Jumatatu, 20 Machi 2023

UADILIFU USHUGULIKIWE KWENYE MAKOSA YA UBAKAJI: JAJI NGWEMBE

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe amesisitiza suala la uadilifu katika jamii hasa katika kipindi hiki ambacho kumekuwa na wimbi kubwa la tuhuma za ubakaji. 

Mhe. Ngwembe ameyasema hayo leo tarehe 20 Machi, 2023 wakati akifungua mafunzo ya wadau wa Haki Jinai awamu ya nne ikiwa ni muendelezo wa mafunzo hayo ambayo yalifunguliwa tarehe 6 Machi, 2023. Amewasihi wadau hao kuwa waadilifu na kufanya kazi kwa weledi kwa mujibu wa taaluma zao, huku akiinyooshea kidole sekta ya upelelezi. 

Kauli hiyo imekuja mara baada ya kuwa na wimbi kubwa la tuhuma za ubakaji katika jamii ambapo Mhe. Ngwembe amesema mara nyingi kesi hizo zinatokana na jamii kutokuwa waadilifu, ikiwemo baadhi yao kuzitumia kama nyenzo ya kukomoana kwa kuwa hupelekea mtu kufungwa muda mrefu gerezani. 

Aidha, Jaji Ngwembe alisema kuwa upelelezi yakinifu wa kisayansi ukitumika utarahisisha kuwatambua waharifu wa ukweli katika kesi za ubakaji ili wawajibishwe na wasio waharifu waachiliwe kuendelea na majukumu yao. 

Pia alisisitiza wanaopelekewa majukumu ya kupeleleza kesi hizo kuwa waadilifu na kufanya kazi kwa weledi kwakuwa wakishindwa kufanya hivyo huwa chanzo cha lawama kwa Mahakama kuwa imeshindwa kutenda haki. “Sasa hivi matukio ya ubakaji yamekuwa kama wimbo katika jamii, niwaambie wazi kuwa vitendo hivi vya kinyama havikubaliki,” aliongeza. 

Kuhusu upande wa upelelezi, Mhe. Ngwembe alisisitiza upelelezi wa kisayansi utumike kuutambua uhalifu kwani sasa ni karne ya 21 ambayo masuala ya tekinolojia yameshika hatamu, hivyo ni vyema wote wakahama kutoka utaratibu wa kizamani ambao umepitwa na wakati na kujikita katika tekinolojia mpya ili iwasaidie kupambanua uharifu. 

“Msitumie utaratibu wa zamani, tumieni upelelezi wa kisayansi kutambua uharifu na Sheria ya Ushahidi wa Kielektroniki (Electronic Evidence Act) tayari imepitishwa na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania itumike,” alisisitiza Mhe. Ngwembe. 

Sambamba na hilo, Mhe. Ngwembe aliwataka washiriki kuzingatia mafunzo yatakayotolewa na wawezeshaji na kuyatumia kuunda fikra mpya zitakazoleta mageuzi katika majukumu yao. 

Awali, akimkaribisha Jaji Mfawidhi kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe, Arnold Kirekiano alitoa takwimu kuwa wameweza kuwafikia wadau wa Haki Jinai kutoka taasisi mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (50), Jeshi la Polisi (100), TAKUKURU (40), TAWA (35), Mamlaka ya Kupambana na Dawa za Kulevya (16) na washiriki 9 kutoka kitengo cha kupambana na fedha haramu. 

Washiriki wa mafunzo hayo watapata nafasi ya kubadilishana uzoefu na kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu haki jinai, lengo likiwa kuongeza ufanisi katika sekta ya utoaji haki. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akifungua mafunzo ya awamu ya nne ya wadau wa Haki Jinai. 
Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Haki Jinai awamu ya nne (juu na chini) wakifuatilia hotuba ya ufunguzi toka kwa mgeni rasmi ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe ( hayupo pichani). 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamona na sehemu ya washiriki wa mafunzo (juu na picha mbili chini). Wengine waliokaa ni Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama kuu ya Tanzania, Mhe Arnold Kirekiano (kushoto) na Kaimu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro, Mhe. Livin Lyakinana (kulia).



Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamona na sehemu ya wawezeshaji wa mafunzo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam).

