Ijumaa, 13 Machi 2026
JAJI MKUU AWAAPISHA WAJUMBE WA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA
Na LYDIA CHURI, Tume ya Utumishi wa Mahakama
Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume
ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. George Masaju leo tarehe 13 Machi, 2026
amewaapisha wajumbe wanne wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Katika hafla iliyofanyika leo kwenye Ofisi za Tume ya
Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma, Jaji Mkuu amemuapisha Jaji wa Mahakama ya
Rufani ya Tanzania, Mhe. Gerson Mdemu kuwa Mjumbe wa Tume kufuatia uteuzi uliofanywa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Aidha, Jaji Mkuu pia amemuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kufuatia
kuteuliwa kwa mara ya pili na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa
Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na
Madiwani uliofanyika Oktoba 29, 2025.
Jaji Mkuu pia amewaapisha kwa mara ya pili Mawakili
Bahame Tom Nyanduga na Dosca Kemilembe Mutabuzi kuwa Wajumbe wa Tume ya
Utumishi wa Mahakama baada ya kumaliza kipindi chao cha miaka mitatu cha kuwa
Wajumbe wa Tume na kuteuliwa tena na Rais kushika nafasi hiyo kwa mujibu wa Ibara
ya 112 (1) (e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania.
Tume ya Utumishi wa Mahakama inaundwa na wajumbe
wafuatao; Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye ni Mwenyekiti, Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Wajumbe wawili wanaoteuliwa na Rais.
Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo kilichoundwa kwa
mujibu wa Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya
mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Sura ya 237.
Chombo hiki kimeundwa kwa lengo la kusimamia utendaji kazi wa Mahakama ya
Tanzania ikiwa ni pamoja na kusimamia Ajira na Nidhamu za Watumishi wa Mahakama.
MSAJILI MAHAKAMA YA RUFANI TANZANIA ASISITIZA UMUHIMU WA KUTUMIA TEKNOLOJIA MAHAKAMANI
Na JAMES BUSANYA & HALIMA MNETE- Mahakama Dodoma.
Msajili
wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert, amesisitiza
umuhimu wa matumizi ya mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.
Mhe. Herbert ametoa msisitizo huo leo tarehe 13 Machi,
2026, wakati anafunga mafunzo ya siku tano kati ya Maofisa wa Mahakama ya Tanzania na Mahkama
ya Zanzibar yaliyokuwa
yanafanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma.
Msajili wa Mahakama ya Rufani ameeleza kuwa teknolojia inaweza kusaidia kuongeza ufanisi wa
kazi pamoja na kupunguza muda wa usikilizaji wa mashauri.
“Ni
muhimu kuendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika Mahakama
zetu, ikiwemo usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mfumo wa kielektroniki, jambo
ambalo linaweza kusaidia kuondoa mlundikano wa mashauri na kuongeza ufanisi
katika utoaji wa haki,” amesema.
Akizungumzia mafunzo hayo, Mhe. Herbert amewasihi washiriki
kutumia maarifa waliyoyapata katika kuboresha utendaji kazi ndani ya Taasisi
zao na kuimarisha utoaji wa haki kwa wananchi.
Amesema kuwa
mafunzo ya kubadilishana uzoefu ni muhimu katika kujenga uwezo wa watumishi wa Mahakama,
hususan katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiutendaji pamoja na
kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia.
Naye Naibu
Mrajisi wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Faraji Shumari Juma, akizungumuza kwenye hafla hiyo alitoa shukrani kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuandaa mafunzo
hayo muhimu, akisema kuwa yamewasaidia washiriki kupata maarifa na uzoefu mpya
wa kiutendaji.
Aidha,
aliomba ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na Mahkama ya Zanzibar
uendelee kuimarishwa ili kusaidia Taasisi hizo
kujifunza zaidi kutoka kwa kila upande.
