Alhamisi, 30 Julai 2026

MWANASHERIA WA SERIKALI MFAWIDHI KIGOMA AJITAMBULISHA RASMI KWA JAJI MFAWIDHI, MHE. RWIZILE

  • Aahidi kudumisha ushirikiano na Mahakama mkoani humo

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni amefanya ziara ya heshima ya kumtembelea Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile lengo likiwa ni kujitambulisha rasmi na kuimarisha ushirikiano wa kikazi katika utoaji haki mkoani humo.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 29 Julai, 2026 katika Ofisi za Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma ambapo Mwanasheria huyo aliambatana na Wakili  wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma, Bw. George Kalenda pamoja na Mfawidhi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Magumbo.

Aidha, wakati wa mazungumzo ya Viongozi hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu upatikanaji haki, ikiwemo kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri na kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani.

Vilevile, walisisitiza juu ya umuhimu wa kuendelea kudumisha nidhamu, weledi na uwajibikaji katika mnyororo mzima wautoaji haki mapema ipasavyo.

Aidha, Mhe. Rwizile amewakaribisha Viongozi hao na kuwapongeza kwa hatua ya kufanya ziara hiyo ya kumtambulisha Mwanasheria Mkuu Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, huku akisisitiza kuwa na ushirikiano wa karibu baina ya Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) ni nguzo kuu katika kuhakikisha haki inatendeka mapema ipasavyo na kwa haki kwa kila mwananchi.

“Mahakama Kigoma itakupa ushirikiano ili utimize wajibu wako katika mnyororo wa haki, hivyo utakapobaini changamoto yoyote inayohitajika kutatuliwa na Mahakama basi usisite kuileta kwa ajili ya kutatuliwa kabla haijaathiri mnyororo wa kutoa haki mapema ipasavyo kwa kila mwananchi,” amesema,  Jaji Rwizile.

Kwa upande wake, Mwanasheria huyo Mfawidhi  wa Mkoa Kigoma, Bw. Said Seni amesema, anaishukuru mamlaka yake kumpangia kazi mkoani Kigoma, kwani amekutana na watu wema, wakarimu na wenye ari ya kufanya kazi kwa weledi na kujituma.

Amesema kuwa, anayo imani kwamba atapata ushirikiano wa kutosha katika kutimiza wajibu wake katika kipindi chote atakachokuwa katika ofisi hiyo Mkoani Kigoma.

Kadhalika, Mwanasheria huyo amemuahidi Jaji Mfawidhi kuwa, atafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na kuhakikisha amri za Mahakama zinatekelezwa kwa wakati na kwa mujibu wa sheria zilizopo.

Ameongeza kwamba, Ofisi hiyo ni mpya katika Mkoa wa Kigoma imeanzishwa kwa lengo la kuongeza nguvu ili kuisaidia Mahakama kutenda haki mapema ipasavyo, kupitia kutimiza wajibu wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama, Bw. Yusuph Kasuka. 

Ziara hiyo imelenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na ushirikiano baina ya Mhimili wa Mahakama na Taasisi za usimamizi wa sheria na uendeshaji wa mashtaka mkoani Kigoma, ili kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa ufanisi na mapema ipasavyo kwa maslahi ya wananchi kwa ujumla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (aliyeketi mbele) akifanya mazungumzo na Ujumbe wa Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma ulipomtembelea  ofisini kwake Mahakama Kuu Kigoma leo tarehe 30 Julai, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa neno kwa wageni wake katika maongezi yaliyofanyika katika ofisi yake iliyopo katika jengo la Mahakama Kuu Kigoma.

Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mfawidhi na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma kwa mapokezi mazuri.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa utambulisho wa Viongozi waliofika katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile leo tarehe 30 Julai, 2026.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi akifurahia jambo alipokuwa akizungumza na Viongozi na Wadau wa Haki Jinai waliofika ofisini kwake kumsabahi na wakimtambulisha Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni.


Wakili wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma,  Bw. George Kalenda akisikiliza kwa makini wakati Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile, alipokuwa akitoa neno wakati wa mazungumzo yao leo tarehe 30 Julai, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile  (wa tatu kulia) akiwa pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (wa tatu kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka (wa kwanza kushoto), Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni, (wa wa pili kulia), Mfawidhi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Magumbo (wa kwanza kulia) na Wakili wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma, Bw. George Kalenda.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (aliyeketi mbele) akitoa neno kwa Viongozi waliofika ofisini kwake kwa ajili ya utambulisho wa Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

WANANCHI KATA YA LENGATEI WATOA KIWANJA CHA UJENZI WA MAHAKAMA

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kupitia kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo Mhe. Dkt. Adam Mambi umekabidhiwa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo huku makabidhiano hayo yakifanywa na Viongozi pamoja na Wananchi wa Kata ya Lengatei iliyopo katika Tarafa ya Kijungu, wilayani Kiteto Mkoa wa Manyara.

