Alhamisi, 3 Septemba 2026

WADAU WA MAHAKAMA MOSHI WAPATIWA MAFUNZO YA MFUMO WA e-CMS

 · Wafundishwa jinsi ya kupakua Nakala za Hukumu na mienendo ya mashauri kupitia mfumo huo

· Wasisitizwa juu ya matumizi ya TEHAMA

Na PAUL PASCHAL, Mahakama-Moshi

Wadau wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Moshi wamepatiwa Mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Ki-elektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyolenga kuwaelekeza juu ya upandishwaji wa mashauri, upakuaji wa taarifa mbalimbali za kimahakama kama upakuaji wa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri.

Mafunzo hayo ambayo yametolewa kwa Wadau kutoka Magereza, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Waendesha Mashtaka wa Serikali yamefanyika leo tarehe 03 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mdogo wa mikutano wa Mahakama Kuu Moshi.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje na mada kuu ikiwasilishwa na Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Moshi, Bi Catherine Mugyabuso.

Akizungumza wakati ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Mwaiseje alisisitiza juu ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya kusaidia uendeshaji wa shughuli za Kimahakama kwa haraka na weledi katika kurahisisha upatikanaji wa taarifa za mashauri kama vile upatikanaji wa nakala za hukumu na mienendo ya shauri kwa haraka na kwa unafuu kupitia Mfumo wa e-CMS ili kuepuka malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa Mahabusu au Wafungwa.

“Ndugu washiriki tumewaita hapa leo ili kuwaongezea maarifa kidogo juu ya maboresho yaliofanyika na yanaoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha ufanisi na weledi katika jukumu zima la utoaji haki nchini kupitia mifumo yetu ya kimahakama huduma zetu zimeboreka na kurahisishwa ili kuondoa malalamiko kwa wote tunaowahudumia,” amesema Mhe. Mwaiseje.

Amewaeleza washiriki hao wa mafunzo kuwa, wao kama Wadau muhimu wa Mahakama katika kuwahudumia Watanzania ni vema nao wakapata ujuzi na kuwa na uelewa wa pamoja katika matumizi ya mfumo huo wa e-CMS.

Ameongeza kuwa, mfumo huo unaosimamia Mashauri Mahakamani    unalenga kuimarisha utoaji haki mapema ipasavyo na kwamba kupitia mfumo huo  kwa upande wa Mahakama Kuu Moshi kwa sasa  haitumii karatasi kupata nakala za hukumu na mwenendo wa shauri bali zinapatikana kupitia kwenye mfumo.

Mshiriki Suzan Kimaro ambaye ni Ofisa Mpelelezi Mkuu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kilimanjaro ameushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Moshi kwa maandalizi mazuri ya mafunzo hayo yanayokwenda kuwajenga na kuwaongezea uwezo wa ufanisi katika kutimiza majukumu yao.

“Kwa niaba ya Washiriki wote nipende kuishukuru Mahakama kwa mafunzo haya kwani yametupa mwanga mzuri wa namna ambavyo tunaweza kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi na weledi kupitia mfumo huu wa e-CMS hii itatusaidia sana kuwahudumia wananchi kwa haraka na pasipo na malalamiko yasio ya msingi,” amesema Bi. Suzan.

Washiriki kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Moshi, Magereza na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kilimanjaro kwa pamoja wakifuatilia mada iliyokuwa ikiwasilishwa wakati wa mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Moshi leo tarehe 03 Septemba, 2026.

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Moshi, Mhe.Sekela Mwaiseje akieleza akifungua mafunzo hayo na kueleza lengo la kufanyika kwa mafunzo hao kwa washiriki walioalikwa (hawapo katika picha).

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Moshi, Mhe. Opportuna Kipeta (aliyevaa miwani) pamoja na Hakimu Mkazi Mkuu Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, Mhe. Herrieth Mhenga (kulia) wakifuatilia mafunzo hayo.

Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Moshi, Bi. Catherine Mugyabuso akitoa Mada kwa washiriki wa Mafunzo kuhusu matumizi wa e-CMS (hawapo katika picha).


