Jumatatu, 9 Machi 2026

MAWAKILI MKOA WA MWANZA WALA KICHAPO GEITA

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita imeibuka na ushindi wa mabao 3–2 dhidi ya Timu ya Mawakili kutoka Mwanza katika mchezo wa kirafiki uliochezwa Machi 7, 2026.

Mchezo huo ulifanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari St. Aloysius vilivyopo Shilabela, Manispaa ya Geita, ambapo timu hizo zilionyesha ushindani mkubwa na burudani kwa mashabiki waliohudhuria.

Katika mchezo huo, bao la kwanza la Mahakama Kuu Geita lilifungwa na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Nyang’hwale, Robert Nyando. Bao la pili lilifungwa na Ateba Stephano huku bao la tatu likifungwa na Mhasibu wa Mahakama Kuu Geita, Goodluck Machange.

Kwa upande wa Timu ya Mawakili Mwanza, bao la kwanza lilifungwa kwa njia ya penalti na Wakili Fredrick Magaiwa baada ya mlinda mlango wa Mahakama Kuu Geita kushika mpira ndani ya eneo la hatari. Bao la pili lilifungwa na Wakili Hensen Emmanuel.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Jaji wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Geita, Griffin Mwakapeje, kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, aliwakaribisha wageni hao katika Mahakama Kuu Geita na kuwashukuru kwa kushiriki mchezo huo.

Alisema lengo la michezo hiyo ni kuimarisha mahusiano, ushirikiano na kubadilishana mawazo kati ya Wadau wa sekta ya sheria.

“Nia ya mashindano haya ni kutuleta pamoja, tusahau kwa muda majukumu ya kesi na kujumuika katika kujenga ushirikiano pamoja na kubadilishana mawazo. Pia inaonyesha kuwa licha ya majukumu mengi ya kisheria tuliyonayo, bado tunashiriki kikamilifu katika michezo,” alisema Jaji Mwakapeje.

Aidha, alimshukuru Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Fredrick Lukuna, kwa kuratibu na kufanikisha mashindano hayo. Aliongeza kuwa baada ya ujio wa Mawakili wa Mwanza mjini Geita, watumishi wa Mahakama Kuu Geita pia watafanya ziara ya kwenda Mwanza kwa ajili ya michezo kama sehemu ya kuimarisha ushirikiano huo.

Aliwasihi Mawakili wa Mwanza kuangalia uwezekano wa kusaidia Mkoa wa Geita kupata chapter yake ya Chama cha Mawakili ili kuimarisha shughuli za kisheria na ushirikiano katika ukanda huo.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Mawakili (Mwanza Chapter) aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Geita kwa kukubali mwaliko na kushiriki mchezo huo.

Alisema licha ya timu yao kupoteza, wamefurahishwa na kiwango cha wachezaji wao na wameuchukulia mchezo huo kama fursa ya kuimarisha timu yao pamoja na afya za Mawakili.

Aliongeza kuwa hatua za Mkoa wa Geita kuwa na chapter yake ya Chama cha Mawakili zinaendelea vizuri, huku akiwakaribisha watumishi wa Mahakama Kuu Geita kutembelea Mwanza kwa ajili ya mchezo mwingine wa kirafiki siku zijazo.

Wachezaji wa Timu ya Mahakama na Mawakili Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kuanza.

Wachezaji wa kikosi cha kwanza kutoka katika Timu ya Mawakili wa Serikali na Kujitegemea Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kuanza.

Wachezaji wa kikosi cha kwanza  kutoka timu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja.

Mchuano ukiwa unaendelea, William Msuya wa Mahakama ya Mwanzo Kharumwa akijaribu kumpokonya mpira Wakili wa Serikali Mwanza.

Wachezaji na Mashabiki wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Griffin Mwakapeje (wa katikati msitari wa kwanza) na Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Fredrick Lukuna wa tatu kushoto mistari wa kwanza).
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 


 

WAFANYAKAZI WANAWAKE WA MAHAKAMA YA TANZANIA WAWAGUSA WATOTO NJITI BENJAMIN MKAPA

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma

Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, watumishi Wanawake wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma tarehe 06 Machi, 2026 walitembelea watoto njiti (premature) wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Watoto hao ni wale waliozaliwa kabla ya wakati na waliokuwa wakipatiwa huduma hospitalini hapo wakiwa na umri wa kuanzia siku moja hadi siku 28 tangu kuzaliwa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Afisa Rasilimali Watu Mwandamizi wa Mahakama, Bi. Gladness Godwin Massawe alisema lengo la wanawake kutembelea Hospitali hiyo ni kujionea hali ya watoto hao pamoja na kutambua umuhimu wao katika jamii.

Alisema katika kuadhimisha siku hiyo waliamua kushiriki katika tendo la kijamii kwa kuwatembelea watoto hao na kuwapatia baadhi ya mahitaji muhimu pamoja na kugharamia matibabu ya mtoto mmoja aliyekuwa akipatiwa huduma katika Chumba cha Uangalizi Maalum (ICU).

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya kuonesha upendo, mshikamano na kuwapa matumaini watoto hao pamoja na familia zao.

Wakati huohuo akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo kwa niaba ya Uongozi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto, Dkt. Rehema Yona alishukuru kwa msaada huo.

"Msaada huu umeleta faraja na matumaini kwa watoto pamoja na wazazi wao na umeonesha moyo wa upendo na kujali jamii," alisema Dkt. Rehema huku akiwatakia heri na baraka kwa kuendelea kushirikiana na jamii katika kusaidia wenye uhitaji.

 Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuwasili katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma tarehe 06 Machi, 2026. 

Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania wakielekea wodini kuona watoto katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH).

 

    Afisa Rasilimaliwatu Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Gladness Massawe akizungumza jambo mara baada ya kupokelewa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa.


    Afisa Rasilimaliwatu Mwandamizi wa Mahakama, Bi Gladness Massawe (wa pili kushoto) akikabidhi zawadi kwa  Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa watoto wa Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Dkt. Rehema Yona mara baada ya kuwasili katika hospitali hiyo.

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dkt. Rehema Yona akitoa shukrani mara baada ya kupokea wageni hao.





Sehemu ya watumishi wanawake kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania walioshiriki katika zoezi la utoaji msaada kwa watoto njiti waliopo Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka tarehe 08 Machi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Jumamosi, 7 Machi 2026

JAJI MAGHIMBI AWAFUTURISHA WATUMISHI KANDA YA DAR ES SALAAM

  •  Achukua fursa hiyo kuwakumbusha watumishi kufanya kazi kwa bidii

 Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi ameandaa Iftar maalum kwa ajili ya kuwafuturisha Watumishi wa Kanda hiyo. 

Mhe. Maghimbi aliyasema hayo wakati wa hafla ya iftar aliyoiandaa kwa ajili wa watumishi wa Kanda hiyo iliyofanyika jana tarehe 06 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Dar es Salaam. 

Aidha, Mhe. Maghimbi amewaasa watumishi wa Kanda hiyo kufanya kazi kwa bidii ili kufikia malengo.

Akizungumza wakati wa kuwakaribisha Majaji na watumishi wengine  kwa ajili ya kufuturu, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo alisema kwa muda sasa, Jaji Mfawidhi huyo amekuwa akiandaa iftar kwa watumishi wa Dar es Salaam, lakini safari hii amepanua wigo na kuwaalika Wafawidhi, mtendaji wa Mkoa wa Pwani na Maafisa na kujumuika pamoja katika Iftar hiyo.

“Tumekuwa tukifanya kwa kuwaalika Wafawidhi wa Dar es Salama tu  pamoja na viongozi wengine lakini safari hii tumeongeza wigo Mahakimu Wafawidhi Mkoa wa Pwani, Watendaji pia pamoja na Maafisa wao,” alisema Mhe. Mbadjo.

Hafla hiyo ilitanguliwa na dua ya kuwaombea watumishi wawili wa Kanda hiyo waliotangulia mbele ya haki na dua hiyo iliongozwa na Msaidizi wa Kumbukumbu kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Khalid Kawiza.

Akitoa shukrani baada kushiriki iftar hiyo, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Arnold Kirekiano alisema anamshukuru Mungu kwa ajili ya Jaji Mfawidhi kwa kutoa sadaka hiyo kwa watumishi maana inaleta umoja baina ya watumishi, ameomba kwa wakati mwingine ifanyike mahali pengine na kwa namna nyingine ambayo Mungu atawajaalia.

Aidha, Mhe. Kirekiano alisema, siku hiyo imewapa fursa ya kutafakari pamoja kutokana na ratiba za kazi na mfungo huo hawajaweza kuonana, lakini kwa jambo hilo wameweza kukaa kwa pamoja.

Kadhalika, Jaji Kirekiano amemtakia heri Mhe. Maghimbi lakini pia watumishi wote walioshiriki jambo hilo ili ikawe heri kuwasaidia katika kuwatumikia wananchi.

Amewakumbusha kwamba wanakutana kwa ajili ya kazi za kuwahudumia wananchi na Jaji Mfawidhi ameonesha ukarimu, nao wanaweza kulipa kwa kuonesha ukarimu kwa wateja wanaowahudumia kwa upendo na kwa furaha.

Mhe. Maghimbi amekuwa na utaratibu wa kuandaa iftar kila mwaka kwa takriban miaka mitatu mfululizo.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akitoa neno kabla ya kupata Iftar jana tarehe 06 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama hiyo. Aliyeketi kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Butamo Phillip  na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale.

 Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam wakiwa katika hafla ya Iftar iliyoandaliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (wa tatu kushoto).





 Majaji na Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam wakipata Iftar.


Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Livin Lyakinana (katikati) na Mhe. Aziza Mbadjo (wa pili kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Jiji, Ubungo, Ilala na Temeke mara baada ya kufuturu iftari iliyoandaliwa na Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo, Mhe. Salma Maghimbi.

 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi (katikati) akiwa na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Kibiti, Mkuranga,Bagamoyo na Kibaha Baada ya Iftar iliyofanyika jana tarehe 06 Machi, 2026 Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Msaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Khalid Kawiza akitoa dua wakati wa hafla ya Iftar.

Watumishi wakifuatilia dua kabla ya Iftar.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Arnold Kirekiano akitoa neno la shukrani baada ya Iftar.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

MSAJILI MKUU AFUNGA MAFUNZO YA MAHAKIMU WAKAZI 92

.Awasisitiza kuzingatia maadili, kuimarisha weledi na kutumia TEHAMA katika utoaji wa haki

Na. James Busanya & Halima Mnete – Mahakama, Dodoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, amewasisitiza Mahakimu Wakazi wapya kuzingatia maadili ya kazi, kuongeza weledi wa kitaaluma na kulinda taswira ya Mhimili wa Mahakama katika utoaji wa haki kwa wananchi.

Mhe. Nkya ametoa wito huo jana tarehe 6 Machi 2026 katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, wakati akifunga rasmi mafunzo elekezi ya siku kumi kwa Mahakimu Wakazi wapya 92, mafunzo yaliyoandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Nkya amesema ana furaha kushiriki hitimisho la mafunzo hayo na kueleza matumaini kuwa siku kumi za mafunzo zimewajengea washiriki uwezo mpana kuhusu majukumu ya uhakimu na misingi ya utoaji wa haki kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Amesema kazi ya uhakimu ni wito unaohitaji umakini mkubwa kwa kuwa sehemu kubwa ya majukumu yake inahusiana moja kwa moja na utoaji wa haki kwa jamii, hivyo Mahakimu wanapaswa kutambua uzito wa dhamana waliyopewa na kuitumikia kwa uadilifu na weledi wa hali ya juu.

Katika kusisitiza hilo, alimnukuu Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliyewahi kusema kuwa zipo kazi nyingi zinazoweza kufanywa na mtu yeyote, lakini kazi ya uhakimu si mojawapo kutokana na uzito wake na mahitaji ya juu ya kitaaluma pamoja na kimaadili.

Aidha, Mhe. Nkya aliwakumbusha Mahakimu hao kuwa uhuru wa Mahakama upo pale Hakimu anapozingatia kiapo chake cha kazi na kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria bila kuingiliwa na mtu au chombo chochote.

Msajili Mkuu huyo, aliwataka kushirikiana na wadau wa sekta ya haki pamoja na viongozi wengine katika maeneo watakayopangiwa kazi, akieleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kuboresha utendaji kazi na kuongeza ufanisi wa huduma ya utoaji haki kwa wananchi.

Vilevile, Mhe. Nkya aliwataka Mahakimu hao kuzingatia Kanuni za Maadili ya Mahakama za mwaka 2020 ndani na nje ya Mahakama kwa kusoma, kuelewa na kuzifuata kikamilifu, akibainisha kuwa Mahakama imara hujengwa na watumishi wenye uadilifu.

“Mahakama imara hujengwa na watumishi wenye uadilifu na kosa la Hakimu mmoja linaweza kuchafua taswira ya Mhimili mzima wa Mahakama,” alisisitiza Mhe Nkya.

Kwa upande wa maendeleo ya kitaaluma, Msajili Mkuu aliwahimiza Mahakimu hao kuendelea kujifunza na kujielimisha ili kuongeza weledi wao katika utoaji wa haki na kuepuka makosa yanayoweza kuepukika katika utendaji wao wa kazi.

Pia aliwataka kujiepusha na vitendo vya rushwa, upendeleo na ubaguzi, kuzingatia nidhamu ya kazi, kutumia lugha ya staha kwa wadau wa Mahakama pamoja na kutumia rasilimali za ofisi kwa ufanisi.

Katika hatua ya kuimarisha utendaji kazi wao, Mahakimu hao walikabidhiwa vitendea kazi ikiwemo kompyuta mpakato zitakazowasaidia katika uandishi wa hukumu na uendeshaji wa mashauri mbalimbali kwa njia ya kidijitali.

Mhe. Nkya pia aliwahimiza kuwakilisha ipasavyo matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kazi zao za kila siku ili kuongeza ufanisi na kasi ya utoaji wa haki.

Aidha, Mhe. Nkya aliwataka Mahakimu hao kulinda taswira ya Mahakama wakati wote na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha kukutana katika mafunzo hayo, huku akiwaombea mafanikio mema katika utekelezaji wa majukumu yao mapya ya kuhudumia jamii kupitia Mhimili wa Mahakama.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya, akifunga rasmi mafunzo elekezi ya siku 10 kwa Mahakimu Wakazi wapya 92, yalioandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania jana tarehe 6 Machi, 2026 katika Ukumbi wa mikutano Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi wapya waliomaliza mafunzo ya siku 10 wakisikiliza hotuba ya Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (hayupo pichani)

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya (Katikati) akiwa Meza Kuu na Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo Bi. Patricia Ngungulu (wa kwanza kulia) wakati wa kufunga mafunzo hayo elekezi kwa Mahakimu Wakazi Wapya 92.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi wapya waliomaliza mafunzo ya siku 10 wakisikiliza hotuba ya Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (hayupo pichani)

 (Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




Ijumaa, 6 Machi 2026

HUDUMA ZA MAHAKAMA KUU KATAVI KUANZA WAKATI WOWOTE KUANZIA SASA

Na. Ally Ramadhani - Katavi

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mkoa wa Katavi Mhe. Silivia S. Lushasi tarehe 5 Machi, 2026 amefanya kikao na wadau wa Mahakama cha maandalizi ya uanzishaji wa masjala ndogo ya Mahakama Kuu, Kanda ya Katavi na kuwapongeza wadau kwa ushiriki wao kwa kuhakikisha masjala hiyo inaanza kuwatumikia wananchi.

Akizungumza katika kikao, Mhe. Lushasi amesema, taarifa itatolewa kwa wananchi muda wowote ya kuanza kupata huduma za Mahakama Kuu Mara tu itakapokuwa imetangazwa rasmi kwenye Tangazo la Serikali.

Naibu Msajili huyo amesema, Mahakama Kuu itakapoanza mkoani Katavi, mashauri yote yaliyo sajiliwa Mahakama Kuu Sumbawanga yataendelea huko huko ila yale mapya yatasikiliziwa masjala mpya ya Katavi na kuongeza kuwa, dira ya Mahakama ya Tanzania ni kutoa haki kwa wakati na mapema kadri iwezekanavyo.

Aidha, Mhe. Lushasi aliongeza kuwa, wadau waliopo kwenye mnyororo wa haki Jinai inabidi kuendana na kasi ya Mahakama kidijitali kwa kuboresha na kuimarisha miundombinu.

Mhe. Lushasi ameongeza kuwa, nguzo ya pili ya Mpango Mkakakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania inasisitiza utoaji haki kwa wakati. Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huo kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hiyo.

Kwa upande wake, Mwakilishi kutokea TANESCO Mhandisi Victor Ng’wigulu alisema, kwa sasa Taasisi zote za umma ikiwemo Mahakama tumeziweka kwenye kipaumbele cha kwanza katika kuhakikisha zinapata nishati ya umeme.

“Tuliwashauri Mahakama ya Tanzania Mkoa wa Katavi wapate kangavuke (Standby Generator) na nitumie nafasi hii kuwashukuru kwa kupata kangavuke zuri na la kisasa tumeliona lipo, hivyo ikitokea changamoto za umeme wa TANESCO naamini shughuli za kimahakama zitaendelea ila tumejipanga vizuri kama TANESCO Mkoa kuendelea kutoa huduma bora kwa Taasisi zote.

Wadau wa Mahakama waliohuduria kwenye kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi ni pamoja na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Takukuru, Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali Sumbawanga, Ofisi ya Magereza Katavi, Chama cha wanasheria Tanganyika (TLS) Katavi, Baraza la Ardhi na Nyumba, Hifadhi ya Taifa Katavi, Afisa Ustawi wa Jamaii Katavi, Mahakimu Wafawidhi, Tanesco, Tume ya Usuluhishi na Upatanishi (CMA) Katavi, Ofisi ya Mganga Mkuu Katavi, Mwanasheria wa Halmashauri za Mpanda, Mlele na Tanganyika.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Silivia S. Lushasi (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama ya Tanzania mkoa wa Katavi mara baada ya kikao cha wadau wa Mahakama.

Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Katavi Bi. Flavia F. Shiyo akichangia hoja wakati wa Kikao cha Wadau wa Mahakama Katavi.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Silivia S. Lushasi (katikati waliokaa mbele) akiongea na Wadau wa Mahakama ya Tanzania mkoa wa Katavi kwenye kikao cha wadau wa Mahakama.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


Alhamisi, 5 Machi 2026

TANZIA

Bi. Lightness Elia Kiula wakati wa uhai wake.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam Kisutu inasikitika kutangaza kifo cha Ofisa Tawala Mwandamizi, Bi. Lightness Elia Kiula, aliyekuwa akihudumu katika Mahakama ya Wilaya Kigamboni.

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Bi. Athanasia Kabuyanja, kifo hicho kimetokea tarehe 04 Machi, 2026 katika Hospitali ya Moyo ya Jakaya (JKCI) iliyopo Upanga Dar es Salaam.

Bwana ametoa, Bwana ametwaa, Jina Lake lihimidiwe. Amen.

MWANANCHI MKOA WA GEITA WAPATIWA ELIMU KUHUSU UTEKELEZAJI WA AMRI ZA MAHAKAMA

Wananchi wa Mkoa wa Geita wamenufaika na mpango wa utoaji elimu kwa Umma ulioratibiwa na Mahakama Kuu Masjala ya Geita.

Utoaji huo wa elimu ulifanyika tarehe 03 Machi, 2026 katika Ukumbi wa Elimu kwa Umma, Kituo Jumuishi (IJC) Geita.

Mada iliyowasilishwa ilikuwa Utekelezaji wa Amri za Mahakama, ikiwa na lengo la kuwajengea wananchi uelewa kuhusu taratibu za kisheria baada ya hukumu kutolewa.

Elimu hiyo ilitolewa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, ambaye alieleza kwa kina hatua zinazofuatwa katika utekelezaji wa amri za Mahakama mara baada ya hukumu kutolewa.

Katika mafunzo hayo, Mhe. Muchunguzi alifafanua kuwa utekelezaji wa amri za Mahakama hufanyika kwa njia mbalimbali, ikiwemo kukamata na kuuza mali za mdaiwa, kuamrisha jambo fulani litendeke ili kumpatia mdai haki yake, au utekelezaji wa kifungo cha madai pale inapobidi. Alieleza kuwa taratibu zote hufuata misingi ya kisheria ili kuhakikisha haki inatendeka kwa pande zote zinazohusika.

Aidha, wananchi walipata fursa ya kuuliza maswali kuhusu migogoro ya ardhi, zuio litolewalo na Mahakama na masuala ya dhamana katika mikopo ya benki.

Akijibu hoja hizo, Mhe. Muchunguzi alisisitiza kuwa endapo mali itauzwa kwa thamani kubwa kuliko deni, kiasi kinachozidi hurudishwa kwa mdaiwa.

Aliongeza kuwa migogoro ya ardhi inapaswa kuanzia Baraza la Ardhi la Kata kwa usuluhishi na baadaye kama hawajaelewana kupeleka mgogoro wa ardhi kwenye Baraza la Ardhi Nyumba na Makazi Wilaya kwa mujibu wa sheria.

Alisema kwamba ni kosa la kukaidi amri ya Mahakama, ambapo anayekiuka zuio halali anaweza kuchukuliwa hatua za kisheria.

Wananchi walieleza kufurahishwa na elimu hiyo, wakisema imewasaidia kuelewa haki na wajibu wao katika masuala ya kisheria. Mahakama imeueleza Umma huo kuwa itaendelea kutoa elimu kama hiyo mara kwa mara ili kuongeza uelewa wa sheria na kuimarisha upatikanaji wa haki kwa jamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akiwahutubia na kuwasalimia wananchi, huku akiwaalika wale wote wenye changamoto au wanaohitaji msaada wa kisheria kujitokeza ili wasikilizwe na kupatiwa msaada stahiki.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilayya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi akiendelea kutoa elimu kwa wananchi Mkoa wa Geita.

Wananchi Mkoa wa Geita wakiendelea kupata mafunzo katika ukumbi wa mafunzo wa Mahakama Kuu Geita.

Hakimu Mfawidhi, Mhe. Mujuni Muchunguzi akiwa katika picha ya pamoja na Wananchi baada ya mafunzo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

FANYENI KAGUZI ZENYE TIJA NA TATHMINI YA UTENDAJI KAZI; JAJI MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amewaagiza Viongozi wa ngazi mbalimbali za Mahakama katika Kanda  hiyo kuhakikisha wanafanya kaguzi zenye tija katika Mahakama zilizo chini yao ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya utendaji kazi katika vituo hivyo lengo likiwa ni kuongeza ufanisi wa kazi za Mahakama.

Mhe. Mahimbali aliyasema hayo katika Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Kanda ya Arusha kilichoketi hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha ambapo aliwaambia wajumbe wa kikao hicho kuwa ni lazima juhudi zao zijikite katika kuibua mikakati bunifu inayolenga kufanikisha malengo ya Mahakama ya kutoa haki kwa wananchi mapema ipasavyo na kwa ubora unaotakiwa.

“Tunapokagua Mahakama zetu, lazima tubainishe mafanikio, changamoto, njia au mbinu za kuondokana na changamoto hizo na kutoa mapendekezo ya namna ya kuboresha utendaji kazi katika mahakama zetu. Ni kwa kufanya kazi namna hiyo ndio tutafikia malengo ya kuondokana na mashauri ya mlundikano yasiyo na sababu za msingi,” alisisitiza Jaji Mahimbali.

Mhe. Mahimbali aliongeza kuwa, kwa kufanya hivyo kutasaidia na kusukuma usikilizaji wa mashauri unaojikita katika kumaliza idadi kubwa ya mashauri kuliko mashauri yanayosajiliwa.

Akiwasilisha Taarifa ya hali ya mashauri katika Kanda ya Arusha, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati aliwaeleza wajumbe kuwa, kasi ya usikilizaji wa mashauri ni nzuri na kwamba wameweza kumaliza kiasi kikubwa cha mashauri ya mlundikano na mikakati madhubuti imewekwa kuhakikisha kasi ya umalizaji mashauri inaongezeka na hivyo kudhibiti kiasi cha mashauri mlundikano mapya.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa na Mhe. Massati, hadi kufikia tarehe 26 Februari, 2026, Mahakama Kuu Arusha ilikuwa imebakiwa na mashauri mlundikano sita tu, na Kanda nzima ya Arusha zikiwemo Mahakama za chini kulikuwa na mashauri mlundikano 15 pekee. 

Aliongeza kuwa, idadi hiyo ya mashauri mlundikano inatarajiwa kupungua kutokana na mikakati iliyowekwa na Kanda ya Arusha kumaliza mashauri kwa wakati.

Naye Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama aliwasilisha taarifa ya utendaji ambayo kwa kiasi kikubwa ilionesha mafanikio makubwa katika kuweka mazingira wezeshi kuwezesha usikilizaji mashauri kufanyika katika mazingira mazuri na rafiki zaidi.

Bi. Kapama alibainisha baadhi ya mafanikio hayo kuwa ni pamoja na ukarabati wa Mahakama za Mwanzo Likamba na Nkoanrua zilizopo wilayani Arumeru zilizokuwa zimefungwa kwa kipindi kirefu na hatimaye kufanikiwa kuzifufua na mpaka sasa zinafanya kazi.

Aidha, katika kikao hicho Wajumbe wamesisitizwa kuwa wabunifu zaidi katika usimamizi wa vituo vyao vya kazi na kuhakikisha huduma za Mahakama kwa wananchi zinakuwa bora zaidi na kutolewa mapema ipasavyo.

Kikao hicho cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilihudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka Mahakama Kanda ya Arusha ikiwemo wajumbe wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya Arumeru, Longido, Karatu, Monduli na Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akiongoza Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati (aliyesimama) akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha. Walioketi kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Dkt. Kassian Mshomba na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mhe. Erasto Philly.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama akiwasilisha Taarifa ya Utendaji wakati wa Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha kilichoketi hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Wajumbe mbalimbali waliohudhuria Kikao cha Menejimenti Kanda ya Arusha wakifuatilia kinachojiri katika kikao hicho.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)