Ijumaa, 21 Agosti 2026

WATUMISHI MBEYA WAPITISHWA KWENYE RASIMU YA MPANGO MKAKATI WA MAHAKAMA 2026/27–2030/31

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, ameongoza mafunzo ya rasimu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa mwaka 2026/27–2030/31 kwa watumishi wa Mahakama Kuu kwa lengo la kuwajengea uelewa wa pamoja ili kila mtumishi aweze kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na kuchangia katika kufikia malengo ya Taasisi.

Mafunzo hayo yamefanyika jana Agosti 20, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, yakijumuisha watumishi wa Mahakama kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya na sehemu ya watumishi hao walishiriki mafunzo hayo kwa njia ya mkutano mtandao.

Akifungua mafunzo hayo, Mhe. Mtulya, alisisitiza umuhimu wa kila mtumishi kuuelewa kwa kina Mpango Mkakati wa Mahakama, akieleza kuwa, uelewa huo ni msingi muhimu wa utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Kila mtumishi wa Mahakama kwa ngazi zote anatakiwa afahamu kwa kina juu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ili kufanikisha malengo ya Taasisi, kwani kwa kufanya hivyo itatujengea ufanisi wa kutekeleza majukumu ili kulifikia lengo mama la Mahakama ya Tanzania la kutoa haki kwa wakati mapema ipasavyo,” alisema Mhe. Mtulya.

Jaji Mtulya ameongeza kuwa, uwasilishaji wa rasimu hiyo kwa watumishi wote unalenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mwelekeo wa Mahakama katika kipindi kijacho, hasa kutokana na changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa Mpango Mkakati uliopita wa mwaka 2021/22-2024/25, ambapo watumishi wengi hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu Mpango Mkakati huo.

Watumishi hao walipitishwa kwenye utekelezaji wa Mpango Mkakati uliopita, ikiwa ni pamoja na mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizojitokeza pamoja na mafunzo yaliyopatikana yanayopaswa kuzingatiwa katika kuandaa na kutekeleza Mpango Mkakati mpya.

Akifafanua umuhimu wa kuweka vipaumbele vinavyotekelezeka na vyenye tija, Mhe. Mtulya alisema: “Tunatakiwa kuwa na vipaumbele muhimu na vyenye tija na kuhakikisha bajeti iliyopo inaendana na vipaumbele vyetu,”

Amesisitiza kuwa, utekelezaji wenye mafanikio wa Mpango Mkakati wa Mahakama hautategemea mpango huo pekee, bali pia utayari, uwajibikaji na ushiriki wa kila mtumishi katika kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia mwelekeo na vipaumbele vya Taasisi.

Aidha, Jaji Mtulya alieleza kwa kina nguzo za kimkakati na maeneo ya msingi ya matokeo yaliyoainishwa katika rasimu hiyo, akifafanua namna malengo ya Taasisi yanavyoweza kufikiwa kupitia utekelezaji madhubuti wa majukumu ya kila mtumishi.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, alisisitiza umuhimu wa kuwa na Mpango Mkakati ambao siyo kwa Taasisi pekee bali hata katika maisha ya mtu mmoja mmoja, akihusianisha umuhimu wa kupanga, kuweka malengo kuyafanyia kazi na utekelezaji wake.

Naye, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, alitoa shukrani kwa Jaji Mfawidhi kwa uwezeshaji wa mafunzo hayo, huku akisisitiza umuhimu wa kila mtumishi kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia nguzo za kimkakati za Mahakama.

“Wote tunahusika katika kuhakikisha kuwa, nguzo hizo za kimkakati zinakuwa msingi wa utekelezaji wa majukumu yetu,” alisema Mhe. Laizer.

Katika hatua nyingine, watumishi walipata fursa ya kutoa maoni, ushauri na mapendekezo kuhusu maboresho ya vipengele mbalimbali vya rasimu hiyo, hatua iliyolenga kuhakikisha kuwa maoni ya watumishi yanazingatiwa katika kuboresha rasimu kabla ya kukamilishwa.

