Na
SETH KAZIMOTO, Mahakama -Arusha
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha na Mgeni Rasmi wa Maadhimisho
ya Siku ya Sheria nchini kwa Kanda hiyo, Mhe. Frank Mahimbali amesema kuwa
lazima Mahakama iwe thabiti na imara kiasi cha kuaminiwa na wananchi na hatimaye
kuwa kimbilio la wanyonge.
Jaji
Mahimbali aliyasema hayo tarehe 02 Februari, 2026 wakati wa Maadhimisho ya Siku
ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji
Haki (IJC) Arusha.
“Tuendelee
kuimarisha Mahakama zetu ili ziwe chombo cha kuaminika, kuheshimika, chenye
uadilifu na mchango wa moja kwa moja katika ustawi wa Taifa letu” aliongeza
Jaji Mahimbali.
Jaji
Mfawidhi aliwakumbusha Viongozi wa Serikali wanaohusika na utekelezaji wa amri
za Mahakama kuhakikisha wanatekeleza amri hizo bila kuweka vikwazo ili
kuwapatia haki wananchi husika mapema ipasavyo na hatimae kuharakisha maendeleo
ya watu na taifa kwa ujumla.
Mhe.
Mahimbali aliahidi kuwa, hatakuwa na uvumilivu kwa Kiongozi yeyote ndani ya
Kanda ya Arusha atakayedharau amri za Mahakama na kushindwa kuzifanyia
utekezaji wakati ni wajibu wake kufanya hivyo.
Maadhimisho
hayo yaliyokuwa na Kaulimbiu isemayo, ‘Mchango wa Mahakama katika Ustawi wa
Maendeleo ya Taifa,’ Jaji Mahimbali aliongeza kuwa, mchango wa Mahakama katika
maendeleo ya Taifa ni wa msingi na wa kudumu kwani Mahakama ni nguzo ya haki,
demokrasia na utawala bora pia ni chombo kinacholinda amani, kukuza uchumi na
kulinda haki za kiraia hivyo, alisisitiza kwamba, ni muhimu kwa Mahakama nchini
kuwa taa ya mwanga katika giza la dhuluma.
Akizungumzia
kuhusu Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Jaji Mahimbali alisema kuwa,Mahakama ni
nguzo muhimu kwa kuhakikisha kuwa upo utawala wa sheria, haki na uwajibikaji
ambavyo ni msingi wa uchumi imara, amani ya kijamii na maendeleo jumuishi na
kwamba bila Mahakama huru, inayoheshimika na yenye ufanisi, malengo ya Dira ya Maendeleo
hayawezi kufikiwa.
Katika
hotuba ya Mwanasheria wa Serikali mkoani Arusha, Bi. Veritas Mlay alisema kuwa Siku
ya Sheria nchini ni siku muhimu na ya kipekee ya kufanya tafakuri ya kitaifa
ambapo wanakumbushwa dhima na wajibu wao wa pamoja katika kulinda haki, amani,
usawa na utawala wa sheria kama nguzo na nyenzo katika kufikia ustawi na
maendeleo ya Taifa.
Mwanasheria
huyo wa Serikali aliongeza kuwa, Tanzania imejikita katika kufanya maendeleo
yanayodhihirishwa na uwepo wa miradi mikubwa ambayo imekamilika na ile ambayo
ipo katika hatua mbalimbali za ukamilishaji katika Sekta mbalimbali ikiwemo
uchumi, ujenzi, nishati, madini na huduma za jamii.
Bi.
Mlay alisisitiza kuwa, uwepo wa miradi hiyo ya maendeleo ni ushahidi tosha wa
ushirikiano baina ya Serikali, Mahakama na Bunge, na kwamba Serikali imeweka mazingira
rafiki na ya kuvutia uwekezaji na hivyo kukuza uchumi na maendeleo ya nchi
kupitia uingizaji wa mitaji na teknolojia na upatikanaji wa ajira.
Kadhalika
Mwanasheria huyo alisema kuwa, Mahakama kama mlinzi wa Katiba, haki na utawala
wa sheria, ni nguzo muhimu katika kukuza na kuendeleza ustawi na maendeleo ya Taifa.
“Mahakama
iliyo huru na inayoheshimika na kuaminika huhakikisha utekelezaji thabiti wa
mikataba, ulindaji wa haki za mali na kudhibiti matendo ya matumizi mabaya ya
madaraka na hatimaye kukuza imani ya wawekezaji na hivyo kuwezesha ukuaji imara
na endelevu wa uchumi wa Taifa,” alisema Bi. Mlay.
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Hamisi
Mkindi alisema kuwa, Kaulimbiu ya Siku ya Sheria mwaka huu inaakisi ukweli
kwamba hakuna maendeleo ya kweli bila ulinzi wa haki, utawala wa sheria na
utawala bora hivyo Mahakama ndicho chombo pekee ambacho huamua mwelekeo wa
haki, uaminifu na utulivu wa kitaifa.
“Taifa
linapokuwa na mfumo wa utoaji haki unaoaminika, unaofanya kazi kwa ufanisi na
unaoweka mbele maslahi ya wananchi bila upendeleo, dhuluma wala hiyana na
kuleta hali ya watu kuwa na matumaini, basi ustawi wa kiuchumi, kijamii na
kisiasa huimarika na maendeleo ya kweli huonekana,” alisisitiza Wakili Mkindi.
Aliongeza
kuwa, ni wajibu wa Mahakama kulinda na kusimamia haki za binadamu na kwamba
jukumu hilo si la Mahakama pekee bali ni pamoja na Wadau wote wa Mahakama ambao
ni Wadau wa haki. Alisema kwamba, haki inapaswa kutolewa bila ubaguzi kama
ilivyoainishwa na Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
toleo la 1977.
Naye
mgeni maalum wa Maadhimisho hayo mkoani Arusha ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa wa
Arusha, Mhe. CPA Amos Makalla alisisitiza kuwa ipo haja kwa Wadau wa Sheria
kutoa elimu kwa wananchi juu ya majukumu ya Mihimili ya Serikali ili wajue ni
aina gani ya lalamiko au huduma inatakiwa kuwasilishwa kwenye Mhimili gani ili
suala hilo liweze kupatiwa ufumbuzi.
Vilevile, Mhe. Makalla aliwaasa Mawakili wa Kujitegemea
kutojihusisha na vitendo vya udanganyifu ambavyo vinaleta migogoro na usumbufu
kwa wananchi.
Aidha,
Mkuu huyo wa Mkoa wa Arusha ameahidi kutoa ushirikiano kwa wadau wote wa haki,
hususani katika kuhakikisha amri za Mahakama zinaheshimika na kutekelezwa kama
taratibu zinavyoelekeza.
Maadhimisho
ya Siku ya Sheria nchini yahudhuriwa na Viongozi wa Taasisi mbalimbali mkoani
Arusha zikiwemo vyombo vya Ulinzi na Usalama, Vyuo, Shule, TAKUKURU, Vyama vya Kiraia,
Viongozi wa Dini na Sekta Binafsi.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akizungumza na Watumishi, Wadau na Wananchi
waliohudhuria katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika
viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha akikagua gwaride maalum kuashiria uzinduzi wa mwaka mpya wa Mahakama wakati wa Maadhimisho
ya Siku ya Sheria nchini ambayo kwa upande wa Arusha yalifanyika katika viwanja vya Kituo
Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.
Mkuu
wa Mkoa wa Arusha na Mgeni Maalum wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini mkoani humo, Mhe. CPA Amos Makalla akiwasalimia Wadau wa Sheria na
wananchi waliohudhuria kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.
Mwenyekiti
wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) mkoani Arusha, Wakili Msomi Hamisi
Mkindi akisoma hotuba ya Chama hicho wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria
nchini zilizofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji
Haki (IJC) Arusha.
Mwanasheria
wa Serikali Mkoa wa Arusha, Bi. Veritas Mlay akisoma hotuba ya Ofisi ya
MwanAsheria Mkuu wa Serikali wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini
yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki
(IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.
Wadau
na wananchi waliohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini
yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki
(IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.
Naibu
Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi na Mhe. Elia Mrema
wakishiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini
yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki
(IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali (katikati)
akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Arusha (walioketi)
pamoja na Majaji wastaafu (waliosimama) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya
Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha
Utoaji Haki (IJC) Arusha. Wa tatu kushoto ni Mkuu
wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Makalla.
Picha za pamoja za makundi mbalimbali ya washiriki waliohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa upande wa Arusha.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)