Jumanne, 9 Juni 2026

JAJI MWENDA AWASISITIZA MAJAJI, MAHAKIMU SINGIDA KUZINGATIA MATUMIZI YA TEHAMA

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda amewasisitiza Wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Singida kuzingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ikiwa ni jitihada za kupunguza matumizi ya karatasi.

Akifungua mkutano wa Chama hicho hivi karibuni uliofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu Singida, Mhe. Mwenda alisema, “nasisitiza kuendelea kutumia TEHAMA kwenye shughuli zetu za kila siku ikiwemo kusikiliza mashauri, maandalizi ya nakala za hukumu, mienendo ya kesi na shughuli nyingine.”

Vilevile, aliwaeleza wajumbe kuwa, jumla ya watumishi 25 wa kada mbalimbali kutoka Mahakama Kuu hadi Mahakama za Mwanzo Singida, walikwenda Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita kujifunza kuhusu matumizi ya TEHAMA katika shughuli mbalimbali za kimahakama na kwamba, zoezi hilo ni endelevu na linaenda sambamba na ununuzi wa vifaa vyenye uwezo kwa kushirikiana na Menejimenti.

Amesema, hatua hiyo ni katika kuhakikisha matumizi ya karatasi yanapungua kwa kiasi kikubwa ili kuendana na kasi ya teknolojia.

Aidha, katika kikao hicho aliwasisitiza wajumbe hao wa TMJA kufanya kazi kwa ushirikiano na watumishi wa kada nyingine ili kufikia malengo ya Taasisi.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi huyo amewasisitiza Mahakimu wafawidhi wa Wilaya kusimamia watumishi walio chini yao ili kuendelea kuwa na nidhamu nzuri kazini na hata nje ya mazingira ya kazi.

Akihitimisha mkutano huo, Mhe. Mwenda amewasisitiza Mahakimu kuviishi viapo vyao vya kazi na kuwajibika ipasavyo kufanya kazi kwa mujibu wa kanuni na taratibu na kuendelea kusimamia maelekezo yote yanayotolewa na viongozi pasipo kuogopa kukosolewa kwani kiongozi mzuri ni yule ambaye anakubali kukosolewa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyesimama) akizungumza na wajumbe (hawapo katika picha) katika ufunguzi wa Mkutano wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Singida. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Nenelwa Mwihambi na kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi.


Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida na Naibu Msajili Mteule, Mhe Allu Nzowa (wa kwanza kulia ) pamoja na wajumbe wengine wa TMJA Singida wakiwa katika mkutano wa Chama hicho. Anayefuata ni Mhe. Fadhili Luvinga, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Singida, akifuatiwa na Mhe. Aloyce Masua, Hakimu Mahakama ya Wilaya Singida, akifuatiwa na Mhe. Luzango Khamsini, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Iramba, akifuatiwa na Mhe. Alisile  Mwankejela, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Manyoni na Mhe. Egdius Byabajuka, Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Shelui.

 Sehemu ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutoka Vituo mbalimbali vya Mkoa wa Singida waliohudhuria katika Mkutano huo.

 Sehemu ya wajumbe wa Mkutano huo wakifuatilia kwa umakini kilichokuwa kikijiri.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Jumatatu, 8 Juni 2026

RC KATAVI AWAHIMIZA TANESCO KUTATUA CHANGAMOTO YA UMEME KWENYE JENGO LA IJC

Na. ALLY RAMADHANI – Mahakama, Katavi

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko hivi karibuni alifanya ziara ya kutembele Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi katika ziara hiyo amefanikiwa kutembelea mradi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).

Katika ziara hiyo Mhe. Mkuu wa Mkoa amefanikiwa kubaini changamoto ya umeme inayolitesa jengo hilo la Mahakama, huku akitioa maelekezo kwa Meneja wa TANESCO Mkoa wa Katavi kwa kumpatia masaa 48 (siku mbili) wawe wametatua changamoto hiyo.

“Changamoto hii ya umeme katika jengo la Mahakama yetu sifurahishwi nayo, hivyo basi nampatia siku mbili Meneja wa TANESCO Mkoa tatizo hili la umeme katika jengo letu la Mahakama liwe limepatiwa jawabu,” alisema Mhe. Mwanamvua Mrindoko

Aidha, kupitia ziara hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya, amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Katavi kwa kusema “Tunatambua mchango wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi kwa kufatilia upatikanaji wa eneo hili na leo unakuja kutembelea jengo likiwa limekamilika tunashukuru sana na nikupongeze kwa hilo”.

