Jumamosi, 11 Julai 2026

WADAU WA HAKI JINAI KIBAHA WAOMBA ASKARI POLISI WAPATIWE MAFUNZO

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Kibaha

Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Jinai kwa Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo katika Wilaya ya Kibaha kimejadili na kuomba Askari wanaokaa Mahakama za Mwanzo kutekeleza amri mbalimbali za Mahakama kupatiwa mafunzo ya namna ya kuendesha mashauri ya jinai.

Hayo yamesemwa jana tarehe 10 Julai, 2026 katika kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Akizungumza katika kikao hicho, namna ambavyo washtakiwa na walalamikaji katika mashauri ya jinai, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mkuza, Mhe. Leah Mkono amesema kuna ugumu unatokea pale Askari wanafika Mahakamani na vielelezo hawavitoi wakati wa usikilizaji wa shauri badala yake wanavitelekeza tu Mahakamani na baada ya shauri kuisha ndipo mlalamikaji anadai vielelezo alikuwa navyo askari wakati huo shauri limeshaisha hali inayosababisha haki za wadaa kupotea.

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mailimoja, Mhe. Honorina Kambadu ameeleza masikitiko yake kuhusiana na hati za mashtaka kukosewa kila mara kutokana na kubadilishwa kila mara kwa Askari wanaofika Mahakamani hapo kiasi kwamba akielekezwa Askari huyu akaelewa, kesho anakuja Askari mwingine hivyo kumekuwa na ugumu wa kufanya kazi na Askari tofauti tofauti.

Wakati, huohuo amesema kumekuwa na uhaba wa Askari Polisi ambapo Mahakimu watano lakini Askari mmoja jambo hilo linasababisha kusubiriana wakati wa kusoma hati za mashtaka na kama kuna hukumu ya kumtia mtu hatiani inabidi wasubiri.

Akizungumzia katika masuala hayo, Katibu wa Kikao hicho ambaye ni Wakili wa Serikali Said Seif amesema, kutokana na changamoto hizo anayapokea hayo yote na kwamba atayafikisha kwa Viongozi wake na kuwashauri wafanye mafunzo ya namna bora ya kuandaa hati za mashtaka kwa Askari Polisi wa Mahakama za Mwanzo kuhusu namna bora ya kuwasilisha vielelezo Mahakamani na pia uwepo wa Askari Mahakamani bila kubadilishwa badilishwa kila siku.

Naye Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Kibaha, Mrakibu Msaidizi wa Polisi Victor Kashai amesema kuna uhaba wa Askari Polisi na hivyo kusababisha kuwepo kwa Askari mmoja Mahakamani lakini kutokana na changamoto hizo atazungumza na Viongozi wake kuongeza Askari ili kuepusha ucheleweshaji wa mashauri kuisha Mahakamani.

Katika kikao hicho Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Emmael Lukumai ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kikao hicho amebainisha kwamba, katika Mahakama ya Wilaya kuna mashauri mawili tu yaliyovuka miezi sita na miongoni mwa mashauri hayo moja liko kwenye hatua ya maamuzi madogo na jingine liko kwenye mashauri ya majadiliano (Pre Bargain).

Aidha, Mhe.Lukumai  amewataka upande wa mashtaka kwa mashauri ya majadiliano (Pre Bargain) yasizidi siku sitini (60) yakitajwa Mahakamani bila kukamilika.

Katika kikao hicho Wadau wa Haki Jinai wameweka maazimio kadhaa ili kikao kijacho waone kama yametekelezeka. Maazimio hayo ni pamoja na Mahakama za Mwanzo ziko karibu na wananchi hivyo Mahakimu wasifungwe kupita kiasi na masharti ya kiufundi (technicalities), Hati za Mashtaka zenye Mapungufu zisipokelewe Mahakamani.

Pia umetolewa ushauri kwa Mahakimu  kutokana na mabadiliko ya Sheria ya Kieletroniki kuruhusu Ushahidi kupokelewa Mahakama za Mwanzo wajitahidi kusoma na kuelewa vizuri na kutofautisha kati ya maudhui ya kidijitali (Digital Content) na maudhui ya Makala (Documentary Content) na taratibu za upokeaji wake na pia kufanya kozi fupi zinazotolewa na Vyuo Vikuu kuhusu Akili Unde (AI) ili kuendana na wakati na hali halisi maana uhalifu mwingi umehamia kwenye mambo ya kimtandao zaidi kuliko uhalifu wa kawaida.

Sambamba na kikao hicho cha kusukuma mashauri ya jinai pia kimefanyika kikao cha kusukuma mashauri ya madai (Bench Bar) ambapo  wito umetolewa kwa Mawakili kuweza kusimamia vema shajara zao ili kuepuka muingiliano wa mashauri kati ya Mahakama moja na nyingine.

Wadau wa Haki Jinai wakiwa katika picha ya pamoja baada ya Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Jinai. Walioketi kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mwenyekiti wa Kikao hicho, Mhe. Emmael Lukumai na kulia ni Katibu wa kikao hicho, Wakili wa Serikali Said Seif.

Wadau wa Haki Jinai wakiendelea na kikao.