Alieleza
kuwa ushirikiano huo ni muhimu hasa katika kuboresha matumizi ya mifumo ya
kiteknolojia kwenye uendeshaji na usikilizaji wa mashauri kwa
njia ya kidijitali ili kuongeza ufanisi na kuharakisha upatikanaji
wa haki kwa wananchi.
Wakati wa mafunzo
hayo ya siku tano yaliyoanza tangu
tarehe 9 Machi, 2026, washiriki wamepata
fursa ya kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali ya utendaji kazi, matumizi
ya mifumo ya kidijitali, maadili ya kazi pamoja na mbinu za kuboresha utoaji wa
huduma za Mahakama.
Washiriki wameeleza
kufurahishwa na elimu waliyoipata na kuahidi kutumia maarifa hayo katika
kuboresha utendaji wa kazi katika Mahakama zao.
NAIBU MSAJILI WA MAHAKAMA KUU KANDA YA LINDI AFANYA KIKAO NA WATUMISHI
Na. Hilary Lorry & Winifrida Kisamo– Mahakama, Lindi
Watumishi wa
Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi pamoja na Mahakama ya Wilaya ya Lindi, tarehe 11
Machi 2026 wamefanya kikao kazi na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Lindi,
Mhe. Elia
Joseph Mrema ambaye amesema Mahakama Kuu Kanda hiyo inayotarajiwa kuanza
kutoa huduma za Mahakama Kuu kwa wananchi hivi karibuni kuanzia sasa.
Kikao hicho kimefanyika
katika ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi ikiwa ni sehemu ya
maandalizi ya kuanza kwa shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Lindi.
Akizungumza wakati
wa kikao hicho, Mtendaji wa Mahakama Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela
aliwapongeza watumishi wa Mahakama hizo kwa uwajibikaji wao na
uchapakazi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Alieleza kuwa
watumishi hao wamekuwa wakitekeleza majukumu yao kwa bidii na kila mmoja
anatambua wajibu wake katika kuhakikisha huduma za kimahakama zinatolewa kwa
ufanisi.
Aidha,
Mtendaji huyo aliwasisitiza watumishi kuendelea kudumisha usafi wa mazingira
katika majengo ya Mahakama pamoja na kuyatunza ipasavyo, akibainisha kuwa
mazingira safi na yakitunzwa vizuri huchangia kuongeza ufanisi katika utendaji
kazi na kutoa taswira nzuri kwa wananchi wanaofika kupata huduma.
Kwa upande
wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter
Singano alisisitiza umuhimu wa utunzaji wa vifaa vya Ofisi pamoja na matumizi
sahihi ya rasilimali za Ofisi.
Alieleza
kuwa, utunzaji mzuri wa vifaa hivyo utasaidia kuvifanya vitumike kwa muda
mrefu, hivyo kuvifanya viweze kutumika kwa mahitaji ya sasa na ya baadaye. Pia
alibainisha kuwa matumizi sahihi ya rasilimali za Ofisi yatasaidia kupunguza
gharama zisizo za lazima katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.
Kwa upande
wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema aliwashukuru
watumishi kwa ushirikiano waliyompatia tangu alipowasili katika Kituo hicho. Vilevile
aliahidi kutoa ushirikiano wa karibu katika utekelezaji wa majukumu ya Mahakama.
Mhe. Mrema
aliongeza kuwa, kwa mara ya kwanza katika Mkoa wa Lindi tunaenda kuwa na
Mahakama Kuu hivyo basi yatupasa kufanya maandalizi muhimu pamoja na kujianda
kwa ujio wa Jaji Mfawidhi, “Sisi
tupo kwenye kufanya maandalizi muhimu pamoja na kujiandaa kwa ujio wa Jaji Mfawidhi ” alisisitiza
Mhe. Mrema.
Aidha,
aliwapongeza watumishi wa Mahakama Kanda ya Lindi kwa kazi nzuri wanayoifanya,
akieleza kuwa tangu alipowasili mkoani humo na kutembelea baadhi ya ofisi, ikiwemo
ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Kamada wa
Polisi Mkoa, Takukuru, Ofisi ya Uhamiaji, Ofisi ya Mawakili wa kujitegemea(TLS)
na wadau wengine hakupokea malalamiko
yoyote kuhusu utendaji wa watumishi.