Hata hivyo, Mhe. Isaya amemuomba Mkuu wa Mkoa swala la kupatiwa maeneo kwa ajili ya uanzishwaji wa Mahakama za Mwanzo kutokana na jiografia ya Katavi ili huduma za utoaji haki zisogezwe karibu na wananchi.

Pia Jaji Mfawidhi hiyo, alisema kuwa, Mahakama ya Tanzania inasisitiza Utoaji Haki kwa wakati mapema ipasavyo, hivyo basi Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huo kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora.

Kupitia ziara hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Katavi amewatangazia wananchi wa Katavi kuwa huduma za Mahakama Kuu zimeanza mkoani hapo tangu tarehe 30 Machi, 2026, hivyo wananchi wasisumbuke kwenda Sumbawanga kwa kufuata huduma za Mahakama Kuu wakati Katavi wanatoa huduma hizo.

Mkuu wa mkoa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko (Katikati Mwenye nguo nyeupe alievaa shungi), wa Kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Katavi Mhe Godfrey Ntemi Isaya, na Wakwanza kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mhe. Bi Jamila Yusuph Kimaro wakiwa kwenye picha ya Pamoja na baadhi ya watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Katavi katika ziara ya Mkuu wa Mkoa Katavi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Katavi bi. Silivia Lushasi akielezea juu ya uwepo wa ofisi za wadau wa Mahakama ndani ya jengo la IJC katika ziara ya Mkuu wa Mkoa Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Katavi, Mhe Godfrey Ntemi Isaya akitoa taarifa fupi wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa Katavi.  

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe Mwanamvua Mrindoko akisalimiana na watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi wakati wa ziara yake alipotembelea Mahakama kuu Katavi.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe Mwanamvua Mrindoko (wa pili kutoka kushoto) akitoa maagizo juu kutatuliwa kwa changamoto ya umeme katika jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi.

(Habari hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

JAJI MFAWIDHI SONGWE AONGOZA HAFLA YA UZINDUZI WA MAHAKAMA YA MWANZO KANGA

Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata aongoza hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga iliyopo Kata ya Kanga, Wilaya ya Songwe hivi karibuni

Hafla hiyo, ilifanyika katika viunga vya Mahakama ya Mwanzo Kanga na ilihudhuriwa na sehemu ya Viongozi wa ngazi ya Mkoa wa Songwe pamoja na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Marvis Miti.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Songwe Bw. Agapto Thomas Kilongosi alitoa pongezi kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuendelea kuimarisha huduma za upatikanaji wa haki ikiwa ni pamoja na kukamilisha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga na kuahidi kuendelea kushirikiana na Mahakama katika kuboresha upatikanaji wa haki katika Jimbo la Songwe.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kanga Bw. Prosper Laurent Nkinga, aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kusogeza huduma ya Mahakama katika Kata ya Kanga na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano na kulinda miundombinu ya Mahakama hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Songwe Mhe. Fadhili Nkurlu aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kusogeza huduma ya upatikanaji wa haki katika Kata ya Kanga na maeneo ya Jirani kwa kujenga Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Mhe. Fadhili Nkurlu aliahidi kuendelea kushirikiana na Mahakama ikiwa ni pamoja na kulinda miundombinu ya Mahakama ili kuhakikisha huduma za utoaji wa haki zinatolewa ipasavyo katika Mahakama ya Mwanzo Kanga na Wilaya ya Songwe kwa ujumla.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Omari Makame alimshukuru Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga kwa ushirikiano aliouonesha wakati Mkoa wa Songwe ulipokuwa ukipata huduma za Mahakama kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya, Pia alimkaribisha Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata na aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano ili kufikisha huduma ya upatikaji wa haki kwa wanachi wa Mkoa wa Songwe.

