Jumatatu, 9 Machi 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA, ZANZIBAR WAANZA MAFUNZO YA KUBADILISHANA UZOEFU DODOMA

  • Washiriki watakiwa kuimarisha maadili, matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa mashauri

Na HALIMA MNETE & JAMES BUSANYA-Mahakama, Dodoma.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, leo tarehe 9 Machi 2026 amefungua mafunzo ya kubadilishana uzoefu kati ya Maofisa wa Mahakama ya Tanzania na wenzao kutoka Mahkama ya Zanzibar, yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo mbele ya washiriki kutoka Zanzibar wakiongozwa na Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim, Mhe. Tengwa alisema mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kimfumo kati ya Taasisi hizo mbili katika kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.

Alisema Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Zanzibar zimeona umuhimu wa kuendelea kubadilishana uzoefu ili kuimarisha weledi, uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa Mahakama, hali itakayosaidia kuongeza imani ya wananchi kwa Mhimili wa utoaji haki.

“Nawapongeza washiriki wote kutoka Zanzibar kwa kufika Dodoma salama. Mafunzo haya ni fursa muhimu ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uwezo wetu katika utoaji wa huduma bora za Mahakama,” alisema Mhe. Tengwa.

Aliongeza kuwa uchaguzi wa Dodoma kama eneo la kufanyia mafunzo hayo umezingatia mazingira yake tulivu yanayofaa kwa kujifunza na kujadiliana masuala muhimu yanayolenga kuboresha utendaji wa Mahakama.

Katika hotuba yake, alieleza kuwa mafunzo hayo yatajadili mada mbalimbali muhimu ikiwemo ukaguzi wa shughuli za Mahakama, utekelezaji wa majukumu ya msingi, maboresho ya huduma za Mahakama, maadili na namna ya kushughulikia malalamiko ya kimaadili, usimamizi wa mashauri, matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano katika usimamizi wa mashauri pamoja na kuharakisha umalizaji wa mashauri.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usawa wa kijinsia katika utoaji wa huduma za Mahakama, akieleza kuwa Mahakama inapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha haki na usawa vinazingatiwa kwa vitendo katika jamii.

Mhe. Tengwa alinukuu kauli ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin William Mkapa, aliyewahi kusema kuwa mtu hawezi kujua kama mama yake ni mpishi mzuri hadi pale atakapoonja chakula kilichopikwa na mama mwingine, akieleza kuwa mfano huo unaonesha umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wengine.

Alisema kuwa kupitia mafunzo hayo washiriki wanatarajiwa kuwa mabalozi wa kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa wakati, kuboresha huduma za Mahakama kupitia ukaguzi pamoja na kuimarisha maadili na usawa wa kijinsia katika utendaji wao.

Mafunzo hayo ya siku tano yatahitimishwa tarehe 13 Machi, 2026, yakilenga kuongeza ufanisi katika usimamizi na utoaji wa haki kwa wananchi.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, akizungumza wakatia anafungua mafunzo hayo. Picha chini ni washiriki wa mafunzo yanayofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

WATUMISHI SUMBAWANGA WAPATIWA MAFUNZO KUHUSU MAFAO & KUSTAAFU

Na. Sharifu Mokiwa - Mahakama, Sumbawanga

Watumishi  wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wamepata mafunzo maalumu kuhusu mafao na maandalizi ya kuustaafu ambayo yalitolewa kwa njia mbili yaani uso kwa uso kwa waliokuwepo ukumbini na kwa njia ya Mtandao kwa waliokuwa  mbali.

Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 6 Machi 2026, katika ukumbi wa Mahakama Kuu  Sumbawanga na yalifunguliwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu  Sumbawanga  Bw. Machumu Essaba, kabla ya kuanza kuwasilishwa kwa mada na Afisa  kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi (PSSF) Bw. Eribariki Nsulau

Akizungumza wakati wa kuwasilisha mada Bw. Nsulau alitoa elimu kuhusu huduma na mafao yanayo tolewa na PSS, alifafanua jinsi ya kujisajili kwenye portal ya PSSF kuangalia michango, kuandikisha michango mipya, nakupata mafao mbalimbali, mafao hayo ni pamoja na fao la mishahara miwili endapo mfanyakazi atapoteza ajira ,fao la uzazi ndani ya siku 90 na malipo ya pensheni kuanzia tarehe 21- 23 au 21-25 ya mwezi, yanayolipwa pia kwa wategemezi wa mstaafu. Mafunzo hayo pia yalisisitiza umuhimu wa uhakiki wa kila mwaka kwa wastaafu na wategemezi ili malipo ya pensheni yaendelee bila usumbufu.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu Sumbawanga, Mhe. Abubakari Mrisha alitoa mwongozo wa kitaalamu kuhusu maandalizi ya kustaafu na alisisitiza kuwa maandalizi ya kustaafu yanapaswa kuanza mapema mara tu mtumishi anapopata cheki namba, kwani namba hiyo inaonesha muda unaotarajiwa wa kustaafu.

