Jumanne, 1 Septemba 2026

JAJI MWENDA ANGOZA ZOEZI LA USAFI SINGIDA

Na EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda tarehe 29 Agosti, 2026 aliwaongoza watumishi katika zoezi la usafi ikiwa ni jitihada za kuhakikisha mazingira yanakuwa safi licha ya kuwa na watoa huduma ya usafi sambamba na kujenga utamaduni wa kutunza mazingira na kujenga mahusiano mazuri baina ya watumishi na kuimarisha umoja.

Akizungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu Singida aliwaeleza kuwa, zoezi hilo ni endelevu na litakuwa likifanyika kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi likihusisha hadi Mahakama za ngazi za chini.  

“Watumishi wenzangu kufanya usafi ni mojawapo ya mazoezi ya viungo lakini pia ni utaratibu mzuri kwani unaimarisha umoja na mshikamano mahala pa kazi na pia kila mmoja wetu atakuwa balozi katika masuala ya utunzwaji wa mazingira kama tulivyoona usafi sio jambo rahisi na zoezi litakuwa endelevu na litahusisha Mahakama ngazi za chini,” alisema Mhe. Mwenda.

Mahakama zilizofanya usafi kwa siku hiyo ni pamoja na Mahakama ya Wilaya Singida, Mahakama ya Wilaya Manyoni, Mahakama ya Mwanzo Itigi, Mahakama ya Mwanzo Mgandu, Mahakama ya Mwanzo Ikungi, Mahakama ya Mwanzo Ipembe na Mahakama ya Mwanzo Utemini.

Aidha, watumishi wamefurahishwa na zoezi hilo ambalo limeleta tija kwa kuonesha jukumu la usafi ni la wote hivyo, wameahidi kuwa mabalozi wazuri katika utunzaji wa Mazingira.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akiwaongoza Watumishi wa Mahakama hiyo kufanya usafi tarehe 29 Agosti, 2026.

  
   Watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Singida wakiwa katika usafi wa Pamoja uliofanyika katika jengo la Mahakama Kuu tarehe 29 Agosti,2026.


 Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Singida, Mhe. Fadhili Luvinga akifanya usafi.

Msaidizi wa Kumbukumbu  Mahakama ya Mwanzo Ikungi, 
Bi. Magreth Mtilimbania akiwa katika zoezi la usafi.

  Mhe. Aggrey Muhigi wa Mahakama ya Mwanzo Mgandu akifanya usafi.

  Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Manyoni kwa wakiendelea kufanya usafi kwa pamoja.


Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Itigi, Bi.Mwajuma Sudi akiwa katika zoezi la kufanya usafi.

  Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Utemini Singida wakiendelea na zoezi la kufanya usafi kwa pamoja.


  Watumishi wa Mahakama Kuu Singida wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuhitimisha zoezi la usafi. Aliyesimama mstari wa kwanza wa tatu kulia ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda, kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Singida, Mhe. Fadhili Luvinga, wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Singida, Bw. Filbert Matotay, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida, Mhe. Aloyce Masua na wa pili kushoto ni Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Mariam Hamisi.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


MWAKA MMOJA WA MAHAKAMA YA MWANZO TERRAT; WAJA NA MAFANIKIO KIUTENDAJI

  • Kiwango cha Uondoshaji mashauri chafurahisha

 Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Mahakama ya Mwanzo Terrat ni miongoni mwa Mahakama za Mwanzo mpya katika Wilaya ya Arusha na miongoni mwa mafanikio makubwa katika juhudi za kuboresha huduma za Mahakama ili kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi. 

Mahakama hii imekuwa chachu muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki kwa urahisi, ufanisi na mapema ipasavyo.

Mahakama ya Mwanzo Terrat ilianza rasmi kutoa huduma tarehe 20 Agosti, 2025, na sasa imetimiza mwaka mmoja tangu kuanza kwa safari yake ya kuhudumia wananchi.

