Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra
Maruma ametoa rai kwa Wasuluhishi nchini kuwa wavumilivu na kusikiliza kwa
makini wakati wanapofanya usuluhishi.
Mhe. Maruma aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akifunga mafunzo ya
siku tatu ya Upatanishi kwa Mahakimu na Wasajili wa Kanda ya Dar es Salaam yaliyofanyika
kuanzia tarehe 11 hadi 13, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha
Utoaji Haki (IJC) Temeke.
Jaji Maruma alisema, endapo Msuluhishi ana haraka, hana uvumilivu na hana
usikivu hawezi kufanya usuluhishi na kwamba kama Msuluhishi akiwa hana usikivu na
uvumilivu hata wale anaowasuluhisha hawawezi kumuamini, wadaawa wakimuangalia
msuluhishi wanajua tu kwamba anawajali na kuwasikiliza ama la.
Ameongeza kuwa, uvumilivu na utulivu unasababisha usuluhishi, hivyo kuwataka
kuwa wavumilivu hata kama wadaawa watawashambulia kwa maneno makali wao wawe chanya
na wavumilie hatua hiyo itasababisha wadaawa kurudi kwenye mstari, hivyo
usuluhishi kuendelea na kufanikiwa.
Awali akifungua mafunzo hayo, Mhe.
Maruma alieleza kuwa, mafunzo hayo ni mwendelezo wa juhudi za Mahakama katika
kuwajengea uwezo watumishi wake ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
Jaji Maruma alisema mafunzo hayo, yanafanyika wakati muafaka na muhimu
sana wakati Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inahimiza usuluhishi kama
nyenzo muhimu ya msingi mkuu katika kuleta amani, umoja na
utulivu katika Taifa letu.
“Hii inaendana na mikakati ya Mahakama
katika kukuza matumizi ya usuluhishi ili kuharakisha upatikanaji wa haki
mapema ipasavyo kama inavyosisitizwa katika ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisisitiza.
Aidha Mhe. Maruma afafanua kwamba Mahakama zinaendelea kukabiliwa na
ongezeko la mashauri ambayo mengi kati yake yanaweza kutatuliwa kwa haraka, kwa
gharama nafuu na kwa maridhiano bila kupita mchakato mrefu wa mashauri ya shauri
la kawaida hivyo kuokoa gharama na muda ambao utatumika katika shughuli za
kiuchumi na kijamii.
Alisema kuwa, upatanishi wa Mahakama umeendelea kuwa nyenzo muhimu
katika kuwezesha migogoro kumalizika kwa haraka na kwa sasa ongezeko la
upatanishi limezidi asilimia 50 tofauti na hali ilivyokuwa miaka minne nyuma.
“Hali hii inatupa matumaini na
chachu ya kuendelea kuwajengea uwezo Mahakimu na wadau wa usuluhishi ili
kuongeza ufanisi katika kutatua migogoro kupitia upatanishi na kufika malengo
yaliyopo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ya kutumia njia hii katika kuleta amani na utulivu katika jamii zetu,” alisema Jaji
Maruma.
Aliongeza kwamba, mafunzo hayo ni maandalizi ya Wiki ya Usuluhishi
ambayo imepangwa kufanyika mwezi Machi nchini kote na kusema kuwa mafunzo hayo
ni mwanzo wa mafunzo ambayo yataendelea kutolewa kwa Majaji, Mahakimu na Wadau
ili kujenga uwezo wa ufanisi wa kutekeleza njia ya upatanishi katika
kuharakisha upatikanaji wa haki.
Kadhalika alisema kwamba, ushiriki wa Majaji, Mahakimu, Wasajili na
wadau wa Taasisi nyingine unaonesha kuwa, usuluhishi si jukumu la mtu mmoja
bali ni juhudi ya pamoja ya taasisi zote zinazohusika na utoaji haki. Majaji na
Mahakimu ingawa si Wasuluhishi katika mashauri yao, ni wasimamizi na walezi wa
mchakato wa usuluhishi, hivyo ni muhimu kuwa na uelewa wa kina wa msingi,
taratibu na falsafa ya usuluhishi.
Naye Naibu Msajili ya Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi Mhe.Augustina
Mmbando alisema, Usuluhishi huimarisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo, kwa
gharama nafuu na kwa kuzingatia mahusiano ya kijamii na kibiashara.
Mhe. Mmbando alisema usuluhishi sio mbadala wa Mahakama bali ni nyenzo
inayosaidia Mahakama kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na kwa mtazamo unaomjali
binadamu.
Akizungumzia kuhusu miongoni mwa Wadau waliohudhuria mafunzo hayo ambao ni
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Mhe. Mmbando alisema uwepo wa
TIRA katika mafunzo hayo una umuhimu wa pekee kwa kuwa Sekta ya Bima ni
miongoni mwa sekta zinazozalisha migogoro mingi ya kibiashara na kimikataba
ambayo kwa asili yake inafaa kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi.
Aliongeza kuwa, ushirikiano kati ya Mahakama na Taasisi za Udhibiti kama
TIRA ni nguzo muhimu katika kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haraka, haki
na kwa namna inayohifadhi mahusiano na kuimarisha imani ya wadau katika mfumo
wa haki.
Naye Mwezeshaji katika mafunzo hayo Mhe. Mhangwa Yunge alisema
usuluhishi ni mzuri kwakuwa unaokoa muda na pia Wadaawa wanabaki na amani na
kuongeza kuwa sio kila mgogoro unaweza kusuluhishwa bali kuna migogoro mingine
wahusika wanakuwa hawako tayari kusuluhishwa.
Mafunzo hayo yaliwezeshwa na Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe.
Angela Bahati na Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke, Mhe. Mhangwa
Yunge.
Mafunzo hayo yalihudhuriwa na Naibu wasajili, Mahakimu, Wadau na Mtendaji
wa Mahakamu Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akifundisha mada wakati wa Mafunzo yaliyotolewa hivi karibuni kwa Wasuluhishi wa Mahakama.
Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo kwa Wasuluhishi wa Mahakama, Mhe. Mhangwa Yunge akiwaongoza washiriki wa mafunzo hayo kuimba wimbo uliotungwa wakati wa mafunzo hayo.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi na Mwezeshaji wa Mafunzo (kulia), Mhe. Angela Bahati Salema na Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Mhangwa Yunge wakisikiliza michango iliyokuwa ikitolewa na washiriki wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu Kituo cha usuluhishi na mwezeshaji wa mafunzo, Mhe. Angela Bahati Salema (kulia) akipokea cheti katika hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo.
Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi (IJC) Temeke na Mwezeshaji wa Mafunzo ya Upatanishi, Mhe. Mhangwa Yunge akipokea cheti katika hafla ya kufunga mafunzo hayo.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbado akipokea cha ushiriki wa mafunzo katika hafla fupi ya kufunga
mafunzo hayo.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)