Alhamisi, 2 Aprili 2026

MSAIDIZI WA SHERIA, WATUNZA KUMBUKUMBU WA MAHAKAMA KIGOMA WAPIGWA MSASA MATUMIZI YA TanzLII

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mkutubi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Rwechungura Achiles ametembelea Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma kuona hali ya huduma za Maktaba zinavyotolewa pamoja na kutoa elimu kuhusu matumizi ya Mfumo wa Taarifa za Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania (TanzLII).

Akitoa elimu ya matumizi ya mfumo wa TanzLII, tarehe 30 Machi, 2026, kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma, Bw. Achiles aliwapitisha vema Watunza Kumbukumbu na Msaidizi wa Jaji, ambao ndio wahusika wakuu wa kupandisha nyaraka katika mfumo huo.

“Mfumo huu ni rahisi kutumia ni maktaba mtandao inayotoa fursa kwa wananchi na wadau wa Mahakama kujipatia nyaraka za maamuzi ya Majaji kutoka Kanda zote za Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na Mahakama ya Rufaa, vilevile wanapata kusoma Gazeti la Serikali, Sheria na Kanuni, hotuba za Viongozi wa Mahakama na machapisho mbalimbali ya elimu kwa umma juu ya uboreshaji wa huduma zinazotolewa na Mahakama ya Tanzania katika Kanda na Mikoa yote nchini,” alisema Mkutubi huyo. 

Aliongeza kwa kusema kuwa, “Kigoma mnafanya vizuri katika upandishaji wa hukumu na maamuzi ya Majaji, nitawaongezea ujuzi kidogo hasa katika eneo la urekebishaji wa taarifa za nyaraka uliyopandisha kwa ajili ya wasomaji na wapakuwaji wa nyaraka hizo katika mfumo wetu wa TanzLII.”  

Kwa upande wake, Msaidizi wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Hassan Galiatano alimshukuru Bw. Achiles kwa kutoa elimu ya matumizi sahihi ya mfumo wa TanzLII, kwani itawasaidia kupandisha hukumu na maamuzi  ya Majaji kwa usahihi, lakini pia imewaongezea weledi wa kuendelea kutoa elimu ya jinsi gani wananchi na wadau wanaweza kupata nyaraka katika mfumo huo. 

Walioshiriki kupata elimu hiyo ya matumizi sahihi ya mfumo wa TanzLII ni Watunza Kumbukumbu na Msaidizi wa Jaji wa Mahakama Kuu Kigoma, ambayo imewaongezea weledi wa kutoa huduma za kupakia na kupakua nyaraka katika mfumo huo.

Mkutubi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Rwechungura Achiles akisisitiza jambo wakati akitoa elimu ya matumizi ya mfumo wa TanzLII kwa Msaidizi wa Sheria wa Jaji na Watunza Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma (hawapo katika picha).


Msaidizi wa Jaji wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Hassan Galiatano (wa kwanza kulia) na wengine wakifuatilia kwa makini elimu iliyokuwa ikitolewa na Mkutubi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Rwechungura Achiles (hayupo katika picha) kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma.

Watunza Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Kigoma, wakifuatilia kwa makini elimu iliyokuwa ikitolewa na Mkutubi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Rwechungura Achiles (hayupo katika picha).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA YAFANYA UTALII SERENGETI

Na KANDANA LUCAS-Mahakama, Musoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, amewaongoza wajumbe wa menejimenti kutembelea mapori ya akiba Ikorongo na Grumeti yaliyopo katika Hifadhi ya Wanyama Serengeti kwa ajili ya kufanya utalii.

Ziara hiyo ilifanyika baada ya kuhitimisha kikao cha menejimenti kilichofanyika mwishoni mwa mwezi Machi 2026. Ziara hiyo pia ililenga kuwapa fursa wajumbe na Watumishi wengine wa Mahakama kupata mapumziko mafupi na kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu uhifadhi wa Wanyamapori.

