Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya
Watumishi
wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe.
Victoria Nongwa, wamefanya ziara ya kutembelea Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha
Nuru. Ziara hiyo imefanyika tarehe 30/01/2026 na kuhusisha watumishi kutoka
Mahakama Kuu Mbeya, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mahakama ya Wilaya pamoja
na sehemu ya watumishi wa Mahakama za Mwanzo mkoani Mbeya. Aidha, ziara hiyo
pia ilihudhuriwa na wadau wengine katika mnyororo wa utoaji haki, wakiwemo
Jeshi la Polisi na Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya.
Watumishi
hao walipokelewa na Meneja wa Kituo hicho, Bi. Mary Kassim Himiri, ambaye
alitoa maelezo ya utangulizi kwa kuelezea historia fupi ya Kituo tangu
kuanzishwa kwake mwaka 2005 hadi sasa, pamoja na hali ya Kituo kwa sasa.
Alieleza kuwa kwa sasa kituo kina watoto arobaini (40), ambapo wanne (04) kati
yao wamehitimu elimu ya Sekondari Kidato cha Nne mwaka 2025. Aliongeza kuwa
baadhi ya watoto wamechukuliwa na watu waliokuwa na nia ya kuwalea, kwa kufuata
taratibu zilizowekwa na Kituo hicho kwa kushirikiana na Ofisi ya Ustawi wa
Jamii Mbeya.
Aidha,
Bi. Mary Himiri alizungumzia suala la ufadhili, ambapo alisema kuwa kwa sasa
kituo hakina mfadhili wa kudumu na kinategemea misaada midogo midogo kutoka kwa
watu binafsi au Taasisi zinazojitolea kusaidia pale inapohitajika.
“Hapo
awali tulipata ufadhili kutoka Ubalozi wa Japan ambao walitujengea majengo
mawili. Hata hivyo, tangu mwaka 2016, baada ya mwanzilishi wa kituo kufariki,
hatuna tena ufadhili wa kudumu. Kwa sasa, tunategemea msaada wa watu binafsi
wanaoguswa na hali ya Kituo na kujitolea kusaidia,” alisema Bi. Mary Kassim
Himiri, Meneja wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru.
Kwa
upande wake, Mhe. Victoria Nongwa akizungumza machache baada ya kukabidhi
zawadi walizokwenda nazo kituoni hapo, ambapo alitoa shukrani na pongezi kwa
uongozi wa kituo kwa kazi kubwa wanayoifanya.
“Tunatambua
mchango mkubwa wa asasi hizi katika malezi ya watoto yatima na wenye mahitaji
maalum. Tunatoa pongezi za dhati kwa uongozi na walezi wote wa Kituo cha Kulea
Watoto Yatima cha Nuru kwa jitihada mnazozifanya. Kwa niaba ya wenzangu wote,
tunawashukuru kwa kila hatua mnayopiga, Mwenyezi Mungu awabariki sana,” alisema
Mheshimiwa Nongwa.
Ziara
hiyo pia ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, akiwemo
Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu; Hakimu Mkazi
Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama
ya Wilaya Mbeya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mbeya Mjini, Mhe.
Ayubu Shelimo, pamoja na viongozi wengine wa Mahakama Mkoa wa Mbeya.
Ziara
hiyo ilihitimishwa kwa kutembelea miundombinu ya Kituo hicho na kufanya
mazungumzo ya pamoja na watoto na walezi wao, ikiwa ni ishara na dhamira ya
Mahakama amabayo siyo tu katika utoaji wa haki, bali pia katika kushiriki
kikamilifu katika ustawi wa jamii.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe.
Victoria Nongwa, akizungumza machache wakati wa ziara hiyo.
Meneja
wa Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Nuru Orphans Centre, Bi. Mary Himiri
(aliyesimama katikati), akitoa neno la shukrani baada ya kupokea zawadi.
Sehemu
ya watumishi waliotembelea kituoni hapo.
Sehemu
ya watumishi walipotembelea kituo cha Nuru Orphans Centre; kutoka kulia ni
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer;
anayefuatia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy
Mlimba.
Naibu
Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya, Mhe. Aziza Temu, akikabidhi zawadi
walizokwenda nazo kituoni hapo.
Watumishi
wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na walezi wa kituo, wapili kushoto ni
Meneja wa kituo, na wa nne kushoto ni mlezi mkuu wa kituo hicho.
Watumishi
wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na walezi wa Kituo cha Kulea Watoto
Yatima cha Nuru Orphans Centre.
%20-%20Copy.jpg)
%20-%20Copy.jpg)
%20-%20Copy.jpg)
%20-%20Copy.jpg)
%20-%20Copy.jpg)
%20-%20Copy.jpg)
%20-%20Copy.jpg)








