Ijumaa, 26 Julai 2024

MAHAKIMU, WADAU WILAYANI ROMBO WAPIGWA MSASA JUU YA WAHANGA WA UKATILI WA KINGONO

Na PAUL PASCAL –Mahakama, Moshi

Mahakama ya Wilaya Rombo mkoani Kilimanjaro imeendesha mafunzo kwa Wadau wa Mahakama na Mahakimu wa Wilaya hiyo juu ya namna ya kujiepusha kurejesha jeraha kwa wahanga wa ukatili wa kingono. 

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo hayo leo tarehe 26 Julai, 2024 yanayofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama hiyo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Rombo, Mhe Nuruprudensia Nasari amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwapa uelewa wa pamoja katika kujiepusha kutonesha jeraha kwa wahanga wa ukatili wa kingono wakati wanapotekeleza majukumu ya utoaji haki ambalo kimsingi ndio jukumu kuu la Mhimili huo.

“Kwanza niwashukuruni nyote kwa kushirikiana na sisi katika dhamira hii yetu ya kuhakikisha tunaiihudumia jamii yetu pasi na kuwakwaza wala kusababisha malalamiko niweke wazi pamoja na mambo mengine niwaombe kutumia fursa hii ya kujifunza mambo haya kwa umakini ili sote tuweze kuzungumza lugha moja pale tunapokuwa na mazingira ya kumuhudumia mtu mwenye jeraha la uhanga wa ukatili wa kingono,” amesema Mhe. Nasari.

Naye Mkufunzi wa mafunzo hayo ambae pia ni Hakimu Mkazi Mkuu, Mhe. Ruth Mkisi aliwaelezea washiriki kwamba, chanzo na dhima ya mafunzo hayo ni kujijengea uwezo ili kujiepusha na lawama kutoka kwa jamii wanayoihudumia na hivyo kuwasihi kuwa na utulivu ili waweze kufikisha yale yote waliyoyaandaa kwa ajili ya washiriki hao.

“Mafunzo haya awali yalitolewa na wenzetu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa Ufadhili wa (Irish Rule of Law International) lakini leo hii Mahkama ya wilaya Rombo wamewaza mbali na kuona ni vema sote kwa pamoja tukapata mafunzo haya,” amesema Mhe. Mkisi.

Mafunzo hayo yamejumuisha jumla ya washiriki 16 kutoka Ofisi za Wadau wa Mahakama katika mnyororo wa utoaji haki ambao ni Ofisi ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali Wilaya ya Rombo, Mawakili wa Kujitegemea kutoka Chama cha Mawakili (TLS), Mkoa wa Kilimanjaro pamoja na maafisa Ustawi wa jamii wa wilayani humo.

Mafunzo hayo ni ya siku moja na mada zitakazowasilishwa kwa washiriki ni pamoja na namna bora ya kujiepusha na kurejesha jeraha kwa wahanga wa ukatili wa kingono. Mada hizo zimeandaliwa na Chuo Cha Uongozi wa Mahakama (IJA) katika mafunzo yaliyofanyika mkoani Arusha ambapo kila mkoa ulitoa washiriki. 

Mahakama ya Wilaya Rombo imeandaa mafunzo hayo ili kuwawezesha wahusika wote katika mnyororo wa utoaji Haki kuwa na uelewa wa pamoja.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Rombo, Mhe. Nuruprudensia Nassari  akitoa hotuba ya ukaribisho kwa washiriki wa mafunzo juu ya namna ya kujiepusha kurejesha jeraha kwa wahanga wa ukatili wa kingono leo tarehe 26 Julai, 2024 katika ukumbi wa Mahakama hiyo.

 

Hakimu Mkazi Mkuu na Mkufunzi katika mafunzo hayo, Mhe. Ruth Mkisi akiwasilisha mada kwa washiriki wa mafunzo ya namna ya kujiepusha kurejesha jeraha kwa wahanga wa ukatili wa kingono (hawapo katika picha).

Mshiriki wa mafunzo hayo kutoka Ofisi ya Ustawi wa Jamii wilayani Rombo akichangia mada wakati mafunzo hayo yakiendelea.

 Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Rombo, Mhe. Innocent Nyella akitoa neno la shukrani kwa uongozi kwa Mahakama  hiyo kwa kuwaandalia mafunzo hayo.

Washiriki na wakufunzi wakiwa katika picha ya pamoja mbele ya jengo la Mahakama ya Wilaya ya Rombo mara baada ya kumalizika kwa mafunzo hayo yaliyofanyika leo tarehe 26 Julai, 2024 katika ukumbi wa Mahakama hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



JAJI MKUU WA ZANZIBAR ATEMBELEA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA DODOMA

Aipongeza Mahakama kwa hatua ya maboresho ya miundombinu ya majengo

Na Jeremia Lubango, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla leo tarehe 26 Julai 2024 ametembelea Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kuipongeza Mahakama kwa hatua kubwa iliyopiga kwa upande wa miundombinu.

Jaji Mkuu wa Zanzibar na ujumbe kutoka Mahkama ya Zanzibar walifika Makao Makuu ya Mahakama majira ya saa 3 asubuhi na kupokelewa na Mwenyeji wake Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani pamoja Mkurugenzi Msaidizi wa Utumishi, Mahakama ya Tanzania, Bw. Stephen Magoha.