 Katika ziara hiyo, wajumbe waliweza kutembelea maeneo yenye Wanyama mbalimbali na walipatiwa elimu kuhusu uhifadhi na namna Wahifadhi wanavyokabiliana na changamoto za ujangili.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (mwenye kofia) na Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Musoma, Bw. Leonard Maufi, wakionesha kundi la Wanyamapori (hawapo pichani).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya akiwaongoza wajumbe wa menejimenti kufanya utalii wa kupanda mlima.

Kundi la Nyati wakiwa kwenye moja ya mapori ya akiba katika hifadhi ya Wanyama Serengeti.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati mwenye kofia mstari wa mbele) akiwa na  Viongozi wa mapori ya akiba Ikorongo na Grumenti pamoja na wajumbe wa menejimenti.

Meneja Mahusiano kutoka Grumeti Fund, Bw. David Mwakipesile, akitoa elimu ya uhifadhi wa Wanyamapori kwa wajumbe wa menejimenti (hawapo pichani).

Picha za wanyama Simba akiwa porini, mmoja akiwa juu ya mti huku mwingine akitembea.

Picha ya wajumbe wakiwa kwenye magari ya watalii.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora, akitoa neno kwa wajumbe wa menejimenti (hawapo pichani) wakati wa ziara ya utalii.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

 

NAIBU MSAJILI MBEYA AONGOZA KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI YA JINAI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama Mbeya

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya imefanya kikao cha kusukuma mashauri ya jinai kilichoongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu kwa lengo la kuimarisha usimamizi na ufanisi wa utoaji haki kwa wakati mapema ipasavyo.

Akizungumza katika kikao hicho Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, alibainisha kuwa azimio la kuhakikisha mashauri ya mlundikano hayavuki Desemba 2025 limefanikiwa kwa kiasi kikubwa, huku juhudi za kupunguza vielelezo mahakamani hasa dawa za kulevya, zikiendelea kwa kushirikiana na vyombo husika ili kuharakisha uteketezaji wake.

Akiwasilisha taarifa ya Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu alieleza kuwa, kwa sasa hakuna mashauri ya mlundikano kwa Mahakama Kuu Mbeya na kwa Mahakama za chini ni machache ambayo yamebaki kwa sababu maalumu ambapo mengine yanasubiri maamuzi ya Mahakama ya Rufani. Aliongeza kuwa, Mahakama Kuu imeweka rekodi mpya kwa kumaliza mashauri yote ya mlundikano.

Kikao pia kilipokea taarifa ya ujio wa Wahe. Majaji na watumishi wengine wa Mahakama ya Rufani mwezi Aprili 2026, pamoja na kuanza kwa vikao vya kesi za mauaji Mahakama Kuu Mbeya kuanzia tarehe 13 Aprili 2026.

Aidha, ilibainishwa kuwa, kutokana na kujitenga kwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mkoa wa Songwe, kutasaidia kupunguza mzigo wa mashauri katika Kanda ya Mbeya na idadi ya wafungwa na mahabusu katika Gereza Kuu la Ruanda Mbeya.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, akiwasilisha taarifa ya Mahakama Mkoa wa Mbeya, alizungumzia kuhusu jitihada za Mahakama kusimamia utoaji wa haki mapema ipasavyo:

“Kufuatia maelekezo ya Jaji Mkuu, mashauri yanapaswa kumalizika ndani ya miezi sita kwa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya na miezi mitatu kwa Mahakama za Mwanzo. Sote tushirikiane kuhakikisha kwamba ukomo huu unazingatiwa” alisema Mhe. Laizer

Vilevile, Mhe. Laizer alisisitiza umuhimu wa taarifa za Wafungwa na Mahabusu hususan utoro wa Mahabusu na wafungwa walio chini ya ulinzi halali, kufikishwa mapema mahakamani ili kuisaidia Mahakama katika kuandaa usikilizwaji wa mashauri mbalimbali.

