Jumanne, 16 Juni 2026

MAHAKAMA SUMBAWANGA YAFANYA ZIARA YA UKAGUZI WA MAGEREZA

Na. SHARIFU MOKIWA – Mahakama, Sumbawanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda amefanya ziara ya kutembelea Gereza la Mahabusu Sumbawanga na Gereza la Mollo la Kilimo kwa ajili ya kusikiliza changamoto mbalimbali za wafungwa na Mahabusu wa magereza hayo, ikiwa ni zaira ya ukaguzi wa kawaida katika kipindi cha Juni, 2026.

Akiwasilisha taarifa fupi ya Gereza Kuu la Mahabusu Sumbawanga jana tarehe 15 Juni, 2026 Mkuu wa Gereza Mahabusu Sumbawanga Kamishna Msaidizi wa Magereza ACP Ally M. Abdallah  alieleza hali za wafungwa na mahabusu waliopo gerezani hapo.  

Mhe. Manyanda alipata fursa ya kukutana na Wafungwa na Mahabusu ambao waliwasilisha changamoto zao kwa viongozi mbalimbali wa Mahakama na wadau wengine wa haki jinai alioambatana nao,

Akijibu hoja mbalimbali Mhe. Manyara alielekeza kuharakishwa kwa hatua za upelelezi wa mashauri mbalimbali yanayohusisha Watoto ili kuhakikisha haki inatendeka kwa wakati mapema ipasavyo na wahusika wanapata huduma stahiki kwa mujibu wa sheria.

Aidha, Mhe. Mnyanda, alielekeza kubainishwa kwa changamoto zinazo kwamisha mwenendo wa mashauri ya jinai na kuzitaka kamati za haki jinai kushirikiana kwa karibu katika kuzitatua pamoja na kusukuma mbele mashauri yaliyopo ili kupunguza mlundikano wa mashauri.

Katika risala yao wafungwa na mahabusu katika Gereza la Mahabusu Sumbawanga waliweza kuwasilisha changamoto mbalimbali zinazowakabili gerezani hapo mbele ya Mhe. Manyanda. Aidha, Mhe. Manyanda aliahidi kuzishughulikia changamoto zote zilizowasilishwa katika risala zao na zile ambazo zipo nje ya uwezo kuziwasilisha katika mamlaka husika.

Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Mahabusu Sumbawanga ACP Ally M. Abdallah alitoa shukurani zake kwa ujio wa ziara hiyo, kwa kuwa umekuwa na tija kubwa kwao kwa kutoa fursa kadhaa ikiwemo matendo ya huruma na kushughulikia suala la kupunguza mlundikano wa mahabusu gerezani hapo.

Katika ziara hiyo Mhe. Manyanda aliambatana na Viongozi mbalimbali wa Mahakama akiwemo Mtendaji Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga  Bw. Machumu Essaba, Msaidizi wa Sheria, Mkuu wa upelelezi Mkoa, Kaimu Hakimu Mkazi Mkoa, Hakimu Mfawidhi wa Wilaya, Afisa Ustawi  Mkoa, Mkuu wa Mashtaka Mkoa, Mwakilishi wa Kamanda Takukuru Mkoa, Ofisi ya Upelelezi Mkoa, Afisa Huduma na Uangalizi, Afisa Uhamiaji Mkoa, Mkuu wa Magereza Mkoa na wadau wengine wa Haki jinai.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Mnyanda (katikati) akiwa pamoja na wadau wengingine wa haki jinai wakiwa katika gereza la kilimo Mollo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (kushoto) akipokea risala kutoka kwa Afisa wa Jeshi la Magereza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (mbele ya picha kulia) akiwasili katika ukaguzi wa Gereza la Mahabusu Sumbawanga. 

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)

  

USHIRIKIANO KAZINI NI NYENZO MUHIMU KATIKA KUBORESHA UTENDAJI KAZI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga amesema ushirikiano na mahusiano mazuri kazini ni nyenzo muhimu katika kuboresha utendaji kazi ujumbe huo ameutoa wakati alipotembelea Mahakama zilizopo Mbeya Mjini ikiwa ni kuanza kwa ukaguzi wa kawaida warobo ya nne ya mwaka 2025/2026.

Ziara hiyo iliyofanyika mwanzoni mwa mwezi Juni, kwa kutembelea sehemu ya Mahakama kwa lengo la kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa katika Mahakama hizo na alipata wasaa wa kuzungumza na watumishi wa Mahakama hizo katika vikao vya pamoja vilivyofanywa wakati wa ziara hiyo.

