Ijumaa, 10 Aprili 2026

KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI DODOMA CHAFANYIKA

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma za haki, akibainisha kuwa misingi hiyo ni nguzo kuu ya utendaji wa Mahakama nchini.

Mhe. Hassan ameyasema hayo leo tarehe 10 Aprili, 2026, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dodoma uliofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi.

Amesema kuwa kila mfanyakazi wa Mahakama ana nafasi muhimu katika kutekeleza jukumu la kikatiba la utoaji haki, akirejea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inayoweka wajibu wa kuhakikisha Wananchi wanapata haki bila ubaguzi.

Aidha, ameipongeza Menejimenti ya Mahakama kwa kuendelea kutekeleza matakwa ya kisheria ya uendeshaji wa mabaraza ya wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na Tamko Na. 1 la mwaka 1970 na kanuni mbalimbali za utumishi wa umma zinazolenga kuwashirikisha katika maamuzi ya kiutendaji.

Jaji huyo amesisitiza kuwa mabaraza ya wafanyakazi yana jukumu la kuishauri Serikali kuhusu usimamizi wa rasilimaliwatu, kuboresha mazingira ya kazi, kulinda haki na wajibu wa Mwajiri na Mwajiriwa pamoja na kuimarisha ustawi wa Watumishi mahali pa kazi.

Amepongeza Wafanyakazi wa Mahakama kwa mchango wao katika utoaji wa haki na kutambua Wafanyakazi hodari wa mwaka 2026, akisema hatua hiyo ni chachu ya kuongeza ari ya utendaji kazi.

Kuhusu maadili, amesisitiza kuwa Watumishi wa Mahakama wanapaswa kuzingatia kanuni za maadili ya utumishi wa umma ili kuhakikisha utoaji wa huduma bora, akibainisha kuwa Mahakama ni chombo kinachobeba dhamana ya haki kwa Wananchi wote bila kujali hali, jinsia, dini au rangi.

Ameeleza kuwa Dira ya Mahakama ni kuhakikisha haki inapatikana kwa wote kwa wakati, akirejea misingi ya kikatiba inayolenga kulinda amani, usalama, maadili na umoja wa kitaifa.

Katika kuimarisha utendaji kazi, Jaji huyo amesisitiza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), akibainisha kuwa Mahakama inaelekea katika mfumo wa Mahakama Mtandao (e-Judiciary) utakaowezesha utoaji wa huduma za haki kwa njia ya kidijitali.

Amewataka Viongozi wa Mahakama ngazi zote kwenye Kanda hiyo kuhakikisha Watumishi wanapatiwa mafunzo ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi, uwazi na kasi ya utoaji haki pamoja na kupunguza mlundikano wa mashauri.

Aidha, Mhe. Hassan amerejea maelekezo ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yaliyotolewa Februari 2, 2026, akisisitiza umuhimu wa kuongeza matumizi ya mifumo ya TEHAMA pamoja na kuzingatia uadilifu katika usimamizi wa sheria na utoaji haki.

Pia ametoa maelekezo kwa Viongozi katika Kanda hiyo kuhakikisha utekelezaji wa sera mbalimbali za mafunzo ya utumishi wa umma na Mahakama pamoja na mipango mkakati inayolenga kuboresha utendaji kazi.

Katika hatua nyingine, amesisitiza umuhimu wa Watumishi kulinda na kutumia kwa uangalifu rasilimali za Mahakama, akirejea wito uliotolewa kwa madereva wa Mahakama kuhusu kuzingatia nidhamu, usalama na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Amesema Mahakama ina wajibu wa kuendelea kuwaelimisha Wananchi kuhusu taratibu na huduma zinazotolewa ili kuongeza uelewa na upatikanaji wa haki kwa urahisi zaidi.

Amehimiza Watumishi kufanya kazi kwa bidii, kuzingatia maadili na kutoa huduma bora kwa wakati, akisisitiza kuwa wao ni Waajiriwa wa Wananchi na wanapaswa kuwahudumia kwa uadilifu na weledi wa hali ya juu.

Vilevile katika baraza hilo kulikuwa na uchaguzi wa Viongozi ambao ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dodoma, Mhe Dickson Tigalyoma, Naibu Katibu Baraza, Bi. Irine Msafiri pamoja na Mjumbe wa Baraza Kuu Taifa Bi. Arapha Rusheke. Aidha katika Mkutano huo Wafanyakazi Hodari wa Mkoa wa Dodoma waliweza kutambuliwa.

Kabla ya Kufungwa kwa kikao hicho cha Baraza wajumbe mbalimbali pamoja na waalikwa walitoa neno la shukrani kwa Viongozi kwa kufanikisha kikao hicho. Baada ya kikao hicho wajumbe wote walirejea katika sehemu zako za kazi.


Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan akisalimiana na wajumbe wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Mahakama ya Wilaya Bahi.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan akisaini kitabu cha wageni katika Ofisi ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Bahi.

 Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan (katikati mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kutoka Mahakama Kuu Dodoma.

 

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan, akifuatilia kwa makini kikao cha Baraza la Wafanyakazi katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi.

Meza kuu ikiongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan (katikati), kulia kwake ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerald Gamba na kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Tughe Mkoa wa Dodoma, Bw. Maulid Kipeneku, wakiimba nyimbo ya mshikamano katika Baraza hilo lilofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya Bahi.

Meza kuu ikiongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Suleimani Haji Hassan (aliyesimama) akisema neno wakati wa kikao hicho.  Kulia kwake ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dodoma Mhe Gerald Gamba na kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Tughe Mkoa wa Dodoma Bw. Maulid Kipeneku, wakiimba nyimbo ya mshikamano katika baraza hilo lilofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya Bahi.

Katibu anayemaliza muda wake, Mhe. Gerald Gamba (kulia) akimkabidhi mkataba Katibu Mpya, Mhe Dickson Tigalyoma, mara baada ya uchaguzi wakati wa kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya Wilaya ya Bahi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam. 

 

WADAU WA SHERIA WAIBUA NGUVU YA USULUHISHI

  • Wahimiza njia za amani kutatua migogoro

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dar es Salaam

Wadau wa sekta ya sheria nchini wameeleza kwa kina namna usuluhishi unavyoendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuhakikisha Wananchi wanapata haki kwa haraka, nafuu na kwa njia ya amani, huku wakisisitiza umuhimu wa kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu mfumo huo.

Maelezo hayo yametolewa tarehe 9 Aprili 2026, katika uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi 2026 uliofanyika katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower, jijini Dar es Salaam, ambapo mgeni rasmi alikuwa Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju.

Katika hafla hiyo, kulikuwepo na mjadala kabambe ulioongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Eliamani Laltaika, ulioshirikisha Wadau mbalimbali waliotoa mitazamo yao kuhusu nafasi ya usuluhishi katika mfumo wa utoaji haki nchini.

Akichangia mada hiyo, Mtaalamu wa Usuluhishi na Mwanzilishi wa Taasisi ya ESS Creative and Legal Foundation, Bw. Eric Mukiza, alisisitiza kuwa mawasiliano ndiyo msingi mkuu wa mafanikio ya usuluhishi.

Alibainisha kuwa ujumuishi (inclusion) ni jambo la msingi, hasa kwa watu wenye ulemavu, ili kuhakikisha kila mmoja anapata fursa sawa ya kusikilizwa na kushiriki kikamilifu katika mchakato wa utatuzi wa migogoro.

Kwa upande wake, kiongozi wa dini, Sheikh Zaila Hassan, alieleza kuwa usuluhishi una mizizi ya kiimani, akisisitiza kuwa ni wajibu wa Wasuluhishi kuzingatia haki, uadilifu na hofu ya Mungu katika kutekeleza majukumu yao.

Naye Chifu Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mtemi Henry Mazengo wa Pili, aligusia umuhimu wa mila na desturi katika kuendeleza utatuzi wa migogoro kwa njia ya maelewano, akibainisha kuwa jamii nyingi za kiafrika zimekuwa zikitumia mbinu hizo tangu zamani kudumisha amani na mshikamano.