Katika kipindi hicho, Mahakama imeendelea kutekeleza wajibu wake kwa uadilifu na weledi, huku ikiwa sehemu muhimu ya mageuzi na maboresho yanayoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza na Mwandishi wetu, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Mhe. Salma Mwamende amesema kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanza, Mahakama ya Mwanzo Terrat imepokea jumla ya mashauri 974. Kati ya mashauri hayo, mashauri 954 yamesikilizwa na kutolewa uamuzi, huku mashauri 20 yakiendelea.

“Kwa mwaka huu wa 2026, kwa kipindi cha Januari hadi Agosti, tumepokea jumla ya mashauri 604 na tayari tumemaliza mashauri 604 na mashauri 20 yanaendelea kusikilizwa, Mahakama yetu ina Mahakimu wawili lakini tunachapa kazi kuhakikisha tunaendana na wingi wa mashauri yanayokuja katika Mahakama yetu,” alisema Mhe. Mwamende.

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento alieleza kuwa, takwimu hizo za mashauri ya Mahakama ya Terrat zinaonesha kiwango cha juu cha ufanisi katika utoaji wa huduma za haki, ambapo Mahakama hiyo imeweza kumaliza zaidi ya asilimia 97.9 ya mashauri yote yaliyopokelewa, na kubakiza takribani asilimia 2.1 ya mashauri yanayoendelea.

“Mahakama hiyo imeweza kusikiliza na kumaliza mashauri ndani ya wastani wa wiki tatu, muda ambao ni mfupi ikilinganishwa na muda wa miezi mitatu unaotajwa katika miongozo kwa mashauri ya Mahakama za Mwanzo kwa shauri kusajiliwa hadi kuamuliwa. Mafanikio haya yanaonesha jitihada za Mahakama katika kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa wakati na wananchi wanapata haki kwa haraka,” alisema Mhe. Manento.

Takwimu hizo zinaonesha kuwa, katika mwaka wake wa kwanza, Mahakama ya Mwanzo Terrat yenye Mahakimu wawili tu, imeweza kutekeleza kwa ufanisi jukumu lake la msingi la kutoa haki kwa wananchi mapema ipasavyo, huku ikidhibiti mlundikano wa mashauri na kuhakikisha muda wa usikilizwaji wa mashauri unapungua.

Mwaka mmoja wa Terat ni zaidi ya kumbukumbu kwani umekuwa mwaka wa mafanikio, huduma na matumaini mapya hasa kwa wananchi wa Kata za Terrat, Muriet, Elerai na Sokoni 1.

Mafanikio hayo ni matokeo ya maono na juhudi za Uongozi wa Mahakama ya Tanzania wakishirikiana na wadau wake wote katika kuhakikisha kuwa huduma za haki zinasogezwa karibu na wananchi na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.


Jengo la Mahakama ya Mwanzo Terrat ambalo limetimiza mwaka mmoja tangu lianze kutumika kutoa huduma.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento alipotembelewa na Mwandishi wetu ofisini kwake tarehe 31 Agosti, 2026 kuzungumzia kuhusu Mahakama ya Mwanzo Terrat kutimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Mhe. Salma Mwamende alipotembelewa na Mwandishi wetu ofisini kwake tarehe 31 Agosti, 2026 kuzungumzia Mahakama hiyo kutimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama ya Mwanzo Terrat; Mhe. Salma Mwamende (kushoto) na Mohamed Nyenye (kulia).

Picha ya pamoja; Wa kwanza kushoto ni Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento katikati ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Salma Mwamende, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Terrat, Mohamed Nyenye, wa pili kushoto ni Kaimu Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Bw. Sunday Kilimba pamoja na Watumishi wengine wa Mahakama hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 



 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

                            

Jumatatu, 31 Agosti 2026

TEKELEZENI MAJUKUMU YENU IPASAVYO KWA KULINDA MASLAHI YA HAKI; JAJI MKUU

·       Jaji Mkuu Masaju awataka Naibu Wasajili hao kuwajibika ipasavyo kwa mujibu wa Katiba

·       Akemea vikali wanaoingilia Uhuru na Maamuzi ya Mahakama

·       Awaonya Maofisa Mahakama hao kutojihusisha na Uanaharakati

·       Awakumbusha kuzingatia Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050

·       Ahimiza ushirikiano na mahusiano mazuri kati ya Naibu Wasajili na Watendaji kwa utekelezaji fasaha wa majukumu

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Naibu Wasajili wa Mahakama nchini kuendelea kutekeleza majukumu yao ipasavyo huku wakilinda maslahi ya haki (Interest of Justice).

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 31 Agosti, 2026 alipokuwa akifungua Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Tuna wajibu wa kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa kulinda maslahi ya haki, kwa kutokufungwa kwa masharti ya kiufundi kupita kiasi hadi kukwamisha upatikanaji haki,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Wasajili wa Mahakama ndio 'injini' ya Mahakama. Hivyo, wana nafasi kubwa katika maendeleo ya Mhimili huo ambao mamlaka yake kwa mujibu wa Ibara ya 4 ni kutekeleza jukumu la utoaji haki.

“Kwa mujibu wa Ibara ya 107A(1), Mahakama ndio yenye kauli ya mwisho kwenye masuala ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano. Na ukiwa unaongozwa na kanuni kadhaa: mojawapo, kutenda haki kwa wote bila kujali hali ya mtu kiuchumi au kijamii, kutochelewesha haki bila kuwepo sababu ya msingi na kwamba itakuwa huru, italazimika tu kuzingatia sheria za nchi na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kama ambavyo Ibara ya 107A inavyoelekeza,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema, shughuli zote za umma huongozwa na kusimamiwa na sheria; hakuna shughuli yoyote ya umma ambayo haiongozwi na kusimamiwa na sheria. Na kwa sababu hiyo, Katiba inakuwa pia sheria, kwa mujibu wa ile Sheria ya Tafsiri za Sheria, sura ya kwanza ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Jaji Mkuu amewakumbusha Naibu Wasajili hao kuwa waadilifu ili wanapofanya maamuzi, watu waone kweli kwamba haki imetendeka. Amesisitiza, “Na katika hilo lazima tuwe waadilifu, tunapoacha kuwa waadilifu, tukiwa wazembe, tukiwa wavivu, uwezo wetu ukiwa mdogo, watu hawatatuheshimu.”

Vilevile, Mhe. Masaju amekemea vikali tabia ya baadhi ya watu kuingilia uhuru na maamuzi ya Mahakama huku akibainisha kuwa, Katiba imeiwekea ulinzi kwa Mahakama kupitia Ibara ya 30(2)(c) inayoelekeza kuhakikisha utekelezaji wa hukumu au amri ya Mahakama iliyotolewa katika shauri lolote la madai au la jinai.

Aidha, Ibara ya 30(2)(d) inatamka kulinda heshima, haki na uhuru wa watu wengine au faragha ya watu wanaohusika katika shauri lolote mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, au kulinda heshima na uhuru wa Mahakama.

“Ni lazima hukumu na amri za Mahakama zitekelezwe, ni Mahakama gani hiyo inaweza ikafanya maamuzi halafu yasitekelezwe, halafu ikabaki kuwa Mahakama?” amehoji Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Katiba hiyo pia inaelekeza kwamba lazima Mahakama iheshimike; uhuru wake, mamlaka, na hadhi yake lazima vilindwe na viheshimiwe. Kwa hiyo, lazima kulinda sifa na haki au uhuru wa watu wengine, au maisha binafsi ya watu wanaohusika katika mashauri mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, kutunza heshima, mamlaka, na uhuru wa Mahakama.

“Hivi karibuni tulivyotaka kusimamia suala hili kwenye Kanda zenu, tulikuwa na sababu za msingi. Hatutaruhusu watu kuidharau Mahakama au kuitisha hii Mahakama. Kwamba sasa nchi itatawaliwaje? Tunahitaji amani! Hivyo tunatakiwa kuwa makini kuliangalia suala hili, hatutaendekeza kitendo ambacho kitafanya Taifa hili liharibike, ni haki za binadamu gani ambazo haziwezi kujali hata hizo Taasisi za kikatiba zilizowekwa kwa ajili ya kutekeleza haki za binadamu?” ameeleza Mhe. Masaju.

