Jumanne, 21 Aprili 2026

JAJI MANYANDA ASISITIZA UTOAJI HAKI USIYOTONESHA MAJERAHA YA UKATILI WA KIJINSIA

Na. SHARIFU MOKIWA-Mahakama, Sumbawanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda amewataka washiriki wa Mafunzo ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia ambao ni Mahakimu wa Mahakama za Wilaya, Waendesha Mashtaka wa Serikali pamoja na Maafisa wa Ustawi wa Jamii kutoka mikoa ya Rukwa na Katavi kuongeza umakini wanaposhughulikia mashauri ya aina hiyo ili kuwajengea imani waathirika wanapofika mahakamani.

Mhe. Manyanda alisema hayo wakati akifungua Mafunzo ya siku tatu kuhusu namna ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia (Sexual and Gender Based Violance-SGBV) Mafunzo hayo yameanza jana tarehe 20 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga.

Mhe. Manyanda ameongeza kuwa, mafunzo hayo yanalenga kuwasaidia washiriki kuhakikisha wanaepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

“Mafunzo haya yakatumike kuhakikisha kuwa tunaepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, tutumie lugha ya staha, tuzingatie weledi na tujenge mazingira ambayo waathirika wanaweza kuwa huru kutoa ushahidi bila kuathiri kumbukumbu zao,” alisema Mhe. Manyanda

Aidha, Jaji Manyanda aliongeza kuwa, utoaji wa haki unapaswa kuzingatia utu, usalama na mazingira rafiki kwa waathirika ili kusaidia upatikanaji wa haki bila kuongeza maumivu ya kihisia na kisaikolojia.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa  Irishi Rule of Law International pamoja na kushirikiana na Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga.

Vilevile, Mafunzo hayo yanawezeshwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo kwa kushirikiana na Hakimu Mkazi Mkuu Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 22 Aprili, 2026 huku yakilenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa haki na kuimalisha ulinzi kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia katika jamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda akifungua mafunzo ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia

Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo wakifuatilia kwa umakini mada mbalimbali zinazoendelea kutolewa na wawezeshaji

Washiriki wa Mafunzo hayo wakiwa kwenye majadiliano ya pamoja wakati wa Mafunzo 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo (aliyesimama) akiwasilisha mada wakati wa mafunzo hayo. 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa Mafunzo hayo. 

Hakimu Mkazi Mkuu Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga (aliyesimama) akiwasilisha mada wakati wa mafunzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga



WATUMISHI SONGWE WAMUAGA MTUMISHI MSTAAFU

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe wamemuaga Mtumishi mwenzao Bw. Sigula Simfukwe ambaye alikuwa ni Mlinzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kishenyi alimpongeza Bw. Sigula Simfukwe kwa kutimiza umri wa kustaafu akiwa na afya njema na alimtakia kila la kheri kwenye maisha yake mapya na pia alimsihi aendelee kuishi kwa upendo na ushirikiano kama alivyokuwa akiishi na Watumishi wenzake mahakamani hapo.

Naye, Mtumishi mwenzake aliyefanya kazi kwa muda mrefu na Bw. Simfukwe mahakamani Bi. Jenitha Sheyo alimpongeza Bw. Simfukwe kwa hatua hiyo na kushukuru kwa ushirikiano wake na kumtakia kila la kheri kwenye maisha yake mapya ya nje ya utumishi wa umma.

Kwa upande wake, Mtoto wa Mstaafu huyo Bw. Joshua Simfukwe alimpongeza baba yake kwa kufikisha umri wa kustaafu akiwa na afya nzuri pia aliwashukuru Watumishi wa Mahakama kwa kumfanyia baba yake hafla hiyo, aliongeza kuwa, hiyo inaonesha baba yake alikuwa akiishi kwa upendo na ushirikiano na Watumishi wenzake mahakamani hapo.

Bw. Sigula Simfukwe aliwashukuru Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe kwa kumfanyia hafla hiyo ya kumuaga, aliwatakia utumishi mwema watumishi wote wanaobaki mahakamani hapo na kwamba hatasahau nyakati zote nzuri alizopitia mahakamani hapo pia aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano wakati wowote utakapohitajika.