Katika maazimio ya kikao hicho ilikubaliwa kuwa, taarifa muhimu za wafungwa, ikiwemo utoro, vifo, msamaha wa Rais au kumaliza kifungo, ziwasilishwe kwa wakati mahakamani ili kusaidia katika upangaji wa Vikao vya kusikiliza mashauri, ili mashauri yote yamalizika ndani ya miezi sita tangu kusajiliwa kwake na yaliyovuka muda huo yapewe kipaumbele yakamilike kabla au ifikapo Juni 2026.

Kikao hicho kilihudhuriwa na wadau wa mnyororo ya haki jinai wakiwemo Wahe. Mahakimu Mkoa wa Mbeya, Magereza, Polisi, Ofisi ya Upelelezi, Ofisi ya Mdhibiti Mali za Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Mbeya (NPS), Ustawi wa Jamii, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitengemea (TLS), Idara ya Marekebisho ya Tabia na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye pia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu (kushoto), akiendesha kikao hicho wakati wa kuwasilisha taarifa ya Mahakama Kuu Mbeya.

Mwakilishi wa Mkuu wa Gereza Kuu Ruanda Afisa Magereza akizungumza jambo katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau walioshiriki kikao hicho.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, akiwakilisha taarifa ya Mkoa wa Mbeya ikijumuisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mahakama za Wilaya na Mahakama zake za Mwanzo.




JAJI NONGWA ATETA NA WADAU WA MAHAKAMA NJOMBE

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amekutana na wadau wa Mahakama Taasisi mbalimbali zinazotoa huduma kwa wananchi ndani ya Kanda hiyo ili kuteta nao juu ya uanzishwaji wa shughuli za Mahakama Kuu Njombe

Akizungumza na wadau hao tarehe 30 Machi, 2026 aliwaeleza kuwa, Mahakama Kuu Kanda ya Njombe imeanza kufanya kazi Jumatatu tarehe 30 Machi, 2026.

Aidha, Mhe. Nongwa alisema kuwa, kuanza kazi kwa Mahakama hiyo kulianza kwa kufunguliwa kwa dirisha la kusajili mashauri. Hivyo, aliwaeleza Wadau wa Mahakama kuwa, lengo la kikao hicho ni kuzungumza kwa pamoja na kupeana ushauri katika kukabiliana na changamoto mbalimbali.

Pamoja na kushauriana na kufafanua zaidi pale penye changamoto za usikilizwaji mashauri kwa njia ya kieletroniki wakati yanapokatiwa rufaa, Jaji Nongwa ameomba ushirikiano wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) hasa kwa mashauri ya mauaji.

Kuhusu Baraza la Kata la Nyumba na Ardhi, Mhe. Nongwa amewasisitiza kuhusu mfumo wao ambao bado haujaungana na Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) hivyo, Baraza hilo litatakiwa kuwa na nakala laini pindi zinapohitajika mahakamani.

Kwa upande wa Madalali wa Mahakama, Jaji Mfawidhi huyo amewataka kufuata sheria kwenye mashauri yanayokaziwa hukumu kwa kuwa mashauri hayo yana hatua mbalimbali.

Alielezea jinsi ya ufunguaji wa mashauri kwa njia ya kieletroniki ya kutotumia karatasi (paperless) kwenye dirisha dogo la ufunguaji wa mashauri kupitia Mfumo wa Kieletroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) la Masjala ndogo ya Mahakama Kuu Kanda ya Njombe iliyoanza kutoa huduma zake kuanzia Siku ya Jumatatu tarehe 30 Machi, 2026.

Kwa upande mwingine Jaji Nongwa alisisitiza umoja na mshikamano kwa Mawakili na kwa  Taasisi nyingine za Haki Jinai ili waweze kutoa huduma kwa wateja ambao ni wananchi kwa weledi na ufanisi hasa kwa kutoa kipaumbele kwa wateja walio kwenye makundi maalum mfano kwa akinamama wajawazito, wazee na akina Mama wenye watoto wadogo.                                                                                     

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe kwa pamoja waliwashukuru Wadau wa Mahakama Kwa utayari wa kufika kwa ajili ya kumsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa na kuhaidi kuendeleza ushirikiano.

