Jumatatu, 7 Septemba 2026

BALOZI MDOGO WA BURUNDI MKOANI KIGOMA AFANYA ZIARA MAHAKAMA KUU KIGOMA

Na AIDAN ROBERT,Mahakama-Kigoma.

Balozi mdogo wa Jamhuri ya Burundi nchini Tanzania anayehudumia Mkoa wa Kigoma, Bw. Kekenwa Jeremia, hivi karibuni alifanya ziara Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Kigoma na kufanya mazungumzo na Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Rwizile.

Lengo kuu la ziara hiyo ya Kiofisi iliyofanyika tarehe 04 Septemba, 2026 lilikuwa ni kujitambulisha upya na kutoa taarifa rasmi kwa Jaji Mfawidhi kuwa ameongezewa muda wa kuhudumu katika nafasi yake ya ubalozi mdogo nchini Tanzania. Hatua hiyo, inatajwa kuwa chachu kubwa ya ushirikiano wa karibu katika kutoa huduma za haki kwa raia wa Burundi.

Aidha, Balozi huyo alitumia fursa hiyo kufikisha salamu maalum za Serikali ya Jamhuri ya Burundi kwa Mahakama Kigoma, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kitaasisi katika nyanja za sheria, haki, na usalama wa wananchi wa nchi hizo mbili Tanzania na Burundi ambao wamekuwa wakiishi kwa amani na udugu wa karibu mkoani Kigoma.

Vile vile alimjulisha Mhe. Rwizile kuwa, Rais wa Jamhuri ya Burundi amependa kumuongezea muda wa kuendelea kufanya kazi katika nafasi hiyo ya Balozi ili kuhudumu katika ubalozi mdogo hapa nchini, uamuzi unaolenga kuendeleza kazi.

“Naleta salamu maalum kutoka Serikali ya Jamhuri ya Burundi kwa lengo la kuendeleza na kuimarisha uhusiano mwema na ushirikiano wa kitaasisi baina yetu, hasa katika masuala yanayohusu huduma za kisheria na kijamii mkoani Kigoma, mahusiano haya thabiti yanazidi kuchochea amani, usalama na ushirikiano mzuri kwa wananchi wetu wanaoishi na kufanya shughuli zao mkoani Kigoma,” alisema Balozi huyo.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Rwizile alimkaribisha na kumpongeza Balozi huyo kwa kuongezewa muda wa kazi, akibainisha utayari wa Mahakama Kuu Kigoma kuendelea kushirikiana ki-taasisi ili kuhakikisha haki inatendeka na ustawi wa jamii unalindwa.

“Ziara hii inazidi kuimarisha daraja la kidiplomasia na udugu uliopo kati ya Tanzania na Burundi, ikithibitisha dhamira ya dhati ya Viongozi wa nchi hizi katika kudumisha amani na maendeleo endelevu,” alisema Jaji Rwizile.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (kulia) akiwa katika mazungumzo Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Burundi, Bw. Kekenwa Jeremia alipotembelewa na Balozi huyo ofisini kwake Mahakama Kuu Kigoma tarehe 04 Septemba, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo na mgeni wake Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Burundi, Bw. Kekenwa Jeremia (hayupo katika picha).


Mazungumzo yakiendelea. Kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (kulia), wa pili kulia ni Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Burundi nchini Tanzania mkoani Kigoma, Bw. Kekenwa Jeremia, wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, wa pili kushoto ni Msaidizi wa Balozi Mdogo wa Burundi Mkoani Kigoma, Bw. Nininahazwe Adalbert.

Picha ya Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Burundi nchini Tanzania Mkoani Kigoma, Bw. Kekenwa Jeremia (katikati). Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili  Mbelwa na kushoto ni Msaidizi wa Balozi Mdogo wa Burundi Mkoani Kigoma, Bw. Nininahazwe Adalbert.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

JAJI MFAWIDHI MBEYA AANZA ZIARA YA UKAGUZI WA SHUGHULI ZA MAHAKAMA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, ameanza ziara ya ukaguzi katika maeneo mbalimbali ya Masjala hiyo kwa lengo la kutathmini utendaji wa kazi ili kubaini mafanikio na changamoto katika utoaji wa huduma, mazingira ya kazi na miundombinu ya Mahakama.

