Jumatatu, 13 Julai 2026

TIMU ZA MAHAKAMA SPORTS KIGOMA, REDIO JOY ZASAKATA KABUMBU

  • Zaibuka kwa sare ya goli mbili kwa mbili
  • Mahakama Sports Kigoma azindua Jezi mpya

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Kapteni wa Timu ya Mahakama Sports Kigoma, Bw. Omary Magege ameongoza Kikosi cha Mpira wa Miguu kilichochuana vikali na Timu ya Redio Joy ya Mkoani humo katika Mechi ya kirafiki baina ya timu hizo iliyolenga kuzindua Jezi/Sare mpya za Timu ya Mahakama sambamba na kudumisha mahusiano na wadau.

Mechi hiyo ilifanyika tarehe 11 Julai, 2026 katika uwanja wa Kajuna uliopo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Kocha wa Timu ya Mpira ya Mahakama Kigoma, Bw. Ramadhani Kufakunoga, alisema, “Tunawashukuru Viongozi wetu wa Mahakama Kigoma, kuona Timu hii inastahili jezi mpya pamoja na vifaa vingine kwa ajili ya mechi mbalimbali ambazo zinaendelea. Uwepo wa vifaa hivi vya michezo kwa Wachezaji ni motisha kubwa sana inayoungwa mkono na Timu hii pamoja na Mashabiki wetu.”

Kabla ya Mechi hiyo, Bw. Kufakunoga aliwataka Wachezaji wa Timu ya Mahakama kucheza kwa upendo na kujiamini ili kuonesha weledi katika mpira wao bila kusababisha majeraha kwa Timu pinzani.

Hata hivyo aliwatia shime kuwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka, ambaye ndio Mdhamini Mkuu wa timu hiyo ameahidi kufanya makubwa yanayoleta motisha katika michezo, hivyo waendelee kuvitumia vipaji vyao ili kuileta Mahakama pamoja na wananchi.

Na kwa upande wake, Mkurugenzi wa Redio Joy Kigoma, Bw. Mwenge Muyombi, alisema kuwa, “Mechi hii ni ya kuimarisha mahusiano hivyo chezeni kwa furaha, hii ni sehemu ya kujenga afya zaidi, pia kujiandaa na mashindano mengine ya kirafiki yanayokuja, hivyo tunategemea burudani nzuri sana, nawatakia mpira mwema.”

Aidha, mechi hiyo iliendelea kwa mchuano mkali ambapo mpaka dakika ya 65, Timu ya Mahakama ilikuwa inaongoza, hata hivyo, Wachezaji wa Mahakama walionesha uimara mkubwa ambapo baadae kibao ikiligeuka kwa Timu ya Redio Joy kujitutumua na kujibu mapigo kwa wapinzani wao na kuiwezesha mechi hiyo kutoka sare ya mbili kwa mbili.

Ushindi huo kwa timu zote mbili ilikuwa ni kipimo kizuri ambapo Makocha wa Timu zote mbili, walibaini wapi wakaboreshe ili kuendelea kuwa na Timu bora zaidi katika mechi zijazo.

Watumishi wa Mahakama na Redio Joy walijumuika na wananchi waliojitokeza katika mechi hiyo, ambapo walionesha kufurahia mchezo huo kwani ulisheheni utulivu na weledi wa kucheza mpira kwa malengo ya mmoja wapo kuwa mshindi ingawa mizani ililingana kwa matokeo ya sare.


Kikosi cha Timu ya Mahakama Sports Kigoma kikiwa katika uzi mpya wa jezi iliyozinduliwa katika Mechi yao na Timu ya  Redio Joy Kigoma.


Kapteni wa Timu ya Mahakama Sports Kigoma, Bw. Omary Magege akitoa neno baada ya dakika 45 kutamatika, wakiongoza kwa goli moja dhidi ya wapinzani wao Timu ya Redio Joy Kigoma.

Mkurugenzi wa Redio Joy Kigoma, Bw.Mwenge Muyombi akisalimiana na  Wachezaji wa Timu zote mbili ya Mahakama Sports Kigoma na ya Redio Joy mara baada ya kutoa neno kwa Wachezaji wote wa Timu hizo.


Kikosi cha Timu ya Redio Joy Kigoma kikiwa maridadi kwa ajili ya mchezo wa kirafiki na Timu ya Mahakama Kigoma,  mechi iliyopigwa katika uwanja wa Kajuna Kigoma.


Sehemu ya Mashabiki wa Timu ya Redio Joy wakifuatilia Mchezo uliokuwa ukiendelea katika Uwanja wa Kajuna uliopo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.


Sehemu ya Mashabiki na Watumishi wa Timu ya Mahakama  wakifuatilia Mchezo uliokuwa ukiendelea katika Uwanja wa Kajuna uliopo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.


Sehemu ya wananchi wakifuatilia mchezo uliokuwa ukiendelea katika Uwanja wa Kajuna uliopo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.

 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

MAHAKAMA YA WILAYA UBUNGO YATIMIZA MIAKA MIWILI BILA MLUNDIKANO WA MASHAURI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Mahakama ya Wilaya Ubungo imefanya kikao cha tathmini ya miaka miwili tangu kufunguliwa kwake ambapo kaulimbiu ya kikao hicho ilikuwa Mahakama ya Wilaya Ubungo bila mashauri ya mlundikano (two years without backlog cases).

Kikao hicho kilifanyika tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama wa wazi wa Mahakama hiyo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Ubungo, Mhe. Tumsifu Barnabas alisema kauli mbiu hiyo ililenga kutokuwepo kabisa kwa Mashauri ya Mlundikano na kwa sasa wametimiza miaka miwili pasipokuwa na mashauri ya Mlundikano.

Mhe. Barnabas alisema kuwa, dhumuni la kikao hicho ni kutathmini utendaji kazi, mafanikio, changamoto na pia kufahamiana na watumishi wapya waliohamia katika Mahakama hiyo kutoka vituo mbalimbali.

Aliwasisitizia Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Ubungo na Mahakama zake za Mwanzo kutimiza lengo la kaulimbiu ya Mahakama na kufanyia kazi kwa kufuata kauli mbiu ya Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji.

Aidha, Mfawidhi huo amesema, muitikio wa wananchi katika Mahakama hiyo umekuwa Mkubwa sana na ndio maana mashauri yanayofunguliwa ni mengi. Kwa kipindi cha mwaka 2024 hadi 2026 ni zaidi ya mashauri 5000 yamefunguliwa.

Katika kikao hicho, elimu kuhusu Mahakama SACCOS ilitolewa ambapo Meneja Mikopo wa Mahakama SACCOS, Bw. Godfrey Lulenga aliwaeleza faida za Chama hicho ambazo ni pamoja na kuweka akiba lakini pia kukopesha, ambapo kuna mikopo ya aina nne.

Bw. Lulenga alitaja mikopo hiyo kuwa ni Anza Maisha; ambapo alisema ni aina ya mkopo ambao mtumishi wa ajira mpya anakopeshwa ili kujikimu na Maisha, kuna mkopo wa dharura, mkopo wa maendeleo na mkopo wa sikukuu na kwamba Mahakama SACCOS wana mgawanyo wa riba.

Sambamba na kikao hicho watumishi hao walipata wasaa wa kukata keki ya upendo wa kusherehekea miaka miwili ya Mahakama hiyo.

Kikao hicho kilihudhuriwa na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Ubungo, Mahakama ya Mwanzo Kimara, Mahakama ya Mwanzo Kwembe na Mahakama ya Mwanzo Sinza/Manzese.

Mahakama ya Wilaya Ubungo ilianza kufanya shughuli za kimahakama tarehe 17 Mei, 2024.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Ubungo, Mhe. Tumsifu Barnabas  akizungumza jambo wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Tathmini ya miaka miwili ya Mahakama ya Wilaya Ubungo kilichofanyika tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama hiyo.

 Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Ubungo wakifungua kikao kwa dua.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Ubungo wakiwa katika picha ya pamoja na wakijiandaa kukata keki ya upendo na ishara ya kuadhimisha miaka miwili ya Mahakama hiyo.

Meneja Mikopo wa Mahakama SACCOS, 
Bw. Godfrey Lulenga akielezea faida na mikopo inayopatikana Mahakama SACCOS wakati wa Kikao cha Tathmini ya miaka miwili ya Mahakama ya Wilaya Ubungo.

Keki ya kusherehekea Maadhimisho ya miaka miwili ya Mahakama ya Wilaya Ubungo.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

Jumamosi, 11 Julai 2026

WADAU WA HAKI JINAI KIBAHA WAOMBA ASKARI POLISI WAPATIWE MAFUNZO

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Kibaha

Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Jinai kwa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo katika Wilaya ya Kibaha kimejadili na kuomba Askari wanaokaa Mahakama za Mwanzo kutekeleza amri mbalimbali za Mahakama kupatiwa mafunzo ya namna ya kuendesha mashauri ya jinai.

Hayo yamesemwa jana tarehe 10 Julai, 2026 katika kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Akizungumza katika kikao hicho, namna ambavyo washtakiwa na walalamikaji katika mashauri ya jinai, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mkuza, Mhe. Leah Mkono amesema kuna ugumu unatokea pale Askari wanafika Mahakamani na vielelezo hawavitoi wakati wa usikilizaji wa shauri badala yake wanavitelekeza tu Mahakamani na baada ya shauri kuisha ndipo mlalamikaji anadai vielelezo alikuwa navyo askari wakati huo shauri limeshaisha hali inayosababisha haki za wadaa kupotea.

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mailimoja, Mhe. Honorina Kambadu ameeleza masikitiko yake kuhusiana na hati za mashtaka kukosewa kila mara kutokana na kubadilishwa kila mara kwa Askari wanaofika Mahakamani hapo kiasi kwamba akielekezwa Askari huyu akaelewa, kesho anakuja Askari mwingine hivyo kumekuwa na ugumu wa kufanya kazi na Askari tofauti tofauti.

Wakati, huohuo amesema kumekuwa na uhaba wa Askari Polisi ambapo Mahakimu watano lakini Askari mmoja jambo hilo linasababisha kusubiriana wakati wa kusoma hati za mashtaka na kama kuna hukumu ya kumtia mtu hatiani inabidi wasubiri.

Akizungumzia katika masuala hayo, Katibu wa Kikao hicho ambaye ni Wakili wa Serikali Said Seif amesema, kutokana na changamoto hizo anayapokea hayo yote na kwamba atayafikisha kwa Viongozi wake na kuwashauri wafanye mafunzo ya namna bora ya kuandaa hati za mashtaka kwa Askari Polisi wa Mahakama za Mwanzo kuhusu namna bora ya kuwasilisha vielelezo Mahakamani na pia uwepo wa Askari Mahakamani bila kubadilishwa badilishwa kila siku.

Naye Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Kibaha, Mrakibu Msaidizi wa Polisi Victor Kashai amesema kuna uhaba wa Askari Polisi na hivyo kusababisha kuwepo kwa Askari mmoja Mahakamani lakini kutokana na changamoto hizo atazungumza na Viongozi wake kuongeza Askari ili kuepusha ucheleweshaji wa mashauri kuisha Mahakamani.

Katika kikao hicho Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kikao hicho amebainisha kwamba, katika Mahakama ya Wilaya kuna mashauri mawili tu yaliyovuka miezi sita na miongoni mwa mashauri hayo moja liko kwenye hatua ya maamuzi madogo na jingine liko kwenye mashauri ya majadiliano (Pre Bargain).

Aidha, Mhe.Lukumai  amewataka upande wa mashtaka kwa mashauri ya majadiliano (Pre Bargain) yasizidi siku sitini (60) yakitajwa Mahakamani bila kukamilika.

Katika kikao hicho Wadau wa Haki Jinai wameweka maazimio kadhaa ili kikao kijacho waone kama yametekelezeka. Maazimio hayo ni pamoja na Mahakama za Mwanzo ziko karibu na wananchi hivyo Mahakimu wasifungwe kupita kiasi na masharti ya kiufundi (technicalities), Hati za Mashtaka zenye Mapungufu zisipokelewe Mahakamani.

Pia umetolewa ushauri kwa Mahakimu  kutokana na mabadiliko ya Sheria ya Kieletroniki kuruhusu Ushahidi kupokelewa Mahakama za Mwanzo wajitahidi kusoma na kuelewa vizuri na kutofautisha kati ya maudhui ya kidijitali (Digital Content) na maudhui ya Makala (Documentary Content) na taratibu za upokeaji wake na pia kufanya kozi fupi zinazotolewa na Vyuo Vikuu kuhusu Akili Unde (AI) ili kuendana na wakati na hali halisi maana uhalifu mwingi umehamia kwenye mambo ya kimtandao zaidi kuliko uhalifu wa kawaida.

Sambamba na kikao hicho cha kusukuma mashauri ya jinai pia kimefanyika kikao cha kusukuma mashauri ya madai (Bench Bar) ambapo  wito umetolewa kwa Mawakili kuweza kusimamia vema shajara zao ili kuepuka muingiliano wa mashauri kati ya Mahakama moja na nyingine.

Wadau wa Haki Jinai wakiwa katika picha ya pamoja baada ya Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Jinai. Walioketi kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mwenyekiti wa Kikao hicho, Mhe. Emmael Lukumai na kulia ni Katibu wa kikao hicho, Wakili wa Serikali Said Seif.

Wadau wa Haki Jinai wakiendelea na kikao.


 Wajumbe wa Kikao cha kusukuma Mashauri ya Madai wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kikao hicho. Walioketi kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha ambaye pia aliyekuwa Mwenyekiti wa kikao hicho, Mhe. Emmael Lukumai na Katibu ambaye ni Wakili wa Kujitegemea, Wakili Werema Maghembe. Waliosimama kutoka kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mailimoja, Mhe. Honorina Kambadu, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mlandizi, Mhe. Anneth Senkoro, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mkuza, Mhe. Leah Mukono, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Fredrick Shayo na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Soga, Mhe Wahabi Mvura.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mwenyekiti wa Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Madai, Mhe. Emmael Lukumai akifungua kikao hicho. Kushoto ni Katibu wa kikao hicho, Wakili Werema Maghembe.


(Habari  hii imehaririwa MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)





 

 

 

 

 

JENGENI UTAMADUNI WA UWAJIBIKAJI NA UWAZI KAZINI; JAJI FRANK MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Kuu Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amewaagiza Viongozi wa ngazi mbalimbali za Mahakama mkoani humo kuwa ni lazima wajenge utamaduni wa uwajibikaji na uwazi kazini katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku kwakuwa ndio njia bora ya kutoa huduma na kuondoa malalamiko ya wananchi wanaohudumiwa.

Mhe. Mahimbali aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa Kikao cha Menejimenti cha Masjala hiyo kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Hoteli ya Sparrow iliyopo wilayani Karatu.

Akizungumza na wajumbe wa kikao hicho, Jaji huyo Mfawidhi alisisitiza kuwa ni lazima Hakimu anaposoma hukumu ahakikishe anatoa na nakala yake siku hiyo ya kusoma hukumu.

Amesisitiza kwa kusema kuwa, kushindwa kutoa nakala ya hukumu kwa wakati ni ukiukwaji wa miongozo iliyopo na kusababisha malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa wateja na wadau wa Mahakama.

Mhe. Mahimbali ametoa maagizo kwa Mahakimu wote Wafawidhi kufuatilia kwa karibu Mahakimu walio chini yao kuhakikisha kuwa, taarifa muhimu kama nakala za hukumu na mienendo ya mashauri wateja wanazipata kwa urahisi na kwa wakati na hivyo kujiepusha na malalamiko yasiyo ya lazima.

Vilevile, Jaji Mahimbali ametoa maelekezo kwa kila Mahakama kuboresha utoaji huduma kwa wateja. Amesisitiza kwa kusema, “Sisi tunafanya kazi kwa Umma, tunahudumia wananchi, Mahakama zetu ni kwa ajili ya wananchi, kwa hiyo maslahi ya wananchi yawe kipaumbele cha kwanza. Tunao wajibu wa kuwahudumia wananchi kwa heshima, utu na usafi.”

Hali kadhalika, Mhe. Mahimbali amewaasa wajumbe kuzingatia maadili ya kazi katika kusimamia Mahakama zao ikiwemo matumizi sahihi ya fedha za ofisi na kujiepusha na tamaa hatarishi.

Aliongeza kuwa, ni wajibu wa Viongozi wa Mahakama husika kuhakikisha kuwa, watumishi walio chini yao wanatekeleza majukumu yao kwa mujibu wa miongozo ya kazi kama sehemu ya kuwaepusha watumishi kufanya matendo yanayokiuka taratibu za kazi na hatimaye kuwekwa nguvuni na vyombo vya sheria.

Pia, Jaji Mahimbali ameelekeza mambo mbalimbali yanayolenga kuongeza ufanisi kazini, ikiwemo Mahakimu kuzingatia muda uliowekwa wa mashauri kuisha, kuepuka kuahirisha mashauri bila sababu za msingi, kusimamia ubora wa hukumu, maamuzi na amri za Mahakama; watumishi kuwa waadilifu na waaminifu kazini, usimamizi bora wa fedha na rasilimaliwatu, kuimarisha ushirikiano kati ya Viongozi na watumishi wa ngazi za chini na watumishi kujiepusha na vitendo vinavyoharibu taswira nzuri ya Mahakama.

Aidha, amewaagiza Mahakimu Wafawidhi kufanya tathmini ya kaguzi wanazofanya na kubaini maeneo yanayohitaji mafunzo na kuchukua hatua ya kuandaa mafunzo ya ndani kwa lengo la kuwaelimisha watumishi walio chini yao na hatimae kuongeza ufanisi wa kazi.

Amezitaka Mahakama mkoani Arusha kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuendelea kutumia mifumo ya Kitehama iliyopo Mahakamani hususan Mifumo ya kuratibu mashauri (e-CMS na Primary Court Mobile App).

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye ni Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mhe. Erasto Philly, aliwasilisha taarifa ambayo ilionesha kuwa hadi kufikia tarehe 18 Machi, 2026, Mahakama Kuu Arusha ilikuwa na mashauri yanayoendelea 593, ambapo kwa kipindi cha kuanzia tarehe 18 Machi, 2026 hadi tarehe 30 Juni, 2026 yalisajiliwa mashauri 324, yalimalizika mashauri 448 na kubaki mashauri 469.

Katika mashauri hayo (469) yaliyobaki, mashauri ya mlundikano ni matatu ambayo yote ni mashauri ya utekelezaji.

Mhe. Philly aliendelea kusema kuwa, hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026 Mahakama ya Hakimu Mkazi ilikuwa na mashauri 72 yaliyokuwa yakiendelea Mahakamani na kwa kipindi cha kuanzia Mwezi Aprili hadi Juni 2026, Jumla ya mashauri 45 yalisajiliwa na mashauri 61 yakasikilizwa. Idadi ya mashauri yaliyobaki kufikia tarehe 30 Juni, 2026 yalikuwa 56.

Naibu Msajili huyo alizitaja pia takwimu za Mahakama za Wilaya mkoani Arusha kuwa, hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026, Mahakama hizo zilikuwa na mashauri 334 yaliyokuwa yanaendelea Mahakamani, na kwa kipindi cha mwezi Aprili hadi Juni 2026, jumla ya mashauri 514 yalisajiliwa na 470 yalisikilizwa. Idadi ya mashauri yaliyobaki kufikia tarehe 30 Juni, 2026 yalikuwa 378.

Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo Mkoa wa Arusha, Mhe. Philly alisema kuwa, zilikuwa na jumla ya mashauri 207 yaliyokuwa yakiendelea Mahakamani hadi kufikia tarehe 30 Machi, 2026, na kwa kipindi cha kuanzia mwezi Aprili hadi Juni yalisajiliwa mashauri 4,169 na yalisikilizwa mashauri 4,121. Mashauri yaliyobaki tarehe 30 Juni, 2026 yalikuwa 255.

Aliongeza kuwa, kumekuwa na changamoto mbalimbali katika usikilizaji wa mashauri hayo, ikiwa ni pamoja na majalada yanayoitishwa kutoka Mabaraza ya Ardhi na Usuluhishi kutokuletwa kwa wakati, Majalada yaliyorudishwa katika Mabaraza ya Ardhi na Tume ya Usuluhishi kwa ajili ya kufanyiwa masahihisho kutorejeshwa kwa wakati, mashahidi kutoletwa kwa wakati katika mashauri ya jinai na kusababisha mashauri kuchelewa kuisha mahakamani na wakati mwingine hata kusababisha vikao maalum vya mashauri ya Jinai kusogezwa mbele.

Naye Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama amebainisha katika wasilisho lake kuwa, kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 Mahakama Arusha imepiga hatua kubwa katika mambo mbalimbali yanayoweka mazingira mazuri katika utekelezaji wa shughuli za Mahakama ikiwemo mafunzo kwa watumishi, kubadilishwa kada watumishi wenye sifa, kulipa stahili za Viongozi kwa wakati.

Mengine ni kuwezesha sare za watumishi wasio Mahakimu, kufanya ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya Mahakama, kuanzisha Mahakama mpya na kufufua Mahakama zilizokuwa zimefungwa kwa muda mrefu.

Pia, Bi. Kapama aliongeza kwa kusema kuwa, Mahakama hiyo imepiga hatua kubwa katika malipo ya fedha za mirathi ambapo katika Mwaka wa Fedha uliopita 2025/2026, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha imefanya malipo ya shilingi za Kitanzania takribani bilioni tatu (3,069,003,707.53/=), sawa na asilimia 86.92. Kiasi kilichobaki kwenye akaunti ya Mirathi kufikia tarehe 30 Juni, 2026 kilikuwa takribani shilingi milioni mia nne na sitini na moja (461,609,115.19/=), ambapo juhudi zinaendelea kumalizia malipo ya fedha hizo za mirathi zilizosalia.

Kikao hicho kimehudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka Mahakama za Mkoa wa Arusha hususan Mahakimu Wakazi Wafawidhi na Maofisa mbalimbali waliowakilisha Mahakama zao.

Wajumbe hao wamejadili mambo mbalimbali ikiwemo mafanikio na changamoto wanazokumbana nazo katika kazi na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuboresha utendaji kazi katika maeneo yao.

Vikao hivyo vya menejimenti ni moja ya fursa inayouwezesha Uongozi wa Mahakama Arusha kufanya tathmini na kujadili kwa pamoja juu ya namna bora ya kutekeleza shughuli za Mahakama na hatimaye kuongeza ufanisi katika kazi.

Vikao hivyo hufanyika katika Mahakama tofauti tofauti kwa mzunguko ambapo kikao hicho kimefanyika Wilayani Karatu, Mahakama ya Wilaya Karatu wakiwa ni wenyeji. Kikao kitakachofuata kitafanyika mwezi Oktoba, 2026 Wilayani Longido.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akifungua Kikao cha Menejimenti cha Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Hoteli ya Sparrow iliyopo Wilayani Karatu. Kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama. 


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mhe. Erasto Philly akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Sparrow mjini Karatu. Kushoto ni Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento.


Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama (aliyesimama) akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Sparrow iliyopo Wilaya Karatu. Kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali. 

Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Monduli na Karatu, Mhe. Pamela Meena (kushoto) na Mhe. Samwel Mushumbusi (kulia) wakishiriki kikamilifu Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Hoteli ya Sparrow Karatu Mjini.

Wajumbe mbalimbali walioshiriki katika Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Sparrow Wilayani Karatu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Ijumaa, 10 Julai 2026

JAJI MKUU AWATAKA MAJAJI WA RUFANI KUWA HURU KUTOA MAONI YA KUBORESHA MAAMUZI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewasihi Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya kuwa huru kutoa maoni au misimamo ya kisheria wanayoamini ni sahihi bila hofu yoyote, kwani kwa kufanya hivyo, watakuwa wanaboresha maamuzi ya Mahakama ya Rufani ambayo ndiyo inategemewa kutoa kauli ya mwisho kwa mashauri yanayofika mbele yake.

Mhe. Masaju amesisitiza hilo kupitia Hotuba yake ya Kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya iliyosomwa na Mwakilishi wake Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Nawasihi muwe huru kutoa maoni au misimamo ya kisheria mnayoamini ni sahihi bila hofu yoyote, kwani kwa kufanya hivyo ndiyo mtakuwa mnaboresha maamuzi ya Mahakama ya Rufani ambayo ndiyo inategemewa kutoa kauli ya mwisho kwa mashauri yanayofika mbele yake lakini ndiyo inayotoa mwongozo wa tafsiri ya sheria unaopaswa kufuatwa na Mahakama zote za chini yake na kujenga au kuendeleza misingi ya kisheria (jurisprudence) nchini,” amesema Mhe. Masaju kupitia hotuba hiyo.

Jaji Mkuu amesema kuwa, moja kati ya Mada waliyojifunza Majaji hao inahusu Ushirikiano katika Mahakama ya Rufani (Collegiality at the Court of Appeal), hivyo, amewaomba pia kujenga utamaduni wa kushirikiana, kusikilizana, kuheshimiana na kujenga maamuzi bora kupitia majadiliano ya kitaaluma. Na kwamba hiyo haimaanishi kukubali tu msimamo wa Majaji wengine hata kama dhamiri na utaalamu wao vinaelekeza vinginevyo.

Aidha, Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, katika mada ya Haki ya Msingi dhidi ya Masharti ya Kiufundi ambapo amesema, “mada hii inatutaka kuamua mashauri kwa kubainisha haki na wajibu wa kila mdaawa, ambalo ndilo jukumu la msingi la Mahakama, kuliko kuamua mashauri kwa kutumia masharti ya kiufundi ambayo hayatatui mgogoro uliopo baina ya wadaawa. Na kama ambavyo mmeona, hili lina msingi wake kuanzia kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo mmeapa kuizingatia, hivyo nawasihi sana mkalitekeleze hilo.”

Amesema kuwa, mada hiyo msingi wake umeanzia kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo wameapa kuizingatia, hivyo amewasisitiza wakalitekeleze hilo ipasavyo. Na kwamba wanapaswa kulitekeleza vema zaidi kwa kutumia hekima na akili kama alivyosema siku ya ufunguzi wa mafunzo hayo, kwani hekima na akili walizobarikiwa na Mwenyezi Mungu zitawawezesha kuwapa upeo wa ziada wa kupata ufumbuzi wa masuala magumu na yanayohitaji ubunifu na kujiongeza (creativity and proactiveness).

Akizungumzia kuhusu umuhimu wa Mafunzo Elekezi, Jaji Mkuu amesema, Mafunzo hayo yalilenga kuwaandaa washiriki kuanza kutekeleza majukumu ya Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa weledi, kujiamini zaidi na kwa ufanisi zaidi.

“Kama tunavyofahamu, Mahakama ya Rufani ndiyo chombo chenye kauli ya mwisho katika mfumo wa utoaji haki nchini, hivyo ni muhimu Majaji wapya wakaandaliwa kuanza kazi hiyo wakiwa wamepigwa msasa ili kuelewa vizuri zaidi Sheria, Kanuni na taratibu zinazotumika katika Mahakama hii licha ya ukweli kuwa ninyi tayari ni wataalam wa Sheria,” imeeleza hotuba hiyo iliyosomwa na Mhe. Mwambegele. 

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema mafunzo hayo yasiwe mwisho wa kujifunza na kuwataka Majaji hao kuendelea kujifunza hata baada ya mafunzo hayo. 

Akizungumzia Wawezeshaji na Mtindo wa Uwasilishaji mada, amesema, “Kama nilivyosema siku ya ufunguzi, wawezeshaji waliowezesha katika mafunzo haya ni wabobezi na wana uzoefu mkubwa wa utendaji kazi katika Mahakama ya Rufani. Waheshimiwa Majaji Wastaafu Mhe. Msoffe na Mhe. Rutakangwa wamehudumu katika Mahakama hii kwa muda mrefu na hukumu zao zimeendelea kutumika kama rejea na mwongozo katika maamuzi yetu mpaka sasa.”

Ameongeza kuwa, wakati mafunzo hayo yakiendelea alipata fursa ya kufika mara kadhaa, na alishuhudia mtindo mzuri wa uwasilishaji ambapo alishuhudia mafunzo hayo yakitolewa kwa mtindo wa majadiliano ya pamoja kama jopo na ushirikishwaji wa kila mmoja badala ya mhadhara wa upande mmoja.

“Mtindo huu unawajenga kufikiri, kuchambua na kufanya kazi kwa pamoja kama ulivyo mtindo wa ufanyaji kazi katika Mahakama ya Rufani,” ameeleza.

Vilevile, Jaji Mkuu amekipongeza Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kuandaa mafunzo hayo, Wawezeshaji wote wa mafunzo sambamba na kuwapongeza Majaji hao kwa kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo na kuwatakia kila la heri kwenye utekelezaji wa majukumu yao huku akiwakumbusha kila mmoja kukiishi kiapo chake na kuzingatia dhamana kubwa waliyopewa na Taifa na matarajio ya wananchi kwao.

Katika hatua nyingine, naye Jaji Mwambegele amewashauri Majaji hao kusoma hukumu za Majaji Wastaafu, Mhe. Msoffe na Mhe. Rutakangwa na nyingine ili kuongeza maarifa zaidi katika utekelezaji wa jukumu la msingi la utoaji haki.

“Someni hukumu zao tangu wakiwa Majaji wa Mahakama Kuu mpaka Majaji wa Mahakama ya Rufani. Nina uhakika hamtajutia, Mimi nimekuwa msomaji wa hukumu za hawa Wawezeshaji tangu nikiwa Wakili wa Serikali, mpaka nikawa Jaji wa Mahakama Kuu, na sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani. Kama alivyosema Mheshimiwa Jaji Mkuu hapa, ni kwamba hawa Wawezeshaji wana uwezo mkubwa, ninachotaka kuwasihi katika kuchomekea kwangu hapa ni kwamba, mpate muda wa kusoma hukumu zao. Uwezo wao sio wa kawaida. Mtakapokuwa mnasoma hukumu zao, mtagundua kwamba ni kwa nini Mahakama bado inawatumia mpaka leo,” amesisitiza Jaji Mwambegele.

Akizungumzia jinsi Mahakama ya Rufani inavyofanya maamuzi, Mhe. Mwambegele amesema maamuzi ya Mahakama hiyo ni maamuzi ya jopo la Majaji watatu, na maamuzi ya Majaji watano au kuendelea kwa (full bench), ambapo amesema, “Na jinsi ya kufanya, tunafanya maamuzi kwa kujadiliana, tukiongozwa na sheria. Pamoja na mlivyofundishwa, nawasihi pia mkasome hukumu ya Ahmadi Chali dhidi ya Jamhuri, imekuwa ‘reported’ katika mwaka 2006 TLR 313. Hukumu hii inaonesha ni jinsi gani hukumu ya Mahakama ya Rufani inaandikwa.”

Ameongeza kuwa, kupitia hukumu hiyo watapata habari ya ziada kuhusiana na nini kifanyike endapo mmoja wa jopo anashindwa kutekeleza jukumu lake, ama kwa sababu ya kiafya, au kwa kufariki na mambo mengine kama hayo. “Mtajua kwamba hukumu ya Mahakama ya Rufani inafanywa kwa pamoja, ‘this is a collegial Court’,” amesisitiza.

Hali kadhalika, Jaji Mwambegele amewasisitiza Majaji hao kuwa na Ushirikiano na Uadilifu wanapotekeleza majukumu yao.

Akitoa neno kwa niaba ya Majaji wenzake wakati wa hafla ya kufunga mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Aboud ameishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto chini ya Mkuu wa Chuo hicho ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo kwa kuandaa mafunzo hayo muhimu.

Kadhalika, Mhe. Aboud amewashukuru Wawezeshaji wote wa Mafunzo hayo wakiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju na Majaji Wastaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. January Msoffe na Mhe. Edward Rutakangwa.

Majaji hao tisa waliopatiwa mafunzo elekezi ambao ni Mhe. Imani Daudi Aboud, Mhe. Rabia Hussein Mohamed, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha, Mhe. Yohane Bokobora Masara, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba na Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim wote kwa pamoja wamepatiwa vyeti vya kuhitimu Mafunzo hayo muhimu ambayo ni moja ya maandalizi ya kuanza kazi rasmi kazi katika Mahakama ya Rufani ambayo ndio ngazi ya juu katika mfumo wa utoaji haki nchini. 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa (waliosimama) waliohitimu Mafunzo Elekezi leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akitoa hotuba ya kutoka Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya pamoja na baadhi ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama na IJA wakisikiliza Hotuba ya Jaji Mkuu ya Kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya  iliyokuwa ikitolewa na Mwakilishi wake Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (hayupo katika picha) leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Daudi Aboud ambaye ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rabia Hussein Mohamed ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Yohane Bokobora Masara ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba ameshiriki mafunzo hayo. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati wa hafla ya kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mahakama (waliosimama) waliohudhuria hafla ya ufungaji wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti ya maandalizi ya Mafunzo hayo (waliosimama). Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

(Picha na MARY GWERA & FAUSTINE KAPAMA, Mahakama)












JAJI TIGANGA ASISITIZA UTEKELEZAJI MIKAKATI YA JAJI MKUU USIKILIZAJI MASHAURI YA MADAI

Na ARAPHA- RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, hivi karibuni ilifanya Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Madai (Bench Bar) kilichowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya sheria na haki, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa mashauri ya madai, kupunguza mlundikano na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa wakati.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, na kuhudhuriwa na wawakilishi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Ofisi ya Msajili wa Hati pamoja na Baraza la Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Akifungua kikao hicho, Jaji Mfawidhi alisisitiza umuhimu wa wadau wote wa sekta ya sheria na haki kuendelea kutekeleza na kufuatilia kwa vitendo mikakati iliyoelekezwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, yenye lengo la kuhakikisha mashauri yanasikilizwa na kuamuliwa mapema ipasavyo, kupunguza mlundikano na kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Akiwasilisha taarifa ya hali ya mashauri ya madai, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, alisema Mahakama inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuhakikisha mashauri yanasikilizwa na kuamuliwa kwa wakati, sambamba na kudhibiti mashauri ya mlundikano.

Alieleza kuwa Mahakama imeendelea kufanya vikao maalum vya kusafisha mashauri (clean-up sessions), kutoa kipaumbele kwa mashauri ya kimkakati na   matumizi ya hati ya maelezo ya shahidi (Witness statement)  kwa dhumuni la kumaliza mashauri haraka na kupata kumbukumbu nzuri ya kile alichokikusudia mteja.

Mikakati mingine ni kusikiliza mashauri kadri inavyokuwa yamekamilika au yameiva bila kujali yamepokelewa lini, kuhimiza matumizi ya usuluhishi pale inapowezekana, kukamilisha hatua za awali  ya mashauri ya awali ndani ya siku 30, kutoa ahirisho lisilozidi wiki mbili na kuimarisha ushirikiano na wadau wa mnyororo wa haki ili kuondoa vikwazo vinavyochelewesha usikilizaji wa mashauri.

Kikao hicho pia kilibaini mashauri yanayokaribia kuwa ya mlundikano na kuweka mikakati ya kuyashughulikia mapema. Aidha, wadau walisisitiza umuhimu wa kushughulikia migogoro katika ngazi zinazotakiwa kisheria kabla ya kufikishwa mahakamani, hususan mashauri ya ardhi, pamoja na kuhakikisha mashauri yanaamuliwa kwa kuzingatia ushahidi na hoja za msingi badala ya kasoro za kiufundi.

Miongoni mwa mikakatii iliyofikiwa ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na Taasisi za mnyororo wa haki, kuongeza matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro, kuharakisha utekelezaji wa hukumu na kuhakikisha mashauri yanayosikilizwa yanakamilika kwa wakati kwa kuzingatia sheria na kanuni.

Mikakati mingine iliyofikiwa ni kutosajili mashauri ya ardhi ambayo yalipaswa kuanzia  kwa Msajili wa Hati kwa mjibu wa sheria pamoja na kufuatilia utekelezaji wa mikakati ya kikao cha Jaji Mkuun na Wadau wa Haki Madai inayolenga kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wote wa sekta ya sheria na haki ili kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama, kupunguza mlundikano wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki mapema ipasavyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiongoza kikao cha kusukuma mashauri ya madai.

 Wadau wa kikao hicho (juu na chin) wakisikiliza hoja mbalimbali ambazo zilikuwa zinatolewa.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, (aliyepo katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe na wadau wa kikao hicho. Kulia kwake waliokaa ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kushoto kwake ni Naibu Msajili, Mhe.Zabibu Mpangule.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.