Ijumaa, 27 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAFANIKISHA MAGEUZI MAKUBWA

  • Malengo yote ya Mradi wa Maboresho wa Mahakama yamefikiwa kwa asilimia 100

Na JAMES BUSANYA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuimarisha utendaji na upatikanaji wa huduma za haki kwa wananchi, ikifikia kiwango cha juu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Mahakama katika mageuzi ya kisheria.

Hayo yamesemwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho (JDU), Mhe. Dkt. Angelo Rumisha, tarehe 25 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, wakati anawasilisha taarifa ya maboresho kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa malengo yote 12 ya maendeleo ya mradi (PDO) yamefikiwa au kuzidi matarajio, huku kiwango cha kuridhika kwa wananchi kikiongezeka kwa asilimia kubwa, ukilinganisha na awali, jambo ambalo ni ishara kubwa ya mafanikio katika kuboresha ufanisi, uwazi na upatikanaji wa haki katika ngazi zote za Mahakama nchini.

Katika kuimarisha miundombinu na upatikanaji wa huduma, Jaji Rumisha alieleza kuwa Mradi wa Maboresho ya Mahakama umejikita katika kuunda miundombinu ya kisasa kwa kujenga Mahakama za Mwanzo 94 na Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJCs) 18.

Hatua hizi zimeleta mapinduzi makubwa kwa wananchi, kwani sasa huduma za kisheria zinapatikana karibu na maeneo yao, kupunguza vikwazo vya kijiografia na gharama kubwa za usafiri ambazo zilikuwa changamoto kubwa kabla ya mwaka 2015,” alisema.

Mhe. Dkt. Rumisha alibainisha kuwa kupungua kwa muda wa mashauri na kuongeza ufanisi, mageuzi ya kimkakati, kidijitali na uboreshaji wa usimamizi wa kesi umepunguza muda wa kusubiri kupata haki kwa kiasi kikubwa.

Alitoa mfano wa kesi za biashara, ambapo katika Mahakama Kuu kuna punguzo la asilimia 64, kesi za familia Mahakama za Mwanzo zimepungua kutoka siku 120 hadi 35, punguzo la asilimia 71, na kesi Mahakama ya Wilaya zimepungua kutoka siku 40 hadi 15, punguzo la asilimia 63.

Punguzo hili limefanikiwa kutokana na matumizi ya TEHAMA, Mahakama tembezi (Mobile Courts), upanuzi wa Mahakama na kuanzishwa kwa IJCs katika Mikoa mbalimbali. Hii imesaidia wananchi kupata haki kwa haraka,” alisema.

Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa katika mageuzi ya kidijitali na uboreshaji wa utendaji, Mradi umejikita pia katika mabadiliko ya kidijitali ya mfumo wa Mahakama. Alieleza kuwa mfumo wa mapitio na tathimini ya utendaji Maofisa wa Mahakama (JOPRAS) hutoa uchambuzi wa muda halisi wa utendaji.

Aidha, alisema kuwa uchapishaji wa uamuzi mtandaoni umeongezeka kutoka asilimia 3 hadi 88, jambo linaloongeza uwazi, uwajibikaji na uelewa wa wananchi kuhusu mfumo wa kisheria.

Alieleza kuwa kiwango cha kuridhika kwa huduma za Mahakama kwa wananchi kimeongezeka kutoka asilimia 61 hadi asilimia 88 kutokana na kupungua kwa muda wa mashauri, hasa ya biashara na familia.

Kuhusu mlundikano wa mashauri, Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa kesi zilizokuwa zinasubiri zimepungua kutoka asilimia 10 mwaka 2021 hadi asilimia 5 mwaka 2025, hivyo kesi zote zenye umri zaidi ya miezi 24 ni asilimia 5 pekee. Alisema kuwa punguzo hilo limefanikiwa kupitia usimamizi makini wa mtiririko wa kesi, upanuzi wa Mahakama tembezi, na kuanzishwa kwa IJCs katika maeneo mbalimbali.

Alibainisha athari za kiuchumi na kijamii kupitia Mahakama tembezi na IJCs, ambapo gharama kwa wananchi zimepunguzwa kwa kiasi kikubwa, jambo ambalo inawawezesha wananchi kupata haki bila kero za kifedha, huku akiba ya Taifa ikifikia mabilioni ya shilingi.

Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa Mahakama imeendelea kudumisha imani ya wananchi kupitia uwajibikaji thabiti na mifumo ya maoni inayoruhusu michango ya umma na kwamba njia mbalimbali za maoni, ikiwemo sanduku la mapendekezo na maoni ya mtandaoni, zimeimarisha uhusiano na wananchi na kuleta uwazi katika utendaji wa Mahakama.

Alihitimisha kwa kusema kwamba mageuzi hayo ya kimkakati, kidijitali na kiutawala yameonesha wazi kwamba mfumo wa Mahakama unaweza kubadilika na kuendeshwa kwa ufanisi, uwazi, uwajibikaji na upatikanaji wa haki karibu na wananchi. 

