Jumamosi, 18 Aprili 2026

ENDELEENI KUWA WANYENYEKEVU HATA BAADA YA MAFANIKIO: JAJI MKUU

Na WAANDISHI WETU, Mahakama -Serengeti Mara

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. George Masaju, amewataka waumini wa Kanisa la Waadventista Wa Sabato na Watanzania wote kwa ujumla kuendelea kuwa wanyenyekevu hata baada ya kubarikiwa na kupata mafanikio, hivyo wanapaswa kuendeleza uhusiano wao mzuri na Mungu.

Mhe. Masaju ameyasema hayo akiwa Mgeni Maalum katika Hafla ya Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wa Sabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati, iliyofanyika leo tarehe 18 Aprili, 2026 katika Kijiji cha Musati Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.

“Ninayo furaha kubwa sana leo kukutana nanyi, jambo hili ni kubwa wengi wetu Mungu anapotubariki tunakuwa na kiburi kwahiyo hatua hii inaonesha jinsi ambavyo Mhe. Dkt. Nyansaho alivyo mnyenyekevu,”amesema Jaji Mkuu. 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Mhe. Masaju ametoa pongezi kwa waumini wa kanisa hilo pamoja na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho, ambao kwa dhati wameshiriki katika ujenzi wa kanisa hilo sambamba na kuendesha zoezi la kuchangia ujenzi wa shule na zahanati kijijini hapo.

Aidha, Jaji Mkuu amesisitiza kuhusu umuhimu wa kufanya kazi na kuwataka watu wafanye kazi kwa bidii wakijishughulisha na shughuli halali kama kilimo, uvuvi na ufugaji huku wakiilinda amani kwa sababu amani ikitoweka watu hawataweza kufanya shughuli nyingine za kiuchumi na kijamii.

Ameongeza kuwa uwepo wa kanisa hilo utasaidia katika kujenga jamii yenye umoja na amani kwani maovu yatakemewa jambo litakalohakikisha uwepo wa amani, usalama, ulinzi wa maadili pamoja na ulinzi wa mila na desturi za Kitanzania.

Kanisa hilo ambalo limezinduliwa na Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Hamis Ulega (MB) ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika hafla hiyo. 

Ujenzi wa Kanisa hilo umegharimu kiasi cha shilingi za kitanzania milioni 500.

Aidha katika Hafla hiyo, imeendeshwa harambee maalum ya kuchangia ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati ambapo Jaji Mkuu ameshiriki pia kuchangia katika zoezi hilo. 

Pamoja na Jaji Mkuu hafla hiyo ilihudhuriwa na Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Hamis Ulega (MB), aliyekuwa Mgeni Rasmi, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Jacob John Mkunda, Wakuu wa Mikoa ya Mara na Tabora, Wakuu wa Wilaya za mkoani Mara, baadhi ya Wabunge wa Mkoa wa Mara, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wilaya, Madiwani, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mara, Viongozi mbalimbali na Wananchi kwa ujumla ambao mwenyeji wao alikuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho. 

Mgeni Rasmi Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega (MB) (wa nne kushoto) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara. Kushoto kwake ni Mgeni Maalum Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, mwenye shati jeupe ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho pamoja na Viongozi wengine walioshiriki katika hafla hiyo.

Zoezi la uzinduzi wa Kanisa likiendelea.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.




Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akipokelewa katika viwanja vya Kanisa jipya ya Waadventista Wasabato alipowasili kushiriki katika Hafla ya Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.  











 Matukio mbalimbali katika picha Hafla ya Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara. 


MAHAKAMA DAR ES SALAAM YAOKOA ZAIDI YA MILIONI 60 KUTOKA KATIKA MATUMIZI YA KARATASI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam imefanya tathmini ya matumizi ya karatasi na matumizi ya kieletroniki na kubaini kuwa, imefanikiwa kuokoa zaidi ya Shilingi Milioni 64.

Hayo yamebainishwa jana tarehe 17 Aprili, 2026 katika Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Hatua hiyo ni moja ya Yatokananyo ya kikao kilichofanyika tarehe 18 Julai, 2025 ambapo moja ya maazimio ilikuwa ni kutathmini gharama zilizokuwa zinatumika kununua karatasi, wino pamoja na kalamu kabla ya Mahakama kuachana na matumizi ya karatasi (paperless) na kutumia njia ya mtandao.

