Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya
Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amesema kuwa, Mahakama ni mali ya wananchi na
kwamba Mahakama hizo zipo kwa ajili kuwahudumia wananchi.
Mhe. Mahimbali ambaye alikuwa Mgeni Rasmi wakati wa
hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya tatu za Ketembeine, Makuyuni na Terrat zilizopo
mkoani Arusha uliofanyika tarehe 10 Aprili 2026 katika Mahakama ya Mwanzo
Makuyuni wilayani Monduli.
Jaji Mfawidhi huyo alisisitiza kuwa, tukio hilo la
uzinduzi na urasimishaji wa Mahakama hizo ni hatua muhimu katika kuimarisha
upatikanaji wa haki kwa wananchi wote wa Tanzania na ujenzi wa Mahakama hizo ni
matunda ya dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa, wananchi wote wanapata haki
mapema ipasavyo na kwa gharama nafuu.
“Kwa muda mrefu, wananchi wa maeneo hayo wamekuwa
wakisafiri umbali mrefu kufuata huduma za Mahakama, kwa mfano; wananchi wa Kata
za Makuyuni, Mswakini, Esiraeli na Nanja walikuwa wakisafiri umbali wa kilomita
36 kwenda katika Mahakama ya Mwanzo Mto wa Mbu au kusafiri kilomita takribani
70 kwenda katika Mahakama ya Mwanzo Kisongo iliyopo Monduli mjini ili kupata
huduma, hivyo ujenzi wa Mahakama hizi umesogeza huduma kwa wananchi hao,”
alisema Jaji Mahimbali.
Vilevile Mhe. Mahimbali aliongeza kuwa, kusafiri
umbali mrefu kufuata huduma za Mahakama kulisababisha baadhi ya wananchi kukata
tamaa na kuacha kufuatilia mashauri yao na hivyo kupoteza haki zao. Pia
wananchi wengine walikuwa wakiamua kujichukulia sheria mkononi mwao, hivyo
Mahakama hizo zinazozinduliwa zinakwenda kuhudumia jamii zinazozizunguka
Mahakama hizo kwa kusogeza huduma karibu na makazi yao na hivyo kurahisisha
upatikanaji wa haki na kupunguza muda wa kupata haki, hivyo kutumia muda wao
mwingi katika shughuli za kiuchumi na kujiongezea kipato.
Jaji Mahimbali amewashukuru wadau wa Mahakama hususan
Halmashauri za Wilaya Arusha, Monduli na Longido wa kushiriki kikamilifu
kufanikisha ujenzi wa Mahakama hizo mpya na kuongeza kuwa, ushirikiano huo ni
kielelezo cha dhana ya kwamba ‘Mahakama ni ya Wananchi na kwa Wananchi.’
Amesisitiza kuwa huduma zitakazopatikana katika majengo hayo ya Mahakama ziwe
ni kwa ajili ya maslahi mapana ya wananchi na si vinginevyo.
Aidha, ameongeza kwa kuwataka wananchi na watumishi wa
Mahakama kutumia Mahakama hizo kwa malengo yaliyokusudiwa, huku akiwasisitiza
wananchi kuwa, wanao wajibu wa kutambua kuwa majengo hayo ni mali yao na kuwa sehemu
ya maisha yao ya kila siku na kuyalinda ikiwa ni pamoja na kuyaheshimu.
Kwa upande mwingine, Jaji Mfawidhi huyo amewasisitiza
watumishi wa Mahakama hususan Mahakimu kwamba wanapaswa kuyatumia majengo hayo
kama nyenzo ya kuimarisha imani ya wananchi kwa mfumo wa utoaji haki nchini.
Akiwasilisha taarifa fupi ya ujenzi wa Mahakama hizo,
Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama
alisema kuwa, ujenzi wa Mahakama hizo ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango
Mkakati wa kwanza na wa pili wa Mahakama uliolenga kuboresha upatikananji na
utoaji haki mapema ipasavyo kupitia uboreshaji wa Miundombinu ya Majengo na
Mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mijini na vijijini.
Bi. Kapama aliongeza kuwa jumla ya miradi minne ya
ujenzi ilitekelezwa, yaani ujenzi wa Mahakama za mwanzo Maji ya Chai, Terat,
Makuyuni na Ketumbeine. Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine ilijengwa kwa fedha za
ndani wakati mahakama hizo nyingine zilijengwa kwa fedha za mkopo kutoka Benki
ya Dunia.
Bi. Kapama alisema kuwa, ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni
na Terrat ulianza tarehe 06 Julai, 2024 na kukamilika tarehe 31 Mei, 2025.
Ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine ulianza 01 Juni, 2024 na kukamilika 06
Oktoba, 2025.
Mahakama za Mwanzo Makuyuni na Terrat zimeanza kutoa
huduma kwa wananchi mnamo mwezi Agosti, 2025 na Mahakama ya Mwanzo Ketumbeine
ilianza kutoa huduma kwa wananchi tarehe 22 Oktoba, 2025.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Groliana Kimathi
alisema kuwa, Serikali itaendelea kuhakikisha kuna amani na usalama ili
kuwezesha shughuli mbalimbali za Kiserikali na wananchi kufanyika katika hali
tulivu. Ameishukuru Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo
zilizozinduliwa na kuongeza kuwa, ujenzi
wa Mahakama hizo ni ishara ya dhati ya Serikali kuwajengea mazingira mazuri
watumishi wa Mahakama katika kutekeleza majukumu yao na kutoa huduma kwa
wananchi.
Aidha, amewasihi watumishi wa Mahakama kuendelea
kufanya kazi kwa weledi na kujiepusha na vitendo vya rushwa ambavyo vinaweza
kutia doa Mhimili wa Mahakama.
Mkuu huyo wa Wilaya ameahidi kuendelea kutoa
ushirikiano kwa Mahakama katika kutekeleza majukumu yote ambayo yapo kwa mujibu
wa taratibu zilizopo. Aidha, ameiomba Mahakama kuendelea kutenga siku maalum ya
kutoa elimu ya sheria kwa wananchi kwani itasaidia kupunguza ukiukwaji wa
sheria miongoni mwa wananchi na hatimaye kuwa na jamii iliyostaarabika.
Akizungumza katika hafla hiyo, Diwani wa Kata ya
Makuyuni, Mhe. Ngayok Mollel ameishukuru Serikali kwa kuwaletea Mahakama katika
Kata yao na kuongeza kuwa, wananchi wa Kata yake katika vijiji vya Makuyuni,
Mbuyuni na Naiti ikiwa ni pamoja na Kata za jirani wanafurahia kupata huduma
katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni kwani ni karibu na makazi yao.
Uzinduzi wa Mahakama hizo unafanya jumla ya Mahakama
za Mwanzo zinazofanya kazi mkoani Arusha kufikia 22 na hivyo kupanua wigo na
kusogeza karibu utoaji wa huduma za Mahakama kwa wananchi katika Wilaya ya
Arusha, wananchi wa Kata za Murieti, Terrat, Sombetini, Mbauda, Eleroi, Sokoni
1 na Olasiti ambao walikuwa wakisafiri
umbali wa takribani kilomita 19 hadi 23 kufuata huduma katika Mahakama za
Mwanzo Arusha Mjini na Themi, sasa wamesogezewa huduma karibu yao kwa kujengewa
Mahakama ya Mwanzo Terrat.
Pia, Katika Wilaya ya Longido, wananchi wa Kata za
Ketumbeine, Lang’atabash, Elerininto, Nondoto, Gelarirumbwa na Gelarimerugwe
walikuwa wakisafiri umbali wa Kilomita 50 kufuata huduma za Mahakama ya Mwanzo
Longido Mjini, kwa sasa wanapata huduma hizo katika Mahakama ya Mwanzo
Ketumbeine.
Hafla hiyo ya uzinduzi rasmi wa Mahakama za Mwanzo
mpya mkoani Arusha imehudhuriwa na Viongozi na Wadau mbalimbali wa Mahakama
wakiwemo Majaji na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Arusha, Mkuu wa Wilaya ya
Monduli, Mahakimu, Viongozi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Diwani wa
Kata ya Makuyuni, Viongozi wa Dini, Viongozi wa Kimila na wananchi kwa ujumla.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe.
Frank Mahimbali akizungumza na wananchi pamoja na wadau waliohudhuria katika hafla
ya uzinduzi wa Mahakama mpya za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni iliyopo wilayani
Monduli.
Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Gloriana Kimath
akitoa salamu kwa wananchi na wadau waliofika katika hafla ya uzinduzi wa
Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10
Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli.
Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Bi. Grace
Kapama akisoma historia fupi ya ujenzi wa Mahakama hizo wakati wa hafla ya uzinduzi
wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo
Makuyuni.
Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Bi. Grace
Kapama (kushoto) akikabidhi taarifa fupi ya historia ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni,
Ketumbeine na Terrat kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kanda ya Arusha, Mhe. Frank
Mahimbali wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo uliofanyika tarehe 10
Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe.
Frank Mahimbali (kushoto picha ya chini) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli. Picha ya juu akiwa na viongozi mbalimbali walioalikwa katika hafla hiyo.
Wananchi na wadau mbalimbali waliohudhuria hafla ya
uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika
tarehe 10 Aprili 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wilayani Monduli.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe.
Frank Mahimbali akipanda mti ikiwa ni ishara ya kumbukumbu na sehemu ya kuboresha mazingira
ya Mahakama ya Mwanzo Makuyuni wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat iliyofanyika tarehe 10 Aprili, 2026.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali (katika) pamoja na Majaji wengine wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Gloriana
Kimathi (wa pili kushoto mstari wa mbele) wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi
wa Mahakama za Mwanzo mpya za Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10
Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni Monduli. Waliosimama nyuma ni kulia Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Dkt. Kassian
Mshomba na kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace
Kapama.
Majaji wa Mahakama Kuu Arusha wakiwa
katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi
rasmi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe
10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Makuyuni Monduli.
Diwani wa Kata ya Makuyuni, Mhe. Ngayok Mollel
akitoa salamu za wananchi wa Kata ya Makuyuni wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi
wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10
Aprili, 2026 Makuyuni Monduli.
Kiongozi wa Mila wa Kabila la Maasai Monduli, Bw.
Samwel Laiza akisoma dua wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa Mahakama
za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika tarehe 10 Aprili, 2026 Makuyuni Monduli.
Kikundi cha Burudani cha Kabila la Wamaasai kutoka
Makuyuni Juu kiitwacho Nashpai Eko kikitumbuiza wakati wa hafla fupi ya
uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Makuyuni, Ketumbeine na Terrat uliofanyika
tarehe 10 Aprili, 2026 Makuyuni Monduli.
Jengo la Mahakama ya Mwanzo Makuyuni moja kati majengo ya Mahakama za Mwanzo mpya tatu zilizozinduliwa.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)