Jumamosi, 4 Julai 2026

MAHAKIMU WA WILAYA NA MWANZO KIBAHA WAPIGWA MSASA KUHUSU MIRATHI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Kibaha

Mahakama ya Wilaya Kibaha imetoa mafunzo ya Mirathi kwa Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo za Wilaya hiyo yakilenga katika maeneo muhimu kuanzia ufunguaji hadi ufungaji wa mashauri ya aina hiyo.

Mafunzo hayo ya siku moja yalifanyika tarehe 03 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Akizungumza wakati akimkaribisha Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha Mhe Emmael Lukumai amesema kutokana na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo Mahakimu katika usikilizaji wa mashauri ya mirathi,wameona ni vyema wapate mafunzo ambayo yatawaweka sawa ili kutatua changamoto wanazokutana nazo.

Mwezeshaji wa mafunzo hayo ambaye ni Hakimu Mkazi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe.Simon Swai amewaeleza Mahakimu hao kuwa, anapoteuliwa Msimamizi wa Mirathi wamueleze taratibu zote kuepuka usumbufu huku akiwataka Mahakimu kuangalia uhalisia wa mali za marehemu ili waweze kutoa muda wa kufanya hesabu kutokana na wingi au uchache wa mali hizo.

"Mfano marehemu alikuwa na mali NSSF tu haihitaji muda mrefu sana wiki tatu tu zinatosha," alisema Mhe. Swai huku akiongeza kuwa, miongoni mwa maeneo hayo ni pamoja na kutambua kama hayo ni maombi ya Mirathi au ni maombi ya barua ya kusimamaia mirathi pamoja fomu zake, Mamlaka ya Mahakama kusikiliza shauri hilo, mchakato wa mapingamizi wakati wa uteuzi wa Msimamizi wa mirathi, uteuzi, uwasilishaji wa hesabu za mali za marehemu, usikilizwaji wa mapingamizi, akaunti maalum ya mirathi, kuhamisha umiliki wa mali za marehemu kwenda kwa warithi na ufungaji wa mirathi.

Aidha, Mhe. Lukumai amemshukuru Mhe. Swai kwa kukubali mwaliko huo wa kufika Mahakamani hapo kutoa mafunzo hayo na kukiri kwamba wamefurahi kwakuwa kulikuwa na changamoto wanazokumbana nazo na wameweza kupata ufumbuzi.

Hakimu Mkazi kutoka Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe. Simon Swai akiwafundisha Mahakimu wa Mahakama ya Wilaya na wa Mwanzo Kibaha namna bora ya usikilizwaji wa mashauri ya mirathi tarehe 03 Julai, 2026 kwenye  ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha.


 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho kwa Mwezeshaji wa Mafunzo ya Mirathi, Mhe.Simon Swai ambaye ni Hakimu Mkazi kutoka Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke.

Baadhi ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo na za Wilaya ya Kibaha wakifuatilia mafunzo ya namna bora ya usikilizwaji wa Mashauri ya Mirathi.

Hakimu Mkazi- Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-TemekeMhe.Simon Swai (kulia) akieleza yaliyomo katika Kitabu chake cha FAMILIA. Kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai.

Hakimu Mkazi- Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, Mhe.Simon Swai (kulia) akikabidhi kitabu cha FAMILIA kwa Mahakama ya Wilaya Kibaha kama zawadi. Kushoto ni Mhe. Emmael Lukumai akipokea kitabu hicho kwa niaba ya Mahakama ya Wilaya Kibaha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 


Ijumaa, 3 Julai 2026

MAHAKAMA MDAU MUHIMU KATIKA KUSIMAMIA USALAMA NA AFYA KAZINI; MTENDAJI MKUU OSHA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda amesema kwamba Mahakama ni mdau muhimu katika kusimamia masuala ya usalama na afya mahala pa kazi kwa kuwa Ofisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Mhimili huo katika kuhamasisha uwepo na uzingatiaji wa sheria, taratibu na kanuni mahala pa kazi.

