Alhamisi, 13 Agosti 2026

MAHAKAMA KUU NJOMBE YAJA NA PROGRAMU MAALUM YA MAZOEZI KWA WATUMISHI KUIMARISHA AFYA

 Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe 

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe wameanza kufanya mazoezi ya pamoja ikiwa ni programu maalum ya kuimarisha afya ya mwili, kuimarisha mahusiano na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi kwa watumishi wa kada zote.

Programu hiyo ilianza tarehe 11 Agosti, 2026 ambapo Majaji, Mahakimu pamoja na Watumishi wengine wa Mahakama Kuu Njombe hukutana baada ya saa za kazi mara mbili kwa wiki kwa siku ya Jumanne na Ijumaa kwa ajili ya kushiriki kwenye mazoezi hayo.  

Katika nyakati tofauti tofauti, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amekuwa akiwasisitiza watumishi kufanya mazoezi mara kwa mara kwa ajili ya kulinda afya ya mwili hasa katika maeneo hayo yenye hali ya hewa ya baridi kali pamoja sambamba na kuimarisha mahusiano na mshikamano kwa watumishi wa kada zote.

Alisema kuwa, Majaji wa Mahakama hiyo wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha mazoezi hayakwami bila sababu za msingi, huku na wao wakishiriki kikamilifu kwenye mazoezi hayo pamoja na kuwahamasisha watumishi wote kushiriki kwa wingi kwakuwa mazoezi ni kwa ajili ya kujenga afya imara pamoja na kukabiliana na hali ya hewa ya baridi iliyopo mkoani Njombe ili waweze kuendelea na majukumu yao bila kutetereka kiafya.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano aliwasisitiza watumishi kuhakikisha mazoezi yanafanyika mara kwa mara na vifaa vyote vinavyohitajika katika mazoezi vinapatikana kwa wakati kama vile jezi, vibao vya mazoezi na mikeka kwa ajili ya mazoezi ya aina mbalimbali ili kuwapa watumishi hamasa ya kufanya mazoezi. Aidha, alieleza kuwa Taasisi nyingine kama Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) ya mkoani humo wameonesha nia ya kuungana na Mahakama katika program hiyo.

Kwa upande wa watumishi wa Mahakama Njombe wameonesha kufurahia programu hiyo ya mazoezi ambayo huwa yanaanza kwa kukimbia umbali wa kilomita tatu (3) yakifuatiwa na mazoezi ya kunyoosha viungo vya mwili ambapo mazoezi hayo yamewafanya watumishi wengi kushiriki bila kukosa kwa kuzingatia ratiba endelevu iliyotolewa na uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe.

Kutoka kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Victoria Nongwa, Viongozi na watumishi wengine kwa pamoja wakiwa kwenye mazoezi ya viungo. Mahakama Kuu Njombe imeanzisha programu hiyo maalum ya mazoezi inayowahusisha watumishi wote wa Mahakama hiyo.

 Jaji wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Obadia Bwegoge (mwenye jaketi la kijivu kushoto) akiwa sambamba na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Liadi Shamshama pamoja na watumishi wengine wakiendelea na mazoezi ya kukimbia.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Joseph Luambano (mwenye kofia nyeusi) akiwa mstari wa mbele kuhamasisha mazoezi ya mwili kwa watumishi wote wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Obadia Bwegoge, viongozi pamoja na  watumishi mbalimbali wakifanya mazoezi ya viungo.


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, kwa ujumla wao waendelea na mazoezi ya viungo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JAJI KIONGOZI AKUTANA NA WAJUMBE BARAZA LA TAASISI YA WASULUHISHI TANZANIA

  • Asema Mahakama ipo tayari kushirikiana ili kuimarisha matumizi ya usuluhishi

Na FAUSTINE KAPAMA na HABIBA MBARUKU-Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, leo tarehe 12 Agosti, 2026, amekutana na Wajumbe wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) na kufanya nao mazungumzo yanayolenga kuimarisha ushirikiano na kukuza utatuzi wa migogoro kwa njia ya mbadala (ADR).