Mhe. Mrema alisema
hali hiyo inaonesha kiwango kizuri cha uwajibikaji na nidhamu ya kazi miongoni
mwa watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo hivyo aliwataka watumishi kuendeleza
juhudi hizo na ikiwezekana kufanya vizuri zaidi.
Naibu
Msajili pia alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, kuaminiana na kuheshimiana
miongoni mwa watumishi pamoja na viongozi, huku akisisitiza kuwa kufanya kazi
kwa ushirikiano na kuheshimu mipaka ya majukumu ya kila mmoja ni msingi muhimu
wa mafanikio katika utendaji wa taasisi, “Tufanye kazi kwa ushirikiano huku tukiheshimu
mipaka na tuhakikishe Lindi inakuwa ya mfano” Alisisitiza Mhe. Mrema.
Vilevile,
aliwataka watumishi kuwa wabunifu na kuchapa kazi kwa bidii na kwa kuzingatia misingi ya uadilifu,
uwajibikaji na weledi katika kutekeleza majukumu yao, hivyo kuimarisha ufanisi
wa kazi na utoaji huduma bora kwa wananchi mapema ipasavyo.
Kikao hicho
ni sehemu ya maandalizi muhimu kuelekea kuanza rasmi kwa shughuli za Mahakama
Kuu Kanda ya Lindi, inayotarajiwa kuanzishwa hivi karibuni, hatua inayotarajiwa
kuimarisha upatikanaji wa huduma za utoaji haki kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi
na maeneo ya jirani.
Naibu
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema akizungumza na
watumishi wa Mahakama Lindi.
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano (aliyesimama) akitoa neno la utambulisho.
Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho.
Afisa Hesabu Mkuu Mahakama ya Wilaya ya Lindi Bw. Lucas M. Kadossa akitoa neno la shukurani kwa niaba ya watumishi.
Waandishi
Waendesha Ofisi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi wakitekeleza jukumu lao la
uchukuaji wa Muhtsari katika kikao hicho.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Jumatano, 11 Machi 2026
JAJI MKUU, MHE. GEORGE MASAJU AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA KATIBU MKUU UMOJA WA MATAIFA
Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 11 Machi, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Bw. Parfait Onanga-Anyanga, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. António Guterres.
Bw. Onanga-Anyanga na ujumbe alioambatana nao waliwasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma majira ya Asubuhi na kupokelewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert.
Mjumbe huyo Maalum amefanya ziara nchini Tanzania kwa lengo la kuonana na Viongozi mbalimbali wa Serikali kwa lengo la kujadili masuala yanayohusu amani, uimarishaji wa demokrasia na utawala wa sheria kwa ujumla.
Bw. Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania pia kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali na kutathmini hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kitaifa na kuendeleza misingi ya utawala wa sheria kufuatia matukio ya uvunjifu wa amani ya kabla na wakati wa Uchaguzi Mkuu tarehe 29 Oktoba, 2025.
Katika ziara hiyo Bw. Onanga-Anyang mbali na wajumbe wengine ameambatana pia na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Bw. Shigeki Komatsubara.
Picha mbalimbali za ziara ya Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa (UN) katika Umoja wa Afrika, Bw. Parfait Onanga-Anyanga Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika, Bw. Parfait Onanga-Anyanga leo tarehe 11 Machi, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati alipomtembelea Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa zawadi kwa wajumbe walioambatana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa waliomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Machi, 2026.
UADILIFU NDIO NGUZO KUU YA UTENDAJI; PROF. NDALICHAKO
Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Mbunge
wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako
amewaeleza Majaji na Mahakimu Wanawake wa Tanzania kuwa, weledi na uadilifu ndizo
nguzo kuu na muhimu za utendaji hivyo hawana budi kuzizingatia wakati
wanapotimiza wajibu wao.