 Wajumbe wa Kikao cha kusukuma Mashauri ya Madai wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kikao hicho. Walioketi kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha ambaye pia aliyekuwa Mwenyekiti wa kikao hicho, Mhe. Emmael Lukumai na Katibu ambaye ni Wakili wa Kujitegemea, Wakili Werema Maghembe. Waliosimama kutoka kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mailimoja, Mhe. Honorina Kambadu, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mlandizi, Mhe. Anneth Senkoro, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mkuza, Mhe. Leah Mukono, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Mhe. Fredrick Shayo na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Soga, Mhe Wahabi Mvura.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mwenyekiti wa Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Madai, Mhe. Emmael Lukumai akifungua kikao hicho. Kushoto ni Katibu wa kikao hicho, Wakili Werema Maghembe.


(Habari  hii imehaririwa MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)





 

 

 

 

 

JENGENI UTAMADUNI WA UWAJIBIKAJI NA UWAZI KAZINI; JAJI FRANK MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Kuu Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amewaagiza Viongozi wa ngazi mbalimbali za Mahakama mkoani humo kuwa ni lazima wajenge utamaduni wa uwajibikaji na uwazi kazini katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku kwakuwa ndio njia bora ya kutoa huduma na kuondoa malalamiko ya wananchi wanaohudumiwa.

Mhe. Mahimbali aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa Kikao cha Menejimenti cha Masjala hiyo kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Hoteli ya Sparrow iliyopo wilayani Karatu.

Akizungumza na wajumbe wa kikao hicho, Jaji huyo Mfawidhi alisisitiza kuwa ni lazima Hakimu anaposoma hukumu ahakikishe anatoa na nakala yake siku hiyo ya kusoma hukumu.

Amesisitiza kwa kusema kuwa, kushindwa kutoa nakala ya hukumu kwa wakati ni ukiukwaji wa miongozo iliyopo na kusababisha malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa wateja na wadau wa Mahakama.

Mhe. Mahimbali ametoa maagizo kwa Mahakimu wote Wafawidhi kufuatilia kwa karibu Mahakimu walio chini yao kuhakikisha kuwa, taarifa muhimu kama nakala za hukumu na mienendo ya mashauri wateja wanazipata kwa urahisi na kwa wakati na hivyo kujiepusha na malalamiko yasiyo ya lazima.

Vilevile, Jaji Mahimbali ametoa maelekezo kwa kila Mahakama kuboresha utoaji huduma kwa wateja. Amesisitiza kwa kusema, “Sisi tunafanya kazi kwa Umma, tunahudumia wananchi, Mahakama zetu ni kwa ajili ya wananchi, kwa hiyo maslahi ya wananchi yawe kipaumbele cha kwanza. Tunao wajibu wa kuwahudumia wananchi kwa heshima, utu na usafi.”

Hali kadhalika, Mhe. Mahimbali amewaasa wajumbe kuzingatia maadili ya kazi katika kusimamia Mahakama zao ikiwemo matumizi sahihi ya fedha za ofisi na kujiepusha na tamaa hatarishi.

Aliongeza kuwa, ni wajibu wa Viongozi wa Mahakama husika kuhakikisha kuwa, watumishi walio chini yao wanatekeleza majukumu yao kwa mujibu wa miongozo ya kazi kama sehemu ya kuwaepusha watumishi kufanya matendo yanayokiuka taratibu za kazi na hatimaye kuwekwa nguvuni na vyombo vya sheria.

Pia, Jaji Mahimbali ameelekeza mambo mbalimbali yanayolenga kuongeza ufanisi kazini, ikiwemo Mahakimu kuzingatia muda uliowekwa wa mashauri kuisha, kuepuka kuahirisha mashauri bila sababu za msingi, kusimamia ubora wa hukumu, maamuzi na amri za Mahakama; watumishi kuwa waadilifu na waaminifu kazini, usimamizi bora wa fedha na rasilimaliwatu, kuimarisha ushirikiano kati ya Viongozi na watumishi wa ngazi za chini na watumishi kujiepusha na vitendo vinavyoharibu taswira nzuri ya Mahakama.

Aidha, amewaagiza Mahakimu Wafawidhi kufanya tathmini ya kaguzi wanazofanya na kubaini maeneo yanayohitaji mafunzo na kuchukua hatua ya kuandaa mafunzo ya ndani kwa lengo la kuwaelimisha watumishi walio chini yao na hatimae kuongeza ufanisi wa kazi.

Amezitaka Mahakama mkoani Arusha kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuendelea kutumia mifumo ya Kitehama iliyopo Mahakamani hususan Mifumo ya kuratibu mashauri (e-CMS na Primary Court Mobile App).

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye ni Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mhe. Erasto Philly, aliwasilisha taarifa ambayo ilionesha kuwa hadi kufikia tarehe 18 Machi, 2026, Mahakama Kuu Arusha ilikuwa na mashauri yanayoendelea 593, ambapo kwa kipindi cha kuanzia tarehe 18 Machi, 2026 hadi tarehe 30 Juni, 2026 yalisajiliwa mashauri 324, yalimalizika mashauri 448 na kubaki mashauri 469.

Katika mashauri hayo (469) yaliyobaki, mashauri ya mlundikano ni matatu ambayo yote ni mashauri ya utekelezaji.