Alieleza kuwa ni muhimu kwa watumishi kupanga maisha yao ya baadae  mapema ili kuepuka changamoto pindi wanapo staafu.

Aidha, watumishi walipata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusu mafao, pensheni, mirathi, na namna ya kujiandaa kustaafu ambapo, mafunzo hayo yamewasaidia kuongeza uelewa na uwajibikaji wa watumishi katika kupanga mustakabali wao wa kifedha, huku wakiongezwa ujuzi muhimu kuhusu hifadhi ya jamii na usimamizi wa michango.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda, Sumbawanga Bw. Machumu Essaba akifungua rasmi mafunzo kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu kwa watumishi wa Mahakama tarehe 6 Machi, 2026.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda, Sumbawanga Mhe. Abubakari Mrisha (aliyenyanyua mkono) akisisitiza umuhimu wa maandalizi mapema ya kustaafu kwa watumishi wa Mahakama Sumbawanga.

Hakimu Mkazi Mhe. Willington Rwabinyasi akiuliza swali kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu wakati wa mafunzo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Sumbawanga wakisikiliza mafunzo kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu.

Afisa kutoka PSSF Bw. Elibariki Nsulau akipokea maswali kwa kuyaandika kutoka kwa watumishi wa Mahakama ya Sumbawanga kuhusu mafao na maandalizi ya kustaafu

Afisa kutoka PSSSF Bw. Elibariki Nsulau (aliyesimama) akieleza jinsi ya kujisajili, kuangalia michango nakufahamu mafao kupitia portal ya PSSF.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




MAHAKAMA KUU KANDA YA MOROGORO YAWAFARIJI WANAWAKE WA GEREZA LA KINGOLWIRA

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, imeungana na wanawake wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kwa kufanya ziara ya kijamii katika Gereza Kuu la Wanawake Kingolwira.

Maadhimisho hayo  ambayo hufanyika tarehe 8 Machi kila mwaka yalianza kwa watumishi wa Mahakama Kuu kushiriki pamoja na wanawake wengine katika siku hiyo muhimu inayolenga kutambua mchango wa wanawake katika jamii.

Maadhimisho hayo yalibeba na kauli mbiu inayosema, “Haki kwa wanawake na wasichana msingi wa maendeleo jumuishi kufikia dirĂ¡ 2050.”

Baada ya kushiriki katika maadhimisho hayo, watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro walifanya ziara maalum ya kutembelea Gereza la Wanawake Kingolwira lililopo mkoani Morogoro.

Ziara hiyo iliongozwa na Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage, ikiwa na lengo la kuwafariji wanawake waliopo gerezani hapo pamoja na kutoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia katika maisha yao ya kila siku wakiwa gerezani.

Watumishi hao walipata fursa ya kujumuika na wanawake waliopo gerezani hapo, kushirikiana nao katika mazungumzo ya faraja pamoja na kuonesha upendo na mshikamano kama sehemu ya kuadhimisha siku hiyo ya wanawake duniani.

Ziara hiyo pia ilikuwa na lengo la kuwapa moyo na matumaini wanawake hao kuwa bado wana nafasi ya kujifunza, kujirekebisha na kuendelea na maisha baada ya kumaliza vifungo vyao.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza ambaye pia ni Mkuu wa Gereza la Wanawake Kingolwira, Afande Nimwindael Mzirai, aliwashukuru watumishi wa Mahakama kwa moyo wao wa kujali na kuwafikia wanawake waliopo gerezani.

Alisema kuwa ujio huo umeleta faraja kubwa kwa wafungwa hao na umeonesha mshikamano wa kijamii kwa wanawake wote bila kujali hali walizonazo.

Aidha, alitoa wito kwa watumishi wa umma pamoja na wananchi kwa ujumla kuendelea kuheshimu sheria za nchi na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kusababisha kuvunja sheria na hatimaye kujikuta wakitumikia vifungo gerezani.