Amewataka Naibu Wasajili hao kutotishwa kwa namna yoyote ile kwakuwa wamepewa madaraka hayo na Katiba hivyo wayatekeleze kwa ufanisi ipasavyo kama ilivyo kawaida ya viapo vyao.

Amerejea Ibara ya 30 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayosema:

"Haki na uhuru wa binadamu ambavyo misingi yake imeorodheshwa katika Katiba hii havitatumika na mtu mmoja kwa maana ambayo itasababisha kuingiliwa kati au kukatizwa kwa haki na uhuru wa watu wengine au masahi ya umma."

Kadhalika, amewakumbusha Naibu Wasajili hao kuwa sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050, kwa kuwa haki ina nafasi kubwa sana.

“Tuna jukumu kubwa sana Mahakama. Na Dira yenyewe inasema: "Taifa jumuishi lenye ustawi, haki na linalojitegemea." Kwa hiyo haki unaona imetajwa pale; ni muhimu, wanaohusika na kutenda haki kwa mujibu wa Ibara ya 4 ya Katiba ya Jamhuri ni kina nani? ni sisi Mahakama. Kwa hiyo, tunapojifunza nanyi mnaochukua nafasi za uongozi katika kipindi hiki, mjue kwamba tunao wajibu wa kutekeleza majukumu wetu lakini kwa kuzingatia yale matakwa ya Dira,” amesema Jaji Mkuu.

Ameongeza kwa kueleza kuwa, pamoja na mambo mengineyo, Dira hiyo inalenga kuwa na jamii yenye mshikamano na kutengamana, ambayo watu wake wanaishi kwa haki, amani, na kuheshimiana. Na msingi mkuu wa Dira hiyo ni utawala, amani, usalama, na utulivu. Ametaja maeneo matano ya kipaumbele ya Dira hiyo kuwa ni Utawala Bora na Haki, Serikali za Mitaa imara na zenye ufanisi.

Amesema kuwa, “Unapozungumzia masuala ya haki, unazungumza juu ya masuala ya sheria. Kwa hiyo, shughuli zote hata zinazoenda kutekelezwa chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2050 zinaongozwa na kusimamiwa na sheria. Na mimi na baadhi ya wasaidizi wangu tumesha 'map out' sheria zote zinazohusika katika utekelezaji wa Dira hii, kwa sababu Dira hii haikuacha kitu. Hapa tulipo, unaweza ukabainisha kwamba mbali na Katiba, swala kama hili, kwa mfano utawala bora, utatekelezwa kupitia sheria zipi. Kwa hiyo, hapo ndipo utakapona masuala ya haki. Na katika utekelezaji wa sheria hizi, kuna kuzivunja na kuzitekeleza.”

Mhe. Masaju ameeleza kwamba, muundo wa Dira hiyo umeweka mazingira ya kukuza uchumi na shughuli nyingine mbalimbali, ikiwemo za kibiashara, hivyo; hali hiyo inaweza kuja ongezeko la migogoro ikiwemo migogoro ya kibiashara, kiwekezaji na migogoro ya kijinai.

Kadhalika, Jaji Mkuu amewataka Maofisa Mahakama hao kuwajibika ipasavyo wanapotekeleza majukumu yao ambao amesema; “Sisi Mahakama tuna nafasi kubwa sana, tulipozungumza nanyi tarehe 17 Juni mwaka huu, tuliwaeleza wajibu wenu. Na mimi niwaombe Wasajili wote mlioko hapa, muendelee kuwajibika katika utekelezaji wa majukumu yenu, kuwajibika ipasavyo kama Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyoelekeza kwenye Ibara ya 25 ya Katiba hii. Ni suala la uwajibikaji, ni suala la kikatiba na wajibu wetu sisi wenyewe. Na ni vizuri mjifunze na kuielewa hii Dira. Tulitoa vitabu tukavisambaza kwenye kanda, lakini pia hii Dira inapatikana kwenye nakala laini (soft copies).”

