Alhamisi, 12 Februari 2026

MTENDAJI MKUU AMETOA WITO KWA MAAFISA USAFIRIRSHAJI KUONGEZA UMAKINI WANAPOTEKELEZA MAJUKUMU YAO

Na. HABIBA MBARUKU & INNOCENT KANSHA - Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka madereva kuongeza umakini wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao ili kupunguza ajali zisizokuwa za lazima pamoja na kupunguza uharibifu wa vyombo vya usafiri na kulinda afya za wateja wao.

Pro. Ole Gabriel ameyasema hayo wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Aidha, Prof. Ole Gabriel, amesema mafunzo hayo maalum kwa madereva wote wa Mahakama, yamelenga kuimarisha huduma kwa mteja, kuzingatia maadili ya kazi na kuongeza usalama barabarani, mafunzo hayo yaliyoandaliwa chini ya mada ya Huduma kwa Mteja kwa kada ya madereva au maafisa usafirishaji yamesisitiza nafasi muhimu ya dereva katika mnyororo wa huduma za utoaji haki ndani ya taasisi, huku akibainisha kuwa kila mtumishi ana mchango wa moja kwa moja katika taswira na ufanisi wa Mahakama.

“Kuna mambo mengi yanachangia utulivu wa mawazo na kufanya kazi kwa timu kama vile kupata stahiki bora ni msingi wa mafanikio katika taasisi yoyote, uzembe wa kada moja unaweza kuathiri kada nyingine, hivyo ni muhimu kila mmoja kutimiza wajibu wake kwa umakini na weledi,” amesisitiza Prof. Ole Gabriel.

Akizungumzia dhana ya mteja, Mtendaji Mkuu huyo amefafanua kuwa, mteja ni yeyote anayenufaika na huduma inayotolewa, akiwemo kiongozi anayeendeshwa, watumishi wa Mahakama pamoja na wadau wengine barabarani. Amesisitiza kuwa utoaji wa huduma haupimwi tu kwa kutekeleza jukumu, bali kwa namna huduma hiyo inavyotolewa.

Vilevile katika mada ya matarajio ya mteja, madereva wamekumbushwa kuzingatia mambo kumi muhimu ikiwemo usahihi na umahiri katika kazi, usafi wa gari na muonekano binafsi, kutunza muda, usalama, utulivu barabarani na kutunza siri za kikazi na binafsi za viongozi wanaowahudumia.

Kadhalika, Prof. Ole Gabriel ameainisha sehemu ya changamoto zinazowakabili maafisa usafirishaji wa Mahakama nchi nzima, zikiwemo usimamizi wa bajeti binafsi, msongo wa mawazo ya kifamilia, bajeti finyu za matengenezo ya magari na wakati mwingine kukosa heshima kutoka kwa baadhi ya viongozi. Hata hivyo, amewataka madereva hao kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi licha ya changamoto hizo.

Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa, katika kuimarisha maadili ya kazi, Itifaki ya Dereva Bora, inajumuisha mavazi ya heshima, kuepuka kupiga honi ili kumuita kiongozi badala yake dereva anaweza kuwasiliana na kiongozi  wake kwa  njia ya ujumbe mfupi wa maandishi au kumpigia simu baada ya dakika kumi ikiwa ujumbe hautajibiwa, kuweka simu katika hali ya ukimya wanapoendesha, kutoingia katika mabishano barabarani, kufika mapema kabla ya muda wa safari walau dakika kumi kabla ya safari na kuepuka matumizi ya pombekabla ya safari na wakati wa safari.

Akizungumza kuhusu usalama, Mtendaji Mkuu amewakumbusha kuwa dereva anakabidhiwa chombo cha thamani kubwa pamoja na uhai wa abiria na uhai wake mwenyewe, hivyo ni lazima kuhakikisha gari liko katika hali nzuri kabla ya safari, dereva asikubali kuendesha gari bovu lisilokaguliwa kabla ya safari, ahakikishe yuko kwenye afya njema ili kuepuka uzembe unaoweza kusababisha ajali na kuleta hasara kubwa kwa taasisi.

Mafunzo hayo pia yaligusia tabia tano za kuepuka ili kutoleta usumbufu kwa kiongozi, zikiwemo kuanza safari bila kukagua gari, kubishana na kiongozi, uzembe katika mapokezi, kutoa taarifa za siri na kufokeana na wadau wengine wa barabara.

