Ijumaa, 31 Julai 2026

JAJI KIONGOZI AONGOZA WAOMBOLEZAJI IBADA YA MAZISHI YA KUMUAGA JAJI MSTAAFU SAMBO

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewaongoza mamia ya waombolezaji katika ibada ya kumuaga na kumsindikiza katika nyumba yake ya milele Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Marehemu Mhe. Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo aliyefariki Dunia mnamo 26 Julai, 2026 jijini Dar es Salaam.

Ibada hiyo ya kumuaga Marehemu Jaji Sambo ili kumpumzisha kwenye nyumba yake ya milele imefanyika leo tarehe 31 Julai, 2026 nyumbani kwa marehemu kitongoji cha Masebe wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya.

Akitoa salamu za pole kwa familia, ndugu, jamaa, majirani na marafiki Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa, maisha ya marehemu Jaji Sambo ni maisha ya mfano kwa aliowaacha kwani aliyaishi maisha yake kama sehemu ya maandalizi ya maisha ambayo sasa ameyaanza.

Jaji Kiongozi amesema kwa wale wanaomjua marehemu Jaji Sambo alikuwa mtu muadilifu mwenye hekima na imani ya Mwenyezi Mungu, na ndiyo maana Majaji na watu kutoka sehemu mbalimbali wakiwemo aliofanya nao kazi na alioshirikiana nao katika shughuli mbalimbali za kijamii wamesafiri kuja kumuaga na kumpumzisha katika nyumba yake ya milele, hali hiyo inaonesha jinsi gani aliweza kuishi na watu vizuri.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa, kwa upande wa Mahakama na tasnia ya Sheria kwa ujumla, Mhe. Sambo alichangia kwa kiasi kikubwa katika kutafsiri sheria kupitia maamuzi mbalimbali ambayo yataendelea kuwepo hata baada ya kuwa yeye amepumzika.

Aliongeza kuwa, maamuzi ambayo aliyatoa yameleta mchango ambao umewasaidia wengi kufahamu haki na namna ambavyo wanaweza kuziendea mahakamani. Mhe Sambo alikuwa na mchango mkubwa katika kuendeleza taaluma za wengine.

Mhe. Dkt.Siyani alirejea salamu za rambirambi kutoka kwa mmoja wa wahadhiri wa chuo kikuu cha Dar Es Salaam na kueleza namna ambavyo alimsaidia mhadhiri huyo kukamilisha tafiti yake. Jambo hilo linaonesha namna ambavyo alifundisha wengi na wengi wataendelea kumkumbuka.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amesema kwamba, pamoja na hadhi yake ya Ujaji, Mhe. Sambo aliendelea kushikilia imani yake kwa Mungu na kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii wakati wa utumishi wake na hata baada ya kustaafu utumishi alijishughulisha na kilimo na ufugaji akiwa Sumbawanga na hata mkoani Arusha.

“Madaraka tunayopewa ni makoti na majoho, Maisha yetu rasmi yapo katika Jamii inayotuzunguka hivyo hatupaswi kujitenga nayo,” alisema Jaji Kiongozi, akisisitiza juu ya mafunzo yapatikanayo katika maisha ya Marehemu Jaji Kakusulo Sambo.

“Nimepata funzo kupitia maisha ya Jaji Sambo hakuwabagua watu waliomzunguka, alikuwa anafikika na watu wote, alikwa tayari kupokea ushauri kutoka kwa mtu yoyote hata walioko chini yake na aliwaunganisha watu akiwa hai lakini leo pia katika kumuaga ametuunganisha pamoja watu wa imani tofauti,” amesisitiza Mhe. Dkt. Siyani.

Jaji Kiongozi alihitimisha kwa kusema kuwa, wanapata faraja wakiyakumbuka maneno ya Mungu yasemayo, “Heri wafu wafao katika Bwana maana watapata kupumzika la milele,”

Kwa upande wake, Mchungaji Michael Bureta aliyeongoza Misa takatifu ya Ibada ya maziko ya Marehemu Jaji Sambo alisema, “Ndugu yetu amelala katika kristo na ni njia mbayo kila mmoja wetu atapita. Tuiombee familia ili iangalie jambo hili katika imani na waendelee kumkumbuka kwa imani na sala wakati wote.”