Prof.
Ndalichako aliyasema hayo jana tarehe 10 Machi, 2026 alipokuwa akifunga
Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu
Wanawake, lililofanyika katika ukumbi wa New Generation Hall Kisasa jijini
Dodoma.
Akizungumza
wakati wa kufunga Kongamano hilo, Prof. Ndalichako amesema kuwa, ameridhishwa
na mjadala wenye afya na nia ya dhati ya kujenga na kuimarisha haki na usawa wa
kijinsia, pamoja na maazimio yaliyowekwa ambayo watakwenda kuyatekeleza.
Aliongeza
kuwa, lengo la kuanzishwa kwa TAWJA ni kutambua mchango wa Majaji Wanawake
duniani na kuhimiza usawa wa kijinsia katika Mhimili wa Mahakama, hivyo
kongamano hilo ni tukio muhimu la kubadilishana maarifa kuonesha uongozi, ujasiri
na dira ya mabadiliko pia ni mwanga unaoangaza nuru na kazi kubwa wanayoifanya
ambayo inaakisiwa hadi nje na si ndani ya kumbi za Mahakama pekee bali katika
jamii nzima.
Prof.
Ndalichako amesisitiza kuwa uadilifu ni nguzo kuu ya utendaji, hivyo ni vema
Majaji na Mahakimu Wanawake kuendelea kuzingatia uadilifu katika masuala ya
haki, huku akinukuu maneno ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.
Samia Suluhu Hassan wakati alipokuwa akiwaapisha Majaji ambapo alisema, “uzoefu
umeonesha kuwa Majaji wanawake huwazidi wenzao wa kiume katika utendaji
unaozingatia masuala ya uadilifu.”
Aliongeza
kuwa, anavutiwa na weledi, mshikamano na kujitoa kwa Majaji na Mahakimu
wanawake hali inayoleta mabadiliko ya kijamii kwa kuzingatia utawala wa haki
unaoleta usawa wa kijinsia.
Aidha,
amesema kuwa haki haitoshi kutolewa bali inapaswa ieleweke na iguse mioyo ya
watu pamoja na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama, hivyo Majaji na Mahakimu
Wanawake wana nafasi muhimu katika kuhakikisha sheria inazungumza kwa haki na
uadilifu.
Katika
hatua nyingine, Prof. Ndalichako alizungumzia kuhusu umuhimu wa kuimarisha
mifumo ya Taasisii ili kulinda afya ya kisaikolojia ya Mahakimu ambapo ameeleza
kuwa mtu hawezi kuponya wengine ikiwa yeye mwenyewe ana maumivu, hivyo ni vema
kulinda afya ya akili ili kuimarisha utendaji.
“Mmesisitizwa
pia kuhusu umuhimu wa kulinda mifumo ya Taasisi ili kulinda afya ya
kisaikolojia ya Mahakimu, huwezi kuponya jamii wakati wewe mwenyewe unaumia
kimyakimya, ni vema kuendelea kuhakikisha kwamba tunalinda afya za akili ndani
ya Makahama ili iendelee kutoa haki endelevu,” alisisitiza Mwenyekiti huyo.
Kadhalika,
alisema kuwa, ni vema kuepuka kuwajeruhi upya wahanga na manusura wa ukatili wa
kijinsia na kusisitiza kuwa, manusura wanastahili kujisikia salama na
kuheshimiwa, hivyo haki lazima irejeshe utu na si kufungua tena majeraha.
Alieleza
kwamba, teknolojia inakua kwa kasi hivyo ni vema itumike katika kuwalinda
waathirika wa masuala ya ukatili wa kijinsia hasa ukatili wa mitandaoni, hivyo ubunifu
ni lazima uendelee kutumika ili kuimarisha ulinzi wa waathirika na kuongeza
uwajibikaji kwa kutumia Mahakama mtandao.