Mhe. Philly aliendelea kusema kuwa, hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026 Mahakama ya Hakimu Mkazi ilikuwa na mashauri 72 yaliyokuwa yakiendelea Mahakamani na kwa kipindi cha kuanzia Mwezi Aprili hadi Juni 2026, Jumla ya mashauri 45 yalisajiliwa na mashauri 61 yakasikilizwa. Idadi ya mashauri yaliyobaki kufikia tarehe 30 Juni, 2026 yalikuwa 56.

Naibu Msajili huyo alizitaja pia takwimu za Mahakama za Wilaya mkoani Arusha kuwa, hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026, Mahakama hizo zilikuwa na mashauri 334 yaliyokuwa yanaendelea Mahakamani, na kwa kipindi cha mwezi Aprili hadi Juni 2026, jumla ya mashauri 514 yalisajiliwa na 470 yalisikilizwa. Idadi ya mashauri yaliyobaki kufikia tarehe 30 Juni, 2026 yalikuwa 378.

Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo Mkoa wa Arusha, Mhe. Philly alisema kuwa, zilikuwa na jumla ya mashauri 207 yaliyokuwa yakiendelea Mahakamani hadi kufikia tarehe 30 Machi, 2026, na kwa kipindi cha kuanzia mwezi Aprili hadi Juni yalisajiliwa mashauri 4,169 na yalisikilizwa mashauri 4,121. Mashauri yaliyobaki tarehe 30 Juni, 2026 yalikuwa 255.

Aliongeza kuwa, kumekuwa na changamoto mbalimbali katika usikilizaji wa mashauri hayo, ikiwa ni pamoja na majalada yanayoitishwa kutoka Mabaraza ya Ardhi na Usuluhishi kutokuletwa kwa wakati, Majalada yaliyorudishwa katika Mabaraza ya Ardhi na Tume ya Usuluhishi kwa ajili ya kufanyiwa masahihisho kutorejeshwa kwa wakati, mashahidi kutoletwa kwa wakati katika mashauri ya jinai na kusababisha mashauri kuchelewa kuisha mahakamani na wakati mwingine hata kusababisha vikao maalum vya mashauri ya Jinai kusogezwa mbele.

Naye Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama amebainisha katika wasilisho lake kuwa, kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 Mahakama Arusha imepiga hatua kubwa katika mambo mbalimbali yanayoweka mazingira mazuri katika utekelezaji wa shughuli za Mahakama ikiwemo mafunzo kwa watumishi, kubadilishwa kada watumishi wenye sifa, kulipa stahili za Viongozi kwa wakati.

Mengine ni kuwezesha sare za watumishi wasio Mahakimu, kufanya ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya Mahakama, kuanzisha Mahakama mpya na kufufua Mahakama zilizokuwa zimefungwa kwa muda mrefu.

Pia, Bi. Kapama aliongeza kwa kusema kuwa, Mahakama hiyo imepiga hatua kubwa katika malipo ya fedha za mirathi ambapo katika Mwaka wa Fedha uliopita 2025/2026, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha imefanya malipo ya shilingi za Kitanzania takribani bilioni tatu (3,069,003,707.53/=), sawa na asilimia 86.92. Kiasi kilichobaki kwenye akaunti ya Mirathi kufikia tarehe 30 Juni, 2026 kilikuwa takribani shilingi milioni mia nne na sitini na moja (461,609,115.19/=), ambapo juhudi zinaendelea kumalizia malipo ya fedha hizo za mirathi zilizosalia.

Kikao hicho kimehudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka Mahakama za Mkoa wa Arusha hususan Mahakimu Wakazi Wafawidhi na Maofisa mbalimbali waliowakilisha Mahakama zao.

Wajumbe hao wamejadili mambo mbalimbali ikiwemo mafanikio na changamoto wanazokumbana nazo katika kazi na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuboresha utendaji kazi katika maeneo yao.

Vikao hivyo vya menejimenti ni moja ya fursa inayouwezesha Uongozi wa Mahakama Arusha kufanya tathmini na kujadili kwa pamoja juu ya namna bora ya kutekeleza shughuli za Mahakama na hatimaye kuongeza ufanisi katika kazi.

Vikao hivyo hufanyika katika Mahakama tofauti tofauti kwa mzunguko ambapo kikao hicho kimefanyika Wilayani Karatu, Mahakama ya Wilaya Karatu wakiwa ni wenyeji. Kikao kitakachofuata kitafanyika mwezi Oktoba, 2026 Wilayani Longido.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akifungua Kikao cha Menejimenti cha Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Hoteli ya Sparrow iliyopo Wilayani Karatu. Kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama. 


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mhe. Erasto Philly akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Sparrow mjini Karatu. Kushoto ni Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento.


Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Bi. Grace Kapama (aliyesimama) akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti kilichofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Sparrow iliyopo Wilaya Karatu. Kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali. 

Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Monduli na Karatu, Mhe. Pamela Meena (kushoto) na Mhe. Samwel Mushumbusi (kulia) wakishiriki kikamilifu Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Hoteli ya Sparrow Karatu Mjini.