Aidha, Prof. Gabriel amesisitiza kuwa, mteja ndiye sababu ya ajira ya mtumishi, hivyo madereva wanapaswa kushirikiana kwa pamoja, kuepuka majungu na kuweka kipaumbele katika utunzaji wa magari pamoja na maisha ya wanaowahudumia.

Mafunzo hayo ni juhudi za Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utendaji kazi na kuhakikisha huduma zinazotolewa kwa umma zinazingatia viwango vya juu vya taaluma na maadili.

 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (katika mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Maafisa Usafirisha wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya mafunzo elekezi kwa huduma kwa mteja.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (katika mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Maafisa Usafirisha wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya mafunzo elekezi kwa huduma kwa mteja.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifanya wasilisho wakati alipotoa mafunzo elekezi kwa madereva wote wa Mahakama ya Tanzania nchini waliohudhuria ana kwa ana na wengine kwa njia ya mahakama Mtandao, leo terehe 12 Februari, 2026, katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiteta jambo na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick (kushoto) wakati wa mafunzo hayo elekezi kwa Maafisa Usafirishaji (hawapo pichani) 

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia mafunzo hayo.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia mafunzo hayo.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

 

 

 

MAAFISA USAFIRISHAJI WA MAHAKAMA WATAKIWA KUZINGATIA TAHADHARI, USALAMA WA VYOMBO VYA MOTO

Na. Halima Mnete & James Busanya - Mahakama

Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania nchini wamehimizwa kuongeza umakini, nidhamu na kuzingatia kwa kina misingi ya udereva wa kujihami ili kupunguza ajali zinazotokea wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ya kimahakama.

Wito huo umetolewa leo tarehe 12 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodma katika kikao maalum kilichowakutanisha madereva hao na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, kilicholenga kujadili masuala ya usalama barabarani, ustawi wa madereva pamoja na changamoto wanazokumbana nazo katika utendaji wa kazi zao za kila siku.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Kitengo cha Usafirishaji cha Mahakama ya Tanzania , Bw. Shedrack Bambaganya, amesema kuwa, katika kipindi cha hivi karibuni kumekuwepo na ajali kadhaa zilizowakumba madereva wa Mahakama wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hali iliyosababisha madhara ya kibinadamu pamoja na uharibifu mkubwa wa magari ya Taasisi.

Ameeleza kuwa, ajali hizo zimeongeza gharama kubwa kwa Mahakama, zikiwemo gharama za matengenezo ya magari, ucheleweshaji wa ratiba za shughuli za kimahakama na hatari ya kupoteza maisha ya watumishi pamoja na wananchi wanaohudumiwa.

“Haya ni matukio ya bahati mbaya, lakini ni wajibu wetu kuongeza tahadhari zaidi barabarani. Tunapaswa kuzingatia kanuni za usalama, kutumia udereva kwa kujihami na kuwa makini muda wote tunapokuwa barabarani. Usalama wa maisha ya wateja wetu na watumiaji wengine wa barabara ni kipaumbele,” amesisitiza Bw. Bambaganya.

Aidha, ameongeza kuwa, zipo changamoto ambazo madereva hukutana nazo, zikiwemo ajali zinazosababishwa na uzembe au mwendo kasi wa madereva wa Taasisi nyingine na watumiaji wengine wa barabara. Akitolea mfano; ajali iliyotokea Nzega mkoani Tabora katika msafara wa Jaji Kiongozi, alisema kuwa msafara huo ulikuwa katika upande sahihi wa barabara, lakini dereva wa Taasisi nyingine ya Umma aliendesha kwa mwendo kasi bila kuchukua tahadhari, hali iliyomfanya ashindwe kudhibiti gari na kusababisha ajali.

Aidha, Bw. Bambaganya amefafanua kuwa, kutokana na umakini, uzoefu na ustadi wa dereva wa Jaji Kiongozi, aliweza kulidhibiti gari kwa haraka na kuokoa maisha ya waliokuwamo ndani ya gari hilo, licha ya gari kuharibika vibaya na kuhitaji matengenezo ya gharama kubwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick aliwashukuru madereva kwa kuitikia wito wa kikao hicho na kutoa maoni yao kwa uwazi na pia kuwasilisha changamoto mbalimbali wanazokutana nazo kazini. Mkurungenzi huyo ameahidi kuwa, uongozi wa Mahakama unatambua mchango mkubwa wa madereva katika kuhakikisha shughuli za kimahakama zinafanyika kwa wakati na kwa usalama.