Aliongeza kuwa gereza hilo pia ni sehemu ya kujifunza na kujenga upya maisha, ambapo wanawake waliopo hapo hupatiwa mafunzo mbalimbali ya stadi za maisha kama vile kilimo, ushonaji wa cherehani pamoja na shughuli nyingine za uzalishaji ili kuwa na ujuzi utakaowasaidia wanaporejea katika jamii.

 Akizungumza wakati wa kuhitimisha ziara hiyo, Mhe. Kinyage aliwahimiza wanawake waliopo gerezani kuwa na uvumilivu, nidhamu pamoja na matumaini katika kipindi chote cha kifungo chao. Aliwaasa kutumia muda wao wakiwa gerezani kujifunza mambo yatakayowasaidia kujenga maisha mapya pindi watakapomaliza vifungo vyao.

“Msijisikie wanyonge kwa kuwa hapa, kwani kila changamoto ina mwisho wake. Muhimu ni kujifunza, kuwa na nidhamu na kujiandaa kwa maisha bora baada ya kutoka hapa,” alisema Mhe.Kinyage

Maadhimisho hayo pamoja na ziara hiyo yameonesha mshikamano, upendo na kujali kwa watumishi wa Mahakama kwa wanawake wote katika jamii, ikiwemo wale waliopo katika mazingira ya kifungo, huku yakilenga kuhamasisha matumaini, marekebisho na mshikamano wa kijamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim, akiwasalimia wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake yakiyofanyika kimkoa Morogoro.

Watumishi wanawake wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakifanya maandamano katika serehe hiyo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakiwa katika Gereza Kuu la Wanawake Kingolwira.

Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage akikabidhi baadhi ya vifaa kwa Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza ambaye pia ni Mkuu wa Gereza la Wanawake Kingolwira, Afande Nimwindael Mzirai.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

  

WATUMISHI WANAWAKE MAHAKAMA YA TANZANIA WAHIMIZWA KUENDELEZA UADILIFU NA KUKUZA USAWA WA KIJINSIA

       Ni katika Hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama-Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani

   Jaji Masabo awahimiza pia kujiendeleza kimasomo 

Na HALIMA MNETE & HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Wanawake watumishi wa Mahakama ya Tanzania wamehimizwa kuendelea kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao sambamba na kuendeleza juhudi za kukuza usawa wa kijinsia katika Mhimili huo.

Wito huo umetolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe.Dkt. Juliana Masabo ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya Watumishi wanawake wa Mahakama ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika tarehe 08 Machi 2026 kwenye Ukumbi wa Cathedral jijini Dodoma, jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa kufungua hafla hiyo, Mhe. Dkt. Masabo aliwashukuru wanawake wote waliojitokeza kushiriki maadhimisho hayo, huku akibainisha kuwa, ushiriki wao unaonesha dhamira ya dhati ya wanawake wa Mahakama katika kuimarisha mchango wao katika utoaji wa haki kwa jamii.

Alisema Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, ambayo yalianza kuadhimishwa mwaka 1911, yanalenga kuikumbusha jamii kuhusu nafasi, haki na mchango wa mwanamke katika maendeleo ya jamii.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Jaji Masabo, kuna jumla ya watumishi wanawake 342 katika Makao Makuu ya Mahakama, Mahakama ya Rufani, Masjala Kuu, Divisheni za Mahakama Kuu pamoja na Mahakama Kuu Dodoma (IJC) wanaofanya kazi katika nafasi mbalimbali ikiwemo Majaji, Naibu Wasajili, Wakurugenzi, Mahakimu, Wasaidizi wa Sheria wa Majaji, Wakuu wa Vitengo pamoja na kada nyingine za utumishi.

Aidha, ilielezwa kuwa, katika Mhimili wa Mahakama kuna maendeleo yanayoonekana katika usawa wa kijinsia kwenye nafasi za uongozi ambapo takwimu zinaonesha, kwamba kati ya Majaji 39 wa Mahakama ya Rufani, Wanawake ni 13 sawa na asilimia 33, huku katika Majaji 104 wa Mahakama Kuu wanawake wakiwa 40 sawa na asilimia 38.

Kadhalika, kati ya Naibu Wasajili 82 waliopo wanawake ni 42 sawa na asilimia 51, jambo linaloonesha ongezeko la ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi ndani ya Mhimili huo.

