Jumapili, 10 Mei 2026

JAJI MKUU AWATAKA VIJANA WA KITANZANIA KUTUMIA VIPAJI VYAO KWA MANUFAA YA TAIFA

  • Ni wakati akizindua Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu
  • Ampongeza Wakili huyo kwa uandishi Kitabu hicho
  • Asisitiza juu ya umuhimu na faida za kuwa na Shukrani katika nyakati zote za maisha

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa wito kwa vijana wa Kitanzania waliopo katika fani mbalimbali kutumia vipaji vyao kuandika vitabu vitakavyotumika kwa manufaa ya Taifa.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 10 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Kitabu kiitwacho SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu. 

“Vijana msisubiri mpaka muwe na kila kitu ili muweze kutumia vipaji vyenu, hivyo natoa wito kwa vijana wa Tanzania; kuandika, kusoma, kutafakari na kuchangia Taifa letu kwa vipaji vyenu. Taifa linalowapa vijana nafasi ya kuandika na kubuni hujenga urithi wa maarifa na mshikamano wa vizazi,” amesema Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju ametoa rai kwa wananchi kuona wajibu wa kuunga mkono Waandishi wa Tanzania kwa kusoma kazi zao, kununua vitabu vyao, kuwapa mrejesho, kuwapa nafasi katika majukwaa ya mijadala na Vyombo vya Habari.

Akizungumzia kuhusu Kitabu hicho cha SING GRATITUDE ambacho amekizindua, Mhe. Masaju amempongeza Wakili Aisha kwa kukiandika na kusema kuwa, Kitabu hicho kina viwango na hadhi ya Kimataifa.

“Napenda kutumia fursa hii kumpongeza Wakili Aisha Saidi Kingu kwa ujasiri wa kuandika. Kuandika si kazi ndogo, inahitaji nidhamu, uvumilivu, kujitafakari na kukubali kubeba ujumbe ambao wengine wanaweza kuusoma, kuuchambua na kuuhoji. Ninampongeza pia kwa kuonesha kuwa kijana anaweza kuchangia ujenzi wa Taifa kwa njia nyingi. Mtu anaweza kuwa, Mwanasheria, Mshairi, Mwanadiplomasia, Msomaji na Mwandishi, kama alivyo Wakili Aisha,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Vitabu vya fasihi vina nafasi kubwa sana katika maendeleo ya jamii kwa sababu husaidia kufundisha, kuelimisha na kuburudisha watu. 

“Kwanza, vitabu vya fasihi hutoa elimu kwa jamii. Kupitia hadithi, riwaya, tamthilia na mashairi, watu hujifunza maadili mema kama vile uaminifu, heshima, uvumilivu na mshikamano. Fasihi pia huwafundisha watu kuhusu historia, mila na desturi za jamii mbalimbali, pili, fasihi huburudisha jamii. Wasomaji hupata furaha na kupunguza mawazo wanaposoma vitabu vya fasihi…,” ameeleza Jaji Mkuu.

Ameeleza Kuandika vitabu vya fasihi ni jambo muhimu sana katika jamii kwa sababu huelimisha, huburudisha, hukemea maovu, huhifadhi utamaduni na kukuza lugha. Hivyo, jamii inapaswa kuwahamasisha waandishi wa fasihi ili waendelee kuandika vitabu vitakavyosaidia kujenga taifa lenye maadili mema na maendeleo.

Kuhusu umuhimu wa kuwa na Shukrani ambapo amesema kuwa, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, ina faida lukuki kwa upande wa Kisaikolojia na Kimaisha, husaidia kupunguza msongo wa Mawazo, husaidia mtu kuona mema hata katika changamoto, na hivyo kupunguza wasiwasi na huzuni.

Mhe. Masaju amesema pia, shukrani huongeza furaha ya mtu binafsi, ambapo amesema, “Watu wanaoshukuru huishi maisha yenye matumaini na amani ya ndani.”

Ameongeza kuwa, manufaa mengine ya kuwa na Shukrani ni pamoja na kuimarisha afya ya akili ambapo Tafiti zinaonesha kuwa, shukrani hupunguza hisia za hasira na wivu na kuongeza kuridhika na maisha.

