Jumamosi, 9 Mei 2026

BSAAT YAKABIDHI VIFAA VYA TEHAMA MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI KISUTU

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Kisutu

Mradi wa Mfumo Endelevu wa Kupambana na Rushwa Tanzania (BSAAT), hivi karibuni umekabidhi vifaa mbalimbali vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.

Hakimu Mkazi Mkuu na Afisa Mwambata wa BSAAT, Mhe. Richard Kabate, alikabidhi vifaa hivyo kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, huku zoezi hilo likishuhudiwa na   Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Bi. Athanasia Kabuyanja.

Watumishi wengine wa Mahakama waliokuwepo wakati wa makabidiano hayo ni Ofisa Utumishi Mwandamizi, Bw. Nkruma Katagira, Mhasibu Mwandamizi, Bi. Prisca Gideon na Ofisa TEHAMA wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Bw. Winfred Nzilano.

Vifaa vilivyokabidhiwa ni Kompyuta Mpakato tano (5) aina ya HP Omnibook X Flip, Begi za Kompyuta Mpakato (Laptop bag) tano (5), Adapta (Type C to HDTV 11 in 1 Adapter) na Vipanya vya Kompyuta (wireless mouse) tano (5) na Vipanga Njia (Portable router) tano (5).

Akizungumza waakati wa zoezi hilo, Mhe. Kabate aligusia umuhimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi katika mapambano dhidi ya rushwa na kwamba Mahakama ya Kisutu imekuwa ikipokea kesi nyingi ambazo zinahusiana na maswala ya rushwa.

Hivyo, alibainisha kuwa makabidhiano hayo ni katika kuhakikisha uondoaji wa mianya ya rushwa katika mifumo ya Mahakama na kuongeza wigo wa kushughulikia mashauri ya rushwa.

Naye Hakimu Mfawidhi aliushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuona kwamba inafaa kuwaletea vitendea kazi. Alisema watavitumia vifaa hivyo kuhakikisha mashauli yanamalizika kwa haraka iwezekanavyo kama kauli mbiu ya Mahakama inavyosema.


Hakimu Mkazi Mkuu na Afisa Mwambata wa Mradi wa Mfumo Endelevu wa Kupambana na Rushwa Tanzania, Mhe. Richard Kabate (kushoto), alikabidhi vifaa hivyo kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga (katikati). Picha chini, Mhe. Kiswaga akizungumza baada ya makabidhiano hayo.


Picha ya pamoja baada ya makabidhiano hayo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Njombe.

 

KAMATI YA JAJI MKUU UFUATILIAJI NA TATHMINI YAFANYA UKAGUZI MAALUM MAHAKAMA PWANI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza amefanya ukaguzi katika Mahakama za Hakimu Mkazi Pwani, Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mahakama ya Mwanzo Mailimoja ili kufanya tathmini ya usahihi wa taarifa na namna ambavyo Mahakama hizo zinavyofanya kazi.

Akizungumza mara baada ya kuwasili ofisini kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi, tarehe 07 Mei, 2026, Mhe. Khyoza alisema wao sio Wakaguzi wa moja kwa moja bali wao wanaangalia taarifa za ukaguzi zinazowafikia na usahihi wake na kumtaarifu Jaji Mkuu kama mambo yako sawa, akieleza kuwa hilo ni jukumu mojawapo la kamati hiyo.

Akizungumza na watumishi baada ya ukaguzi, Mhe. Kahyoza alisema mara yake ya mwisho kufika kwenye jengo la Mahakama hiyo ni siku jengo lilipokabidhiwa tarehe 21 Septemba, 2016 ambapo amewapongeza wasimamizi wa jengo hilo, wakuwa wameweza kuzingatia usafi wa jengo. Aliongeza kwa kusema, “Kwahiyo nimefurahi kitu cha kwanza kufika kwenye jengo hili tena nikaridhishwa na usafi kweli niwapongeze sana mnaosimamia na mnaofanya usafi wa mazingira na kuyatunza pia.”

Aliendelea kuwapongeza zaidi na kusema kuwa, usafi ni jambo jema linalotia nguvu na kuna kipindi kulikuwa kuna azimio linalozungumzia utunzaji wa mazingira. Amekumbusha pia alikuwa Jaji Mfawidhi Mwanzilishi wa  Mahakama Kuu Musoma walipanda miti ya vivuli na matunda, jambo ambalo Jaji Mkuu wa kipindi hicho ambacho anakabidhi Mahakama Kuu Musoma alisema makabidhiano yaambatane na mazingira safi.

Akiwaeleza watumishi wa Mahakama hiyo, lengo la ujio wake alisema wao kazi yao kubwa wanaangalia namna Wakaguzi wanavyokagua ili kuona wanachowaambia kama ni sahihi pia wataangalia namna Mahakama za Mwanzo zinavyofanya kazi ili kile wanachoambiwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi kama ni sahihi.

Amesema pia, wameona rejesta ya malalamiko kwenye shughuli za kiutawala japo kwenye masuala ya pesa hawaingii huko sana japo wameona taarifa ya utekelezaji. Alibainisha kuwa, utekelezaji wa Mpango Mkakati hauwezi kufanikiwa bila kujua bajeti na Nguzo ya Kwanza ya mpango huo ambayo ni Usimamizi wa Rasilimali za Mahakama.

Ameongeza kwamba, wakati anasimamia mambo ya utawala alikuwa anatumia neno GAP ambapo ameeleza kuwa, ukilijua neno hilo unaweza kuujua Mpango Mkakati wa Mahakama kwa urahisi.

Akieleza maana ya neno (GAP), Mhe. Khyoza amesema “G inasimamia (Governance) Usimamizi wa rasilimaliwatu, rasilimali fedha na utawala, A inasimamia nguzo ya (Access to Justice and Expeditiousness) na P ni (Public Trust and Stakeholders’ Engagement).

Amesema kuwa, mtu hawezi kuzitekeleza nguzo hizo bila mambo ya utawala kukaa vizuri, kuwepo na pesa bila usimamizi mzuri zitaishia kufanya vitu visivyoeleweka. Pia majengo yasipotunzwa vizuri Jaji au Hakimu hawezi kuendesha mashauri lakini pia haki za watumishi zisipolipwa na kuandaliwa vyeo kupanda pia haiwezekani kufanya kazi vizuri.

Amebainisha kuwa, “Nguzo ya ‘Access to Justice’ ndio nguzo mama kila siku tunashinda nayo.”

Pamoja na ukaguzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya, Jaji Kahyoza amekagua pia Mahakama ya Mwanzo Mailimoja, ambapo amewashauri Mahakimu wakichapa mwenendo wa mashauri wahifadhi katika Kompyuta ya Masjala na sehemu nyingine. Hiyo itasaidia hata kama haiwezi kupatikana sehemu mojawapo basi itapatikana sehemu nyingine.

Amesema kuwa, kitendo cha mtu mmoja kukaa na mwenendo si kizuri, ikitokea amehama anaweza kuondoka na mwenendo na wakati mwingine inaweza ikawa ngumu kupatikana.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kahyoza amewapongeza Mahakimu wa Mahakama hiyo kwa kuwahi kufika kazini maana matarajio yake ilikuwa ni kufika saa tatu asubuhi hivyo alitoka mapema sana kuogopa foleni lakini hakukuta foleni na kuwahi kufika tofauti na muda lakini aliwakuta Mahakimu na watumishi wengine tayari wameshafika ofisini.

Akizungumza wakati wa kumkaribisha Mjumbe wa Kamati ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Jaji Mkuu, Ofisa kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Mhe. Elias Migella amesema majukumu ya Kamati hiyo ni kufanya ufuatiliaji na tathmini ya huduma katika masuala ya kimahakama na kiutawala. 

Kadhalika, Mhe. Migella alizungumza na watumishi  wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Kamati ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Jaji Mkuu ina wajumbe nane ambao watatembelea Mahakama nchi nzima kwa lengo la kufanya ukaguzi na kurejesha taarifa kwa Jaji Mkuu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza (kulia) akiwasili Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani tarehe 07 Mei, 2026 tayari kwa kuendelea na jukumu la ukaguzi katika Mahakama hiyo. Kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi akimuongoza Jaji Kahyoza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza akisaini kitabu cha wageni alipowasili kwenye Ofisi ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi-Pwani.

Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini ykutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Bw. Elias Migella akimkaribisha Mhe. John Kahyoza ili azungumze na watumishi (hawapo katika picha). 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati  ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathimini, Mhe. John Kahyoza akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani na Mahakama ya Wilaya Kibaha mara baada ya ukaguzi katika Mahakama hizo. Kulia ni Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini ykutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Bw. Elias Migella na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi. 

Baadhi wa watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati  ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathimini, Mhe. John Kahyoza (hayupo katika picha).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza (katikati)  akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi wa Mahakama ya Mwanzo Mailimoja. Aliyeasimama kushoto mstari wa mbele ni Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini ykutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Bw. Elias Migella na kulia ni  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi. 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

Ijumaa, 8 Mei 2026

JAJI MFAWIDHI KATAVI ASISITIZA MATUMIZI YA TEHAMA MAHAKAMA ZA MWANZO

Na. ALLY RAMADHANI – Mahakama, Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi, Mhe. Godfrey Ntemi Isaya amewasisitiza watumishi wa Mahakama za Mwanzo katika Masjala hiyo kutumia Mifumo ya TEHAMA katika shughuli zao za kiutendaji.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Mhe. Isaya alipokuwa kwenye ziara yake ya ukaguzi wa Mahakama ili kuangalia utendaji kazi wa kila siku wa utoaji huduma za haki kwa wananchi, ziara hiyo ya ukaguzi ilifanyika kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026 hadi 07 Mei 2026 katika Wilaya za Mpanda, Mlele na Tanganyika.

Katika ziara hiyo, Mhe. Isaya alifanikiwa kutembelea Vituo vyote vya Mahakama za Mwanzo zinazoendelea kujengwa ndani ya Mkoa wa Katavi kama vile Sibwesa, Ugalla na Mamba na kupata wasaa wa kuwasisitiza watumishi wa maeneo hayo kuendeleza na mapambano ya matumizi ya TEHAMA ili kurahisisha utoaji haki kwa wananchi wanaowahudumia.

Kupitia ziara hiyo Mhe. Isaya aliwakumbusha watumishi wa Mahakama za Mwanzo mkoani Katavi kuendelea kutumia Mifumo ya TEHAMA ikiwemo Primary Court App, ili kurahisha utendaji kazi wa Mahakama kwa ujumla.

Aidha, Mhe. Isaya aliongeza kuwa, kazi ya kutoa haki sio jambo dogo hivyo watumishi wasijiingize katika vitendo viovu vinavyoweza kuharibu taswira ya Mahakama na kupunguza imani kwa wananchi,

“Ndugu watumishi nawasisitiza kuwa waadilifu kwa kuwa ndiyo msingi mkubwa wa kutoa haki, hivyo muwe na tabia njema kazini na nje ya kazi na tuendelee kuchapa kazi tuwatumikie wananchi, tuepuke ile hali ya kuwa miungu watu kwenye ofisi zetu na kuongeza kuwa, kila mmoja kufanya kazi kwa bidii na umoja “If people cannot pay you, the nature will,” alisema Jaji Isaya.

Kwa upande mwingine, Mhe Isaya aliwapongeza watumishi wote kwa ujumla kwa kazi nzuri inayofanyika hususani usikilizwaji wa mashauri kwani katika taarifa zote zilizowasilishwa zimeonyesha kuwa mashauri yanafunguliwa na yanaisha kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (katikati) akiwa kwenye Picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali wa Masjala hiyo alipotembelea jengo la Mahakama ya Mwanzo Wilaya Mpanda Kituo  cha Ugalla.

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi, Mhe. Silivia S. Lushasi (aliyesimama) akiongea na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Wilaya Mpanda kituo cha Mpanda Mjini alipokua kwenye ziara ya Mhe Jaji Mfawidhi Kanda ya Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (wa kwanza Kulia mwenye suti nyeusi) akikagua baadhi ya mipaka ya eneo la Mahakama ya Mwanzo Wilaya Mpanda Kituo cha Shanwe.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)





MAHAKIMU NJOMBE PUNGUZENI KUKAA NA MASHAURI MAHAKAMANI KWA MUDA MREFU; JAJI NONGWA

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe, Victoria Nongwa amewataka Mahakimu wa Mahakama za Wilaya pamoja na za Mwanzo  kutokukaa na mashauri Mahakamani kwa muda Mrefu.