Eneo hilo lilikabidhiwa rasmi na Viongozi na wananchi wa Kata hiyo, wakati wakimpokea Mhe. Dkt. Mambi alipofanya ziara ya ukaguzi wa shughuli za Mahakama katika eneo hilo mnamo tarehe 27 Julai, 2026.

Aidha, wananchi na viongozi hao wameonesha uhitaji wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo lao kwa kuwa, kwa sasa wanapata changamoto kusafiri kwenda mpaka Mahakama ya Mwanzo Kijungu kupata huduma za kimahakama ambapo kuna umbali wa Kilometa zaidi ya 12 kutoka kwenye Kata hiyo.

Akizungumza wakati wa mapokezi ya Kiwanja hicho, Mhe. Dkt. Mambi aliwashukuru viongozi pamoja na wananchi hao kwa kutoa kiwanja hicho kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo itakayo wasaidia wananchi kurahishisha kutoa huduma za kimahakama katika Kata hiyo na maeneo ya jirani.

“Tunawashukuru sana kwa kuwa mmeuona umuhimu wa Mhimili wa Mahakama katika dhima nzima ya utoaji wa haki mpaka mkaamua kutoa kiwanja hiki. Tunaahidi kushirikiana nanyi bega kwa bega mpaka tutakapokamilisha ujenzi wa Mahakama hii, naahidi ushirikiano kutoka kwa Mahakama ili shughuli hii ikamilike mapema,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Akizungumza wakati wa kukabidhi kiwanja hicho, Afisa Mtendaji wa Kata ya Lengatei Bw. Julius Kelato kwa niaba ya viongozi na wananchi wa kata hiyo, alishukuru uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kufika katika maeneo hayo na kuahidi kuanza mchakato wa ujenzi mara baada ya mchakato wa upatikanaji wa hati utakapokamilika.

“Tukishamaliza suala la upatikanaji wa hati ya kiwanja hiki, tumekusudia kuanza ujenzi wa Mahakama hii kwa kutumia nguvu za wananchi wetu kama ambavyo tumekuwa tukifanya kwa taasisi nyingine za Serikali,” alisema Bw. Kelato,

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mambi na timu yake ya ukaguzi walitembelea katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya, Mhe. Fakii Lulandala ambapo Mhe. Dkt. Mambi, alimuomba Mkuu wa Wilaya asaidie katika zoezi la upatikanaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa hati za umiliki wa viwanja hivyo ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima wakati wa matumizi yake.

Naye, Mhe. Lulandala aliahidi kufanya hayo. “Siku zote, tumekuwa tukishirikiana na Mahakama katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo na hususan katika kusaidia upatikanaji wa haki na amani katika maeneo yetu. Kwa sababu hizo ninakuahidi Mhe. Jaji kuwa, nitajitahidi kuwasaidia katika suala hili,” alisema Mhe. Lulandala.

Jaji Mfawidhi Mhe. Dkt. Mambi akiwa wilayani Kiteto alifanikiwa kukagua Mahakama ya Wilaya ya Kiteto, pamoja na Mahakama za Mwanzo Kibaya, Dosidosi na Kijungu. Kwa upande wa Wilaya ya Simanjiro, alikagua Mahakama ya Wilaya Simanjiro, Mahakama za Mwanzo Engasmet, Shambarai na Msitu wa Tembo.

Aidha, akiwa wilayani Simanjiro Mhe. Dkt. Mambi alipewa na kupokea ahadi kutoka kwa wananchi wa Kata ya Msitu wa Tembo kupitia viongozi wao walioahidi kuanza ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo lao kama walivyoahidi wananchi wa Kata ya Lengatei wilayani Kiteto. 

Viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa tano kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi na wananchi wa Kata ya Lengatei wilayani Kiteto walipotembelea kiwanja ambacho kimetolewa na wananchi wa Lengatei kwa Uongozi wa Mahakama, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo hilo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama) akiwa anazungumza na viongozi na wananchi wa Kata ya Lengatei alipowatembelea ofisini kwao wakati wa ziara ya Ukaguzi wa Mahakama wilayani Kiteto. Wengine ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe Charles Mnzava (kulia) na kushoto ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kiteto Mhe. Aron Losioki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (kulia) akizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mhe. Fakii Lulandala mara baada ya kumtembelea Mkuu huyo wa Wilaya katika Ofisi yake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Shambarai iliyopo Wilayani Simanjiro mara baada ya kufika Kituoni hapo kwa ajili ya Ukaguzi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Shambarai iliyopo Wilayani Simanjiro akisoma taarifa mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi na viongozi wengine waliofika kituoni hapo kwa ajili ya ukaguzi (hawapo pichani)

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Simanjiro, mbele ya Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro ambalo linaendelea kujengwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi, akisalimiana na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto mara baada ya kuwasili kituoni hapo kwa ajili ya Ukaguzi wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyenyoosha mkono) akizungumza na sehemu ya viongozi na wananchi wa Kata ya Msitu wa Tembo, Wilayani Simanjiro mara baada ya kufika katika Mahakama ya Mwanzo Msitu wa Tembo kwa ajili ya Ukaguzi.

 (Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Jumatano, 29 Julai 2026

TMJA DODOMA YAKUTANA, YASISITIZA UMOJA, KUSHIRIKI MAFUNZO NA KUJIBIDIISHA KIELIMU

Na ARAPHA RUSHEKEMahakama-Dodoma

Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma chini ya Mwenyekiti wake, Mhe. Faisal Kahamba hivi karibuni walifanya kikao cha wanachama wote kilicholenga kujadili maendeleo ya tawi hilo, kuimarisha mshikamano wa wanachama pamoja na kujengeana uwezo katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama

Kikao hicho kilichohudhuriwa na wanachama wa TMJA kutoka Mahakama mbalimbali za Mkoa wa Dodoma kilifanyika kwenye Ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma.

Miongoni mwa ajenda muhimu za kikao hicho ilikuwa ni kuwapokea Wanachama wapya 11 wakiongozwa na Mlezi mpya wa TMJA Dodoma ambae ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga ambaye amehamishiwa katika Kituo hicho hivi karibuni akitokea Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya.

Akizungumza wakati akitoa salamu zake, Jaji Mfawidhi na Mlezi wa TMJA Dodoma, Mhe. Tiganga alisema, “ninafurahi kuwa sehemu ya familia hii lakini pia niwashukuru Viongozi kwa kuandaa kikao hiki muhimu kwangu mimi ni kikao muhimu sana kwani karibia wanachama wote mmekuja na tumeonana, niwapongeze kwa umoja huu sio kitu rahisi kupata wajumbe wengi namna hii, wote tunafahamu umuhimu wa kuwa na chama kilicho hai na chenye malengo yanayotekeleza wanachama wenye utayari wa kutekeleza malengo hayo.”

Amesisitiza kuwa, pamoja na mafunzo wanayoyaandaa Wanachama hao wajitahidi kuhudhuria mafunzo wanapopata nafasi kwa kuwa ni muhimu lakini pia kila mmoja aendelee kujiongezea elimu na kujifunza kwani elimu haina mwisho.

Vilevile Mhe. Tiganga aliendelea kusema, “kila mmoja wetu ajitahidi kujibidiisha lengo ni kwamba pamoja na kuhakikisha kazi za Mwajiri zinakwenda vizuri tujiandae kukua kitaaluma pia ni vizuri kutambua tunao Mfumo unaotupima JOPRAS, mpimaji anajaza eneo dogo sana hasa la maadili kwa kiasi kikubwa mfumo wenyewe unakupima kutokana na utendaji wako wa kazi unachakata zile taarifa za kwenye mfumo kwahiyo niwakumbushe na tuendelee kufahamu kwamba kujibidiisha ndipo kutafanya tuonekane kuwa utendaji kazi wetu umebadilika mnatakiwa mfahamu kuwa hatutakiwi kumuacha mtu yoyote nyuma hivyo tushirikiane kwa muda wote ushauri na kila kitu kama mlezi na kiongozi wenu wa sasa napenda ushirikiano na ninapenda kila mmoja wenu asonge mbele.”

Jaji Mfawidhi huyo amewahakikishia Wana TMJA Tawi la Dodoma kuwa ataendelea kuwa mlezi na mshauri lakini pia atatekeleza wajibu wake kama Mwanachama kama ambavyo Katiba inamtaka pamoja na miongozo inavyotaka huku akisisitiza suala la uhai wa Chama liwe la msingi sana na kuhakikisha chama hicho kinakuwa imara.

Kikao hicho kiliambatana na mafunzo kuhusu mbinu za uchukuaji wa ushahidi wakati wa usikilizaji wa mashauri ya jinai, yaliyowasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Suleiman Hassan.

Katika Mafunzo hayo Viongozi na Wajumbe mbalimbali walichangia, akiwemo Mhe. Tiganga, Mhe. Biswalo Mganga (Jaji), Mhe. Irene Msokwa (Jaji).

Washiriki walieleza kuwa mafunzo hayo yameongeza uelewa na yatachangia kuboresha utoaji haki kwa kuzingatia misingi ya sheria na weledi.

Mbali na mafunzo hayo, Wanachama walijadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya Tawi, hususan namna ya kuendelea kuimarisha umoja, mshikamano na upendo miongoni mwa Wanachama.

Akizungumza wakati wa kufunga mjadala huo, Mwenyekiti wa TMJA Dodoma, Mhe. Faisal Kahamba, aliwahimiza wanachama kuendelea kutekeleza maazimio ya vikao vya TMJA na kushiriki kikamilifu katika shughuli zote za Chama kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na mafanikio ya Tawi.

Vilevile, wanachama walikumbushwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia kaulimbiu ya Mahakama ya Tanzania isemayo "Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji," ambayo ndiyo msingi wa utoaji wa huduma bora za haki kwa wananchi.

Katika kikao hicho pia, wajumbe walihimizwa kushiriki kwa wingi katika ziara ya Bagamoyo inayotarajiwa kufanyika mwezi Septemba, 2026 ambayo itaambatana na Bonanza la kuimarisha afya, ushirikiano na mahusiano miongoni mwa Wanachama wa TMJA.

Kwa upande mwingine, Wanachama walitoa pongezi kwa uongozi wa TMJA Dodoma kwa kuendelea kusimamia matendo ya huruma katika jamii. Kupitia programu hiyo, tawi limefanikiwa kutoa misaada mbalimbali ikiwemo vyakula, nguo, magodoro na vifaa tiba kwa taasisi zenye uhitaji katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Dodoma katika kipindi cha mwaka 2024 hadi 2026.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa wito uliotolewa kwa Wanachama kuendelea kudumisha mshikamano, kuongeza ushirikiano na kutekeleza majukumu yao kwa weledi ili kuendeleza mafanikio ya TMJA Dodoma na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa  Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (aliyesimama katikati mstari wa mbele) na Viongozi na Wajumbe wa TMJA mkoani huo mara baada ya kikao.

 

Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa  Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga akiwasilisha hotuba yake kwa wajumbe wa TMJA Dodoma wakati wa kikao chao kilichofanyika hivi karibuni.


Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Feisal Kahamba akiwasilisha hotuba ya ufunguzi wa kikao wakati wa kikao hicho.

  Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TMJA Tawi la Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma ambapo pia ni Wanachama wa TMJA, aliyesimama kushoto ni Mhe. Biswalo Mganga, katikati ni Mhe. Irene Musokwa na kulia ni Mhe. Mhe. Suleiman Hassan. Walioketi na Jaji Mfawidhi kushoto  ni Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Feisal Kahamba na kulia ni Katibu wa Chama hicho, Mhe Getrude Misana. 

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TMJA Tawi la Dodoma,  Mhe. Joachim Tiganga (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na 
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Bw. Bedson Mariba (aliyesimama). Walioketi kushoto ni Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Feisal Kahamba na kulia ni Katibu wa Chama hicho, Mhe. Getrude Misana. 


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

MAHAKAMA KUU DODOMA YAWAKARIBISHA MAJAJI NA WATUMISHI WALIOHAMISHIWA KITUO HICHO; YAWAAGA WALIOHAMA

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma

Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma imefanya hafla ya kuwakaribisha Majaji pamoja na Watumishi waliohamia katika Mahakama hiyo na kuwaaga waliohamishwa kutoka Mahakama hiyo.

Hafla hiyo ilifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita katika Ukumbi wa 'Royal Village' jijini Dodoma na kuwakutanisha Majaji, Wasajili, Viongozi na Watumishi wa Mahakama kutoka katika Vituo mbalimbali vya Mahakama Dodoma ililenga kuwaaga watumishi waliopata uhamisho pamoja na kuwakaribisha wale waliopangiwa kuanza majukumu katika Mahakama hiyo.

Miongoni mwa Viongozi waliohudhuria hafla hiyo walikuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Masabo ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma aliagwa kufuatiwa kuteuliwa kwake kuwa Jaji wa Rufani, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga aliyekaribishwa baada ya kuhamia Dodoma kuwa Mfawidhi wa Masjala hiyo, Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara,  Mhe. Evarist  Longopa ambaye aliagwa baada ya kuhamishiwa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara Dar es Salaam. 

Viongozi wengine waliohudhuria sherehe hiyo ni Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga, Mhe. Suleiman Hassan, Mhe. Irene Musokwa pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama hiyo.

Kulikuwa pia na Watumishi wa kada mbalimbali ambao wameagwa na kukaribishwa, watumishi hao ni pamoja na wa Kada za Watunza kumbukumbu, Wasaidizi wa Ofisi, Madereva, Mwandishi Mwendesha Ofisi pamoja na Wasaidizi wa Sheria.

Shughuli za hafla zilianza kwa kuwasili kwa wageni waalikwa na wageni rasmi, zikafuatiwa na dua fupi, utambulisho wa wageni, kukata keki na shughuli mbalimbali za kijamii zilizolenga kuimarisha mshikamano na ushirikiano miongoni mwa watumishi wa Mahakama pamoja na wadau .

Aidha, wageni walipata fursa ya kutoa salamu za pongezi na shukrani, kutoa zawadi kwa wahusika pamoja na kusikiliza nasaha na hotuba zilizosisitiza umuhimu wa kudumisha maadili, uwajibikaji na ushirikiano katika utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Hafla hiyo ilipambwa na shamrashamra pamoja na muziki kutoka Bendi ya Magereza Dodoma ambao ni Wadau wakubwa wa Mahakama.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa kupata chakula cha pamoja na burudani ya muziki, ambapo washiriki walipata nafasi ya kuendelea kujenga mahusiano mema na kuimarisha umoja ndani ya familia ya Mahakama.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt Juliana Masabo (kulia) akisikiliza kwa makini ujumbe wa zawadi yake kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma ambayo iliwasilishwa kwake na Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Joachim Tiganga wakati wa sherehe ya kuwaaga na kuwakaribisha Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma iliyofanyika katika ukumbi wa Royal Village jijini Dodoma.


    Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.Dkt Juliana Masabo wa kwanza kulia akisikiliza kwa makini ujumbe wa zawadi yake kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma ambayo iliwasilishwa kwake na Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu Dodoma Mhe Joachim Tiganga wakati wa sherehe hiyo.


Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masajala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (kulia) akipokea  dhawadi yake kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma iliyowasilishwa kwake na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga wakati wa sherehe hiyo.


 
 Matukio katika picha Sherehe ya Kuwakaribisha watumishi waliohamia Mahakama Kuu na kuwaaga Watumishi waliohama kutoka Mahakama hiyo.



(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

UONGOZI WA MAHAKAMA KUU KIGOMA WATEMBELEA KIWANDA CHA CHUMVI UVINZA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile hivi karibuni aliongoza Viongozi na Wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama hiyo kufanya ziara ya kujifunza na kuimarisha ushirikiano na wadau wa Sekta Binafsi katika Kiwanda cha Chumvi Lishe cha ‘Nyanza Salt Mine’ kilichopo Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma.

Mara baada ya kumaliza Kikao chao cha Uongozi kilichofanyika katika Mahakama ya Wilaya Uvinza, Viongozi hao walitembelea Kiwanda hicho ili kujionea pia uwekezaji mkubwa wa Serikali katika Sekta ya Madini.

Akiwa kituoni hapo, Mhe. Rwizile na ujumbe wake walipata fursa ya kipekee ya kujionea kwa vitendo mchakato mzima wa uzalishaji wa chumvi ya lishe ya mifugo maarufu kama "Cattle Lick" pamoja na mnyororo mzima wa uzalishaji kuanzia kuchimbwa kwa madini hayo ardhini hadi kufikia hatua ya mwisho ya bidhaa bora iliyo tayari kwa matumizi ya walaji na wafugaji.

Aidha, Uongozi wa Mahakama haukuacha kusifu jitihada zinazofanywa katika uwekezaji huo, huku wakitoa pongezi za dhati kwa Kampuni ya Chumvi ya Nyanza (Nyanza Salt Mine) kwa kutoa ajira kwa wananchi wa Kigoma na kuchangia kwa kiwango kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa Mkoa na Taifa kwa ujumla.

Akitoa taarifa na elimu kwa Viongozi hao wa Mahakama, Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho, Bw. Mukesh Mamlani, alieleza kuwa, kiwanda hicho kimekuwa na historia ndefu ya uzalishaji na kwamba kiliizinduliwa rasmi Agosti, 2025 na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde.

Uwekezaji huo ni utekelezaji halisi wa maono ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha rasilimali na madini ya nchi yanaongezewa thamani hapa nchini na kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazotoka nje ya nchi.

Uvinza sasa inashuhudia mabadiliko makubwa; kutoka kutegemea machimbo ya jadi yaliyodumu tangu zama za chuma, eneo hilo limegeuka kuwa kitovu cha viwanda vya kisasa vya kuchakata chumvi.

“Chumvi lishe ni hitaji muhimu kwa afya ya mifugo. Kupitia kiwanda hiki, tutahakikisha tunazalisha bidhaa bora kwa kuzingatia viwango vya kimataifa, ili wafugaji wa Tanzania waweze kupata bidhaa salama, bora na kwa bei nafuu. Lengo letu ni kuinua ustawi wa sekta ya mifugo nchini,” alisema Bw. Mamlani.

Aidha, Mkurugenzi Mtendaji huyo, alibainisha kuwa, Kampuni hiyo ina mpango kabambe wa kuongeza uwekezaji hadi kufikia Shilingi bilioni 20, hatua itakayosaidia kuongeza wigo wa uzalishaji na kuchochea kwa kasi maendeleo ya kiuchumi katika Mkoa wa Kigoma na Taifa kwa ujumla.

Kadhlika, Viongozi na Wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kuu Kigoma walikiri kuridhishwa na uzalishaji wa Kiwanda hicho pamoja na miundombinu inayotumika na Watanzania wanaojipatia kipato katika shughuli mbalimbali za kuzalisha chumvi lishe ya wanyama katika kiwanda hicho cha chumvi wilayani Uvinza.

Wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha ‘Nyanza Salt Mine’, Bw. Mukesh Mamlani (aliyenyoosha mkono) wakati Viongozi hao walipotembelea Kiwanda hicho kilichopo Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa pili kushoto) akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho, Bw. Mukesh Mamlani mara baada ya Viongozi na Wajumbe wa Mahakama kuwasili katika Kiwanda cha Chumvi Uvinza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (aliyevaa kofia), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (wa kwanza kushoto), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masijala ndogo Kigoma Mhe. Fadhili Mbelwa (wa kwanza kulia) wakifanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha ‘Nyanza Salt Mine’, Bw. Mukesh Mamlani wakati Viongozi hao walipotembelea Kiwanda hicho hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya Kasulu, Mhe. Imani Batenzi,(kushoto), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa wilaya Uvinza Mhe. Misana Majula (kulia) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Buhigwe, Mhe. Mwakitalu Venance (katikati) wakisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho, Bw. Mukesh Mamlani (hayupo katika picha).


Viongozi na Wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma wakisikiliza kwa makini juu ya elimu ya uzalishaji wa chumvi kutoka kwa Ofisa Mwandamizi wa Kiwanda hicho wakati Viongozi hao walipotembelea Kiwanda cha Chumvi Uvinza hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kuu Kigoma wakipata elimu ya uzalishaji wa chumvi kutoka kwa Ofisa Mwandamizi wa Kiwanda hicho (aliyenyoosha mkono).


Picha ya mlima mdogo uliotengenezwa na ujazo wa chumvi 
iliyozalishwa tayari ili kuingia katika mitambo maalumu kwa ajili ya kuchakatwa na kuingizwa katika vifungashio na kupelekwa kwa sokoni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa sita kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (aliyesimama kushoto kwa Jaji Mfawidhi), akifuatiwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka (wa kwanza kulia) pamoja na Wajumbe wengine wa Kikao cha Uongozi walioambatana na Jaji Mfawidhi katika kutembela kiwanda hicho hivi karibuni.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)








 

 

 

 

 

 

Jumanne, 28 Julai 2026

MAHAKIMU MBEYA WAKUMBUSHWA KUZINGATIA MAADILI, WELEDI KATIKA UTOAJI HAKI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Wilaya ya Mbeya imefanya kikao kazi kilichowakutanisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo zilizopo jijini Mbeya kwa lengo la kusisitiza uimarishaji wa maadili, uwajibikaji na kuzingatia ubora wa utoaji wa huduma za Mahakama sambamba na kujadili changamoto zinazojitokeza katika ushughulikiaji wa malalamiko na uandaaji wa kumbukumbu za mashauri ya rufaa.