Akizungumza kwa upande wa sekta ya fedha, Bw. Ramadhani Myonga kutoka Benki Kuu ya Tanzania alieleza kuwa hapo awali kulikuwepo changamoto za mifumo ya kushughulikia migogoro ya kifedha kutokana na kukosekana kwa miongozo mahsusi (internal guidelines), hali iliyosababisha malalamiko kutoka kwa wananchi.

Hata hivyo, alisema maboresho yaliyofanyika yamewezesha kuanzishwa kwa mfumo wa “Sema na BoT” unaorahisisha Wananchi kuwasilisha na kutatua malalamiko yao bila gharama.

Kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Peter Ernest Mogoro alieleza kuwa moja ya majukumu ya Wizara hiyo ni kusaidia Wananchi kutatua changamoto zao kupitia njia mbadala za utatuzi wa migogoro, ikiwemo usuluhishi. Aliongeza kuwa programu kama “Mama Samia Legal Aid” zimekuwa msaada mkubwa kwa Wananchi katika kupata haki.

Naye Bw. Lucas Malunde kutoka Ofisi ya Rais – TAMISEMI, alisisitiza kuwa Taasisi hiyo inalenga kuhakikisha uwepo wa utangamano ndani ya jamii kwa kuhimiza matumizi ya usuluhishi katika ngazi za chini za utawala.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, alibainisha kuwa chama hicho kinaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa usuluhishi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupunguza migogoro inayofikishwa mahakamani.

Kwa ujumla, Wadau hao walikubaliana kuwa usuluhishi umeleta manufaa makubwa kwa wananchi kwa kuokoa muda na gharama, huku ukitoa nafasi ya kufikia suluhu za kudumu kwa njia ya maelewano badala ya migogoro ya muda mrefu mahakamani.

Uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi 2026 umefanyika chini ya kauli mbiu isemayo: “Kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama mbinu inayopendelewa nchini Tanzania,” ikiwa ni jitihada za kuhamasisha matumizi ya mfumo huo kwa manufaa ya jamii nzima.

 


Wadau mbalimbali walioshiriki kwenye mjadala wakiwa kwenye picha ya pamoja. Picha chini ni wageni mbalimbali aliohudhuria uzinduzi wa Wiki ya Uuluhishi nchini.




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.



SERIKALI YASISITIZA UMUHIMU WA MATUMIZI YA NJIA MBADALA ZA UTATUZI WA MIGOGORO

  • Naibu Waziri asema usuluhishi nguzo muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dar es Salaam

Serikali imesisitiza umuhimu wa matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro, hususan usuluhishi, kama njia bora ya kuharakisha upatikanaji wa haki na kudumisha amani katika jamii.

Msisitizo huo umetolewa tarehe 9 Aprili, 2026 na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainabu Katimba, wakati akitoa salamu zake katika hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi 2026 uliofanyika katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower, jijini Dar es Salaam.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, ambaye alikuwa mgeni rasmi pamoja na Viongozi mbalimbali wa Mahakama, Serikali, sekta binafsi na Wadau wa Sheria.

Uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi ulikuwa na kauli mbiu isemayo: “Kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama mbinu inayopendelewa nchini Tanzania.”

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Katimba amesema usuluhishi umeendelea kuwa nguzo muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini kutokana na uwezo wake wa kupunguza gharama, kuokoa muda na kulinda mahusiano ya kijamii na kiuchumi.

Aidha, ameeleza kuwa jitihada za kuimarisha usuluhishi zinaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kujenga mfumo wa haki wenye ufanisi na unaoweza kutoa huduma kwa wakati kwa Wananchi wote.

“Matumizi ya usuluhishi ni sehemu ya dhamira ya Serikali kuhakikisha Mahakama inakuwa chombo chenye ufanisi katika utoaji wa haki kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema Mhe. Katimba.

Amefafanua kuwa tofauti na mwenendo wa kawaida wa mashauri mahakamani, usuluhishi hutoa fursa kwa pande zinazohusika kufikia makubaliano kwa hiari, kwa haraka na kwa gharama nafuu, hali inayochangia kuimarisha mshikamano na utengamano katika jamii.

Kwa mujibu wa Mhe. Katimba, Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria itaendelea kuunga mkono na kuimarisha matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania pamoja na Wadau mbalimbali.

Katika hatua nyingine, amesema Wiki ya Usuluhishi inayotarajiwa kufanyika kuanzia Aprili 13 hadi 17, 2026, itatoa fursa kwa Wananchi kupata elimu na huduma za usuluhishi bure katika Mahakama mbalimbali nchini.

Amesema hatua hiyo inalenga kuwahamasisha Wananchi kutumia zaidi njia za maelewano katika kutatua migogoro yao, badala ya kutegemea mashauri marefu na yenye gharama kubwa mahakamani.

Aidha, amewahimiza Wadau wa sekta ya sheria, wakiwemo Mawakili, Wasuluhishi na Watumishi wa Mahakama, kuendelea kuhamasisha matumizi ya usuluhishi pamoja na kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa na imani ya Wananchi katika mfumo huo.

Kwa upande wa Serikali, Mhe. Katimba amesema juhudi zinaendelea kufanyika katika kuboresha sekta ya sheria ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya Mahakama, kuongeza rasilimali watu na kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Amesisitiza pia umuhimu wa maadili, weledi na uadilifu kwa Wasuluhishi ili kuhakikisha mchakato wa usuluhishi unafanyika kwa haki, uwazi na kwa kuzingatia misingi ya sheria.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Katimba ametoa wito kwa Wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Wiki ya Usuluhishi na kutumia fursa hiyo kumaliza migogoro yao kwa njia ya amani na maelewano.

Uzinduzi huo umeacha mwamko mpya miongoni mwa wadau wa sekta ya sheria na jamii kwa ujumla, ukiashiria hatua muhimu katika juhudi za Serikali za kuimarisha upatikanaji wa haki kwa njia mbadala na endelevu nchini.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainabu Katimba, akitoa salama katika hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhisho 2026 uliofanyika tarehe 9 Aprili 2026 katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower jijini Dar es Salaam.

Viongozi mbalimbali wa Mahakama, Serikali, Sekta binafsi na wadau wa sheria walioudhuria katika hafla ya Wiki ya Usuluhishi 2026 iliyofanyika katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower, jijini Dar es salaam.

 




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.



 

 

Alhamisi, 9 Aprili 2026

'USULUHISHI SI NJIA MBADALA YA UTATUZI WA MIGOGORO; NI NJIA HALALI YA UPATIKANAJI HAKI'

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa, Usuluhishi haupaswi kuitwa njia mbadala ya utatuzi wa migogoro kwakuwa ni njia mojawapo inayotambulika kikatiba.

Mhe. Masaju ameeleza hayo leo tarehe 09 Aprili, 2026 wakati wa Hafla ya Uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi nchini iliyofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF Golden Jubilee jijini Dar es Salaam.

“Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa Ibara ya 107(A)(2)(d) ambayo inaitaka Mahakama kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro, hii ni njia halali ya utatuzi wa migogoro, kwahiyo tunachokifanya hapa kina uhalali wa kikatiba, sasa kitu kipo kwenye Katiba, kitakuwaje njia mbadala, hata usuluhishi ni njia ya kufikia haki,” amesema Jaji Mkuu.;

Mhe. Masaju amesema kuwa, Usuluhishi ni njia muhimu kwa kuwa una faida nyingi na pia unatambulika katika katika dini kuu mbili (Ukristo na Uislamu) huku akirejea Kitabu cha Mathayo Sura ya 5:9 imeandikwa kwamba, Heri Wapatanishi maana wataitwa Wana wa Mungu.

Vilevile, amerejea katika Kitabu cha Quran Tukufu (Quran: 9-10) inasema,Na ikiwa makundi mawili katika waumini yanapigana, basi yapatanisheni…. Hakika waumini ni ndugu, basi patanisheni baina ya ndugu zenu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mrehemewe.

Maneno haya matakatifu yanatufundisha kuwa usuluhishi wa migogoro kwa njia ya upatanishi ambayo ni moja ya mbinu za usuluhishi wa migogoro si takwa la kisheria pekee, bali ni msisitizo unaoelezwa pia katika vitabu vyetu vitakatifu,” ameeleza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju amewataka Wasuluhishi kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, kuwajibika ipasavyo na kuvaa vazi la kiMungu wanapotekeleza jukumu hilo muhimu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju amezitaja pia njia za usuluhishi wa migogoro kwa njia za asili kwa kuzingatia mila na desturi za jamii husika kama njia mbadala ni kusema kuwa, njia hizo pia ni muhimu kuziendeleza kwakuwa hata katika kiapo cha Majaji kinawataka kuzingatia na kuheshimu mila na desturi zilizopo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Katika hilo, Jaji Mkuu amesema kuna haja ya kufanyia marekebisho Sheria ya Serikali za Mitaa ili kuwatambua na kuwapa mamlaka ya kisheria Machifu ambapo pamoja na mambo mengine, watafanya usuluhishi kisheria kwakuwa wao pia husaidia kuhimiza uzingatiwaji wa usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii na umoja wa Kitaifa.

Mhe. Masaju amesema kuwa, kupitia Sheria hiyo ana imani kuwa, Machifu watafanya vizuri katika usuluhuhishi mfano wa masuala ya ardhi, ndoa na kadhalika.

Ameongeza kwamba, Mahakama ya Tanzania inaunga mkono Taasisi au wadau wote wanaotumia njia halali zinazoleta Suluhu ili mradi kutekeleza masharti ya Katiba na Sheria ili watu waishi kwa amani, utulivu na udugu.

Aidha, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, suala la kuendeleza matumizi ya njia za usuluhishi wa migogoro linaendana sambamba na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambayo inajengwa katika msingi mkuu wa utawala bora, amani, usalama na utulivu.

"Usuluhishi ni moja ya nyezo inayolenga katika kuleta amani, usalama na utulivu.  Hivyo, katika kutekeleza msingi wa Dira ya 2050 hii jukumu la wadau na Mahakama ni kuhamasisha na kuhakikisha usuluhishi unatumika ipasavyo pale migororo inapojitokeza katika jamii na shughuli za kibiashara," amesema Mhe. Masaju. 

Jaji Mkuu ametaja Vipaumbele vinne vya Dira hiyo kuwa ni pamoja na; Utawala Bora na Haki, Serikali za Mitaa Imara na zenye ufanisi, Utumishi wa Umma Unaowajibika na Amani, Usalama na Utulivu.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu ametoa rai kwa Majaji, Mahakimu na Watumishi wa Mahakama kwa ujumla kuandika vitabu kwa kuwa hazina kubwa ipo kwenye vitabu, hivyo ni muhimu kufanya hivyo.

“Nirejee tena kuwashauri Majaji, Mahakimu na Watumishi wote wa Mahakama, wale mlio na uwezo wa kuandika, andikeni hazina kubwa ipo kwenye vitabu na sio kwenye hizi ‘electronic devices’ambazo hata hazina uhakika tu wa kuwepo kwa hiyo tukiandika tunasaidiana,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amekishukuru na kukipongeza Kituo cha Usuluhishi wakishirikiana pamoja na wadau kwa kufanikisha kuandaa Wiki ya Usuluhishi nchini sambamba na Watoa mada wote walioshiriki katika majadiliano.

Akitoa neno la utangulizi katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma amesema uanzishaji wa wiki ya usuluhishi ni mkakati mmoja wapo wa kuelimisha umma kuhusu uwepo wa sheria hizi na fursa zilizopo za kumaliza migogoro inayojitokeza kwa njia za usuluhishi bila ya ulazima wa kufika Mahakamani.

"Uzinduzi huu ni moja ya tukio muhimu na la kihistoria nchini kwetu katika kukuza mfumo wa utoaji haki na kuendeleza juhudi za kitaifa katika kukuza utamaduni wa kutatua migogoro kwa njia za Usuluhishi," amesema Mhe. Maruma.

Jaji Mfawidhi huyo amesema kuwa, Wiki ya Usuluhishi ni moja ya mkakati wa kukuza uelewa na kuhamasisha utekelezaji wa matakwa ya sheria mbalimbali zinazotoa fursa ya usuluhishi wa migogoro kabla ya kuifikisha Mahakamani.