Mafanikio hayo ni ishara tosha kwamba Tanzania ina mfumo wa Mahakama wa kisasa, unaojali wananchi, unaotumia teknolojia na mbinu za kisasa za usimamizi wa mashauri na unaendelea kuboresha maisha ya raia kwa kuharakisha upatikanaji wa haki, kupunguza gharama na kuongeza kuridhika kwa umma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho (JDU), Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (juu na chini), akiwasilisha taarifa ya maboresho kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.


Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania (juu na picha mbili) wakichangia mada kwenye kikao hicho.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Alhamisi, 26 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAIMARISHA MIUNDOMBINU KUPITIA MIRADI YA MAJENGO

Na HALIMA MNETE – Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imeendelea kutekeleza kwa kasi miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama katika Mikoa na Wilaya mbalimbali nchini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi na kuboresha mazingira ya utoaji huduma za kimahakama.

Hayo yalibainishwa jana tarehe 25 Februari, 2026 na Mkurugenzi wa Uendelezaji na Matengenezo ya Majengo wa Mahakama, Mhandisi Moses Lwiwa, wajati anawasilisha Taarifa ya Miradi ya Majengo ya Mahakama katika Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Akiwasilisha taarifa hiyo mbele ya Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Mahakama Tanzania, Mhe. George Masaju, na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt Mustapher Mohmed Siyani, ambaye ni Mwenyekiti wa kikao hicho, Mhandisi Lwiwa alieleza kuwa Mahakama inaendelea na utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Vituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJCs) katika Mikoa mbalimbali pamoja na majengo ya Mahakama za Mwanzo na Wilaya (SBCs), kwa lengo la kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kupunguza changamoto za miundombinu.

Kwa upande wa miradi ya IJCs, alibainisha kuwa miradi katika Mikoa ya Geita, Njombe, Simiyu, Songea, Pemba, Singida, Songwe na Lindi ipo katika hatua za mwisho za utekelezaji, ambapo baadhi ya majengo tayari yamekamilika na yanafanya kazi, huku mengine yakiwa katika kipindi cha uangalizi baada ya kukamilika (Defect Liability Period).

Alieleza kuwa Mahakama imeweka mkakati wa kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi hiyo kwa kushirikiana na Washauri Elekezi ili kuhakikisha mapungufu yote yanayojitokeza yanarekebishwa kwa wakati.

“Mwelekeo wetu ni kuhakikisha kila jengo linalokabidhiwa kwa Mahakama linakidhi viwango vya ubora vinavyotakiwa na linaweza kutumika kikamilifu katika utoaji wa huduma za haki,” alisisitiza.

Kwa upande wa miradi ya SBCs, Mhandisi Lwiwa alieleza kuwa miradi mingi iliyopo katika vifurushi mbalimbali (Packages na Lots) imekamilika kwa kiwango kikubwa na ipo kwenye kipindi cha uangalizi. Miradi hiyo inahusisha Mahakama za Mwanzo na Wilaya katika maeneo mbalimbali ikiwemo Kigoma, Mtwara, Manyara, Katavi, Rukwa, Mbeya, Dar es Salaam na Mikoa mingine.

Alifafanua kuwa miradi hiyo inatekelezwa kwa awamu na kwa mikataba maalum inayosimamiwa kwa karibu na Mahakama, kwa kushirikiana na Washauri Elekezi, ili kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana na majengo yanakuwa na ubora unaokidhi mahitaji ya watumishi na wananchi.

Katika hatua za mbele, amesema Mahakama imepanga kuimarisha usimamizi wa kiufundi katika miradi yote inayoendelea, kuweka msisitizo wa uwajibikaji kwa Wakandarasi pamoja na kuhakikisha kuwa marekebisho ya kasoro zozote zinazobainika katika kipindi cha uangalizi yanafanyika kwa wakati.

Utekelezaji wa miradi hiyo ya majengo unaenda sambamba na jitihada za Mahakama katika kufanya mageuzi ya kiutawala na kidijitali, kwa lengo la kujenga Mahakama imara yenye miundombinu ya kisasa, inayowezesha utoaji wa haki kwa ufanisi, uwazi na kwa wakati.

Mkurugenzi wa Uendelezaji na Matengenezo ya Majengo wa Mahakama, Mhandisi Moses Lwiwa, akiwasilisha Taarifa ya Miradi ya Majengo ya Mahakama katika Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Majaji wa Wafawidhi wa Mahakama Kuu [juu na picha mbili chini] wakichangia mada kwenye kikao hicho.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma


 

MAHAKAMA YA TANZANIA KUJENGA MAHAKAMA DIJITALI KWA KUZINGATIA DIRA YA TAIFA 2050

Na HALIMA MNETE – Mahakama, Dodoma

Uboreshaji wa kidijitali unaoendelea ndani ya Mahakama ya Tanzania unalenga siyo kuimarisha mifumo ya ndani ya Mahakama pekee, bali pia kuendana moja kwa moja na mipango na dira ya maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Hayo yalisemwa jana tarehe 25 Februari, 2026 na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA], Bw. Kalege Enock, wakati akiwasilisha taarifa ya matumizi ya TEHAMA katika usikilizaji wa mashauri kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi kinachofanyika Makao Makuu ya Mahakama, jijini Dodoma.

