·
Jaji Mkuu Masaju awataka Naibu
Wasajili hao kuwajibika ipasavyo kwa mujibu wa Katiba
·
Akemea vikali wanaoingilia Uhuru na
Maamuzi ya Mahakama
·
Awaonya Maofisa Mahakama hao kutojihusisha na Uanaharakati
·
Awakumbusha kuzingatia Utekelezaji wa
Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050
·
Ahimiza ushirikiano na mahusiano
mazuri kati ya Naibu Wasajili na Watendaji kwa utekelezaji fasaha wa majukumu
Na MARY GWERA,
Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Naibu Wasajili wa Mahakama nchini
kuendelea kutekeleza majukumu yao ipasavyo huku wakilinda maslahi ya haki
(Interest of Justice).
Mhe. Masaju ameyasema
hayo leo tarehe 31 Agosti, 2026 alipokuwa akifungua Mafunzo Elekezi kwa Naibu
Wasajili wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
“Tuna wajibu wa kuendelea
kutekeleza majukumu yetu kwa kulinda maslahi ya haki, kwa kutokufungwa kwa
masharti ya kiufundi kupita kiasi hadi kukwamisha upatikanaji haki,” amesema
Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amesema kuwa,
Wasajili wa Mahakama ndio 'injini' ya Mahakama. Hivyo, wana nafasi kubwa katika
maendeleo ya Mhimili huo ambao mamlaka yake kwa mujibu wa Ibara ya 4 ni kutekeleza
jukumu la utoaji haki.
“Kwa mujibu wa Ibara ya
107A(1), Mahakama ndio yenye kauli ya mwisho kwenye masuala ya utoaji haki katika
Jamhuri ya Muungano. Na ukiwa unaongozwa na kanuni kadhaa: mojawapo, kutenda
haki kwa wote bila kujali hali ya mtu kiuchumi au kijamii, kutochelewesha haki
bila kuwepo sababu ya msingi na kwamba itakuwa huru, italazimika tu kuzingatia
sheria za nchi na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kama ambavyo Ibara
ya 107A inavyoelekeza,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amesema,
shughuli zote za umma huongozwa na kusimamiwa na sheria; hakuna shughuli yoyote
ya umma ambayo haiongozwi na kusimamiwa na sheria. Na kwa sababu hiyo, Katiba
inakuwa pia sheria, kwa mujibu wa ile Sheria ya Tafsiri za Sheria, sura ya
kwanza ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aidha, Jaji Mkuu
amewakumbusha Naibu Wasajili hao kuwa waadilifu ili wanapofanya maamuzi, watu
waone kweli kwamba haki imetendeka. Amesisitiza, “Na katika hilo lazima tuwe
waadilifu, tunapoacha kuwa waadilifu, tukiwa wazembe, tukiwa wavivu, uwezo wetu
ukiwa mdogo, watu hawatatuheshimu.”
Vilevile, Mhe. Masaju
amekemea vikali tabia ya baadhi ya watu kuingilia uhuru na maamuzi ya Mahakama
huku akibainisha kuwa, Katiba imeiwekea ulinzi kwa Mahakama kupitia Ibara ya 30(2)(c)
inayoelekeza kuhakikisha utekelezaji wa hukumu au amri ya Mahakama iliyotolewa
katika shauri lolote la madai au la jinai.
Aidha, Ibara ya 30(2)(d)
inatamka kulinda heshima, haki na uhuru wa watu wengine au faragha ya watu
wanaohusika katika shauri lolote mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, au kulinda
heshima na uhuru wa Mahakama.
“Ni lazima hukumu na amri
za Mahakama zitekelezwe, ni Mahakama gani hiyo inaweza ikafanya maamuzi halafu
yasitekelezwe, halafu ikabaki kuwa Mahakama?” amehoji Jaji Mkuu.
Ameongeza kuwa, Katiba
hiyo pia inaelekeza kwamba lazima Mahakama iheshimike; uhuru wake, mamlaka, na
hadhi yake lazima vilindwe na viheshimiwe. Kwa hiyo, lazima kulinda sifa na
haki au uhuru wa watu wengine, au maisha binafsi ya watu wanaohusika katika
mashauri mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, kutunza heshima, mamlaka, na
uhuru wa Mahakama.
“Hivi karibuni
tulivyotaka kusimamia suala hili kwenye Kanda zenu, tulikuwa na sababu
za msingi. Hatutaruhusu watu kuidharau Mahakama au kuitisha hii Mahakama.
Kwamba sasa nchi itatawaliwaje? Tunahitaji amani! Hivyo tunatakiwa kuwa makini
kuliangalia suala hili, hatutaendekeza kitendo ambacho kitafanya Taifa hili liharibike,
ni haki za binadamu gani ambazo haziwezi kujali hata hizo Taasisi za kikatiba
zilizowekwa kwa ajili ya kutekeleza haki za binadamu?” ameeleza Mhe. Masaju.
