Jumatatu, 18 Mei 2026

MAHAKIMU KIGAMBONI, WADAU WA HAKI JINAI WAPIGWA MSASA UANDAAJI WA HOJA ZA AWALI

  • Watumishi wasio Mahakimu nao wapatiwa elimu matumizi ya TEHAMA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo wilayani Kigamboni kwa kushirikiana na Wadau wa Haki Jinai, Mawakili wa Serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) wamepatiwa mafunzo ya namna bora ya uandaaji wa hoja za awali, kuzisoma, jinsi ya kuzirekodi, umuhimu na madhara ya kutoweka umuhimu wa hatua hiyo muhimu katika usikilizaji wa mashauri ya jinai.

Mafunzo hayo yalitolewa tarehe 15 Mei, 2026 na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa kwenye ukumbi wa Mahakama ya wazi ya Wilaya ya Kigamboni.

Wakati akifundisha, Mhe. Mbagwa aliwataka washiriki kueleza kwa namna wanavyojua maana na namna ya kuandaa na kushughulikia hoja za awali ambapo washiriki kila mmoja kwa uelewa wake alieleza.

Akitoa mafunzo hayo, Mhe. Mbagwa alianza kwa kueleza historia ya kuanzishwa kwa hatua hiyo ya hoja za awali katika mashauri ya jinai na kueleza lengo la kuanzishwa kwake ilikuwa ni kuharakisha usikilizwaji wa mashauri ya jinai kwa kuwa zile hoja zinazobishaniwa ndizo zinapaswa kuthibitishwa na upande wa mashtaka wakati wa uendeshwaji wa shauri.

Akifundisha kwa mfano, alisema iwapo mshtakiwa hakatai kuwa alikamatwa na kupelekwa Kituo cha Polisi upande wa mashtaka hawana sababu ya kumpeleka Mahakamani. Askari Mkamataji huthibitisha kuwa, mshtakiwa alikamatwa na katika hoja za awali mshtakiwa hakupinga kukamatwa kwake.

Mhe. Mbagwa aliwasisitiza Waendesha Mashtaka kuandika hoja muhimu zinazojenga msingi wa shauri na si kuandika mambo ambayo hata kama yakithibitika hayana uzito wowote katika shauri hivyo kuandaa hoja hizo kwa kuzingatia mambo muhimu katika shauri husika (essential facts).

Aidha, Jaji Mbagwa aliwasisistiza Washiriki wa mafunzo hayo kuzingatia hatua sita muhimu za kufuata wakati wa hatua hiyo muhimu ya kisheria kwa kuzingazita klifungu cha 198 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai. Hatua hizo ni kama Mwendesha Mashtaka kuzisoma hoja hizo, Mahakama kurekodi majibu ya Mshtakiwa, kuandaa muhtasari wa hoja zisizobishaniwa, Mshtakiwa kusomewa hoja zisizobishaniwa na mwisho Mwendesha Mashtaka, Mshtakiwa na Hakimu kuweka saini zao.

Akifungua mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib alimshukuru Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa kwa utayari wake na kukubali kujitoa na kufika Kigamboni kuwapatia mafunzo hayo.

Alimueleza pia, Mhe. Mbagwa kuwa, kuna mafunzo yanayohusiana na uandaaji na umuhimu wa hoja za awali kwa Mahakimu na Mawakili wa Serikali huku watumishi wengine wasiokuwa Mahakimu watapatiwa mafunzo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo yatatolewa na Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima.

Kadhalika, Mhe. Mwanakombo alimueleza Jaji Mbagwa kwamba, wameamua kuchagua mada hiyo, kwa kuwa Hoja za Awali ni hatua muhimu katika usikilizaji wa mashauri ya jinai. 

“Mhe. Jaji na washiriki wenzangu mtakubaliana na mimi kuwa ‘PH’ ni ‘road map’ ya shauri zima, maana hapa tunaona hoja zinazobishaniwa na zisizobishaniwa,” alisema Mfawidhi huyo wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni.

Aliongeza kuwa, mafunzo hayo yamekusudiwa kuwapa uelewa wa pamoja na mambo ya kuzingatia katika hatua hiyo muhimu.

Naye Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima aliwafundisha watumishi wasio Mahakimu namna bora ya kutumia mifumo mbalimbali ya ki-TEHAMA mahakamani ikiwemo matumizi ya Ofisi Mtandao (e-Office, Mfumo wa Kielektroniki wa Menejimenti ya Mashauri (e-CMS), (e-Filling) na mingine.