“Kwa upande wa Kijamii na Kiutamaduni, Shukrani huimarisha mshikamano wa kijamii: Jamii yenye shukrani hujenga uhusiano wa heshima na mshikamano, kwani watu wanapohisi kuthaminiwa, hujitolea zaidi kushirikiana, hujenga maadili ya uwajibikaji: Shukrani ni kiashiria cha kutambua mchango wa wengine, na hivyo kuimarisha utamaduni wa kuheshimiana na kusaidiana,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema, Shukrani hujenga maadili ya uwajibikaji: Shukrani ni kiashiria cha kutambua mchango wa wengine, na hivyo kuimarisha utamaduni wa kuheshimiana na kusaidiana, uendeleza utamaduni wa amani.

Katika upande wa Kidini na Kiroho, Jaji Mkuu amesema, ni tendo la imani: Katika dini nyingi, shukrani ni ibada na ishara ya kutambua ukuu wa Mungu. Mfano, “Shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu” (1 Wathesalonike 5:18).

“Shukrani huimarisha maadili ya kiroho, Shukrani hujenga moyo wa unyenyekevu na kutambua neema za Mungu katika maisha ya kila siku na kwa upande wa Kiuchumi na Kimaendeleo, huongeza tija kazini: Wafanyakazi wanaothaminiwa huonyesha bidii na uaminifu zaidi, huimarisha uongozi bora: Viongozi wanaoshukuru mchango wa wananchi hujenga imani na mshikamano wa kitaifa, huendeleza mshikamano wa kizazi kipya,” ameeleza.

Kwa upande mwingine, Mhe. Masaju amesema, kukosa shukrani kuna hatari kadhaa ikiwa ni pamoja na kujenga malalamiko na chuki, kupoteza mshikamano wa kijamii, kudhoofisha maadili ya kiroho na kitaifa:

“Kukosa shukrani ni ishara ya kutokubali uongozi wa Mungu na kupuuza mchango wa wengine. Shukrani si neno dogo bali ni nguzo ya maadili, mshikamano na maendeleo ya kijamii. Jamii inayojenga moyo wa shukrani huimarisha furaha ya watu wake, hujenga mshikamano wa kitaifa, na kuendeleza maadili ya uwajibikaji,” amesisitiza.

Akiwa katika mahojiano maalum wakati wa hafla hiyo, Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha amesema wazo la kuandika kitabu hicho lilianzia kwenye neno lisemalo ‘Muujiza upo katika asante’ (The Miracle is in the thank you).

Wakili Aisha amesema, njia kuu mojawapo ya shukrani ni kutambua na kuelewa uwepo wa sasa ambapo amesema, “kuchagua kushukuru kunakufanya usonge mbele, kushukuru kwenye udogo ndipo kuna ukubwa…..”

Ameongeza kuwa, ana ndoto ya kuona vijana wanakuwa katika maadili mema ya Kitanzania, pamoja na kuendelea kuandika kuhusu masuala mbalimbali ya kuelimisha jamii ya Kitanzania.

Wakizungumzia umuhimu wa shukrani nao Viongozi wa Dini ya Kiislamu na Kikristo, Sheikh Issa Issa pamoja na Padri Faustine Furaha, kwa pamoja wamesema neno Shukrani limesisitizwa pia hata katika vitabu vya dini hizo. Mfano katika Biblia 1 Watheselonike 5:18 inasema; Shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu. Na Katika Quran Tukufu- Surah Ibrahim 14:7 inasema, Mkinishukuru, hakika nitawazidishia.

“Tujenge utamaduni wa kumshukuru Mungu, Zaburi 136:1, nitamshukuru Bwana kwa ajili ya Haki yake na nitaliimbia.........Kwa muda mrefu sana dhana ya shukrani imepuuzwa, kuhesabu baraka huongeza nyingine,” amesema Padri Furaha.