Wajumbe mbalimbali walioshiriki katika Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Arusha kilichofanyika hivi karibuni kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Sparrow Wilayani Karatu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Ijumaa, 10 Julai 2026

JAJI MKUU AWATAKA MAJAJI WA RUFANI KUWA HURU KUTOA MAONI YA KUBORESHA MAAMUZI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewasihi Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya kuwa huru kutoa maoni au misimamo ya kisheria wanayoamini ni sahihi bila hofu yoyote, kwani kwa kufanya hivyo, watakuwa wanaboresha maamuzi ya Mahakama ya Rufani ambayo ndiyo inategemewa kutoa kauli ya mwisho kwa mashauri yanayofika mbele yake.

Mhe. Masaju amesisitiza hilo kupitia Hotuba yake ya Kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya iliyosomwa na Mwakilishi wake Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Nawasihi muwe huru kutoa maoni au misimamo ya kisheria mnayoamini ni sahihi bila hofu yoyote, kwani kwa kufanya hivyo ndiyo mtakuwa mnaboresha maamuzi ya Mahakama ya Rufani ambayo ndiyo inategemewa kutoa kauli ya mwisho kwa mashauri yanayofika mbele yake lakini ndiyo inayotoa mwongozo wa tafsiri ya sheria unaopaswa kufuatwa na Mahakama zote za chini yake na kujenga au kuendeleza misingi ya kisheria (jurisprudence) nchini,” amesema Mhe. Masaju kupitia hotuba hiyo.

Jaji Mkuu amesema kuwa, moja kati ya Mada waliyojifunza Majaji hao inahusu Ushirikiano katika Mahakama ya Rufani (Collegiality at the Court of Appeal), hivyo, amewaomba pia kujenga utamaduni wa kushirikiana, kusikilizana, kuheshimiana na kujenga maamuzi bora kupitia majadiliano ya kitaaluma. Na kwamba hiyo haimaanishi kukubali tu msimamo wa Majaji wengine hata kama dhamiri na utaalamu wao vinaelekeza vinginevyo.

Aidha, Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, katika mada ya Haki ya Msingi dhidi ya Masharti ya Kiufundi ambapo amesema, “mada hii inatutaka kuamua mashauri kwa kubainisha haki na wajibu wa kila mdaawa, ambalo ndilo jukumu la msingi la Mahakama, kuliko kuamua mashauri kwa kutumia masharti ya kiufundi ambayo hayatatui mgogoro uliopo baina ya wadaawa. Na kama ambavyo mmeona, hili lina msingi wake kuanzia kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo mmeapa kuizingatia, hivyo nawasihi sana mkalitekeleze hilo.”

Amesema kuwa, mada hiyo msingi wake umeanzia kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo wameapa kuizingatia, hivyo amewasisitiza wakalitekeleze hilo ipasavyo. Na kwamba wanapaswa kulitekeleza vema zaidi kwa kutumia hekima na akili kama alivyosema siku ya ufunguzi wa mafunzo hayo, kwani hekima na akili walizobarikiwa na Mwenyezi Mungu zitawawezesha kuwapa upeo wa ziada wa kupata ufumbuzi wa masuala magumu na yanayohitaji ubunifu na kujiongeza (creativity and proactiveness).

Akizungumzia kuhusu umuhimu wa Mafunzo Elekezi, Jaji Mkuu amesema, Mafunzo hayo yalilenga kuwaandaa washiriki kuanza kutekeleza majukumu ya Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa weledi, kujiamini zaidi na kwa ufanisi zaidi.

“Kama tunavyofahamu, Mahakama ya Rufani ndiyo chombo chenye kauli ya mwisho katika mfumo wa utoaji haki nchini, hivyo ni muhimu Majaji wapya wakaandaliwa kuanza kazi hiyo wakiwa wamepigwa msasa ili kuelewa vizuri zaidi Sheria, Kanuni na taratibu zinazotumika katika Mahakama hii licha ya ukweli kuwa ninyi tayari ni wataalam wa Sheria,” imeeleza hotuba hiyo iliyosomwa na Mhe. Mwambegele. 

Kadhalika, Mhe. Masaju amesema mafunzo hayo yasiwe mwisho wa kujifunza na kuwataka Majaji hao kuendelea kujifunza hata baada ya mafunzo hayo. 

Akizungumzia Wawezeshaji na Mtindo wa Uwasilishaji mada, amesema, “Kama nilivyosema siku ya ufunguzi, wawezeshaji waliowezesha katika mafunzo haya ni wabobezi na wana uzoefu mkubwa wa utendaji kazi katika Mahakama ya Rufani. Waheshimiwa Majaji Wastaafu Mhe. Msoffe na Mhe. Rutakangwa wamehudumu katika Mahakama hii kwa muda mrefu na hukumu zao zimeendelea kutumika kama rejea na mwongozo katika maamuzi yetu mpaka sasa.”

Ameongeza kuwa, wakati mafunzo hayo yakiendelea alipata fursa ya kufika mara kadhaa, na alishuhudia mtindo mzuri wa uwasilishaji ambapo alishuhudia mafunzo hayo yakitolewa kwa mtindo wa majadiliano ya pamoja kama jopo na ushirikishwaji wa kila mmoja badala ya mhadhara wa upande mmoja.

“Mtindo huu unawajenga kufikiri, kuchambua na kufanya kazi kwa pamoja kama ulivyo mtindo wa ufanyaji kazi katika Mahakama ya Rufani,” ameeleza.

