Jumatano, 17 Juni 2026

‘ZINGATIENI MASLAHI YA UMMA, TAIFA KWA KULINDA HESHIMA, UHURU WA MAHAKAMA’

·       Jaji Mkuu awataka Naibu Wasajili wapya kuwajibika ipasavyo

·       Awataka kusimamia ipasavyo utekelezaji wa hukumu

·       Jaji Mkuu awataka kuimarisha ushirikiano na watumishi walio chini yao

·       Awataka pia kusimamia Masjala Ndogo za Mahakama Rufaa na kuandaa vema kumbukumbu za rufaa

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Naibu Wasajili wapya 31 kuzingatia maslahi ya umma na ya Taifa katika kulinda, kutunza heshima, mamlaka na uhuru wa Mahakama kama unavyotajwa katika Ibara ya 30(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma alipokuwa akizungumza na Naibu Wasajili wapya 31 walioapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

“Tunapotambua kwamba mnazo sifa za kuwa Viongozi na Tume tukawateua nendeni mziishi hizo sifa, lakini pia tambueni tunaishi wakati gani, ni wakati ambao unasisitizwa sana uwajibikaji na hatuwezi kuwa tu tunafurahia kuteuliwa. Kila nafasi ya uongozi na kila nafasi ya mafanikio inakuja na wajibu mkubwa kwa mhusika,” amesema Jaji Mkuu.

Amewataka Naibu Wasajili hao kutambua kuwa, Mahakama ya Tanzania inawategemea kwa kuwa wao ni kada muhimu na ndio Meneja na Injini ya shughuli za kila siku za Mahakama katika ngazi zote kuanzia Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Wilaya, Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani.

“Ingawa mtapatiwa mafunzo elekezi, matarajio ni kwamba tayari mna ufahamu wa majukumu yenu kutokana na uzoefu mlio nao hususan kwa wale ambao wamewahi kukaimu nafasi hizi lakini hata wale waliokuwa Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi ngazi ya Mkoa, ngazi ya Wilaya na mambo ni yaleyale kwa mfano masuala ya ‘execution’ kama Naibu Wasajili ninyi ndio wapishi au waratibu Wakuu wa shughuli za kimahakama, ninyi ni Mameneja na Injini ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika amewataka Wasajili hao wa Mahakama kusoma sheria mbalimbali zinazoelezea majukumu yao ili wawe katika nafasi nzuri ya kutekeleza majukumu yao ya kila siku ipasavyo huku akisema kuwa, “jitambueni na muwajibike kama Viongozi katika maeneo yenu ya kazi, jitoleeni kwa moyo wote ili kuleta ufanisi katika Vituo vyenu na kwa Mahakama kwa ujumla, kuweni na ari, ubunifu na utayari wa kutatua changamoto zinazojitokeza katika maeneo yenu ya kazi, leteni Makao Makuu ya Mahakama changamoto zilizo nje ya uwezo wenu badala ya kusubiri vikao ndipo muwasilishe hizo changamoto.”

Kadhalika, Mhe. Masaju amewataka Naibu Wasajili hao kuimarisha ushirikiano na Watumishi wa Kada nyingine waliopo chini yao. “Kwenye ngazi ya Mkoa au Kanda wapo Watendaji wa Mahakama lazima muwape ushirikiano ipasavyo, tumegawana majukumu ninyi mnashughulika na shughuli za kimahakama, wenzetu wanashughulika na shughuli za kiutawala lakini ushirikiano ni jambo la lazima, kuhusu suala ya kutunishiana misuli lazima mshirikiane, mheshimiane kwa sababu mafanikio yetu yanategemea tunashirikiana namna gani,” amesema Jaji Mkuu.

Amesema kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja ambacho amekaa Mahakamani amebaini kuwa, watumishi wanawasikiliza Viongozi lakini kumekuwa na changamoto ya kutokuchukua hatua wakidhani mambo hayo yanatekelezwa na waliopo Makao Makuu pekee wakidhani kuwa wao hawahusiki, hivyo amewataka kubadilika na Uongozi watawapima ipasavyo.