Vilevile, miongoni mwa changamoto zilizotajwa na madereva ni suala la kupanda vyeo kwa waliopo katika madaraja ya chini, pamoja na uhitaji wa mafunzo ya mara kwa mara ya usalama barabarani. Bi. Beatrice aliahidi kuwa uongozi utayafanyia kazi masuala hayo kwa kushirikiana na kitengo cha ndani cha malalamiko cha kuwahudumia watumishi (Judiciary Internal Customer Services) ili kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza motisha kwa madereva hao.

Kikao hicho kimetajwa kuwa hatua muhimu ya kuimarisha mawasiliano na ushirikiano kati ya uongozi na madereva kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuboresha usalama barabarani, kulinda rasilimali za Mahakama na kuhakikisha utekelezaji wa majukumu ya kimahakama unafanyika kwa ufanisi, uwajibikaji na weledi.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Beatrice Patrick akijibu baadhi ya hoja zilizowasilishwa na Maafisa Usafirishaji kwenye mafunzo elekezi yaliyoendeshwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani)

Mkuu wa Kitengo cha Usafirishaji cha Mahakama ya Tanzania Bw. Shedrack Bambaganya akifafanua jambo wakati wa mafunzo elekezi kwa Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.
Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.


Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa wanafuatilia kwa makini mafunzo hayo elekezi.

Sehemu ya Maafisa Usafirishaji wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya mafunzo hayo elekezi yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha)

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

 

 

Jumatano, 11 Februari 2026

MAJAJI WA MAHAKAMA YA RUFANI WAPO MUSOMA KUSIKILIZA MASHAURI

Na FRANCISCA SWAI-Mahakama, Musoma

Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani wapo mjini Musoma kwa ajili ya usikilizaji wa mashauri 48 kwenye kikao kitakachofanyika kwenye masjala ndogo iliyopo katika jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma.

Kikao hicho kilichoanza tarehe 09 Februari, 2026 kitahitimishwa tarehe 06 Machi, 2026.  Kinaongozwa na Mhe. Dkt. Gerald Ndika ambeye ni Mwenyekiti. Majaji wengine wanaounda jopo hilo ni Mhe. Patricia Fikirini na Mhe. Mustapha Ismail.

Usikilizaji wa mashauri hayo ulitanguliwa na kikao cha maandalizi (Pre Session), huku Majaji wakisisitiza Wadau kukamilisha maandalizi yao mapema, kuzingatia muda ili kuhakikisha mashauri yanasikilizwa kama ilivyopangwa.

Kwenye kikao hicho, kwa mujibu wa Naibu Msajili, Mhe. Omary Kingwele, mashauri yatakayosililizwa ni rufaa mbili za madai na mengine yanahusu jinai.

Kabla ya kuanza kikao hicho, Jopo la Majaji hao lilipata nafasi ya kusalimiana na watumishi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma. Watumishi hao waliwakaribisha Majaji hao na kuahidi kuwapa ushirikiano.

Sehemu ya wadau walioshiriki katika kikao cha maandalizi (Pre Session) kilichofanyika Mahakama Kuu Musoma na kuongozwa na Jaji Patricia Fikirini na Jaji Mustapha Ismail.

Watumishi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakisikiliza kwa makini wakati wa mapokezi ya Jopo la Majaji hao.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, akisalimiana na Viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu Musoma pamoja na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mbeya.


 

KIKAO KAZI CHA MAPITIO, MAREKEBISHO YA KANUNI ZA MAHAKAMA ZA WATOTO CHAFANYIKA

Na ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro

Mahakama imeendelea kuchukua hatua madhubuti katika kuimarisha utoaji wa haki kwa watoto kwa kuandaa kikao kazi maalum,  kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), ili kupitia kanuni za Mahakama za Watoto  za mwaka 2016 kwa ajili ya kuziboresha.

Uboreshaji huo unalenga kuzifanya kanuni hizo ziendane na mabadiliko ya sheria yaliyotokea, kuongeza ufanisi, tija na weledi katika usikilizaji na uamuzi wa mashauri ya watoto.

