Alhamisi, 18 Juni 2026

TUTEKELEZE MAJUKUMU YETU VEMA; JAJI NGUNYALE

Na MICHAEL RITTE, Mahakama-Bukoba

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Nyanguye amewasihi watumishi wa Masjala hiyo kuhakikisha kazi za usikilizwaji wa mashauri zinaendeshwa vema pasipo kukwama na jukumu hilo liambatane na juhudi katika utendaji wa majukumu ya kila siku kwa kuzingatia Maadili na kanuni za nafasi husika wanazozitumikia.

Mhe. Ngunyale aliyasema hayo jana tarehe 17 Juni, 2026 katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wakati wa makabidhiano ya Ofisi kati yake na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ambaye ameteuliwa hivi karibuni kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani.

Kabla ya makabidhiano ya ofisi, kulikuwa na  mapokezi ya awali katika viwanja vya Mahakama hiyo.

Jaji Ngunyale alisema kuwa, kila mtumishi ana wajibu wa kuhakikisha huduma za utoaji haki zinafanyika kwa uadilifu na weledi. Huku akisisitiza kuwa, “tujivunie nafasi tulizopewa na kuzisimamia ipasavyo.”

“Tukifanikiwa kusimamia majukumu yetu na kuwekeza nguvu na muda katika kazi, itatuletea nafasi thabiti ya kujengeana uwezo katika kazi na katika majukumu mbalimbali,” amesisitiza Mhe. Ngunyale.

Ameongeza kuwa, katika utekelezaji wa majukumu ni muhimu kujali afya, familia zetu na jamii sambamba na kuwa na ukaribu na kutenga muda na  nafasi kushiriki shughuli za kijamii ambazo kwa namna moja hudumisha afya ya kiakili na kiutendaji kwa mtumishi.

Alisisistiza kwa kunukuu, “To be trusted is a greater Compliment than to be loved,” Usemi kutoka kwa Mwandishi George MacDonald ambao unamaanisha kuwa, ‘Kuaminiwa ni sifa kubwa kuliko kupendwa.’

Kwa upande wake, aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, aliwasihi watumishi hao kuendelea kuishi kwa upendo kama walivyoishi naye kipindi akiwa katika nafasi hiyo.

Kadhalika, Mhe. Banzi amewasihi watumishi hao kuendeleza ushirikiano. Na kuhitimisha kwa kumtakia Mhe. Ngunyale kila la kheri katika utekelezaji wa majukumu mapya katika Kituo hicho.

Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Ngunyale akisalimiana na Watumishi wa Mahakama hiyo alipowasili katika Kituo chake kipya cha kazi jana tarehe 17 Juni, 2026. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi (kulia) akimkabidhi taarifa ya makabidhiano ya ofisi Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Ngunyale.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi (wa pili kulia) akiwa katika picha na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Ngunyale (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Lillian Itemba (wa kwanza kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Ferdinand Kiwonde. 

 Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi (wa pili kushoto) akizungumza jambo wakati wa hafla ya makabidhiano ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba kwa Mhe. David Ngunyale. Wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Lillian Itemba na wa kwanza kulia ni Mhe. Ferdinand Kiwonde, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, wakiwa kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Bukoba.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Said Mkasiwa akitoa neno la kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama hiyo, Mhe. David Ngunyale (wa kwanza kushoto).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 


WATUMISHI DODOMA WAMPONGEZA NAIBU MSAJILI MPANGULE

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Biswalo Mganga, amewaongoza Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma katika hafla fupi ya kumpongeza Mhe. Zabibu Mpangule, mara baada ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma.

Hafla hiyo imefanyika tarehe 17 Juni 2026 katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi, Mhe. Mganga amempongeza Mhe. Mpangule kwa kuaminiwa na kupewa nafasi hiyo muhimu, akieleza kuwa uteuzi wake ni matokeo ya utendaji kazi uliotukuka, uadilifu na kujituma katika kutekeleza majukumu yake.

Kabla ya uteuzi huo, Mhe. Mpangule alikuwa akihudumu kama Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma ambapo alitoa mchango mkubwa katika utoaji wa huduma za haki kwa Wananchi.

Kwa upande wake, Mhe. Mpanguke aliwashukuru Watumishi kwa pongezi zao na kuhahidi kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi, uadilifu na kujituma kwa manufaa ya Mahakama na Wananchi kwa ujumla.

Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma pamoja na Wilaya zake walimtakiwa kila la kheri katika majukumu yake mapya.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga (wa kwanza kushoto) akimkabidhi zawadi Naibu Msajili, Mhe. Zabibu Mpangule, katika hafla ya kumpongeza.

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja na kumpatia dhawadi  Naibu Msajili mteule (wa nne kutoka kushoto).

 

Naibu Msajili, Mhe. Zabibu Mpangule akikata keki ambayo ameandaliwa katika hafla ya kumpongeza.

Watumishi wa Mahakama Dodoma waliohudhuria hafla hiyo wakiwa katika picha ya pamoja wakifanya ibada kabla ya kuanza hafla hiyo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja mara baada kumpokea Naibu Msajili, Mhe. Zabibu Mpangule, mara baada ya kuwasili kutokea kula kiapo katika Ofisi za Tume ya utumishi wa Mahakama.

 

 

 

JAJI FAHAMU MTULYA AAGWA MUSOMA KUFUATIA UHAMISHO WA KITUO

  • Yamkaribisha pia Jaji Kakolaki katika Kituo hicho

Na FRANCISCA SWAI, Mahakama-Musoma

Uongozi na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Musoma wamejumuika kumuaga Jaji Fahamu Mtulya kufuatia uhamisho wake kwenda Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya na kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki aliyehamia kutokea Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mtwara.

Hafla ya kumuaga Jaji Mtulya na kumkaribisha Jaji Kakolaki ilifanyika tarehe 14 Juni, 2026 katika Viwanja vya Mahakama Kuu Musoma.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mtulya aliwashukuru watumishi na wadau wote wa Mahakama Musoma kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote cha utumishi wake akiwa Musoma.

Pia, aliwaasa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa umoja na upendo, kuzingatia maadili ya kazi na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Zaidi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano na wadau katika kuhakikisha shughuli za Mahakama zinafanyika kama inavyopaswa.

Naye Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki aliwashukuru Uongozi, watumishi na wadau wote wa Mahakama Kanda ya Musoma kwa kumkaribisha na kuahidi kutoa ushirikiano pamoja na kufanya kazi kwa bidii.

Kwa upande wao watumishi wa Mahakama Kuu Musoma walimshukuru Jaji Mtulya kwa uongozi wake thabiti, malezi bora kwa watumishi wa kada zote, kuwa mfano hai wa mchapakazi, uadilifu, upendo na kujitoa kwake katika kazi, matukio ya kijamii, kuhamasisha umoja, michezo na utalii wa ndani.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kiserikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Mtambi, Mkuu wa Wilaya Musoma, Mhe. Juma Chikoka pamoja na Wadau mbalimbali wa Mahakama ambao wote kwa pamoja walitoa salamu na zawadi mbalimbali kumshukuru Jaji Mtulya kwa uongozi wake imara uliothibitika kwa uwajibikaji, uadilifu, na mashirikiano mzuri na wadau.

 Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (wa pili kushoto) akijiandaa kukata keki na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati)wakati wa hafla ya kumuaga Jaji Mtulya na kumkaribisha Jaji Kakolaki (katikati). Wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Musoma, Mhe. Marlin Komba, wa kwanza kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Musoma, Mhe. Kamazima Idd na wa pili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mara, Mhe. Kanali Evans Mtambi.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Musoma, Mhe.Edwin Kakolaki (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (kushoto) na Mkuu wa Mkoa wa Mara, Mhe. Kanali Evans Mtambi (kulia).

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akipokea mkono wa kwaheri kutoka kwa Chama cha  Mahakimu na Majaji (TMJA) Tawi la Musoma.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Musoma.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (wa pili kushoto) akiwa ameshika zawadi aliyopatiwa ikiwa ni ishara ya shukrani na kumtakia kheri kutoka kwa Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma ambao ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Omari Kingwele (wa kwanza kushoto), wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Musoma,  Mhe. Monica Ndyekobora na wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Masjala Ndogo ya Musoma, Bw. Leonard Maufi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akipokea zawadi ikiwa ni ishara ya mkono wa kwaheri na shukrani kutoka kwa watumishi ambao ni wadau wa utalii Masjala ndogo Musoma.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Kamati ya maandalizi ya hafla ya kumuaga ambao ni watumishi wa Kanda ya Musoma.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wadau walioshiriki katika hafla ya kumuaga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (kulia) akipokea mkono wa kwaheri na shukrani kutoka kwa Mkuu wa Wilaya Musoma, Mhe. Juma Chikoka.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akipokea mkono wa kwaheri na shukrani kutoka wadau wa Mahakama kwa namna alivyokuwa mstari wa mbele kuhamasisha shughuli za utalii wa ndani.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

Jumatano, 17 Juni 2026

‘ZINGATIENI MASLAHI YA UMMA, TAIFA KWA KULINDA HESHIMA, UHURU WA MAHAKAMA’

·       Jaji Mkuu awataka Naibu Wasajili wapya kuwajibika ipasavyo

·       Awataka kusimamia ipasavyo utekelezaji wa hukumu

·       Jaji Mkuu awataka kuimarisha ushirikiano na watumishi walio chini yao

·       Awataka pia kusimamia Masjala Ndogo za Mahakama Rufaa na kuandaa vema kumbukumbu za rufaa

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Naibu Wasajili wapya 31 kuzingatia maslahi ya umma na ya Taifa katika kulinda, kutunza heshima, mamlaka na uhuru wa Mahakama kama unavyotajwa katika Ibara ya 30(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma alipokuwa akizungumza na Naibu Wasajili wapya 31 walioapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

“Tunapotambua kwamba mnazo sifa za kuwa Viongozi na Tume tukawateua nendeni mziishi hizo sifa, lakini pia tambueni tunaishi wakati gani, ni wakati ambao unasisitizwa sana uwajibikaji na hatuwezi kuwa tu tunafurahia kuteuliwa. Kila nafasi ya uongozi na kila nafasi ya mafanikio inakuja na wajibu mkubwa kwa mhusika,” amesema Jaji Mkuu.

Amewataka Naibu Wasajili hao kutambua kuwa, Mahakama ya Tanzania inawategemea kwa kuwa wao ni kada muhimu na ndio Meneja na Injini ya shughuli za kila siku za Mahakama katika ngazi zote kuanzia Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Wilaya, Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani.

“Ingawa mtapatiwa mafunzo elekezi, matarajio ni kwamba tayari mna ufahamu wa majukumu yenu kutokana na uzoefu mlio nao hususan kwa wale ambao wamewahi kukaimu nafasi hizi lakini hata wale waliokuwa Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi ngazi ya Mkoa, ngazi ya Wilaya na mambo ni yaleyale kwa mfano masuala ya ‘execution’ kama Naibu Wasajili ninyi ndio wapishi au waratibu Wakuu wa shughuli za kimahakama, ninyi ni Mameneja na Injini ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika amewataka Wasajili hao wa Mahakama kusoma sheria mbalimbali zinazoelezea majukumu yao ili wawe katika nafasi nzuri ya kutekeleza majukumu yao ya kila siku ipasavyo huku akisema kuwa, “jitambueni na muwajibike kama Viongozi katika maeneo yenu ya kazi, jitoleeni kwa moyo wote ili kuleta ufanisi katika Vituo vyenu na kwa Mahakama kwa ujumla, kuweni na ari, ubunifu na utayari wa kutatua changamoto zinazojitokeza katika maeneo yenu ya kazi, leteni Makao Makuu ya Mahakama changamoto zilizo nje ya uwezo wenu badala ya kusubiri vikao ndipo muwasilishe hizo changamoto.”

Kadhalika, Mhe. Masaju amewataka Naibu Wasajili hao kuimarisha ushirikiano na Watumishi wa Kada nyingine waliopo chini yao. “Kwenye ngazi ya Mkoa au Kanda wapo Watendaji wa Mahakama lazima muwape ushirikiano ipasavyo, tumegawana majukumu ninyi mnashughulika na shughuli za kimahakama, wenzetu wanashughulika na shughuli za kiutawala lakini ushirikiano ni jambo la lazima, kuhusu suala ya kutunishiana misuli lazima mshirikiane, mheshimiane kwa sababu mafanikio yetu yanategemea tunashirikiana namna gani,” amesema Jaji Mkuu.

Amesema kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja ambacho amekaa Mahakamani amebaini kuwa, watumishi wanawasikiliza Viongozi lakini kumekuwa na changamoto ya kutokuchukua hatua wakidhani mambo hayo yanatekelezwa na waliopo Makao Makuu pekee wakidhani kuwa wao hawahusiki, hivyo amewataka kubadilika na Uongozi watawapima ipasavyo.

Aidha, amewataka Naibu Wasajili hao kutumia vizuri kipindi cha miezi sita ya uangalizi (Probation) kwa kuwajibika, na kwamba wao kama Viongozi watakuwa wanawafuatilia kwa karibu kwa sababu nia yao ni njema hawawaangalii kwa karibu ili kuwaadhibu bali waendelee kupanda katika vyeo vya juu zaidi.

“Sasa hivi kuna nafasi zipo kwa ajili ya Majaji wa Mahakama Kuu, tunataka kadri tunavyostaafu na wengine wanavyopanda kwenda Mahakama ya Rufani, wengine wanaziba zile nafasi, ninyi mmeshaaminiwa na tungependa hao Majaji watokane na ninyi, na ndio maana tunasema kwamba ile Mahakama ya Mkoa itakapokuwa imeanzishwa itakuwa ndio Kituo cha Mafunzo cha kuwaandaa ninyi kuteuliwa kuwa Majaji na mimi kitu ninachokizingatia sana ni uadilifu na uwezo wa kumudu majukumu kwa ufanisi ipasavyo, kwahiyo tutakapokuwa tunawaangalia kwa namna ya kuwalea  ili kuwaandaa kushika majukumu makubwa zaidi sio kwa maana ya kutaka kuwaadhibu,” ameeleza Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, moja ya majukumu ya Naibu Wasajili ni usimamizi wa masjala na hilo ndilo jukumu kubwa, hivyo wao kama injini ya Mahakama na meneja wa masjala wanapaswa kufahamu vema mwenendo wa masjala zilizopo chini ya usimamizi wao.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewataka Naibu Wasajili hao kudhibiti na kupunguza mlundikano wa mashauri katika Masjala zao huku akiwataka kushughulikia ipasavyo mashauri ya mirathi na mashauri ya watu wengine dhaifu katika jamii (vulnerable groups) yanashughulikiwa na kuhitimishwa mapema ipasavyo na kwamba zipo kanuni zilizotungwa na Jaji Mkuu kwa ajili hiyo.

“Na ni kwa sababu hiyo nimewasomea Zaburi ya 82:2-4, kwa hiyo sio suala la Zaburi tu, hata sisi tumetambua; zipo kanuni zilitungwa na Jaji Mkuu kwa ajili ya kuzingatia makundi hayo, hivyo mashauri ya mirathi na mengine ya aina hiyo yanayohusu watoto, masuala ya ndoa na masuala mengine, mmeshika hapa misaafu wengine Biblia, mimi ningependa kipimo chenu kiwe ni kwa namna gani mnamtendeka haki huyu mtu ambaye ni maskini, wajane, watoto na hasa wanaochukuliwa kuwa dhaifu kutokana na hali yao katika jamii. Haina maana tutawapendelea hapana lakini tusiwadhulumu haki zao kwa sababu ya hali zao,” amesema.

Mhe. Masaju ametoa rai kwa Wasajili hao kuendelea kuwa wanyenyekevu, huku akisema kuwa, kipimo cha mtu kipo katika mambo mawili, mosi anapopata mali na anapopata Madaraka.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amewataka Naibu Wasajili hao kuwasimamia vizuri Mahakimu wa Mahakama za Wilaya na kuhakikisha pia wao nao wanawasimamia vizuri Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo.

“Tutatengeneza vigezo vya kuwapima kwenye miezi hii sita, na ni pamoja na kigezo hiki cha ni kwa namna gani mnazisimamia hizo masjala zilizopo chini yenu, kuna ufanisi kiasi gani kwahiyo haya yaangalieni sana.

Aidha, Mhe. Masaju amewataka Naibu Wasajili hao kuimarisha usimamizi na ukaguzi wa shughuli za kimahakama ili kubaini na kuondoa vikwazo vinavyochelewesha usikilizaji wa mashauri.

“Kama Majaji wenu huko watakuwa na changamoto, tujulisheni lakini hatutaki tushindwe kufanya vizuri kule kwenye Kanda kwa sababu tu ya udhaifu wetu sisi yaani ninyi Wasajili, tekeleza wajibu wako ya Jaji tutayajua tu sisi huku lakini wewe ukiwa umetekeleza wajibu wako. Chukueni hatua haraka pale panapotokea mkwamo katika usikilizaji wa mashauri, lizingatieni sana hili,” amesema.

