Jumanne, 28 Aprili 2026

WAJUMBE BARAZA LA WAFANYAKAZI KIGOMA KUWAJIBIKA IPASAVYO

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kutumia kikao hicho kama jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji wa waatumishi katika masuala ya kiutumishi.

Mhe. Rwizile aliyasema hayo hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma wakati akiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Kigoma kilicholenga kujadili ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Jaji Rwizile alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha mahusiano kazini kwa kuzingatia mkataba mpya unaolenga kuboresha maslahi ya mwajiri na watumishi wake.

Jaji Mfawidhi huyo alieleza kuwa, “Baraza hili lipo kisheria na mkataba mpya umejikita katika kujenga Taasisi yetu kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho tunayoyahitaji katika usimamizi wa shughuli za usimamizi wa usikilizwaji mashauri katika Mahakama zetu.”

Hata hivyo, aliwajulisha wajumbe kuwa, kupitia kikao hicho kulikuwa na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza kwa mujibu wa mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi, hivyo aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita amba oni Mhe.  Victor Kagina, aliyekuwa Katibu na Bi. Naomi Chawe aliyekuwa Katibu Msaidizi wa Baraza hilo.

Zoezi la uchaguzi liliongozwa na Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi na shirikishi kwa wajumbe wote kwa  mujibu wa Mkataba.  

Baada ya zoezi la kupiga kura kukamilia, Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Julius Manyanya alichaguliwa kuwa Katibu mpya wa Baraza hilo na  Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Mburalina Maira aliteuliwa kuwa Katibu Msaidizi na Bi. Naomi Chawe alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE Baraza la Wafanyakazi Taifa.

Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa zenye tija zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa watumishi na ufanisi wa utendaji kazi.

Aidha, Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika mjadala, ilisisitizwa kuwa, watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo.

Wajumbe wa Baraza hilo wamesisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2025/2026, huku wakichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia mara tu changamoto zilizobainika ili kutatuliwa.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akitoa neno la ufunguzi wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kigoma kilichofanyika hivi karibuni.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala  Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) akimkabidhi Mkataba wa Baraza la Wafanyakazi Katibu wa Baraza mpya, Bw. Julius Manyanya mara baada ya kuibuka mshindi katika nafasi hiyo kwa kupata kura nyingi za kishindo kutoka kwa wajumbe.


Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kigoma wakifuatilia kwa makini mjadala ulikuwa ukiendelea wakati wa kikao cha Baraza hilo.


Ofisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Festo Sanga akiwasilisha taarifa ya utendaji wa shughuli za kimahakama kwa mwaka 2025/2026.

Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro akitoa ufafanuzi juu ya utaratibu wa uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi wa  Mahakama Kigoma.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

MASHAURI 48 YA MAHAKAMA YA RUFANI KUSIKILIZWA MASJALA NDOGO MBEYA

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Mashauri ya Rufaa 48 ya Ardhi, Kazi na Ndoa yanatarajiwa kumalizika katika kikao cha Uendeshaji wa Mashauri (session) katika Masjala Ndogo ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania mkoani Mbeya.

Kikao hicho kinachoendeshwa na Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, kikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye ambaye ameambatana na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Eliezer M. Feleshi na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Deo J. Nangela, wakisaidiwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Daudi P. Kinywafu pamoja na watumishi wengine wa Mahakama ya Rufani.

Akiongea katika kikao cha mapokezi, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Mkuye aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya unaongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim C. Tiganga kwa maandalizi na mapokezi mazuri. Alifafanua kuwa, ushirikiano kutoka kwa wadau na wahusika, utawezesha umalizaji wa mashauri hayo kama ilivyopangwa.

“Tunawashukuru sana kwa mapokezi na maandalizi mazuri ya kikao hiki kwa hakika tumefarijika sana na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu tunaamini kuwa mashauri haya yote tutayasikiliza bila kikwazo chochote,” alisema Mhe. Mkuye.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ameahidi kutoa ushirikiano kwa kipindi chote ambacho Waheshimiwa hao watakuwepo Masjala Ndogo ya Mbeya kuendesha usikilizaji wa mashauri hayo ya Mahakama ya Rufani.

Kikao cha usikilizaji wa Mashauri hayo kimeanza jana tarehe 27 Aprili, 2026 na kinatarajiwa kuhitimishwa tarehe 22 Mei, 2026.

Mwenyekiti wa jopo la Majaji ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye akisaini katika kitabu cha wageni mara tu baada ya kuwasili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakiwa pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya wakisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili Masjala Ndogo Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho kwa waheshimiwa Majaji hao mara baada ya kuwapokea.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Daudi kinywafu (wa pili kushoto kushoto), Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya Mhe. Aziza Temu (kulia), Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya Mhe. Judith lyimo (wa kwanza kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti wakishiriki mapokezi hayo.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.



