Na AIDAN ROBERT,Mahakama-Kigoma.
Balozi mdogo wa Jamhuri ya Burundi nchini Tanzania anayehudumia Mkoa wa Kigoma, Bw. Kekenwa Jeremia, hivi karibuni alifanya ziara Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Kigoma na kufanya mazungumzo na Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Rwizile.
Lengo kuu la ziara hiyo ya Kiofisi iliyofanyika tarehe 04 Septemba, 2026 lilikuwa ni kujitambulisha upya na kutoa taarifa rasmi kwa Jaji Mfawidhi kuwa ameongezewa muda wa kuhudumu katika nafasi yake ya ubalozi mdogo nchini Tanzania. Hatua hiyo, inatajwa kuwa chachu kubwa ya ushirikiano wa karibu katika kutoa huduma za haki kwa raia wa Burundi.
Aidha,
Balozi huyo alitumia fursa hiyo kufikisha salamu maalum za Serikali ya Jamhuri
ya Burundi kwa Mahakama Kigoma, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea
kuimarisha ushirikiano wa kitaasisi katika nyanja za sheria, haki, na usalama
wa wananchi wa nchi hizo mbili Tanzania na Burundi ambao wamekuwa wakiishi kwa
amani na udugu wa karibu mkoani Kigoma.
Vile
vile alimjulisha Mhe. Rwizile kuwa, Rais wa Jamhuri ya Burundi amependa kumuongezea
muda wa kuendelea kufanya kazi katika nafasi hiyo ya Balozi ili kuhudumu katika
ubalozi mdogo hapa nchini, uamuzi unaolenga kuendeleza kazi.
“Naleta
salamu maalum kutoka Serikali ya Jamhuri ya Burundi kwa lengo la kuendeleza na
kuimarisha uhusiano mwema na ushirikiano wa kitaasisi baina yetu, hasa katika
masuala yanayohusu huduma za kisheria na kijamii mkoani Kigoma, mahusiano haya
thabiti yanazidi kuchochea amani, usalama na ushirikiano mzuri kwa wananchi wetu
wanaoishi na kufanya shughuli zao mkoani Kigoma,” alisema Balozi huyo.
Kwa
upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Rwizile
alimkaribisha na kumpongeza Balozi huyo kwa kuongezewa muda wa kazi,
akibainisha utayari wa Mahakama Kuu Kigoma kuendelea kushirikiana ki-taasisi
ili kuhakikisha haki inatendeka na ustawi wa jamii unalindwa.
“Ziara
hii inazidi kuimarisha daraja la kidiplomasia na udugu uliopo kati ya Tanzania
na Burundi, ikithibitisha dhamira ya dhati ya Viongozi wa nchi hizi katika
kudumisha amani na maendeleo endelevu,” alisema Jaji Rwizile.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo
na mgeni wake Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Burundi, Bw. Kekenwa Jeremia (hayupo katika picha).
Picha ya Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Burundi nchini Tanzania Mkoani Kigoma, Bw. Kekenwa Jeremia (katikati). Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa na kushoto ni Msaidizi wa Balozi Mdogo wa Burundi Mkoani
Kigoma, Bw. Nininahazwe Adalbert.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



























