· Awataka pia wazingatie matakwa ya Kifungu cha 134 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai na Kanuni za Jaji Mkuu
· Asisitiza Polisi kutoa dhamana kwa watuhumiwa kwa mujibu wa sheria
· Amtaka kila mdau kusimama ipasavyo katika eneo lake kuboresha Haki Jinai
Na
MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji
Mkuu Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka
Wadau wa Haki Jinai nchini kuendelea kuimarisha umakini katika upelelezi wa
mashauri ya Jinai ya aina zote na uendeshaji wa mashauri ya jinai Mahakamani
kwa kuzingatia Katiba na Sheria ipasavyo.
Mhe.
Masaju aliyasema hayo jana tarehe 11 Juni, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau kuhusu ushirikiano na
mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani uliofanyika
kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama ya
Tanzania jijini Dodoma.
Jaji
Mkuu amesema kuwa, “miongoni mwa Taasisi ambazo zinaongoza kufanya/kushiriki
Mafunzo ya ndani na nje ya Nchi ni Taasisi zinazohusika na upelelezi, hivyo
tunataka kuona matunda yake na matokeo yake kazini.”
Jaji
Mkuu amesema, zoezi la upelelezi liendane na Kifungu cha 134 cha Sheria ya
Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kinachotaka mashauri yafunguliwe Mahakamani mara
baada ya upelelezi kukamilika isipokuwa kwa makosa ambayo ni makubwa na yale
ambayo yanasikilizwa na Mahakama Kuu kama ilivyotajwa katika kifungu cha
134(4).
Aidha,
amempongeza Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kwa kuweka Mwongozo ambao ni Sheria ambayo
hata katika mashauri makubwa, upelelezi uwe umekamilika ndani ya siku 90 ili
shauri lianze kusikilizwa.
“Yazingatieni
hayo, lakini pia endeleeni kuzingatia na kanuni zilizotolewa na Jaji Mkuu
kuhusu watuhumiwa kupata maelezo ya ushahidi dhidi yao, kabla ya kusomewa
mashtaka kwa mara ya kwanza (Preliminary hearing) na kesi kuanza kusikilizwa
ili kesi zinaposikilizwa wawe wanafamu ushahidi dhidi yao kama ilivyo kawaida katika
Mahakama Kuu, hapo ndipo kutakuwa na usikilizwaji kikamilifu ile (fair trial)
inayozungumzwa katika Katiba Ibara ya 13(6),” amesema Mhe. Masaju.
Sambamba
na hilo, Jaji Mkuu amesema kuwa, kuna changamoto ya dhamana kwa upande wa
Polisi ambapo amesema, “niwaombe Polisi, mmepewa mamlaka chini ya kifungu namba
65 mpaka 70 vya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai na bahati mbaya sisi
tunawafamu ninyi Polisi peke yenu, lakini kuna Taasisi nyingine ambazo
zinakamata watu zinaleta kwenye vituo vyenu. Vituo vyenu unakuta vimejaa, sasa
sijui kama mna fedha za kutosha au ni vikubwa kiasi gani, hii yenyewe ni sababu
ya msingi kwa makosa yale ambayo yanadhaminika kuwapa dhamana,” ameeleza Jaji
Mkuu.
Mhe.
Masaju amewashauri Polisi kutoa dhamana kwakuwa kifungu namba 65 mpaka 70 vya
Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai kimeeleza vizuri. “Wapeni dhamana itatupunguzia
pia na hizi tuhuma nyingine zisizokuwa na sababu mtu anaweza akajidhamini au
anaweza akadhaminiwa na mtu, mpeni dhamana, msipoweka utaratibu wa kuwa dhamana
watajaa mahabusu na kusababisha magonjwa ya mlipuko hata wengine wanaweza
wakafia Mahabusu ikawa shida, kwahiyo hakuna sababu ya kuogopa kuwapa dhamana
kama umewakamata kwa usahihi kabisa wapeni dhamana,” amesisitiza Mhe. Masaju.