Alisema
kuwa, yeye kama Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake anawahakikishia kuwa, Bunge
pamoja na Wabunge wengine wataendelea kushirikiana katika kuimarisha sheria
zinazolinda wanawake na watoto, hivyo ujumbe alioubeba katika mijadala ya leo
utatumika ili kuendelea kukuza usawa wa kijinsia.
Katika
hatua nyingine, Prof. Ndalichako ameeleza kuwa mojawapo ya mafanikio makubwa
kwa Mahakama na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA) ni kufikia usawa
wa asilimia 50 kwa 50 kwa Majaji jambo ambalo ni la msingi katika kukuza imani
kwa wananchi.
Kama
Kaulimbiu ya mwaka huu inavyokumbusha, amewataka Majaji na Mahakimu hao
wanawake kutoka mahakamani na kwenda kwenye jamii wakitoa haki kwa uadilifu
huku wakijihusisha kikamilifu katika shughuli za uelimishaji hususan kupitia
vyombo vya habari, kuzalisha maarifa na kujengeana uwezo jambo litalaojenga
uaminifu kwa jamii ya watoto wa kike kuwa ndoto zao ni halali na matarajio yanawezekana
na mustakabali wa maisha yake hauna mashaka.
Kauli
mbiu ya Kongamano hilo kwa mwaka huu ni “Kutoka mahakamani kuifikia jamii: Majaji
na Mahakimu wanawake mstari wa mbele kuongoza mapambano dhidi ya ukatili wa
kijinsia.
Awali,
kongamano hilo lilifunguliwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Juma Homera, ambaye
alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi. Kongamano hilo lilihudhuriwa na Mtendaji
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, UN Women, Mwakilishi
kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mwakilishi kutoka Ofisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka na wageni wengine waalikwa.
Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako akizungumza alipokuwa mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma.
Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) baada ya kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. Aliyekaa kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winifrida Korosso.
Mgeni rasmi Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (kushoto) akifuatilia kinachojiri wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake. Kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Kongamano hilo, Mhe. Winifrida Korosso.
Mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Majaji Wanaume waliohudhuria katika Kongamano hilo.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)
UJENZI WA MAHAKAMA ZA MWANZO TATU MKOANI RUVUMA WAKAMILIKA
Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea
Mahakama ya Tanzania imekamilisha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo tatu,
Lilolndo, Likuyusekamaganga na Nalasi, zilizopo katika Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Songea, mkoani Ruvuma.
Mahakama za Mwanzo Lilondo ipo Wilaya ya Songea katika Halimashauri ya
Madaba, Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga ipo katika Wilaya ya Namtumbo na Mahakama
ya Mwanzo Nalasi ipo katika Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma.
Ujenzi huo uliokuwa unatekelezwa na Mkandalasi Mkuu (Pivotech), akisaidiana
na Mkadalasi Msaidizi(Cadson) na majengo hayo matatu ya Mahakama yamegharimu jumla
ya Shilingi za Kitanzania 2,954,059,829.18.
Mahakama ya Mwanzo Lilondo imegharimu 985,625,739/=, Mahakama ya Mwanzo
Likuyusekamaganga imegharimu 961,400,162/= na Mahakama ya Mwanzo Nalasi imegharimu
1,007,033,928.18/=.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele, alikabidhiwa majengo hayo hivi karibuni kwa nyakati tofauti na Mkandarasi Arqes Africa Architects and Interior Designers Ltd.
Alitoa shukrani kwa wananchi
wa maeneo hayo kwa ushirikiano waliouonyesha tangu kuanza hadi kumalizika kwa
miradi hiyo.
Alieleza kuwa uzinduzi wa Mahakama hizo umepangwa kufanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Lilondo, kama kuashiria kuanza kwa huduma za kimahakama zitakazoanza kutolewa katika majengo hayo mapya yaliyokamilika.
Jengo la Mahakama ya Mwanzo Lilondo.
Jengo la Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga.
Jengo la Mahakama ya Mwanzo Nalasi.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa pili kulia) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Lilondo.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa
katikati) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (kushoto) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Nalasi.
Wananchi na wakazi wa Nalasi wakiwa katika eneo la tukio wakishuhudia makabidhiano hayo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.
Jumanne, 10 Machi 2026
MAJAJI NA MAHAKIMU WANAWAKE WAUNGANA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA
●
Wajadili nafasi ya wanamke katika kuimarisha utoaji haki na
kuifikia jamii
Na HALIMA MENETE, Mahakama-Dodoma
Kongamano maalumu la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji
na Mahakimu Wanawake limefanyika leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New
Generation jijini Dodoma, likiwakutanisha Viongozi wa Serikali, Mahakama ya
Tanzania pamoja na wadau wa maendeleo kujadili nafasi ya Majaji na Mahakimu
wanawake katika kupambana na ukatili wa kijinsia.
Kongamano hilo lililobeba Kauli mbiu, “Kutoka Mahakamani
Kuifikia Jamii: Majaji na Mahakimu Wanawake Mstari wa Mbele Kuongoza Mapambano
Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia” lilihudhuriwa na mgeni rasmi Waziri wa Katiba
na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania,
Prof. Elisante Ole Gabriel, Majaji na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania bara na
visiwani pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo UN Women, RITA, Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka.
Katika kongamano hilo pia, kulikuwa na nafasi ya utoaji mada
mbalimbali, ambapo moja wa mada ilihusu “Nafasi ya Mwanamke kama Kiongozi
katika Kuleta Mabadiliko kwenye Jamii kupitia Utoaji wa Haki unaozingatia
Masuala ya Kijinsia.”
Mada hiyo iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe.
Rehema Joseph Kerefu huku ikiendeshwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya
Dar es Salaam, Mhe. Salma Magimbi, na ilijadiliwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu
Moshi Mhe. Dkt Lilian Mongela, Naibu Msajiri Mhe. Upendo Ngitiri na Hakimu
Mkazi, Mhe. Juliana Mvungi.
Akifafanua kwa kina mada hiyo, Mhe. Kerefu amesema kuwa,
katika juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia katika utoaji wa haki, tayari
kuna misingi na nyenzo mbalimbali zilizowekwa kimataifa na kitaifa ambazo
zinaweza kusaidia katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.
Amesema miongoni mwa nyenzo hizo ni pamoja na maandiko ya
kitaaluma kama kitabu kilichoandikwa na Kosana Beker kinachojadili Gender
and Diversity in the Judiciary, ambacho kinaeleza kwa kina umuhimu wa
kuzingatia masuala ya kijinsia na utofauti katika mfumo wa utoaji haki.
Kwa mujibu wa Jaji Kerefu, uwepo wa vitendea kazi hivyo
unaonesha wazi kuwa, kuna uwanja mpana wa kuhakikisha haki za binadamu
zinalindwa ipasavyo na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.
Hata hivyo, ameeleza kuwa, pamoja na uwepo wa misingi hiyo
imara ya kisheria na kitaaluma bado kuna changamoto zinazotokana na baadhi ya
mila, desturi na tamaduni katika jamii ambazo wakati mwingine zimekuwa
zikikwamisha juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia.
Amesema baadhi ya mila na desturi hizo zimejikita katika
mfumo dume, hali ambayo wakati mwingine imekuwa ikiweka vikwazo kwa watoa haki
katika kuhakikisha misingi ya usawa wa kijinsia kama ilivyoainishwa katika
mikataba ya kimataifa, Katiba ya nchi na sheria mbalimbali zinazozingatia
masuala ya kijinsia zinatekelezwa kikamilifu.
Aidha, amesema licha ya maendeleo yaliyopatikana katika
kuimarisha haki za wanawake, bado kuna changamoto mbalimbali zinazoendelea
kujitokeza katika jamii ikiwemo ongezeko la mashauri ya ubakaji, unyanyasaji wa
kingono, ukatili wa majumbani pamoja na ndoa za utotoni.
Ameongeza kuwa, hata katika masuala ya umiliki wa mali na
mirathi bado kuna changamoto zinazowakabili wanawake katika jamii, huku baadhi
ya sheria zilizopo zikionekana kutokidhi kikamilifu matakwa ya usawa wa
kijinsia.
Ametolea mfano wa ‘Customary Law Declaration Order’ ya mwaka
1963 pamoja na baadhi ya vipengele vya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ambavyo
bado vinaibua mjadala kutokana na kuwepo kwa vipengele vinavyohusishwa na
ruhusa ya ndoa za utotoni.
Kwa upande mwingine, washiriki wa mada hiyo walieleza kuwa, changamoto
hizo zinapaswa kuwa chachu kwa wadau wa sekta ya sheria, hususan majaji na
Mahakimu wanawake, kuendelea kutumia elimu yao ya sheria pamoja na misingi
iliyowekwa kuhakikisha vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.
Vilevile ilielezwa kuwa mapambano dhidi ya ukatili wa
kijinsia yanahitaji ushirikiano mpana wa taasisi mbalimbali, ikiwemo Mahakama,
Serikali, Wadau wa maendeleo pamoja na jamii kwa ujumla.
Akizungumzia uwakilishi wa wanawake katika Sekta ya Mahakama
duniani, Mhe. Kerefu alieleza kuwa baadhi ya nchi zimepiga hatua kubwa katika
kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi za kimahakama, akitolea mfano wa
Italia ambapo wanawake wanawakilisha zaidi ya asilimia 52.9 ya Majaji.
Hata hivyo, alisema bado kuna nchi ambazo uwakilishi wa
wanawake katika Mahakama uko chini, akitolea mfano wa Iraq yenye takribani
asilimia 7.6 na Nepal yenye asilimia 3.8.
Kwa upande wa Tanzania, washiriki wa kongamano hilo
walieleza kuwa, kumekuwa na mafanikio makubwa katika kuongeza uwakilishi wa
wanawake katika ngazi mbalimbali za Mahakama.
Imeelezwa kuwa Mahakama ya Rufani tangu ilipoanzishwa mwaka
1979 ilianza na Majaji watano wote wakiwa wanaume, lakini kwa sasa idadi hiyo
imeongezeka na kufikia Majaji 37, ambapo wanaume ni 25 na wanawake ni 12, idadi
inayozidi asilimia 30 ya uwakilishi wa wanawake.
Aidha, katika Mahakama Kuu kuna jumla ya Majaji 104 ambapo
wanaume ni 65 na wanawake 39, wakati Mahakama za Hakimu Mkazi zina jumla ya
Mahakimu 1,434 ambapo wanaume ni 746 na wanawake 688 sawa na takribani asilimia
48.
Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo, kuna Mahakimu 189 ambapo
wanaume ni 111 na wanawake 78 sawa na asilimia 41.
Kwa upande wa Zanzibar, Mahakama Kuu ina jumla ya majaji 14
ambapo wanaume ni tisa na wanawake watano sawa na asilimia 35, huku katika
ngazi ya mahakimu kukiwa na jumla ya Mahakimu 66 ambapo wanawake ni 23 na
wanaume 43.
Washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa takwimu hizo
zinaonesha wazi juhudi za Serikali katika kuhakikisha wanawake wanapata nafasi
katika ngazi mbalimbali za uongozi ndani ya Mhimili wa Mahakama.
Hata hivyo, walisisitiza kuwa pamoja na ongezeko hilo la
uwakilishi wa wanawake, bado kuna umuhimu wa kuhakikisha kuwa nafasi hizo
zinatumika ipasavyo kuimarisha utoaji wa haki na kuchangia kikamilifu katika
mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.














.jpeg)




