Mhe. Masaju amerejea Ibara ya 146(2)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa moja ya majukumu ya Serikali za Mitaa ni kuhakikisha utekelezaji wa sheria na ulinzi wa wananchi kwenye maeneo hayo na ndio maana Mahakama inao mpango wa kujenga Mahakama za Mwanzo kila kata.

“Na tumeshawaomba mketi kwenye maeneo yenu, mhakikishe kwamba mnashirikiana na Serikali ngazi ile ya Mkoa na Wilaya kupata viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama hizi,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju ameongeza kuwa, katika kutekeleza hayo, wanatekeleza Katiba, hivyo, ushirikiano ambao umeendelea kuwa nao watendaji kwenye Kanda na Naibu Wasajili, waudumishe utasaidia kufanikisha jambo hilo.

Amewasisitiza Naibu Wasajili hao kuwajibika ipasavyo huku akirejea kipaumbele cha tatu cha Dira cha utumishi wa umma unaowajibika. Ambapo amewashauri kuendelea kuwajibika kwakuwa ni swala la kisheria na ni wajibu wao.

“Lakini kipaumbele cha nne ni amani, usalama, na utulivu. Ukiangalia yote haya, unaona ni kwa namna gani Mahakama ya Tanzania itaendelea kuwa na mchango muhimu katika kuhakikisha ustawi na maendeleo ya Taifa hili kiuchumi, kijamii, na kisiasa,” amesema Jaji Mkuu.

Aidha, ameeleza kuwa, ili Mahakama iweze kutekeleza jukumu hilo, lazima moja iwe na uwezo wa kulitekeleza. Kuna suala la miundombinu, kuna suala la rasilimaliwatu.

Akizungumzia suala la Utu, Jaji Mkuu Mkuu amewataka Naibu Wasajili hao kuweka mbele suala la utu huku akiwakumbusha kuwazingatia pia Watu wenye mahitaji maalum.

Kadhalika amewakumbusha Watumishi wote wa Mahakama kwa ujumla kuwa watu wenye uwezo wa kutekeleza wajibu kwa ufanisi ipasavyo (the capacity to deliver, competence), kuwa waadilifu (integrity), kuwa wabunifu; kuwa watu wa kujiongeza, na kujiongeza pia kumeelezwa katika Ibara ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 25 kwenye uwajibikaji pale.

“Tunapaswa kuwa ni watu ambao ni 'sensitive to justice', mnao wivu wa kuona kutenda haki na kuitenda haki ipasavyo. Na haki nimeshasema ni maamuzi yanayofanywa na Mahakama huru kwa kuzingatia Katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na kwenye viapo vyetu tunaapa kwamba tutatekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa ile sheria ya viapo, kwa kuzingatia Katiba, sheria, mila, na desturi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tukiwa huru, bila hofu, woga, upendeleo, wala chuki. Kitu hicho lazima tukisimamie na kukitekeleza ipasavyo, bila kufanya hivyo, tunakosa sifa hiyo ya kuwa watu wa kutoa haki,” amesisitiza.

Mafunzo hayo muhimu yenye kulenga kutoa mwongozo wa utendaji wa Naibu Wasajili hao yamefanyika kwa mara ya kwanza kwenye ukumbi mpya wa mikutano uliopo ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jambo ambalo limeonesha kufurahiwa na Viongozi pamoja na watumishi wengi walioshiriki katika ufunguzi wa Mafunzo hayo.

“Ninayo furaha kubwa kwa tukio hili muhimu. Na nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuliwezesha tukio hili. Lakini pia na kuiwezesha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuweza kutenda mambo haya makubwa. Na leo sisi, Mahakama ya Tanzania, tumekuwa na ukumbi huu muhimu sana. Mikutano yetu mingiambayo ilikuwa na sababu za msingitutakuwa tunaifanyia hapa. Ni ukumbi wa kisasa sana,” amesema Mhe. Masaju.

