Jumamosi, 28 Machi 2026

KITABU KIPYA CHAFUNGUA UKURASA MPYA WA SHERIA YA MAKOSA YA KUJAMIANA

       Msajili Mkuu apongeza juhudi za Majaji katika kuandika na kushirikisha maarifa

Na HALIMA MNETE, MAHAKAMA- DODOMA

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya amesema kuwa uandishi wa vitabu vya kisheria ni nyenzo muhimu katika kukuza taaluma ya sheria na kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Mhe. Nkya aliyasema hayo jana tarehe 27 Machi 2026, jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa kitabu kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Nkya alisema kuwa, kitabu hicho kinagusa moja kwa moja maisha ya jamii na kina mchango mkubwa katika kujenga uelewa wa masuala ya haki ya jinai, hususani katika makosa ya kujamiiana.

Alieleza kwamba, makosa ya kujamiiana yanahusiana moja kwa moja na utu na hadhi ya binadamu, hivyo kuwepo kwa maandiko ya kitaaluma kunasaidia kutoa mwanga kuhusu dhana muhimu za hatia na adhabu ambazo ni msingi wa sheria ya jinai duniani kote.

“Kitabu hiki kinakuja kutoa mchango wa kitaaluma katika eneo ambalo limekuwa na mashauri mengi mahakamani, pamoja na kuwa na idadi kubwa ya wafungwa magerezani,” ameeleza Msajili Mkuu.

Aidha, amempongeza Jaji Ngwembe Mwandishi wa kitabu hicho kwa kuchangia maarifa yake kupitia maandishi, akibainisha kuwa uandishi unasaidia kuhifadhi maarifa na kuyaacha kama kumbukumbu ya kudumu kwa vizazi vijavyo.

“Sisi kama Mahakama tunajivunia juhudi hizi za Majaji na Mahakimu wanaoandika vitabu, kwani vinachangia kuendeleza taaluma ya Sheria na kuzalisha vyanzo vya maarifa,” ameongeza.

Mhe. Nkya pia alisema kitabu hicho kinatarajiwa kuwa rejea muhimu kwa wadau mbalimbali wa sheria wakiwemo Majaji, Mahakimu, Mawakili wa Serikali, Mawakili binafsi pamoja na Wanataaluma wa Sheria.

Vilevile alitoa shukrani kwa Jaji Mkuu wa Tanzania kwa kukubali kuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha dhamira ya Mahakama katika kukuza taaluma na utafiti wa sheria nchini.

Uzinduzi huo ni sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania kuhamasisha uandishi wa kitaaluma miongoni mwa watumishi wake na wadau wa sekta ya sheria kwa lengo la kuboresha mfumo wa utoaji haki nchini.



 Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa neno wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe. Hafla hiyo ilifanyika jana tarehe 27 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.



Sehemu ya washiriki waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Kitabu kilichoandikwa na Jaji Ngwembe.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa tatu kushoto) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Kitabu kiitwacho 
“Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe. 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


Ijumaa, 27 Machi 2026

JAJI MKUU AZINDUA KITABU CHA SHERIA HATIA NA ADHABU KATIKA MAKOSA YA JINAI...

 ·       Kitabu hicho chaandikwa na Jaji wa Rufani, Mhe. Paul Ngwembe

·       Kinatoa pia Tafakari ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana

·       Hafla ya uzinduzi yashuhudiwa na Majaji wa Rufani, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Kiongozi, Viongozi wa Mahakama na wageni waalikwa

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 27 Machi, 2026 amezindua kitabu kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Kitabu hicho iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Masaju amempongeza Jaji Ngwembe kwa hatua hiyo kubwa ya kuandika kitabu hicho.

“Ninakupongeza Mhe. Ngwembe kwa hatua hii kubwa ya kuandika kitabu hiki licha ya majukumu makubwa yaliyopo mbele yako,” amesema Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amempongeza pia Jaji Ngwembe kwa kuandika Kitabu hicho kwa Lugha ya Kiswahili, ambapo amesema kuwa, amefanya vizuri kutumia Lugha ya Taifa.

Aidha, Jaji Mkuu ametoa rai kwa Majaji wengine kutumia maarifa na ujuzi walionao katika kazi zao kuandika vitabu kwa manufaa ya Majaji, Mahakimu na Sekta ya Sheria kwa ujumla na kuwahakikishia kuwa, Mahakama iko tayari kutoa ushirikiano utakaohitajika kwa Majaji au Mahakimu walio tayari kwa uandishi wa vitabu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Watunga Sera wana wajibu wa kuangalia sheria zilizopo na zinazotungwa ili ziende sambamba na kuziunganisha na mila na desturi za jamii.

Akitoa neno la utangulizi, naye Jaji Ngwembe amesema, Kitabu hicho alichoandika ni matokeo ya utafiti wa muda mrefu wa Sheria zenye Adhabu za Chini (Minimum sentence) ikiwa ni pamoja na adhabu za Makosa ya Kujamiiana uliofanywa ili kubaini mahusiano ya Jamii ya Tanzania na Misingi ya Utungaji wa Sheria nchini.

“Utafiti huo wa muda mrefu umeunganishwa na uzoefu wa kusilikiza mashauri yanayohusu makosa hayo.  Hivyo Kitabu hiki ni matokeo ya utafiti na uzoefu wa kusikiliza mashauri mbalimbali katika Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani, ni kitabu kilichobeba mifano halisi siyo nadharia pekee,” amesema Mhe. Ngwembe.

Amesema kuwa, ameandika Kitabu hicho ili kuongeza wigo wa vitabu vya Sheria katika jamii ya Watanzania na pia kuhimiza wasomi na Majaji kuona haja ya kuandika michango yao katika ustawi wa nchi.

“Mahakama na Wasomi walioko kwenye taaluma za Sheria wanakutana na mambo mengi ambayo wakati mwingine yanakinzana na dhamiri (Counscience). Lakini kwa asili ya kazi za Ujaji au Uhakimu hawawezi kulalamika au kuzigomea Sheria hizo, badala yake wanakaa kimya. Basi Kitabu hiki kinalenga kushawishi  na kuwahamasisha Wasomi wetu kutafiti na kuandika kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo” ameeleza Jaji Ngwembe.  

Amesema kwamba, ameandika kitabu hicho kwa Lugha ya Kiswahili rahisi kinachoeleweka kwa mtu yeyote anayejua kusoma na kuandika kwa lugha ya Kiswahili.

“Nimelenga kitabu hiki kiwafikie Wanazuoni wa vyuo vikuu, Majaji na Mahakimu wa ngazi zote, Wanasheria, Watunga Sheria na Watungiwa Sheria,” amesema.

Ameongeza kuwa, Kitabu hicho kimechambua kwa mtiririko wa Kihistoria, misingi ya Jamii na utunzi wa Sheria zinazoongoza jamii husika, Changamoto ya mifumo mbalimbali ya jamii katika mabadiliko  chanya yaliyoletwa na maendeleo ya Kisasa.

Aidha, Mhe. Ngwembe amesema kuwa, kupitia kitabu hicho amechambua kwa uwazi mifano hai ya madhara hasi ya sheria zinazotungwa bila utafiti wa kina wa mahitaji halisi ya jamii. Vilio visivyo kwisha vya kuwepo kwa sheria zilizotungwa bila ushirikishwaji wa jamii na nje ya mahitaji halisi ya jamii na mwisho kimetoa mapendekezo na maoni ya jumla.

Katika hatua nyingine, Jaji Ngwembe amemshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na afya njema hadi kufika siku hii muhimu na vilevile amemshukuru Jaji Mkuu kwa utayari wake kuwa mgeni rasmi katika tukio hilo adhimu. 

Kadhalika amewashukuru Majaji wenzake wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu kwa kuacha kazi zao na kuitikia mwaliko wake, sambamba na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na watendaji wake kwa kubeba jukumu hilo.

Amewashukuru pia Maprofesa wote wakiongozwa na Profesa Ilomo wa Chuo Kikuu cha Iringa aliyeshiriki kuhariri kitabu hicho pamoja na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Nangela kwa uchambuzi alioufanya kuhusu Kitabu hicho.

Vitabu vingine alivyowahi kuandika Jaji Ngwembe ni pamoja na Kitabu cha Historia ya Kijiji cha Nyanyembe (1900 - 2019) Mapinduzi chanya Yaliyoletwa na Kanisa na Serikali ambacho kilizinduliwa mwaka 2020, Kitabu cha tafakari ya Familia ya Joel Ngwembe Tulikotoka, Mafanikio, Changamoto na Tunakokwenda (1921 - 2022)  kilichozinduliwa 2023, Tafakari ya Maisha ya Jesse Jonathan Mtisi, alikuwa mkandarasi aliyejenga Mahakama za Mwanzo nyingi na kukarabati Jengo la Mahakama Kuu Tanga na pia alijenga Cathedraw ya Dayosisi ya Mufindi na pia  anakamilisha Kitabu cha Historia ya Wilaya ya Mufindi, Utawala, Uchumi na Utamaduni.

Matukio katika picha, hafla ya uzinduzi wa Kitabu kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa tatu kushoto) akizindua kitabu kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe. Hafla hiyo imefanyika leo tarehe 27 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwandishi wa Kitabu hicho, Mhe. Paul Ngwembe, wa kwanza kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari na wa kwanza kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza leo tarehe 27 Machi, 2026 wakati wa hafla ya uzinduzi wa kitabu kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe. Hafla hiyo imefanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.


Jaji wa Mahakama Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe akitoa neno kuhusu Kitabu alichoandika kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana.”


Sehemu ya makundi mbalimbali ya watu waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa kitabu hicho wakiwemo Majaji, Viongozi wengine wa Mahakama, Watumishi na Wageni waalikwa waliohudhuria katika hafla hiyo.

    Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Kitabu kilichoandikwa na Jaji Ngwembe.Wa pili kushoto ni Jaji wa Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Paul Ngwembe, wa kwanza kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari na wa kwanza kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya washiriki waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa kitabu.

Mchambuzi wa kitabu ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Deo John Nangela akitoa neno wakati wa hafla ya uzinduzi wa kitabu 
kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kiichoandikwa na Jaji Ngwembe.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa neno wakati wa hafla ya uzinduzi wa kitabu kilichoandikwa na Jaji Ngwembe.

Mhariri wa Kitabu 
kiitwacho “Hatia na Adhabu katika Makosa ya Jinai: Kwa Kadri ya Sheria ya Makosa ya Kujamiiana” kilichoandikwa na Jaji wa Mahakama Rufani Tanzania, Mhe. Paul Joel Ngwembe, Profesa Falres Ipyana Ilomo akitoa neno wakati wa uzinduzi wa kitabu hicho.










 

MAHAKAMA KANDA YA KIGOMA YAPOKEA MTENDAJI MPYA

·       Ni Bw. Yusuph Mhoja Kasuka

·       Aonesha furaha ya kupangiwa Kituo hicho

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewaongoza Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda Kigoma kushuhudia makabidhiano ya Ofisi baina ya Bw. Filbert Matotay na Mtendaji mpya wa Kanda hiyo, Bw. Yusuph Mhoja Kasuka.

Makabidhiano yalifanyika tarehe 24 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma.

Akizungumza katika hafla ya chakula cha jioni kilichoandaliwa maalum kwa ajili ya ukaribisho wa Mtendaji huyo, Mhe. Rwizile alimueleza Bw. Kasuka kuwa, Mahakama Kanda ya Kigoma ina timu nzuri ya watumishi na vilevile ni sehemu nzuri ya kufanya kazi kwa kuwa ina mazingira na hali ya hewa nzuri.

“Tunakukaribisha sana Kigoma tuna ari kubwa ya kufanya kazi na watu wa Kigoma ni wema sana tutakupa ushirikiano mkubwa hivyo utafurahia maisha, ni vema ukawa na familia yako karibu kwa ajili ya utulivu wako katika majukumu mazito uliyoaminiwa nayo na kuletwa Kigoma kufanya kazi,” alisema Jaji Rwizile.

Vilevile, alitoa pongezi kwa Bw. Matotay aliyekuwa Mtendaji wa Mahakama hiyo kabla ya uhamisho, kuwa ni mchapa kazi,  mwenye ushirikiano mkubwa katika kazi zake za utendaji, hata hivyo amemtakia kazi njema katika kituo chake kipya cha Mahakama Kuu Kanda ya Singida.

Aidha kikao hicho kilihudhuriwa na watumishi  wa kanda ya kigoma kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court) kutoka Mahakama za wilaya Kigoma, Kasulu, Kibondo, Uvinza, Buhigwe na Kakonko.

Picha ya makabidhiano ya Ofisi kati ya aliyekuwa Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma kutoka kwa  Bw. Filbert Matotay (kushoto) na  Bw. Yusuph Mhoja Kasuka Mtendaji mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.

Mtendaji mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma Bw. Yusuph Mhoja Kasuka akipokea ua kutoka kwa mtumishi wa Mahakama hiyo, Bi. Regina Kija kama ishara ya ukaribisho mara baada ya Mtendaji huyo kuwasili katika viwanja vya Mahakama Kuu hiyo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa neno la ukaribisho kwa Mtendaji mpya wa Mahakama Kuu Kigoma, Bw. Yusuph Mhoja Kasuka (hayupo katika picha) wakati wa chakula jioni. Kushoto ni aliyekuwa Mtendaji wa Mahakama Kuu Kigoma ambaye amehamishiwa Mahakama Kuu Kanda ya Singida, Bw. Filbert Matotay.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa kwanza kushoto). Katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi, kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza, kwa pamoja wakisoma kwa makini taarifa ya makabidhiano ya Ofisi ya Mtendaji wa Mahakama hiyo.


Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Yusuph Mhoja Kasuka akitoa neno la shukrani kwa mapokezi na kuahidi kufanya kazi kwa ushirikiano na watumishi wote.

Watumishi wakifuatilia kwa makini uwasilishwaji wa taarifa ya makabidhiano ya Ofisi ya Mtendaji iliyokuwa ikiwasilishwa na Bw. Filbert Matotay.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

JAJI NONGWA AAGWA MBEYA KWA TAFRIJA KABAMBE

Na. MUKSINI NAKUVAMBA- Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, ameongoza viongozi na watumishi wa Mahakama katika hafla maalum ya kumtakia kheri na baraka, Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Victoria Mlonganile Nongwa kufuatia uteuzi wake wa kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe.

Hafla hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, ilihudhuriwa na Viongozi na Watumishi mbalimbali wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Njombe, Songwe na Iringa. Vilevile watumishi walipata wasaa wa kutoa shukrani, pongezi na kumbukumbu za namna Mhe. Nongwa alivyogusa maisha ya wengi kupitia uongozi wake.

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga alimpongeza Mhe. Nongwa kwa utendaji wake uliotukuka na uwezo wake wa kujenga mshikamano miongoni mwa watumishi, akibainisha kuwa ameacha alama isiyofutika katika utumishi wa Mahakama hiyo.

“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuteuliwa kwako kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, tumeshuhudia uongozi wenye busara, upendo na ushirikiano kutoka kwako. Umeweza kuunganisha watumishi na kujenga mazingira ya kazi yenye kuheshimiana na kusaidiana,” alisema Mhe. Tiganga.