Ziara hiyo iliyoanza tarehe 03 Septemba 2026 ni sehemu ya utekelezaji wa Mahakama kusogeza huduma za haki karibu na wananchi, ambapo Mhe. Mtulya anatembelea Mahakama zinazotoa huduma pamoja na maeneo ambayo kwa sasa hayatoi huduma kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo uchakavu wa miundombinu, ukosefu wa majengo ya kutolea huduma na maeneo ambayo tayari yametengwa na Serikali za vijiji kwa kushirikiana na wananchi kwa ajili ya uanzishwaji wa huduma za Mahakama.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mtulya ametembelea Mahakama ya Wilaya ya Kyela pamoja na Mahakama za Mwanzo Busale, Ndobo, Ikolo na Kyela Mjini, ambapo amekagua hali ya utendaji, mazingira ya kazi na miundombinu ya Mahakama hizo.

Aidha, Mhe. Mtulya ametembelea maeneo ya Lema, Ipande, Mwaya na Kajunjumele, ambayo kwa sasa hayatoi huduma za Mahakama, huku baadhi ya maeneo hayo yakiwa na viwanja vilivyotengwa na Serikali za Vijiji kwa kushirikiana na wananchi kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Mtulya ameeleza kuwa kutembelea maeneo yenye viwanja vilivyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ni muhimu katika kuhakikisha maeneo hayo yanalindwa na kutumika kwa madhumuni yaliyokusudiwa.

“Katika kutekeleza mkakati wa Mahakama wa kusogeza huduma za Mahakama karibu na wananchi, ndiyo maana sisi tumekuja kutekeleza ziara hii ili kufanikisha mkakati huo,” amesema Mhe. Mtulya.

Katika kuhakikisha maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama yanalindwa, Mhe. Mtulya amewaelekeza viongozi wa maeneo husika kufuatilia upatikanaji wa hati za umiliki na kuweka alama za utambuzi katika kingo za viwanja hivyo ili kuvilinda dhidi ya uvamizi na matumizi yasiyokusudiwa.

Vilevile, amesisitiza umuhimu wa kutunza miundombinu ya Mahakama iliyopo na kuboresha mazingira ya kazi, ikiwa ni pamoja na usafi wa mazingira, upandaji na utunzaji wa miti na kuhakikisha majengo pamoja na maeneo ya Mahakama yanatunzwa ipasavyo.

Katika eneo la utoaji wa haki mapema ipasavyo, Mhe. Mtulya ameelekeza kuendelea kuweka mkazo katika usikilizaji na utatuzi wa mashauri ya vipaumbele, hususan mashauri ya mirathi na ndoa, ili kupunguza muda wa wananchi kusubiri haki na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za Mahakama.

Viongozi wengine walioshiriki ziara hiyo ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Ndobo. Viongozi wengine alioambatana nao (wanne kushoto) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo (wanne kulia) na watatu kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Rosta Mofuga.



Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiwa katika ukaguzi wa viwanja mbalimbali vya mahakama katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiwa katika ukaguzi wa viwanja mbalimbali vya mahakama katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiwa katika ukaguzi wa viwanja mbalimbali vya mahakama katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiwa katika ukaguzi wa viwanja mbalimbali vya mahakama katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, akipokelewa Mahakama na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kyela.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Serikali ya Kijiji cha Ipande katika uwanja wa Mahakama uliotengwa na Serikali ya Kijiji cha Ipande, (wanne kulia) ni Afisa Mtendaji wa Kata ya Ipande Bw. Lugano Mwabulanga na (watano kushoto) ni Afisa Ugani Kata ya Ipande Bw. Hamadi Mussa Kassim.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Serikali ya Kijiji cha Lema katika eneo wa lililotengwa na Serikali ya Kijiji cha Lema, wanne kulia ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Lema Bw. Charles Emily Mwakabulufu, wanne kushoto ni Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Lema Bi. Joice Mkumbwa Kaminyoge.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiongoza kikao cha pamoja na watumishi (hawapo pichani) wa Mahakama ya Wilaya Kyela, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya na Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya na Viongozi wengine alioambatana nao wakiwa kwenye picha ya Pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kyela.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Kyela Mjini Mhe, Nassir Alfred Msafiri akiwasilisha taarifa, kwa Viongozi hao waliowasili katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, akipokelewa Mahakama ya Mwanzo Ndobo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

Jumapili, 6 Septemba 2026

WATUMISHI MAHAKAMA NJOMBE WAFUNDISHWA MBINU ZA KUJIKINGA NA MAJANGA YA MOTO

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Njombe, wamepatiwa mafunzo ya siku moja kuhusu namna ya kujikinga na majanga ya moto pamoja na kuchukua tahadhali dhidi ya moto mahali pa kazi na nyumbani.

Mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Njombe yalifunguliwa na ASF. Bw. Bahati Mkutani tarehe 03 Septemba, 2026 na kuhudhuriwa na Viongozi pamoja na Watumishi wa Mahakama hiyo.

Akitoa mafunzo hayo, Ofisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, ZMK-FC Bi. Blandina Kayuya, alieleza kuhusu vifaa vya awali vya kuzimia moto, ikiwemo (portable fire extinguishers) za aina mbalimbali kama vile poda, povu na gesi ya kaboni dioksidi, pamoja na (fire blanket).

Bi. Kayuya alisema kuwa, miongoni mwa mambo yanayoweza kumfanya mtu ashindwe kukabiliana na moto katika hatua za awali ni uwoga na kutokuwa na vifaa sahihi vya kuzimia moto.

Alisisitiza umuhimu wa kuchukua tahadhali na kuwa na uelewa wa namna sahihi ya kutumia vifaa vya kuzimia moto ili kuhakikisha usalama wa watu na majengo dhidi ya majanga ya moto.

Akieleza hatua za kuchukua mtu anapogundua moto, Bi. Kayuya alisema; “moto unapotokea mtu hushindwa kuukabili kutokana na uwoga, unatakiwa ufanye yafuatayo pindi unapogundua moto: piga king’ora na yowe, piga simu ya bure Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kupitia namba 114, watu wasiojiweza wapewe kipaumbele kutoka eneo hatarishi, na jaribu kuzima moto bila kuhatarisha usalama wako na watu wengine.”

Aidha, alieleza kuwa vyanzo vikuu vinavyoweza kusababisha majanga ya moto ni pamoja na hitilafu za umeme, uzembe jikoni, uvutaji wa sigara, hujuma na uhalifu, pamoja na matukio ya asili kama vile radi.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Victoria Nongwa, baada ya kushiriki mafunzo ya nadharia na vitendo kuhusu namna ya kuzima moto, alilishukuru Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kutoa mafunzo katika Mahakama hiyo.

Mhe. Nongwa aliwaalika tena Maofisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kufika katika Mahakama hiyo kutoa mafunzo zaidi watakapopata nafasi, huku akiwashukuru Viongozi na Watumishi wote walioshiriki katika mafunzo hayo.

Mafunzo hayo, yaliyotolewa kwa ushirikiano na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Njombe, yalihusisha vipindi vya nadharia na vitendo. 

Mafunzo hayo yaliwajengea watumishi uelewa kuhusu matumizi sahihi ya vifaa vya kuzimia moto, namna ya kukabiliana na moto ukiwa katika hatua za awali, kutambua aina mbalimbali za moto na njia sahihi za kuukabili, pamoja na mbinu za kujiokoa pindi moto unapotokea.

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Njombe, wakishiriki mafunzo ya vitendo kuhusu namna ya kuzima moto na kujikinga na majanga ya moto. Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 03 Septemba, 2026.

Maofisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Njombe wakiwafundisha Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Njombe namna ya kujikinga na kukabiliana na majanga ya moto. Kutoka kushoto ni ZMK Bi. Blandina Kayuya, akifuatiwa na ZMM Bw. Msiwa Iddi, ASF Bw. Bahati Mkutani, na ZMM Bw. Kelvin Ngonyani. Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 03 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama hiyo.

Ofisa Hesabu Mahakama Kuu Njombe, Bw. Juma Nyenzi akiuliza swali kwa Maofisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wakati wa mafunzo huku baadhi ya watumishi wa Mahakama Kuu wakisikiliza kwa umakini.


Ofisa Utumishi, Bi. Happy Merere akijifunza kwa vitendo namna ya kutumia kifaa cha kuzimia moto, huku watumishi wengine wakifuatilia kwa karibu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




 

Alhamisi, 3 Septemba 2026

WADAU WA MAHAKAMA MOSHI WAPATIWA MAFUNZO YA MFUMO WA e-CMS

 · Wafundishwa jinsi ya kupakua Nakala za Hukumu na mienendo ya mashauri kupitia mfumo huo

· Wasisitizwa juu ya matumizi ya TEHAMA

Na PAUL PASCHAL, Mahakama-Moshi

Wadau wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Moshi wamepatiwa Mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Ki-elektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyolenga kuwaelekeza juu ya upandishwaji wa mashauri, upakuaji wa taarifa mbalimbali za kimahakama kama upakuaji wa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri.

Mafunzo hayo ambayo yametolewa kwa Wadau kutoka Magereza, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Waendesha Mashtaka wa Serikali yamefanyika leo tarehe 03 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mdogo wa mikutano wa Mahakama Kuu Moshi.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje na mada kuu ikiwasilishwa na Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Moshi, Bi Catherine Mugyabuso.

Akizungumza wakati ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Mwaiseje alisisitiza juu ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya kusaidia uendeshaji wa shughuli za Kimahakama kwa haraka na weledi katika kurahisisha upatikanaji wa taarifa za mashauri kama vile upatikanaji wa nakala za hukumu na mienendo ya shauri kwa haraka na kwa unafuu kupitia Mfumo wa e-CMS ili kuepuka malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa Mahabusu au Wafungwa.

“Ndugu washiriki tumewaita hapa leo ili kuwaongezea maarifa kidogo juu ya maboresho yaliofanyika na yanaoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha ufanisi na weledi katika jukumu zima la utoaji haki nchini kupitia mifumo yetu ya kimahakama huduma zetu zimeboreka na kurahisishwa ili kuondoa malalamiko kwa wote tunaowahudumia,” amesema Mhe. Mwaiseje.

Amewaeleza washiriki hao wa mafunzo kuwa, wao kama Wadau muhimu wa Mahakama katika kuwahudumia Watanzania ni vema nao wakapata ujuzi na kuwa na uelewa wa pamoja katika matumizi ya mfumo huo wa e-CMS.

Ameongeza kuwa, mfumo huo unaosimamia Mashauri Mahakamani    unalenga kuimarisha utoaji haki mapema ipasavyo na kwamba kupitia mfumo huo  kwa upande wa Mahakama Kuu Moshi kwa sasa  haitumii karatasi kupata nakala za hukumu na mwenendo wa shauri bali zinapatikana kupitia kwenye mfumo.

Mshiriki Suzan Kimaro ambaye ni Ofisa Mpelelezi Mkuu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kilimanjaro ameushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Moshi kwa maandalizi mazuri ya mafunzo hayo yanayokwenda kuwajenga na kuwaongezea uwezo wa ufanisi katika kutimiza majukumu yao.

“Kwa niaba ya Washiriki wote nipende kuishukuru Mahakama kwa mafunzo haya kwani yametupa mwanga mzuri wa namna ambavyo tunaweza kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi na weledi kupitia mfumo huu wa e-CMS hii itatusaidia sana kuwahudumia wananchi kwa haraka na pasipo na malalamiko yasio ya msingi,” amesema Bi. Suzan.

Washiriki kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Moshi, Magereza na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kilimanjaro kwa pamoja wakifuatilia mada iliyokuwa ikiwasilishwa wakati wa mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Moshi leo tarehe 03 Septemba, 2026.

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Moshi, Mhe.Sekela Mwaiseje akieleza akifungua mafunzo hayo na kueleza lengo la kufanyika kwa mafunzo hao kwa washiriki walioalikwa (hawapo katika picha).

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Moshi, Mhe. Opportuna Kipeta (aliyevaa miwani) pamoja na Hakimu Mkazi Mkuu Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, Mhe. Herrieth Mhenga (kulia) wakifuatilia mafunzo hayo.

Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Moshi, Bi. Catherine Mugyabuso akitoa Mada kwa washiriki wa Mafunzo kuhusu matumizi wa e-CMS (hawapo katika picha).


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)

 

Jumatano, 2 Septemba 2026

TMJA GEITA, BUKOBA WAIMARISHA UJIRANI MWEMA, USHIRIKIANO

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Geita

Tawi la Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Geita, tarehe 28 Agosti, 2026 lilipokea ugeni kutoka Tawi la TMJA Bukoba kwa lengo la kuimarisha ujirani mwema, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanachama katika kutekeleza majukumu yao ya kimahakama na kijamii.

Ugeni huo uliwasili na kuongozwa na Mlezi wa Tawi la TMJA Bukoba, Jaji Mfawidhi, Mhe. David Patrick Ngunyale. Ugeni huo ulipokelewa na Mlezi wa Tawi la TMJA Geita, Jaji Mfawidhi, Mhe. Projestus Kahyoza.

Katika ziara hiyo, Majaji na Mahakimu kutoka matawi hayo walishiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii na michezo, zikiwemo matendo ya huruma katika Hospitali ya Wilaya ya Geita, bonanza la michezo mbalimbali pamoja na chakula cha jioni.

Siku ya pili yake, yaani tarehe 29 Agosti, 2026 bonanza la michezo lilifanyika katika viwanja vya Geita Gold Mining Limited (GGML), likihusisha michezo mbalimbali, ikiwemo mpira wa miguu, mpira wa pete, mbio za yai na kijiko, kufukuza kuku  pamoja na mchezo wa karata.

Katika michezo hiyo, washiriki walionesha ushindani wa hali ya juu, huku wakidumisha mshikamano na urafiki. Bonanza hilo lililenga kutumia michezo kama fursa ya kujenga urafiki na mshikamano baina ya wanachama, kuimarisha afya na ustawi wa wanachama, pamoja na kuimarisha mahusiano ya kikazi na kikanda katika utendaji wa huduma za umma.

Baada ya kumalizika kwa shughuli za Bbonanza na kuagana na wageni kutoka Bukoba, tarehe 30 Agosti 2026, Tawi la TMJA Geita lilifanya Mkutano Mkuu wa Tawi katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Geita.

Mkutano huo ulilenga kujadili masuala mbalimbali yanayohusu utendaji wa chama, ustawi wa wanachama pamoja na namna ya kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa shughuli za kimahakama.

Akifungua Mkutano Mkuu huo, Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa viongozi kuwa mstari wa mbele katika kuonesha mfano bora wa uongozi, ushirikiano na uwajibikaji.

Mhe. Kahyoza aliwataka viongozi kutanguliza maslahi ya chama na kuwa mfano katika kutekeleza majukumu yao, akieleza kuwa uongozi bora ni msingi wa kujenga chama imara chenye uwezo wa kuwahudumia wanachama wake kwa ufanisi.

Akitoa taarifa ya shughuli za chama, Katibu wa TMJA Geita, Mhe. Ally Mgomba, alisema kuwa tawi limeendelea kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii kwa kushirikiana na Ofisi ya Mlezi wa Tawi.

Alisema TMJA Geita imekuwa ikitoa mchango na kuwafariji wanachama wakati wa misiba, kushiriki katika matukio ya furaha, pamoja na kutekeleza shughuli mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuwasaidia watu wenye mahitaji.

Miongoni mwa shughuli hizo ni ziara katika Shule yenye Mahitaji Maalumu Bukoba, ziara katika Magereza ya Wilaya ya Chato, ziara za ujirani mwema kati ya matawi na kanda mbalimbali, ikiwemo Bukoba na Kigoma, pamoja na ziara ya utalii katika Mgodi wa Geita Gold Mining Limited (GGML), iliyotanguliwa na shughuli za matendo ya huruma katika Hospitali ya Wilaya ya Geita.

Katika taarifa yake, Katibu huyo alieleza kuwa tawi limepata mafanikio mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa ushirikiano kati ya wanachama na uongozi wa tawi, pamoja na kuendelea kushirikiana katika kuwasaidia watu wenye changamoto na kushiriki katika matukio mbalimbali ya furaha ya wanachama.

Aidha, tawi limefanikiwa kuimarisha mfuko wake, kufanya ziara mbalimbali za kujenga mahusiano na ushirikiano na kupata tuzo mbalimbali kutokana na shughuli zake.

Pamoja na mafanikio hayo, Mhe. Mgomba alibainisha kuwa moja ya changamoto zinazolikabili tawi ni ushiriki mdogo wa wanachama katika mazoezi ya mwili. Alieleza kuwa hali hiyo inaweza kuathiri ushiriki wa wanachama katika shughuli za michezo na juhudi za kuimarisha afya na ustawi wao.

Kwa ujumla, ziara ya TMJA Bukoba pamoja na Mkutano Mkuu wa TMJA Geita imekuwa fursa muhimu ya kuimarisha ujirani mwema, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanachama.

Aidha, shughuli hizo zimetoa nafasi kwa wanachama kubadilishana uzoefu, kujadili mafanikio na changamoto, pamoja na kuweka mikakati ya kuimarisha chama na ustawi wa wanachama wake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza akiwakaribisha wageni kutoka Kanda ya Bukoba kushiriki hafla ya ujirani mwema.

Picha ya pamoja kati ya TMJA Geita na TMJA Bukoba baada ya kuwasili katika Mahakama Kuu Geita.


Wenyeviti wa TMJA Geita na Bukoba wakikabidhi baadhi ya sabuni na mafuta kwa Madakitari wa Hospitari ya Wilaya ya Geita.

Picha ya pamoja kati ya TMJA Geita na Bukoba katika mgodi wa madini wa Geita.

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Geita (juu) ikiwa katika picha kabla ya kuanza mchuano na timu ya Mgodi wa Geita iliyopo hapo chini.


Timu ya kuvuta kamba kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Bukoba ikivutana na Timu ya Mgodi wa Geita.


Uongozi wa TMJA Geita na Bukoba pamoja na Mgodi wa Geita ukiwa katika picha ya pamoja na wachezaji wa Mahakama Kuu Bukoba baada ya kuwakabidhi kombe.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.









JAJI MFAWIDHI MUSOMA AMUAPISHA AFISA USULUHISHI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki, tarehe 31 Agosti, 2026 alimwapisha Bw. Said Mmbando, kuwa Afisa Usuluhishi II.

Uapisho huo ulifanyika ofisini kwa Jaji Mfawidhi na kushuhudiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw. Leonard Maufi, pamoja na Msuluhishi Mkuu II, Bw. Peter Mahindi.

Pamoja na uapisho huo, Mhe. Kakolaki alitoa nasaha kwa Bw. Mmbando kufanya kazi hiyo bila upendeleo, huba au chuki. Alimsihi siku zote atambue kuwa kazi ya uamuzi ni kazi ya Mungu, hivyo aifanye kwa uadilifu na weledi mkubwa kwa zingatia sheria, taratibu na miongozo iliyopo.

Uapisho wa Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (kulia), mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (aliyesimama katikati), ukishuhudiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, Mtendaji wa Mahakama Musoma, Bw, Leonard Maufi, pamoja na Msuluhishi Mkuu II, Bw. Peter Mahindi.

Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (kulia) akisaini kiapo chake mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto), akisaini kiapo cha Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (katikati) wakati Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia) akishuhudia tukio hilo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto), akimkabidhi hati ya kiapo Afisa Usuluhishi II, Bw. Said Mmbando (katikati) wakati Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (wa pili kulia) pamoja na Msuluhishi Mkuu, Bw. Peter Mahindi (wa kwanza kulia) wakishuhudia tukio hilo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

 

 

MAHAKAMA YA RUFANI YAFANIKIWA KUSIKILIZA ASILIMIA 82 YA MASHAURI ARUSHA

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Arusha

Kikao cha nne cha Mahakama ya Rufani kwa mwaka, 2026 kilichoketi Arusha kuanzia tarehe 03 hadi 28 Agosti, 2026 kimefanikiwa kusikiliza jumla ya mashauri 31 kati ya 38 yaliyopangwa, sawa na asilimia 82 ya mashauri yote.

 Jopo la Majaji wa kikao hicho kiliongozwa na Mhe. Lilian Mashaka huku Majaji wengine wakiwa Mhe. Gerson Mdemu, na Mhe. Imani Aboud.

Akiwasilisha taarifa ya Tathmini ya Kikao hicho cha Mashauri ya Rufani hivi karibuni, Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Flora Mtarania alisema kuwa, mashauri 38 yalipangwa kusikilizwa ambapo kati ya hayo, 12 yalikuwa Rufaa za Jinai, 25 Rufaa za Madai, na moja ilikuwa Maombi ya Madai. Idadi ya mashauri yaliyosikilizwa ni 31 na mashauri yaliyoahirishwa ni 7.

Mhe. Mtarania ameongeza kwa kusema kuwa, Mashauri saba yaliyoahirishwa ni kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kukosekana kwa nyaraka muhimu za Baraza la Ardhi, Vifo kwa baadhi ya Wadaawa na Wasimamizi wa Mirathi kutoongezwa shaurini, kukosekana kwa wadaawa katika anuani zilizowekwa kwenye rekodi za rufaa na kutofautiana kwa majina ya wadaawa kwenye nyaraka za Mahakama Kuu.

Naibu Msajili huyo aliyataja mafanikio kadhaa yaliyopatikana katika kikao hicho kuwa ni pamoja na Mashauri yaliyopangwa kusikilizwa na kumalizika kwa asilimia 82, Wadaawa wote waliopata wito walihudhuria mahakamani kwa wakati, hivyo kuwezesha usikilizaji wa mashauri kwa wakati na Maamuzi yaliyosomwa kutolewa kwa wadaawa kwa wakati na kupandishwa katika Maktaba Mtandao ya Mahakama (TanzLII).

Kikao hicho cha Mashauri ya Mahakama ya Rufani Kanda ya Arusha kilifanyika sanjari na vikao vingine tisa katika Kanda za Mwanza, Shinyanga, Moshi, Bukoba, Dar es Salaam, Iringa, Mbeya, Sumbawanga na Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Jopo la Majaji, Mhe. Lillian Mashaka akiongoza Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Aboud. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi (IJC) Arusha.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu (kushoto) akifafanua mambo kadhaa wakati wa Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akichangia jambo wakati wa Kikao hicho. Aliyeketi upande wa kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Aisha Bade. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi (IJC) Arusha.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Seif Kulita akichangia jambo wakati wa Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Nyigulila Mwaseba. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Flora Mtarania akiwasilisha Taarifa ya Tathmini ya Kikao cha Mashauri ya Mahakama ya Rufani kilichofanyika mkoani Arusha.



Wajumbe mbalimbali waliohudhuria Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)