Viongozi hao wakiongozwa na Rais wa TIArb, Wakili Msomi Aderickson Njunwa, wamekutana na Jaji Kiongozi kwenye ofisi yake iliyopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wajumbe wengine walioambatana na Rais wa TIArb, ni Wakili Nasra Songoro, Wakili Sultan Rajab, Wakili Marydenisia Katemana na Bi. Mariam Mruma, ambaye ni Katibu wa Baraza hilo.

Akizungumza na Wajumbe hao, Mhe. Dkt. Siyani alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania ipo tayari kushirikiana na TIArb kuimarisha matumizi ya usuluhishi au upatanshi, kwani ndiyo mfumo ambao kwa sasa unapewa uzito mkubwa duniani katika utatuzi wa migogoro, iwe ya kibiashara kiuchumi na usalama.

“Mahakama itajitahidi kadri inavyowezekana kuwa karibu na nyinyi, tushirikisheni tukutane katikati pale ambapo mkono wetu na mkono wenu hauwezi kufika. Tumefungua milango, msione shida kugonga pale ambapo mkono wenu unafika, tutawafungulia,” amesema.

Jaji Kiongozi amewaambia Wajumbe hao kuwa Mahakama ya Tanzania ina wataalam wengi, ambao wana ujuzi wa masuala ya usuluhishi, wanaoweza kusaidia pale kunapotokea changamoto kwenye masuala hayo.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amewaeleza kuwa TIArb inachokifanya ni kitu kikubwa ambacho jamii ya Watanzania bado haijapata elimu ya kutosha, hivyo wanayo kazi kubwa ya kuifanya Taasisi hiyo inafahamika zaidi kwa wananchi ili wanaopaswa kuitumia wasiwe wageni pekee.

“Nchi yetu inakua kiuchumi na uchumi unapokua kunakuwa na migogoro mingi ya kiuchumi. Ufanisi katika eneo la usuluhishi ni jambo ambalo lina faida kubwa kwani njia hii imeonekana kuokoa muda zaidi, tofauti na mchakato wa kimahakama,” amesema.

Jaji Kiongozi ametumia fursa hiyo kuwakumbusha Wajumbe hao kuwa Tanzania imeanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo eneo kubwa linahusu haki, hivyo kila Taasisi, ikiwemo TIArb ina mchango wa kutoa ili kuwa na jamii inayokusudia kufikia malengo ya Dira hiyo.

Mhe. Dkt. Siyani amebainisha kuwa Mahakama ya Tanzania inapoanda Mpango Mkakati wake, inajaribu kuamsha ndoto hiyo namna gani inaweza kutoa mchango wake katika utekelezaji wa dira hiyo.

“Ninyi kama TIArb hamtaweza kama sheria hazitakuwa haziwapi fursa ya kujielekeza huko, ni wakati muafaka sana wa kuishirikisha ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, mkiwa na mawazo yenu ya nini kitarahisisha kukuza usuluhishi katika nchi yetu. Hili ni jambo muhimu sana na huu ndiyo wakati sahihi zaidi kuliko utekelezaji wa Dira utakapokaposhika kasi,” amesema.

Awali, akizungumza baada ya kukutana na Jaji Kiongozi, Wakili Njunwa alieleza malengo ya kufanya ziara hiyo, ikiwemo kumshukuru kwa kuwafungulia Mkutanao wa nane wa Taasisi hiyo kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George M. Masaju, uliofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Rais wa TIArb alimweleza Jaji Kiongozi kuwa lengo lingine ilikuwa kueleza namna Mkutano huo ulivyofanyika hadi kumalizika kwake, maazimio yaliyofikiwa na kusikiliza ushauri au malelekezo yake kwa Taasisi hiyo.

Aidha, Rais wa TIArb aliomba Mahakama kushirikiana na Taasisi hiyo katika mambo mbalimbali, ikiwemo kupata mwongozo wa namna bora ya utendaji kazi ambao utasaidia kufikia lengo kuu la kuisaidia Serikali katika kuboresha mifumo ya haki.

Rais huyo alifafanua kuwa majukumu ya TIArb, ni usimamizi wa mashauri ya usuluhishi na kujenga uwezo kwa kuandaa vipindi mbalimbali vya mafunzo, yanayolenga kukuza matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania ofisini kwake jijini Dodoma (juu na chini).


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao hicho.

Rais wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania, Wakili Msomi Aderickson Njunwa (juu na picha chini katikati), akizungumza wakati wa kikao hicho. 


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (juu) na Makatibu wa Viongozi (chini) wakichukua kumbukumbu wakati wa kikao hicho.


Kikao kinaendelea.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa nne kutoka kulia picha ya juu na wa sita kutoka kulia picha ya chini) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza la Usuluhishi Tanzania na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania baada ya kufanyika kwa kikao hicho.



 

Jumatano, 12 Agosti 2026

MAHAKAMA, TUME YA MIPANGO KUSHIRIKIANA UTEKELEZAJI DIRA YA TAIFA YA MAENDELEO 2050

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu pamoja na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na baadhi ya Viongozi wengine wa Mhimili huo leo tarehe 12 Agosti, 2026 wametembelewa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida pamoja na baadhi ya Viongozi wengine wa Tume hiyo kwa lengo la kufanya mazungumzo na Mahakama ya Tanzania ili kujadiliana kuhusu namna Taasisi  hizo mbili zitakavyoshirikiana katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

Dkt. Kida amesema, Mahakama ya Tanzania ina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira hiyo.

Aidha, Dkt. Jingu amesema Mahakama ya Tanzania imeshaanza utekelezaji wa Dira hiyo na ipo tayari kushirikiana na Tume ya Taifa ya Mipango kwa ustawi wa maendeleo ya Taifa la Tanzania.

Matukio katika picha mazungumzo kati ya Mahakama ya Tanzania na Tume ya Taifa ya Mipango.


Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida (katikati) akiteta jambo na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (kushoto) pamoja na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya leo tarehe 12 Agosti 2026 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida akisaini  kitabu cha wageni alipowasili katika Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu leo tarehe 12 Agosti, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Viongozi wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania na Viongozi kutoka Tume ya Taifa ya Mipango wakiwa katika kikao cha majadiliano juu ya ushirikiano katika ya Ofisi hizo katika utekelezaji wa pamoja wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 leo tarehe tarehe 12 Agosti, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Anyeongoza kikao hicho (aliyeketi mbele katikati) ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, kushoto ni Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida na kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.


Mazungumzo kati ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Taifa ya Mipango yakiendelea leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (katikati) akipokea Nyenzo ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2025 kutoka kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida leo tarehe 12 Agosti 2026 jijini Dodoma katika kikao kati ya Mahakama ya Tanzania na Tume ya Mipango kilicholenga kujadiliana kuhusu namna Mahakama itakavyoshirikiana na Tume hiyo katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu akimpatia Nyenzo za Utekelezaji Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mkurugenzi wa Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bw. Erasmus Uisso.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida (kulia) pamoja na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

(Picha na HALIMA MNETE, Mahakama)







DKT. JINGU AWATAKA WAANDISHI WAENDESHA OFISI, WASAIDIZI OFISI KUTENDA KAZI KWA WELEDI

 ·       Awakumbusha kutunza Siri na Vifaa vya Ofisi

·       Awasisitiza kushirikiana, kuheshimiana, kupendana na kuthaminiana katika nyakati mbalimbali za maisha

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu ametoa rai kwa Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa weledi na kujituma huku wakizingatia taratibu zilizopo zinazowaongoza kutekeleza ipasavyo majukumu ya kada zao.

Dkt. Jingu ametoa rai hiyo leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma alipokutana na kufanya mazungumzo na Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi wanaohudumu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu Masjala Kuu na Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma.

“Mnafanya kazi nzuri, niwaombe tu muendelee kufanya vizuri, tunakumbushana tu sio kwamba kuna changamoto kubwa, nyie wote mnafanya kazi vizuri, lakini nawaomba tuendelee kufanya hivyo kufanya kazi kwa weledi, kujituma lakini kwa kuzingatia maadili ya kazi zilizopo,” amesema Dkt. Jingu.