Akitoa mchanganuo Mahakama Kuu pekee, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti amesema Mahakama hiyo imefanikiwa kuokoa shilingi 21,418,724/= kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2024/2025.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam imeokoa shilingi 21,496,555/= ikijumlisha na Mahakama zake zote za Wilaya yaani Ilala, Temeke na Kigamboni.

Kwa upande wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Bw. Manoti amesema imefanikiwa kuokoa shilingi 16,653,508 pamoja na Mahakama zake za Wilaya yaani Kinondoni na Ubungo.

Ameongeza kuwa, Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani imeokoa kiasi cha shilingi 9,200,000/= pamoja na Mahakama zake za Wilaya yaani Kibaha, Bagamoyo, Kisarawe, Mkuranga, Rufiji, Kibiti na Mafia.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amewapongeza Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Kanda hiyo na kueleza kuwa, amepokea pia pongezi kutoka Gereza la Mahabusu Segerea kwa utendaji kazi mzuri wa Kanda hiyo na kueleza kuwa, pongezi hizo sio zake ni za Wafawidhi maana wao ndio wana mashauri hayo na wamejitahidi kuyaondoa. Pamoja na pongezi hizo amewataka kukaa kwa amani.

Aidha, Mhe. Maghimbi amewatahadharisha wajumbe hao kuwa kuna viashiria vya mlundikano wa mashauri kukaribia hivyo, amewaomba kujitahidi kuyafanyia kazi mashauri hayo ili kuondokana na mlundikano ambao umekuwepo kipindi cha nyuma lakini kwa juhudi na mshikamano walifanikiwa kuyaondoa kabisa hivyo yasije kurudi tena. 

“Mwanzo wa mwaka waanze ndio wakati wa kupanga mikakati jinsi gani umeyazuia, unayachukua hayo yenye viashiria unayafanyi kazi vikao vya kuyasukuma ili mmalizane nayo,” alisema Jaji Maghimbi.

Katika jitihada za kuhakikisha huduma za Mahakama zinasogezwa karibu na wananchi, Jaji Mfawidhi huyo amewataka Wafawidhi kupitia Uongozi wa Serikali za vijiji kuomba kupatiwa viwanja vya kujenga Mahakama za Mwanzo kwa Kata zilizopo katika maeneo yao. Baadhi ya Wilaya ambazo tayari zimeshapata viwanja. Mhe. Maghimbi amewataka kufuatilia hati za maeneo hayo.

Sambamba na kikao hicho wajumbe wamepata fursa ya kujifunza kuhusu Mfuko wa Wekeza Maisha (UTT AMIS) na kujua faida zinazopatikana kupitia mfuko huo.

Miongoni mwa maazimio ya kikao hicho ni pamoja na kuandaa  ya uandishi wa muhtasari  wa vikao, Dira ya Taifa ya 2050 na huduma kwa wateja kwa Maofisa Mahakama Kanda ya Dar es Salaam, Kanda kuandaa mafunzo maalum kwa Maofisa  wa Mahakama  kwa ajili ya kuwajengea uwezo katika kusikiliza mashauri na uandishi wa hukumu, Mahakimu Wafawidhi kuwajulisha Mahakimu walio chini yao pamoja na Watendaji juu ya umuhimu wa  takwa la kisheria la kufungua akaunti maalum ya Mirathi, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, Maofisa Utumishi na Maofisa Tawala kufuatilia upatikanaji wa viwanja na hati kwa ajili ya Kata ambazo hazina Mahakama za Mwanzo.

Wajumbe wa Kikao cha Menejimenti cha Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam  wakifuatilia kikao hicho kilichofanyika jana tarehe 17 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni.

Baadhi wa wajumbe wa kikao cha Menejimenti wakifuatilia somo kwa meneja masoko wa mfuko wa uwekeza wa Pamoja (UTT) Bi. Paskazia Charles (hayupo pichani).


Meneja Masoko wa Mfuko wa Wekeza Maisha (UTT) Bi. Pakazia Charles  akiwapa somo wajumbe wa Kikao cha Menejimeneti cha Mahakama Kanda ya Dar es Salaam.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikao cha Menejimenti, Mhe. Salma Maghimbi (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Livin Lyakinana (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu kanda ya Dart es Salaam, Bw. Sumera Manoti wakiwa katika kikao hicho.

Meza kuu wakiwa na katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam. Kutoka kushoto waliosimama ni Mhe. Aziza Mbadjo, Mhe. Hussein Mushi na  Mhe. Franco Kiswaga. 

 Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Kada mbalimbali wa Makhakama Kanda ya Dar es Salaam ambao ni wajumbe wa Kikao cha Menejimenti.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara)

Ijumaa, 17 Aprili 2026

MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO SIMIYU YASHIRIKI MAADHIMISHO YA WIKI YA USULUHISHI

  •   Yawaelimisha Wadau wa Mahakama umuhimu wa Usuluhishi kupitia Kongamano maalum

Na NAUMI SHEKILINDI, Mahakama-Simiyu

Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Simiyu nayo imeungana pamoja na Mahakama nyingine nchini kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi nchini iliyoanza tarehe 14 Aprili, 2026 na kufikia tamati tarehe leo tarehe 17 Aprili, 2026.

Katika Maadhimisho hayo, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu imefanikiwa kufanya kongamano la Usuluhishi tarehe 16 Aprili, 2026 likiongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Hussein Mtembwa pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo Watumishi wa Mahakama, Polisi, Taasisi za kibenki, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Uhamiaji, Wakala wa Vipimo, TUGHE, Viongozi wa dini na wananchi.

 Mhe. Mtembwa alifungua kongamano hilo na kueleza kuwa lengo la Wiki ya Usuluhishi ni kupunguza muda wa mashauri mahakamani, kupunguza gharama za mashauri na kuwezesha suluhu ya haraka na ya kirafiki, “Mfano benki wanapofanya usuluhishi baina ya benki na mteja inajenga mahusiano mema na ya kirafiki baina ya benki na mteja” amesisitiza Jaji Mtembwa.

Aidha, Mhe. Mtembwa aliongeza kwa kusema, “Haki sio tu kuhukumu bali pia kusuluhisha,” alieleza kuwa usuluhishi una mchango mkubwa katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwani amani, usalama na utulivu ndio msingi utakaojenga umoja ndani ya nchi, vilevile Mahakama imejipanga kukuza dhana ya usuluhishi kama ilivyo kwenye Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, (1977) na kwamba ana imani kongamano hilo litaleta tija kwa jamii.

Naye, Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Elimo Daniel Massawe alitoa mada juu ya usuluhishi wa migogoro ya Tanzania ambapo alieleza maana ya usuluhishi, lengo, faida zake pamoja na mbinu za kufanya usuluhishi.

Mhe. Massawe alieleza kwamba, usuluhishi ni sehemu rasmi ya mfumo wa sheria unaotambuliwa na taratibu za Mahakama nchini, pia ni utaratibu unaowapa wahusika nafasi ya kusuluhisha mgogoro wao kwa hiari na kwa msaada wa mtu wa kati asiye na upendeleo, lakini pia mpatanishi sio mtoa uamuzi bali wahusika ndio wenye mamlaka ya mwisho.

Wakati wa kuhitimisha kongamano hilo, Kaimu Jaji Mfawidhi alisema kuwa, kongamano hilo litakua chachu katika kuimarisha usuluhishi na kuwaomba wadau waende kuwa Mabalozi wa Usuluhishi  kabla ya wadaawa kufika Mahakamani.

   Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Hussein Mtembwa akifungua Kongamano la Usuluhishi kwa wadau waliohudhuria kongamano hilo lililofanyika tarehe 16 Aprili, 2026 katika Mahakama hiyo.


Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Elimo Daniel Massawe akitoa mada juu ya Usuluhishi kwa wadau waliohudhuria Kongamano hilo.

   Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Simiyu, Mhe. Elimo Massawe (aliyesimama) akimkaribisha Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Hussein Salum Mtembwa (katikati) kuzungumza  na wadau wakati wa Kongamano hilo.

    Wadau mbalimbali waliohudhuria kongamano wakisikiliza mada kutoka kwa Mhe. Elimo Daniel Massawe, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Simiyu.

   Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Hussein Mtembwa (katikati mstari wa mbele ) akiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali aliohudhuria Kongamano la Usuluhishi katika Mahakama Kuu Masjala ndogo Simiyu.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara) 

Hitimisho Wiki ya Usuluhishi Dodoma

WATUMISHI IJC DODOMA WANUFAIKA NA MAFUNZO YA USULUHISHI

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma

Watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma wamepatiwa mafunzo maalum yanayohusu matumizi ya usuluhishi katika kushughulikia migogoro ya kiutawala na kikazi, ikiwa ni sehemu ya hitimisho la Wiki ya Usuluhishi kwenye Mahakama hiyo.

Mafunzo hayo yamefanyika leo tarehe 17 Aprili, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano, kuhitimisha Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi. Mafunzo hayo yalilenga kuimarisha ufanisi kazini na kujenga utamaduni wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo.

Mafunzo hayo yalisimamiwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ametoa elimu ya kina kuhusu dhana nzima ya usuluhishi na matumizi yake katika mazingira ya kazi.

Amesisitiza kuwa usuluhishi ni nyenzo muhimu katika kuongeza tija, kuimarisha mahusiano ya kikazi na kupunguza migogoro isiyo ya lazima katika Taasisi za umma.

Mafunzo hayo yaliwashirikisha pia Viongozi wa Dini ambao walitoa mchango mkubwa katika kuelezea nafasi ya usuluhishi kwa mtazamo wa kidini.

Kwa upande wa dini ya Kikristo, Bw. Ford Saileni alitoa mafundisho yaliyolenga kuhimiza amani, msamaha na maridhiano kama msingi wa kutatua migogoro.

Aidha, kwa upande wa dini ya Kiislamu, Ustadh Bwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma alieleza umuhimu wa suluhu (usuluhishi) kama sehemu ya mafundisho ya dini, akisisitiza haki, uvumilivu na maelewano katika jamii.

Mafunzo hayo hayakuwa ya kawaida, bali yalipambwa na shamrashamra mbalimbali zilizoongeza hamasa kwa washiriki. Vipengele vya maigizo vilivyowasilishwa na baadhi ya Watumishi pamoja na Wasanii walioalikwa vilionyesha kwa vitendo namna usuluhishi unavyoweza kutumika katika kutatua migogoro kwa njia ya kirafiki na yenye tija.

Watumishi walioshiriki walionesha kufurahishwa na mafunzo hayo, wakieleza kuwa yamewajengea uelewa mpana zaidi na kuwapa mbinu bora za kushughulikia changamoto za kikazi. Walibainisha kuwa elimu hiyo ina manufaa makubwa katika kuboresha utendaji wao pamoja na kuimarisha mshikamano kazini.

Kwa ujumla, mafunzo hayo yameacha alama chanya kwa Watumishi wa IJC Dodoma, yakionesha wazi umuhimu wa usuluhishi katika kujenga mazingira bora ya kazi na utoaji haki wenye ufanisi zaidi.

Ikumbukwe kuwa Wiki ya Usuluhishi nchini yalizinduliwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, tarehe 13 Aprili, 2026. Maadhimisho hayo yalienda sambamba na kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania.”

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (aliyesimama) akizungumza wakati wa kutoa mafunzo ya usuluhishi kwa Watumishi wa Mahakama IJC Dodoma.

Mchungaji Ford Saileni (aliyesimama) akiwasilisha mada ya usuluhishi kwa upande wa dini ya kikristo katika mafunzo ya watumishi wa IJC Dodoma.

 

Ustadhi Mbwana Haji akiwasilisha mada ya usuluhishi kwa upande wa Kiislamu wakati wa mafunzo ya usuluhishi kwa watumishi wa Mahakama wa IJC Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo kutoka Wizara ya Katiba na Sheria. Waliokaa kushoto kwake ni Ustadh Mbwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma na kulia kwake ni Mchungaji Ford Saileni.


 Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo ambao Maofisa Usafirishaji wa IJC Dodoma. Waliokaa kushoto kwake ni Ustadh Mbwana Haji kutoka Masjid Sunni Nunge Dodoma na kulia kwake ni Mchngaji Ford Saileni.

 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki na wakufunzi wa mafunzo hayo ambao ni Mahakimu, Mawakili pamoja na Watumishi (waigizaji) waliopamba mafunzo hayo ya usuluhishi kwa watumishi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Wiki ya Usuluhishi Dodoma

WANAFUNZI UDOM WAPATA ELIMU KUHUSU USULUHISHI

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma.

Katika kuendelea kuadhimisha Wiki ya Usuluhishi nchini, Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamepata fursa adhimu ya kupatiwa elimu muhimu ya usuluhishi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwaandaa vijana kuwa mabalozi wa amani na utatuzi wa migogoro katika jamii.

Elimu hiyo imetolewa jana tarehe 16 Aprili, 2026 katika moja ya kumbi za mikutano zilizopo ndani ya Chuo hicho, ambapo Wanafunzi walijitokeza kwa wingi kushiriki na kujifunza kwa kina kuhusu mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro, nje ya mfumo wa kawaida wa Mahakama.

Watoa mada katika mafunzo hayo walikuwa ni Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria, wakiwemo Mahakimu, Mawakili wa Serikali pamoja na Mawakili wa Kujitegemea. Wadau hao waliotoa uzoefu wao wa vitendo na kusisitiza umuhimu wa usuluhishi katika kuharakisha haki, kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani na kudumisha mahusiano mema katika jamii.

Mafunzo hayo yalisimamiwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan.  Kupitia usimamizi wake, zoezi hilo lilifanikiwa kwa kiwango cha juu, likiwaacha Wanafunzi na uelewa mpana pamoja na hamasa ya kujifunza zaidi kuhusu taaluma ya sheria na mbinu za kisasa za utatuzi wa migogoro.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mhe. Dkt Fatma   alisisitiza kuwa kuwafikia Wanafunzi ni uwekezaji muhimu kwa mustakabali wa Taifa, kwani wao ndio watakaobeba dhamana ya kusimamia haki na amani katika jamii siku zijazo.

Kwa upande wao, Wanafunzi walionesha mwamko mkubwa na shauku ya kujifunza, wakieleza kuwa elimu hiyo imewafungua macho na kuwapa mtazamo mpya juu ya namna bora ya kushughulikia migogoro bila migongano mikali.

Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi yanaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini, yakilenga kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro, badala ya kutegemea Mahakama pekee.

Kwa ujumla, utoaji wa elimu hiyo kwa Wanafunzi wa UDOM, ambao wanachukua taaluma ya sheria ni hatua muhimu katika kujenga kizazi chenye uelewa, busara na uwezo wa kuleta suluhu za kudumu katika jamii, ikiwa ni msingi imara wa amani na maendeleo ya Taifa.

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan, akiwa katika Ukumbi Chuo cha Udom pamoja na Wanafunzi wakisikiliza neno la ukaribisho kutoka kwa Mkufunzi, Dkt Gamba (hayupo pichani)).

 

Wanafunzi wa Sheria Chuoni cha UDOM wakisikiliza kwa makini elimu ya usuluhishi kutoka kwa watoa mada.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, akifafanua jambo wakati wa utoaji elimu ya usluhishi kwa Wanafunzi wanaosomea sheria UDOM.

 

Wakili wa Kujitegemea, B. Elias Macibya, akifafanua jambo kuhusu usuluhishi wakati wa mafunzo hayo.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (aliyevaa mtandio wa blue) akiwa katika picha ya pamoja na watoa mada pamoja na baadhi ya Wanafunzi mara baada ya mafunzo hayo.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

LINDI YAWASISITIZA WADAU KUIMARISHA USHIRIKIANO, KUBORESHA UTOAJI HAKI

Na. HILARI GDIYE NA WINIFRIDA KISAMO – Mahakama, Lindi

Wadau wa Sekta ya Haki mkoani Lindi wamehimizwa kuongeza na kuimarisha ushirikiano katika uendeshaji wa mashauri ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema ipasavyo na kwa ufanisi.

Akizungumza katika kikao cha wadau kilichofanyika hivi karibuni, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Sylester Kainda alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu miongoni mwa wadau wote wa Sekta ya haki ili kutotoa nafasi ya kuchelewesha mashauri yanapofunguliwa mahakamani.

Mhe. Kainda amesema kuwa, mafanikio ya Mahakama yanategemea mchango wa pamoja wa kila mdau. Alibainisha kuwa kikao hicho kililenga kuweka mkakati madhubuti wa namna bora ya kuendesha shughuli za Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Lindi kwa ufanisi, uwazi na kasi na kuhakikisha huduma za haki zinatolewa kwa wakati mapema ipasavyo na kwa viwango vinavyotarajiwa.

Aidha, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa, Mahakama haiwezi kusimama peke yake bila ushirikiano wa wadau wake, akiwataka wadau wote kutambua nafasi zao katika kuhakikisha mchakato wa haki unakuwa thabiti na wenye matokeo chanya kwa jamii.

Vilevile, Mhe. Kainda alisisitiza umuhimu wa kumaliza mashauri kwa wakati ili kuwawezesha wananchi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi bila ucheleweshaji usio wa lazima, kwa mujibu wa takwimu Mkoa wa Lindi una mashauri machache, hali inayotoa fursa kwa Mahakama kuhakikisha kesi zote zinakamilika kabla ya mwezi Disemba, 2026.

“Kwa idadi ndogo ya mashauri yaliyopo ni matarajio yetu kwamba, Mahakama zetu zifike hatua ya kumaliza kesi zote kwa wakati na hata kuwa, katika nafasi ya kusubiri mashauri mapya,” alisema Jaji Kainda.

Jaji Mfawidhi huyo, alifafanua kuwa, mfumo wa kimahakama hupima ufanisi kwa kuzingatia muda unaotumika kusikiliza na kumaliza mashauri, hivyo Mahakama zinapaswa kuepuka uwepo wa kesi za muda mrefu zinazoleta mlundikano wa mashauri.

Akizungumzia suala la mashahidi, Mhe. Kainda alisema kuwa, matumizi ya teknolojia yamerahisisha usikilizwaji wa mashahidi kwa njia ya mtandao (remote hearing), hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya umbali na gharama.

Hata hivyo, alionya kuwa baadhi ya mashauri huathirika kutokana na mapungufu katika uendeshaji wake, akiwataka Mahakimu na wadau kuongeza umakini katika maandalizi na usikilizwaji wa mashauri ili kulinda haki za wahusika wote katika shauri husika. Pia alikemea vitendo vya rushwa na ucheleweshaji wa majalada ya kesi, akisisitiza kuwa maadili na uadilifu vinapaswa kupewa kipaumbele katika utoaji wa haki.

Katika jitihada za kurahisisha huduma kwa wananchi, Jaji Kainda alieleza kuwa, utambulisho wa wadhamini unaweza kuthibitishwa kwa kutumia Kitambulisho cha Taifa (NIDA) pekee, bila ulazima wa kuwasilisha barua za utambulisho kutoka kwa viongozi wa vijiji au Serikali za mitaa.

Kwa upande wa maboresho ya mifumo kiteknolojia, Mhe. Kainda alisema kuwa, Mahakama Kuu Lindi na Mahakama zake za chini zimeshanza kutumia mfumo wa kielektroni (paperless), hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kupunguza matumizi ya karatasi.

Jaji Mfawidhi huyo, ameyahimiza mabaraza ya ardhi kuhakikisha yanatoa nakala za hukumu kwa wakati ili kuwawezesha wananchi kupata haki zao bila ucheleweshaji usio wa lazima.

Wadau walikubaliana juu ya umuhimu wa ushirikiano, uwajibikaji na matumizi ya teknolojia katika kuimarisha utoaji wa haki, hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi wa Mahakama katika utoaji wa haki kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi akiwasilisha Mada wakati wa Kikao na Wadau. Wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (kulia)

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.


Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (aliyesimama) akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.

Mdau wa Mahakama Kutoka Ofisi ya Huduma ya Uangalizi wa Jamii Bi. Wilhelmina Qambalo akitoa hoja wakati wa kikao hicho.

Wadau wakifuatilia kwa Makini Mada zilizokuwa zinawasilishwa wakati wa kikao.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Sylivester Kainda (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)