Aidha, amewataka Naibu Wasajili hao kutumia vizuri kipindi cha miezi sita ya uangalizi (Probation) kwa kuwajibika, na kwamba wao kama Viongozi watakuwa wanawafuatilia kwa karibu kwa sababu nia yao ni njema hawawaangalii kwa karibu ili kuwaadhibu bali waendelee kupanda katika vyeo vya juu zaidi.

“Sasa hivi kuna nafasi zipo kwa ajili ya Majaji wa Mahakama Kuu, tunataka kadri tunavyostaafu na wengine wanavyopanda kwenda Mahakama ya Rufani, wengine wanaziba zile nafasi, ninyi mmeshaaminiwa na tungependa hao Majaji watokane na ninyi, na ndio maana tunasema kwamba ile Mahakama ya Mkoa itakapokuwa imeanzishwa itakuwa ndio Kituo cha Mafunzo cha kuwaandaa ninyi kuteuliwa kuwa Majaji na mimi kitu ninachokizingatia sana ni uadilifu na uwezo wa kumudu majukumu kwa ufanisi ipasavyo, kwahiyo tutakapokuwa tunawaangalia kwa namna ya kuwalea  ili kuwaandaa kushika majukumu makubwa zaidi sio kwa maana ya kutaka kuwaadhibu,” ameeleza Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, moja ya majukumu ya Naibu Wasajili ni usimamizi wa masjala na hilo ndilo jukumu kubwa, hivyo wao kama injini ya Mahakama na meneja wa masjala wanapaswa kufahamu vema mwenendo wa masjala zilizopo chini ya usimamizi wao.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewataka Naibu Wasajili hao kudhibiti na kupunguza mlundikano wa mashauri katika Masjala zao huku akiwataka kushughulikia ipasavyo mashauri ya mirathi na mashauri ya watu wengine dhaifu katika jamii (vulnerable groups) yanashughulikiwa na kuhitimishwa mapema ipasavyo na kwamba zipo kanuni zilizotungwa na Jaji Mkuu kwa ajili hiyo.

“Na ni kwa sababu hiyo nimewasomea Zaburi ya 82:2-4, kwa hiyo sio suala la Zaburi tu, hata sisi tumetambua; zipo kanuni zilitungwa na Jaji Mkuu kwa ajili ya kuzingatia makundi hayo, hivyo mashauri ya mirathi na mengine ya aina hiyo yanayohusu watoto, masuala ya ndoa na masuala mengine, mmeshika hapa misaafu wengine Biblia, mimi ningependa kipimo chenu kiwe ni kwa namna gani mnamtendeka haki huyu mtu ambaye ni maskini, wajane, watoto na hasa wanaochukuliwa kuwa dhaifu kutokana na hali yao katika jamii. Haina maana tutawapendelea hapana lakini tusiwadhulumu haki zao kwa sababu ya hali zao,” amesema.

Mhe. Masaju ametoa rai kwa Wasajili hao kuendelea kuwa wanyenyekevu, huku akisema kuwa, kipimo cha mtu kipo katika mambo mawili, mosi anapopata mali na anapopata Madaraka.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amewataka Naibu Wasajili hao kuwasimamia vizuri Mahakimu wa Mahakama za Wilaya na kuhakikisha pia wao nao wanawasimamia vizuri Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo.

“Tutatengeneza vigezo vya kuwapima kwenye miezi hii sita, na ni pamoja na kigezo hiki cha ni kwa namna gani mnazisimamia hizo masjala zilizopo chini yenu, kuna ufanisi kiasi gani kwahiyo haya yaangalieni sana.

Aidha, Mhe. Masaju amewataka Naibu Wasajili hao kuimarisha usimamizi na ukaguzi wa shughuli za kimahakama ili kubaini na kuondoa vikwazo vinavyochelewesha usikilizaji wa mashauri.

“Kama Majaji wenu huko watakuwa na changamoto, tujulisheni lakini hatutaki tushindwe kufanya vizuri kule kwenye Kanda kwa sababu tu ya udhaifu wetu sisi yaani ninyi Wasajili, tekeleza wajibu wako ya Jaji tutayajua tu sisi huku lakini wewe ukiwa umetekeleza wajibu wako. Chukueni hatua haraka pale panapotokea mkwamo katika usikilizaji wa mashauri, lizingatieni sana hili,” amesema.

Vilevile, Jaji Mkuu amesema, usimamizi wa uandaaji wa kumbukumbu za rufaa ni moja ya majukumu ya Naibu Wasajili na hasa rufaa zinazokuja Mahakama ya Rufani, hivyo Wasajili wanaofanya kazi katika Mahakama Kuu watambue kuwa Masjala Ndogo za Mahakama ya Rufani zilizopo katika majengo ya Mahakama Kuu ni za kwao na hivyo majukumu yanayopaswa kutekelezwa katika Masjala Ndogo hzio yanawahusu moja kwa moja.

“Baadhi ya Wasajili wanajiona kama sio wajibu wao kuandaa kumbukumbu za rufaa, kwahiyo hawajishughulishi kwa ufanisi ipasavyo na uandaaji wa hizi rufaa, sasa zinaandaliwa kwa namna ambayo wakati fulani hazikidhi kile kilichotegemewa na matokeo yake inasababisha haki kuchelewa kwahiyo hatutaki kuliendekeza na hatutavumilia ucheleweshaji wa kumbukumbu,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Mahakama itachukua hatua ipasavyo, “na hivi ninavyozungumza nipo katika hatua za kukamilisha marekebisho ya kanuni, tutaweka na muda (timeline) unapaswa kuwa umekamilisha kuandaa kumbukumbu za rufaa na ziwe zimeandaliwa kwa ufanisi ipasavyo zisije zikachelewesha haki kutendeka, hatutavumilia ucheleweshaji wa kumbukumbu za rufaa” amesema Mhe. Masaju.

Vilevile, amewataka Wasajili hao kusimamia ipasavyo utekelezaji wa hukumu za Mahakama kwakuwa eneo hilo lina changamoto huku akisisitiza kwa kusema kuwa, “kuweni makini, na waadilifu katika utekelezaji wa hukumu.”

Aidha ameeleza kuwa, pamoja na kuwepo kwa vitendea kazi vya kawaida kama vile viti, meza majengo na kompyuta vipo vitendea kazi vingine ambavyo ni uwajibikaji kama unavyoelezewa katika Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, uadilifu kama unavyoelezwa katika Sheria za Utumishi wa Umma, kuwiwa kuona haki inatendeka na kuitenda ipasavyo, uwezo wa kumudu utendaji kazi wa majukumu ya kila siku, kujituma, ubunifu katika kutatua changamoto, kuzingatia maslahi ya Umma na Taifa pamoja na kuzingatia ukweli na uhalisia bila kupendelea upande wowote.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amesema kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kuwa na mchango mkubwa na wa pekee katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ambayo inasisitiza kuhusu utawala bora na amani ya jamii, Naibu Wasajili hao watambue kuwa taifa haliwezi uwa na na maendeleo bila kuwa na amani hivyo wanapaswa Kutenda wakizingatia utawala wa sheria kama ilivyoelezwa katika Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Vilevile Mhe. Masaju amewataka Naibu Wasajili hao kuendelea kuwaheshimu wake na waume zao bila kujali dhamana na cheo walichokipata “endeleeni kuwa waadilifu kwa wenza wenu, msiwadharau wenza wenu kwa ajili ya vyeo mlivyovipata” amesisitiza Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Naibu Wasajili wapya leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama mara baada ya Wasajili hao kuapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Naibu Wasajili wapya walioapishwa leo tarehe 17 Juni, 2026 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakifuatilia kwa umakini hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).



Sehemu ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na wageni wengine waliohudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya wakifuatilia hotuba iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).

Sehemu ya Naibu Wasajili wapya kati ya 31 wakila kiapo kushika wadhifa huo mbele ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto). Uapisho huo umefanyika leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya 31 walioapishwa leo tarehe 17 Juni, 2026 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wapya (waliosimama) walioapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania (waliosimama) ambao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Naibu Wasajili wa Mahakama (waliosimama) ambao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (waliosimama) ambao nao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya ndugu, jamaa na marafiki (waliosimama) wa Naibu Wasajili wapya waliopishwa  ambao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiteta na kufurahia jambo na mtoto ambaye naye ameshiriki katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama)











JAJI KIONGOZI AWATAKA NAIBU WASAJILI WAPYA KUTOBWETEKA

Na HABIBA MBARUKU- Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewataka Naibu Wasajili wapya 31 kutobweteka na kutowaangusha Viongozi waliowaamini kutekeleza jukumu la utoaji haki kupitia nafasi hizo.

Mhe. Siyani ameyasema hayo baada ya kuwaapisha Naibu Wasajili hao leo tarehe 17 Juni, 2026 katika Ukumbi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

“Sisi tunaofanya kazi katika Mahakama ya Tanznaia ni Watumishi wa Serikali. Nafasi tunazozipata, ziwe ni nafasi za ajira au nafasi za uongozi kama hizi, ni nafasi ambazo wenzetu wengi zaidi ya milioni 60 hawajabahatika kuzipata, ni nafasi ambazo zinabeba dhamana kubwa, kwa hiyo nitumie nafasi hii kuwasihi sana kutobweteka,” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Ameongeza kuwa Naibu Wasajili wa Mahakama ndio injini, moyo na uhai wa Mahakama, hivyo watakapokwenda katika maeneo ambayo watapangiwa watambue kuwa wamebeba matarajio ya wale waliowaamini, kwa niaba ya Watanzania wote.

Amesema kuwa katika Taasisi, zipo changamoto ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu na kwamba wao wanatarajiwa kwenda kuzifanyia kazi, huku akibainisha moja ya changamoto inayoikabili Mahakama ni watu kutoridhika na huduma za Mahakama, licha ya uwepo wa takwimu zinazoonesha kuridhika kwa Wananchi, hivyo wanapaswa kuwajibika bila kubweteshwa na takwimu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Siyani amewataka Naibu Wasajili wapya kufanya kazi bila hofu, huku wakitenda haki, kwa kuzingatia Katiba, Sheria mbalimbali, mila na desturi pamoja na maelekezo ya Viongozi. Amewaeleza kuwa wasiwe na hofu katika kutekeleza majukumu yao kwa sababu wanatarajiwa kwenda kuwahudumia watu, na wanapaswa kuwa na hofu na Mungu pekee ambaye wameapa kwake.

“Msiende kupeleka hofu zenu kazini, mnatarajiwa kwenda kuwahudumia watu na mkiwa na weledi hakuna sababu ya kuwa na hofu, timizeni majukumu yenu vile inavyotarajiwa, hofu itawafanya mkosee, hofu yenu iwe kwa Mungu ambaye mmeapa kwake, msipoweza kudhibiti hali hiyo mtakosea. Katika zama tulizonazo haitajariwi Maaoisa wenye hadhi yenu kufanya makosa yasiyotarajiwa….mkachape kazi,” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Ameongeza kuwa miezi sita ijayo itakuwa miezi ya matazamio, hivyo wakienda kubweteka watakosa sifa za kuendelea kuwa Naibu Wasajili kwa sababu uvivu na ukosefu wa weledi ni vitu ambavyo havina nafasi ya kuvumiliwa katika nyakati za sasa na kuwa kila mtu atapimwa kwa haki juu ya namna anavyofanya kazi.

Jaji Kiongozi amewatakiwa kila la heri, huku akiwakumbusha kuiishi kauli mbiu ya Mahakama inayosema, “Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji,” akieleza kuwa mambo hayo matatu ndio masingi wa utendaji ulio imara.

Amesema kwamba atakayekosa uadilifu, weledi na kushindwa kuwajibika atakuwa amepoteza sifa ya kuwa Naibu Msajili, hivyo wawe kundi la mageuzi na kundi ambalo litaleta taswira ya kuwa hakukuwa na makosa kwenye kuweka imani kwao.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza baada ya kuwaapisha Naibu Wasajili hao leo tarehe 17 Juni, 2026 katika Ukumbi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

Sehemu ya Naibu Wasajili wapya wakimsikiliza Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, baada ya kuwaapisha.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).


Sehemu ya Wananchi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).


Sehemu nyingine ya Wananchi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).


Sehemu nyingine ya tatu ya Wananchi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).

Picha na Mary Gwera na Halima Mnete-Mahakama, Dodoma.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

JAJI MFAWIDHI AHITIMISHA ZIARA YA UKAGUZI MBEYA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya.

·        Amepongeza jitihada zinazofanywa kulinda miundombinu ya Mahakama mpya za mwanzo.

·        Amepongeza Serikali za Kata na Vijiji kwa ushirikiano wao katika kuboresha miundombinu ya Mahakama kwa kusaidia ukarabati na hata kutoa Majengo yao kwa matumizi ya Mahakama.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga amehitimisha ziara ya siku kumi za ukaguzi ulioanza mwanzoni mwa mwezi Juni 2026 kwa kutembelea Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo Mbarali, Chunya, Kyela na Rungwe zilizopo Masjala Ndogo ya Mbeya.

Lengo la ukaguzi huo ni kukumbushana juu ya majukumu ya kila siku, kubaini, mapungufu na changamoto na kuona mapendekezo ya njia sahihi za kukabiliana na changamoto hizo.

Katika vikao mbalimbali vilivyofanyika wakati wa ziara hiyo Mhe. Tiganga aliwasisitiza watumishi kuongeza kasi katika usikilizwaji wa mashauri, kudumisha nidhamu kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma na kudumisha ushirikiano kazini.

“Ninawapongeza kwa kuendelea kudumisha nidhamu, tuendelee kuchapa kazi, tutunze maadili yetu na ninawapongeza kwa kazi nzuri mnazozifanya na ninawatakieni kila la heri katika utekelezaji wa majukumu yenu,” alisema Mhe. Tiganga.  

Aidha, Mhe. Tiganga alizipongeza Serikali za Kata na vijiji na wananchi wa maeneo hayo kwa ushirikiano wao mzuri kwa kuisaidia Mahakama kutekeleza majukumu yake ya kutoa haki kwa wakati ikiwa ni pamoja na kusaidia katika harakati za ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Makongorosi iliyopo wilaya ya Chunya na kupatiwa Jengo kwa ajili ya matumizi ya Mahakama ya Mwanzo Ilongo wilayani Mbarali.

Katika ziara hiyo Mhe. Tiganga aliongozana na viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya ambao ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawad Laizer.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) akiwa kwenye picha ya Pamoja na watumishi wa mahakama ya Wilaya Rungwe

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) akiwa kwenye picha ya Pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chunya.

Sehemu ya watumishi wakimsikiliza Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (hayupo pichani) akiongoza kikao katika ziara hiyo ya ukaguzi.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wa tatu kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na watumishi wa mahakama ya mwanzo Chimala –Mbarali



Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, wakipanda mti wa matunda kwa Pamoja katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Madibira- Mbarali.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (watatu kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na watumishi wa mahakama ya mwanzo Madibira –Mbarali

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akipanda mti wa matunda katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Madibira- Mbarali.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti akipanda mti wa matunda katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Ndobo Kyela.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (aliyesimama) akizungumza jambo kwenye moja ya vikao katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akiongoza kikao katika ziara hiyo ya ukaguzi.



Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akisaini kitabu cha wageni na baadae akiongoza kikao katika ziara hiyo ya ukaguzi.