Mkuu wa Mkoa huyo akatumia jukwaa hilo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Goerge Masaju kwa maono yao ya kuendelea kuboresha miundombinu ya Mahakama ya Tanzania, Pia aliwaomba na kuwahimiza wananchi wa Kanga na Songwe kwa ujumla kuilinda na kuitunza miundombinu ya Mahakama kwa sababu imejengwa ili kusogeza huduma ya upatikanaji wa haki katika maeneo yao.

Vilevile, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga alipongeza uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga na alishukuru kwa ushirikiano alioupata wakati Mkoa wa Songwe ulivokuwa ukipata huduma kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, pia alipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kusogeza huduma ya Makama Kuu na Mahakama ya Rufani kwa kuanzisha Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe.

Naye, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata alieleza kuwa, Mahakama ya Mwanzo Kanga imejengwa ili kusogeza huduma ya utoaji wa haki katika Kata ya Kanga na maeneo ya jirani pia aliwataarifu wananchi kwamba, huduma za Mahakama kuanzia ngazi ya Mahakama ya Mwanzo, Mahakama ya Wilaya, Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani zinatolewa na kupatikana ndani ya Mkoa wa Songwe.

Mhe. Malata alisisitiza kwamba, wananchi wote wanawajibika kulinda na kutunza miundombinu ya Mahakama kwa sababu ni mali ya umma na imejengwa kwa kodi za wananchi, pia Mhe. Malata aliwapongeza wananchi wa Kanga kwa kusimama kidete kuitunza na kuilinda Mahakama ya Kanga ilipotaka kuchomwa moto mwezi Oktoba mwaka jana.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati) akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga, wengine (wa kwanza kulia) ni Mkuu wa Wilaya ya Songwe Mhe. Fadhili Nkurlu, (wa pili kulia) ni Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Omari Makame, (wa nne kutoka kulia) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga na (wa tano kulia) ni Diwani wa Kata ya Kanga Bw. Prosper Laurent Nkinga.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa kamati ya ulinzi na usalama Mkoa wa Songwe mara baada ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata akipanda mti wa kivuli katika viunga vya Mahakama ya Mwazo Kanga baada ya uzinduzi wa Mahakama hiyo.

Sehemu ya wageni waalikwa waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kushoto), Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Makame (wa tatu kushoto), Mkuu wa Wilaya ya Songwe Mhe. Fadhili Nkurlu (wanne kushoto) na Katibu wa Mhe. Mbunge wa Jimbo la Songwe Bw. Agapto Kilongosi katika zoezi la kukata utepe kuashiria uzinduzi wa Mahakama hiyo Mwanzo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata akihotubia wakati wa uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga akitoa neno katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Bw. Sostenes January Mayoka akifurahia jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde akitoa neno la ukaribisho katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Kanga.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)




MAHAKAMA KUU MBEYA YAZINDUA MPANGO WA MALEZI YA KITAALUMA KWA MAHAKIMU

Na. MUKSINI NAKUVAMBA- Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, amezindua rasmi Mpango wa Malezi ya Kitaaluma kwa Mahakimu (Mentorship Program) hivi karibuni. Mpango huo unalenga kuimarisha utendaji kazi wa Mahakimu na kuongeza imani ya wananchi kwa Mahakama pamoja na huduma zinazotolewa mahakamani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Tiganga alisema kuwa, mpango huo umeanzishwa kwa lengo la kuwajengea Mahakimu uwezo zaidi wa kiutendaji kupitia ushauri, mwongozo na malezi kutoka kwa viongozi na watendaji wenye uzoefu mkubwa katika tasnia ya sheria na utoaji wa haki.

“Ukimpata mtu wa kukwambia madhaifu yako, huyo anakujenga. Utafakari ushauri huo na kuufanyia kazi akisisitiza umuhimu wa kupokea ushauri kwa lengo la kujiboresha kitaaluma na kiutendaji,” alisema Mhe. Tiganga.

Aidha, Mhe. Tiganga aliongeza kuwa Mahakama inatarajia mpango huo kuzalisha viongozi bora wenye uwezo wa kuongoza, kukua binafsi na kuwainua wengine katika taaluma yao.

“Tunatarajia kuwa, baada ya kumalizika kwa programu hii, tutakuwa na viongozi wazuri wanaotambua vyema dhana ya uongozi, kukua na kukuza wengine kitaaluma na kiutendaji,” alisisitiza Mhe. Tiganga.

Kwa upande wao, baadhi ya Mahakimu walioshiriki katika uzinduzi wa Mpango huo wamepongeza hatua hiyo, wakieleza kuwa mpango huo utakuwa chachu ya kuboresha utendaji kazi wao na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kimahakama.

“Tumelipokea jambo hili kwa mikono miwili na tunaamini kuwa litatunufaisha sana sisi Mahakimu na kuboresha utendaji kazi wetu. Tunatarajia kujifunza zaidi na kufikia viwango vya juu zaidi vya utendaji kazi katika vituo vyetu vya kazi,” alisema Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Paul Ntumo.

Uzinduzi huo, ulihusisha Mahakimu kutoka maeneo mbalimbali, ambapo sehemu yao walishiriki kupitia mfumo wa mkutano mtandao (video conference), jambo lililowezesha ushiriki mpana wa watumishi wa Mahakama ndani ya Masjala Ndogo ya Mbeya.

Mpango wa Malezi ya Kitaaluma kwa Mahakimu unatarajiwa kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha uwezo wa watumishi wa Mahakama, kuongeza ubora wa utoaji wa haki na kuendeleza dhamira ya Mahakama ya Tanzania ya kutoa huduma bora kwa wananchi kwa wakati na kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) akiongoza uzinduzi huo, kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo, na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (kulia).

Sehemu ya Mahakimu walioshiriki katika kikao cha uzinduzi huo.

Sehemu ya Mahakimu walioshiriki katika uzinduzi huo kwa njia ya Mtandao (Video conference).


Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (wa kwanza kushoto), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer (katikati), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba (kulia) wakifuatilia kwa karibu kikao cha uzinduzi wa program ya Malezi kitaaluma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



MAHAKAMA KUU YAFANYA ZIARA YA UKAGUZI WA GEREZA KUU LA RUANDA MBEYA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA, Mahakama Mbeya

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu amefanya ziara ya kutembelea Gereza Kuu la Ruanda jijini Mbeya hivi karibuni kwa ajili ya kusikiliza changamoto mbalimbali za wafungwa na Mahabusu wa Gereza hilo, ikiwa ni zaira ya ukaguzi wa kawaida gerezani hapo katika kipindi cha Aprili –Juni, 2026.

Akiwasilisha taarifa fupi ya Gereza Kuu la Ruanda Mkuu wa Gereza Kamishna Msaidizi wa Magereza ACP Christopher Fungo, alieleza hali za wafungwa na mahabusu waliopo gerezani hapo.  

Katika ziara hiyo Mhe. Temu alipata fursa ya kukutana na Wafungwa na Mahabusu ambao waliwasilisha changamoto zao kwa viongozi mbalimbali wa Mahakama na wadau wengine wa haki jinai alioambatana nao katika ziara hiyo.

Katika risala yao wafungwa na mahabusu waliweza kuwasilisha changamoto mbalimbali zinazowakabili gerezani hapo. Aidha Mhe. Temu aliahidi kuzishughulikia changamoto zote zilizowasilishwa katika risala zao na zile ambazo zipo nje ya uwezo kuziwasilisha katika mamlaka husika.

Kwa upande wake Mkuu wa Gereza Ruanda ACP Christopher Fungo alitoa shukurani zake kwa ujio wa ziara hiyo, kwa kuwa umekuwa na tija kubwa kwao kwa kutoa fursa kadhaa ikiwemo matendo ya huruma na kushughulikia suala la kupunguza mlundikano wa mahabusu gerezani hapo.

Katika ziara hiyo Mhe. Temu aliambatana na Viongozi mbalimbali wa Mahakama akiwemo Kaimu Mtendaji Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Alintula Ngalile, Mahakimu Wakazi wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Mwenyekiti TLS Chapta ya Mbeya, Maafisa wa TAKUKURU, Ofisi ya Upelelezi Mkoa wa Mbeya, Afisa Huduma na Uangalizi Mbeya na wadau wengine wa Haki jinai.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (wanne kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na viongozi wa Grezeza Ruanda na Mahakama kanda ya Mbeya na wadau wengine wa haki jinai alioambatana nao mbele ya Lango la Gereza Kuu Ruanda Mbeya. watatu kulia ni Mkuu wa Gereza Kuu Ruanda Mbeya Kamisha Msaidizi ACP Christopher Fungo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer (watano kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba (wapili kulia).