Baada ya kuwasili katika jengo hilo, Mhe. Abdalla alipata fursa ya kujionea na kujifunza shughuli mbalimbali za kiutendaji zinazoendelea mahali hapo.

Akiwa ofisini kwa Jaji Kiongozi, Mhe. Abdalla alipata wasaa wa kupokea maelezo mafupi kutoka kwa mwenyeji wake, Mhe. Siyani juu ya namna taratibu za uendeshaji wa shughuli za Mahakama zinavyoendeshwa Makao Makuu.

Baada ya hapo Jaji Mkuu huyo akiwa ameambatana pamoja na baadhi ya Majaji, Watendaji, Wasajili na Maafisa mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Afisa kutoka Kurugenzi ya Usimamizi wa Majengo Mahakama ya Tanzania, Bi. Kailat Bakari walimpitisha maeneo ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama.

Mhe. Abdalla alitembelea ofisi mbalimbali zilizomo katika jengo hilo ikiwemo Ofisi ya Jaji Mkuu, Ofisi ya Msajili Mkuu, Chumba cha Mifumo ya Kutolea Taarifa Muhimu za Mahakama (Judiciary Situation Room), Kumbi za Mahakama (Court Rooms), Ofisi ya Huduma kwa Mteja (Call Centre) pamoja na kujionea miundombinu iliyomo ndani ya jengo hilo.

Alipokuwa Chumba cha Mifumo ya Kutolea Taarifa Muhimu za Mahakama alijionea namna Chumba hicho kinavyofanya kazi  a kuipongeza Mahakama ya Tanzania kwa hatua kubwa waliyopiga.

“Nilikuwa naambiwa leo nimejiona kwa macho yangu hakika kwa Afrika ndio Nchi pekee yenye Chumba cha kutolea taarifa muhimu kwa majengo ya Mahakama,” alisema.

Baada ya hapo, Jaji Mkuu huyo alihitimisha ujio wake kwa kutembelea na kujionea nyumba za Majaji zilizojengwa Iyumbu jijini hapa.


Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akimsikiliza Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (kulia) pindi alipowasili ofisini kwa Jaji Kiongozi tayari kwa kutembelea na kujionea jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania leo tarehe 26 Julai, 2024 jijini Dodoma. 
 
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (wa pili kushoto) akimsikiliza Afisa kutoka Kurugenzi ya Usimamizi wa Majengo Mahakama ya Tanzania, Bi. Kailat Bakari (mwenye ushungi) wakati alipotembelea kwenye moja ya kumbi za Mahakama zilizopo katika jengo la Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma leo tarehe 26 Julai, 2024. Wa kwanza kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, wa tatu kushoto ni Jaji wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, Mhe. Edwin Elias Kakolaki pamoja na Maafisa wengine wa Mahakama. 
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (wa pili kushoto) akizungumza jambo wakati alipokuwa akipitishwa katika maeneo mbalimbali ndani ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wa kwanza kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa pamoja na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (kulia) walipokuwa katika moja ya kumbi za Mahakama ndani ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama. Kushoto ni Afisa kutoka Kurugenzi ya Usimamizi wa Majengo Mahakama ya Tanzania, Bi. Kailat Bakari.
Afisa na Msimamizi wa Mifumo ya TEHAMA- Mahakama ya Tanzania, Bw. Witness Ndenza (kulia) akimuelezea Jaji Mkuu wa Zanzibar namna Chumba maalum cha Kutolea Taarifa za Mahakama kinavyofanya kazi wakati Jaji Mkuu huyo alipotembelea Chumba hicho leo tarehe 26 Julai, 2024.
Jaji Mkuu wa Zanzibar akiwa katika Ofisi ya Huduma kwa Mteja (Call Centre) alipotembelea Ofisi hiyo iliyopo ndani ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania leo tarehe 26 Julai, 2024 jijini Dodoma.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (aliyenyanyua mkono) akizungumza jambo katika Ofisi ya Huduma kwa Mteja wakati Jaji Mkuu wa Zanzibar alipotembelea Ofisi hiyo.
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto). Wa pili kulia ni Jaji wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, Mhe. Edwin Elias Kakolaki, wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Utumishi, Mahakama ya Tanzania, Bw. Stephen Magoha pamoja na Watumishi wengine wa Mahakama.

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto) na Jaji wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, Mhe. Edwin Elias Kakolaki (kulia).

Mkurugenzi Msaidizi wa Utumishi, Mahakama ya Tanzania, Bw. Stephen Magoha (kulia) akimuongoza Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (wa pili kulia) kutembelea nyumba za Majaji zilizopo Iyumbu jijini Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

MAHAKAMA, BENKI YA DUNIA WAMTAKA MKANDARASI MRADI WA UJENZI 'IJC' NJOMBE KUONGEZA KASI

Na Abdallah Salum, Mahakama-Njombe

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama, Mhe. Dkt, Angelo Rumisha sanjari na ujumbe kutoka Benki ya Dunia wamemtaka Mkandarasi, Bw. Lee Manchao kutoka Kampuni ya Shadong inayosimamia ujenzi wa Kituo cha Utoaji Haki (IJC) Njombe kuongeza kasi ya ujenzi wa Kituo hicho ili kukamilisha kwa wakati waliokubaliana.

