Jumamosi, 2 Desemba 2023

WAZIRI GWAJIMA AZINDUA MAHAKAMA YA MFANO KUPINGA UKATILI, ULAGHAI DHIDI YA WATOTO MTANDAONI

 Na. Innocent Kansha - Mahakama

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima amefungua rasmi mafunzo yanayoendeshwa kwa njia ya Mahakama ya Mfano yenye kauli mbiu isemayo “ukatili na ulaghai dhidi ya watoto mtandaoni” (Moot Court on Children Cyber Bullying and Online Grooming) ikiwa ni sehemu ya kauli mbiu ya kitaifa ya kampeni ya siku 16 ya kupinga ukatili wa kijinsia ambayo ni ‘Wekeza: Kupinga Ukatili wa Kijinsia’.

Akifungua Mahakama hiyo ya Mfano iliyoandaliwa na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) iliyoendeshwa kwenye ukumbi wa mikutano wa Nkrumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam leo tarehe 2 Desemba, 2023, Waziri Gwajima amesema, kauli mbiu ya kitaifa ina lenga kuhamasisha kila Mtanzania, popote alipo na kwa nafasi aliyokuwa nayo anatakiwa kuchukua hatua kupinga ukatili wa kijinsia.

“Niwapongeze wanachama wa TAWJA ambao ni Majaji na Mahakimu, kwa kuchukua hatua katika nafasi walizonazo na kuamaua kupaza sauti kwa kuandaa Mahakama ya Mfano iliyojikita kwenye kesi ya mfano ya ukatili dhidi ya watoto mitandaoni kwani kutokana na ukuaji wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), kesi za aina hii zimeanza kufikishwa Mahakamani”, amesema Waziri Gwajima.

Mhe. Gwajima amesema, takwimu zilizotolewa mwezi wa Oktoba, 2023, na Waziri mwenye dhamana ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, wakati akifungua Kongamano la saba la TEHAMA, zinaonyesha kuwa matumizi ya TEHAMA yameongezeka kutoka watumiaji milioni 29.9 kwa mwezi Aprili 2022 hadi kufikia watu milioni 34.04 kwa mwezi Juni 2023 ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 13. Pamoja na mafanikio mengi yaliyoletwa na TEHAMA, pamekuwepo pia changamoto ya uhalifu wa kimtandao ikiwemo uhalifu wa unyanyasaji wa kimtandao dhidi ya wanawake na watoto.

Vilevile, Mhe. Gwajima akatoa Taarifa ya Utafiti kuhusu Hali ya Ukatili wa Watoto Mtandaoni nchini, kwa mwaka 2022 (Disrupting Harm Report in Tanzania) inaeleza tathmini ya kina ya hali ya ukatili wa kijinsia nchini, athari za ukatili wa kingono, mitazamo ya watoto juu ya ukatili wa kingono mtandaoni na mwitikio wa kitaifa wa namna ya kupambana na aina hii ya ukatili.

Matokeo ya utafiti yanaonesha kuwa, asilimia 4 ya watumiaji wa mtandao wenye umri wa miaka 12-17 nchini Tanzania ni manusura wa ukatili wa mtandaoni. Watoto wengi hufanyiwa vitendo vya ukatili kupitia mitandao ya kijamii kama vile WhatsApp, Instagram, Facebook, Tik Tok pamoja na mitando mengine ya kijamii.

Mhe. Gwajima amebainisha athari zingine ikiwa ni wanaofanya vitendo vya ukatili ni watu wanaofahamika na watoto wakiwemo ndugu wa karibu na marafiki na pia watoto wanaofanyiwa ukatili hawajui namna na sehemu ya kutoa taarifa ili wapate msaada.

Aidha, Waziri Gwajima akafafanua kuhusu hatua mbalimbali ambazo Serikali pamoja na Wizara yake imezichukua ili kukabiliana na uwepo wa aina mpya ya Ukatili dhidi ya Watoto Mitandaoni unaosababishwa na kukua kwa maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Mhe. Waziri Gwajima akatanabaisha kuwa kufuatia kuanza kwa kushamiri kwa matukio haya ya ukatili wa kimtandao dhidi ya Watoto, Serikali imeunda kikosi kazi cha Taifa cha Ulinzi na Usalama wa Mtoto mtandaoni chenye lengo la kuhakikisha kuwa watoto wanalindwa dhidi ya ukatili wa mtandaoni na kuwasaidia kutumia vifaa vya kieletroniki kwa usahihi na usalama,

Vilevile, kuanza mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Mtoto ili iweze kuakisi mazingira ya sasa ikiwa ni pamoja na ukatili wa watoto mtandaoni (online child abuse) na Serikali inafanya mapitio ya Sera ya hali ya usalama katika mitandao ili kubaini maeneo ya kuboresha, amesisitiza Mhe. Waziri Gwajima.