Vilevile, Jaji Mkuu amekipongeza Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kuandaa mafunzo hayo, Wawezeshaji wote wa mafunzo sambamba na kuwapongeza Majaji hao kwa kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo na kuwatakia kila la heri kwenye utekelezaji wa majukumu yao huku akiwakumbusha kila mmoja kukiishi kiapo chake na kuzingatia dhamana kubwa waliyopewa na Taifa na matarajio ya wananchi kwao.

Katika hatua nyingine, naye Jaji Mwambegele amewashauri Majaji hao kusoma hukumu za Majaji Wastaafu, Mhe. Msoffe na Mhe. Rutakangwa na nyingine ili kuongeza maarifa zaidi katika utekelezaji wa jukumu la msingi la utoaji haki.

“Someni hukumu zao tangu wakiwa Majaji wa Mahakama Kuu mpaka Majaji wa Mahakama ya Rufani. Nina uhakika hamtajutia, Mimi nimekuwa msomaji wa hukumu za hawa Wawezeshaji tangu nikiwa Wakili wa Serikali, mpaka nikawa Jaji wa Mahakama Kuu, na sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani. Kama alivyosema Mheshimiwa Jaji Mkuu hapa, ni kwamba hawa Wawezeshaji wana uwezo mkubwa, ninachotaka kuwasihi katika kuchomekea kwangu hapa ni kwamba, mpate muda wa kusoma hukumu zao. Uwezo wao sio wa kawaida. Mtakapokuwa mnasoma hukumu zao, mtagundua kwamba ni kwa nini Mahakama bado inawatumia mpaka leo,” amesisitiza Jaji Mwambegele.

Akizungumzia jinsi Mahakama ya Rufani inavyofanya maamuzi, Mhe. Mwambegele amesema maamuzi ya Mahakama hiyo ni maamuzi ya jopo la Majaji watatu, na maamuzi ya Majaji watano au kuendelea kwa (full bench), ambapo amesema, “Na jinsi ya kufanya, tunafanya maamuzi kwa kujadiliana, tukiongozwa na sheria. Pamoja na mlivyofundishwa, nawasihi pia mkasome hukumu ya Ahmadi Chali dhidi ya Jamhuri, imekuwa ‘reported’ katika mwaka 2006 TLR 313. Hukumu hii inaonesha ni jinsi gani hukumu ya Mahakama ya Rufani inaandikwa.”

Ameongeza kuwa, kupitia hukumu hiyo watapata habari ya ziada kuhusiana na nini kifanyike endapo mmoja wa jopo anashindwa kutekeleza jukumu lake, ama kwa sababu ya kiafya, au kwa kufariki na mambo mengine kama hayo. “Mtajua kwamba hukumu ya Mahakama ya Rufani inafanywa kwa pamoja, ‘this is a collegial Court’,” amesisitiza.

Hali kadhalika, Jaji Mwambegele amewasisitiza Majaji hao kuwa na Ushirikiano na Uadilifu wanapotekeleza majukumu yao.

Akitoa neno kwa niaba ya Majaji wenzake wakati wa hafla ya kufunga mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Aboud ameishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto chini ya Mkuu wa Chuo hicho ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo kwa kuandaa mafunzo hayo muhimu.

Kadhalika, Mhe. Aboud amewashukuru Wawezeshaji wote wa Mafunzo hayo wakiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju na Majaji Wastaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. January Msoffe na Mhe. Edward Rutakangwa.

Majaji hao tisa waliopatiwa mafunzo elekezi ambao ni Mhe. Imani Daudi Aboud, Mhe. Rabia Hussein Mohamed, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha, Mhe. Yohane Bokobora Masara, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba na Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim wote kwa pamoja wamepatiwa vyeti vya kuhitimu Mafunzo hayo muhimu ambayo ni moja ya maandalizi ya kuanza kazi rasmi kazi katika Mahakama ya Rufani ambayo ndio ngazi ya juu katika mfumo wa utoaji haki nchini. 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa (waliosimama) waliohitimu Mafunzo Elekezi leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akitoa hotuba ya kutoka Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya pamoja na baadhi ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama na IJA wakisikiliza Hotuba ya Jaji Mkuu ya Kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya  iliyokuwa ikitolewa na Mwakilishi wake Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (hayupo katika picha) leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Daudi Aboud ambaye ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rabia Hussein Mohamed ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Yohane Bokobora Masara ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba ameshiriki mafunzo hayo. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele akimpatia cheti cha Kuhitimu Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim ameshiriki mafunzo hayo. Anayeshuhudia kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati wa hafla ya kufunga Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mahakama (waliosimama) waliohudhuria hafla ya ufungaji wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya leo tarehe 10 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo hayo, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti ya maandalizi ya Mafunzo hayo (waliosimama). Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo na kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania na mmoja kati ya waliokuwa Wawezeshaji wa Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya, Mhe. Edward Rutakangwa. Jaji Mwambegele amemwakilisha Jaji Mkuu katika hafla ya ufungaji wa mafunzo hayo.