Kikao hicho kinahudhuriwa na Majaji Wafawidhi wa Kanda zote za Mahakama Kuu, kikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakam Kuu ta Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, kama Mwenyekiti wa kikao hicho huku Mgeni Rasmi akiwa ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, George Masaju.

Katika taarifa yake, Bw. Kalege alieleza kuwa safari ya Mahakama kuelekea Mahakama Dijitali (Smart Court) imejengwa juu ya misingi ya kimkakati inayojumuisha Mpango Mkakati wa Mahakama, Sera ya Taifa ya TEHAMA, Mkakati wa Serikali Mtandao, pamoja na Mfumo wa Kimkakati wa Uchumi wa Kidijitali na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akisisitiza mwelekeo huo wa kitaifa, alisema: “uboreshaji wote unaofanyika mahakamani katika eneo la kidijitali tunazingatia siyo tu mipango ya Mahakama, bali pia mipango ya nchi, tukianzia na Mfumo wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050. Hii yote tunaitumia kama dira ya kutuongoza katika kufikia maono mapana ya nchi yetu.”

Alifafanua kuwa mageuzi hayo yanalenga kuboresha usimamizi wa mashauri, kupunguza mrundikano wa mashauri, kuongeza uwazi na uwajibikaji, pamoja na kuwezesha maamuzi yanayotegemea takwimu sahihi.

Aidha, alieleza kuwa Mahakama imeendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya kielektroniki ikiwemo mfumo wa usimamizi wa mashauri (e-Case Management System), huduma za Mahakama Mtandao, pamoja na matumizi ya Akili Unde (Artificial Intelligence – AI) katika kunakili na kutafsiri mwenendo wa mashauri kwa Kiswahili na Kiingereza, uchambuzi wa takwimu za mashauri na utafiti wa kisheria.

Kuhusu maadili na usalama wa taarifa, Bw. Kalege alisisitiza kuwa Mahakama inazingatia kikamilifu matakwa ya Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ya mwaka 2022, pamoja na kuimarisha mifumo ya usalama wa mtandao ili kulinda kumbukumbu na ushahidi wa kimahakama.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kikao hicho, Mhe. Dkt. Siyani alieleza umuhimu wa Viongozi wa Mahakama katika ngazi za kanda kuhakikisha mifumo hiyo inatumika ipasavyo ili kuleta matokeo chanya katika utoaji wa haki.

Naye Jaji Mkuu alisisitiza dhamira ya Mahakama kuendelea kuwa Taasisi inayoendana na mabadiliko ya teknolojia duniani, akieleza kuwa katika zama hizi, utoaji wa haki unahitaji kuungwa mkono na mifumo imara ya kidijitali ili kuongeza ufanisi na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama.

 

Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA], Bw. Kalege Enock [juu na chini], akiwasilisha taarifa ya matumizi ya TEHAMA katika usikilizaji wa mashauri kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi Makao Makuu ya Mahakama, jijini Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi, akichangia mada kwenye kikao hicho. Picha chini ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, akichangia mada kwenye kikao hicho. 

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

MAHAKAMA YA TANZANIA YAFANYA MAAJABU MWAKA 2025

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imetekeleza kwa mafanikio makubwa jukumu lake la utoaji haki nchini kwa mwaka 2025. Kiwango cha uondoshaji wa mashauri kimeongezeka kutoka asilimia 83 hadi 88 na kiwango cha umalizaji kikiongezeka kutoka asilimia 101 hadi 105.

Hayo yamebainishwa jana tarehe 25 Februari, 2026 na Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha, wakati anawasilisha taarifa ya Utendaji wa Mahakama kwa Mwaka 2025 kwenye Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kinachofanyika jijini Dodoma.

Mhe. Kamugisha aliwaeleza Majaji hao kuwa mashauri yaliyofunguliwa kwa mwaka 2025 yalikuwa 243,848, sawa na ongezeko la asilimia 0.6 ya mashauri ya mwaka 2024. Mashauri hayo yanajumuisha 105,480 ya madai na 138,368 ya jinai.

Alibainisha kuwa, mashauri yaliyofunguliwa katika Mahakama ya Rufani yalikuwa 3,214, Mahakama Kuu yalikuwa 21,518, Mahakama za Hakimu Mkazi 6,033, Mahakama za Wilaya 35,144, Mahakama za Watoto 1,225, na Mahakama za Mwanzo 176,687, hivyo kufanya jumla ya 243,848.

‘Mashauri yaliyoamuliwa na Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2025 yalikuwa 4,405, Mahakama Kuu zilikuwa 22,164, Mahakama za Hakimu Mkazi 5,967, Mahakama za Wilaya zilikuwa 40,367, Mahakama za Watoto 1,372 na Mahakama za Mwanzo 180,518, hivyo kufanya jumla ya 254,793,’ alisema.

Kwa upande wa mashauri yanayoendelea, Mhe. Kamugisha alieleza kuwa Mahakama ya Rufani ni 5,039, Mahakama Kuu 10,381, Mahakama za Hakimu Mkazi 2,303, Mahakama za Wilaya 8,214, Mahakama za Watoto 202 na Mahakama za Mwanzo 7,240, hivyo kufanya jumla ya 33,379.

Aidha, alibainisha kuwa kiwango cha jumla cha umalizaji wa mashauri kwa 2025 kilikuwa asilimia 105, huku Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, ikiongoza kwa asilimia 141, wakifuatiwa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara kwa asilimia 111.

Kwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi, Mhe. Kamugisha alieleza kuwa Iringa iliongoza kwa asilimia176, wakifuatiwa na Mtwara kwa asilimia 168, huku upande wa Mahakama za Wilaya, Newala ilikuwa ya kwanza baada ya kuzoa asilimia 156, wakifuatiwa na Geita iliyopata asilimia 142.

'Kiwango cha jumla cha uondoaji wa mashauri kwa mwaka huo kilikuwa asilimia 88.4, huku Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke kikiongoza kwa asilimia 94, wakifuatiwa na Geita iliyopata asilimia 90,' alisema.

Aliongeza kuwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi, walioongoza ni Simiyu kwa asilimia 97, wakifuatiwa na Mahakama ya Watoto Temeke kwa asilimia 92, huku upande wa Mahakama za Wilaya, Kilolo iliongoza kwa asilimia 99, wakifuatiwa kwa karibu na Newala wenye asilimia 98.

Alibainisha pia mafanikio yaliyopatikana kwa mwaka 2025 kuwa malengo yote ya Mpango Mkakati wa Mahakama na mradi wa kupeleka huduma karibu na mwananchi yalifikiwa kikamilifu.

Mhe. Kamugisha aliongeza kuwa, kumekuwa na ongezeko la kiwango cha umalizaji mashauri kwa asilimia nne kutoka asilimia 101 kwa mwaka 2024 hadi asilimia 105 kwa mwaka 2025.

Kadhalika, alisema, kumekuwa na ongezeko la kiwango cha uondoshaji wa mashauri kwa asilimia tano kutoka asilimia 83 kwa mwaka 2024 hadi asilimia 88 kwa mwaka 2025.

Mhe. Kamugisha alibainisha pia kuwa muda wa wastani wa kuamua mashauri ulipungua kwa siku 12 kutoka wastani wa siku 78 kwa mwaka 2024 hadi siku 66 kwa mwaka 2025 na wastani wa mzigo wa kazi ulipungua kwa asilimia 2.6 kutoka 228 kwa mwaka 2024 hadi 222 kwa mwaka 2025.

‘Matokeo haya chanya yanaonesha utayari wa Mahakama ya Tanzania kukidhi mahitaji yanayokuwa ya haki kwa kuongeza nguvu kazi na kutekeleza mikakati madhubuti ya usimamizi wa mashauri, ikijumuisha mapitio ya kimkakati ya kanuni za taratibu na matumizi makubwa ya teknolojia,’ alisema.

Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha [juu na chini], akiwasilisha taarifa ya Utendaji wa Mahakama kwa Mwaka 2025 kwenye Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kinachofanyika jijini Dodoma.


Viongozi na Wakurugenzi wa Mahakama ya Tanzania [juu na chini] wakifuatilia mambo mbalimbali yanayojiri kwenye kikao hicho.


Sehemu nyingine ya Viongozi wa Mahakama [juu na chini] ikiwa kwenye kikao hicho. 



Meza Kuu inayoogozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju ikiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania [juu na chini]. 




Jumatano, 25 Februari 2026

JAJI MKUU AWATAKA MAJAJI, MAHAKIMU KUWAJIBIKA IPASAVYO

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, amewataka Majaji na Mahakimu nchini kutekeleza majukumu yao ipasavyo na kwa kujituma bila kusubiri maelekezo kutoka kwa Viongozi.

Mhe. Masaju ametoa maagizo hayo leo tarehe 25 Februari, 2026 wakati akifungua Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

“Mimi siku zote naimba wimbo juu ya kujituma (Proactivity) na hili sio sharti langu kama nimelibuni, ni sharti la Katiba lipo kwenye Ibara ya 25 ya Katiba na kujituma huku kunatokana na kuwajibika,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema Ibara ya 25 ya Katiba inazungumza juu ya uwajibikaji wa watumishi wote wa Serikali na kila mtu, katika hotuba yangu nilipoongea na Wasajili tarehe 22 Desemba, 2025 nilizungumza kwamba hatuwezi kuishi kwa maelekezo, sisi ni binadamu tuna akili kuliko Wanyama, tunatambua wajibu wetu na tunapaswa kujua kwamba ili kama binadamu tuweze kuendelea kimwili, kiroho na kiakili tunapaswa tufanye nini,” amesema Mhe. Masaju.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amewataka Maafisa Mahakama hao kujituma wanapotimiza majukumu yao kwa kuwa pia ni takwa la kikatiba kwa mujibu wa Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Masaju ameongeza kwa kuwataka Majaji hao kuwajibika kama Viongozi kwa kuimarisha uwazi na uwajibikaji kwa kuwa Mahakama inapaswa kukimbiliwa na wananchi.

Kadhalika, Jaji Mkuu ametoa rai kwa Majaji Wafawidhi kusimamia nidhamu za Mahakimu na Watumishi wengine wa Mahakama sambamba na kujiepusha na vitendo vya rushwa.

 

“Endeleeni kusimamia kikamilifu nidhamu za watumishi wote walioko chini yenu na hasa Mahakimu. Kama nilivyosema kwenye Mkutano wa TMJA kuwa tutarekebisha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama ( Judiciary Administration Act, Cap. 237) ili Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama za Mikoa na Wilaya zisimamiwe na Maafisa wa Mahakama wenyewe,” amesisitiza Mhe. Masaju.

 

Jaji Mkuu amesema suala la nidhamu na maadili linahitaji ujasiri, uadilifu mkubwa na dhamira ya ndani ili kulisimamia na kusema kuwa, “tusiposimamia eneo hili kwa umakini,  mabadiliko yanayopendekezwa yanaweza kutafsiriwa kuwa yalilenga kufichiana madhaifu yetu na si vinginevyo.”

 

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju amewapongeza Majaji na Mahakimu kwa kuendelea kutekeleza jukumu la utoaji haki kikamilifu.

 

“Mwaka 2024, Mahakama ilipokea jumla ya mashauri 242,309, huku mashauri 244,808 yakiamuliwa katika mwaka huo, mwaka 2025, Mahakama ilipokea jumla ya mashauri 243,848, sawa na ongezeko la takribani asilimia 0.6 ya mashauri yaliyopokelewa ikilinganishwa na mwaka 2024. Katika mwaka huo, Mahakama iliamua jumla ya mashauri 254,793,” amesema Jaji Mkuu.

 

Amesema takwimu hizo zinaonesha mambo makuu matatu yenye umuhimu mkubwa, ambayo mosi ni licha ya kuongezeka kwa idadi ya mashauri yanayopokelewa, jitihada zimefanyika ili kukabiliana na ongezeko hilo, pili ni kwa miaka yote miwili (2024 na 2025), Mahakama imefanikiwa kuamua mashauri mengi zaidi kuliko yaliyopokelewa katika mwaka husika.

 

Mhe. Masaju amesema ongezeko kubwa la mashauri yaliyoamuliwa mwaka 2025 (254,793) linaonesha kasi iliyoimarishwa ya utoaji haki, nidhamu katika usimamizi wa mashauri, pamoja na kujituma kwa watumishi wa Mahakama katika kutekeleza wajibu wao.

 

“Sambamba na hilo, nawapongeza pia kwa jitihada mlizochukua kusikiliza na kuyatolea uamuzi mashauri ya kiuchumi katika zoezi lililoanza mwezi Oktoba 2025 na kumalizika Desemba, 2025 kwa mafanikio makubwa,” amesema Jaji Mkuu.

 

Mhe. Masaju amebainisha kwamba, kwa kipindi kifupi cha mwezi Oktoba hadi Desemba, 2025, jumla ya mashauri 2,973 yenye thamani ya Tshs. 13,190,729,076,332 yalisikilizwa na kumalizika.

 

“Baadhi ya fedha hizo zimeingia kwenye matumizi, biashara na uwekezaji, hivyo kuchangia katika ukuaji wa Uchumi,” amesema Jaji Mkuu.

 

“Tuendelee na mikakati hii kuhakikisha kuwa Mahakama inatoa mchango wake katika kukuza uchumi kupitia jukumu lake la utoaji haki. Kufanya hivyo pia ni kutekeleza kwa vitendo Nguzo ya Kwanza ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambayo ni Uchumi Imara, Jumuishi na Shindani,” amesisitiza Mhe. Masaju.

 

Kwa upande mwingine, Mhe. Masaju ametoa maelekezo kwa Majaji Wafawidhi kuyapa kipaumbele mashauri ya Mirathi ambapo amesema, “tarehe 22 Desemba, 2025 nilipofanya kikao na Wasajili na Naibu Wasajili niliwasisitiza kuweka kipaumbele kwenye usikilizaji wa mashauri ya mirathi.”

 

Jaji Mkuu amesema kwa upande wa Mahakama ya Rufani tayari hatua zimechukuliwa ambapo mashauri 68 ya mirathi yaliyoiva kusikilizwa yamepangwa kwenye kikao cha Mahakama ya Rufani cha Mwezi Februari, 2026.

 

“Haya ni mashauri yanayohitaji kushughulikiwa kwa uharaka ili wanufaika wake ambao mara nyingi ni wanawake na watoto wapate haki zao mapema ipasavyo,” amesema Mhe. Masaju.

 

Ameongeza kuwa, ucheleweshaji wa usikilizaji wa mashauri hayo husababisha changamoto nyingi hasa kwa wananwake na watoto, pia fedha nyingi huzuiliwa kuingia kwenye uchumi.

 

Jaji Mkuu amesema hakuna sababu ya kuyaweka mashauri hayo kwenye utaratibu wa kawaida wa kupanga mashauri (FIFO). Mashauri mengine ya kuyapa kipaumbele ni mashauri yanayogusa Wanawake na Watoto ni takwa la kisheria kupitia Kanuni ya 5 (Rule 5) ya The Judicature and Application of Laws (Practice and Procedure in Cases Involving Vulnerable Groups) Rules, 2019 GN No. 110 of 2019).

 

Aidha, Mhe. Masaju ametoa rai kwa Majaji hao kutoa mapendekezo ya uboreshaji wa sheria na kanuni mbalimbali na kuzitumia ipasavyo katika kuharakisha jukumu la utoaji haki mapema ipasavyo. Amesema tangu Juni hadi Desemba, 2025 kanuni mbalimbali zipatazo 22 zimetungwa na kuboreshwa.

Akizungumzia kuhusu viwanja na ujenzi, Jaji Mkuu amewataka Majaji kuwa sehemu ya ufuatiliaji na upatikanaji wa Viwanja vya Ujenzi wa Mahakama za Mwanzo na Nyumba za Mahakimu.

 

“Kila mmoja awe sehemu ya mkakati huu, tumeieleza Serikali kuwa, jukumu la ujenzi wa Mahakama za Mwanzo katika kila Kata ni jukumu lao na ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu lao la kikatiba kwa mujibu wa Ibara 146(2)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na wamelikubali na kulichukua jukumu hilo,” amesema Mhe. Masaju.

 

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alishaelekeza kuwa TAMISEMI itekeleze jukumu hilo, hivyo ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha kuwa, kwenye kanda yake kila Kata inapata kiwanja chenye ukubwa usiopungua hekari mbili  kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Mahakama za Mwanzo na nyumba za Mahakimu.

 

Sambamba na hilo, Mhe. Masaju ametoa rai kwa Majaji  hao kusimamia utunzaji wa Majengo ya Mahakama ambapo amesisitiza kwa kusema, “Jitihada za ujenzi wa Mahakama majengo ya ya Mahakama ziende sambamba na utunzaji wa majengo hayo.”

 

Amesema Rais Samia alipozindua jengo la Makao Makuu ya Mahakama alielekeza Watumishi wa Mahakama kutunza majengo ya Mhimili huo.

 

“Kwa sasa tunayo majengo mengi na mazuri na mengine yanakamilika mwezi Machi mwaka huu. Natoa rai kwa watumishi wote wa Mahakama na wadau wanaotumia majengo hayo kuyatunza, na pia kuweka mpango endelevu wa kuyatunza majengo hayo,” amesisitiza.

 

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewataka Majaji Wafawidhi na Viongozi wengine wa Mahakama kuzingatia na kutekeleza ipasavyo maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Viongozi, huku akiwakumbusha maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa Mahakama  na Wadau aliyoyatoa katika hotuba yake ya Siku ya Sheria Nchini tarehe 02 Februari, 2026 ambayo ni pamoja na Kutoa haki kwa kuzingatia masharti yaliyoainishwa kwenye ibara ya 107A(2)(a)-(e) na 107B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kuheshimu na kuulinda uhuru wa Mahakama bila kuutumia vibaya.

 

Maelekezo mengine ni Kutotumia uhuru huo kama kichaka cha kuficha uzembe na vitendo visivyo vya haki, Kutenda kwa uadilifu na uwazi na mengine.

 

Vilevile, amewataka kutekeleza na kuisimamia mikakati ya Mkutano wa Wadu wa Kutathmini kuhusu Mikakati ya Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi na Ushindani wa Kibiashara na pia Mikakati ya Mkutano wa Mahakama na Wadau Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji wa Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani.

 

“Pamoja na kwamba mikakati ya mikutano yote miwili ilichapishwa katika tovuti ya Mahakama,  nimeona ni vyema nikawakumbusha tena mikakati hiyo, nikianza na mikakati ya Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji wa Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani; ambapo Kila taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa utendaji haki mahakamani iwajibike ipasavyo kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia Katiba, sheria na maadili ya utumishi yanayosimimamia taasisi husika, Wadau wote waheshimu na kulinda hadhi na ukuu wa Mahakama. Aidha, Mahakama kwa upande wake, isimamie ipasavyo sheria na kanuni zilizopo, ikiwemo sheria inayohusu kosa la kuidharau Mahakama (contempt of court) ili kulinda hadhi na ukuu wake,” amesema.

 

Lengo la Kikao hicho ni Kutathmini taarifa za utendaji kazi kwa mwaka 2025 – Taarifa ya Mashauri, Ukaguzi wa Mahakama, Maboresho ya Huduma za Mahakama, TEHAMA, Utekelezaji wa bajeti 2025/2026 na mipango ya 2026/2027 na miradi ya majengo ya Mahakama.

 

Lengo lingine ni kubaini mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa majukumu hayo, kutafuta ufumbuzi kwa pamoja, kuweka mikakati ya utekelezaji wa majukumu yetu kwa mwaka 2026, kupata taarifa fupi kutoka kwa kila Jaji Mfawidhi kuhusu utekelezaji wa shughuli za Mahakama katika eneo lake na Kubadilishana uzoefu kupitia mawasilisho hayo.


Aidha, Katika kuyaenzi maisha ya marehemu Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo, wakati wa hafla ya ufunguzi wa Kikao hicho, Jaji Mkuu aliwaongoza Majaji Wafawidhi na Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania walioshiriki kusimama kwa dakika moja ikiwa ni Ishara ya kumkumbuka mtumishi huyo wa Mungu aliyetangulia mbele za haki.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju [juu na chini], akizungumza wakati anafungua Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 25 Februari, 2026 katika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akitoa utambulisho wa Majaji mbalimbali wanaohudhuria kikao hicho.

Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania [juu na chini] ikiwa kwenye kikao hicho.

Sehemu nyingine ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania [juu na chini] ikiwa kwenye kikao hicho.



Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji Wafawidhi hao.
(Picha na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)







JAJI KIONGOZI AHIMIZA UTEKELEZAJI WA MIKAKATI YA VIKAO

  • Ataka mashauri ya rushwa, uhujumu uchumi kupewa kipaumbele

Na HABIBA MBARUKU- Mahakama Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustepher Mohamed Siyani, amewasisitiza Majaji, Mahakimu na Wakurugenzi wa Mahakama ya Tanzania kuhakikisha wanatekeleza mikakati inayowekwa na vikao mbalimbali pamoja na kuwasilisha utekelezaji wake kwa wakati.

Mhe. Dkt. Siyani ametoa rai hiyo leo tarehe 25 Februari, 2026 kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, kufungua kikao cha mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kwa mwaka 2026, kinachofanyika katika ukumbi wa Mahakama, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi amesema kuwa lengo na shabaha ya vikao hivyo ambavyo hufanyika walau mara moja kila mwaka ni kupata fursa ya kujipima na kujitathmini juu ya utendaji kazi wa Mahakama, sambamba na utekelezaji wa Dira na Dhima ya Mahakama.

“Kwa hiyo, lengo la vikao hivi ni kujitathmini wapi tumefanya vizuri lakini pia maeneo gani hatukufanya vizuri, matokeo ya tathmini hii ni kuboresha mchakato mzima wa utoaji haki nchini, jukumu ambalo Mahakama imekasimiwa na umma kupitia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema Mhe. Dkt. Siyani.

Ameeleza kuwa siyo vema hata kidogo kwa Viongozi kusubiri maelekezo ili kutekeleza mikakati inayowekwa. Amemtambua kwa namna ya pekee Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mhe. Alvin Mgeta, ambaye amekua akitekeleza mikakati ya vikao mbalimbali bila kusubiri barua au maelekezo kutoka Mahakama Kuu.

“Ninalolisema kwa Waheshimiwa Majaji nalisema pia kwa Wakurugenzi wengine ambao kwa nafasi zao wanahudhuria vikao hivi na hivyo wana wajibu wa kutekeleza mikakati na yale ambayo yanaelekezwa, siyo vema hata kidogo kwa Viongozi kusubiri maelekezo ili kutekeleza mikakati inayowekwa,’amesisitiza Jaji Kiongozi.

Akitoa taswira ya utendaji kazi wa Mahakama Kuu na Mahakama zilizopo chini yake, Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa Mahakama ya Tanzania ilivuka mwaka 2024 kukiwa na mashauri yaliyobaki 38,121.

Jaji Kiongozi amebainisha kuwa mwaka 2025, jumla ya mashauri 240,607 yalipokelewa na mashauri 250,388 yalimalizika, huku kiwango cha uondoshaji wa mashauri kikiongezeka kutoka asilimia 83 mwaka 2024, hadi kufikia asilimia 88 mwaka 2025.

Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kuwa mafanikio hayo ni sawa na ongezeko la asilimia 5.4 kwa Mahakama Kuu na Mahakama za chini. Ameeleza pia kuwa wastani wa muda wa shauri kukaa mahakamani umeendelea kupungua kutoka siku 78 mwaka 2024 hadi siku 66 mwaka 2025.

Ameongeza kuwa pamoja na ongezeko la mashauri yaliyopokelewa mwaka 2025, mzigo wa mashauri kwa kila Jaji au Hakimu umeendelea kupungua, ambapo wastani kwa mwaka 2024 ulikuwa mashauri 228 kwa kila Jaji au Hakimu na umepungua hadi kufikia 222 kwa mwaka 2025.

Kadhalika, Jaji Kiongozi amebainisha kuwa uimarishaji wa Mahakama Inayotembea umeendelea, ambapo kwa mwaka 2025 Mahakama hiyo imewafikia wananchi 9,069 na hivyo kuvuka shabaha ya mwaka 2024 ambayo ilikuwa kufikia watu 5,833.