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)

 

Jumatano, 2 Septemba 2026

TMJA GEITA, BUKOBA WAIMARISHA UJIRANI MWEMA, USHIRIKIANO

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Geita

Tawi la Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Geita, tarehe 28 Agosti, 2026 lilipokea ugeni kutoka Tawi la TMJA Bukoba kwa lengo la kuimarisha ujirani mwema, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanachama katika kutekeleza majukumu yao ya kimahakama na kijamii.

Ugeni huo uliwasili na kuongozwa na Mlezi wa Tawi la TMJA Bukoba, Jaji Mfawidhi, Mhe. David Patrick Ngunyale. Ugeni huo ulipokelewa na Mlezi wa Tawi la TMJA Geita, Jaji Mfawidhi, Mhe. Projestus Kahyoza.

Katika ziara hiyo, Majaji na Mahakimu kutoka matawi hayo walishiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii na michezo, zikiwemo matendo ya huruma katika Hospitali ya Wilaya ya Geita, bonanza la michezo mbalimbali pamoja na chakula cha jioni.

Siku ya pili yake, yaani tarehe 29 Agosti, 2026 bonanza la michezo lilifanyika katika viwanja vya Geita Gold Mining Limited (GGML), likihusisha michezo mbalimbali, ikiwemo mpira wa miguu, mpira wa pete, mbio za yai na kijiko, kufukuza kuku  pamoja na mchezo wa karata.

Katika michezo hiyo, washiriki walionesha ushindani wa hali ya juu, huku wakidumisha mshikamano na urafiki. Bonanza hilo lililenga kutumia michezo kama fursa ya kujenga urafiki na mshikamano baina ya wanachama, kuimarisha afya na ustawi wa wanachama, pamoja na kuimarisha mahusiano ya kikazi na kikanda katika utendaji wa huduma za umma.

Baada ya kumalizika kwa shughuli za Bbonanza na kuagana na wageni kutoka Bukoba, tarehe 30 Agosti 2026, Tawi la TMJA Geita lilifanya Mkutano Mkuu wa Tawi katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Geita.

Mkutano huo ulilenga kujadili masuala mbalimbali yanayohusu utendaji wa chama, ustawi wa wanachama pamoja na namna ya kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa shughuli za kimahakama.

Akifungua Mkutano Mkuu huo, Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa viongozi kuwa mstari wa mbele katika kuonesha mfano bora wa uongozi, ushirikiano na uwajibikaji.

Mhe. Kahyoza aliwataka viongozi kutanguliza maslahi ya chama na kuwa mfano katika kutekeleza majukumu yao, akieleza kuwa uongozi bora ni msingi wa kujenga chama imara chenye uwezo wa kuwahudumia wanachama wake kwa ufanisi.

Akitoa taarifa ya shughuli za chama, Katibu wa TMJA Geita, Mhe. Ally Mgomba, alisema kuwa tawi limeendelea kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii kwa kushirikiana na Ofisi ya Mlezi wa Tawi.

Alisema TMJA Geita imekuwa ikitoa mchango na kuwafariji wanachama wakati wa misiba, kushiriki katika matukio ya furaha, pamoja na kutekeleza shughuli mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuwasaidia watu wenye mahitaji.

Miongoni mwa shughuli hizo ni ziara katika Shule yenye Mahitaji Maalumu Bukoba, ziara katika Magereza ya Wilaya ya Chato, ziara za ujirani mwema kati ya matawi na kanda mbalimbali, ikiwemo Bukoba na Kigoma, pamoja na ziara ya utalii katika Mgodi wa Geita Gold Mining Limited (GGML), iliyotanguliwa na shughuli za matendo ya huruma katika Hospitali ya Wilaya ya Geita.

Katika taarifa yake, Katibu huyo alieleza kuwa tawi limepata mafanikio mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa ushirikiano kati ya wanachama na uongozi wa tawi, pamoja na kuendelea kushirikiana katika kuwasaidia watu wenye changamoto na kushiriki katika matukio mbalimbali ya furaha ya wanachama.

Aidha, tawi limefanikiwa kuimarisha mfuko wake, kufanya ziara mbalimbali za kujenga mahusiano na ushirikiano na kupata tuzo mbalimbali kutokana na shughuli zake.

Pamoja na mafanikio hayo, Mhe. Mgomba alibainisha kuwa moja ya changamoto zinazolikabili tawi ni ushiriki mdogo wa wanachama katika mazoezi ya mwili. Alieleza kuwa hali hiyo inaweza kuathiri ushiriki wa wanachama katika shughuli za michezo na juhudi za kuimarisha afya na ustawi wao.

Kwa ujumla, ziara ya TMJA Bukoba pamoja na Mkutano Mkuu wa TMJA Geita imekuwa fursa muhimu ya kuimarisha ujirani mwema, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanachama.

Aidha, shughuli hizo zimetoa nafasi kwa wanachama kubadilishana uzoefu, kujadili mafanikio na changamoto, pamoja na kuweka mikakati ya kuimarisha chama na ustawi wa wanachama wake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza akiwakaribisha wageni kutoka Kanda ya Bukoba kushiriki hafla ya ujirani mwema.

Picha ya pamoja kati ya TMJA Geita na TMJA Bukoba baada ya kuwasili katika Mahakama Kuu Geita.


Wenyeviti wa TMJA Geita na Bukoba wakikabidhi baadhi ya sabuni na mafuta kwa Madakitari wa Hospitari ya Wilaya ya Geita.

Picha ya pamoja kati ya TMJA Geita na Bukoba katika mgodi wa madini wa Geita.

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Geita (juu) ikiwa katika picha kabla ya kuanza mchuano na timu ya Mgodi wa Geita iliyopo hapo chini.


Timu ya kuvuta kamba kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Bukoba ikivutana na Timu ya Mgodi wa Geita.


Uongozi wa TMJA Geita na Bukoba pamoja na Mgodi wa Geita ukiwa katika picha ya pamoja na wachezaji wa Mahakama Kuu Bukoba baada ya kuwakabidhi kombe.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.









JAJI MFAWIDHI MUSOMA AMUAPISHA AFISA USULUHISHI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki, tarehe 31 Agosti, 2026 alimwapisha Bw. Said Mmbando, kuwa Afisa Usuluhishi II.

Uapisho huo ulifanyika ofisini kwa Jaji Mfawidhi na kushuhudiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw. Leonard Maufi, pamoja na Msuluhishi Mkuu II, Bw. Peter Mahindi.

Pamoja na uapisho huo, Mhe. Kakolaki alitoa nasaha kwa Bw. Mmbando kufanya kazi hiyo bila upendeleo, huba au chuki. Alimsihi siku zote atambue kuwa kazi ya uamuzi ni kazi ya Mungu, hivyo aifanye kwa uadilifu na weledi mkubwa kwa zingatia sheria, taratibu na miongozo iliyopo.

Uapisho wa Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (kulia), mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (aliyesimama katikati), ukishuhudiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw, Leonard Maufi, pamoja na Msuluhishi Mkuu II, Bw. Peter Mahindi.

Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (kulia) akisaini kiapo chake mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto), akisaini kiapo cha Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (katikati) wakati Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia) akishuhudia tukio hilo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto), akimkabidhi hati ya kiapo Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (katikati) wakati Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (wa pili kulia) pamoja na Msuluhishi Mkuu, Bw. Peter Mahindi (wa kwanza kulia) wakishuhudia tukio hilo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

 

 

MAHAKAMA YA RUFANI YAFANIKIWA KUSIKILIZA ASILIMIA 82 YA MASHAURI ARUSHA

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Arusha

Kikao cha nne cha Mahakama ya Rufani kwa mwaka, 2026 kilichoketi Arusha kuanzia tarehe 03 hadi 28 Agosti, 2026 kimefanikiwa kusikiliza jumla ya mashauri 31 kati ya 38 yaliyopangwa, sawa na asilimia 82 ya mashauri yote.

 Jopo la Majaji wa kikao hicho kiliongozwa na Mhe. Lilian Mashaka huku Majaji wengine wakiwa Mhe. Gerson Mdemu, na Mhe. Imani Aboud.

Akiwasilisha taarifa ya Tathmini ya Kikao hicho cha Mashauri ya Rufani hivi karibuni, Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Flora Mtarania alisema kuwa, mashauri 38 yalipangwa kusikilizwa ambapo kati ya hayo, 12 yalikuwa Rufaa za Jinai, 25 Rufaa za Madai, na moja ilikuwa Maombi ya Madai. Idadi ya mashauri yaliyosikilizwa ni 31 na mashauri yaliyoahirishwa ni 7.

Mhe. Mtarania ameongeza kwa kusema kuwa, Mashauri saba yaliyoahirishwa ni kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kukosekana kwa nyaraka muhimu za Baraza la Ardhi, Vifo kwa baadhi ya Wadaawa na Wasimamizi wa Mirathi kutoongezwa shaurini, kukosekana kwa wadaawa katika anuani zilizowekwa kwenye rekodi za rufaa na kutofautiana kwa majina ya wadaawa kwenye nyaraka za Mahakama Kuu.

Naibu Msajili huyo aliyataja mafanikio kadhaa yaliyopatikana katika kikao hicho kuwa ni pamoja na Mashauri yaliyopangwa kusikilizwa na kumalizika kwa asilimia 82, Wadaawa wote waliopata wito walihudhuria mahakamani kwa wakati, hivyo kuwezesha usikilizaji wa mashauri kwa wakati na Maamuzi yaliyosomwa kutolewa kwa wadaawa kwa wakati na kupandishwa katika Maktaba Mtandao ya Mahakama (TanzLII).

Kikao hicho cha Mashauri ya Mahakama ya Rufani Kanda ya Arusha kilifanyika sanjari na vikao vingine tisa katika Kanda za Mwanza, Shinyanga, Moshi, Bukoba, Dar es Salaam, Iringa, Mbeya, Sumbawanga na Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Jopo la Majaji, Mhe. Lillian Mashaka akiongoza Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Aboud. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi (IJC) Arusha.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu (kushoto) akifafanua mambo kadhaa wakati wa Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akichangia jambo wakati wa Kikao hicho. Aliyeketi upande wa kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Aisha Bade. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi (IJC) Arusha.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Seif Kulita akichangia jambo wakati wa Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Nyigulila Mwaseba. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Flora Mtarania akiwasilisha Taarifa ya Tathmini ya Kikao cha Mashauri ya Mahakama ya Rufani kilichofanyika mkoani Arusha.



Wajumbe mbalimbali waliohudhuria Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)

 

 

MAHAKAMA KUU NJOMBE YAMUAGA BI. GRACE MTEMELA ALIYESTAAFU UTUMISHA WA UMMA

  •  Adumu katika Utumishi wa Umma kwa miaka 42 

 Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Njombe imefanya hafla fupi ya kumuaga aliyekuwa Mtumishi wa Mahakama hiyo, wake, Bi. Grace Mtemela, aliyestaafu utumishi wa umma.

Hafla ya kumuaga Mtumishi huyo aliyekuwa akihudumu katika Kada ya Msaidizi wa Ofisi ilifanyika tarehe 31 Agosti, 2026 iliandaliwa na Ofisi ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Njombe.

Bi. Mtemela alianza kuhudumu Mahakama ya Tanzania mwaka 1984, katika kipindi cha miaka 42 ya utumishi wake, amewahudumia Viongozi na Maofisa mbalimbali wa Mahakama, wakiwemo Mahakimu Wafawidhi wa Wilaya mkoani Njombe. Aidha, amestaafu akiwa anahudumu katika Ofisi ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Njombe.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Njombe, Bw. Richard Mbambe, aliwakaribisha watumishi wa Mahakama na kutoa neno la shukrani kwa mstaafu huyo kwa utumishi wake na mchango wake katika Mahakama.

Naye, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa, alimpongeza Bi. Mtemela kwa kumaliza salama kipindi chake cha utumishi wa umma.

“Tunashukuru kwa huduma yako katika kipindi cha miaka 42 katika utumishi wa Mahakama. Wewe utabaki kuwa sehemu ya familia ya Mahakama.Tutakapokuhitaji, usisite kutusikiliza, na pia kama utatuhitaji, usisite kuja. Wewe bado ni mtumishi wa Mahakama,” alisema Mhe. Nongwa.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, alimshukuru Bi. Mtemela kwa kipindi chote alichohudumu katika ofisi yake. Pia aliwataka watumishi wengine kujifunza kutokana na nidhamu, kujituma na uzoefu aliouonesha katika kipindi cha utumishi wake. 

