Ijumaa, 20 Machi 2026

JAJI MFAWIDHI MOSHI AHAIDI KUKAMILISHA UANZISHWAJI WA MAHAKAMA YA MWANZO KWAKOA

Na PAUL PASCAL-Mahakama, Moshi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella, tarehe 18 Machi, 2026 alifanya ziara kwa ajili ya kuzungumza na Viongozi wa Serikali na Wananchi wa Kata ya Kwakoa juu ya ombi lao kuhusu kupatiwa huduma ya Mahakama katika eneo lao.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Mongela aliambatana na Viongozi wa Mahakama Kuu Moshi na Mahakama ya Wilaya Mwanga, kufuti ombi la Wananchi hao kutoka Kijiji cha Ngulu kilichoko Kata ya Kwakoa, Wilayani Mwanga, Mkoa wa Kilimanjaro.

Kwenye ombi hilo waliloliwasilisha kwenye Ofisi ya Jaji Mfawidhi, wananchi walieleza hitaji la kupata huduma za kimahakama kutokana na adha wanayoipata kwa kufuata huduma hiyo umbali wa zaidi ya kilometa 40.

Akisoma taarifa fupi ya Kata ya Kwakoa, Diwani wa eneo hilo, ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Kata, Mhe. Kiende Mvungi, alieleza kuwa kwenye Kata nne zinazounda ukanda kwenye eneo lao hakuna hata moja yenye huduma ya kimahakama.

“Naomba nikufahamishe kuwa Kata yetu ya Kwakoa inaundwa na Vijiji viwili; Kijiji cha Kwakoa na Kijiji cha Ngulu. Ukanda huu umeundwa na Kata nne; Toroa, Kigonigoni, Jipe na Kwakoa na katika Kata zote, hakuna yenye Mahakama ya Mwanzo. Wananchi wote wa Kta hizi wanafuata huduma za kimahakama katika Mahakama ya Mwanzo Lembeni, ambayo iko zaidi ya kilometa 40 kutoka hapa,” alisema Mhe. Kiende.

Diwani huyo alibainisha kuwa katika kata yao wana Kituo cha Polisi, lakini mnyororo wa utoaji haki hauwezi kukamilika pasipo kuwepo kwa Mahakama ambayo ndiyo yenye jukumu la kutafsiri sheria za nchi na kwa kuliona hilo Serikali ya Kata ya Kwakoa ikawasilisha ombi la kuanzishwa Mahakama ya Mwanzo Kwakoa ili iweze kuhudumia Kata zote nne katika ukanda huo.

“Tumetenga eneo lenye ukubwa wa ekari nne kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Mahakama na makazi ya Watumishi kwa mpango wetu wa muda mfupi, tunaomba tuwakibidhi jengo la kuanzia kutoa huduma za kimahakama katika eneo hili, wakati michakato ya muda mrefu wa ujenzi ukiendelea ili nasi tupate huduma tuliyoikosa katika eneo letu tangu tulipopata uhuru,” lisema Mhe. Kiende.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi aliwashukuru Wananchi na Viongozi wa Kata ya Kwakoa kwa kutambua na kuwa na imani na Mahakama. Alipongeza juhudi katika kuhakikisha huduma zote muhimu zinapatikana ndani ya Kata pasipo kuzifuata mbali.

“Tumefurahishwa na jitihada zote mlizofanya ili muweze kupata huduma ya Mahakama katika eneo lenu, niwaahidi kwa juhudi hizi jambo lenu linakwenda kukamilika, tunakwenda kutekeleza matakwa ya kisheria ya uanzishaji wa Mahakama ya Mwanzo ndani ya miezi mitatu. Tutahakikisha michakato yote inakamilika na huduma za kimahakama katika Kata hii zinaanza,” alisema.