Bi. Mwenda alieleza hayo jana tarehe 02 Julai, 2026 akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Mafunzo haya si tu kwamba ni kwa wafanyakazi kwa kuwa ninyi ni wafanyakazi wa ndani ya Mahakama, lakini vilevile tunatambua kazi yenu kubwa ya kufanya maamuzi. Kwa hiyo kuifahamu Sheria ya Usalama na Afya, majukumu yake... Tunafahamu mnafahamu ipo, lakini inavyotekeleza majukumu yake na mafunzo yatakayotolewa hapa basi hata katika kutoa maamuzi mna inakuwa wepesi, lakini tunategemea sana Mhimili huu wa Mahakama na Wahe. Majaji ninyi muweze kuwa msaada mkubwa sana kwetu katika kuhakikisha kwamba maeneo ya kazi yanazingatia sheria,” amesema Mtendaji Mkuu huyo.

Amesema kuwa, suala hilo pia inakutokana na kwamba Sheria ya Usalama na Afya imekuwa ni haki na kanuni ya msingi mahali pa kazi. Kwa hiyo kutozingatia Sheria ya Usalama na Afya maanake ni kutozingatia haki za binadamu.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo wa OSHA, amebainisha kuwa, uzingatiaji wa masuala ya usalama na afya mahala pa kazi ni sehemu ya haki za msingi za binadamu, kama ilivyopitishwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwaka 2022 kupitia Mikataba Namba 155 na 187.

Ameongeza kwa kusema kuwa, Majaji wana uwezo wa kusaidia kutoa mwongozo wa namna gani ambavyo pia Nchi inaendelea kuwa salama katika uzingatiaji wa haki za binadamu mahali pa kazi.

Kadhalika Bi. Mwenda amemshukuru Jaji Mkuu kwa kuruhusu mafunzo hayo kufanyikia katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma. Amewapongeza pia Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani walioteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia kwa kuaminiwa na kupewa dhamana hiyo kubwa.

"Sheria ya Usalama na Afya ya mwaka 2003 inatutaka kulinda nguvu kazi ya Taifa ili kuhakikisha uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kwa watumishi unaleta tija. Tunataka Majaji wetu wafanye kazi kwa miaka yote waliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu wakiwa na afya njema na salama," alisema Kiongozi huyo wa OSHA.

Ameongeza kwamba, kupitia mafunzo hayo, Majaji hao watapata uelewa wa kina wa jinsi OSHA inavyofanya kazi, hatua zinazofuatwa kuthibitisha magonjwa yanayotokana na kazi (work-related diseases), jambo litakalorahisisha utoaji wa maamuzi na utendaji wa haki pale ambapo mashauri ya namna hiyo yanapofikishwa Mahakamani.

Katika mafunzo hayo ya siku mbili, Wataalam wa OSHA na Madaktari Bingwa watatoa elimu kuhusu vihatarishi vya kemikali, biolojia, na vihatarishi vya ki-ergonomia vinavyotokana na uhusiano wa mfanyakazi na mazingira yake.

Mbali na mafunzo hayo, OSHA imeweka kambi maalum ya Madaktari Bingwa wa Mifupa, Mgongo na Macho kwa ajili ya kuwafanyia uchunguzi wa afya na kutoa ushauri wa kitiba kwa Viongozi na watumishi wa Mahakama, pamoja na kutoa mafunzo ya vitendo ya Uokoaji na Huduma ya Kwanza.

OSHA imesisitiza utayari wake wa kuendelea kushirikiana na Mhimili wa Mahakama, ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mazingira ya kazi katika majengo mbalimbali ya Mahakama nchini ili kuhakikisha yanakuwa salama wakati wote.

Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) ni Taasisi ya Serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) yenye jukumu la kusimamia Sheria Namba 5 ya Mwaka 2003 (Sura namba 297) ili kuzuia ajali, magonjwa na vifo vinavyotokana na mazingira ya kazi nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani, Kaimu Jaji Kiongozi, pamoja na Viongozi na Watendaji wakuu wa Mahakama na OSHA. 


Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda akitoa neno wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Baadhi ya Viongozi na Watumishi mbalimbali wa Mahakama na OSHA wakiwa katika hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akimkabidhi zawadi ya Saa Bi. Khadija Mwenda, Mtendaji Mkuu wa OSHA wakati wa Hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akipokea zawadi ya (First Aid Tool Box) kutoka kwa Bi. Khadija Mwenda, Mtendaji Mkuu wa OSHA wakati wa Hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa OSHA walioshiriki ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Alhamisi, 2 Julai 2026

‘USALAMA NA AFYA MAHALI PA KAZI; MSINGI WA UTAWALA BORA NA UTOAJI HAKI’

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina amesema kuwa, masuala ya usalama na afya si jambo la hiyari bali ni sehemu muhimu ya utawala bora na utoaji haki wenye ufanisi.