Naye, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu alisema, Uongozi bora wa Mhe. Nongwa ulipekea kutunukiwa tuzo mbalimbali za uchapakazi bora kwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.

“Umekuwa kiongozi na mshauri mzuri katika kutekeleza majukumu ya utumishi wako hapa Mbeya, umekuwa na utayari wa kipekee sana mpaka kutunukiwa tuzo mapema Februari 2026 na Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya kwa kutambua na kuthamini utayari wako wakati wote katika kutekeleza majukumu ya kimahakama hata pale uliposhtukizwa wewe ulikuwa tayari kupokea majukumu hayo ya usikilizaji wa mashauri ambalo ni jukumu mama la Mahakama ya Tanzania,” alisema Naibu Msajili huyo.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi mteule wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe Mhe. Victoria Nongwa alitoa shukrani kwa watumishi wenzake kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote cha utumishi wake katika Kanda ya Mbeya, akieleza kuwa mafanikio aliyoyapata yametokana na mshikamano na moyo wa pamoja kazini.

“Naondoka nikiwa na kumbukumbu nzuri ya kufanya kazi na timu yenye upendo na mshikamano. Nitaendelea kuthamini mahusiano haya hata ninapoanza majukumu yangu mapya mkoani Njombe na nayabeba mazuri yote ya Mbeya,” alisema Mhe. Nongwa.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa, Mhe. Nongwa alikuwa kiongozi aliyesikiliza, aliyejali ustawi wa watumishi na aliyehamasisha utendaji kazi wa pamoja, hali iliyochangia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za haki.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (aliyesimama) akitoa nasaa zake kwa Viongozi na watumishi wa Mahakama (hawapo pichani) wakati wa hafla hiyo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe Mhe. Victoria Nongwa (aliyesimama) akizungumza machache na Viongozi na Watumishi wa Mahakama katika hafla ya kuagwa kwake.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Bi. Marvis Miti (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya na Njombe wakiwa wameshikana mikono kwa pamoja ikiwa ni ishara ya upendo na mshikamano.

Sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (aliyesimama) akitoa shukurani kwa niaba ya Mahakimu wa Kanda ya Mbeya na Songwe waliohudhuria katika hafla hiyo.

Mmoja wa watumishi (aliyesimama) akitoa neno la shukurani kwa niaba ya watumishi wengine katika hafla hiyo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya na Njombe wakiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya watumishi waliohudhuria katika hafla hiyo mbele ya Jengo la Mahakama Kuu Kanda ya mbeya.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)









Alhamisi, 26 Machi 2026

SONGWE YAJIVUA RASMI KUTOKA MAHAKAMA KUU KANDA YA MBEYA

Na. IMAN PATSON – Mahakama, Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga jana tarehe 25 Machi, 2026 alikabidhi rasmi eneo jipya la kiutawala la Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kanda ya Songwe kwa Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo Mhe. Gabriel Malata, katika hafla iliyofanyika katika Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe.

Aidha, Mhe. Tiganga alifanya ukaguzi wa jengo hilo jipya ambapo alipitia miundombinu ya jengo na vifaa vya Ofisi na kisha kufanya makabidhi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songwe Mhe. Malata.

Mhe. Tiganga alipongeza wakandarasi wa Jengo hilo kwa kazi nzuri waliofanya na pia aliwasihi wafanyakazi wa jengo hilo kumalizia kazi iliyobakia kwa muda mfupi ili kazi zingine za kimahakama ziweze kuendelea.

Aidha, baada ukaguzi huo Mhe, Tiganga alifanya kikao cha kuagana na watumishi wa Mahakama Kanda ya Songwe na kuwashukuru kwa ushiriakiano alioupata kutoka kwao na aliwaahidi kuwa ataendelea kutoa ushirikiano wakati wote atakapo hitajika. Vilevile, aliwakumbusha umuhimu wa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi Mhe. Malata aliwasisitiza watumishi kuhusu suala la nidhamu, kuthaminiana, upendo, ulinzi wa miundombinu, vitendea kazi wa vya Ofisi na utendaji wa kazi mzuri kwa watumishi wote ili kuwezesha kutoa huduma bora ya haki kwa wananchi.

Mhe. Malata Uongozi wa Mahakama kwa kumteua kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songwe na kuahidi kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha haki inatolewa kwa wananchi kwa wakati mapema ipasavyo.

Kufuatia makabidhiano hayo, Mhe. Tiganga aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mavis Miti.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (kulia) akifanya makabidhiano na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (kushoto) kuashiria shughuli rasmi za Mahakama Kuu, Kanda ya Songwe.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kanda ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa kwanza kushoto) akionesha hati ya makabidhiano.

Muonekano wa Jengo la Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kanda ya Songwe lilipofikia.

Mhandisi wa jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji haki Kanda Songwe Bw. Victor akielezea maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo lilipofikia na akiahidi kuwa kufikia Aprili 1, 2026 jengo hilo litakua lipo tayari kwa matumizi.

Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe mara baada ya makabidhiano, wa tatu kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa tatu kulia), Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (wa pili kushoto), Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Mhe. Joyce Minde (wa pili kulia), Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songwe Bw. Sostenes Mayoka (wa kwanza

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)




JAJI MFAWIDHI MBEYA AFUNGUA MAFUNZO YA USULUHISHI KWA NAIBU WASAJILI, MAHAKIMU WAKAZI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga amefungua mafunzo maalum ya Usihi na Usuluhishi kwa Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi kutoka katika Kanda mbalimbali za Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Iringa, Njombe, Sumbawanga, Songwe na Katavi.

Mafunzo hayo yaliyofunguliwa tarehe 24 Machi, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya. Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Tiganga alisema kuwa usuluhishi unalenga kuimarisha upatikananaji wa haki mapema ipasavyo na kwa gharama nafuu.

“Usuluhishi ni nguzo muhimu sana katika utoaji haki, kwani hupunguza migogoro baina ya wanajamii na kupunguza gharama kwa wadaawa katika kutatua migogoro yao,” alisema Mhe. Tiganga.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mafunzo hayo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Mhe. Gloria Shuma akizungumza na washiriki alisema kuwa, mafunzo hayo yatakayodumu kwa muda wa siku tatu yana lengo mahususi la kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani na kupunguza athari za upatikanaji wa vidonda na makovu ambayo ni matokeo ya migogoro katika jamii.

Aidha, washiriki walieleza kuwa matarajio yao katika mafunzo hayo ni kujifunza kwa kubadilishana uzoefu baina yao namna ya kufanya usihi na usuluhishi, kujifunza namna ya kuwa wasuluhishi bora na kubaini changamoto mbalimbali zinazojitokeza wakati wa usuluhishi na namna ya kuzitatua kwa pamoja.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mafunzo ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2013, Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania pamoja na sera ya Mafunzo ya Mahakama ya Tanzania ya mwaka 2019.

    Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Waheshimiwa Naibu Wasajili na Waheshimiwa Mahakimu Wakazi kutoka katika Kanda mbalimbali za Nyanda za Juu Kusini wanaoshiriki mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi ambao ni Naibu Wasajili wanaoshiriki Mafunzo ya Usuluhishi kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.


Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (aliyesimama kwenye podium) akifungua mafunzo hayo maalum kwa Waheshimiwa Naibu Wasajili na Waheshimiwa Mahakimu Wakazi.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto) akiwa sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba ambaye pia ni mwezeshaji Mhe. Raymond Kaswaga akitoa mada kwenye mafunzo hayo ya Usuluhishi

Sehemu ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada zinazotolewa na wawezeshaji kwenye mafunzo hayo.


Mratibu wa mafunzo hayo Mhe. Gloria Shuma (kulia) kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) akifuatilia mafunzo hayo, kushoto ni Hakimu Mkazi Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Franco Msuja