WANACHAMA TMJA TAWI LA RUKWA WAFANYA KIKAO KAZI, MAFUNZO

Na. SHARIFU MOKIWA -Mahakama, Sumbawanga 

Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (Tanzania Magistrates and Judges Association (TMJA) Tawi la Rukwa walikutana hivi karibuni na kufanya kikao maalumu kilicholenga kuimalisha ushirikiano wa kitaaluma, kujadili maendeleo ya chama ili kujenga mshikamano miongoni mwa wanachama. Kikao hicho kilifanyika katika ufukwe wa Kasanga ziwa Tanganyika.

Akizungumza wakati wa kufungua kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda alisisitiza umuhimu wa umoja, ushirikiano na ushiriki wa wanachama katika kuimalisha utendaji wa Chama pamoja na utoaji wa haki kwa jamii.

Wakati wa kikao hicho Baraza Tendaji la TMJA Tawi la Rukwa lilipokea taarifa mbali mbali ikiwemo tarifa ya uimarishaji wa Tawi, taarifa ya mwakilishi wa TMJA pamoja na taarifa ya Mhazini wa Tawi ambapo wanachama walipata nafasi ya kujadili maendeleo yaliyofikiwa pamoja na changamoto zinazokikabili Chama.

Aidha, majadiliano mbali mbali yalifanyika na maazimio muhimu kutolewa kwa lengo la kuimalisha Tawi na kuboresha ushirikiano wa wanachama katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Wanachama pia walipata mafunzo maalum kuhusu program ya Mentorship yaliyotolewa na Mhe. Manyanda, mafunzo hayo yalilenga kuongeza uelewa wa kitaaluma, kurejesha utendaji wa kazi pamoja na kujenga mazingira bora ya ushauri na uongozi ndani ya Taasisi.

Vilevile, baada ya kikao na mafunzo wanachama waliendelea na shughuli za utalii katika eneo la Kasanga, hatua iliyosaidia kuongeza ukaribu kujenga mahusiano bora ya kikazi pamoja na kuweka kumbukumbu nzuri za pamoja.

Kikao hicho kilihudhuliwa na   na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo pamoja na Mahakimu wa ngazi mbali mbali.

Picha ya pamoja ya Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Rukwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda akifungua kikao cha TMJA Tawi la Rukwa.

Wanachama wa TMJA Tawi la Rukwa wakiwa kwenye kikao wakifatilia na kusikiliza kwa makini taarifa zilizokuwa zikiwasilishwa.

Mwakilishi wa TMJA Tawi la Rukwa Mhe. David Mbembela (aliyesimama) wa Baraza la TMJA Taifa akiwasilisha taarifa wakati wa kikao

Sehemu ya Wanachama wakiwa katika Fukwe za ziwa Tanganyika ikiwa ni sehemu ya Utalii.

Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Rukwa (kulia) akimpa mkono wa shukrani wakati wa kumuaga Mhe. Elisha Daudi Mwasomola (kushoto) ambaye amehamishiwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe.

Picha ya pamoja ya Wanachama wapya na waliohamia (TMJA) Tawi la Rukwa.                             


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Masjala ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi (kulia) wakikata keki iliyoandaliwa na Chama cha (TMJA )Tawi la Rukwa.

  





 

Jumatatu, 27 Aprili 2026

WATUMISHI MAHAKAMA KUU DODOMA WALIPATIWA ELIMU KUHUSU AFYA YA AKILI

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma, hivi karibuni walipatiwa elimu muhimu kuhusu afya ya akili na ustawi wa maisha, iliyogusa moja kwa moja maisha yao ya kazini na nyumbani.

Elimu hiyo ilitolewa katika Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma na Jaji wa Mahakama Kuu kutoka Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale.

Mbali na majukumu yake ya kusikiliza mashauri mkoani Dodoma, Mhe. Ngunyale aliona vyema kutumia nafasi hiyo kuwajengea uelewa Watumishi hao kwenye eneo hilo.

Kabla ya kuanza zoezi hilo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, alimpongeza Jaji Ngunyale kwa moyo wa kujitoa na upendo wa dhati aliouonesha kwa Watumishi hao, akisisitiza kuwa afya ya akili ni msingi muhimu wa utendaji bora na maisha yenye mafanikio.

Kupitia elimu hiyo, Watumishi walipata fursa ya kujifunza kwa kina viashiria vya afya ya akili, mbinu za kukabiliana na changamoto za kisaikolojia pamoja na namna ya kujijenga kiakili na kitaaluma.

Si hivyo tu, mada ya uongozi bora (leading skills) iliyotolewa wakati wa zoezi hilo la utoaji elimu iliongeza chachu mpya kwa washiriki wengi, ikiwapa mwanga wa kuwa Viongozi bora katika nafasi zao na katika jamii.

Kilichovutia zaidi ni namna atumishi walivyoshiriki kwa hamasa kubwa, wakionesha wazi kufurahishwa na elimu hiyo ambayo waliieleza kuwa imewafungua macho na kuwapa mwelekeo mpya wa maisha.

Walimshukuru Jaji Ngunyale kwa kuwapatia maarifa yenye tija na yenye kugusa uhalisia wa maisha yao ya kila siku.

Zoezi hilo lilihudhuriwa na Watumishi mbalimbali ana kwa ana wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt Fatma Khalfan, pamoja na wengine waliounganishwa kwa njia ya mtandao kutoka wilayani, jambo lililoongeza ushirikishwaji na kuifanya elimu hiyo kuwafikia wengi zaidi kwa wakati mmoja.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo (aliyesimama) akimkaribisha Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale, aliyepo kulia kwake, ili kuwapa elimu Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma. Kushoto kwake ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Bw. Bedson Mariba.



Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma wakiskiliza kwa makini elimu ya Afya ya Akili kutoka kwa Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale (hayupo pichani).


 Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale akitoa somo kuhusu afya ya akili kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Simiyu.

 

 

Jumapili, 26 Aprili 2026

JAJI MKUU MASAJU AHUDHURIA IBADA YA SHUKRANI KUMBUKIZI YA KUZALIWA BI. LOYCE NYALALI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 26 Aprili, 2026 amehudhuria Ibada maalum ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.

Ibada hiyo maalum ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai imefanyika katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro Oysterbay jijini Dar es Salaam ikiongozwa na Paroko wa Kanisa hilo, Padri Bartholomew Mrosso na Padri mwenzake.

Katika mahubiri yake wakati wa ibada hiyo, Padri Mrosso ametoa rai kwa Waumini kumshukuru Mungu kwa uzima kwa kuwa uzima ni zawadi kubwa ambayo kwayo yatupasa kumshukuru Mungu. Amesisitiza kwa kusema, “tumshukuru Mungu kwa uzima kwanza halafu vingine ndio vifuate.”

Kadhalika Padri huyo, amewakumbusha Viongozi kusimamia haki, na kutenda mema kwa walio chini yao na wanaowaongoza.

“Katika Injili ya Jumapili ya leo ya Mchungaji Mwema msingi wake ni Uongozi, namna fulani ya Uongozi ambao Kristo anaudhihirisha kupitia matendo yake mema,” ameeleza.

Ameongeza kuwa, Kiongozi anapaswa kusimama kwa ajili ya wale anaowaongoza hivyo, Uongozi usichukuliwe kama ajira bali kujitoa na kuwajali watu waliopo chini.

Ibada hiyo imehudhuriwa pia na baadhi ya Viongozi wakiwemo Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba, Majaji Wastaafu wa Mahakama Rufani na Mahakama Kuu, Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakili Tom Nyanduga, Wenza wa Majaji Wakuu Wastaafu akiwemo Mama Marina Juma, Mama Sada Chande pamoja na ndugu, jamaa na marafiki na wageni wengine waalikwa.

Baada ya ibada hiyo, imefanyika sherehe maalum ya kumpongeza Bi. Loye Nyalali iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Kadinali Rugambwa uliopo pembeni ya Kanisa la Mt. Petro jijini Dar es Salaam.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kushoto mwenye tai nyekundu) akiwa katika misa ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, marehemu Francis Nyalali. Ibada hiyo imefanyika leo tarehe 26 Aprili, 2026 katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro jijini Dar es Salaam. Kulia kwa Jaji Mkuu ni Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba na aliyeketi mbele ni Mama Loyce Nyalali anayeadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimsalimia na kumpongeza Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.
 
Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiingia ndani ya Kanisa Katoliki la Mtakatifa Petro lililopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya ibada maalum ya kumshukuru Mungu kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiwa katika uso wa furaha ikiwa ni siku yake maalum ya kuadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Stephen Bwana (kushoto) pamoja na mwenza wake (katikati) na wengine wakiwa katika ibada ya shukrani maalum kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Paroko wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro, Padri Bartholomew Mrosso akiongoza ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Mama Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.


Picha mbalimbali za matukio ya Ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)