KUNDI LA KUMI LAANZA MAFUNZO YA UDALALI NA USAMBAZAJI NYARAKA ZA MAHAKAMA

 

·       Washiriki kujengewa weledi na umahiri katika eneo hilo

·       Watakaofaulu kupata cheti cha kuwawezesha kuomba kazi hiyo

Na. Innocent Kansha - Mahakama

Naibu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Bw. Goodluck Chuwa leo tarehe 20 Machi, 2023 amefungua mafunzo kwa watu 27 wenye nia ya kufanya kazi ya udalali na usambaza nyaraka za Mahakama, washiriki wa mafunzo hayo ni kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania.

Akifungua mafunzo hayo ya kundi la 10 toka kuanzishwa kwake yanayofanyika katika Taasisi ya Mafunzo ya Sheria kwa Vitendo jijini Dar es Salaam, yanayoendeshwa na IJA kwa muda wa wiki mbili. Bw. Chuwa amesema, mafunzo yanayotolewa ni sehemu ya maboresho ya Mahakama yenye lengo la kujenga weledi na umahiri kwa wadau hao na hivyo kupunguza malalamiko na kujenga taswira nzuri ya Mahakama mbele ya umma.

“Msingi na msukumo wa uendeshaji wa mafunzo haya unatokana na malalamiko ya wadau wa Mahakama yanayoelekezwa moja kwa moja kwa madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama dhidi ya ukosefu wa maadili na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao”, alisema Chuwa

Aidha, Bw. Chuwa alisema, washiriki watakapomaliza mafunzo hayo na kuhitimu kisha kusajiliwa na Mahakama kutekeleza majukumu ya udalali na usambazaji nyaraka za Mahakama wataisaidia Mahakama kutenda haki kwani nafasi hizo watakazozitumikia zitaongeza imani ya wananchi kwa Mahakama.

Niwasihi kuwa baada ya kupata mafunzo haya, kufuzu mitihani yenu mkafanye kazi mkitanguliza uadilifu kwa kuzingatia kanuni na maadili mliyofundishwa ili kukidhi kiu ya Mahakama ya kuwahudumia wananchi kwa kutoa haki kupitia wadau wengine ikiwemo madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama”, Chuwa alisisitiza.

Akifafanua moja ya malengo ya kuazisha progamu hiyo, mgeni rasmi huyo alisema, kuanzishwa kwa mafunzo ni mojawapo ya zao la maboresho makubwa yanayoendelea katika mhimili wa Mahakama wenye lengo la kuondoa malalamiko mengi yaliyokuwepo kutoka kwa wananchi na moja ya eneo lenye kulalamikiwa ni ukosefu wa uadilifu wakati wa utekelezaji wa majukumu ya udalali na usambazaji wa nyaraka za Mahakama, kwa kufanya hivyo kutawawezesha Madalali na Wasambaza nyaraka za Mahakama kufanya kazi kwa uadilifu na kufuata kanuni zilizopo.

Bw. Chuwa aliongeza kuwa, ni vizuri kutambua kuwa uamuzi wa kuanzisha mafunzo hayo ya wenye nia ya kufanya kazi ya udalali na usambaza nyaraka za Mahakama ni kutokana na changamoto ya muda mrefu ya  upatikanaji wa Madalali na Wasambaza nyaraka za Mahakama wenye sifa na hivyo Mahakama kupitia Mpango Mkakati wake wa kwanza wa mwaka 2015/2016 – 2019/2020 na Mradi wa Uboreshaji wa Mahakama kupitia mradi wa huduma zinazomlenga mwananchi, iliandaa kanuni ziitwazo Kanuni za Uteuzi, Gharama, Malipo na Nidhamu za Madalali na Wasambaza Nyaraka za Mahakama kwa Tangazo la Serikali Namba 363 la 2017 (The Court Brokers and Process Servers (Appointment, Remuneration and Disciplinary) Rules, GN. 363 of 2017).

Kanuni hizo zilitoa maelekezo kwamba, madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama wanapaswa kusoma kozi za muda mfupi ambazo itawapa weledi katika kufanya kazi ya udalali na usambaza nyaraka kwa ufanisi.

Chuwa alifafanuwa kwa washiriki hao kuwa, watajifunza mambo mengi sana katika kipindi hicho cha wiki mbili, yakiwemo masuala ya muundo wa Mahakama ya Tanzania, utaratibu wa mashauri ya madai, usambazaji wa nyaraka za mahakama, utekelezaji wa tuzo na amri za Mahakama na maadili ya madalali na wasambaza nyaraka za mahakama na nyinginezo.

Ninawasihi watumieni wawezeshaji wenu ambao ni Jaji wa Mahakama ya Tanzania, Naibu Wasajili na Mahakimu ambao  ni wabobevu, wazoefu na mahiri katika eneo la sheria na taratibu za udalali na usambaza nyaraka za Mahakama kuibua mijadala huru itakayowasaidia kuongeza ujuzi na Msisite kuchangia uzoefu wenu kwa lengo la kuongezeana maarifa”, Chuwa aliwashauri washiriki hao

Washiriki hao, watafundishwa na wataalamu wabobezi na mwisho wa siku watapewa mtihani na wale tu watakaofaulu ndiyo watapewa cheti kitakachowawezesha kuomba kazi hiyo Mahakama Kuu ya Tanzania.

Kutokana na msingi huo, kundi hili la watu wenye nia ya kufanaya kazi ya udalali na usambazaji wa nyaraka za Mahakama ni la kumi (10) tangia mafunzo ya namna hiyo yazinduliwe na hadi kufikia sasa jumla ya washiriki 262 wamedahiliwa kwa mafunzo hayo na washiriki 141 wamefaulu na kufuzu kigezo cha kuomba kazi ya udalali na au usambaza nyaraka za Mahakama.

MAHAKAMA SPORTS YANG’ARA KWENYE BONANZA

·Yaizabua TEMESA bao nne, yakwea nafasi ya kwanza

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu imeng’ara katika Bonanza lililoshirikisha timu tatu, zikiwemo Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) na Wakili FC baada ya kuibuka vinara kwa kuzoa pointi nne na mabao matano.

Katika Bonaza hilo lililofanyika kwenye Viwanja vya Shule ya Sheria kwa Vitendo (Law School) Dar es Salaam, timu ya Wakili FC ilishika nafasi ya pili baada ya kupata pointi nne na magori manne, huku TEMESA ikiburuza mkia kwa kupata pointi moja na magori mawili.

Kulikuwepo na mechi tatu zilizoshirikisha timu hizo ambapo mechi ya kwanza ilikuwa kati ya Wakili FC na TEMESA na Wakili FC kuibuka washindi kwa mabao 3:1. Mechi ya pili ilikuwa kati ya Mahakama na Wakili FC ambapo timu hizo zilitoka suluhu kwa kufungana 1:1, huku goli la Mahakama likifungwa na Robert Tende.

Mechi ya tatu ilikuwa kati ya TEMESA na Mahakama ambapo Mahakama iliwazabua TEMESA bao 4:1, magoli ya Mahakama yakifungwa na Kariho Mrisho (2), goli la tatu likipachikwa na Martin Mpanduzi, kabla ya Chilemba Hassan kutikisa nyavu kwa kufunga goli la nne.

Mbali na kutangazwa mabingwa katika Bonanza hilo, Mahakama Sports ilizawadiwa kombe na kutoa mchezaji bora, ambaye ni Kariho Mrisho, Wakili FC nayo ilipata zawadi ya kombe la mshindi wa pili, huku TEMESA ikiambulia kutangazwa kama timu yenye nidhamu.

Akizungumza baadaye, Katibu wa Mahakama Sports Taifa Donald Tende amesema Bonanza hilo liliandaliwa na viongozi wawakilishi wa timu ya Mahakama, Kanda ya Dar es Salaam, lengo likiwa kuboresha afya na kuimarisha ujirani mwema, hatua ambayo ni utekelezaji wa nguzo ya tatu ya Mpango Mkakati wa Mahakama katika kushirikiana na wadau.

Tende, kwa niaba ya uongozi wa Kanda ya Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Jamal Mkumba na Katibu Chilemba Hassan, alisema pia kuwa wamelichukulia Bonanza hilo kama maandalizi ya Mahakama Sports katika ushiriki na mashindano ya Mei Mosi yanayotarajiwa kuanza tarehe 14 Aprili, 2023 mkoani Morogoro.

“Kila Mkoa una uongozi wakilishi ambao uliteuliwa na viongozi wa Mahakama Sports Taifa ili kusaidiana katika kusimamia michezo na kufanya mazoezi ili kuboresha afya mahala pakazi. Kwa hiyo kila Mkoa wamekuwa wakifanya mazoezi na kushiriki mabonanza mbalimbali ya ndani na nje,” amesema.

Sehemu ya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu ikishangilia baada ya kukabidhiwa kombe.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu kabla ya mchezo.