Jaji Mfawidhi, aliwashukuru watumishi kwa kushiriki katika mafunzo hayo na kuwataka kutambua thamani ya nafasi waliyonayo kama watumishi wa umma. Aidha, amewasisitiza kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kuzingatia misingi ya utumishi wa umma katika kutekeleza majukumu yao.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (Katikati), akiwasilisha rasimu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania kwa watumishi ya mwaka 2026/27–2030/31, Kulia ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer na (kushoto) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (aliyesimama) akizungumzia rasimu pendekezwa ya Mpango Mkakati wa Mahakama katika kikao hicho.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Sehemu ya Watumishi kutoka Mahakama mbalimbali Masjala Ndogo ya Mbeya walioshiriki na kupata mafunzo juu ya rasimu mpya ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31 katika mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Paul Dandi Ntumo akitoa maoni yake ya kuboresha katika rasimu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ya Mwaka 2026/27–2030/31.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (katikati) akichangia jambo katika Mafunzo hayo ya watumishi wa Masjala Ndogo ya Mbeya. 

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)





DKT. MAMBI AJITAMBULISHA KWA MKUU WA MKOA MANYARA

Na CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi amemtembelea Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbert Sendiga ofisini kwake jana tarehe 20 Agosti, 2026 kwa ajili ya kujitambulisha kwa viongozi na wadau wa Mkoa wa Manyara tangu alipohamia Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mwezi Juni, 2026.

Mhe. Dkt. Mambi alimshukuru Mhe. Sendiga kwa kumkaribisha ofisini kwake kwa ajili ya mazungumzo, kufahamiana na kujadiliana juu ya utendaji kazi na ushirikiano unaopaswa kuwepo baina ya Ofisi hizo.

Aidha, Mhe. Dkt. Mambi alimuomba Mkuu wa Mkoa huyo aweze kusaidia katika suala la upatikanaji wa viwanja kila Kata za Mkoa wa Manyara kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo.

“Kwa kuwa huduma za Mahakama zinaendelea kukua kila siku, tunaomba utusaidie katika michakato mzima wa kupata viwanja pamoja na hati za umiliki katika Kata ambazo hamna huduma za Mahakama ili tuweze kujenga Mahakama hizo na kusogeza huduma karibu na wananchi,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Kwa upande wake, Mhe. Sendiga alimuahidi Mhe. Dkt. Mambi kutekeleza jukumu hilo kwa kuwasiliana na mamlaka zilizopo chini yake ili viwanja hivyo vipatikane ili kukidhi adhima ya Mahakama ya kusogeza huduma za haki karibu na wananchi.

“Ninatambua kuwa Mkoa wetu wa Manyara una changamoto ya uhalifu na hususan mashauri ya kijinsia, na kwa sababu hiyo ni kweli kila mahali panahitaji kufikiwa na huduma hizi za Mahakama. Kwa sababu hiyo Mhe Jaji nitajitahidi kuwasiliana na viongozi wa Mamlaka nyingine ili tufanikiwe katika upatikanaji wa viwanja na hati hizo,” alisema Mhe. Sendiga.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mambi, alikukutana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa kwa ajili ya kujitambulisha na kufanya nao mazungumzo juu ya ushirikiano wa Taasisi zao katika mnyonyoro wa Utoaji haki. Viongozi hao wa Kamati ya Ulinzi na Usalama walimkaribisha na kumuahidi ushirikiano wa kutosha katika kuhakikisha kazi za Mahakama zinakwenda ipasavyo.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Mambi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemei.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa pili kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga (katikati), (wa pili kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava, (kulia) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemed, na (kushoto) ni Hakimu Mkazi na Msaidizi wa Sheria Mhe. Kuruthumu Mkundawantu.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Manyara Mhe Charles Mnzava (aliyesimama) akichangia jambo wakati wa mazungumzo kati ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemed (kushoto) akifuatilia mazungumzo kati ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi na Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga walipomtembelea Mkuu huyo wa Mkoa Ofisini kwake na kulia ni Hakimu Mkazi na Msaidizi wa Sheria Mhe. Kuruthumu Mkundawantu.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga (katikati) akichangia neno mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi (kulia) pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava mara baada ya kumtembelea ofsini kwake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi akiwa anamsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga (hayupo pichani) mara baada ya kumtembelea ofisini kwake.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbert Sendiga akiwa ofisini kwake akifanya mazungumzo na  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi (hayupo pichani) wakati alipomtelea ofisini kwa ajili ya kujitambulisha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyekaa kwenye kiti) akiwa katika picha ya pamoja na timu ya viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Manyara.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


VIONGOZI WA MAHAKAMA CHINA WATEMBELEA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA KAZI, KISUTU

Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama ya Kazi na WINFRED NZILANO-Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.