Hafla hiyo iliyohudhuriwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Mhe. Nemes Chami na baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbozi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe, Mhe. Francis Kishenyi (kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Nemes Chami (kulia) akifungua hafla ya kumuaga Mtumishi Mstaafu Bw. Sigula Simfukwe.

Mtumishi Mstaafu wa Mahakama Songwe Bw. Sigula Simfukwe akitoa neno katika hafla ya kuagwa kwake.

Hakimu Mkazi Mwandamizi Mhe. Vitalis Changwe (kushoto) akimkabidhi Bw. Sigula Simfukwe zawadi ya jezi ya Kilabu ya Simba.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbozi Mhe. Nemes Chami (kushoto), akimkabidhi zawadi Bw. Sigula Simfukwe.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbozi wakiwa katika hafla ya kumuaga Mtumishi Mstaafu Bw. Sigula Simfukwe.






 

Jumatatu, 20 Aprili 2026

WANANCHI KIGOMA WAPATIWA ELIMU YA USULUHISHI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Veronica John ametoa elimu kwa wananchi kuhusu kutumia njia ya usuluhishi katika utatuzi wa migogoro mingi inayojitokeza katika jamii akieleza kuwa inaleta amani, utengamano wa kijamii na kudumisha udugu miongoni mwa jamii.

Bi. Veronica amesisitiza hayo hivi karibuni wakati akitoa elimu kwa wananchi waliokuwa wakisubiri kupata huduma mbalimbali Mahakama Kuu Kigoma.

Aidha, aliwajulisha wananchi hao kuwa, zipo njia nyingi za kutatua migogoro katika jamii ikiwemo njia ya Usuluhishi, amesema, “njia hii inapendelewa kwa kuwa inaleta maridhiano ya pamoja kwa amani bila kuathiri haki ya mtu katika mgogoro husika.”

Bi. Veronica amewaeleza wananchi hao kuwa, njia ya usuluhishi ina faida nyingi kuliko njia nyingine za utatuzi wa migogoro katika jamii, ambapo amesema kuwa, usuluhishi unadumisha udugu na ushirikiano wa jamii kuliko njia nyingine, upatikanaji haki kwa njia ya kirafiki na kucheka na kuendelea kushirikiana kwenye mambo kadhaa, kupunguza gharama za wananchi katika kuendesha mashauri Mahakamani kwakuwa  usuluhishi hauhitaji Wakili wala gharama za vikao kwa msuluhishi kwani Mahakama inao utajiri wa wasuluhishi kutoka ndani na nje ya Mahakama.

Kwa upande wake Bw. Bakari Abdallah Mfaume, Mkazi wa Gungu, ameishauri Mahakama kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili wananchi kufahamu zaidi faida za usuluhishi ili kuleta amani zaidi katika migogoro ya Ardhi, ikiwa ni pamoja na kuona eneo la mgogoro ili kuweza kung’amua kiini cha mgogoro na kuutatua kwa njia ya amani.

Elimu ya usuluhishi iliyoanza tarehe 13, Aprili 2026 hadi tarehe 17 Aprili, 2026 ilitolewa vema katika Vituo vya Mahakama Kuu Kigoma, Mahakama za Wilaya Kigoma, Kibondo, Kasulu, Uvinza, Kakonko na Buhigwe ikienda na sambamba na utoaji elimu kupitia Redio ambapo Wilaya hizo zilishiriki kuwahabarisha wananchi kuhusu Wiki ya Usuluhishi iliyofanyika katika Mahakam azote nchini.

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Bi. Veronica John akifafanua jambo hivi karibuni alipokuwa akitoa elimu ya Usuluhishi kwa wananchi Mahakama Kuu Kigoma.

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bi. Veronica John akisisitiza jambo alipokuwa akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi Mahakama Kuu Kigoma hivi karibuni.


Mwananchi Mkazi wa Gungu-Kigoma, Bw. Bakari Abdallah Mfaume (katikati) akitoa neno la kuishauri Mahakama baada ya kupewa elimu juu ya faida za Usuluhishi katika jamii.

Sehemu ya wananchi wakisikiliza kwa makini elimu iliyokuwa ikitolewa na Wakili Veronica John, Mahakama Kuu Kigoma.

Mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bi. Veronica John akisikiliza kwa makini swali alilokuwa akiulizwa na mmoja wa wananchi wakati alipokuwa akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi hao hivi karibuni.

 (Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

'TUMIENI UJUZI WA USULUHISHI MLIOUPATA KUISAIDIA JAMII KUMALIZA MIGOGORO KWA AMANI'

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa amewataka washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi ambao ni Mahakimu kutoka Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza kutumia ujuzi walioupata kuisaidia jamii kumaliza migogoro yao kwa amani na utengamano.

Mhe. Mbelwa aliyasema hayo hivi karibuni mkoani Kigoma wakati akifunga mafunzo ya Usuluhishi yaliyoendeshwa kwa siku tano na kuhudhuriwa na washiriki 16. 

“Tumieni ujuzi huu wa usuluhishi kuisaidia jamii kutatua migogoro kwa njia ya amani ili kuleta utengamano wa kijamii ili kupunguza utitiri wa migogoro katika Mahakama zetu na hii itaboresha upatikanaji haki kwa wananchi,” alisema Mbelwa.

Alibainisha kuwa, mafunzo hayo yamefanikiwa kwani washiriki wamepewa mbinu zote muhimu za usuluhishi, hivyo ni matarajio ya Mahakama na Jamii kwa ujumla wake kuona wanatumia vema ujuzi na weledi walioupata kuleta tija katika utatuzi wa migogoro Mahakamani ili kupunguza mashauri.

Aidha, alifafanua kuwa, mafunzo hayo yamefanyika sambamba na Wiki ya Usuluhishi Kitaifa, huku akitoa pongezi kwa washiriki ambavyo wameshiriki vema Wiki ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi, ambapo wametumia weledi walioupata kufanya usuluhishi na umeleta tija kwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma kwa mashauri waliyosimamia ambayo usuluhishi wake umefanikiwa.

Aidha, alimshukuru Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju kukubali mafunzo hayo yafanyike Kigoma na washiriki kutoka maeneo tajwa walioshiriki katika mafunzo hayo.

Vilevile alimshukuru Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo kwa kuridhia Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa kuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo ya Usuluhishi.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nyamagana, Mhe. Ramla Shehagilo alitoa shukrani kwa niaba ya washiriki, ambapo aliwashukuru Wakufunzi wa Mafunzo hayo sambamba na Waandaaji wa mafunzo hayo ambao ni Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) pamoja na Mahakama ya Tanzania kwa kuwachagua wao kuwa washiriki wa mafunzo ya usuluhishi katika Wiki ya Kitaifa ya Usuluhishi.

Naye, Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna Rweikiza akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Chuo IJA, Mhe. Dkt. Kihwelo alibainisha kuwa washiriki wamejifunza mbinu zote za usuluhishi hivyo, malengo ya mafunzo hayo yamefikiwa, na kubainisha kuwa wasuluhishi hao watakuwa na tija katika kuongeza juhudi za kuimarisha ufanisi na upatikanaji wa haki Mahakamani.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania).


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa hotuba ya kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyika kwa siku tano Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi Mahakama Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (katikati) akitoa neno kwa washiriki siku ya mwisho wa Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyika kwa siku tano mkoani Kigoma. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na kushoto ni Bi. Rose Nyatega kutoka Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ Tanzania).

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa  Mahakama ya Wilaya Nyamagana, Mhe. Ramla Shehagilo akitoa neno la shukrani kwa niaba ya washiriki wote wakati wa kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyikia Mahakama Kuu Kigoma.

Hakimu Mkazi na Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Husna Rweikiza akitoa neno kwa niaba ya Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto wakati wa kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyotolewa kwa washiriki 16 kutoka Mahakama Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (kulia) akitoa cheti kwa moja ya washiriki wa Mafunzo ya Usuluhishi wakati wa kufunga mafunzo hayo yaliyowahusisha washiriki 16 kutoka 
Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.

Picha ya pamoja baada ya kufunga Mafunzo ya Usuluhishi yaliyofanyika Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

MAHAKAMA GEITA YAPOKEA UGENI KUTOKA DIVISHENI YA BIASHARA, MASJALA NDOGO SINGIDA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, imeendelea kujipambanua katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), baada ya kupokea ugeni kutoka Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara ya Dar es Salaam pamoja na Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

Lengo la ziara hizo lilikuwa ni kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya TEHAMA katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.

Ugeni wa kwanza uliwasili tarehe 16 Aprili, 2026 ukitokea Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, ukiwa na wajumbe wanane ukiongozwa na Naibu Msajili, Mhe. Suzan Kihawa, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Anatory Kagaruki.

Ugeni wa pili ulitoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, ukiwa na Watumishi tisa, wakiongozwa na Naibu Msajili, Mhe. Evodia Kyaruzi, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Filbert Matotay.

Katika ziara hiyo, kulifanyika mafunzo yaliyofunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, ambaye aliwakaribisha wageni na kuwashukuru kwa kuchagua Geita kama Kituo cha kujifunza.

Alieleza kuwa ziara hiyo ni fursa muhimu ya kubadilishana mawazo na uzoefu kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama kwa kutumia TEHAMA.

Jaji Mhina alibainisha kuwa mafanikio ya Mahakama Kuu Geita yametokana na misingi madhubuti iliyowekwa tangu kuanzishwa kwake, ikiwemo maelekezo ya Viongozi wakuu wa Mahakama, yaliyosisitiza umuhimu wa kuifanya Mahakama kuwa ya kisasa kidijitali.

Aliongeza kuwa matumizi ya TEHAMA yameongeza uwazi, yamepunguza gharama za uendeshaji, yamerahisisha upatikanaji wa taarifa na kuboresha mifumo ya ukaguzi wa shughuli za Mahakama.

Aidha, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa mafanikio hayo yanatokana na mambo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara wa mifumo, usimamizi thabiti wa Watumishi, ufuatiliaji wa karibu wa utendaji kazi, utoaji wa motisha, pamoja na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa Watumishi bila kujali kada zao.

Mafunzo hayo yalihusisha jumla ya mada tano zilizowasilishwa na Watumishi mbalimbali wa Mahakama, kwa lengo la kupeana uzoefu na kuboresha utendaji wa kazi.

Mada hizo zilitolewa na Naibu Msajili, Mhe. Fredrick Lukuna, Mtendaji wa Mahakama Bi. Masalu Kisasila, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, pamoja na Mtunza Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Geita, Bi. Winfirda Ng’humbu.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mhe. Lukuna, alisisitiza kuwa mafanikio ya Taasisi yoyote yanategemea mshikamano wa pamoja miongoni mwa Watumishi wake.

Alieleza kuwa ni muhimu kuwa na malengo ya pamoja, kushirikiana kikamilifu katika utekelezaji wa majukumu, kukubali makosa na kujifunza kutokana nayo, pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa vitendea kazi vya kutosha.

Aidha, alihimiza utambuzi wa mapema wa changamoto zinazoweza kujitokeza ili zisikwamishe utekelezaji wa malengo yaliyowekwa.

Kwa upande wa mada ya utawala na matumizi ya TEHAMA, Mtendaji wa Mahakama Geita alieleza kuwa wamefanikiwa kuendesha shughuli nyingi za kiutawala bila matumizi ya karatasi.

Alifafanua kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano wa Watumishi wote pamoja na utayari wao wa kuendana na dira ya uongozi wa Mahakama Kuu Geita ya kuimarisha matumizi ya TEHAMA.

Akizungumza kwa niaba ya wageni, Mhe. Kihawa alitoa shukrani kwa mapokezi mazuri pamoja na mafunzo waliyoyapata, akieleza kuwa uzoefu huo utasaidia kuboresha utendaji katika Mahakama zao.

Naye Mhe. Kyaruzi alieleza kuridhishwa na mafunzo hayo na kuahidi kutumia maarifa hayo kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika Masjala zao.

Wageni walipata fursa ya kujionea kwa karibu namna Mahakama Kuu ya Geita ilivyofanikiwa kufikia hatua ya matumizi kamili ya TEHAMA katika utoaji wa huduma zake.

Kupitia uzoefu huo, wageni hao waliondoka wakiwa na matarajio na dhamira ya kutekeleza maboresho makubwa zaidi katika maeneo yao ya kazi, wakilenga kuiga na kuendeleza mifumo waliyoishuhudia.