Akizungumza katika vikao hivyo, vilivyofanyika katika ukaguzi huo, Mhe. Tiganga alisisitiza kudumisha nidhamu, ushirikiano na mahusiano mazuri mahala pa kazi ikiwa ni pamoja na ushirikishwaji wa watumishi katika kupanga mambo mbalimbali ya kiutendaji.

“Nasisitiza kudumisha nidhamu na mahusiano mazuri kazini, tuishi kwa upendo na tujifunze kuvumiliana pale inapotokea kupishana baina yetu, tuepuke mambo ambayo hayana ulazima Kutugawa, tusitengeneze ugumu wa kazi kwa kuwekeana vinyongo na vikwazo baina yetu. Pia nawakumbusha kuhusu umuhimu wa ushirikishwaji wa watumishi katika kupanga mambo mbalimbali ya kiutendaji katika ofisi zetu,” alisema Mhe. Tiganga katika ziara yake hiyo.

Mhe. Tiganga aliongezea kwa kusisitiza umuhimu wa kutunza na kulinda rasilimali za Mahakama na kuzingatia hasa vipaumbele vya ofisi kulingana na bajeti zenu kila fedha za matumizi ya ndani zinapoletwa.

Aidha Mahakimu Wafawidhi wa Vituo hivyo alivyotembelea walitoa shukrani zao kwa ziara hiyo na kuahidi kuwa wako tayari kutekeleza yale yote waliyoelekezwa na viongozi wao ili kuboresha utendaji kazi katika vituo vyao na kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Aidha, kupitia taarifa mbalimbali zilizowasilishwa na Mahakimu Wafawidhi wa Vituo mbalimbali alivyotembelea zilieleza juu ya usimamizi wa rasilimali mbalimbali zilizopo, utekelezaji wa majukumu ikiwa ni pamoja na hali ya mashauri katika vituo hivyo.

Sambamba na hilo, Taarifa hizo zilieleza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo katika vituo vyao ambapo wengi wao walieleza hasa kuhusu uhaba wa watumishi hasa kada ya walinzi, uchakavu wa vyombo vya usafiri na uchakavu wa majengo hasa kwa Mahakama za mwanzo.

Katika ziara hiyo Mhe. Tiganga, aliambatana na viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, akiwemo Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo, Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Moses Luoga na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wa pili kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Watoto Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa ndani ya Ofisi ya Mahakama ya hakimu mkazi Mbeya, kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Majala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (katikati walioketi mbele). akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, walioketi mbele, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (watatu kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya wilaya Mbeya katika ukaguzi huo, wanne kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akizungumza kwenye moja ya vikao vilivyofanyika katika ziara hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti (katikati) akizungumza jambo kwenye moja ya vikao katika ziara hiyo.

Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (hayupo pichani) akizungumza kwenye moja ya vikao vilivyofanyika katika ziara hiyo.
Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (aliyekaa mbele)akizungumza kwenye moja ya vikao vilivyofanyika katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (aliyekaa mbele)akizungumza kwenye moja ya vikao vilivyofanyika katika ziara hiyo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)

MAHAKAMA KUU GEITA YAMUAGA JAJI MFAWIDHI MHINA

Na DOTTO NKAJA –Mahakama,  Geita

Uongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjla Ndogo Geita hivi karibuni walifanya hafla ya kumuaga aliyekuwa Jaji Mfawidhi, Mhe. Kevin Mhina, kufuatia uhamisho wake wa kwenda kutekeleza majukumu katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara.

Hafla hiyo ilifanyika Juni 10, 2026, katika Viwanja vya Mahakama Kuu Geita. Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mhina aliwashukuru wote kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote cha utumishi wake. Alisema amefurahishwa na maandalizi ya hafla hiyo na kupongeza mshikamano ulioonyeshwa na Watumishi.

Aidha, aliwahimiza kuendelea kuzingatia maadili ya kazi, ushirikiano, utu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Pia alisisitiza umuhimu wa kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuimarisha utoaji wa huduma za haki na kuifanya Mahakama Geita kuwa mfano katika matumizi ya teknolojia ndani ya Mhimili wa Mahakama.

Kwa niaba ya watumishi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Griffin Mwakapeje, alimpongeza Mhe. Mhina kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Mahakama Geita, hususan katika kusimamia uanzishwaji wa Masjala ya Mahakama Kuu Geita.

Alisema uongozi wake wenye maono, uthabiti na kujitolea umechangia kuimarika kwa huduma za Mahakama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa Wananchi.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alimpongeza Mhe. Mhina kwa juhudi zake katika kuhamasisha na kuendeleza matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Mahakama.

