Ijumaa, 11 Julai 2025

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA ATEMBELEA BANDA LA MAHAKAMA MAONESHO YA 77

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Daniel Ndumbaro leo tarehe 11 Julai 2025 ametembelea Banda la Mahakama katika maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba), 2025 yanayoendelea kufanyika katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa Temeke Dar es Salaam.

Mhe. Dkt. Ndumbaro akiwa kwenye mabanda hayo alijionea watumishi wa Mahakama wanaotoa elimu kwa Wananchi mbalimbali wanaofika kupewa elimu hiyo ya kisheria na taratibu mbalimbali za uendeshaji wa shughuli za kimahakama.

“Mimi nimekuwa mdau na mpiga debe wa maboresho ya shughuli za Mahakama kwa mda mrefu na nitaendelea kufanya hivyo kwani Mahakama ni chombo chetu sote, vilevile niwapongeze kwa kazi kubwa mnayofanya ya kutoa elimu kwa umma hili ni jambo jema sana,” amesema Mhe. Dkt. Ndumbaro

Itakumbukwa kwamba, maonesho hayo yatahitimishwa tarehe 13 Julai, 2025 na Waziri huyo akatoa rai kwa wananchi mbalimbali kuendelea kutembelea Banda la Mahakama ya Tanzania lililopo katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba), 2025 yanayoendelea kufanyika katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa Temeke Dar es Salaam.





































(PICHA NA INNOCENT KANSHA - Mahakama 77)



ASHANTI GOLD YAKABIDHI NYUMBA YA KUTUNZIA VIELELEZO MAHAKAMA KUU GEITA

Na. DOTTO NKAJA-Mahakakama, Geita

Kampuni ya Uchimbaji Madini Mkoa wa Geita (Ashanti Geita Gold Mine Limited) hivi karibuni ilikabidhi nyumba ya kisasa ya kutunzia vielelezo katika Mahakama Kuu Geita kama sehemu ya kurejesha huduma kwa jamii.

Kitendo hicho pia ni kutambua mchango mkubwa unaotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Geita, hasa katika utoaji haki kwa wakati na kupunguza malalamiko katika jamii.

Mradi huo uliokabidhiwa kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina ulijengwa na kampuni hiyo katika mwaka wa fedha (2024/2025) baada ya Mahakama kukabiliwa na ufinyu wa nafasi ya kutunzia vielelezo.

Makamu Rais wa kampuni hiyo barani Afrika, Bw. Simon Shayo, ambaye aliambatana na Meneja Mwandamizi eneo la Mahusiano ya Jamii, Bw. Gilbert Mwulia, Mkuu wa Kitengo cha Wanasheria, Bw. David Nzaligo na Maofisa wengine ndiye aliyekabidhi nyumba hiyo kwa Jaji Mfawidhi.

Wakati akikabidhi nyumba hiyo yenye vyumba vitatu, Makamu Rais huyo alisema kuwa msaada wa ujenzi wa nyumba hiyo ni sehemu ya majukumu ya Kampuni yao kurejesha wanachokipata kwa jamiii.

Alisema pia kuwa hawatoishia kujenga nyumba hiyo bali wataendelea kuwezesha kama uhitaji utajitokeza kwa sababu Kampuni yake inatambua mchango wa Mahakama katika kutatua changamoto za utoaji haki mkoani Geita.

Naye Wakili Mwandamizi wa Sheria wa Kampuni hiyo alieleza kuwa moja ya thamani kubwa katika kampuni yao ni jamii kunufaika kupitia wanachokizalisha, hivyo wameona ni vyema wajenge nyumba ya kuhifadhia vielelezo kwa sababu mchakatoa mzima wa utaoji haki unahitaji pia utunzaji salama wa nyaraka.

Jaji Mfawidhi aliwashukuru kwa jambo kubwa walilolifanya na kueleza kuwa jengo hilo litasaidia kutatua tatizo la sehemu ya kutunzia vielelezo. Aliongeza kuwa nyumba hiyo itatumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA   kuhifadhi vielelezo ili kwenda na dhima ya Kanda ya Geita ya matumizi sahihi ya TEHAMA na kuacha matumizi ya karatasi.

Tukio hilo la kukabidhi nyumba lilishuhudiwa na Jaji wa Mahakama Kuu kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Fredrick Lukuna Viongozi wengine.

Makamu wa Rais wa Kampuni ya Geita Gold Mine Barani Afrika, Bw. Simon Shayo akikabidhi funguo ya nyumba ya kuhifadhia vielelezo kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina akizungumuza na Viongozi wa Kampuni la Uchimaji Madini Mkoa wa Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina akitoa shukrani kwa niaba ya watumishi wote wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita kwa wawakilishi kutoka Kampuni hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.



Alhamisi, 10 Julai 2025

JAJI MKUU AAHIDI KUSHUGHULIKIA CHANGAMOTO ZA KIMAHAKAMA ZINAZOWAKABILI MAHABUSU, WAFUNGWA

  • Atoa ahadi hiyo alipotembelea Gereza la Isanga Dodoma
  • Apongeza uboreshaji huduma za magereza nchini

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju ameahidi kushughulikia changamoto za kimahakama zinazowakabili mahabusu na wafungwa waliopo gerezani lengo likiwa ni kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wakati.

Mhe. Masaju amebainisha hayo leo tarehe 10 Julai, 2025 wakati akizungumza na Mahabusu na Wafungwa alipotembelea Gereza Kuu la Isanga mkoani Dodoma kwa lengo la kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili wafungwa na mahabusu waliopo kwenye gereza hilo.

“Kwetu sisi hizi taarifa ambazo tumezipata hapa, malalamiko haya yatatusaidia kutambua tatizo liko wapi, hivyo yatatusaidia kubuni mikakati ya namna ya kushughulikia changamoto hizi ipasavyo na kwa ufanisi,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema kuwa, moja ya malengo ya kutembelea Gereza hilo ni pamoja na kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati alipomuapisha Mhe. Masaju kushika nafasi hiyo ambapo alimuelekeza kufanyia kazi maoni na mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai ikiwa ni pamoja na kuangalia eneo la Magereza.

“Pamoja na kwamba ninapenda kutembelea Magereza mara kwa mara, lakini hii ziara imekuja nikiwa na sababu mahsusi, nilipoapishwa siku ile moja ya maelekezo ambayo Rais aliniambia ni kwamba niyafanyie kazi mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai,” ameeleza Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, pamoja na kwamba taarifa za Tume hiyo zipo ofisini ni muhimu kuzungumza na wahusika kwakuwa wanatoa picha halisi ya wapi pa kuanzia na kujua ni mikakati gani ya kuweka katika kushughulikia mapendekezo yaliyoainishwa na Tume ya Haki Jinai.

Akizungumzia kuhusu baadhi ya hoja, malalamiko na changamoto zilizotolewa na Mahabusu, wafungwa, Mhe. Masaju amewaahidi kuwa, yatafanyiwa kazi na matokeo yake watayaona. Amewataka pia, Mahabusu na wafungwa hao waendelee kuwa raia wema.

Baadhi ya changamoto zilizowasilishwa na mahabusu na wafungwa kupitia taarifa zao walizowasilisha mbele ya Jaji Mkuu na ujumbe alioambatana nao ni pamoja na ucheleweshaji wa vitabu vya rufani, kukosa nakala za nia, unyanyasaji katika vituo vya Polisi ikiwemo vipigo, mashahidi kutofika mahakamani kwa wakati na kadhalika.

Aidha, Jaji Mkuu amempongeza Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu kwa kuendelea kuboresha huduma za magereza nchini.

“Nalipongeza Jeshi la Magereza kwa hatua kubwa za uboreshaji wa huduma kwa kuwa hali haikuwa hivi siku za nyuma, mimi nimekuwa nikitembelea magereza mara kwa mara, nimetembelea sehemu wanapolala wafungwa wenye adhabu za kunyongwa pameboreshwa sana tofauti na ilivyokuwa awali, vilevile nawapongeza kwa kutumia nishati safi kupikia,” amesema Mhe. Masaju.

Kwa upande wake, Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu akitoa taarifa ya hali ya magereza mbele ya Jaji Mkuu amesema, kwa sasa kumekuwa na upungufu wa wahalifu huku akiishukuru Mahakama ya Tanzania kwa ushirikiano inaotoa pamoja na wadau wengine wa haki jinai.

"Jeshi la Magereza lina jumla ya Magereza 129 nchini, na Magereza haya yana uwezo wa kuhifadhi wahalifu 29,902, kwa tarehe 10 Julai, 2025 tumekuwa na wahalifu pungufu ya nafasi zilizopo, tunahifadhi wahalifu takribani 27,000 kwa siku na nafasi zilizopo ni 29,902 tafsiri yake ni kwamba tumekuwa na upungufu wa wahalifu kulingana na nafasi zilizopo," amesema Kamishna Jenerali Katungu.

Kadhalika, Kamishna huyo, amemshukuru Rais Samia kwa kuunda Tume ya Haki Jinai kwakuwa wamefanyika kazi mapendekezo yaliyotolewa na Tume hiyo kuhusu Magereza na manufaa yake yameanza kuonekana kwakuwa kumekuwa na upungufu wa wahalifu. 

Ameongeza kwa kuushukuru Mhimili wa Mahakama kwa kuendelea kushirikiana na Jeshi hilo hususani katika usikilizwaji wa mashauri ya mahabusu na wafungwa hususani katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano sambasamba na kaguzi za mara kwa mara zinazofanywa na Majaji. 

Mhe. Masaju amepata fursa ya kukagua maeneo kadhaa katika gereza hilo ikiwa ni pamoja na vyumba wanapolala wafungwa wa kunyongwa, jikoni na sehemu nyingine kadhaa.

Gereza la Isanga limekuwa ni Gereza la kwanza kutembelewa tangu Jaji Mkuu, Mhe. Masaju alipoteuliwa kushika nafasi hiyo. Jaji Mkuu ameambatana na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Bw. Sylvester Mwakitalu, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama ya Rufani (T), Mhe. Emmanuel Mrangu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, Mwakilishi wa Uhamiaji, Watumishi wengine wa Mahakama na wadau.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Mahabusu na Wafungwa wa Gereza la Isanga lililopo mkoani Dodoma leo tarehe 10 Julai, 2025 alipotembelea gereza hilo. Kushoto ni Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akisisitiza jambo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju (mwenye tai nyekundu) akifanya ukaguzi wa Gereza la Isanga leo tarehe 10 Julai, 2025 alipotembelea gereza hilo. Kushoto kwake ni Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju (mwenye tai nyekundu) akiwa katika eneo la Gereza la Isanga Dodoma alipofanya ziara katika gereza hilo leo tarehe 10 Julai, 2025.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju (wa pili kulia) akiwa ndani ya kasha maalum la kisasa lililotolewa na Mahakama linalotumika katika gereza hilo kuendeshea mashauri kwa njia ya mtandao bila washtakiwa kufikishwa mahakamani. Kulia kwa Jaji Mkuu ni Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu na anayefuata ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na kulia kwa Mhe. Dkt. Siyani ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akikagua gwaride maalum aliloandaliwa na Jeshi la Magereza alipotembelea Gereza la Isanga mkoani Dodoma leo tarehe 10 Julai, 2025.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akisaini kitabu cha wageni alipowasili katika Gereza la Isanga Dodoma kwa lengo la kufanya ukaguzi.


Sehemu ya Maofisa kutoka Mahakama ya Tanzania wakifuatilia kwa makini kilichokuwa kikijiri wakati wa ziara ya Jaji Mkuu katika Gereza la Isanga mkoani Dodoma.Wa kwanza kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, wa pili kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, katikati ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, wa pili kulia ni Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama ya Rufani (T), Mhe. Emmanuel Mrangu na wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ambaye pia ni Msaidizi Binafsi wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju (wa pili kulia) akipokea taarifa kutoka kwa Mkuu wa Gereza la Isanga leo tarehe 10 Julai, 2025 alipotembelea gereza hilo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na Maofisa wa Mahakama na Magereza na wadau wengine wa Haki Jinai. Wa pili kushoto ni Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu, wa pili kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo na wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Bw. Sylvester Mwakitalu.

Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu (kushoto) akikabidhi zawadi ya begi kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju baada ya kukamilisha ziara ya ukaguzi aliyofanya katika Gereza la Isanga lililopo jijini Dodoma.

Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu (kushoto) akimkabidhi zawadi Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kulia). Anayeshuhudia katikati ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju na wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (kulia) akipokea zawadi kutoka kwa Kamishna Jenerali wa Magereza Tanzania, Jeremiah Yoram Katungu.

(Picha na MARY GWERA na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma)






TANZIA; NAIBU MSAJILI MAHAKAMA KUU KANDA YA ARUSHA, MHE. FRANCIS KABWE AFARIKI DUNIA


Marehemu Francis Jacob Kabwe enzi za uhai wake.

 TANZIA

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake aliyekuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Francis Jacob Kabwe. 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 10 Julai, 2025 na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi, marehemu Kabwe alifikwa na umauti Siku ya Jumanne tarehe 08 Julai, 2025 katika Hospitali ya KCMC Moshi mkoani Kilimanjaro alipokuwa akipatiwa matibabu.

Mhe. Msumi amesema kuwa, taratibu za mazishi zinaendelea kufanyika na marehemu Kabwe anatarajiwa kuzikwa Siku ya Jumapili tarehe 13 Julai, 2025 katika eneo la Mamba Miamba Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro.

Marehemu Kabwe alizaliwa tarehe 20 Novemba, 1976 mkoani Kilimanjaro na kupata elimu katika Shule ya Sekondari Bulima mwaka 1995 na Shule ya Sekondari Ikizu mwaka 1998.

Aidha, Mhe. Kabwe alihitimu katika Chuo Kikuu cha Tumaini-Iringa mwaka 2002 ambapo alisomea taaluma ya Sheria.

Marehemu Francis Kabwe aliajiriwa na Mahakama tarehe 19 Mei, 2003 na kuanza kufanya kazi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi mkoani Kilimanjaro na kufanya kazi katika vituo mbalimbali vya Mahakama nchini. Aliteuliwa kuwa Naibu Msajili mwaka 2009.

Mhe. Kabwe alianza kuugua mwaka 2021 ambapo amekuwa akipata huduma ya matibabu katika hospitali mbalimbali ndani na nje ya nchi hadi alipofariki dunia tarehe 08 Julai, 2025. Marehemu ameacha Mke na Watoto wawili.

Mahakama ya Tanzania inaungana na ndugu, jamaa na marafiki katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza msiba huo mzito wa kuondokewa na Mpendwa wetu.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA, JINA LAKE LIHIMIDIWE.