· Wafundishwa jinsi ya kupakua Nakala za Hukumu na mienendo ya mashauri kupitia mfumo huo
· Wasisitizwa juu ya matumizi ya TEHAMA
Na PAUL PASCHAL, Mahakama-Moshi
Mafunzo
hayo ambayo yametolewa kwa Wadau kutoka Magereza, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa (TAKUKURU) na Waendesha Mashtaka wa Serikali yamefanyika
leo tarehe 03 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mdogo wa mikutano wa Mahakama Kuu
Moshi.
Mafunzo
hayo yalifunguliwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Moshi,
Mhe. Sekela Mwaiseje na mada kuu ikiwasilishwa na Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu
Moshi, Bi Catherine Mugyabuso.
Akizungumza wakati ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Mwaiseje
alisisitiza juu ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa
ajili ya kusaidia uendeshaji wa shughuli za Kimahakama kwa haraka na weledi
katika kurahisisha upatikanaji wa taarifa za mashauri kama vile upatikanaji wa
nakala za hukumu na mienendo ya shauri kwa haraka na kwa unafuu kupitia Mfumo
wa e-CMS ili kuepuka malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa Mahabusu au
Wafungwa.
“Ndugu washiriki tumewaita hapa leo ili kuwaongezea
maarifa kidogo juu ya maboresho yaliofanyika na yanaoendelea kufanywa na
Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha ufanisi na weledi katika jukumu zima la
utoaji haki nchini kupitia mifumo yetu ya kimahakama huduma zetu zimeboreka na
kurahisishwa ili kuondoa malalamiko kwa wote tunaowahudumia,” amesema Mhe.
Mwaiseje.
Amewaeleza washiriki hao wa mafunzo kuwa, wao kama Wadau
muhimu wa Mahakama katika kuwahudumia Watanzania ni vema nao wakapata ujuzi na
kuwa na uelewa wa pamoja katika matumizi ya mfumo huo wa e-CMS.
Ameongeza kuwa, mfumo huo unaosimamia Mashauri
Mahakamani unalenga kuimarisha utoaji haki mapema ipasavyo na
kwamba kupitia mfumo huo kwa upande wa Mahakama Kuu Moshi kwa sasa
haitumii karatasi kupata nakala za hukumu na mwenendo wa shauri bali
zinapatikana kupitia kwenye mfumo.
Mshiriki Suzan Kimaro ambaye ni
Ofisa Mpelelezi Mkuu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)
Mkoa wa Kilimanjaro ameushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Moshi kwa maandalizi
mazuri ya mafunzo hayo yanayokwenda kuwajenga na kuwaongezea uwezo wa ufanisi
katika kutimiza majukumu yao.
“Kwa niaba ya Washiriki wote
nipende kuishukuru Mahakama kwa mafunzo haya kwani yametupa mwanga mzuri wa
namna ambavyo tunaweza kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi na weledi kupitia
mfumo huu wa e-CMS hii itatusaidia sana kuwahudumia wananchi kwa haraka na
pasipo na malalamiko yasio ya msingi,” amesema Bi. Suzan.
Washiriki kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Moshi, Magereza na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kilimanjaro kwa pamoja wakifuatilia mada iliyokuwa ikiwasilishwa wakati wa mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Moshi leo tarehe 03 Septemba, 2026.
Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Moshi, Mhe.Sekela Mwaiseje akieleza akifungua mafunzo hayo na kueleza lengo la kufanyika kwa mafunzo hao kwa washiriki walioalikwa (hawapo katika picha).
Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Moshi, Bi. Catherine Mugyabuso akitoa Mada kwa
washiriki wa Mafunzo kuhusu matumizi wa e-CMS (hawapo katika picha).
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)






























