· Alishukuru pia Bunge la Tanzania kwa
ushirikiano
· Ni wakati akifunga Mkutano Mkuu wa Baraza
la Wafanyakazi wa Mahakama
· Aipongeza Menejimenti ya Mahakama kwa
usimamizi na utekelezaji thabiti wa majukumu
· Awataka
watumishi wa Mahakama kuishi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana,
kusaidiana.......
Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Tanzania,
Mhe. George Masaju amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.
Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania
hususan katika kuuwezesha Mhimili huo kupata fedha za kutekeleza majukumu yake
ikiwa ni pamoja na miradi ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya
Dunia (WB).
Mhe. Masaju ambaye
pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania ameyasema
hayo leo tarehe 14 Mei, 2026 alipokuwa akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa
Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini
Dodoma.
“Ninamshukuru
Rais Samia, Mkuu wa Nchi hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano
anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania wanavyotafuta fedha hata za mikopo kuwezesha
sisi kutekeleza majukumu yetu ikiwa ni pamoja na miradi hii ya ujenzi ambayo
imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia,” amesema Jaji Mkuu.
Kadhalika, Mhe.
Masaju amesema, wakati Rais Samia aliposhiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama
cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) pamoja na hotuba ya Maadhimisho ya Siku
ya Sheria nchini ya mwaka huu, 2026 alielekeza kwamba wataendelea kuboresha bajeti
ya Mahakama na maslahi ya watumishi kwa kadri bajeti inavyoruhusu.
Sambamba na hilo,
Jaji Mkuu amelishukuru pia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa
Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu.
Mhe. Masaju amesema,
“Nalishukuru Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake,
Mhe. Mussa Azzan Zungu, muda mfupi uliopita wamepitisha bajeti yetu ya Mahakama
ya Tanzania, bajeti ilivyoenda kule haikuwa hivyo lakini kwa sababu ya Wabunge
kutambua umuhimu wa Mhimili huu wakaongeza hizo bilioni 26 kwa hiyo nawashukuru
sana Viongozi hayo wa Mihimili hiyo ya Serikali kwa ushirikiano wanaotoa kwa
Mahakama ya Tanzania.”
Katika
hatua nyingine, Jaji Mkuu amewapongeza washiriki wote wa Mkutano Mkuu wa Baraza
la Wafanyakazi wa Mahakama kwa ushiriki wao mzuri uliosheheni mijadala yenye
tija, uwazi wa hoja pamoja na mapendekezo na mikakati mbalimbali inayolenga
kuimarisha utendaji wa Mahakama ya Tanzania.
“Baraza
hili si tukio la kawaida pekee, bali ni sehemu muhimu ya kujitathmini kama Taasisi, kusikilizana kama familia ya Mahakama
na kupanga mustakabali wa utoaji haki hapa nchini kwa pamoja na kila mmoja wetu
hapa ana wajibu na anawajibika,” amesema Mhe. Masaju huku pia akiwashukuru watoa mada wote kwa mada zao zenye kujenga na kuelimisha kwa maslahi ya
watumishi wa Mahakama na Taifa kwa ujumla.
“Kama
nilivyowaeleza katika hotuba yangu ya ufunguzi wa baraza hili jana, hii ni mara
yangu ya kwanza kuongoza Baraza Kuu la Wafanyakazi na nililenga kujifunza zaidi
na hivyo, nilijikita zaidi katika kujifunza na hakika nimejifunza mambo mengi sana kutoka
kwenu wajumbe na pia kwa watoa mada wetu,” ameeleza Jaji Mkuu.
Aidha,
Mhe. Masaju ametoa pongezi za dhati kwa Menejimenti
ya Mahakama kwa maandalizi mazuri ya mkutano huo, usimamizi
mzuri wa shughuli wezeshi zinazowezesha Mahakama kutekeleza jukumu lake la
kikatiba la utoaji haki, kuendelea kusimamia
mageuzi mbalimbali ya kimfumo na kiutendaji.
“Vilevile, nawapongeza Menejimenti kwa kusimamia matumizi bora ya TEHAMA katika utoaji
haki, kuimarisha mazingira ya
kazi kwa watumishi wa Mahakama na kipekee
kabisa nipongeze mpango wa suala la ‘Supplementary’ Bima ya Afya kwa watumishi
wa Mahakama ambalo litaimarisha afya za watumishi na kuongeza ufanisi kazini,”
amesisitiza Jaji Mkuu.
Akizungumzia kuhusu bima hiyo, Mhe. Masaju amewaomba Watumishi wa
Mahakama kutumia bima hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa yaani kuimarisha afya za
Watumishi.
Vilevile, amewapongeza Viongozi
wote wa Mahakama katika ngazi mbalimbali kwa usimamizi wa mashauri, ufuatiliaji wa utendaji kazi, usimamizi wa maadili ya watumishi sambamba na kuendeleza nidhamu
na uwajibikaji.
“Mafanikio tunayoyaona leo ndani ya Mahakama yanatokana na mshikamano, uwajibikaji, uongozi wenye maono na
ushirikiano baina ya watumishi wote,”
amesema.
Mbali na Viongozi, Jaji Mkuu amewapongeza pia Watumishi wa Mahakama kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya kila siku hasa kwa kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri; kupunguza mlundikano wa mashauri, kuendelea kutekeleza majukumu
yao hata katika mazingira magumu.
“Aidha, niwaombe watumishi wote kuendelea kutafuta suluhisho la
changamoto mnazokabiliana nazo, na zile zilizoko nje ya uwezo wenu zileteni
kwetu Makao Makuu ili tuzitafutie ufumbuzi,” ameeleza Mhe. Masaju huku
akiwataka Viongozi wa Mahakama kutafuta suluhu ya changamoto na hoja mbalimbali
zilizowasilishwa na watumishi wakati wa Mkutano huo.
“Tumesikia vilio vya
wawakilishi wa watumishi hasa katika kada za chini kuwa ni maslahi duni na mazingira
magumu ya kazi, niendelee kuwasisitiza viongozi wote (Menejimenti na Viongozi wa Kanda)
kuendelea kuwa wabunifu ili kuboresha maslahi na mazingira ya watumishi wa Mahakama
ili kuimarisha ustawi
wao,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Hali kadhalika amewakumbusha watumishi wote wa Mahakama kuzingatia Maadili na Uwajibikaji katika kazi, kutunza siri za kazi, kuwa
waadilifu pamoja na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kushusha hadhi ya Mahakama.
Amewasisitiza
watumishi kuendelea kufanya Kazi kwa ushirikiano, mshikamano,
kuheshimiana, kusaidiana na kujenga utamaduni wa uwajibikaji.
Kwa upande mwingine, Jaji Mkuu amezungumzia kuhusu umuhimu wa Viongozi kusikiliza Watumishi
ambapo amesema, “moja ya
mafanikio makubwa ya mabaraza haya ni kuwapa watumishi nafasi ya kutoa maoni; kueleza changamoto; kupendekeza maboresho; hivyo, ni muhimu sana kuhakikisha kuwa hoja zote zilizowasilishwa hazibaki
kwenye makabrasha.”
Vilevile
amewataka wajumbe wa Baraza walioshiriki Mkutano huo kutoa Mrejesho kwa Watumishi kuhusu maazimio ya mkutano
huo; mikakati iliyokubaliwa pamoja na wajibu wa kila upande
katika utekelezaji wake.
Kuhusu, Bajeti na Mpango Mkakati
wa Mahakama, Mhe. Masaju amesema Taasisi yoyote yenye mafanikio
lazima iwe na mipango; vipaumbele na matumizi
yenye tija na kusisitiza kwa kusema
kuwa, “kwakuwa tayari tulishapanga bajeti ya Mahakama kwa mwaka
2026/2027, tuelekeze matumizi ya bajeti hiyo kulingana na mipango yetu, utekelezaji wake uzingatie kufikia
malengo na shabaha
ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Na
hapa niwakumbushe kuendelea
kuisoma Dira ya Taifa
ya Maendeleo 2050 ili kuifahamu misingi mikuu ya dira hiyo.”
Mkutano huo ulihitimishwa kwa maazimo yafuatayo; Fursa finyu za ufadhili wa masomo kwa watumishi; Mwajiri
aweke utaratibu
wa wazi katika utoaji wa fursa za mafunzo kwa udhamini wa Mahakama kwa watumishi wanaohitaji kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo vya
miundo mbalimbali ya kiutumishi.
Mahakama
kutoshiriki katika baadhi ya michezo kwenye mashindano mbalimbali; Mahakama iongeze idadi ya michezo itakayoshiriki katika mashindano
mbalimbali ya ndani pamoja na yale yanayoshirikisha Taasisi zingine.
Mafunzo
ya Matumizi ya Mifumo ya TEHAMA kutowafikia watumishi wa kada zote; Mafunzo ya matumizi
ya mifumo TEHAMA yatolewe kwa watumishi wote ili kuongeza ufanisi katika
utekelezaji wa majukumu yao.
Kutokubaliwa
kwa maombi ya uhamisho kwa baadhi ya watumishi ndani ya taasisi; Mwajiri aweke .utaratibu wa kuwahamisha watumishi ambao wamekaa kwa muda mrefu katika eneo moja la kazi na walio mbali na familia zao, ili kuimarisha ustawi wao wa kiutumishi na kifamilia.
Upandishwaji
vyeo kwa RMAs na MMOs
walioajiriwa kwa sifa ya darasa la saba na kidato cha nne waliokwama kupanda
cheo kwa kukosa sifa za kimuundo; Mwajiri awasilishe
maombi ya kibali maalumu cha kulegezewa masharti ya kimuundo kwa Katibu
Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili watumishi husika wafikiriwe kupandishwa vyeo kwa mserereko.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto), Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bw. Victor Kategere pamoja na wajumbe wengine wa Baraza la Wafanyakazi wakiwa katika siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.
Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza.
Makundi mbalimbali ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza hilo uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa PSSSF jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiongoza Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026. Kushoto ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando na kulia ni Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.
Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama aliyoitoa leo wakati wa kufunga kikao hicho kilichofanyika kwa siku mbili tarehe 13 na 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.