Agizo hilo lilitolewa jana tarehe 25 Julai, 2024 katika kikao cha pamoja na Mkandarasi huyo kilichohusisha ujumbe kutoka Mahakama ya Tanzania na Benki ya Dunia walipofanya ziara ya ukaguzi wa Mradi wa ujenzi huo.

Ripoti mbalimbali kutoka kwa Wahandisi wa Mradi wa IJC Njombe zinaonesha kuwa, ujenzi wa ghorofa ya kwanza umekamilika kwa asilimia 26.0 na ujenzi wa uzio umekamilika kwa asimilia 45, hali hiyo inaonesha Mradi bado upo nyuma ukilinganisha na mkataba waliokuwa wamekubaliana kufikia kipindi cha mwezi Julai ambapo ulitakiwa uwe umefikia asilimia 82.5.

Kwa upande wake, Kiongozi wa msafara kutoka Benki ya Dunia (WB), Bi. Christine  Owour alisema kuwa, Mradi huo unakwenda  taratibu, hivyo, amewashauri Wahandisi waweze kujadiliana kufikia lengo ili Mradi huo uweze kumalizika kwa  wakati.

Naye, Afisa Mwandamizi kutoka Benki ya Dunia, Bw. Benjamin Mtesigwa aliwashauri Wakandarasi kuwa na mpango kazi ili kufidia muda uliopotea.

“Mkandarasi yupo nje ya muda kwa asilimia 50, hivyo wanavyoomba kuongezewa muda wanatakiwa wawe na maelezo ya kujitosheleza, pia wakae na Mhandisi Mshauri awape mpango wa kufidia muda waliopoteza hasa kuwapa ratiba na  muda wa kazi ili kufidia muda  waliopoteza,” alisema Bw. Mtesigwa.

Naye Afisa Mazingira, Bi. Edina Kashangaki alifanya tathmini ya maendeleo ya ujenzi na kutoa pongezi kwa upande wa wafanyakazi kwamba hakuna unyanyasaji wa kijinsia, lakini pia alipitia mikataba ya wafanyakazi na kuangalia  michango yao  inaingia  kwenye mfuko  wa  NSSF.

Aidha, Mkandarasi wa Mradi huo  alitoa sababu ambazo zimechelewesha kuwa ni pamoja na hali ya hewa iliyochangiwa na mvua nyingi za masika kuanzia  Januari-Aprili mwaka huu pamoja na  vifaa kucheleweshwa kufika eneo husika.   

Mradi wa Ujenzi wa IJC Njombe pamoja na Vituo vingine nane vinavyoendelea kujengwa nchini unafadhiliwa na fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia. 

 

Mhandisi ujenzi IJC Njombe, Bw.Harold Ngumuo (kushoto) akiwaonesha wajumbe kutoka Mahakama na Benki ya Dunia jinsi ramani ya Kituo hicho ilivyokaa na ujenzi unavyoendelea jana tarehe 25 Julai, 2024. Kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha anayefuata Kiongozi wa Msafara kutoka Benki ya Dunia, Bi. Christine Owour na aliyesimama kushoto kwa Mhandisi Afisa Mazingira, Bi. Edina Kashangaki pamoja na Wakandarasi wengine.

Wakandarasi pamoja na Wajumbe kutoka Mahakama na Benki ya Dunia wakiwa kwenye eneo inapojengwa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki 'IJC' Njombe wakielekea kwenye kikao cha majadiliano kuhusu ujenzi wa Kituo hicho jana tarehe 25 Julai, 2024 wakati ujumbe kutoka Mahakama na Benki ya Dunia walipofanya ziara ya ukaguzi wa Mradi huo.
 
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (mbele) pamoja na sehemu ya Wajumbe wengine wakiwa katika kikao pamoja na Mkandarasi wa Mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe wakati walipofanya ziara ya kukagua Mradi huo jana tarehe 25 Julai, 2024.
 Mtaalamu wa Manunuzi kutoka Benki ya Dunia,  Bw. Fredrick Nkya akichangia jambo wakati wa kikao kati ya Mkandarasi wa Mradi wa ujenzi wa IJC Njombe na ujumbe kutoka Mahakama ya Tanzania na Benki ya Dunia.
Wajumbe wakifuatilia kinachojiri katika kikao.
 
Wajumbe kutoka Mahakama ya Tanzania, Benki ya Dunia pamoja na Mkandarasi wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki 'IJC' Njombe  wakijadili juu ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la 'IJC' Njombe.
Muonekano wa mbele wa jengo jipya la 'IJC' Njombe linaloendelea kujengwa likiwa limefikia hatua ya ghorofa ya kwanza.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



Alhamisi, 25 Julai 2024

USHIRIKIANO WA TUME NA CHUO CHA MAHAKAMA UTAIMARISHA UTOAJI HAKI

 ·       Tume kuendelea kusimamia suala la kuwajengea uwezo Watumishi wa  Mahakama

Na Lydia Churi-Tume ya Utumishi wa Mahakama, Lushoto-Tanga

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Mary Caroline Levira amesema Ushirikiano Kati ya Tume ya Utumishi wa Mahakama na chuo hicho utaiwezesha Mahakama ya Tanzania kutekeleza ipasavyo jukumu lake la kikatiba ka kutoa haki kwa wananchi.

Akizungumza na Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama waliofanya ziara kwenye chuo hicho jana, Jaji Levira alisema ushirikiano kati ya Tume na Chuo cha Uongozi wa Mahakama utaleta matokeo chanya katika kuimarisha utendaji kazi wa Mahakama kwa kuwa chuo hicho hutoa mafunzo ya kimahakama kwa watumishi wa Mahakama ya Tanzania.

”Tunawashukuru kwa kufika chuoni hapa na kuzungumza nasi, mazungumzo haya ni moja ya mikakati ya kusaidia kuendeleza malengo ya Chuo hiki, Tume pamoja na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla” , alisema.

 Kwa upande wake, Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Ajira) Bi. Enziel Mtei amesema Tume itaendelea kusimamia suala la kuwajengea uwezo Maafisa Mahakama pamoja na watumishi wasio Maafisa Mahakama ili kuiwezesha Mahakama kutimiza lengo lake la kutoa huduma bora za haki.

”Tume ya Utumishi wa Mahakama ndiyo mamlaka ya ajira na uteuzi wa Viongozi mbalimbali wa Mahakama kwa mujibu wa sheria, ukiacha wale ambao mamlaka yao ya uteuzi ni Mhe. Rais,”alisema.

Alisema ili Mahakama iweze kutoa huduma bora na kwa ufanisi, inahitaji rasilimali bora na hili litawezekana kwa kuwa na watumishi wenye weledi wa kutosha, hivyo kuiwezesha Mahakama kutimiza matarajio yake ya kutoa huduma za haki kwa wakati na kwa ubora.

Akielezea ziara ya Makamishna chuoni hapo, Bi. Mtei alisema ni utaratibu wa Tume kuwa wanapoteuliwa Makamishna wapya hutembelea chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kwa lengo la kujifunza namna chuo kinavyotekeleza jukumu la kuwajengea uwezo watumishi wa Mahakama ya Tanzania.

Alisema mikakati inayotekelezwa na Tume ni kusimamia Mahakama na kuhakikisha kwamba watumishi wapya wanapoajiriwa wanapatiwa mafunzo elekezi kwa lengo la kuelewa Utumishi na misingi yake ikiwemo sera, kanuni na taratibu mbalimbali za utendaji kazi Serikalini, kufahamu majukumu yao na kuzingatia maadili, nidhamu, uadilifu na ustahimilifu.

Bi. Mtei alisema kuwa ni matarajio ya Tume kuwa mafunzo ya aina hiyo yanapofanyika, chuo kitakuwa na utaratibu wa kufanya tathmini kwa kila kundi na mshiriki moja moja, kuainisha mapungufu au ubora katika eneo lolote na kuwasilisha Taarifa hiyo Tume ili kuiwezesha kuboresha namna inavyotekeleza majukumu yake hasa kwenye eneo la ajira, upandishaji vyeo pamoja na uteuzi.

Katika ziara hiyo, Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama walipata nafasi ya kujifunza utendaji kazi wa chuo hicho kupitia mada iliyowasilishwa na Mkuu wa Chuo hicho, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul Kihwelo. Mada nyingine iliyotolewa ilihusu Muundo wa Mahakama ya Tanzania ambayo iliwasilishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Tanga Mhe. Katarina Revokati Mteule.

Aidha, Makamishna walipata wasaa wa kuchangia mada hizo ambapo kwa upande wake, Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika alikishauri chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kuongeza msukumo wa kufundisha zaidi kwenye eneo la uandishi wa hukumu ili kuimarisha utendaji kazi wa Mahakama ya Tanzania.

Naye Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakili Bahame Tom Nyanduga alikishauri chuo hicho kuimarisha ufundishaji kwenye somo la Haki za Binadamu kwa lengo la kuwajenga na kuwaandaa Mahakimu na Waendesha Mashtaka kuzingatia haki za binadamu wanapotekeleza majukumu yao ya utoaji wa haki.

Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo cha kikatiba kilichopewa jukumu la kusimamia uendeshaji wa Mahakama ya Tanzania. Moja ya jukumu lake ni kusimamia Maadili ya Maafisa Mahakama ili kuhakikisha Mhimili wa Mahakama unatekeleza jukumu lake la msingi na la kikatiba la kutoa haki kwa wananchi. 

Jukumu la kusimamia Maadili ya Maafisa Mahakama, pamoja na majukumu mengine ya Tume, yameainishwa katika Ibara ya 113 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kifungu cha 29 cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Sura ya 237. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Mary Caroline Levira akizungumza na Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wakati wa ziara yao kwenye Chuo hicho jana. 
Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Ajira) Bi. Enziel Mtei nakizungumza wakati wa ziara hiyo.
Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wakifuatilia jambo wakati wa ziara yao katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto jana. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Mary Caroline Levira akiongoza Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kutembelea majengo ya Chuo hicho.  

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto Mhe. Dkt. Paul Kihwelo (kulia) akiwa na Viongozi wengine wa chuo hicho wakati wa ziara ya Makamishna wa Tume kwenye Chuo hicho jana. Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akielezea utendaji kazi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tanga Mhe. Katarina Revokati Mteule akielezea Muundo wa Mahakama ya Tanzania kwa Makamishna wa Tume wakati wa ziara yao kwenye Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto jana.




