Jumatano, 1 Aprili 2026

MAHUSIANO KATI YA MAHAKAMA NA TAASISI ZA USULUHISHI NCHINI NI YA MSINGI; JAJI MKUU

  •    Jaji Mkuu abainisha hayo alipoteta na TIArb
  • Asema Usuluhishi una faida lukuki ikiwemo kuokoa muda, kupunguza gharama, kujenga & kuimarisha mahusiano.....

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa mahusiano kati ya Mahakama ya Tanzania na Taasisi za Usuluhishi nchini ni ya msingi kwakuwa kwa kufanya hivyo Mhimili huo unatekeleza takwa la kikatiba kwa mujibu wa Ibara ya 107(A)(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaitaka Mahakama kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 01 Aprili, 2026 katika ofisi yake ndogo iliyopo Mahakama ya Rufani Tanzania jijini Dar es Salaam wakati alipotembelewa na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb).

“Viongozi nawashukuru katika hatua hii ya kututembelea Mahakamani, katika hatua hiyohiyo ya kuimarisha mahusiano baina yetu na kama unavyoona Katiba inatupa maelekezo pamoja na kwamba sisi ndio wenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia tunatakiwa kukuza na kuendeleza Usuluhishi baina ya watu wanaohusika katika migogoro, kwa hiyo sisi kukutana nanyi ni sehemu pia ya utekelezaji wa maelekezo ya Katiba kwa sababu ninyi mnahusika, lakini pia tuna mahusiano haya ya kisheria kwamba mnaanza kusuluhisha halafu utekelezaji hatimaye unaishia mahakamani,” amesema Jaji Mkuu.

Hivyo, Mhe. Masaju ameeleza kuwa, mahusiano kati ya Mahakama na Taasisi zinazohusika na Usuluhishi si tu ya msingi bali pia yanapaswa kuwa endelevu.

Kuhusu masuala mtambuka yanayohusu ustawi katika utekelezaji wa jukumu la Usuluhishi, Mhe. Masaju amewashauri Viongozi wa TIArb kuzishirikisha pia Wizara za Kisekta zinazohusika na mambo hayo, mfano kuhusu mabadiliko ya Sheria ni vema kushirikisha Wizara ya Katiba na Sheria au Mwanasheria Mkuu wa Serikali kama ambavyo wanaishirikisha Mahakama, kadhalika Wizara ya Mipango na Uwekezaji inayoongozwa na Mhe. Prof. Kitila Mkumbo.

Jaji Mkuu ameongeza kuwa, Mahakama inaunga mkono utekelezaji wa Usuluhishi unaofanywa na Taasisi hiyo kwa kuwa Usuluhishi una faida nyingi ikiwa ni pamoja na utatuzi wa migogoro mapema, inajenga na kuimarisha mahusiano, inapunguza matumizi ya gharama pamoja na kuokoa muda.

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju amewashauri Viongozi na Wafanyakazi wa Taasisi hiyo kuimarisha uwezo wa kumudu majukumu yao (competency) kuwa na uadilifu katika utekelezaji wa jukumu hilo muhimu sambamba na kutatua na kumaliza migogoro mapema ipasavyo.

“Kwa upande wetu huku Mahakamani tunachukua hatua ya kurekebisha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai na yale majedwali  ’ zinarekebishwa na Jaji Mkuu akishirikiana na Waziri mwenye dhamana, tutarekebisha huu mwenendo ili tuondoe vile vifungu vya kiurasimu vinavyofanya migogoro ichelewe kumalizika,” ameeleza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewaeleza viongozi hayo kuwa, “ninyi ambao mnafanya hii kazi ya Usuluhishi mnafanya jambo jema na imeandikwa katika Kitabu cha Mathayo sura ya 5 kwamba, heri Wapatanishi maana wataitwa Wana wa Mungu; kwa hiyo ushauri wangu ni kwamba muifanye kazi hii kwa nia njema (passion).”