Kadhalika, Bw. Malima aliwasisistiza watumishi hao kuwapatia nakala za hukumu wateja ambao hawana uwakilishi mahakamani  na hawana akaunti za kuwezesha kupata nakala hizo.

Naye Mkuu wa Mashtaka wa Wilaya ya Kigamboni, Bi. Anita Sinare alimshukuru Mhe. Mbagwa kwa elimu aliyowapatia na kuahidi kuifikisha kwa Mawakili wenzao ambao hawakubahatika kuhudhuria mafunzo hayo.

Kwa upande wake, Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kigamboni, Bi. Bibiana Bundala alisema japo yeye sio Mwanasheria lakini mafunzo hayo yamempa uelewa mkubwa kuhusu nini kinapaswa kufanyika katika hatua hiyo muhimu na hivyo, itawezesha kuwabana watumishi walio chini yake na kusimamia ufanyikaji wa hatua hizo muhimu pale shauri linapofunguliwa Mahakamani.

Akitoa salamu za shukrani kwa Jaji Mbagwa baada ya mafunzo hayo, Mhe.  Christina Lugulu alisema kuwa, wamepata chakula cha akili na aliwashukuru wadau kwa kuhudhuria mafunzo hayo. 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa akifundisha Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwambo Kigamboni pamoja na washiriki wengine wa mafunzo (Wadau wa Haki Jinai) hayo kuhusu mada ya namna bora ya uandaaji wa hoja za awali. Mafunzo hayo yalitolewa tarehe 15 Mei, 2026.


Hakimu Mkazi  Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib (kushoto) akitoa neno la ufunguzi wa mafunzo. Aliyeketi katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa ambaye pia alikuwa Mwezeshaji wa mafunzo hayo na  kulia ni Bi. Pendo Kilusu, Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Awamu Mbagwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Kigamboni mara baada ya mafunzo yaliyofanyika katika Mahakama hiyo tarehe 15 Mei, 2026.


Jaji Awamu Mbagwa (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi  wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana  Rushwa  (TAKUKURU) na wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) Wilaya ya Kigamboni. Wa pili kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigambo, Mhe. Mwanakombo Twalib.


Watumishi wasio Mahakimu wakiendelea na Mafunzo ya TEHAMA.

Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Tumaini Malima akifundisha kuhusu Mafumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS).

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Awamu Mbagwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mhe. Mwanakombo Twalib (kushoto) na Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Bi. Upendo Kilusu (kulia).

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya mwanzo Kigamboni, Mhe. Christina Lugulu  akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mbagwa ambaye alikuwa Mwezeshaji wa Mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 

 

 

Alhamisi, 14 Mei 2026

JAJI MKUU GEORGE MASAJU AMSHUKURU RAIS SAMIA KUIWEZESHA MAHAKAMA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAKE IPASAVYO

·     Alishukuru pia Bunge la Tanzania kwa ushirikiano

·     Ni wakati akifunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama

·      Aipongeza Menejimenti ya Mahakama kwa usimamizi na utekelezaji thabiti wa majukumu

· Awataka watumishi wa Mahakama kuishi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana, kusaidiana.......

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania hususan katika kuuwezesha Mhimili huo kupata fedha za kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na miradi ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia (WB).

Mhe. Masaju ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania ameyasema hayo leo tarehe 14 Mei, 2026 alipokuwa akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

“Ninamshukuru Rais Samia, Mkuu wa Nchi hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano anaoutoa kwa Mahakama ya Tanzania wanavyotafuta fedha hata za mikopo kuwezesha sisi kutekeleza majukumu yetu ikiwa ni pamoja na miradi hii ya ujenzi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Benki ya Dunia,” amesema Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema, wakati Rais Samia aliposhiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) pamoja na hotuba ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ya mwaka huu, 2026 alielekeza kwamba wataendelea kuboresha bajeti ya Mahakama na maslahi ya watumishi kwa kadri bajeti inavyoruhusu.

Sambamba na hilo, Jaji Mkuu amelishukuru pia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Mhe. Masaju amesema, “Nalishukuru Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kwa Spika wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu, muda mfupi uliopita wamepitisha bajeti yetu ya Mahakama ya Tanzania, bajeti ilivyoenda kule haikuwa hivyo lakini kwa sababu ya Wabunge kutambua umuhimu wa Mhimili huu wakaongeza hizo bilioni 26 kwa hiyo nawashukuru sana Viongozi hayo wa Mihimili hiyo ya Serikali kwa ushirikiano wanaotoa kwa Mahakama ya Tanzania.”

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewapongeza washiriki wote wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama kwa ushiriki wao mzuri uliosheheni mijadala yenye tija, uwazi wa hoja pamoja na mapendekezo na mikakati mbalimbali inayolenga kuimarisha utendaji wa Mahakama ya Tanzania.

“Baraza hili si tukio la kawaida pekee, bali ni sehemu muhimu ya kujitathmini kama Taasisi, kusikilizana kama familia ya Mahakama na kupanga mustakabali wa utoaji haki hapa nchini kwa pamoja na kila mmoja wetu hapa ana wajibu na anawajibika,” amesema Mhe. Masaju huku pia akiwashukuru watoa mada wote kwa mada zao zenye kujenga na kuelimisha kwa maslahi ya watumishi wa Mahakama na Taifa kwa ujumla.

“Kama nilivyowaeleza katika hotuba yangu ya ufunguzi wa baraza hili jana, hii ni mara yangu ya kwanza kuongoza Baraza Kuu la Wafanyakazi na nililenga kujifunza zaidi na hivyo, nilijikita zaidi katika kujifunza na hakika nimejifunza mambo mengi sana kutoka kwenu wajumbe na pia kwa watoa mada wetu,” ameeleza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju ametoa pongezi za dhati kwa Menejimenti ya Mahakama kwa maandalizi mazuri ya mkutano huo, usimamizi mzuri wa shughuli wezeshi zinazowezesha Mahakama kutekeleza jukumu lake la kikatiba la utoaji haki, kuendelea kusimamia mageuzi mbalimbali ya kimfumo na kiutendaji.

“Vilevile, nawapongeza Menejimenti kwa kusimamia matumizi bora ya TEHAMA katika utoaji haki, kuimarisha mazingira ya kazi kwa watumishi wa Mahakama na kipekee kabisa nipongeze mpango wa suala la ‘Supplementary’ Bima ya Afya kwa watumishi wa Mahakama ambalo litaimarisha afya za watumishi na kuongeza ufanisi kazini,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumzia kuhusu bima hiyo, Mhe. Masaju amewaomba Watumishi wa Mahakama kutumia bima hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa yaani kuimarisha afya za Watumishi.

Vilevile, amewapongeza Viongozi wote wa Mahakama katika ngazi mbalimbali kwa usimamizi wa mashauri, ufuatiliaji wa utendaji kazi, usimamizi wa maadili ya watumishi sambamba na kuendeleza nidhamu na uwajibikaji.

“Mafanikio tunayoyaona leo ndani ya Mahakama yanatokana na mshikamano, uwajibikaji, uongozi wenye maono na ushirikiano baina ya watumishi wote,” amesema.

Mbali na Viongozi, Jaji Mkuu amewapongeza pia Watumishi wa Mahakama                        kwa              kazi                      kubwa wanayoendelea kuifanya kila siku hasa kwa kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri; kupunguza mlundikano wa mashauri, kuendelea kutekeleza majukumu yao hata katika mazingira magumu.

“Aidha, niwaombe watumishi wote kuendelea kutafuta suluhisho la changamoto mnazokabiliana nazo, na zile zilizoko nje ya uwezo wenu zileteni kwetu Makao Makuu ili tuzitafutie ufumbuzi,” ameeleza Mhe. Masaju huku akiwataka Viongozi wa Mahakama kutafuta suluhu ya changamoto na hoja mbalimbali zilizowasilishwa na watumishi wakati wa Mkutano huo.

“Tumesikia vilio vya wawakilishi wa watumishi hasa katika kada za chini kuwa ni maslahi duni na mazingira magumu ya kazi, niendelee kuwasisitiza viongozi wote (Menejimenti na Viongozi wa Kanda) kuendelea kuwa wabunifu ili kuboresha maslahi na mazingira ya watumishi wa Mahakama ili kuimarisha ustawi wao,” amesisitiza Jaji Mkuu.


Hali kadhalika amewakumbusha watumishi wote wa Mahakama kuzingatia Maadili na Uwajibikaji katika kazi, kutunza siri za kazi, kuwa waadilifu pamoja na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kushusha hadhi ya Mahakama.

Amewasisitiza watumishi kuendelea kufanya Kazi kwa ushirikiano, mshikamano, kuheshimiana, kusaidiana na kujenga utamaduni wa uwajibikaji.

Kwa upande mwingine, Jaji Mkuu amezungumzia kuhusu umuhimu wa Viongozi kusikiliza Watumishi ambapo amesema, “moja       ya mafanikio makubwa        ya                        mabaraza     haya                    ni          kuwapa watumishi nafasi ya kutoa maoni; kueleza changamoto; kupendekeza maboresho; hivyo, ni muhimu sana kuhakikisha kuwa hoja zote zilizowasilishwa hazibaki kwenye makabrasha.”

Vilevile amewataka wajumbe wa Baraza walioshiriki Mkutano huo kutoa Mrejesho kwa Watumishi kuhusu maazimio ya mkutano huo; mikakati iliyokubaliwa pamoja na wajibu wa kila upande katika utekelezaji wake.


Kuhusu, Bajeti na Mpango Mkakati wa Mahakama, Mhe. Masaju amesema Taasisi yoyote yenye mafanikio lazima iwe na mipango; vipaumbele na matumizi yenye tija na kusisitiza kwa kusema kuwa, “kwakuwa tayari tulishapanga bajeti ya Mahakama kwa mwaka 2026/2027, tuelekeze matumizi ya bajeti hiyo kulingana na mipango yetu, utekelezaji wake uzingatie kufikia malengo na shabaha ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Na hapa niwakumbushe kuendelea kuisoma Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kuifahamu misingi mikuu ya dira hiyo.


Mkutano huo ulihitimishwa kwa maazimo yafuatayo; Fursa finyu za ufadhili wa masomo kwa watumishi; Mwajiri aweke utaratibu wa wazi katika utoaji wa fursa za mafunzo kwa udhamini wa Mahakama kwa watumishi wanaohitaji kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo vya miundo mbalimbali ya kiutumishi.


Mahakama kutoshiriki katika baadhi ya michezo kwenye mashindano mbalimbali; Mahakama iongeze idadi ya michezo itakayoshiriki katika mashindano mbalimbali ya ndani pamoja na yale yanayoshirikisha Taasisi zingine.


Mafunzo ya Matumizi ya Mifumo ya TEHAMA kutowafikia watumishi wa kada zote; Mafunzo ya matumizi ya mifumo TEHAMA yatolewe kwa watumishi wote ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.


Kutokubaliwa kwa maombi ya uhamisho kwa baadhi ya watumishi ndani ya taasisi; Mwajiri aweke .utaratibu wa kuwahamisha watumishi ambao wamekaa kwa muda mrefu katika eneo moja la kazi na walio mbali na familia zao, ili kuimarisha ustawi wao wa kiutumishi na kifamilia.


Upandishwaji vyeo kwa RMAs na MMOs walioajiriwa kwa sifa ya darasa la saba na kidato cha nne waliokwama kupanda cheo kwa kukosa sifa za kimuundo; Mwajiri awasilishe maombi ya kibali maalumu cha kulegezewa masharti ya kimuundo kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili watumishi husika wafikiriwe kupandishwa vyeo kwa mserereko.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto), Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bw. Victor Kategere pamoja na wajumbe wengine wa Baraza la Wafanyakazi wakiwa katika siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza.

Makundi mbalimbali ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika Mkutano Mkuu wa Baraza hilo uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa PSSSF jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiongoza Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 14 Mei, 2026. Kushoto ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Ezra Kyando na kulia ni Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania.


Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama aliyoitoa leo wakati wa kufunga kikao hicho kilichofanyika kwa siku mbili tarehe 13 na 14 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.











 

 

HAKI MILIKI NGUZO YA MSINGI KATIKA KUKUZA UCHUMI MAENDELEO YA TEKNOLOJIA, UVUMBUZI...; JAJI MKEHA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Haki miliki imekuwa nguzo ya msingi katika kukuza uchumi, maendeleo ya teknolojia, uvumbuzi, biashara na msingi wa maendeleo ya viwanda  katika nchi.

Hayo yamebainishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa kwa Majaji na Naibu wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam na Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara.

Mhe. Mkeha amesema mafunzo hayo, yamekuwa na umuhimu mkubwa si tu kwa Mahakama ya Tanzania bali hata kwa Taifa kwa ujumla huku Tanzania ikiendelea kukumbatia  uchumi unaotokana na maarifa na uvumbuzi, hivyo ni jukumu la Mahakama kuhakikisha utekelezaji na ulinzi wa haki miliki unazidi kuwa muhimu.

Ameongeza kuwa, Dunia inazunguka kwa kasi kupitia teknolojia ya kidijitali, akili unde, biashara ya mtandaoni na muunganisho wa kimataifa. “Maendeleo haya yanapoendelea kupanuka, mizozo inayohusiana na alama za biashara, hataza, haki miliki, miundombinu ya viwanda, siri za biashara na haki zingine za uvumbuzi inazidi kuwa ngumu,” ameeleza.

Jaji Mfawidhi huyo amesema kuwa, katika kipindi chote cha mafunzo hayo washiriki wamepata fursa ya kuongeza ufahami katika sintofahamu zao katika maeneo muhimu ikiwa ni pamoja na misingi ya sheria ya haki miliki, mifumo ya usajili, uchambuzi wa ukiukaji, tathmini ya ushahidi wa kiufundi, masuluhisho ya mwingiliano wa habari, uharibifu na changamoto za kisiasa kama vile uharamia wa kidijitali.

Pia amesema Kikao cha Amri za Muda (Temporary injuction) maagizo ya Mareva (Mareva Injuction), uhifadhi wa ushahidi na hatua za utekelezaji wa mipaka zimekuwa muhimu sana katika kuimarisha mbinu za kimahakama za migogoro ya dharura na ngumu ya haki miliki.

Vivyo hivyo, Mhe. Mkeha amesema majadiliano juu ya tathmini ya ushahidi wa kitaalamu na ushahidi wa kiufundi yamesisitiza hitaji linaloongezeka la Maofisa wa Mahakama kuendelea kuonesha hali halisi ya kisheria na kiteknolojia inayoendelea.

Jaji Mkeha amesisitiza kuwa, mpango huo wa mafunzo haujazingatia tu nadharia za kisheria lakini masomo na mijadala ya vitendo, ushirikishwaji wa vitendo kama huo ni muhimu katika kukuza uthabiti, uwiano na kutabirika katika sheria ya haki miliki nchini Tanzania.

Aidha, amewaomba washiriki wa mafunzo hayo kuendelea kujihusisha na maendeleo yanayojitokeza katika Sheria ya Haki Miliki, kubadilishana uzoefu na Maofisa wenzao wa Mahakama katika mamlaka nyingine na kutumia ujuzi uliopatikana katika utoaji haki unaofaa na thabiti wa mashauri yaliyopo katika  Mahakama zao. 

Amewashukuru Waandaaji, Wawezeshaji, Taasisi zilizosaidia pamoja na Washiriki wote kwa ushirikiano na kujitolea kwa muda wote wa mafunzo hayo.

“Ninaamini kwamba ujuzi na uzoefu uliopatikana hapa utachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha maamuzi ya Mahakama na kuimarisha utekelezaji wa Haki Miliki nchini Tanzania,” alisema Mhe. Mkeha. 

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam, Mhe. Lumuli Mbuya akizungumza wakati akitoa neno la shukrani amemshukuru Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi kwa kuwezesha kufanikisha kufanyika kwa mafunzo hayo kwakuWa anapenda kuhakikisha kwamba wanasoma na kupata kupata mafunzo mbalimbali kwa ajili ya kuwajengea uwezo.

Mhe. Mbuya amewashukuru pia Sekretarieti kwa kuandaa mada nzuri na kuwachagua Wawezeshaji mahiri kwa kutoa mafunzo hayo.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliandaliwa na Mahakama ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam. Katika siku ya pili ya mafunzo hayo, mada zilizofundishwa ni pamoja na uthibitishaji wa ukiukwaji wa Haki Miliki (Element of Proving IP Infringement) na masuala yanayoibuka katika utekelezaji wa Haki Miliki (Emerging Issues in IP Enforcement) ambapo Profesa Saudin Mwakaje alifundisha na mada nyingine.

Mwisho wa mafunzo hayo Washiriki na Wakufunzi wa mafunzo hayo walipokea vyeti vya ushiriki.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha akitoa hotuba ya kufunga Mafunzo ya Miliki Bunifu tarehe 12 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.




Washiriki wa mafunzo ya Miliki Bunifu wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Mussa Maghimbi (kushoto) akipokea cheti cha ushiriki wa mafunzo ya Miliki Bunifu kutoka kwa Mhe. Cyprian Mkeha.


wakili Shehzada Walli akipokea cheti cha uwezeshaji wa mafunzo.