Mchungaji Bureta aliongeza kuwa, Marehemu alikuwa na mchango mkubwa sana katika Kanisa alinunua vifaa mbalimbali vya Kanisa, kuwezesha safari za kikanisa ndani na nje ya nchi na alikuwa Mfadhili wa Kwaya ya Kanisa hadi kuteuliwa mnamo mwaka 2023 kuwa Mwenyekiti wa kwaya ya “Nuru Angaza” kanisani kwake alipokuwa mkoani Arusha.

Naye, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mashtaka Mkoa wa Mbeya alisema kuwa, msiba wa kuondokewa na Jaji Mstaafu, Marehemu Mhe. Sambo umeacha pengo kubwa kwa watu ambao mpaka sasa walikuwa wanategemea huduma kutoka kwake.

Marehemu Jaji Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo ameacha mjane mmoja, Watoto watano na Wajukuu 11 “BWANA ALITOA, BWANA AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE” AMEN.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiaga mwili wa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo mara baada ya Ibada Takatifu ya mazishi iliyofanyika nyumbani kwa marehemu kitongoji cha Masebe wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya, leo tarehe 31 Julai, 2026.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali akiaga mwili wa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati), akiwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali (wapili kushoto), na Majaji wengine wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa kwenye mazishi ya marehemu Jaji Sambo. Walioketi mbele (wa kwanza kushoto) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Iringa Mhe. Dustun Beda Ndunguru, Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo (wa pili kulia) na (wa kwanza kulia) ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Thadeo Marco Mwenempazi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akihutubia waombolezaji katika mazishi hayo.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Masjala Kuu Makao Makuu ya Mahakama Mhe. Chiganga Mashauri Tengwa akifanya utambulisho wa Viongozi walioshiriki katika mazishi hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Rungwe Mhe. Jackson Banobi akitoa salamu za rambirambi za Mahakama ya Wilaya Rungwe na kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya Rungwe.

Sehemu ya Viongozi wa Kamati ya ulinzi na usalama Wilaya ya Rungwe wakiwa katika mazishi hayo

Sehemu ya Watoto wa Marehemu wakiongozwa na Bw. Gwakisa Kakusulo Sambo (aliyeshika kipaza sauti) akisoma wasifu wa Marehemu Jaji Mstaafu Sambo.

Kwaya ya Angaza nuru ikitumbuiza katika mazishi hayo, kwaya ambayo Marehemu Jaji Sambo alikuwa Mwenyekiti wake.


Mwili wa Marehemu Jaji Mstaafu Sambo ukipumzishwa katika Nyumba yake ya milele.

Sehemu ya mamia ya waombolezaji katika mazishi hayo.


Sehemu ya mamia ya waombolezaji katika mazishi hayo

Sehemu ya mamia ya waombolezaji katika mazishi hayo.

Majaji wakiwa wamebeba Jeneza lenye mwili wa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo wakati wa shughuli ya mazishi.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali akisaini Kitabu cha waombolezaji nyumbani kwa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisaini Kitabu cha waombolezaji nyumbani kwa marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo 

Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania walioshiriki msiba huo wakiaga Mwili wa Marehemu Jaji Mstaafu Kakusulo Mwakipome Mbutolwe Sambo mara baada ya Ibada Takatifu ya mazishi iliyofanyika nyumbani kwa marehemu kitongoji cha Masebe wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


JAJI KAHYOZA ATETA NA MAWAKILI MASJALA NDOGO GEITA

Na. Dotto Nkaja, Mahakama - Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, Julai 28, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea mkoani Geita katika kikao kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mafunzo wa Mahakama Kuu Geita kwa lengo la kujengeana uwezo na kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa haki.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Kahyoza aliwashukuru mawakili kwa kuitikia wito na kueleza kuwa mkutano huo ulilenga kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na wadau wa sheria, kujadiliana masuala yanayohusu utoaji wa haki, kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya mifumo ya Mahakama pamoja na kufahamiana, kwa kuwa yeye ni mgeni katika Masjala Ndogo ya Geita.

