Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa rai kwa wadau wanaoshughulikia
Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa
Kibiashara kuchukua tahadhari na hatua madhubuti za kukabiliana na mvua za
Elnino kufuatia taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)
juu ya uwepo wa mvua hizo kuanzia mwezi Oktoba mwaka huu.
Mhe. Masaju ametoa
ushauri huo tarehe 16 Septemba, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa nne wa
Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya
Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara
uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania
jijini Dodoma.
Akizungumza na Wadau hao,
Mhe. Masaju amesema kuwa, Serikali inachukua hatua za kujikinga na kukabiliana
na janga hilo hivyo, na wao wanapaswa kuchukua tahadhari kila mmoja na kutazama
ni kwa namna gani wanaweza kuendeleza shughuli ikiwa mvua hizo zitakuwepo, pia
kila mmoja kwa imani yake kumuomba Mwenyezi Mungu bila kusubiri kuambiwa na
viongozi wa dini na pasipo kuringia kiburi cha uzima.
“Wadau wa haki mmejiandaa
vipi, TLS mmeshaandaa namna gani ya kuendelea kusikiliza mashauri haya, wakati
pengine njia barabarani hazifikiki, kwenye ‘Law fame’ zenu mna vyumba vya
kutosha, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na wadau
wengine humu tumejiandaa namna gani, hayo ndiyo ya kutafakari, sisi wenyewe
kwenye sekta hii tuchukue hatua namna gani tutaendeleza shughuli zetu kama hilo
janga litakuwepo, lakini pia na kumuomba Mwenyezi Mungu atukinge alitupilie
mbali hilo janga, tusiwe na kiburi cha uzima, tuone kama Mungu yupo, maji yana
nguvu Ghorofa hazisaidii kitu chochote,” amesema Jaji Mkuu.
Aidha, amesisitiza juu ya
maombi huku akirejea Kitabu cha Zaburi 103, kama muongozo katika maombi ambayo
itawawezesha wadau kuomba kwa yale ambayo yapo nje ya uwezo wao kuyadhibiti,
basi Mwenyezi Mungu kwa rehema na fadhili zake aingilie kati na kuliepusha
Taifa na janga hilo kwa sababu hakuna ambaye ana kinga ya uhakika ya kujiweka
salama pindi janga hilo litakapotokea.
“Sisi wengine hatuna
kinga ya kutofikiwa na hayo majanga ya elnino kama yatakuwepo, yapo mengine
yapo nje ya uwezo wetu, na mimi naamini uwepo wa Mwenyezi Mungu, kila mmoja
hapa hakuna ambaye anakinga ya kutokufa kwa majanga, kila mmoja achukue
tahadhari na kumuomba Mwenyezi Mungu, lazima tuwe tayari kumuomba kwa rehema,
neema na fadhili zake kwa mujibu wa Zaburi ya 103 ambayo tunaishi kwayo,
anaweza kuingilia kati akatunusuru kwakuwa hata uwezo wetu wa kujikinga na hayo
majanga ni mdogo,” ameongeza Mhe. Masaju.
Katika hatua nyingine,
Jaji Mkuu amebainisha changamoto ambazo zinasababisha ucheleweshaji wa
usikilizaji wa mashauri ya kiuchumi, ambazo amezitaja kuwa ni changamoto
zinazotokana na Mahakama yenyewe, changamoto za kisheria na changamoto
zinazotokana na wadau.
Amesema kuwa, changamoto
zinazotokana na Mahakama yenyewe ni hasa zile za kisheria, ambazo zinaambatana
na mfumo wa kitaasisi na kushauri kuwa wadau waendelee kubaini changamoto hizo
na kuzijadili kwa pamoja ili kuzipatia ufumbuzi pale ambapo mhusika amekwama
kuzitatua.
Amezitaja changamoto hizo
kuwa ni ufunguaji wa mashauri kwa lengo la kuchelewesha ulipaji wa madeni,
ambapo watu hufungua mashauri mahakamani ili wasiwajibike kulipa deni na
kuongeza kuwa, kukiwa na riba rafiki na upatikanaji wa elimu hususan elimu ya
mikopo na masuala ya bima watu watapata uelewa wa kutosha na kufahamu wajibu
wao na namna gani wanawajibika.
Kadhalika, ameitaja
changamoto nyingine kuwa, ni matumizi ya mbinu za kiufundi ili kuchelewesha
usikilizaji na uamuzi wa mashauri, hali ya kuwa Katiba imetoa muongozo wa
kutofungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki
kutendeka akirejelea Ibara ya 107A(2)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, (1977).
“Matumizi ya mbinu za
kiufundi ili kuchelewesha usikilizaji na uamuzi wa mashauri hizi (legal
technicalities), wakati Katiba imetoa mwongozo kwamba tusifungwe kupita kiasi
na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka, hilo sharti
limetajwa kwenye Ibara ya 107A(2)(e) haki inapaswa itendeke, tunapojiendekeza
kwenye hizi hili tunaahirisha tu mgogoro hatuwezi kutatua mgogoro,” ameongeza
Mhe. Masaju.
Pamoja na hayo, Jaji Mkuu
amesema kwamba, wadau wanapaswa kuendelea kudhibiti hatua zinazochelewesha
usikilizaji wa migogoro kwa kurahisisha matumizi ya notisi ya siku 90, kwa
kuangalia wanaohusika kumfanya yule anayepewa notisi kutaka kushtakiwa, awajibike
kuchukua hatua ambazo ni za kutatua na ikiwa ni hatua za usuluhishi wajadiliane
ili kurahisisha usikilizaji wa migogoro na kuwataka wanaohusika na kuchakata
notisi wawajibike ili kumaliza migogoro mapema ipasavyo.
“Wale wanaohusika na
kuchakata hizo notisi zinazotolewa na watu wanaotaka kuishtaki Serikali na
Taasisi zake, wawajibike kushughulikia hiyo changamoto inayopelekea watake
kushtakiwa, kwa namna hiyo migogoro mingi itaisha,” amesema Mhe. Masaju.
Katika hatua nyingine,
Jaji Mkuu ameongeza kuwa, uwajibikaji ni moja ya nyenzo inayotajwa katika Dira
ya Taifa ya Maendeleo, 2050 pia ni sharti la kikatiba kama Ibara ya 25 ya
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyosisitiza juu ya uwajibikaji, kujituma
na kuzingatia nidhamu ili kufikia malengo yaliyowekwa, hivyo ameipongeza Tume
ya Taifa ya Mipango kwa mkakati wanaouweka ili kuleta uwajibikaji.
“Uwajibikaji ni sharti la
kikatiba, kitu kikishawekwa kwenye sheria tunawajibika kukitekeleza kwa sababu
huwa kuna adhabu usipokitekeleza kwa hiyo Ibara ya 25 ya Katiba inatusisitiza
juu ya uwajibikaji lakini pia inasisitiza juu ya kujituma na inasisitiza juu ya
kuzingatia nidhamu ya kazi ili kufikia malengo tuliyojiwekea,” amesema Mhe.
Masaju.
Aidha, katika matumizi ya
Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), amesema Mahakama imepiga hatua
kubwa kwa kuweka mifumo mbalimbali ya matumizi ya TEHAMA huku mifumo mingine
ikiendelezwa na kuwasisitiza wadau hao
kuendelea kuimarisha matumizi ya TEHAMA kama yanavyosisitizwa katika Dira ya
Taifa ya Maendeleo, 2050. Ametaja manufaa ya kutumia TEHAMA katika utendaji
kuwa ni pamoja na kupunguza matumizi ya karatasi ili kuimarisha mwenendo wa
mashauri, kupunguza muda na gharama za kiutawala, kuongeza uwazi na
uwajibikaji, kuwezesha upatikanaji wa taarifa mapema ipasavyo na kutoa takwimu
zinazoweza kusaidia katika kupanga na kupima utendaji wa Mahakama.
Akihitimisha hotuba yake,
Jaji Mkuu amemtaka kila mdau wa haki kujitathmini, kubaini changamoto zake za
kiuwezo, kiutendaji na kimaadili na kuzifanyia kazi ili kwa pamoja kufikia
matarajio ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.















































