Alhamisi, 21 Mei 2026

MAHAKAMA YAOKOA ZAIDI YA BILIONI TATU

Na HABIBA MBARUKU na JAMES BUSANYA - Mahakama Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amesema kuwa Mahakama ya Tanzania, kwa kipindi cha mwaka Jnuari, 2021 hadi Aprili, 2026 imeokoa jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 3.6 wakati ikitekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, ishara ya kuwa imara katika matumizi na usimamizi wa fedha za Umma.

Prof. Ole Gabriel ameyasema hayo alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi ya Mahakama mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti iliyofanya ziara ya kikazi Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Jijini Dodoma tarehe 20 Mei, 2026 ili kupata uzoefu wa Mhimili wa Mahakama katika kusimamia miradi ya maendeleo kwa kutumia fedha za ndani na za Nje.

Akizungumza wakati wa wasilisho lake, Prof. Ole Gabriel ameeleza kuwa Mahakama ya Tanzania imefanikiwa kusimamia matumizi ya fedha kwa ufanisi, ambapo kwa kipindi kilichotajwa zaidi ya miradi ya ujenzi wenye thamani ya Tsh Biliopni 460 ilitekelezwa.

Aidha, Mtendaji Mkuu amefafanua kuwa katika hatua ya kwanza Mahakama ya Tanzania imefanikiwa kujenga majengo ya kwanza ya Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita katika Mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Mwanza pamoja na Arusha vilivyogharimu zaidi ya bilioni 51.

Katika hatua nyingine, Prof. Ole Gabriel ameeleza kuwa Mahakama imepiga hatua kubwa katika mapinduzi ya kidigitali ambayo yameokoa gharama na kupunguza matumizi ya fedha, huku maboresho katika majengo, hasa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki ambavyo vimeongeza urahisi wa upatikanaji wa huduma pamoja na taarifa. Akitolea mfano wa Kitumo Jumuishi ambapo Mahakama za ngazi zote zinapatikana katika jengo moja.

Mtendaji MKuu alibainisha kuwa hii inamfanya mwananchi kukata rufaa kwenye Mahakama ya ngazi ya juu ambayo ipo kwneye jengo hilohilo sekafu inayofuatia. Ifahamike kuwa kwenye Kitua Jumuishi, Mahakam ya mwanzo inakuwa sakafu ya chini, Mahakama ya Wilaya Sakafu ya kwanza, Mahakama ya Hakimu Mkazi Sakafu ya Pili, Mahakama Kuu sakafu ya Tatu.

Kadhalika, Prof. Ole Gabriel ameainisha miradi iliyokamilika ni Pamoja na vituo vingine Jumuish 9 na kwamba kwa kujumlisha na zile 6 za awali sasa kunakuwa na vituo jumuishi 15 Nchini kikiwepo cha Pemba, Zanzibar.

Sambamba na hilo, amesema kuwa Mahakama inazidi kusogeza huduma karibu na mwananchi kwa kuendelea kujenga miundombinu ya majengo katika maeneo mbalimbali nchini, na kwamba katika Wilaya 139 Nchini tayari kuna Mahakama za Wilaya katika Wilaya 137.

Prof. Ole Gabriel ameweka wazi kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kushirikiana na Mihimili mingine ya Serikali katika kutekeleza miradi mbalimbali, hususan TAMISEMI ili kutimiza azma ya kujenga Mahakama katika kila kata nchini ambapo kwa sasa Tanzania ina Kata 3,956.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Mashimba Ndaki (MB) ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa hatua kubwa iliyopiga katika maendeleo, hususan katika matumizi ya TEHAMA.

Mhe. Ndaki amesema, Mhimili wa Mahakama ni mfano wa kuigwa katika usimamizi za rasilimali za Umma na pia Matumizi ya TEHAMA kwa viwango vya kimataifa.