Amewataka Naibu Wasajili
hao kutotishwa kwa namna yoyote ile kwakuwa wamepewa madaraka hayo na Katiba hivyo
wayatekeleze kwa ufanisi ipasavyo kama ilivyo kawaida ya viapo vyao.
Amerejea Ibara ya 30 ya
Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayosema:
"Haki na uhuru wa
binadamu ambavyo misingi yake imeorodheshwa katika Katiba hii havitatumika na
mtu mmoja kwa maana ambayo itasababisha kuingiliwa kati au kukatizwa kwa haki
na uhuru wa watu wengine au masahi ya umma."
Kadhalika, amewakumbusha
Naibu Wasajili hao kuwa sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo,
2050, kwa kuwa haki ina nafasi kubwa sana.
“Tuna jukumu kubwa sana
Mahakama. Na Dira yenyewe inasema: "Taifa jumuishi lenye ustawi, haki
na linalojitegemea." Kwa hiyo haki unaona imetajwa pale; ni muhimu, wanaohusika
na kutenda haki kwa mujibu wa Ibara ya 4 ya Katiba ya Jamhuri ni kina nani? ni
sisi Mahakama. Kwa hiyo, tunapojifunza nanyi mnaochukua nafasi za uongozi
katika kipindi hiki, mjue kwamba tunao wajibu wa kutekeleza majukumu wetu
lakini kwa kuzingatia yale matakwa ya Dira,” amesema Jaji Mkuu.
Ameongeza
kwa kueleza kuwa, pamoja na mambo mengineyo, Dira hiyo inalenga kuwa na jamii
yenye mshikamano na kutengamana, ambayo watu wake wanaishi kwa haki, amani, na
kuheshimiana. Na msingi mkuu wa Dira hiyo ni utawala, amani, usalama, na
utulivu. Ametaja maeneo matano ya kipaumbele ya Dira hiyo kuwa ni Utawala Bora
na Haki, Serikali za Mitaa imara na zenye ufanisi.
Amesema kuwa, “Unapozungumzia
masuala ya haki, unazungumza juu ya masuala ya sheria. Kwa hiyo, shughuli zote
hata zinazoenda kutekelezwa chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2050
zinaongozwa na kusimamiwa na sheria. Na mimi na baadhi ya wasaidizi wangu
tumesha 'map out' sheria zote zinazohusika katika utekelezaji wa Dira hii, kwa
sababu Dira hii haikuacha kitu. Hapa tulipo, unaweza ukabainisha kwamba mbali
na Katiba, swala kama hili, kwa mfano utawala bora, utatekelezwa kupitia sheria
zipi. Kwa hiyo, hapo ndipo utakapona masuala ya haki. Na katika utekelezaji wa
sheria hizi, kuna kuzivunja na kuzitekeleza.”
Mhe. Masaju ameeleza
kwamba, muundo wa Dira hiyo umeweka mazingira ya kukuza uchumi na shughuli
nyingine mbalimbali, ikiwemo za kibiashara, hivyo; hali hiyo inaweza kuja
ongezeko la migogoro ikiwemo migogoro ya kibiashara, kiwekezaji na migogoro ya
kijinai.
Kadhalika, Jaji Mkuu
amewataka Maofisa Mahakama hao kuwajibika ipasavyo wanapotekeleza majukumu yao
ambao amesema; “Sisi Mahakama tuna nafasi kubwa sana, tulipozungumza nanyi
tarehe 17 Juni mwaka huu, tuliwaeleza wajibu wenu. Na mimi niwaombe Wasajili
wote mlioko hapa, muendelee kuwajibika katika utekelezaji wa majukumu yenu,
kuwajibika ipasavyo kama Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
inavyoelekeza kwenye Ibara ya 25 ya Katiba hii. Ni suala la uwajibikaji, ni suala
la kikatiba na wajibu wetu sisi wenyewe. Na ni vizuri mjifunze na kuielewa hii
Dira. Tulitoa vitabu tukavisambaza kwenye kanda, lakini pia hii Dira
inapatikana kwenye nakala laini (soft copies).”
Mhe. Masaju amerejea Ibara
ya 146(2)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa moja ya
majukumu ya Serikali za Mitaa ni kuhakikisha utekelezaji wa sheria na ulinzi wa
wananchi kwenye maeneo hayo na ndio maana Mahakama inao mpango wa kujenga Mahakama
za Mwanzo kila kata.
“Na tumeshawaomba mketi
kwenye maeneo yenu, mhakikishe kwamba mnashirikiana na Serikali ngazi ile ya Mkoa
na Wilaya kupata viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama hizi,” amesema Jaji
Mkuu.
