Alhamisi, 25 Aprili 2024

JAJI KIONGOZI: TEHAMA IMEPUNGUZA MUDA WA SHAURI KUKAA MAHAKAMANI NA MLUNDIKANO

 Na Magreth Kinabo-Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani amesema matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika mchakato wa usikilizaji wa mashauri, yamesaidia kupunguza muda wa shauri kuwa mahakamani na mlundikano wa mashauri, hivyo ni hatua ambayo Mahakama inapaswa kujivunia

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 25 Aprili, 2024 na Mhe. Siyani wakati akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa kikao cha tatu cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Masjala Kuu katika ukumbi wa hoteli ya Alexander mjini Iringa.

Mwaka 2023, kwa mfano; Mahakama ilikuwa na mlundikano wa asilimia nne (4), hata hivyo kufikia mwezi Machi, 2024 mlundikano wa mashauri umepungua hadi kufikia asilimia tatu (3). TEHAMA pia imewezesha muda wa kumaliza mashauri unaopimwa kila mwisho wa mwaka kupungua. 

Kwa mfano mwaka 2023 mahakama ilitumia wastani wa siku themanini na nne (84) kukamilisha usikilizwaji na utoaji wa maamuzi kwa shauri, ukilinganisha na siku 95 kwa mwaka 2022. Haya ni mafanikio makubwa tunayopaswa kujivunia,” amesema Jaji Kiongozi

Aidha Mhe. Jaji Siyani kupitia baraza hiloamesisitiza juu ya umuhimu wa watumishi wote kukumbuka malengo tuliyojiwekea kama taasisi katika kutoa huduma kwa wananchi sambamba na kufahamu mipango ya kufanikisha malengo hayo ili kuwezesha kila mmoja kushiriki kikamilifu kutekeleza mipango hiyo. Malengo makuu yameainishwa katika mpango Mkakati wa Mahakama tunaoutekeleza sasa ambayo ni kupunguza muda wa mashauri kuwa Mahakamani na kuongeza imani kwa wananchi kwa kutoa huduma bora kwa wakati. 

Kwa hiyo kila mmoja wetu anao wajibu wa kuhakikisha malengo hayo yanatimia katika viwango stahiki. Ni vyema watumishi wa mahakama wakafahamu vigezo vinavyotumika kupima ufanisi wetu wa kazi  ili kila mmoja aweze kujua jinsi ya kuchangia katika vipimo hivyo na hii itatutoa katika utendaji kazi kwa mazoea na hivyo kutekeleza majukumu yetu kimkakati. Hili ni muhimu kwa sababu, jukumu la kuhakikisha lengo la kutoa haki sawa kwa wote na kwa wakati linafikiwa, ni la kila mmoja wetu,amesisitiza.

Akizungumzia kuhusu Baraza hilo la wafanyakazi, amesema ni fursa ya kisheria kwa watumishi kujadiliana na menejimenti ya taasisi yao juu ya masuala mbalimbali ya msingi yanayohusu tija na ufanisi kwa upande mmoja; na maslahi yao kama watumishi kwa upande mwingine. Kwa hiyo; mabaraza haya ni chombo cha ya kusikiliza changamoto za wafanyakazi lakini ni mashine ya kuchakata changamoto hizo kwa lengo la kuimarisha mazingira ya kazi kwa faida ya pande zote mbili. 

Mhe. Jaji Siyani amewakumbusha umuhimu wa kufanya kazi kwa uadilifu na uweledi. Huku akisema mambo haya mawili ni kama ibada, hatuwezi kuacha kukumbushana kila tunapokutana

Nitumie fursa hii kuwapongeza watumishi wote wa mahakama kote nchini wanaoendelea kuchapa kazi kwa juhudi, uadilifu, akili na weledi licha ya changamoto zilizopo. Ninatambua yapo matukio machache yanayoashiria ukosefu wa maadili. Niwahakikishie uongozi wa Mahakama utaendelea kuchukua hatua stahiki dhidi ya vitendo hivyo ili kulinda hadhi ya mhimili wetu na kujenga imani ya wananchi kwa taasisi hii,” amesema

Aliwataka watumishi hao kujenga umoja, amani na mshikamano miongoni mwaoKwa kuwa mambo haya matatu ni muhimu na ya msingi kwa mendeleo ya taasisi yoyote.Hivyo ni lazima sote tuepuke majungu na mambo yanayoweza kuharibu mahusiano yetu. Badala ya watu kupiga ubuyu kazini, ni bora wapige kazi. 

Jaji Kiongozi huyo amefafanua kuwa mahusiano kazini yanaweza kujengwa kwa njia nyingi. Moja wapo ni ushiriki wa michezo na uanzishwaji wa vikundi vya mazoezi, hivyo  kupitia baraza hilaliwaomba viongozi wa mahakama kote nchini, kuanzisha utaratibu wa mazoezi kazini pamoja na michezo katika muda ambao hautaathiri majukumu ya kazi.

Amewasihi wajumbe wa baraza hilo kuwa wa kwanza kubadilika kutokana na elimu watakayojifunza, kisha waifikishe wenzao waliobaki vituoni, ili nao iwasaidie kubadilika na hatimaye mabadiliko hayo yaongeze tija katika utekelezaji wa kazi zao.

 Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania,Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akisisitiza jambo wakati akiongea na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu - Masjala Kuu.

  Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) wakifuatilia mjadala wakati wa kikao hicho.

 Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) (juu na picha mbili chini) wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (mwenye miwani aliyekaa katikati)


 

 

 

WATUMISHI WA MAHAKAMA WASISITIZWA KUWA WAADILIFU, WELEDI

Na Lusako Mwang’onda-Mahakama, Iringa

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania wametakiwa kufanya kazi kwa ueledi na uadilifu wa hali ya juu wakiwa katika majukumu yao ya kuwatumikia wananchi. 

Hayo yamesemwa leo tarehe 25 Aprili, 2024 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustafa Mohamed Siyani wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu (Masjala Kuu) kilichofanyika mjini hapa katika Hoteli ya Mount Royal Villa. 

Mhe. Siyani amesema si vyema kwa mtumishi wa Mahakama kuwa na uadilifu unaotiliwa shaka maana hali hiyo hushusha Imani ya wananchi kwa Mahakama.

Jaji Kiongozi, ambaye kikanuni ndiyo Mwenyekiti wa Kikao hicho amesema, “imani ya wananchi ni kubwa sana kwa Mahakama, hivyo uongozi wa Mahakama hautamfumbia macho mtu yeyote ambaye kwa namna yeyote ile atataka kuitia doa Imani waliyonayo wananchi kwa muhimili huu”.

Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi ambacho kikanuni kinakuwa chini ya uenyekiti wa Jaji Kiongozi kimehudhuriwa pia na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) na kwa upande mwingine viongozi na wawakilishi wa Chama cha Wafanyakazi yaani TUGHE nao walikuwepo kuwasilisha hoja za Wafanyakazi.

Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi kimetoka na maazimio mbalimbali, ikiwemo Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kuendelea kupewa kipaumbele katika uendeshaji wa shughuli mbalimbali za kimahakama. 

Naye mwenyekiti wa kikao hicho, amesisitiza kuwa kufanya kazi kwa weledi katika zama hizi ni lazima kuendane na matumizi ya TEHAMA. 


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustafa Mohamed Siyani akisisitiza jambo wakati akiongea na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu - Masjala Kuu.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) wakifuatilia mjadala wakati wa kikao hicho.

Mtendaji wa Mahakama ya Kuu ya Tanzania (MMK), Bw.Leonard Magacha akifuatilia kwa makini mijadala mbalimbali wakati wa kikao hicho cha Baraza.

Makundi mbambali ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) (juu na chini) wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustafa Mohamed Siyani (mwenye miwani aliyekaa katikati).

Makundi mengine ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) (juu na picha mbili chini) wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustafa Mohamed Siyani (mwenye miwani aliyekaa katikati).


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam).


VIONGOZI WA TUGHE MKOANI SINGIDA WAIPONGEZA MAHAKAMA KWA KUWAJALI WATUMISHI

Na Eva Leshange- Mahakama, Singida

Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wameipongeza Mahakama Kanda ya Dodoma kwa kuwajali watumishi ikiwa ni pamoja na kuzingatia maslahi yao.

Pongezi hizo zilitolewa na Viongozi hao waliohudhuria katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dodoma lililofanyika jana tarehe 24 Aprili, 2024 mkoani Singida.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Singida, Dkt. Athuman Bunto alisema, “naipongeza sana Mahakama kwa kuzingatia na kufuata Sheria za utumishi kwani wamezingatia maslahi ya watumishi, sehemu kubwa ya bajeti inawagusa watumishi, mafunzo kutolewa katika Kada zote kwa ajili ya kujengeana uwezo, hiki ni kitu kizuri.” 

Aidha, amelisifu Baraza hilo kuwa, limeendeshwa kwa uwazi watumishi wameonekana kuridhika na limekuwa shirikishi kwani hoja zilizotolewa zilipatiwa majibu na kwa zile ambazo zilikuwa chini ya uwezo wa Kanda wajumbe wamekubaliana kuziwasilisha katika Baraza Kuu.

Kikao hicho kiliongozwa na Mhe Jaji Mfawidhi  Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza hilo.


Katika Baraza hilo, taarifa za bajeti zilisomwa kutoka Mikoa yote Miwili ya Singida na Dodoma na kuona utekelezaji wake hususani kwenye maeneo yanayowahusu watumishi moja kwa moja na pia kuona vipaumbele vya bajeti kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Akihitimisha kikao cha Baraza hilo, Mhe. Dkt. Masabo aliwasisitiza watumishi kuendelea kuwaelekeza na kuwasaidia wateja wanaofika mahakamani kuhusiana na mabadiliko ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano TEHAMA na Mifumo mbalimbali ya Mahakama kwa kuwatia moyo na kuona mabadiliko ya TEHAMA ni msaada kwao. 

Vilevile, aliwataka wajumbe wa Baraza kuzingatia azimio la Morogoro kuhusu utunzaji wa Mazingira kwa kuendelea kutunza mazingira na kupanda miti ya vivuli na matunda.



Viongozi wa Baraza la wafanyakazi Kanda ya Dodoma wakifurahia jambo katika kikao cha Baraza la Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 24 Aprili, 2024, aliyeketi mbele (katikati) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo, Mhe. Dkt. Juliana Masabo. Wa kwanza kushoto ni Katibu wa TUGHE Mkoa wa Singida, Bw.Shedrack anayemfuatia ni Bw. Gerald Gamba, Katibu wa Baraza hilo na walioketi mbele, wa kwanza kushoto ni Katibu Msaidizi wa Baraza, Bi Dorice Busanji akifuatiwa na Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Singida, Dkt. Athumani Bunto.


Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Bw. Yusuph Kasuka akichangia jambo katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kanda ya Dodoma.

Sehemu ya wajumbe waliohudhuria Baraza hilo kutoka Wilaya za Dodoma.

Sehemu ya wajumbe kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma waliohudhuria Baraza hilo mkoani Singida.


Sehemu ya wajumbe kutoka Mahakama za Wilaya Singida waliohudhuria kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)

 

 

Jumatano, 24 Aprili 2024

MAHAKAMA SPORTS YANG’ARA MASHINDANO YA MEI MOSI 2024

Na Seth Kazimoto - Mahakama Kuu Arusha

 

Timu ya Mahakama Sports imeshinda mechi zake zote ilizocheza mpaka sasa katika mashindano ya Mei Mosi yanayoendelea katika viwanja vya Ngarenaro jijini Arusha baina ya Taasisi mbalimbali za Serikali.

 

Mahakama inashiriki mchezo wa kuvuta kamba kwa wanawake na wanaume ambapo Timu ya Wanawake ipo katika kundi D lenye Timu za Wizara ya Mambo ya Ndani, Mahakama, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Arusha Jiji na Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania.

 

Timu ya Kuvuta Kamba Wanaume ipo katika kundi A pamoja na timu za Wizara ya Maliasili, Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Wizara ya Mawasiliano na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

 

Mpaka sasa, Timu ya Kuvuta Kamba Wanawake imecheza mechi tatu na kushinda zote. Katika mechi hizo, Mahakama ilizichapa bila huruma Timu za Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu (TPHPA), Arusha Jiji na Wizara ya Mambo ya Ndani.

 

Vilevile, Timu ya Wanaume mpaka kufikia tarehe 19 Aprili, 2024 ilikuwa tayari imecheza mechi mbili na kushinda zote, katika mechi hizo, Mahakama ilizikung’uta Timu za Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA).

 

Aidha, Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ukiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. JoachimTiganga, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Mariam Mchomba na Mtendaji wa Mahakama Kuu Arusha, Bw. Festo Chonya, ulikutana na Timu ya Mahakama katika ukumbi wa mikutano uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha na kuipongeza timu kwa umahiri wake na kuwatia moyo kuendeleza ushindi kwa mechi zote zilizobaki. 

 

Timu ya Mahakama inanolewa na Kocha mahiri, Bw. Spear Dunia Mbwembwe na imeambatana na Viongozi wa Timu hiyo wakiwemo Naibu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Bw. Fidelis Choka, Afisa Michezo wa Mahakama, Bw. Peter Machalo na Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Donald Tende. 

 

Mashindano hayo baina ya wafanyakazi wa Umma yanalenga kudumisha umoja, mshikamano na kuimarisha afya. Taasisi mbalimbali zinashiriki mashindano hayo ambazo ni pamoja na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Mamlaka ya Ununuzi wa Umma Tanzania (PPRA), Ikulu, Wizara ya Mipango, Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na Wizara ya Maji.

 

Maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Mei Mosi kitaifa mwaka huu yanatarajiwa kufanyika mkoani Arusha huku maandalizi ya awali yakifanyika katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini humo ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha akiwapongeza na kuwatia moyo wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports katika ukumbi wa mikutano uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 19 Aprili, 2024.


 


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Mariam Mchomba akiwa na wachezaji wa Mahakama Sports katika ukumbi wa mikutano (IJC) Arusha tarehe 19 Aprili, 2024 alipokutana nao kwa lengo la kuwapongeza na kuwatia moyo.



Kocha wa Mahakama Sports, Bw. Spear Dunia Mbwembwe.


Timu ya Mahakama Sports ikiwa mazoezini katika viwanja vya Ngarenaro Jijini Arusha wakiongozwa na kocha wa tumu (anayeonekana mbele) Bw. Spear Dunia Mbwembwe.



Wachezaji wa Mahakama Sports wakiwa katika picha ya pamoja.


Timu ya Wanawake ya Kuvuta Kamba ya Mahakama (upande wa kushoto) wakiwavuta kwa ujasiri Timu ya Wizara ya Mambo ya Ndani (upande wa kulia) tarehe 19 Aprili, 2024 katika viwanja vya Ngarenaro Arusha. Timu ya Mahakama iliishinda Timu ya Wizara ya Mambo ya ndani mivuto 2 kwa nunge (0).



Timu ya Mahakama Sports ikishangilia ushindi baada ya kuishinda timu ya Wizara ya Mambo ya ndani mivuto miwili kwa sifuri.

 

(Habari hii imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)

Jumanne, 23 Aprili 2024

JAJI KIHWELO AHIMIZA UWELEDI, UADILIFU KATIKA KUKABILI UHALIFU DHIDI YA WANYAMAPORI

NA MWANDISHI WETU

Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo amesema kuwa uweledi na uadilifu unahitajika zaidi katika kushughulikia mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori ukiwemo ujangili na makosa ya misitu kwa sababu mashauri hayo yana changamoto kubwa katika kuyaendesha, ikizingatiwa kuwa uhalifu huo unavuka mipaka.

Jaji Kihwelo amesema hayo wakati akifungua mafunzo ya kundi la nne yanayohusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori ukiwemo ujangili na makosa yanayohusiana kwa wadau wa haki jinai zaidi ya 60  tarehe 22/04/2024 hapa Chuoni Lushoto.

Mafunzo hayo yatakayochukuwa wiki mbili mpaka tarehe 03/05/2024 yanaendeshwa na IJA kwa ufadhili wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya PAMS Foundation inayojihusisha na uhifadhi wa mazingira na usalama wa Wanyamapori na washiriki ni Majaji wa Mahakama Kuu, Mahakimu, Waendesha Mashtaka   na Wapelelezi wa vyombo mbalimbali vya Serikali wakiwemo TAWA, TANAPA, TFS, NCCA , kutoka mikoa ya Arusha, Manyara, Singida, Kilimanjaro na Tanga. 

 “Mashauri ya makosa dhidi ya Ujangili na misitu yana changamoto kubwa sana, kwa sababu haya makosa yanagusa uchumi wa taifa, nani makosa ya kimataifa,hivyo ili watu waweze kuamua mashauri hayo kwa wakati na inavyostahili, ni vema wawe na uelewa wa kutosha, na matarajio yetu baada ya mafunzo haya kutakuwa na uboreshaji mkubwa katika kukabiliana na makosa haya,” amesema Mhe. Dkt. Kihwelo.

Pia, Mhe. Jaji Kihwelo amewapa wito maafisa wote wanaoshiriki mafunzo hayo na wengineo kushughulikia mashauri ya uhalifu dhidi ya Wanyamapori kwa uweledi na uadilifu pamoja na kuongozwa na dhamira zaidi.

Kwa Upande wake, Samson Kasaala ambaye ni Mkurugenzi wa Mafunzo na Operesheni wa PAMS Foundation, amebainisha kuwa taasisi yake imefadhili mafunzo haya ili kuhakikisha wadau hao wanaboresha uweledi  katika utendaji wao wa kazi na hivyo kukabiliana ipasavyo na uhalifu huo wa wanyamapori.

Pia ameongeza: “Niwaombe wadau hao wawe na uweledi na kutenda haki, kuhakikisha kesi zote zinasikilizwa kwa haki na hukumu zinakuwa za haki, kwa sababu wao wana wajibu wakulinda mali zetu ambazo ni sehemu muhimu ya uchumi kama utalii.”

Wawezeshaji wa mafunzo hayo ni Majaji wa Mahakama Kuu, Waendesha Mashita kutoka Ofisi ya Mashtaka ya Taifa, Maafisa kutoka Jeshi la Polisi na Mamlaka mbalimbali zinazojihusisha na upelelezi pamoja na uhifadhi wa Maliasili.

Nao baadhi ya washiriki wa Mafunzo hayo akiwemo Afisa Uhifadhi wa Wanyama Pori kutokea Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori nchini (TAWA)Kanda ya Arusha Matika Chacha amesema kuwa mafunzo hayo yatasaidia katika kuboresha masuala ya upelelezi na hivyo kupatikana kwa ushahidi mzuri utakaowezesha kuwajibishwa kwa wahusika wa uhalifu dhidi ya Wanyamapori na makosa ya misitu.

Kwa upande wake Afisa Misitu kutokea wakala wa huduma za Misitu (TFS) Kanda ya Kaskazini Zayana Mrisho amesema kuwa mafunzo hayo yatawasadia kupata uelewa mpana juu ya taratibu bora za ukamataji wa wahalifu na kuwafikisha watuhumiwa Mahakamani bila kuathiri mwenendo mzima wa tukio zima.

Aidha, makundi matatu ya mafunzo haya yamekwishafanyika katika mikoa ya Morogoro, Katavi na Iringa huku awamu ya tano ikitarajiwa kufanyika wilayani Tarime mkoani Mara mwezi Mei mwaka huuu ambapo mpaka kumalizika kwa mafunzo, jumla ya washiriki 785 watakuwa wamepatiwa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akihutubia na kufungua mafunzo ya yanayohusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori na misitu Chuoni Lushoto mkoani Tanga.

3. 

Mratibu wa mafunzo Endelevu ya Kimahakama wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Hakimu Mkazi, Mhe. Husna Rweikiza akitoa neno la utangulizi wakati wa Mafunzo  yanayohusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori na misitu yanayofanyika  Chuoni Lushoto mkoani Tanga.

Baadhi ya washiriki wa Mafunzo  yanayohusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori na misitu yanayofanyika  Chuoni Lushoto mkoani Tanga.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Tanga, Mhe. Katarina Mteule akitoa neno la ukaribisho wakati wa Mafunzo  yanayohusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori na misitu yanayofanyika  Chuoni Lushoto mkoani Tanga.

Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Washiriki ambao ni Majaji wa Mahakama Kuu wakati wa Mafunzo  yanayohusu namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori na misitu Chuoni Lushoto mkoani Tanga. Kushoto  ni Jaji wa Mahakama Kuu (T) kanda ya Moshi, Mhe. Adrian Kilimi, anayefuata ni Mhe. Salma Maghimbi, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu(T) kanda ya Dar es Salaam, na wa mwisho ni Jaji wa Mahakama Kuu (T), kanda ya Manyara, Mhe.Setephen Magoiga.