Aidha Mwenyekiti amesisitiza kuwa ni vyema Taasisi nyingine za Umma zifike Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania kujifunza jinsi ambavyo mifumo ya TEHAMA ya Mahakama inasomana vizuri ambapo hata yeye aliweza kuona hali ya jengo la Mahakam ya Mwanzo kwenye jimbo lake akiwa ndani ya chumba cha TEHEMA Jumuishi (Judiciary Situation Room).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akiwasilisha ripoti ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi ya Mahakama mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti iliyofanya ziara yake ya kikazi Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jana tarehe 20 Mei, 2026.


Sehemu ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakisikiliza wasilisho la Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel, katika ziara yao ya kikazi waliyoifanya jana tarehe 20 Mei, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.


Sehemu nyingine ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakisikiliza wasilisho la Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel, katika ziara yao ya kikazi waliyoifanya jana tarehe 20 Mei, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.


Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakifuatilia maelezo ya Chumba Maalumu cha Mifumo ya Utoaji Taariza za Mahakama (Judicial Situation Room).

Sehemu ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mashimba Ndaki (aliyeshika kisemeo, MB) katika Chumba Maalumu cha Mifumo ya Utoaji Taarifa za Mahakama (Judicial Situation Room).

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakati wanawasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jana tarehe 20 Mei, 2026 kwa ziara ya kikazi.



Picha ya pamoja baada ya ziara hiyo.








Jumatano, 20 Mei 2026

RAIS SAMIA ATEUA MAJAJI TISA WAPYA WA MAHAKAMA YA RUFANI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi wa Majaji tisa wa Mahakama Kuu kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, Bw. Bakari Machumu, leo tarehe 20 Mei, 2026, imesema kuwa wateule hao wataapishwa tarehe itakayotangazwa baadaye.

Walioteuliwa ni Majaji saba wa Mahakama Kuu ya Tanzania na wengine wawili kutoka Mahkama Kuu ya Zanzibar.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, walioteuliwa ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Yohane Bokobora Masara.

Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi na Jaji wa Mahkama Kuu ya Zanzibar, Mhe. Rabia Hussein Mohamed.

Wateule wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Dar es Salaam, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Dar es Salaam, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina.

Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Dodoma, Mhe. Iman, Daud Aboud, Jaji wa Mahkama Kuu ya Zanzibar, Mhe. Mzee Ibrahim Ibrahim na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo.


Mhe. Abdi Shaaban Kagomba.

Mhe. Yohane Bokobora Masara.

Mhe. Immaculata Kajetan Banzi.

Mhe. Rabia Hussein Mohamed.

Mhe. Cyprian Phocas Mkeha.

Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina.

Mhe. Iman, Daud Aboud.

Mhe. Mzee Ibrahim Ibrahim.


Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo.

 

WATUMISHI WA MAHAKAMA KUU NJOMBE WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO GEITA

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Griffin Mwakapeje, ameipongeza Mahakama Kuu Njombe kwa kufanya ziara ya mafunzo katika Mahakama ya Geita yenye lengo la kubadilishana uzoefu wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji wa haki kwa wananchi.

Mhe. Mwakapeje alitoa pongezi hizo juzi tarehe 18 Mei, 2026 katika Ukumbi wa Mafunzo wa Mahakama Kuu Geita wakati akiwakaribisha wajumbe kutoka Mahakama Kuu Njombe. Alisema kuwa Geita imeendelea kuwa mfano bora katika matumizi ya TEHAMA ndani ya Mhimili wa Mahakama.

“Mmefanya uamuzi sahihi sana kuichagua Mahakama Kuu Geita kama sehemu ya kujifunza matumizi ya TEHAMA, hivyo natarajia mafunzo haya yawe na mafanikio chanya katika kuongeza kasi ya utoaji haki kwa wakati,” alisema Jaji Mwakapeje.

Aidha, aliwashukuru Viongozi wa Mahakama Masjala Ndogo Njombe kwa kujipanga kujifunza kwa vitengo mbalimbali vya Mahakama ili kuongeza ufanisi wa kazi na kuondoa changamoto zinazoweza kujitokeza katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika ziara hiyo, mada mbalimbali ziliwasilishwa na menejimenti ya Mahakama Kuu Geita, zikieleza namna mifumo ya TEHAMA inavyotumika kurahisisha utoaji wa haki kwa wakati pamoja na kuongeza uwazi katika utendaji kazi wa Mahakama.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa usimamizi wa mashauri na namna Mahakama hiyo inavyoendesha shughuli zake bila matumizi ya karatasi.

Alieleza kuwa mfumo huo umeongeza ufanisi, uwazi na urahisi wa usimamizi wa shughuli za Mahakama, huku Viongozi wakipata uwezo wa kukagua mwenendo wa kazi kupitia mfumo huo bila kufika moja kwa moja katika maeneo husika.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, alifafanua jinsi Mahakama za Wilaya zinavyotumia mifumo ya kidijitali katika usimamizi wa mashauri na shughuli za kiutawala.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, alieleza namna Mahakama za Mwanzo zilivyoondokana na matumizi ya karatasi kupitia mfumo maalum uliobuniwa na unaotumika katika Mahakama zote za Mwanzo Masjala Ndogo Geita.

Mada nyingine iliwasilishwa na Winifrida Nghumbu, ambaye alieleza namna huduma ya KIOSK inavyowasaidia wananchi kupata taarifa za kesi, kusajili kesi na kufuatilia mwenendo wa mashauri yao kwa urahisi, hata kwa wale wasio na uelewa wa mifumo ya Mahakama.

Pia, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Geita, Happiness Mushi, alieleza namna utawala wa Mahakama hiyo ulivyoachana na matumizi ya karatasi kwa kutumia mifumo ya e-Office pamoja na mawasiliano ya barua pepe.

Akitoa neno la shukrani baada ya mawasilisho hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph Luambano, alisema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwao kutokana na mafunzo waliopata kuhusu matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki.

“Kufuatia ziara hii ya kubadilishana uzoefu, tumejifunza mambo mengi yenye kujenga na kutuonesha maeneo tunayopaswa kuboresha katika matumizi ya TEHAMA. Tunaahidi kuwa walimu kwa wengine na kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati kwa kuzingatia taratibu bila kumuathiri mtu yeyote,” alisema Mhe. Luambano.

Ziara hiyo iliongozwa na Mhe. Luambano, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Liad Chamshama, na watumishi wawakilishi kutoka kada mbalimbali za Mahakama ya Njombe.

Jaji wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje, akifungua mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akitoa ufafanuzi juu ya ushirikiano biana ya Viongozi na Watumishi unavyoleta mafanikio katika kuongeza ufanisi wa matimizi ya Tekinolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph Luambano, akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa Mahakama Geita.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, akielezea namna Mahakama za Wilaya zilivyoachana na matumizi ya karatasi katika uendeshaji wa kesi na shughuli za kiutawala.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, akilekeza jinsi Mahakama za Mwanzo zilivyoachana na matumizi ya karatasi.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Happines Mushi, akielezea namna utawala ulivyoachana na matumizi ya karatasi.

Ofisa Kumbukumbu, Bi. Winifrida Warsha, akiekelezea huduma ya KIOSK inavyowasaidia wananchi kusajili kesi na kuelewa mienendo ya kesi.

Picha ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na watumishi wa Mahakama Kuu Njombe katika jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Geita.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

Jumatatu, 18 Mei 2026

MAHAKIMU KIGAMBONI, WADAU WA HAKI JINAI WAPIGWA MSASA UANDAAJI WA HOJA ZA AWALI

  • Watumishi wasio Mahakimu nao wapatiwa elimu matumizi ya TEHAMA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo wilayani Kigamboni kwa kushirikiana na Wadau wa Haki Jinai, Mawakili wa Serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) wamepatiwa mafunzo ya namna bora ya uandaaji wa hoja za awali, kuzisoma, jinsi ya kuzirekodi, umuhimu na madhara ya kutoweka umuhimu wa hatua hiyo muhimu katika usikilizaji wa mashauri ya jinai.