Ameongeza kuwa kwa mwaka 2025 mchakato wa uchaguzi mkuu ulisababisha kufunguliwa kwa mashauri 15 kabla ya uchaguzi, na kwamba ni shauri moja pekee ambalo limesalia Mahakama Kuu kwa sababu ya uwepo wa shauri la marejeo katika Mahakama ya Rufani.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa baada ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi, jumla ya mashauri 12 ya kupinga matokeo ya ubunge na mashauri madogo 11 yanayotokana na mchakato huo yalifunguliwa kwenye Masjala mbalimbali za Mahakama Kuu, huku Mahakama za Hakimu Mkazi zikipokea mashauri 29 ya kupinga matokeo ya udiwani na mashauri ya maombi madogo 24 yanayohusiana na mashauri hayo, hiyo kufanya jumla ya mashauri yote yaliyotokana na matokeo ya uchaguzi kuwa mashauri 76.

Jaji Kiongozi amesema kuwa usikilizaji wa mashauri hayo unaendelea na hadi kufikia tarehe 25 Februari, 2026, mashauri matatu ya msingi na madogo mawili pekee yamebaki kati ya mashauri 23 ya Mahakama Kuu,  huku upande wa Mahakama ya Hakimu Mkazi yakiwa yamesalia mashauri matatu peke kati ya mashauri 53 yaliyofunguliwa.

Sambamba na hayo, Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kuwa mkakati wa kusikiliza mashauri yanayochochea ukuaji wa uchumi, uliwekwa katika vikao vilivyofanyika mwezi Septemba na Oktoba, 2025 na utekelezaji wake ulifanyika, ambapo Mahakama Kuu na Mahakama za Hakimu Mkazi zilifanikiwa kusikiliza mashauri 2,675 yaliyowezesha kuachilia kiasi cha shilingi za Kitanzania 11,940,395,000,000.

Vilevile, ameeleza kuwa, ugatuzi uliofanywa kwa wasimamizi wa mashauri ya uhujumu uchumi,kupitia uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa kwenda kwa Majaji wote wa Mahakama Kuu, umechangia kufanikisha usikilizaji wa mashauri 28 chini ya usimamizi wa Masjala mbalimbali nchini.

Jaji Kiongozi ameeleza kuwa Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ikimaliza mashauri 16 kati ya 88 yaliyokuwepo wakati hati hiyo inatolewa. Ameongeza kuwa pamoja na uwepo wa hati hiyo, bado kuna wastani wa mashauri 133 yanayoendelea kwenye Masjala mbalimbali za Mahakama Kuu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Siyani amewataka Majaji kuyapa kipaumbele mashauri ya rushwa na uhujumu uchumi kama ambavyo wanayapa kipaumbele mashauri mengine ambayo yapo katika Masjala zao.

“Nichukue fursa hii kuwataka Waheshimiwa Majaji kuyapa kipaumbele mashauri haya kama mnavyoyapa mashauri mengine yaliyopo katika Masjala zao” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa hatua imepigwa katika eneo la usimamizi wa mashauri ya mirathi, hususan ulipaji wa fedha za mirathi na utekelezaji wa kanuni mpya za mirathi.

Amesema kuwa kumbukumbu zilizopo zinaonesha kati ya tarehe 01 Oktoba, 2025 na tarehe 17 Februari, 2026, fedha za mirathi zilizokuwa kwenye akaunti za Mahakama zimepungua kutoka wastani wa shilingi Kitanzania 53 bilioni hadi bilioni 36.

Jaji Kiongozi amesisitiza kuwa takwimu hizo zinaonesha kuwa bado Mahakama ina kazi kubwa ya kufanya katika eneo hilo, huku akiwasihi Majaji kutumia kikao hicho kama fursa ya kubadilishana uzoefu ili kuimarisha usimamizi wa mashauri.

“Takwimu hizi zinaonesha kuwa bado tuna kazi ya kufanya katika eneo hili, ni matumaini yangu kuwa Waheshimiwa Majaji watapata fursa ya kubadilishana uzoefu na hivyo kuimarisha usimamizi wa mashauri haya, hususan ulipaji wa fedha za mirathi zilizopo kwenye akaunti za Mahakama,” amesema Jaji Kiongozi.

Akizungumza kuhusu matumizi ya mifumo mbalimbali ya kieletroniki mahakamani, Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa Mahakama inaendelea kutilia mkazo matumizi hayo kwa lengo la kurahisisha na kuharakisha upatikanaji wa haki mapema ipasavyo, pamoja na matumzi ya mifumo mingine ya TEHAMA kama Mfumo wa Kuratibu na Kusikiliza Mashauri (ESMS).

Jaji Kiongozi ameongeza kuwa mwaka 2025, Mahakama ilianza rasmi kutumia mfumo wa kieletroniki wa upimaji na utendaji kazi kwa Maofisa wa Mahakama.

Kadhalika, amesema kuwa Mahakama imeendelea kuimarisha ukaguzi wa Mahakama na Magereza kama sehemu ya kupima na kupata mrejesho wa ubora, ufanisi pamoja na kubaini changamoto za utoaji haki.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani [juu na chini], akizungumza kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 25 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania [juu na chini] ikiwa kwenye kikao hicho.




Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, akizungumza kabla ya ufunguzi wa kikao hicho.
Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju [juu na chini] ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma