Jumanne, 4 Agosti 2026

MAHAKAMA YA RUFANI KUENDESHA MASHAURI 38 YA MADAI, JINAI MASJALA NDOGO MBEYA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Rufani ya Tanzania inayoketi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya imeanza kuendesha Kikao chake cha kusikiliza mashauri 38 ya rufaa za madai na jinai ambacho kimeanza jana tarehe 03 Agosti, 2026 na kinatarajiwa kuhitimishwa mnamo tarehe 29 Agosti, 2026.

Kikao hicho kinachoongozwa na Jopo moja la Majaji wa Mahakama ya Rufani ambalo Mwenyekiti wake ni Jaji wa Rufaa ya Tanzania ya Tanzania, Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika, Majaji wengine katika Jopo hilo ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Benhajj Shaban Masoud na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina.

Akiwasilisha taarifa katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya, ambacho ni kikao cha maandalizi ya uendeshaji wa kikao hicho (Pre- Session Meeting), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernad Mpepo alisema kuwa, jumla ya mashauri 38 ya rufaa za madai na jinai yamepangwa kusikilizwa katika Masjala Ndogo ya Mbeya ikiwa rufaa za madai ni 27 na rufaa za jinai 11.

Aidha, Mhe. Mpepo aliongeza kuwa, Katika kikao hicho kinachoketi Mbeya pia kuna mashauri kutoka Kanda za Songwe, Tabora na Iringa na katika kuhakikisha ufanisi wa kikao hicho na kufikiwa kwa malengo yaliyokusudiwa ratiba ya kikao ilitolewa kwa wakati na hati za kuitwa shaurini za wadaawa kwa ajili ya usikilizwaji wa mashauri zimesambazwa na juhudi za kuwapata wadaawa amabao hawajapatikana zinaendelea.

Naye, Mwenyekiti wa kikao hicho, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika, alisisitiza kuhusu kuzingatia upachikaji wa nyaraka zote muhimu zinazohitajika hasa nyaraka zinazopandishwa kielektroniki kuhakikisha kuwa, zinaambatanishwa pia kama nyaraka ngumu kwenye vitabu na majalada husika.

Aidha, Mhe. Dkt. Ndika alihitimisha kwa kuomba ushirikiano baina ya wadau na kusisitiza kufuata kanuni na sheria ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

“Ninawashukuru sana kwa kuhudhuria kwenu, tufuate kanuni na tushirikiane ili tufikie mafanikio yaliyokusudiwa. Lengo letu ni kutafuta haki kwa pamoja na ni matarajio yetu kuwa, kutokana na kwamba mpango wa kusikiliza mashauri haya uliandaliwa mapema pamoja kwa ufuatiliaji wa karibu wa kila jalada, kikao hiki kitafikia malengo yaliyokusudiwa bila akukwama,” alisema Mhe. Dkt. Ndika.

Kwa upande wao Jeshi la Magereza kupitia mwakilishi wa Mkuu wa Gereza Ruanda Mbeya alisema kuwa, watahakikisha wafungwa wanafikishwa kwa wakati mahakamani na watahakikisha wanatoa kibali kwa mawakili kuwaona wateja wao walipo gerezani hata kwa siku za mapumziko ambazo ni jumamosi na jumapili ili kuweka utaratibu sawa.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya akiwemo Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernad Mpepo, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Mawakili na Wadau wengine wa Haki Jinai na madai kutoka Mbeya, Songwe na Tabora.

Mwenyekiti wa jopo la Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika, (katikati) akiongoza kikao cha wadau cha uendeshaji wa shauri ya rufaa za Mahakama ya Rufani, kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina na kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Benhajj Shaban Masoud

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernad Mpepo akiwasilisha taarifa ya mashauri yanayotarajiwa kusikilizwa katika kikao hicho.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiongozwa na (wa kwanza kulia) ambaye ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo (aliyesimama katikati) na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kushoto).

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho

Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili wa Kujitegemea Tanganyika (TLS) Chapta ya Mbeya wakili msomi Bw. Philip Mwakilima akizungumza jambo katika kikao hicho.

Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani Tanzania wakipokelewa na Waheshimiwa Majaji, Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya walipowasili katika viwanja vya Mahakama hiyo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha- Mahakama)







JAJI MFAWIDHI NJOMBE AZINDUA JENGO LA MAHAKAMA YA MWANZO LUPEMBE

·       Azindua pia Vifaa vya TEHAMA awakabidhi Mahakimu na Watumishi wengine wa Mahakama

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amezindua Mahakama ya Mwanzo Lupembe katika Wilaya ya Njombe baada ya ujenzi wake kukamilika na shughuli zake zikiendelea.

Uzinduzi wa Mahakama hiyo ulifanyika hivi karibuni sambamba na uzinduzi wa vifaa vya Teknolojia ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kugawa vishikwambi kwa Mahakimu na Maofisa wa Mahakama pamoja na kwa Watumishi mbalimbali.

Uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe lenye vifaa vya kisasa vya TEHAMA unalenga kuimarisha upatikanaji haki kwa wananchi mapema ipasavyo na kwa gharama nafuu.

Katika hafla hizo za uzinduzi wa jengo hilo pamoja na uzinduzi wa ugawaji wa Vifaa vya TEHAMA, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Njombe alizungumzia kuhusu dhima ya Mahakama katika kutoa haki kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji bila kuchelewesha huduma za msingi kwa Wananchi.

Mhe. Nongwa, aliwaasa Watumishi waweze kutumia vifaa vya TEHAMA pamoja na kuvitunza ambapo alizungumza na Wananchi wa Lupembe wa maeneo hayo kuhakikisha wanatunza jengo hilo na miundombinu yake ili liweze kudumu kwa muda mrefu kwa kuwa jengo hilo limetokana na kodi za wananchi wenyewe.

“Kuanzishwa kwa Mahakama hii kutasaidia kupunguza msongamano wa mashauri na kuharakisha utoaji haki, hatua hii ni sehemu ya juhudi za Mahakama ya Tanzania na Serikali ya Tanzania kuhakikisha kila Mwananchi anapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu,” alisema Jaji Nongwa.

Mhe. Nongwa aliongeza kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Msajili Mkuu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Njombe kwa kuwezesha na kusimamia ujenzi wa jengo hilo.

Kwa upande wake, Mgeni Maalum katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Mhe. Juma Swedi aliwaasa wananchi kushirikiana na Watumishi wa Mahakama kwa ajili ya kulinda msingi wa amani na kudumisha ustawi wa utoaji haki kwa wananchi.

“Hii Mahakama ni mali yetu, hivyo ni wajibu wetu sote kushirikiana na kutunza jengo la Mahakama hii kwa umoja na tutunze miundombinu yote ili Kazi ya Mahakama na Mahakimu ya kutafsiri sheria ifanyike kwa ufasaha” alisema Mhe. Swedi.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe, alipata wasaa wa kuwasilisha Taarifa fupi ya Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa Miradi ya Mahakama ya Mwanzo Lupembe lililopo Wilaya ya Njombe ambapo jengo hilo ambalo limejengwa kwa fedha za mradi zilizotolewa na Benki ya Dunia (WB) zilizotumika mpaka kukamilika kwa ujenzi wake.

Aidha, alisema Jengo la zamani la Mahakama ya Mwanzo Lupembe, lilikuwa kwenye hifadhi ya Barabara, hivyo hali hiyo ilisababisha utafutaji wa eneo jingine kwa ajili ya kujenga Mahakama mpya ikiwa ni moja ya mikakati ya Mahakama ya Tanzania na Serikali kwa ujumla kuboresha majengo ya Mahakama ambayo ni ya zamani  ili yaweze kuwa ya kisasa zaidi.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Njombe akiwemo Jaji wa Mahakama ya Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njomba, Mhe. Obadia Bwegoge, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye pia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya za Njombe, Ludewa, Wanging’ombe na Makete pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (aliyesimama mbele kushoto) akiwa tayari amekata utepe kuashiria uzinduzi wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo Lupembe Wilaya ya Njombe.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe,Victoria Nongwa (wa pili kushoto) akikata utepe akizindua vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wanaoshuhudia ni baadhi ya Viongozi na watumishi wengine wa Mahakama Njombe. Wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge.

Watumishi wakifuatilia kinachojiri.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (aliyeketi katikati), Jaji wa Mahakama ya Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe.Obadia Bwegoge (kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph Luambano wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Njombe baadhi wakiwa wameshika vifaa vya TEHAMA ambavyo ni vishikwambi walivyokabidhiwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Nongwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe.Victoria Nongwa akipanda mti wa mparachichi kwa ajili ya kumbukumbu. Waliosimama ni Viongozi mbalimbali pamoja na wageni waalikwa waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe wilayani Njombe.

 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe.Matilda Kayombo (wa kwa kushoto) akimuonesha kitu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe.Victoria Nongwa (wa pili kushoto) wakiwa pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Mhe. Juma Swedi. Wengine wa kwanza kulia  ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge, aliyesimama nyuma wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph Luambano na viongozi wengine.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama mbalimbali kutoka Mahakama Njombe wakiwa katika picha ya pamoja.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama)

 

 


Jumatatu, 3 Agosti 2026

MTENDAJI MKUU MAHAKAMA ASHIRIKI MKUTANO WA MAZUNGUMZO MAALUM KUHUSU UTEKELEZAJI DIRA 2050

  • Apokea Nyenzo za Utekelezaji Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa niaba ya Jaji Mkuu
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu leo tarehe 03 Agosti, 2026 ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba,Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo na Viongozi wengine mbalimbali kushiriki katika Mkutano wa Mazungumzo Maalum na Sekta Binafsi na Sekta ya Umma kuhusu Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

Katika Mkutano huo uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais Samia amezindua pia Nyenzo za Utekelezaji wa Dira 2050 na kukabidhi Ufunguo wa Mtazamo Mpya, unaoashiria mwanzo mpya wa ushirikiano wenye uwazi na uaminifu kati ya Serikali na Sekta Binafsi.

Aidha, Rais, Mhe. Dkt. Samia amewapatia Nyenzo za Utekelezaji wa Dira 2050 Viongozi kadhaa akiwemo Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu ambaye alipokea kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Viongozi mbalimbali wa Serikali na Sekta binafsi wamehudhuria katika mkutano huo muhimu.

Matukio katika picha Mkutano wa Mazungumzo Maalum na Sekta Binafsi na Sekta ya Umma kuhusu Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 na Uzinduzi wa Nyenzo za Utekelezaji wa Dira 2050.


 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan (kulia) akimkabidhi Nyenzo za Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, George Masaju.


 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Viongozi wengine wakiwa katika Mkutano wa Mazungumzo Maalum na Sekta Binafsi na Sekta ya Umma kuhusu Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 na Uzinduzi wa Nyenzo za Utekelezaji wa Dira 2050 uliofanyika leo tarehe 03 Agosti, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizindua Nyenzo za Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa Mkutano wa Mazungumzo Maalum na Sekta Binafsi na Sekta ya Umma kuhusu Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 na Uzinduzi wa Nyenzo za Utekelezaji wa Dira 2050 leo tarehe 03 Agosti, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwakabidhi mfano wa Ufunguo kama ishara ya mtazamo mpya, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo (wa pili kushoto), Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, Dkt. Juma Malick Akil (wa kwanza kushoto), Rais wa Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) Bi. Angelina Ngalula (wa pili kulia) pamoja na Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara Zanzibar (ZNCC), Bw. Ali Amour (wa kwanza kulia) baada ya uzinduzi Nyenzo za Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Agosti, 2026.






Ijumaa, 31 Julai 2026

JAJI KIONGOZI AONGOZA WAOMBOLEZAJI IBADA YA MAZISHI YA KUMUAGA JAJI MSTAAFU SAMBO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewaongoza mamia ya waombolezaji katika ibada ya kumuaga na kumsindikiza katika nyumba yake ya milele Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Marehemu Mhe. Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo aliyefariki Dunia mnamo 26 Julai, 2026 jijini Dar es Salaam.

Ibada hiyo ya kumuaga Marehemu Jaji Sambo ili kumpumzisha kwenye nyumba yake ya milele imefanyika leo tarehe 31 Julai, 2026 nyumbani kwa marehemu kitongoji cha Masebe wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya.

Akitoa salamu za pole kwa familia, ndugu, jamaa, majirani na marafiki Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa, maisha ya marehemu Jaji Sambo ni maisha ya mfano kwa aliowaacha kwani aliyaishi maisha yake kama sehemu ya maandalizi ya maisha ambayo sasa ameyaanza.

Jaji Kiongozi amesema kwa wale wanaomjua marehemu Jaji Sambo alikuwa mtu muadilifu mwenye hekima na imani ya Mwenyezi Mungu, na ndiyo maana Majaji na watu kutoka sehemu mbalimbali wakiwemo aliofanya nao kazi na alioshirikiana nao katika shughuli mbalimbali za kijamii wamesafiri kuja kumuaga na kumpumzisha katika nyumba yake ya milele, hali hiyo inaonesha jinsi gani aliweza kuishi na watu vizuri.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa, kwa upande wa Mahakama na tasnia ya Sheria kwa ujumla, Mhe. Sambo alichangia kwa kiasi kikubwa katika kutafsiri sheria kupitia maamuzi mbalimbali ambayo yataendelea kuwepo hata baada ya kuwa yeye amepumzika.

Aliongeza kuwa, maamuzi ambayo aliyatoa yameleta mchango ambao umewasaidia wengi kufahamu haki na namna ambavyo wanaweza kuziendea mahakamani. Mhe Sambo alikuwa na mchango mkubwa katika kuendeleza taaluma za wengine.

Mhe. Dkt.Siyani alirejea salamu za rambirambi kutoka kwa mmoja wa wahadhiri wa chuo kikuu cha Dar Es Salaam na kueleza namna ambavyo alimsaidia mhadhiri huyo kukamilisha tafiti yake. Jambo hilo linaonesha namna ambavyo alifundisha wengi na wengi wataendelea kumkumbuka.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amesema kwamba, pamoja na hadhi yake ya Ujaji, Mhe. Sambo aliendelea kushikilia imani yake kwa Mungu na kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii wakati wa utumishi wake na hata baada ya kustaafu utumishi alijishughulisha na kilimo na ufugaji akiwa Sumbawanga na hata mkoani Arusha.

“Madaraka tunayopewa ni makoti na majoho, Maisha yetu rasmi yapo katika Jamii inayotuzunguka hivyo hatupaswi kujitenga nayo,” alisema Jaji Kiongozi, akisisitiza juu ya mafunzo yapatikanayo katika maisha ya Marehemu Jaji Kakusulo Sambo.

“Nimepata funzo kupitia maisha ya Jaji Sambo hakuwabagua watu waliomzunguka, alikuwa anafikika na watu wote, alikwa tayari kupokea ushauri kutoka kwa mtu yoyote hata walioko chini yake na aliwaunganisha watu akiwa hai lakini leo pia katika kumuaga ametuunganisha pamoja watu wa imani tofauti,” amesisitiza Mhe. Dkt. Siyani.

Jaji Kiongozi alihitimisha kwa kusema kuwa, wanapata faraja wakiyakumbuka maneno ya Mungu yasemayo, “Heri wafu wafao katika Bwana maana watapata kupumzika la milele,”

Kwa upande wake, Mchungaji Michael Bureta aliyeongoza Misa takatifu ya Ibada ya maziko ya Marehemu Jaji Sambo alisema, “Ndugu yetu amelala katika kristo na ni njia mbayo kila mmoja wetu atapita. Tuiombee familia ili iangalie jambo hili katika imani na waendelee kumkumbuka kwa imani na sala wakati wote.”

Mchungaji Bureta aliongeza kuwa, Marehemu alikuwa na mchango mkubwa sana katika Kanisa alinunua vifaa mbalimbali vya Kanisa, kuwezesha safari za kikanisa ndani na nje ya nchi na alikuwa Mfadhili wa Kwaya ya Kanisa hadi kuteuliwa mnamo mwaka 2023 kuwa Mwenyekiti wa kwaya ya “Nuru Angaza” kanisani kwake alipokuwa mkoani Arusha.

Naye, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mashtaka Mkoa wa Mbeya alisema kuwa, msiba wa kuondokewa na Jaji Mstaafu, Marehemu Mhe. Sambo umeacha pengo kubwa kwa watu ambao mpaka sasa walikuwa wanategemea huduma kutoka kwake.

Marehemu Jaji Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo ameacha mjane mmoja, Watoto watano na Wajukuu 11 “BWANA ALITOA, BWANA AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE” AMEN.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiaga mwili wa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo mara baada ya Ibada Takatifu ya mazishi iliyofanyika nyumbani kwa marehemu kitongoji cha Masebe wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya, leo tarehe 31 Julai, 2026.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali akiaga mwili wa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati), akiwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali (wapili kushoto), na Majaji wengine wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa kwenye mazishi ya marehemu Jaji Sambo. Walioketi mbele (wa kwanza kushoto) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Iringa Mhe. Dustun Beda Ndunguru, Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo (wa pili kulia) na (wa kwanza kulia) ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Thadeo Marco Mwenempazi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akihutubia waombolezaji katika mazishi hayo.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Masjala Kuu Makao Makuu ya Mahakama Mhe. Chiganga Mashauri Tengwa akifanya utambulisho wa Viongozi walioshiriki katika mazishi hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Rungwe Mhe. Jackson Banobi akitoa salamu za rambirambi za Mahakama ya Wilaya Rungwe na kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya Rungwe.

Sehemu ya Viongozi wa Kamati ya ulinzi na usalama Wilaya ya Rungwe wakiwa katika mazishi hayo

Sehemu ya Watoto wa Marehemu wakiongozwa na Bw. Gwakisa Kakusulo Sambo (aliyeshika kipaza sauti) akisoma wasifu wa Marehemu Jaji Mstaafu Sambo.

Kwaya ya Angaza nuru ikitumbuiza katika mazishi hayo, kwaya ambayo Marehemu Jaji Sambo alikuwa Mwenyekiti wake.


Mwili wa Marehemu Jaji Mstaafu Sambo ukipumzishwa katika Nyumba yake ya milele.

Sehemu ya mamia ya waombolezaji katika mazishi hayo.


Sehemu ya mamia ya waombolezaji katika mazishi hayo

Sehemu ya mamia ya waombolezaji katika mazishi hayo.

Majaji wakiwa wamebeba Jeneza lenye mwili wa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo wakati wa shughuli ya mazishi.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali akisaini Kitabu cha waombolezaji nyumbani kwa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisaini Kitabu cha waombolezaji nyumbani kwa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo 

Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania walioshiriki msiba huo wakiaga Mwili wa Marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo mara baada ya Ibada Takatifu ya mazishi iliyofanyika nyumbani kwa marehemu kitongoji cha Masebe wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


JAJI KAHYOZA ATETA NA MAWAKILI MASJALA NDOGO GEITA

Na DOTTO NKAJA, Mahakama - Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, Julai 28, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea mkoani Geita katika kikao kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mafunzo wa Mahakama Kuu Geita kwa lengo la kujengeana uwezo na kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa haki.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Kahyoza aliwashukuru mawakili kwa kuitikia wito na kueleza kuwa mkutano huo ulilenga kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na wadau wa sheria, kujadiliana masuala yanayohusu utoaji wa haki, kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya mifumo ya Mahakama pamoja na kufahamiana, kwa kuwa yeye ni mgeni katika Masjala Ndogo ya Geita.

Alisema uwepo wa wadau wengi wa sheria mkoani Geita ni fursa muhimu ya kuendeleza utoaji wa haki kwa ufanisi na kuongeza kuwa Mahakama ya Geita imeendelea kuwa mstari wa mbele katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha utoaji wa huduma za Mahakama.

Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA kusomana na kufanya kazi kwa pamoja ili kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa watumiaji. Aidha, aliwahimiza mawakili kuanza kutumia Kiapo cha Ushahidi (Witness Statement), hususan katika mashauri ya madai, akieleza kuwa utaratibu huo unasaidia kuharakisha usikilizaji na utoaji wa maamuzi ya mashauri.

Pia aliwataka mawakili kuendelea kutoa taarifa na mapendekezo wanapokutana na changamoto katika matumizi ya mifumo ya Mahakama ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake na kwa niaba ya mawakili, Wakili Marina Mashimba aliipongeza Mahakama ya Geita kwa maboresho ya mifumo ya kidijiti ambayo imepunguza gharama na muda wa uwasilishaji wa mashauri. Alipendekeza pia kuimarishwa kwa ushirikiano wa mifumo ya Mahakama na taasisi nyingine za utoaji wa haki, ikiwemo Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) pamoja na Mabaraza ya Ardhi.

Aidha, aliomba mafunzo ya mara kwa mara kwa mawakili ili kuwaongezea uwezo wa kitaaluma na kuwawezesha kupata alama za maendeleo endelevu ya taaluma kupitia chama chao cha kitaaluma.

Naye, Wakili George Alfred aliipongeza Mahakama kwa maboresho ya huduma, huku akiainisha baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika matumizi ya mfumo wa kielektroniki. Alieleza kuwa, baadhi ya kampuni hazionekani wakati wa usajili wa mashauri, baadhi ya vijiji havipo kwenye mfumo, na wakati mwingine mfumo humtambua wakili anayesajili shauri kama mlalamikaji badala ya mwakilishi wa mlalamikaji. Alisisitiza umuhimu wa kuwawezesha mawakili kutumia kikamilifu mifumo ya kielektroniki ili kupunguza matumizi ya karatasi na kuongeza ufanisi.

Akijibu hoja hizo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alisema changamoto zote zilizowasilishwa zimepokelewa na zitafanyiwa kazi. Alieleza kuwa, changamoto zinazohusu mashauri ya mirathi, nyaraka kutokuonekana kwenye mfumo pamoja na usajili wa kampuni zitawasilishwa kwa wajenzi wa mfumo ili zipatiwe ufumbuzi.

Akihitimisha kikao hicho, Mhe. Kahyoza aliwashukuru mawakili kwa ushiriki wao na maoni yao yaliyolenga kuboresha huduma za Mahakama. Aliwahimiza kuendelea kutoa taarifa kuhusu changamoto wanazokutana nazo, kuimarisha ushirikiano na Mahakama, pamoja na kutumia huduma za usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Aidha, aliwakumbusha mawakili umuhimu wa kufanya mazoezi na kushiriki michezo mbalimbali ili kuimarisha afya ya mwili na kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (katikati mbele) akiwakaribisha Mawakili wa Serikali na Mawakili wa Kujitegemea katika kikao kazi hicho cha kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji.


Wakili wa Serikali  Wakili Msomi George Alfred (aliyesimama) akichangia hoja.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna akijibu maswali na hoja mbalimbali zilizoibuliwa na Mawakili katika kikao kazi hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita Bi. Masalu Kisasila aliyesimama akitoa shukurani kwa ushirikiano mzuri katika uendeshaji wa shughuli za kiutawala baina ya Mawakili na Uongozi wa Mahakama. 


Wakili wa Serikali Bw. Robert Neophitus (aliyesimama) akitoa maoni juu ya Mfumo wa kielektroniki wa kusimamia Mashauri (e-CMS).

(Habari Hii Imehaririwa na INNOCENT KANSHA, Mahakama-Dodoma)