Kikao kazi hicho cha siku tano kilianza tarehe 9 Februari, 2026 kikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha,  Mhe. Nyigulila Mwaseba, kikihusisha mijadala ya kina, mapendekezo ya kitaalamu pamoja na kubadilishana uzoefu juu ya utekelezaji wa sheria na  kanuni hizo.

Aidha, kikao hicho  kinafanyika katika ukumbi wa mkutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki  (IJC) Morogoro na  kimewakutanisha wataalamu mbalimbali wa haki za mtoto, wakiwemo Naibu Wasajili, Mahakimu,Wizara za Kisekta, Taasisi za Kiserikali na Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Maafisa Ustawi wa Jamii, Maafisa wa Jeshi la Polisi, pamoja na Mawakili na Wanasheria kutoka Taasisi mbalimbali za kisheria.

Mwenyekiti wa kikao hicho,  alieleza kuwa Kanuni za Mahakama ya Watoto hazijawahi kufanyiwa mapitio tangu kuanza kutumika mwaka 2016. Alibainisha kuwa hali hii imezua changamoto katika utekelezaji wake kutokana na mabadiliko ya kisheria yaliyotokea baada ya kipindi hicho. Aliweka msisitizo mkubwa katika umuhimu wa kuzingatia ulinganifu wa kanuni hizi na sheria mama pamoja na misingi ya maslahi bora ya mtoto.

“Nadhani sheria hizi hazijawahi kufanyiwa marekebisho tangu mwaka 2016, nimekua nikiona changamoto mbalimbali haswa kutokana na mabadiliko ya teknolojia na sheria mbalimbali,” alisema Mhe. Mwaseba.

Kwa ujumla, kikao kazi hiki kinatarajiwa kuwa chachu ya maboresho makubwa katika mfumo wa utoaji haki kwa watoto nchini, kwa kuhakikisha kuwa sheria zinazotumika zinaendana na mahitaji ya sasa ya kijamii, kisheria na kiteknolojia, huku maslahi ya mtoto yakiendelea kuwa kipaumbele cha juu.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha,  Mhe. Nyigulila Mwaseba akifungua kikao hicho.

Picha ya kikao kazi wakiwa wanajadili maboresho ya kanuni hizo.

Picha ya pamoja ya kikao kazi hicho.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mbeya.

MAHAKAMA KANDA YA SONGEA YAFANYA KIKAO KUJADILI MPANGO MKAKATI WA MASHAURI, UTAWALA

Na NOEL SYLIVESTER - Mahakama Kuu, Songea

Uongozi wa Mahakama Kanda ya Songea, hivi karibuni ulikutana na  Mahakimu wote kujadili mpango mkakati wa kimahakama na kiutawala kwa mwaka 2026 ili kuboresha utendaji kazi, uadilifu na ushilikiano.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Taasisi ya Kupamba na Kuzuia Rushwa (PCCB) wilayani Songea mkoani Ruvuma, kiliongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. James Karayemaha na kuhudhuriwa na Viongozi wengine wa Mahakama kwenye Kanda hiyo.

Viongozi hao ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe, Naibu Msajili, Mhe. Elizabeth Nyembele pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Bw. Allan Mwela.

katika hotuba yake ya ufunguzi wa kikao hicho, Jaji Mfawidhi alielezxa kuwa wamekutana kujadili mpango huo kuhusu mashauri na masuala ya kiutawala kwa mwaka 2026, ambao unalenga kuimarisha utoaji wa haki kwa wakati, kwa uwazi, kwa usawa na kwa kuzingatia misingi ya sheria.

‘Tunatarajia mpango huu utatusaidia kupunguza mlundikano wa mashauri, kuboresha usimamizi wa mashauri, kuimarisha nidhamu ya kazi na kuongeza ufanisi katika utawala wa Mahakama zetu. Tukifanya mipango yetu vizuri hatutakuwa na msongo wa mawazo, tutajijengea uaminifu, tutaboresha namna ya kutoa uamuzi na tutapata matunda tunayoyatamani,’ alisema.

Mhe. Karayemaha aliongeza kuwa wakati wa kutekeleza jukumu la utoaji haki lazima kukumbuka viapo vyao vya kutoa uamuzi wa haki kwa kuzingatia matakwa ya Ibara ya 4, 107A na 107B ya Katiba.