Ameongeza
kuwa, Sheria inaelekeza kuhusu mtuhumiwa kutakiwa kufikishwa Mahakamani ndani
ya saa 24 tangu alipokamatwa, hii itasaidia na kwa upande wa makosa ya uhujumu
Uchumi wanatakiwa kufikishwa Mahakama ya Wilaya iliyo jirani na alipokamatwa ndani
ya saa 48.
Kadhalika,
amewataka kuzingatia masharti ya Kifungu cha 34 cha Sheria ya Mwenendo wa
Mashauri ya Jinai kinachowataka Mkuu wa Kituo cha Polisi kutoa taarifa ya kila
Mtuhumiwa aliyekamatwa bila kibali cha Mahakama (Warrant of Arrest) na ambao
wako ndani ya Vituo vya Polisi na wale waliopata dhamana. “Hili ni takwa la
kisheria, zingatieni haya masharti, faida zake ni nyingi na tumezitafakari hapa
wote, hapa hakutakuwa na cha Mswalia Mtume, zingatieni hayo masharti ili twende
kwa sababu hata tusiposema hayo mengine ni vizuri tukayazingatia yote haya,”
amesisitiza.
“Kwa
upande wa Mahakama, wajibu wetu tuutekeleze ipasavyo bila kutumia madaraka yetu
vibaya,” amesema Jaji Mkuu huku akiwaahidi Wadau hao kuwa, Mahakama itaendelea
kuwa makini kwa kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa Ibara ya 107A(1)(2) ya
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) kwa sababu ndio Wasimamizi wa
Sheria hizo kwa sababu kuna changamoto katika eneo la upelelezi.
“Lakini
wajibu wetu wa kuandaa vitabu vya Rufaa kwa Wafungwa wanaotoka Mahakama Kuu
kuja Mahakama ya Rufani, tuviandae na kuvikamilisha hivi vitabu na kuwapatia
wahusika ili waweze kukamilisha sababu zao za Rufaa, hivyo hivyo Mahakama
tuwapatie wengine wanaotaka kukata rufaa labda kutoka Mahakama ya Wilaya au
Hakimu Mkazi kuja Mahakama Kuu, wanaotaka nakala za hukumu, wanaotaka mwenendo
wa mashauri tuwapatie mapema ipasavyo ili waweze kuandaa rufaa zao,” amesema
Mhe. Masaju huku akisisitiza yote ambayo yamesemwa kuhusu Mahakama yatekelezwe
na kila mdau wa mkutano huo atekeleze majukumu yake ipasavyo ili kushughulikia
changamoto.
Jaji
Mkuu amewataka Wadau hao wa Haki Jinai wakiwemo Magereza, Polisi, TLS na Wadau
wengine kama kuna changamoto zozote zinazokwamisha upatikanaji haki wasisite kutoa
taarifa Mahakama badala ya kusubiri siku ya vikao tu.
“Mahakama
ina nafasi kubwa sana katika ustawi na maendeleo ya Taifa letu, bila na kuwa na
amani na utengamano katika Taifa, maendeleo gani yatatoka katika Taifa hilo,
watu hawatafanya siasi, watu hawatafanya shughuli zao za kiuchumi, hawatafanya
shughuli zao za kijamii ikiwa ni pamoja na shughuli za siasa na kufunga ndoa na
kushiriki katika matamasha, kwahiyo tuna dhamana kubwa katika hili ili Taifa
hili lidumu kuwa la udugu kama ilivyokuwa zamani tunaitana ndugu. Amani na
udugu ndivyo vinavyohimizwa katika Katiba kupitia Ibara ya 9, hivyo simamieni
utekelezaji wa sheria kwa ufanisi ipasavyo,” amesema.
Aidha,
Jaji Mkuu amesema kuwa, katika hotuba yake ya Siku ya Sheria nchini mwaka huu
alieleza mambo ambayo Mahakama inafanya katika kuchangia ustawi na maendeleo ya
Taifa. Amesema, “Kaulimbiu yetu ya Mahakama kwa mwaka huu 2026 ni; Mchango wa
Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.”
Ameeleza
kuwa, Mahakama na wadau wake ni watu muhimu katika kuchangia utekelezaji wa
Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 ambayo msingi wake mkuu ni Utawala, Amani,
Usalama na Utulivu na vipaumbele vinne ambao ni Utawala Bora na Haki, Serikali
za Mitaa Imara na zenye ufanisi, Utumishi wa Umma unaowajibika na Amani,
Usalama na Utulivu ambapo kila mdau anahusika.
Amesema
kuwa, pamoja na kwamba, Mahakama inatekeleza wajibu wake, inajikita kuangalia
ni kwa namna gani Mhimili huo unachangia katika ustawi na maendeleo ya Taifa.
“Sasa moja tunajua umuhimu wa Mahakama katika jamii, sasa katika kipindi hiki
tangu tulivyokutana tarehe 02 Machi, 2026 mwaka huu Mahakama Kuu sita ambazo ni
Njombe, Singida, Lindi, Simiyu, Songwe na Katavi zimezinduliwa na kufanya kazi
na Mahakama za Mwanzo 15 nazo zimezinduliwa na kuanza kufanya kazi. Amesema kwa
Tanzania Bara umebaki Mkoa mmoja pekee ambao hauna Masjala ya Mahakama Kuu
ambao ni Pwani.
“Tumesogeza
huduma zetu za Mahakama kwa watu ili haki ipatikane, kuwepo na amani na utulivu
watu waweze kushiriki shughuli zao za kiuchumi, za kisiasa na kijamii kwa
ufanisi ipasavyo. Kwa hiyo wenzetu mnaohusika na huduma za upelelezi mjue sasa
kuna huduma za Mahakama Kuu katika hiyo Mikoa,” amesema Mhe. Masaju.
Ameongeza
kuwa, Ibara ya 25(1) ya Katiba inasema; Kazi pekee ndio huzaa utajiri wa mali
katika jamii, ndilo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha Utu. Na kila
mtu anao wajibu wa: - a) kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi
halali na ya uzalishaji mali na b) kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi
kufikia malengo ya uzalishaji mali ya binafsi na yale malengo ya pamoja
yanayotakiwa au yaliyowekwa na sheria.
Kadhalika,
Jaji Mkuu amewakumusha Wadau hao kuhusu mikakati waliyokubaliana ambayo ni endelevu,
ambapo mkakati wa kwanza unasema, kila Taasisi ambayo ni Mdau wa Mnyororo wa Utendaji
Haki Mahakamani iwajibike ipasavyo kwa kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia
Katiba, Sheria na maadili ya utumishi yanayosimamia Taasisi ipasavyo.
Na
Mkakati wa pili ni kwamba Wadau wote Waheshimu na kulinda hadhi ya Mahakama,
aidha Mahakama kwa upande wake, isimamie sheria na kanuni zilizopo ikiwemo
sheria inayohusu kosa la kuidharau Mahakama yaani ‘Contempt of Court’ ili
kulinda hadhi na ukuu wake.
Amesema
kuwa, Sharti hilo ni la Kikatiba na lipo kwenye Ibara ya 30 (1) na ya (2d) kulinda
hadhi, heshima na uhuru wa Mahakama, si kama sisi tunataka kuheshimiwa tu hapa,
hili ni takwa la Kikatiba.
Mkakati
wa tatu ni; Mahakama na Wadau wa mnyororo wa haki waimarisha mahusiano miongoni
mwao kwa lengo la kuchukua hatua haraka ili kutatua changamoto za utoaji haki
zitakapojitokeza.
Mwingine
ni, Mahakama na Wadau wote watambue nafasi ya kila mmoja, wadumishe heshima,
nidhamu ya kazi na wazingatie sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza utendaji
kazi wa majukumu ya kila mdau.
Taasisi
ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki, iimarishe ufuatiliaji mashauri na
uwajibikaji kwa kutoa taarifa sahihi na za mara kwa mara kuhusu utekelezaji wa
mikakati iliyowekwa na kutumia mifumo inayosomana ili kurahisisha mawasiliano.
Wadau
wanaokiuka maadili wachukuliwe hatua ipasavyo kwa mujibu wa sheria na kanuni
zinazosimamiwa na kila mdau husika.
“Mkakati
wa saba, Mahakama iongeze na kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali
(Virtual Court) katika kuendesha mashauri yanayohusu watuhumiwa waliohamishiwa
katika Magereza mbalimbali kutoka kwenye Wilaya zisizo na Magereza na ili upatikanaji
wa haki uwe wa haraka na wa gharama nafuu.
Mkakati
mwingine ni Vikao kuhusu ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa jukumu
la utoaji haki mahakamani vifanyike angalau mara nne kwa mwaka ilikujadili
changamoto na kufuatilia utekelezaji wa mikakati hiyo. Mkakati wa tisa ni kila
Taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa utoaji haki Mahakamani iweke utaratibu madhubuti
wa ndani ya Taasisi utakaofanikisha utekelezaji wa mikakati hiyo.
Aidha,
katika Mkutano huo uliofanyika jana uliongezeka mkakati mwingine mpya unaosema
kwamba, migogoro yote inayopaswa kwa mujibu wa sheria kutatuliwa kwanza katika
ngazi mbalimbali kwa njia ya kimadai au kiutawala ishughulikiwe na kukamilishwa
katika hatua na ngazi zote husika badala ya kufunguliwa kama jinai moja kwa
moja na hili ni sharti la kisheria.
Jaji
Mkuu amesema kwamba, mikakati hiyo ikitekelezwa yatasaidia kuboresha mfumo wa
haki jinai na haki itakuwa inapatikana mapema, kwa changamoto ambazo
zinatatulika kwa urahisi.
“Huu
mkakati wa mwisho pia ni wa kisheria, katika kifungu cha 4 cha Sheria ya
Mwenendo wa Mashauri ya Jinai ndipo kinapopatikana....., mikakati yote
tuliyoiweka ni mikakati ya kisheria ipo kwenye sheria hakuna kitu hapa ambacho
hakipo kwenye sheria na ndio maana tunaweka mikakati, kilichopo kwenye sheria
lazima kinapaswa kitekelezwa, hatuwezi kuwekewa maazimio kwahiyo kwenye vikao
vyetu sisi tumeshakataa maazimio huwezi kuazimia kutekeleza au kutotekeleza
sheria, sheria ni lazima uitekeleze vinginevyo utaivunja na ukiivunja
unawajibika. Kwahiyo tuna wajibu wa kutekeleza haya yote, tuna wajibu wa
kutekeleza hii mikakati ambayo ni ya kisheria, vinginevyo tutawajibika,”
ameeleza Mhe. Masaju.
Amesema,
kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba inayoweka Utawala wa Sheria, inasema kila
mtu ana wajibu wa kufuata na kutii Katiba hii na Sheria za Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Ibara 26(2) inasema kila mtu ana haki kwa kufuata utaratibu
uliowekwa na Sheria kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na
Sheria za Nchi.
“Hata
mikutano yetu hii, ni katika hatua tunazochukua kuhakikisha kwamba Katiba na
Sheria za nchi zinatekelezwa ipasavyo na Ibara ya 25 inatutaka kila mmoja
awajibike kwenye hili, na sisi wote tunafanya kazi sasa kwa nafasi mbalimbali,
wengine ni Majaji, wengine ni Majaji Wakuu, wengine ni Wakurugenzi, wengine ni
Maofisa wa Polisi, wengine Ofisi ya Magereza, wengine Ofisi ya PCCB, Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, watumishi wote
wa Taasisi zilizowakilishwa hapa tuna majibu tuonafanya kazi hizi,” amesema
Jaji Mkuu.






