Wadau  walioshirikiki katika kikao  hicho ni  Ofisi ya  Mwendesha Mashtaka Mkoa wa Njombe, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa Njombe (RCO), Baraza La Nyumba na Ardhi, Mawakili wa Kujitegemea pamoja na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali kutoka Mkoa wa Njombe ambao walichangia hoja mbalimbali kwa pamoja juu ya uendeshaji wa Masjala ndogo ya Mahakama Kuu Njombe.

 Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania  Kanda ya Njombe,  Mhe. Victoria Nongwa akizungumza na Wadau wa mkoani Njombe. (hawapo katika picha) tarehe 30 Machi, 2026.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano  akizungumza na Wadau na Mawakili wa Mkoa wa Njombe (hawapo katika picha).

       Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu mkazi Mkoa Njombe Mhe. Liadi Chamshamu akitoa neno la shukrani kwa Wadau (hawapo katika picha) walioshiriki katika kikao.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Njombe, Bw. Richard Mbambe  akitoa neno la shukrani kwa wadau wa Mkoa wa Njombe. Nyuma yake ni Ofisa Utumishi, Bi. Happy Merere pamoja na wadau wengine waliohudhuria katika kikao hicho.

Wadau wa Mahakama pamoja wakifuatilia kinachojiri katika kikao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama mkoani humo. Aliyeketi kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano na kulia ni Mtendaji Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 

 

 

 

 

Jumatano, 1 Aprili 2026

MAHUSIANO KATI YA MAHAKAMA NA TAASISI ZA USULUHISHI NCHINI NI YA MSINGI; JAJI MKUU

  •    Jaji Mkuu abainisha hayo alipoteta na TIArb
  • Asema Usuluhishi una faida lukuki ikiwemo kuokoa muda, kupunguza gharama, kujenga & kuimarisha mahusiano.....

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa mahusiano kati ya Mahakama ya Tanzania na Taasisi za Usuluhishi nchini ni ya msingi kwakuwa kwa kufanya hivyo Mhimili huo unatekeleza takwa la kikatiba kwa mujibu wa Ibara ya 107(A)(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaitaka Mahakama kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 01 Aprili, 2026 katika ofisi yake ndogo iliyopo Mahakama ya Rufani Tanzania jijini Dar es Salaam wakati alipotembelewa na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb).

“Viongozi nawashukuru katika hatua hii ya kututembelea Mahakamani, katika hatua hiyohiyo ya kuimarisha mahusiano baina yetu na kama unavyoona Katiba inatupa maelekezo pamoja na kwamba sisi ndio wenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia tunatakiwa kukuza na kuendeleza Usuluhishi baina ya watu wanaohusika katika migogoro, kwa hiyo sisi kukutana nanyi ni sehemu pia ya utekelezaji wa maelekezo ya Katiba kwa sababu ninyi mnahusika, lakini pia tuna mahusiano haya ya kisheria kwamba mnaanza kusuluhisha halafu utekelezaji hatimaye unaishia mahakamani,” amesema Jaji Mkuu.

Hivyo, Mhe. Masaju ameeleza kuwa, mahusiano kati ya Mahakama na Taasisi zinazohusika na Usuluhishi si tu ya msingi bali pia yanapaswa kuwa endelevu.

Kuhusu masuala mtambuka yanayohusu ustawi katika utekelezaji wa jukumu la Usuluhishi, Mhe. Masaju amewashauri Viongozi wa TIArb kuzishirikisha pia Wizara za Kisekta zinazohusika na mambo hayo, mfano kuhusu mabadiliko ya Sheria ni vema kushirikisha Wizara ya Katiba na Sheria au Mwanasheria Mkuu wa Serikali kama ambavyo wanaishirikisha Mahakama, kadhalika Wizara ya Mipango na Uwekezaji inayoongozwa na Mhe. Prof. Kitila Mkumbo.

Jaji Mkuu ameongeza kuwa, Mahakama inaunga mkono utekelezaji wa Usuluhishi unaofanywa na Taasisi hiyo kwa kuwa Usuluhishi una faida nyingi ikiwa ni pamoja na utatuzi wa migogoro mapema, inajenga na kuimarisha mahusiano, inapunguza matumizi ya gharama pamoja na kuokoa muda.

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju amewashauri Viongozi na Wafanyakazi wa Taasisi hiyo kuimarisha uwezo wa kumudu majukumu yao (competency) kuwa na uadilifu katika utekelezaji wa jukumu hilo muhimu sambamba na kutatua na kumaliza migogoro mapema ipasavyo.

“Kwa upande wetu huku Mahakamani tunachukua hatua ya kurekebisha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai na yale majedwali  ’ zinarekebishwa na Jaji Mkuu akishirikiana na Waziri mwenye dhamana, tutarekebisha huu mwenendo ili tuondoe vile vifungu vya kiurasimu vinavyofanya migogoro ichelewe kumalizika,” ameeleza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewaeleza viongozi hayo kuwa, “ninyi ambao mnafanya hii kazi ya Usuluhishi mnafanya jambo jema na imeandikwa katika Kitabu cha Mathayo sura ya 5 kwamba, heri Wapatanishi maana wataitwa Wana wa Mungu; kwa hiyo ushauri wangu ni kwamba muifanye kazi hii kwa nia njema (passion).”

Hata hivyo, Jaji Mkuu amewataka Viongozi hao kutoka TIArb kuitangaza Taasisi hiyo ili ijulikane na vilevile wasisite kuishirikisha Mahakama kuhusu jambo lolote kuhusiana na suala zima la utekelezaji wa jukumu la usuluhishi huku akiwaalika kujumuika na Mahakama katika Wiki ya Usuluhishi nchini anayotarajia kuizindua tarehe 09 Aprili, 2026.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Taasisi wa Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Bw. Usaje Mwambene amemueleza Jaji Mkuu kuwa Taasisi hiyo ilianzishwa mwaka 1997 lengo likiwa ni kushughulikia migogoro ya kimkataba, kibiashara na kadhalika.

Bw. Mwambene amesema tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo imekua kwa kasi na sasa ina jumla ya wajumbe 363 wakiwemo Wanasheria, Wahandisi, Wahasibu, Wafamasia na wengine na pia imejumuisha wajumbe wa kimataifa (international members) ambapo kwa sasa wapo wajumbe sita.

Ameeleza kuwa, Taasisi hiyo pia inatoa ushauri kwenye masuala ya migogoro ya kibiashara na kwamba inahusika kujenga uwezo (capacity building) kupitia mafunzo mbalimbali inayotoa kwa wajumbe waliopo na wapya.

Aidha, Makamu huyo wa Rais wa TIArb amesema, Taasisi hiyo inaomba ushirikiano wa karibu na Mahakama hususan katika maeneo ya kujengeana uwezo kupitia mafunzo mbalimbali, kushirikiana katika baadhi ya matukio ya Kitaasisi ikiwemo Mkutano wa Mwaka wa Wasuluhishi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) walipomtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 01 Aprili, 2026 katika ofisi yake ndogo iliyopo Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akizungumza na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) walipomtembelea leo tarehe 01 Aprili, 2026 katika ofisi yake ndogo iliyopo Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam.

 Makamu wa Rais wa Taasisi wa Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Bw. Usaje Mwambene akizungumza jambo na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati yeye pamoja na wenzake walipomtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 01 Aprili, 2026 ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam. 

Mazungumzo yakiendelea....

Sehemu ya Washiriki wa Kikao wakichangia na kufuatilia kinachojiri katika mazungumzo hayo.

 Makamu wa Rais wa Taasisi wa Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Bw. Usaje Mwambene (kushoto) akimpatia Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju zawadi ya makablasha ya taarifa mbalimbali zinazohusu Taasisi hiyo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati ) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) walipomtembelea leo tarehe 01 Aprili, 2026 ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam. 

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)










 

 

 

 

 

JAJI MFAWIDHI MTWARA AFANYA UKAGUZI WA MAHAKAMA

Na SOJO STEPEHEN-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, amefanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Mkoa wa Mtwara ili kujionea utendaji kazi, hasa katika Mahakama za ya chini na kati kuhakikisha huduma ya utoaji haki inaendelea kufanya vyema.