Amesema, kushukuru ni kuangalia tulicho nacho na sio kile ambacho hatuna na kwamba shukrani ni tunda la uvumilivu na kwamba yatupasa kushukuru kabla ya kumuomba Mungu kwa kuwa moyo usiokuwa na shukrani hukausha mema yote.

Naye Sheikh Issa amesema, kushukuriwa na kupendwa ni miongoni mwa mahitaji ya binadamu.

Kwa upande wao Mchambuzi wa Kitabu, Bw. Joram Nkumbi pamoja na Mhariri wa Kitabu hicho, Dkt. Ishmail Mwambapa kwa pamoja wamempongeza Wakili Aisha na kusema kuwa, kitabu kilichoandikwa kwa mfumo wa mashairi kinaelimisha na kusisitiza juu ya umuhimu wa kuwa na shukrani katika hali yoyote katika maisha.

Bw. Nkumbi amesema, Kitabu kinaonyesha moyo wa Shukrani na kwamba muujiza mkubwa upo katika neno Asante, amesema “shukrani ni kama kuomba ten, ruhusu moyo wa shukrani uingie moyoni mwako, kitabu pia kinasisitiza mambo ya maadili.”

Katika kitabu hicho cha SING GRATITUDE kinamfundisha mtu kusema ahsante kwa mambo mema na makubwa, na pia kwa mambo madogo ambayo mara nyingi hupita bila kutambuliwa kirahisi.

Uzinduzi wa kitabu hicho ni ushahidi kuwa taifa letu lina hazina kubwa ya fikra na vipaji. Vijana kama Wakili Aisha wanapochukua kalamu na kuandika, wanajenga msingi wa leo na kesho yenye maarifa na matumaini.

Hafla hiyo imehudhuriwa pia na baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Majaji Wastaafu wa Mahakama Kuu, Mabalozi, Wazazi pamoja na ndugu jamaa na marafiki wa familia ya Aisha Saidi Kingu.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akizindua Kitabu kiitwacho SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Msomi Aisha Saidi Kingu. Hafla ya uzinduzi wa Kitabu hicho imefanyika leo tarehe 10 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mwandishi wa Kitabu hicho, Wakili Aisha Saidi Kingu.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiteta jambo na Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha Saidi Kingu mara baada ya kukizindua kitabu hicho.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji waliohudhuria katika hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu (wa tatu kushoto).

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba yake wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu kiitwacho SING GRATITUDE kilichoandaliwa na Wakili Aisha Saidi Kingu.

Picha za makundi mbalimbali ya wageni waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu.

Baba Mzazi wa Wakili Aisha Saidi Kingu, Dkt. Saidi Kingu Mtemi akizungumza wakati wa hafla hiyo. Kulia ni Mama Mzazi wa Wakili huyo.

Kiongozi wa Dini ya Kiislamu, Sheikh Issa Issa akizungumza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu. 

Padri Faustine Furaha akizungumza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kitabu cha SING GRATITUDE kilichoandikwa na Wakili Aisha Saidi Kingu. 

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha Saidi Kingu (kushoto) na kulia ni Mchambuzi wa Kitabu, Bw. Joram Nkumbi.

Mwandishi wa Kitabu cha SING GRATITUDE, Wakili Aisha Saidi Kingu (kushoto) akifanyiwa mahojiano kuhusu Kitabu hicho leo tarehe 10 Mei, 2026 wakati wa uzinduzi wa kitabu hicho.

(Picha na BAKARI MTAULLAH)













Jumamosi, 9 Mei 2026

BSAAT YAKABIDHI VIFAA VYA TEHAMA MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI KISUTU

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Kisutu

Mradi wa Mfumo Endelevu wa Kupambana na Rushwa Tanzania (BSAAT), hivi karibuni umekabidhi vifaa mbalimbali vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.

Hakimu Mkazi Mkuu na Afisa Mwambata wa BSAAT, Mhe. Richard Kabate, alikabidhi vifaa hivyo kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, huku zoezi hilo likishuhudiwa na   Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Bi. Athanasia Kabuyanja.

Watumishi wengine wa Mahakama waliokuwepo wakati wa makabidiano hayo ni Ofisa Utumishi Mwandamizi, Bw. Nkruma Katagira, Mhasibu Mwandamizi, Bi. Prisca Gideon na Ofisa TEHAMA wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Bw. Winfred Nzilano.

Vifaa vilivyokabidhiwa ni Kompyuta Mpakato tano (5) aina ya HP Omnibook X Flip, Begi za Kompyuta Mpakato (Laptop bag) tano (5), Adapta (Type C to HDTV 11 in 1 Adapter) na Vipanya vya Kompyuta (wireless mouse) tano (5) na Vipanga Njia (Portable router) tano (5).

Akizungumza waakati wa zoezi hilo, Mhe. Kabate aligusia umuhimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi katika mapambano dhidi ya rushwa na kwamba Mahakama ya Kisutu imekuwa ikipokea kesi nyingi ambazo zinahusiana na maswala ya rushwa.

Hivyo, alibainisha kuwa makabidhiano hayo ni katika kuhakikisha uondoaji wa mianya ya rushwa katika mifumo ya Mahakama na kuongeza wigo wa kushughulikia mashauri ya rushwa.

Naye Hakimu Mfawidhi aliushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuona kwamba inafaa kuwaletea vitendea kazi. Alisema watavitumia vifaa hivyo kuhakikisha mashauli yanamalizika kwa haraka iwezekanavyo kama kauli mbiu ya Mahakama inavyosema.


Hakimu Mkazi Mkuu na Afisa Mwambata wa Mradi wa Mfumo Endelevu wa Kupambana na Rushwa Tanzania, Mhe. Richard Kabate (kushoto), alikabidhi vifaa hivyo kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga (katikati). Picha chini, Mhe. Kiswaga akizungumza baada ya makabidhiano hayo.


Picha ya pamoja baada ya makabidhiano hayo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Njombe.

 

KAMATI YA JAJI MKUU UFUATILIAJI NA TATHMINI YAFANYA UKAGUZI MAALUM MAHAKAMA PWANI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza amefanya ukaguzi katika Mahakama za Hakimu Mkazi Pwani, Mahakama ya Wilaya Kibaha na Mahakama ya Mwanzo Mailimoja ili kufanya tathmini ya usahihi wa taarifa na namna ambavyo Mahakama hizo zinavyofanya kazi.

Akizungumza mara baada ya kuwasili ofisini kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi, tarehe 07 Mei, 2026, Mhe. Khyoza alisema wao sio Wakaguzi wa moja kwa moja bali wao wanaangalia taarifa za ukaguzi zinazowafikia na usahihi wake na kumtaarifu Jaji Mkuu kama mambo yako sawa, akieleza kuwa hilo ni jukumu mojawapo la kamati hiyo.

Akizungumza na watumishi baada ya ukaguzi, Mhe. Kahyoza alisema mara yake ya mwisho kufika kwenye jengo la Mahakama hiyo ni siku jengo lilipokabidhiwa tarehe 21 Septemba, 2016 ambapo amewapongeza wasimamizi wa jengo hilo, wakuwa wameweza kuzingatia usafi wa jengo. Aliongeza kwa kusema, “Kwahiyo nimefurahi kitu cha kwanza kufika kwenye jengo hili tena nikaridhishwa na usafi kweli niwapongeze sana mnaosimamia na mnaofanya usafi wa mazingira na kuyatunza pia.”

Aliendelea kuwapongeza zaidi na kusema kuwa, usafi ni jambo jema linalotia nguvu na kuna kipindi kulikuwa kuna azimio linalozungumzia utunzaji wa mazingira. Amekumbusha pia alikuwa Jaji Mfawidhi Mwanzilishi wa  Mahakama Kuu Musoma walipanda miti ya vivuli na matunda, jambo ambalo Jaji Mkuu wa kipindi hicho ambacho anakabidhi Mahakama Kuu Musoma alisema makabidhiano yaambatane na mazingira safi.