Kikao hicho kiliitishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba na kuwashirikisha viongozi kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, walitoa maelekezo na miongozo kadhaa ya utendaji kazi kwa Maafisa Mahakama wakiwa katika vituo vyao.

Viongozi walioshiriki kikao kazi hicho ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo aliwataka Mahakimu kuendelea kudumisha nidhamu, uadilifu na uzingatiaji wa sheria katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yao. Alisisitiza kuwa utoaji wa haki unapaswa kuongozwa na misingi ya haki, uwazi na weledi ili kulinda hadhi ya Mahakama.

“Mahakama ina jukumu la kumfuta machozi mtu aliyedhurumiwa haki zake na nasisitiza kuwa kila shauri linapaswa kushughulikiwa kwa umakini, usawa na kwa kuzingatia sheria ili kuhakikisha haki inatendeka na kuonekana kutendeka,” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, aliwahimiza Mahakimu kuendelea kuzingatia maadili ya kazi, kuwahudumia wananchi kwa weledi na kwa lugha yenye staha, pamoja na kutekeleza kwa vitendo maelekezo yanayotolewa na viongozi kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano, kuheshimiana na kujenga mahusiano mazuri mahali pa kazi. Pia aliwakumbusha Maofisa hao kutunza afya zao, akieleza kuwa afya njema ni msingi wa utendaji bora na huchangia katika kulinda na kutunza rasilimali za Mahakama na kuongeza ufanisi wa taasisi kwa ujumla.

Maofisa Mahakama katika kikao hicho, walikumbushwa umuhimu wa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, missing ya taaluma inayoongoza kazi zao na kuhakikisha kuwa majukumu yao yanatekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Pamoja na hayo, washiriki walijadili mbinu za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi ili kuongeza ufanisi na kuimarisha imani ya jamii kwa Mhimili wa Mahakama.

Aidha, Viongozi hao walisisitiza na kuhimiza Maofisa hao kuhakikisha wananchi wanapatiwa nakala za hukumu na mwenendo wa mashauri kwa wakati, matumizi sahihi ya mifumo ya TEHAMA katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama, kuzingatia mipaka ya mamlaka hayo wakati wa kusikiliza mashauri na kufuata sheria na kanuni katika utekelezaji wa tuzo na amri za Mahakama.

Mahakama ya Tanzania inaendelea kuimarisha uwezo wa watumishi wake kupitia mafunzo ya ndani na vikao vya kitaalamu vinavyolenga kuboresha utendaji kazi, kuimarisha maadili na kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki zenye ubora, kwa wakati na kwa kuzingatia misingi ya sheria na haki.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (wa pili kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo jijini Mbeya.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (wa pili kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo jijini Mbeya.

Viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa kikao hicho, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, (wa pili kulia) ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, (wa pili kushoto) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


 

MASJALA NDOGO GEITA YAFANYA KIKAO CHA MENEJIMENTI

Na. DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, amewataka watumishi wa Mahakama kuongeza ubunifu na uwajibikaji ili kuleta tija katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za utoaji haki kwa wakati.

Wito huo ametolewa wakati akifungua kikao cha Menejimenti cha Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Geita, kilichofanyika hivi karibuni, katika ukumbi wa mafunzo uliopo Kituo Jumuishi cha utoaji haki mjini Geita.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Kahyoza alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha viongozi na watumishi kukutana kwa lengo la kutathmini utendaji wa kazi wa Mahakama na kujadili mbinu bora za kuendelea kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.

Mhe. Kahyoza alisema kuwa, kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kinatoa fursa ya kutathmini utekelezaji wa majukumu, kubaini mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuongeza ufanisi katika maeneo yanayohitaji maboresho.

Alieleza kuwa, pamoja na kikao hicho kuwa sehemu ya utaratibu wa kisheria wa Mahakama, umuhimu wake unakwenda mbali zaidi ya kutekeleza matakwa ya kisheria, kwani kinatoa nafasi ya kutafakari namna ya kuifanya Mahakama iendelee kupiga hatua katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Jaji Kahyoza alisisitiza kuwa, utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama unapaswa kuzingatia maslahi mapana ya wananchi wa Mkoa wa Geita na Tanzania kwa ujumla. Alibainisha kuwa kila mtumishi anapaswa kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na viwango vya juu vya weledi.

“Ni muhimu kila mmoja wetu kutathmini tumefanikiwa kwa kiwango gani, ni maeneo yapi tunasuasua na ni hatua zipi tunapaswa kuchukua ili kuhakikisha shughuli zetu zinaendelea kufanyika kwa ufanisi zaidi,” alisema Jaji Kahyoza.

Nao, Wakuu wa vitengo pamoja na Viongozi wa Utawala kutoka Mahakama za Wilaya na Mahakama Kuu waliwasilisha taarifa za maeneo yao ya kiutendaji.

Wajumbe walipata nafasi ya kujadili taarifa mbalimbali zilizowasilishwa, huku mijadala ikijikita katika namna ya kuongeza ubunifu na tija katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama, hususan kuimarisha usikilizaji na utoaji wa maamuzi ya mashauri kwa wakati.

Miongoni mwa changamoto zilizojadiliwa ni uchakavu wa baadhi ya majengo ya Mahakama pamoja na kuwepo kwa fedha za mirathi ambazo hazijachukuliwa na wanufaika wake.

Taarifa ya Mashauri ilionesha Mahakama zote kufanya vizuri kwa kipindi cha Machi mpaka Juni 30, 2026. Mashauri ya Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, na Wilaya zote hazikuwa na shauri la mlundikano kwa mashauri yaliyofunguliwa mwaka 2025.

Pongezi pia zilienda Mahakama za Mwanzo kwa kuendelea kuondosha Mashauri kwa wakati kwani Mahakama zote zina wastani wa siku 9 wa umri wa shauri kukaa mahakamani.

Hata hivyo, kikao kilibaini kuwa bado kuna changamoto kuhusu fedha za mirathi, ambapo baadhi ya fedha hizo zimeendelea kubaki bila kuchukuliwa kutokana na kutopatikana kwa wanufaika au baadhi yao kukataa kuzichukua kwa madai kuwa kiasi kilichopo ni kidogo.

Wajumbe kutoka Mahakama za Wilaya za Chato, Geita, Bukombe, Mbogwe na Nyang'hwale walieleza kuwa changamoto hiyo imeendelea kujitokeza katika maeneo yao. Kutokana na hali hiyo, Mwenyekiti alisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za haraka ili kupata suluhisho la kudumu.   

Katika kikao hicho, wajumbe walichangia umuhimu wa kuendelea kutafuta viwanja na kuvipatia hati angalau viwanja viwili kwa kila Halmashauri. Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita Bi. Masalu Kisasila asisitiza kuwa, hatua hiyo ni muhimu katika kuwezesha upatikanaji wa miradi ya maendeleo na kulinda mali za Mahakama.

Kutokana na umuhimu wa suala hilo, Mwenyekiti wa kikao hicho alielekeza kuwa, ifikapo Septemba 30, 2026, viwanja na majengo yote ya Mahakama ambayo bado hayana hati miliki viwe vimekamilisha taratibu za umiliki.

Aidha, viongozi wa Mahakama waliagizwa kushirikiana kwa karibu na Wakurugenzi wa Halmashauri katika maeneo yao ili kutatua kwa wakati changamoto zinazohusu miundombinu pamoja na masuala mengine ya kiutendaji.

Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama na taasisi nyingine za Serikali, akieleza kuwa ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika kuhakikisha mipango ya maendeleo ya Mahakama inatekelezwa kwa ufanisi na huduma kwa wananchi zinaendelea kuimarika.

Mhe. Kahyoza alisisitiza kuwa, ubunifu, uwajibikaji, matumizi bora ya rasilimali na tathmini ya mara kwa mara ya utekelezaji wa mipango ni nguzo muhimu za kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za Mahakama. Alieleza kuwa hatua hizo zitawezesha Mahakama kuendelea kuboresha mazingira ya utendaji, kuharakisha usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (kulia) akiwa anaongoza kikao cha menejimenti Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita.

Mhasibu wa Mahakama Kuu Geita, Bw. Goodluck Machange akiwasilisha Taarifa ya utekelezaji wa Fedha.

Sehemu ya washiriki wa kikao cha menejiment Masjala Ndogo ya Geita.

Afisa Ugavi wa Mahakama Kuu Geita, Bw. Abel Bunzali akiwasilisha Taarifa ya utekelezaji wa robo ya nne ya mwaka 2025/2026.

Meza Kuu katika kikao cha menejimenti, aliyesimama ni Katibu wa kikao, Bi. Masalu kisasila, katikati ni Mwenyekiti wa Kikao, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mhe. Fredrick Lukuna.