Na AIDAN ROBERT-Mahakama Kigoma
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania
Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile ameongoza hafla ya
uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Bangwe, Wilaya ya Kigoma, Manyovu iliyopo Wilaya
Buhigwe na Heru Juu iliyopo Wilaya ya Kasulu.
Akizungumza katika
hafla hiyo iliyofanyika tarehe 19 Juni, 2026, Mhe. Rwizile amesisitiza kuwa, “tunachokishuhudia leo ni maono
ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju,
aliwahi kusema, alipokuwa anahutubia Mkutano wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania
(TMJA) Tarehe 13 Mwezi Januari, 2026 Dodoma, ninamnukuu; - "Ujenzi wa
majengo ya Mahakama, uwezeshaji wa rasilimali watu na fedha, pamoja na
kuboresha mazingira ya kazi kwa Majaji, Mahakimu, na watumishi wa Mahakama ni
nguzo muhimu zinazowezesha uhuru wa Mahakama kuwa halisi, unaoonekana na
unaotekelezeka kwa ustawi wa wananchi na utawala wa sheria kwa ujumla."
Jaji Rwizile amesema, maneno hayo ya Kiongozi
Mkuu wa Mhimili wa Mahakama, yanasadifu haja ya watu kupata haki katika maeneo
ambayo si tu haki inakuwa imetendeka bali pia inaonekana kutendeka kwa
kuzingatia unadhifu wa watoa haki, ubora wa haki yenyewe na mazingira mazuri ya
mahali ambapo haki hiyo hutolewa.
“Kupitia maono hayo ya viongozi wetu wakuu
wa Mahakama na Serikali, leo hii tunafurahia uzinduzi wa majengo haya
tukitambua kuwa, kinachozinduliwa hapa si Majengo wala Samani au Nakshi
zinazopendezesha majengo haya, Bali ni dhana thabiti ya Mahakama kama chombo
pekee cha utoaji haki kwa vitendo kwa wananchi wetu,” amesema Mhe. Rwizile.
Aidha, ameongeza kuwa, Mahakama hizo tayari wameshazipangia
watumishi mahsusi wa kutoa huduma zilizo bora kuendana na ubora wa majengo
yenyewe, amesema, “leo hii baada ya ufunguzi, mashauri yataanza kusajiliwa hapa
Bangwe na pale Heru Juu na Manyovu kadhalika wataendelea kupatiwa huduma kwa
kadri ya mahitaji yao,” amebainisha Jaji Mfawidhi huyo.
“Nitoe
Wito kwa Mahakimu na Watumishi wa Mahakama hizi mpya, pamoja na Wengine kwa
ujumla, ninyi ndio nguzo kuu ya usimamiaji haki katika ngazi hii. Tendeni kazi
kwa mujibu wa viapo vyenu kwani kiapo chetu ni kizuri kinasema bila ya Huba,
Woga, Chuki wala upendeleo wa aina yoyote, mnapaswa kuendelea kulinda imani ya
wananchi kwa Mahakama kwa kutoa maamuzi yasiyokuwa na upendeleo, hila au
ushawishi wa aina yoyote,” amesisitiza Jaji Mfawidhi huyo.
Kadhalika, amesema kuwa, ni muhimu kutoa
maamuzi yenye rejea thabiti katika sheria na misingi iliyowekwa na Mahakama za
ngazi za juu, “hii inawataka muwe wa kisasa, wenye kujiongezea maarifa
na kufuatilia mabadiliko katika maeneo mbalimbali ya kisheria mtakayokuwa
mkiyafanyia kazi,” alisema Jaji Rwizile.
“Majengo haya mapya ni mwendelezo wa utatuzi
wa changamoto za muda mrefu za kijiografia katika Mkoa wa Kigoma, hakuna shaka
kwamba kipindi cha nyuma wakazi wengi walilazimika kusafiri umbali mrefu na
kuingia gharama kubwa kufuata huduma katika Mahakama za Mwanzo zilizokuwa mbali
na makazi yao kiasi cha kupoteza muda mwingi kwenye mashauri na sio shughuli za
kiuchumi na kijamii,” alieleza Mhe. Rwizile.
Aliongeza kuwa, kupitia maboresho hayo ya
ujenzi wa Mahakama mpya za Mwanzo, wananchi wataendelea kufikiwa na huduma hizo
na kuokoaa muda na gharama.
“Sote tunakubalina kuwa, umbali wa kutoka
Bangwe, Kigoma Mjini, Katonga, Gungu, Kibirizi, Mwanga Kusini na Mwanga
Kaskazini, Katubuka na maeneo mengine jirani, haikuwa rahisi kutembea na
kufuata huduma Mwandiga au Ujiji ambako Mahakama zinapatikana. Kwa sasa uwepo
wa Mahakama ya Mwanzo Bangwe ni faraja na majibu ya wengi katika kufuata haki.
Inakadiriwa takribani watu 62,582 watanufaika na huduma hii,” alisema Jaji
Rwizile.
Kadhalika alisema kwamba, kwa Mahakama za
Mwanzo Heru Juu na Manyovu; Wananchi wa Maeneo ya jirani na Mahakama hizo
wataondolewa adha ya kusafiri umbali mrefu kuitafuta haki huku shughuli zao
binafsi zikikwama, wanufaika wa huduma hiyo inakadiriwa kuwa watu 24,242 kwa
kuzingatia Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, pia huduma ya Mahakama ya
Mwanzo Manyovu hapo awali ilikuwa inapatikana Tarafa ya Munanila, na baadae
kutokana na uchakavu wa jengo la awali kushindwa kuwa salama kwa matumizi ya
binadamu huduma ikahamia kwa muda katika
Ofisi za Serikali ya Kijiji.
Hata hivyo, Mhe. Rwizile alibainisha kuwa,
kwa sasa Mahakama imesogezwa karibu na mpaka wa Tarafa mbili yaani Manyovu na
Mnanila, Tarafa ambazo zina idadi kubwa ya watu, ambapo Tarafa ya Manyovu ina
wastani wa watu 131,298 wakati Tarafa ya Munanila ina wastani wa watu 15,273 kwa
mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022.
“Kumbe uwepo wa Jengo hili kwa sasa litatoa
huduma Kata za Munzeze, Janda, Rusaba, Muhinda, Mwayaya, Mkatanga, Mubanga,
Kinazi, Kibwigwa na Bukuba, wakati huohuo Kata za Munanila na Nyakimwe nazo
zikipata huduma za Mahakama katika jengo hilo jipya,” alieleza Jaji Rwizile.
Kwa upande wake Mgeni wa Heshima katika
hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro, alisema
kuwa, uzinduzi wa majengo hayo mapya ni kielelezo tosha kuwa Mahakama
imedhamiria kwa dhati kuhakikisha kuwa wananchi hawapati tu haki, bali
wanaipata katika mazingira yenye staha, hadhi na usalama.
“Ujenzi na uzinduzi wa miundombinu hii ya
kisasa sio jambo la bahati mbaya ni taswira halisi ya utambuzi wa kina na
dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita, kupitia Wizara ya Katiba na
Sheria, maboresho haya makubwa ya miundombinu ni tafsiri ya maono ya kimkakati
ya Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa mstari
wa mbele kuhakikisha tunaimarisha, tunakuza na kulinda kikamilifu Uhuru wa
Mahakama ikiwa ni utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” alisema
Balozi Mhe. Sirro.
Hafla hiyo iliyofanyika katika viunga vya
Mahakama ya Mwanzo Bangwe ilihudhuriwa na Viongozi wa ngazi ya Wilaya na Mkoa
wa Kigoma pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John
Francis Nkwabi, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe.
Fadhili Mbelwa pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw.
Yusufu Kasuka.
Wageni wengine ni Kamati ya Ulinzi na Usalama
ya Mkoa na Wilaya, Wakuu wa Wilaya za Kasulu na Buhigwe, pamoja Mahakamu
wafawidhi wa Wilaya za Buhigwe, Kigoma, Kasulu, Kibondo, Kakonko na Uvinza,
sambamba na wadau wa Mahakama na wananchi pamoja na vikundi vya burudani.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akikata utepe kuashiria ufunguzi wa Mahakama za Mwanzo tatu za Bangwe, Manyovu na Heru Juu uliofanyika tarehe 19 Juni, 2026. Wanaoshuhudia kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi na kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Kigoma Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon Nyakoro Sirro (kushoto) kwa pamoja wakifungua kitambaa cha jiwe la msingi la Jengo hilo ikiwa ni ishara ya kufunguliwa kwa Mahakama.
Jaji Mfawidhi
wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba
Rwizile akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mahakama za Mwanzo tatu katika hafla
iliyofanyikia katika Viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Bangwe.
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi
Simon Nyakoro Sirro akitoa salamu za Serikali katika ufunguzi wa Mahakama za Mwanzo tatu katika hafla iliyofanyikia katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo
Bangwe.
Jaji Mfawidhi
wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe ikiwa ni
ishara ya alama na historia katika Mahakama hiyo ya Mwanzo Bangwe mara baada ya
kufunguliwa.
Jaji wa
Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi akipanda mti
wa matunda katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe ikiwa ni ishara ya alama na
historia katika Mahakama hiyo ya mwanzo hiyo mara baada ya kufunguliwa.
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi
Simon Nyakoro Sirro akipanda mti wa matunda katika eneo la Mahakama ya Mwanzo
Bangwe ikiwa ni ishara ya alama na historia katika Mahakama hiyo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine
Karichuba Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (kushoto), Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Balozi Simon
Nyakoro Sirro (kulia). Waliosimama ni Watumishi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)