Akiwaeleza watumishi wa Mahakama hiyo, lengo la ujio wake alisema wao kazi yao kubwa wanaangalia namna Wakaguzi wanavyokagua ili kuona wanachowaambia kama ni sahihi pia wataangalia namna Mahakama za Mwanzo zinavyofanya kazi ili kile wanachoambiwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi kama ni sahihi.

Amesema pia, wameona rejesta ya malalamiko kwenye shughuli za kiutawala japo kwenye masuala ya pesa hawaingii huko sana japo wameona taarifa ya utekelezaji. Alibainisha kuwa, utekelezaji wa Mpango Mkakati hauwezi kufanikiwa bila kujua bajeti na Nguzo ya Kwanza ya mpango huo ambayo ni Usimamizi wa Rasilimali za Mahakama.

Ameongeza kwamba, wakati anasimamia mambo ya utawala alikuwa anatumia neno GAP ambapo ameeleza kuwa, ukilijua neno hilo unaweza kuujua Mpango Mkakati wa Mahakama kwa urahisi.

Akieleza maana ya neno (GAP), Mhe. Khyoza amesema “G inasimamia (Governance) Usimamizi wa rasilimaliwatu, rasilimali fedha na utawala, A inasimamia nguzo ya (Access to Justice and Expeditiousness) na P ni (Public Trust and Stakeholders’ Engagement).

Amesema kuwa, mtu hawezi kuzitekeleza nguzo hizo bila mambo ya utawala kukaa vizuri, kuwepo na pesa bila usimamizi mzuri zitaishia kufanya vitu visivyoeleweka. Pia majengo yasipotunzwa vizuri Jaji au Hakimu hawezi kuendesha mashauri lakini pia haki za watumishi zisipolipwa na kuandaliwa vyeo kupanda pia haiwezekani kufanya kazi vizuri.

Amebainisha kuwa, “Nguzo ya ‘Access to Justice’ ndio nguzo mama kila siku tunashinda nayo.”

Pamoja na ukaguzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya, Jaji Kahyoza amekagua pia Mahakama ya Mwanzo Mailimoja, ambapo amewashauri Mahakimu wakichapa mwenendo wa mashauri wahifadhi katika Kompyuta ya Masjala na sehemu nyingine. Hiyo itasaidia hata kama haiwezi kupatikana sehemu mojawapo basi itapatikana sehemu nyingine.

Amesema kuwa, kitendo cha mtu mmoja kukaa na mwenendo si kizuri, ikitokea amehama anaweza kuondoka na mwenendo na wakati mwingine inaweza ikawa ngumu kupatikana.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kahyoza amewapongeza Mahakimu wa Mahakama hiyo kwa kuwahi kufika kazini maana matarajio yake ilikuwa ni kufika saa tatu asubuhi hivyo alitoka mapema sana kuogopa foleni lakini hakukuta foleni na kuwahi kufika tofauti na muda lakini aliwakuta Mahakimu na watumishi wengine tayari wameshafika ofisini.

Akizungumza wakati wa kumkaribisha Mjumbe wa Kamati ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Jaji Mkuu, Ofisa kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Mhe. Elias Migella amesema majukumu ya Kamati hiyo ni kufanya ufuatiliaji na tathmini ya huduma katika masuala ya kimahakama na kiutawala. 

Kadhalika, Mhe. Migella alizungumza na watumishi  wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Kamati ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Jaji Mkuu ina wajumbe nane ambao watatembelea Mahakama nchi nzima kwa lengo la kufanya ukaguzi na kurejesha taarifa kwa Jaji Mkuu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza (kulia) akiwasili Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani tarehe 07 Mei, 2026 tayari kwa kuendelea na jukumu la ukaguzi katika Mahakama hiyo. Kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi akimuongoza Jaji Kahyoza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza akisaini kitabu cha wageni alipowasili kwenye Ofisi ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi-Pwani.

Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini ykutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Bw. Elias Migella akimkaribisha Mhe. John Kahyoza ili azungumze na watumishi (hawapo katika picha). 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati  ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathimini, Mhe. John Kahyoza akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani na Mahakama ya Wilaya Kibaha mara baada ya ukaguzi katika Mahakama hizo. Kulia ni Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini ykutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Bw. Elias Migella na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi. 

Baadhi wa watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati  ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathimini, Mhe. John Kahyoza (hayupo katika picha).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Shinyanga na Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini, Mhe. John Kahyoza (katikati)  akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi wa Mahakama ya Mwanzo Mailimoja. Aliyeasimama kushoto mstari wa mbele ni Mjumbe wa Kamati ya Jaji Mkuu ya Ufuatiliaji na Tathmini ykutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Maadili, Bw. Elias Migella na kulia ni  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi. 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

Ijumaa, 8 Mei 2026

JAJI MFAWIDHI KATAVI ASISITIZA MATUMIZI YA TEHAMA MAHAKAMA ZA MWANZO

Na. ALLY RAMADHANI – Mahakama, Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi, Mhe. Godfrey Ntemi Isaya amewasisitiza watumishi wa Mahakama za Mwanzo katika Masjala hiyo kutumia Mifumo ya TEHAMA katika shughuli zao za kiutendaji.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Mhe. Isaya alipokuwa kwenye ziara yake ya ukaguzi wa Mahakama ili kuangalia utendaji kazi wa kila siku wa utoaji huduma za haki kwa wananchi, ziara hiyo ya ukaguzi ilifanyika kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026 hadi 07 Mei 2026 katika Wilaya za Mpanda, Mlele na Tanganyika.

Katika ziara hiyo, Mhe. Isaya alifanikiwa kutembelea Vituo vyote vya Mahakama za Mwanzo zinazoendelea kujengwa ndani ya Mkoa wa Katavi kama vile Sibwesa, Ugalla na Mamba na kupata wasaa wa kuwasisitiza watumishi wa maeneo hayo kuendeleza na mapambano ya matumizi ya TEHAMA ili kurahisisha utoaji haki kwa wananchi wanaowahudumia.

Kupitia ziara hiyo Mhe. Isaya aliwakumbusha watumishi wa Mahakama za Mwanzo mkoani Katavi kuendelea kutumia Mifumo ya TEHAMA ikiwemo Primary Court App, ili kurahisha utendaji kazi wa Mahakama kwa ujumla.

Aidha, Mhe. Isaya aliongeza kuwa, kazi ya kutoa haki sio jambo dogo hivyo watumishi wasijiingize katika vitendo viovu vinavyoweza kuharibu taswira ya Mahakama na kupunguza imani kwa wananchi,

“Ndugu watumishi nawasisitiza kuwa waadilifu kwa kuwa ndiyo msingi mkubwa wa kutoa haki, hivyo muwe na tabia njema kazini na nje ya kazi na tuendelee kuchapa kazi tuwatumikie wananchi, tuepuke ile hali ya kuwa miungu watu kwenye ofisi zetu na kuongeza kuwa, kila mmoja kufanya kazi kwa bidii na umoja “If people cannot pay you, the nature will,” alisema Jaji Isaya.

Kwa upande mwingine, Mhe Isaya aliwapongeza watumishi wote kwa ujumla kwa kazi nzuri inayofanyika hususani usikilizwaji wa mashauri kwani katika taarifa zote zilizowasilishwa zimeonyesha kuwa mashauri yanafunguliwa na yanaisha kwa wakati.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (katikati) akiwa kwenye Picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali wa Masjala hiyo alipotembelea jengo la Mahakama ya Mwanzo Wilaya Mpanda Kituo  cha Ugalla.

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi, Mhe. Silivia S. Lushasi (aliyesimama) akiongea na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Wilaya Mpanda kituo cha Mpanda Mjini alipokua kwenye ziara ya Mhe Jaji Mfawidhi Kanda ya Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (wa kwanza Kulia mwenye suti nyeusi) akikagua baadhi ya mipaka ya eneo la Mahakama ya Mwanzo Wilaya Mpanda Kituo cha Shanwe.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)





MAHAKIMU NJOMBE PUNGUZENI KUKAA NA MASHAURI MAHAKAMANI KWA MUDA MREFU; JAJI NONGWA

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe, Victoria Nongwa amewataka Mahakimu wa Mahakama za Wilaya pamoja na za Mwanzo  kutokukaa na mashauri Mahakamani kwa muda Mrefu.

