Jumamosi, 29 Agosti 2026

MTENDAJI MKUU AZUNGUMZA NA WATUMISHI WA MAHAKAMA ZA CHINI DAR ES SALAAM

Na WINFRED NZILANO-Mahakama Kisutu, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, tarehe 27 Agosti, 2026, alifanya kikaokatika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, kuzungumza na watumishi.

Watumishi hao walitoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Kinondoni, wawakilishi kutoka Mahakama za Wilaya Kivukoni, Temeke, Kigamboni, Ilala na Ubungo.

Hii ni mara yake ya kwanza tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kushika wadhifa huo. Dkt. Jingu aliambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Kikao hicho kililenga kufanya utambulisha kwa watumishi, kufahamu mwenendo wa utekelezaji wa majukumu na kusikiliza changamoto zinazowakabili katika mazingira yao ya kazi.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Jingu alitoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uteuzi wake. Alieleza ujio wake ni sehemu ya juhudi za uongozi wa Mahakama kuendelea kuwa karibu na watumishi na kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu changamoto wanazokutana nazo katika kutekeleza majukumu yao.

Katika kikao hicho, watumishi walipata fursa ya kuwasilisha changamoto, hoja na mapendekezo mbalimbali yanayohusu mazingira ya kazi na utekelezaji wa majukumu yao. Dkt. Jingu aliahidi kuzifanyia kazi kwa kuzingatia taratibu na mamlaka zilizopo.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu aliwasihi watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma katika kutekeleza majukumu yao. Alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora kwa wote wanaofika mahakamani ili kujenga taswira nzuri ya Mahakama kwa wananchi.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, alitoa shukrani kwa juhudi ambazo zimefanyika kuboresha masilahi ya watumishi na miondombinu ya Mahakama.

Kikao hicho kimeonesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuwa karibu na watumishi, kusikiliza changamoto zao na kuweka mazingira bora ya utendaji kazi.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, akizungumza na watumishi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam. Picha chini ni sehemu ya watumishi kutoka Mahakama za chini za Mkoa wa Dar es Salaam.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, akifanya utambulisho wa watumishi waliohudhulia katika kikao.

Mmoja ya watumishi akiwasilisha hoja wakati wa kikao hicho.

Picha ya pamoja na Watendaji na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni.

Picha ya pamoja na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo.

Picha ya pamoja na Maafisa utumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Mahakama ya Wilaya Kinondoni, Mahakama ya Wilaya Ilala, Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mahakama ya Wilaya Ubungo na Mahakama ya Wilaya Temeke.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

JAJI MKUU MASAJU AMUAPISHA MHE. DEOGRATIUS NDEJEMBI KUWA MAKAMU WA RAIS WA TANZANIA

  •   Rais, Mhe. Dkt. Samia ampongeza Mhe. Ndejembi kwa kushika wadhifa huo
  •    Amtaka Makamu wa Rais huyo kuwa tayari kujifunza
  •   Asema bidii, nidhamu, weledi na utayari vitamsaidia kutekeleza majukumu yake ipasavyo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 29 Agosti, 2026 amemuapisha Mhe.  Deogratius John Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hafla ya Uapisho huo imefanyika katika Viwanja vya Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma na kushuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Viongozi mbalimbali wa kitaifa akiwemo pia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Mawaziri, Viongozi wengine na Wageni waalikwa mbalimbali.

Uteuzi na uapisho wa Mhe. Ndejembi unakuja baada ya kujiuzulu kwa aliyekuwa Makamu wa Rais wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi tarehe 25 Agosti, 2026 ikiwa ni pamoja na kupitishwa na kuidhinishwa kwa kauli moja ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika, Mhe. Mussa Azzan Zungu, kufuatia pendekezo lililoridhiwa na Kamati Kuu pamoja na Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Akizungumza mara baada ya hafla hiyo, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amempongeza na kumpa pole Mhe. Ndejembi kwa kupewa jukumu hilo kubwa katika umri wake mdogo, huku akibainisha kuwa, uamuzi huo ulilenga kurudisha nafasi hiyo kwa vijana wenye nguvu, ari, na kasi ya kujituma serikalini.

“Nitumie fursa hii kukupa pole Mhe. Ndejembi katika umri mdogo tumekutwisha jukumu kubwa bila kukushauri, lakini kipekee nivishukuru sana vikao vya Chama Cha Mapinduzi, Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi kwa kupendekeza na kuliridhia jina la Mhe. Deogratius John Ndejembi katika nafasi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na hii ni baada ya kuzingatia sifa na vigezo alivyo navyo, ikiwa ni pamoja na umri wake, ambao kwa kweli bado ni kijana mwenye nguvu, ari, na kasi ya kujituma na kutekeleza shughuli za Serikali. Kwa kauli moja tuliamua nafasi ile tuirudishe kwa vijana na tuendelee kulea, imetoka kwa kijana, tumeirudisha kwa kijana, sasa kijana tukuombe ukakue si kwa umri lakini ukakue akili,” amesema Rais, Mhe. Dkt. Samia.

Aidha, Mhe. Dkt. Samia amesema kuwa hana shaka na utendaji kazi wa Makamu wa Rais, Mhe. Deogratius Ndejembi kwani kabla ya wadhifa huo alishika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na sekta binafsi, hivyo, uzoefu huo utamsaidia katika kutekeleza majukumu ya dhamana hiyo aliyopewa.

“Hakuna shule inayosomesha Umakamu wa Rais, hakuna. Ila sifa zako za bidii, nidhamu, weledi, na utayari wako wa kujifunza, kufuatilia, na kusimamia utekelezaji wa shughuli mbalimbali zitakusaidia kutimiza majukumu hayo. Nakuhimiza neno kujifunza; kujifunza ni pamoja na kusoma kwa wengine waliopo nawe,” amesisitiza.

Mambo makuu aliyoyasisitiza Rais Samia kwa Makamu wa Rais mpya ni pamoja na Ukuaji wa Kiakili na Nidhamu, kuwa na bidii, nidhamu, weledi na utayari wa kujifunza kutoka kwa viongozi wengine na waliotangulia.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Samia amemkumbusha Makamu wa Rais, Mhe.  Ndejembi kutambua kuwa, cheo alichopewa ni dhamana kutoka kwa Watanzania na sio ufalme, hivyo anapaswa kuwatumikia wananchi wote bila ubaguzi au kujali tofauti zao.

“Nakusihi uweke maanani kwamba cheo ni dhamana. Cheo hiki tulichokupa si ufalme; ni dhamana. Dhamana uliyopewa na Watanzania kupitia Chama Kikuu kinachoongoza Dola, Chama Cha Mapinduzi, na kupitia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo nenda ukawatumikie bila kujali tofauti zao,” amesisitiza Rais Samia.

Vilevile amemsisitiza kuwa na Uzalendo na Uadilifu kwa kutekeleza majukumu kwa utii, uaminifu, utu, busara, hekima na maarifa huku akimtanguliza Mwenyezi Mungu mbele.

Mbali na hayo, Rais, Mhe. Dkt. Samia amezungumzia kuhusu Utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo: Kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

“Tunayo mambo mengi tuliyoahidi kupitia Ilani ya Chama chetu ya mwaka 2020-2025 na kwenda mbele 2030. Aidha, kama unavyofahamu, tumeanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 inayokuja, ambayo imebeba matamanio na matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi wetu," amesema. 

Ameongeza kuwa, ili kutekeleza yote hayo kwa maslahi yanayostahili wananchi na taifa kwa ujumla, wanahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu, na uongozi bora na ushirikiano kwakuwa mambo hayo ni muhimu kuyazingatia katika utekelezaji majukumu na kuyafikia matamanio na matarajio ya Watanzania.

Aidha, Rais Samia amewashukuru Viongozi mbalimbali pamoja na Mabalozi na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa waliohudhuria hafla hiyo, akieleza kuwa mahudhurio yao yanadhihirisha amani, utulivu, na uimara wa Katiba na mifumo ya kisiasa ya Tanzania katika kuendesha mabadiliko ya uongozi kwa amani bila misukosuko.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimuapisha Mhe. Deogratius John Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 29 Agosti, 2026 katika Viwanja vya Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma. Anayeshuhudia katikati ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.


Mhe. Deogratius John Ndejembi akila kiapo cha kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mbele ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo (hayupo katika picha). Hafla ya Uapisho wake imefanyika leo tarehe 29 Agosti, 2026 katika Viwanja vya Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi akisaini Hati ya Kiapo mara baada ya kula kiapo cha kushika wadhifa huo leo tarehe 29 Agosti, 2026 Ikulu Chamwino jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akisaini Hati ya Kiapo mara baada ya kumuapisha Mhe. Deogratius John Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 29 Agosti, 2026 Ikulu Chamwino jijini Dodoma.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Watanzania mara baada ya Uapisho wa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 29 Agosti, 2026 Ikulu Chamwino jijini Dar es Salaam.

Viongozi mbalimbali wa Serikali, Vyama vya Siasa na Wageni waalikwa wakishuhudia na kushangilia uapisho wa Mhe. Deogratius John Ndejembi wa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 29 Agosti, 2026 katika viwanja vya Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu pamoja na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya ni miongoni mwa waliohudhuria katika Hafla ya Uapisho wa Makamu wa Rais, Mhe. Deogratius John Ndejembi leo tarehe 29 Agosti, 2026 katika viwanja vya Ikulu Chamwino jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya Uapisho wa Makamu wa Rais mpya. Wa nne kushoto ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi, wa nne kushoto ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, wa tatu kushoto ni Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, wa kwanza kushoto ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, wa tatu kulia ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azzan Zungu, wa pili kushoto ni Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mhe. Zubeir Ali Maulid, wa kwanza kulia ni Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Balozi Dkt. Moses Mpogole Kusiluka na wa kwanza kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Stephen Masato Wasira.

Meza kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakiwa katika picha ya pamoja na Mawaziri mbalimbali wa Kisekta waliohudhuria Hafla ya Uapisho wa Makamu wa Rais mpya, Mhe. Deogratius John Ndejembi (wa nne kushoto).

Meza kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama.

Meza kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama hiyo, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (aliyesimama wa tatu kushoto).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na familia ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi (wa tatu kushoto).













 

 

Ijumaa, 28 Agosti 2026

WATUMISHI MBEYA WATEMBELEA KITUO CHA KUFUA UMEME MTERA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya amewaongoza Watumishi wa Masjala hiyo kufanya ziara ya kujifunza katika Kituo cha kupooza na kusambaza umeme cha Mtera, kilichopo Bwawa la Mtera mkoani Iringa kwa lengo kuwajengea watumishi uelewa wa masuala ya uzalishaji wa nishati ya umeme kwa njia ya maji.

Watumishi hao, walipata elimu ya kina kuhusu mchakato wa uzalishaji wa umeme, kuanzia hatua za awali za uzalishaji hadi umeme unapofikia hatua ya mwisho ya kumwezesha mtumiaji kupata huduma hiyo.

Aidha, elimu hiyo iliambatana na uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi, hususan katika matumizi ya majumbani na kwenye vyombo vya usafiri, huku watumishi wakifafanuliwa namna matumizi ya nishati safi yanavyoweza kuwa na mchango mkubwa katika kupunguza athari za kimazingira na kuboresha maisha na ustawi wa jamii.

Matumizi ya nishati safi yana manufaa mathalani kuokoa muda, kupunguza gharama, kutunza mazingira na kulinda afya za watumiaji, hivyo ni wito kwa jamii kuendelea kuhamasishwa na kuelimishwa kuhusu fursa na manufaa yanayotokana na matumizi ya nishati hiyo.

Watumishi hao wameaswa kuendelea kuwa mabalozi wazuri katika kutunza miundombinu ya umeme kwani umeme unachagiza maaendeleo ya Taifa, huku wataalum hao wakitoa wito kwa Majaji na Mahakimu kuchukulia kwa uzito wa aina yake suala uendeshaji wa mashauri yanayo husu uharibifu wa miundo mbinu ya umeme.

Ziara hiyo pia ilitoa fursa kwa watumishi hao kutembelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Iringa, ambapo walikutana na kufanya mazungumzo na viongozi pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala hiyo.

Mazungumzo ambayo yaliweka msisitizo katika umuhimu wa kuendelea kujenga ushirikiano, mshikamano na kubadilishana uzoefu miongoni mwa watumishi wa Mahakama katika Masjala hizo, kwa lengo la kuimarisha utendaji na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.

Sehemu ya watumishi na viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakipewa maelezo na elimu mbalimbali juu ya namna umeme unavyochakatwa katika ziara hiyo.

Sehemu ya watumishi na viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakipewa maelezo na elimu mbalimbali juu ya namna umeme unavyochakatwa katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiteta jambo na Waandishi wa Habari katika ziara hiyo. 

Sehemu ya matukio mbalimbali ya watumishi wakiwa katika kituo cha Mtera

Sehemu ya watumishi na viongozi wakiwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Iringa ikiwa sehemu ya ziara hiyo.

Kaimu Meneja wa Kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Mtera Mhandisi William Modesti akiwapa elimu na kutoa historia ya kituo hicho na maendeleo yake kwa watumishi wa Mahakama Mbeya waliotembelea katika kituo hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya akitoa utambulisho na kuzungumza machache katika ziara hiyo wakiwa Mtera.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (kushoto), akipewa Zawadi ya jiko la umeme la kupikia “Electrical pressure cooker” wakati walipotembelea katika kituo cha kupooza na kusambaza umeme cha Mtera.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

WATUMISHI WA MAHAKAMA ARUSHA WAPATIWA MAFUNZO YA NAMNA YA KUPAMBANA NA MAJANGA YA MOTO

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Arusha

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wamepatiwa mafunzo ya namna ya kupambana na Majanga ya Moto mahali pa kazi.  

Mafunzo hayo yalifunguliwa hivi karibuni na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Frank Mahimbali ambapo alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwakuwa, yanasaidia kuokoa maisha ya wafanyakazi.

Akizungumzia suala la kupambana na majanga ya moto, Jaji Mahimbali alisema pia, mafunzo ya kupambana na majanga ya moto mahali pa kazi ni jambo muhimu kwa sababu, kulinda mali za Taasisi, na kupunguza hasara kubwa za kiuchumi zinazoweza kusababishwa na ajali za moto za ghafla.

Amesisitiza kuwa, umuhimu wa mafunzo hayo hauishii tu kazini bali pia hata nyumbani wanapoishi watumishi hao.

Faida za mafunzo ya moto ni nyingi na muhimu kwani husaidia kuokoa maisha, Wafanyakazi wanapata uelewa jinsi ya kutoka nje kwa usalama na haraka, wanapata ujuzi wa kutumia vizima moto kabla moto haujasambaa na hivyo kupunguza hasara kwa kuepusha mali na vifaa vya ofisi kuungua.

Utoaji wa elimu na mafunzo ya kupambana na majanga ya moto mahali pa kazi ni takwa la kisheria linalowataka Waajiri kuhakikisha usalama na afya ya wafanyakazi wao. Nchini Tanzania, sheria kuu inayosimamia suala hili ni Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi Na. 5 ya 2003.

Kwa mujibu wa sheria hiyo, wajibu wa Mwajiri ni kutoa elimu kwa kuwapa wafanyakazi mafunzo ya kuzuia na kupambana na moto, kuweka vifaa sahihi vya kuzimia moto mahali pa kazi, kuandaa njia za dharura na milango ya kutokea wakati wa hatari, na ukaguzi wa mara kwa mara kwa lengo la kuhakikisha mifumo ya tahadhali na kuzimia moto inafanya kazi vizuri.

Aidha, katika mafunzo hayo watumishi pia walijengewa uelewa juu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ili kuwajengea uelewa wa kutosha watumishi na hivyo kuwawezesha kuwa na taarifa sahihi zinazowasaidia kufanya maamuzi sahihi kila inapohitajika.

Mahakama Kanda ya Arusha ilialika Kampuni ya TGN ya Arusha ambayo hujishughulisha na masuala ya kupambana na majanga ya moto na utoaji elimu juu ya namna bora ya kupambana na moto.

Wataalamu wa kampuni hiyo walitoa elimu ya nadharia na vitendo ambapo watumishi mbalimbali waliweza kuzima moto kwa vitendo huku wengine wakishuhudia namna uzimaji moto unavyofanyika.


Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wakifanya mafunzo ya kuzima moto kwa vitendo wakisimamiwa na Wataalamu kutoka Kampuni ya TGN inayojishughulisha na kupambana na majanga ya moto, mafunzo haya yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akifungua Mafunzo ya namna ya kupambana na Majanga ya Moto mahali pa kazi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Watumishi wa Mahakama  Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mafunzo hayo.

Mtaalamu wa kupambana na majanga ya moto kutoka Kampuni ya TGN Arusha, Bw. Badru Juma akitoa elimu ya kuzima moto kwa watumishi wa Mahakama Arusha. Mafunzo hayo yalifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Arusha.


Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wakifanya mafunzo ya kuzima moto kwa vitendo wakisimamiwa na Wataalamu kutoka Kampuni ya TGN inayojishughulisha na kupambana na majanga ya moto, mafunzo haya yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Arusha.


Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama akitoa mada juu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa watumishi wa Mahakama Arusha. Mafunzo hayo yaliyofanyika hivi karibuni yalienda sambamba na ya namna ya kupambana na Majanga ya Moto mahali pa kazi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



                            

 

                                                           

 


 

WATUMISHI MBEYA WAZURU MAKAO MAKUU, TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA

Na MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya wamefanya ziara ya kikazi ya kuzuru Makao Makuu ya Mahakama na Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma, kwa lengo la kuongeza uelewa wa masuala ya kiutumishi, kujifunza mifumo ya uendeshaji wa shughuli Mahakama na kubadilishana uzoefu ili kuimarisha utendaji kazi na utoaji wa huduma.

Ziara hiyo imeongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, akiambatana na Viongozi pamoja na watumishi.

Aidha, Watumishi hao walipata fursa ya kujifunza kwa kina kuhusu masuala yanayohusu utumishi ndani ya Mahakama, ikiwemo utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo inayosimamia utendaji wa Mahakama.

Aidha, watumishi hao walitembelea Ofisi za Tume ya Utumishi wa Mahakama, ambako walipata maelezo kuhusu majukumu ya Tume, hususan katika usimamizi wa masuala ya rasilimali watu, nidhamu, maadili na maendeleo ya watumishi wa Mahakama.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Naibu Katibu Tume ya Utumishi wa Mahakama anayeshughulikia Nidhamu na Maadili, Bi. Alesia Mbuya, aliwakaribisha watumishi hao na kuwapongeza kwa kutenga muda wa kutembelea Ofisi za Tume, akieleza kuwa, ziara hizo ni muhimu katika kuongeza uelewa na kuimarisha ushirikiano pamoja na kubadilishana uzoefu katika masuala ya kiutumishi.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, alieleza umuhimu wa watumishi kupata fursa za kujifunza kutoka katika maeneo mbalimbali ya Mahakama, akisisitiza kuwa maarifa na uzoefu unaopatikana kupitia ziara hizo ni muhimu katika kuboresha utendaji kazi wa kila siku.

Mbali na Ofisi za Tume ya Utumishi wa Mahakama, watumishi hao walitembelea maeneo mbalimbali ya kimkakati katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, ambako walijifunza namna matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) inavyotumika katika kurahisisha na kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya Mahakama.

Miongoni mwa maeneo yaliyotembelewa ni ukumbi mpya wa mikutano ulioandaliwa kwa mifumo ya kisasa ya TEHAMA, ambapo watumishi hao walijionea namna teknolojia inavyowezesha uendeshaji wa mikutano, mafunzo na shughuli mbalimbali za kitaasisi kwa ufanisi.

Vilevile, walitembelea Chumba cha Mifumo ya TEHAMA, ambacho ni miongoni mwa maeneo muhimu katika miundombinu ya kiteknolojia iliyopo ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama. Katika eneo hilo, watumishi walipata maelezo kuhusu uratibu, usimamizi na uendeshaji wa mifumo ya TEHAMA inayosaidia shughuli za Mahakama.

Ziara hiyo pia iliwapa watumishi hao fursa ya kutembelea Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, ambako walipokelewa na na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

Mhe. Tiganga, aliwashukuru watumishi hao kwa dhamira yao ya kuendelea kuimarisha ushirikiano, kujenga molari ya utendaji kazi kwa watumishi, matumizi ya teknolojia, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi, kwa kuweka mkazo katika kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuendeleza rasilimaliwatu kama msingi wa ufanisi.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa Mbele ya jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama walipotembelea katika ziara hiyo.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na mwenyeji wao Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma Mhe, Joachim Tiganga, Mbele ya jengo la Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma walipotembelea katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja viongozi wa Masjala hiyo walipotembelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo wa Dodoma.




Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama mbele) akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya walipotembelea ofisi ya Tume ya utumishi wa Mahakama

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa ndani ya ukumbi mpya wakisasa uliopo ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa Mbele ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


MTENDAJI MKUU ATEMBELEA KITUO CHA USULUHISHI, MAHAKAMA YA ARDHI

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, tarehe 26 Agosti, 2026 alifanya ziara katika Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi pamoja na Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi kwa lengo la kujitambulisha.

Ziara hiyo imekuwa ya kwanza kufanyika tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huo.

Lengo lingine lilikuwa kufahamu kwa kina utekelezaji wa majukumu ya Mahakama hizo, kutathmini mafanikio yaliyopatikana pamoja na kubaini changamoto zilizopo katika utekelezaji wa majukumu.

Akizungumza na watumishi, Dkt. Jingu aliwasisitiza kuwa na upendo, mshikamano na kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuhakikisha Mahakama inaendelea kutoa huduma bora na kwa ufanisi kwa wananchi.

Alisisitiza umuhimu wa watumishi kushirikiana katika kutatua changamoto na kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kujituma.

Katika ziara hiyo, Mtendaji Mkuu aliambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, ambaye aliwapongeza watumishi kwa kazi nzuri wanayoifanyika na kusisitiza umuhimu wa kutenga muda kwa ajili ya kufanya mazoezi ya mwili ili kuimarisha afya na ustawi wao wanapotekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Mhe. Nkya pia aliwahimiza watumishi wa Mahakama hizo kuiishi salamu ya Mahakama inayosisitiza uadilifu, weledi na uwajibukaji katika kazi na kuwataka kuwa na maadili na matumizi ya lugha nzuri wanapowahudumia wananchi.

Naye Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani, alimshukuru Mtendaji Mkuu kwa kufanya ziara hiyo, kufanya majadiliano na watumishi na kuahidi kuzifanyia kazi changamoto zilizowasilishwa.

Ziara hiyo imekuwa muhimu katika kuimarisha mawasiliano, ushirikiano na uongozi kati ya watumishi na uongozi wa Mahakama ya Tanzania, pamoja na kuweka msisitizo katika utoaji wa huduma bora na ufanisi wa Mahakama.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt, John Jingu, akisalimiana na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani. Kulia akishuhudia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akichukua nafasi yake baada ya kuwasili kwenye Ofisi za Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi. Kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (kulia) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kushoto) wakizungumza na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani (katikati).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, akisaini kwenye kitabu cha wageni katika Ofisi ya Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa, akitoa utambulisho wa Viongozi mbalimbali kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (hayupo kwenye picha). 


Viongozi wa Mahakama wakimsikiliza Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani (hayupo kwenye picha).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu akiwa katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda (picha chini).



Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza akiwa katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Bw. Donald Makawia, akitoa utambulisho wakati wa kikao hicho.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao hicho. Katikati ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Njingu na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Niku Mwakatobe (kulia) akichukua kumbukumbu muhimu wakati wa kikao hicho.


Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi na Divisheni ya Ardhi (juu na chini), wakimsiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Njingu (hayupo katika picha).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.