Aidha, Jaji Mkuu ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuwezesha kutimia kwa ndoto ya kuwa jengo kubwa na la kisasa, vilevile amewashukuru na kutambua kazi kubwa iliyofanywa na Majaji Wakuu Watangulizi wake kuanzia mwaka 1920 mpaka sasa.

“Viongozi waliotangulia wamefanya kazi kubwa. Sisi ambao tunapata fursa ya kutumika katika Mahakama ya Tanzania kipindi hiki, tunakaa kwenye jengo ambalo lilianza kujengwa na wenzetu wakati huo, na linaendelea kujengwa na kuimarika. Kwa hiyo, niwashukuru sana hawa viongozi wote, Maofisa wa Mahakama (Judicial Officers) na hao ambao sio 'Judicial Officers' waliokuwepo kuanzia mwaka 1920 mpaka sasa hivi. Na kwa sababu hiyo, nikupongeze Mtendaji Mkuu na watangulizi wako kwa kufikia hatua hii. Na nanyi Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki sana,” ameeleza Mhe. Masaju.

Matukio katika picha Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili (waliosimama). Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Faustine Kihwelo, wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Fatma Khalfan, wa kwanza kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu na wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na Viongozi na Watumishi wengine wa Mahakama wakisikiliza hotuba ya Mgeni Rasmi Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa ufunguzi Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.






 

MAFUNZO ELEKEZI NI MUHIMU KWA UENDESHAJI WA KAZI YA UTOAJI HAKI; JAJI KIHWELO

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Paul Faustine Kihwelo amesema Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wa Mahakama ni muhimu kwa mustakabali wa uendeshaji wa Mahakama na utoaji wa haki nchini.

Mhe. Dkt. Kihwelo ameeleza hayo leo tarehe 31 Agosti, 2026 wakati akitoa neno la utangulizi wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo hayo iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“"Mhe. Jaji Mkuu, kama nilivyosema awali, mafunzo haya yameandaliwa ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati. Na moja ya eneo muhimu sana ni kujengea uwezo watumishi wa Mahakama ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi. Na mafunzo elekezi haya yanakusudia kulifikia huko,” amesema Jaji Kihwelo.

Mkuu huyo cha Chuo cha IJA amesema kuwa, mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama na Sera ya Mafunzo ya Mahakama ya mwaka 2019, lakini pia ni sehemu ya Sera ya Mafunzo ya Taifa ambayo inataka Viongozi wote katika ngazi mbalimbali pamoja na watumishi waweze kupata mafunzo elekezi kabla ya kuanza kutumikia nyadhifa mpya.

Aidha, Mhe. Dkt. Kihwelo amemshukuru Jaji Mkuu, Mhe. Masaju kwa kukubali kuwa Mgeni Rasmi na kuona umuhimu wa kufanyika kwa mafunzo hayo na kuweza kuja kufungua mafunzo hayo yeye mwenyewe bila kutuma Mwakilishi. kutumikia nafasi hizo."

Kadhalika, Jaji Kihwelo amewapongeza Naibu Wasajili hao ambao wamepata nafasi hizo kwa imani ambayo Uongozi wa Mahakama umeonesha kwao. Hivyo, amewatakia kila la heri katika utumishi wao wakitumikia nafasi hiyo ya muhimu sana ambapo amesisitiza kuwa siku zote anaamini kuwa, injini ya Mahakama ni Wasajili pamoja na Watendaji.

Kuhusu ratiba ya mafunzo hayo kwa Naibu Wasajili, Mhe. Dkt. Kihwelo amesema kwamba, ratiba hiyo imeandaliwa kwa umakini sana. Lakini pia uteuzi au uchaguzi wa Wawezeshaji umefanyika kwa umakini ili kuhakikisha kwamba Wasajili hao watapitishwa kwa muda muda mdogo wa siku tano, lakini kile watakachokipata ni kikubwa.

“Wawezeshaji wengi ni wabobezi kama nilivyosema, walio wengi kwa kweli wamekuwa na uzoefu wa kufanya kazi katika maeneo yao. Kwa hiyo naamini waheshimiwa watapata fursa nzuri sana,” ameeleza Jaji Kihwelo.

Ameongeza kuwa, ratiba hiyo imejikita kwenye kutatua au kwenye maeneo ambayo ni changamoto za Mahakama kwa sasa na baadaye.

“Mara nyingi tukisema mafunzo lazima yajikite kwenye kuhakikisha tuna tunatibu changamoto zilizopo na changamoto za baadaye. Ndio maana kwa mara ya kwanza, kwa kweli, naona kuna mafunzo kabisa maalum kwa ajili ya Waendeshaji wa Masjala ya Mahakama ya Rufani katika Masjala ndogo za Mahakama ya Rufani katika ngazi tofauti,” amesema Jaji Kihwelo.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Kihwelo amewapongeza washiriki hao kushiriki mafunzo kwa mara ya kwanza katika ukumbi mpya wa Mahakama uliopo ndani ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na kuchukua fursa hiyo kumpongeza Jaji Mkuu na Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Paul Faustine Kihwelo  akitoa neno la utangulizi leo tarehe 31 Agosti, 2026 wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo hayo iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Naibu Wasajili wapya pamoja, Viongozi na Watumishi wengine wa Mahakama waliohudhuria Hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 31 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


 



WATUMISHI MBEYA WAZURU HIFADHI YA NGORONGORO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, wamefanya ziara ya kitalii katika Hifadhi ya Ngorongoro mkoani Arusha, ikiwa ni sehemu ya kuwapa fursa ya kupumzika, kujifunza, kutambua na kuthamini urithi wa asili na utamaduni wa Tanzania.

Ziara hiyo ya kitalii katika hifandhi ya Ngorongoro imeongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, akiwa Pamoja na viongozi wengine wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya.

Akiongoza ziara hiyo, Mhe. Mtulya amesisitiza umuhimu wa watumishi kupata fursa za kujifunza na kutembelea maeneo mbalimbali, akieleza kuwa shughuli hizo zina nafasi katika kujenga mahusiano mazuri, kuimarisha mshikamano na kuongeza ari ya watumishi katika kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Viongozi walioshiriki katika ziara ya kitalii ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya, Mahakimu wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba na watumishi wengine kutoka vituo mbalimbali vya Masjala Ndogo ya Mbeya.

Watumishi hao walipata fursa ya kutembelea na kujifunza kuhusu vivutio vya kiutalii vilivyopo katika eneo la Ngorongoro na kujionea wanyama na Ndege wa aina mbalimbali wanaopatikana katika hifandhi hiyo maarufu Duniani inayopatikana Tanzania.

Miongoni mwa maeneo yaliyotembelewa ni Bonde la Ngorongoro, eneo linalojulikana kwa utajiri wake wa wanyamapori na mandhari ya kipekee ya kijiolojia. Eneo la Ngorongoro pia ni miongoni mwa maeneo yenye hadhi ya urithi wa dunia kutokana na umuhimu wake wa asili, kiikolojia na kiutamaduni.

Watumishi hao pia walitembelea Ziwa Manyara pamoja na Makumbusho ya Ngorongoro–Lengai UNESCO Global Geopark, ambako walipata fursa ya kujifunza kuhusu historia, jiolojia, mazingira, utamaduni na namna ambavyo urithi wa asili unavyohifadhiwa na kutumika kwa ajili ya elimu na utalii.

Mbali na shughuli za utalii, ziara hiyo pia iliwawezesha watumishi hao kutembelea Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo Jumuishi cha utoaji haki Arusha, hatua iliyolenga kuwapa fursa ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mahusiano ya kikazi baina ya watumishi wa Mahakama kutoka Masjala hizo.

Ziara hiyo ya kiutalii imekuwa pia fursa ya kuwapa watumishi nafasi ya kujenga mshikamano, kuimarisha mahusiano baina yao na kupata muda wa kupumzika nje ya mazingira ya kawaida ya kazi, jambo linaloweza kuchangia kuongeza ari, morali na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Ziara hiyo imehitimisha kwa kuwa fursa muhimu kwa watumishi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya kujifunza zaidi kuhusu utajiri wa asili, historia, utamaduni na vivutio vya utalii vilivyopo nchini, huku wakijenga kumbukumbu na uzoefu ambao utachangia kuimarisha mshikamano na mahusiano yao ya kikazi.

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa mbele ya lango Kuu la kuingilia hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro.

Picha na matukio mbalimbali ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo y a Mbeya wakiwa katika ziara hiyo ya utalii katika hifadhi ya Ngorongoro.

Picha na matukio mbalimbali ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo y a Mbeya wakiwa katika ziara hiyo ya utalii katika hifadhi ya Ngorongoro.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa katika eneo la ziwa Manyara ambapo ilikuwa sehemu ya ziara hiyo ya kitalii.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa mbele ya Jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini Arusha.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati), Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (kulia) wakiwa mbele ya lango la kuingilia hifadhi ya ngorongoro walipotembelea katika hifadhi hiyo.

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya wakipewa maelekezo na historia ya Hifadhi ya Ngorongoro kutoka kwa Mwongoza watalii (wa kwanza kushoto)

Picha na matukio mbalimbali ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo y a Mbeya wakiwa katika ziara hiyo ya utalii katika hifadhi ya Ngorongoro.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

 

Jumamosi, 29 Agosti 2026

MTENDAJI MKUU AZUNGUMZA NA WATUMISHI WA MAHAKAMA ZA CHINI DAR ES SALAAM

Na WINFRED NZILANO-Mahakama Kisutu, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, tarehe 27 Agosti, 2026, alifanya kikaokatika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, kuzungumza na watumishi.

Watumishi hao walitoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Kinondoni, wawakilishi kutoka Mahakama za Wilaya Kivukoni, Temeke, Kigamboni, Ilala na Ubungo.

Hii ni mara yake ya kwanza tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kushika wadhifa huo. Dkt. Jingu aliambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Kikao hicho kililenga kufanya utambulisha kwa watumishi, kufahamu mwenendo wa utekelezaji wa majukumu na kusikiliza changamoto zinazowakabili katika mazingira yao ya kazi.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Jingu alitoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uteuzi wake. Alieleza ujio wake ni sehemu ya juhudi za uongozi wa Mahakama kuendelea kuwa karibu na watumishi na kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu changamoto wanazokutana nazo katika kutekeleza majukumu yao.

Katika kikao hicho, watumishi walipata fursa ya kuwasilisha changamoto, hoja na mapendekezo mbalimbali yanayohusu mazingira ya kazi na utekelezaji wa majukumu yao. Dkt. Jingu aliahidi kuzifanyia kazi kwa kuzingatia taratibu na mamlaka zilizopo.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu aliwasihi watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma katika kutekeleza majukumu yao. Alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora kwa wote wanaofika mahakamani ili kujenga taswira nzuri ya Mahakama kwa wananchi.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, alitoa shukrani kwa juhudi ambazo zimefanyika kuboresha masilahi ya watumishi na miondombinu ya Mahakama.

Kikao hicho kimeonesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuwa karibu na watumishi, kusikiliza changamoto zao na kuweka mazingira bora ya utendaji kazi.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, akizungumza na watumishi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam. Picha chini ni sehemu ya watumishi kutoka Mahakama za chini za Mkoa wa Dar es Salaam.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, akifanya utambulisho wa watumishi waliohudhulia katika kikao.

Mmoja ya watumishi akiwasilisha hoja wakati wa kikao hicho.

Picha ya pamoja na Watendaji na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni.

Picha ya pamoja na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo.

Picha ya pamoja na Maafisa utumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Mahakama ya Wilaya Kinondoni, Mahakama ya Wilaya Ilala, Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mahakama ya Wilaya Ubungo na Mahakama ya Wilaya Temeke.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma