Jumatano, 22 Julai 2026

"USULUHISHI NI NGUZO MUHIMU YA UTOAJI HAKI TANZANIA"

Na HABIBA MBARUKU – Mahakama Dar es Salaam

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amesema kuwa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya usuluhishi na upatanishi, unapaswa kutambuliwa kama sehemu muhimu ya mfumo wa utoaji haki nchini.

Mhe. Siyani ameyasema hayo leo tarehe 22 Julai, 2026, katika hotuba  aliyoisoma kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) ya mwaka 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Delta jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaielekeza Mahakama kukuza na kuimarisha utatuzi wa migogoro miongoni mwa wahusika wa migogoro kama ilivyofafanuliwa katika Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo usuluhishi na upatanishi unapaswa kutazamwa kama mwendelezo wa jukumu la Mahakama katika utoaji wa haki ndani ya mfumo wa utawala wa sheria.

"Utoaji wa haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umepewa Mahakama. Hata hivyo, mamlaka hiyo haiwazuii wahusika wa mgogoro kutafuta haki kwa njia nyingine walizokubaliana, kama inavyoainishwa katika Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inaielekeza Mahakama kukuza na kuimarisha utatuzi wa migogoro miongoni mwa watu wanaohusika katika migogoro hiyo,” amesisitiza Mhe. Siyani.

Amesema mifumo ya jadi ya utatuzi wa migogoro iliyokuwepo kabla ya ukoloni, iliyojengwa katika misingi ya maridhiano na maelewano, bado ina mchango mkubwa katika maendeleo ya mifumo ya kisasa ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya Usuluhishi, huku akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha mifumo hiyo inaendana na mazingira ya Tanzania na inayokidhi viwango vya kimataifa.

"Uhalali wa mfumo wowote wa utatuzi wa migogoro hautegemei tu uhalali wake wa kisheria, bali pia kukubalika kwake na jamii pamoja na kuendana kwake na mila na utamaduni wa wananchi. Kwa hiyo, mustakabali wa mifumo ya Usuluhishi/upatanishi nchini Tanzania unapaswa kuwa shirikishi, ukichota mema kutoka katika mila na desturi mbalimbali huku ukizingatia misingi ya haki, kutopendelea upande wowote na utawala wa sheria,” amesema Jaji Kiongozi.

Aidha, ameeleza kuwa, usuluhishi na upatanishi havipaswi kuonekana kama njia zinazotumika pale Mahakama zinapokuwa na mlundikano wa mashauri, bali ni miongoni mwa njia kamili za utoaji haki zilizoidhinishwa na Katiba na Sheria za nchi, zenye uwezo wa kusaidia upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Amebainisha kuwa, katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kushuhudia ongezeko la uwekezaji katika miundombinu, Sekta ya Nishati, rasilimali asilia na biashara za kimataifa, mifumo ya Usuluhishi na Upatanishi ina nafasi muhimu katika kushughulikia migogoro yenye thamani kubwa na masuala ya kitaalamu kwa ufanisi, kuongeza uhakika wa mazingira ya biashara na kuimarisha imani ya wawekezaji.

Mhe. Siyani ameeleza kuwa, pamoja na uhuru wa mchakato wa usuluhishi, Mahakama inaendelea kuwa na jukumu la kuhakikisha taratibu za usuluhishi zinafuatwa, tuzo za usuluhishi zinatekelezwa, maslahi ya umma yanalindwa na mfumo wa sheria unabaki kuwa thabiti kwa kuwa Mahakama na usuluhishi ni mifumo inayokamilishana katika kufanikisha utoaji haki.

Aidha, amewataka Wadau wa Sekta ya Sheria kuendelea kuimarisha uwezo wa kitaaluma, kutumia teknolojia katika uendeshaji wa mashauri ya usuluhishi, kuendeleza utaalamu katika sekta mbalimbali na kuoanisha mifumo ya ADR na viwango vya kimataifa ili kuiwezesha Tanzania kujijengea nafasi kama kitovu cha usuluhishi kimataifa.

Pamoja na hayo, Jaji Kiongozi amewahimiza washiriki kutumia mkutano huo kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza matumizi ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala nchini.

Katika hatua nyingine Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari, ametaja hatua mbalimbali zinazofanywa na Ofisi hiyo huku akisisitiza kuwa haki inapaswa kupatikana mapema ipasavyo.

Pamoja na hayo, amewataka kuzingatia R4 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambazo ni Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Kujenga Upya.

Kwa upande wake Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) Wakili Aderickson Njunwa, ameeleza kuwa, Taasisi hiyo iliyoanzishwa mwaka 1997, imebeba dhima kubwa ya kuisaidia jamii kutatua migogoro kwa njia ya upatanishi, kadhalika kukuza uwekezaji na kuimarisha uchumi endelevu.

Wakili Njunwa amefafanua kuwa miongoni mwa majukumu mengine ya (TIArb) ni kuhakikisha kuwa jamii ya Tanzania inapata elimu kuhusu maana ya usuluhishi na umuhimu wake kwa maendeleo endelevu pamoja na kuendeleza uwajibikaji kwa kujengeana uwezo na majukumu ya kitaasisi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akifungua Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026 kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju uliofanyika leo tarehe 22 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Delta jijini Dar es Salaam.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria katika ufunguzi wa mkutano huo wakifuatilia kinachojiri.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja. Wa pili kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari, wa pili kushoto ni Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Aderickson Njunwa, wa kwanza kushoto ni Makamu wa Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Usaje Mwambene na wa kwanza kulia ni Meneja wa Uwekezaji wa Taasisi hiyo, Bw. Daudi Riganda.

Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Aderickson Njunwa akizungumza kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya  Delta jijini Dar es Salaam.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.







Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha za pamoja na Wadau mbalimbali walioshiriki katika ufunguzi wa Mkutano huo.

 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

MAHAKAMA MANYARA YAENDELEA KUTOA MAFUNZO KWA WANAFUNZI TASNIA YA WANYAMAPORI

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara kupitia Mahakama ya Wilaya ya Babati imeendelea kuwapokea Wanafunzi wa vyuo mbalimbali vya Usimamizi wa Wanyamapori ikiwa ni pamoja na wanafunzi kutoka Chuo cha Wanyamapori Pasiansi cha jijini Mwanza waliofika mahakamani hapo kwa ajili ya mafunzo ya uendeshaji wa mashauri yanayohusu Wanyamapori.

Katika mafunzo hayo, jumla ya wanafunzi 149 kutoka Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi kutoka Mwanza wakiwa wameambatana na walimu wao watatu (3) wamefika kwa lengo la kujifunza taratibu za kisheria na masuala mbalimbali yanayotokea mahakamani kwa njia ya Mahakama mtandao ili njia hizo iweze kuwasaidia katika masomo wanayojifunza chuoni.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Charles Mnzava, aliwasihi wanafunzi hao kuzingatia yale yote ambayo watafundishwa na wataalamu wa masuala ya kisheria ili yaweze kuwasaidia katika masomo yao chuoni na hata katika maisha baada ya chuo pale ambapo watakuwa wameajiriwa au kujiajiri katika maeneo mbalimbali.

“Chuoni mnasoma zaidi kwa nadharia, nawapongeza kwa kuja leo na kushuhudia namna mashauri haya yanayohusu wanyamapori na nyara za Serikali yanavyoendeshwa Mahakamani. Mafunzo haya yataongeza tija na uelewa wenu zaidi katika hayo mnayojifunza chuoni na hata baadae mtakapokuwa katika ajira zenu.” alisema Mhe. Mnzava.

“Pamoja na hayo tunawapongeza kwa kuchagua Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya kupata mafunzo haya. Kwetu Mahakama ni furaha kubwa sana kuweza kuunganisha Taasisi mbili kama mlivyokuja jana na leo kwa ajili ya mafunzo haya ya kimahakama na hususan namna ya uendeshaji na usikilizaji wa mashauri yanayohusu wanyamapori,” ameongeza Mhe. Mnzava

Katika hatua nyingine, Mhe Mnzava alitumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi hao juu ya Muundo wa Mahakama ya Tanzania ulivyo. “Mahakama zetu hapa nchini, kuanzia Mahakama ya Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu Pamoja na Mahakama ya Rufaa zina taratibu zake za usikilizwaji wa mashauri kulingana na uzito wa mashauri husika hivyo ni vema mkafahamu kuwa hata haya mashauri ya Wanyamapori mathalani hayawezi kusikilizwa katika ngazi za Mahakama za Mwanzo”.

Aidha, wanafunzi wa Taasisi hizo waliweza kuhoji na kujibiwa maswali mbalimbali kwa wawezeshaji wa Mafunzo hayo ambao walikuwa ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Joseph Kimaro pamoja na Mahakimu Wakazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao na Mhe. Jumaa Mwambago.

Akishukuru baada ya mafunzo hayo Mwakilishi wa Walimu waliombatana na wanafunzi hao kutoka Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi Mwalimu Hamisi Philimon Matinde, alishukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kuwapokea vema na kuwapa Elimu waliyokuwa wakiihitaj.

“Tunashukuru sana Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kutupokea na kwa ushirikiano mliotupa, tuaamini kuwa elimu hii itatusaidia sana na tutaendelea kuja hapa kwa ajili ya mafunzo mengine,” alisema Mwalimu Matinde.

Utaratibu wa kutoa Elimu, unaendelea kufanyika kwa kuwawezesha wanafunzi na wanataaluma mbalimbali kutoka Taasisi za Elimu kujifunza masuala mbalimbali kama walivyofanya Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi Mwanza.

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakiwa katika picha ya Pamoja na walimu wao na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara mbele ya jengo la Mahakama Kuu Manyara.

Mahakimu Wakazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao (aliyesimama kushoto) na Mhe. Jumaa Mwambago wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yanatolewa kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi.

Wanafunzi wa Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi wakiwa katika picha ya Pamoja na walimu wao na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara mbele ya jengo la Mahakama Kuu Manyara.

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza wakifuatilia mada ambazo zilikuwa zinatolewa katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza wakifuatilia mada ambazo zilikuwa zinatolewa katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.




Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava (wa kwanza kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victo Kimario wakiendelea kutoa Elimu kwa wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza (hawapo pichani) walipofika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kupata mafunzo.


Jumanne, 21 Julai 2026

WANAFUNZI MWEKA WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO MAHAKAMA YA WILAYA YA BABATI

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka kilichopo Moshi mkoani Kilimanjaro wamefanya ziara ya kujifunza taratibu mbalimbali za kimahakama katika katika uendeshaji wa mashauri yanayohusu uendeshaji wa mashauri yanayohusu wanyamapori.

Mafunzo hayo yanaendeshwa katika ukumbi namba Tatu wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara ambao unatumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Babati katika kuendesha shughuli za Mahakama.

Katika ziara hiyo, jumla ya wanafunzi Hamsini na nane (58) kutoka Chuo hicho waliambatana na walimu wao wanne (4) kwa lengo la kujifunza taratibu na masuala mbalimbali yanayotokea mahakamani kwa njia ya vitendo mtandao ili ziweze kuwasaidia katika elimu yao wanayojifunza chuoni.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava, aliwasihi wanafunzi hao kuzingatia yale yote ambayo watafundishwa na wataalamu wa masuala ya kisheria ili yaweze kuwasaidia katika masomo yao ya chuoni na hata katika maisha ya baada ya chuo pale ambapo watakuwa wameajiriwa au kujiajiri katika maeneo mbalimbali.

“Chuoni mnasoma zaidi kwa nadharia, nawapongeza kwa kuja leo na kushuhudia namna mashauri haya yanayohusu wanyamapori na nyara za Serikali yanavyoendeshwa mahakamani. Mafunzo haya yatawaongeza tija na uelewa wenu zaidi katika hayo mnayojifunza chuoni na hata baadae mtakapokuwa katika ajira zenu” alisema Mhe. Mnzava.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mnzava alitumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi hao juu ya Muundo wa Mahakama Tanzania ulivyo. “Mahakama zetu hapa nchini, kuanzia Mahakama ya Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu Pamoja na Mahakama ya Rufani zina taratibu zake za usikilizwaji wa mashauri kulingana na uzito wa mashauri husika hivyo ni vema mkafahamu kuwa hata haya mashauri ya Wanyamapori mathalani hayawezi kusikilizwa katika ngazi za Mahakama za Mwanzo”.

Aidha, wanafunzi wa chuo hicho cha Mweka waliweza kuhoji na kujibiwa maswali mbalimbali kwa wawezeshaji wa Mafunzo hayo ambao walikuwa ambaye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati, Mhe. Victor Joseph Kimaro pamoja na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo Mhe. Martin Massao.

Akishukuru baada ya mafunzo hayo Mwakilishi wa Walimu waliombatana na wanafunzi hao Mwalimu Melckezedeck Tarimo alishukuru uongozi wa Mahakama Kuu Manyara kwa kuwapokea vema na kuwapa Elimu waliyokuwa wakiihitaji.

“Tunashukuru sana Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kutupokea na kwa ushirikiano mliotupa, tuaamini kuwa elimu hii itatusaidia sana na tutaendelea kuja hapa kwa ajili ya mafunzo mengine,” alisema Mwalimu Tarimo.

Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara imeendelea na utaratibu wa kutoa elimu kwa wananchi wanaofika mahakamani kila wakati lakini pia kwa kupitia vyombo vya Habari vilivyopo hapa mkoani kwa lengo la kutimiza mahusiano bora kati ya Mahakama na wadau wanaosaidia utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Mahakama.

Walimu na wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara walipohudhuria mafunzo katika Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Sehemu ya wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakaifuatilia mada zilizokuwa zinafundishwa wakati wa mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wao kutoka kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Mmoja wa wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka akichangia mada wakati wa mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wao kutoka kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Walimu wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka (waliosimama) wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wao kutoka kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao akiendelea na mafunzo kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka waliofika katika Mahakama ya Wilaya ya Babati kwa ajili ya Mafunzo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Kimario (mwenye suti ya rangi ya buluu) akiendelea na mafunzo kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka waliofika katika Mahakama ya Wilaya ya Babati kwa ajili ya Mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava (aliyevaa suti nyeusi) akitoa Neno la Ukaribisho kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka waliofika katika Mahakama ya Wilaya ya Babati kwa ajili ya Mafunzo.



 

Jumatatu, 20 Julai 2026

WATUMISHI MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA ARDHI WAMUAGA JAJI MANDIA

  • Wamkaribisha pia Jaji Otaru

Na DHILLON UISSO – Mahakama Ardhi Dar es Salaam

Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, tarehe 17 Julai, 2026 walishiriki katika hafla ya kumuaga aliyekuwa Jaji Nehemia Mandia, Jaji, aliyehamishiwa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi.

Katika hafla hiyo, Waumishi pia walimkaribisha Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Monica Otaru, ambaye amehamia Divisheni ya Ardhi, maarufu udongoni.

Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi na kuhudhuriwa na Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Arafa Msafiri na baadhi ya Majaji na Naibu Wasajili, Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, pamoja na Watumishi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Msafiri alimpongeza Mhe. Mandi kwa ushirikiano, upendo na mchango mkubwa kipindi chote alichohudumu katika Divisheni ya Ardhi.

“Tunakupongeza sana Mhe. Mandia kwa uchapakazi, upendo na ushirikiano wako na ukawe balozi wetu huko. Wewe bado ni mwana udongoni,” alisema.

Kaimu Jaji Mfawidhi alitumia fursa hiyo kumkaribisha Mhe. Otaru kwa kujiunga na timu ya Divisheni ya Ardhi yenye upendo na ushirikiano mkubwa.

“Najua wewe ni mchapakazi na mwenye upendo mkubwa, karibu sana kwenye familia ya udongoni. Tutakupa ushirikiano na “team work,” Mhe. Msafiri alisema.

Kwa upande wake, Mhe. Mandia alitoa shukrani kwa Majaji, Viongozi wengine na watumishi wote aliobahatika kufanya nao kazi kwa kipindi chote. Alisema ushirikiano, upendo na mshikamano alioupata kutoka kwao ulichangia mafanikio yake katika kazi za kila siku.

Aliwaasa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, bidii na uaminifu, akisisitiza kuwa mafanikio katika utumishi yanatokana na kuipenda kazi na kutimiza wajibu kwa moyo wa kujituma.

Naye Mhe. Otaru alitoa neno la kushukuru kwa kukaribishwa na kuanza kushughulikia majalada kwa kasi na ushirikiano kutoka kwa Majaji, Viongozi na Watumishi kwa ujumla na kufanya kazi yake kuwa rahisi.

Majaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Nehemia Mandi na Mhe. Monica Otaru, wakikata keki.


Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Monica Otaru akitoa neno.

Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Arafa Msafiri, akimkabidhi Mhe. Mandia zawadi.

Majaji wa Mahakama Kuu wakifurahia jambo wakati wa hafla hiyo.

 Watumishi wa Divisheni ya Ardhi wakiwa kwenye hafla hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam. 

“UBORA WA MAHAKAMA UNAPIMWA NA WATENDAJI KAZI WAKE”

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Naibu Msajili ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga amesema ubora wa Mahakama unapimwa na Watendaji kazi wake na si majengo pekee.

Mhe. Kiswaga aliyasema hayo tarehe 17 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke alipokuwa akifungua Mafunzo ya siku moja ya namna ya kupokea Ushahidi wa kieletroniki hususan kwa Mahakama za Mwanzo za Wilaya yaliyotolewa kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo na Wilaya katika Wilaya za Temeke na Kigamboni.

Mhe. Kiswaga aliwakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuwa Mahakama haiwezi kuwa bora kuliko uwezo wa watendaji wake ambapo alisema, “ubora wa Mahakama ni namna watumishi wanavyowahudumia wananchi.”

Aliongeza kuwa, Wananchi hawawezi kuhudumiwa hewani bila kuwa na elimu na maarifa na kadri wanavyojifunza ndio wanaimarisha uaminifu wa wananchi kwa Mhimili wa Mahakama.

“Tunaishi zama ambazo teknolojia imebadili kila kitu, imebadili namna ya watu wanavyoishi, wanavyowasiliana na hata wanavyofanya biashara,” alisema Mhe. Kiswaga.

Aliongeza zaidi kwa kusema, “leo ushahidi unaoweza kuamua shauri unaweza kupatikana kupitia simu za mikononi, ujumbe mfupi mawasiliano ya WhatsApp, telegram, majukwaa mengine ya kidijitali CCTV rekodi za benki, miamala ya fedha kwa njia ya kielektoniki.”

Aidha, aliwapongeza Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Temeke na Kigamboni kwa kuona umuhimu wa kuandaa mafunzo hayo ili kuboresha utendaji kazi na kuendana na mabadiliko ya Sheria ya Ushahidi katika Mahakama za Mwanzo (The Magistrates Courts (Rules of Evidence in Primary Courts) (Amendment) Regulation, 2026 GN No. 143 iliyoongeza kanuni ya 8A.

Baada ya kufungua mafunzo hayo Mhe. Kiswaga alitoa mada ya juu wa kaulimbiu ya Mahakama na kuifafanua namna ambavyo kama Maofisa wa Mahakama wanatakiwa kuiishi.

Kadhalika Naibu Msajili huyo alieleza kuwa, Kanuni za Maadili za Maofisa wa Mahakama zinajengwa juu ya misingi sita ambayo ni uhuru wa Mahakama, kutokuwa na upendeleo, uadilifu, mwenendo unaofaa, usawa na umahiri.

Alipokuwa akifafanua maana ya Uadilifu na Uwajibikaji, Mhe. Kiswaga alieleza kuwa, Maofisa wa Mahakama kama Viongozi wanapaswa kujua namna bora ya kuaminiana wao kwa wao, watumishi wengine wasio Mahakimu pamoja na Wananchi.

Aliongeza kwa kusema kuwa, kama kuna mtumishi mwenye maadili yasiyofaa basi  Viongozi wajitahidi kumbadili na kuwa naye karibu ili aweze kubadilika na Viongozi  wasiathiriwe na matendo yake.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam Kisutu, Mhe. Romuli Mbuya alitoa mada juu ya uchukuaji, upokeaji na tathmini ya ushahidi wa kieletroniki hususan kwa Mahakama za Mwanzo kwa kuzingatia Kanuni ya 8A ya Kanuni za Ushahidi katika Mahakama za Mwanzo.

Mhe. Mbuya aliwasisitiza Mahakimu kusimamia mwenendo wa shauri wakati wa usikilizaji ikiwepo kumtaka Shahidi aweke msingi kwa kueleza chanzo cha ushahidi wake.

Aidha, katika Mafunzo hayo Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Temeke, Mhe. Frank Lukosi alitoa mada juu ya hatua za kuzingatia na namna ya kuendesha shauri la kuidharau Mahakama pale linapoibuka wakati wa usikilizwaji wa shauri.  

Katika mafunzo hayo, Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima alipata wasaa wa kuwakumbusha Mahakimu wa Mahakama za Wilaya juu ya mambo mbalimbali yaliyoboreshwa kwenye Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) ni pamoja kuwa na uwezo wa kuandaa wito kwa mashahidi (Summons), eneo la kuandika adhabu (sentence), sehemu ya kuweka vielelezo na kuandaa hati mbalimbali.

Pia katika Mfumo wa Mahakama za Mwanzo umeongeza watumiaji kwa mfano Polisi anaweza kufungua shauri Mahakama ya Mwanzo akiwa Polisi, lakini pia kwa mashauri ya madai mfumo utakuwa na uwezo wa kutengeneza namba za malipo (control number) na mashauri yatapewa namba kwenye mfumo na hii itapunguza matumizi ya rejesta ngumu.

Mfumo huo bado haujaanza kutumika, pindi utakapoanza kutumika matumizi ya karatasi na rejesta ngumu utapungua kwa kiwango kikubwa.

Alipokuwa akitoa neno la ukaribisho Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Temeke, Mhe. Vicky Mwaikambo alisema kuwa, wameandaa mafunzo hayo ili kuwajengea uwezo Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kuendana na mabadiliko ya Sheria ya Ushahidi yaliyofanyika hivi karibuni.

Akifunga mafunzo hayo kwa niaba ya Naibu Msajili, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuona umuhimu wa kuziruhusu Mahakama za Mwanzo kuweza kupokea ushahidi wa kielekroniki, kwani kwa sasa matumizi ya ushahidi huo hayakwepeki katika mfumo mzima wa utoaji haki.

Mafunzo hayo pia yaliwahusisha watumishi waliofanyiwa mabadiliko ya kada na kuwa Mahakimu kutoka Wilaya ya Temeke na Kigamboni ambapo mafunzo hayo yatawasaidia watakapopangiwa vituo vya kazi.

Sambamba na mafunzo hayo Mahakamu hao walipata wasaa wa kuwapongeza na Mahakimu waliofanyiwa mabadiliko ya kada kuwa Mahakimu kwa kukata keki maalum iliyoandaliwa ikiwa ni ishara ya upendo.

Naibu Msajili ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya namna ya kupokea Ushahidi wa kieletroniki hususan kwa Mahakama za Mwanzo za Wilaya yaliyotolewa kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo na Wilaya katika Wilaya za Temeke na Kigamboni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke.

Washiriki wa Mafunzo wakifuatilia mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Temeke, Mhe. Vicky Mwaikambo akitoa neno wakati wa mafunzo hayo.

Naibu Msajili kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam-Kisutu, Mhe. Romuli Mbuya akitoa mafunzo ya namna ya uchukuaji, upokeaji na tathmini ya Ushahidi wa Kielektroniki.

Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaama Bw. Tumain Malima akiwakumbusha Mahakimu namna ya kutumia Mfumo na kuwaeleza baadhi ya maboresho yaliyofanyika katika mfumo wa kusikiliza mashauri.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib akitoa neno la kufunga mafunzo hayo.
Naibu Msajili na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam-Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Temeke na Kigamboni. Aliyeketi kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Temeke, Mhe.Vicky Mwaikambo  na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama wa Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib.
Mahakimu Wakazi Wafawidhi, Mhe. Vicky Mwaikambo wa Temeke (kushoto) na Mhe. Mwanakombo Twalib wa Kigamboni (kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Watumishi waliobadilishwa Kada hivi karibuni kuwa Mahakimu Wakazi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 


 

 

 

 

 

 

 

 

 

MAHAKAMA MOROGORO YAFANYA KIKAO CHA MENEJIMENTI, UONGOZI

Na. ASHA JUMA-Mahakama Morogoro.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, imefanya kikao cha menejimenti na uongozi kilicholenga kutathmini utendaji wa Mahakama, kujadili changamoto mbalimbali pamoja na kuweka mikakati ya kuendelea kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Kikao hicho kilifanyika tarehe 17 Julai, 2026  katika ukumbi wa mikutano uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro, na kuongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Rose Ebrahim, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kikao hicho.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Majaji wa Mahakama Kuu Morogoro, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Morogoro, Mtendaji wa Mahakama Morogoro, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya, pamoja na Viongozi na Maafisa kutoka vitengo mbalimbali, wakiwemo Maafisa Utumishi, Afisa TEHAMA, Afisa Ugavi na Mkaguzi wa Ndani.

Miongoni mwa ajenda zilizojadiliwa ni tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, hususan kuhusu uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama. Kikao kilibaini kuwa changamoto zilizokuwa zikihusu upatikanaji wa maji, umeme na huduma za mtandao katika baadhi ya Mahakama zimefanyiwa kazi kwa kiwango kikubwa.

Aidha, kikao kilijadili namna ya kuboresha utaratibu wa upokeaji wa taarifa kutoka Taasisi mbalimbali, ikiwemo Jeshi la Magereza, pamoja na kufanya tathmini ya hali ya miundombinu katika Mahakama mpya ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu kama maji, umeme na mawasiliano ya mtandao kwa ajili ya kuongeza ufanisi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Jaji Mfawidhi aliwataka Viongozi na Watumishi kuendelea kushirikiana katika kujenga mazingira bora ya kazi na kuimarisha mawasiliano ndani ya Taasisi.

"Vikao hivi ni kama vikao vya kifamilia au vya kitaasisi. Morogoro tunaamini katika uwazi na mawasiliano mazuri, hivyo naomba ushirikiano wa Viongozi na Watumishi wote ili kwa pamoja tuendelee kuijenga Mahakama ya Morogoro kuwa mfano wa utendaji bora," alisema Mhe. Ebrahim.

Akiwasilisha taarifa ya uongozi na utendaji, Mtendaji wa Mahakama Morogoro, Bw. Ahmed Ngéni, alieleza hali ya majengo, utekelezaji wa miradi mipya pamoja na hali ya vyombo vya usafiri katika Mahakama hiyo.

Aidha, alibainisha kuwa miongoni mwa changamoto zinazoikabili Mahakama hiyo ni upungufu wa watumishi uliotokana na baadhi yao kubadilishwa kada, hali ambayo imeathiri utekelezaji wa baadhi ya majukumu.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Morogoro, Mhe. Amiri Msumi, akiwasilisha taarifa ya hali ya mashauri, alisisitiza matumizi sahihi ya mifumo ya uendeshaji wa mashauri, utunzaji wa vielelezo na uingizaji wa taarifa sahihi katika mifumo mbalimbali ya uendeshaji wa mashauri.

Mhe. Msumi alisema kuwa wanaendelea kufanya vizuri katika kupunguza mashauri ya mlundikano, kwani mengi yanamalizika kwa wakati na ipo haja ya kuandaa mipango ya kimkakati ambayo itaweka mfumo wa kujitathmini, kurekebisha maeneo yanayoonekana kuwa na mapungufu na kuboresha namna na kasi ya utekelezaji wa majukumu yao.

Nasisitiza kuwa jukumu mama la Mahakama ni kusikiliza na kufanya maamuzi mapema iwezekanavyo ili kuepusha mlundikano wa mashauri mahakamani, matumizi sahihi ya mifumo ya kielektroniki na tukumbuke kuingiza taarifa sahihi katika mifumo hiyo kwani taarifa zisizo sahihi zinaweza kusababisha wananchi kukosa haki zao," alisema Mhe. Msumi.

Akihitimisha kikao hicho, Jaji Mfawidhi aliwashukuru Majaji, Mahakimu na Viongozi wote walioshiriki kikao hicho kwa michango yao. Aliwasisitiza kuendelea kuzingatia misingi ya uongozi bora, uwajibikaji na kufuata taratibu za kazi ili kuhakikisha haki inatendeka kwa wananchi.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa Watumishi wa Mahakama, huku akiahidi kuandaa ratiba maalumu ya kufanya ukaguzi katika Mahakama zote zilizopo Morogoro ili kutambua na kutatua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, akizungumza wakati wa kikao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ibrahim, (aliyekaa katikati), akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga (kushoto) na Mhe. Aisha Sinda (kulia).

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Morogoro, Mhe. Amiri Msumi, akisoma taarifa ya mashauri katika kikao hicho.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage, akichangia mada katika kikao hicho.

Mtendaji wa Mahakama Morogoro, Bw. Ahmed Ng’eni, akisoma taarifa ya utendaji katika kikao hicho.

Wajumbe wa kikao cha menejimenti ya Mahakama Morogoro wakifuatilia taarifa mbalimbali wakati wa kikao.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.