Mafunzo hayo yalitolewa tarehe 15 Mei, 2026 na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa kwenye ukumbi wa Mahakama ya wazi ya Wilaya ya Kigamboni.

Wakati akifundisha, Mhe. Mbagwa aliwataka washiriki kueleza kwa namna wanavyojua maana na namna ya kuandaa na kushughulikia hoja za awali ambapo washiriki kila mmoja kwa uelewa wake alieleza.

Akitoa mafunzo hayo, Mhe. Mbagwa alianza kwa kueleza historia ya kuanzishwa kwa hatua hiyo ya hoja za awali katika mashauri ya jinai na kueleza lengo la kuanzishwa kwake ilikuwa ni kuharakisha usikilizwaji wa mashauri ya jinai kwa kuwa zile hoja zinazobishaniwa ndizo zinapaswa kuthibitishwa na upande wa mashtaka wakati wa uendeshwaji wa shauri.

Akifundisha kwa mfano, alisema iwapo mshtakiwa hakatai kuwa alikamatwa na kupelekwa Kituo cha Polisi upande wa mashtaka hawana sababu ya kumpeleka Mahakamani. Askari Mkamataji huthibitisha kuwa, mshtakiwa alikamatwa na katika hoja za awali mshtakiwa hakupinga kukamatwa kwake.

Mhe. Mbagwa aliwasisitiza Waendesha Mashtaka kuandika hoja muhimu zinazojenga msingi wa shauri na si kuandika mambo ambayo hata kama yakithibitika hayana uzito wowote katika shauri hivyo kuandaa hoja hizo kwa kuzingatia mambo muhimu katika shauri husika (essential facts).

Aidha, Jaji Mbagwa aliwasisistiza Washiriki wa mafunzo hayo kuzingatia hatua sita muhimu za kufuata wakati wa hatua hiyo muhimu ya kisheria kwa kuzingazita klifungu cha 198 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai. Hatua hizo ni kama Mwendesha Mashtaka kuzisoma hoja hizo, Mahakama kurekodi majibu ya Mshtakiwa, kuandaa muhtasari wa hoja zisizobishaniwa, Mshtakiwa kusomewa hoja zisizobishaniwa na mwisho Mwendesha Mashtaka, Mshtakiwa na Hakimu kuweka saini zao.

Akifungua mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib alimshukuru Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa kwa utayari wake na kukubali kujitoa na kufika Kigamboni kuwapatia mafunzo hayo.

Alimueleza pia, Mhe. Mbagwa kuwa, kuna mafunzo yanayohusiana na uandaaji na umuhimu wa hoja za awali kwa Mahakimu na Mawakili wa Serikali huku watumishi wengine wasiokuwa Mahakimu watapatiwa mafunzo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo yatatolewa na Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima.

Kadhalika, Mhe. Mwanakombo alimueleza Jaji Mbagwa kwamba, wameamua kuchagua mada hiyo, kwa kuwa Hoja za Awali ni hatua muhimu katika usikilizaji wa mashauri ya jinai. 

“Mhe. Jaji na washiriki wenzangu mtakubaliana na mimi kuwa ‘PH’ ni ‘road map’ ya shauri zima, maana hapa tunaona hoja zinazobishaniwa na zisizobishaniwa,” alisema Mfawidhi huyo wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni.

Aliongeza kuwa, mafunzo hayo yamekusudiwa kuwapa uelewa wa pamoja na mambo ya kuzingatia katika hatua hiyo muhimu.

Naye Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima aliwafundisha watumishi wasio Mahakimu namna bora ya kutumia mifumo mbalimbali ya ki-TEHAMA mahakamani ikiwemo matumizi ya Ofisi Mtandao (e-Office, Mfumo wa Kielektroniki wa Menejimenti ya Mashauri (e-CMS), (e-Filling) na mingine.