Ziara hiyo ilifanyika tarehe 23 mpaka 25, Machi 2026. Miongoni mwa Mahakama zilizokaguliwa na ni Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya Tandahimba, Newala, Nanyumbu, Masasi, Mahakama za Mwanzo Makuta, Mkunya, Mchaulo na Lukuledi.

Ziara hiyo pia ilijumuisha mazungumzo ya pamoja na Watumishi wa Mahakama alizopita kwa ajili ya ukaguzi. Aliweza kupata taarifa za utendaji kazi, mafanikio, changamoto, mapato na matumiz.

Aidha, Jaji Mfawidhi pia alipokea mawazo na maoni kutoka kwa Watumishi wa Mahakama hizo na kuhimiza weredi wa kuihudumia jamii inayowazunguka.

Mhe. Kakolaki aliwapongeza Mahakimu na Watumishi wa Mahakama kwa utendaji bora na mzuri, hasa kumaliza mashauri kwa wakati, kutokuwa na mlundikano na kuwa na aina bora ya utunzaji kumbukumbu.

Katika ukaguzi huo pia, Jaji Mfawidhi aliwapongeza Watumishi wa Mahakama katika matumizi wa mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo inawezesha kufuatilia na kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao. Aliwasisitiza kuendelea kuwaelewesha Wananchi kwenye matumizi ya mifumo hiyo ili kupunguza gharama za kila mara.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Kanda ya Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga na Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi, Mhe. Stella Shindika

Jaji Mfawidhi pia alitembelea na kukagua Mahakama za Mwanzo zilizokuwa katika ujenzi na zile ambazo zilizokuwa tayari zimekamilika. Aidha, aliendelea kusisitiza ujenzi ufanyike kwa kuzingatia ubora na kwenda kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akipokelewa na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Newala.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, (wa tano kulia) katika picha ya pamoja na Watumishi alipotembelea Mahakama ya Mwanzo Mahuta Wilaya ya Tandahimba.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mkunya Wilaya ya Newala Mhe. Apatesile Mbalasila(kushoto), akisoma taarifa fupi ya Mahakama hiyo mara baada ya kumkaribisha Jaji Mfawidhi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto) akiwa na Mhe. David Msalilwa(katikati), Mhe Charles Mnzava (kulia) katika mazungumzo na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Tandahimba.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitembelea Mahakama ya Mwanzo Mchauru.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akiwa anakagua jengo la Mahakama ya Mwanzo Mchauru, ambalo lilipata maafa na kusababisha uharibifu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akikagua ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Masasi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


MAHAKAMA ZA MWANZO TATU KANDA YA MTWARA ZAZINDULIWA

Na SOJO STEPHEN-Mahakama, Mtwara

Mahakama za Mwanzo tatu zilizokuwa zinajengwa ndani ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, zimezinduliwa katika jitihada za kusogeza huduma za haki karibu zaidi na Wananchi, hasa waliopo katika maeneo ya vijijini.

Uzinduzi huo wa pamoja ulifanyika tarehe 27 Machi, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Chikundi kwa niaba ya Mahakama nyingine za Mwanzo Kitangari na Newala Mjini na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali pamoja na Wadau wa sekta ya sheria.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akiwa ameambatana na Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana na Mtendaji wa Mahakama ya Mtwara, Bw. Yusuph Msawana.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kakolaki alisema kuwa kuanzishwa kwa Mahakama hizo kutasaidia kupunguza msongamano wa mashauri na kuharakisha utoaji wa haki kwa Wananchi.

Alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Mahakama na Serikali kuhakikisha kila Mwananchi anapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Aidha, aliwahimiza Wananchi kutumia Mahakama kama njia sahihi ya kutafuta haki, badala ya kutumia mbinu au sheria zisizo sahihi ambazo zinaweza kusababisha migogoro zaidi.

Vilevile, aliwasihi Wananchi na Watendaji wa Mahakama kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha shughuli za Mahakama, kuharakisha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mashauri.

Mhe. Kakolaki aliwashukuru Wananchi, Viongozi wa Serikali pamoja na Wadau mbalimbali wa kijamii kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki uzinduzi wa Mahakama hizo zilizozinduliwa katika maeneo ya Chikundi, Kitangari na Newala Mjini.

“Napenda kuwashukuru Wananchi, Viongozi na Wadau wote kwa kushiriki uzinduzi huu wa Mahakama za Mwanzo za Chikundi, Kitangari na Newala Mjini. Ushiriki wenu unaonesha namna ambavyo jamii inathamini uwepo wa huduma za haki karibu na Wananchi,” alisema.

Alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania ina mikakati madhubuti ya kuhakikisha Wananchi wanapata haki bila kucheleweshwa wala kubaguliwa, na kwamba moja ya mikakati hiyo ni ujenzi wa Mahakama za Mwanzo katika maeneo mbalimbali nchini.

“Mahakama ya Tanzania imejipanga kuhakikisha kila Mwananchi anapata huduma ya kisheria kwa wakati na kwa usawa. Ndiyo maana tunaendelea kujenga Mahakama za Mwanzo ili kusogeza huduma hizi karibu zaidi na Wananchi,” aliongeza.

Naye Mtendaji wa Mahakama Mtwara alieleza kuwa Mahakama ina mkakati wa kuendelea kujenga majengo mapya na bora kwa ajili ya Mahakama mbalimbali nchini ili kuwezesha shughuli zote za utoaji wa haki kufanyika katika mazingira mazuri na yenye ufanisi.

“Ujenzi wa majengo haya ni sehemu ya mkakati wa kuboresha mazingira ya kazi kwa Watumishi wa Mahakama na kuhakikisha Wananchi wanapata huduma za haki katika maeneo yaliyo karibu nao na yenye miundombinu bora,” alisema.

Aidha, aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa juhudi zake za kuboresha miundombinu ya utoaji wa huduma za kisheria katika jamii, akisema hatua hiyo itaongeza ufanisi na kuimarisha imani ya Wananchi kwa Taasisi hiyo.

Vilevile, aliwasisitiza watumishi wa Mahakama kuyatunza majengo hayo na miundombinu mingine iliyojengwa ili yaweze kudumu na kuendelea kutoa manufaa kwa jamii pamoja na watumishi kwa ujumla.

Kwa upande wao, baadhi ya Wananchi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakisema itapunguza umbali waliokuwa wakisafiri kufuata huduma za Mahakama.

Mbali na viongozi hao, hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi, Fatima Saidi Kubenea. Katika hotuba yake, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwepo kwa ushirikiano mzuri kati ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Mahakama ili kuhakikisha huduma za haki zinawafikia wananchi kwa ufanisi zaidi.

Mahakama za mwanzo zitakuwa na jukumu la kusikiliza na kuamua kesi ya ngazi ya kwanza, madai kulingana na mamlaka yao kisheria. Wananchi wamehimizwa kutumia vyema fursa hiyo kwa kufuata taratibu za kisheria na kuepuka kujichukulia sheria mkononi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akiwasili katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Wageni waalikwa walioshiriki kwenye uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mtwra, Mhe. Said Ding’ohi (kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea pamoja wasikiliza taarifa ya ujenzi wa majengo ya Mahakama.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Mtwara akitoa hotuba yake katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo iliyofanyika Chikundi.

Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea akihutubia katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitoa hutuba katika uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo eneo la Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akikata utepe katika shughuli ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto,) Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya (katikati) na Jaji wa Mahakama ya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara (kulia) kwa pamoja wakikagua ukumbumbi wa wazi wa Mahakama ya Mwanzo Chikundi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Said Ding’ohi (wa pili kushoto), Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana (wa kwanza kushoto), Naibu Msajili, Mhe. Elia Mrema (wa kwanza kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Masasi Fatima Saidi Kubenea (wa pili kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Kanda ya Mtwara.

Habari hii imehaririwa na FAUSSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.