·Mahakama Sports Mpira wa Miguu yaifumua Ras Kigoma 8:0
Na
Faustine Kapama -Mahakama, Iringa
Lilikuwa suala la muda tu
kwa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu kuyaanza Mashindano
ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika
mkoani hapa kwa kishindo kufuatia mchezo wake wa kwanza kukipiga kipute na
Kilimo kuahirishwa kwa sababu ya msiba.
Leo tarehe 30 Septemba,
2023 imeingia katika Uwanja wa Samora kuvaana na timu ya Ras Kigoma na kuzabua
mabao nane kwa nunge kwenye mchezo uliotawaliwa na ufundi wa kimpira uliokuwa
unaonyeshwa na vijana wa Mhimili wa utoaji haki.
Mchezo huo uliochezwa
majira ya alasili ulianza kwa kasi huku timu zote zikishambuliana kwa zamu,
huku Mahakama Sports ikilisakama lango la wapinzani mara kwa mara. Katika
mchezo huo, mshambuliaji hatari wa Mahakama Sports Martin Mpanduzi alifanikiwa
kuondoka na mpira baada ya kupachika mabao matatu.
Ilikuwa katika dakika ya
12 ambayo Mpanduzi alifungulia mlango wa magori kwa timu yake kwa kupachika bao
safi kutokana na pasi murua kutoka kwa kiungo punda Selemani Magawa.
Katika dakika ya 16,
Magawa alitikisa nyavu za Ras Kigoma kwa kupachika bao safi baada ya shuti kali
lililomshinda mlinda mlango. Mvua ya magoli iliendelea kunyesha langoni mwa Ras
Kigoma baada ya Bundi kuzengea zengea eneo hilo.
Kwenye dakika ya 22 ya
mchezo, Mpanduzi tena alipachika bao lingine la tatu baada ya kupokea pasi safi
kutoka kwa Magawa kabla ya kutikisa nyavu kwa mara nyingine katika dakika ya 31.
Magawa alipachika bao
lingine katika dakika ya 35, huku Nasoro Mwampamba akihitimisha karamu ya magori
katika kipindi cha kwanza baada ya kuachia shuti kali lililomshinda mlinda
mlango wa Ras Kigoma.
Katika kipindi cha pili,
timu ya Mahakama Sports ilianza kucheza pasi fupi fupi na kuzidisha
mashambulizi, hivyo kuendelea kulishambulia lango la wapinzani na kufanikiwa
kwa muda wote kuwachezea Ras Kigoma nusu uwanja.
Katika dakika ya 50, Abdi
Sasamalo alipachika mpira kwenye nyavu na kuiandikia timu yake bao la saba
kabla ya dakika mbili baadaye, Gabriel Mwita akahitimisha karamu ya magori baada
ya kwenda kwenye kamba, hivyo kuiwezesha timu yake kuondoka na ushindi mnono.
Wakati wa mchezo huo,
mwamuzi aliwazawadia wachezaji wawili wa Ras Kigoma kadi za njano baada ya
kuwachezea rafu wachezaji wawili wa Mahakama Sports.
Wachezaji wa Mahakama
Sports waliosakata kambumbu ni Fahamu Kibona, Nasoro Mwampamba, Nkuruma Katagira,
Emmanuel Mwamole, Akida Mzee, Kelvin Muhagama, Frank Obadia, Gabriel Mwita,
Martin Mpanduzi na Seleman Magawa.
Wengine ni Abdi Sasamalo,
Mbura Minja, Iman Zumbwe, Gisbert Chentro, Rashid Hamis, Devis Munubi, Seif
Shamte na Ramadhani Seif. Benchi la ufundi liliongozwa na Kocha Mkuu Spear
Mbwembe na Kocha Msaidizi Said Albea.
Alikuwepo pia Timu Meneja
Shaibu Kanyachole, Meneja wa Vifaa Eliya Ngule na Daktari Janeth Mapunda.
Akizungumza baada ya
mchezo kumalizika, Mwalimu wa timu Spear Mbwembwe amesema wachezaji wake
wamecheza vizuri, ingawa hawakufuata mfumo wa pasi fupi fupi, hasa katika
kipindi cha kwanza.
Amesema baada ya kuanza kipindi
cha pili, vijana wake walirudi kwenye mfumo na kuanza kuonyesha kandanda safi
na kucheza mpira wa kwenye vitabu, hivyo kuwafaya timu pinzani kupoteana.
“Nadhani umejionea
mwenyewe katika kipindi cha pili. Kama muda wote wangecheza hivyo, hawa jamaa (Ras
Kigoma) walikuwa wanakula zaidi ya goli 10. Hata hivyo, niwapongeze vijana wangu
kwa kujituma na kupata matokeo haya mazuri,” amesema.
Naye Mwenyekiti wa
Mahakama Sports Wilson Dede hakuwa nyuma kumwaga sifa kwa wachezaji kwa kazi
nzuri waliyokuwa wanaifanya uwanjani. Amesema kuwa ushindi huo ni mwanzo mzuri
kwa timu yake na anaamini kila timu itakayothubutu kukanyaga uwanjani itachezea
kichapo.
“Hizi ni mvua za rasharasha,
mazika bado hayajaanza. Tuna timu imara sana mwaka huu, lengo letu kila timu
itakayojaribu kuja uwanjani itapata dozi ya kutosha, kuliko hata hii ambayo Ras
Kigoma wameipata. Tunataka wapinzani wetu watuelewe, kwa hili hatutanii, tuna
maanisha, wasije wakasema hatukuwatahadhalisha,” amesema.
Kwa
mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, timu ya Mahakama Mpira
wa Miguu imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS
Kigoma na Kilimo katika kutafuta nafasi ya kutinga 16 bora.
Mahakama Sports inashiriki
katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira
wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.
Katika mashindano ya
SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa
makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.
Michezo ambayo Mahakama
Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa
kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa
kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume
walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.