MAHAKAMA YAANZISHA MFUMO MPYA WA UTOAJI HUDUMA KWA WATEJA

Walenga kuongeza ufanisi wa kuhudumia wateja

Una uwezo wa kuhudumia watu wengi kwa mkupuo

Na Jeremia Lubango, Mahakama-Dodoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya ameipongeza Idara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ya Mahakama kwa kuja na Mfumo mpya wa Utoaji Huduma kwa Wateja (Call Centre Application System) ambao unaenda kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama.

Akizungumza leo tarehe 25 Julai, 2024 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati akifunga mafunzo elekezi kwa Maafisa wa Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha Mahakama juu ya namna ya kuutumia mfumo huo, Mhe. Nkya amesema Mfumo huo utaweza kurekodi na kuhudumia wateja wengi zaidi kwa wakati mmoja.

“Dunia ya sasa inaongozwa na TEHAMA na dhamira ya Mahakama ni kuhakikisha shughuli zote zinafanyika kwa kutumia TEHAMA, hivyo nipongeze ubunifu huu ambao utarahisisha utoaji huduma kwa wananchi,” amesema Msajili Mkuu.

Kadhalika, amezipongeza pia Kurugenzi ya Ukaguzi, Huduma za Mahakama na Maadili pamoja na Kurugenzi ya Mipango na Ufuatiliaji kwa jinsi wanavyosimamia utendaji kazi mzuri wa Kituo cha Huduma kwa Mteja ambao umesaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha huduma za Mahakama.

Amesema, Mfumo huo ambao una uwezo wa kuhudumia watu wengi zaidi ndani ya dakika moja, utatoa ripoti ya siku, wiki, mwezi na mwaka na kuongeza kuwa, Mfumo huo unapatikana kwa kupiga namba ya bure ya 0800 750 247.

Ameongeza kwamba, anafahamu ipo mirejesho inayowahusu watumishi wenye vyeo mbalimbali kwenye Mhimili wa Mahakama ambapo amewasihi Maafisa wa Kituo hicho kufuatilia mirejesho hiyo kwa heshima na kuzingatia utu wa watumishi wengine bila hofu wala upendeleo lakini pia kuzingatia maadili, Katiba, sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali ya Mahakama.

Ametoa rai pia kwa watoa huduma kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuimarisha huduma. Amesisitiza hilo kwa kusema, “kushirikiana kutatua changamoto zinazowakabili kutasaidia kuongeza ufanisi mzuri wa ufanyaji kazi na kutachangia kuleta huduma bora na kuimarisha imani kwa wananchi na Mahakama kwa ujumla.”

Akizungumzia umuhimu wa Kituo hicho, Msajili Mkuu ameeleza kwamba, “Kituo cha Huduma kwa Mteja kimehusika katika ongezeko la kiwango cha kuridhika kwa watumiaji wa huduma za Mahakama kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na REPOA kutoka asilimia 78 kwa mwaka 2019 hadi asilimia 88 kwa mwaka 2023 kwa kutatua baadhi ya changamoto za wateja wa Mahakama na hivyo kupunguza malalamiko.”

Naye Mkurugenzi wa Ukaguzi, Huduma za Mahakama na Maadili wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Maira Kasonde amesema kwamba, Mfumo huo utaunganisha kurasa za Mahakama za mitandao ya kijamii ambazo ni ‘facebook’ (Mahakama ya Tanzania), ‘twitter’ (judiciarytz) na ‘instagram’ (judiciarytz) ambapo utasaidia kusogeza huduma karibu na wananchi.

Mafunzo hayo ya siku nne yaliyoongozwa na Afisa na Msimamizi wa Mifumo ya TEHAMA, Mahakama ya Tanzania, Bw. Witness Ndenza pamoja na Bw. Mussa Ulekwe kutoka kampuni ya Utengenezaji wa Mifumo (MFI).

Mafunzo haya yalihudhuriwa na Viongozi kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi, Huduma za Mahakama na Maadili pamoja na Watumishi kutoka Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama.

Afisa na Msimamizi wa Mifumo ya TEHAMA, Mahakama ya Tanzania, Bw. Witness Ndenza (kushoto) akitoa maelezo kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa tatu kushoto) leo tarehe 25 Julai, 2024 wakati alipotembelea chumba maalum cha Maafisa wanatoa huduma kwa wateja kilichopo ndani ya jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kulia kwa Msajili Mkuu ni Mkurugenzi wa Ukaguzi, Huduma za Mahakama na Maadili wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Maira Kasonde pamoja na Watumishi wengine wa Kituo hicho.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akizungumza wakati wa kufunga mafunzo elekezi mfumo mpya wa ushughulikiaji wa mirejesho kwa wateja yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 25 Julai, 2024.

Afisa na Msimamizi wa Mifumo ya TEHAMA, Mahakama ya Tanzania, Bw. Witness Ndenza (aliyesimama mbele) akitoa maelezo wakati wa ufungaji wa mafunzo elekezi ya mfumo mpya wa ushughulikiaji wa mirejesho yaliyofanyika  katika Chumba cha Mifumo ya Kutolea Taarifa Muhimu za Mahakama (Judiciary Situation Room).

Mkurugenzi wa Ukaguzi, Huduma za Mahakama na Maadili wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Maira Kasonde (aliyesimama mbele) akizungumza jambo wakati wa hafla ya kufunga mafunzo elekezi kwa Maafisa wa Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha Mahakama juu ya namna ya kuutumia Mfumo mpya wa Utoaji Huduma kwa Wateja (Call Centre Application System).

Sehemu ya Maafisa kutoka Ofisi ya Huduma kwa Mteja ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika hafla fupi ya ufungaji wa mafunzo elekezi juu ya mfumo mpya wa ushughulikiaji wa mirejesho iliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 25 Julai, 2024. 


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa sita kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi na Maafisa wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya kufunga mafunzo elekezi ya namna ya kuutumia mfumo mpya wa ushughulikiaji wa mirejesho yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 25 Julai, 2024.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)









KITUO CHA MASUALA YA FAMILIA TEMEKE CHAKUTANA NA WADAU

Waja na Mpango wa Kumaliza Mashauri ya Mlundikano.

Kituo kimedhamiria kutoa elimu kwa Wadau walio karibu na wananchi.

Changamoto za mashauri ya Mirathi zabainishwa na kuwekewa mikakati

Na Naomi Kitonka, Kituo Jumuishi cha Masuala Ya Ndoa na Familia- Temeke

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Ndoa na Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa jana tarehe 24 Julai, 2024 aliwaongoza Mahakimu na wadau mbalimbali wa Mahakama katika kikao cha Kamati ya kusukuma Mashauri ya Madai (Bench Bar Meeting) kuwawezesha kupitia mashauri ya mlundikano kwa pamoja na kuona namna bora ya usikilizwaji wa haraka pamoja na kuweka mikakati ya pamoja ya kuyamaliza mashauri hayo.

Akizungumza wakati akifungua kikao hicho kilichofanyikia katika ukumbi wa mikutano wa Kituo hicho, Mhe. Mnyukwa alizungumzia juu ya umuhimu wa kikao hicho kwa wajumbe ambao ni wadau wa Mahakama kutoka katika Taasisi mbalimbali na mchango wao mkubwa katika kusukuma mashauri ya mlundikano katika Mahakama.

“Tunawashukuru wadau wetu kwa kuitikia wito wetu katika kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa kusukuma Mashauri ya madai na kama Mahakama ya Kituo Jumuishi Temeke tunatambua mchango wenu mkubwa katika upatikanaji wa haki kwa wananchi pamoja na nafasi kubwa ya kusaidia kuwaelimisha wananchi na kuongeza uelewa wao katika zoezi zima la upatikanaji wa haki kwa kujua mambo muhimu hasa katika mashauri ya madai,” alisema Jaji Mnyukwa.

Pamoja na hayo wadau walipata wasilisho kutoka kwa Katibu wa kikao ambaye ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Frank Moshi ambaye alitoa takwimu za hali ya mashauri kutoka Mahakama Kuu, Mahakama ya Watoto, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo paoja na sababu zilizochangia kutokumalizika kwa wakati katika Mahakama zote katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka.

Kadhalika, Wadau nao walipata nafasi ya kutoa maoni yao baada ya wasilisho, walieleza kwamba, changamoto kubwa ni kuwa na muda mrefu wa kufuatilia mashauri ya mirathi pamoja na kuchelewa kufunga mirathi kwa wakati.

Kuhusu changamoto hiyo,  Jaji Mfawidhi alijibu kwa kusema, “changamoto hiyo inatokana na wananchi wengi kutokuwa na elimu ya kutosha kuhusu taratibu sahihi za kufuata wanaposhughulikia masuala ya mirathi, lakini pia ukosefu wa elimu kwa wadau inachangia wao kutokutoa taarifa muhimu na msaada wa kutosha hivyo kuchangia ukwamishaji wa zoezi la kusukuma mashauri na upatikanaji wa haki kwa wakati.”

Aliongeza kuwa, lengo la Kituo hicho ni kuhakikisha mashauri yote katika kila ngazi ya Mahakama yanamalizika kwa muda husika na kutoa huduma bora kwa wananchi na wadau wengine.

Alisema pamoja na kuwa na maendeleo ya Sayansi na Teknolojia yaliyoibua changamoto mpya, Mahakama kama Taasisi imekuwa makini katika kuzipatia ufumbuzi na kutoathiri kasi ya uondoshwaji wa mashauri na changamoto zimetumika kama fursa ya kuonesha weledi katika utendaji na kuhakikisha huduma za uhakika zinapatikana kwa wananchi kwa wakati.

Vilevile, Jaji Mfawidhi huyo alieleza kuwa, kama Mahakama ya Kituo Jumuishi Temeke imekusudia kuwa na hatua na mpango wa vikao vya usikilizwaji  mashauri vya mara kwa mara.

Aidha, kikao hicho kilitoka na maazimio ili kuhakikisha wateja wanafutwa machozi kama kauli mbiu ya Kituo hicho inavyosema ‘kutoa haki kwa wanachi kwa muda unaotakiwa na kuongeza ufanisi wa kituo katika ngazi zote za utendaji’.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Mtendaji wa Kituo, Bw. Samson Mashalla, Naibu Wasajili, Mhe. Frank Moshi na Mhe. Evodia Kyaruzi, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya-Temeke, Mhe. John Msafiri, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo-Temeke, Mhe. Aloyce Mwageni akiambatana na Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Watoto, Mhe. Orupa Solomon Mtae.

Pamoja na hao, Wadau waliohudhuria kikao hicho ni kutoka PSSSF, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hati, Maafisa Ustawi wa Jamii, Mwakilishi kutoka Chama Cha Mawakili Tanganyika (TLS) pamoja na Watoa Msaada wa Kisheria  (WiLDAF, WLAC) waliopo katika Kituo Jumuishi Temeke.

Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa (kushoto) akiwa kwenye kikao  cha Kamati ya kusukuma Mashauri ya Madai (Bench Bar Meeting)  kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo hicho jana tarehe 24 Julai, 2024. Kulia ni Jaji wa Mahakama hiyo, Mhe. Sharmillah Sarwatt. 

Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai ambao ni wadau wa Mahakama kutoka Taasisi mbalimbali wakisikiliza kwa makini kinachojiri katika kikao hicho kilichofanyika jana tarehe 24 Julai, 2024 IJC Temeke.

Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai wakimsikiliza kwa makini Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa (hayupo katika picha). Kikao hicho kilifanyika jana tarehe 24 Julai, 2024. 

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya-Temeke, Mhe. John Msafiri (aliyesimama) akichangia mada katika katika kikao cha Kamati ya Kusukuma Mashauri ya Madai kilichofanyika jana tarehe 24 Julai 2024 IJC Temeke.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



Jumanne, 23 Julai 2024

MAHAKAMA NJOMBE YAVUKA MWAKA BILA MASHAURI MLUNDIKANAO

Na Innocent Kansha-Mahakama, Njombe

Mahakama mkoani Njombe ilivuka mwaka 2023 ikiwa na mashauri sifuri ya mlundikano na kufikia Disemba 2023, mashauri yaliyobaki yalikuwa 522 na hivyo kufikia lengo la kuondosha mashauri ya muda mrefu mahakamani.

Akiongea na Mkuu wa Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano cha Mahakama ya Tanzania leo tarehe 23 Julai, 2024 Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe Bw. Richard Mbambe amesema, Mahakama ya Hakimu Mkazi ilibakiwa na mashauri 19 Disemba, 2023, huku Mahakama za Wilaya zilibakiwa na mashauri 207 na Mahakama za Mwanzo mashauri 296.

“Mahauri yaliyofunguliwa kuanzia Januari 2024 hadi Juni 2024 Mahakama ya Hakimu Mkazi ilipokea mashauri 27, Mahakama za Wilaya mashauri 201 na Mahakama za Mwanzo mashauri 1132 takimu hizo zinafanya jumla ya mashauri yamefikia takribani 1360,” amesema Mtendaji Bw. Mbambe.

Bw. Mbambe amesema, mashauri yaliyosikilizwa kunzia Januari, 2024 hadi Juni, 2024 Mahakama ya Hakimu Mkazi imesikiliza mashauri 30, wakati Mahakama za Wilaya zimesikiliza mashauri 348 na Mahakama za Mwanzo zimesikiliza mashauri 900 na kufanya jumla ya mashauri 1278.

Mashauri yaliyobakia kufikia Juni, 2024 kwa upande wa Mahakama ya Hakimu Mkazi ni mashauri 16, Mahakama za Wilaya ni mashauri 60 na Mahakama za Mwanzo ni mashauri 528 na kufanya jumla ya mashauri yaliyobaki kufikia 604, amesema Mtendaji huyo.

Kwa upande wa mashauri yaliyoendeshwa kwa njia ya Mahakama Mtandao (video Conference) ni mashauri 12 kunzia Januari hadi Juni, 2024 mashauri yaliyosikilizwa Mahakama ya Hakimu Njombe ambayo hayakusajili wa Njombe ni mashauri manne (4) kutoka Mtwara shauri moja (1), Kigoma moja (1) na Iringa mashauri mawili (2) hii inatokana na uimarishaji wa matumizi ya mifumo ya kuendeshea mashauri kwa njia ya mtandao.

Bw. Mbambe amesema, Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe hupokea wastani wa wateja 668 kwa mwezi, ikiwa ni sawa na wastani wa wateja 167 kwa wiki wanaofika mahakamani hapo kupata huduma mbalimbali za utoaji haki. Vilevile malalamiko yaliyowasilishwa na wateja kwa mwaka 2023 yalikuwa saba (7) na Mwaka 2024 kuanzia Januari hadi Juni 2024 Mahakama imepokea malalamiko mawili (2) na tayari uongozi umeshayashughulikiwa.

Akielezea maendeleo ya miradi ya ujenzi inayotekelezwa mkoani Njombe na Mahakama ya Tanzania, Bw. Mbambe amesema Mahakama kwa sasa inatekeleza miradi miradi mitatu (3) ya ujenzi, ikiwemo ujenzi wa  Mahakama Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Njombe ambao ujenzi wake umefikia asilimia 21, ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe na Mahakama ya Mwanzo Manda.

Ujenzi wa Kituo Jumuishi Njombe ulianza tarehe 12 Disemba, 2023 na unatarajiwa kukamilika tarehe 11 September, 2024. Mradi huu unatarajiwa kugharimu Tshs. 7,647,179,528.62/= (VAT). Mkandarasi anayejenga mradi huu ni Shandon Hi – Speed Dejian Group chini ya usimamiziwa mkandarasi Mshauri (Consultant) Crystal Consultant.

Aidha, mradi upo katika hatua ya ukamilishaji wa sakafu ya ghorofa ya kwanza (first floor slab concrete) hivyo kufanya asilimia ya utekelezaji wa mradi kuwa asilimia 21.

Mtendaji huyo ameongeza kuwa, mradi huo ukikamilika utasaidia kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi badala ya kusafiri kufuata huduma za Mahakama Kuu, Kanda ya Iringa kama ilivyo sasa, pia itapunguza gharama za kuleta Waheshimiwa Majaji toka Mahakama Kuu vilevile itapunguza mlundikano wa mshauri, itawasaidia wananchi kutumia muda wao katika uzalishaji mali na kujiongezea kipato na kurahisiha upatikanaji wa haki kwa wakati.

Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 Mkoa wa Njombe una idadi ya wakazi wapatao 889,946 ambao watanufaika na ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kitakapo kamilika na kuanza kutumika kutoa huduma za haki mkoani Njombe.

Kwa mujibu wa takwimu Mkoa wa Njombe una Mahakama ya Hakimu Mkazi 1, Mahakama za Wilaya nne (4) na Mahakama za Mwanzo 26 kama inavyobainishwa hapo chini.

Wilaya ya Njombe ina Mahakama moja ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo saba (7), ambazo ni Njombe mjini, Makambako, Lupembe, Matola, Igominyi, Mtwango na Uwemba/Mahenye.

Wilaya ya Ludewa inayo Mahakama ya Wilaya moja na Mahakama za Mwanzo saba (7), ambazo ni Ludewa mjini, Mlangali, Mawengi, Lugarawa, Mavanga na Manda/Masasi na Luilo.

Wilaya ya Makete ina Mahakama ya Wilaya moja ambayo mashauri yake hufanyika katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Makete mjini. Aidha, kuna Mahakama za Mwanzo nane (8) ambazo ni Makete mjini, Bulongwa, Matamba, Lupalilo, Lupila, Ukwama, Mfumbi na Ipelele.

Wilaya ya Wanging’ombe ina Mahakama ya Wilaya moja, aidha Wilaya ya Wanging’ombe inazo Mahakama nne (4) za Mwanzo ambazo ni Wanging’ombe, Mdandu, Kipengere na Imalinyi.











 

MAHAKAMA KANDA YA KIGOMA YAPOKEA JAJI MPYA

Ni Jaji Projestus Kahyoza

Aonesha furaha ya kupangiwa Kituo hicho

Aidan Robert, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile leo tarehe 23 Julai, 2024 amewaongoza Watumishi wa Kanda hiyo katika viwanja vya Mahakama Kuu  kumpokea Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza, Jaji wa Mahakama Kuu ambaye amepangiwa kazi katika Kituo hicho.

Akizungumza mara baada ya kumpokea Jaji Kahyoza, Mhe. Rwizile amemueleza kuwa, Mahakama Kanda ya Kigoma ina timu nzuri ya kazi na vilevile ni sehemu nzuri ya kufanya kazi kwa kuwa mazingira na hali ya hewa ni nzuri.

Kwa upande wake Mhe. Kahyoza ameushukuru uongozi wa Mahakama Kanda ya Kigoma ukiongozwa na Jaji Mfawidhi kwa mapokezi mazuri waliyoyafanya katika kituo chake kipya cha kazi na kuongeza kwamba, Mkoa wa Kigoma ilikuwa ni ndoto yake ya siku nyingi kufanyia kazi.  

“Wametimiza ndoto yangu ya siku nyingi ya kunipangia Kituo hiki cha Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma,” amesema Jaji Kahyoza.

Mhe. Kahyoza ni miongoni mwa Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania walioteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

Ujio wa Jaji huyo utaongeza nguvu katika usikilizwaji wa mashauri katika Kanda hiyo, hata hivyo Kanda hiyo itakuwa na jumla ya Majaji watatu ambao wamejipanga kuhakikisha mashauri yanayosajiliwa yanasikilizwa na kuamuliwa kwa haraka ili kuendana Dira ya Mahakama ya utoaji wa haki sawa kwa wote na kwa wakati.

Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) akisalimiana na kumkaribisha Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma mara baada ya kuwasili leo tarehe 23 Julai, 2024 kwa lengo la kuripoti katika Kituo chake kipya cha kazi.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza (kushoto) akipokea zawadi ya ua kama alama ya ukaribisho katika Kanda hiyo. Anayemkabidhi ua ni Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Eva Mushi.

Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma akizungumza jambo mara baada kusaini kitabu cha wageni  katika ofisi ya Jaji Mfawidhi Kanda ya Kigoma aliporipoti leo tarehe 23 Julai, 2024. 

Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma,  Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) akisikiliza kwa makini jambo alilokuwa akizungumza Mhe. Kahyoza (katikati). Kushoto ni Jaji wa Kanda hiyo, Mhe. John Francis Nkwabi akifuatilia mazungumzo katika ofisi ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kanda ya Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma mara baada ya kumpokea Jaji mpya wa Mahakama Kuu, Mhe. Projestus Rweyongeza Kahyoza (wa pili kulia) aliyepangiwa kufanya kazi katika Kituo hicho. Wa pili kushoto Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe.  John Francis Nkwabi, wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay na wa kwanza kushoto ni  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Gadiel Mariki.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)