Vilevile, Jaji Mkuu amesema, usimamizi wa uandaaji wa kumbukumbu za rufaa ni moja ya majukumu ya Naibu Wasajili na hasa rufaa zinazokuja Mahakama ya Rufani, hivyo Wasajili wanaofanya kazi katika Mahakama Kuu watambue kuwa Masjala Ndogo za Mahakama ya Rufani zilizopo katika majengo ya Mahakama Kuu ni za kwao na hivyo majukumu yanayopaswa kutekelezwa katika Masjala Ndogo hzio yanawahusu moja kwa moja.

“Baadhi ya Wasajili wanajiona kama sio wajibu wao kuandaa kumbukumbu za rufaa, kwahiyo hawajishughulishi kwa ufanisi ipasavyo na uandaaji wa hizi rufaa, sasa zinaandaliwa kwa namna ambayo wakati fulani hazikidhi kile kilichotegemewa na matokeo yake inasababisha haki kuchelewa kwahiyo hatutaki kuliendekeza na hatutavumilia ucheleweshaji wa kumbukumbu,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Mahakama itachukua hatua ipasavyo, “na hivi ninavyozungumza nipo katika hatua za kukamilisha marekebisho ya kanuni, tutaweka na muda (timeline) unapaswa kuwa umekamilisha kuandaa kumbukumbu za rufaa na ziwe zimeandaliwa kwa ufanisi ipasavyo zisije zikachelewesha haki kutendeka, hatutavumilia ucheleweshaji wa kumbukumbu za rufaa” amesema Mhe. Masaju.

Vilevile, amewataka Wasajili hao kusimamia ipasavyo utekelezaji wa hukumu za Mahakama kwakuwa eneo hilo lina changamoto huku akisisitiza kwa kusema kuwa, “kuweni makini, na waadilifu katika utekelezaji wa hukumu.”

Aidha ameeleza kuwa, pamoja na kuwepo kwa vitendea kazi vya kawaida kama vile viti, meza majengo na kompyuta vipo vitendea kazi vingine ambavyo ni uwajibikaji kama unavyoelezewa katika Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, uadilifu kama unavyoelezwa katika Sheria za Utumishi wa Umma, kuwiwa kuona haki inatendeka na kuitenda ipasavyo, uwezo wa kumudu utendaji kazi wa majukumu ya kila siku, kujituma, ubunifu katika kutatua changamoto, kuzingatia maslahi ya Umma na Taifa pamoja na kuzingatia ukweli na uhalisia bila kupendelea upande wowote.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amesema kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kuwa na mchango mkubwa na wa pekee katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ambayo inasisitiza kuhusu utawala bora na amani ya jamii, Naibu Wasajili hao watambue kuwa taifa haliwezi uwa na na maendeleo bila kuwa na amani hivyo wanapaswa Kutenda wakizingatia utawala wa sheria kama ilivyoelezwa katika Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Vilevile Mhe. Masaju amewataka Naibu Wasajili hao kuendelea kuwaheshimu wake na waume zao bila kujali dhamana na cheo walichokipata “endeleeni kuwa waadilifu kwa wenza wenu, msiwadharau wenza wenu kwa ajili ya vyeo mlivyovipata” amesisitiza Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Naibu Wasajili wapya leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama mara baada ya Wasajili hao kuapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Naibu Wasajili wapya walioapishwa leo tarehe 17 Juni, 2026 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakifuatilia kwa umakini hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).



Sehemu ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na wageni wengine waliohudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya wakifuatilia hotuba iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).

Sehemu ya Naibu Wasajili wapya kati ya 31 wakila kiapo kushika wadhifa huo mbele ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto). Uapisho huo umefanyika leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya 31 walioapishwa leo tarehe 17 Juni, 2026 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wapya (waliosimama) walioapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania (waliosimama) ambao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Naibu Wasajili wa Mahakama (waliosimama) ambao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (waliosimama) ambao nao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya ndugu, jamaa na marafiki (waliosimama) wa Naibu Wasajili wapya waliopishwa  ambao wamehudhuria katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Amir Mruma, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiteta na kufurahia jambo na mtoto ambaye naye ameshiriki katika hafla ya uapisho wa Naibu Wasajili wapya leo tarehe 17 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama)











JAJI KIONGOZI AWATAKA NAIBU WASAJILI WAPYA KUTOBWETEKA

Na HABIBA MBARUKU- Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amewataka Naibu Wasajili wapya 31 kutobweteka na kutowaangusha Viongozi waliowaamini kutekeleza jukumu la utoaji haki kupitia nafasi hizo.

Mhe. Siyani ameyasema hayo baada ya kuwaapisha Naibu Wasajili hao leo tarehe 17 Juni, 2026 katika Ukumbi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

“Sisi tunaofanya kazi katika Mahakama ya Tanznaia ni Watumishi wa Serikali. Nafasi tunazozipata, ziwe ni nafasi za ajira au nafasi za uongozi kama hizi, ni nafasi ambazo wenzetu wengi zaidi ya milioni 60 hawajabahatika kuzipata, ni nafasi ambazo zinabeba dhamana kubwa, kwa hiyo nitumie nafasi hii kuwasihi sana kutobweteka,” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Ameongeza kuwa Naibu Wasajili wa Mahakama ndio injini, moyo na uhai wa Mahakama, hivyo watakapokwenda katika maeneo ambayo watapangiwa watambue kuwa wamebeba matarajio ya wale waliowaamini, kwa niaba ya Watanzania wote.

Amesema kuwa katika Taasisi, zipo changamoto ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu na kwamba wao wanatarajiwa kwenda kuzifanyia kazi, huku akibainisha moja ya changamoto inayoikabili Mahakama ni watu kutoridhika na huduma za Mahakama, licha ya uwepo wa takwimu zinazoonesha kuridhika kwa Wananchi, hivyo wanapaswa kuwajibika bila kubweteshwa na takwimu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Siyani amewataka Naibu Wasajili wapya kufanya kazi bila hofu, huku wakitenda haki, kwa kuzingatia Katiba, Sheria mbalimbali, mila na desturi pamoja na maelekezo ya Viongozi. Amewaeleza kuwa wasiwe na hofu katika kutekeleza majukumu yao kwa sababu wanatarajiwa kwenda kuwahudumia watu, na wanapaswa kuwa na hofu na Mungu pekee ambaye wameapa kwake.

“Msiende kupeleka hofu zenu kazini, mnatarajiwa kwenda kuwahudumia watu na mkiwa na weledi hakuna sababu ya kuwa na hofu, timizeni majukumu yenu vile inavyotarajiwa, hofu itawafanya mkosee, hofu yenu iwe kwa Mungu ambaye mmeapa kwake, msipoweza kudhibiti hali hiyo mtakosea. Katika zama tulizonazo haitajariwi Maaoisa wenye hadhi yenu kufanya makosa yasiyotarajiwa….mkachape kazi,” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Ameongeza kuwa miezi sita ijayo itakuwa miezi ya matazamio, hivyo wakienda kubweteka watakosa sifa za kuendelea kuwa Naibu Wasajili kwa sababu uvivu na ukosefu wa weledi ni vitu ambavyo havina nafasi ya kuvumiliwa katika nyakati za sasa na kuwa kila mtu atapimwa kwa haki juu ya namna anavyofanya kazi.

Jaji Kiongozi amewatakiwa kila la heri, huku akiwakumbusha kuiishi kauli mbiu ya Mahakama inayosema, “Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji,” akieleza kuwa mambo hayo matatu ndio masingi wa utendaji ulio imara.

Amesema kwamba atakayekosa uadilifu, weledi na kushindwa kuwajibika atakuwa amepoteza sifa ya kuwa Naibu Msajili, hivyo wawe kundi la mageuzi na kundi ambalo litaleta taswira ya kuwa hakukuwa na makosa kwenye kuweka imani kwao.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza baada ya kuwaapisha Naibu Wasajili hao leo tarehe 17 Juni, 2026 katika Ukumbi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

Sehemu ya Naibu Wasajili wapya wakimsikiliza Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, baada ya kuwaapisha.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).


Sehemu ya Wananchi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).


Sehemu nyingine ya Wananchi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).


Sehemu nyingine ya tatu ya Wananchi, Watumishi wa Mahakama na Tume ya Utumishi wakiwa kwenye uapisho huo (juu na chini).

(Picha na Mary Gwera na Halima Mnete-Mahakama, Dodoma.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.)