Jumamosi, 30 Septemba 2023

MSIBA MWINGINE MZITO SHIMIWI IRINGA

·Mahakama Sports Mpira wa Miguu yaifumua Ras Kigoma 8:0

Na Faustine Kapama -Mahakama, Iringa

Lilikuwa suala la muda tu kwa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu kuyaanza Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa kwa kishindo kufuatia mchezo wake wa kwanza kukipiga kipute na Kilimo kuahirishwa kwa sababu ya msiba.

Leo tarehe 30 Septemba, 2023 imeingia katika Uwanja wa Samora kuvaana na timu ya Ras Kigoma na kuzabua mabao nane kwa nunge kwenye mchezo uliotawaliwa na ufundi wa kimpira uliokuwa unaonyeshwa na vijana wa Mhimili wa utoaji haki.

Mchezo huo uliochezwa majira ya alasili ulianza kwa kasi huku timu zote zikishambuliana kwa zamu, huku Mahakama Sports ikilisakama lango la wapinzani mara kwa mara. Katika mchezo huo, mshambuliaji hatari wa Mahakama Sports Martin Mpanduzi alifanikiwa kuondoka na mpira baada ya kupachika mabao matatu.

Ilikuwa katika dakika ya 12 ambayo Mpanduzi alifungulia mlango wa magori kwa timu yake kwa kupachika bao safi kutokana na pasi murua kutoka kwa kiungo punda Selemani Magawa.

Katika dakika ya 16, Magawa alitikisa nyavu za Ras Kigoma kwa kupachika bao safi baada ya shuti kali lililomshinda mlinda mlango. Mvua ya magoli iliendelea kunyesha langoni mwa Ras Kigoma baada ya Bundi kuzengea zengea eneo hilo.

Kwenye dakika ya 22 ya mchezo, Mpanduzi tena alipachika bao lingine la tatu baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Magawa kabla ya kutikisa nyavu kwa mara nyingine katika dakika ya 31.

Magawa alipachika bao lingine katika dakika ya 35, huku Nasoro Mwampamba akihitimisha karamu ya magori katika kipindi cha kwanza baada ya kuachia shuti kali lililomshinda mlinda mlango wa Ras Kigoma.

Katika kipindi cha pili, timu ya Mahakama Sports ilianza kucheza pasi fupi fupi na kuzidisha mashambulizi, hivyo kuendelea kulishambulia lango la wapinzani na kufanikiwa kwa muda wote kuwachezea Ras Kigoma nusu uwanja.

Katika dakika ya 50, Abdi Sasamalo alipachika mpira kwenye nyavu na kuiandikia timu yake bao la saba kabla ya dakika mbili baadaye, Gabriel Mwita akahitimisha karamu ya magori baada ya kwenda kwenye kamba, hivyo kuiwezesha timu yake kuondoka na ushindi mnono.

Wakati wa mchezo huo, mwamuzi aliwazawadia wachezaji wawili wa Ras Kigoma kadi za njano baada ya kuwachezea rafu wachezaji wawili wa Mahakama Sports.

Wachezaji wa Mahakama Sports waliosakata kambumbu ni Fahamu Kibona, Nasoro Mwampamba, Nkuruma Katagira, Emmanuel Mwamole, Akida Mzee, Kelvin Muhagama, Frank Obadia, Gabriel Mwita, Martin Mpanduzi na Seleman Magawa.

Wengine ni Abdi Sasamalo, Mbura Minja, Iman Zumbwe, Gisbert Chentro, Rashid Hamis, Devis Munubi, Seif Shamte na Ramadhani Seif. Benchi la ufundi liliongozwa na Kocha Mkuu Spear Mbwembe na Kocha Msaidizi Said Albea.

Alikuwepo pia Timu Meneja Shaibu Kanyachole, Meneja wa Vifaa Eliya Ngule na Daktari Janeth Mapunda.

Akizungumza baada ya mchezo kumalizika, Mwalimu wa timu Spear Mbwembwe amesema wachezaji wake wamecheza vizuri, ingawa hawakufuata mfumo wa pasi fupi fupi, hasa katika kipindi cha kwanza.

Amesema baada ya kuanza kipindi cha pili, vijana wake walirudi kwenye mfumo na kuanza kuonyesha kandanda safi na kucheza mpira wa kwenye vitabu, hivyo kuwafaya timu pinzani kupoteana.

“Nadhani umejionea mwenyewe katika kipindi cha pili. Kama muda wote wangecheza hivyo, hawa jamaa (Ras Kigoma) walikuwa wanakula zaidi ya goli 10. Hata hivyo, niwapongeze vijana wangu kwa kujituma na kupata matokeo haya mazuri,” amesema.

Naye Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede hakuwa nyuma kumwaga sifa kwa wachezaji kwa kazi nzuri waliyokuwa wanaifanya uwanjani. Amesema kuwa ushindi huo ni mwanzo mzuri kwa timu yake na anaamini kila timu itakayothubutu kukanyaga uwanjani itachezea kichapo.

“Hizi ni mvua za rasharasha, mazika bado hayajaanza. Tuna timu imara sana mwaka huu, lengo letu kila timu itakayojaribu kuja uwanjani itapata dozi ya kutosha, kuliko hata hii ambayo Ras Kigoma wameipata. Tunataka wapinzani wetu watuelewe, kwa hili hatutanii, tuna maanisha, wasije wakasema hatukuwatahadhalisha,” amesema.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, timu ya Mahakama Mpira wa Miguu imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo katika kutafuta nafasi ya kutinga 16 bora.

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Mchezaji wa Mahakama Sports Martin Mpanduzi akikabidhiwa mpira baada ya kupachika mabao matatu kwenye mchezo huo. Picha chini Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede akimpongeza mchezaji huyo.

Wachezaji wa Mahakama Sports wakishangilia baada ya kupachika bao  kwenye lango la timu pinzani. Picha chini wachezaji wakilisakama lango la Ras Kigoma.

Kipa wa Ras Kigoma akipishana na mpira baada ya Martin Mpanduzi (wa tatu kulia)  kupachika bao. 
Kipa wa Ras Kigoma akilamba nyasi baada ya mchezaji wa Mahakama Sports Seleman Magawa kwenda kwenye nyavu. Picha chini Magawa (kulia) akifuhia na wachezaji wenzake.

Mashambulizi yakiendelea. 
Kocha Mkuu wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe akiongea na vijana wake wakati wa mapumziko. 
Mwamuzi akimpa kadi ya njano mchezaji wa Ras Kigoma baada ya kumchezea vibaya mchezaji wa Mahakama Sports. 
Mwamuzi wa pembeni akinyoosha kibendera kuashiria kuotea kwa mchezaji.

Ulikuwa mwendo wa Aziz Key leo, si mchezo.

Vyuma hivi hapa, mtu na nusu. 

TIMU YA MAHAKAMA NETIBOLI MOTO, UNACHOMA

· Bendera ya Mahakama juu SHIMIWI Iringa

·Elimu yakimbiwa na mashabiki wake

Na Faustine Kapama -Mahakama, Iringa

Ukichezea moto utakuunguza. Ndicho inachokifanya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) mkoani hapa.

Katika mchezo huo uliochezwa leo tarehe 30 Septemba, 2023 katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Ruaha, timu ya Mahakama ilikutana na timu ngumu ya Maji ambayo imeungua vibaya baada ya kupokea kichapo cha vikapu 28 kwa 16.

Mchezo huo uliochezwa kuanzia saa 5:00 asubuhi ulianza kwa timu zote mbili kukamiana huku tupia tupia vikapu ikawa bandika bandua. Kila timu inapotupia, timu nyingine nayo inatupia.

Ilikuwa timu ya Elimu iliyoanza kutupia dakika za mwanzo za mchezo, lakini Mahakama Sports ikachomoa baada ya muda mfupi. Kitendo cha Elimu kutangulia kutupia vikapu kiliwaamusha wachezaji wa Mahakama na kuanza kulisakama lango la wapinzani wao.

Tupia tupia vikapu iliendelea na hadi timu zote zinaenda mapumziko, Mahakama Sports ilikuwa mbele kwa kutumbukiza vikapu 15 kwa 11. Kipindi cha pili kiliendelea kwa Mahakama kuzidisha mashambulizi na kuzidi kuwakandamiza wapinzani wao.

Baada ya kugundua utoaji wa dozi unazidi kuendelea, mashabiki wa timu ya Elimu walizima muziki na mavuvuzela yao na kutokomea kusikojulikana na kuiacha timu yao ikiendelea kubamizwa na Mahakama Sports. Hadi kipenga cha mwisho kinapulizwa, Mahakama Sports ikazoa vikapu 28 kwa 16 walizoambulia Elimu.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Katibu wa Mahakama Sport Robert Tende amesema moto waliouwasha utaendelea kuwaunguza wote wanaojitia kimbelembele kucheza nao kwenye mashindano hayo na hawatabaki salama.

“Mjomba, huu sio moto wa kifuu, ukichomeka kidole chako utaungua, tena vibaya mno. Timu yoyote itakayoingiza timu uwanjani ikubali kuvumulia maumivu, hawatabaki salama, amini nakwambia,” alisema.

Mwalimu wa timu Paul Mathias amewashukuru vijana wake kwa kupambana na kuibuka na ushindi huo muhimu dhidi ya timu hiyo ngumu. “Nawapongeza sana vijana wangu, kwa kweli hawajaniangusha. Tulipoanzia ndipo tutakapomalizia, hakuna kupoa,” alisema.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.

Katika mpira wa miguu, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.

Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma, Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya Uchaguzi (NEC).

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Mashabiki wa timu ya Mahakama Sports wakiwa mitaani mjini Iringa kushangilia vipigo vinavyoendelea kutolewa na timu yao kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI).
Mchezaji Philomena Haule ambaye ni mtupiaji vikapu hatari akinyanyuliwa na mashabiki baada ya mchezo huo.
Mashabiki wa Mahakama Sports wakinyanyua mtupiaji kinara wa vikapu,Tatu Mawazo baada ya kumalizika kwa mchezo.
Shangwe za mashabiki zikiendelea.
Hii hapa miamba ya Netiboli kwenye mashindano ya SHIMIWI.
Mpira huooooo unatumbukia kwenye kikapu.
Mchezaji wa timu ya Mahakama akipokea pasi safi iliyozaa kikapu.
Timu ya Elimu iliyopokea kichapo.

MAHAKAMA YASAMBARATISHA MAWASILIANO SHIMIWI

· Tume ya Utumishi wameyataka wenyewe

Na Faustine Kapama -Mahakama, Iringa

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) leo tarehe 30 Septemba, 2023 imeendelea kutoa dozi baada ya kuzoa pointi mbili katika kila timu kwenye mchezo wa Kamba Wanaume na Kamba Wanawake. 

Katika michezo hiyo iliyofanyika katika uwanja wa Mkwawa mjini hapa, Kamba Wanaume walikutana na Mawasiliano, huku Kamba Wanawake wakikabana koo na Tume ya Utumishi na kufanikiwa kuzilambisha nyasi timu hizo.

Ulikuwa mchezo wa Kamba Wanawake ulioanza ambapo timu ya Tume ya Utumishi nusra iondolewe kwenye mashindano baada ya kuingia uwanjani kwa kusitasita wakihofia kichapo.

Mwamuzi alipouita mchezo huo, Tume ya Utumishi walijitokeza haraka haraka, lakini walipoziona ‘Tembo za Mahakama’ wakatokomea, wakidai haikuwa mechi yao.

Baada ya kujiridhisha, huku timu ya Mahakama ikiwa inasubiri mpinzani uwanjani, waamuzi waliwaita tena Tume ya Utumishi lakini wakahofia kuingia. Walipoitwa kwa mara ya tatu ndipo wakaibuka kutoka mafichoni kukabiliana na miamba ya Mahakama.

Mchezo huo ulipoanza, Mahakama hawakuwa na huruma na mtu, wakawachakaza vibaya wapinzani wao kwenye mivuto yote miwili, hivyo kuzoa pointi zote mbili.

Baadaye, mchezo wa Kamba Wanaume ulifuata kwa Mahakama kutifuana na Mawasiliano. Kipigo kikaendelea kutembea ambapo Mawasiliano walikiona cha mtema kuni baada ya kuchakazwa vibaya kwenye mivuto yote miwili.

Kufuatia ushindi huo, timu za Mahakama zinaendelea kupeperusha vyema bendera ya Mahakama, huku Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede akiwapongeza vijana wake kwa kuendeleza kile wanachokitaka.

"Kazi inaendelea, kwani bado hatujamaliza. Niwakumbushe tu wapinzani wetu kuwa vipigo kama hivi vinaendelea na yoyote tutakayekutana naye ajiandae kisaikolojia kupokea kipigo," amesema.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.

Katika mpira wa miguu, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.

Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma, Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya Uchaguzi (NEC).

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Timu ya Mahakama Sports Kamba Wanawake kazi inaendelea.
Timu ya Mahakama Sports Kamba Wanaume (juu) wakiwaonyesha kazi na Mawasiliano (chini).
Timu ya Mawasiliano ikitaabika baada ya kuchakazwa vibaya. Picha chini, mchezaji wa Tume ya Utumishi akilamba nyasi baada ya kuzidiwa.

Mashabiki wa Timu ya Mahakama Sports wakishangilia baada ya wapinzani kuchezea kichapo.


MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI MOSHI YAFANYA KIKAO KAZI CHA TATHIMINI

Na. Paul Paschal – Mahakama, Moshi

Uongozi na Watumishi wa Mahakma ya Hakimu Mkazi Moshi wamekutana na kufanya kikao kazi cha mapitio ya kiutendaji ya mwezi septemba wenye lengo la kuainisha mafanikio, changamoto na namna ya kuboresha utoaji huduma za kimahakama kwa wananchi na wadau.

Akifungua kikao kazi hicho kilichofanyika tarehe 29 Septemba, 2023 Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi Mhe. Salome Mshasha alisema,  aliwakumbusha Watumishi wote kutambua dira ya Mahakama  ni moja tu kutoa  haki kwa wananchi  wote na kwa wakati, hivyo ni vyema  katumia maarifa na weledi kufanikisha hilo ni lazima kusimamia misingi ya maadili, nidhamu na uwajibikaji.

Naye Afisa Tawala wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi Bw. Paul Mushi alisema, Watumishi wanapaswa kutunza na kusimamia rasilimali za ofisi ili kuwezesha kutimiza malengo ya ofisi.

“tukiweza kuzimamia rasilimali za ofisi yetu mambo yatakuwa mzauri na kuondoa changamoto. Pia niwaombe kuongeza jitihada katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHEMA), vile vile tuhahikikishe taarifa za mashauri yote katika kituo chetu zinauhishwa kwa wakati ili tuwe na taarifa sahihi za kiutendaji”. aliongeza Afisa Tawala huyo. 

Kwa upande wake mtumishi wa Mahakama hiyo, Bw. Robert Cornel alisema, swala la kutoa lugha nzuri kwa mtumishi anapo muhudumia mteja ni la msingi sana katika utoaji haki, hii inajenga faraja kwa wateja hata pale ambapo maamuzi yanakuwa  hayajatolewa kwa upande wake na lugha nzuri daima inapunguza malalamiko.

Kikao hicho hufanyika kila mwisho wa mwezi kwa lengo la kufungua tathimini ya kiutendaji wa shughuli za Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi sambamba na kuweka mipango kwa mwezi unafuata.

Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi Mhe. Salome Mshasha akifafanua jambo wakati wa kikao kazi cha mwezi Septemba cha tathimini kwa watumishi wa Mahakama hiyo (hawapo pichani).


Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi wakifuatilia agenda za kikao kazi hicho cha tathimini cha mwezi Septemba.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




JAJI EBRAHIM AFANYA UKAGUZI GEREZA LA WILAYA YA LINDI

Na. Hilary Lorry – Mahakama Lindi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe.Rose Ebrahim hivi karibuni amefanya ziara ya kikazi katika gereza la Wilaya ya Lindi.

Akizungumza na mahabusu na wafungwa katika gereza hilo Wilaya ya Lindi Mhe. Ebrahim aliwataka wafungwa na mahabusu watakapo toka gerezani hapo kuwa mabalozi wazuri wakupinga vitendo viovu pindi watakaporudi uraiani. Vilevile aliwaasa vijana kutumia muda wao mwingi vizuri katika kujikita katika shughuli za kuichumi na siyo kutenda mambo maovu.

“Nasikitika sana kusema Kanda hii ya Mtwara imekuwa na kasumba ya matukio mengi ya ukatili wa kijinsia hasa matukio ya ubakaji hii inafanya taifa kupoteza nguvu kazi, hivyo nawaomba  kama Mama na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda hii mtakapo toka hapa gerezani mkawe mabalozi wazuri wakupinga matendo maovu”, aliongeza Jaji Ebrahim.

Mhe. Ebrahim aliendelea kwa kutoa pongezi kwa Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Lindi pamoja na watumishi wenzake kwa juhudi kubwa za kuwahudumia wateja wao ambao ni wafungwa na mahabusu katika gereza hilo. vilevile aliwapongeza  kwa jitihada wanazofanya katika kuhakikisha gereza la  Wilaya ya Lindi linakaa katika hali ya usafi muda wote.

Jaji Ebrahim aliwataka Mahakimu wa ngazi zote kuendelea kusaidiana kwa karibu na timu ya haki jinai kuendesha mashauri kwa haraka ili kuepusha mashauri ya mlundikano (backlog cases). Aidha aliwapongeza Mahakimu wa Mkoa wa Lindi kwa kutozalisha mashauri ya mlundikano na kwa jitihada za kutoa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri kwa wakati.

“Nafahamu Mkoa wa Lindi hauna mashauri mengi ya muda mrefu, naomba jitihada zilizopo ziboreshwe ili tusizalisha mashauri ya muda mrefu (backlog cases) ikiwa ni pamoja na kutoa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri kwa wakati. Aidha natambua mpango tuliojiwekee kama Kanda na Mkoa wa Lindi wakutoa nakala za hukumu na mwenendo mara tu shauri linapofika tamati naomba mpango huu uendelee kutiliwa mkazo ili tusije kuwakwamisha hawa ndugu zetu wakati wa kukata rufaa” alisema Jaji Ebrahim.

Aidha, wakizungumza kwa nyakati tofauti Mkuu wa Gereza la wilaya ya Lindi ASP.Dominic Byamungu, wafungwa na mahabusu wameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa hatua kubwa waliyoipiga katika masuala ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHEMA) yaani Mahakama Mtandao (video conference) kwakurahisha zoezi la usikilizaji wa mashauri kwa wakati.

“Awali ilikuwa lazima mahabusu, mfungwa au hata shahidi kufika katika mahakamani lakini kutokana na Mahakama kuboresha mifumo ya TEHAMA sasa tunaweza tukawa na mahabusu na wafungwa  mwenye mashauri  ya rufaa Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani au Mahakama yoyote hapa nchini na wakasikilizwa wakiwa  gerezani…,

…hii imepunguza suala la mashauri kuchukua muda mrefu bila kusikilizwa na imepunguza gharama kwa Serikali na Magereza, imerahisisha upatikanaji wa haki kwa wakati na pia imeongezea serikali kipato kwa kulinda nguvu kazi kusafiri umbali mrefu”, alisema Mkuu wa gereza hilo.

Katika ziara hiyo  Jaji Mfawidhi Kanda ya Mtwara aliongozana na  Mahakimu, Viongozi waandamizi wa Mahakama kwa kanda ya Mtwara na Lindi pamoja na  timu ya haki jinai kwa Mkoa wa Lindi.

Ziara ya Jaji Ebrahim ni mwendelezo wa ziara yake katika Kanda ya Mtwara na Mkoa wa Lindi, Ziara yake katika Gereza la Wilaya ya Lindi imelenga zaidi kusikiliza na kuangali namna bora ya kutatua changamoto zinazo wakabili wafungwa na Mahabusu katika gereza hilo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu) akiwa kwenye picha ya pamoja na Maafisa waandamizi wa Gereza Kuu la Wilaya ya Lindi alipofanya ziara ya ukaguzi hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu kulia) akiwasili  gereza Kuu la Wilaya ya Lindi na kupokelewa na mwenyeji wake Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Lindi  ASP. Dominic Byamungu.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu kulia) akibadilishana mawazo na mwenyeji wake Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Lindi  ASP. Dominic Byamungu  alipowasili  gerezani hapo. 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu) akiwa katika picha ya Pamoja na Maafisa waandamizi wa magereza pamoja na timu ya Haki jinai Mkoa wa Lindi.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Ijumaa, 29 Septemba 2023

JAJI MKUU AWAHIMIZA WANANCHI NA WADAU KUSOMA SHERIA ZA KAZI

 Na. Innocent Kansha – Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ametoa rai kwa wananchi na wadau mbalimbali nchini kuendelea kujielimisha ili waweze kuzifahamu kwa ufasaha sheria zinazotumika kutatua migogoro ya kazi.

Azungumza katika hafla ya uzinduzi wa Mfumo wa sheria za kazi kiganjani ‘Labour Law Mobile App’, Juzuu ya Maamuzi ya migogoro ya kazi ya Mahakama ya Rufani ‘Court of Appeal Labour law Report’ na pia uzinduzi wa machapisho ya sheria na kanuni za kazi ‘A compilation of Labour statutes and regulations’ Mhe. Prof. Juma amesema, unapomwezesha mwananchi kuzipata sheria zote za kazi kiganjani ifahamike kuwa mawasiliano ya kisheria ni nguvu, hii itaonyesha kwamba Mahakama inamjali mwananchi na kusaidia kukuza imani ya wananchi kwa chombo chao cha utoaji haki vilevile inamwezesha kuipata haki hiyo kwa ukaribu zaidi.

“Siku zote Mawasiliano ya kisheria ni nguvu, unapomwezesha mwananchi wa kawaida kupata taarifa muhimu kuhusu mashauri na sheria unampa nguvu kwa sababu silaha ya kwanza ya kupigania haki yako ni uelewa, kama unaelewa wa sheria na taratibu, unaelewa wa wapi pa kufungua shauri lako, ndani ya muda gani, kuna utaratibu gani unaotumika huo ndiyo uwezeshaji mkubwa kwa mwananchi”, aliongeza Jaji Mkuu

Aidha, Prof. Juma alisema kama taarifa hizo zote za msingi zinapatikana kiganjani zimewezeshwa kwa mwananchi wa kawaida na kwamba kabla ya kukimbilia mahakamani mwananchi anatambua mipaka ya haki zake iko wapi na kupima uwezekano wa kushinda ama kutoshinda, uwezeshaji wa namna hiyo unakupa uhuru na uwezo wa kufanya maamuzi ambayo ni muhimu sana juu ya jambo husika.

“Kutokana na zoezi hili naona tunamwezesha mwananchi wa kawaida kupata taarifa zote kiganjani wake na tunapomwezesha kuelewa haki zake vilevile tunapunguza mlundikano wa migogoro katika taasisi zinazotoa haki kwa sababu mwananchi tayari atakuwa na uelewa, mathalani katika mgogoro wa namna flani sina haki, hivyo hakuna haja ya kuendelea kung’ang’ania kuendelea na mgogoro husika”, aliongeza Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu Mhe. Prof Juma aliongeza kuwa, uwezeshaji wa namna hiyo unaleta usawa kwani wanasheria wanapata fedha zao hasa mawakili kutokana na kuuza taarifa za kisheria mfano, pale ambapo mwananchi anatatizo akakutana na mwanasheria na kupewa kiini cha tatizo, atamwambia hilo ni tatizo jepesi sana na kumtaka alipe kiasi Fulani cha fedha ili aweze kusaidia kulitatua.

Jaji Mkuu amesema, mwananchi anapowezeshwa kufahamu sheria inayotumiwa na mawakili, wanasheria na Mahakama inamuweka katika mizani sawa na wanansheria hivyo basi inampa nguvu ya kujiuliza kwa nini amlipe mwanasheria ili apate taarifa ambayo anauwezo wa kuipata kiganjani.

“Wananchi wote wakiweza kuiishi sheria, kuviishi vifungu vya Katiba hapo ndipo tutakuwa na amani ya kudumu kwa sababu kila mtu atakuwa anaelewa mipaka yake, haki zake na kuelewa wajibu wake, hivyo hiki ni kielelezo muhimu sana kutokana na uzinduzi huu”, alisisitiza Mhe. Prof. Juma.

Jaji Mkuu Mhe. Prof. Juma akataja faida nyingine za uzinduzi huo kama kielelezo cha kusaidia usuluhishi wa utatuzi wa migogoro mathalani ukichukulia mzigo mkubwa wa migogoro ya kazi inafanywa kwa kiasi kikubwa katika ngazi ya Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ‘Commission for Mediation & Abitration’ (CMA) “hawa wana kazi kubwa sana ya kutatua migogoro ya kazi kwa kuangalia takwimu kama haya mabaraza upatanishi yasinge kuwepo Mahakama pekee zisingeweza kutatua migogoro ya kazi kwa sababu migogoro mingi inaishia kwenye mabaraza hayo” alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma amesema migogoro ya kazi pamoja na mambo mengine inatoa taswira ya urahisi wa kufanya biashara katika maeneo husika kwa sababu nchi yenye migogoro mingi ya kazi hakuna mwekezaji atapenda kwenda kuwekeza mtaji wake, wala hakuna mfanyabiashara atakae kwenda kuwekeza biashara katika mazingira ambayo siku zote yamegubikwa na migogoro.

Hivyo mabaraza hayo yanasaidia sana katika usuluhishi na upatanishi vilevile wananchi wakipata uelewa wa sheria na taratibu za migogoro ya kazi, kazi za mabaraza zitakuwa nyepesi zaidi kwa kusaidia kuondosha migogoro hiyo, hii itapelekea kujenga taswira chanya na kuimarisha imani ya wananchi na kwa wawekezaji wa ndani na nje.

“Ombi langu ni kwamba tuishi namna sheria inavyoelekeza kwa sababu kuna uwezekano tukawa na sheria nzuri kabisa lakini tabia zetu na mienendo yetu ikawa tofauti kabisa na sheria zilivyo na mara nyingi watu wa nje wanatuangalia kwa kusoma sheria zetu zinasemaje kuhusu migogoro ya kazi na kuziona ni zuri sana ila wanafika wanaona tabia zetu na mienendo yetu haiendani na sheria zetu moja kwa moja wanatudharau, kwamba hatuna utamaduni wa kuheshimu sheria”, aliongeza Jaji Mkuu.

Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi Mhe. Dkt. Yose Mlyambina ametoa shukrani za dhati kwa Majaji, Wasajili na watumishi wote wa Mahakama Divisheni ya Kazi kwa kushirikiana bega kwa bega kuhakikisha mfumo huo wa wa sheria za kazi kiganjani ‘Labour Law Mobile App’ unakamilika na kuzinduliwa rasmi ikiwa ni ubunifu wa kumsaidia mwananchi kuzifahamu vema sheria za kazi.

“Uazishwaji wa mfumo wa sheria za kazi kiganjani ‘Tz Mobile App’ ni wazo lililotokana na hamasa ya kuibua vipaji vya watumishi wa Divisheni ya Kazi niliyoitoa katika kikao changu cha kwanza tarehe 9 Februari, 2023 katika kikao hicho niliagiza kila mtumishi mwenye wazo zuri lenye manufaa kwa Mahakama na kwa Taifa aandike kwenye ukurasa mmoja wa karatasi au afike ofisini kwangu kunieleza”, amesema Jaji Mfawidhi Mhe. Dkt. Mlyambina

Mhe. Dkt. Mlyambina anasema, katika kikao hicho aliwapa matumaini kuwa Mahakama ipo tayari kuwaunga mkono kwa kila namna ikiwezekana kwa kutoa zawadi kwa mtumishi yoyote ambaye angejitokeza na wazo jipya na chanya hasa kwenye eneo la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

“Mwanafunzi wetu wa ndani anayejitolea katika kitengo cha TEHAMA anayeitwa Bi. Lightness Kabaju alifika ofisini akiwa na wazo la kuanzisha Mahakama ya Kazi Kiganjani baada ya mazungumzo niliona ni wazo zuri nikanuia kulitekeleza na sote tulilipokea na kulitekeleza kwakuwa tuliona linalenga kusaidia wadau wetu Mahakama na jamii kwa ujumla ili kupata sheria za kazi kwa pamoja na kwa urahisi zaidi”, ameongeza Jaji Mlyambina.

Jaji Mlyambina anasema, mfumo huo mpya wa kiganjani umepakiwa sheria zote za kazi hapa Tanzania, Mikataba ya Kimataifa ya sheria za kazi, Sheria za Usalama Mahali pa Kazi (OSHA) pamoja na Sheria za Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF). Hivyo kwa kupita mfumo huo unaweza kupatikana kupitia simu janja ni wazi kuwa kila mdau anayetafuta sheria za kazi ataweza kuzipata kwa njia rahisi zaidi.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (mwenye tai nyekundu) akizinduzi wa Mfumo mpya wa sheria za kazi kiganjani ‘Labour Law Mobile App’, wakati wa hafla hiyo iliyofanyika leo tarehe 29 Septemba, 2023 katika ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi. Wengine wanaoshuhudia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (wa pili kushoto), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha (wa pili kulia), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi (watatu kushoto), Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Prof. Kennedy Gastorn (wa kwanza kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi Mhe. Enock Matembele)


Muonekano wa Mfumo mpya wa sheria za kazi kiganjani ‘Labour Law Mobile App’ uliopakiwa sheria zote za kazi hapa Tanzania, Mikataba ya Kimataifa ya sheria za kazi, Sheria za Usalama Mahali pa Kazi (OSHA) pamoja na Sheria za Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF).


Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Juzuu ya Maamuzi ya migogoro ya kazi ya Mahakama ya Rufani ‘Court of Appeal Labour law Report’ na pia uzinduzi wa machapisho ya sheria na kanuni za kazi ‘A compilation of Labour statutes and regulations’ akishudiwa na Viongozi mbalimbali walihudhuria hafla hiyo (hawapo pichani). Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (wa kwanza kushoto), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha (wa pili kulia), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi (watatu kushoto), na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi Mhe. Enock Matembele aliyeshika kisemeo

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akinyoosha Juzuu hilo juu kuashiria uzinduzi wa Juzuu ya Maamuzi ya migogoro ya kazi ya Mahakama ya Rufani ‘Court of Appeal Labour law Report’ na pia uzinduzi wa machapisho ya sheria na kanuni za kazi ‘A compilation of Labour statutes and regulations’ akishudiwa na Viongozi mbalimbali walihudhuria hafla hiyo (hawapo pichani). Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (wa kwanza kushoto), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha (wa pili kulia) na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi (wa pili kushoto).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi Mhe. Dkt. Yose Mlyambina kitoa historia fupi ya namna watumishi walivyoshiriki ubunifu wa kuandaa Mfumo mpya wa sheria za kazi kiganjani ‘Labour Law Mobile App' pamoja na ubunifu wa uandaaji wa Juzuu na Machapisho mengine. 



Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Divisheni hiyo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimpongeza  mbunifu wa kuandaa Mfumo mpya wa sheria za kazi kiganjani ‘Labour Law Mobile App'   Bi. Lightness Kabaju wakati wa hafla hiyo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa kwenye picha ya pamoja na Wadau wa muhimu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi waliohudhuria hafla hiyo. 

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)



 

TIMU YA MAHAKAMA NETIBOLI ‘YAUA MTU’ SHIMIWI

·Yaikandamiza Ras Kilimanjaro vikapu 49

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Netiboli imeyaanza vyema mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) leo tarehe 29 Septemba, 2023 baada ya kuiadhibu vikali timu ya Ras Kilimanjaro kwa jumla ya vikapu 49:6.

Katika mchezo huo uliochezwa majira ya alasili, timu ya Mahakama ilienda mapumziko ikiwa imeshatumbukiza vikapu 31kwa 2 na kuifanya kuongeza katika kipindi cha kwanza. 

Baada ya mapumziko, Mahakama Sports waliendelea kulisakama lango la Ras Kilimanjaro na waliwabana pumzi wapinzani wao wasifurutike hadi dakika ya mwisho.

Tupia tupia ya vikapu iliendelea, huku timu ya Mahakama ikiwachachafya wapinzani wao. Hadi mwamuzi anapuliza kipenga cha mwisho, Mahakama Sports ilikuwa imeshatupia vikapu 49 kwa 6 walizoambulia wapinzani wao, Ras Kilimanjaro. 

Akizungumza baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema kipigo hicho kitaendelea na ni onyo kali kwa yule atakayethubutu kuwachezea.

"Nilisema tangu mwanzo, hatutamchekea mtu tusije tukaambulia mabua. Sisi tunachotaka ni makombe. Natoa onyo, wasijaribu kutuchezea, wataumia," Mwenyekiti Dede ameonya.

Naye Mwalimu wa Timu Paul Mathias amewapongeza vijana wake kwa kuonyesha mchezo mzuri na kuzingatia maelekezo aliyowapa. "Kama tutaendelea hivi, kuna mtu atakula mia hapa. Hatuna utani na mtu sisi," amesema. 

Wachezaji walioiwakilisha Mahakama ni Tatu Mawazo, Philomena Haule, Upendo Gustav, Nyangi Kisangenta, Shani Ally, Eunice Chengo na  Sophia Songoro. Waliokuwa kwenye mbao ndefu ni Leah Danda, Agnes Mwanyika, Lulu Nchimbi, Rohiba Makassi, Malkia Nondo, Angela Dismas, Akinzia Kimaro na Lucy Kibona.

Matokeo hayo ni mwendelezo wa ushindi ambao timu za Mahakama zimeupata. Mapema leo asubuhi, Mahakama Sports Kamba Wanaume na Kamba Wanawake walianza vizuri mashindano hayo baada ya kutembeza vipigo kwa wapinzani wao Ras Kigoma na Waziri Mkuu Sera ambao waliamua kuingia mitini.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.

Katika mpira wa miguu, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.

Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma, Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya Uchaguzi (NEC).

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.


Mashabiki wa Mahakama Sports wakinyanyua mtupiaji kinara wa vikapu,Tatu Mawazo baada ya kumalizika kwa mchezo. Picha chini wakimnyanyua mtupiaji mwingine hatari Philemona Haule.


Hawa hapa vijana wa Professa walioipeperusha vyema bendera ya Mahakama.


Tazama mpira unavyotumbukia kwenye kikapu.
Pasi ya kutafuta kikapu ilianzia hapa.
Ikapokelewa hapa.
Ikatupiwa hapa.

Hatimaye mpira ukajaa kwenye nyavu.

Mpira huooooo unatumbukia.
Ni shangwa kila kona.
Benchi la wachezaji likiongozwa na Katibu Msaidizi Theodosia Mwangoka (wa pili kulia) likowa na furaha tele. Kulia ni Mwalimu Paul Mathias akiendelea kutoa maelekezo kwa vijana wake.
Ilikuwa shangwa kila kona (juu na chini).


Hawa hapa Ras Kilimanjaro waliopokea kichapo.