Akizungumza katika hafla hiyo, Bi. Mtemela aliwashukuru Viongozi na Watumishi wa Mahakama kwa kujitolea kufika katika hafla hiyo na kwa kumuandalia tukio hilo pamoja na kumpatia zawadi mbalimbali. Alieleza kuwa hakutarajia kuandaliwa hafla hiyo kwa namna hiyo.

Mstaafu huyo alionesha kufurahishwa na tukio hilo na kuwaomba radhi viongozi na watumishi wenzake endapo kuna wakati aliwahi kutenda jambo kinyume na taratibu au kusababisha usumbufu katika kipindi cha utumishi wake. Aidha, aliwatakia kila la heri watumishi wote wanaoendelea na utumishi wa Mahakama.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Njombe, imemtakia Bi. Grace Mtemela afya njema na maisha mema katika kipindi chake kipya cha kustaafu.


Mtumishi Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Bi.Grace Mtemela (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili Mhe.Joseph Luambano (wa pili kulia) pamoja na Watumishi wengine wa Mahakama hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Jumanne, 1 Septemba 2026

JAJI MWENDA ANGOZA ZOEZI LA USAFI SINGIDA

Na EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda tarehe 29 Agosti, 2026 aliwaongoza watumishi katika zoezi la usafi ikiwa ni jitihada za kuhakikisha mazingira yanakuwa safi licha ya kuwa na watoa huduma ya usafi sambamba na kujenga utamaduni wa kutunza mazingira na kujenga mahusiano mazuri baina ya watumishi na kuimarisha umoja.

Akizungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu Singida aliwaeleza kuwa, zoezi hilo ni endelevu na litakuwa likifanyika kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi likihusisha hadi Mahakama za ngazi za chini.  

“Watumishi wenzangu kufanya usafi ni mojawapo ya mazoezi ya viungo lakini pia ni utaratibu mzuri kwani unaimarisha umoja na mshikamano mahala pa kazi na pia kila mmoja wetu atakuwa balozi katika masuala ya utunzwaji wa mazingira kama tulivyoona usafi sio jambo rahisi na zoezi litakuwa endelevu na litahusisha Mahakama ngazi za chini,” alisema Mhe. Mwenda.

Mahakama zilizofanya usafi kwa siku hiyo ni pamoja na Mahakama ya Wilaya Singida, Mahakama ya Wilaya Manyoni, Mahakama ya Mwanzo Itigi, Mahakama ya Mwanzo Mgandu, Mahakama ya Mwanzo Ikungi, Mahakama ya Mwanzo Ipembe na Mahakama ya Mwanzo Utemini.

Aidha, watumishi wamefurahishwa na zoezi hilo ambalo limeleta tija kwa kuonesha jukumu la usafi ni la wote hivyo, wameahidi kuwa mabalozi wazuri katika utunzaji wa Mazingira.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akiwaongoza Watumishi wa Mahakama hiyo kufanya usafi tarehe 29 Agosti, 2026.

  
   Watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Singida wakiwa katika usafi wa Pamoja uliofanyika katika jengo la Mahakama Kuu tarehe 29 Agosti,2026.


 Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Singida, Mhe. Fadhili Luvinga akifanya usafi.

Msaidizi wa Kumbukumbu  Mahakama ya Mwanzo Ikungi, 
Bi. Magreth Mtilimbania akiwa katika zoezi la usafi.

  Mhe. Aggrey Muhigi wa Mahakama ya Mwanzo Mgandu akifanya usafi.

  Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Manyoni kwa wakiendelea kufanya usafi kwa pamoja.


Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Itigi, Bi.Mwajuma Sudi akiwa katika zoezi la kufanya usafi.

  Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Utemini Singida wakiendelea na zoezi la kufanya usafi kwa pamoja.


  Watumishi wa Mahakama Kuu Singida wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuhitimisha zoezi la usafi. Aliyesimama mstari wa kwanza wa tatu kulia ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda, kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Singida, Mhe. Fadhili Luvinga, wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Singida, Bw. Filbert Matotay, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida, Mhe. Aloyce Masua na wa pili kushoto ni Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Mariam Hamisi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


MWAKA MMOJA WA MAHAKAMA YA MWANZO TERRAT; WAJA NA MAFANIKIO KIUTENDAJI

  • Kiwango cha Uondoshaji mashauri chafurahisha

 Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Mahakama ya Mwanzo Terrat ni miongoni mwa Mahakama za Mwanzo mpya katika Wilaya ya Arusha na miongoni mwa mafanikio makubwa katika juhudi za kuboresha huduma za Mahakama ili kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi. 