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (aliyeketi mbele) na wadau wengine wa haki jinai alioambatana nao katika ziara hiyo wakiwa ndani ya ofisi ya Mkuu wa Gereza la Ruanda Mbeya. Aliyesimama ni Mkuu wa Gereza Kuu la Ruanda Mbeya Kamishna Msaidizi wa Magereza ACP Christopher Fungo.


Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kulia) akilakiwa na Mkuu wa Gereza Kuu la Ruanda Mbeya Kamishna Msaidizi wa Magereza ACP Christopher Fungo (kushoto) wakati wa ziara hiyo

Viongozi wa Mahakama na Maafisa kutoka Taasisi mbalimbali za haki jinai walioshiriki katika ziara hiyo wakiwa Mbele ya kasha linalotoa huduma ya mahakama mtandao Gereza Kuu Ruanda

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (wa kwanza aliyeketi kushoto) na wadau wengine wa haki jinai alioambatana nao katika ziara hiyo wakiwa ndani ya ofisi ya Mkuu wa Gereza la Ruanda Mbeya. Aliyesimama ni Mkuu wa Gereza Kuu la Ruanda Mbeya Kamishna Msaidizi wa Magereza ACP Christopher Fungo.

DCM YAFANYA TATHIMINI YA MWENENDO WA MAHAKAMA INAYOTEMBEA MBEYA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) ilifanya ziara katika Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya hivi karibuni kutathimini juu ya hali ya utoaji wa huduma zitolewazo na Mahakama Inayotembea katika Masjala hiyo.

Katika kikao kilichofanyika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Masjala hiyo kikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) Mhe. Moses Betwel Ndelwa, ili kujadili juu ya changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo katika utoaji wa huduma za Mahakama Inayotembea.

 Aidha, Mhe. Ndelwa aliwasisitiza wasimamizi na watumiaji wote wa gari la Mahakama Inayotembea (Mobile court Service) kuzingatia misingi na taratibu za matumizi ya gari hilo.

“Matumizi ya Gari la Mahakama Inayotembea (Mobile court Service) yazingatie huduma za Mahakama Inayotembea tu na si vinginevyo,” alisisitiza Mhe. Ndelwa

Mhe. Ndelwa aliongeza kuwa, usikilizwaji wa mashauri kwenye Mahakama Inayotembea usizidi siku thelathini (30) tangu tarehe ya kufunguliwa kwa shauri. Sambamaba na hilo aliwasisitiza watumishi wanaofanya kazi katika Mahakama Inayotembea kufanya kazi kwa bidii na uadilifu na kuwa mfano wa kuigwa katika utoaji wa huduma bora za kimahakama.

Vilevile, Mhe. Ndelwa aliwashukuru Idara ya fundi sanifu, umeme, maji na TEHAMA Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya kwa kuwa mstari wa mbele katika kutatua changamoto ndogo ndogo zinazojitokeza kwenye Gari la Mahakama Inayotembea na kupelekea utendaji bora wa kazi. 

Pia aliwaasa Mahakimu Wafawidhi Mkoa na Wilaya ya Mbeya kufanya ziara za mara kwa mara ili kufuatilia hali ya huduma zitolewazo kwenye Mahakama inayotembea.

Sambamba na kikao hicho, ugeni huo ulifanya ziara ya ukaguzi wa miundombinu ya Gari linalotoa huduma ya Mahakama inayotembea na kutembelea moja ya kituo cha kutolea huduma za Mahakama inayotembea katika Kata ya Uyole ndani ya jiji la Mbeya na kujionea Mazingira ya utolewaji wa huduma za Mahakama Inayotembea kwa  wananchi.

Mwenyekiti wa kikao, Naibu Msajili Mahakama ya Tanzania kutoka Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) Mhe. Moses Betwel Ndelwa (katikati) akizungumza katika kikao cha Tathmini ya utendaji kazi wa Mahakama Inayotembea, kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mhe. Sifa Jacob.

Maafisa Mahakama kutoka Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) wakiwa katika ziara ya kutembelea moja ya kituo cha kutolea huduma ya Mahakama inayotembea (Mobile Court Service) 

Maafisa Mahakama kutoka Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) wakiwa katika ziara ya kutembelea moja ya kituo cha kutolea huduma ya Mahakama inayotembea (Mobile Court Service) 


Maafisa Mahakama kutoka Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) wakiwa katika ziara ya kutembelea moja ya kituo cha kutolea huduma ya Mahakama inayotembea (Mobile Court Service) wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Kata ya Uyole Bi. Sikuzani Kibona


Maafisa Mahakama kutoka Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) na Viongozi wa Mahakama Kuu kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya Pamoja na Watumishi wanaohudumu katika Mahakama inayotembea (Mobile Court Service), Nyuma yao ni Gari linalotoa huduma ya Mahakama inayotembea likiwa mbele ya jengo la mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

Sehemu ya washiriki wa kikao hicho cha tathmini.

Sehemu ya washiriki wa kikao hicho cha tathmini.



Jumapili, 7 Juni 2026

TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA MASJALA NDOGO IRINGA AFARIKI DUNIA

Bw. Renatus Mlingi enzi za uhai wake.

 TANZIA 

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake Bw. Renatus Mlingi aliyekuwa Dereva Mwandamizi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Iringa. 

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, marehemu Renatus amefariki dunia jana tarehe 06 Juni, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa iliyopo jijini Dodoma alipokuwa anapatiwa matibabu baada ya kupewa rufaa kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa ambapo ndipo alipokuwa akitibiwa awali.

Bi. Melea amesema kuwa, Marehemu Bw. Renatus anatarajiwa kuzikwa Iringa Mjini siku ya Jumanne tarehe 09 Juni, 2026.

Marehemu Renatus alizaliwa tarehe 21 Januari, 1974 na aliajiriwa na Mahakama ya Tanzania tarehe 01 Oktoba, 2013 kwa Kada ya Dereva Daraja II.

Mahakama ya Tanzania inaungana na ndugu, jamaa na marafiki katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza msiba huo mzito wa kuondokewa na Mpendwa wetu Renatus Mlingi.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA, JINA LAKE LIHIMIDIWE.

 

Jumapili, 31 Mei 2026

TMJA GEITA YAFANYA ZIARA YA KUBADILISHANA UZOEFU MAHAKAMA KUU KIGOMA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile amewaongoza Wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma na Geita katika Mafunzo ya kubadilishana uzoefu wa utendaji kazi.

Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 29 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama ya Wazi uliopo katika Jengo la Mahakama Kuu Kigoma.

Akizungumza na wajumbe wa TMJA wa matawi hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Rwizile alieleleza lengo la ziara hiyo ni kuwawezesha Majaji na Mahakimu kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma na Geita kuendelea kujinoa kwa njia ya kubadilishana uzoefu ili kuongeza ujuzi katika utendaji kazi wa kila siku sambamba na kuleta tija na ufanisi wa utoaji huduma ya Utoaji Haki mapema ipasavyo.

“Waheshimiwa (Majaji na Mahakimu) kwa kupitia Chama chetu cha TMJA niwakaribishe Kigoma, huku tunafanya tofauti hivyo, kupitia ziara yenu Geita tutajifunza mengi nanyi mtajifunza pia kwani yapo mengi ambayo kwetu sisi yanapatikana Kigoma tu, tumejipanga kuboresha maeneo mengi baada ya hii ziara ya kubadilishana uzoefu katika utendaji wetu,” alisema Mhe. Rwizile.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina alieleza kwa ufupi historia ya maendeleo ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)k atika Masjala hiyo.

Alibainisha kuwa, juhudi za matumizi ya TEHAMA zilianza  kufuatia maelekezo na maono ya Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, alisisitiza kuwa, Mahakama Kuu Geita iwe mfano wa kuigwa katika matumizi ya TEHAMA ndani ya Mahakama.

Mhe. Mhina aliendelea kusema kuwa, Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Prof. Juma alisimamia kwa karibu utekelezaji wa maono hayo kwa kuwahamasisha watumishi na kuwaeleza msimamo wake kwamba matumizi ya karatasi yanapaswa kupunguzwa kwa kiwango kikubwa, kwani Mahakama isiyotumia karatasi inawezekana.