Hata hivyo, Jaji Mkuu amewataka Viongozi hao kutoka TIArb kuitangaza Taasisi hiyo ili ijulikane na vilevile wasisite kuishirikisha Mahakama kuhusu jambo lolote kuhusiana na suala zima la utekelezaji wa jukumu la usuluhishi huku akiwaalika kujumuika na Mahakama katika Wiki ya Usuluhishi nchini anayotarajia kuizindua tarehe 09 Aprili, 2026.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Taasisi wa Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Bw. Usaje Mwambene amemueleza Jaji Mkuu kuwa Taasisi hiyo ilianzishwa mwaka 1997 lengo likiwa ni kushughulikia migogoro ya kimkataba, kibiashara na kadhalika.

Bw. Mwambene amesema tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo imekua kwa kasi na sasa ina jumla ya wajumbe 363 wakiwemo Wanasheria, Wahandisi, Wahasibu, Wafamasia na wengine na pia imejumuisha wajumbe wa kimataifa (international members) ambapo kwa sasa wapo wajumbe sita.

Ameeleza kuwa, Taasisi hiyo pia inatoa ushauri kwenye masuala ya migogoro ya kibiashara na kwamba inahusika kujenga uwezo (capacity building) kupitia mafunzo mbalimbali inayotoa kwa wajumbe waliopo na wapya.

Aidha, Makamu huyo wa Rais wa TIArb amesema, Taasisi hiyo inaomba ushirikiano wa karibu na Mahakama hususan katika maeneo ya kujengeana uwezo kupitia mafunzo mbalimbali, kushirikiana katika baadhi ya matukio ya Kitaasisi ikiwemo Mkutano wa Mwaka wa Wasuluhishi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) walipomtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 01 Aprili, 2026 katika ofisi yake ndogo iliyopo Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akizungumza na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) walipomtembelea leo tarehe 01 Aprili, 2026 katika ofisi yake ndogo iliyopo Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam.

 Makamu wa Rais wa Taasisi wa Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Bw. Usaje Mwambene akizungumza jambo na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati yeye pamoja na wenzake walipomtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 01 Aprili, 2026 ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam. 

Mazungumzo yakiendelea....

Sehemu ya Washiriki wa Kikao wakichangia na kufuatilia kinachojiri katika mazungumzo hayo.

 Makamu wa Rais wa Taasisi wa Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Bw. Usaje Mwambene (kushoto) akimpatia Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju zawadi ya makablasha ya taarifa mbalimbali zinazohusu Taasisi hiyo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati ) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) walipomtembelea leo tarehe 01 Aprili, 2026 ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam. 

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)










 

 

 

 

 

JAJI MFAWIDHI MTWARA AFANYA UKAGUZI WA MAHAKAMA

Na SOJO STEPEHEN-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, amefanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Mkoa wa Mtwara ili kujionea utendaji kazi, hasa katika Mahakama za ya chini na kati kuhakikisha huduma ya utoaji haki inaendelea kufanya vyema.

Ziara hiyo ilifanyika tarehe 23 mpaka 25, Machi 2026. Miongoni mwa Mahakama zilizokaguliwa na ni Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya Tandahimba, Newala, Nanyumbu, Masasi, Mahakama za Mwanzo Makuta, Mkunya, Mchaulo na Lukuledi.

Ziara hiyo pia ilijumuisha mazungumzo ya pamoja na Watumishi wa Mahakama alizopita kwa ajili ya ukaguzi. Aliweza kupata taarifa za utendaji kazi, mafanikio, changamoto, mapato na matumiz.

Aidha, Jaji Mfawidhi pia alipokea mawazo na maoni kutoka kwa Watumishi wa Mahakama hizo na kuhimiza weredi wa kuihudumia jamii inayowazunguka.

Mhe. Kakolaki aliwapongeza Mahakimu na Watumishi wa Mahakama kwa utendaji bora na mzuri, hasa kumaliza mashauri kwa wakati, kutokuwa na mlundikano na kuwa na aina bora ya utunzaji kumbukumbu.

Katika ukaguzi huo pia, Jaji Mfawidhi aliwapongeza Watumishi wa Mahakama katika matumizi wa mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo inawezesha kufuatilia na kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao. Aliwasisitiza kuendelea kuwaelewesha Wananchi kwenye matumizi ya mifumo hiyo ili kupunguza gharama za kila mara.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Kanda ya Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga na Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi, Mhe. Stella Shindika

Jaji Mfawidhi pia alitembelea na kukagua Mahakama za Mwanzo zilizokuwa katika ujenzi na zile ambazo zilizokuwa tayari zimekamilika. Aidha, aliendelea kusisitiza ujenzi ufanyike kwa kuzingatia ubora na kwenda kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akipokelewa na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Newala.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, (wa tano kulia) katika picha ya pamoja na Watumishi alipotembelea Mahakama ya Mwanzo Mahuta Wilaya ya Tandahimba.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mkunya Wilaya ya Newala Mhe. Apatesile Mbalasila(kushoto), akisoma taarifa fupi ya Mahakama hiyo mara baada ya kumkaribisha Jaji Mfawidhi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto) akiwa na Mhe. David Msalilwa(katikati), Mhe Charles Mnzava (kulia) katika mazungumzo na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Tandahimba.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitembelea Mahakama ya Mwanzo Mchauru.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akiwa anakagua jengo la Mahakama ya Mwanzo Mchauru, ambalo lilipata maafa na kusababisha uharibifu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akikagua ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Masasi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


MAHAKAMA ZA MWANZO TATU KANDA YA MTWARA ZAZINDULIWA

Na SOJO STEPHEN-Mahakama, Mtwara

Mahakama za Mwanzo tatu zilizokuwa zinajengwa ndani ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, zimezinduliwa katika jitihada za kusogeza huduma za haki karibu zaidi na Wananchi, hasa waliopo katika maeneo ya vijijini.

Uzinduzi huo wa pamoja ulifanyika tarehe 27 Machi, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Chikundi kwa niaba ya Mahakama nyingine za Mwanzo Kitangari na Newala Mjini na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali pamoja na Wadau wa sekta ya sheria.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akiwa ameambatana na Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana na Mtendaji wa Mahakama ya Mtwara, Bw. Yusuph Msawana.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kakolaki alisema kuwa kuanzishwa kwa Mahakama hizo kutasaidia kupunguza msongamano wa mashauri na kuharakisha utoaji wa haki kwa Wananchi.

Alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Mahakama na Serikali kuhakikisha kila Mwananchi anapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Aidha, aliwahimiza Wananchi kutumia Mahakama kama njia sahihi ya kutafuta haki, badala ya kutumia mbinu au sheria zisizo sahihi ambazo zinaweza kusababisha migogoro zaidi.

Vilevile, aliwasihi Wananchi na Watendaji wa Mahakama kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha shughuli za Mahakama, kuharakisha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri.

Mhe. Kakolaki aliwashukuru Wananchi, Viongozi wa Serikali pamoja na Wadau mbalimbali wa kijamii kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki uzinduzi wa Mahakama hizo zilizozinduliwa katika maeneo ya Chikundi, Kitangari na Newala Mjini.

“Napenda kuwashukuru Wananchi, Viongozi na Wadau wote kwa kushiriki uzinduzi huu wa Mahakama za Mwanzo za Chikundi, Kitangari na Newala Mjini. Ushiriki wenu unaonesha namna ambavyo jamii inathamini uwepo wa huduma za haki karibu na Wananchi,” alisema.

Alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania ina mikakati madhubuti ya kuhakikisha Wananchi wanapata haki bila kucheleweshwa wala kubaguliwa, na kwamba moja ya mikakati hiyo ni ujenzi wa Mahakama za Mwanzo katika maeneo mbalimbali nchini.

“Mahakama ya Tanzania imejipanga kuhakikisha kila Mwananchi anapata huduma ya kisheria kwa wakati na kwa usawa. Ndiyo maana tunaendelea kujenga Mahakama za Mwanzo ili kusogeza huduma hizi karibu zaidi na Wananchi,” aliongeza.