‘Msingi wake ni kuimarisha amani na udugu wa wananchi. Kwa hiyo, sisi waamuzi inatupasa kuzingatia sheria na maadili ya utumishi wetu. Tukifanya kazi yetu ipasavyo bila woga tutadumisha utawala wa sheria, ambalo ni jukumu letu pia. Hii sio hiari, tumeelekezwa na Ibara ya 26 ya Katiba kuwaadhibu na kuwawajibisha ipasavyo wanaokiuka masharti ya Katiba na sheria zetu,’ alisema.

Aliwakumbusha Mahakimu hao kuwa wanalo pia jukumu la kulinda uhuru wa Mahakama unaolindwa na kuhifadhiwa katika Ibara ya 30(2)(d) ya Katiba ikichagizwa na Kifungu cha 114 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu.

Jaji Mfawidhi alibainisha kuwa pale inapotokea uhuru wa Mahakama umechokonolewa au kupakwa matope kwa kauli au vitendo, wanapaswa kumama imara kuwakumbusha hao kuhusu heshima na uhuru wa Mahakama.

‘Woga ni sumu ya mafanikio na mabadiliko na inakinzana na malengo ya Mwenyezi Mungu, ni matarajio yangu kuwa katika kikao hiki tutajadili kwa uwazi changamoto zilizopo katika mashauri na utawala, tutoe mapendekezo ya vitendo na kujenga mikakati itakayotekelezeka kwa ufanisi katika mwaka 2026 na kuendelea,’ Mhe. Karayemaha alisema.

 









Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mbeya.


 

 

WATUMISHI MBEYA WAPATIWA ELIMU YA AFYA YA KINYWA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya wamepata elimu muhimu ya afya ya kinywa na meno tarehe 9 Februari, 2026. Elimu hiyo ilitolewa na Daktari Melkzedeck Japhet kutoka kliniki ya Confort Dental Care iliyopo Mwanjelwa, Jijini Mbeya.

Akitoa elimu hiyo Daktari Japhet alisisitiza mambo muhimu yakuzingatia ikiwemo, usafi wa kinywa ambapo Daktari alisisitiza kuhusu kusafisha meno angalau mara mbili kwa siku hasa usiku kabla ya kulala, kupunguza ulaji wa vyakula vyenye sukari nyingi ili kuzuia kuoza kwa meno na afya ya fizi ambapo daktari alisema dalili za magonjwa ya fizi, namna ya kuyatambua na matibabu yake.

Aidha Daktari Japhet aliongezea kwa kuwaasa watumishi hao kuvunja dhana potofu kuhusiana na magonjwa ya meno na matibabu ya meno kwa mama mjamzito na kueleza kuwa Mama mjamzito anaweza kupata matibabu ya meno inapohitajika, hakuna “mdudu mtoboa jino” bali ni bakteria na asidi zinazotokana na sukari na kwamba kung’oa jino si lazima kufanyika asubuhi pekee na chakula kinaweza kuliwa kabla ya kung’oa jino kulingana na ushauri wa daktari, mambo ambayo walio wengi huwa na dhana potofu.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga, alitoa shukrani kwa daktari kwa kutenga muda na kutoa elimu hiyo, alisisitiza kuwa elimu hiyo imewafanya watumishi wa mahakama kutambua zaidi umuhimu wa kujali afya ya kinywa na meno kwa maisha bora na ufanisi kazini.

Daktari Melkzedeck Japhet (aliyesimama) akitoa elimu ya Afya ya kinywa na meno mbele ya watumishi wa Mahakama kuu Mbeya. 

Afisa Utumishi kutoka Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Bi. Sarah Rossi (wa pili kushoto) akiuliza swali kwenda kwa mtaalamu wa afya wakati wa utoaji elimu ya afya ya kinywa na meno.


Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (wa pili kulia) akiuliza swali Kwenda kwa mtaalamu wa afya wakati wa utoaji elimu ya afya ya kinywa na meno.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza Kulia), Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (Katikati), na wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mervis Miti wakipata elimu ya afya ya kinywa na meno.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Mbeya wakipata elimu kutoka kwa Mtaalamu wa Afya 



 

Jumatatu, 9 Februari 2026

MAJAJI, MAHAKIMU TABORA WAPATIWA MAFUNZO YA TEHAMA

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora imeendesha mafunzo maalum kwa Majaji na Mahakimu yanayolenga kuimarisha uelewa wa dhana na taratibu za kupokelewa kwa ushahidi wa kielektroniki pamoja Maadili na Mienendo (Nidhamu) ya Kimahakama.

Mafunzo hayo yaliendeshwa hivi karibuni na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Juma Mambi aliyewasilisha mada kuhusu ushahidi wa kielektroniki, pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert Martin Chuma aliyefundisha kuhusu maadili na nidhamu ya kimahakama kwa njia ya mtandao.

Akitoa mada yake, Mhe. Dkt. Mambi alieleza kwa kina dhana ya ushahidi wa kielektroniki, aina zake na masharti ya kisheria yanayozingatiwa ili ushahidi huo upokelewe mahakamani. Alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria husika, taratibu, pamoja na misingi ya uhalisia, uaminifu na uadilifu wa ushahidi huo.

“Katika zama hizi za teknolojia, Mahakama haziwezi kukwepa ushahidi wa kielektroniki. Hata hivyo, ni wajibu wa Mahakama kuhakikisha kuwa, ushahidi huo umepatikana na kuhifadhiwa kwa njia halali na kwamba haujabadilishwa,” alisema  Jaji Dkt. Mambi.

Aliongeza kuwa Mahakimu na Majaji wanapaswa kuwa makini katika kupima uzito wa ushahidi wa aina hiyo, hususan ujumbe wa simu, barua pepe, rekodi za miamala ya kielektroniki na vielelezo vinavyotokana na mitandao ya kijamii.

Kwa upande wake,  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert Martin Chuma alipowasilisha mada ya Maadili na Mienendo ya Kimahakama kwa njia ya Mtandao, alisisitiza kuwa maadili ni nguzo kuu ya uaminifu wa Mhimili wa Mahakama akieleza kuwa, huo ni wajibu wa kikatiba kisheria, kitaaluma na kimaadili akitolea mifano mbalimbali ya ibara za katiba, vifungu vya sheria na kanuni za maadili.

“Heshima na imani ya wananchi kwa Mahakama inaanzia kwenye mienendo yetu sisi Majaji na Mahakimu. Nidhamu ya kimahakama ni wajibu wa kikatiba, kisheria na kitaaluma,” alieleza.

Alifafanua kuhusu misingi ya uhuru wa kimahakama kwa kufanya kazi bila kupendelea, huba, hofu wala chuki na kuzingatia uadilifu, kujiepusha na mgongano wa maslahi pamoja na wajibu wa kuilinda hadhi ya Mahakama ndani na nje ya mazingira ya kazi.

Mafunzo hayo yaliwashirikisha Majaji wa Kanda hiyo wakiwemo Mhe. Dkt. Zainabu Mango na Mhe. Frank Mirindo pamoja na Naibu Msajili, Mahakimu Wakazi Wafawidhi na Mahakimu wa ngazi mbalimbali kutoka katika Kanda husika.

Washiriki walipata fursa ya kuuliza maswali, kubadilishana uzoefu, na kujadili changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa sheria na maadili ya kimahakama katika mazingira ya sasa yanayokua kwa kasi ya matumizi ya teknolojia.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Juma Mambi akiwasilisha mada kuhusu halali wa kupokelewa kwa ushahidi wa kielektroniki kwa Majaji na Mahakimu wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora yaliyotolewa hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi-Mahakama ya Hakimu Mkazi Tabora, 
Mhe. Gabriel Patrick Ngaeje akieleza wasifu wa 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert  Martin Chuma ambaye alifundisha kwa njia ya mtandao kuhusu Maadili na Mienendo ya Kimahakama wakati wa mafunzo.

Mahakimu wa ngazi mbalimbali wakifuatilia mada kwa umakini ili kuimarisha utoaji wa haki.

Washiriki wa mafunzo
wakifurahia mada jambo wakati wa mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, 
Mhe. Pamela Mazengo  akizungumza wakati wa mafunzo hayo.


Hakimu Mkazi, Mhe. Felix Ginene (aliyesimama) akichangia mada wakati wa Mafunzo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

Jumamosi, 7 Februari 2026

WATUMISHI WA MAHAKAMA MBEYA WATEMBELEA KITUO CHA KULEA WATOTO YATIMA CHA NURU

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa, wamefanya ziara ya kutembelea Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru. Ziara hiyo imefanyika tarehe 30/01/2026 na kuhusisha watumishi kutoka Mahakama Kuu Mbeya, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mahakama ya Wilaya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama za Mwanzo mkoani Mbeya. Aidha, ziara hiyo pia ilihudhuriwa na wadau wengine katika mnyororo wa utoaji haki, wakiwemo Jeshi la Polisi na Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya.

Watumishi hao walipokelewa na Meneja wa Kituo hicho, Bi. Mary Kassim Himiri, ambaye alitoa maelezo ya utangulizi kwa kuelezea historia fupi ya Kituo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2005 hadi sasa, pamoja na hali ya Kituo kwa sasa. Alieleza kuwa kwa sasa kituo kina watoto arobaini (40), ambapo wanne (04) kati yao wamehitimu elimu ya Sekondari Kidato cha Nne mwaka 2025. Aliongeza kuwa baadhi ya watoto wamechukuliwa na watu waliokuwa na nia ya kuwalea, kwa kufuata taratibu zilizowekwa na Kituo hicho kwa kushirikiana na Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya.

Aidha, Bi. Mary Himiri alizungumzia suala la ufadhili, ambapo alisema kuwa kwa sasa kituo hakina mfadhili wa kudumu na kinategemea misaada midogo midogo kutoka kwa watu binafsi au Taasisi zinazojitolea kusaidia pale inapohitajika.

“Hapo awali tulipata ufadhili kutoka Ubalozi wa Japan ambao walitujengea majengo mawili. Hata hivyo, tangu mwaka 2016, baada ya mwanzilishi wa kituo kufariki, hatuna tena ufadhili wa kudumu. Kwa sasa, tunategemea msaada wa watu binafsi wanaoguswa na hali ya Kituo na kujitolea kusaidia,” alisema Bi. Mary Kassim Himiri, Meneja wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru.

Kwa upande wake, Mhe. Victoria Nongwa akizungumza machache baada ya kukabidhi zawadi walizokwenda nazo kituoni hapo, ambapo alitoa shukrani na pongezi kwa uongozi wa kituo kwa kazi kubwa wanayoifanya.

“Tunatambua mchango mkubwa wa asasi hizi katika malezi ya watoto yatima na wenye mahitaji maalum. Tunatoa pongezi za dhati kwa uongozi na walezi wote wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru kwa jitihada mnazozifanya. Kwa niaba ya wenzangu wote, tunawashukuru kwa kila hatua mnayopiga, Mwenyezi Mungu awabariki sana,” alisema Mheshimiwa Nongwa.

Ziara hiyo pia ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, akiwemo Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu; Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mbeya Mjini, Mhe. Ayubu Shelimo, pamoja na viongozi wengine wa Mahakama Mkoa wa Mbeya.

Ziara hiyo ilihitimishwa kwa kutembelea miundombinu ya Kituo hicho na kufanya mazungumzo ya pamoja na watoto na walezi wao, ikiwa ni ishara na dhamira ya Mahakama amabayo siyo tu katika utoaji wa haki, bali pia katika kushiriki kikamilifu katika ustawi wa jamii.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa, akizungumza machache wakati wa ziara hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu (aliyeketi katikati) akiwa sehemu ya watu walioshiriki matatendo ya huruma katika ziara hiyo.

Meneja wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru Orphans Centre, Bi. Mary Himiri (aliyesimama katikati), akitoa neno la shukrani baada ya kupokea zawadi.

Sehemu ya watumishi waliotembelea kituoni hapo.

Sehemu ya watumishi walipotembelea kituo cha Nuru Orphans Centre; kutoka kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer; anayefuatia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu, akikabidhi zawadi walizokwenda nazo kituoni hapo.


Watumishi wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na walezi wa kituo, wapili kushoto ni Meneja wa kituo, na wa nne kushoto ni mlezi mkuu wa kituo hicho.


Watumishi wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na walezi wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru Orphans Centre.


Watumishi wa Mahakama wakiwa mbele ya Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru (Nuru Orphans Centre) Mbeya wakati wa ziara hiyo, (kushoto) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba, (wa pili kushoto) ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu na wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa.