Jumanne, 28 Julai 2026

MAHAKIMU MBEYA WAKUMBUSHWA KUZINGATIA MAADILI, WELEDI KATIKA UTOAJI HAKI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Wilaya ya Mbeya imefanya kikao kazi kilichowakutanisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo zilizopo jijini Mbeya kwa lengo la kusisitiza uimarishaji wa maadili, uwajibikaji na kuzingatia ubora wa utoaji wa huduma za Mahakama sambamba na kujadili changamoto zinazojitokeza katika ushughulikiaji wa malalamiko na uandaaji wa kumbukumbu za mashauri ya rufaa.

Kikao hicho kiliitishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba na kuwashirikisha viongozi kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, walitoa maelekezo na miongozo kadhaa ya utendaji kazi kwa Maafisa Mahakama wakiwa katika vituo vyao.

Viongozi walioshiriki kikao kazi hicho ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo aliwataka Mahakimu kuendelea kudumisha nidhamu, uadilifu na uzingatiaji wa sheria katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yao. Alisisitiza kuwa utoaji wa haki unapaswa kuongozwa na misingi ya haki, uwazi na weledi ili kulinda hadhi ya Mahakama.

“Mahakama ina jukumu la kumfuta machozi mtu aliyedhurumiwa haki zake na nasisitiza kuwa kila shauri linapaswa kushughulikiwa kwa umakini, usawa na kwa kuzingatia sheria ili kuhakikisha haki inatendeka na kuonekana kutendeka,” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, aliwahimiza Mahakimu kuendelea kuzingatia maadili ya kazi, kuwahudumia wananchi kwa weledi na kwa lugha yenye staha, pamoja na kutekeleza kwa vitendo maelekezo yanayotolewa na viongozi kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano, kuheshimiana na kujenga mahusiano mazuri mahali pa kazi. Pia aliwakumbusha Maofisa hao kutunza afya zao, akieleza kuwa afya njema ni msingi wa utendaji bora na huchangia katika kulinda na kutunza rasilimali za Mahakama na kuongeza ufanisi wa taasisi kwa ujumla.

Maofisa Mahakama katika kikao hicho, walikumbushwa umuhimu wa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, missing ya taaluma inayoongoza kazi zao na kuhakikisha kuwa majukumu yao yanatekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Pamoja na hayo, washiriki walijadili mbinu za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi ili kuongeza ufanisi na kuimarisha imani ya jamii kwa Mhimili wa Mahakama.

Aidha, Viongozi hao walisisitiza na kuhimiza Maofisa hao kuhakikisha wananchi wanapatiwa nakala za hukumu na mwenendo wa mashauri kwa wakati, matumizi sahihi ya mifumo ya TEHAMA katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama, kuzingatia mipaka ya mamlaka hayo wakati wa kusikiliza mashauri na kufuata sheria na kanuni katika utekelezaji wa tuzo na amri za Mahakama.

Mahakama ya Tanzania inaendelea kuimarisha uwezo wa watumishi wake kupitia mafunzo ya ndani na vikao vya kitaalamu vinavyolenga kuboresha utendaji kazi, kuimarisha maadili na kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki zenye ubora, kwa wakati na kwa kuzingatia misingi ya sheria na haki.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (wa pili kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo jijini Mbeya.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (wa pili kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo jijini Mbeya.

Viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa kikao hicho, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, (wa pili kulia) ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, (wa pili kushoto) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


 

MASJALA NDOGO GEITA YAFANYA KIKAO CHA MENEJIMENTI

Na. DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, amewataka watumishi wa Mahakama kuongeza ubunifu na uwajibikaji ili kuleta tija katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za utoaji haki kwa wakati.

Wito huo ametolewa wakati akifungua kikao cha Menejimenti cha Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Geita, kilichofanyika hivi karibuni, katika ukumbi wa mafunzo uliopo Kituo Jumuishi cha utoaji haki mjini Geita.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Kahyoza alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha viongozi na watumishi kukutana kwa lengo la kutathmini utendaji wa kazi wa Mahakama na kujadili mbinu bora za kuendelea kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.

Mhe. Kahyoza alisema kuwa, kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kinatoa fursa ya kutathmini utekelezaji wa majukumu, kubaini mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuongeza ufanisi katika maeneo yanayohitaji maboresho.

Alieleza kuwa, pamoja na kikao hicho kuwa sehemu ya utaratibu wa kisheria wa Mahakama, umuhimu wake unakwenda mbali zaidi ya kutekeleza matakwa ya kisheria, kwani kinatoa nafasi ya kutafakari namna ya kuifanya Mahakama iendelee kupiga hatua katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Jaji Kahyoza alisisitiza kuwa, utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama unapaswa kuzingatia maslahi mapana ya wananchi wa Mkoa wa Geita na Tanzania kwa ujumla. Alibainisha kuwa kila mtumishi anapaswa kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na viwango vya juu vya weledi.

“Ni muhimu kila mmoja wetu kutathmini tumefanikiwa kwa kiwango gani, ni maeneo yapi tunasuasua na ni hatua zipi tunapaswa kuchukua ili kuhakikisha shughuli zetu zinaendelea kufanyika kwa ufanisi zaidi,” alisema Jaji Kahyoza.

Nao, Wakuu wa vitengo pamoja na Viongozi wa Utawala kutoka Mahakama za Wilaya na Mahakama Kuu waliwasilisha taarifa za maeneo yao ya kiutendaji.

Wajumbe walipata nafasi ya kujadili taarifa mbalimbali zilizowasilishwa, huku mijadala ikijikita katika namna ya kuongeza ubunifu na tija katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama, hususan kuimarisha usikilizaji na utoaji wa maamuzi ya mashauri kwa wakati.

Miongoni mwa changamoto zilizojadiliwa ni uchakavu wa baadhi ya majengo ya Mahakama pamoja na kuwepo kwa fedha za mirathi ambazo hazijachukuliwa na wanufaika wake.

Taarifa ya Mashauri ilionesha Mahakama zote kufanya vizuri kwa kipindi cha Machi mpaka Juni 30, 2026. Mashauri ya Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, na Wilaya zote hazikuwa na shauri la mlundikano kwa mashauri yaliyofunguliwa mwaka 2025.

Pongezi pia zilienda Mahakama za Mwanzo kwa kuendelea kuondosha Mashauri kwa wakati kwani Mahakama zote zina wastani wa siku 9 wa umri wa shauri kukaa mahakamani.

Hata hivyo, kikao kilibaini kuwa bado kuna changamoto kuhusu fedha za mirathi, ambapo baadhi ya fedha hizo zimeendelea kubaki bila kuchukuliwa kutokana na kutopatikana kwa wanufaika au baadhi yao kukataa kuzichukua kwa madai kuwa kiasi kilichopo ni kidogo.

Wajumbe kutoka Mahakama za Wilaya za Chato, Geita, Bukombe, Mbogwe na Nyang'hwale walieleza kuwa changamoto hiyo imeendelea kujitokeza katika maeneo yao. Kutokana na hali hiyo, Mwenyekiti alisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za haraka ili kupata suluhisho la kudumu.   

Katika kikao hicho, wajumbe walichangia umuhimu wa kuendelea kutafuta viwanja na kuvipatia hati angalau viwanja viwili kwa kila Halmashauri. Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita Bi. Masalu Kisasila asisitiza kuwa, hatua hiyo ni muhimu katika kuwezesha upatikanaji wa miradi ya maendeleo na kulinda mali za Mahakama.

Kutokana na umuhimu wa suala hilo, Mwenyekiti wa kikao hicho alielekeza kuwa, ifikapo Septemba 30, 2026, viwanja na majengo yote ya Mahakama ambayo bado hayana hati miliki viwe vimekamilisha taratibu za umiliki.

Aidha, viongozi wa Mahakama waliagizwa kushirikiana kwa karibu na Wakurugenzi wa Halmashauri katika maeneo yao ili kutatua kwa wakati changamoto zinazohusu miundombinu pamoja na masuala mengine ya kiutendaji.

Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama na taasisi nyingine za Serikali, akieleza kuwa ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika kuhakikisha mipango ya maendeleo ya Mahakama inatekelezwa kwa ufanisi na huduma kwa wananchi zinaendelea kuimarika.

Mhe. Kahyoza alisisitiza kuwa, ubunifu, uwajibikaji, matumizi bora ya rasilimali na tathmini ya mara kwa mara ya utekelezaji wa mipango ni nguzo muhimu za kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za Mahakama. Alieleza kuwa hatua hizo zitawezesha Mahakama kuendelea kuboresha mazingira ya utendaji, kuharakisha usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (kulia) akiwa anaongoza kikao cha menejimenti Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita.

Mhasibu wa Mahakama Kuu Geita, Bw. Goodluck Machange akiwasilisha Taarifa ya utekelezaji wa Fedha.

Sehemu ya washiriki wa kikao cha menejiment Masjala Ndogo ya Geita.

Afisa Ugavi wa Mahakama Kuu Geita, Bw. Abel Bunzali akiwasilisha Taarifa ya utekelezaji wa robo ya nne ya mwaka 2025/2026.

Meza Kuu katika kikao cha menejimenti, aliyesimama ni Katibu wa kikao, Bi. Masalu kisasila, katikati ni Mwenyekiti wa Kikao, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mhe. Fredrick Lukuna.


Jumatatu, 27 Julai 2026

TANZIA: JAJI MSTAAFU KAKUSULO SAMBO AFARIKI DUNIA


Mhe.
 Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo enzi za uhai wake.

TANZIA

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo, kilichotokea tarehe 26 Julai, 2026 jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, marehemu Jaji Kakusulo anatarajiwa kuzikwa tarehe 31 Julai, 2026 Kiwila Tukuyu mkoani Mbeya.

Marehemu Jaji Kakusulo aliajiriwa na Mahakama ya Tanzania tarehe 04 Februari, 1989 kama Hakimu Mkazi Daraja III na kuapishwa tarehe 04 Februari, 1989 mbele ya aliyekuwa Jaji Mkuu, Marehemu Francis Nyalali.

Katika maisha yake Jaji Sambo aliitumikia Mahakama ya Tanzania kama Hakimu Mkazi kwenye Mikoa ya Iringa, Mbeya, na pia aliteuliwa mnamo tarehe 04 Mei, 1994 kuwa Naibu Mwenyekiti wa Baraza la Nyumba, Mkoa wa Mbeya ambapo alitumikia kwa miaka zaidi ya mitatu.

Hata hivyo, aliteuliwa kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Ruvuma mnamo tarehe 05 Julai, 1993 na kutumikia cheo hicho katika Mkoa wa Arusha baada ya kuteuliwa mnamo tarehe 01 Januari, 2000.

Marehemu Jaji Sambo aliteuliwa kukaimu Ofisi ya Msajili wa wilaya Mahakama Kuu, Kanda ya Arusha na baadae mnamo tarehe 02 Novemba, 2001 aliteuliwa kuwa Msajili wa Wilaya (District Registrar) na kupangiwa kutumika katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tanga. 

Aidha, alitumikia kituo hicho kwa weledi mkubwa na kujitolea kwa moyo wake wote na mamlaka za uteuzi ziliona kazi yake iliyotukuka akiwa Hakimu Mkazi Mwandamizi na ndipo mnamo tarehe 28 Novemba, 2006 aliteuliwa kuwa Naibu Mwenyekiti wa Mahakama ya Kazi (Deputy Chairman, Industrial Court).

Jaji Sambo aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania tarehe 18 Desemba, 2006 na alihudumu kwa uadilifu na weledi mkubwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo za Bukoba, Arusha nafasi hiyo na mnamo tarehe 18 Februari, 2013 aliteuliwa kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga na hadi alipostaafu mnamo 01 Mei, 2016. Na hata baada ya kustaafu kama Jaji wa Mahakama Kuu, bado tuliendelea kushirikiana nae katika masuala mbalimbali ya kitaasisi na kitaifa kwa ujumla. 

Kufuatia msiba huo mzito, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amemtumia salamu za rambirambi Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju kupitia taarifa kwa umma iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano-Ikulu leo tarehe 27 Julai, 2026.

Aidha, Mahakama ya Tanzania inaungana na Ndugu, Jamaa na Marafiki kuomboleza msiba huo mzito wa kuondokewa na Mpendwa wetu Mhe.  Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo.

BWANA ALITOA, BWANA AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE.

WATUMISHI MBEYA WANOLEWA NAMNA BORA YA UANDAAJI KUMBUKUMBU ZA RUFAA MASHAURI YA JINAI

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya wamehitimisha mafunzo ya siku mbili ya namna bora ya kuandaa kumbukumbu za rufaa za mashauri ya jinai, yaliyofanyika hivi karibuni jijini Mbeya yakilenga kuimarisha ufanisi katika uandaaji wa nyaraka na kumbukumbu za Mahakama ya Rufani.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, ambaye alisisitiza umuhimu wa watumishi wa kada zote kuwa na uelewa wa pamoja kuhusu taratibu za uandaaji wa kumbukumbu za rufaa na kuongeza kuwa, ubora wa uandaaji wa nyaraka za Mahakama ni msingi muhimu wa utoaji wa haki kwa wakati.

Washiriki wa mafunzo hayo walitoka kada mbalimbali ikiwemo Mahakimu, wasaidizi wa kumbukumbu, waandishi waendesha ofisi, wasaidizi wa ofisi na walinzi, hatua inaonesha dhamira ya Mahakama ya kuwajengea uwezo watumishi wote ili kuboresha utendaji kazi wa taasisi.

Akitoa mada katika mafunzo hayo, Hakimu Mkazi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Hassan Yahaya Mbojellah, aliwaelekeza washiriki kuhusu taratibu na mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa kuandaa kumbukumbu za Mahakama ya Rufani kwa mashauri ya jinai.

Alifafanua tofauti za uandaaji wa kumbukumbu kwa mashauri yanayotoka Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, pamoja na mashauri yenye asili ya Mahakama Kuu.

Mbali na mafunzo ya nadharia, washiriki walipata fursa ya kujifunza kwa vitendo kupitia kazi za makundi, ambapo waliandaa kumbukumbu za rufaa na vitabu mbalimbali vya Mahakama ya Rufani kwa kutumia mifano halisi. Mbinu hiyo iliwawezesha kuongeza uelewa na umahiri katika kuandaa nyaraka kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

Kwa upande wao, washiriki walieleza kuridhishwa na mafunzo hayo na kuomba yawe endelevu, wakisema yatawasaidia kuongeza uelewa kuhusu masuala ya mashauri, uandaaji na utunzaji wa kumbukumbu za mahakama.

Washiriki wa mafuzo hayo walisisitiza kuwa, kwa kuwa mashauri ndiyo kiini cha shughuli za Mahakama, mafunzo ya mara kwa mara yataongeza ubora wa huduma na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya za kuendelea kuwajengea uwezo watumishi wake, kuboresha usimamizi wa mashauri na kuhakikisha nyaraka na kumbukumbu za Mahakama ya Rufani zinaandaliwa kwa usahihi kwa kuzingatia weledi, taratibu na viwango vinavyotakiwa.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo akifungua mafunzo ya siku mbili ya namna bora ya kuandaa kumbukumbu za rufaa za mashauri ya jinai kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeyav (hawapo pichani).

Mtoa mada katika mafunzo hayo Hakimu Mkazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Hassan Yahaya Mbojellah (aliyesimama) akitoa madini katika mafunzo hayo.

Mtoa mada katika mafunzo hayo Hakimu Mkazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Hassan Yahaya Mbojellah (aliyesimama) akitoa madini katika mafunzo hayo.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Alintula Watson Ngalile (aliyesimama) akizungumza katika mafunzo hayo, kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Msaidizi wa Ofisi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Editha Exavery Mhiliwa (aliyesimama) akieleza kwa muhtasari mada zilizofundishwa katika siku ya kwanza ya mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi walioshiriki katika Mafunzo hayo. 

Sehemu ya Watumishi walioshiriki katika Mafunzo hayo. 

Sehemu ya Watumishi walioshiriki katika Mafunzo hayo. 

Sehemmu ya washiriki katika mafunzo hayo wakiwa kwenye makundi wakifanya kwa vitendo yale waliyojifunza ambapo ilikuwa ni sehemu ya mafunzo hayo.



 

MAHAKIMU SUMBAWANGA WAPIGWA MSASA MATUMIZI YA USHAHIDI WA KIELEKTRONIKI, MAADILI

Na SHARIFU MOKIWA - Mahakama, Sumbawanga

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga imetoa Mafunzo maalum kwa Mahakimu yaliyolenga kuimarisha uwezo wao katika kushughulikia mashauri yanayohusisha ushahidi wa kielektroniki pamoja na kuwakumbusha kuendelea kuzingatia maadili ya kimahakama katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda na kujumuisha Mahakimu Wakazi 27 kutoka Wilaya za Kalambo, Sumbawanga na Nkasi ili kuwajengea washiriki hao uelewa wa pamoja kuhusu uchukuaji wa ushahidi wa kielektroniki, kanuni zinazosimamia upokeaji na tathmini ya ushahidi huo mahakamani.

Aidha, Mafunzo hayo yalijikita katika kuondoa dosari na makosa ya kawaida yanayoweza kujitokeza wakati wa kushughulikia ushahidi wa kidijiti, pamoja na mbinu bora za kuhakikisha ushahidi huo unatumika kwa usahihi na kwa kuzingatia sheria wakati wote wa uendeshaji mashauri yanayohusu matumizi hayo.

Kupitia Mada mbalimbali, washiriki walijadili changamoto zinazotokana na maendeleo ya teknolojia katika utoaji wa haki na namna Mahakama zinavyoweza kuendana na mabadiliko hayo. Washiriki walisisitizwa umuhimu wa kuendelea kujenga uwezo wa Mahakimu katika masuala ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa maamuzi yenye haki na yanayozingatia ushahidi wa kisasa.

Mbali na mada za ushahidi wa kielektroniki, mafunzo hayo pia yaliendeshwa kwa njia ya mkutano mtandao kwenye mada iliyowasilishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Masjala Ndogo  ya Simiyu Mhe. Wilbert Martin Chuma ambaye alitoa mada kuhusu Utamaduni na Maadili ya Mahakama kwa Mahakimu hao (Judicial Ethics and Culture). Katika wasilisho hilo, alielezea umuhimu wa maadili ya kimahakama katika kujenga na kuimarisha imani ya wananchi/umma kwa Mhimili wa Mahakama.

Aidha, Mhe. Chuma alisisitiza kuwa, maadili ya kimahakama yanapaswa kuonekana si tu katika maamuzi yanayotolewa bali pia katika mwenendo, mawasiliano na utendaji kazi wa kila siku wa Hakimu.

Mhe. Chuma aliongeza kwa kusema kwamba, utamaduni mzuri wa kimahakama hujengwa kupitia weledi, uadilifu na uwajibikaji kwa kuzingatia misingi iyokuwa na upendeleo, kuheshimu sheria na kuendelea kujifunza na kujielimisha mambo mapya ya kisheria yanayojitokeza mara kwa mara ili kuendana na mabadiliko ya mazingira ya utoaji wa haki.

Washiriki walipata nafasi ya kuuliza maswali, kubadilishana uzoefu na kujadili mifano mbalimbali ya vitendo kuhusu matumizi ya ushahidi wa kielektroniki pamoja na masuala ya maadili katika utoaji wa haki. Majadiliano hayo yalichangia kuongeza uelewa na kutoa mbinu za kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika mazingira ya sasa ya kidijitali.

Mafunzo hayo yametumika kama jukwaa la kuimarisha uwezo wa Mahakimu katika matumizi sahihi ya ushahidi wa kielektroniki na kuwakumbusha umuhimu wa kuendelea kuzingatia maadili ya kimahakama kama msingi bora wa utoaji haki wenye ufanisi, uwazi na unaojenga imani kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela  Manyanda (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Washiriki wa mafunzo  ya Ushahidi wa Kielekroniki na Maadili ya kimahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda akizungumza wakati wa kufungua mafunzo maalum kwa Mahakimu yaliyolenga kuimarisha uwezo wao katika kushughulikia mashauri yanayohusisha ushahidi wa kielektroniki.


Viongozi walioshiriki katika Mafunzo hayo, (kushoto) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda, (katikati) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Bw. Machumu Essaba na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (katikati aliyesimama) akijibu Maswali yaliyo ulizwa na washiriki wa Mafunzo hayo ya Ushahidi wa Kielektroniki.

Waheshimiwa Mahakimu wakiwa katika ukumbi wa Mahakama Kuu Sumbawanga, wakifatilia kwa umakini mafunzo hayo yaliyo kuwa yakitolewa.

Televisheni ikionesha Mkutano mtandao wakati wa mafunzo hayo yaliyokuwa yakiwasilishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Simiyu Mhe. Wilbert Martin Chuma.




 

TIMU ZA MAHAKAMA SPORTS KIGOMA, HALMASHAURI YA WILAYA UVINZA ZASAKATA KABUMBU

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile, amewaongoza wajumbe wa kikao cha Kamati ya Uongozi ya Mahakama kushuhudia mchezo wa mpira wa miguu wa kirafiki kati ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza.

Mchezo huo uliofanyika hivi karibuni katika Uwanja wa Shule ya Msingi Rugufu, ulikuwa na lengo la kuimarisha na kudumisha ushirikiano pamoja na mahusiano mema kati ya Mahakama na wadau wake katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma.

Katika mchezo huo, kikosi cha Mahakama Sports Kigoma kiliongozwa na Kapteni wake, Bw. Omary Magege.

Akizungumza kabla ya kuanza kwa pambano hilo, Kocha wa Timu ya Mahakama Sports Kigoma, Bw. Ramadhan Kufakunoga aliwahimiza Wachezaji wake kucheza kwa kujituma na nidhamu ya hali ya juu.

"Wachezaji wenzangu chezeni mpira kwa kujituma maana bidii yenu ndiyo itakayofikia malengo ya kuwa washindi wa mechi hii. Hata hivyo, matokeo yanapatikana baada ya dakika 90, hivyo chezeni bila kusababisha majeruhi kwa timu pinzani kwa kuwa hii ni mechi ya kirafiki," alisema Bw. Kufakunoga.

Kocha huyo aliongeza kuwa, mchezo huo ni sehemu ya kupima uwezo wa timu yake ili kubaini na kurekebisha mapungufu kabla ya kushiriki michuano mingine inayoratibiwa na Viongozi wa Mahakama Sports Kigoma.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi, Mhe. Rwizile alisisitiza umuhimu wa mchezo huo katika kujenga afya na kuimarisha mahusiano ya kiutendaji.

Alisema, "Mechi hii ni ya kuimarisha mahusiano, hivyo chezeni kwa furaha, hii ni sehemu ya kujenga afya zenu na tunategemea burudani nzuri kupitia ushindani wa mechi hii."

Baada ya dakika 90 za mchezo huo, Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 2-0 dhidi ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma.

Licha ya kufungwa, benchi la ufundi la Mahakama Sports lilieleza kuwa matokeo hayo yamekuwa kipimo kizuri cha kubaini maeneo yanayohitaji uboreshaji ili kujenga timu imara zaidi kwa ajili ya mechi zijazo.

Waliohudhuria walipongeza kiwango cha nidhamu, utulivu na weledi kilichooneshwa na timu zote mbili katika kufanikisha malengo ya mchezo huo.

Mchezo huo ulihudhuriwa pia na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Uvinza, Wajumbe wa Kikao cha Uongozi pamoja na wananchi waliojitokeza kushuhudia.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa mkono wa salamu kwa vikosi vya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza kabla ya mechi kuanza hivi karibuni.


Kapteni wa Timu ya Mahakama Sports, Bw. Omary Magege akionesha uwezo wa kusakata kabumbu katika mechi ya kirafiki kati ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza iliyofanyika hivi karibuni.

Mchuano mkali ukiendelea baina ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza,  katika uwanja wa Shule ya Msingi Rugufu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma (wa kwanza kulia), Mhe. John  Francis Nkwabi pamoja na wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kigoma wakifuatilia mechi iliyokuwa ikiendelea baina ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na  Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza iliyochezwa, katika uwanja wa Shule ya Msingi Rugufu mara baada ya kikao chao kumalizika.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa 10 kulia aliyevaa shati jeupe) akiwa katika picha ya pamoja ya Wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports Kigoma (kulia)na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe.John  Francis Nkwabi (wa kwanza kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa Kigoma, Mhe. Aristida Valerian Tarimo na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya za Kigoma Uvinza, Buhigwe na Kibondo.

 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 



 



 

 



Jumamosi, 25 Julai 2026

JAJI MKUU MASAJU ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA KUMBUKUMBU YA MASHUJAA TANZANIA

Na MARY GWERA, Mahakama - Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 25 Julai, 2026 ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania (JWTZ) Jenerali Jacob John Mkunda, Viongozi wa Serikali na Watanzania wote kwa ujumla kuadhimisha Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa nchini.

Hafla ya  Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa nchini imefanyika katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali-Mtumba jijini Dodoma huku ikitawaliwa na ratiba mbalimbali ikiwemo utoaji wa dua na sala.

Katika maadhimisho hayo, Viongozi mbalimbali pia walishiriki kutoa heshima kwa kuweka vifaa na alama za jadi kwenye Mnara wa Mashujaa wakiongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye aliweka Mkuki na Ngao kwenye Mnara wa Kumbukumbu ya Mashujaa ikiwa ni ishara ya kuwaenzi, kuwakumbuka na kuthamini mchango wa mashujaa waliopigania uhuru, amani na maendeleo ya Taifa.

Kadhalika Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Jacob John Mkunda aliweka Sime; Balozi wa Burundi nchini Tanzania, Mhe. Leontine Nzeyimana aliweka shada la maua kwa niaba ya Mabalozi, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Mhe. Alimwoni Chaula aliweka Upinde na Mshale huku Brigedia Jenerali (Mstaafu), Wilfred Paul Mwakalambile Kabunda akiweka Shoka.

Mbali na Jaji Mkuu, Viongozi wengine waliohudhuria katika Sherehe hizo ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi,  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule na wengine.

Aidha kwa upande wa Mahakama, sherehe hizo zimehudhuriwa pia na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Sam Rumanyika, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na baadhi ya Viongozi wengine.

Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania huadhimishwa tarehe 25 Julai kila mwaka lengo likiwa ni kuwakumbuka na kuwaenzi Mashujaa wote waliopoteza maisha yao wakitetea, kupigania na kulinda uhuru, amani, umoja na maslahi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Maadhimisho hayo yanaendelea kuwa chachu ya kuhamasisha uzalendo, mshikamano na uwajibikaji kwa vizazi vya sasa na vijavyo katika kulijenga Taifa la Tanzania.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa katika sherehe za Siku ya Kumbukumbu ya  Mashujaa Tanzania leo tarehe 25 Julai, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Wa pili kushoto ni  Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania (JWTZ) Jenerali Jacob John Mkunda, anayefuata ni Balozi wa Burundi nchini Tanzania, Mhe. Leontine Nzeyimana, anayefuata ni Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Mhe. Alimwoni Chaula na wa kwanza kulia ni Brigedia Jenerali (Mstaafu), Wilfred Paul Mwakalambile Kabunda.
Matukio katika picha Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Nchini leo tarehe 25 Julai, 2026 
katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiingia katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma leo tarehe 25 Julai, 2026. 


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Sam Rumanyika (wa pili kushoto) akifuatiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, akifuatiwa na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanania na Katibu wa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Venance Mlingi na Katibu Msaidizi wa Jaji Mkuu, Mhe. Wilberforce Luhwago wakiwa katika Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania leo tarehe 25 Julai, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. 

Vikosi mbalimbali vya Gwaride maalum vilivyoandaliwa kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania.

Baadhi ya Maofisa kutoka Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika sherehe za Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania.

Picha mbalimbali za matukio ya Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa nchini leo tarehe 25 Julai, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. 

Burudani ikiendelea.

Mnara wa Mashujaa.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiondoka  katika Viwanja vya Mashujaa-Mtumba jijini Dodoma mara baada ya kukamilika kwa sherehe hizo.

                         (Picha na MARY GWERA, Mahakama)