Katika ziara hiyo, Jaji Mongella aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje, Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Moshi, Bi. Maria Itala na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mwanga, Mhe. Marium Mfanga.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika katika Kata ya Kwakoa wilayani Mwanga.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella akisalimiana na Mwenyekiti wa Kijiji cha Ngulu, Kata ya Kwakoa, Bw. Said Mvungi mara baada yakuwasili katika ziara yake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella akizungumza na Wananchi wa Kata ya Kwakoa wilayani Mwanga (hawako pichani) wakati wa ziara yake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella akiongozana na Viongozi wa Serikali ya Kata ya Kwakoa kukagua jengo kwa ajili ya kutolea huduma za  Mahakama ya Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella (aliyesimama mbele katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Kata ya kwakoa mbele ya jengo linalotazamiwa kutumika kutolea huduma za Mahakama ya Mwanzo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

WAFUNGWA, MAHABUSU WAIPONGEZA MAHAKAMA MUSOMA

Na FRANCISCA SWAI - Mahakama Musoma

Wafungwa na Mahabusu katika Magereza tofauti ndani ya Mkoa wa Mara, wameipongeza Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Musoma, kwa namna inavyotoa huduma zake.

Pongezi hizo zimetolewa wakati wa ukaguzi wa Magereza uliofanywa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mtulya alitembelea na kukagua Magereza ya Tabora B, Gereza Mugumu na Gereza Musoma. Aliambatana na Wadau wa Haki Jinai kwa ajili ya kusikiliza na kutatua changamoto.

Pamoja na pongezi hizo, Wafungwa na Mahabusu waliibua na kujibiwa changamoto zao mbalimbali, hasa wanazokutana nazo kutoka kwa Wadau kuhusiana na namna wanavyokamatwa, upelelezi unavyofanyika na uletaji wa mashahidi mahakamani.

Naye Mkuu wa Gereza la Musoma, Afande John Murya, alimshukuru Jaji Mtulya kwa namna Mahakama inavyowapa ushirikiano. Alieleza kuwa katika Gereza hilo wanaendelea na ujenzi wa jengo litakalotumika kwa ajli ya Mahakama Mtadao (Virtual Court).

Aidha, katika ukaguzi huo Mhe. Mtulya alitoa pongezi kwa Jeshi la Magereza kwa namna wanavyokaa na Wafungwa na Mahabusu hao na namna wanavyowasaidia kwa kuwapa elimu juu ya masuala mbalimbali ya kisheria na kijamii.

Zaidi aliwapongeza kwa ushirikiano wao katika matumizi ya Mahakama Mtandao ili kuhakikisha utoaji wa haki unafanywa kwa wakati kwakuwa jukumu la utoaji haki ni la pamoja kati ya Mahakama na Wadau wake wote.

Jaji Mfawidhi pia aliwaasa Wafungwa na Mahabusu hao pale watakapomaliza kutumkia adhabu zao, wakawe raia wema, wazingatie sheria na taratibu za nchi ili kuleta amani na ustawi kwa Taifa na familia zao.

 







Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma; Naibu Msajili, Mhe. Monica Ndyekobora (wa pili kulia), Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw. Leonard Maufi (wa kwanza kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Serengeti, Mhe. Jacob Ndira (wa kwanza kulia). Wengine katika picha ni Kaimu Mkuu wa Gereza, Afande Malele (wa pili kushoto), Watumishi wa Mahakama Serengeti na  Wadau wa Haki Jinai.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (mbele) akiwa anasisitiza jambo katika taarifa iliyosomwa kwake na Kaimu Mkuu wa Gereza la Wafungwa Tabora B, Afande Majuto Mabele (wa kwanza kulia kwa Mhe. Mtulya) pamoja na Viongozi, Wadau na Watumishi wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (mbele) akiwa anafuatilia na kusisitiza taarifa iliyotolewa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (aliyesimama), wakati wa kujadili changamoto za Wafungwa katika kikao chake na watumishi wa Mahakama Serengeti pamoja na Wadau wa Haki Jinai walipotembelea Gereza la Wafungwa Tabora B.

