Ijumaa, 28 Agosti 2026

WATUMISHI MBEYA WATEMBELEA KITUO CHA KUFUA UMEME MTERA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya amewaongoza Watumishi wa Masjala hiyo kufanya ziara ya kujifunza katika Kituo cha kupooza na kusambaza umeme cha Mtera, kilichopo Bwawa la Mtera mkoani Iringa kwa lengo kuwajengea watumishi uelewa wa masuala ya uzalishaji wa nishati ya umeme kwa njia ya maji.

Watumishi hao, walipata elimu ya kina kuhusu mchakato wa uzalishaji wa umeme, kuanzia hatua za awali za uzalishaji hadi umeme unapofikia hatua ya mwisho ya kumwezesha mtumiaji kupata huduma hiyo.

Aidha, elimu hiyo iliambatana na uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi, hususan katika matumizi ya majumbani na kwenye vyombo vya usafiri, huku watumishi wakifafanuliwa namna matumizi ya nishati safi yanavyoweza kuwa na mchango mkubwa katika kupunguza athari za kimazingira na kuboresha maisha na ustawi wa jamii.

Matumizi ya nishati safi yana manufaa mathalani kuokoa muda, kupunguza gharama, kutunza mazingira na kulinda afya za watumiaji, hivyo ni wito kwa jamii kuendelea kuhamasishwa na kuelimishwa kuhusu fursa na manufaa yanayotokana na matumizi ya nishati hiyo.

Watumishi hao wameaswa kuendelea kuwa mabalozi wazuri katika kutunza miundombinu ya umeme kwani umeme unachagiza maaendeleo ya Taifa, huku wataalum hao wakitoa wito kwa Majaji na Mahakimu kuchukulia kwa uzito wa aina yake suala uendeshaji wa mashauri yanayo husu uharibifu wa miundo mbinu ya umeme.

Ziara hiyo pia ilitoa fursa kwa watumishi hao kutembelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Iringa, ambapo walikutana na kufanya mazungumzo na viongozi pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala hiyo.

Mazungumzo ambayo yaliweka msisitizo katika umuhimu wa kuendelea kujenga ushirikiano, mshikamano na kubadilishana uzoefu miongoni mwa watumishi wa Mahakama katika Masjala hizo, kwa lengo la kuimarisha utendaji na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.

Sehemu ya watumishi na viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakipewa maelezo na elimu mbalimbali juu ya namna umeme unavyochakatwa katika ziara hiyo.

Sehemu ya watumishi na viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakipewa maelezo na elimu mbalimbali juu ya namna umeme unavyochakatwa katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akiteta jambo na Waandishi wa Habari katika ziara hiyo. 

Sehemu ya matukio mbalimbali ya watumishi wakiwa katika kituo cha Mtera

Sehemu ya watumishi na viongozi wakiwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Iringa ikiwa sehemu ya ziara hiyo.

Kaimu Meneja wa Kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Mtera Mhandisi William Modesti akiwapa elimu na kutoa historia ya kituo hicho na maendeleo yake kwa watumishi wa Mahakama Mbeya waliotembelea katika kituo hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya akitoa utambulisho na kuzungumza machache katika ziara hiyo wakiwa Mtera.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (kushoto), akipewa Zawadi ya jiko la umeme la kupikia “Electrical pressure cooker” wakati walipotembelea katika kituo cha kupooza na kusambaza umeme cha Mtera.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

WATUMISHI WA MAHAKAMA ARUSHA WAPATIWA MAFUNZO YA NAMNA YA KUPAMBANA NA MAJANGA YA MOTO

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Arusha

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wamepatiwa mafunzo ya namna ya kupambana na Majanga ya Moto mahali pa kazi.  

Mafunzo hayo yalifunguliwa hivi karibuni na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Frank Mahimbali ambapo alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwakuwa, yanasaidia kuokoa maisha ya wafanyakazi.

Akizungumzia suala la kupambana na majanga ya moto, Jaji Mahimbali alisema pia, mafunzo ya kupambana na majanga ya moto mahali pa kazi ni jambo muhimu kwa sababu, kulinda mali za Taasisi, na kupunguza hasara kubwa za kiuchumi zinazoweza kusababishwa na ajali za moto za ghafla.

Amesisitiza kuwa, umuhimu wa mafunzo hayo hauishii tu kazini bali pia hata nyumbani wanapoishi watumishi hao.

Faida za mafunzo ya moto ni nyingi na muhimu kwani husaidia kuokoa maisha, Wafanyakazi wanapata uelewa jinsi ya kutoka nje kwa usalama na haraka, wanapata ujuzi wa kutumia vizima moto kabla moto haujasambaa na hivyo kupunguza hasara kwa kuepusha mali na vifaa vya ofisi kuungua.

Utoaji wa elimu na mafunzo ya kupambana na majanga ya moto mahali pa kazi ni takwa la kisheria linalowataka Waajiri kuhakikisha usalama na afya ya wafanyakazi wao. Nchini Tanzania, sheria kuu inayosimamia suala hili ni Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi Na. 5 ya 2003.

Kwa mujibu wa sheria hiyo, wajibu wa Mwajiri ni kutoa elimu kwa kuwapa wafanyakazi mafunzo ya kuzuia na kupambana na moto, kuweka vifaa sahihi vya kuzimia moto mahali pa kazi, kuandaa njia za dharura na milango ya kutokea wakati wa hatari, na ukaguzi wa mara kwa mara kwa lengo la kuhakikisha mifumo ya tahadhali na kuzimia moto inafanya kazi vizuri.

Aidha, katika mafunzo hayo watumishi pia walijengewa uelewa juu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ili kuwajengea uelewa wa kutosha watumishi na hivyo kuwawezesha kuwa na taarifa sahihi zinazowasaidia kufanya maamuzi sahihi kila inapohitajika.

Mahakama Kanda ya Arusha ilialika Kampuni ya TGN ya Arusha ambayo hujishughulisha na masuala ya kupambana na majanga ya moto na utoaji elimu juu ya namna bora ya kupambana na moto.

Wataalamu wa kampuni hiyo walitoa elimu ya nadharia na vitendo ambapo watumishi mbalimbali waliweza kuzima moto kwa vitendo huku wengine wakishuhudia namna uzimaji moto unavyofanyika.


Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wakifanya mafunzo ya kuzima moto kwa vitendo wakisimamiwa na Wataalamu kutoka Kampuni ya TGN inayojishughulisha na kupambana na majanga ya moto, mafunzo haya yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akifungua Mafunzo ya namna ya kupambana na Majanga ya Moto mahali pa kazi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Watumishi wa Mahakama  Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mafunzo hayo.

Mtaalamu wa kupambana na majanga ya moto kutoka Kampuni ya TGN Arusha, Bw. Badru Juma akitoa elimu ya kuzima moto kwa watumishi wa Mahakama Arusha. Mafunzo hayo yalifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Arusha.


Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha wakifanya mafunzo ya kuzima moto kwa vitendo wakisimamiwa na Wataalamu kutoka Kampuni ya TGN inayojishughulisha na kupambana na majanga ya moto, mafunzo haya yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Arusha.


Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama akitoa mada juu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa watumishi wa Mahakama Arusha. Mafunzo hayo yaliyofanyika hivi karibuni yalienda sambamba na ya namna ya kupambana na Majanga ya Moto mahali pa kazi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



                            

 

                                                           

 


 

WATUMISHI MBEYA WAZURU MAKAO MAKUU, TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA

Na MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya wamefanya ziara ya kikazi ya kuzuru Makao Makuu ya Mahakama na Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma, kwa lengo la kuongeza uelewa wa masuala ya kiutumishi, kujifunza mifumo ya uendeshaji wa shughuli Mahakama na kubadilishana uzoefu ili kuimarisha utendaji kazi na utoaji wa huduma.

Ziara hiyo imeongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, akiambatana na Viongozi pamoja na watumishi.

Aidha, Watumishi hao walipata fursa ya kujifunza kwa kina kuhusu masuala yanayohusu utumishi ndani ya Mahakama, ikiwemo utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo inayosimamia utendaji wa Mahakama.

Aidha, watumishi hao walitembelea Ofisi za Tume ya Utumishi wa Mahakama, ambako walipata maelezo kuhusu majukumu ya Tume, hususan katika usimamizi wa masuala ya rasilimali watu, nidhamu, maadili na maendeleo ya watumishi wa Mahakama.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Naibu Katibu Tume ya Utumishi wa Mahakama anayeshughulikia Nidhamu na Maadili, Bi. Alesia Mbuya, aliwakaribisha watumishi hao na kuwapongeza kwa kutenga muda wa kutembelea Ofisi za Tume, akieleza kuwa, ziara hizo ni muhimu katika kuongeza uelewa na kuimarisha ushirikiano pamoja na kubadilishana uzoefu katika masuala ya kiutumishi.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, alieleza umuhimu wa watumishi kupata fursa za kujifunza kutoka katika maeneo mbalimbali ya Mahakama, akisisitiza kuwa maarifa na uzoefu unaopatikana kupitia ziara hizo ni muhimu katika kuboresha utendaji kazi wa kila siku.

Mbali na Ofisi za Tume ya Utumishi wa Mahakama, watumishi hao walitembelea maeneo mbalimbali ya kimkakati katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, ambako walijifunza namna matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) inavyotumika katika kurahisisha na kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya Mahakama.

Miongoni mwa maeneo yaliyotembelewa ni ukumbi mpya wa mikutano ulioandaliwa kwa mifumo ya kisasa ya TEHAMA, ambapo watumishi hao walijionea namna teknolojia inavyowezesha uendeshaji wa mikutano, mafunzo na shughuli mbalimbali za kitaasisi kwa ufanisi.

Vilevile, walitembelea Chumba cha Mifumo ya TEHAMA, ambacho ni miongoni mwa maeneo muhimu katika miundombinu ya kiteknolojia iliyopo ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama. Katika eneo hilo, watumishi walipata maelezo kuhusu uratibu, usimamizi na uendeshaji wa mifumo ya TEHAMA inayosaidia shughuli za Mahakama.

Ziara hiyo pia iliwapa watumishi hao fursa ya kutembelea Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, ambako walipokelewa na na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

Mhe. Tiganga, aliwashukuru watumishi hao kwa dhamira yao ya kuendelea kuimarisha ushirikiano, kujenga molari ya utendaji kazi kwa watumishi, matumizi ya teknolojia, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi, kwa kuweka mkazo katika kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuendeleza rasilimaliwatu kama msingi wa ufanisi.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa Mbele ya jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama walipotembelea katika ziara hiyo.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na mwenyeji wao Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma Mhe, Joachim Tiganga, Mbele ya jengo la Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma walipotembelea katika ziara hiyo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja viongozi wa Masjala hiyo walipotembelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo wa Dodoma.




Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama mbele) akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya walipotembelea ofisi ya Tume ya utumishi wa Mahakama

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa ndani ya ukumbi mpya wakisasa uliopo ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama.

Viongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa Mbele ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


MTENDAJI MKUU ATEMBELEA KITUO CHA USULUHISHI, MAHAKAMA YA ARDHI

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, tarehe 26 Agosti, 2026 alifanya ziara katika Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi pamoja na Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi kwa lengo la kujitambulisha.

Ziara hiyo imekuwa ya kwanza kufanyika tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huo.

Lengo lingine lilikuwa kufahamu kwa kina utekelezaji wa majukumu ya Mahakama hizo, kutathmini mafanikio yaliyopatikana pamoja na kubaini changamoto zilizopo katika utekelezaji wa majukumu.

Akizungumza na watumishi, Dkt. Jingu aliwasisitiza kuwa na upendo, mshikamano na kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuhakikisha Mahakama inaendelea kutoa huduma bora na kwa ufanisi kwa wananchi.

Alisisitiza umuhimu wa watumishi kushirikiana katika kutatua changamoto na kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kujituma.

Katika ziara hiyo, Mtendaji Mkuu aliambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, ambaye aliwapongeza watumishi kwa kazi nzuri wanayoifanyika na kusisitiza umuhimu wa kutenga muda kwa ajili ya kufanya mazoezi ya mwili ili kuimarisha afya na ustawi wao wanapotekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Mhe. Nkya pia aliwahimiza watumishi wa Mahakama hizo kuiishi salamu ya Mahakama inayosisitiza uadilifu, weledi na uwajibukaji katika kazi na kuwataka kuwa na maadili na matumizi ya lugha nzuri wanapowahudumia wananchi.

Naye Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani, alimshukuru Mtendaji Mkuu kwa kufanya ziara hiyo, kufanya majadiliano na watumishi na kuahidi kuzifanyia kazi changamoto zilizowasilishwa.

Ziara hiyo imekuwa muhimu katika kuimarisha mawasiliano, ushirikiano na uongozi kati ya watumishi na uongozi wa Mahakama ya Tanzania, pamoja na kuweka msisitizo katika utoaji wa huduma bora na ufanisi wa Mahakama.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt, John Jingu, akisalimiana na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani. Kulia akishuhudia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akichukua nafasi yake baada ya kuwasili kwenye Ofisi za Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi. Kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (kulia) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kushoto) wakizungumza na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani (katikati).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, akisaini kwenye kitabu cha wageni katika Ofisi ya Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Bi. Hellen Mkumbwa, akitoa utambulisho wa Viongozi mbalimbali kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (hayupo kwenye picha). 


Viongozi wa Mahakama wakimsikiliza Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Isaya Arufani (hayupo kwenye picha).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu akiwa katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda (picha chini).



Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza akiwa katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Bw. Donald Makawia, akitoa utambulisho wakati wa kikao hicho.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao hicho. Katikati ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Njingu na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Niku Mwakatobe (kulia) akichukua kumbukumbu muhimu wakati wa kikao hicho.


Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi na Divisheni ya Ardhi (juu na chini), wakimsiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Njingu (hayupo katika picha).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma. 

Alhamisi, 27 Agosti 2026

MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA ATEMBELEA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA KAZI

Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama ya Kazi, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, amefanya ziara katika Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, ikiwa ni ziara yake ya kwanza katika Mahakama hiyo tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huo.

Dkt. Jingu aliambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, pamoja na Katibu wa Mtendaji Mkuu, Bw. Thomas Mdenya na Katibu wa Msajili Mkuu, Mhe. Jovin Bishanga.

Ziara hiyo ililenga kujitambulisha rasmi kwa watumishi, kufahamu mwenendo wa utekelezaji wa majukumu na kusikiliza changamoto zinazowakabili katika mazingira yao ya kazi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Dkt. Jingu alisema ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za uongozi wa Mahakama kuendelea kuwa karibu na watumishi na kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu changamoto wanazokutana nazo katika kutekeleza majukumu yao.

Alisisitiza umuhimu wa watumishi kushirikiana na uongozi katika kutafuta suluhisho la changamoto hizo, huku wakizingatia wajibu wao wa kutoa huduma bora, kwa wakati na kwa weledi kwa wananchi.

Katika kikao hicho, watumishi walipata fursa ya kuwasilisha changamoto, hoja na mapendekezo mbalimbali yanayohusu mazingira ya kazi na utekelezaji wa majukumu yao. Dkt. Jingu aliahidi kuzifanyia kazi kwa kuzingatia taratibu na mamlaka zilizopo.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu aliwasihi watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma katika kutekeleza majukumu yao. Alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, mshikamano na misingi ya kazi, akieleza kuwa ushirikiano miongoni mwa watumishi ni muhimu katika kufanikisha malengo ya Mahakama.

Ziara hiyo imeendelea kuonesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuwa karibu na watumishi, kusikiliza changamoto zao na kuweka mazingira bora ya utendaji kazi.

Dhamira hiyo inaenda sambamba na jukumu la Mahakama la kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya haki mapema ipasavyo, kwa ufanisi na kwa kuzingatia misingi ya haki na utawala wa sheria.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt.  John Jingu, akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi (juu na chini).

Mtumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi akitoa hoja kwenye kikao hicho.

Meza Kuu inayoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (katikati).

Picha ya Meza Kuu inayoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (katikati waliokaa) na Viongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi.

Picha ya Meza Kuu inayoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (katikati waliokaa) na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Jumatano, 26 Agosti 2026

TRAB YATEMBELEA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA YA TANZANIA

Na HABIBA MBARUKU-Mahakama, Dodoma

Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania (Tanzania Revenue Appeals Board-TRAB) leo tarehe 26 Agosti, 2026 wametembelea Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania ili kujifunza kwa vitendo jinsi mifumo mbalimbali ya Mahakama, hususan Mfumo wa Kielektronki wa Usimamamizi wa Mashauri (e-CMS) inavyofanya kazi.

Ziara hiyo inalenga kuimarisha uelewa wa namna mifumo ya Mahakama kwenye utoaji haki inavyotekeleza majukumu yake kwa kutumia teknolojia za kisasa.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Richard Kabate, pamoja na Wataalamu wa TEHAMA wa Mahakama, walieleza kwa vitendo namna mfumo wa e-CMS wa Mahakama unavyofanya kazi zake za kusimamia mashauri katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

Wajumbe hao walipata fursa ya kuuliza maswali kuhusu mfumo huo, na baadaye kutembelea Chumba Maalumu cha Usimamizi wa Taarifa za Mahakama (Judiciary Situation Room) pamoja na Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre).

Ugeni huo uliongozwa na Mwenyekiti Msaidizi wa TRAB, huku Wajumbe wengine wakiwa Katibu Mtendaji wa TRAB, Mkurugenzi wa Sheria wa TRAB, Maofisa kutoka Wizara ya Fedha pamoja na wengine.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Richard Kabate, akitoa wasilisho kwa Menejimenti, Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania pamoja na Maofisa kutoka Wizara ya Fedha namna Mfumo wa Kielektronki wa Usimamamizi wa Mashauri unavyofanya kazi leo tarehe 26 Agosti, 2026, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Sheria wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania, Bi. Sekela Mwabukusi akisikiliza wasilisho kutoka kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Richard Kabeta (hayupo pichani).

Katibu Mtendaji Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania, Bi. Bahati Ndoserua, akisikiliza wasilisho.

Menejiment na Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania wakifuatilia maelekezo ya namna Mahakama inavyofuatilia mwenendo wa shughuli zake kupitia Chumba Maalumu cha Usimamizi wa Taarifa za Mahakama (Judiciary Situation Room).

Picha ya pamoja ya Menejiment, Wajumbe wa TRAB na Watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania, walipotembelea Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha Mahakama ya Tanzania.

Picha nyingine ya pamoja ikijumuisha Menejiment, Wajumbe wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania na Watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania baada ya kumaliza ziara yao Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Picha ya Meza Kuu, kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Richard Kabate, na kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Rufaa za Mapato ya Kodi Tanzania, Bw. Christopher David.