“Elimu itakayotolewa leo na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi kuhusu namna Mahakama zetu zinavyoshughulikia kesi za ukatili wa kimtandao dhidi ya Watoto ambao ni Taifa la kesho, kuwapa uafahamu wa matendo ya ukatili yanayofanyika kwenye mitandao na changamoto zitokanazo na uhalifu wa unyanyasaji wa kimtandao hasa kwenye ukusanyaji wa ushahidi na itasaidia pia kutahadharisha vijana wetu kuwa makini na matumizi salama na bora ya huduma na bidhaa za TEHAMA’’, amefafanua Mhe. Gwajima.

Mhe. Waziri Gwajima amehitimisha kwa kutoa shukrani za kipekee kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Jaji Mkuu wa Tanzania Zanzibar, Jaji Kiongozi, Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Uongozi mzima wa Mahakama ya Tanzania Bara na Visiwani. Nitakuwa mchoyo wa fadhila nikiwasahau Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambao wametupatia ukumbi wa kufanya Mafunzo hayo. Pia niwashukuru Chuo cha Sheria kwa Vitendo na Chuo Kikuu cha Tumaini kwa kutoa taarifa na kuwaruhusu wanavyuo kushirki mafunzo hayo.

Naye Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti Wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel amesema Chama kimeandaa mkakati wa kuratibu mafunzo ya kupinga ukatili wa kijinsia kwa njia ya Mahakama ya Mfano katika mikoa 5 ya Tanzania Bara na Zanzibar katika mikoa ya Arusha, Dodoma, Mbeya, Mwanza na Zanzibar kwa tarehe tofauti tofauti ili wadau wengi waweze kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo.

Mhe. Sehel amesema kuwa tayari mafunzo kama hayo wamekwisha kutolewa katika Kanda 2 za Mahakama Kuu ambazo ni Dodoma na Arusha na yalikuwa ya mafanikio makubwa sana kutokana na mwitikio wa wadau wanaopinga ukatili wa kijinsia.

“Kama tunavyofahamu kuna sheria mbalimbali zilizotungwa na serikali yetu dhidi ya uhalifu wa kimtandao, hata hivyo maendeleo ya teknolojia yamekuwa yakikuwa na kusafiri kwa kasi ya mwanga na hata matumizi yake yanaendelea kukua kila siku. Hii inaleta kuibuka kwa makosa mapya ya kimtandao na hivyo kufanya baadhi ya sheria zetu kupitwa na wakati”, amesisitiza Mhe. Sehel

Mwenyekiti huyo wa TAWJA akatoa mfano wa sheria hizo kama sheria ya makosa ya kimtandao, unyanyasaji wa kimtandao (Cyber Bullying) ni kosa la kijinai na adhabu yake ni kifungo kisichopungua miaka 3 au faini isiyopungua shilingi milioni 5 au kutumikia kifungo na faini kutegemeana na mazingitra ya kesi.

“Hata hivyo sheria hii ya makosa ya kimtandao aihakisi mazingira na uhalisia, kwa sasa kumeibuka uhalifu wa kurusha moja kwa moja picha za unyanyasaji wa kijinsia mtandaoni (Live streaming of sexual abuse) uhalifu huu bado sheria haija itambua hivyo tunaomba Mhe. Waziri utambue hilo”, ameongeza Mhe. Sehel

…..Ni matumaini yetu kuwa sheria pamoja na sera za nchi zitarekebishwa mapema iwezekanavyo ili kukidhi matakwa ya karne ya sasa ya maendeleo ya viwanda na teknolojia na kesi ya Mahakama ya Mfano itakayosikilizwa hii leo inahusu unyanyasaji wa kijinsia wa kimtandao”, amefafanua Mhe. Sehel.  

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (kulia) akipokea zawadi ya Kitabu kilichoandaliwa na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake kutoka kwa Mwenyekiti wa chama hicho Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti Wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel leo tarehe 2 Desemba, 2023 katika ukumbi wa Nkrumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam baada ya uzinduzi wa Mafunzo yanayoendeshwa kwa Mahakama ya Mfano.


Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima akitoa hotuba yake wakati wa uzinduzi wa mafumzo hayo


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti Wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel akitoa hotuba yake wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam na Mlezi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) akitoa neno la utangulizi wakati wa mafunzo iliyoendeshwa kwa njia ya Mahakama ya Mfano kwenye ukumbi wa mikutano wa Nkrumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji na sehemu ya wanafunzi kutoka vyuo vikuu walioshiriki mafunzo hayo.

Sehemu ya wanafunzi kutoka vyuo vikuu walioshiriki mafunzo hayo.

Sehemu ya wanafunzi kutoka vyuo vikuu walioshiriki mafunzo hayo.

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (wa pili kushoto) akiwa na sehemu ya Majaji na viongozi waandamizi wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania wakati wa hafla hiyo

Sehemu ya wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi
Sehemu ya wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (wa pili kushoto) akiwa na sehemu ya Majaji na viongozi waandamizi wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania wakati wa hafla hiyo wakibadilisha mawazo.

Sehemu ya Mawakili walioendesha mafuzo kwa njia ya Mahakama ya Mfano wakiwasilisha hoja jazo mbele ya jopo la Majaji (hawapo pichani) na wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itakayo saidia kuelimisha wananchi unyanyasaji wa kijinsia mitandaoni


Sehemu ya wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi

         Sehemu ya Mawakili walioendesha mafuzo kwa njia ya Mahakama ya Mfano           wakiwasilisha hoja jazo mbele ya jopo la Majaji (hawapo pichani) na wadau          wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itakayo saidia   kuelimisha wananchi unyanyasaji wa kijinsia mitandaoni

                                (Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

MTENDAJI MOSHI AKAGUA UKARABATI WA JENGO LA MAHAKAMA MWANZO KILEMA

Na. Paul Pascal – Mahakama, Moshi

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya moshi Bi. Maria Itala amefanya ukaguzi katika jengo linaloendelea kufanyiwa kukarabati la Mahakama ya Mwanzo Kilema.

Ukaguzi huo umefanyika tarehe 30 novemba 2023 ukiwa na lengo la kujionea maendeleo ya uboreshaji wa miundo mbinu ya Mahakama hiyo ili kuweka mazingira rafiki ya utoaji huduma kwa watumishi wa Mahakama pamoja na wananchi wa kata ya kilema kusini na vitongoji vya jirani vilivyopo katika Wilaya ya Moshi Vijijini.

“Nipende kuwahaikishia wananchi wote wa kilema kati na vijiji vya jirani ya kuwa mahkama ya Tanzania itahakikisha jengo hili linakua bora na zuri kwa matumizi yetu sote ili kuwezesha wananchi wote wanapata sehemu nzuri ya kupatia haki zao”, alisema Mtendaji huyo

Ukarabati wa Mahakama ya Mwanzo Kilema ulianza mwezi Oktoba 2023 na unatazamiwa kukamilika tarehe 15 Desemba 2023 ukitekelezwa kwa fedha za ndani kutoka ofisi ya Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi ukiwa na thamani ya milioni 17, kukamilika kwa ukarabati huu kutawezesha shughuli za kimahakama kufanyika katika jengo linalomilikiwa na Mahakama ya Tanzania. Kwa sasa shughuli za Mahakama ya Mwanzo Kilema zinaendeshwa katika jengo la serikali ya Kata ya Kilema Kusini.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya moshi Bi. Maria Itala akifanya ukaguzi katika jengo linaloendelea kufanyiwa kukarabati la Mahakama ya Mwanzo Kilema.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya moshi Bi. Maria Itala akifanya ukaguzi katika jengo linaloendelea kufanyiwa kukarabati la Mahakama ya Mwanzo Kilema.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya moshi Bi. Maria Itala akifanya ukaguzi katika jengo linaloendelea kufanyiwa kukarabati la Mahakama ya Mwanzo Kilema.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya moshi Bi. Maria Itala akifanya ukaguzi katika jengo linaloendelea kufanyiwa kukarabati la Mahakama ya Mwanzo Kilema.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya moshi Bi. Maria Itala akisaini kitabu cha wageni mara alipofika Mahakama ya Mwanzo kilema kabla ya kuanza zoezi la ukaguzi katika jengo linaloendelea kufanyiwa kukarabati la Mahakama ya Mwanzo Kilema.

Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha -Mahakama.


 

Ijumaa, 1 Desemba 2023

JAJI MKUU AWAONYA MAWAKILI WANAOTUMIA LUGHA ZINAZOKIUKA MAADILI MAHAKAMANI

Na. Innocent Kansha - Mahakama.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof.  Ibrahim Hamis Juma amesema kapokea malalamiko kutoka kwa majaji kuhusu mawakili wa kujitegemea wanaowasilisha hoja zao Mahakamani kwa kutumia lugha zinazokiuka maadili ndani ya Mahakama na amekitaka Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) kuchukua hatua kabla ya majaji kulalamika.


Akizungumza katika sherehe ya 69 ya mahafali ya kuwakubali na kuwapokea mawakili wapya wapatao 279, idadi hiyo ikijumuisha wanawake 118 na wanaume 161 na kufanya jumla ya mawakili kufika 11,916 kutoka idadi ya awali ya mawakili 11,636 katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo tarehe mosi Desemba, 2023, Jaji Mkuu Prof. Juma amesema, uwakili ni taaluma yenye heshima, vitendo, kauli sahihi na mihuli vyote vinatakiwa kuwa na heshima.


"Nimekuwa nikipokea malalamiko mengi kutoka kwa Majaji, malalamiko yanayokiuka maadili hasa pale mawakili wa kijitegemea wanapowasilisha hoja zao mahakamani kwa kiburi, jeuri na kutumia lugha zisizostahili, malalamiko mengi yanakiuka kanuni ya 92 ya kanuni ya maadili ya mawakili, ukiwa unajibizana na Jaji au Hakimu unakuwa unakiuka moja kwa moja  kanuni yenu ambayo inawaongoza, wajibu wa kuheshimu Mahakama  na kutunza lugha tunazotumia si hapo Tanzania tu, pengine sheria zetu zinanyima uhuru wa kusema tu unachotaka mahakamani, naomba jambo kama hilo likitokea sio Jaji alalamike bali mawakili wenyewe wachukue hatua " amesema Jaji Mkuu

Mhe. Prof. Juma amesema kitendo kimoja tu cha ukiukwaji wa maadili ambacho pengine kimefanywa na wakili mmoja tu Tanzania, kinaweza kuharibu taswira yote ya taaluma ya uwakili nchini.

"Eneo hili mnatakiwa muwe waangalifu, tendo lolote la wakili mmoja kukiuka maadili, linaweza kuchafua taswira ya soko la ajira la mawakili wa Tanzania kwasababu siku zote inaweza kutumika kama ndiyo mfano wa hali ya maadili kwa mawakili wa Tanzania" amesema Mhe. Prof. Juma

"Hii ni Karne ya habari, chochote kinachofanyika leo kinaweza kusambaa kwa haraka zaidi na kwa muda mfupi kwa hiyo tuwe wangalifu sana katika eneo la maadili kwasababu kinaweza kukuchafua wewe na taswira ya taaluma yote ya mawakili Tanzania" ameongeza 

Jaji Mkuu Prof. Juma amesema, kama ilivyo kwa Majaji na Mahakimu, Uwakili ni taaluma inayoheshimika sana na ni taaluma ya heshima hivyo vitendo, kauli na myenendo yeo yote iwe ya heshima kwasababu  wakiruhusu mihuri yao kutumiwa vibaya inapunguza hadhi na heshima ya uwakili.

"Saini zenu mnazosaini ni heshima, nguvu ya taaluma yetu inatokana na heshima, jamii ikikosa heshima kwetu inakuwa haina maana, siku zote tuwe na tahadhari kubwa ya kutambua kwamba mamlaka yanu ni makubwa sana" amesema Mhe. Prof. Juma 

Jaji Mkuu huyo amesema, kuna kanuni za kitaaluma zinazotakiwa kuzingatiwa zinazosaidia kusafisha taaluma ya mawakili. Kila taaluma duniani inatarajiwa kujidhibiti na kuwadhibiti wanataaluma wake kwenye masuala ya nidhamu kabla chombo chochote cha nje kuja kumsimamia nidhamu kwa kujisimamia wenyewe.

 

Mhe. Prof. Juma amesema Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) kikifanya hivyo hakuna mtu atakayewaingilia kikiwa kinajichukulia hatua na kudhibiti wanachama wake katika masuala ya kinidhamu, tofauti na sasa chombo kikichukua hatua mawakili wanakusanyika kuteteana.


"Sasa Chama chenyewe kichukue hatua za kinidhamu , tumieni mamlaka mlinayo kujidhibiti wenyewe, tumieni kanuni zenu za uwakili za mwaka 2022 kujidhibiti, ni wajibu wenu kuonyesha nidhamu kwa Mahakama.


Mhe. Prof. Juma aliwataka mawakili hao kuwa na umakini wa kuchagua mawakili wa kuwa mfano wa kuigwa. Amesema wakili wa kuigwa siyo lazima awe mwandamizi tu bali wachague wale ambao watakao wahamasisha, kuwafundisha na kuwapa hamasa ya kuendelea katika fani hiyo, kuwapa miongozo na mrejesho wa kazi wanazofanya.


Pia aliwataka mawakili hao kuwa na tabia ya kujisomea kwani hakuna ukomo na kwamba wapo miongoni mwao ambao tangu walipohitimu chuo Kikuu hawajawahi kusoma kitabu hata kimoja.


“Acheni tabia za kukumbatia madesa someni kuongeza maarifa mapya ili muweze kukabiliana na ushindani wa karne ya 21, mambo mengi hivi sasa yapo hata mitandao”, ameongeza Jaji Mkuu.


Katika jambo lingine, Jaji Mkuu aliwataka mawakili hao kuwa na uwezo wa kufanya kazi kwani wamekuwa mawakili baada ya kuonesha uwezo Sekondari, Chuoni, shule ya sheria kwa vitendo, Baraza la Elimu ya Sheria na kusailiwa mbele ya Jaji Mkuu.


Jaji Mkuu amesema, kanuni za maadili ya uwakili zinataka huo uwezo muendelee kuwanao na msipojiendeleza na kukabiliana na hali ya mabadiliko itawaacha nyuma na mtakuwa mmekiuka maadili na kupoteza uwezo unaozungumzwa kwenye maadili.


Katika jambo lingine Jaji Mkuu amewasihi mawakili hao kuendana na hali ya mabadiliko ya teknolojia ambayo hayawasubiri mawakili. Amesema taaluma ya sheria na mawakili haiwezi kukwepa mapinduzi ya viwanda ambayo tayari yameshaingia mahakamani.


"Tumeanza kujifunza utaratibu mpya wa kuratibu na kumsimamia mashauri mahakamani  kwa njia ya mtandao , mfumo huu ni muhimu sana , ulikuja kuchukua nafasi mfumo uliokuwepo ambao ulizidiwa , unafaida nyingi, zipo changamoto kadhaa ambazo zinafanyiwa kazi , lakini faida zitakazopatikana ni kubwa kuliko changamoto ambazo tunazotumia kuimarisha huu mfumo" amesema Jaji Mkuu.


Kabla ya kuzungumza hayo aliwakubali na kuwatunuku vyeti mawakili hao 279.


"Kwa mamlaka niliyopewa na Sheria ya mwakili sura ya 341 Toledo la 2019, kifungu cha 8(3) nina tamka kwamba wale wote ambao majina yao yamesomwa hapa wamekubaliwa kuwa mawakili na wamerodheshwa rasmi kwenye orodha ya mawakili kuanzia leo Desemba Mosi,"amesema Jaji Mkuu. 


Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa serikali Mhe. Dkt Eliezer Mbuki Feleshi akitoa nasaha zake aliwataka mawakili hao kuzingatia sheria, kanuni na miongozo mbalimbali wanapotekeleza majukumu yao. 


Dkt. Feleshi amewakumbusha kwamba mawakili ni maofisa wa Mahakama hivyo wamepewa dhamana ya kuisaidia Mahakama katika utowaji haki kwa wakati na usawa kwa wote kwani ni jukumu lao kuhakikisha mahakama inatenda haki. 

Jaji Feleshi ameongeza kuwa, kanuni ya 92 ya kanuni za maadili ya amawakili inahusu myenendo ya mawakili, inakataza hujuma kwa Mahakama katika utowaji haki ikiwemo kutoa taarifa za uongo na kueleza jambo litakaloipotosha Mahakama katika kufika maamuzi ambayo yasingefikiwa kama si upotoshaji huo, usingekuwepo.

Dkt. Feleshi amesema kanuni hizo pia zinatakaza mawakili kutoa maoni ya kesi iliyo mahakamani katika mambo ambayo yanaweza kuathiri matokeo ya kesi husika.

"Mawakili mkumbuke kuwa tasinia ya uwakili ni nyeti, mnapaswa kuzingatia kanuni na miongozo mbalimbali iliyowekwa mnapotekeleza majukumu yenu hususani kanuni zote za maadili na myenendo ya kazi zenu" amesema Jaji Feleshi

…..Kumekuwa na tuhuma kwa baadhi ya mawakili wa kujitegemea kujihusisha na vitendo vya rushwa kwa baadhi yetu, kuwasaliti wateja wao kwa kupokea rushwa, kutoudhuria mahakamani, kutotunza siri za mteja, kutokuwa na mawasiliano mazuri kati ya wakili na mteja, kutumia mihuri isiyo halali”, ameongeza Jaji Feleshi 

Mwanasheria Mkuu huyo amesema mabadiliko ya sheria ya mawakili ya mwaka huu imeeleza kuwa wakili atakayefanya kazi bila kuwa na sifa ya uwakili atapewa adhabu ya kutozwa faini ya shilingi milioni tano na isiyozidi milioni 20 au kifungo cha mwaka mmoja gerezani mpaka miaka mitatu au vyote kwa pamoja.

"Nitumie fursa hii kuwaonya wale wote wanaofanya vitendo hivi vya kinyume na utaratibu kuacha mara moja" alisema Dokta Feleshi.

Naye, Rais wa Chama cha wanasheria Tanganyika (TLS) Wakili Msomi Harold Sungusia akuzungumza katika hafla hiyo, amesema wako katika oparesheni ya kupambana na mawakili vishoka katika maeneo yote na kuwaasa mawakili hao kuzingatia maadili na kwamba taaluma hiyo inahitaji kujitambua, kujitambua na kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa.

"Kuwa wakili msomi, siyo matangazo ya majigambo na majivuno kama upatu uvumao, bali ni haki ya mhusika kuipenda kusoma kujitafutia taarifa na Maarifa sehemu sahihi, kujielimisha, kujikosoa, kujituma na kushirikiana na mawakili wengine katika kuboresha tasnia hii" amesema Rais huyo 

Mhe. Sungusia ameongeza kuwa, wanajitahidi kusimamia vyema maadili, mihuli holela na wanahakikisha mihuli ya mawakili haughushiwi. Kama chama wameanzisha Kituo Suluhishi cha Migogoro ya ndani na nje ya nchi ili kupunguza msongamano wa kesi Mahakamani.

Aliwataka mawakili wapya kusimamia haki za wateja bila kupendelea wala kuogopa.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof.  Ibrahim Hamis Juma akitoa hotuba wakati wa mahafali ya kuwakubali na kuwapokea mawakili wapya katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo tarehe mosi Desemba, 2023,

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof.  Ibrahim Hamis Juma (wa nne kutoka kushoto) akiwa na jopo la Majaji akipokea heshima kutoka kwa mawakili wapya aliowakubali na kuwapokea kuingia kwenye orodha ya daftari la mawakili

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa tamko rasmi kwa mamlaka niliyopewa na Sheria ya mwakili sura ya 341 Toledo la 2019, kifungu cha 8(3) nina tamka kwamba wale wote ambao majina yao yamesomwa hapa wamekubaliwa kuwa mawakili na wamerodheshwa rasmi kwenye orodha ya mawakili

Jopo la Mwasheria Mkuu wa Serikali likipokea heshima kutoka kwa mawakili wapya aliokubaliwa na kuwapokelewa kuingia kwenye orodha ya daftari la mawakili.

Jopo la Balaza la Shule ya Sheria likipokea heshima kutoka kwa mawakili wapya aliokubaliwa na kuwapokelewa kuingia kwenye orodha ya daftari la mawakili.

Sehemu ya mawakili wapya wakila kiapo cha maadili mara baada ya kukubali na kupokelewa 


Mwanasheria Mkuu wa serikali Mhe. Dkt Eliezer Mbuki Feleshi akitoa hotuba wakati wa hafla ya kuwakubali na kuwapokea mawakili wapya

Sehemu ya mawakili wapya wakitoa heshima mara baada ya kukubaliwa na kupokelewa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani).


Sehemu ya mawakili wapya wakitoa heshima mara baada ya kukubaliwa na kupokelewa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani).


Sehemu ya mawakili wapya wakipokea maelekezo kutoka kwa kaimu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Projustus Kahyoza mara baada ya kukubaliwa na kupokelewa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani).

Sehemu ya mawakili wapya wakipokea maelekezo kutoka kwa kaimu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Projustus Kahyoza mara baada ya kukubaliwa na kupokelewa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani).

Sehemu ya wazazi, walezi na wananchi waliohudhuria hafla hiyo ya kuwakubali na kuwapokea mawakili wapya


Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria hafla hiyo ya kuwakubali na kuwapokea mawakili wapya.


Sehemu ya Majaji wastaafu wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria hafla hiyo ya kuwakubali na kuwapokea mawakili wapya.

Mwanasheria Mkuu wa serikali Mhe. Dkt Eliezer Mbuki Feleshi (kulia) na Wakili Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Boniphace Luhende (kushoto) wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani)

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na jopo la Majaji wakiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya mawakili walioingia rasmi kwenye orodha ya daftari la mawakili mara baada ya kuskubali na kupokelewa.

Picha na Innocent Kansha - Mahakama



MKANDARASI UJENZI WA JENGO LA 'IJC' SIMIYU AKABIDHIWA ENEO LA MRADI

  • Ujenzi kuanza tarehe Mosi Desemba, 2023

Na Naumi Shekilindi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu

Makabidhiano ya eneo kwa ajili ya kuanza kwa Mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Mkoa wa Simiyu yamefanyika huku yakishuhudiwa na Wawakilishi kutoka Makao Makuu ya Mahakama na Viongozi wa Mahakama mkoani Simiyu huku utekelezaji wake ukitarajiwa kuanza rasmi leo tarehe 01 Desemba, 2023.

Makabidhiano hayo yalifanyika tarehe 27 Novemba, 2023 huku yakishuhudiwa na Mhandisi Peter Mrosso, ‘QS’ Deogratius Lukansola, Mtendaji Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Bw. Gasto Kanyairita, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Mhe. Martha Mahumbuga, Mhandisi Mshauri (Consultant) Bw. Humphrey Massawe, Mkandarasi, Bw. Riziki Nkona pamoja na timu yake. 

Mwenyekiti wa kikao hicho cha makabidhiano, Mhandisi Mshauri Humphrey Massawe alielezea kuwa Mradi huo ni wa muda wa miezi tisa (9) na utaanza rasmi tarehe 01 Desemba, 2023 na unatarajiwa kukamilika tarehe 31 Agosti, 2024 na kukabidhiwa mnamo tarehe 01 Septemba, 2024. 

Mhandisi Massawe aliongeza kuwa, “ikumbukwe kuwa, zile siku 14 ambazo Mkandarasi anatakiwa kupewa kabla ya kuanza ujenzi zitakua ndani ya miezi hiyo tisa (9) kutokana na muda wa Mradi kuwa mfupi.” 

Mhandisi Massawe alisisitiza mambo mbalimbali kwa Mkandarasi wa Mradi kwamba, endapo Mkandarasi atahusisha Kampuni nyingine kufanya baadhi ya kazi basi atatakiwa kuleta taarifa (profile) za Kampuni hiyo kwa ajili ya upekuzi na kujiridhisha. 

Pia alisisitiza jinsi ya kuratibu uzalishaji na utupaji taka; kwamba lazima waainishe aina ya taka wanazozalisha na wapi wanatupa ili kuepuka madhara kwa watu wanaoishi au kuzunguka eneo hilo.

Mwenyekiti wa kikao alimuelekeza Mkandarasi kujisajili Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Halmashauri- Idara ya Zimamoto kabla hawajaanza shughuli zao za ujenzi.

Mhandisi Mshauri na Mkandarasi walikubaliana kufanya kazi usiku na mchana ili kukidhi Mradi kwa muda waliopewa na Mahakama, pia wamekubaliana kuwepo kwa vikao vya kila mwezi ambavyo vitahusisha wadau  wote wa Mradi  na vikao vya ‘technical’ ambavyo vitakuwa vinafanyika mara kwa mara kwa ajili ya kuwepo ufanisi wa kazi.

Aidha, Mwenyekiti alihitimisha kwa kumuasa Mkandarasi pamoja na timu yake kuzingatia ubora (quality control) katika hatua zote za ujenzi.

Naye, Afisa Mazingira kutoka Makao Makuu ya Mahakama, Bw. Castory Kyula alisisitiza  Wakandarasi juu ya utunzaji wa mazingira na uthibiti wa kelele na vumbi katika kipindi chote cha utekelezaji wa Mradi.

Kwa upande wake, Mtendaji Mahakama Mkoa Simiyu Bw. Gasto Kanyairita aliahidi kuwapa ushirikiano wakandarasi na kufanya mawasiliano na taasisi zote zinazo husika kutoa vibali ndani ya Mkoa wa Simiyu.


Makabidhiano ya mkataba kwa ajili ya ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Simiyu kati ya Mkandarasi, Bw. Riziki Nkona na Mtendaji Mahakama Mkoa Simiyu, Bw. Gasto Kanyairita. Makabidhiano ya 'site' hiyo yalifanyika tarehe 27 Novemba, 2023.
Picha ya pamoja na timu nzima inayohusika na ujenzi wa IJC wakati wa makabidhiano ya cheti baada ya kukabidhiana site.

Wajumbe wakimsikiliza Mwenyekiti wakati wa  kikao cha makabidhiano, Mhandisi Mshauri Humphrey Massawe kabla ya  makabidhiano ya eneo 'site' litakapojengwa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Simiyu.

(Habari hii imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)


WATUMISHI MAHAKAMA MKOA WA SINGIDA WASISITIZWA UHIFADHI NA UTUNZAJI WA MAZINGIRA

Na Eva Leshange- Mahakama, Singida

 Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo amewasisitiza watumishi wa Mahakama mkoani Singida kuyatunza vema mazingira yanayowazunguka kwa faida yao na wananchi wanaopata huduma.

Mhe. Dkt. Masabo aliyasema hayo hivi karibuni katika ziara yake ya ukaguzi wa shughuli za Mahakama katika Wilaya ya Manyoni ambapo aliwaambia watumishi hao kuhakikisha wanatunza vizuri bustani na kupanda miti katika maeneo ya Mahakama.

“Nimefurahi na kuvutiwa na ubunifu wa utunzaji wa mazingira wilayani Manyoni hasa kwa kila mtumishi kupewa mti wa kuutunza ni jambo jema na la kulichukua na ndio ukawa mkakati wa Kanda kwa ujumla,” alisema Jaji Masabo.

Aidha, aliwapongeza Mahakimu pamoja na watumishi kwa kazi nzuri wanayofanya hasa katika usikilizwaji wa mashauri, amewataka kuongeza kasi zaidi na kuhakikisha hakuna kabisa mashauri ya mlundikano (Backlog Free).

Aliwapongeza pia Mahakimu kwa kutumia ya Mfumo mpya wa Kieletroniki wa usajili na usikilizaji wa mashauri Mahakamani (Advanced e-Case Management System) na kuwasihi kuwa, changamoto wanazokutana nazo zinafanyiwa kazi na zitaisha wawe na subira kwani ni kipindi cha mpito.

Katika ukaguzi huo Dkt. Masabo alitoa barua za pongezi kwa Wilaya ya Singida na Manyoni kwa kuweza kupata hati nyingi za viwanja vya Mahakama, ambapo Wilaya ya Singida katika Kata 49 wamefanikiwa kupata hati 38, Wilaya ya Manyoni katika Kata 17 wamepata hati 16.

Kufuatia hatua hiyo ya upatikanaji wa viwanja, Jaji Mfawidhi huyo alielekeza kupandwa miti katika viwanja hivyo ili kulinda mipaka.

Katika ziara yake ya siku mbili (2) Mkoani Singida, alipata pia fursa ya kutembelea Magereza ya Wilaya Singida, Iramba na Manyoni na kusikiliza kero za wafungwa na mahabusu. Aidha, aliwapongeza wadau wote wa haki jinai kwa kazi nzuri wanayofanya kwani hali ya magereza ilionekana ni nzuri hakuna msongamano na changamoto zote zilizoibuliwa walizitolea majibu.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo (aliyeketi katikati) akizungumza jambo wakati wa ziara yake ya ukaguzi aliyofanya mkoani Singida.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Mhe.Allu Omary Nzowa akisoma taarifa ya utekelezaji  mnamo mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo aliyeketi mbele (kushoto) pembeni yake ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Sylivia Lushasi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Manyoni, Mhe. Alisile Mwankejela akisoma taarifa mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo alipowasili kituoni hapo kwa ajili ya ziara ya ukaguzi mnamo tarehe 30 Novemba, 2023.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida wakimsikiliza Jaji Mfawidhi (hayupo katika picha) alipofanya ziara ya ukaguzi kituoni hapo.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Manyoni wakimsikiliza Mhe. Dkt. Masabo (hayupo katika picha) alipofanya ziara ya ukaguzi wilayani hapo.

(Habari hii imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)