Jengo linaloendelea na ujenzi kwa ajili ya kutumiwa kwa shughuli za Mahakama Mtandao katika Gereza Musoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

  

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

.

WAFUNGWA, MAHABUSU GEREZA LA KIGONGONI WAIPONGEZA MAHAKAMA, WADAU HAKI JINAI KWA KUHARAKISHA MASHAURI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Wafungwa na Mahabusu wa Gereza la Kilimo la Kigongoni lililopo Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani wameipongeza Mahakama na Wadau wa Haki Jinai kwa kuondoa kero zao.

Waliyasema hayo tarehe 18 Machi, 2026 walipotembelewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi katika ziara yake ya ukaguzi katika gereza hilo.

Kabla ya kupokea pongezi hizo, Jaji Maghimbi alipata taarifa kutoka kwa Mkuu wa Gereza hilo, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Hassan Lidenge ambaye alisema kuwa, Gereza la Kilimo Kigongoni lilianzishwa miaka ya 1970 ambapo shughuli kubwa inayofanyika ni kilimo na hasa kilimo cha mpunga. 

Alisema, Gereza hilo lina uwezo wa kuhifadhi Wafungwa na Mahabusu (Authorized Accommodation Capacity) 198. Idadi ya wahalifu waliokuwepo tarehe 18 Machi 2026, Wafungwa Watanzania wanaume walikuwa 26, Waethiopia watano, Raia wa Burundi 28, Mahabusu wanaume nane na Mahabusu wanawake watatu, jumla ya wafungwa na mahabusu wanawake na wanaume 70 na hivyo kueleza kwamba, katika Gereza hilo hakuna msongamano.

Mkuu huyo wa Gereza, alisema sambamba na huduma za kuwapeleka wafungwa/mahabusu katika Mahakama mbalimbali,  agizo la matumizi ya Mahakama Mtandao limetekelezwa kwa kutengwa chumba chenye vifaa kwa ajili ya shughuli za Mahakama mtandao, na kueleza kuwa, “tayari kesi za kuahirishwa au kutajwa zimefanyika kwa kutumia huduma hiyo.”

Aidha Mrakibu huyo Mwandamizi, amekiri kupata ushirikiano kutoka ngazi zote za Mahakama kila wakati wanapohitaji msaada ambapo amesema, “naomba kutumia fursa hii, kutoa shukrani kwako binafsi Jaji Mfawidhi na timu uliyoambatana nao kwa kuweka ratiba ya kutembelea Gereza hili.”

Mkuu huyo ametoa pongezi kwa ngazi zote katika Mhimili wa Mahakama kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakitimiza majukumu yao kwa weledi na kuwa sio tu chachu katika utoaji haki kwa jamii lakini utendaji wao umekuwa ni sababu ya kuondoa hali ya msongamano magerezani.

Baada ya kupokea  taarifa ya Mkuu wa Gereza hilo,  Mhe Maghimbi alizipokea pongezi hizo na kuzielekeza kwa Wasaidizi wake Mahakimu Wakazi Wafawidhi na kusema mara nyingi amekuwa akipata bahati ya kufanya kazi na Wafawidhi wanawake ambapo amejifunza kwamba wamekuwa na maadili mema kusema kuwa, “hivyo najisikia vizuri zaidi na ikizingatiwa huu ni mwezi wa wanawake.”

Lakini pia Jaji Mfawidhi huyo aliongeza kuwa, hata sasa anafanya kazi vizuri na Naibu Msajili Mfawidhi wa kiume ambaye ni Mhe. Livin Lyakinana na Mtendaji wa Kanda ya Dar es Salaam ambaye ni mwanaume, Bw. Sumera Manoti.

Akisoma risala kwa niaba ya wafungwa na mahabusu, Mahabusu namba 274/2025 Kassian Pomoni alitoa pongezi za dhati kwa wadau wote wa utoaji wa haki na haki jinai wakiongozwa na Mahakama.

Aliongeza kwa kusema kwamba, hatua hiyo inatokana na ukweli usiopingika kuwa, changamoto nyingi zilizokuwa zinawakabili huko nyuma zimefanyiwa kazi na kupungua kama sio kumalizika kabisa.

Akiainisha pongezi hizo, alieleza kuwa, hapo awali mashahidi walikuwa hawaletwi kwa wakati hali iliyokuwa ikisababisha mashauri kukaa kwa muda mrefu na kusababisha msongamano  wa Mahabusu gerezani na kukiri kuwa, “kwa sasa changamoto hiyo haipo tena kwa vile mamlaka  husika zinajitahidi kuhakikisha  mashahidi wanaletwa kwa wakati.”

Akizungumzia kuhusu Jeshi la Polisi kupitia Idara ya Upelelezi, Mahabusu hao wamesema mashauri yanachukua muda mfupi mpaka kukamilika kwa upelelezi tofauti na ilivyokuwa huko nyuma na kwamba hatua hiyo inawezesha mashauri kuamriwa mapema na wahusika kujua hatima zao.

Kwa upande wa Jeshi la Magereza, amesema jitihada za kutosha zimekuwa zikifanyika ili kuhakikisha Mahabusu wanahudhuria mahakamani kwa tarehe zilizopangwa.

Mahabusu hao walimshukuru Mhe. Maghimbi pamoja na wote alioongozana nao kwenda kuwatembelea na kuwasikiliza japo hawana changamoto zaidi bali ni pongezi na kuwatakia majukumu mema ya kutimiza wajibu na majukumu yao kwa weledi.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi  akisalimiana na Askari Magereza alipowasili tarehe 18 Machi, 2026 katika ziara ya ukaguzi katika Gereza la Kilimo la Kigongoni lililopo wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Gereza la Kilimo la Kigongoni lililopo wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani. 
Viongozi waliombatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam katika ziara ya ukaguzi. Kutoka kushoto ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi na  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bagamoyo, Mhe. Yasinta Kingwala.

 
Mkuu wa Gereza la Kilimo Kigongoni, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Hassan Lidenge (kulia) akisoma taarifa mbele ya Jaji Mfawidhi (hayupo katika picha). Katikati ni Mwanasheria wa Serikali Mwandamizi, Bi. Bonisia Mollel na kushoto ni Mwanasheria wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Bi.Maria Mwakatobe. 

Jaji  Mfawidhi na Timu ya Wadau wa Haki Jinai  aliyoambatana nayo katika ziara ya ukaguzi wakipata maelezo kutoka kwa Mkuu wa Gereza la Kilimo Kigongoni wakiwa kwenye chumba cha Mahakama mtandao (virtual court) wakati walipofanya ziara ya ukaguzi katika gereza hilo. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu y Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (aliyeketi katikati). Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana na kushoto ni Mkuu wa Gereza la Kigongoni Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Hassan Lidenge.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

Alhamisi, 19 Machi 2026

NCHI WANACHAMA UMOJA WA MATAIFA WAKUTANA KUJADILI HALI YA WANAWAKE DUNIANI

  •  Mkutano Wa Hali Ya Wanawake Duniani (CSW 70) Wafunguliwa Rasmi Jijini New York
  • Waziri Gwajima atoa Taarifa Ya Tanzania
  • Wanachama wa TAWJA nao washiriki katika mkutano huo

Na WMJJWM, New York-Marekani

Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa zimekutana jijini New York nchini Marekani kwa lengo la kujadili hali ya wanawake katika nchi hizo.

Mkutano huo ni wa 70 kuhusu Hali ya Wanawake Duniani unaoongozwa na Kaulimbiu isemayo "Kuhakikisha na Kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa Wanawake na Wasichana wote, ikiwa ni pamoja na kukuza mifumo ya kisheria nyenye usawa na jumuishi, kuondoa sheria, sera, na desturi za kibaguzi na kushughulikia vikwazo vya kimuundo", (Ensuring and Strengthening access to justice for all Women and Girls, including by promoting inclusive and equitable legal system, eliminating discriminatory laws, policies, and practices and addressing structural barriers”).

Mkutano huo ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  António Guterres tarehe 09 Machi, 2026 na kumalizika leo tarehe 19 Machi, 2026.

Miongoni mwa washiriki waliohudhuria katika Mkutano huo ni pamoja na sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho, Mhe. Barke Sehel.

Mkutano huo umejadili masuala mbalimbali ya upatikanaji wa haki na huduma kwa Wanawake ikiwemo haki ya upatikanaji wa Ardhi, haki kwa upatikanaji wa Elimu, haki ya kujua masuala ya sheria na upatikanaji wa haki za kisheria, kushiriki katika masuala ya uongozi na siasa, haki ya kumilili na upatikanaji wa huduma bora za Afya.

Siku ya kwanza ya mkutano huo, Tanzania iliongozwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Felister Mdemu, Wataalamu kutoka Wizara hiyo, Wizara nyingine za Kisekta, Taasisi za Serikali na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.

Aidha taarifa ya Nchi katika Mkutano huo ilitolewa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima.

Madhumuni ya mkutano huo yalikuwa kutafakari juu ya kuimarisha sauti ya Afrika katika CSW, kupokea taarifa kuhusu mazungumzo na kubadilishana maoni kuhusu ugombea wa Afrika kuwa mwenyeji wa mzunguko wa kwanza wa kikanda wakati wa CSW74 utakaofanyika mwaka wa 2030.

Aidha, katika mkutano huo masuala mbalimbali yalijadiliwa ikiwa ni pamoja na Mkataba wa Wanawake wa Afrika wa Kukomesha Unyanyasaji Dhidi ya Wanawake, masuala mbalimbali yanayohitaji kushughulikiwa kimkakati Afrika na kuja na sauti moja na mengine.

Katika mkutano huo iliamuliwa kuwa ili kuimarisha msimamo wa pamoja, Ofisi ya CSW inapaswa kujumuisha wawakilishi na wanachama kutoka Afrika katika hatua zote, kitaifa na kimataifa, ⁠Afrika inapaswa kusimama imara juu ya yale ambayo yamefikiwa kutoka kwa jukwaa la Beijing na inapaswa kutumika kama sehemu ya marejeo.

Iliamriwa pia kuwe na ushirikiano thabiti na mawasiliano ya Kimkakati yanayoungwa mkono na data yanapaswa kutumika kufuatilia maendeleo yaliyopatikana kufikia sasa.

Wana-TAWJA (Tanzania Women Judges Association) walishiriki katika side event ya MOCLA iliyokuwa na kichwa cha habari: "Kuimarisha Upatikanaji wa Haki kwa Wanawake na Wasichana. Huduma za Misaada ya Kisheria katika Kukabiliana na Ukatili wa Kijinsia na Kuwawezesha Wanawake".

Katika side event hiyo, Mhe. Barke Sehel Jr., Mwenyekiti wa TAWJA, ndio aliyefungua, na ilifungwa na Mhe. Sauda Mjasiri (Rtd J).

Matukio katika picha Mkutano wa Mkutano Wa Hali Ya Wanawake Duniani (CSW 70) na ushiriki wa Wana Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) katika Jiji la New York nchini Marekani.


Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (wa pili kushoto) pamoja na Wanachama wengine wa Chama hicho wakiwa kwenye Mkutano Wa Hali Ya Wanawake Duniani (CSW 70) jijini New York nchini Marekani.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima akiwasilisha mada katika mkutano huo.









Jaji Mkuu wa Mahakama ya Kenya na Rais wa Mahakama ya Juu ya Kenya, Mhe. Martha Koome (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sauda Mjasiri katika Mkutano wa Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.


Juu ni picha mbalimbali za Wana TAWJA na wanachama wengine walioshiriki Mkutano wa CSW katika Jiji la New York nchini Marekani wakiwa katika picha ya pamoja na 
Waziri  wa Wanawake, jinsia na maendeleo ya jamii, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Jumatano, 18 Machi 2026

HAKIMU MKAZI MFAWIDHI PWANI AWATAKA WAKRISTO NA WAISLAMU KUWA KITU KIMOJA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi amewataka Wakristo na Waislam kuwa wamoja maana hata vitabu vya Mungu vinasema watu wote ni sawa.

Mhe. Mkhoi aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa hafla ya Iftar iliyoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani.

Amesema hata wakiangalia kwa sasa, Waislamu wamefunga na Wakristo nao wako Kwaresma, ameeleza, “hii haitokei kwa bahati mbaya ni jinsi tu Mungu anavyoendela kutuonesha kuwa, sisi ni kitu kimoja tunatakiwa kuishi kwa kupendana, kushirikiana lakini pia tudumishe ushirikiano kama ambavyo vile tumeweza kuyadumisha.”

Akizungumza wakati wa Iftar hiyo, Ustadhi Mohamed alisema, kuna watu kila siku kazi zao kuingiza huzuni kwenye mioyo ya wenzao, huku akimpongeza Mhe. Mkhoi kwa kuandaa kitu cha kuwakutaniasha watu. 

“Katika mkusanyiko huu kuna watu inawezekana walikuwa na tofauti zao lakini kupitia mkusanyiko huu inawezekana tofauti zao zikaisha  lakini pia kupitia mkusanyiko huu tunaweza kupata marafiki wengi  watu wakabadilishana mawasiliano lakini mwisho wa siku wakatengeneza amani zaidi na upendo na mshikamano kwa sababu tu iliyosababishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani,” amesisitiza Ustadhi Mohamed. 

Iftar hiyo iliyoandaliwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani iliwajumuisha watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mahakama ya Wilaya Kisarawe.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi  ( wa kwanza kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama hiyo baada ya kushiri Iftar hivi karibuni.

Sehemu ya watumishi na waalikwa katika hafla ya iftar iliyofanyika katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mwanza)

 

 

 

 

 

Jumanne, 17 Machi 2026

JAJI MKUU ASHIRIKI KUMBUKIZI MIAKA MITANO YA HAYATI DKT. JOHN POMBE MAGUFULI

  •   Asema Hayati Dkt. Magufuli alikuwa mnyenyekevu, mwenye huruma na mchapakazi

  • Apongeza Kanisa kwa kuhimiza usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii, umoja wa kitaifa na maslahi ya Taifa

Na MARY GWERA, Mahakama-Chato

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Viongozi wengine wa Serikali, Wanafamilia na Watanzania kwa ujumla leo tarehe 17 Machi, 2026 kwa pamoja wameungana na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi, kuadhimisha miaka mitano ya Kumbukizi ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  

Katika Kumbukizi hiyo, Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Nchimbi amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan huku Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa Mgeni Maalum.

Ibada Maalum ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Kifo cha Hayati Dkt. Magufuli imefanyika katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.

Aidha, shughuli za Maadhimisho hayo zilianza majira ya saa 3:30 Asubuhi kwa Adhimisho la Ibada Takatifu iliyoongozwa na Maaskofu mbalimbali wakiongozwa na Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki la Rulenge-Ngara.

Mara baada ya ibada kukamilika, Viongozi mbalimbali walipata wasaa wa kutoa neno miongoni mwao akiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju ambaye ameishukuru familia ya Hayati Magufuli kwa mwaliko wa kushiriki katika Kumbukizi hiyo.

“Nashukuru Mama Janeth kwa ukarimu wako na kutualika, hii ni fursa ambayo inatukutanisha, lakini yatosha tu kusema kwamba nikushukuru Mhashamu Baba Askofu kwa ibada kubwa hii na muhimu uliyoifanya, ninawashukuru Kanisa kwa kuendelea kuhimiza usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii, umoja wa kitaifa na maslahi ya Taifa,” amesema Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, alimfahamu Hayati Magufuli wakati akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alipokuja kusoma Shahada ya Pili wakati yeye (Mhe. Masaju) akiwa anasoma Shahada ya kwanza.

Aidha, Mhe. Masaju amesema kuwa, baadaye mwaka 2015, Hayati Magufuli alimteua kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali mara baada ya kuwa ametumika kama Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa uteuzi wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Jaji Mkuu ameongeza kuwa, alifanya kazi na Hayati Dkt. Magufuli kwa miaka miwili katika nafasi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na baadaye alimteua kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na hatimaye Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akamteua kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania Juni, 2025.

“Ninawashukuru sana Viongozi hawa, Rais Kikwete, Rais Magufuli, Rais Samia, Rais Mwinyi ‘Senior’ na Rais Mkapa wana mchango mkubwa sana katika utumishi wangu,” ameeleza Mhe. Masaju.

Kadhalika, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, Hayati Magufuli alikuwa na huruma, mnyenyekevu na mchapakazi.

“Hayati Magufuli alikuwa mchapakazi na uchapakazi ule ndio maana tunayashuhudia haya aliyoyafanya na ambaye mrithi wake ambaye mimi naamini ilikuwa timu nzuri ameyakamilisha na mengine ameendelea kuyaibua na kuyafanya. Huu ni utaratibu mzuri kwa Taifa letu,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu alitumia nafasi hiyo pia kuitakia heri familia ya Hayati Magufuli kuendelea kwa kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu kuwabariki katika maisha yao, katika utumishi wao na katika shughuli zao.

“Tunajua hili ni pengo, Mwanadamu yeyote anapofariki anaacha pengo kubwa ambalo halizibiki lakini pia linaloumiza kwa sababu pia kila mwanadamu ana utambulisho wake, faraja yangu mimi kwenu ni kwamba Mungu yupo pamoja na ninyi,” amesema Mhe. Masaju huku akimsihi Mama Janeth Magufuli kuendelea kuwa imara katika kuisimamia familia huku akimtanguliza Mungu.  

Viongozi mbalimbali waliopata nafasi ya kuzungumza wakiongozwa na Makamu wa Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Nchimbi wamemuelezea Hayati Magufuli kwa mema aliyoyafanya enzi za uhai wake na kutoa rai kwa Watanzania kuyaenzi yote mema aliyoyafanya.

Wakati wa kumbukizi hiyo, Makamu wa Rais ameendesha Harambee maalum ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Parokia ya Mlimani-Chato ambayo ilikuwa ndoto ya Hayati Magufuli ambapo imepatikana Ahadi za jumla ya Shilingi 474,000,000/=.

Shughuli ya Kumbukizi imehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Mawaziri, Viongozi Waastafu, Wanafamilia na Wananchi kwa ujumla.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa neno wakati wa Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 17 Machi, 2026 katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.



Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi (katikati) aliyemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na viongozi wengine wa Serikali wakiwa katika Maadhimisho ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Viongozi wa dini wakiingia tayari kwa ajili ya kuendesha Ibada maalum ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi akizungumza kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 17 Machi, 2026 katika maadhimisho ya Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Picha za makundi mbalimbali ya Viongozi wa Serikali, wa Dini, Wanafamilia pamoja na Wananchi kwa ujumla wakiwa katika Maadhimisho ya Kumbukizi ya Miaka Mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Maadhimisho hayo yamefanyika leo tarehe 17 Machi, 2026 katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje wakiwa katika Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiweka shada la ua katika kaburi la Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ikiwa ni ishara ya kumkumbuka na kumuenzi.  Kulia kwa Jaji Mkuu ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi na baadhi ya Viongozi wengine.


(Picha na Jeremia Lubango, Mahakama)