Jaji Mlyambina ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Rufani ameyasema hayo leo tarehe 02 Julai, 2026 alipokuwa akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

"Tumekuza utamaduni wa usalama na afya mahala pa kazi ndani ya Mhimili wa Mahakama. Kupitia ushirikiano huu thabiti na OSHA, tumeshaendesha mafunzo kwa Majaji, Wasajili, Mahakimu, watumishi wa kada za utendaji, na hata watumishi wenye ulemavu. Msisitizo wetu ni kwamba usalama na afya ni haki ya kila mfanyakazi bila ubaguzi," amesema Jaji Mlyambina.

Mratibu huyo ameeleza juu ya mafanikio ya mafunzo ya aina yake yaliyofanyika mwaka jana (2025) jijini Mwanza (Malaika Hoteli) ambapo teknolojia ya kisasa ilitumika kuunganisha kumbi mbili tofauti ili Viongozi na Kada saidizi (Majaji na Madereva) wapate mafunzo yanayoendana na majukumu yao kwa wakati mmoja.

Mhe. Dkt. Mlyambina amesema baada ya mafunzo hayo, walitembelea katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ambapo waliendelea kujifunza kuhusu haki kazi katika mazingira ya mbugani, ambapo walidhihirisha kwamba usalama na afya mahala pa kazi ni suala ambalo linahusu kila eneo la kazi na kila mazingira ya utendaji.

Aidha, Mhe. Dkt. Mlyambina amesema kwa awamu hii, mafunzo yanalenga kujenga uwezo wa Majaji wa Rufani wapya na viongozi waandamizi, kutekeleza Sheria ya OSHA, inayomtaka kila mwajiri kuweka mazingira salama ya kazi, kuhimili changamoto za kisaikolojia, hasa kukabiliana na msongo wa mawazo (stress) na madhara ya kisaikolojia yanayotokana na kazi za utoaji haki (vicarious trauma) na kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Mwaka, 2050 kupitia watumishi wenye afya bora na tija kubwa.

Ameongeza kwamba, lengo ni kuwafikia Viongozi na Watumishi wote wa Mahakama kwa awamu ili kila mmoja, popote alipo, apate uelewa na ujuzi wa kujilinda na kulinda wenzake mahala pa kazi.

“Tunamini kwamba Mahakama yenye Viongozi na Watumishi wanaozingatia usalama na afya mahala pa kazi ndio inayoweza kutoa haki kwa ufanisi zaidi na kuchangia maendeleo endelevu ya taifa, na hasa katika kutekeleza Dira ya Taifa ya mwaka 2050,” ameeleza Jaji Mlyambina.

Kadhalika, Jaji Mlyambina ameongeza kuwa, ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na OSHA unaendelea kuwa mfano wa kuigwa katika Taasisi za umma, ukionesha namna utekelezaji wa Sheria za Usalama kazini unavyoweza kuongeza ufanisi, kulinda nguvu kazi ya Taifa na kuhakikisha haki inatendeka katika mazingira salama na yenye staha.

“Mhe. Jaji Mkuu, kwangu binafsi, mafunzo haya yana maana ya kipekee. Mbali na kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, ninayo heshima ya kuwa Mratibu wa mafunzo haya. Katika kipindi nilichohudumu kama Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mahakama imejenga na kuimarisha ushirikiano wa karibu na Wadau wa haki kazi, ikiwemo pamoja na OSHA Tanzania,” ameeleza Mhe. Dkt. Mlyambina.

Aidha, Jaji Mlyambina amempongeza Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, kwa utendaji kazi wake uliotukuka na wa kizalendo, ikiwa ni pamoja na kufadhili mafunzo hayo na kutoa vifaa kinga ili kuboresha mazingira ya utendaji kazi wa Majaji.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mlyambina ametumia jukwaa hilo kumpongeza Dkt. John Anthony Jingu kufuatia kuteuliwa kwake na Rais wa Jamhuri ya Munungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania.

Mafunzo hayo yamebeba Kaulimbiu isemayo, "Nafasi ya Haki Kazi, Afya na Usalama Mahala pa Kazi kwa Maendeleo Endelevu."