Kadhalika, Mtendaji Mkuu amewataka watumishi hao kuendeleza ushirikiano, kuheshimiana, kupendana na kuthaminiana katika nyakati mbalimbali za kimaisha.

Aidha, amewaeleza Watumishi hao kuwa, wao ni miongoni mwa kada muhimu katika maendeleo ya Taasisi kwakuwa kazi zao ambazo mara nyingi wanafanya kazi nyuma ya pazia zina mchango mkubwa katika ustawi wa Taasisi.

Katika hatua nyingine, Dkt. Jingu amewakumbusha watumishi hao kutunza siri za ofisi pamoja na vifaa vyote vya Ofisi na kusisitiza kuwa, kutofanya hivyo, kunahatarisha usalama wa Ofisi.

Mtendaji Mkuu ameitisha kikao hicho na watumishi hao ikiwa ni mara yake ya kwanza kuanza kukutana na watumishi wa Mahakama wa Kada mbalimbali tangu aapishwe kushika nafasi hiyo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tarehe 19 Juni, 2026.

Katika kikao hicho kililenga kusikiliza na kupokea masuala na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi hao ili kuona namna ya kuzifanyia kazi ili kuboresha utendaji kazi.

Miongoni mwa masuala mbalimbali ambayo watumishi hao wameomba kuboreshewa ni pamoja na huduma ya usafiri, semina/mafunzo, maslahi na mengine.

Aidha, Mtendaji Mkuu amewahakikishia watumishi hao kuwa, Mahakama itafanyia kazi yaliyowasilishwa na kwamba milango ya ofisi yake iko wazi kukaribisha ushauri na maoni mbalimbali ili mambo yaende vizuri.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu-Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick, Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo-Mahakama, Bi. Patricia Ngungulu, Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala-Mahakama, Bw. Stephen, Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimaliwatu, Bi. Sharifa Mbaraka pamoja na baadhi ya Maofisa wengine wa Mahakama. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu na  Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi wa Makao Makuu ya Mahakama, Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu Masjala Kuu na Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi kikiendelea leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu-Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick akiwa katika Kikao cha Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi kilichofanyika leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo-Mahakama, Bi. Patricia Ngungulu, (katikati), Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala-Mahakama, Bw. Stephen Magoha (kushoto) na Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimaliwatu, Bi. Sharifa Mbaraka (kulia) wakiwa katika Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi kilichofanyika leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Watumishi hao wakichangia jambo wakati wa kikao hicho.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu, Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick (aliyesimama mbele) akizungumza jambo wakati wa Kikao kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Waandishi Waendesha Ofisi na Wasaidizi wa Ofisi kilichofanyika leo tarehe 12 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na JEREMIA LUBANGO, Mahakama)























JAJI MFAWIDHI MBEYA ATETA NA KAMATI YA UTATU YASISITIZA KUIMARISHA UTOAJI HAKI

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Kamati ya Utatu inayojumuisha Jeshi la Polisi Tanzania (PT), Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), imefanya ziara Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kubaini maeneo yanayohitaji maboresho katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi za haki jinai.

Kamati hiyo iliongozwa na Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Bw. Basilius Namkambe ilikutana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya ofisini kwake jana tarehe 11 Agust 2026, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake ya kufanya ukaguzi wa utendaji kazi wa vyombo hivyo na kukutana na wadau wanaoshirikiana navyo katika kutekeleza majukumu ya haki jinai.

Ziara hiyo imelenga kupata maoni, kubaini changamoto na kupokea mapendekezo kutoka kwa wadau wa mfumo wa haki jinai, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kuboresha namna vyombo hivyo vinavyotekeleza majukumu yao kwa pamoja.

Akizungumza wakati wa kukutana na Kamati hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya amesisitiza kuwa ushirikiano wa karibu miongoni mwa vyombo vya haki jinai ni msingi muhimu katika kulinda haki, usalama na ustawi wa jamii.

“Vyombo vyote vya haki jinai vikishirikiana kwa pamoja itasaidia kurahisisha kulinda usalama na haki kwa jamii. Nashukuru sana kwa ujio wenu na tunaahidi kama Mahakama tutatoa ushirikiano wa kutosha kila itakapohitajika kufanya hivyo,” alisema Mhe. Mtulya.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, amesema kuwa, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya imeendelea kupata ushirikiano mzuri kutoka kwa wadau hao katika uendeshaji wa mashauri na utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya kimahakama yanayohitaji ushirikiano wa vyombo vya haki jinai.

Mhe. Laizer aliongeza kuwa, ushirikiano huo ni muhimu katika kuhakikisha mnyororo wa utoaji haki jinai unafanya kazi kwa ufanisi, huku kila chombo kikitekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.

Ziara ya Kamati ya Utatu Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya ni miongoni mwa hatua zinazolenga kuimarisha uratibu na mahusiano ya kikazi baina ya Mahakama na wadau wake, hususan katika masuala yanayohusu utekelezaji wa haki jinai.

Aidha, ziara hiyo inaendana na utekelezaji wa Nguzo ya Tatu ya Mahakama ya Tanzania, inayolenga kujenga na kuboresha mahusiano mazuri na wadau pamoja na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama.

Kwa mantiki hiyo, Mahakama ya Tanzania imeendelea kutambua kuwa ufanisi katika utoaji wa haki unahitaji ushirikiano wa karibu na endelevu kati ya Mahakama na wadau wote wa mfumo wa haki, kwa lengo la kuhakikisha haki inatendeka kwa wakati, kwa usawa mapema ipasavyo na kwa kuzingatia sheria.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati waliosimama mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na Moafisa wa Taasisi zinazounda Utatu waliomtembelea ofisini kwake, pamoja na sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya mara baada ya mazungumzo yanayohusu Taasisi hizo. Wengine ni (kushoto) Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, (wa pili kushoto) ni Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma kutoka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Bw. Joseph Kasongwa Mwaiswelo, (wa kwanza kulia) ni Naibu Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Mbeya, Bw. Jasper Luoga na (wa pili kulia) ni Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Bw. Basilius Namkambe.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, akiwa ofisini kwake akizungumza na Wageni ambao ni Kamati ya Utatu inayojumuisha Jeshi la Polisi Tanzania (PT), Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), walipomtembelea ofisini kwake (hawapo pichani) jana tarehe 11 Agosti, 2026.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

Jumanne, 11 Agosti 2026

JAJI KIONGOZI AKAGUA JENGO LINALOTARAJIWA KUWA MAHAKAMA YA FAMILIA DODOMA

Na ARAPHA RUSHEKE -Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, jana tarehe 10 Agosti, 2026, alifanya ziara katika jengo la zamani la Mahakama Kuu Dodoma, linalotarajiwa kutumika kwa ajili ya Mahakama inayoshughulikia masuala ya familia.

Akiwa ameambatana na Viongozi mbalimbali wa Mahakama, Jaji Kiongozi alikagua miundombinu ya jengo hilo na kujionea maboresho yanayoendelea kufanyika.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani alitoa maelekezo mbalimbali yanayolenga kusaidia katika uboreshaji wa miundombinu na mazingira ya jengo hilo, ili liweze kuwa na mazingira bora kwa ajili ya utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Mahakama katika kuhakikisha miundombinu yake inaendelea kuboreshwa, sambamba na kuimarisha mazingira ya utoaji wa huduma za haki.

PICHA CHINI ZINAOONESHA ZIARA HIYO

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiendelea na ukaguzi mara baada ya kuwasilia katika jengo la zamani la Mahakama Kuu Dodooma, ambalo linatarajiwa kuwa Mahakama ya Familia Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiangalia sehemu ya mapokezi ya jengo hilo ambalo linatarajiwa kuwa Mahakama ya Familia Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisikiliza maelezo ambayo yalikuwa yanatolewa na moja ya wakandarasi waliokuwa katika jengo hilo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akikagua mazingira ya nje ya jengo hilo(juu na chini).


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwaelekeza jambo wakandarasi wakati wa ukaguzi huo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Viongozi alioambatana nao katika ukaguzi huo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akijadili jambo na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga pamoja na Msajili Mkuu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Habari hii imehririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.