Kadhalika, Bw. Malima aliwasisistiza watumishi hao kuwapatia nakala za hukumu wateja ambao hawana uwakilishi mahakamani  na hawana akaunti za kuwezesha kupata nakala hizo.

Naye Mkuu wa Mashtaka wa Wilaya ya Kigamboni, Bi. Anita Sinare alimshukuru Mhe. Mbagwa kwa elimu aliyowapatia na kuahidi kuifikisha kwa Mawakili wenzao ambao hawakubahatika kuhudhuria mafunzo hayo.

Kwa upande wake, Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kigamboni, Bi. Bibiana Bundala alisema japo yeye sio Mwanasheria lakini mafunzo hayo yamempa uelewa mkubwa kuhusu nini kinapaswa kufanyika katika hatua hiyo muhimu na hivyo, itawezesha kuwabana watumishi walio chini yake na kusimamia ufanyikaji wa hatua hizo muhimu pale shauri linapofunguliwa Mahakamani.

Akitoa salamu za shukrani kwa Jaji Mbagwa baada ya mafunzo hayo, Mhe.  Christina Lugulu alisema kuwa, wamepata chakula cha akili na aliwashukuru wadau kwa kuhudhuria mafunzo hayo. 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa akifundisha Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwambo Kigamboni pamoja na washiriki wengine wa mafunzo (Wadau wa Haki Jinai) hayo kuhusu mada ya namna bora ya uandaaji wa hoja za awali. Mafunzo hayo yalitolewa tarehe 15 Mei, 2026.


Hakimu Mkazi  Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib (kushoto) akitoa neno la ufunguzi wa mafunzo. Aliyeketi katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa ambaye pia alikuwa Mwezeshaji wa mafunzo hayo na  kulia ni Bi. Pendo Kilusu, Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Kigamboni mara baada ya mafunzo yaliyofanyika katika Mahakama hiyo tarehe 15 Mei, 2026.


Jaji Awamu Mbagwa (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi  wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana  Rushwa  (TAKUKURU) na wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Wilaya ya Kigamboni. Wa pili kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigambo, Mhe. Mwanakombo Twalib.


Watumishi wasio Mahakimu wakiendelea na Mafunzo ya TEHAMA.

Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima akifundisha kuhusu Mafumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS).

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Awamu Mbagwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib (kushoto) na Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Bi. Upendo Kilusu (kulia).

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya mwanzo Kigamboni, Mhe. Christina Lugulu  akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mbagwa ambaye alikuwa Mwezeshaji wa Mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 

 

 

Alhamisi, 14 Mei 2026

JAJI MKUU GEORGE MASAJU AMSHUKURU RAIS SAMIA KUIWEZESHA MAHAKAMA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAKE IPASAVYO

·     Alishukuru pia Bunge la Tanzania kwa ushirikiano

·     Ni wakati akifunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama

·      Aipongeza Menejimenti ya Mahakama kwa usimamizi na utekelezaji thabiti wa majukumu

· Awataka watumishi wa Mahakama kuishi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana, kusaidiana.......

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania hususan katika kuuwezesha Mhimili huo kupata fedha za kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na miradi ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia (WB).

Mhe. Masaju ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania ameyasema hayo leo tarehe 14 Mei, 2026 alipokuwa akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

“Ninamshukuru Rais Samia, Mkuu wa Nchi hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania wanavyotafuta fedha hata za mikopo kuwezesha sisi kutekeleza majukumu yetu ikiwa ni pamoja na miradi hii ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia,” amesema Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema, wakati Rais Samia aliposhiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) pamoja na hotuba ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ya mwaka huu, 2026 alielekeza kwamba wataendelea kuboresha bajeti ya Mahakama na maslahi ya watumishi kwa kadri bajeti inavyoruhusu.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amelishukuru pia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Mhe. Masaju amesema, “Nalishukuru Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu, muda mfupi uliopita wamepitisha bajeti yetu ya Mahakama ya Tanzania, bajeti ilivyoenda kule haikuwa hivyo lakini kwa sababu ya Wabunge kutambua umuhimu wa Mhimili huu wakaongeza hizo bilioni 26 kwa hiyo nawashukuru sana Viongozi hayo wa Mihimili hiyo ya Serikali kwa ushirikiano wanaotoa kwa Mahakama ya Tanzania.”

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewapongeza washiriki wote wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama kwa ushiriki wao mzuri uliosheheni mijadala yenye tija, uwazi wa hoja pamoja na mapendekezo na mikakati mbalimbali inayolenga kuimarisha utendaji wa Mahakama ya Tanzania.

“Baraza hili si tukio la kawaida pekee, bali ni sehemu muhimu ya kujitathmini kama Taasisi, kusikilizana kama familia ya Mahakama na kupanga mustakabali wa utoaji haki hapa nchini kwa pamoja na kila mmoja wetu hapa ana wajibu na anawajibika,” amesema Mhe. Masaju huku pia akiwashukuru watoa mada wote kwa mada zao zenye kujenga na kuelimisha kwa maslahi ya watumishi wa Mahakama na Taifa kwa ujumla.

“Kama nilivyowaeleza katika hotuba yangu ya ufunguzi wa baraza hili jana, hii ni mara yangu ya kwanza kuongoza Baraza Kuu la Wafanyakazi na nililenga kujifunza zaidi na hivyo, nilijikita zaidi katika kujifunza na hakika nimejifunza mambo mengi sana kutoka kwenu wajumbe na pia kwa watoa mada wetu,” ameeleza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju ametoa pongezi za dhati kwa Menejimenti ya Mahakama kwa maandalizi mazuri ya mkutano huo, usimamizi mzuri wa shughuli wezeshi zinazowezesha Mahakama kutekeleza jukumu lake la kikatiba la utoaji haki, kuendelea kusimamia mageuzi mbalimbali ya kimfumo na kiutendaji.

“Vilevile, nawapongeza Menejimenti kwa kusimamia matumizi bora ya TEHAMA katika utoaji haki, kuimarisha mazingira ya kazi kwa watumishi wa Mahakama na kipekee kabisa nipongeze mpango wa suala la ‘Supplementary’ Bima ya Afya kwa watumishi wa Mahakama ambalo litaimarisha afya za watumishi na kuongeza ufanisi kazini,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumzia kuhusu bima hiyo, Mhe. Masaju amewaomba Watumishi wa Mahakama kutumia bima hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa yaani kuimarisha afya za Watumishi.

Vilevile, amewapongeza Viongozi wote wa Mahakama katika ngazi mbalimbali kwa usimamizi wa mashauri, ufuatiliaji wa utendaji kazi, usimamizi wa maadili ya watumishi sambamba na kuendeleza nidhamu na uwajibikaji.

“Mafanikio tunayoyaona leo ndani ya Mahakama yanatokana na mshikamano, uwajibikaji, uongozi wenye maono na ushirikiano baina ya watumishi wote,” amesema.

Mbali na Viongozi, Jaji Mkuu amewapongeza pia Watumishi wa Mahakama                        kwa              kazi                      kubwa wanayoendelea kuifanya kila siku hasa kwa kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri; kupunguza mlundikano wa mashauri, kuendelea kutekeleza majukumu yao hata katika mazingira magumu.

“Aidha, niwaombe watumishi wote kuendelea kutafuta suluhisho la changamoto mnazokabiliana nazo, na zile zilizoko nje ya uwezo wenu zileteni kwetu Makao Makuu ili tuzitafutie ufumbuzi,” ameeleza Mhe. Masaju huku akiwataka Viongozi wa Mahakama kutafuta suluhu ya changamoto na hoja mbalimbali zilizowasilishwa na watumishi wakati wa Mkutano huo.

“Tumesikia vilio vya wawakilishi wa watumishi hasa katika kada za chini kuwa ni maslahi duni na mazingira magumu ya kazi, niendelee kuwasisitiza viongozi wote (Menejimenti na Viongozi wa Kanda) kuendelea kuwa wabunifu ili kuboresha maslahi na mazingira ya watumishi wa Mahakama ili kuimarisha ustawi wao,” amesisitiza Jaji Mkuu.


Hali kadhalika amewakumbusha watumishi wote wa Mahakama kuzingatia Maadili na Uwajibikaji katika kazi, kutunza siri za kazi, kuwa waadilifu pamoja na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kushusha hadhi ya Mahakama.

Amewasisitiza watumishi kuendelea kufanya Kazi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana, kusaidiana na kujenga utamaduni wa uwajibikaji.

Kwa upande mwingine, Jaji Mkuu amezungumzia kuhusu umuhimu wa Viongozi kusikiliza Watumishi ambapo amesema, “moja       ya mafanikio makubwa        ya                        mabaraza     haya                    ni          kuwapa watumishi nafasi ya kutoa maoni; kueleza changamoto; kupendekeza maboresho; hivyo, ni muhimu sana kuhakikisha kuwa hoja zote zilizowasilishwa hazibaki kwenye makabrasha.”

Vilevile amewataka wajumbe wa Baraza walioshiriki Mkutano huo kutoa Mrejesho kwa Watumishi kuhusu maazimio ya mkutano huo; mikakati iliyokubaliwa pamoja na wajibu wa kila upande katika utekelezaji wake.


Kuhusu, Bajeti na Mpango Mkakati wa Mahakama, Mhe. Masaju amesema Taasisi yoyote yenye mafanikio lazima iwe na mipango; vipaumbele na matumizi yenye tija na kusisitiza kwa kusema kuwa, “kwakuwa tayari tulishapanga bajeti ya Mahakama kwa mwaka 2026/2027, tuelekeze matumizi ya bajeti hiyo kulingana na mipango yetu, utekelezaji wake uzingatie kufikia malengo na shabaha ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Na hapa niwakumbushe kuendelea kuisoma Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kuifahamu misingi mikuu ya dira hiyo.


Mkutano huo ulihitimishwa kwa maazimo yafuatayo; Fursa finyu za ufadhili wa masomo kwa watumishi; Mwajiri aweke utaratibu wa wazi katika utoaji wa fursa za mafunzo kwa udhamini wa Mahakama kwa watumishi wanaohitaji kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo vya miundo mbalimbali ya kiutumishi.


Mahakama kutoshiriki katika baadhi ya michezo kwenye mashindano mbalimbali; Mahakama iongeze idadi ya michezo itakayoshiriki katika mashindano mbalimbali ya ndani pamoja na yale yanayoshirikisha Taasisi zingine.


Mafunzo ya Matumizi ya Mifumo ya TEHAMA kutowafikia watumishi wa kada zote; Mafunzo ya matumizi ya mifumo TEHAMA yatolewe kwa watumishi wote ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.


Kutokubaliwa kwa maombi ya uhamisho kwa baadhi ya watumishi ndani ya taasisi; Mwajiri aweke .utaratibu wa kuwahamisha watumishi ambao wamekaa kwa muda mrefu katika eneo moja la kazi na walio mbali na familia zao, ili kuimarisha ustawi wao wa kiutumishi na kifamilia.


Upandishwaji vyeo kwa RMAs na MMOs walioajiriwa kwa sifa ya darasa la saba na kidato cha nne waliokwama kupanda cheo kwa kukosa sifa za kimuundo; Mwajiri awasilishe maombi ya kibali maalumu cha kulegezewa masharti ya kimuundo kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili watumishi husika wafikiriwe kupandishwa vyeo kwa mserereko.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto), Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bw. Victor Kategere pamoja na wajumbe wengine wa Baraza la Wafanyakazi wakiwa katika siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza.

Makundi mbalimbali ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza hilo uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa PSSSF jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiongoza Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026. Kushoto ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando na kulia ni Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.


Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama aliyoitoa leo wakati wa kufunga kikao hicho kilichofanyika kwa siku mbili tarehe 13 na 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.