"Wakati nchi jirani wanaweka juhudi  za kutunga sheria za usuluhishi, Tanzania imekuwa mfano  bora wa kuwa na sheria nyingi zaidi ya ishirini na nne zinazotoa fursa ya matumizi ya usuluhishi zikiwemo Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai (Sura ya 33 Marejeo 2023), Sheria ya Mahakama za Migogoro ya Ardhi (Sura ya 216), Sheria ya Ndoa (Sura ya 29, Marejeo ya 2023), Sheria ya Mabaraza ya Kata (Sura ya 209), Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini (Sura ya 366), Sheria ya Ndoa (Sura 29), Sheria ya Migogoro ya Bima Sura ya 394, Toleo la Marejeo la 2023, Sheria ya Bima za Magari Sura ya 169 (2023), Sheria ya Mikataba Sura ya 345 (2019) na Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote Sura ya 161 (2023)," ameeleza Jaji Maruma.

Ameongeza kuwa, Matumizi ya usuluhishi hususan njia ya upatanishi ni moja ya mikakati wa Mahakama kupitia Mpango Mkakati wa Mahakama kutoka mwaka  2015-2020/2021 – 2025/26 lengo likiwa ni kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo na kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri kama vile ada za mawakili na mud awa  wadaawa ambaounaweza kutumika katika shughuli zingine za kiuchumi. Vile vile kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani, kuongeza ufanisi, na kutoa haki inayogusa mazingira halisi ya wananchi haraka mapema ipasavyo.

"Uanzishaji wa wiki ya usuluhishi ni mkakati mmoja wapo wa kuelimisha umma kuhusu uwepo wa sheria hizi na fursa zilizopo za kumaliza migogoro inayojitokeza kwa njia za usuluhishi bila ya ulazima wa kufika Mahakamani," amesema Mhe. Maruma.

Amesema, lengo na chimbuko la kuanzisha Wiki ya Usuluhishi nchini ni moja ya utekelezaji wa maelekezo ya Jaji Mkuu ambayo amekuwa ukiyatoa mara kwa mara katika kuhakikisha tunatekeleza jukumu la kikatiba chini ya ibara ya 107A (2) (d) la kukuza na kuendeleza matumizi ya usuluhishi. 

Wiki ya Usuluhishi nchini kwa mwaka huu imebeba kaulimbiu isemayo; 'Kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama mbinu inayopendelewa nchini Tanzania,' inatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026 nchi nzima na inalenga kuelimisha umma kuhusu sheria za usuluhishi kwa ujumla, kuhamasisha matumizi ya usuluhishi na kadhalika.

Wadau mbalimbali wa Kituo cha Usuluhishi wameshiriki katika hafla hiyo na baadhi yao wameshiriki kutoa uzoefu katika kazi ya Usuluhishi.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba yake wakati wa Hafla ya Ufunguzi wa Wiki ya Usuluhishi nchini leo tarehe 09 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF Golden Jubilee Tower jijini Dar es Salaam.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi nchini leo tarehe 09 Aprili, 2026 wakati wa hafla ya uzinduzi wa Wiki hiyo.

Sehemu ya washiriki mbalimbali wakiwemo Majaji, Wasajili, Watumishi wengine wa Mahakama pamoja na wadau waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi iliyofanyika leo tarehe 09 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa PSSSF Golden Jubilee Tower jijini Dar es Salaam.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akitoa neno la utangulizi wakati wa Hafla ya Uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi nchini iliyofanyika leo tarehe 09 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam.


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi (waliosimama nyuma). Aliyeketi wa kwanza kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Paul Ngwembe, wa pili kulia ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, wa kwanza kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi na wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma. 

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba akitoa neno wakati wa hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi leo tarehe 09 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju katika picha ya pamoja na Wadau wa Kituo cha Usuluhishi waliopatiwa tuzo na Mahakama hiyo kwa mchango wao katika kazi ya Usuluhishi.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama nyuma katikati) pamoja na Viongozi wengine wa meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wadau waliotoa uzoefu wao kuhusu Usuluhishi wakati wa hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Sheria leo tarehe 09 Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam.

JENGENI UTAMADUNI WA KUKUTANA MARA KWA MARA KAMA KATIBA INAVYOELEKEZA; JAJI KIONGOZI

Na. HABIBA MBARUKU- Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu, amewataka wanachama wa chama hicho kujenga utamaduni wa kukutana mara kwa mara ili kulinda uhai wa chama hicho.

Mhe. Dkt. Siyani ameyasema hayo wakati alipofungua mafunzo na michezo kwa Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu, leo tarehe 9 Aprili, 2026 katika ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa, upo umuhimu wa wanachama wa TMJA Tawi la Masjala Kuu kukutana mara kwa mara, kama ambavyo vyama katika Taasisi nyingine hufanya, hivyo ni muhimu kuhakikisha kwamba vikao vya Chama vinaandaliwa na wajumbe wanakutana kama ambavyo Katiba ya Chama inaelekeza huku akiwahimiza wanachama na wajumbe kuhudhuria vikao vya chama bila visingizio.

“Umuhimu wa kukutana mara kwa mara, uhai wa vyama hivi kama ilivyo kwa taasisi nyingine unategemea wajumbe wake kukutana, inategemea uwepo wa vikao, chama au taasisi yoyote ambayo haikutani uhai wake unakuwa mashakani, kwa hiyo tawi hili kama matawi mengine yote yanao wajibu wa kikatiba kwa mujibu wa Katiba yetu ya chama kukutana, ni muhimu kuhakikisha kwamba vikao hivi vinaandaliwa na watu wanakutana, ujengwe huo utamaduni na tusirudi tena kwenye historia ya kukaa muda mrefu bila kukutana ili kulinda uhai wa chama” amesema Mhe. Dkt. Siyani.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani ameongeza kuwa, kama ambavyo kila mmoja hulinda afya yake, ni muhimu kila mwanachama kuanza kuitazama afya ya akili na kuipa kipaumbele kwa sababu tatizo la afya ya akili linaweza kuathiri utendaji wa shughuli za kila mmoja na hasa zile za kiofisi, hivyo ni vyema kuanza kutazama mambo yanayoweza kupunguza msongo wa mawazo ili kutunza afya ya akili.

Akizungumza kuhusu umuhimu wa mafunzo yatakayotolewa, Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kuwa, mafunzo hayo yatawasaidia kutambua ni shughuli gani wanaweza kufanya ili kujiongezea kipato bila kuathiri uwajibikaji wao kama Maofisa Mahakama, kupitia mada mbalimbali zitakazotolewa ikiwemo masuala ya uwekezaji salama na wenye tija na kuwataka wajumbe kuchangia kwa uhuru na kuachana na utamaduni wa kutotoa mawazo au hoja na kuongeza kuwa jamii itapiga hatua katika maendeleo kama kila mtu atatoa mawazo na kuzungumza katika majadiliano.

Kupitia mada ya utafiti wa sheria kwa njia ya mtandao itakayofundishwa wakati wa mafunzo, Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kuwa, Maofisa Mahakama hawataweza kutimiza wajibu wao bila kufanya utafiti na kwamba utafiti utawasaidia kujenga hoja na kuonesha sababu za kufanya maamuzi fulani, hivyo suala la utafiti lina umuhimu mkubwa katika kujenga uelewa wa kutosha jambo linatalosaidia wakati wa kutoa maamuzi yaliyo sahihi na kutenda kwa haki.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amewahimiza wajumbe waliohudhuria mafunzo hayo kushiriki katika michezo itakayofanyika jioni baada ya mafunzo kukamilika ili kuendelea kulinda afya ya akili na kuimarisha afya ya mwili.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu, akizungumza wakati alipofungua mafunzo na michezo kwa Wanachama wa TMJA Tawi la Masjala Kuu, leo tarehe 9 Aprili, 2026 katika ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Naibu Msajili Mahakama Kuu na Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania Mhe. Desdery Kamugisha ambaye pia ni Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Masjala Kuu akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa TMJA Tawi la Masjala Kuu ili afungua mafunzo na michezo kwa wanachama wa Tawi hilo.

Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na uongozi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu (katikati), kulia ni Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania na Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Masjala Kuu Mhe. Desdery Kamugisha na kushoto ni Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Amani Aboud. 

Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.

Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe Wanawake wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.


Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)





 

Jumatano, 8 Aprili 2026

WADAU WA HAKI JINAI KIGOMA WAKUTANA

  • Wafanya Tathmini ya mwenendo wa mashauri ya Jinai

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma hivi karibuni ilifanya Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Jinai kilichoongozwa na Naibu Msajili wa Kanda hiyo, Mhe. Fadhili Mbelwa kikilenga kutathimini na kuimarisha usimamizi na ufanisi wa utoaji haki kwa wananchi mapema ipasavyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mbelwa alibainisha kuwa kikao hicho kilijikita kuweka mikakati ya kuhakikisha mashauri ya jinai kwa ngazi ya Mahakama Kuu yanasikilizwa haraka ili kuepuka mashauri ya mlundikano huku zikiendelea juhudi za kuhimizana wadau kila mmoja kutimiza wajibu wake katika mnyororo wa haki jinai ili waisaidie Mahakama kutekeleza jukumu lake la msingi haraka iwezekanavyo.

“Tunafahamu kwamba, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju alikwishaelekeza  umri wa mashauri kwa kila ngazi ya Mahakama, hivyo mashauri yanapaswa kumalizika ndani ya muda uliowekwa, hivyo sote tushirikiane kuhakikisha kwamba ukomo wa muda kwa kila ngazi ya Mahakama unazingatiwa ili mashauri ya mlundikano ibaki historia kwa Mahakama Kanda ya Kigoma,” alisema Naibu Msajili huyo.

Kwa upande wake, Mjumbe mwalikwa kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) Mkoa wa Kigoma ambaye ni Ofisa Uhifadhi Wakimbizi, Bw. Aganyira Rugemarila, aliishukuru Mahakama na kuipongeza kwa jinsi ilivyojipanga kiuhudumia mashauri ya wakimbizi kutoka nchi za Jirani.

“Tunaipongeza Mahakama Kigoma, kwa hakika mnafanya kazi nzuri sana kwenye mashauri ya wakimbizi kwani mnasikiliza na kutoa hukumu kwa  wakati, hata hivyo tumeona wakimbizi wengi wanaokutwa na hatia, Mahakama imekuwa ikitoa vifungo mbadala yaani kifungo cha nje chini ya Idara ya Huduma kwa Jamii, wakimbizi wanafanya adhabu hizo kisha wanamaliza salama badala ya kukaa gerezani kwa muda wote waliofungwa,” alisema Bw. Rugemarila

Aidha, shukrani hizo zilienda sambamba kwa wadau wa haki jinai kwa ushirikiano wanaoutoa katika kutatua changamoto za wakimbizi zinapojitokeza, kwani wadau wa haki jinai wamekuwa mstari wa mbele kushirikiana na Idara ya Wakimbizi katika kuhakikisha maisha ya wakimbizi  Mkoa wa Kigoma yanafuata sheria za nchi ndani na nje ya Kambi walizohifadhiwa  Mkoani Kigoma.

Waliohudhuria kikao hicho ni wajumbe kutoka Ofisi ya  Mkuu wa Magereza, Polisi, Ofisi ya Upelelezi Mkoa, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Kigoma (NPS), Ustawi wa Jamii, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Idara ya Marekebisho ya Tabia, Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mjumbe kutoka UNHCR Mkoa wa Kigoma.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akizungumza jambo hivi karibuni wakati wa Kikao cha Kamati ya Haki Jinai ya Mahakama Kanda ya Kigoma.

 Mkuu wa Gereza la Mkoa wa Kigoma, Bw. Bosco Lupala akisikiliza kwa makini mjadala uliokuwa ukiendelea wakati wa Kikao cha Kamati ya Haki Jinai Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.

Sehemu ya wajumbe wakifuatilia kwa makini taarifa yaliyokuwa yakijiri  wakati wa Kikao cha Kamati ya Wadau wa Haki Jinai Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.

Mjumbe mwalikwa kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) Mkoa wa Kigoma, Bw.Aganyira Rugemarila akitoa pongezi na shukrani kwa Wadau wa Haki Jinai wakati wa Kikao cha Kamati ya Haki Jinai.

Ofisa Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Uhamiaji, Bw. Rudger Kilala akifuatilia taarifa za kikao wakati wa Kikao cha Kamati ya Wadau wa Haki Jinai kilichofanyika hivi karibuni Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)