Jumatano, 4 Februari 2026

TEHAMA YAONDOA MLUNDIKANO WA MASHAURI MAHAKAMANI GEITA

Na DOTTO MKAJA-Mahakama, Geita

Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yameiwezesha Mahakama Kuu Kanda ya Geita kuondoa mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama kwa mwaka 2025.

Hayo yamebainishwa jana Februari 2, 2026 na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, wakati akitoa hotuba yake katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini yaliyofanyika katika Uwanja wa Kituo Jumuishi Geita (Jengo Jipya).

Mhe. Mhina alisema Mahakama ni chombo muhimu katika kuchochea ukuaji wa uchumi na kulinda amani ya wananchi, akibainisha kuwa bila uwepo wa Mahakama, vyombo vya ulinzi na usalama, Magereza na Serikali, hata siku moja haviwezi kupita bila kutokea uvunjifu mkubwa wa amani.

Akizungumza kuhusu utendaji wa Mahakama Kanda ya Geita, alisema kuwa kwa mwaka 2025 Mahakama zote zilifanikiwa kumaliza mashauri kwa wakati, huku wastani wa umalizaji wa mashauri katika Mahakama za Wilaya tano ukiwa siku 35.

Aliongeza kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita ilikuwa na wastani wa siku 60, Mahakama Kuu siku 46 na Mahakama za Mwanzo siku 15. Alisema kuwa wastani wa muda wa usikilizaji mashauri kwa mwaka 2025 umepanda kulinganisha na mwaka 2024.

Akifafanua mafanikio hayo, alisema yameleta ongezeko la ufanisi katika usikilizwaji wa mashauri, kupungua kwa muda wa mashauri kusikilizwa na kuamuliwa, pamoja na kuondolewa kabisa kwa mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama Kanda ya Geita.

Aidha, alisema Mahakama ilisikiliza na kumaliza mashauri yote ya kimkakati yaliyokuwa yameshikilia uchumi, hali iliyosababisha fedha zilizokuwa zimezuiwa kurejeshwa katika mzunguko wa uchumi na kuhamasisha uwekezaji.

Mhe. Mhina alisema mafanikio hayo yametokana na matumizi ya TEHAMA, akieleza kuwa teknolojia hiyo imeongeza uwazi kwa wadau wa haki na kuimarisha ushirikiano kati ya Taasisi mbalimbali kupitia mifumo inayosomana, ikiwemo NIDA, RITA, Magereza na taasisi nyingine.

Aliwasihi wadau wa sheria kuendelea kufanya kazi kwa kuzingatia uadilifu, weledi na ushirikiano.

Kwa upande wake, Mgeni Mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, aliipongeza Mahakama Kuu Kanda ya Geita kwa kumaliza mashauri kwa wakati na kwa haki, akisema hali hiyo imepunguza kwa kiasi kikubwa malalamiko kutoka kwa wananchi.

“Sipokei malalamiko kutoka mahakamani, jambo linaloonesha kuwa haki inatendeka kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji,” alisema Mhe. Shigela.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina, akitoa hutuba Siku ya Sheria katika uwanja wa Mahakama Kuu Geita (Jengo Jipya).

Mchungaji kutokKanisa la KKKT akitoa maombi ya kufungua Maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Uwanja wa Kituo Jumuishi Geita (IJC - Geita).

Meza kuu katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria iliyofanyika katika kituo Jumuishi Geita (IJC – Geita).

Mahakimu wakikiwa katika picha ya pamoja Siku ya Sheria nchini katika uwanja wa Kituo Jumuishi Geita(IJC - Geita).

Maofisa kutoka ofisi ya Mwendasha Mashitaka wakiwa katika picha ya pamoja.

Mawakili wa Kujitegemea wakiwa katika picha ya pamoja na meza kuu kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Kevin Mhina, akikagua gwalide Siku ya Sheria katika uwanja wa kituo Jumuishi Geita.

 

Watumishi wanawake Mahakama Kuu Geita na Mahakama ya Wilaya Geita katika picha ya pamoja wakiadhisha Siku ya Sheria 2026 katika Kituo Jumuishi Geita.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma


 

HAKI MSINGI MKUU WA USTAWI WA MAENDELEO YA TAIFA; JAJI MFAWIDHI MTWARA

Na OBADIA KAWONGA-Mahakama, Mtwara

Utawala bora na unaozingatia sheria ni msingi wa haki wa kufikia ustawi wa maendeleo ya Taifa, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, amesema.

Akizungumza kwenye Maadhimsho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika kikanda tarehe 2 Februari, 2026 katika Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Kakolaki alisema kuwa Mahakama kwa kushirikiana na Serikali imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha utoaji haki kwa wakati kwa Taasisi, mashirika na jamii kwa ujumla.

'Utawala bora na wa sheria unazingatia misingi ya haki na ndio msingi mkuu wa kufikia ustawi wa maendeleo ya Taifa.' aliongezea Mhe. Edwin Kakolaki.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrick Sawala, alihimiza utoaji haki kwa wananchi mapema ipasavyo ili kudumisha amani na utulivu katika Mkoa na Taifa kwa ujumla.

'Nchi yenye amani na utulivu inakaribisha wawekezaji kwa kuwa hawana mashaka ya kupoteza mali zao. Wito wangu tuendelee kuitunza amani yetu,' alisema.

Aidha, Mhe. Sawala alitoa rai kwa wadau wote wa haki jinai na madai kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uadilifu ili kuisaidia Mahakama kustawisha maendeleo ya Taifa kupitia utoaji haki bila ucheleweshaji.

Naye Wakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mkoa wa Mtwara, Bi. Nunu Mangu, alibainisha kuwa Mahakama inalinda amani katika jamii na kuzuia wananchi kuangukia kwenye kutafuta haki kwa njia zisizo rasmi.

'Nchi imeshuhudia mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa utoaji haki ikiwemo ongezeko la Majaji na Mahakimu, matumizi ya mifumo ya kisasa pamoja na uboreshaji wa mazingira ya kazi,' Bi. Mangu alisema.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, wadau wa sekta ya Sheria: Wakili wa Serikali wa Kujitegemea, Mahakimu kutoka Wilaya ya Mkoa wa Mtwara, Viongozi wa Dini, Wanafunzi wa Vyuo mbalimbali pamoja na Wananchi kwa ujumla.

Kabla ya kuhitimisha Maadhimisho hayo kulikuwepo na gwaride maalum lilioandaliwa na Jeshi la Polisi wa Mkoa wa Mtwara ambalo lilikagua na Jaji Mfawidhi kuashiria mwanzo wa shughuli za kimahakama kwa mwaka 2026.

Sambamba na maadhimisho hayo, kulikuwepo na burudani mbalimbali zilizotolewa na wachezaji wa ngoma za asili pamoja na Kwaya ya Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, ambao waliweza kufurahisha na kuburudisha nyoyo za waliohudhuria kwa uchezaji mzuri na ujumbe ulioakisi Kauli mbiu ya Maadhimisho hayo.

Baada ya Maadhimisho hayo, kulifanyika bonanza katika Viwanja vya Nangwanda lililoongozwa na Jaji Mfawidhi ambaye alishiriki kikamilifu katika mazoezi na michezo mbalimbali pamoja na watumishi wa Mahakama.

Akizungumza wakati wa bonanza hilo, Mhe. Kakolaki alisisitiza umuhimu wa michezo na mazoezi kwa watumishi wa Mahakama, akisisitiza kuwa shughuli hizo zinaleta afya imara na kuwawezesha watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

'Mtumishi mwenye afya njema ni rasilimali muhimu kwa Taifa. Tunapofanya mazoezi tunajenga miili yetu na akili zetu, na hivyo tunakuwa na uwezo mkubwa wa kutoa huduma bora kwa wananchi,' alisema Mhe. Kakolaki.

Bonanza hiyo iliyojaa shangwe na furaha ilihusisha michezo mbalimbali ikiwemo mbio, kuvuta kamba, mpira wa miguu pamoja na wa kikapu. Watumishi Pamoja na wadau mbalimbali walishiriki kwa hamasa kubwa huku wakiimarisha udugu na ushirikiano miongoni mwao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, akikagua gwaride.

Wadau pamoja na wananchi katika maandamano kuelekea viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, akitoa utambulisho wa Viongozi pamoja na kukaribisha wageni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akihutubia katika maadhimisho ya Siku ya Sheria mkoani Mtwara.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara,Kanali Patrick Sawala, akitoa salamu katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara.

Wachezaji wa ngoma za asili wakitoa burudani kwa wageni waalikwa wa hafla hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Saidi Ding’ohi (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Martha Mpaze (kulia), Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Partick Sawala (w apili kushoto) pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mhe, Abdallah Mwaipaya (kushoto) katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (wa tatu kushoto) katika uzinduzi wa bonanza lililoandaliwa baada ya hafla ya maadhimisho ya Siku ya Sheria.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama Dodoma

 

 

MAHAKAMA IWE KIMBILIO LA WANYONGE NA NGAO YA HAKI; JAJI MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama -Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha na Mgeni Rasmi wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa Kanda hiyo, Mhe. Frank Mahimbali amesema kuwa lazima Mahakama iwe thabiti na imara kiasi cha kuaminiwa na wananchi na hatimaye kuwa kimbilio la wanyonge.

Jaji Mahimbali aliyasema hayo tarehe 02 Februari, 2026 wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

“Tuendelee kuimarisha Mahakama zetu ili ziwe chombo cha kuaminika, kuheshimika, chenye uadilifu na mchango wa moja kwa moja katika ustawi wa Taifa letu” aliongeza Jaji Mahimbali.

Jaji Mfawidhi aliwakumbusha Viongozi wa Serikali wanaohusika na utekelezaji wa amri za Mahakama kuhakikisha wanatekeleza amri hizo bila kuweka vikwazo ili kuwapatia haki wananchi husika mapema ipasavyo na hatimae kuharakisha maendeleo ya watu na taifa kwa ujumla.

Mhe. Mahimbali aliahidi kuwa, hatakuwa na uvumilivu kwa Kiongozi yeyote ndani ya Kanda ya Arusha atakayedharau amri za Mahakama na kushindwa kuzifanyia utekezaji wakati ni wajibu wake kufanya hivyo.

Maadhimisho hayo yaliyokuwa na Kaulimbiu isemayo, ‘Mchango wa Mahakama katika Ustawi wa Maendeleo ya Taifa,’ Jaji Mahimbali aliongeza kuwa, mchango wa Mahakama katika maendeleo ya Taifa ni wa msingi na wa kudumu kwani Mahakama ni nguzo ya haki, demokrasia na utawala bora pia ni chombo kinacholinda amani, kukuza uchumi na kulinda haki za kiraia hivyo, alisisitiza kwamba, ni muhimu kwa Mahakama nchini kuwa taa ya mwanga katika giza la dhuluma.

Akizungumzia kuhusu Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Jaji Mahimbali alisema kuwa,Mahakama ni nguzo muhimu kwa kuhakikisha kuwa upo utawala wa sheria, haki na uwajibikaji ambavyo ni msingi wa uchumi imara, amani ya kijamii na maendeleo jumuishi na kwamba bila Mahakama huru, inayoheshimika na yenye ufanisi, malengo ya Dira ya Maendeleo hayawezi kufikiwa.

Katika hotuba ya Mwanasheria wa Serikali mkoani Arusha, Bi. Veritas Mlay alisema kuwa Siku ya Sheria nchini ni siku muhimu na ya kipekee ya kufanya tafakuri ya kitaifa ambapo wanakumbushwa dhima na wajibu wao wa pamoja katika kulinda haki, amani, usawa na utawala wa sheria kama nguzo na nyenzo katika kufikia ustawi na maendeleo ya Taifa.

Mwanasheria huyo wa Serikali aliongeza kuwa, Tanzania imejikita katika kufanya maendeleo yanayodhihirishwa na uwepo wa miradi mikubwa ambayo imekamilika na ile ambayo ipo katika hatua mbalimbali za ukamilishaji katika Sekta mbalimbali ikiwemo uchumi, ujenzi, nishati, madini na huduma za jamii.

Bi. Mlay alisisitiza kuwa, uwepo wa miradi hiyo ya maendeleo ni ushahidi tosha wa ushirikiano baina ya Serikali, Mahakama na Bunge, na kwamba Serikali imeweka mazingira rafiki na ya kuvutia uwekezaji na hivyo kukuza uchumi na maendeleo ya nchi kupitia uingizaji wa mitaji na teknolojia na upatikanaji wa ajira. 

Kadhalika Mwanasheria huyo alisema kuwa, Mahakama kama mlinzi wa Katiba, haki na utawala wa sheria, ni nguzo muhimu katika kukuza na kuendeleza ustawi na maendeleo ya Taifa.

“Mahakama iliyo huru na inayoheshimika na kuaminika huhakikisha utekelezaji thabiti wa mikataba, ulindaji wa haki za mali na kudhibiti matendo ya matumizi mabaya ya madaraka na hatimaye kukuza imani ya wawekezaji na hivyo kuwezesha ukuaji imara na endelevu wa uchumi wa Taifa,” alisema Bi. Mlay.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Hamisi Mkindi alisema kuwa, Kaulimbiu ya Siku ya Sheria mwaka huu inaakisi ukweli kwamba hakuna maendeleo ya kweli bila ulinzi wa haki, utawala wa sheria na utawala bora hivyo Mahakama ndicho chombo pekee ambacho huamua mwelekeo wa haki, uaminifu na utulivu wa kitaifa.

“Taifa linapokuwa na mfumo wa utoaji haki unaoaminika, unaofanya kazi kwa ufanisi na unaoweka mbele maslahi ya wananchi bila upendeleo, dhuluma wala hiyana na kuleta hali ya watu kuwa na matumaini, basi ustawi wa kiuchumi, kijamii na kisiasa huimarika na maendeleo ya kweli huonekana,” alisisitiza Wakili Mkindi.

Aliongeza kuwa, ni wajibu wa Mahakama kulinda na kusimamia haki za binadamu na kwamba jukumu hilo si la Mahakama pekee bali ni pamoja na Wadau wote wa Mahakama ambao ni Wadau wa haki. Alisema kwamba, haki inapaswa kutolewa bila ubaguzi kama ilivyoainishwa na Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania toleo la 1977.

Naye mgeni maalum wa Maadhimisho hayo mkoani Arusha ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Makalla alisisitiza kuwa ipo haja kwa Wadau wa Sheria kutoa elimu kwa wananchi juu ya majukumu ya Mihimili ya Serikali ili wajue ni aina gani ya lalamiko au huduma inatakiwa kuwasilishwa kwenye Mhimili gani ili suala hilo liweze kupatiwa ufumbuzi.

Vilevile, Mhe. Makalla aliwaasa Mawakili wa Kujitegemea kutojihusisha na vitendo vya udanganyifu ambavyo vinaleta migogoro na usumbufu kwa wananchi.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa wa Arusha ameahidi kutoa ushirikiano kwa wadau wote wa haki, hususani katika kuhakikisha amri za Mahakama zinaheshimika na kutekelezwa kama taratibu zinavyoelekeza.

Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yahudhuriwa na Viongozi wa Taasisi mbalimbali mkoani Arusha zikiwemo vyombo vya Ulinzi na Usalama, Vyuo, Shule, TAKUKURU, Vyama vya Kiraia, Viongozi wa Dini na Sekta Binafsi.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akizungumza na Watumishi, Wadau na Wananchi waliohudhuria katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha akikagua gwaride maalum kuashiria uzinduzi wa mwaka mpya wa Mahakama wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ambayo kwa upande wa Arusha yalifanyika katika viwanja vya  Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha na Mgeni Maalum wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini mkoani humo, Mhe. CPA Amos Makalla akiwasalimia Wadau wa Sheria na wananchi waliohudhuria kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) mkoani Arusha, Wakili Msomi Hamisi Mkindi akisoma hotuba ya Chama hicho wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini zilizofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Mwanasheria wa Serikali Mkoa wa Arusha, Bi. Veritas Mlay akisoma hotuba ya Ofisi ya MwanAsheria Mkuu wa Serikali wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.




Wadau na wananchi waliohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.

Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi na Mhe. Elia Mrema wakishiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 02 Februari, 2026.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama  Kuu ya  Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Arusha (walioketi) pamoja na Majaji wastaafu (waliosimama) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha. Wa tatu kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Makalla.






Picha za pamoja za makundi mbalimbali ya washiriki waliohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa upande wa Arusha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

JAJI KIONGOZI AKUTANA NA VIONGOZI WA TMJA TAWI LA MASJALA KUU

Na. Mwandishi Wetu-Mahakama.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu, amekutana na kufanya mazungumzo na Viongozi wa Tawi hilo leo tarehe 4 Februari, 2026 Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma na kuweka mikakati mbalimbali itakayokiwezesha Chama kuweka misingi imara itakayoacha alama chanya isiyosahaulika kwa ajili ya wanachama wa sasa na wajao.

Kufuatia misingi hiyo iliyowekwa, Mhe. Dkt. Siyani kama mlezi ameahidi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa uongozi huo ili kuwezesha utekelezaji wa mikakati hiyo itakayowezesha usimamizi bora wa Chama na msaada kwa wanachama na jamii kwa ujumla.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA)Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu, akizungumza wakati alipotembelewa ofisini kwake na viongozi wa TAMJA Tawi la Mahakama Kuu Masjala Kuu, leo tarehe 4 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodooma 

Viongozi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA)Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu, wakiwasilisha mikakati ya Chama hicho kwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama hicho. 
Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA)Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu, Mhe. Desidery Kamugisha ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, akiwasilisha mikakati ya Chama hicho kwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo pichani) ambaye pia ni Mlezi wa Chama hicho. 

Sehemu ya viongozi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu.

Katibu wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu, Mhe. Kifungu Mrisho Kariho ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, akichangia mada wakati wa kikao hicho  mbele ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo pichani) ambaye pia ni Mlezi wa Chama hicho. 
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (aliyesimama katikati) ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Mahakama Kuu Tawi la Masjala Kuu akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa chama hicho.

PICHA NA INNOCENT KANSHA - MAHAKAMA

Jumanne, 3 Februari 2026

JAJI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA RAIS WA MAHAKAMA YA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 03 Februari, 2026 ametembelewa na kufanya mazungumzo na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera.

Akizungumzia kuhusu lengo la kumtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Kayobera amesema lengo mojawapo ni kumsalimia na kumpongeza kwa kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania tangu Juni, 2025.

Aidha, Rais huyo wa EACJ amesema kuwa, anafurahishwa na ushirikiano ambao Mahakama hiyo inapata kutoka Serikali ya Tanzania na Mahakama kwa ujumla na kukiri kuwa, mazingira yaliyopo ya amani yanawawezesha kutekeleza majukumu yao kwa amani na utulivu.

Kadhalika, Mhe. Kayobera amemueleza Jaji Mkuu kwamba, katika kuhakikisha kuwa, Mahakama hiyo inaendelea kufanya kazi ipasavyo na kwa diplomasia, tangu alipoingia katika Mahakama hiyo mwaka 2021 aliweka Falsafa tatu muhimu ikiwa ni pamoja na Kufanya kazi kwa pamoja (Teamwork) ambapo amesema kuwa, Mahakama ni Taasisi ya pamoja na si ya mtu mmoja, hivyo ushirikiano wa Majaji na wadau wengine ni muhimu na huchochea ufanisi, uwajibikaji na utoaji haki kwa wakati.

Ametaja Falsafa nyingine kuwa ni Kutekeleza majukumu kwa nia njema (Good Faith) na kwamba tafsiri na utekelezaji wa Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ufanyike kwa uaminifu ili kuepuka mbinu za kukwepa haki kwa ujanja wa kisheria.

Rais huyo wa Mahakama ya Jumuiya Afrika Mashariki ameongeza kuwa, Falsafa nyingine anayotumia ni kuzingatia Diplomasia ya Kimahakama (Judicial Diplomacy) lengo likiwa ni kudumisha mahusiano mazuri na Taasisi za Jumuiya na Nchi Wanachama, Kutoa maamuzi yenye nguvu kisheria lakini kwa lugha na mtazamo unaojenga ujumuishaji, si kuvunja wala kuyumbisha uhuru wa Mahakama, bali kusawazisha haki na uhai wa Jumuiya.

Vilevile, Mhe. Kayobera amemshukuru Jaji Mkuu kufuatia Mahakama hiyo kupatiwa Ofisi kwa ajili ya Masjala ndogo ya Mahakama hiyo iliyopo ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Kwa upande wake Jaji Mkuu amemuhakikishia Rais huyo wa EACJ kuwa, Mahakama ya Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano wa dhati katika utendaji kazi wake na kujenga mahusiano mazuri ya Mahakama hiyo na Mahakama ya Tanzania.

Mhe. Masaju ameonesha na kukiri kufurahishwa na ujio wa Mhe. Kayobera aliyeambatana na Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara, Msaidizi wa Rais wa  Jumuiya ya Afrika Mashariki, Wakili Nina Sokoine na Afisa Masjala Mkuu wa Mahakama hiyo-Masjala Ndogo ya EACJ Dodoma, Wakili Mennas Mafwere na kuwaeleza kuwa wasisite kufanya mawasiliano wakati wowote wanapopata changamoto.

Kadhalika Jaji Mkuu ameikaribisha Mahakama hiyo kuja Mahakama ya Tanzania kufanyia vikao vyake kama ambavyo imefanya na kuendelea kufanya katika baadhi ya Nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na  Rais wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera alipomtembelea Jaji Mkuu tarehe 03 Februari, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera (kulia) akisaini kitabu cha wageni leo tarehe 03 Februari, 2026 alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju na katikati ni Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara.


Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara akisaini kitabu cha wageni leo tarehe 03 Februari, 2026 alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mazungumzo yakiendelea. Wa kwanza kushoto ni 
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju , wa kwanza kulia ni Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera, wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Yohane Masara na wa pili kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wakifuatilia mazungumzo kati ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.George Masaju na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera yaliyofanyika ofisini kwa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. Kutoka kushoto ni Msaidizi wa Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Wakili Nina Sokoine, anayefuata ni Afisa Masjala Mkuu wa Mahakama hiyo-Masjala Ndogo ya EACJ Dodoma, Wakili Mennas Mafwere, Naibu Msajili wa Mahakama na Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi na Katibu Msaidizi wa Jaji Mkuu, Mhe. Clarence Mhoja.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.George Masaju na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera (hayupo katika picha).

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.George Masaju (kulia) akimpatia Jarida na Kalenda za Mahakama Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera alipomtembelea Jaji Mkuu tarehe 03 Februari, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. 

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera (kushoto) pamoja  na Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara alipomtembelea Jaji Mkuu tarehe 03 Februari, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. 


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera (wa tatu kushoto), Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara (wa pili kulia), Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, Naibu Msajili na Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi (wa kwanza kushoto), Msaidizi wa Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Wakili Nina Sokoine pamoja na  Afisa Masjala Mkuu wa Mahakama hiyo-Masjala Ndogo ya EACJ Dodoma, Wakili Mennas Mafwere.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)