(Picha na MARY GWERA & FAUSTINE KAPAMA, Mahakama)












JAJI TIGANGA ASISITIZA UTEKELEZAJI MIKAKATI YA JAJI MKUU USIKILIZAJI MASHAURI YA MADAI

Na ARAPHA- RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, hivi karibuni ilifanya Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Madai (Bench Bar) kilichowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya sheria na haki, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa mashauri ya madai, kupunguza mlundikano na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa wakati.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, na kuhudhuriwa na wawakilishi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Ofisi ya Msajili wa Hati pamoja na Baraza la Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Akifungua kikao hicho, Jaji Mfawidhi alisisitiza umuhimu wa wadau wote wa sekta ya sheria na haki kuendelea kutekeleza na kufuatilia kwa vitendo mikakati iliyoelekezwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, yenye lengo la kuhakikisha mashauri yanasikilizwa na kuamuliwa mapema ipasavyo, kupunguza mlundikano na kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Akiwasilisha taarifa ya hali ya mashauri ya madai, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, alisema Mahakama inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuhakikisha mashauri yanasikilizwa na kuamuliwa kwa wakati, sambamba na kudhibiti mashauri ya mlundikano.

Alieleza kuwa Mahakama imeendelea kufanya vikao maalum vya kusafisha mashauri (clean-up sessions), kutoa kipaumbele kwa mashauri ya kimkakati na   matumizi ya hati ya maelezo ya shahidi (Witness statement)  kwa dhumuni la kumaliza mashauri haraka na kupata kumbukumbu nzuri ya kile alichokikusudia mteja.

Mikakati mingine ni kusikiliza mashauri kadri inavyokuwa yamekamilika au yameiva bila kujali yamepokelewa lini, kuhimiza matumizi ya usuluhishi pale inapowezekana, kukamilisha hatua za awali  ya mashauri ya awali ndani ya siku 30, kutoa ahirisho lisilozidi wiki mbili na kuimarisha ushirikiano na wadau wa mnyororo wa haki ili kuondoa vikwazo vinavyochelewesha usikilizaji wa mashauri.

Kikao hicho pia kilibaini mashauri yanayokaribia kuwa ya mlundikano na kuweka mikakati ya kuyashughulikia mapema. Aidha, wadau walisisitiza umuhimu wa kushughulikia migogoro katika ngazi zinazotakiwa kisheria kabla ya kufikishwa mahakamani, hususan mashauri ya ardhi, pamoja na kuhakikisha mashauri yanaamuliwa kwa kuzingatia ushahidi na hoja za msingi badala ya kasoro za kiufundi.

Miongoni mwa mikakatii iliyofikiwa ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na Taasisi za mnyororo wa haki, kuongeza matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro, kuharakisha utekelezaji wa hukumu na kuhakikisha mashauri yanayosikilizwa yanakamilika kwa wakati kwa kuzingatia sheria na kanuni.

Mikakati mingine iliyofikiwa ni kutosajili mashauri ya ardhi ambayo yalipaswa kuanzia  kwa Msajili wa Hati kwa mjibu wa sheria pamoja na kufuatilia utekelezaji wa mikakati ya kikao cha Jaji Mkuun na Wadau wa Haki Madai inayolenga kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wote wa sekta ya sheria na haki ili kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama, kupunguza mlundikano wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki mapema ipasavyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiongoza kikao cha kusukuma mashauri ya madai.

 Wadau wa kikao hicho (juu na chin) wakisikiliza hoja mbalimbali ambazo zilikuwa zinatolewa.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, (aliyepo katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe na wadau wa kikao hicho. Kulia kwake waliokaa ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kushoto kwake ni Naibu Msajili, Mhe.Zabibu Mpangule.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 


JAJI MSTAAFU RUTAKANGWA AMTEMBELEA JAJI MKUU MASAJU

  • Atoa mada kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Edward Rutakangwa jana tarehe 09 Julai, 2026 alimtembelea  Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju na kupata fursa ya kufanya naye mazungumzo mafupi ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.  

Aidha, kabla ya kumtembelea Jaji Mkuu, Mhe. Rutakangwa alitoa mada tatu kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wapya tisa wanaopatiwa Mafunzo Elekezi kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Mafunzo hayo yanalenga kuwaandaa kuanza kutekeleza majukumu yao katika ngazi hiyo ya juu katika mfumo wa utoaji haki nchini.

Mada alizotoa kwa Majaji hao ni Sheria ya Mahakama ya Rufani (Appellate Jurisdiction Act) pamoja na Kanuni za Uendeshaji Mashauri katika Mahakama ya Rufani (Court of Appeal Rules, Madaraka ya Mahakama ya Rufani kurejea maamuzi (Suo Motto Revisional Powers of the Court of Appeal) pamoja na Maombi ya Marejeo (Application for Revision).

Mhe. Rutakangwa leo tarehe 10 Julai, 2026 anawapitisha Majaji hao wapya wa Mahakama ya Rufani katika mada inayohusu Maombi ya Mapitio (Application for Review) na mwisho eneo la ufanyaji kazi wa pamoja (Collegiality at the Court of Appeal).


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akisalimiana na Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Edward Rutakangwa wakati Jaji Mstaafu, Mhe. Rutakangwa alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 09 Julai, 2026.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) na Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Edward Rutakangwa wakiwa katika wakizungumza jambo wakati Jaji Mstaafu, Mhe. Rutakangwa alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 09 Julai, 2026.

Picha ya pamoja, kulia ni
 Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akiwa na Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Edward Rutakangwa wakati Jaji Mstaafu, Mhe. Rutakangwa alipomtembelea na kufanya mazungumzo mafupi na Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 09 Julai, 2026.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na
Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Edward Rutakangwa wakati Jaji Mstaafu huyo alipomtembelea na kufanya mazungumzo mafupi na Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 09 Julai, 2026.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyesimama mbele kushoto) akizungumza na Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Edward Rutakangwa wakati Jaji Mstaafu huyo alipotoa mada kwa Majaji wapya wa mahakama ya Rufani tarehe 09 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 

Alhamisi, 9 Julai 2026

YAZINGATIENI NA KUYAJALI MAKUNDI YENYE MAHITAJI MAALUM: JAJI MKUU

Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama - Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Mawakili wapya wa Kujitegemea kutenda haki huku wakiyazingatia, kuyaheshimu, kuyajali na kuyapa kipaumbele makundi yenye mahitaji maalum wakiwemo Wajane,  Watoto, Wajawazito, Wazee na Watu wenye ulemavu.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 09 Julai, 2026 alipokuwa akitoa hotuba yake katika Hafla ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza na Mawakili hao Jaji Mkuu amewasisitiza kuendelea kutekeleza majukumu yao huku wakimtanguliza Mungu kama ambavyo wote wamekiri uwepo wa Mungu kupitia viapo vyao.

Ameeleza kuwa, Mawakili wana mchango mkubwa katika kuisaidia Mahakama kufanya maamuzi yanayozingatia haki kutokana na uhalisia wa matukio bila upendeleo huku wakitenda haki bila kufungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi na kutekeleza jukumu la kusimamia upatikanaji haki kwa ufanisi, jambo litakaloiwezesha Mahakama kuifikia azma ya kutoa haki mapema ipasavyo.

“Moja nikiwakumbusha sisi wenzetu huku mahakamani umuhimu wa kutenda haki bila kufungwa na masharti ya kiufundi kupita kiasi. Sasa sisi mahakamani, Mahakimu na Majaji hatukai peke yetu. Tunasaidiwa na ninyi Mawakili mlioko kwenye utumishi wa umma na Mawakili mnaojitegemea. Ninazungumza na ninyi kuwataka mtusaidie,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Aidha, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, Serikali imetunga sheria inayowawezesha Mawakili kutoa msaada wa kisheria kwa Watanzania wasio na Mawakili na wale wasio na uwezo wa kumudu gharama za Mawakili hivyo ni jukumu la Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kutekeleza jukumu hilo, huku akiwasihi kutekeleza jukumu hilo kwa ufanisi ipasavyo na si kwa unyonge kwa kuwa dhamira yao ni njema kuwasaidia watu masikini…...” Na mnavyotekeleza hilo jukumu litekelezeni kwa ufanisi ipasavyo na wala sio kwa unyonge. Kwa sababu dhamira yenu ni njema mmejiwekea hiyo ninyi wenyewe.”

Akizungumzia kuhusu uhuru wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), kama ilivyoanzishwa na Ibara ya 59B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, hiyo ndio ofisi iliyopewa mamlaka ya kufungua, kuendesha na kusimamia mashauri yote, na kwamba inapokuwa ikitekeleza jukumu hilo ikiongozwa na Mkurugenzi wa Mashtaka, Katiba imeelekeza katika Ibara ya 59B(4) kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa huru, hataingiliwa na mtu yeyote au na mamlaka yeyote isipokuwa itazingatia mambo matatu, moja nia ya kutenda haki, kuzuia matumizi mabaya ya taratibu za utoaji haki na maslahi ya umma. Akisisitiza kwa kusema “ishini mambo hayo yote kwa namna ambayo tunataka watu wapate haki.”

Ameongeza kuwa, zipo kanuni zilizotungwa na Mahakama mahsusi kwa ajili ya makundi ya watu maalum katika jamii ambazo zilitangazwa katika gazeti la Serikali namba 110 mwaka 2019 kanuni zinazowahusu watu wa makundi maalum ambao ni Wajane, Watoto, Wajawazito,Wazee na Watu wenye ulemavu ambao wanatambulika kutokana na tamaduni za kijamii, kiuchumi zilizopo katika jamii ambazo sio rafiki na wanabaguliwa au wamekuwa waathirika wa muda mrefu wa ukiukwaji wa haki.

Kadhalika, amewataka kutenda kwa umakini na kuendelea kuwajibika vema na kwamba ikiwa hawatafanya hivyo basi watawajibishwa na Mahakama endapo Mungu atachelewa kuwaadhibu hapa duniani.

Mimi nataka kila mmoja wetu anaposhughulika na mashauri haya awe makini. Sisi hatutamfuata mmoja mmoja huko na kuanza kumchapa viboko lakini tukimjua kwamba anacheza na haki za watu hawa, kama Mwenyezi Mungu atachelewa kumuwajibisha, sisi hapa tutamuwajibisha,” amesema Mhe. Masaju.

Amefafanua kuwa, kanuni zinaeleza wazi kuwa, mashauri yoyote ya Haki Jinai au Haki Madai yanayohusu watu kutoka katika makundi maalum yanapaswa kuhitimishwa ndani ya miezi sita kuanzia tarehe ya kuanza kwa usikilizaji wake isipokuwa kama Mahakama inaweza katika hali ya kipekee kuongeza muda huo kwa kipindi kisichozidi miezi mitatu.

“Jaji au Hakimu anayesikiliza kesi inayohusu mtu kutoka katika kundi maalum atatakiwa kuzipa kipaumbele kesi hizo kuliko kesi nyingine zote katika hatua zote ikiwemo usajili, usikilizaji na utoaji wa maamuzi na ninyi mtawakumbusha wanaozembea kwamba kuna maelekezo ya Mheshimiwa Jaji Mkuu, mzipe kipaumbele kesi hizi,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameeleza kuwa, ni wajibu wa Mahakama kuteua Afisa Dawati ili kusimamia kesi za makundi maalum huku akirejelea kitabu cha Zaburi 41: 1-3, inayosisitiza kumkumbuka mnyonge…. Heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu, Bwana atamlinda na kumhifadhi hai, naye atafanikiwa katika nchi, wala usimtie katika hali wamtakiayo adui zake…… akaongeza kuwa “msipowahudumia kwa haki wanyonge mnakaribisha laana katika familia zenu kuanzia kizazi cha kwanza hadi cha nne, hatuwezi kufanikiwa katika nchi kama tutakuwa tunawadharau wanyonge.”

Amezitaja kazi za Afisa Dawati kuwa ni pamoja na kutambua kesi na wahusika na kuwasilisha taarifa hizo kwa Jaji au Hakimu aliyepangiwa kesi hiyo, kuwatambua watu wenye uhitaji maalum, kuanzisha na kutunza kanzidata ya kesi zinazohusu makundi maalumu, kutoa elimu na kuwaongoza wafanyakazi wengine kuhusu masuala ya makundi maalumu na kutekeleza majukumu mengine yote kama yatakavyoelekezwa na Jaji au Hakimu Mfawidhi, huku mahakamani hilo litekelezeni kwa ufanisi ipasavyo.

Aidha, amewataka Mawakili kushirikiana na Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama katika utekelezaji wa majukumu yao na yenu huku wakizingatia uadilifu, faraja kwa wanyonge, staha, uaminifu, uwezo wa kumudu majikumu na ushirikiano.

Katika hatua nyingine, ameitaka TLS kulinda na kusimamia sheria na utekelezaji wa kanuni zinazogusa makundi maalum huku wakiwa sauti kwa wasio na sauti, wakitoa mchango wao wa usaidizi wa sheria kwa makundi hayo wakitekeleza majukumu yao kwa uadilifu, akili weledi na busara.

Amewataka Mawakili hao kutimiza wajibu wao wa kuwa mstari wa mbele kuwakumbusha Majaji na Mahakimu katika mashauri ya Haki Jinai na Haki Madai kwa heshima na si kulaumu, pia wajiulize wanatekeleza wajibu gani kama inavyoelekezwa katika kifungu cha 75 cha Sheria ya Mawakili (Sura ya 341 Marejeo ya 2023), hivyo ni vema kwa pamoja kutekeleza ipasavyo sheria na kanuni zilizowekwa.

Pia, amewaasa Mawakili hao kuendelea kuwaenzi wazazi, wenza wao, ndugu, jamaa na marafiki ambao walikuwa pamoja nao kwa kipindi chote hadi walipofika walipo…… amesema, “muwaenzi wazazi wenu na ninyi mliooa na mlioolewa muwaheshimu wenzi wenu kwa kuheshimu mchango wao kwani ni kuenzi utu na heshima kama inavyoelezwa katika amri ya 4 inayosema waheshimu baba yako na mama yako, upate miaka mingi na heri duniani…… nendeni mkatekeleze majukumu yenu kwa haki, usawa na uadilifu Mahakama itaendelea kufuatilia utendaji wenu.”

Ameuhakikishia Umma wa Watanzania kwamba, Mahakama itaendelea jukumu lake la msingi la kutoa haki mapema ipasavyo kwa mujibu wa sheria.

Hii ni sherehe ya 74 ya kuwapokea Mawakili, tangu kuanzishwa kwake mwaka 1986 kupokelewa na kukubaliwa waombaji hao 655 kunafanya idadi ya Mawakili walioandikishwa kufikia 14,875.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba yake wakati wa Hafla ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika leo tarehe 09 Julai, 2026 katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Baadhi ya Mawakili wapya kati ya 655 waliokubaliwa na Kuwapokewa na Jaji Mkuu leo tarehe 09 Julai, 2026 katika Viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama na Mawakili wapya wakifuatilia yanayojiri katika hafla
ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika leo tarehe 09 Julai, 2026 katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Picha mbalimbali za Mawakili wapya 655 waliokubaliwa na kupokewa leo tarehe 09 Julai, 2026 na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria Sherehe ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya na wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katiba (aliyesimama kushoto) na Katibu wa Bunge la Tanzania, Bw. Baraka Leonard katika Sherehe ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya na wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Wataalam wa Sheria waliohudhuria katika Sherehe ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya na wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja Mawakili wapya (walioketi nyuma). Wa nne kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa tatu kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya, wa nne kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa kwanza kushoto ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba na wa kwanza kulia ni Katibu wa Bunge la Tanzania, Bw. Baraka Leonard.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama)