Jumatano, 19 Agosti 2026

AMANI NA USALAMA NDIO MSINGI WA UWEKEZAJI: JAJI MRISHA

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe, Mhe. Abubakar Mrisha amesema amani na usalama ndio msingi mkuu wa kuvutia uwekezaji nchini na kusisitiza kuwa, utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 haiwezi kufanikiwa bila mambo hayo mawili kuwepo.

Mhe. Mrisha ameyasema hayo leo tarehe 19 Agosti, 2026 kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Gabriel Malata wakati akitoa salamu za Mahakama katika Jukwaa la Dira 2050 na Uwekezaji lililofanyika mkoani Songwe.

“Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa upande wa Mahakama ndio msingi mkuu katika kutekeleza yote yanayotakiwa kutekelezwa kutokana na Dira kwanini nalisema hili, ni kwa sababu ili Dira iweze kutekelezwa lazima kuwepo na amani, kuwepo na usalama na haya yote ndiyo yatakayokuwa ni kivutio cha wawekezaji na wafanyabiashara katika nchi yetu,” amesema Mhe. Mrisha.

Mhe. Mrisha ameeleza kuwa, jukumu kubwa la Mahakama ni kutafsiri sheria zinazotungwa na Bunge pamoja na sheria ndogo (by-laws) zinazotungwa na Madiwani pale msuguano unapotokea, ili kuhakikisha sheria hizo zinaleta amani na usalama kwa jamii.

Akitoa mfano wa usogezwaji wa huduma karibu na wananchi, Jaji Mrisha amebainisha kuwa kuanzishwa kwa Mahakama Kuu ndani ya Mkoa wa Songwe kumesaidia kupunguza kero na gharama za wananchi waliokuwa wakisafiri umbali mrefu kwenda Mbeya ili kupata huduma za rufaa, hatua ambayo imesaidia kuongeza muda wa kusikiliza mashauri na kuharakisha utoaji haki.

Amebainisha kwamba, haki ikichelewa inahesabika kuwa imekosekana, ndio maana Mahakama inaendelea na ujenzi wa Mahakama za Mwanzo na za Wilaya zikiwa zimeunganishwa na mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) itakayowezesha kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao, pamoja na matumizi ya Mahakama Inayotembea (Mobile Courts) ili kwenda na kasi ya utekelezaji wa Dira hiyo.

“Lakini kwa maendeleo ya TEHAMA Mahakama ina lengo la kufanya maendeleo na kuweka mfumo ambao kesi zitasikilizwa kwa njia ya mtandao, kwa hiyo utaona ni kwa kiasi gani tutakuwa tumepunguza gharama,” ameongeza Mhe. Mrisha.

Aidha, amewasihi wananchi na wadau mkoani Songwe kutumia fursa ya elimu na wataalam walioshiriki kwenye jukwaa hilo ili kuelewa fursa zilizopo na kuzitumia kuwekeza katika rasilimali za Mkoa huo kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Jukwaa la Dira 2050 na Uwekezaji limehudhuriwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo kama Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mkuu wa Wilaya wa Songwe pamoja na viongozi vingine wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Songwe.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe, Mhe. Abubakar Mrisha akitoa salamu za Mahakama kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Gabriel Malata katika Jukwaa la Dira 2050 na Uwekezaji lililofanyika leo tarehe 19 Agosti, 2026 mkoani Songwe. 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

JAJI MFAWIDHI MAHAKAMA YA KAZI ATEMBELEA TUME YA USULUHISHI NA UAMUZI

Na MWANDISHI WETU-Mahakama ya Kazi, Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, jana tarehe 18 Agosti, 2026 alitembelea Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Lengo la ziara hiyo ni kujionea utendaji, kufahamu kwa undani namna inavyotekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama ya Kazi na Tume katika kuhakikisha migogoro ya kikazi inatatuliwa kwa ufanisi na kwa wakati.

Ziara hiyo imekuwa ya kwanza kwa Mhe. Dkt. Kilekamajenga  katika Tume hiyo tangu alipoteuliwa kuwa Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuendelea kujenga uelewa na ushirikiano wa kiutendaji kati ya Taasisi zinazohusika katika mnyororo wa utoaji wa haki kazi nchini.

Jaji Mfawidhi alipokelewa na uongozi wa Tume na kupata fursa ya kutembelea baadhi ya ofisi, ambapo alijionea mazingira ya kazi na namna watumishi wanavyotekeleza majukumu yao ya kila siku.

Uongozi wa Tume ulimweleza Jaji Mfawidhi na wajumbe aliokuwa ameambatana nao kuhusu majukumu mbalimbali ya CMA, muundo wa utendaji kazi pamoja na nafasi ya Tume katika utatuzi wa migogoro ya kikazi nchini.

Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ni Taasisi huru ya utatuzi wa migogoro ya kikazi iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Taasisi za Kazi. Miongoni mwa majukumu yake ni kufanya usuluhishi wa migogoro ya kikazi inayowasilishwa mbele yake na, kwa mujibu wa sheria, kuamua migogoro kupitia mchakato wa uamuzi.

Akizungumza katika kikao cha pamoja, Mkurugenzi Mkuu wa CMA, Mhe. Usekelege Mpulla, alimweleza Jaji Mfawidhi kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri ya Usuluhishi na Uamuzi unaojulikana kama e-Utatuzi.

Mfumo huo ulianza kutumika rasmi Januari 21, 2026, ukiwa na lengo la kuboresha usimamizi na uendeshaji wa mashauri ya migogoro ya kikazi kwa kutumia teknolojia ya kidijitali.

Mfumo huo unamwezesha mdau kusajili na kufuatilia shauri lake kwa njia ya mtandao, bila kulazimika kufika ofisi za Tume kwa kila hatua.

Mpaka sasa, zaidi ya mashauri 1,678 yamewasilishwa kwa njia ya mfumo  ambapo mashauri 622 yameisha kwa njia ya usuluhishi na mashauri 277 yameisha kwa njia ya uamuzi.

Hata hivyo, Kiongozi huyo alieleza kwamba jitihada za kufanya mfumo huo usomane na mfumo wa usimamizi wa mashauri unaotumiwa na Mahakama ya Tanzania.

Akielezea umuhimu wa mfumo huo, Mkurugenzi wa CMA alisema matumizi ya e-Utatuzi yanalenga kuongeza ufanisi katika utendaji wa Tume, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kupunguza gharama ambazo wadaawa wanaweza kuzitumia katika kufuatilia mashauri yao.

Mfumo huo umesaidia kupunguza utegemezi wa majalada ya nakala ngumu, kuimarisha usimamizi wa nyaraka za mashauri na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika hatua mbalimbali za mchakato wa utatuzi wa migogoro.

Aidha, matumizi ya mfumo huo yanaongeza uwezekano wa huduma za utatuzi wa migogoro kufikiwa kwa urahisi zaidi na wananchi walioko maeneo mbalimbali nchini.

Mhusika anaweza kusajili na kufuatilia mwenendo wa shauri lake akiwa mahali alipo, kwa kutumia kifaa chenye mtandao, jambo linalosaidia kupunguza ulazima wa kusafiri mara kwa mara kwenda katika ofisi za Tume.

Kwa upande wake, Mhe. Dkt. Kilekamajenga aliipongeza Tume kwa namna inavyotekeleza majukumu yake katika kusaidia kutatua migogoro ya kikazi na kwa hatua zinazochukuliwa katika kuboresha huduma kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi alieleza kuwa ziara hiyo imempa fursa ya kupata uelewa mpana zaidi kuhusu utendaji wa CMA, changamoto zinazokabili Tume pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kuboresha huduma za usuluhishi na uamuzi.

Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama ya Kazi na CMA, akieleza kuwa Taasisi hizo zina nafasi muhimu katika mfumo wa utoaji wa haki za kazi nchini.

Jaji Mfawidhi aliwataka viongozi na watumishi wa Taasisi hizo kuendelea kushirikiana katika kubaini maeneo yanayohitaji maboresho, kubadilishana uzoefu na kutafuta njia bora za kuongeza ufanisi katika utatuzi wa migogoro ya kikazi.

Aidha, aliwasihi viongozi wa CMA kuendelea kufanya jitihada ili kuhakikisha mifumo hiyo inasomana na kurahisisha uendeshaji wa mashauri katika utoaji haki kazi.

Ziara hiyo imeonesha umuhimu wa mawasiliano na ushirikiano wa mara kwa mara kati ya Taasisi zinazohusika katika utoaji wa haki za kazi. Kwa kuwa CMA na Mahakama ya Kazi zina majukumu yanayogusana katika mnyororo wa utatuzi wa migogoro ya kikazi, ushirikiano wao unaweza kusaidia kubaini changamoto za kiutendaji na kutafuta suluhisho kwa pamoja.










BEIJING HIGH PEOPLE’S COURT SENIOR OFFICIALS VISIT JUDICIARY OF TANZANIA

  • Exchange knowledge, experience on labour dispute resolutions

By JUDICIARY REPORTER-Dodoma

Senior Officials from Beijing High People’s Court are in Tanzania for knowledge and experience sharing visit to the Judiciary of Tanzania and getting incites on issues relating to determination of labour disputes.

They are led by Standing Member of the Adjudication Committee of Beijing High People’s Court, Hon. Shan Guojun. The other officer in the delegation is Judge of the First Civil of Beijing High People’s Court, Hon. Wang Fei.

The rest are Deputy Chief Judge of the Sixth Civil Division of Beijing First Intermediate People’s Court, Hon. Wu Bowen and Deputy Chief Judge of the First Civil Division of Changping Primary People’s Court, Beinjing, Hon. Li Guodong.

They arrived at the Judiciary Square, the Headquarters of the Judiciary of Tanzania in Dodoma, at around 9.00am and were received by Acting Registrar of the High Court of Tanzania, Hon. Mary Moyo and other Deputy Registrars.

Presented at the warm welcome of officials of the Judiciary of China are Deputy Registrars Enock Matembele, Mary Mrio, Franco Kiswaga and Mwajabu Mvungi. After exchanging greetings, the guests were escorted to a conference room for other engagements.

In her welcoming note, Hon. Moyo, who is also Deputy Registrar of the High Court of Tanzania, Dodoma Main Registry, told the delegation that the visit provides a valuable platform for mutual learning on labour justice, judicial practice and institutional development.

“As reflected in the programme, our discussions will focus on the organizational structure and operational mechanisms of labour dispute adjudication, the role of courts in labour justice, the coordination between judicial and non-judicial dispute resolution bodies, and recent trends in judicial reform,” she said.

Hon. Moyo explained that the Judiciary of Tanzania attaches great importance to labour justice because labour disputes touch directly on human dignity, fairness in the workplace, economic stability and social harmony.

Therefore, she said, the Labour Division of the High Court plays a significant role not only in deciding disputes, but also in ensuring consistency in legal interpretation, fairness in adjudication, and confidence in the justice system as a whole.

“We believe that today’s engagement will strengthen professional understanding between our institutions and give us an opportunity to reflect on shared challenges, comparative experiences, and possible reforms in the administration of labour justice. It is our sincere hope that the exchanges scheduled for this visit will be fruitful, practical, and intellectually enriching to all of us,” Hon. Moyo said.

It was Hon. Matembele, who took on board the distinguished guests from the People’s Republic of China on the first presentation concerning “Experience sharing on organizational structure and operational mechanism of judicial governance system for labor disputes.

They were taken through on “Functional position of courts in labor dispute adjudication; coordination and linkage mechanisms among the judiciary courts, labor administrative department and mediation arbitration bodies and development trends in the judicial reform system.”

The presentation centered on organizational structure of judicial governance system for labour disputes and operational mechanism of judicial governance system for labour disputes.

It also covered functional position of courts in labour dispute adjudication; coordination and linkage mechanism among the judiciary, courts, labour; administrative departments and mediation and arbitration bodies and developments and trends in judicial reforms.

The second presentation related to judicial practice and the application of labour law in Tanzania: the role of the Labour Division of the High Court in governance, consistency, and reform of labour dispute adjudication.

Hon. Mrio presented the third presentation relating to the the Court of Appeal of Tanzania and the unification of legal application; Tanzania’s experience on appellate mechanisms, precedent, resolution of judicial disagreement, practical outcomes and challenges.

After the presentations, the officials discussed different issues and shared experiences on determination of labour disputes.

The delegations is scehduled tomorrow to visit the High Court Labour Division and later at the Kisutu Resident Magistrate's Court in Dar es Salaam to contune with the visit.

Deputy Registrars of the High Court of Tanzania in group picture with Senior Officials from Beijing High People’s Court few moments after arriving at the Headquarters of the Judiciary of Tanzania in Dodoma.


Acting Registrar of the High Court of Tanzania, Hon. Mary Moyo, who is also Deputy Registrar of the High Court, Main Registry, giving welcoming remarks to the guests.

Member of the Adjudication Committee of Beijing High People’s Court, Shan Guojun who is head of the delegation, giving introduction remarks on the purposes of the visit.

Senior Officials from Beijing High People’s Court following presentations during the session.


Deputy Registrars of the High Court of Tanzania during the session.


Deputy Registrar in Charge of the High Court Labour Division, Hon. Enock Matembele, stessing a point when making a presentation.




JOPO LA MAJAJI WA RUFANI LAFANYA TATHMINI YA UENDESHAJI MASHAURI MASJALA MBEYA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Rufani ya Tanzania hivi karibuni imefanya kikao cha tathmini ya utekelezaji wa shughuli za usikilizaji wa mashauri ya rufaa za madai na jinai katika Masjala Ndogo ya Mbeya, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhitimisha rasmi kikao cha Mahakama hiyo kilichoanza tarehe 3 Agosti, 2026 na kinachotarajiwa kumalizika tarehe 28 Agosti, 2026.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufaa ya Tanzania, Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani walioambatana naye katika kikao hicho ambao ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Dkt. Benhajj Shaban Masoud na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa kikao hicho, Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo alisema kuwa, kati ya mashauri 38 yaliyopangwa kusikilizwa, mashauri 33 sawa na asilimia 87% yameshasikilizwa na kupatiwa maamuzi.

Aidha, alieleza kuwa, mashauri 05 ya rufaa za madai yameahirishwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kuwapa warufani nafasi ya kuwafikishia wajibu rufaniwa hati za mashauri, kumpa nafasi mrufani kumteua wakili mwingine na kutoa nafasi ya kupatikana kwa mwakilishi wa kisheria wa mjibu rufani aliyefariki, hali iliyolazimu wahusika kuongezewa muda wa kufanya mabadiliko hayo.

Katika tathmini hiyo, ilibainika kuwa kumekuwa na changamoto kadhaa ikiwemo wadaawa kutokuleta taarifa za kuondoa mashauri mapema jambo ambalo lingesaidia kupanga mashauri mengine, kutokufuata taratibu za uendeshaji wa mwenendo kabidhi (committal proceedings), washtakiwa wengi wanaotajana kuwakilishwa na wakili mmoja, na kutokuzingatia kanuni inayotaka mdaawa akifariki ateuliwe msimamizi wa mirathi ndani ya miezi 12 kwa mujibu wa kanuni ya 105(2) ya kanuni za mahakama ya Rufani.

Aidha, pamoja na changamoto hizo, kikao kilieleza kuridhishwa na mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo kusikilizwa kwa mashauri 33 kati ya 38 yaliyopangwa pamoja na ushirikiano mzuri uliooneshwa na Warufani kwenye rufaa za madai, Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea waliohudhuria kwenye vikao hivyo kwa wakati.

Mafanikio hayo yameendelea kuimarisha juhudi za Mahakama ya Rufani ya Tanzania za kuongeza ufanisi katika usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema ipasavyo.

Viongozi wengine walishiriki kikao hicho ni kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya ambao ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo.

Wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Mahakimu mbalimbali wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya wilaya Mbeya Mhe. Teddy Mlimba, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Alintula Ngalile na wadau wengine wa haki Madai na Jinai Mawakili na wadau wengine wa Haki Jinai na madai kutoka Mbeya, Songwe na Tabora.

Mwenyekiti wa Jopo la Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika, (katikati) akiongoza kikao cha kufanya tathmini ya uendeshaji wa mashauri ya Madai na Jinai Masjala Ndogo Mbeya, kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina na kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Benhajj Shaban Masoud.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliohudhuria kikao cha tathmini (kulia) ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa pili kushoto) na Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer (kushoto)

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernad Mpepo akiwasilisha taarifa ya Naibu Msajili ya tathmini kuhusu uendeshaji wa mashauri ya rufaa Masjala Ndogo Mbeya katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho.

Mwakilishi kutoka Gereza Kuu Ruanda Mbeya akitoa neno la shukurani kwa Jopo la Majaji wa Rufani katika kikao hicho.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)








WATUMISHI MASJALA NDOGO TABORA WAFANYA ZIARA YA KIKAZI MANYARA

Na CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara iliwaalika watumishi kutoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora kwa ajili ya mafunzo na kubadilishana uzoefu wa majukumu. Ziara hiyo imefanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 17 na 18 Agosti, 2026 ili kuwapa watumishi hao fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ya kimahakama.

Aidha, watumishi hao waliofika kutoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda

Akizungumza wakati wa ziara hiyo ya kikazi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi aliwapongeza watumishi hao wa Tabora kwa kuichagua Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya mafunzo hayo na kuwaeleza kuwa Manyara ni mahali sahihi pa kujifunza.

“Tunawakaribisha Manyara, hapa ni mahala sahihi kwenu pa kujifunza. Tumekuwa tukiwawezesha hata wanafunzi wa vyuo mbalimbali kupata mafunzo yao kwa ajili ya kutimiza vigezo na matakwa yao ya kielimu hivyo nanyi tunawakaribisha ili mjifunze na sisi pia tujifunze kutoka kwenu,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara kwa mapokezi mazuri ikiwa ni pamoja na kuwapa nafasi ya kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu majukumu ya kila siku ya mahakamani.

“Tumesikia mambo mazuri ambayo Wanamanyara mnayafanya hivyo nasi tukaona ni vema tufike tujifunze kutoka kwenu pamoja na kushiriki uzoefu wa Masjala zetu ili tuboreshe utendaji kazi wetu wa kila siku”, alisema Mhe. Ngimilanga.

Pamoja na kushiriki namna wanavyotekeleza majukumu yao ya kila siku, viongozi hao wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora waliweza kujifunza namna ya uandaaji bora wa taarifa mbali mbali za kimashauri pamoja na zile za Kiutawala ambazo huwa zinapaswa kuwasilishwa katika vikao mbalimbali. Katika hatua hiyo, viongozi hao waliweza kushiriki Kikao cha pamoja na viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara ambacho hufanyika kila wiki kwa ajili ya kupeana taarifa na maelekezo mbalimbali ya kikazi.

Akitoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda aliwapongeza watumishi wa Manyara pamoja na viongozi wao kwa kufanya kazi kwa bidii na kwa weledi hali ambayo inawezesha mashauri yao kwenda kwa haraka jambo ambalo linapunguza mlundikano wa mashauri.

“Kwa kweli tumeona jitihada zenu Wanamanyara katika usikilizwaji wa mashauri ya kila siku lakini pia katika usimamizi wa rasilimali zenu, tunaahidi kutumia elimu hii tuliyoipata katika kuboresha utendaji kazi wetu tutakaporejea Tabora.

Pamoja na kupata elimu na kubadilishana uzoefu juu ya utendaji kazi, Viongozi wa Mahakama hizo waliweka mikakati ya kuwa Masjala rafiki hata katika masuala ya kijamii na viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora waliweka ahadi ya kuwakaribisha watumishi wa Manyara kwenda Tabora kwa ajili ya kujifunza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyekaa mbele), pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu wakiwa katika mazungumzo ndani ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara pamoja na wageni waliotoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora kwa ajili ya mafunzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama wa nne kutoka upande wa kulia) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara pamoja na wageni wao waliotoka Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Tabora.

Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Manyara, Bw. Christopher Msagati akiwasilisha mada katika mafunzo waliyokuwa wanapatiwa viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda (kushoto), pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yakitolewa katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe Bw. Emmanuel Munda (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao cha kutoa taarifa kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora. Aidha, katika Runinga wanaoonekana ni washiriki wa kutoka Mahakama za Wilaya na za Mwanzo zilizopo katika Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara wakishiriki kwa njia ya video.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao cha kutoa taarifa kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (kulia) akifuatilia taarifa mbalimbali zilizokuwa zinatolewa katika Kikao kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora na (kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Kansha)





Jumanne, 18 Agosti 2026

MTENDAJI MKUU ATEMBELEA DIVISHENI YA MAKOSA YA RUSHWA NA UHUJUMU UCHUMI

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu leo tarehe 18 Agosti, 2026 amefanya ziara ya kikazi Mahakama Kuu ya Tanzania - Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi Mikocheni B jijini Dar es Salaam.

Dkt. Jingu ametembelea Mahakama hiyo kwa lengo la kuzungumza na watumishi pamoja na kujua hoja na changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Aidha, Mtendaji Mkuu amewasikiliza Watumishi hao na kujibu baadhi ya hoja zilizotolewa na nyingine ameahidi kuzishughulikia.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi alipotembelea Mahakama hiyo leo tarehe 18 Agosti, 2026 Mikocheni B jijini Dar es Salaam. Aliyeketi kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Divisheni Maalum, Bi. Mary Shirima na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Magdalena Ntandu.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Sharmillah Sarwatt (kushoto) na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Dkt. Dafina Ndumbaro.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Sharmillah Sarwatt (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Dkt. Dafina Ndumbaro (wa pili kulia), Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Divisheni Maalum, Bi. Mary Shirima (wa kwanza kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Mhe. Magdalena Ntandu.


























TMJA MTWARA WAVUKA BAHARI KUTALII URITHI WA DUNIA VISIWANI KILWA

Na SOJO MWAKOBA – Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Mtwara, hivi karibuni aliwaongoza wanachama wao katika ziara ya siku mbili ya utalii iliyofanyika katika Visiwa vya Kilwa Masoko.

Katika ziara hiyo ya siku mbili ambayo Mhe. Mteule aliongozana na Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Mtwara, Mhe. Aisha Ndossy, wanachama walitembelea magofu ya mali kale yaliyopo Kilwa Kisiwani, ikiwemo Msikiti Mkuu wa Malindi na makaburi ya kale (Malindi Gravestones), kabla ya kufanya utalii wa majini na kuvuka hadi Kisiwa cha Songo Mnara ambako walitembelea magofu ya Ikulu ya Kale ya Masultani (Sultan’s Palace Ruins).

Lengo la ziara hiyo lilikuwa ni utalii, elimu pamoja na kuchangamsha na kuburudisha akili na mwili baada ya majukumu ya kazi. Wanachama walitembelea na kujionea mabaki ya mali kale zilizopo visiwani humo, kujua historia ya urithi huo, huku pia wakipata elimu ya uendeshaji wa mashauri yanayohusu uhifadhi wa wanyamapori kutoka kwa mwanasheria wa  Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA).

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliwapongeza wanachama kwa ushirikiano wao na moyo wa kupenda kujumuika pamoja katika matukio muhimu kama hayo, huku akisisitiza umuhimu wa kushirikiana na kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza ipasavyo kauli mbiu ya Mahakama ya “Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji.”

“Niwapongeze wanachama kwa umoja na ushirikiano wenu wa kupenda kujumuika katika shughuli kama hizi. Tuendelee kushirikiana na kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza ipasavyo kauli mbiu ya Mahakama yetu,” alisema Mhe. Mteule.

Miongoni mwa waliohudhuria ziara hiyo ni Mahakimu, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, wakiwa ni sehemu ya wanachama wa TMJA Tawi la Mtwara, pamoja na Mtendaji wa Mahakama Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga.

Ziara hiyo imeongeza mshikamano miongoni mwa wanachama huku ikiwapa fursa ya kujifunza historia na urithi wa mali kale za Kilwa, historia ya urithi huo,  pamoja na umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na wanyamapori.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (wapili kulia) akiwasili Kilwa Kisiwani kutembelea magofu ya Malindi.

Mwanasheria kutoka TAW A(kulia) akiwakaribisha wanachama wa TMJA Mtwara kabla ya kuanza kutembelea magofu ya Kilwa Kisiwani.

Wanachama wa TMJA Mtwara wakipata elimu ya historia ya urithi wa Dunia ulioachwa hapo Kilwa Kisiwani.

Mahakimu wakitembelea moja ya majumba la kale yaliyopo Kilwa Kisiwani.

Wanachama wa TMJA Mtwara wakiwa kwenye picha ya pamoja kama kumbukumbu ya ziara yao ya utalii visiwani Kilwa.

Wanachama wa TMJA Mtwara wakiwa kwenye boti katika utalii wa majini baada ya kutembelea magofu ya Kilwa Kisiwani.

Mahakimu wakisoma mchoro wa ramani mara baada ya kufika Kisiwa cha Songo Mnara ikiwa ni siku ya pili ya ziara yao.

Picha ya pamoja ya wanachama wa TMJA Tawi la Mtwara mbele ya Magofu yanayopatikana Songo Mnara (Kilwa).

Wanachama wa TMJA Mtwara wakifurahia mandhari tulivu na upepo wakiwa kwenye kibanda cha kitamaduni.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAOFISA MAGEREZA SINGIDA WANOLEWA KUHUSU MIFUMO YA KIELEKTRONI YA MAHAKAMA

EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama – Singida

Maofisa Magereza wanaohusika na Mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mkoani Singida wamepatiwa mafunzo ya Mifumbo mbalimbali ya Kielektroni ya Mahakama lengo likiwa ni kuwajengea uelewa Maofisa hao juu ya mifumo mbalimbali ya kimahakama ikiwemo Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-Case Management System), Mahakama Mtandao (Virtual Court) na Mfumo wa Taarifa za Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania (TanzLII).

Akifungua mafunzo hayo jana tarehe 17 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Singida, Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Jasmin Abdul aliwasisitiza washiriki kuongeza ufanisi katika kutoa huduma na kuwa wabunifu ili kutoa Haki kwa wakati.Aidha mafunzo haya yalihusisha maafisa kutoka Ofisi ya Mkuu wa Magereza Mkoa wa Singida,Maafisa kutoka Magereza ya Wilaya Singida, Iramba,Ushora na Manyoni.

“Watumishi wenzangu napenda kuwajulisha kuwa Mahakama ya Tanzania kwa sasa inatumia mifumo ya TEHAMA katika kuendesha shughuli zake za kila siku hususan za utoaji haki na Magereza ni miongoni mwa Wadau muhimu wa Mahakama, ni matarajio yangu kuwa katika mafunzo haya mtajifunza kwa vitendo, mtabadilishana uzoefu na mwisho kubaini changamoto na kuzitafutia suluhu hivyo muwe wazi na tayari kujifunza,” alisema Naibu Msajili huyo.

Aidha, aliwasisitiza kufanya kazi kwa ushirikiano wanapopata changamoto za kimfumo kuziwasilisha kwa haraka na kwamba mafunzo hayo yatakuwa endelevu kwa kadri mabadiliko kimifumo yanayotokea.

Mada za mafunzo hayo ya TEHAMA ziliwasilishwa na Ofisa TEHAMA Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Bi.Valentina Nkullanga ambapo katika uwasilishaji wake aliwaeleza Maofisa Magereza kuwa matumizi ya mifumo hiyo katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama umeleta manufaa makubwa kwa Mahakama na Wadau kwani imeongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri, imepunguza matumizi ya karatasi.

Manufaa mengine ni kupunguza ucheleweshwaji wa mashauri, kuimarika kwa usalama, kupunguza gharama za usafirishwaji wa Mahabusu na kuongezeka kwa upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Katika mafunzo, walijifunza pia kwa vitendo hatua zote kuanzia shauri linavyosajiliwa hadi kukatiwa rufaa na waliona maandalizi ya awali katika kuandaa mashauri yanayosikilizwa kwa njia ya mtandao namna ya kuandaa vitendea kazi, kuviunganisha na mtandao.

Kadhalika, walielekezwa namna ya kuingia katika mfumo wa TanzLII kwa ajili ya kupata nakala za hukumu za wafungwa wao na kupata rejea mbalimbali kwa ajili ya kujifunza.

Akihitimisha mafunzo hayo Naibu Msajili wa Mahakama, Mhe. Allu Nzowa aliwasisitiza washiriki kufanya kazi kama timu na kuyachukulia mabadiliko hayo katika mtazamo chanya ili kuleta ufanisi zaidi.

  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Jasmin Abdul akizungumza jambo na Washiriki wa Mafunzo ya Mifumo ya Kielektroni ya Mahakama (hawapo katika picha) wakati wa ufunguzi wa Mafunzo kwa Maofisa Magereza tarehe 17 Agosti, 2026.

  Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Bi Valentina Nkullanga (aliyesimama) akitoa mada kwa washiriki wa Mafunzo hao (hawapo katika picha) wakati wa mafunzo na  Maofisa Magereza.

 CPL Yondani Kibuti kutoka Gereza la Wilaya Singida akichangia jambo wakati wa mafunzo hayo.

  Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Washiriki wa Mafunzo kutoka Gereza la Wilaya Manyoni. Aliyeketi kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti Kamati ya Elimu Kanda, Mhe. Aloyce Masua na kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.

 Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Washiriki kutoka Gereza la Wilaya Iramba. Aliyeketi kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti Kamati ya Elimu Kanda, Mhe. Aloyce Masua na kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.

  Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki kutoka Gereza la Wilaya Singida. Aliyeketi kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti Kamati ya Elimu Kanda, Mhe. Aloyce Masua na kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)