Mhe. Nongwa aliyasema hayo akiwa kwenye ziara ya kikazi aliyoianza tarehe 28 Aprili ,2026 hadi tarehe 4 Mei, 2026, ambapo alisema, “Hakikisheni mashauri yote yanayotokea Polisi yana ushahidi uliokamilika au mashahidi wamepatikana ili mashauri hayo yaweze kusikilizwa na kumalizika haraka ipasavyo na siyo kuchelewesha mashauri hayo bila sababu za msingi na yale mashauri ambayo hayana Mashahidi yasipokelewe mahakamani.”

Aidha, Jaji Nongwa aliwasisitiza Mahakimu kuwa, anatarajia kuona mashauri yanasikilizwa kwa haki, uadilifu na kwa wakati ili kutimiza dhana ya utoaji haki kwa wananchi mapema ipasavyo.

Katika ziara hiyo ya kikazi kwa Mahakama za Wilaya za Ludewa, Wanging’ombe na Makete waliwasilisha taarifa mbalimbali za Mashauri zilizosomwa na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya pamoja na taarifa za Utawala huku Mhe. Nongwa akisikiliza hoja mbalimbali zilizotolewa na watumishi wasio Mahakimu na kuzitafutia ufumbuzi ambazo nyingine zilijibiwa na Viongozi aliombatana nao.

 Akiendelea kuzungumza na watumishi,  aliwasisitiza juu ya umuhimu wa kila mmoja wao kujua  Nguzo Kuu za Mpango Mkakati wa Mahakama na kila mtumishi anatakiwa kujua wajibu wake pamoja na uwajibikaji huku akikemea vitendo viovu vinavyoashiria mazingira ya rushwa pamoja na kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mahakamani.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi huyo aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mtendaji wa Mahakama Kuu Njombe, Bw. Richard Mbambe na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama ambao waliweza kujibu hoja mbalimbali za watumishi pamoja na kutoa neno la shukrani katika ziara hiyo.  


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Wanging'ombe (waliosimama). Wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Bw. Richard Mbambe, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama na wa pili kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Wanging’ombe, Mhe. James Muhoni.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe(hawapo katika picha) alipofanya ziara katika Mahakama hiyo hivi karibuni.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe,Mhe. Victoria Nongwa (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe, Mhe. Joseph Luambano (wa pili kulia), wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe. Matilda Kayombo, wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama, wa pili kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe, Mhe. Godfrey Msemwa na wa tatu kushoto ni anayefata ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Bw,Richard Mbambe na waliosimama nyuma ni sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Lupembe.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini. Kutoka kushoto ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini, Mhe. Lisa Abel  anayefuata ni Mtumishi aitwaye Bi. Beatrice Liahumi,  nyuma ya kiti upande wa kulia ni Mwandishi Mwendesha Ofisi, Bi. Agusta Msingwa akiwa pamoja na Mwenzake  Mwandishi Mwendesha Ofisi Bi.Sofia Kimena ambapo viti vya nyuma  kulia ni Watumishi wa Mahakama, Bw. Justin Kiduli pamoja na Hashimu.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania ,kanda ya Njombe,Mhe, Victoria Nongwa (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Njombe wakiwa katika picha ya pamoja na  sehemu ya watumishi wa Mahakama ya wilaya Makete.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania ,kanda ya Njombe,Mhe, Victoria Nongwa (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Njombe wakiwa katika picha ya pamoja na  sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Manda alipofanya ziara katika Mahakama hiyo hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa akimwagilia Mche wa Mparachichi mara baada ya kuupanda katika viunga vya Mahakama ya Wilaya Wanging’ombe alipofanya ziara katia Mahakama hiyo hivi karibuni.  Kushoto ni Ofisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Wanging’ombe,  Bw.Riziki Sanga.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

Jumatano, 6 Mei 2026

BARAZA LA WAFANYAKAZI MAHAKAMA KUU MASJALA NDOGO SINGIDA LAKETI

Na EVA LESHANGE, Mahakama-Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo  ya Singida na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama hiyo, Mhe.Ayoub Mwenda ameongoza  kikao cha Baraza la Wafanyakazi ambapo amewasihi Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kutumia vizuri fursa ya kikao hicho kuchangia hoja na kutoa mapendekezo mbalimbali yatakayoboresha mazingira ya kazi.

