Ijumaa, 26 Juni 2026

JAJI MTULYA AONGOZA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI YA JINAI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, ameongoza kikao cha usimamizi wa mwenendo wa mashauri ya jinai (Case Flow Management) kilichofanyika tarehe 25 Juni 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya kwa lengo la kujadili mwenendo wa mashauri ya jinai na hali ya upatikanaji wa haki jinai.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Judith Lyimo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, Mahakimu pamoja na wadau mbalimbali wa haki jinai.

Miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa ni mustakabali wa mashauri ya jinai ya mlundikano na yanayotarajiwa kuingia kwenye mstari wa mlundikano ifikapo Disemba, 2026, ambapo mikakati iliwekwa ili kuhakikisha kuwa mashauri hayo yanamalizika hadi ifikapo Novemba 2026.

Aidha, kikao hicho pia kilipitia kwa pamoja utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, ikiwemo uteketezaji wa vielelezo vya madawa ya kulevya ambao ulitekelezwa tangu mwezi Mei, 2026 ikiwa ni katika mikakati ya kupunguza mlundikano wa vielelezo mahakamani.

Vilevile, Mhe. Mtulya aliielekeza Ofisi ya Mwendesha Mashtaka (NPS) kupitia majalada ya mashauri 26 yanayotarajiwa kuwa ya mlundikano ifikapo mwezi Disemba, 2026 ili kuandaa vikao maalum vitakavyosaidia kuharakisha usikilizwaji wa mashauri hayo.

Naye, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer alisisitiza ushirikiano wa taasisi zote za haki jinai katika kutekeleza majukumu yao kwa wakati.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mahakama Kuu masjala ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo aliiomba taasisi ya Magereza kuwasaidia wafungwa kusajili mashauri yao kwa wakati.

Nao, Magereza walipendekeza wafungwa walio tayari kukiri makosa yao wasikilizwe mapema ili kurahisisha mwenendo wa mashauri, huku Mawakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Mwendesha Mashitaka (NPS) wakiahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa katika kikao hicho.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za wadau wa haki jinai Masjala Ndogo ya Mbeya za kuimarisha usimamizi wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema ipasavyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akizungumza katika kikao hicho, kulia ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer na kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo.

Sehemu ya washiriki wa kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo (wa pili kushoto), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Judith Lyimo (wa kwanza kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer (wa kwanza kulia) wakiwa wanaendesha kikao cha kusukuma mashauri ya jinai.

Sehemu ya washiriki wa kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani).

Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer akiwasilisha taarifa katika kikao hicho, kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya.


Mmoja wa washiriki wa kikao cha kusukuma mashauri ya jinai akichangia jambo katika kikao hicho.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


JAJI MKUU AMUAPISHA DKT. JINGU KUWA KATIBU WA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 26 Juni, 2026 amemuapisha Dkt. John Antony Jingu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. 

Dkt. Jingu anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Mtangulizi wake Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel. Hafla hiyo fupi ya Uapisho imefanyika kwenye ukumbi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa Kifungu cha 15 cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Sura ya 237, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ndiye Katibu wa Tume na Mtekelezaji wa Maamuzi ya Tume hiyo.

Tume ya Utumishi wa Mahakama ni Chombo kilichoundwa kusimamia utendaji kazi wa Mahakama ya Tanzania.

Mamlaka ya Tume ya Utumishi wa Mahakama kama Chombo cha kusimamia ajira na nidhamu za Watumishi wa Mahakama yanatokana na Ibara ya 113(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Kifungu cha 29(1) cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama. 

Matukio katika picha-Uapisho wa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Dkt. John Antony Jingu. 


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akimuapisha Dkt. John Antony Jingu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo tarehe 26 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Tume hiyo jijini Dodoma. Anayeshuhudia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. Gerson Mdemu.


Dkt. John Antony Jingu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania akila kiapo kuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo tarehe 26 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Tume hiyo. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (kulia) akisaini hati ya kiapo cha Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo tarehe 26 Juni, 2026. Anayeshuhudia ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju akisaini hati ya kiapo cha Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Dkt. John Antony Jingu aliyeapishwa leo tarehe 26 Juni, 2026.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (kushoto) akimpongeza Dkt. John Antony Jingu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye amemuapisha kuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo tarehe 26 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Tume hiyo. Anayeshuhudia ni Bi. Enziel Mtei, Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Ajira na Uteuzi).

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Dkt. John Antony Jingu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye amemuapisha leo tarehe 26 Juni, 2026 kuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (kushoto) ambaye ameapishwa kuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. Kulia ni Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama na aliyekuwa Katibu wa Tume hiyo, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (aliyeketi) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Makamishna pamoja na Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama waliohudhuria katika hafla ya Uapisho wa Katibu wa Tume hiyo, Dkt. John Antony Jingu (aliyesimama wa kwanza kushoto).

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (aliyeketi) akiwa katika picha ya pamoja na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Dkt. John Antony Jingu (wa pili kushoto), Manaibu Katibu wa Tume hiyo, Bi. Enziel Mtei (wa kwanza kushoto) na Bi. Alesia Mbuya (wa kwanza kulia), wa pili kulia ni Mtendaji Mkuu Mstaafu na aliyekuwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (aliyeketi) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti ya Tume ya Utumishi wa Mahakama. Aliyesimama katikati ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Dkt. John Antony Jingu.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju (aliyeketi) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. Aliyesimama katikati ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Dkt. John Antony Jingu.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)










 


JAJI MTULYA AKUTANA NA KUFANYA KIKAO NA MADALALI, WASAMBAZA NYARAKA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masijala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, jana tarehe 25 Juni, 2026 amefanya kikao na Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, kwa lengo la kukumbushana majukumu yao ya kila siku, kubaini changamoto zinazowakabili na kujadili mapendekezo ya namna ya kuboresha utendaji kazi ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wananchi kwa wakati mapema ipasavyo.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Mtulya aliwataka Madalali kuendelea kudumisha umoja, mshikamano na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yao huku wakizingatia kikamilifu taratibu, sheria na kanuni zinazoongoza kazi zao.

Mhe. Mtulya alisisitiza kuwa, utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia misingi ya taaluma na maadili utasaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za Mahakama.

Aidha, Mhe. Mtulya alieleza kwamba, ni muhimu kwa kila mdau kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa mipaka ya mamlaka aliyopewa, akibainisha kuwa Mawakili wanapaswa kuheshimu majukumu ya Madalali na kuepuka kuingilia utekelezaji wa kazi zinazowahusu Madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama ili kuimarisha uwajibikaji na ufanisi katika mfumo wa utoaji haki.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo aliwashauri Madalali kufanya vikao vya ndani kwa lengo la kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao na kuziwasilisha rasmi katika Ofisi ya Naibu Msajili ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati na kwa utaratibu unaostahili.

Nao, Madalali na Wasambaza nyaraka za Mahakama, walieleza kuwa moja ya changamoto kubwa wanazokutana nazo ni uelewa mdogo wa baadhi ya wananchi pamoja na viongozi wa Serikali za Mitaa kuhusu nafasi, umuhimu na majukumu ya Madalali wa Mahakama. walisema kuwa, hali hiyo wakati mwingine husababisha ugumu katika utekelezaji wa majukumu yao na kuchelewesha baadhi ya hatua za utekelezaji wa amri za Mahakama.

Akijibu hoja hiyo, Mhe. Mtulya alisisitiza umuhimu wa kuwashirikisha wadau mbalimbali katika vikao vijavyo, ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ili kusaidia kutoa elimu kwa viongozi wa Serikali za Mitaa, Halmashauri na Manispaa kuhusu nafasi na umuhimu wa Madalali katika kusaidia Mahakama kutekeleza majukumu yake ya utoaji haki kwa wananchi.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za Mahakama za kuendelea kuimarisha ushirikiano na wadau wake muhimu, kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya (kushoto) akiongoza kikao cha Madalali Mbeya, kulia ni Naibu Msajili Mahakama kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo.

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani)

Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani)

Mmoja wa Madalali wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mbeya akichangia jambo katika kikao hicho.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



WATUMISHI MBEYA WAWAAGA VIONGOZI WAO

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliandaa hafla maalumu ya kuwaaga viongozi wao waliowahi kufanya kazi nao kwa karibu, wakielezea shukrani zao kwa mchango mkubwa walioutoa katika kuimarisha utendaji kazi, ustawi wa watumishi na maendeleo ya Taasisi.

Hafla hiyo iliyofanyika katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya iliwakutanisha viongozi na watumishi mbalimbali katika mazingira yaliyojaa hisia za furaha na huzuni kwa wakati mmoja.

Aidha, furaha ilitokana na kuwatakia viongozi hao kila la heri na mafanikio katika majukumu yao mapya, huku huzuni ikitokana na kuondoka kwa viongozi ambao walijijengea heshima na upendo mkubwa miongoni mwa watumishi kutokana na uongozi wao wenye busara, ushirikiano na kujali maslahi ya watumishi.

Viongozi walioagwa ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Emily Temu, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo na Mtendaji wa Mahakama kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti, ambao kwa nyakati tofauti walipokea pongezi na maneno ya shukrani kutoka kwa watumishi waliopata fursa ya kufanya kazi chini ya uongozi wao.

Kwa upande wao, viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya pamoja na watumishi waliopata nafasi ya kuzungumza walieleza kuwa viongozi hao wameacha alama kubwa katika taasisi kutokana na uadilifu, uwajibikaji na moyo wa kujali watu waliouonesha katika kipindi chote cha utumishi wao.

Miongoni mwa shughuli zilizofanyika katika hafla hiyo ni utoaji wa maneno ya shukrani kwa waagwa, utoaji wa zawadi maalum kama ishara ya kuthamini mchango wao, kukata keki pamoja na kula chakula cha pamoja, matukio yaliyoongeza mshikamano na kuacha kumbukumbu ya pekee kwa washiriki wote.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa dua na salamu za heri, ambapo watumishi walisisitiza kuwa milango ya Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya itaendelea kuwa wazi kwa viongozi hao na kwamba mchango wao utaendelea kukumbukwa kwa muda mrefu kutokana na athari chanya waliyoiacha katika taasisi na kwa watumishi kwa ujumla.

Waagwa wakiwa kwenye picha ya Pamoja katika hafla hiyo kushoto ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu, (katikati) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti na kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo

Viongozi waagwa katika hafla hiyo wakikata keki kwa Pamoja ikiwa ni Ishara ya upendo na mshikamano

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo akitoa neno wakati wa hafla ya kuagwa.

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Said Kalunde (kushoto) akitoa nasaa kwa Viongozi Waagwa.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki kwenye hafla hiyo.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa wamebeba zawadi zilizoandaliwa kwa ajili ya Viongozi wanaoagwa (hawapo pichani).

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akizungumza katika hafla hiyo.

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Paul Dandi Ntumo akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akikabidhi Zawadi kwa Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo.

Viongozi wa Mahakama Kuu masjala Ndogo ya Mbeya kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Mussa Pomo, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Said Kalunde (wa pili kushoto), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya (wa pili kulia) na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Angaza Mwipopo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya akimlisha keki Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti.






 

Alhamisi, 25 Juni 2026

JAJI KIONGOZI AHITIMISHA ZIARA YA MAHAKAMA MKOANI RUVUMA

  • Ataka ufanisi katika kutekeleza majukumu ili kuongeza imani ya Wananchi kwa Mahakama
  • Ahimiza Watumishi kutambua maeneo Mahakama inayolalamikiwa na kuchukua hatua

Na FAUSTINE KAPAMA na Noel Daud-Mahakama, Songea

Ziara ya kimahakama ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, aliyokuwa anaifanya kukagua Mahakama na Magereza mkoani Ruvuma, imehitimishwa leo tarehe 25 Juni, 2026.

Mhe. Dkt. Siyani amehitimsha ziara hiyo kwa kukagua Gereza la Wafungwa na Mahabusu Tunduru na Mahakama ya Wilaya Tunduru na kisha kuongea na Watumishi wa Mahakama hiyo na baadaye Wawakilishi wa Watumishi wa Mahakama Masjala Ndogo Songea.

Katika kikao cha majumuisho, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Kuu Dodoma, Bw. Ginaweda Nashoni, waliwasilisha hoja mbalimbali zilizoibuliwa na Watumishi, Wafungwa na Mahabusu wakati wa ziara hiyo.

Miongoni mwa hoja hizo ni pamoja na maslahi ya Watumishi wa Mahakama katika Masjala Ndogo Songea, kwa Wafungwa na Mahabusu kucheleweshwa kupata nakala za hukumu na vitabu vya rufaa katika Mahakama ya Rufani na wito wa kuanza kusikiliza mashauri Mahakama Kuu.

Changamoto nyingine ni kwa Watuhumiwa kubaki kwenye Vituo vya Polisi kwa muda mrefu bila kufikishwa mahakamani. Viongozi hao wameeleza, kwa nyakati tofauti, namna hoja hizo zitakavyoshughulikiwa na nyingine tayari zimeshaanza kufanyiwa kazi na kutatuliwa.

Wakati wa kuhitimisha ziara hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, alimshukuru Jaji Kiongozi kwa kuamua kuja Songea kuwatembelea na kuonesha njia ya namna ya kuzungumza na Watumishi, Wafungwa na Mahabusu.

Ametumia fursa hiyo kuushukuru uongozi wa Mahakama kwa kuja Songea na kuahidi yote ambayo Jaji Kiongozi ameyatoa kama ushauri na maelekezo watayafanyia kazi na kufanya kila linalowezekana ili kuyatimiza na kujenga imani ya watu kwa Mahakama.

Akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tunduru, Mhe. Dkt. Siyani amewahimiza kufanya kazi kwa bidii na kuweka utaratibu wa kujipima, kwani kutokufanya hivyo kunaweza kusababisha watu kutokuwa na imani na Mahakama.

“Vinavyowaondolea watu imani siyo utovu wa maadili pekee, hata msipotimiza wajibu ipasavyo. Kama watu wanakuja mahakamani na mashauri yanachukua muda mrefu, wanaweza kukata tamaa na kuona hakuna sababu ya kwenda mahakamani,” Jaji Kiongozi amesema.

Amesisitiza kuwa kila Mtumishi wa Mahakama anapaswa kuaminiwa na umma na mtaji wa Mahakama kuendelea kuaminiwa ni imani ya umma, kwani watu wasipokuwa na imani na Mahakama, hakutakuwa na sababu ya uwepo wake.

“Kila Mtumishi anapaswa kujua kuwa namna anavyotenda au kutimiza wajibu wake kunachangia watu kuwa na imani na Mahakama. Watu wasipokuwa na imani na Mahakama, hawataitumia. Uhalali wetu wa kuwepo mahakamani ni kwa sababu watu wanatuamini kwamba tunaweza kufanya kazi ya kutoa haki,” amesema.

Aidha, Jaji Kiongozi amewasihi Mahakimu kutumia nafazi waliyonayo kujenga imani ya Wananchi katika nyanja zote, ikiwemo kutoa haki mapema ipasavyo.

Halikadhalika, Mhe. Dkt. Siyani amewataka Watumishi wote wa Mahakama ya Tanzania kutambua maeneo ambayo Mahakama inalalamikiwa, kuchukua hatua na kuzifanyia kazi changamoto zote kwa ufasaha.

Kabla ya kuzungumza na Watumishi hao, Jaji Kiongozi alipokea taarifa ya utendaji iliyowasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Shughuli Mwampashe.

Katika taarifa yake, Mhe. Mwampashe ameeleza kuwa kwa kipindi cha mwezi Januari hadi Juni, 19 2026, Mahakama ya Wilaya ya Tunduru na Mahakama zake za Mwanzo zimesajili na pia kuamua mashauri mbalimbali.

Amesema kuwa kwa upande wa Mahakama ya Wilaya, mashauri yaliyobaki Desemba 2025 yalikuwa 13, yaliyopokelewa January 2026 hadi Juni 19, 2026 yalikuwa 65 na yaliyoa, yaliyosikilizwa kwa kipindi hicho ni 59 na mashauri yaliyobaki ni 19.

Katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo, hapakuwemo na mashauri yaliyobaki mwaka 2025, mashauri yaliyosajiliwa kuanzia Januari hadi June 19, 2026 yalikuwa 378, yaliyosikilizwa ni 353 na yaliyobaki ni 25.

Aidha, ameleeza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha Januari hadi Juni 2026 kama kusimamia uharakishwaji na usikilizwaji wa mashauri kwa Mahakama wa Wilaya na Mwanzo, kufunga mashauri 44 ya mirathi na kupokea na kutuma barua na taarifa mbalimbali kwa njia ya Ofisi Mtandao (e-Office).

Ameeleza pia kuwa wanaendelea kusikiliza mashauri kwa njia ya Mtandao (Virtual Court), ikiunganisha Mikoa tofauti na kutoa elimu kwa Wadaawa kabla ya kuanza shughuli za Mahakama.

Katika ziara yake, Jaji Kiongozi aliambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu. Mahakama za Wilaya Songea, Nyasa, Mbinga na Namtumbo na Watumishi wengine wa Mahakama Songea.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tunduru (hawapo kwenye picha).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, akizungumza kwenye kikao cha majumuisho ya ziara ya Jaji Kiongozi Songea. Kushoto ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa. Picha chini akiongea kwenye kikao hicho.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Tunduru, Mhe. Shughuli Mwampashe akiwasilisha taarifa ya utendaji kwenye kikao hicho.

Sehemu ya Mahakimu Wafawidhi Mahakama za Wilaya wakiwa kwenye kikao hicho.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Tunduru (juu na chini) wakiwa kwenye kikao hicho cha majumuisho ya ziara ya Jaji Kiongozi.




Meza kuu inayoongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, ikiwa kwenye picha ya pamoja. Picha chini ni makundi mbalimbali baada ya kikao cha majumuisho ya ziara ya Jaji Kiongozi.






Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwasili kwenye Gereza la Mahabusu na Wafungwa Tunduru.

Picha na Magoiga Mtatiro-Mahakama, Songea.