Naye Mtendaji wa Mahakama Mtwara alieleza kuwa Mahakama ina mkakati wa kuendelea kujenga majengo mapya na bora kwa ajili ya Mahakama mbalimbali nchini ili kuwezesha shughuli zote za utoaji wa haki kufanyika katika mazingira mazuri na yenye ufanisi.

“Ujenzi wa majengo haya ni sehemu ya mkakati wa kuboresha mazingira ya kazi kwa Watumishi wa Mahakama na kuhakikisha Wananchi wanapata huduma za haki katika maeneo yaliyo karibu nao na yenye miundombinu bora,” alisema.

Aidha, aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa juhudi zake za kuboresha miundombinu ya utoaji wa huduma za kisheria katika jamii, akisema hatua hiyo itaongeza ufanisi na kuimarisha imani ya Wananchi kwa Taasisi hiyo.

Vilevile, aliwasisitiza watumishi wa Mahakama kuyatunza majengo hayo na miundombinu mingine iliyojengwa ili yaweze kudumu na kuendelea kutoa manufaa kwa jamii pamoja na watumishi kwa ujumla.

Kwa upande wao, baadhi ya Wananchi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakisema itapunguza umbali waliokuwa wakisafiri kufuata huduma za Mahakama.

Mbali na viongozi hao, hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi, Fatima Saidi Kubenea. Katika hotuba yake, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwepo kwa ushirikiano mzuri kati ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Mahakama ili kuhakikisha huduma za haki zinawafikia wananchi kwa ufanisi zaidi.

Mahakama za mwanzo zitakuwa na jukumu la kusikiliza na kuamua kesi ya ngazi ya kwanza, madai kulingana na mamlaka yao kisheria. Wananchi wamehimizwa kutumia vyema fursa hiyo kwa kufuata taratibu za kisheria na kuepuka kujichukulia sheria mkononi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akiwasili katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Wageni waalikwa walioshiriki kwenye uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mtwra, Mhe. Said Ding’ohi (kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea pamoja wasikiliza taarifa ya ujenzi wa majengo ya Mahakama.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Mtwara akitoa hotuba yake katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo iliyofanyika Chikundi.

Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea akihutubia katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitoa hutuba katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo eneo la Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akikata utepe katika shughuli ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto,) Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya (katikati) na Jaji wa Mahakama ya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara (kulia) kwa pamoja wakikagua ukumbumbi wa wazi wa Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Said Ding’ohi (wa pili kushoto), Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana (wa kwanza kushoto), Naibu Msajili, Mhe. Elia Mrema (wa kwanza kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea (wa pili kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Kanda ya Mtwara.

Habari hii imehaririwa na FAUSSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKAMA MUSOMA YAFANYA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama Musoma.

Mahakama Kanda ya Musoma hivi karibuni, imefanya mkutano wa Baraza la Wafanayaka kwa mwaka 2026 na kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji.

Akifungua Baraza hilo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Fahamu Mtulya, aliwasisitiza wajumbe wote kuwa huru kueleza changamoto zao.

Mhe. Mtulya alisema kuwa sehemu ya kutatua changamoto zilizo ndani ya uwezo wa Kanda ni katika Baraza hilo na zile zilizo nje ya uwezo wa Kanda zichukuliwe na kuwasilishwa kwa Mwajiri.

Alisema Baraza la Wafanyakazi ndio sehemu muhimu ambayo Watumishi wanapata nafasi ya kuongea na Mwajiri pamoja na Wawakilishi wa Chama cha Wafanyakazi, yaani TUGHE, ili kupata ufumbuzi wa changamoto wanazokutana nazo lakini pia kujua nini Mwajiri na Serikali kwa pamoja wanafanya ili kuboresha mazingira ya kazi.

Naye katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara, Bw. Hamis Mwisa, alipata wasaa wa kuelezea na kutoa elimu juu ya mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi na kutoa pongezi kwa namna ulivyoweza kuainisha wajumbe ambao wanabeba uwakilishi mzuri wa Watumishi, jambo litakaloongeza ufanisi na uwazi katika Mabaraza ya Wafanyakazi.

Aidha, Mjumbe wa Baraza Kuu Serikalini anayeteuliwa na TUGHE Makao Makuu, Dkt. John Bomani, alimpongeza Mwenyekiti wa Baraza kwa namna anavyoliendesha kwa kuzingatia kanuni za demokrasia na kuruhusu uhuru wa maoni.

Alisema kuwa mwenendo huo wa uwazi ni kiashiria cha mahusiano mazuri kati ya Viongozi na Watumishi, jambo ambalo linasaidia katika kuweka mazingira bora na rafiki ya kazi.

Katika mkutano wa Baraza hilo, wajumbe walipata nafasi ya kuelezwa kilichojiri katika Baraza la mwaka 2025 pamoja na matokeo ya hoja zilizowasilishwa. Pia walieleza hoja mbalimbali ambazo zilikubalika zichukuliwe na kuwasilishwa kwa Mwajiri katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.

Pamoja na hayo, katika Baraza hilo wajumbe walipitishwa katika taarifa mbalimbali za kiutendaji, ikiwemo taarifa ya bajeti inayoendelea ya mwaka wa fedha 2025/2026 pamoja na makisio ya bajeti ijayo ya mwaka 2026/2027, huku majukumu yaliyopangwa kutekelezwa kwa kila ngazi ya Mahakama ndani ya Kanda yakianishwa.

Vilevile, wajumbe wa Baraza hilo walipata nafasi ya kupendekeza na kuchagua mtumishi hodari wa Mahakama Kanda ya Musoma, zoezi lililosimamiwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo.

Akihitimisha Baraza hilo, Mwenyekiti aliwashukuru na kuwapongeza Watumishi kwa namna walivyowasilisha hoja zao, pamoja na Viongozi wa TUGHE Mkoa wa Mara, hususan Katibu, Bw. Hamis Mwisa, kwa namna anavyojitoa kushiriki katika vikao na kutoa elimu kwa wajumbe juu ya masuala mbalimbali, ikiwemo elimu ya Mabaraza ya Wafanyakazi.

Viongozi na wajumbe wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi, Kanda ya Musoma, wakiimba kwa pamoja wimbo wa mshikamano daima wakati wa ufunguzi.

Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Musoma, Bw. Kandana Lucas, akisema neno wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, akisisitiza jambo wakati wa mkutano huo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Musoma, Bw. Kandana Lucas (kushoto) pamoja na Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi Musoma, Bi. Teckla Patrick, wakihesabu kura za wajumbe wakati wa zoezi la kuchagua mtumishi hodari wa Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Simo Lubili (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya kikao cha Baraza la Wafanyakazi la mwaka 2025 pamoja na majibu ya hoja zilizowasilishwa mwaka huo.

Katibu wa TUGHE Mkoa wa Mara, Bw. Hamis Mwisa (aliyesimama) akifafanua mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi wakati wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa Baraza Kuu Serikalini, Dkt. John Bomani, akitoa ufafanuzi wa jambo wakati wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Musoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Jumanne, 31 Machi 2026

KITUO JUMUISHI CHA MASUALA YA FAMILIATEMEKE CHATOA MAFUNZO KWA WAJANE

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam

Kituo Jumuishi cha Masuala ya FamiliaTemeke tarehe 28 Machi, 2026 kiliendesha mafunzo maalum kwa wajane wa Wilaya ya Temeke kwa lengo la kuwajengea uelewa kwenye haki zao za kisheria, hususan katika masuala ya urithi na mirathi.

Halikadhalika, washiriki wa mafunzo hayo walipatiwa elimu ya kisheria itakayowasaidia kulinda haki zao na za watoto wao, kusimamia mali za marehemu kwa mujibu wa sheria na kuepuka migogoro ya mirathi katika familia na jamii

Mafunzo hayo yalifunguliwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, ambaye alisisitiza umuhimu wa wajane kufahamu haki zao, kufungua mirathi kwa wakati na kutumia mifumo ya kisheria ili kuepusha migogoro ya kifamilia.

Mtandao wa Mashirika yanayotoa Msaada wa Sheria Tanzania (TANLAP), uliowakilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa TANLAP, Wakili Fransisca Silaya, ndiyo uliofadhili mafunzo hayo.

Wakili Silaya, akizungumza wakati wa mafunzo hayo, alionesha dhamira ya Taasisi hiyo kuendelea kuunga mkono juhudi za utoaji wa elimu ya kisheria kwa makundi maalum katika jamii.

Mafunzo hayo yalijumuisha mada kuu nne zilizowasilishwa na wakufunzi wenye uzoefu, ikiwemo Urithi na Mirathi na Sheria za Urithi Tanzania zilizowasilishwa na Mhe. Magdalena Malaba.

Nyingine ni Kufungua Mirathi na Nyaraka Muhimu na Wosia na Ulinzi wa Haki zilizowasilishwa na Mhe. Edna Mollel.

Katika mada hizo, washiriki walipata uelewa wa kina kuhusu taratibu za mirathi, haki zao za kisheria, umuhimu wa nyaraka sahihi pamoja na namna ya kuandika wosia na kulinda haki zao.

Mafunzo yalihusisha wajane kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Temeke, wakiwemo wanachama wa vikundi vya kijamii, hususan kikundi cha VIWOTA Women Group. Washiriki walionesha hamasa kubwa ya kujifunza na kuchangia mijadala.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, alifunga mafunzo hayo na kuwasihi washiriki wote kutumia maarifa waliyoyapata maarifa kwenye maisha yao na kuwafikishia wengine elimu hiyo kwani ni nyenzo ya kujikomboa dhidi ya dhuluma na kuhakikisha haki inatendeka.

“Napenda pia kuwakumbusha kuwa taasisi zetu za haki, ikiwemo Kituo Jumuishi Temeke, zipo kwa ajili yenu. Msisite kufika pale mnapohitaji msaada wa kisheria au ushauri,” alisema.

Bw. Mashalla alitumia fursa hiyo kuushukuru Mtandao wa Asasi za Msaada wa Sheria Tanzania (TANLAP) kwa mchango wao katika kufanikisha mafunzo hayo, kwani mchango wao umeleta mabadiliko chanya katika maisha ya washiriki.

Aliwashukuru pia wakufunzi kwa kujitolea kutoa maarifa na kwa uvumilivu wao katika kuhakikisha kila mshiriki anaelewa mada zilizowasilishwa. “Mafunzo haya yamekuwa ya manufaa makubwa na yamegusa moja kwa moja maisha yetu ya kila siku,” alisema.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo (Picha na Maktaba).

Kaimu Mkurugenzi wa Mtandao wa Asasi za Msaada wa Sheria Tanzania (TANLAP), Bi. Fransisca Silaya.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya kwenye Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Magdalena Malaba, akiwsilisha mada kwenye mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo kwenye Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Moleli, akiwasilisha mada kwenye mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo wakifuatilia kilichokuwa kinajiri.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Bw. Samson Mashalla, akizungumza wakati anahitimisha mafunzo hayo.

Picha ya pamoja ya washiriki wakati wa mafunzo hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA YAFANYA KIKAO CHA MENEJIMENTI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, amewapogeza Watumishi wa Mahakama Kanda ya Musoma kwa uwajibikaji mzuri uliowezesha Mahakama hiyo kuwa ya pili kitaifa kwa kasi nzuri ya umalizaji wa mashauri.

Mhe. Mtulya alitoa pongezi hizo katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma kilichofanyika hivi karibuni wilayani Serengeti katika ukumbi wa Ofisi ya Mashtaka.

Alisisitiza umuhimu wa vikao vya menejimenti ambavyo vinatumika kuweka mikakati mbalimbali ya kiutendaji pamoja na kusisitiza utekelezaji wa maelekezo ya Viongozi wa juu, jambo lililodhihirishwa kwa matokea mazuri ya usikilizaji na umalizaji wa mashauri.

Aidha, katika kikao hicho kinachoundwa na wajumbe kutoka Mahakama Kuu Musoma, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma na Mahakama za Wilaya za Musoma, Butiama, Bunda, Serengeti, Tarime na Rorya, ziliwasilishwa taarifa mbalimbali za utendaji kazi kwa robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26.

Kuliwasilishwa pia taarifa za Mkaguzi wa Ndani, Ofisa TEHAMA, miradi inayoendelea ndani ya Kanda na ushiriki katika matukio ya kijamii.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, alisisitiza utekelezaji wa maelekezo ya Viongozi wa Mahakama, ikiwemo ufungaji wa mirathi, kuendelea na utoaji wa adhabu mbadala pamoja na usikilizaji wa mashauri kwa wakati ili kuepuka kuzalisha mlundikano.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Leonard Maufi, alielezea mikakati mbalimbali ya Kanda, ikiwemo uboreshaji wa miundombinu. Alisema kwa mwaka wa fedha, Kanda inaendelea na ukarabati mkubwa wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Nyaburongo iliyoko Wilayani Rorya kwa kutumia fedha za ndani.

Pia alielezea hatua iliyofikiwa katika miradi inayoendelea ya ujenzi wa Mahakama za Wilaya Serengeti na Tarime. Aidha, aliwaasa Watumishi kuendelea kuzingatia kanuni, taratibu na miongozo ya utumishi wa umma.

Akihitimisha kikao hicho, Mhe. Mtulya aliwakumbusha wajumbe mafanikio yaliyopatikana ndani ya Kanda, ikiwemo kutovuka mwaka na mashauri mlundikano kwa miaka mitatu mfululizo na ukarabati wa majengo ya Mahakama, hasa za Mwanzo.

Alitaja mafanikio mengine kama ulinzi wa mipaka ya maeneo ya Mahakama, upatikanaji wa hati, umoja na ushirikiano wa kikanda kwenye kazi na matukio ya kijamii kma kushiriki matukio ya huzuni na furaha.

Hivyo aliwaasa wajumbe hao kwenda kuwasimamia vyema Watumishi katika maeneo yao ili, kwa pamoja waweze kufikia malengo ya Kanda yaliyowekwa.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Leonard Maufi (kushoto), wakichambua kwa makini baadhi ya taarifa zilizowasilishwa na wajumbe wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Wajumbe wa kikao cha Menejiment Kanda ya Musoma kutoka Wilaya mbalimbali wakiwasilisha taarifa za utendaji kazi katika vituo vyao vya kazi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mhe. Veronica Mugendi (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa kituo chake katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Kandana Lucas (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na taarifa ya miradi inayotekelezwa ndani, huku wajumbe wakifuatilia kwa makini taarifa hiyo wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Mkaguzi wa Ndani wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Andala Odock (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya ukaguzi katika kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Afisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Japhet Mnyetta (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya hali ya miundombinu na matumizi ya TEHAMA ilivyo ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, akiwasilisha taarifa ya hali ya mashauri ilivyo ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma Bw. Leonard Maufi (aliyesimama), akifafanua jambo wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Mjumbe wa kamati ya utalii (matukio ya kijamii) ambaye ni Mhasibu wa Mahakama Kuu Musoma, Bi. Samira Nkya (aliyesimama), akiwasilisha taarifa ya ushiriki katika matukio ya kijamii ndani ya Kanda ya Musoma wakati wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), akisisitiza jambo kwa wajumbe wa kikao cha Mnenejimenti Kanda ya Musoma wakati wa kikao hicho.

Picha ya pamoja ya wajumbe wa kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma walipotembelea mmoja ya miradi inayoendelea ndani ya Kanda hiyo, ambayo ni ujenzi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Serengeti, mara baada ya kikao cha Menejimenti Kanda ya Musoma kilichofanyika Wilayani Serengeti. 

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.