Akifungua kikao hicho kilichofanyika tarehe 02 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Mahakama Kuu ya Singida, Mhe. Mwenda alisema kuwa, Mabaraza ya Wafanyakazi yapo kisheria na yana umuhimu mkubwa katika kulinda haki na maslahi ya watumishi mahala pa kazi sambamba na kuleta amani na utulivu mahali pa kwa kazi kwa kutatua migogoro kwa njia ya mazungumzo baina ya mwajiri na wafanyakazi.

“Matarajio yangu ni kuwa kila mjumbe katika kikao hiki atashiriki kikamilifu na kwa pamoja tutaibua hoja nzuri za kuwasilisha katika kikao cha Baraza Kuu la Mahakama ya Tanzania,” alisema Jaji Mfawidhi huyo.

Aidha, katika Baraza hilo wajumbe walipata fursa ya kufanya uchaguzi wa kuchagua Katibu, Katibu Msaidizi na Mjumbe mmoja atakayewakilisha watumishi katika Baraza kuu la Wafanyakazi Taifa.

Uchaguzi huo ulisimamiwa na Ofisa Kazi- Mkoa wa Singida, Bw. Boniface Ntalula ambaye aliwaelewesha wajumbe wa kikao hicho kwamba, Mabaraza ya Wafanyakazi kazi yapo kisheria na yalianza tangu mwaka 1970 na yana umuhimu mkubwa ikiwemo kushauri juu ya masuala mbalimbali ya kiutumishi, kutatua migogoro kazini na pia kuimarisha mshikamano baina ya mwajiri na waajiriwa.

Wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, alitoa utaratibu wa uchaguzi na wajumbe wanaopaswa kupiga kura kwa mujibu wa Mkataba. Baada ya zoezi la kupiga kura kukamilika Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Amiri Bakari aliibuka kuwa Katibu mpya wa Baraza hilo, Bi. Anna Kisambale, Katibu Msaidizi na Bi. Dorisi Busanji alichaguliwa kuwa Mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Baraza Kuu la Wafanyakazi Taifa.

Aidha, taarifa ya utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2025/2026 ilisomwa na kuona utekelezwaji wa masuala mbalimbali hususan yanayolenga watumishi moja kwa moja, kuona mafanikio na changamoto na namna zilivyotatuliwa kwa mwaka wa fedha  ujao wa 2026/2027.

Akihitimisha kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi, Mwenyekiti wa Kikao, Mhe.  Mwenda aliwasisitiza watumishi kutekeleza wajibu wao na kufanya kazi kwa bidii na kutumia mafanikio yao katika kujenga hoja za kuboreshewa maslahi.

Vilevile aliwasisitiza viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Mkoa na wale wenyekiti wa Matawi ya TUGHE Mahakama kuendelea kuwasisitiza watumishi kujiunga na Chama hicho kwani ni muhimu na vipo kisheria.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama hiyo, Mhe. Ayoub Mwenda (aliyesimama) akisalimia wajumbe waliohudhuria kikao hicho cha baraza (hawapo katika picha).  Kushoto ni Ofisa Kazi Mkoa wa Singida, Bw. Boniface Ntalula na  kulia ni Bw. Tamsoni Mshigati, Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Mkoa wa Singida.

Ofisa Kazi Mkoa wa Singida, Bw.Boniface Ntalula (aliyesimama) akjitambulisha na kufungua Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Singida waliohudhuria kikao hicho kilichofanyika tarehe 02 Mei, 2026 kwenye Ukumbi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

 Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda akikata keki kuashiria kuzinduliwa kwa Baraza la Wafanyakazi Singida ikiwa ni Baraza la Kwanza tangu Mahakama hiyo ilipotangazwa rasmi kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)