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina akitoa neno leo tarehe 02 Julai, 2026 wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Washiriki wa mafunzo pamoja na baadhi ya Viongozi waalikwaJaji  kutoka Mahakama wakimsikiliza Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina alipokuwa akitoa neno leo tarehe 02 Julai, 2026 wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
















 

ILO DAR ES SALAAM YAMUAGA JAJI MLYAMBINA

  • Yaahidi kuendeleza ushirikiano na Jaji Mfawidhi mpya

Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama, Divisheni ya Kazi

Viongozi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) Ofisi ya Dar es Salaam, jana tarehe 1 Julai, 2026 walikutana na Viongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kwa ajili ya kumuaga aliyekuwa Jaji Mfawidhi, Mhe.  Dkt. Yose Mlyambina, ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani.

Katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano ILO Kazi House, Viongozi hao walimkaribisha pia Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na wawakilishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ILO na Wadau wengine wa haki kazi na ajira.

Mhe. Dkt. Mlyambina aliwasilisha shukrani zake kwa ILO kwa kuwa bega kwa bega na Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi katika kufanikisha shughuli mbalimbali kwa kipindi chote alichohudumu katika ofisi hiyo. 

Alieleza kuwa ILO imekuwa ikishirikiana na Mahakama hiyo katika kuimarisha haki kazi nchini. Ushirikiano huo ni pamoja na kuwezesha machapisho ya (Labour Case Reports) ambazo zimekuwa msaada mkubwa katika kuimarisha utoaji wa haki kazi.

Aidha, alieleza kuwa ILO imekuwa ikiwezesha mafunzo mbalimbali ndani na nje ya nchi ambapo watumishi na Wadau wengine wamekuwa wakinufaika kwa kuongeza ufanisi katika utendaji kazi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Ofisi ya ILO, anayehudumia Tanzania, Kenya, Rwanda na Uganda, Bi. Caroline Mugalla, alisema kuwa mfumo madhubuti wa haki za kazi ni msingi muhimu wa kuendeleza ajira zenye staha na haki za kijamii.  

Vilevile, alisisitiza kuwa ushirikiano wa muda mrefu kati ya ILO na Mahakama ya Tanzania umechangia kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wafanyakazi na waajiri kupitia mfumo wenye ufanisi wa utoaji haki.

Bi. Caroline, kwa niaba ya ILO, alitumia nafasi hiyo kumshukuru Jaji Mlyambina kwa utendaji kazi wake katika kipindi chote alichohudumu, huku akimpongeza kwa  kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani.

Katika kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya, Bi. Caroline alieleza kuwa ILO itaendelea kushirikiana na Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha mfumo wa haki kazi nchini kwa manufaa ya Taifa kwa ujumla.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe.  Dkt. Yose Mlyambina, ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, akimkabidhi zawadi Mkurugenzi wa Ofisi ya ILO, anayehudumia Tanzania, Kenya, Rwanda na Uganda, Bi. Caroline Mugalla.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe.  Dkt. Yose Mlyambina, ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, akiwa kwenye picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Ofisi ya ILO, anayehudumia Tanzania, Kenya, Rwanda na Uganda, Bi. Caroline Mugalla.

Viongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na wale kutoka  Ofisi ya ILO Dar es Salaam wakiwa kwenye mazungumzo. 

Mkurugenzi wa Ofisi ya ILO, anayehudumia Tanzania, Kenya, Rwanda na Uganda, Bi. Caroline Mugalla (kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe.  Dkt. Yose Mlyambina, ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na mkabidhi Mkurugenzi wa Ofisi ya ILO, anayehudumia Tanzania, Kenya, Rwanda na Uganda, Bi. Caroline Mugalla (kulia) na Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga.


Picha ya pamoja kati ya Viongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na wale kutoka  Ofisi ya ILO Dar es Salaam.

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.

JUSTICE MLYAMBINA VISITS ILO COUNTRY DIRECTOR DAR ES SALAAM OFFICE

  • Expresses appreciation for technical, financial support to Labour Court Division
  • Congratulates ILO for Economy Convention adoption

From FAUSTINE KAPAMA-Judiciary, Singida

The outgoing Judge in-Charge of the High Court Labour Division and incumbent Justice of Appeal. Hon. Dr. Yose Mlyambina, has expressed gratitude to the International Labour Organization (ILO) for remarkable partnership, friendship and support extended throughout his tenure.