 Profesa Saudin Mwakaje akipokea cheti cha uwezeshaji wa mafunzo ya Haki Miliki.

Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Cleophace Morris Mwezeshaji wa Mafunzo ya Miliki Bunifu akifundisha wakati wa mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJIDHATITI KUBORESHA HUDUMA YA UTOAJI HAKI MAPEMA IPASAVYO

Na MARY GWERA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imetunga jumla ya kanuni mpya tano (5) na kufanyia marekebisho kanuni nane (8) na hivyo kufanya uwepo wa jumla ya kanuni 13 za uendeshaji wa mashauri, lengo likiwa ni kurahisisha mchakato wa usikilizaji mashauri ili haki iweze kupatikana mapema ipasavyo.

Hayo yamebainishwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, alipokuwa akiwasilisha Taarifa kuhusu Kazi za Kimahakama za mwaka 2025 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama lililofunguliwa jana tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

Mhe. Nkya ametaja Kanuni hizo kuwa ni pamoja na The Primary Courts-Administration of Estates) (Amendment) Rules 2025 GN No.  428 published on 11th July, 2025, The Civil Procedure Code (Amendment of the First Schedule) Rules, 2025 GN No. 569 published on 12th September, 2025.

Nyingine ni Judicature and Application of Laws (Electronic Filing) (Amendment) Rules, 2025 GN No. 39 published on 17th October, 2025, Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Madiwani za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na.433 la tarehe 11 Julai, 2025, Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Wabunge za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na.431 la tarehe 11 Julai, 2025, Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka 2025 Tangazo la Serikali Na. 430 la tarehe 11 Julai, 2025.

Kanuni za Marekebisho ya Kanuni za Mashauri ya Uchaguzi wa Wabunge za Mwaka 2025, Tangazo la Serikali Na 610 la tarehe 17 Oktoba, 2025, The Judiciary Administration Regulations (The Judiciary Administration (Judiciary Flag) (Amendment) Regulations, 2025, GN 608/2025 na nyingine.

Akizungumzia kuhusu mafanikio ya Mahakama yaliyopatikana, Msajili Mkuu ameeleza kuwa kumekuwa na ongezeko la usikilizaji mashauri kwa asilimia tatu sambamba na kupungua kwa wastani wa mzigo wa kazi toka 227 hadi 222.

Kadhalika, Msajili Mkuu ameeleza kuwa, kumekuwa na kasi ya kupungua kwa wastani wa muda wa kumaliza shauri kutoka siku 78 hadi 66.

Kadhalika, amebainisha kwamba, Mahakama imefanikiwa kufikia malengo ya kiashiria cha kiwango cha mashauri ya mlundikano kwa asilimia tano na usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (lengo lilikuwa 18,500 - 62,041).

“Mafanikio mengine yaliyopatikana ni pamoja na kuanzishwa kwa Masjala ndogo tano za Mahakama Kuu, kuanzishwa kwa Vituo vya Mahakama ya Mwanzo 15,” amesema Mhe. Nkya.

Kwa upande wa kiwango cha ukaguzi wa Mahakama na Magereza, Mahakama imefanikiwa kwa asilimia 1.6 na 11.6 mtawalia na kusababisha kupungua kwa mahabusu na wafungwa gerezani, huku Mahakama za Mwanzo kukiwa hakuna mahabusu.

Kwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, Mhe. Nkya amebainisha kuwa, zilikaguliwa kwa 100.

“Kuhusu ushughulikiaji wa mrejesho ulikuwa asilimia 99.9 ambapo jumla ya mirejesho 3,144 kati ya 3,149 (ikiwepo mitano “5” iliyobaki mwaka 2024) ilishughulikiwa,” ameeleza.

Amebainisha kuwa, kati ya mirejesho hiyo ushughulikiaji wa malalamiko ulikuwa ni asilimia 99.8 ambapo jumla ya malalamiko 1,609 kati ya 1,611 yaliyokuwepo (yakiwepo matano “5” yaliyobaki mwaka 2024) yalishughulikiwa.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya alipokuwa akiwasilisha Taarifa kuhusu Kazi za Kimahakama za mwaka 2025 katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama lililofunguliwa jana tarehe 13 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.





Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia wasilisho la Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (hayupo katika picha).