Jumamosi, 25 Julai 2026

JAJI MKUU MASAJU ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA KUMBUKUMBU YA MASHUJAA TANZANIA

Na MARY GWERA, Mahakama - Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 25 Julai, 2026 ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania (JWTZ) Jenerali Jacob John Mkunda, Viongozi wa Serikali na Watanzania wote kwa ujumla kuadhimisha Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa nchini.

Hafla ya  Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa nchini imefanyika katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali-Mtumba jijini Dodoma huku ikitawaliwa na ratiba mbalimbali ikiwemo utoaji wa dua na sala.

Katika maadhimisho hayo, Viongozi mbalimbali pia walishiriki kutoa heshima kwa kuweka vifaa na alama za jadi kwenye Mnara wa Mashujaa wakiongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye aliweka Mkuki na Ngao kwenye Mnara wa Kumbukumbu ya Mashujaa ikiwa ni ishara ya kuwaenzi, kuwakumbuka na kuthamini mchango wa mashujaa waliopigania uhuru, amani na maendeleo ya Taifa.

Kadhalika Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Jacob John Mkunda aliweka Sime; Balozi wa Burundi nchini Tanzania, Mhe. Leontine Nzeyimana aliweka shada la maua kwa niaba ya Mabalozi, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Mhe. Alimwoni Chaula aliweka Upinde na Mshale huku Brigedia Jenerali (Mstaafu), Wilfred Paul Mwakalambile Kabunda akiweka Shoka.

Mbali na Jaji Mkuu, Viongozi wengine waliohudhuria katika Sherehe hizo ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi,  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule na wengine.

Aidha kwa upande wa Mahakama, sherehe hizo zimehudhuriwa pia na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Sam Rumanyika, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na baadhi ya Viongozi wengine.

Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania huadhimishwa tarehe 25 Julai kila mwaka lengo likiwa ni kuwakumbuka na kuwaenzi Mashujaa wote waliopoteza maisha yao wakitetea, kupigania na kulinda uhuru, amani, umoja na maslahi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Maadhimisho hayo yanaendelea kuwa chachu ya kuhamasisha uzalendo, mshikamano na uwajibikaji kwa vizazi vya sasa na vijavyo katika kulijenga Taifa la Tanzania.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa katika sherehe za Siku ya Kumbukumbu ya  Mashujaa Tanzania leo tarehe 25 Julai, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Wa pili kushoto ni  Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania (JWTZ) Jenerali Jacob John Mkunda, anayefuata ni Balozi wa Burundi nchini Tanzania, Mhe. Leontine Nzeyimana, anayefuata ni Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Mhe. Alimwoni Chaula na wa kwanza kulia ni Brigedia Jenerali (Mstaafu), Wilfred Paul Mwakalambile Kabunda.
Matukio katika picha Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Nchini leo tarehe 25 Julai, 2026 
katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiingia katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma leo tarehe 25 Julai, 2026. 


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Sam Rumanyika (wa pili kushoto) akifuatiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, akifuatiwa na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanania na Katibu wa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Venance Mlingi na Katibu Msaidizi wa Jaji Mkuu, Mhe. Wilberforce Luhwago wakiwa katika Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania leo tarehe 25 Julai, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. 

Vikosi mbalimbali vya Gwaride maalum vilivyoandaliwa kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania.

Baadhi ya Maofisa kutoka Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika sherehe za Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa Tanzania.

Picha mbalimbali za matukio ya Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa nchini leo tarehe 25 Julai, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa vilivyopo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. 

Burudani ikiendelea.

Mnara wa Mashujaa.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiondoka  katika Viwanja vya Mashujaa-Mtumba jijini Dodoma mara baada ya kukamilika kwa sherehe hizo.

                         (Picha na MARY GWERA, Mahakama)



 


 


Jumatano, 22 Julai 2026

"USULUHISHI NI NGUZO MUHIMU YA UTOAJI HAKI TANZANIA"

Na HABIBA MBARUKU – Mahakama Dar es Salaam

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amesema kuwa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya usuluhishi na upatanishi, unapaswa kutambuliwa kama sehemu muhimu ya mfumo wa utoaji haki nchini.

Mhe. Siyani ameyasema hayo leo tarehe 22 Julai, 2026, katika hotuba  aliyoisoma kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) ya mwaka 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Delta jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaielekeza Mahakama kukuza na kuimarisha utatuzi wa migogoro miongoni mwa wahusika wa migogoro kama ilivyofafanuliwa katika Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo usuluhishi na upatanishi unapaswa kutazamwa kama mwendelezo wa jukumu la Mahakama katika utoaji wa haki ndani ya mfumo wa utawala wa sheria.

"Jukumu la utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limekasimiwa kwa Mahakama. Hata hivyo, mamlaka hiyo haiwazuii wahusika wa mgogoro kutafuta haki kwa njia nyingine walizokubaliana, kama inavyoainishwa katika Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inaielekeza Mahakama kukuza na kuimarisha utatuzi wa migogoro miongoni mwa watu wanaohusika katika migogoro hiyo,” amesisitiza Mhe. Siyani.

Amesema mifumo ya jadi ya utatuzi wa migogoro iliyokuwepo kabla ya ukoloni, iliyojengwa katika misingi ya maridhiano na maelewano, bado ina mchango mkubwa katika maendeleo ya mifumo ya kisasa ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya Usuluhishi, huku akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha mifumo hiyo inaendana na mazingira ya Tanzania na inayokidhi viwango vya kimataifa.

"Uhalali wa mfumo wowote wa utatuzi wa migogoro hautegemei tu uhalali wake wa kisheria, bali pia kukubalika kwake na jamii pamoja na kuendana kwake na mila na utamaduni wa wananchi. Kwa hiyo, mustakabali wa mifumo ya Usuluhishi/upatanishi nchini Tanzania unapaswa kuwa shirikishi, ukichota mema kutoka katika mila na desturi mbalimbali huku ukizingatia misingi ya haki, kutopendelea upande wowote na utawala wa sheria,” amesema Jaji Kiongozi.

Aidha, ameeleza kuwa, usuluhishi na upatanishi havipaswi kuonekana kama njia zinazotumika pale Mahakama zinapokuwa na mlundikano wa mashauri, bali ni miongoni mwa njia kamili za utoaji haki zilizoidhinishwa na Katiba na Sheria za nchi, zenye uwezo wa kusaidia upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Amebainisha kuwa, katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kushuhudia ongezeko la uwekezaji katika miundombinu, Sekta ya Nishati, rasilimali asilia na biashara za kimataifa, mifumo ya Usuluhishi na Upatanishi ina nafasi muhimu katika kushughulikia migogoro yenye thamani kubwa na masuala ya kitaalamu kwa ufanisi, kuongeza uhakika wa mazingira ya biashara na kuimarisha imani ya wawekezaji.

Mhe. Siyani ameeleza kuwa, pamoja na uhuru wa mchakato wa usuluhishi, Mahakama inaendelea kuwa na jukumu la kuhakikisha taratibu za usuluhishi zinafuatwa, tuzo za usuluhishi zinatekelezwa, maslahi ya umma yanalindwa na mfumo wa sheria unabaki kuwa thabiti kwa kuwa Mahakama na usuluhishi ni mifumo inayokamilishana katika kufanikisha utoaji haki.

Aidha, amewataka Wadau wa Sekta ya Sheria kuendelea kuimarisha uwezo wa kitaaluma, kutumia teknolojia katika uendeshaji wa mashauri ya usuluhishi, kuendeleza utaalamu katika sekta mbalimbali na kuoanisha mifumo ya ADR na viwango vya kimataifa ili kuiwezesha Tanzania kujijengea nafasi kama kitovu cha usuluhishi kimataifa.

Pamoja na hayo, Jaji Kiongozi amewahimiza washiriki kutumia mkutano huo kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza matumizi ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala nchini.

Katika hatua nyingine Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari, ametaja hatua mbalimbali zinazofanywa na Ofisi hiyo huku akisisitiza kuwa haki inapaswa kupatikana mapema ipasavyo.

Pamoja na hayo, amewataka kuzingatia R4 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambazo ni Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Kujenga Upya.

Kwa upande wake Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) Wakili Aderickson Njunwa, ameeleza kuwa, Taasisi hiyo iliyoanzishwa mwaka 1997, imebeba dhima kubwa ya kuisaidia jamii kutatua migogoro kwa njia ya upatanishi, kadhalika kukuza uwekezaji na kuimarisha uchumi endelevu.

Wakili Njunwa amefafanua kuwa miongoni mwa majukumu mengine ya (TIArb) ni kuhakikisha kuwa jamii ya Tanzania inapata elimu kuhusu maana ya usuluhishi na umuhimu wake kwa maendeleo endelevu pamoja na kuendeleza uwajibikaji kwa kujengeana uwezo na majukumu ya kitaasisi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akifungua Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026 kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju uliofanyika leo tarehe 22 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Delta jijini Dar es Salaam.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria katika ufunguzi wa mkutano huo wakifuatilia kinachojiri.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja. Wa pili kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari, wa pili kushoto ni Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Aderickson Njunwa, wa kwanza kushoto ni Makamu wa Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Usaje Mwambene na wa kwanza kulia ni Meneja wa Uwekezaji wa Taasisi hiyo, Bw. Daudi Riganda.

Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Aderickson Njunwa akizungumza kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya  Delta jijini Dar es Salaam.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.







Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha za pamoja na Wadau mbalimbali walioshiriki katika ufunguzi wa Mkutano huo.

 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

MAHAKAMA MANYARA YAENDELEA KUTOA MAFUNZO KWA WANAFUNZI TASNIA YA WANYAMAPORI

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara kupitia Mahakama ya Wilaya ya Babati imeendelea kuwapokea Wanafunzi wa vyuo mbalimbali vya Usimamizi wa Wanyamapori ikiwa ni pamoja na wanafunzi kutoka Chuo cha Wanyamapori Pasiansi cha jijini Mwanza waliofika mahakamani hapo kwa ajili ya mafunzo ya uendeshaji wa mashauri yanayohusu Wanyamapori.

Katika mafunzo hayo, jumla ya wanafunzi 149 kutoka Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi kutoka Mwanza wakiwa wameambatana na walimu wao watatu (3) wamefika kwa lengo la kujifunza taratibu za kisheria na masuala mbalimbali yanayotokea mahakamani kwa njia ya Mahakama mtandao ili njia hizo iweze kuwasaidia katika masomo wanayojifunza chuoni.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Charles Mnzava, aliwasihi wanafunzi hao kuzingatia yale yote ambayo watafundishwa na wataalamu wa masuala ya kisheria ili yaweze kuwasaidia katika masomo yao chuoni na hata katika maisha baada ya chuo pale ambapo watakuwa wameajiriwa au kujiajiri katika maeneo mbalimbali.

“Chuoni mnasoma zaidi kwa nadharia, nawapongeza kwa kuja leo na kushuhudia namna mashauri haya yanayohusu wanyamapori na nyara za Serikali yanavyoendeshwa Mahakamani. Mafunzo haya yataongeza tija na uelewa wenu zaidi katika hayo mnayojifunza chuoni na hata baadae mtakapokuwa katika ajira zenu.” alisema Mhe. Mnzava.

“Pamoja na hayo tunawapongeza kwa kuchagua Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya kupata mafunzo haya. Kwetu Mahakama ni furaha kubwa sana kuweza kuunganisha Taasisi mbili kama mlivyokuja jana na leo kwa ajili ya mafunzo haya ya kimahakama na hususan namna ya uendeshaji na usikilizaji wa mashauri yanayohusu wanyamapori,” ameongeza Mhe. Mnzava

Katika hatua nyingine, Mhe Mnzava alitumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi hao juu ya Muundo wa Mahakama ya Tanzania ulivyo. “Mahakama zetu hapa nchini, kuanzia Mahakama ya Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu Pamoja na Mahakama ya Rufaa zina taratibu zake za usikilizwaji wa mashauri kulingana na uzito wa mashauri husika hivyo ni vema mkafahamu kuwa hata haya mashauri ya Wanyamapori mathalani hayawezi kusikilizwa katika ngazi za Mahakama za Mwanzo”.

Aidha, wanafunzi wa Taasisi hizo waliweza kuhoji na kujibiwa maswali mbalimbali kwa wawezeshaji wa Mafunzo hayo ambao walikuwa ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Joseph Kimaro pamoja na Mahakimu Wakazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao na Mhe. Jumaa Mwambago.

Akishukuru baada ya mafunzo hayo Mwakilishi wa Walimu waliombatana na wanafunzi hao kutoka Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi Mwalimu Hamisi Philimon Matinde, alishukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kuwapokea vema na kuwapa Elimu waliyokuwa wakiihitaj.

“Tunashukuru sana Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kutupokea na kwa ushirikiano mliotupa, tuaamini kuwa elimu hii itatusaidia sana na tutaendelea kuja hapa kwa ajili ya mafunzo mengine,” alisema Mwalimu Matinde.

Utaratibu wa kutoa Elimu, unaendelea kufanyika kwa kuwawezesha wanafunzi na wanataaluma mbalimbali kutoka Taasisi za Elimu kujifunza masuala mbalimbali kama walivyofanya Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi Mwanza.

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakiwa katika picha ya Pamoja na walimu wao na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara mbele ya jengo la Mahakama Kuu Manyara.

Mahakimu Wakazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao (aliyesimama kushoto) na Mhe. Jumaa Mwambago wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yanatolewa kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi.