Hon. Dr. Mlyambina voiced out such appreciation on Monday dated July 1, 2026, when he paid a courtesy visit to the ILO Country Director, Dar es Salaam Office, Madam Caroline Mugalla.

“The partnership between the International Labour Organization and the Labour Court has existed for many years and has consistently contributed to the advancement of labour justice in Tanzania.,” he said.

Justice Mlyambina made particular reference to the period between January 2023 and May 2026, during which their cooperation reached remarkable heights.  During such relatively short period, the ILO extended generous technical and financial support that has left a lasting institutional legacy.

He pointed out one of the most significant achievements was the sponsorship of the first publication of the Court of Appeal Labour Cases Report, 2023.

He said that such important publication was followed by the publication of the Compilation of Principal and Subsidiary Labour Laws, and subsequently the publication of the High Court Labour Cases Report, 2025, comprising two comprehensive volumes.

“These publications represent much more than collections of judicial decisions and statutes. They are indispensable tools in the administration of labour justice,” said Justice Mlyambina.

According to him, another notable achievement for which they remain deeply grateful is the generous donation by the ILO of a substantial collection of labour law textbooks and reference materials to the High Court Labour Division Library.

These books, he said, have greatly enriched our legal resources and strengthened legal research within the Division.

“Although the world is progressively transitioning towards digital libraries and electronic legal databases, the reality in developing countries such as Tanzania is that printed legal materials continue to play an indispensable role,” he said.

He also congratulated the Organization at the global level for another historic milestone reached on June 12, 2026, during the 114th Session of the International Labour Conference in Geneva, with the adoption of the Decent Work in the Platform Economy Convention, No. 193 of 2026.

“This Convention demonstrates once again the ILO's leadership in responding to the changing nature of work across the world,” Justice Mlyambina told the ILO Country Director.

He pointed out that the rapid expansion of digital labour platforms has created enormous employment opportunities, while simultaneously presenting new legal and policy challenges relating to workers' rights, social protection, occupational safety and health, fair remuneration and effective access to justice.

According to him, the Convention provides a timely international framework for balancing innovation with social justice.

Hon. Dr. Mlyambina said that for countries such as Tanzania, where the platform economy continues to expand, the Convention offers valuable guidance in developing legal and policy frameworks that protect workers while encouraging entrepreneurship, innovation and investment.

He told the Country Director that the Convention No. 193 comes at an opportune moment, thus providing an international framework within which Member States can respond to emerging challenges, while fostering innovation and sustainable economic growth. 

“It is also noteworthy that the platform economy is steadily blurring the traditional distinction between an employee and an independent contractor, a distinction upon which much of our labour legislation has historically been built,” Justice Mlyambina said.

He pointed out further that Convention No. 193 provides an important normative framework to guide that evolution while respecting national legal systems. The Convention will only attain its intended impact when it is ratified and effectively implemented by ILO Member States, including Tanzania.

“We therefore look forward to the ILO continuing to support the United Republic of Tanzania including the Judiciary of Tanzania, through technical assistance, legislative advisory services, capacity building and institutional strengthening,” he said.

Justice Mlyambina added that such an undertaking would ensure that the aspirations embodied in Convention No. 193 are translated into meaningful improvements in the world of work, while simultaneously fostering innovation, entrepreneurship and sustainable economic development.

During the visit, Justice Mlyambina was accompanied by other senior judicial official, including his successor, High Court Judge, Hon. Dr. Ntemi Kilekamajenga, who has assumed the responsibility of Judge In-Charge of the High Court Labour Division since on June 22, 2 2026.

He took such opportunity to introduce him to the ILO Country Director and expressed his confidence that under his capable leadership, the Division will continue to grow from strength to strength.

Justice Mlyambina request that the excellent cooperation and partnership that has existed between the International Labour Organization and the High Court Labour Division continues under his stewardship.

Other judicial official in attendance during the visit were Deputy Registrar In-Charge of the High Court Labour Division, Hon. Cassian Enock Matembele, Deputy Registrar of the High Court Labour Division, Hon. Mary Mrio, another Deputy Registrar of the High Court Labour Division, Hon. Ritha Tarimo, Judge’s Law Assistant of the High Court Labour Division, Hon. Jane Masua and Acting Court Administrator of the High Court Labour Division, Ms. Joyce Mulugu.

The outgoing Judge in-Charge of the High Court Labour Division and incumbent Justice of Appeal. Hon. Dr. Yose Mlyambina,presents a gift to Internatioanl Labour Organization Country Director, Dar es Salaam Office, Madam Caroline Mugalla. The picture below, the duo is in a group picture.



The host and visiting judicial officials sharing information.

The ILO Country Director, Dar es Salaam Office, Madam Caroline Mugalla (right) in a group picture with Judge In-Charge of the High Court Labour Division, Hon. Dr. Ntemi Kilekamajenga.

A group photo of three officials. Middle if the outgoing Judge in-Charge of the High Court Labour Division and incumbent Justice of Appeal. Hon. Dr. Yose Mlyambina, left is Judge in Charge of the High Court Labour Division, Hon. Dr. Ntemi Kilekamajenga and right if ILO Country Director, Dar es Salaam Office, Madam Caroline Mugalla. The picture below comprises other judicial officials who were part of the visit.



 

MASJALA NDOGO MBEYA YAWAKARIBISHA VIONGOZI WAPYA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA –Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya wamekutana katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu kwa ajili ya hafla ya kuwakaribisha na kuwatambulisha viongozi wapya waliohamia kuhudumu katika kanda hiyo.

Viongozi waliokaribishwa katika hafla hiyo ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya.

Hafla hiyo, iliongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Said Kalunde na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu, Mahakimu wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo zilizopo Jijini Mbeya.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo alisisitiza umuhimu wa kujenga ushirikiano mzuri kati ya viongozi na watumishi ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi. .

Aidha, aliwahimiza watumishi kuendelea kuendana na maboresho yanayoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania, hususan katika matumizi ya mifumo ya TEHAMA, ambayo imekuwa nyenzo muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma za haki.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, aliwahimiza watumishi kuendelea kudumisha upendo, kuheshimiana na kushirikiana katika kutekeleza majukumu yao.

Pia alisisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, kuhakikisha usafi na usalama wa miundombinu ya Mahakama, kutumia mifumo ya TEHAMA kwa usahihi na kuwajibika kikamilifu katika maeneo yao ya kazi.

Hafla hiyo pia, ilitoa fursa kwa wawakilishi wa watumishi kutoka katika kila Mahakama kutoa salamu za ukaribisho kwa viongozi hao wapya na kuahidi ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya Mahakama.

Aidha, hafla hiyo ya utambulisho na ukaribisho wa viongozi wapya ni hatua muhimu katika kuimarisha mshikamano, kujenga uhusiano mzuri wa kikazi na kuweka msingi wa ushirikiano kati ya viongozi na watumishi.

Vilevile, hutoa fursa ya kuelekeza matarajio ya utendaji, kuimarisha uwajibikaji na kuongeza ari ya pamoja katika kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi kwa kuzingatia maadili, ueledi na matumizi bora ya mifumo ya kisasa ya Mahakama.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho cha kuwakaribisha Viongozi, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya, na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo akizungumza na watumishi katika kikao hicho. (hawapo pichani) kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya, akizungumza na watumishi wa kanda ya Mbeya katika kikao hicho. (hawapo pichani)

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika hafla fupi ya kuwakaribisha Viongozi wapya wa Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia kwa makini shughuli zilizokuwa zikiendelea katika kikao hicho.

 

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika hafla fupi ya kuwakaribisha Viongozi wapya wa Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia kwa makini shughuli zilizokuwa zikiendelea katika kikao hicho.

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika hafla fupi ya kuwakaribisha Viongozi wapya wa Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia kwa makini shughuli zilizokuwa zikiendelea katika kikao hicho

Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Happines Chuwa (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika kikao hicho kwa niaba ya watumishi.


Afisa Utumishi Mahakama Kuu na Mahakama ya Watoto Mbeya Bw. Ibrahim Mgallah (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho katika kikao hicho.






 

“OSHA ENDELEENI KUFANYA UKAGUZI WA MIUNDOMBINU MAHALI PA KAZI; NI TAKWA LA KISHERIA”

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa rai kwa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kuendelea kufanya ukaguzi katika miundombinu yote ya maeneo ya kazi ili kuhakikisha usalama mahali pa kazi sambamba na kutekeleza takwa la Sheria ya Afya na Usalama Kazini.

Mhe. Masaju ametoa rai hiyo leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania.

“Ushauri wangu kwenu ni kwamba endeleeni kufanya ukaguzi katika miundombinu yote kama ilivyotajwa katika Sheria ya Afya na Usalama Kazini, na ikiwemo miundombinu ya Mahakama. Sababu hii ya kwenu sio utashi, ni maelekezo ya sheria. Sheria lazima itekelezwe tu," amesema Jaji Mkuu na kuongeza:

"Na Mwalimu Nyerere aliwahi kusema mwaka 1988, alipokuwa anafunga mkutano wa ALAT, alisema hivi, 'Serikali ni Sheria.' Hakuna kitu kinaitwa Serikali bila sheria, na sheria zikishatungwa lazima zifuatwe.”

Mhe. Masaju aliongezea, “Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaweka msingi wa Utawala wa Sheria na inamtaka kila mtu kuitii Katiba hii na Sheria za Jamhuri ya Muungano, na kwamba kila mtu ana haki ya kuchukua hatua kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa kuhakikisha hifadhi ya Katiba na Sheria za Nchi.”

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu ameipongeza OSHA, chini ya Mtendaji Mkuu Bi. Khadija Mwenda, kwa kwenda mbali zaidi ya kusimamia Sheria, kufanya mafunzo na kutoa vitendea kazi vinavyozingatia mifumo ya kiorganomia (ergonomics) ili kuwakinga watumishi na magonjwa yatokanayo na mazingira ya kazi.

Ameongeza kuwa, haki ya kuishi imewekwa katika ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nayo inasema hivi, "Kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake kwa mujibu wa sheria." Amesema Sheria ya Afya na Usalama Kazini, msingi wake ni huo: watu kuishi. “Kazi hizi zisifanye tukafa, ndio maana inasisitiza... sasa ukishakufa una maana gani? Na... ukishakufa unaishia pale.”

Amesema, msingi mwingine wa Sheria ya Afya na Usalama Kazini ni Ibara ya 12 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, inayosema kwamba kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake. 

“Na sasa sisi Taifa hili lina kaulimbiu inayosema, "Kazi na Utu". Tufanye hizi kazi lakini tukiwa tumezingatia utu ikiwa ni pamoja na kuzingatia ustawi wetu, kwamba hizi kazi zisifanye tukafa mapema halafu kuwepo kwetu kukawa hakuna maana yoyote,” amesema Jaji Mkuu.

Amesema, suala hilo limehusishwa moja kwa moja na Ibara ya 14 ya Katiba inayofafanua haki ya kuishi, pamoja na Ibara ya 12 inayosisitiza heshima na utu wa binadamu, ikizingatiwa Kaulimbiu ya sasa ya Taifa ya "Kazi na Utu."

"Maendeleo yanapangwa na binadamu na ni kwa ajili yao; hayawezi kupangwa na mashine wala wanyama. Ndio maana uwekezaji katika afya zao ni muhimu. Kadri mtu anavyofanikiwa, ndivyo anavyotaka kuendelea kuishi ili atoe mchango kwa Taifa lake," amesisitiza Mhe. Masaju huku akiongeza kuwa mafunzo hayo yanaendana na Nguzo ya Pili ya Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inayolenga kujenga nguvu kazi yenye ujuzi, motisha na ubunifu na Kipaumbele cha kwanza cha Dira hiyo kinachohusu Utawala Bora na Haki.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, Taifa hili linastahili ustawi wa binadamu wote, wakiwemo Wakulima kwa wafanyakazi na wafanyabiashara na kila mmoja. Amesema, “Na sisi tunaofanya kazi, wawe Mahakimu au Waamuzi kama tulivyo sisi, na kila mmoja wetu anahitaji ustawi. Mafunzo haya pia yanatupeleka kwenye utekelezwaji wa hiyo Dira kwenye ustawi, lakini imeandamana na kitu cha msingi sana: haki, hivyo Mahakama itaendelea kusimamia utoaji haki ipasavyo.”