Mhe. Masaju ameongeza
kuwa, katika kutekeleza hayo, wanatekeleza Katiba, hivyo, ushirikiano ambao
umeendelea kuwa nao watendaji kwenye Kanda na Naibu Wasajili, waudumishe
utasaidia kufanikisha jambo hilo.
Amewasisitiza Naibu
Wasajili hao kuwajibika ipasavyo huku akirejea kipaumbele cha tatu cha Dira cha
utumishi wa umma unaowajibika. Ambapo amewashauri kuendelea kuwajibika kwakuwa
ni swala la kisheria na ni wajibu wao.
“Lakini kipaumbele cha
nne ni amani, usalama, na utulivu. Ukiangalia yote haya, unaona ni kwa namna
gani Mahakama ya Tanzania itaendelea kuwa na mchango muhimu katika kuhakikisha
ustawi na maendeleo ya Taifa hili kiuchumi, kijamii, na kisiasa,” amesema Jaji
Mkuu.
Aidha, ameeleza kuwa, ili
Mahakama iweze kutekeleza jukumu hilo, lazima moja iwe na uwezo wa
kulitekeleza. Kuna suala la miundombinu, kuna suala la rasilimaliwatu.
Akizungumzia suala la
Utu, Jaji Mkuu Mkuu amewataka Naibu Wasajili hao kuweka mbele suala la utu huku
akiwakumbusha kuwazingatia pia Watu wenye mahitaji maalum.
Kadhalika amewakumbusha
Watumishi wote wa Mahakama kwa ujumla kuwa watu wenye uwezo wa kutekeleza
wajibu kwa ufanisi ipasavyo (the capacity to deliver, competence), kuwa waadilifu
(integrity), kuwa wabunifu; kuwa watu wa kujiongeza, na kujiongeza pia
kumeelezwa katika Ibara ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya
25 kwenye uwajibikaji pale.
“Tunapaswa kuwa ni watu
ambao ni 'sensitive to justice', mnao wivu wa kuona kutenda haki na kuitenda
haki ipasavyo. Na haki nimeshasema ni maamuzi yanayofanywa na Mahakama huru kwa
kuzingatia Katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na kwenye viapo
vyetu tunaapa kwamba tutatekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa ile sheria ya
viapo, kwa kuzingatia Katiba, sheria, mila, na desturi za Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, tukiwa huru, bila hofu, woga, pendelio, wala chuki. Kitu hicho
lazima tukisimamie na kukitekeleza ipasavyo, bila kufanya hivyo, tunakosa sifa hiyo ya
kuwa watu wa kutoa haki,” amesisitiza.
Mafunzo hayo
muhimu yenye kulenga kutoa mwongozo wa utendaji wa Naibu Wasajili hao yamefanyika
kwa mara ya kwanza kwenye ukumbi mpya wa mikutano uliopo ndani ya Jengo la Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jambo ambalo limeonesha kufurahiwa na Viongozi pamoja na watumishi wengi
walioshiriki katika ufunguzi wa Mafunzo hayo.
“Ninayo furaha kubwa kwa
tukio hili muhimu. Na nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuliwezesha
tukio hili. Lakini pia na kuiwezesha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuweza
kutenda mambo haya makubwa. Na leo sisi, Mahakama ya Tanzania, tumekuwa na
ukumbi huu muhimu sana. Mikutano yetu mingiambayo ilikuwa na sababu za msingitutakuwa
tunaifanyia hapa. Ni ukumbi wa kisasa sana,” amesema Mhe. Masaju.
Aidha, Jaji Mkuu
ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuwezesha kutimia kwa ndoto ya kuwa jengo
kubwa na la kisasa, vilevile amewashukuru na kutambua kazi kubwa iliyofanywa na
Majaji Wakuu Watangulizi wake kuanzia mwaka 1920 mpaka sasa.
“Viongozi waliotangulia wamefanya kazi kubwa.
Sisi ambao tunapata fursa ya kutumika katika Mahakama ya Tanzania kipindi hiki,
tunakaa kwenye jengo ambalo lilianza kujengwa na wenzetu wakati huo, na
linaendelea kujengwa na kuimarika. Kwa hiyo, niwashukuru sana hawa viongozi
wote, Maofisa wa Mahakama (Judicial Officers) na hao ambao sio 'Judicial
Officers' waliokuwepo kuanzia mwaka 1920 mpaka sasa hivi. Na kwa sababu hiyo,
nikupongeze Mtendaji Mkuu na watangulizi wako kwa kufikia hatua hii. Na nanyi
Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki sana,” ameeleza Mhe. Masaju.
Matukio katika picha Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.






















.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpg)
.jpeg)





.jpg)

.jpg)