Lengo kuu ni kuhakikisha kuwa wanakuwa sehemu ya mabadiliko chanya yatakayochochea utoaji wa huduma za haki kwa Wananchi kwa ufanisi zaidi, uwazi ulioboreshwa na kwa wakati muafaka.

Kwa mtazamo wa jumla, ziara hizi zimekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA ndani ya Mahakama za Tanzania.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina akifungua mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akitoa ufafanuzi juu ya ushirikiano biana ya Viongozi na Watumishi unavyoleta mafanikio katika kuongeza ufanisi wa matimizi ya Tekinolojia ya Habari na mawasiliano (TEHAMA).

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Suzan Kihawa akitoa shukrani wakati wa ziara waliyoifanya Mahakama Kuu Geita.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi akieleza jinsi Geita ilivyowavutia kwenye matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, akielezea namna utawala Mahakama Geita ulivyoachana na matumizi ya karatasi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, akieleza jinsi Mahakama za Wilaya wanavyotumia mifumo katika Mahakama za Wilaya.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, akieleza jinsi Mahakama za Mwanzo zilivyoachana na matumizi ya karatasi kwa kubuni Mfumo wa Mahakama za Mwanzo.

Picha ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara.


 Picha ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na Mahakama Kuu Singida.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKAMA SONGEA YAZINDUA MAJENGO MATATU YA MAHAKAMA ZA MWANZO

Na NOEL SYLIVESTER – Mahakama, Songea

Mahakama ya Tanzania katika Mkoa wa Ruvuma, tarehe 17 Aprili, 2026 imezindua Mahakama za Mwanzo tatu kwenye Wilaya mbalimbali baada ya ujenzi wake kukamilika.

Uzinduzi huo uliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, ambao ulifanyika kwa pamoja katika Viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Lilondo katika Wilaya ya Songea.

Mahakama nyingine zilizozinduliwa ni Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga iliyopo katika Wilaya ya Namtumbo na Mahakama ya Mwanzo Nalasi iliyopo Wilaya ya Tunduru.

Uzinduzi wa Mahakama hizo unalenga kurahisisha upatikanaji wa haki kwa Wananchi, kupunguza umbali wa kufuata huduma za kimahakama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa wakati na garama nafuu.

Katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi aliongelea dhima ya Mahakama katika kutoa haki kwa wakati unaostahili bila kuchelewesha huduma hizo za msingi kwa Wananchi.

Vilevile, Mhe. Karayemaha aliwaasa Watumishi na Wananchi wa maeneo hayo  kuhakikisha wanayatunza majengo hayo na miundombinu yake ili yaweze kudumu kwa muda mrefu.

“Kuanzishwa kwa Mahakama hizi kutasaidia kupunguza msongamano wa mashauri na kuharakisha utoaji wa haki. Hatua hii ni sehemu ya juhudi za Mahakama na Serikali ya Tanzania kuhakikisha kila Mwananchi anapata haki kwa wakati na kwa ghalama nafuu,”alisema.

Kwa upande wake, mgeni maalumu katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Kapenjama Ndile, aliwaasa Wananchi kushirikiana na Watumishi wa Mahakama kwa ajili ya kulinda msingi wa amani na kudumisha ustawi wa utoaji haki kwa Wananchi.

“Mahakama ni mali ya Wananchi, hivyo ni wajibu wetu sote kushirikiana na kuyatunza majengo ya Mahakama zetu pamoja na miundombinu yake kwa ujumla,” alisema Mhe. Ndile.

Katika taarifa yake, Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, alitoa ufafanuzi kuhusu majengo hayo ambayo yamezinduliwa na gharama zilizotumika mpaka kukamilika kwa ujenzi wa majengo hayo yote matatu.

Alibainisha kuwa Mahakama ya Mwanzo Lilondo mpaka kukamilika kwake imetumia 985,625,739/=. Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga imegharimu 961,400,162/= na Mahakama ya Mwanzo Nalasi imegharimu 1,007,033,928.18/=, hivyo kufanya  jumla ya 2,954,059,829.18/=

Hafla hiyo pia ilihudhuliwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Songea, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Songea, Mbinga, Nyasa, Namtumbo na Tunduru, pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha akihutubia katika hafra ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo tatu baada ya ujenzi wake kukamilika.

Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Kapenjama Ndile, akihutubia katika hafla hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, akisoma taarifa ya ujenzi wa Mahakama hizo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha (wa tatu kutoka kushoto) akikata utepe kuashiria kuzinduliwa wa Mahakama hizo.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama waliohudhulia hafla hiyo.

Kikundi cha Ngoma za Asili kikitumbuiza wakati wa halfa hiyo.

Sehemu ya Wananchi wa Lilondo wakishuhudia uzinduzi wa Mahakama hizo.

Sehemu ya Wanafunzi waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Serikali waliohudhuria katika hafla hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKIMU WAPATIWA MAFUNZO KUHUSU TARATIBU UCHUKUAJI MAELEZO YA UNGAMO

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Mahakama Dodoma tarehe 17 Aprili, 2026 iliendesha mafunzo ya taratibu za uchukuaji wa maelezo ya ungamo, yakihusisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutoka Dodoma na Singida.

Mafunzo hayo yaliyoendeshwa kwa mfumo mseto, yalifanyika katika ukumbi wa Mahakama uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Baadhi ya washiriki walihudhuria ana kwa ana ukumbini, huku wengine wakishiriki kwa njia ya mtandao kupitia kiunganishi maalumu. Hatua hiyo iliwezesha ushiriki mpana zaidi wa Mahakimu, wakiwemo wale ambao hawakuweza kufika eneo la mafunzo.

Akifungua mafunzo hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, alisisitiza umuhimu wa Mahakimu kuzingatia kikamilifu taratibu za kisheria katika uchukuaji wa maelezo ya ungamo ili kulinda haki na kuhakikisha ushahidi unaokubalika mahakamani.

“Ubora wa uamuzi wa Mahakama huanza na ubora wa ushahidi unaowasilishwa, ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa maelezo ya ungamo yanachukuliwa kwa kuzingatia kikamilifu sheria, miongozo na kanuni zilizowekwa,” alisema Dkt. Masabo.

Katika hotuba yake, aliwashukuru kwa dhati wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa kujitoa kwao, hususan wale waliowezesha mafunzo kwa njia ya mtandao, akiwemo Naibu Msajili na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Huduma za Mahakama, Ukaguzi, Mrejesho kwa Umma na Maadili, Mhe. Maira Kasonde, pamoja na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mombo, ambaye pia ni mwezeshaji wa mafunzo hayo.

Aidha, alitambua na kushukuru ushiriki wa Viongozi wa juu wa Mahakama waliohudhuria kwa njia ya mtandao, akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayubu Mwenda, ambaye alifuatilia mafunzo hayo kama sehemu ya kuimarisha utoaji haki katika maeneo yao.

Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea Mahakimu uelewa wa kina kuhusu taratibu sahihi za kisheria katika uchukuaji wa maelezo ya ungamo, pamoja na kuwapa mbinu bora za vitendo zitakazosaidia kuepuka makosa ya kiutaratibu yanayoweza kuathiri ushahidi na uamuzi wa Mahakama.

Kupitia mafunzo hayo, Mahakimu wamekumbushwa umuhimu wa kufuata miongozo ya sheria katika kila hatua ya uchukuaji wa maelezo ya ungamo, ikiwemo kuhakikisha mtuhumiwa anafahamishwa haki zake, kurekodi maelezo kwa usahihi, na kuthibitisha uhalali wa maelezo hayo kwa mujibu wa sheria.

Mafunzo hayo yameacha alama muhimu kwa washiriki, yakiwakumbusha wajibu wao mkubwa katika kulinda haki za Wananchi kupitia uzingatiaji sahihi wa sheria na taratibu.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya mifumo ya utoaji haki na changamoto zinazoendelea kujitokeza, utoaji wa mafunzo hayo kwa njia ya ana kwa ana pamoja na mtandao unaonesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha Mahakimu wanakuwa na uelewa wa kisasa unaokidhi mahitaji ya wakati.

Hatua hiyo si tu inalenga kuboresha utendaji kazi wa Mahakimu, bali pia inalenga kuimarisha imani ya jamii kwa Mhimili wa Mahakama, ambapo haki haitolewi tu bali inaonekana ikitendeka kwa uwazi, weledi na uadilifu.

Akimhitimisha mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule, amewashukuru washiriki kwa ushiriki wao mzuri, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yatachangia kuleta mabadiliko chanya katika utoaji wa haki na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masab,o akisoma hotuba ya ufunguzi wa mafunzo ya taratibu za uchukuaji wa maelezo ya ungamo (Extra-Judicial Statements) kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo Dodoma.

 

Meza kuu ikiongoza na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo Dodoma Mjini waliohudhuria mafunzo hayo. Kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule na kushoto kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe Thurstone Kombe.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Jumapili, 19 Aprili 2026

BARAZA ELIMU YA SHERIA LAKAGUA MAZINGIRA UTOAJI ELIMU YA SHERIA VYUO VIKUU

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam na REHEMA AWET-Mahakama, Mwanza

Baraza la Elimu ya Sheria nchini, chini ya Mwenyekiti, ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, hivi karibuni lilifanya ziara maalum, kukagua Vyuo Vikuu vitatu, kama sehemu ya juhudi za kuimarisha ubora wa elimu ya sheria nchini.

Wajumbe wa Baraza hilo walifanya ukaguzi katika Chuo cha Kimataifa Kampala, Chuo Kikuu Huria Tanzania na Chuo cha St. Augustine Mwanza.

Ziara hiyo ni sehemu ya mpango mpana wa Baraza la Elimu ya Sheria wa kutembelea na kukagua mazingira ya vyuo mbalimbali nchini ili kuhakikisha elimu ya sheria inatolewa kwa viwango vinavyokubalika na vinavyoendana na mahitaji ya jamii

Akizungumza wakati wa ziara hizo, Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria alisema kuwa lengo kuu ni kukagua na kuboresha mifumo ya ufundishaji, mitaala, pamoja na miundombinu inayotumika kufundishia sheria ili kuhakikisha wahitimu wanakidhi viwango vinavyotakiwa kitaifa na kimataifa.

Alisema kuwa Baraza la Elimu ya Sheria lina jukumu la kusimamia na kudhibiti ubora wa elimu hiyo nchini, hivyo ziara kama hizo ni muhimu katika kubaini changamoto na kuweka mikakati ya kuzitatua kwa kushirikiana na Taasisi husika.

Wakuu wa vyuo hivyo walipongeza ziara hiyo, wakieleza ni fursa muhimu kwao ya kubadilishana mawazo na kupokea ushauri utakaosaidia kuboresha utoaji wa elimu ya sheria.

Katika ziara hizo, Baraza pia lilipata nafasi ya kukutana na Wanafunzi wa kitivo cha sheria vyuoni hapo na kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili, pamoja na kupokea mapendekezo yao ya namna ya kuboresha mazingira bora ya kujifunzia ili kuweza kupatikana wanasheria bora.

Baraza pia lilipata wasaa wa kutembelea baadhi ya maeneo katika vyuo vikuu hivyo, ikiwemo Moot Court, Maktaba, Mabweni ya Wanavyuo, Ofisi za Viongozi pamoja na Walimu.

Aidha, Baraza hilo lilifanya mazungumzo na uongozi wa vyuo hivyo na kupokea taarifa ili kuona namna wanavyoweza kuboresha mitaala ili kuendana na soko la ajira.

Pamoja na hayo, Mwenyekiti wa Baraza alishauri namna bora ambayo inaweza kusaidia uhusiano mzuri kati ya vyuo hivyo, Mahakama na Taasisi mbalimbali za elimu katika kuandaa Wanafunzi bora na wenye tija katika soko la ajira.

Mapokezi ya Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini katika Chuo Kikuu cha Kimataifa Kampala.

Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria pamoja na Wanafunzi wa Chuo Kikuu Kampala.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani (katikati), Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kimataifa Kampala, Prof. Honoratha Mushi (tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini.

Mapokezi ya Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini katika Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria pamoja na Uongozi wa Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini akitembelea Maktaba ya Chuo Kikuu cha St. Augustine.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani (katikati), Mkuu wa Chuo cha St. Augustine, Padre. Prof. Juvenalis Asantemungu (tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.