Aidha, alieleza kuwa kutokana na Mahakama za Mwanzo kutokuwa na mfumo rasmi wa matumizi ya TEHAMA, aliwaagiza Ofisa TEHAMA pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutafuta njia mbadala za kuondokana na matumizi ya karatasi. Kufuatia maelekezo hayo, timu husika ilibuni mifumo mitano yenye sifa na uwezo tofauti. Baada ya kufanya tathmini, walibaini mfumo mmoja uliokuwa bora zaidi, ambao ndio unaotumika hadi sasa.

Mhe. Mhina aliongeza kuwa, baada ya kushirikisha Mahakama Kuu mbalimbali nchini kuhusu mfumo huo, walipokea ushauri wa kuuboresha kwa kuanzisha Kituo cha Kuhifadhi na Kusimamia Taarifa (Data Center) kitakachowezesha upatikanaji wa taarifa za Mahakama za Mwanzo kwa urahisi badala ya kutegemea mawasiliano ya simu.

Kutokana na ushauri huo, waliibua wazo la kuanzisha (Repository System), mfumo unaomuwezesha kila Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo kupakia (upload) kumbukumbu zote za mashauri anayoyasimamia.

Amesema, Mfumo huo unarahisisha upatikanaji wa nyaraka za mashauri pale rufaa inapowasilishwa katika Mahakama za juu. Vilevile, unawasaidia Majaji, Naibu Wasajili, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mikoa na Wilaya pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama kufanya ukaguzi na ufuatiliaji wa kazi za Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kwa urahisi zaidi, kupitia akaunti maalum zinazowawezesha kuona nyaraka na taarifa zote zilizopakiwa kwenye mfumo huo.

Aidha, ziara hiyo iliongozwa na Jaji Mfawidhi Geita ambaye pia alipata nafasi ya kupanda miti ya kivuli katika Mahakama ya Mwanzo Bangwe, vilevile TJMA pia walishiriki mashindano ya michezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Mchezo wa Mpira wa Miguu, Kuvuta Kamba, Riadha ya mbio fupi na kukimbia kwenye magunia.

Katika michezo hiyo kipindi cha kwanza Geita ilionekana kuwa kasi sana kwa kushinda bao tatu kwa nunge kutoka timu ya Kigoma. Magoli hayo yalifungwa ndani ya dakika 90.

Sehemu ya Wajumbe wa Chama Cha Mahakimu na Majaji Tanzania kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Kigoma na Geita wakisikiliza kwa makini mada iliyokuwa ikiwasilishwa katika kikao hicho cha kubadilishana uzoefu wa utendaji wa kazi kati ya Mahakama Kuu Kigoma na Mahakama Kuu Geita tarehe 29, Mei 2026. Wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile, kulia kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, wa kwanza kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi na wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe.Griffin Mwakapeje. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akifungua kikao kazi cha kubadilishana uzoefu kati ya Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Geita na Wanachama wa TMJA Kigoma kilichofanyika tarehe 29 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Kevin Mhina akipanda mti wa kumbukumbu katika eneo la Mahakama ya Mwanzo Bangwe Kigoma wakati wa ziara ya kubadilishana uzoefu wa utendaji kazi  kati ya TMJA Geita na Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitambulisha wajumbe wa TMJA tawi la Kigoma, kwenye kikao cha kubadilishana uzoefu wa utendaji kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masijala ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna akifanya utambulisho wa wajumbe wa TMJA tawi la Geita kwenye kikao cha kubadilishana uzoefu wa utendaji kazi kati ya TMJA Geita na TMJA Kigoma kilichofanyika tarehe 29 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Mhe. Misana Majura akiwasilisha mada ya namna bora ya kusikiliza Mashauri ya Mirathi ikiwa ni sehemu ya kubadilishana uzoefu katika eneo hilo, katika kikao kazi kati ya TMJA Geita na TMJA Kigoma kilichofanyika tarehe 29 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Picha ya pamoja ya Wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma na Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Geita. Aliyeketi katikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile,  wa tatu kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, wa tatu kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe.Griffin Mwakapeje, wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya Buhigwe na Mwenyekiti wa Tawi la TMJA Kigoma, Mhe. Venance Mwakitalu, wa pili kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Nyang’hwale,  Mhe. Robert Nyando.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)