Na HALIMA MNETE- Mahakama, Dodoma
Serikali imeendelea kuimarisha Mhimili wa Mahakama pamoja na
Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, katika jitihada za kuhakikisha haki
inapatikana kwa wakati, kwa usawa na kwa kuzingatia misingi ya utawala wa
sheria.
Akiwasilisha bungeni mpango na makadirio ya mapato na
matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2026/2027 leo tarehe
24 Aprili, 2026, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera, amesema
mageuzi yanayoendelea yanalenga kuifanya Mahakama kuwa Mhimili imara
unaochochea maendeleo ya Taifa.
Aidha, Waziri Homela amelieleza Bunge jijini Dodoma kuwa katika
jitihada za kuimarisha mifumo ya utoaji haki, Serikali pia imeendelea kuboresha
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kupitia mifumo kama
Mahakama Mtandao na e-CMS, ambayo imerahisisha usikilizaji wa mashauri na
upatikanaji wa nyaraka kwa wakati.
Kwa upande wa elimu na mafunzo, amesema kuwa IJA imeendelea
kuwa kitovu muhimu cha kujenga uwezo wa watendaji wa Mahakama. Kupitia chuo
hicho, mafunzo ya kitaaluma na kiutawala yamekuwa yakitolewa ili kuongeza
ufanisi, maadili na weledi katika utoaji haki.
Aidha, Waziri Homela ameeleza kuwa IJA imeendelea kushiriki
katika utoaji wa huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi, ikiwa ni sehemu ya
jitihada za Serikali za kusogeza huduma za haki karibu na jamii, hususan kwa
makundi yenye uhitaji.
Sambamba na hayo, Serikali imeendelea kuhimiza matumizi ya
mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR) ili kupunguza mzigo wa mashauri
mahakamani na kuharakisha upatikanaji wa haki bila urasimu mrefu.
Katika hotuba hiyo, Waziri Homera alitoa shukrani za kipekee
kwa uongozi wa Mhimili wa Mahakama kwa mchango wao katika kuimarisha utoaji wa
haki nchini.
Aidha, amempongeza Mhe. George Masaju kwa kuaminiwa na
kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania. Uteuzi wake unadhihirisha
umahiri na uzoefu alionao katika Sekta ya Sheria kwa ujumla, ikiwemo Mhimili wa
Mahakama.
Katika hotuba hiyo, Mhe. Homera ametoa pia shukrani za
kipekee kwa uongozi wa mhimili wa Mahakama kwa mchango wao katika kuimarisha
utoaji wa haki nchini. Amewataja Viongozi wengine wa juu wa Mahakama akiwemo
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha IJA, Mhe. Dkt. Paul Faustine
Kihwelo, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed
Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel,
na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.
Mhe. Homera alisisitiza kuwa uongozi huo umeendelea kuwa
nguzo muhimu katika mageuzi ya kimfumo ndani ya sekta ya sheria na kuongeza
imani ya Wananchi kwa vyombo vya utoaji haki. “Sekta ya Sheria siyo tu
msimamizi wa sheria pekee, bali ni injini ya uthabiti wa Taifa na kichocheo cha
maendeleo ya uchumi katika kufikia malengo ya DIRA 2050.”
Waziri Homera alieleza kuwa uongozi huo umekuwa mstari wa
mbele kusukuma mageuzi ya kimfumo ndani ya Mahakama, hususan katika kuongeza
matumizi ya teknolojia, kuboresha usimamizi wa mashauri na kuimarisha
uwajibikaji.
Alisisitiza kuwa mchango wa viongozi hao umeendelea kujenga
imani ya Wananchi katika Mhimili wa Mahakama na kuhakikisha haki inapatikana
kwa wakati na kwa usawa.
Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha Mahakama
pamoja na Taasisi zake ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wote, kwa wakati na
kwa usawa, ikiwa ni msingi muhimu wa amani, utulivu na maendeleo ya Taifa.









