Jumanne, 18 Agosti 2026

MAOFISA MAGEREZA SINGIDA WANOLEWA KUHUSU MIFUMO YA KIELEKTRONI YA MAHAKAMA

EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama – Singida

Maofisa Magereza wanaohusika na Mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mkoani Singida wamepatiwa mafunzo ya Mifumbo mbalimbali ya Kielektroni ya Mahakama lengo likiwa ni kuwajengea uelewa Maofisa hao juu ya mifumo mbalimbali ya kimahakama ikiwemo Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-Case Management System), Mahakama Mtandao (Virtual Court) na Mfumo wa Taarifa za Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania (TanzLII).

Akifungua mafunzo hayo jana tarehe 17 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Singida, Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Jasmin Abdul aliwasisitiza washiriki kuongeza ufanisi katika kutoa huduma na kuwa wabunifu ili kutoa Haki kwa wakati.Aidha mafunzo haya yalihusisha maafisa kutoka Ofisi ya Mkuu wa Magereza Mkoa wa Singida,Maafisa kutoka Magereza ya Wilaya Singida, Iramba,Ushora na Manyoni.

“Watumishi wenzangu napenda kuwajulisha kuwa Mahakama ya Tanzania kwa sasa inatumia mifumo ya TEHAMA katika kuendesha shughuli zake za kila siku hususan za utoaji haki na Magereza ni miongoni mwa Wadau muhimu wa Mahakama, ni matarajio yangu kuwa katika mafunzo haya mtajifunza kwa vitendo, mtabadilishana uzoefu na mwisho kubaini changamoto na kuzitafutia suluhu hivyo muwe wazi na tayari kujifunza,” alisema Naibu Msajili huyo.

Aidha, aliwasisitiza kufanya kazi kwa ushirikiano wanapopata changamoto za kimfumo kuziwasilisha kwa haraka na kwamba mafunzo hayo yatakuwa endelevu kwa kadri mabadiliko kimifumo yanayotokea.

Mada za mafunzo hayo ya TEHAMA ziliwasilishwa na Ofisa TEHAMA Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Bi.Valentina Nkullanga ambapo katika uwasilishaji wake aliwaeleza Maofisa Magereza kuwa matumizi ya mifumo hiyo katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama umeleta manufaa makubwa kwa Mahakama na Wadau kwani imeongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri, imepunguza matumizi ya karatasi.

Manufaa mengine ni kupunguza ucheleweshwaji wa mashauri, kuimarika kwa usalama, kupunguza gharama za usafirishwaji wa Mahabusu na kuongezeka kwa upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Katika mafunzo, walijifunza pia kwa vitendo hatua zote kuanzia shauri linavyosajiliwa hadi kukatiwa rufaa na waliona maandalizi ya awali katika kuandaa mashauri yanayosikilizwa kwa njia ya mtandao namna ya kuandaa vitendea kazi, kuviunganisha na mtandao.

Kadhalika, walielekezwa namna ya kuingia katika mfumo wa TanzLII kwa ajili ya kupata nakala za hukumu za wafungwa wao na kupata rejea mbalimbali kwa ajili ya kujifunza.

Akihitimisha mafunzo hayo Naibu Msajili wa Mahakama, Mhe. Allu Nzowa aliwasisitiza washiriki kufanya kazi kama timu na kuyachukulia mabadiliko hayo katika mtazamo chanya ili kuleta ufanisi zaidi.

  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Jasmin Abdul akizungumza jambo na Washiriki wa Mafunzo ya Mifumo ya Kielektroni ya Mahakama (hawapo katika picha) wakati wa ufunguzi wa Mafunzo kwa Maofisa Magereza tarehe 17 Agosti, 2026.

  Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Bi Valentina Nkullanga (aliyesimama) akitoa mada kwa washiriki wa Mafunzo hao (hawapo katika picha) wakati wa mafunzo na  Maofisa Magereza.

 CPL Yondani Kibuti kutoka Gereza la Wilaya Singida akichangia jambo wakati wa mafunzo hayo.

  Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Washiriki wa Mafunzo kutoka Gereza la Wilaya Manyoni. Aliyeketi kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti Kamati ya Elimu Kanda, Mhe. Aloyce Masua na kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.

 Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Washiriki kutoka Gereza la Wilaya Iramba. Aliyeketi kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti Kamati ya Elimu Kanda, Mhe. Aloyce Masua na kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.

  Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe. Allu Nzowa (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki kutoka Gereza la Wilaya Singida. Aliyeketi kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti Kamati ya Elimu Kanda, Mhe. Aloyce Masua na kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

IDARA YA MIPANGO, URATIBU YAENDESHA MAFUNZO KUSHUGHULIKIA VIHATARISHI NYANDA ZA JUU KUSINI

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Idara ya Mipango na Uratibu ya Mahakama ya Tanzania inaendesha Mafunzo kuhusu matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Uratibu wa Vihatarishi kwa watendaji wa Mahakama Kuu pamoja na Maafisa Vihatarishi kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Songwe, Iringa, Njombe, Songea, Sumbawanga na Mbeya.

Mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 17 Agosti, 2026 katika Masjala Ndogo ya Mbeya, yanalengo la kuwajengea uwezo watendaji na Maafisa bajeti wa Mahakama ya Tanzania katika kubaini, kutathmini na kukabiliana na vihatarishi vinavyoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu na malengo ya Mahakama katika suala zima la utoaji wa haki kwa wananchi.

Akifungua mafunzo hayo ya mfumo mpya unaotambulika kama GERMIS (Government Enterprise Risk Management Information System), Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti, Uendelezaji na Ubunifu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bw. Kisingi Salehe Mhando, amesema kuwa, mafunzo yanalenga kuimarisha uelewa na uwezo wa washiriki katika matumizi ya mfumo mpya wa kielektroniki wa kubaini na kuratibu vihatarishi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Mahakama katika kuhakikisha malengo yake yanafikiwa kwa ufanisi.

Bw. Mhando amesema kwamba, mfumo huo utasaidia Mahakama kubaini vihatarishi kwa wakati, kuvifanyia tathmini na kuweka mikakati stahiki ya kukabiliana navyo kabla havijaathiri utekelezaji wa mipango na shughuli za Mahakama.

Aliongeza kuwa mfumo mpya unaleta maboresho katika namna ya kuratibu vihatarishi ikilinganishwa na mfumo wa awali, hususan katika kurahisisha mchakato wa kutambua, kurekodi, kufuatilia na kuchukua hatua dhidi ya vihatarishi vinavyoweza kujitokeza katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali.

Katika siku ya kwanza ya mafunzo, washiriki wamejifunza kuhusu asili ya vihatarishi, matokeo hasi na chanya ya vihatarishi, pamoja na tofauti kati ya kihatarishi (risk) na tatizo (problem). Aidha, wamepata uelewa kuhusu aina na mgawanyo wa vihatarishi pamoja na misingi ya namna ya kukabiliana navyo kupitia dhana ya Usimamizi wa Vihatarishi (Risk Management).

Akifafanua zaidi kuhusu tofauti kati ya kihatarishi na tatizo, Bw. Mhando amesisitiza umuhimu wa kuchukua hatua mapema ili kuzuia kihatarishi kisifikie hatua ya kuwa tatizo linalohitaji rasilimali kubwa zaidi katika kulitatua.

“Rasilimali zinazotumika kutatua kihatarishi ni chache na gharama ndogo ukilinganisha na rasilimali na gharama zinazotumika kutatua tatizo. Hivyo, tuweke nguvu kubwa katika kuthibiti vihatarishi kabla haijafikia hatua ya kuwa tatizo,” alisema Bw. Mhando

Kwa upande wake, Mtakwimu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu ya Mahakama ya Tanzania Bw. Mussa Wigute, ameongeza kwa kusema kuwa, usimamizi wa vihatarishi haukusudii kuondoa vihatarishi vyote, bali ni kuweka mikakati inayowezesha taasisi kuendelea kufikia malengo yake licha ya uwepo wa vihatarishi.

Mafunzo hayo yanaendeshwa na timu ya wakufunzi kutoka Idara ya Mipango na Uratibu ya Mahakama ya Tanzania, inayoongozwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti, Uendelezaji na Ubunifu Bw. Kisingi Salehe Mhando, akisaidiwa na Mtakwimu, Bw. Mussa Wigute, pamoja na Mchumi Bi. Reine Kissae.

Mafunzo hayo yatawasaidia washiriki kupata ujuzi na maarifa ili kwenda kuwa mabalozi kwa watumishi wengine wanaoshughulikia vihatarishi kuhusu matumizi ya mfumo huo mpya wa kielektroniki na namna utakavyotumika katika kuimarisha usimamizi wa vihatarishi, utekelezaji wa mipango na matumizi bora ya rasilimali za Mahakama.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa (wa kwanza kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songea Bw. Allan Mwela (Katikati), na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Bw. Richard Mbambe (wa kwanza kulia) wakiwa katika mafunzo hayo.

Afisa Utumishi kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Sarah Rossi akichangia jambo kama sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe, Bw. Sostenes Mayoka (kushoto) wakifuatilia kwa karibu mafunzo hayo.

Sehemu ya watendaji wa Mahakama ambao ni washiriki katika mafunzo hayo.

Mchumi kutoka Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bi. Reine Kissae. (aliyesimama) akitoa elimu juu ya mfumo mpya wa GERMIS unavyofanya kazi.

Mtakwimu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bw. Mussa Wigute akitoa ufafanuzi juu ya kukabiliana na vihatarishi katika mafunzo hayo.

Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti, Uendelezaji na Ubunifu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bw. Kisingi Salehe Mhando akiendesha mafunzo hayo kwa washiriki (hawapo pichani)

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

UIMARA WA MAHAKAMA NI MSINGI WA USTAWI WA NCHI; DKT. JINGU

Na AMINA SAID - Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, amewataka watumishi wa Mahakama Kuu-Divisheni ya Biashara kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na weledi huku akisisitiza umuhimu wa kila mtumishi kutambua nafasi yake katika kuimarisha utendaji kazi na kufanikisha malengo ya Taasisi.

Dkt. Jingu aliyasema hayo tarehe 17 Agosti, 2026 wakati wa ziara yake katika Divisheni hiyo, iliyolenga zaidi kuimarisha mahusiano, kufahamiana na kujenga mawasiliano ya karibu kati ya uongozi na watumishi, pamoja na kupata fursa ya kusikiliza maoni na hoja mbalimbali zinazohusu utekelezaji wa majukumu na mazingira ya kazi.

Akizungumza na watumishi hao, Dkt. Jingu amesisitiza kuwa, Mahakama ni Mhimili wa kutenda haki na kwamba uimara wake una umuhimu mkubwa kwa ustawi wa nchi.

“Mahakama ni Mhimili wa kutenda haki, ukikaa vizuri, Nchi inakaa vizuri; ikiyumba, Nchi inayumba. Kwa hiyo tuna jukumu la kuilinda Mahakama yetu,” alisema Mtendaji Mkuu.

Kadhalika, amesema jukumu la kuilinda Mahakama linaanzia kwa kila mtumishi kutekeleza wajibu wake kwa uadilifu, weledi na kujituma, akieleza kuwa utendaji mzuri wa watumishi ni sehemu muhimu ya kuimarisha Taasisi na kujenga hoja zenye msingi kuhusu maboresho na maslahi mbalimbali ya watumishi.

Dkt. Jingu pia amewataka watumishi kuwa wabunifu katika nafasi zao za kazi kwa kutumia rasilimali zilizopo na kutafuta njia bora za kutekeleza majukumu yao.

Amesisitiza kuwa, ubunifu hauhitaji rasilimali nyingi kila wakati, bali unahitaji utayari wa kutumia fursa zilizopo na kuboresha namna ya kufanya kazi.

Aidha, Mtendaji amewataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano na kujenga utamaduni wa kusaidiana, kuthaminiana na kuheshimiana, huku akisisitiza kuwa kila mtumishi ana mchango katika kufanikisha majukumu ya Mahakama.

Katika ziara hiyo, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Bw. Anathory Kagaruki aliwasilisha taarifa ya kiutawala kuhusu hali ya Divisheni hiyo.

Taarifa hiyo ilihusu maeneo mbalimbali ya uendeshaji, ikiwemo hali ya watumishi, hali ya kifedha, vyombo vya usafiri na maslahi ya watumishi pamoja na masuala mengine yanayohusu utekelezaji wa majukumu ya Mahakama hiyo.

Baada ya taarifa hiyo, watumishi walipata fursa ya kuwasilisha hoja, maoni na changamoto mbalimbali kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.

Hoja hizo zilihusu masuala mbalimbali yanayowagusa watumishi katika utekelezaji wa majukumu yao na mazingira ya kazi, huku wakitoa mapendekezo yenye lengo la kuboresha utendaji na ustawi wa watumishi.

Katika ziara hiyo, Dkt. Jingu amewataka watumishi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kujituma na kwa kuzingatia wajibu wao wa kulinda heshima, uadilifu na hadhi ya Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (aliyesimama) akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara alipotembelea Mahakama hiyo jana tarehe 17 Agosti, 2026. Aliyeketi kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni Maalum, Bi. Mary Shirima na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Bw. Anatory Kagaruki.

Baadhi ya Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara wakisikiliza kwa makini maelekezo ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza nao.


Mwandishi Mwendesha Ofisi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Bi. Tausi Mwambujule akiwasilisha hoja mbele ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (hayupo katika picha).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina (kulia) akizungumza na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (kushoto) alipowasili katika Mahakama hiyo jana tarehe 17 Agosti, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Kevin Mhina (aliyeketi mbele) akiwa katika kikao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (aliyeketi wa kwanza kulia kwa Jaji Mfawidhi) pamoja na sehemy ya Viongozi walioambatana na Mtendaji Mkuu (kushoto). Kulia ni Majaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni Maalum, Bi. Mary Shirima (aliyesimama) akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara wakati wa ziara ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama katika Mahakama hiyo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (kushoto) akisalimiwa na kukaribishwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Bw. Anatory Kagaruki (kulia) wakati Mtendaji Mkuu alipowasilisha katika Divisheni hiyo tarehe 17 Agosti, 2026. Wa pili kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni Maalum, Bi. Mary Shirima na wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Suzan Kihawa.

Picha ya pamoja kati ya Viongozi wa meza kuu na Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara. Aliyeketi katikati ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni Maalum, Bi. Mary Shirima na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Bw. Anatory Kagaruki.

(Picha na IMAN KASSIAN, Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara)


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Jumatatu, 17 Agosti 2026

JAJI KIREKIANO MWENYEKITI MPYA TMJA TAWI LA DAR ES SALAAM

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Arnold Kirekiano amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dar es Salaam  baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho, Jaji, Mhe. David Ngunyale kuhamishiwa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Bukoba.

Mhe. Kirekiano alichaguliwa katika Mkutano Mkuu Maalum, uliofanyika tarehe 14  Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho,  Jaji Kirekiano, ambaye alimuwakilisha Mlezi wa Tawi hilo, ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi aliwasisitiza Majaji na Mahakimu kuendelea kufanya kazi kwa bidii kwa kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji katika utendaji kazi wao.

“Sisi Wanachama wa TMJA ambao ni sehemu ya watumishi wa Mahakama, tunapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutimiza wajibu wetu katika mambo yote ambayo Mahakama inayafanya katika kuhudumia wananchi. Haitaleta picha nzuri, ikiwa mambo ambayo tulipaswa kuyafanya hatuyafanyi,” alisisitiza Mhe. Kirekiano.

Aidha, aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa, matumaini ya Jaji Mfawidhi ni kwamba, kikao hicho kitakuwa ni mwanzo wa kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Akiendelea kutoa salamu za Mlezi wa Chama hicho, Mhe. Kirekiano pia aliwajulisha wajumbe wa mkutano huo, kuwa Mahakama inaendelea na maboresho mbalimbali na kwa sasa rasimu ya Mpango Mkakati, inaandaliwa na ipo katika hatua ya ushirikishwaji wa ndani kabla haijatoka nje kama nyaraka rasmi.

Jaji Kirekiano aliwataka wanachama hao kuwa mstari wa mbele katika kutoa maoni yao pindi rasimu hiyo itakaposhushwa kwao na kwamba wao kama Maofisa wa Mahakama  ambao wanafanya jukumu la msingi la utoaji haki, wanapaswa kufanya hivyo ili wakati wa utekelezaji wawe wamepata kile ambacho kimekuwa kikitarajiwa.

Mhe. Kirekiano alitumia mkutano huo kutoa mwaliko kwa wajumbe wote kwa niaba ya  Jaji Mfawidhi kushiriki kikamilifu katika Bonanza lililoandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dar es Salaam litakalofanyika Jumamosi tarehe 22 Agosti, 2026 katika Viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Saalam.

Katika mkutano huo pia kulikuwa na uchaguzi wa Mwenyekiti wa Chama hicho, Tawi la Dar es salaam, ambapo wajumbe, walipiga kura na kumchagua Mhe. Jaji Kirekiano kuwa Mwenyekiti wa Chama hicho.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Dar es Salaam, Mhe. Arnold Kirekiano (aliyesimama) ambaye pia ni Mwenyekiti mpya wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dar es Salaam akitoa shukrani kwa Wanachanma kwa kumchagua kuwa Mwenyekiti wa TMJA- Dar es Salaam. Kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Dar es Salaam, Mhe. Ramadhan Rugemalira na kulia ni Katibu wa TMJA, Mhe. Marko Mochiwa.

Baadhi ya wanachama wa TMJA Tawi la Dar es Salaam wakiwa katika kikao cha chama hicho.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dar es Salaam na Mwenyekiti mpya wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA), Mhe. Arnold Kirekiano (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wanachama wa TMJA Tawi la Dar es Salaam. Wa pili kulia ni Mhe. Ramadhan Rugemalira, Makamu Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Dar es Salaam, wa kwanza kulia ni Mhe. Jacqline Rugemalira, Mhazini wa TMJA Tawi la Dar es Salaam, wa kwanza kushoto ni Mhe. Ishaq Kuppa, Mwakilishi wa TMJA Tawi la Dar es Salaam  na wa pili kushoto ni Katibu wa Tawi hilo, Mhe. Marko Mochiwa.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

Ijumaa, 14 Agosti 2026

MASJALA NDOGO SONGWE YAANZISHA PROGRAMU YA MAZOEZI KUIMARISHA AFYA

Na IMAN MZUMBWE - Mahakama, Songwe

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe imeanzisha programu maalum ya mazoezi ya viungo ili kujenga utimamu wa mwili ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kujiandaa na mashindano mbalimbali, kuimarisha afya na kuongeza mshikamano miongoni mwa watumishi wa Mahakama. Programu hayo ya mazoezi itakuwa inafanyika katika viunga vya Mahakama Kuu iliyopo Nselewa-Mlowo.

Programu hiyo ya mazoezi inafanyika kwa kuwashirikisha watumishi mbalimbali wa Mahakama na wadau ambao wanapata nafasi ya kufanya mazoezi ya viungo na michezo mbalimbali chini ya usimamizi wa viongozi wa michezo ambao ni Afisa michezo Bi. Collether Amos Carlos, Mwenyikiti wa michezo Bw. Iman Patson na Katibu wa michezo Bi. Joyce Simba.

Akizungumza wakati wa kuanza mazoezi hayo, Afisa Michezo Bi. Collether Amos Carlos, amewaasa na kuwahimiza watumishi kujitokeza kwa wingi kushiriki kikamilifu katika mazoezi hayo na akisisitiza kuwa, michezo ni muhimu katika kuimarisha afya, kujenga umoja, ushirikiano na kuongeza morali ya utendaji kazi.

Aidha, Bi. Collether ameongeza kuwa, mazoezi hayo yataendelea kwa utaratibu maalum ili kuhakikisha watumishi wanakuwa katika hali nzuri kiafya na kuwa tayari kushiriki katika mashindano mbalimbali yatayokutanisha watumishi wa Mahakama na wadau wengine, huku Kaulimbiu ya programu hiyo ikiwa ni; “Afya bora, umoja na ushiriakiano kwa utendaji bora wa kazi”.

Afisa Michezo Bi. Collether Amos Carlos wa (kwanza kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Songwe.

Mwalimu wa michezo Bw. Martin Pales Kambengwa akitoa mazoezi mbele ya watumishi wa Mahakama ambao hawapo katika picha.

Watumishi wa Mahakama wakifanya mazoezi ya kucheza mpira wa mikono yaani netball

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Songwe wakifanaya mazoezi mepesi (warm up)

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Songwe wakifanaya mazoezi mepesi ya kupasha misuli.


 

 

Alhamisi, 13 Agosti 2026

MAHAKAMA KUU NJOMBE YAJA NA PROGRAMU MAALUM YA MAZOEZI KWA WATUMISHI KUIMARISHA AFYA

 Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe 

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe wameanza kufanya mazoezi ya pamoja ikiwa ni programu maalum ya kuimarisha afya ya mwili, kuimarisha mahusiano na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi kwa watumishi wa kada zote.

Programu hiyo ilianza tarehe 11 Agosti, 2026 ambapo Majaji, Mahakimu pamoja na Watumishi wengine wa Mahakama Kuu Njombe hukutana baada ya saa za kazi mara mbili kwa wiki kwa siku ya Jumanne na Ijumaa kwa ajili ya kushiriki kwenye mazoezi hayo.  

Katika nyakati tofauti tofauti, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amekuwa akiwasisitiza watumishi kufanya mazoezi mara kwa mara kwa ajili ya kulinda afya ya mwili hasa katika maeneo hayo yenye hali ya hewa ya baridi kali pamoja sambamba na kuimarisha mahusiano na mshikamano kwa watumishi wa kada zote.

Alisema kuwa, Majaji wa Mahakama hiyo wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha mazoezi hayakwami bila sababu za msingi, huku na wao wakishiriki kikamilifu kwenye mazoezi hayo pamoja na kuwahamasisha watumishi wote kushiriki kwa wingi kwakuwa mazoezi ni kwa ajili ya kujenga afya imara pamoja na kukabiliana na hali ya hewa ya baridi iliyopo mkoani Njombe ili waweze kuendelea na majukumu yao bila kutetereka kiafya.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano aliwasisitiza watumishi kuhakikisha mazoezi yanafanyika mara kwa mara na vifaa vyote vinavyohitajika katika mazoezi vinapatikana kwa wakati kama vile jezi, vibao vya mazoezi na mikeka kwa ajili ya mazoezi ya aina mbalimbali ili kuwapa watumishi hamasa ya kufanya mazoezi. Aidha, alieleza kuwa Taasisi nyingine kama Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) ya mkoani humo wameonesha nia ya kuungana na Mahakama katika program hiyo.

Kwa upande wa watumishi wa Mahakama Njombe wameonesha kufurahia programu hiyo ya mazoezi ambayo huwa yanaanza kwa kukimbia umbali wa kilomita tatu (3) yakifuatiwa na mazoezi ya kunyoosha viungo vya mwili ambapo mazoezi hayo yamewafanya watumishi wengi kushiriki bila kukosa kwa kuzingatia ratiba endelevu iliyotolewa na uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe.

Kutoka kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Victoria Nongwa, Viongozi na watumishi wengine kwa pamoja wakiwa kwenye mazoezi ya viungo. Mahakama Kuu Njombe imeanzisha programu hiyo maalum ya mazoezi inayowahusisha watumishi wote wa Mahakama hiyo.

 Jaji wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Obadia Bwegoge (mwenye jaketi la kijivu kushoto) akiwa sambamba na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Liadi Shamshama pamoja na watumishi wengine wakiendelea na mazoezi ya kukimbia.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Joseph Luambano (mwenye kofia nyeusi) akiwa mstari wa mbele kuhamasisha mazoezi ya mwili kwa watumishi wote wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Obadia Bwegoge, viongozi pamoja na  watumishi mbalimbali wakifanya mazoezi ya viungo.


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, kwa ujumla wao waendelea na mazoezi ya viungo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JAJI KIONGOZI AKUTANA NA WAJUMBE BARAZA LA TAASISI YA WASULUHISHI TANZANIA

  • Asema Mahakama ipo tayari kushirikiana ili kuimarisha matumizi ya usuluhishi

Na FAUSTINE KAPAMA na HABIBA MBARUKU-Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, leo tarehe 12 Agosti, 2026, amekutana na Wajumbe wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) na kufanya nao mazungumzo yanayolenga kuimarisha ushirikiano na kukuza utatuzi wa migogoro kwa njia ya mbadala (ADR).

Viongozi hao wakiongozwa na Rais wa TIArb, Wakili Msomi Aderickson Njunwa, wamekutana na Jaji Kiongozi kwenye ofisi yake iliyopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wajumbe wengine walioambatana na Rais wa TIArb, ni Wakili Nasra Songoro, Wakili Sultan Rajab, Wakili Marydenisia Katemana na Bi. Mariam Mruma, ambaye ni Katibu wa Baraza hilo.

Akizungumza na Wajumbe hao, Mhe. Dkt. Siyani alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania ipo tayari kushirikiana na TIArb kuimarisha matumizi ya usuluhishi au upatanshi, kwani ndiyo mfumo ambao kwa sasa unapewa uzito mkubwa duniani katika utatuzi wa migogoro, iwe ya kibiashara kiuchumi na usalama.

“Mahakama itajitahidi kadri inavyowezekana kuwa karibu na nyinyi, tushirikisheni tukutane katikati pale ambapo mkono wetu na mkono wenu hauwezi kufika. Tumefungua milango, msione shida kugonga pale ambapo mkono wenu unafika, tutawafungulia,” amesema.

Jaji Kiongozi amewaambia Wajumbe hao kuwa Mahakama ya Tanzania ina wataalam wengi, ambao wana ujuzi wa masuala ya usuluhishi, wanaoweza kusaidia pale kunapotokea changamoto kwenye masuala hayo.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amewaeleza kuwa TIArb inachokifanya ni kitu kikubwa ambacho jamii ya Watanzania bado haijapata elimu ya kutosha, hivyo wanayo kazi kubwa ya kuifanya Taasisi hiyo inafahamika zaidi kwa wananchi ili wanaopaswa kuitumia wasiwe wageni pekee.

“Nchi yetu inakua kiuchumi na uchumi unapokua kunakuwa na migogoro mingi ya kiuchumi. Ufanisi katika eneo la usuluhishi ni jambo ambalo lina faida kubwa kwani njia hii imeonekana kuokoa muda zaidi, tofauti na mchakato wa kimahakama,” amesema.

Jaji Kiongozi ametumia fursa hiyo kuwakumbusha Wajumbe hao kuwa Tanzania imeanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo eneo kubwa linahusu haki, hivyo kila Taasisi, ikiwemo TIArb ina mchango wa kutoa ili kuwa na jamii inayokusudia kufikia malengo ya Dira hiyo.

Mhe. Dkt. Siyani amebainisha kuwa Mahakama ya Tanzania inapoanda Mpango Mkakati wake, inajaribu kuamsha ndoto hiyo namna gani inaweza kutoa mchango wake katika utekelezaji wa dira hiyo.

“Ninyi kama TIArb hamtaweza kama sheria hazitakuwa haziwapi fursa ya kujielekeza huko, ni wakati muafaka sana wa kuishirikisha ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, mkiwa na mawazo yenu ya nini kitarahisisha kukuza usuluhishi katika nchi yetu. Hili ni jambo muhimu sana na huu ndiyo wakati sahihi zaidi kuliko utekelezaji wa Dira utakapokaposhika kasi,” amesema.

Awali, akizungumza baada ya kukutana na Jaji Kiongozi, Wakili Njunwa alieleza malengo ya kufanya ziara hiyo, ikiwemo kumshukuru kwa kuwafungulia Mkutanao wa nane wa Taasisi hiyo kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George M. Masaju, uliofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Rais wa TIArb alimweleza Jaji Kiongozi kuwa lengo lingine ilikuwa kueleza namna Mkutano huo ulivyofanyika hadi kumalizika kwake, maazimio yaliyofikiwa na kusikiliza ushauri au malelekezo yake kwa Taasisi hiyo.

Aidha, Rais wa TIArb aliomba Mahakama kushirikiana na Taasisi hiyo katika mambo mbalimbali, ikiwemo kupata mwongozo wa namna bora ya utendaji kazi ambao utasaidia kufikia lengo kuu la kuisaidia Serikali katika kuboresha mifumo ya haki.

Rais huyo alifafanua kuwa majukumu ya TIArb, ni usimamizi wa mashauri ya usuluhishi na kujenga uwezo kwa kuandaa vipindi mbalimbali vya mafunzo, yanayolenga kukuza matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania ofisini kwake jijini Dodoma (juu na chini).


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao hicho.

Rais wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania, Wakili Msomi Aderickson Njunwa (juu na picha chini katikati), akizungumza wakati wa kikao hicho. 


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (juu) na Makatibu wa Viongozi (chini) wakichukua kumbukumbu wakati wa kikao hicho.


Kikao kinaendelea.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa nne kutoka kulia picha ya juu na wa sita kutoka kulia picha ya chini) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza la Usuluhishi Tanzania na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania baada ya kufanyika kwa kikao hicho.