Na
HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Jaji
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa, Haki
Jinai si mali ya Taasisi moja bali ni mfumo wenye Taasisi nyingi, wenye lengo
la kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo kwa usawa, uadilifu na kwa
kuzingatia Katiba na Sheria za nchi huku akieleza kuwa wadau wote wanapaswa
kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha haki haicheleweshwi bila sababu za
msingi.
Mhe.
Masaju ameyasema hayo wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki
Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki
Mahakamani leo tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
“Haki
jinai ni mfumo mmoja wenye taasisi nyingi lakini wenye lengo moja, yaani
kuhakikisha kuwa haki inapatikana mapema ipasavyo tunapaswa kuzungumza kuhusu
mfumo mzima kwa sababu udhaifu wa kiungo kimoja katika mnyororo wa haki jinai
unaweza kuchelewesha haki kwa mfumo mzima,” amesema Jaji Mkuu.
Mhe.
Masaju ametoa mfano wa Mtume Paulo anapozungumza kuhusu kanisa ambapo amesema,
“ni kama mwili wa binadamu, kama ambavyo kuna mikono, macho, miguu, lakini hivyo
vyote ndiyo vinakamilisha mwili. Yaani macho hayawezi kujifanya yenyewe ni bora
kuliko mguu na vile viungo vilivyoonekana kama ni dhaifu, hivyo Mungu
alivifanya kuwa vya maana zaidi lakini ukweli hapa wote hakuna kiungo dhaifu,
hizi Taasisi zote ni muhimu.”
Ameongeza
kuwa, jukumu la kwanza la sheria duniani kote ni kusimamia utawala wa sheria,
amani na usalama katika jamii na jukumu la pili ni kukusanya kodi kwa ajili ya
maendeleo mbalimbali na kuongeza kuwa hata Mwenyezi Mungu huko mbinguni aliweka
sheria, na aliyekwenda kinyume na sheria aliwajibika kama ambavyo Lucifer alivyowajibika.
“Kwa
hiyo, mkishakuwa zaidi ya mtu mmoja tu lazima mjiwekee sheria namna ya kufanya
mambo yenu na kwetu Tanzania utawala wa sheria unapatikana katika Ibara ya 26
ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mfumo wowote lazima uwe unaongozwa
na utawala wa sheria, hata Mwenyezi Mungu kule mbinguni aliweka sheria, na
bwana mkubwa yule akiitwa Lucifer alipoasi akawajibika” amesema Mhe. Masaju.
Katika
hatua nyingine Jaji Mkuu amefafanua kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050
inasisitiza juu ya amani, usalama na utulivu, ulinzi wa haki, uhuru wa msingi,
uimara wa Taasisi na utawala wa sheria ambao ni kipengele muhimu cha utawala
bora kinachosaidia kujenga jamii yenye usawa, uwajibikaji, haki na kuaminiana.
Aidha,
ameeleza kuwa, mashauri ya jinai hayaanzii mahakamani wala polisi pekee kwa
kuwa vyombo hivyo vyote haviwi sehemu na wakati ambapo matukio hayo ya kihalifu
yanatokea hivyo, wadau wote wanapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja kama
ambavyo viungo katika mwili vinavyofanya kazi kwa pamoja na kutegemeana.
“Kesi
ya jinai inaanza kwenye jamii huko tukio linapotokea, inaenda kwenye vyombo vya
uchunguzi iwe ni Polisi, ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, ni
Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, inaenda Ofisi ya Taifa ya
Mashtaka, hatimaye kama kuna ushahidi inaenda mahakamani, na waliohusika
kumkamata mshukiwa wanakuja kutoa ushahidi mahakamani kama amepatikana na hatia
anarudi gerezani kwa ajili ya reform, utaona kwamba huu mnyororo ni
mpana ni mnyororo mrefu lakini mnyororo imara, ” ameeleza Mhe. Masaju.
Katika
hatua nyingine, amesema kuwa, ni vema kukawa na mtiririko mzuri wa kimfumo wa
usimamizi wa mashauri ya jinai ili
kuondoa changamoto zinazokwamisha mashauri kumalizika na kuongeza kuwa Mahakama
haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100, ikiwa hatua zilizotangulia hazifanyi
kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi na kwamba kunaweza kuwa na Mahakama yenye
uwezo wa kusikiliza Mashauri Majaji na Mahakimu wenye uwezo lakini kama
uchunguzi haujakamilika au kuwepo kwa changamoto yoyote shauri haliwezi
kuendelea.
“Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia
100 ikiwa hatua zilizotangulia Mahakama hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa
ufanisi. Tunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza mashauri, Majaji
na Mahakimu wenye uwezo, na mifumo ya kielektroniki au miundombinu, lakini pia
ni waadilifu. Lakini kama uchunguzi haujakamilika, jalada halijawasilishwa,
mashahidi hawapatikani, maelezo hayajakamilika, hati za mashtaka zina kasoro,
mshtakiwa hajaletwa mahakamani, au nyaraka muhimu hazijafikishwa mahakamani
mapema, katika mtiririko kama huu kesi haiwezi kwenda mbele, hivyo ni vema
kukawa na ile systematic flow ya criminal justice ya case
management ili kuondoa hizo changamoto” amesisitiza Jaji Mkuu.
Akizungumza
kuhusu uwajibikaji na kujituma, Mhe. Masaju amesema kuwa, kila Taasisi ya Haki
Jinai inapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuondoa ucheleweshaji wa mashauri bila
kusubiri shauri lifike mahakamani huku akirejea Ibara ya 25 ya Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasisitiza juu ya uwajibikaji na
kujituma katika kila kazi kwa kufahamu chanzo cha kukwama kwa shauri, wapi lilipofikia
katika utekelezaji, imefikia hatua zipi za ushahidi, jambo litakalosaidia
mnyororo mzima wa haki jinai kufanya kazi vizuri.
Kadhalika,
Mhe. Masaju amewakumbusha wadau wa Haki Jinai kwamba, mfumo unahitaji
ushirikiano thabiti, mawasiliano ya karibu na uratibu mzuri ambayo ndio nguzo
ya mafanikio hivyo, taasisi zote zifanye kazi bila kujitenga.
“Ni
vyema tukumbuke kuwa, mfumo wetu wa haki jinai unahitaji ushirikiano thabiti (cooperation),
mawasiliano ya karibu (communication), na uratibu mzuri (coordination).
Hivi vitu vitatu yaani Cooperation, Communication, and Coordination ndivyo
nguzo kuu za mafanikio yetu katika usimamizi wa haki jinai. Kama taasisi moja
inafanya kazi kwa kujitenga au bila kutoa taarifa kwa nyingine, ni wazi kuwa,
kutakuwa na kukwama kwa mashauri au kuchelewa kwa haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Kadhalika,
Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuzingatia matumizi ya
Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuhakikisha mifumo inasomana
ili kurahisisha mchakato mzima wa kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo
bila kucheleweshwa na sababu zisizo na msingi.
Akihitimisha
hotuba yake. Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuchukua
tahadhari juu ya uwepo wa mvua za El nino kwa kuhakikisha wanaweka miundombinu
imara itakayowawezesha kufanya kazi pindi mvua hizo zitakapoanza kunyesha.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji, Viongozi na Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Baadhi ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakisikiliza hotuba ya Jaji Mkuu alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati kwa upande wa Mahakama wakati wa Mkutano kati ya Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)