Ijumaa, 1 Mei 2026

MSIWE CHANZO CHA MAFARAKANO NA CHUKI KWA JAMII; JAJI SALMA MAGHIMBI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Msata

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amewataka watumishi wa Mahakama Mkoa wa Pwani kutokuwa chanzo cha mafarakano na chuki kwa jamii.

Mhe. Maghimbi ameyasema hayo jana tarehe 30 Aprili, 2026 alipokuwa akifungua jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata lililopo Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani.

Akizungumza wakati akitoa hotuba yake Jaji Maghimbi amesema jengo hilo ni nyumba ya haki na kuleta amani kwenye jamii hivyo watumishi wasiwe chanzo cha mafarakano na chuki kwenye jamii.

“Tumekabidhiwa kwa Mwenyezi Mungu sisi na jengo, hivyo; tujue anatuangalia na kutuonya tabia na matendo yetu mema na mabaya yatawekwa kwenye mizani, tutende yaliyo mema na yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu,” alisema Jaji Mfawidhi huyo.

Katika hotuba yake, Mhe. Maghimbi ameeleza kuwa, katika Wilaya ya Bagamoyo kuna Mahakama za Mwanzo saba ikiwemo Mahakama ya Mwanzo Msoga- Lugoba ambayo siku za hivi karibuni jengo lake lote liliungua kwa moto, hivyo upelelezi unaenddelea kubaini chanzo cha moto huo.

Kupitia ufunguzi wa jengo hilo pia, Mhe. Maghimbi amewaarifu na kuwatangazia wananchi wote  kuwa, huduma za Mahakama ya Wilaya Bagamoyo zilizokuwa zikisogezwa na kutolewa katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Lugoba/Msoga zitaanza kutolewa katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata.

Aidha, Mhe. Maghimbi amesema kujengwa kwa jengo hilo la Mahakama ya Mwanzo Msata siyo kwa bahati mbaya bali ni utekelezaji wa programu ya maboresho inayofanywa na Mahakama ya Tanzania kupitia Mpango Mkakati wake ulioanza awamu ya kwanza mwaka 2015 hadi 2016 na awamu ya pili 2020 hadi 2025.

“Mpango Mkakati huu wa Mahakama unaongozwa na nguzo tatu za Utawala bora, uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali, upatikanaji wa haki kwa wakati na uimarishaji wa imani ya wananchi kwa Mahakama pamoja na ushirikishwaji wa wadau katika shughuli za Mahakama,” ameeleza Jaji Maghimbi.

Mhe. Maghimbi amesema Mahakama hiyo itahudumia wananchi wa maeneo ya Kata za Mbwewe, Kibindu, Msata, Mandesa na Kimange. Kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2022 ujenzi huo umeboresha huduma za Mahakama kwa wakazi zaidi ya 92,890 wanaoishi katika Kata hizo tano.

Kadhalika amewakumbusha wananchi kuwa, haki ndio msingi wa ustawi wa Taifa kwa kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kuongeza kwamba, ili shughuli yoyote ya kiuchumi iweze kufanyika  kwa ufanisi, inahitaji mazingira ya amani, utulivu, utawala bora, utawala wa sheria na mfumo rafiki wa utatuzi wa migogoro inapotokea. Kwa mantiki hiyo haki huinua Taifa.

Amesema pia kujenga jengo kama hilo ni jambo adhimu, lakini pia kulitumia jengo hilo katika kutoa huduma bora na zinazomlenga mwananchi ni jambo lingine.

Ametumia fursa hiyo, kuwajulisha kuwa, maboresho ya huduma za Mahakama hayajalenga tu majengo bali pia yamelenga kubadili mitazamo ya watumishi wa Mahakama katika kutoa huduma za haki kwa mtazamo wa zamani wa Mahakama inayotisha na sasa kutoa huduma za kimahakama zinazomlenga Mwananchi.

Katika hotuba yake amesema programu ya maboresho ya Mahakama imeleta utamaduni mpya wa utoaji huduma wenye mitazamo ya utoaji haki kwa haraka, weledi, uwazi, ufanisi na unaomjali mwananchi (Citizen Centric Justice Delivery) ili mwananchi atumie muda wake mwingi kwenye uzalishaji wa mal ibadala ya kupoteza muda katika kutatua migogoro Mahakamani.

Amesema katika kuyafikia hayo watajipima kwenye Dira ya Mahaklama ya Tanzania isemayo “Utoaji Haki kwa Wote Mapema ipasavyo.’

Jaji Mfawidhi ametoa maelekezo muhimu kwa watumishi wa Mahakama kulilinda na kulitunza jengo hilo ili lidumu kwa muda mrefu na utunzaji huo uende sambamba na upandaji miti, jengo litumike katika kutoa huduma bora zinazoendana na utekelezaji wa maboresho yanayozingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo.

Ameongeza kuwa, Kituo hicho kinapaswa kuongezewa watumishi ili kiendane na kasi ya kuwahudumia wananchi pamoja na vitendea kazi vingine ikiwemo vifaa vya TEHAMA sambamba na kuimarisha weledi, uadilifu, uwazi, umoja na maelewano baina ya watumishi na wateja.

Kadhalika, Mhe. Maghimbi amewataka Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea kuhakikisha hawatakuwa kikwazo katika utoaji huduma za Mahakama hiyo kwa kuchelewesha haki bila sababu ya msingi ili kusaidia Mahakama kutoa huduma bora, kulinda na kutunza heshima na uhuru wa Mahakama.

Vilevile, Jaji Mfawidhi huyo ametoa rai kwa Viongozi wa Serikali  kusaidia kutoa huduma bora kwa kuweka mazingira wezeshi ua ulinzi na usalama katika jengo la Mahakama, kuisaidia Mahakama kupata maeneo mengine ya kujenga Mahakama mpya hususan katika Kata ambazo hazina Mahakama, kuwafikishia taarifa wananchi wa Kata zingine kuhusu kuanza kwa huduma za Mahakama ya Mwanzo Msata ili waitumie.

Kwa upande wa wananchi, Mhe. Maghimbi amewaomba kufikisha mahakamani migogoro yote inayohitaji kushughulikiwa  na Mahakama sambamba na kusaidia ulinzi wa jengo  hilo na mali za Mahakama ili zitumike kwa manufaa ya umma wa Watanzania.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo ametoa mwelekeo wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ya kuwa shughuli za utoaji haki za Kanda hiyo inasimamia Mikoa miwili ya Dar es salaam na Pwani na inasimamaia Mahakama za Hakimu Mkazi nne na Mahakama za Wilaya 12 na Mahakama za Mwanzo 54.

Pamoja na uzinduzi huo, mwezi uliopita Mhe. Maghimbi alizindua Mahakama mpya ya Wilaya ya Kigamboni inayoketi Somangila  iliyopo Mkoa wa Dar es Salaam, majengo mapya matatu ya Mahakama za Mwanzo ambazo ni Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Temeke inayoketi Mbagala, Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Mkuranga inayoketi Kimanzichana na Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Kibiti inayoketi Bungu. 

Amesema pia iko safari ya kufikisha huduma za Mahakama Mkoa wa Pwani na Mahakama za Mwanzo katika Kata za Talawanda, Pera, Vigwaza, Ubena Zomozi, Kimange, Mbwewe, Kibindu, Mandera, Mkange, Makurunge, Fukayosi, Mapinga, Yombo, Kiromo, Zinga, Nianjema, Kisutu, Lugoba na Magomeni. 

Naye Mhandisi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhandisi Francis Deogratius Upendo akitoa taarifa ya Mradi wa Mahakama ya Mwanzo Msata amesema, usanifu wa mradi wa Mahakama ya Mwanzo Msata umezingatia mazingira bora ya kufanyia kazi katika ofisi mbalimbali, urahisi wa kufikika na miundombinu wezeshi kwa makundi maalum.

Pia matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma na uendeshaji wa shughuli za Mahakama, ulinzi na usalama kwa watumiaji wa jengo pamoja na muonekano na taswira pekee ya Mahakama.

Akitoa salamu za Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya hiyo, Bi. Jesca  Samson amesema Mkuu huyo ametuma salamu za pongezi kwa Mhimili wa Mahakama kwa kuboresha maeneo ya kutolea haki wananchi wa Msata wamefurahi sana.

Baada ya ufunguzi wa Jengo la Mahakama hiyo, Jaji Mfawidhi Maghimbi pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Dar es Salaam, Mhe. Hamidu Mwanga, Mtendaji wa Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestor Mujunangoma, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bagamoyo, Mhe. Yasinta Kingwala walipata wasaa wa kupanda miti katika eneo la Mahakama hiyo.

  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam akihutubia watumishi wa Mahakama, Wadau kutoka Taasisi mbalimbali na wananchi walioshiriki katika sherehe za uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata-Bagamoyo iliyofanyika jana tarehe 30 Aprili, 2026.


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (katikati). wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Hamidu Mwanga, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mhakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Livin Lyakinana na wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Jesca  Samson.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Livin Lyakinana akitoa utambulisho wa wageni waliohudhuria Sherehe ya Ufunguzi wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Bagamoyo inayoketi Msata.


Mhandisi wa Majengo wa Mahakama Kuu, Bw. Francis Deogratius Upendo akitoa taarifa ya mradi huo wakati wa hafla ya uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata lililopo Wilaya ya Bagamoyo.

Kikundi cha Hamasa cha Watumishi wa Mahakama Pwani wakitumbuiza wakati wa sherehe hizo.

Kwaya ya Mahakama ya Tanzania (Ng’aring’ari Quir one) wakiimba katika sherehe za ufunguzi wa Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Bagamoyo inayoketi Msata.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi akikata utepe kuashiria ufunguzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata.


Jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata lililozinduliwa.


Meza kuu aktika picha ya pamoja na Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama Dar es Salaam na Pwani. Katikati ni 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Hamidu Mwanga, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mhakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Livin Lyakinana na wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Jesca  Samson.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



 

  

5345 wananchi waliohudhuria sherehe za ufunguzi wa jingo la Mahakama ya Mwanzo ya Wialaya ya Bagamoyo iliyoketi Msata.

 

 


 



Alhamisi, 30 Aprili 2026

MSAJILI MKUU ASISITIZA WATUMISHI KUILINDA HADHI YA MAHAKAMA

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, amewaasa Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Musoma kuilinda hadhi ya Mahakama kupitia utendaji wao wa kazi na hata katika maisha nje ya kazi.

Mhe. Nkya alitoa wito huo jana tarehe 29 Aprili, 2026 alipofanya kikao kazi na Watumishi hao pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma.

Awali akifungua kikao kazi hicho, Mhe Nkya alisema yuko Musoma kwa siku tatu kwa ajili ya ufuatiliaji na tathmini ya shughuli mbalimbali za kimahakama ambazo zimefanyika katika baadhi ya Mahakama za Masjala Ndogo Musoma.

Vilevile kupitia kikao hicho, Mhe. Nkya aliwasisitiza Watumishi kupenda kujisomea ili kujiongezea maarifa ya vitu tofauti vitakavyoboresha utendaji wao wa kazi, afya na maisha kwa ujumla.

Kupitia kikao kazi hicho, Watumishi mbalimbali walipata nafasi ya kuwasilisha hoja, changamoto na mapendekezo ya maboresho mbalimbali ili kuboresha mazingira ya kazi, maslahi na huduma kwa mteja.

Aidha, pamoja na ufuatiliaji na tathmini ya shughuli mbalimbali za kimahakama Mhe. Nkya alikabidhi vifaa vya kazi ambavyo ni kompyuta mpakato kwa Majaji wa Mahakama Kuu Musoma.

Katika ziara hiyo, Msajili Mkuu ametembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mahakama ya Wilaya Musoma, Mahakama ya Wilaya Butiama, Mahakama za Mwanzo Musoma Mjini, Mukendo na Kukirango na kote alikopita ameongea na Watumishi wa maeneo hayo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyesimama) akiwasalimia watumishi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakati wa kikao kazi hicho.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (aliyesimama) akimkaribisha Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Mkurugenzi wa Ufuatiliaji, Ukaguzi na Mrejesho wa Huduma za Mahakama, Mhe. Maira Kasonde (wa pili kushoto) akichangia jambo wakati wa kikao kazi na watumishi wa Mahakama Musoma.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakifuatilia kwa makini kikao kazi cha Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakimsikiliza kwa makini Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Marlin Komba (kushoto) akipokea kompyuta mpakato kutoka kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kulia) alipokuwa katika ziara ya Mahakama Musoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Geita.

 

 

 

 

 

 

Jumanne, 28 Aprili 2026

WAJUMBE BARAZA LA WAFANYAKAZI KIGOMA KUWAJIBIKA IPASAVYO

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kutumia kikao hicho kama jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji wa waatumishi katika masuala ya kiutumishi.

Mhe. Rwizile aliyasema hayo hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma wakati akiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Kigoma kilicholenga kujadili ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Jaji Rwizile alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha mahusiano kazini kwa kuzingatia mkataba mpya unaolenga kuboresha maslahi ya mwajiri na watumishi wake.

Jaji Mfawidhi huyo alieleza kuwa, “Baraza hili lipo kisheria na mkataba mpya umejikita katika kujenga Taasisi yetu kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho tunayoyahitaji katika usimamizi wa shughuli za usimamizi wa usikilizwaji mashauri katika Mahakama zetu.”

Hata hivyo, aliwajulisha wajumbe kuwa, kupitia kikao hicho kulikuwa na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza kwa mujibu wa mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi, hivyo aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita amba oni Mhe.  Victor Kagina, aliyekuwa Katibu na Bi. Naomi Chawe aliyekuwa Katibu Msaidizi wa Baraza hilo.

Zoezi la uchaguzi liliongozwa na Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi na shirikishi kwa wajumbe wote kwa  mujibu wa Mkataba.  

Baada ya zoezi la kupiga kura kukamilia, Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Julius Manyanya alichaguliwa kuwa Katibu mpya wa Baraza hilo na  Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Mburalina Maira aliteuliwa kuwa Katibu Msaidizi na Bi. Naomi Chawe alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE Baraza la Wafanyakazi Taifa.

Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa zenye tija zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa watumishi na ufanisi wa utendaji kazi.

Aidha, Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika mjadala, ilisisitizwa kuwa, watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo.

Wajumbe wa Baraza hilo wamesisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2025/2026, huku wakichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia mara tu changamoto zilizobainika ili kutatuliwa.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akitoa neno la ufunguzi wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kigoma kilichofanyika hivi karibuni.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala  Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) akimkabidhi Mkataba wa Baraza la Wafanyakazi Katibu wa Baraza mpya, Bw. Julius Manyanya mara baada ya kuibuka mshindi katika nafasi hiyo kwa kupata kura nyingi za kishindo kutoka kwa wajumbe.


Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kigoma wakifuatilia kwa makini mjadala ulikuwa ukiendelea wakati wa kikao cha Baraza hilo.


Ofisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Festo Sanga akiwasilisha taarifa ya utendaji wa shughuli za kimahakama kwa mwaka 2025/2026.

Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro akitoa ufafanuzi juu ya utaratibu wa uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi wa  Mahakama Kigoma.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

MASHAURI 48 YA MAHAKAMA YA RUFANI KUSIKILIZWA MASJALA NDOGO MBEYA

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Mashauri ya Rufaa 48 ya Ardhi, Kazi na Ndoa yanatarajiwa kumalizika katika kikao cha Uendeshaji wa Mashauri (session) katika Masjala Ndogo ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania mkoani Mbeya.

Kikao hicho kinachoendeshwa na Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, kikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye ambaye ameambatana na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Eliezer M. Feleshi na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Deo J. Nangela, wakisaidiwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Daudi P. Kinywafu pamoja na watumishi wengine wa Mahakama ya Rufani.

Akiongea katika kikao cha mapokezi, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Mkuye aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya unaongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim C. Tiganga kwa maandalizi na mapokezi mazuri. Alifafanua kuwa, ushirikiano kutoka kwa wadau na wahusika, utawezesha umalizaji wa mashauri hayo kama ilivyopangwa.

“Tunawashukuru sana kwa mapokezi na maandalizi mazuri ya kikao hiki kwa hakika tumefarijika sana na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu tunaamini kuwa mashauri haya yote tutayasikiliza bila kikwazo chochote,” alisema Mhe. Mkuye.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ameahidi kutoa ushirikiano kwa kipindi chote ambacho Waheshimiwa hao watakuwepo Masjala Ndogo ya Mbeya kuendesha usikilizaji wa mashauri hayo ya Mahakama ya Rufani.

Kikao cha usikilizaji wa Mashauri hayo kimeanza jana tarehe 27 Aprili, 2026 na kinatarajiwa kuhitimishwa tarehe 22 Mei, 2026.

Mwenyekiti wa jopo la Majaji ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye akisaini katika kitabu cha wageni mara tu baada ya kuwasili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakiwa pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya wakisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili Masjala Ndogo Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho kwa waheshimiwa Majaji hao mara baada ya kuwapokea.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Daudi kinywafu (wa pili kushoto kushoto), Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya Mhe. Aziza Temu (kulia), Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya Mhe. Judith lyimo (wa kwanza kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti wakishiriki mapokezi hayo.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.



WANACHAMA TMJA TAWI LA RUKWA WAFANYA KIKAO KAZI, MAFUNZO

Na. SHARIFU MOKIWA -Mahakama, Sumbawanga 

Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (Tanzania Magistrates and Judges Association (TMJA) Tawi la Rukwa walikutana hivi karibuni na kufanya kikao maalumu kilicholenga kuimalisha ushirikiano wa kitaaluma, kujadili maendeleo ya chama ili kujenga mshikamano miongoni mwa wanachama. Kikao hicho kilifanyika katika ufukwe wa Kasanga ziwa Tanganyika.

Akizungumza wakati wa kufungua kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda alisisitiza umuhimu wa umoja, ushirikiano na ushiriki wa wanachama katika kuimalisha utendaji wa Chama pamoja na utoaji wa haki kwa jamii.

Wakati wa kikao hicho Baraza Tendaji la TMJA Tawi la Rukwa lilipokea taarifa mbali mbali ikiwemo tarifa ya uimarishaji wa Tawi, taarifa ya mwakilishi wa TMJA pamoja na taarifa ya Mhazini wa Tawi ambapo wanachama walipata nafasi ya kujadili maendeleo yaliyofikiwa pamoja na changamoto zinazokikabili Chama.

Aidha, majadiliano mbali mbali yalifanyika na maazimio muhimu kutolewa kwa lengo la kuimalisha Tawi na kuboresha ushirikiano wa wanachama katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Wanachama pia walipata mafunzo maalum kuhusu program ya Mentorship yaliyotolewa na Mhe. Manyanda, mafunzo hayo yalilenga kuongeza uelewa wa kitaaluma, kurejesha utendaji wa kazi pamoja na kujenga mazingira bora ya ushauri na uongozi ndani ya Taasisi.

Vilevile, baada ya kikao na mafunzo wanachama waliendelea na shughuli za utalii katika eneo la Kasanga, hatua iliyosaidia kuongeza ukaribu kujenga mahusiano bora ya kikazi pamoja na kuweka kumbukumbu nzuri za pamoja.

Kikao hicho kilihudhuliwa na   na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo pamoja na Mahakimu wa ngazi mbali mbali.

Picha ya pamoja ya Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Rukwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda akifungua kikao cha TMJA Tawi la Rukwa.

Wanachama wa TMJA Tawi la Rukwa wakiwa kwenye kikao wakifatilia na kusikiliza kwa makini taarifa zilizokuwa zikiwasilishwa.

Mwakilishi wa TMJA Tawi la Rukwa Mhe. David Mbembela (aliyesimama) wa Baraza la TMJA Taifa akiwasilisha taarifa wakati wa kikao

Sehemu ya Wanachama wakiwa katika Fukwe za ziwa Tanganyika ikiwa ni sehemu ya Utalii.

Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Rukwa (kulia) akimpa mkono wa shukrani wakati wa kumuaga Mhe. Elisha Daudi Mwasomola (kushoto) ambaye amehamishiwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe.

Picha ya pamoja ya Wanachama wapya na waliohamia (TMJA) Tawi la Rukwa.                             


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Masjala ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi (kulia) wakikata keki iliyoandaliwa na Chama cha (TMJA )Tawi la Rukwa.

  





 

Jumatatu, 27 Aprili 2026

WATUMISHI MAHAKAMA KUU DODOMA WAPATIWA ELIMU KUHUSU AFYA YA AKILI

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma, hivi karibuni walipatiwa elimu muhimu kuhusu afya ya akili na ustawi wa maisha, iliyogusa moja kwa moja maisha yao ya kazini na nyumbani.

Elimu hiyo ilitolewa katika Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma na Jaji wa Mahakama Kuu kutoka Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale.

Mbali na majukumu yake ya kusikiliza mashauri mkoani Dodoma, Mhe. Ngunyale aliona vyema kutumia nafasi hiyo kuwajengea uelewa Watumishi hao kwenye eneo hilo.

Kabla ya kuanza zoezi hilo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, alimpongeza Jaji Ngunyale kwa moyo wa kujitoa na upendo wa dhati aliouonesha kwa Watumishi hao, akisisitiza kuwa afya ya akili ni msingi muhimu wa utendaji bora na maisha yenye mafanikio.

Kupitia elimu hiyo, Watumishi walipata fursa ya kujifunza kwa kina viashiria vya afya ya akili, mbinu za kukabiliana na changamoto za kisaikolojia pamoja na namna ya kujijenga kiakili na kitaaluma.

Si hivyo tu, mada ya uongozi bora (leading skills) iliyotolewa wakati wa zoezi hilo la utoaji elimu iliongeza chachu mpya kwa washiriki wengi, ikiwapa mwanga wa kuwa Viongozi bora katika nafasi zao na katika jamii.

Kilichovutia zaidi ni namna atumishi walivyoshiriki kwa hamasa kubwa, wakionesha wazi kufurahishwa na elimu hiyo ambayo waliieleza kuwa imewafungua macho na kuwapa mwelekeo mpya wa maisha.

Walimshukuru Jaji Ngunyale kwa kuwapatia maarifa yenye tija na yenye kugusa uhalisia wa maisha yao ya kila siku.

Zoezi hilo lilihudhuriwa na Watumishi mbalimbali ana kwa ana wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt Fatma Khalfan, pamoja na wengine waliounganishwa kwa njia ya mtandao kutoka wilayani, jambo lililoongeza ushirikishwaji na kuifanya elimu hiyo kuwafikia wengi zaidi kwa wakati mmoja.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo (aliyesimama) akimkaribisha Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale, aliyepo kulia kwake, ili kuwapa elimu Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma. Kushoto kwake ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Bw. Bedson Mariba.



Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma wakiskiliza kwa makini elimu ya Afya ya Akili kutoka kwa Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale (hayupo pichani).


 Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale akitoa somo kuhusu afya ya akili kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Simiyu.

 

 

Jumapili, 26 Aprili 2026

JAJI MKUU MASAJU AHUDHURIA IBADA YA SHUKRANI KUMBUKIZI YA KUZALIWA BI. LOYCE NYALALI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 26 Aprili, 2026 amehudhuria Ibada maalum ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.

Ibada hiyo maalum ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai imefanyika katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro Oysterbay jijini Dar es Salaam ikiongozwa na Paroko wa Kanisa hilo, Padri Bartholomew Mrosso na Padri mwenzake.

Katika mahubiri yake wakati wa ibada hiyo, Padri Mrosso ametoa rai kwa Waumini kumshukuru Mungu kwa uzima kwa kuwa uzima ni zawadi kubwa ambayo kwayo yatupasa kumshukuru Mungu. Amesisitiza kwa kusema, “tumshukuru Mungu kwa uzima kwanza halafu vingine ndio vifuate.”

Kadhalika Padri huyo, amewakumbusha Viongozi kusimamia haki, na kutenda mema kwa walio chini yao na wanaowaongoza.

“Katika Injili ya Jumapili ya leo ya Mchungaji Mwema msingi wake ni Uongozi, namna fulani ya Uongozi ambao Kristo anaudhihirisha kupitia matendo yake mema,” ameeleza.

Ameongeza kuwa, Kiongozi anapaswa kusimama kwa ajili ya wale anaowaongoza hivyo, Uongozi usichukuliwe kama ajira bali kujitoa na kuwajali watu waliopo chini.

Ibada hiyo imehudhuriwa pia na baadhi ya Viongozi wakiwemo Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba, Majaji Wastaafu wa Mahakama Rufani na Mahakama Kuu, Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakili Tom Nyanduga, Wenza wa Majaji Wakuu Wastaafu akiwemo Mama Marina Juma, Mama Sada Chande pamoja na ndugu, jamaa na marafiki na wageni wengine waalikwa.

Baada ya ibada hiyo, imefanyika sherehe maalum ya kumpongeza Bi. Loye Nyalali iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Kadinali Rugambwa uliopo pembeni ya Kanisa la Mt. Petro jijini Dar es Salaam.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kushoto mwenye tai nyekundu) akiwa katika misa ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, marehemu Francis Nyalali. Ibada hiyo imefanyika leo tarehe 26 Aprili, 2026 katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro jijini Dar es Salaam. Kulia kwa Jaji Mkuu ni Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba na aliyeketi mbele ni Mama Loyce Nyalali anayeadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimsalimia na kumpongeza Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.
 
Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiingia ndani ya Kanisa Katoliki la Mtakatifa Petro lililopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya ibada maalum ya kumshukuru Mungu kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiwa katika uso wa furaha ikiwa ni siku yake maalum ya kuadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Stephen Bwana (kushoto) pamoja na mwenza wake (katikati) na wengine wakiwa katika ibada ya shukrani maalum kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Paroko wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro, Padri Bartholomew Mrosso akiongoza ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Mama Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.


Picha mbalimbali za matukio ya Ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)