Alisema maarifa, uongozi na moyo wake wa kusaidia wengine vimechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha matumizi ya teknolojia katika uendeshaji wa mashauri, usikilizaji wa kesi na shughuli za kiutawala.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, alisema Mhe. Mhina ameacha alama ya uongozi bora kutokana na malezi ya kitaaluma, msimamo wake katika kusimamia maadili na weledi kazini, pamoja na juhudi zake za kuwajengea uwezo Watumishi.

Alibainisha kuwa uongozi wake umeweka msingi imara wa uwajibikaji, uadilifu na heshima katika mazingira ya kazi, hali iliyochangia kuimarika kwa utendaji wa Mahakama Geita.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa Viongozi na Watumishi mbalimbali kutoa salamu za shukrani na pongezi kwa Mhe. Mhina kwa mchango wake katika maendeleo ya Mahakama Geita, huku wakimtakia mafanikio zaidi katika majukumu yake mapya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina, akitoa shukurani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akimulishakeki Jaji wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna Pamoja na Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Kuu Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya Pamoja na watumishi wa mahakama ya wilaya Geita.

Picha Namba 7. Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chato.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Bukombe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nyanghwale.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Mbogwe.

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


Jumatatu, 15 Juni 2026

SUMBAWANGA YAMPONGEZA KISASILA SAGUDA KWA UTEUZI WA UNAIBU MSAJILI

Na. SHARIFU MOKIWA – Mahakama, Sumbawanga

Watumishi na Viongozi wa Mahakama wampongeza Mhe. Kisasila Saguda kwa kuteuliwa kwake kuwa Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, katka hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga.

katika hafla hiyo maalumu ya kumpongeza Mhe. Saguda iliwakutanisha Watumishi na Viongozi mbalimbali wa Mahakama ili kumpongeza aliyekuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa Sumbawanga kufuatia kuteuliwa kwake kuwa Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania.

Hafla hiyo ilifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Manyanda na ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama pamoja na watumishi kutoka Idara mbalimbali. Miongoni mwa viongozi walioshiriki ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Thadeo  Mwenempazi, Mtendaji  wa  Mahakama  Kuu Masjala Ndogo ya  Sumbawanga,  Bw. Machumu  Essaba,  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala ndogo  ya Sumbawanga  Mhe, Pamela Mazengo  pamoja na watumishi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Saguda alitoa shukrani zake kwa uongozi wa Mahakama kwa imani waliyoionesha kwake kupitia uteuzi huo, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano, upendo na uwajibikaji katika utendaji wa kazi.

“Ushirikiano, upendo na kazi vinakwenda pamoja, hivyo tusiviache nyuma. Napenda kushukuru uongozi wa Mahakama kwa namna ambavyo wameniona nafaa kuchukua nafasi hii ya Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania na ninaahidi kuwa nitahakikisha nachapa kazi kuonyesha kwamba uteuzi walioufanya hawakukosea,” alisema Mhe. Saguda

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Mwenempazi, alimtakia kila la heri Mhe. Saguda katika majukumu yake mapya, akieleza kuwa mafanikio aliyoyapata yametokana na utendaji wake mzuri wa kazi na mahusiano mema na wenzake.

“Tunakutakia kheri katika yote utakayoyatenda katika nafasi yako. Lakini yote uliyokuwa unatufanyia sisi hapa, popote utakapoenda usisahau kuyafanya hivyo, kwani baraka zako zimekuja kwa sababu ya hayo mazuri uliyoyafanya,” alisema Mhe. Mwenempazi.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Manyanda, alitumia fursa hiyo kueleza kanuni muhimu zinazopaswa kuongoza maisha na utendaji wa Afisa wa Mahakama ili kufikia mafanikio katika kazi.

“Kuna kanuni sita ambazo Afisa wa Mahakama akiziishi lazima atafanikiwa; uhuru wa kufanya jambo lolote bila kuingiliwa na bila uoga, kutokuwa na upendeleo, uadilifu ambao ndiyo msingi wa majukumu yetu, mwenekano, usawa pamoja na weledi. Hivyo sote tuzingatie kanuni hizi. Lakini pia namtakia kheri, naamini anaweza, alistahili, anastahili na ataweza. Mwenyezi Mungu aendelee kumuinua zaidi na zaidi,” alisema Jaji Manyanda.

Katika kuonesha kuthamini mchango wake katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Saguda alipokea Kitabu maalum cha kumbukumbu za utendaji kazi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga kutoka kwa Jaji Mfawidhi Mhe. Manyanda. Kitabu hicho kinajumuisha historia ya utendaji kazi wa Mahakama hiyo pamoja na picha na majina ya watumishi wake, ikiwa ni sehemu ya kumbukumbu na ukumbusho wa ushirikiano na mchango wake.

Kwa ujumla, hafla hiyo ilikuwa ishara ya kuthamini utumishi uliotukuka, kujenga moyo wa kufanya kazi kwa bidii na kuhamasisha watumishi wengine kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kujituma kwa manufaa ya taasisi na wananchi wanaohudumiwa na Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Sumbawanga, Mhe Frederick Manyanda (aliyesimama) akitoa Nasaha fupi wakati wa hafla ya kumpongeza Mhe, Kisasila Saguda wakati wa pongezi hizo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mteule Mhe. Kisasila Saguda aliyekuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa Sumbawanga   akitoa Shukrani baada ya kuteuliwa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi akimpongeza na kumtakia kheri Mhe. Kisasila Saguda baada ya Uteuzi huo wa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo (aliyesimama) akitoa neno wakati wa afla hiyo, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga  Machumu Essaba na kushoto ni Mhe Kisasila Saguda aliyeteuliwa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda [kushoto] akimpatia kitabu Mhe. Kisasila Saguda [Kulia] kikiwa na picha na majina ya watumishi wake, ikiwa ni sehemu ya kumbukumbu.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama waliohudhulia katika hafla hiyo maalum ya kumpongeza Mhe. Saguda kwa Uteuzi huo.


JAJI MFAWIDHI MPYA GEITA APOKELEWA RASMI OFISINI

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, tarehe 12 Juni 2026 alikabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus Kahyoza, baada ya kuripoti katika kituo chake kipya cha kazi.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Mhe. Mhina alisema kuwa taratibu zote za kikazi na taarifa muhimu za ofisi zilishakabidhiwa kwa njia ya barua pepe za kikazi.

Aidha, alibainisha kuwa anamwachia Jaji Kahyoza timu ya Watumishi wenye ushirikiano mkubwa na wenye kujituma katika kuhakikisha majukumu ya Mahakama yanatekelezwa kwa ufanisi.

“Nimekuachia Watumishi wenye ushirikiano mzuri sana ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa kujituma na kuhakikisha huduma za utoaji haki zinaendelea kutolewa kwa Wananchi kwa wakati,” alisema Mhe. Mhina.

Kwa upande wake, akizungumza wakati wa kumpokea Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Mwakapeje alimhakikishia ushirikiano wa hali na mali kutoka kwa Watumishi wote wa Mahakama Geita.

Alieleza kuwa Watumishi wa Mahakama hiyo ni wenye maadili mema na wako tayari kushirikiana ili kuhakikisha majukumu ya Mahakama yanaendelea kutekelezwa kwa ufanisi.

Akizungumza baada ya kupokea ofisi, Mhe. Kahyoza aliwashukuru Viongozi na Watumishi wote wa Mahakama Geita kwa mapokezi mazuri aliyoyapata. Alisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano uliopo ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa Wananchi.

“Naomba tuendelee kushirikiana kwa dhati ili kuendeleza mafanikio yaliyopatikana na kuimarisha zaidi utoaji wa haki kwa wakati kwa kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na mawasiliano (TEHAMA),” alisema Mhe. Kahyoza.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alimpongeza Jaji Kahyoza kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuongoza Mahakama Geita. Alimhakikishia kuwa Watumishi wa Mahakama wataendelea kumpa ushirikiano unaohitajika ili kufanikisha majukumu yake mapya.

Mhe. Lukuna pia alieleza kuwa Mahakama Geita itaendelea kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Mahakama kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa Wananchi.

Katika kuonyesha furaha ya ujio wake, Watumishi wa Mahakama Kuu Geita waliandaa keki maalum kwa ajili ya kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya katika kituo chake kipya cha kazi.

Makabidhiano hayo yanaashiria mwanzo wa hatua mpya ya uongozi katika Mahakama Geita, huku yakionesha dhamira ya kuendeleza ushirikiano, ubunifu na matumizi ya teknolojia katika kuimarisha utoaji wa haki kwa Wananchi.

Watumishi wa Mahakama Kuu Geita wakimpokea Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus Kahyoza.

Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus  Kahyoza akisaini kitabu baada ya kuripoti katika kituo chake kipya.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Geita, Mhe Kevin Mhina, akipeana mkono kama ishara ya makabidhiano na Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Projestus Kahyoza.

Picha ya Majaji.

Keki iliyoandaliwa kumkaribisha Jaji Mfawidhi, Mhe. Projestus Kahyoza.

Watumishi wa Mahakama Kuu Geita wakiwa katika kikao kifupi cha kumpokea Jaji Mfawidhi mpya.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.