Mahakama hii imekuwa chachu muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki kwa urahisi, ufanisi na mapema ipasavyo.

Mahakama ya Mwanzo Terrat ilianza rasmi kutoa huduma tarehe 20 Agosti, 2025, na sasa imetimiza mwaka mmoja tangu kuanza kwa safari yake ya kuhudumia wananchi.

Katika kipindi hicho, Mahakama imeendelea kutekeleza wajibu wake kwa uadilifu na weledi, huku ikiwa sehemu muhimu ya mageuzi na maboresho yanayoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza na Mwandishi wetu, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Mhe. Salma Mwamende amesema kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanza, Mahakama ya Mwanzo Terrat imepokea jumla ya mashauri 974. Kati ya mashauri hayo, mashauri 954 yamesikilizwa na kutolewa uamuzi, huku mashauri 20 yakiendelea.

“Kwa mwaka huu wa 2026, kwa kipindi cha Januari hadi Agosti, tumepokea jumla ya mashauri 604 na tayari tumemaliza mashauri 604 na mashauri 20 yanaendelea kusikilizwa, Mahakama yetu ina Mahakimu wawili lakini tunachapa kazi kuhakikisha tunaendana na wingi wa mashauri yanayokuja katika Mahakama yetu,” alisema Mhe. Mwamende.

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento alieleza kuwa, takwimu hizo za mashauri ya Mahakama ya Terrat zinaonesha kiwango cha juu cha ufanisi katika utoaji wa huduma za haki, ambapo Mahakama hiyo imeweza kumaliza zaidi ya asilimia 97.9 ya mashauri yote yaliyopokelewa, na kubakiza takribani asilimia 2.1 ya mashauri yanayoendelea.

“Mahakama hiyo imeweza kusikiliza na kumaliza mashauri ndani ya wastani wa wiki tatu, muda ambao ni mfupi ikilinganishwa na muda wa miezi mitatu unaotajwa katika miongozo kwa mashauri ya Mahakama za Mwanzo kwa shauri kusajiliwa hadi kuamuliwa. Mafanikio haya yanaonesha jitihada za Mahakama katika kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa wakati na wananchi wanapata haki kwa haraka,” alisema Mhe. Manento.

Takwimu hizo zinaonesha kuwa, katika mwaka wake wa kwanza, Mahakama ya Mwanzo Terrat yenye Mahakimu wawili tu, imeweza kutekeleza kwa ufanisi jukumu lake la msingi la kutoa haki kwa wananchi mapema ipasavyo, huku ikidhibiti mlundikano wa mashauri na kuhakikisha muda wa usikilizwaji wa mashauri unapungua.

Mwaka mmoja wa Terat ni zaidi ya kumbukumbu kwani umekuwa mwaka wa mafanikio, huduma na matumaini mapya hasa kwa wananchi wa Kata za Terrat, Muriet, Elerai na Sokoni 1.

Mafanikio hayo ni matokeo ya maono na juhudi za Uongozi wa Mahakama ya Tanzania wakishirikiana na wadau wake wote katika kuhakikisha kuwa huduma za haki zinasogezwa karibu na wananchi na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.


Jengo la Mahakama ya Mwanzo Terrat ambalo limetimiza mwaka mmoja tangu lianze kutumika kutoa huduma.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento alipotembelewa na Mwandishi wetu ofisini kwake tarehe 31 Agosti, 2026 kuzungumzia kuhusu Mahakama ya Mwanzo Terrat kutimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Mhe. Salma Mwamende alipotembelewa na Mwandishi wetu ofisini kwake tarehe 31 Agosti, 2026 kuzungumzia Mahakama hiyo kutimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama ya Mwanzo Terrat; Mhe. Salma Mwamende (kushoto) na Mohamed Nyenye (kulia).

Picha ya pamoja; Wa kwanza kushoto ni Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento katikati ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Salma Mwamende, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Mohamed Nyenye, wa pili kushoto ni Kaimu Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Bw. Sunday Kilimba pamoja na Watumishi wengine wa Mahakama hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)