Mhe. Nongwa aliyasema hayo akiwa kwenye ziara ya kikazi aliyoianza tarehe 28 Aprili ,2026 hadi tarehe 4 Mei, 2026, ambapo alisema, “Hakikisheni mashauri yote yanayotokea Polisi yana ushahidi uliokamilika au mashahidi wamepatikana ili mashauri hayo yaweze kusikilizwa na kumalizika haraka ipasavyo na siyo kuchelewesha mashauri hayo bila sababu za msingi na yale mashauri ambayo hayana Mashahidi yasipokelewe mahakamani.”

Aidha, Jaji Nongwa aliwasisitiza Mahakimu kuwa, anatarajia kuona mashauri yanasikilizwa kwa haki, uadilifu na kwa wakati ili kutimiza dhana ya utoaji haki kwa wananchi mapema ipasavyo.

Katika ziara hiyo ya kikazi kwa Mahakama za Wilaya za Ludewa, Wanging’ombe na Makete waliwasilisha taarifa mbalimbali za Mashauri zilizosomwa na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya pamoja na taarifa za Utawala huku Mhe. Nongwa akisikiliza hoja mbalimbali zilizotolewa na watumishi wasio Mahakimu na kuzitafutia ufumbuzi ambazo nyingine zilijibiwa na Viongozi aliombatana nao.

 Akiendelea kuzungumza na watumishi,  aliwasisitiza juu ya umuhimu wa kila mmoja wao kujua  Nguzo Kuu za Mpango Mkakati wa Mahakama na kila mtumishi anatakiwa kujua wajibu wake pamoja na uwajibikaji huku akikemea vitendo viovu vinavyoashiria mazingira ya rushwa pamoja na kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mahakamani.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi huyo aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mtendaji wa Mahakama Kuu Njombe, Bw. Richard Mbambe na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama ambao waliweza kujibu hoja mbalimbali za watumishi pamoja na kutoa neno la shukrani katika ziara hiyo.  


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Wanging'ombe (waliosimama). Wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama na wa pili kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Wanging’ombe, Mhe. James Muhoni.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe(hawapo katika picha) alipofanya ziara katika Mahakama hiyo hivi karibuni.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe,Mhe. Victoria Nongwa (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph Luambano (wa pili kulia), wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe. Matilda Kayombo, wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama, wa pili kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe, Mhe. Godfrey Msemwa na wa tatu kushoto ni anayefata ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Bw,Richard Mbambe na waliosimama nyuma ni sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini. Kutoka kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini, Mhe. Lisa Abel  anayefuata ni Mtumishi aitwaye Bi. Beatrice Liahumi,  nyuma ya kiti upande wa kulia ni Mwandishi Mwendesha Ofisi, Bi. Agusta Msingwa akiwa pamoja na Mwenzake  Mwandishi Mwendesha Ofisi Bi.Sofia Kimena ambapo viti vya nyuma  kulia ni Watumishi wa Mahakama, Bw. Justin Kiduli pamoja na Hashimu.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania ,kanda ya Njombe,Mhe, Victoria Nongwa (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Njombe wakiwa katika picha ya pamoja na  sehemu ya watumishi wa Mahakama ya wilaya Makete.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania ,kanda ya Njombe,Mhe, Victoria Nongwa (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Njombe wakiwa katika picha ya pamoja na  sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Manda alipofanya ziara katika Mahakama hiyo hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa akimwagilia Mche wa Mparachichi mara baada ya kuupanda katika viunga vya Mahakama ya Wilaya Wanging’ombe alipofanya ziara katia Mahakama hiyo hivi karibuni.  Kushoto ni Ofisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Wanging’ombe,  Bw.Riziki Sanga.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

Jumatano, 6 Mei 2026

BARAZA LA WAFANYAKAZI MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO SINGIDA LAKETI

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo  ya Singida na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama hiyo, Mhe.Ayoub Mwenda ameongoza  kikao cha Baraza la Wafanyakazi ambapo amewasihi Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kutumia vizuri fursa ya kikao hicho kuchangia hoja na kutoa mapendekezo mbalimbali yatakayoboresha mazingira ya kazi.

Akifungua kikao hicho kilichofanyika tarehe 02 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu ya Singida, Mhe. Mwenda alisema kuwa, Mabaraza ya Wafanyakazi yapo kisheria na yana umuhimu mkubwa katika kulinda haki na maslahi ya watumishi mahala pa kazi sambamba na kuleta amani na utulivu mahali pa kwa kazi kwa kutatua migogoro kwa njia ya mazungumzo baina ya mwajiri na wafanyakazi.

“Matarajio yangu ni kuwa kila mjumbe katika kikao hiki atashiriki kikamilifu na kwa pamoja tutaibua hoja nzuri za kuwasilisha katika kikao cha Baraza Kuu la Mahakama ya Tanzania,” alisema Jaji Mfawidhi huyo.

Aidha, katika Baraza hilo wajumbe walipata fursa ya kufanya uchaguzi wa kuchagua Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe mmoja atakayewakilisha watumishi katika Baraza kuu la Wafanyakazi Taifa.

Uchaguzi huo ulisimamiwa na Ofisa Kazi- Mkoa wa Singida, Bw. Boniface Ntalula ambaye aliwaelewesha wajumbe wa kikao hicho kwamba, Mabaraza ya Wafanyakazi kazi yapo kisheria na yalianza tangu mwaka 1970 na yana umuhimu mkubwa ikiwemo kushauri juu ya masuala mbalimbali ya kiutumishi, kutatua migogoro kazini na pia kuimarisha mshikamano baina ya mwajiri na waajiriwa.

Wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, alitoa utaratibu wa uchaguzi na wajumbe wanaopaswa kupiga kura kwa mujibu wa Mkataba. Baada ya zoezi la kupiga kura kukamilika Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Amiri Bakari aliibuka kuwa Katibu mpya wa Baraza hilo, Bi. Anna Kisambale, Katibu Msaidizi na Bi. Dorisi Busanji alichaguliwa kuwa Mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Baraza Kuu la Wafanyakazi Taifa.

Aidha, taarifa ya utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2025/2026 ilisomwa na kuona utekelezwaji wa masuala mbalimbali hususan yanayolenga watumishi moja kwa moja, kuona mafanikio na changamoto na namna zilivyotatuliwa kwa mwaka wa fedha  ujao wa 2026/2027.

Akihitimisha kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi, Mwenyekiti wa Kikao, Mhe.  Mwenda aliwasisitiza watumishi kutekeleza wajibu wao na kufanya kazi kwa bidii na kutumia mafanikio yao katika kujenga hoja za kuboreshewa maslahi.

Vilevile aliwasisitiza viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Mkoa na wale wenyekiti wa Matawi ya TUGHE Mahakama kuendelea kuwasisitiza watumishi kujiunga na Chama hicho kwani ni muhimu na vipo kisheria.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama hiyo, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyesimama) akisalimia wajumbe waliohudhuria kikao hicho cha baraza (hawapo katika picha).  Kushoto ni Ofisa Kazi Mkoa wa Singida, Bw. Boniface Ntalula na  kulia ni Bw. Tamsoni Mshigati, Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Mkoa wa Singida.

Ofisa Kazi Mkoa wa Singida, Bw.Boniface Ntalula (aliyesimama) akjitambulisha na kufungua Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Singida waliohudhuria kikao hicho kilichofanyika tarehe 02 Mei, 2026 kwenye Ukumbi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

 Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akikata keki kuashiria kuzinduliwa kwa Baraza la Wafanyakazi Singida ikiwa ni Baraza la Kwanza tangu Mahakama hiyo ilipotangazwa rasmi kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

Jumanne, 5 Mei 2026

JAJI NONGWA AHITIMISHA MICHEZO NJOMBE KWA WANA MAHAKAMA SPORTS

·        Mahakama Sports yashinda Makombe manne Njombe mashindano ya michezo Mei Mosi

·       Asisitiza umuhimu wa Michezo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amewasisitiza Wanamichezo wa Mahakama Sports na Watumishi wengine Mahakama juu ya umuhimu wa Michezo na kusema kuwa ina faida nyingi ikiwemo kulinda afya ya mwili, pia ni ajira, vilevile huleta furaha pamoja na ushirikiano.

 

Mhe. Nongwa aliyasema hayo hivi karibuni alipohudhuria hafla ya usiku ya kuhitimisha michezo Mkoani Njombe iliyofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya ‘Agreement’ mkoani Njombe.

 

Katika hafla hiyo, alikuwepo pia Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Martine Mushi, Makamu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Maria Mayalla na Wanamichezo wa Mahakama Sports.

 

Naye, Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Donald Tende aliwasilisha taarifa aliyoisoma mbele ya Mhe. Nongwa pamoja na Wanamichezo ambapo alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwalinda na kuwajaalia afya njema na kuwakinga na maradhi na majeraha mbalimbali wakati wote wa mashindano.

 

“Pili, naushukuru Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kutupatia ruhusa na uwezeshaji wa rasilimali fedha wa kutuwezesha kushiriki kikamilifu katika mashindano ya Mei Mosi, 2026,” alisema Bw. Tende.

 

Vilevile, aliwashukuru Wachezaji wa Mahakama Sports walioshiriki mazoezi na mashindano kwa kujituma na kujitoa kwao katika kipindi chote kwa manufaa ya Timu ya Mahakama ya Tanzania.

 

Katibu huyo wa Mahakama Sports aliendelea kusema kuwa, “Wafanyakazi wanaoshiriki michezo ni kundi mojawapo la wafanyakazi wanaotegemewa na Taifa kiuchumi, kijamii na huduma mbalimbali kwa umma.” 

Bw. Tende aliongeza kuwa, Timu ya Michezo ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ilishiriki kikamilifu katika Mashindano ya Mei mosi yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe kuanzia tarehe 13 Aprili, 2026 hadi 01 Mei, 2026.

Alisema kuwa, Mashindano hayo yalifunguliwa rasmi tarehe 20 Aprili, 2022 na Mgeni Rasmi aliyekuwa Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo.

 Mashindano ya Mei Mosi yamelenga kusherehesha Sikukuu ya Wafanyakazi ili kuboresha mahusiano baina ya watumishi wa umma,  kutoka Wizara, Mashirika, Taasisi na Idara mbalimbali za Serikali, pamoja na jamii lengo likiwa ni kuboresha na kulinda afya za watumishi na kuimarisha nguvu kazi katika utumishi wa umma. 

Bw. Tende alibainisha kupitia taarifa yake kuwa katika michezo hiyo jumla ya Wizara, Idara, Taasisi za Umma, Mashirika ya Umma 61   walishiriki mashindano hayo ikiwemo Mahakama ya Tanzania.

Alieleza kuwa, Timu ya Mahakama ilijumuisha washiriki 84 na Timu ya ‘Mahakama Sports Club’ ilishiriki jumla ya michezo saba ambapo  iliweza kunyakua jumla ya Makombe manne ambayo ni Kamba mshindi wa tatu, Karata mshindi wa kwanza, Baiskeli mshindi wa pili na Mchezo wa Bao ni mshindi wa pili.

Wanamichezo wa Mahakama Sports ni watumishi kutoka katika Mahakama mbalimbali zilizopo nchini Tanzania ambapo wanamichezo hao wamejikita katika michezo  kama vile Mpira wa Miguu, Netiboli, Kamba Wanawake, Kamba Wanaume, Riadha, Kurusha Tufe, Drafti Karata, Baiskeli na Bao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wana Mahakama Sports. Wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, wa pili kushoto ni  Mwenyekiti wa Michezo Mahakama Sports, Mhe. Martine Mushi, wa kwanza kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Maria Mayalla na wa kwanza kushoto ni Katibu wa Michezo Mahakama Sports, Bw. Robert  Tende. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (aliyesimama) akizungumza na Wana Mahakama Sports kuhusu umuhimu wa michezo na kutoa hongera kwa wana michezo hao. Kushoto ni Mwenyekiti wa Michezo wa Mahakama Sports Mhe. Martine Mushi.

Katibu wa Mahakama Sports Club,  Bw. Robert  Tende akisoma taarifa ya michezo tangu walipoanza mpaka walipomaliza na mashindano ya michezo ya Mei Mosi, 2026.



Sehemu ya wageni waalikwa na wanamichezo waliohudhuria kwenye hafla hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

 

 

 

 

 

 

 


ENDELEZENI UZALENDO KATIKA UTENDAJI KAZI WENU; JAJI MSTAAFU, MHE. DKT. STEVEN BWANA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana ametoa rai kwa watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma kufanya kazi kwa uzalendo ili kujenga Mahakama yenye sifa njema katika Taifa lenye umoja na uzalendo wa kweli katika utumishi wa umma.

Akizungumza katika kikao kifupi na watumishi wa Mahakama hiyo jana tarehe 04 Mei, 2026 alipotembelea Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Bwana alisema, “Nimeambiwa mnafanya vizuri Kigoma, ni rai yangu kwenu kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, uzalendo wa kweli kwa Taifa na bila kuangalia utapata nini kesho, maana kazi zako zitakupa kukua, kuaminiwa na kutengeneza nafasi kubwa zaidi katika utumishi wenu.”

Jaji Mstaafu huyo amewaeleza watumishi hao kukumbuka kuwa shughuli zao za kila siku ndio msingi na kichocheo cha maendeleo ya Taifa na kusisitiza kuwa, “Wastaafu tulifanya sehemu yetu, ambapo teknolojia katika Mahakama kipindi hicho ilikuwa kidogo sana lakini tulifanya kwa uzalendo na kujituma na shughuli za kusikiliza mashauri na utawala zilifanyika vema.”

Aidha, Mhe. Dkt. Bwana alisema kuwa, ni mara yake ya kwanza kufika mkoani Kigoma, hivyo ni vema kuacha alama ya zawadi ya kitabu chake kiitwacho, ‘Maisha yangu, Utumishi wangu” chenye Tawasifu yake, ili kiwekwe kwenye Maktaba ya Mahakama hiyo hatimaye watumishi waweze kusoma maudhui ya kitabu hicho na kuongeza weledi wa kizalendo katika eneo la maisha ya utumishi wa umma.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile alipata wasaa wa kumzungumzia walau kwa kifupi Jaji Mstaafu, Mhe. Dkt. Steven Bwana kupitia kitabu chake kuwa ni moja ya Majaji wa Rufani ambaye alihudumu kwa weledi, kujituma kwa uzalendo mkubwa wakati wa kipindi chake, hivyo kufika kwake Kigoma ni jambo la muhimu na kuigwa na watumishi wa sasa hasa kwa umakini wake na utumishi uliotukuka katika kuwahudumia wananchi katika nafasi mbalimbali alizowahi kuaminiwa na Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, alitoa neno la shukrani kwa Jaji Mstaafu, Mhe. Dkt. Bwana aliyeambatana na Mkewe kutembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Aidha, Mhe. Mbelwa alimuomba Jaji huyo kupanda mti ili kuacha alama ya ujio wake wa kutembea kituo hicho, hata hivyo Jaji Mstaafu huyo aliridhia kupanda mti kama kumbukumbu ya ujio wake Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kulia) akimkabidhi Kitabu cha wasifu wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Karichuba Rwizile wakati Jaji Mstaafu huyo alipotembelea Mahakama Kuu Kigoma jana tarehe 04 Mei, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile akisoma Kitabu alichokabidhiwa na Jaji msatafu wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dr. Steven Bwana kwa ajili ya watumishi kusoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile (katikati) akimkaribisha Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kulia) alipowasili katika viunga vya Mahakama Kuu Kigoma jana tarehe 04 Mei, 2026. Aliyesimama kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Steven Bwana (hayupo katika picha), na mkewe kwa niaba ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana, na  Mkewe wakikata keki maalum ya upendo iliyoandaliwa kwa ajili yao walipotembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana akipanda mti katika eneo la mbele ya jengo la Mahakama Kuu Kigoma alipotembelea Mahakama hiyo jana tarehe 04 Mei, 2026.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na 
Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kushoto) na mkewe, Mama Steven Bwana.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)