- Aahidi kudumisha ushirikiano na Mahakama mkoani humo
Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma
Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw.
Said Seni amefanya ziara ya heshima ya kumtembelea Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile lengo likiwa
ni kujitambulisha rasmi na kuimarisha ushirikiano wa kikazi katika utoaji haki
mkoani humo.
Ziara hiyo
imefanyika leo tarehe 29 Julai, 2026 katika Ofisi za Mahakama Kuu Masjala
Ndogo Kigoma ambapo Mwanasheria huyo aliambatana na Wakili wa
Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma, Bw. George Kalenda pamoja na Mfawidhi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka
Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Magumbo.
Aidha, wakati wa mazungumzo ya Viongozi
hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu upatikanaji haki, ikiwemo kuongeza
kasi ya usikilizaji wa mashauri na kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani.
Vilevile, walisisitiza juu
ya umuhimu wa kuendelea kudumisha nidhamu, weledi na uwajibikaji katika
mnyororo mzima wautoaji haki mapema ipasavyo.
Aidha, Mhe. Rwizile amewakaribisha
Viongozi hao na kuwapongeza kwa hatua ya kufanya ziara hiyo ya kumtambulisha
Mwanasheria Mkuu Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, huku akisisitiza kuwa na ushirikiano
wa karibu baina ya Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya
Taifa ya Mashtaka (NPS) ni nguzo kuu katika kuhakikisha haki inatendeka mapema
ipasavyo na kwa haki kwa kila mwananchi.
“Mahakama Kigoma itakupa
ushirikiano ili utimize wajibu wako katika mnyororo wa haki, hivyo utakapobaini
changamoto yoyote inayohitajika kutatuliwa na Mahakama basi usisite kuileta kwa
ajili ya kutatuliwa kabla haijaathiri mnyororo wa kutoa haki mapema ipasavyo kwa
kila mwananchi,” amesema, Jaji Rwizile.
Kwa upande wake, Mwanasheria
huyo Mfawidhi wa Mkoa Kigoma, Bw. Said
Seni amesema, anaishukuru mamlaka yake kumpangia kazi mkoani Kigoma, kwani
amekutana na watu wema, wakarimu na wenye ari ya kufanya kazi kwa weledi na
kujituma.
Amesema kuwa, anayo imani
kwamba atapata ushirikiano wa kutosha katika kutimiza wajibu wake katika
kipindi chote atakachokuwa katika ofisi hiyo Mkoani Kigoma.
Kadhalika, Mwanasheria
huyo amemuahidi Jaji Mfawidhi kuwa, atafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na
kuhakikisha amri za Mahakama zinatekelezwa kwa wakati na kwa mujibu wa sheria
zilizopo.
Ameongeza kwamba, Ofisi hiyo
ni mpya katika Mkoa wa Kigoma imeanzishwa kwa lengo la kuongeza nguvu ili
kuisaidia Mahakama kutenda haki mapema ipasavyo, kupitia kutimiza wajibu wa Ofisi
ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Mazungumzo hayo yamehudhuriwa
na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Mtendaji
wa Mahakama, Bw. Yusuph Kasuka.
Ziara hiyo imelenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na ushirikiano baina ya Mhimili wa Mahakama na Taasisi za usimamizi wa sheria na uendeshaji wa mashtaka mkoani Kigoma, ili kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa ufanisi na mapema ipasavyo kwa maslahi ya wananchi kwa ujumla.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (aliyeketi mbele) akifanya mazungumzo na Ujumbe wa Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma ulipomtembelea ofisini kwake Mahakama Kuu Kigoma leo tarehe 30 Julai, 2026.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa neno kwa wageni
wake katika maongezi yaliyofanyika katika ofisi yake iliyopo katika jengo la
Mahakama Kuu Kigoma.
Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mfawidhi na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma kwa mapokezi mazuri.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa utambulisho wa Viongozi waliofika katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile leo tarehe 30 Julai, 2026.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi akifurahia jambo alipokuwa akizungumza na Viongozi na Wadau wa Haki Jinai waliofika ofisini kwake kumsabahi na
wakimtambulisha Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi
Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa tatu kulia) akiwa pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (wa tatu kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka (wa kwanza kushoto), Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni, (wa wa pili kulia), Mfawidhi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Magumbo (wa kwanza kulia) na Wakili wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma, Bw. George Kalenda.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (aliyeketi mbele) akitoa neno kwa Viongozi waliofika ofisini kwake kwa ajili ya utambulisho wa Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




