Alisema uwepo wa wadau wengi wa sheria mkoani Geita ni fursa muhimu ya kuendeleza utoaji wa haki kwa ufanisi na kuongeza kuwa Mahakama ya Geita imeendelea kuwa mstari wa mbele katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha utoaji wa huduma za Mahakama.

Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA kusomana na kufanya kazi kwa pamoja ili kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa watumiaji. Aidha, aliwahimiza mawakili kuanza kutumia Kiapo cha Ushahidi (Witness Statement), hususan katika mashauri ya madai, akieleza kuwa utaratibu huo unasaidia kuharakisha usikilizaji na utoaji wa maamuzi ya mashauri.

Pia aliwataka mawakili kuendelea kutoa taarifa na mapendekezo wanapokutana na changamoto katika matumizi ya mifumo ya Mahakama ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake na kwa niaba ya mawakili, Wakili Marina Mashimba aliipongeza Mahakama ya Geita kwa maboresho ya mifumo ya kidijiti ambayo imepunguza gharama na muda wa uwasilishaji wa mashauri. Alipendekeza pia kuimarishwa kwa ushirikiano wa mifumo ya Mahakama na taasisi nyingine za utoaji wa haki, ikiwemo Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) pamoja na Mabaraza ya Ardhi.

Aidha, aliomba mafunzo ya mara kwa mara kwa mawakili ili kuwaongezea uwezo wa kitaaluma na kuwawezesha kupata alama za maendeleo endelevu ya taaluma kupitia chama chao cha kitaaluma.

Naye, Wakili George Alfred aliipongeza Mahakama kwa maboresho ya huduma, huku akiainisha baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika matumizi ya mfumo wa kielektroniki. Alieleza kuwa, baadhi ya kampuni hazionekani wakati wa usajili wa mashauri, baadhi ya vijiji havipo kwenye mfumo, na wakati mwingine mfumo humtambua wakili anayesajili shauri kama mlalamikaji badala ya mwakilishi wa mlalamikaji. Alisisitiza umuhimu wa kuwawezesha mawakili kutumia kikamilifu mifumo ya kielektroniki ili kupunguza matumizi ya karatasi na kuongeza ufanisi.

Akijibu hoja hizo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alisema changamoto zote zilizowasilishwa zimepokelewa na zitafanyiwa kazi. Alieleza kuwa, changamoto zinazohusu mashauri ya mirathi, nyaraka kutokuonekana kwenye mfumo pamoja na usajili wa kampuni zitawasilishwa kwa wajenzi wa mfumo ili zipatiwe ufumbuzi.

Akihitimisha kikao hicho, Mhe. Kahyoza aliwashukuru mawakili kwa ushiriki wao na maoni yao yaliyolenga kuboresha huduma za Mahakama. Aliwahimiza kuendelea kutoa taarifa kuhusu changamoto wanazokutana nazo, kuimarisha ushirikiano na Mahakama, pamoja na kutumia huduma za usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Aidha, aliwakumbusha mawakili umuhimu wa kufanya mazoezi na kushiriki michezo mbalimbali ili kuimarisha afya ya mwili na kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (katikati mbele) akiwakaribisha Mawakili wa Serikali na Mawakili wa Kujitegemea katika kikao kazi hicho cha kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji.

Wakili wa Serikali  Wakili Msomi George Alfred (aliyesimama) akichangia hoja.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna akijibu maswali na hoja mbalimbali zilizoibuliwa na Mawakili katika kikao kazi hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita Bi. Masalu Kisasila aliyesimama akitoa shukurani kwa ushirikiano mzuri katika uendeshaji wa shughuli za kiutawala baina ya Mawakili na Uongozi wa Mahakama. 

Wakili wa Serikali Bw. Robert Neophitus (aliyesimama) akitoa maoni juu ya Mfumo wa kielektroniki wa kusimamia Mashauri (e-CMS).

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

MAHAKAMA YA RUFANI KUENDESHA MASHAURI 38 YA RUFAA SUMBAWANGA

Na. SHARIFU MOKIWA-Mahakama, Sumbawanga

 Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania wamewasili mkoani Rukwa kwa ajili ya kusikiliza mashauri ya rufaa katika Kikao cha Mahakama ya Rufani kinachotarajiwa kufanyika katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga kuanzia tarehe 3 hadi 28 Agosti 2026.

Majaji hao wanaotarajiwa kuendesha vikao hivyo ni pamoja na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali, Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Lucia Gamuya Kairo na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Mustapha Ismail ambao wamewasili Sumbawanga kwa ajili ya kazi hiyo.

Majaji hao wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania walipokelewa mjini Sumbawanga na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga, Bw. Machumu Essaba pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Sumbawanga.

Kikao hicho kinatarajiwa kusikiliza jumla ya mashauri 38 ya jinai na madai, ambayo yanatoka katika maeneo mbalimbali ikiwemo Sumbawanga, Katavi, Mbeya, Mpanda na Songea, huku usikilizwaji wake ukifanyika katika Mahakama Kuu ya Masjala Ndogo ya Sumbawanga.

Akizungumzia kuhusu kikao hicho, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo alisema kuwa, matarajio ya Mahakama ni kuhakikisha mashauri yote yaliyopangwa yanasikilizwa na kumalizika ndani ya kipindi cha kikao hicho kama ilivyopangwa.

“Matarajio yetu ni mashauri yote yaliyopangwa kusikilizwa na kumalizika, kwa kuwa hatua hii itawawezesha wahusika kutambua hatima ya mashauri yao na pia kupunguza mashauri yanayosubiri kusikilizwa,” alisema Mhe. Mazengo.

Aidha, Mhe. Mazengo alisema kuwa, kufanyika kwa kikao hicho Sumbawanga ni sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania kuboresha huduma za kimahakama kwa kuwafikishia wananchi huduma hizo kwa urahisi zaidi, pamoja na kupunguza mzigo wa mashauri yanayosubiri kusikilizwa.

Mapokezi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiwasili Uwanja wa Ndege (wa kwanza kulia) ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali, (wa pili kulia) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda, (wa pili kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Mhe. Wanje Hamza (wa kwanza kulia) na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Lucia Kairo, (aliyevalia kitenge) walipopokelewa baada ya kuwasili mjini Sumbawanga.


Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Lucia Kairo (kushoto) akisalimiana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Sumbawanga Mhe. Lillian Ndelwa.

Viongiozi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Sumbawanga wakisalimiana na Jaji wa Mahakama ya Rufani mara walipowasili mjini Sumbawanga, (Kulia) ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali, akisalimiana na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Bw. Machumu Essaba, na (katikati) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda.



Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali, (kulia) akisalimiana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo.

 

Alhamisi, 30 Julai 2026

MWANASHERIA WA SERIKALI MFAWIDHI KIGOMA AJITAMBULISHA RASMI KWA JAJI MFAWIDHI, MHE. RWIZILE

  • Aahidi kudumisha ushirikiano na Mahakama mkoani humo

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni amefanya ziara ya heshima ya kumtembelea Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile lengo likiwa ni kujitambulisha rasmi na kuimarisha ushirikiano wa kikazi katika utoaji haki mkoani humo.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 29 Julai, 2026 katika Ofisi za Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma ambapo Mwanasheria huyo aliambatana na Wakili  wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma, Bw. George Kalenda pamoja na Mfawidhi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Magumbo.

Aidha, wakati wa mazungumzo ya Viongozi hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu upatikanaji haki, ikiwemo kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri na kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani.

Vilevile, walisisitiza juu ya umuhimu wa kuendelea kudumisha nidhamu, weledi na uwajibikaji katika mnyororo mzima wautoaji haki mapema ipasavyo.

Aidha, Mhe. Rwizile amewakaribisha Viongozi hao na kuwapongeza kwa hatua ya kufanya ziara hiyo ya kumtambulisha Mwanasheria Mkuu Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, huku akisisitiza kuwa na ushirikiano wa karibu baina ya Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) ni nguzo kuu katika kuhakikisha haki inatendeka mapema ipasavyo na kwa haki kwa kila mwananchi.

“Mahakama Kigoma itakupa ushirikiano ili utimize wajibu wako katika mnyororo wa haki, hivyo utakapobaini changamoto yoyote inayohitajika kutatuliwa na Mahakama basi usisite kuileta kwa ajili ya kutatuliwa kabla haijaathiri mnyororo wa kutoa haki mapema ipasavyo kwa kila mwananchi,” amesema,  Jaji Rwizile.

Kwa upande wake, Mwanasheria huyo Mfawidhi  wa Mkoa Kigoma, Bw. Said Seni amesema, anaishukuru mamlaka yake kumpangia kazi mkoani Kigoma, kwani amekutana na watu wema, wakarimu na wenye ari ya kufanya kazi kwa weledi na kujituma.

Amesema kuwa, anayo imani kwamba atapata ushirikiano wa kutosha katika kutimiza wajibu wake katika kipindi chote atakachokuwa katika ofisi hiyo Mkoani Kigoma.

Kadhalika, Mwanasheria huyo amemuahidi Jaji Mfawidhi kuwa, atafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na kuhakikisha amri za Mahakama zinatekelezwa kwa wakati na kwa mujibu wa sheria zilizopo.

Ameongeza kwamba, Ofisi hiyo ni mpya katika Mkoa wa Kigoma imeanzishwa kwa lengo la kuongeza nguvu ili kuisaidia Mahakama kutenda haki mapema ipasavyo, kupitia kutimiza wajibu wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama, Bw. Yusuph Kasuka. 

Ziara hiyo imelenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na ushirikiano baina ya Mhimili wa Mahakama na Taasisi za usimamizi wa sheria na uendeshaji wa mashtaka mkoani Kigoma, ili kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa ufanisi na mapema ipasavyo kwa maslahi ya wananchi kwa ujumla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (aliyeketi mbele) akifanya mazungumzo na Ujumbe wa Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma ulipomtembelea  ofisini kwake Mahakama Kuu Kigoma leo tarehe 30 Julai, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa neno kwa wageni wake katika maongezi yaliyofanyika katika ofisi yake iliyopo katika jengo la Mahakama Kuu Kigoma.

Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mfawidhi na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma kwa mapokezi mazuri.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa utambulisho wa Viongozi waliofika katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile leo tarehe 30 Julai, 2026.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi akifurahia jambo alipokuwa akizungumza na Viongozi na Wadau wa Haki Jinai waliofika ofisini kwake kumsabahi na wakimtambulisha Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni.


Wakili wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma,  Bw. George Kalenda akisikiliza kwa makini wakati Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile, alipokuwa akitoa neno wakati wa mazungumzo yao leo tarehe 30 Julai, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile  (wa tatu kulia) akiwa pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (wa tatu kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusuph Kasuka (wa kwanza kushoto), Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni, (wa wa pili kulia), Mfawidhi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Magumbo (wa kwanza kulia) na Wakili wa Serikali Mfawidhi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mkoa wa Kigoma, Bw. George Kalenda.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi (aliyeketi mbele) akitoa neno kwa Viongozi waliofika ofisini kwake kwa ajili ya utambulisho wa Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Kigoma, Bw. Said Seni.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

WANANCHI KATA YA LENGATEI WATOA KIWANJA CHA UJENZI WA MAHAKAMA

Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara

Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kupitia kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo Mhe. Dkt. Adam Mambi umekabidhiwa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo huku makabidhiano hayo yakifanywa na Viongozi pamoja na Wananchi wa Kata ya Lengatei iliyopo katika Tarafa ya Kijungu, wilayani Kiteto Mkoa wa Manyara.

Eneo hilo lilikabidhiwa rasmi na Viongozi na wananchi wa Kata hiyo, wakati wakimpokea Mhe. Dkt. Mambi alipofanya ziara ya ukaguzi wa shughuli za Mahakama katika eneo hilo mnamo tarehe 27 Julai, 2026.

Aidha, wananchi na viongozi hao wameonesha uhitaji wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo lao kwa kuwa, kwa sasa wanapata changamoto kusafiri kwenda mpaka Mahakama ya Mwanzo Kijungu kupata huduma za kimahakama ambapo kuna umbali wa Kilometa zaidi ya 12 kutoka kwenye Kata hiyo.

Akizungumza wakati wa mapokezi ya Kiwanja hicho, Mhe. Dkt. Mambi aliwashukuru viongozi pamoja na wananchi hao kwa kutoa kiwanja hicho kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo itakayo wasaidia wananchi kurahishisha kutoa huduma za kimahakama katika Kata hiyo na maeneo ya jirani.

“Tunawashukuru sana kwa kuwa mmeuona umuhimu wa Mhimili wa Mahakama katika dhima nzima ya utoaji wa haki mpaka mkaamua kutoa kiwanja hiki. Tunaahidi kushirikiana nanyi bega kwa bega mpaka tutakapokamilisha ujenzi wa Mahakama hii, naahidi ushirikiano kutoka kwa Mahakama ili shughuli hii ikamilike mapema,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Akizungumza wakati wa kukabidhi kiwanja hicho, Afisa Mtendaji wa Kata ya Lengatei Bw. Julius Kelato kwa niaba ya viongozi na wananchi wa kata hiyo, alishukuru uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kufika katika maeneo hayo na kuahidi kuanza mchakato wa ujenzi mara baada ya mchakato wa upatikanaji wa hati utakapokamilika.

“Tukishamaliza suala la upatikanaji wa hati ya kiwanja hiki, tumekusudia kuanza ujenzi wa Mahakama hii kwa kutumia nguvu za wananchi wetu kama ambavyo tumekuwa tukifanya kwa taasisi nyingine za Serikali,” alisema Bw. Kelato,

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mambi na timu yake ya ukaguzi walitembelea katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya, Mhe. Fakii Lulandala ambapo Mhe. Dkt. Mambi, alimuomba Mkuu wa Wilaya asaidie katika zoezi la upatikanaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa hati za umiliki wa viwanja hivyo ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima wakati wa matumizi yake.

Naye, Mhe. Lulandala aliahidi kufanya hayo. “Siku zote, tumekuwa tukishirikiana na Mahakama katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo na hususan katika kusaidia upatikanaji wa haki na amani katika maeneo yetu. Kwa sababu hizo ninakuahidi Mhe. Jaji kuwa, nitajitahidi kuwasaidia katika suala hili,” alisema Mhe. Lulandala.

Jaji Mfawidhi Mhe. Dkt. Mambi akiwa wilayani Kiteto alifanikiwa kukagua Mahakama ya Wilaya ya Kiteto, pamoja na Mahakama za Mwanzo Kibaya, Dosidosi na Kijungu. Kwa upande wa Wilaya ya Simanjiro, alikagua Mahakama ya Wilaya Simanjiro, Mahakama za Mwanzo Engasmet, Shambarai na Msitu wa Tembo.

Aidha, akiwa wilayani Simanjiro Mhe. Dkt. Mambi alipewa na kupokea ahadi kutoka kwa wananchi wa Kata ya Msitu wa Tembo kupitia viongozi wao walioahidi kuanza ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo lao kama walivyoahidi wananchi wa Kata ya Lengatei wilayani Kiteto. 

Viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa tano kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi na wananchi wa Kata ya Lengatei wilayani Kiteto walipotembelea kiwanja ambacho kimetolewa na wananchi wa Lengatei kwa Uongozi wa Mahakama, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo hilo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama) akiwa anazungumza na viongozi na wananchi wa Kata ya Lengatei alipowatembelea ofisini kwao wakati wa ziara ya Ukaguzi wa Mahakama wilayani Kiteto. Wengine ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe Charles Mnzava (kulia) na kushoto ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kiteto Mhe. Aron Losioki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (kulia) akizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mhe. Fakii Lulandala mara baada ya kumtembelea Mkuu huyo wa Wilaya katika Ofisi yake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Shambarai iliyopo Wilayani Simanjiro mara baada ya kufika Kituoni hapo kwa ajili ya Ukaguzi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Shambarai iliyopo Wilayani Simanjiro akisoma taarifa mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi na viongozi wengine waliofika kituoni hapo kwa ajili ya ukaguzi (hawapo pichani)

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Simanjiro, mbele ya Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro ambalo linaendelea kujengwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi, akisalimiana na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kiteto mara baada ya kuwasili kituoni hapo kwa ajili ya Ukaguzi wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyenyoosha mkono) akizungumza na sehemu ya viongozi na wananchi wa Kata ya Msitu wa Tembo, Wilayani Simanjiro mara baada ya kufika katika Mahakama ya Mwanzo Msitu wa Tembo kwa ajili ya Ukaguzi.

 (Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)