Mei, 2026 kwenye Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Jaji Kiongozi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Mhe. Aboud alisema katika uchumi wa dunia ya leo hati miliki imekua moja ya mali ya thamani zaidi kuendesha uvumbuzi, ukuaji wa viwanda, ubunifu na biashara za kimataifa.

Jaji Abood alisema pia Nchi zinazoongoza kwa uchumi duniani hazijengwi juu ya rasilimali asili tu bali pia mawazo, uvumbuzi chapa, kazi za kisanii miundo na teknolojia za kidijitali ambazo huchangia ushindani na ustawi wa Taifa.

Aliongeza kuwa, kwa Tanzania ulinzi madhubuti na utekelezaji wa haki miliki unaendana moja kwa moja na lengo pana chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 na msukumo unaoendelea kuelekea ukuaji wa viwanda, uvumbuzi na uchumi unaotegemea maarifa.

Amesema, Mahakama inasimama katikati ya utekelezaji wa hati miliki wakati Mashirika kama vile Tume ya Ushindani (FCC), BRELA, TIRDO na COSOTA hushugulikia masuala ya utawala, Mahakama zinahakikisha kwamba haki inapatikana na kuheshimiwa kikamilifu.

Akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Abood alisema kuwa, yeye amemwakilisha Jaji Kiongozi ambaye ndiye alitakiwa kuwepo ila kutokana na majukumu mengine aliyonayo hakuweza kushiriki.

Amesema mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam wakishirikiana na Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara pamoja na Wadau wengine wa Mahakama kama Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Ofisi ya Haki Miliki Tanzania (COSOTA), Tume ya Ushindani (FCC) na wengine ambao wapo mahsusi kwa ajili kuwawezesha Majaji kupata elimu zaidi na pia kubadilishana uzoefu kuhusu Miliki Bunifu. Ameongeza, “kama unavyojua maendeleo kuchelewa sana inategemea na ubunifu.”

“Mahakama kama Watafsiri wa Sheria zinazohusu hayo na kuhakikisha kunakuwa na utekelezaji inabidi kuelewa kwa undani mchakato mzima na nini maana ya Miliki Bunifu wameona ni muhimu sana kupata mafunzo hayo ya siku mbili kwa sababu maamuzi yao sio tu kwamba yatatumika ndani ya nchi bali pia yamechaguliwa kuwekwa kwenye kanzidata (database) ambapo nchi nyingine wanasoma na wanaweza kuyatumia pia,” ameeleza Jaji Abood.

Ameongeza kuwa, mtu anaweza kubuni mradi wake wa kusuka nywele tu na ukachukuliwa na watu wengine wakanufaika wakati yeye ndiye mnufaika wa kwanza. Pia ilielezwa kuwa, kuna watu wanatumia taswira za watu kubuni katika Makampuni mbalimbali na watu wakapelekea shauri na kulalamika kwa hiyo ikaonekana ni ngumu kwa Majaji na Mahakimu kama watoa haki ambao wanatafsiri sheria kutoa hukumu na kuhakikisha zinatekelezeka waelewe kiundani.

Jaji Abood amemnukuu Jaji Kiongozi kuwa, “huu ni mwanzo tu mafunzo haya yataendelea kuwezesha na baadae kuwapata Majaji na Mahakimu wataalam kwenye eneo hili la miliki bunifu. Na kama ikiendelea hivyo watu watahakikisha kwamba hizo miliki bunifu zinalindwa na wawekezaji pia watakaribishwa.”

Amesema, kwa hatua hiyo watu wataamua kuanzisha bidhaa mbalimbali ambazo watabuni pamoja na kumiliki miradi mbalimbali. Hatua hiyo itachochea ukuaji wa uchumi wa nchi na kuhakikisha kwamba wanatimiza lengo la Dira ya Taifa ya Maendeleo.

Akijibu swali aliloulizwa na Mwandishi wa Azam Media kuhusu idadi ya Majaji wenye utaalam wa Miliki Bunifu, Mhe. Abood amesema hana uhakika ni wangapi wana utaalam huo japo amesema wameona shida ni kubwa ndio maana wameona kuna umuhimu na haja ya kufanya  mafunzo hayo na wameanza na Dar es Salaam lakini mpango mkakati ni kwamba Majaji wote nchi nzima waweze kupata mafunzo hayo.

Akimkaribisha Jaji Abood, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Salma Maghimbi amesema wizi halisi wa haki miliki sio tu kutoa nakala bali pia ni unyang’anyi wa haki za ubunifu.

Mhe. Maghimbi amesema, kwa sasa Mahakama zinashughulikia mashauri yanayohusisha alama za biashara, haki miliki, usanifu wa viwanda, viashiria vya kijiografia na siri za biashara. Changamoto mpya kama ukiukaji mitandaoni, uharamia wa kidijitali, maudhui ya akili unde na utekelezaji wa sheria mipakani hizi zinachanganya michakato ya Mahakama licha ya kuwepo mfumo wa kisheria. 

“Maofisa wa Mahakama bado wanakabiliwa na mapungufu ya uwezo wa kusimamia, ufundi, kiutaratibu na ushahidi na vipengele vya utekelezaji wa miliki bunifu, hii imewapa nguvu ya kuendesha mafunzo hayo,” amesema Jaji Maghimbi. 

Ameeleza kwamba, mpango huo utatoa mwelekeo wa vitendo na wa Mahakama juu ya mada ya haki miliki, taratibu za usajili na athari zake katika mashauri, kuthibitisha ukiukwaji, tathmini ya ushahidi wa kiufundi, muingiliano wa nafuu, changamoto ya kisiasa katika utekelezaji wa haki miliki.

Naye Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Cleophas Moriss amesema, mafunzo hayo yatawasaidia kuelewa kwa sababu mada zimepangwa katika mtiririko ambao utawapatia nafasi ya pekee kuongeza ujuzi kwakuwa mada zimepangwa kumuwezesha mtu kufahamu kuanzia chanzo na chimbuko la haki hiyo na maendeleo yake kitaifa na kimataifa.

Mhe. Morris amesema wataangalia jinsi kanuni zinavyozidi kukua katika tasnia husika na kwa nchi na kimataifa na pia wanaangalia sheria za nchi zimepangwa vipi au zimetengenezwa kwa mtindo gani katika kuleta uwiano wa kikanuni wa kitaifa na kimataifa.

Naye, Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa amesema sio mara ya kwanza wao kutoa mafunzo hayo, wameshawahi kutoa kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani.

“Lengo la kutoa mafunzo haya ni kuwapa elimu Majaji uelewa kuhusu masuala mazima ya miliki ubunifu kwa sababu eneo hili ni geni  kidogo hapa nchini na baada ya kuangalia hukumu kadhaa ambazo zimekuwa zikitolewa na Majaji wakaona kuna umuhimu sasa wa kupeana elimu hiyo ili wawe pamoja,” ameeleza Bw. Nyaisa.

Amesema katika maamuzi ya Majaji huwa wanagusa maslahi ya Nchi katika eneo la miliki ubunifu na kwamba zipo hukumu kadhaa ambazo zimetolewa na Majaji zimewasaidia sana katika utendaji wa majukumu yao.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani, Bi. Khadija Ngasongwa amesema wameungana na Mahakama kutoa mafunzo ya miliki bunifu ambazo katika sehemu ya sheria alama ya bidhaa wao ni kama Polisi au Wasimamizi wa kulinda miliki bunifu nchini hasa katika upande wa alama za bidhaa (IPR) imeelezewa katika sheria ambayo kwa sasa wanaifanyia marekebisho.

Amesema katika uzalishaji wa kusajili alama ya bidhaa au nembo inayofanywa na wakala wa BRELA wao kazi yao wanazirekodi ili waweze kuzitambua sokoni bidhaa halisi ni ipi na ambayo sio halisi.

Mafunzo hayo ya siku mbili baada ya kufunguliwa wameanza kwa masomo ya muhtasari wa Haki Miliki, Mfumo wa Kisheria wa Taasisi wa Haki Miliki nchini Tanzania, uamuzi na utekelezaji wa haki miliki na umuhimu wa kisheria wa hatua za usajili katika madai. Masomo hayo yamefundishwa na Mkufunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. Saudine Mwakaje na Wakili Mshirika  wa ‘Next Law Advocates’, Bw.  Seka Kasera na Msajili Msaidizi/Meneja wa Alama za Biashara na Huduma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood akitoa hotuba  ya ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu jana tarehe 11 Mei, 2026 kwa niaba ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani. 


Sehemu ya washiriki wa mafunzo Miliki Bunifu wakifuatailia hotuba ya mgeni rasmi (hayupo katika picha).

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akitoa neno fupi wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana akifanya utambulisho wa washiriki wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu.

Mtendaji  Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa akitoa salam wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu jana tarehe 11 Mei, 2026 jijini Dar es Salaam.


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa akitoa salamu wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Miliki Bunifu.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wanaoshiriki katika Mafunzo ya Miliki Bunifu (waliosimama baadhi). Walioketi wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi,  wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa na wa kwanza kulia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa.

Meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na Wawezeshaji wa Mafunzo ya Miliki Bunifu. Walioketi katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Iman Abood, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi,  wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa na wa kwanza kulia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)