Baadhi ya viongozi kutoka Mahakama nchini China jana tarehe 20 Agosti, 2026, waitembelea Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi na katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu uendeshaji wa mashauri ya kazi.

Viongozi hao ni Shan Guojun, ambaye ni mjumbe wa kudumu wa kamati ya uamuzi wa mashauri Mahakama Kuu ya Watu Beijing na Wang Fei, ambaye ni Jaji wa Divisheni ya Kwanza ya Mashauri ya Madai ya Mahakama ya Watu Beijing.

Wengine ni Wu Bowen, ambaye ni Naibu Mkuu wa Divisheni ya Sita ya Madai Mahakama ya Watu Beijing pamoja na Li Guodong, ambaye ni Naibu Jaji Mkuu wa Divisheni ya Kwanza ya Madai ya Changping Beijing.

Wakiwa katika Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, wageni hao walipata maelezo kutoka kwa Naibu Msajili Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi, Mhe. Enock Matembele, ambaye aliwaelezea kwa kina namna uendeshaji na usimamizi wa mashauri ya kazi unavyofanyika, ikiwemo hatua mbalimbali zinazohusika katika mchakato wa utoaji haki.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, aliwashukuru viongozi hao kwa kutenga muda wa kuitembelea Mahakama na kushiriki katika ziara hiyo ya kubadilishana uzoefu.

Aidha, aliwakaribisha tena kutembelea Mahakama hiyo wakati mwingine, akieleza kuwa ushirikiano na kubadilishana uzoefu miongoni mwa Taasisi za Mahakama kutoka nchi mbalimbali ni muhimu katika kuimarisha utoaji wa haki na ufanisi wa huduma za Mahakama.

Viongozi hao wa Mahakama China pia walitembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa lengo la kubadilishana uzoefu kuhusiana na mamalaka ya Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya na namna mashauri ya kazi yanayohusiana na jinai na madai.

Ziara hiyo imekuwa sehemu muhimu ya kubadilishana uzoefu na maarifa kati ya mifumo ya utoaji haki ya Tanzania na China, hususan katika eneo la utatuzi wa migogoro ya kazi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akisalimiana na Mhe. Shan Guojun baada ya kuwasili kwenye Mahakama hiyo kwa ziara ya mafunzo na kubadilishana uzoefu kuhusu usikilizaji wa mashauri ya kazi.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi, Mhe. Enock Matembele, akiwaeleza wageni hao namna Mahakama hiyo inavyoendesha mashauri.

Uongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na Viongozi wengine wa wakiwa katika kikao cha pamoja.

Picha ya pamoja ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga (mbele kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama nchini China.

Picha ya pamoja ya Viongozi wa Mahakama nchini China na Mahakama ya Tanzania.

Viongozi wa Mahakama China wakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Viongozi wa Mahakama China wakipitishwa kwenye mada mbalimbali.

Viongozi wa Mahakama China na Vingozi Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ziara hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


Jumatano, 19 Agosti 2026

AMANI NA USALAMA NDIO MSINGI WA UWEKEZAJI: JAJI MRISHA

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe, Mhe. Abubakar Mrisha amesema amani na usalama ndio msingi mkuu wa kuvutia uwekezaji nchini na kusisitiza kuwa, utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 haiwezi kufanikiwa bila mambo hayo mawili kuwepo.

Mhe. Mrisha ameyasema hayo leo tarehe 19 Agosti, 2026 kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Gabriel Malata wakati akitoa salamu za Mahakama katika Jukwaa la Dira 2050 na Uwekezaji lililofanyika mkoani Songwe.

“Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa upande wa Mahakama ndio msingi mkuu katika kutekeleza yote yanayotakiwa kutekelezwa kutokana na Dira kwanini nalisema hili, ni kwa sababu ili Dira iweze kutekelezwa lazima kuwepo na amani, kuwepo na usalama na haya yote ndiyo yatakayokuwa ni kivutio cha wawekezaji na wafanyabiashara katika nchi yetu,” amesema Mhe. Mrisha.

Mhe. Mrisha ameeleza kuwa, jukumu kubwa la Mahakama ni kutafsiri sheria zinazotungwa na Bunge pamoja na sheria ndogo (by-laws) zinazotungwa na Madiwani pale msuguano unapotokea, ili kuhakikisha sheria hizo zinaleta amani na usalama kwa jamii.

Akitoa mfano wa usogezwaji wa huduma karibu na wananchi, Jaji Mrisha amebainisha kuwa kuanzishwa kwa Mahakama Kuu ndani ya Mkoa wa Songwe kumesaidia kupunguza kero na gharama za wananchi waliokuwa wakisafiri umbali mrefu kwenda Mbeya ili kupata huduma za rufaa, hatua ambayo imesaidia kuongeza muda wa kusikiliza mashauri na kuharakisha utoaji haki.

Amebainisha kwamba, haki ikichelewa inahesabika kuwa imekosekana, ndio maana Mahakama inaendelea na ujenzi wa Mahakama za Mwanzo na za Wilaya zikiwa zimeunganishwa na mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) itakayowezesha kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao, pamoja na matumizi ya Mahakama Inayotembea (Mobile Courts) ili kwenda na kasi ya utekelezaji wa Dira hiyo.

“Lakini kwa maendeleo ya TEHAMA Mahakama ina lengo la kufanya maendeleo na kuweka mfumo ambao kesi zitasikilizwa kwa njia ya mtandao, kwa hiyo utaona ni kwa kiasi gani tutakuwa tumepunguza gharama,” ameongeza Mhe. Mrisha.

Aidha, amewasihi wananchi na wadau mkoani Songwe kutumia fursa ya elimu na wataalam walioshiriki kwenye jukwaa hilo ili kuelewa fursa zilizopo na kuzitumia kuwekeza katika rasilimali za Mkoa huo kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Jukwaa la Dira 2050 na Uwekezaji limehudhuriwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo kama Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mkuu wa Wilaya wa Songwe pamoja na viongozi vingine wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Songwe.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe, Mhe. Abubakar Mrisha akitoa salamu za Mahakama kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Songwe, Mhe. Gabriel Malata katika Jukwaa la Dira 2050 na Uwekezaji lililofanyika leo tarehe 19 Agosti, 2026 mkoani Songwe. 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

JAJI MFAWIDHI MAHAKAMA YA KAZI ATEMBELEA TUME YA USULUHISHI NA UAMUZI

Na MWANDISHI WETU-Mahakama ya Kazi, Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, jana tarehe 18 Agosti, 2026 alitembelea Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Lengo la ziara hiyo ni kujionea utendaji, kufahamu kwa undani namna inavyotekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama ya Kazi na Tume katika kuhakikisha migogoro ya kikazi inatatuliwa kwa ufanisi na kwa wakati.

Ziara hiyo imekuwa ya kwanza kwa Mhe. Dkt. Kilekamajenga  katika Tume hiyo tangu alipoteuliwa kuwa Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuendelea kujenga uelewa na ushirikiano wa kiutendaji kati ya Taasisi zinazohusika katika mnyororo wa utoaji wa haki kazi nchini.

Jaji Mfawidhi alipokelewa na uongozi wa Tume na kupata fursa ya kutembelea baadhi ya ofisi, ambapo alijionea mazingira ya kazi na namna watumishi wanavyotekeleza majukumu yao ya kila siku.

Uongozi wa Tume ulimweleza Jaji Mfawidhi na wajumbe aliokuwa ameambatana nao kuhusu majukumu mbalimbali ya CMA, muundo wa utendaji kazi pamoja na nafasi ya Tume katika utatuzi wa migogoro ya kikazi nchini.

Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ni Taasisi huru ya utatuzi wa migogoro ya kikazi iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Taasisi za Kazi. Miongoni mwa majukumu yake ni kufanya usuluhishi wa migogoro ya kikazi inayowasilishwa mbele yake na, kwa mujibu wa sheria, kuamua migogoro kupitia mchakato wa uamuzi.

Akizungumza katika kikao cha pamoja, Mkurugenzi Mkuu wa CMA, Mhe. Usekelege Mpulla, alimweleza Jaji Mfawidhi kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri ya Usuluhishi na Uamuzi unaojulikana kama e-Utatuzi.

Mfumo huo ulianza kutumika rasmi Januari 21, 2026, ukiwa na lengo la kuboresha usimamizi na uendeshaji wa mashauri ya migogoro ya kikazi kwa kutumia teknolojia ya kidijitali.

Mfumo huo unamwezesha mdau kusajili na kufuatilia shauri lake kwa njia ya mtandao, bila kulazimika kufika ofisi za Tume kwa kila hatua.

Mpaka sasa, zaidi ya mashauri 1,678 yamewasilishwa kwa njia ya mfumo  ambapo mashauri 622 yameisha kwa njia ya usuluhishi na mashauri 277 yameisha kwa njia ya uamuzi.

Hata hivyo, Kiongozi huyo alieleza kwamba jitihada za kufanya mfumo huo usomane na mfumo wa usimamizi wa mashauri unaotumiwa na Mahakama ya Tanzania.

Akielezea umuhimu wa mfumo huo, Mkurugenzi wa CMA alisema matumizi ya e-Utatuzi yanalenga kuongeza ufanisi katika utendaji wa Tume, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kupunguza gharama ambazo wadaawa wanaweza kuzitumia katika kufuatilia mashauri yao.

Mfumo huo umesaidia kupunguza utegemezi wa majalada ya nakala ngumu, kuimarisha usimamizi wa nyaraka za mashauri na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika hatua mbalimbali za mchakato wa utatuzi wa migogoro.

Aidha, matumizi ya mfumo huo yanaongeza uwezekano wa huduma za utatuzi wa migogoro kufikiwa kwa urahisi zaidi na wananchi walioko maeneo mbalimbali nchini.

Mhusika anaweza kusajili na kufuatilia mwenendo wa shauri lake akiwa mahali alipo, kwa kutumia kifaa chenye mtandao, jambo linalosaidia kupunguza ulazima wa kusafiri mara kwa mara kwenda katika ofisi za Tume.

Kwa upande wake, Mhe. Dkt. Kilekamajenga aliipongeza Tume kwa namna inavyotekeleza majukumu yake katika kusaidia kutatua migogoro ya kikazi na kwa hatua zinazochukuliwa katika kuboresha huduma kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi alieleza kuwa ziara hiyo imempa fursa ya kupata uelewa mpana zaidi kuhusu utendaji wa CMA, changamoto zinazokabili Tume pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kuboresha huduma za usuluhishi na uamuzi.

Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama ya Kazi na CMA, akieleza kuwa Taasisi hizo zina nafasi muhimu katika mfumo wa utoaji wa haki za kazi nchini.

Jaji Mfawidhi aliwataka viongozi na watumishi wa Taasisi hizo kuendelea kushirikiana katika kubaini maeneo yanayohitaji maboresho, kubadilishana uzoefu na kutafuta njia bora za kuongeza ufanisi katika utatuzi wa migogoro ya kikazi.

Aidha, aliwasihi viongozi wa CMA kuendelea kufanya jitihada ili kuhakikisha mifumo hiyo inasomana na kurahisisha uendeshaji wa mashauri katika utoaji haki kazi.

Ziara hiyo imeonesha umuhimu wa mawasiliano na ushirikiano wa mara kwa mara kati ya Taasisi zinazohusika katika utoaji wa haki za kazi. Kwa kuwa CMA na Mahakama ya Kazi zina majukumu yanayogusana katika mnyororo wa utatuzi wa migogoro ya kikazi, ushirikiano wao unaweza kusaidia kubaini changamoto za kiutendaji na kutafuta suluhisho kwa pamoja.










BEIJING HIGH PEOPLE’S COURT SENIOR OFFICIALS VISIT JUDICIARY OF TANZANIA

  • Exchange knowledge, experience on labour dispute resolutions

By JUDICIARY REPORTER-Dodoma

Senior Officials from Beijing High People’s Court are in Tanzania for knowledge and experience sharing visit to the Judiciary of Tanzania and getting incites on issues relating to determination of labour disputes.

They are led by Standing Member of the Adjudication Committee of Beijing High People’s Court, Hon. Shan Guojun. The other officer in the delegation is Judge of the First Civil of Beijing High People’s Court, Hon. Wang Fei.

The rest are Deputy Chief Judge of the Sixth Civil Division of Beijing First Intermediate People’s Court, Hon. Wu Bowen and Deputy Chief Judge of the First Civil Division of Changping Primary People’s Court, Beinjing, Hon. Li Guodong.

They arrived at the Judiciary Square, the Headquarters of the Judiciary of Tanzania in Dodoma, at around 9.00am and were received by Acting Registrar of the High Court of Tanzania, Hon. Mary Moyo and other Deputy Registrars.

Presented at the warm welcome of officials of the Judiciary of China are Deputy Registrars Enock Matembele, Mary Mrio, Franco Kiswaga and Mwajabu Mvungi. After exchanging greetings, the guests were escorted to a conference room for other engagements.

In her welcoming note, Hon. Moyo, who is also Deputy Registrar of the High Court of Tanzania, Dodoma Main Registry, told the delegation that the visit provides a valuable platform for mutual learning on labour justice, judicial practice and institutional development.

“As reflected in the programme, our discussions will focus on the organizational structure and operational mechanisms of labour dispute adjudication, the role of courts in labour justice, the coordination between judicial and non-judicial dispute resolution bodies, and recent trends in judicial reform,” she said.

Hon. Moyo explained that the Judiciary of Tanzania attaches great importance to labour justice because labour disputes touch directly on human dignity, fairness in the workplace, economic stability and social harmony.

Therefore, she said, the Labour Division of the High Court plays a significant role not only in deciding disputes, but also in ensuring consistency in legal interpretation, fairness in adjudication, and confidence in the justice system as a whole.

“We believe that today’s engagement will strengthen professional understanding between our institutions and give us an opportunity to reflect on shared challenges, comparative experiences, and possible reforms in the administration of labour justice. It is our sincere hope that the exchanges scheduled for this visit will be fruitful, practical, and intellectually enriching to all of us,” Hon. Moyo said.

It was Hon. Matembele, who took on board the distinguished guests from the People’s Republic of China on the first presentation concerning “Experience sharing on organizational structure and operational mechanism of judicial governance system for labor disputes.

They were taken through on “Functional position of courts in labor dispute adjudication; coordination and linkage mechanisms among the judiciary courts, labor administrative department and mediation arbitration bodies and development trends in the judicial reform system.”

The presentation centered on organizational structure of judicial governance system for labour disputes and operational mechanism of judicial governance system for labour disputes.

It also covered functional position of courts in labour dispute adjudication; coordination and linkage mechanism among the judiciary, courts, labour; administrative departments and mediation and arbitration bodies and developments and trends in judicial reforms.

The second presentation related to judicial practice and the application of labour law in Tanzania: the role of the Labour Division of the High Court in governance, consistency, and reform of labour dispute adjudication.

Hon. Mrio presented the third presentation relating to the the Court of Appeal of Tanzania and the unification of legal application; Tanzania’s experience on appellate mechanisms, precedent, resolution of judicial disagreement, practical outcomes and challenges.

After the presentations, the officials discussed different issues and shared experiences on determination of labour disputes.

The delegations is scehduled tomorrow to visit the High Court Labour Division and later at the Kisutu Resident Magistrate's Court in Dar es Salaam to contune with the visit.

Deputy Registrars of the High Court of Tanzania in group picture with Senior Officials from Beijing High People’s Court few moments after arriving at the Headquarters of the Judiciary of Tanzania in Dodoma.


Acting Registrar of the High Court of Tanzania, Hon. Mary Moyo, who is also Deputy Registrar of the High Court, Main Registry, giving welcoming remarks to the guests.

Member of the Adjudication Committee of Beijing High People’s Court, Shan Guojun who is head of the delegation, giving introduction remarks on the purposes of the visit.

Senior Officials from Beijing High People’s Court following presentations during the session.


Deputy Registrars of the High Court of Tanzania during the session.


Deputy Registrar in Charge of the High Court Labour Division, Hon. Enock Matembele, stessing a point when making a presentation.




JOPO LA MAJAJI WA RUFANI LAFANYA TATHMINI YA UENDESHAJI MASHAURI MASJALA MBEYA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Rufani ya Tanzania hivi karibuni imefanya kikao cha tathmini ya utekelezaji wa shughuli za usikilizaji wa mashauri ya rufaa za madai na jinai katika Masjala Ndogo ya Mbeya, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhitimisha rasmi kikao cha Mahakama hiyo kilichoanza tarehe 3 Agosti, 2026 na kinachotarajiwa kumalizika tarehe 28 Agosti, 2026.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufaa ya Tanzania, Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani walioambatana naye katika kikao hicho ambao ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Dkt. Benhajj Shaban Masoud na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa kikao hicho, Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo alisema kuwa, kati ya mashauri 38 yaliyopangwa kusikilizwa, mashauri 33 sawa na asilimia 87% yameshasikilizwa na kupatiwa maamuzi.

Aidha, alieleza kuwa, mashauri 05 ya rufaa za madai yameahirishwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kuwapa warufani nafasi ya kuwafikishia wajibu rufaniwa hati za mashauri, kumpa nafasi mrufani kumteua wakili mwingine na kutoa nafasi ya kupatikana kwa mwakilishi wa kisheria wa mjibu rufani aliyefariki, hali iliyolazimu wahusika kuongezewa muda wa kufanya mabadiliko hayo.

Katika tathmini hiyo, ilibainika kuwa kumekuwa na changamoto kadhaa ikiwemo wadaawa kutokuleta taarifa za kuondoa mashauri mapema jambo ambalo lingesaidia kupanga mashauri mengine, kutokufuata taratibu za uendeshaji wa mwenendo kabidhi (committal proceedings), washtakiwa wengi wanaotajana kuwakilishwa na wakili mmoja, na kutokuzingatia kanuni inayotaka mdaawa akifariki ateuliwe msimamizi wa mirathi ndani ya miezi 12 kwa mujibu wa kanuni ya 105(2) ya kanuni za mahakama ya Rufani.

Aidha, pamoja na changamoto hizo, kikao kilieleza kuridhishwa na mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo kusikilizwa kwa mashauri 33 kati ya 38 yaliyopangwa pamoja na ushirikiano mzuri uliooneshwa na Warufani kwenye rufaa za madai, Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea waliohudhuria kwenye vikao hivyo kwa wakati.

Mafanikio hayo yameendelea kuimarisha juhudi za Mahakama ya Rufani ya Tanzania za kuongeza ufanisi katika usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema ipasavyo.

Viongozi wengine walishiriki kikao hicho ni kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya ambao ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo.

Wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo, Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Mahakimu mbalimbali wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya wilaya Mbeya Mhe. Teddy Mlimba, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Alintula Ngalile na wadau wengine wa haki Madai na Jinai Mawakili na wadau wengine wa Haki Jinai na madai kutoka Mbeya, Songwe na Tabora.

Mwenyekiti wa Jopo la Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Dkt. Gerald A. M. Ndika, (katikati) akiongoza kikao cha kufanya tathmini ya uendeshaji wa mashauri ya Madai na Jinai Masjala Ndogo Mbeya, kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina na kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Benhajj Shaban Masoud.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliohudhuria kikao cha tathmini (kulia) ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa pili kushoto) na Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer (kushoto)

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernad Mpepo akiwasilisha taarifa ya Naibu Msajili ya tathmini kuhusu uendeshaji wa mashauri ya rufaa Masjala Ndogo Mbeya katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao hicho.

Mwakilishi kutoka Gereza Kuu Ruanda Mbeya akitoa neno la shukurani kwa Jopo la Majaji wa Rufani katika kikao hicho.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)








WATUMISHI MASJALA NDOGO TABORA WAFANYA ZIARA YA KIKAZI MANYARA

Na CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara iliwaalika watumishi kutoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora kwa ajili ya mafunzo na kubadilishana uzoefu wa majukumu. Ziara hiyo imefanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 17 na 18 Agosti, 2026 ili kuwapa watumishi hao fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ya kimahakama.

Aidha, watumishi hao waliofika kutoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda

Akizungumza wakati wa ziara hiyo ya kikazi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi aliwapongeza watumishi hao wa Tabora kwa kuichagua Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya mafunzo hayo na kuwaeleza kuwa Manyara ni mahali sahihi pa kujifunza.

“Tunawakaribisha Manyara, hapa ni mahala sahihi kwenu pa kujifunza. Tumekuwa tukiwawezesha hata wanafunzi wa vyuo mbalimbali kupata mafunzo yao kwa ajili ya kutimiza vigezo na matakwa yao ya kielimu hivyo nanyi tunawakaribisha ili mjifunze na sisi pia tujifunze kutoka kwenu,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara kwa mapokezi mazuri ikiwa ni pamoja na kuwapa nafasi ya kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu majukumu ya kila siku ya mahakamani.

“Tumesikia mambo mazuri ambayo Wanamanyara mnayafanya hivyo nasi tukaona ni vema tufike tujifunze kutoka kwenu pamoja na kushiriki uzoefu wa Masjala zetu ili tuboreshe utendaji kazi wetu wa kila siku”, alisema Mhe. Ngimilanga.

Pamoja na kushiriki namna wanavyotekeleza majukumu yao ya kila siku, viongozi hao wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora waliweza kujifunza namna ya uandaaji bora wa taarifa mbali mbali za kimashauri pamoja na zile za Kiutawala ambazo huwa zinapaswa kuwasilishwa katika vikao mbalimbali. Katika hatua hiyo, viongozi hao waliweza kushiriki Kikao cha pamoja na viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara ambacho hufanyika kila wiki kwa ajili ya kupeana taarifa na maelekezo mbalimbali ya kikazi.

Akitoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda aliwapongeza watumishi wa Manyara pamoja na viongozi wao kwa kufanya kazi kwa bidii na kwa weledi hali ambayo inawezesha mashauri yao kwenda kwa haraka jambo ambalo linapunguza mlundikano wa mashauri.

“Kwa kweli tumeona jitihada zenu Wanamanyara katika usikilizwaji wa mashauri ya kila siku lakini pia katika usimamizi wa rasilimali zenu, tunaahidi kutumia elimu hii tuliyoipata katika kuboresha utendaji kazi wetu tutakaporejea Tabora.

Pamoja na kupata elimu na kubadilishana uzoefu juu ya utendaji kazi, Viongozi wa Mahakama hizo waliweka mikakati ya kuwa Masjala rafiki hata katika masuala ya kijamii na viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora waliweka ahadi ya kuwakaribisha watumishi wa Manyara kwenda Tabora kwa ajili ya kujifunza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyekaa mbele), pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu wakiwa katika mazungumzo ndani ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara pamoja na wageni waliotoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora kwa ajili ya mafunzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama wa nne kutoka upande wa kulia) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara pamoja na wageni wao waliotoka Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Tabora.

Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Manyara, Bw. Christopher Msagati akiwasilisha mada katika mafunzo waliyokuwa wanapatiwa viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda (kushoto), pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yakitolewa katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe Bw. Emmanuel Munda (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao cha kutoa taarifa kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora. Aidha, katika Runinga wanaoonekana ni washiriki wa kutoka Mahakama za Wilaya na za Mwanzo zilizopo katika Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara wakishiriki kwa njia ya video.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao cha kutoa taarifa kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (kulia) akifuatilia taarifa mbalimbali zilizokuwa zinatolewa katika Kikao kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora na (kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Kansha)