Mwalimu wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu , Spear Mbwembe (juu) akiongea na wachezaji (chini) wakati wa mapumziko. 

Mgeni Rasmi katika Bonanza hilo Rajab Mwaliko (juu) akizungumza na wachezaji (chini).



Timu ya TEMESA.
Timu ya Mahakama Sports.

Timu ya Wakili FC.

Orodha ya Makombe yaliyokabidhiwa kwa washindi mbalimbali.
Mchezaji bora wa Bonanza Kariho Mrisho akikabidhiwa kombe lake.


Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende (kushoto) akimpongeza Nahodha wa Timu ya Mpira wa Miguu, Gisbert Chentro, baada ya kuibuka mabingwa wa Bonanza hili.

Alhamisi, 16 Machi 2023

KAMATI KATIBA NA SHERIA YASTAAJABISHWA NA UZURI MAJENGO YA MAHAKAMA, YASHAURI YATUNZWE

Na Mary Gwera, Mahakama-Mwanza

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imeitaka Mahakama ya Tanzania kuwa na kifungu maalum kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya majengo yake ili yaweze kudumu kwa muda mrefu na kutumika hata kwa vizazi vijavyo.

Hayo yamebainishwa leo tarehe 16 Machi, 2023 wakati Wajumbe wa Kamati hiyo walipotembelea na kukagua jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC)-Mwanza lililopo Wilaya ya Ilemela Kata ya Buswelu jijini Mwanza.

Akizungumza mara baada ya kukagua jengo hilo, Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Rashid Abdallah Shangazi (Mb) amesema kuwa Mahakama imepiga hatua kubwa katika uboreshaji wa miundombinu ya majengo yake hivyo ni muhimu kuyatunza vyema na kushauri kuwa, Mhimili huo unatakiwa kutengeneza kifungu maalum ambacho kitatengewa fedha zitakazowezesha kufanya ukarabati wa majengo ili yaweze kudumu kwa muda mrefu.

“Napenda kuipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuboresha miundombinu ya majengo, hatua ya ujenzi wa miundombinu ya majengo ya Mahakama ni hatua ya juu kwa nchi yetu, kwahiyo ni muhimu majengo hayo kuyatunza ili yaweze kudumu kwa muda mrefu, kuna majengo yaliyotumika enzi za ukoloni lakini yamedumu hadi sasa mfano; Ikulu ya Dar es Salaam, Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na kadhalika, hii ni dhahiri kuwa majengo hayo yametunzwa na kukarabatiwa mara kwa mara na hivyo kuendelea kutoa huduma mpaka sasa,” amesema.

 Kadhalika Mjumbe mwingine wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Ighondo Ramadhani (Mb) amesema kwamba, Tanzania imepiga hatua kubwa katika uimarishaji wa miundombinu na utoaji haki kwa ujumla, hivyo, ameishauri Mahakama kuutangazia umma kuhusu uboreshaji wa huduma mbalimbali unaoendelea kufanyika.

Kwa ujumla Wabunge hao wameridhishwa na jengo hilo na kukiri kuwa limezingatia haki za binadamu kwa makundi yote na kuipongeza Mahakama kwa kuboresha miundombinu.

Akizungumza kwenye kikao kilichofanyika mara baada ya ukaguzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Mwanza, naye Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro ameishukuru Kamati hiyo na Serikali kwa ujumla kupitia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha kuipatia fedha Mahakama za kuendelea na ujenzi na ukarabati wa majengo yake pamoja na kuipa Wizara yake fursa mbalimbali zenye lengo la kuboresha sekta ya sheria kwa ujumla.

“Napenda kuchukua fursa hii, kuishukuru Kamati na Serikali kwa ujumla., na nakiri kuwa, mchakato wa mabadiliko ya utoaji huduma ‘transformation’ mahakamani ni wa kasi kubwa sana, maboresho haya ya Mahakama si tu yanajulikana nchini bali pia hata kwa baadhi ya nchi za wenzetu wanaitaja Mahakama ya Tanzania kama Mahakama ya mfano na iliyopiga hatua katika kuboresha huduma zake ikiwa ni pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya majengo” ameeleza Mhe. Dkt. Ndumbaro.

Aidha, Waziri ameeleza kuwa, Mahakama inaendelea kusogeza huduma za utoaji haki karibu na wananchi huku akibainisha kuwa, kwa mwaka huu wa fedha, Mahakama imepanga kujenga Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJC) tisa vitakavyojengwa katika mikoa ya Njombe, Simiyu, Ruvuma, Geita, Katavi, Manyara, Singida, Songwe na Lindi.

Akihitimisha kikao hicho, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo ameipongeza Mahakama Kanda ya Mwanza kwa jengo zuri na kumtaka Waziri kuwasilisha randama ya bajeti ya Wizara na Mahakama kwa ajili ya maandalizi ya bajeti ya mwaka ujao wa fedha.

Awali, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha akitoa taarifa ya jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Mwanza, kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, amesema Mradi huo ulianza tarehe 24 Januari 2020 na kumalizika 28 February 2022 na umetumia kiasi cha fedha za Kitanzania bilioni 8,561,314,505.91 ambapo mpaka sasa Mkandarasi ameshalipwa shilingi 8,133,248,779.75.

“Jengo hili ni miongoni mwa majengo sita (6) yaliyozinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tarehe 6 Oktoba, 2021 na dhana ya Vituo jumuishi inalenga kusogeza huduma karibu na wananchi, kusogeza huduma za Mahakama karibu na wananchi, kurahisisha na kuharakisha upatikanaji wa huduma za mahakama kwa kuweka huduma za ngazi zote katika jengo moja,” ameeleza Bw. Magacha.

Mtendaji huyo ameongeza kuwa upatikanaji wa Vituo hivyo, umerahisisha pia uendeshaji wa shughuli za Kimahakama kwa kuwa wadau wote muhimu katika mnyororo wa utoaji haki wanapatikana katika jengo moja na vilevile kupunguza gharama kwa wateja wa Mahakama.

Kamati hiyo imehitimisha ziara yake ya kukagua Miradi ya Mahakama, ambapo siku ya kwanza ya ziara yao ilifanyika tarehe 14 Machi, 2023 kwa kukagua Mradi wa Ukarabati na Upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha ( wa pili kulia) akiwaonesha Wajume wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria sehemu ya Mapokezi ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza wakati walipotembelea Kituo hicho leo tarehe 16 Machi, 2023. Kulia kwa Bw. Magacha ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo na wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Mhe. Chiganga Tengwa.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha (kulia) akieleza namna Mahakama ya Watoto inavyofanya kazi, Mahakama hiyo ipo ndani ya jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Mwanza. Kulia kwake ni Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Mhe. Chiganga Tengwa akifuatiwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro. Wajumbe wa Kamati hiyo wametembelea katika Kituo hicho leo tarehe 16 Machi, 2023.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha akieleza kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria namna Mahakama ya wazi zilivyotengenezwa katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akizungumza jambo wakati wa kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ilipotembelea jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza leo tarehe 16 Machi, 2023.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Bw. Florent Laurent Kyombo akizungumza jambo wakati wa kikao cha Kamati hiyo kilichofanyika mara baada ya ukaguzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Mwanza.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw.Leonard Magacha (aliyesimama katikati) akiwasilisha mada juu ya jengo la kituo Jumuishi cha Utoaji Haki 'IJC' Mwanza na faida zake.

Makamu mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Florent Laurent Kyombo akieleza jambo wakati wa kikao cha Kamati hiyo iliyotembelea jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Mwanza.

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ambaye pia ni Mbunge wa Mlalo, Mhe. Rashid Abdallah Shangazi akichangia jambo mara baada wasilisho la Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ambaye pia  ni Mbunge wa Jimbo la Nyangh'wale, Mhe. Hussein Nassor Amar akichangia jambo wakati Kamati hiyo ilipotembelea jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Mwanza.

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ambaye pia ni Mbunge anayewakilisha Wafanyakazi, Mhe. Dkt .Alice Kaijage akichangia jambo wakati kamati hiyo ilipofanya kikao mara baada ya kukagua jengo la 'IJC' Mwanza.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (aliyesimama katikati) akiwa na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria  na baadhi ya Watumishi wa Mahakama. Wa tatu kushoto aliyesimama mbele ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Bw. Florent Laurent Kyombo.

(Picha na Stephen Kapiga-Mahakama Kuu-Mwanza)

 

 

 


KAMATI YA BUNGE YASHAURI UJENZI MAJENGO YA MAHAKAMA UZINGATIE VYUMBA VYA MAMA WANAONYONYESHA

 Na Mwandishi wetu, Mahakama-Mwanza

Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria imeshauri Mahakama ya Tanzania kuendelea kutenga chumba cha mama wanaonyonyesha katika miradi ya ujenzi wa miundombinu inayoendelea katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 16 Machi, 2023 mjini Mwanza na mmoja wa Wajumbe wa Kamati hiyo Mhe. Dkt. Alice Kaijage wakati wa ziara ya ukaguzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Mwanza.

Amesema mfano walioona leo katika Jengo la Kituo Jumuishi cha UtoajiHhaki cha Mwanza ni vema ramani hiyo ikawa sehemu ya michoro ya Mahakama zote mpya zitakazojengwa hapa nchini kama hatua ya kutambua haki ya mama kunyonyesha mwanae katika mazingira rafiki.

“Niwapongezeni kwa kazi nzuri ya ujenzi wa jengo la kisasa ambalo limethamini wanawake wanaonyonyesha kwa kuwawekea ya  faragha…nashauri ramani za majengo ya Mahakama ambazo mnatarajia kuyajenga ziwe na sehemu ya kunyonyoshea kama tuliyoiona katika jengo hili” amesisitiza.

Katika hatua nyingine Mjumbe wa Kamati hiyo Mhe. Rashid Shangazi aliishauri Mahakama na jamii kuhakikisha wanaitunza ili iweze kusaidia katika utoaji haki kwa muda mrefu.

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ambaye pia ni Mbunge anayewakilisha wafanyakazi, Mhe. Dkt. Alice Kaijage akichangia jambo wakati Kamati hiyo ilipotembelea jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza. Mhe. Dkt. ameonesha kufurahishwa na uwepo wa chumba maalum cha kunyonyeshea na kushauri majengo mengine ya Mahakama yatakayojengwa yawe na chumba hicho.


JAJI NGWEMBE AWATAKA MADALALI, WASAMBAZA NYARAKA WA MAHAKAMA KUFUATA SHERIA

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe amewataka Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kufuata kanuni na taratibu zilizowekwa wakati wa utekelezaji wa majukumu yao. 

Mhe. Ngwembe alitoa rai hiyo jana tarehe 15 Machi, 2023 alipokutana na wadau hao muhimu wa Mahakama katika Kanda ya Morogoro ili kuzungumzia masuala mbalimbali ya kiutendaji. 

Jaji Mfawidhi huyo aliwasisitiza kutumia lugha nzuri kwa wateja na wananchi kwa ujumla muda wote wanapokuwa katika maeneo ya kazi, kwani kwa kufanya hivyo kutamaliza malalamiko. 

“Fanyeni kazi kwa mujibu wa taaluma zenu ili kuondoa malalamiko wakati wa utekelezaji wa amri za Mahakama,” alisema Jaji Ngwembe na kuonya tabia ya baadhi ya Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama kutumia watu wengine ambao hawajasajiliwa na Mahakama kufanya shughuli hizo. 

Amesema hatua zitachukuliwa kwa Dalali ambaye atakiuka utaratibu huo, ikiwemo kufutiwa leseni yake kwani jambo hilo ni kinyume cha kanuni za Madalali, kwa kuzingatia watu hao hawana uelewa wa kutosha kwani hawajapatiwa mafunzo ya udalali. 

Sambamba na hilo, Mhe. Ngwembe alionya kama kuna Dalali anajihusisha na vitendo vya kutapeli wateja, maarufu kwa jina na “Kishoka,” kuacha mara moja tabia hizo na kusimamia majukumu yake kwa mujibu wa sheria na si vinginevyo. 

Baada ya kikao hicho, Jaji Mfawidhi huyo aliwaomba Madalali na Wasambaza Nyaraka hao kwenda katika eneo linalotumika kutolea elimu ya Sheria Mbashara ndani ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kwa ajili ya kujitambulisha kwa wananchi na kutoa elimu kuhusu kazi na majukumu yao.

Hatua hiyo ilijitokeza kufuatia baadhi ya wateja kutowatambua Madalali hao wanapotekeleza majukumu yao, ikiwemo kusimamia utekelezaji wa hukumu za Mahakama. 

Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama wapo kwa mujibu wa Kanuni za Madalali na Wasambaza Nyaraka za Mahakama za Mwaka 2017 ambao majukumu yao makubwa ni kutekeleza hukumu na amri baada ya Mahakama kusikiliza mashauri na kutoa uamuzi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe aliyeendesha kikao cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama.
Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro kilipofanyikia kikao cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (aliyekaa wa kwanza kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa kikao cha Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama. Kushoto kwa Jaji Ngwembe ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe Augustina Mmbando.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam). 

Jumatano, 15 Machi 2023

MSAJILI MKUU ATEMBELEA MAHAKAMA YA MWANZO BAGAMOYO

Na Mwandishi wetu-Mahakama ya Tanzania

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma amewahimiza watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Bagamoyo kuzingatia na kuyapa kipaumbele maelekezo ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika shughuli za kimahakaka kama inavyosisitizwa mara kwa mara na viongozi wa Mahakama.

Mhe. Chuma alitoa wito huo jana tarehe 14 Machi, 2023 alipofanya ziara ya siku moja katika Mahakama hiyo inayoketi Msoga-Lugoba kwa lengo la kujionea namna shughuli za Mahakama zinavyotekelezwa.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama hiyo, Msajili Mkuu aliwataka kuwahudumia wananchi kwa viwango vya juu na kuzingatia utoaji wa huduma bora kwa mteja, kwa maana ya customer care.

Mhe. Chuma aliwahimiza kuimarisha tunu ya upendo kati ya mtumishi na mtumishi na hatimaye kuwa na utumishi wenye tija na kufanya kazi kwa weledi, kuzingatia maadili ya kazi na kuwa na uwezo wa kufanya kazi zaidi ya moja.

Kadhalika, Msajili Mkuu huyo alihimiza wasimamizi wa mirathi kufunga mirathi kwa mujibu wa sharia.

Aidha, Mhe. Chuma alielekeza kuwekwa kwa tangazo karibu na barabara kuu linatotambulisha Mahakama ya Msoga-Lugoba ilipo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma akikagua maeneo ya Mahakama ya Mwanzo Bagamoyo katika ziara aliyoifanya jana tarehe 14 Machi, 2023.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma akisaini kitabu cha wageni.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma (katikati katika picha ya juu na chini) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama hiyo, akiwemo Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bagamoyo, Mhe. Sameera Suleiman (wa pili kushoto).


Jumanne, 14 Machi 2023

KAMATI YA BUNGE KATIBA NA SHERIA YAIMWAGIA SIFA MAHAKAMA UBORESHAJI MIUNDOMBINU

-Yashauri huduma zitolewazo ziendane na uzuri wa majengo

Na Tiganya Vincent, Mahakama -Tabora

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria leo tarehe 14 Machi, 2023 imekagua Mradi wa Ukarabati na Upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora na kuridhishwa kwa kazi iliyofanyika na kuipongeza Mahakama kwa utekelezaji mzuri wa Miradi mbalimbali ya uboreshaji wa miundombinu ya majengo yake.

Akizungumza mara baada ya ziara ya siku moja ya ukaguzi wa Utekelezaji wa Mradi wa Ukarabati na Upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe.  Florent Laurent Kyombo amesema kuwa Mahakama ni moja ya Taasisi inayofanya vizuri katika miradi yake ya ujenzi na hivyo kuwasihi Watumishi wa Mhimili huo kutoa huduma zinazoendana na uzuri wa miundombinu hiyo.

"Kama Kamati tuna 'oversee' mambo mbalimbali yanayofanyika Serikalini, hivyo napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Mahakama ya Tanzania kwa uboreshaji wa huduma mbalimbali unaoendelea ikiwa ni pamoja na maboresho ya miundombinu ya majengo, kwakweli mnaupiga mwingi," amesema Mhe. Kyombo.

Mhe. Kyombo ameishukuru Serikali kwa kuendelea kutoa fedha kwa Mahakama ya Tanzania kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu ya utoaji haki kwa wananchi.

Naye, Mbunge wa Jimbo la Kiteto ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati hiyo,  Mhe. Edward Ole Lekaita amesema ubora wa majengo ya Mahakama unaridhisha na kuongeza Mahakama imeitendea haki fedha waliyopewa na Serikali kwa ajili ya shughuli hiyo ya ukarabati.

Amesema uboreshaji na ukarabati wa Mahakama hiyo umewawezesha Maafisa wa Mahakama na Wadau wao kutekeleza majukumu yao ya utoaji wa haki kwa wananchi katika mazingira mazuri.

Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Khadija Shaaban almaarufu Keysha amesema Mahakama imeitendea haki fedha za ukarabati walizopatiwa na Serikali na kushauri kuweka 'Lift' maalum kwa ajili ya watu wenye mahitaji maalum.

Awali, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema Mradi huo umetumia kiasi cha fedha za Kitanzania bilioni 2.5 na ulianza kutekelezwa mwezi Juni mwaka 2021 na kukamilika Septemba, 2022.

Amesema kuwa, hadi sasa Mkandarasi ameshalipwa kiasi cha shilingi bilioni 1.5 ambayo ni sawa ya asilimia 61 na bado anadai milioni 900 ambazo wanaendelea kushughulikia.

Prof. Ole Gabriel, ameongeza kuwa, kukamilika kwa mradi huo kumesaidia kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora na kuahidi kuwa watahakikisha kuwa haki inapatikana kwa ubora.

Aidha Mtendaji huyo amewataka Wajumbe wa Kamati hiyo kuisaidia Mahakama kwa kuwaeleza wananchi kuhusu uboreshaji wa huduma mbalimbali za Mahakama unaoendelea ikiwemo matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wakati ufunguaji wa mashauri na usikilizaji wa mashauri.

Kamati hiyo inatarajia pia kutembelea jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC)-Mwanza tarehe 16 Machi, 2023.

Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwakaribisha Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria pindi walipotembelea Mradi wa Ukarabati na upanuzi wa Jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania-Kanda ya Tabora leo tarehe 14 Machi, 2023. Kulia ni Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe.  Florent Laurent Kyombo (Mb).

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha (kushoto) akiwaonesha Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria kibao cha uzinduzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora pamoja na kuelezea historia jengo hilo ambalo awali lilikuwa likitumika kama Ofisi ya Serikali za Mitaa.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha (kulia) akiwapitisha Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakati walipokuwa wakikagua Mradi wa Ukarabati na upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania-Kanda ya Tabora.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Amour Khamis akizungumza jambo na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo (hayupo katika picha) wakati Makamu Mwenyekiti huyo na baadhi ya Wajumbe alioambatana nao walipomtembelea Jaji Mfawidhi ofisini kwake Mahakama Kuu-Tabora.

Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza jambo alipokuwa ofisini kwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Tabora.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Paulina Gekul akizungumza jambo wakati yeye pamoja sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria walipokuwa ofisini kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Amour Khamis (hayupo katika picha).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Amour Khamis akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya ujumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, wa tatu kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe.  Florent Laurent Kyombo (Mb). Wa pili kulia ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Paulina Gekul, wa pili kushoto ni Mtendaji Mkuu-Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa tatu kushoto ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Rashid Abdallah Shangazi (Mb), wa kwanza kushoto ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Dkt. John Rogath Mboya na wa kwanza kulia ni Mtendaji-Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Bw. Ginaweda Nashon.

Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasilisha taarifa ya Ukarabati na Upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria walipotembelea Mradi huo mapema leo kwa ajili ya ukaguzi.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria, Watumishi wa Mahakama na wageni waalikwa wakifuatilia kwa umakini wasilisho lililokuwa likitolewa na Mtandaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha).

Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Kudumu ya Utawala, Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo (Mb) akizungumza jambo baada la wasilisho lililotolewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama. Mwenyekiti huyo amepongeza kazi nzuri ya ukarabati na upanuzi wa jengo wa Mahakama Kuu Tabora ulivyofanyika. Kulia ni Katibu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Bw. Frank Nkya.

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Edward Ole Lekaita (Mb), akipongeza kazi nzuri ya ukarabati na upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Tabora.

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe. Seleman Zedi akichangia jambo mara baada ya wasilisho lililotolewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.
Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Mahakama, Mkoa wa Tabora na Wajumbe wa Kamati hiyo. Wa pili kulia ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Paulina Gekul, wa pili kushoto ni Mtendaji Mkuu-Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa kwanza kushoto ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Dkt. John Rogath Mboya na wa kwanza kulia ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe. Rashid Abdallah Shangazi.
Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Mahakama, Watumishi wa Mahakama, Mkoa wa Tabora na Wajumbe wa Kamati hiyo. Wa pili kulia ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Paulina Gekul, wa pili kushoto ni Mtendaji Mkuu-Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa kwanza kushoto ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Dkt. John Rogath Mboya na wa kwanza kulia ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe. Rashid Abdallah Shangazi.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama-Tabora)