Katika hafla hiyo, Watumishi wanawake wa Mahakama walipongezwa pia kwa kushiriki matendo ya huruma kwa kutembelea watoto wenye mahitaji maalum katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma, ambapo walitoa msaada wa mahitaji mbalimbali pamoja na kugharamia matibabu ya mtoto mchanga aliyekuwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

Akizungumzia, Maadhimisho ya mwaka huu, Mhe. Dkt. Masabo alisema Kaulimbiu ya mwaka 2026 inayosema, “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050” inapaswa kuwa chachu kwa wanawake kujitathmini namna wanavyotekeleza wajibu wao katika kuhakikisha haki na usawa vinazingatiwa katika utoaji wa huduma za haki.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo aliwahimiza wanawake kuendelea kupendana, kusaidiana na kuinuana ili kuwa daraja la mafanikio kwa wanawake wengine, huku akitoa wito kwa Menejimenti ya Mahakama kuendelea kuwaamini na kuwapa fursa zaidi za uongozi na maendeleo ya kitaaluma.

Aidha, kupitia maadhimisho hayo washiriki walipata fursa ya kupata ushauri kutoka kwa Mkufunzi katika Masuala ya Afya ya Akili kutoka Hospitali ya Taifa-Muhimbili, Dkt. Garvin Kweka kuhusu umuhimu wa usawazishaji wa majukumu ya kazi na familia (work-life balance), elimu inayolenga kuwasaidia wanawake kuboresha afya ya akili, kuimarisha utendaji kazi kazini pamoja na kuendeleza ustawi wa familia.

Watumishi wanawake walioshiriki katika sherehe hiyo ni kutoka Makao Makuu ya Mahakama, Mahakama ya Rufani, Masjala Kuu, Divisheni za Mahakama Kuu pamoja na Mahakama Kuu Dodoma (IJC).

Matukio katika picha Hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama-Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe.Dkt. Juliana Masabo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma katika hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama katika kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Irene Msokwa na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mwajabu Mvungi.

Sehemu ya Watumishi wanawake wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika hafla ya Usiku wa Wanawake wa Mahakama kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani jana tarehe 08 Machi, 2026 kwenye Ukumbi wa Cathedral uliopo jijini Dodoma.

Burudani ikiendelea...
Wanawake wakionesha vipaji vyao katika Siku yao muhimu.

Muda wa Dua ukawadia.

 Kamati ya Maandalizi katika ubora wake.


Ukataji keki maalum zilizoandaliwa kwa ajili ya kusherehekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi, 2026.

Masuala ya Afya ya Akili kutoka Hospitali ya Taifa-Muhimbili, Dkt. Garvin Kweka akitoa mada kwa watumishi wanawake wa Mahakama ya Tanzania walioshiriki katika Usiku wa Wanawake wa Mahakama-Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

MAWAKILI MKOA WA MWANZA WALA KICHAPO GEITA

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita imeibuka na ushindi wa mabao 3–2 dhidi ya Timu ya Mawakili kutoka Mwanza katika mchezo wa kirafiki uliochezwa Machi 7, 2026.

Mchezo huo ulifanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari St. Aloysius vilivyopo Shilabela, Manispaa ya Geita, ambapo timu hizo zilionyesha ushindani mkubwa na burudani kwa mashabiki waliohudhuria.

Katika mchezo huo, bao la kwanza la Mahakama Kuu Geita lilifungwa na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Nyang’hwale, Robert Nyando. Bao la pili lilifungwa na Ateba Stephano huku bao la tatu likifungwa na Mhasibu wa Mahakama Kuu Geita, Goodluck Machange.

Kwa upande wa Timu ya Mawakili Mwanza, bao la kwanza lilifungwa kwa njia ya penalti na Wakili Fredrick Magaiwa baada ya mlinda mlango wa Mahakama Kuu Geita kushika mpira ndani ya eneo la hatari. Bao la pili lilifungwa na Wakili Hensen Emmanuel.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Jaji wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Geita, Griffin Mwakapeje, kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, aliwakaribisha wageni hao katika Mahakama Kuu Geita na kuwashukuru kwa kushiriki mchezo huo.

Alisema lengo la michezo hiyo ni kuimarisha mahusiano, ushirikiano na kubadilishana mawazo kati ya Wadau wa sekta ya sheria.

“Nia ya mashindano haya ni kutuleta pamoja, tusahau kwa muda majukumu ya kesi na kujumuika katika kujenga ushirikiano pamoja na kubadilishana mawazo. Pia inaonyesha kuwa licha ya majukumu mengi ya kisheria tuliyonayo, bado tunashiriki kikamilifu katika michezo,” alisema Jaji Mwakapeje.

Aidha, alimshukuru Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Fredrick Lukuna, kwa kuratibu na kufanikisha mashindano hayo. Aliongeza kuwa baada ya ujio wa Mawakili wa Mwanza mjini Geita, watumishi wa Mahakama Kuu Geita pia watafanya ziara ya kwenda Mwanza kwa ajili ya michezo kama sehemu ya kuimarisha ushirikiano huo.

Aliwasihi Mawakili wa Mwanza kuangalia uwezekano wa kusaidia Mkoa wa Geita kupata chapter yake ya Chama cha Mawakili ili kuimarisha shughuli za kisheria na ushirikiano katika ukanda huo.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Mawakili (Mwanza Chapter) aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Geita kwa kukubali mwaliko na kushiriki mchezo huo.

Alisema licha ya timu yao kupoteza, wamefurahishwa na kiwango cha wachezaji wao na wameuchukulia mchezo huo kama fursa ya kuimarisha timu yao pamoja na afya za Mawakili.

Aliongeza kuwa hatua za Mkoa wa Geita kuwa na chapter yake ya Chama cha Mawakili zinaendelea vizuri, huku akiwakaribisha watumishi wa Mahakama Kuu Geita kutembelea Mwanza kwa ajili ya mchezo mwingine wa kirafiki siku zijazo.

Wachezaji wa Timu ya Mahakama na Mawakili Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kuanza.

Wachezaji wa kikosi cha kwanza kutoka katika Timu ya Mawakili wa Serikali na Kujitegemea Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kuanza.

Wachezaji wa kikosi cha kwanza  kutoka timu ya Mahakama Kuu Kanda ya Geita wakiwa katika picha ya pamoja.

Mchuano ukiwa unaendelea, William Msuya wa Mahakama ya Mwanzo Kharumwa akijaribu kumpokonya mpira Wakili wa Serikali Mwanza.

Wachezaji na Mashabiki wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Griffin Mwakapeje (wa katikati msitari wa kwanza) na Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Fredrick Lukuna wa tatu kushoto mistari wa kwanza).
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 


 

WAFANYAKAZI WANAWAKE WA MAHAKAMA YA TANZANIA WAWAGUSA WATOTO NJITI BENJAMIN MKAPA

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma

Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, watumishi Wanawake wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma tarehe 06 Machi, 2026 walitembelea watoto njiti (premature) wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Watoto hao ni wale waliozaliwa kabla ya wakati na waliokuwa wakipatiwa huduma hospitalini hapo wakiwa na umri wa kuanzia siku moja hadi siku 28 tangu kuzaliwa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Afisa Rasilimali Watu Mwandamizi wa Mahakama, Bi. Gladness Godwin Massawe alisema lengo la wanawake kutembelea Hospitali hiyo ni kujionea hali ya watoto hao pamoja na kutambua umuhimu wao katika jamii.

Alisema katika kuadhimisha siku hiyo waliamua kushiriki katika tendo la kijamii kwa kuwatembelea watoto hao na kuwapatia baadhi ya mahitaji muhimu pamoja na kugharamia matibabu ya mtoto mmoja aliyekuwa akipatiwa huduma katika Chumba cha Uangalizi Maalum (ICU).

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya kuonesha upendo, mshikamano na kuwapa matumaini watoto hao pamoja na familia zao.

Wakati huohuo akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo kwa niaba ya Uongozi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto, Dkt. Rehema Yona alishukuru kwa msaada huo.

"Msaada huu umeleta faraja na matumaini kwa watoto pamoja na wazazi wao na umeonesha moyo wa upendo na kujali jamii," alisema Dkt. Rehema huku akiwatakia heri na baraka kwa kuendelea kushirikiana na jamii katika kusaidia wenye uhitaji.

 Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuwasili katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma tarehe 06 Machi, 2026. 

Watumishi wanawake wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania wakielekea wodini kuona watoto katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH).

 

    Afisa Rasilimaliwatu Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Gladness Massawe akizungumza jambo mara baada ya kupokelewa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa.


    Afisa Rasilimaliwatu Mwandamizi wa Mahakama, Bi Gladness Massawe (wa pili kushoto) akikabidhi zawadi kwa  Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa watoto wa Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Dkt. Rehema Yona mara baada ya kuwasili katika hospitali hiyo.

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dkt. Rehema Yona akitoa shukrani mara baada ya kupokea wageni hao.





Sehemu ya watumishi wanawake kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania walioshiriki katika zoezi la utoaji msaada kwa watoto njiti waliopo Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka tarehe 08 Machi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)