Ameongeza kuwa, Taifa jumuishi lenye ustawi ni Taifa ambalo halimwachi mtu nyuma, huku akirejea na kupongeza mafunzo ambayo OSHA wameshatoa kwa makundi mbalimbali ya watu. 

Katika hatua nyingine; Jaji Mkuu amemshukuru Rais Samia kwa Uteuzi wa Majaji tisa wa Mahakama ya Rufani kwa jitihada zake za makusudi za kuendelea kuimarisha Mhimili huo kupitia rasilimali watu na vitendeakazi.

“Ninamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha Mhimili huu wa Mahakama kwa rasilimaliwatu, vitendeakazi na rasilimali nyingine ili Mhimili huu uweze kuendelea kutekeleza jukumu lake la utoaji haki kwa ufanisi zaidi. Na kwa sababu hiyo, ninamshukuru kwa uteuzi huu alioufanya mwezi uliopita na akawaapisha hawa Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani tisa kwa wakati mmoja; hilo ni kazi kubwa sana amefanya. Mheshimiwa Rais namshukuru sana sio kazi ndogo,” amesema Mhe. Masaju.

Ameongeza kuwa, “Unapomteua Jaji, umeteua watu wengine tisa nyuma yake, kwa uchache. Kwa hiyo, anapoteua ni kwamba amedhamiria kwa dhati kabisa. Na hii inaonesha utayari wake wa kuendelea kuimarisha Mhimili huu kuweza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ipasavyo ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninamshukuru sana.”

Jaji Mkuu amesema, uamuzi wa hivi karibuni wa Mkuu wa Nchi wa kuteua na kuwaapisha Majaji tisa wa Mahakama ya Rufani kwa wakati mmoja umetajwa kama uthibitisho wa utayari wake wa dhati wa kuhakikisha haki inatendeka kwa ufanisi mkubwa nchini. 

Aidha, Jaji Mkuu amewapongeza Majaji walioteuliwa hivi karibuni, ambapo amesema, “Ninakutana nanyi mara ya kwanza katika tukio hili rasmi. Niwapongeze sana kwa mwenendo wenu mwema, kuwa na sifa za kuweza kuteuliwa hata kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani. Na Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki sana katika maisha yenu, katika utumishi wenu, na katika shughuli zenu.”

Kadhalika Mhe. Masaju amempongeza Jaji Mlyambina aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama kwa kuwa na ushirikiano mzuri na Wadau wa Haki Kazi ambapo umeiwezesha Mahakama kunufaika na mambo mengi ikiwemo mafunzo kwa Watumishi wake wakiwemo Majaji, Naibu Wasajili, Mahakimu, Madereva na kadhalika.

Viongozi wengine wakuu waliohudhuria tukio hilo ni pamoja na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe.Dkt. Paul Faustine Kihwelo, Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu, baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania, Watumishi wa OSHA, watumishi wengine wa Mahakama.

Wengine waliohudhuria ni pamoja na Wataalamu Wabobezi/Madaktari na Wauguzi kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na Chuo Kikuu cha Tiba na Afya Muhimbili (MUHAS) na Taasisi ya Mifupa (MOI).

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akifungua Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Majaji na Viongozi wengine wa Mahakama na OSHA wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipokuwa akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akitoa neno wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda akitoa neno wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Antony Jingu (kushoto) pamoja na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Victor Kategere wakiwa katika hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu-Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick (kulia) pamoja na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bw. Victor Kategere wakifuatilia kinachojiri katika hafla ya ufunguzi wa mafunzo hayo.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimpatia zawadi ya saa Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda baada ya hafla ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda (kulia) akimpatia zawadi Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ya Vifaa tiba vya huduma ya kwanza (First Aid Tool Box) baada ya hafla ufunguzi wa Mafunzo ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) yanayotolewa kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 02 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya Mahakama ya Rufani (waliosimama) wanaopatiwa mafunzo ya Usalama na Afya mahali pa Kazi yanayotolewa na OSHA. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma (aliyesimama). Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania (waliosimama). Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Watumishi wa OSHA (waliosimama). Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

Meza Kuu katika picha ya pamoja na Wataalamu wa Afya kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili na MOI.

Meza Kuu katika picha ya pamoja na Wawezeshaji wa Mafunzo ya Usalama na Afya mahali pa Kazi yanayotolewa na Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

(Picha na MARY GWERA & JEREMIA LUBANGO, Mahakama)