Wanafunzi wa Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi wakiwa katika picha ya Pamoja na walimu wao na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara mbele ya jengo la Mahakama Kuu Manyara.

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza wakifuatilia mada ambazo zilikuwa zinatolewa katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza wakifuatilia mada ambazo zilikuwa zinatolewa katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.




Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava (wa kwanza kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victo Kimario wakiendelea kutoa Elimu kwa wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza (hawapo pichani) walipofika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kupata mafunzo.


Jumanne, 21 Julai 2026

WANAFUNZI MWEKA WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO MAHAKAMA YA WILAYA YA BABATI

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka kilichopo Moshi mkoani Kilimanjaro wamefanya ziara ya kujifunza taratibu mbalimbali za kimahakama katika katika uendeshaji wa mashauri yanayohusu uendeshaji wa mashauri yanayohusu wanyamapori.

Mafunzo hayo yanaendeshwa katika ukumbi namba Tatu wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara ambao unatumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Babati katika kuendesha shughuli za Mahakama.

Katika ziara hiyo, jumla ya wanafunzi Hamsini na nane (58) kutoka Chuo hicho waliambatana na walimu wao wanne (4) kwa lengo la kujifunza taratibu na masuala mbalimbali yanayotokea mahakamani kwa njia ya vitendo mtandao ili ziweze kuwasaidia katika elimu yao wanayojifunza chuoni.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava, aliwasihi wanafunzi hao kuzingatia yale yote ambayo watafundishwa na wataalamu wa masuala ya kisheria ili yaweze kuwasaidia katika masomo yao ya chuoni na hata katika maisha ya baada ya chuo pale ambapo watakuwa wameajiriwa au kujiajiri katika maeneo mbalimbali.

“Chuoni mnasoma zaidi kwa nadharia, nawapongeza kwa kuja leo na kushuhudia namna mashauri haya yanayohusu wanyamapori na nyara za Serikali yanavyoendeshwa mahakamani. Mafunzo haya yatawaongeza tija na uelewa wenu zaidi katika hayo mnayojifunza chuoni na hata baadae mtakapokuwa katika ajira zenu” alisema Mhe. Mnzava.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mnzava alitumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi hao juu ya Muundo wa Mahakama Tanzania ulivyo. “Mahakama zetu hapa nchini, kuanzia Mahakama ya Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu Pamoja na Mahakama ya Rufani zina taratibu zake za usikilizwaji wa mashauri kulingana na uzito wa mashauri husika hivyo ni vema mkafahamu kuwa hata haya mashauri ya Wanyamapori mathalani hayawezi kusikilizwa katika ngazi za Mahakama za Mwanzo”.

Aidha, wanafunzi wa chuo hicho cha Mweka waliweza kuhoji na kujibiwa maswali mbalimbali kwa wawezeshaji wa Mafunzo hayo ambao walikuwa ambaye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati, Mhe. Victor Joseph Kimaro pamoja na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo Mhe. Martin Massao.

Akishukuru baada ya mafunzo hayo Mwakilishi wa Walimu waliombatana na wanafunzi hao Mwalimu Melckezedeck Tarimo alishukuru uongozi wa Mahakama Kuu Manyara kwa kuwapokea vema na kuwapa Elimu waliyokuwa wakiihitaji.

“Tunashukuru sana Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kutupokea na kwa ushirikiano mliotupa, tuaamini kuwa elimu hii itatusaidia sana na tutaendelea kuja hapa kwa ajili ya mafunzo mengine,” alisema Mwalimu Tarimo.

Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara imeendelea na utaratibu wa kutoa elimu kwa wananchi wanaofika mahakamani kila wakati lakini pia kwa kupitia vyombo vya Habari vilivyopo hapa mkoani kwa lengo la kutimiza mahusiano bora kati ya Mahakama na wadau wanaosaidia utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Mahakama.

Walimu na wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara walipohudhuria mafunzo katika Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Sehemu ya wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakaifuatilia mada zilizokuwa zinafundishwa wakati wa mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wao kutoka kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Mmoja wa wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka akichangia mada wakati wa mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wao kutoka kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Walimu wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka (waliosimama) wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wao kutoka kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao akiendelea na mafunzo kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka waliofika katika Mahakama ya Wilaya ya Babati kwa ajili ya Mafunzo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Kimario (mwenye suti ya rangi ya buluu) akiendelea na mafunzo kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka waliofika katika Mahakama ya Wilaya ya Babati kwa ajili ya Mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava (aliyevaa suti nyeusi) akitoa Neno la Ukaribisho kwa Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka waliofika katika Mahakama ya Wilaya ya Babati kwa ajili ya Mafunzo.