Ijumaa, 13 Machi 2026

TAARIFA KWA UMMA


 

JAJI MKUU AWAAPISHA WAJUMBE WA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA

Na LYDIA CHURI, Tume ya Utumishi wa Mahakama

Jaji Mkuu wa  Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. George Masaju leo tarehe 13 Machi, 2026 amewaapisha wajumbe wanne wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Katika hafla iliyofanyika leo kwenye Ofisi za Tume ya Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma, Jaji Mkuu amemuapisha Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Gerson Mdemu kuwa Mjumbe wa Tume kufuatia uteuzi uliofanywa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, Jaji Mkuu pia amemuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kufuatia kuteuliwa kwa mara ya pili na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani uliofanyika Oktoba 29, 2025.

Jaji Mkuu pia amewaapisha kwa mara ya pili Mawakili Bahame Tom Nyanduga na Dosca Kemilembe Mutabuzi kuwa Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama baada ya kumaliza kipindi chao cha miaka mitatu cha kuwa Wajumbe wa Tume na kuteuliwa tena na Rais kushika nafasi hiyo kwa mujibu wa Ibara ya 112  (1) (e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tume ya Utumishi wa Mahakama inaundwa na wajumbe wafuatao; Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye ni Mwenyekiti, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Wajumbe wawili wanaoteuliwa na Rais.

Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo kilichoundwa kwa mujibu wa Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Sura ya 237. Chombo hiki kimeundwa kwa lengo la kusimamia utendaji kazi wa Mahakama ya Tanzania ikiwa ni pamoja na kusimamia Ajira na Nidhamu za Watumishi wa Mahakama.


Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. George Masaju akimuapisha Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Gerson Mdemu kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo jijini Dodoma. 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza Johari akiapa mbele ya  Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. George Masaju kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo jijini Dodoma. 

Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. George Masaju akimuapisha Wakili Bahame Tom Nyanduga kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo jijini Dodoma. 

Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama,  Mhe. George Masaju akimuapisha Wakili Dosca Kemilembe Mutabuzi kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo jijini Dodoma. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani kwenye hafla ya kuapishwa kwa Wajumbe wa Tume leo tarehe 13 Machi, 2026 jijini Dodoma. Jaji Ndika amemaliza muda wake kwa mujibu wa Sheria. 











 

MSAJILI MAHAKAMA YA RUFANI TANZANIA ASISITIZA UMUHIMU WA KUTUMIA TEKNOLOJIA MAHAKAMANI

Na JAMES BUSANYA & HALIMA MNETE- Mahakama Dodoma.

Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert, amesisitiza umuhimu wa matumizi ya mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.

Mhe. Herbert ametoa msisitizo huo leo tarehe 13 Machi, 2026, wakati anafunga mafunzo ya siku tano kati ya Maofisa wa Mahakama ya Tanzania na Mahkama ya Zanzibar yaliyokuwa yanafanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma.

Msajili wa Mahakama ya Rufani ameeleza kuwa teknolojia inaweza kusaidia kuongeza ufanisi wa kazi pamoja na kupunguza muda wa usikilizaji wa mashauri.

“Ni muhimu kuendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika Mahakama zetu, ikiwemo usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mfumo wa kielektroniki, jambo ambalo linaweza kusaidia kuondoa mlundikano wa mashauri na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki,” amesema.

Akizungumzia mafunzo hayo, Mhe. Herbert amewasihi washiriki kutumia maarifa waliyoyapata katika kuboresha utendaji kazi ndani ya Taasisi zao na kuimarisha utoaji wa haki kwa wananchi.

Amesema kuwa mafunzo ya kubadilishana uzoefu ni muhimu katika kujenga uwezo wa watumishi wa Mahakama, hususan katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiutendaji pamoja na kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia.

Naye Naibu Mrajisi wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Faraji Shumari Juma, akizungumuza kwenye hafla hiyo alitoa shukrani kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuandaa mafunzo hayo muhimu, akisema kuwa yamewasaidia washiriki kupata maarifa na uzoefu mpya wa kiutendaji.

Aidha, aliomba ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na Mahkama ya Zanzibar uendelee kuimarishwa ili kusaidia Taasisi hizo kujifunza zaidi kutoka kwa kila upande.

Alieleza kuwa ushirikiano huo ni muhimu hasa katika kuboresha matumizi ya mifumo ya kiteknolojia kwenye uendeshaji na usikilizaji wa mashauri kwa njia ya kidijitali ili kuongeza ufanisi na kuharakisha upatikanaji wa haki kwa wananchi.

Wakati wa mafunzo hayo ya siku tano yaliyoanza tangu tarehe 9 Machi, 2026, washiriki wamepata fursa ya kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali ya utendaji kazi, matumizi ya mifumo ya kidijitali, maadili ya kazi pamoja na mbinu za kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama.

Washiriki wameeleza kufurahishwa na elimu waliyoipata na kuahidi kutumia maarifa hayo katika kuboresha utendaji wa kazi katika Mahakama zao.

Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert, akizungumza wakati anafunga mafunzo hayo leo tarehe 13 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma.

Naibu Mrajisi wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Faraji Shumari Juma, akitoa neno la shukrani kwenye hafla hiyo.

Sehemu ya Washiriki wa mafunzo hayo kutoka Mahkama ya Zanzibar wakifuatilia yaliyokuwa yanajiri.

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim (katikati). Wengine ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert (kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Kinabo Minja.


Sehemu ya Washiriki wa mafunzo hayo (juu na chini) ikiwa kwenye picha ya pamoja. Aliyekaa ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

NAIBU MSAJILI WA MAHAKAMA KUU KANDA YA LINDI AFANYA KIKAO NA WATUMISHI

Na. Hilary Lorry  & Winifrida Kisamo– Mahakama, Lindi

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi pamoja na Mahakama ya Wilaya ya Lindi, tarehe 11 Machi 2026 wamefanya kikao kazi na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Lindi, Mhe. Elia Joseph Mrema ambaye amesema Mahakama Kuu Kanda hiyo inayotarajiwa kuanza kutoa huduma za Mahakama Kuu kwa wananchi hivi karibuni kuanzia sasa.

Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuanza kwa shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Lindi.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mtendaji wa Mahakama Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela aliwapongeza watumishi wa Mahakama hizo kwa uwajibikaji wao na uchapakazi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Alieleza kuwa watumishi hao wamekuwa wakitekeleza majukumu yao kwa bidii na kila mmoja anatambua wajibu wake katika kuhakikisha huduma za kimahakama zinatolewa kwa ufanisi.

Aidha, Mtendaji huyo aliwasisitiza watumishi kuendelea kudumisha usafi wa mazingira katika majengo ya Mahakama pamoja na kuyatunza ipasavyo, akibainisha kuwa mazingira safi na yakitunzwa vizuri huchangia kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na kutoa taswira nzuri kwa wananchi wanaofika kupata huduma.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano alisisitiza umuhimu wa utunzaji wa vifaa vya Ofisi pamoja na matumizi sahihi ya rasilimali za Ofisi.

Alieleza kuwa, utunzaji mzuri wa vifaa hivyo utasaidia kuvifanya vitumike kwa muda mrefu, hivyo kuvifanya viweze kutumika kwa mahitaji ya sasa na ya baadaye. Pia alibainisha kuwa matumizi sahihi ya rasilimali za Ofisi yatasaidia kupunguza gharama zisizo za lazima katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema aliwashukuru watumishi kwa ushirikiano waliyompatia tangu alipowasili katika Kituo hicho. Vilevile aliahidi kutoa ushirikiano wa karibu katika utekelezaji wa majukumu ya Mahakama.

Mhe. Mrema aliongeza kuwa, kwa mara ya kwanza katika Mkoa wa Lindi tunaenda kuwa na Mahakama Kuu hivyo basi yatupasa kufanya maandalizi muhimu pamoja na kujianda kwa ujio wa Jaji Mfawidhi, “Sisi  tupo kwenye kufanya maandalizi muhimu pamoja na kujiandaa  kwa ujio wa Jaji Mfawidhi ” alisisitiza Mhe. Mrema.

Aidha, aliwapongeza watumishi wa Mahakama Kanda ya Lindi kwa kazi nzuri wanayoifanya, akieleza kuwa tangu alipowasili mkoani humo na kutembelea baadhi ya ofisi, ikiwemo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Kamada wa Polisi Mkoa, Takukuru, Ofisi ya Uhamiaji, Ofisi ya Mawakili wa kujitegemea(TLS) na wadau wengine  hakupokea malalamiko yoyote kuhusu utendaji wa watumishi.

Mhe. Mrema alisema hali hiyo inaonesha kiwango kizuri cha uwajibikaji na nidhamu ya kazi miongoni mwa watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo hivyo aliwataka watumishi kuendeleza juhudi hizo na ikiwezekana kufanya vizuri zaidi.

Naibu Msajili pia alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, kuaminiana na kuheshimiana miongoni mwa watumishi pamoja na viongozi, huku akisisitiza kuwa kufanya kazi kwa ushirikiano na kuheshimu mipaka ya majukumu ya kila mmoja ni msingi muhimu wa mafanikio katika utendaji wa taasisi, “Tufanye kazi kwa ushirikiano huku tukiheshimu mipaka na tuhakikishe Lindi inakuwa ya mfano” Alisisitiza Mhe. Mrema.

Vilevile, aliwataka watumishi kuwa wabunifu na kuchapa kazi kwa bidii na  kwa kuzingatia misingi ya uadilifu, uwajibikaji na weledi katika kutekeleza majukumu yao, hivyo kuimarisha ufanisi wa kazi na utoaji huduma bora kwa wananchi mapema ipasavyo.

Kikao hicho ni sehemu ya maandalizi muhimu kuelekea kuanza rasmi kwa shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Lindi, inayotarajiwa kuanzishwa hivi karibuni, hatua inayotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa huduma za utoaji haki kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi na maeneo ya jirani.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema akizungumza na watumishi wa Mahakama Lindi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano (aliyesimama) akitoa neno la utambulisho.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho.

Afisa Hesabu Mkuu Mahakama ya Wilaya ya Lindi Bw. Lucas M. Kadossa akitoa neno la shukurani kwa niaba ya watumishi.

Waandishi Waendesha Ofisi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi wakitekeleza jukumu lao la uchukuaji wa Muhtsari katika kikao hicho.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


Jumatano, 11 Machi 2026

JAJI MKUU, MHE. GEORGE MASAJU AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA KATIBU MKUU UMOJA WA MATAIFA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 11 Machi, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Bw. Parfait Onanga-Anyanga,  Mjumbe Maalum  wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. António Guterres.

Bw. Onanga-Anyanga na ujumbe alioambatana nao waliwasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma majira ya Asubuhi na kupokelewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert.

Mjumbe huyo Maalum amefanya ziara nchini Tanzania kwa lengo la kuonana na Viongozi mbalimbali wa Serikali kwa lengo la kujadili masuala yanayohusu amani, uimarishaji wa demokrasia na utawala wa sheria kwa ujumla.

Bw. Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania pia kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali na kutathmini hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kitaifa na kuendeleza misingi ya utawala wa sheria kufuatia matukio ya uvunjifu wa amani ya kabla na wakati wa Uchaguzi Mkuu tarehe 29 Oktoba, 2025.

Aidha, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa hatua inayoendelea kuchukua kufuatia matukio ya uvunjivu wa amani wakati na baada ya uchaguzi wa tarehe 29 Oktoba, 2025. Ameeleza kuwa hatua hizo ni pamoja na; kuunda Tume Huru ya Uchunguzi ya Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025, dhamira ya kufanya mazungumzo jumuishi na mchakato wa mabadiliko ya Katiba.

Bw. Onanga–Anyanga ameeleza kuwa Umoja wa Mataifa unaendelea kuitambua Tanzania kama nchi yenye historia ya muda mrefu ya amani na pia wanatambua umuhimu wa kuwa na taasisi imara mfano Mahakama kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Kwa upande wake Mhe. Jaji Mkuu amemshukuru Mjumbe huyo Maalum kwa kutambua juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania.

Aidha, Mhe. Masaju amemueleza Bw. Onanga-Anyanga kwamba, Mahakama ya Tanzania imeendelea kuwa huru na kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba mashauri yaliyofunguliwa kuhusiana na mchakato wa uchaguzi na pia baada ya uchaguzi yameshughuliwa ipasavyo.

Katika ziara hiyo Bw. Onanga-Anyang mbali na wajumbe wengine ameambatana pia na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Bw. Shigeki Komatsubara.

Picha mbalimbali za ziara ya Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa (UN) katika Umoja wa Afrika, Bw. Parfait Onanga-Anyanga Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika, Bw. Parfait Onanga-Anyanga leo tarehe 11 Machi, 2026 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati alipomtembelea Jaji Mkuu. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akimpokea Bw. Parfait Onanga-Anyanga, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati yeye na ujumbe alioambatana nao walipowasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma kwa lengo la kuonana na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) pamoja na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert wakiongoza Ujumbe wa Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulipowasili Makao Makuu ya Mahakama kuonana na kufanya mazungumzo na Jaji Mkuu.


Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Parfait Onanga-Anyanga akisaini kitabu cha wageni alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 11 Machi, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mazungumzo kati ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Ujumbe maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na sehemu ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakiendelea na mazungumzo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimpatia zawadi 
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Parfait Onanga-Anyanga.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimpatia zawadi Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Bw. Shigeki Komatsubara.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa zawadi kwa wajumbe walioambatana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa waliomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 11 Machi, 2026.







UADILIFU NDIO NGUZO KUU YA UTENDAJI; PROF. NDALICHAKO

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako amewaeleza Majaji na Mahakimu Wanawake wa Tanzania kuwa, weledi na uadilifu ndizo nguzo kuu na muhimu za utendaji hivyo hawana budi kuzizingatia wakati wanapotimiza wajibu wao.

Prof. Ndalichako aliyasema hayo jana tarehe 10 Machi, 2026 alipokuwa akifunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake, lililofanyika katika ukumbi wa New Generation Hall Kisasa jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa kufunga Kongamano hilo, Prof. Ndalichako amesema kuwa, ameridhishwa na mjadala wenye afya na nia ya dhati ya kujenga na kuimarisha haki na usawa wa kijinsia, pamoja na maazimio yaliyowekwa ambayo watakwenda kuyatekeleza.

Aliongeza kuwa, lengo la kuanzishwa kwa TAWJA ni kutambua mchango wa Majaji Wanawake duniani na kuhimiza usawa wa kijinsia katika Mhimili wa Mahakama, hivyo kongamano hilo ni tukio muhimu la kubadilishana maarifa kuonesha uongozi, ujasiri na dira ya mabadiliko pia ni mwanga unaoangaza nuru na kazi kubwa wanayoifanya ambayo inaakisiwa hadi nje na si ndani ya kumbi za Mahakama pekee bali katika jamii nzima.

Prof. Ndalichako amesisitiza kuwa uadilifu ni nguzo kuu ya utendaji, hivyo ni vema Majaji na Mahakimu Wanawake kuendelea kuzingatia uadilifu katika masuala ya haki, huku akinukuu maneno ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati alipokuwa akiwaapisha Majaji ambapo alisema, “uzoefu umeonesha kuwa Majaji wanawake huwazidi wenzao wa kiume katika utendaji unaozingatia masuala ya uadilifu.”

Aliongeza kuwa, anavutiwa na weledi, mshikamano na kujitoa kwa Majaji na Mahakimu wanawake hali inayoleta mabadiliko ya kijamii kwa kuzingatia utawala wa haki unaoleta usawa wa kijinsia.

Aidha, amesema kuwa haki haitoshi kutolewa bali inapaswa ieleweke na iguse mioyo ya watu pamoja na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama, hivyo Majaji na Mahakimu Wanawake wana nafasi muhimu katika kuhakikisha sheria inazungumza kwa haki na uadilifu.

Katika hatua nyingine, Prof. Ndalichako alizungumzia kuhusu umuhimu wa kuimarisha mifumo ya Taasisii ili kulinda afya ya kisaikolojia ya Mahakimu ambapo ameeleza kuwa mtu hawezi kuponya wengine ikiwa yeye mwenyewe ana maumivu, hivyo ni vema kulinda afya ya akili ili kuimarisha utendaji.

“Mmesisitizwa pia kuhusu umuhimu wa kulinda mifumo ya Taasisi ili kulinda afya ya kisaikolojia ya Mahakimu, huwezi kuponya jamii wakati wewe mwenyewe unaumia kimyakimya, ni vema kuendelea kuhakikisha kwamba tunalinda afya za akili ndani ya Makahama ili iendelee kutoa haki endelevu,” alisisitiza Mwenyekiti huyo.

Kadhalika, alisema kuwa, ni vema kuepuka kuwajeruhi upya wahanga na manusura wa ukatili wa kijinsia na kusisitiza kuwa, manusura wanastahili kujisikia salama na kuheshimiwa, hivyo haki lazima irejeshe utu na si kufungua tena majeraha.

Alieleza kwamba, teknolojia inakua kwa kasi hivyo ni vema itumike katika kuwalinda waathirika wa masuala ya ukatili wa kijinsia hasa ukatili wa mitandaoni, hivyo ubunifu ni lazima uendelee kutumika ili kuimarisha ulinzi wa waathirika na kuongeza uwajibikaji kwa kutumia Mahakama mtandao.

Alisema kuwa, yeye kama Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake anawahakikishia kuwa, Bunge pamoja na Wabunge wengine wataendelea kushirikiana katika kuimarisha sheria zinazolinda wanawake na watoto, hivyo ujumbe alioubeba katika mijadala ya leo utatumika ili kuendelea kukuza usawa wa kijinsia. 

Katika hatua nyingine, Prof. Ndalichako ameeleza kuwa mojawapo ya mafanikio makubwa kwa Mahakama na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA) ni kufikia usawa wa asilimia 50 kwa 50 kwa Majaji jambo ambalo ni la msingi katika kukuza imani kwa wananchi.

Kama Kaulimbiu ya mwaka huu inavyokumbusha, amewataka Majaji na Mahakimu hao wanawake kutoka mahakamani na kwenda kwenye jamii wakitoa haki kwa uadilifu huku wakijihusisha kikamilifu katika shughuli za uelimishaji hususan kupitia vyombo vya habari, kuzalisha maarifa na kujengeana uwezo jambo litalaojenga uaminifu kwa jamii ya watoto wa kike kuwa ndoto zao ni halali na matarajio yanawezekana na mustakabali wa maisha yake hauna mashaka.

Kauli mbiu ya Kongamano hilo kwa mwaka huu ni “Kutoka mahakamani kuifikia jamii: Majaji na Mahakimu wanawake mstari wa mbele kuongoza mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Awali, kongamano hilo lilifunguliwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Juma Homera, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi. Kongamano hilo lilihudhuriwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, UN Women, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka na wageni wengine waalikwa.


Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako akizungumza alipokuwa mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. 


Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) baada ya kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. Aliyekaa kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winifrida Korosso. 


Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) baada ya kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake lililofanyika kwenye ukumbi wa New Generation Hall jijini Dodoma. Aliyekaa kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winifrida Korosso. 


Mgeni rasmi Mbunge wa Kuteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Joyce Ndalichako (kushoto) akifuatilia kinachojiri wakati wa kufunga Kongamano maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake. Kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Kongamano hilo, Mhe. Winifrida Korosso.

Mgeni rasmi wakati wa kufunga Kongamano Maalum la Kusheherekea Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake, Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Majaji Wanaume waliohudhuria katika Kongamano hilo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

UJENZI WA MAHAKAMA ZA MWANZO TATU MKOANI RUVUMA WAKAMILIKA

Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea

Mahakama ya Tanzania imekamilisha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo tatu, Lilolndo, Likuyusekamaganga na Nalasi, zilizopo katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, mkoani Ruvuma.

Mahakama za Mwanzo Lilondo ipo Wilaya ya Songea katika Halimashauri ya Madaba, Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga ipo katika Wilaya ya Namtumbo na Mahakama ya Mwanzo Nalasi ipo katika Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma.

Ujenzi huo uliokuwa unatekelezwa na Mkandalasi Mkuu (Pivotech), akisaidiana na Mkadalasi Msaidizi(Cadson) na majengo hayo matatu ya Mahakama yamegharimu jumla ya Shilingi za Kitanzania 2,954,059,829.18.

Mahakama ya Mwanzo Lilondo imegharimu 985,625,739/=, Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga imegharimu 961,400,162/= na Mahakama ya Mwanzo Nalasi imegharimu 1,007,033,928.18/=.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele, alikabidhiwa majengo hayo hivi karibuni kwa nyakati tofauti na  Mkandarasi Arqes Africa Architects and Interior Designers Ltd. 

Alitoa shukrani kwa wananchi wa maeneo hayo kwa ushirikiano waliouonyesha tangu kuanza hadi kumalizika kwa miradi hiyo.

Alieleza kuwa uzinduzi wa Mahakama hizo umepangwa kufanyika tarehe 10 Aprili, 2026 katika Mahakama ya Mwanzo Lilondo, kama  kuashiria kuanza kwa huduma za kimahakama zitakazoanza kutolewa katika majengo hayo mapya yaliyokamilika.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Lilondo.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga.

Jengo la Mahakama ya Mwanzo Nalasi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa pili kulia) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Lilondo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa katikati) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (kushoto) akikabidhiwa hati ya jengo Mahakama ya Mwanzo Nalasi.

Wananchi na wakazi wa Nalasi wakiwa katika eneo la tukio wakishuhudia makabidhiano hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

  

WIKI YA USULUHISHI


 

Jumanne, 10 Machi 2026

MAJAJI NA MAHAKIMU WANAWAKE WAUNGANA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA

     Wajadili nafasi ya wanamke katika kuimarisha utoaji haki na kuifikia jamii

Na HALIMA MENETE, Mahakama-Dodoma

Kongamano maalumu la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake limefanyika leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New Generation jijini Dodoma, likiwakutanisha Viongozi wa Serikali, Mahakama ya Tanzania pamoja na wadau wa maendeleo kujadili nafasi ya Majaji na Mahakimu wanawake katika kupambana na ukatili wa kijinsia.

Kongamano hilo lililobeba Kauli mbiu, “Kutoka Mahakamani Kuifikia Jamii: Majaji na Mahakimu Wanawake Mstari wa Mbele Kuongoza Mapambano Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia” lilihudhuriwa na mgeni rasmi Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Majaji na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania bara na visiwani pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo UN Women, RITA, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka.

Katika kongamano hilo pia, kulikuwa na nafasi ya utoaji mada mbalimbali, ambapo moja wa mada ilihusu “Nafasi ya Mwanamke kama Kiongozi katika Kuleta Mabadiliko kwenye Jamii kupitia Utoaji wa Haki unaozingatia Masuala ya Kijinsia.”

Mada hiyo iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Joseph Kerefu huku ikiendeshwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Magimbi, na ilijadiliwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Moshi Mhe. Dkt Lilian Mongela, Naibu Msajiri Mhe. Upendo Ngitiri na Hakimu Mkazi, Mhe. Juliana Mvungi.

Akifafanua kwa kina mada hiyo, Mhe. Kerefu amesema kuwa, katika juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia katika utoaji wa haki, tayari kuna misingi na nyenzo mbalimbali zilizowekwa kimataifa na kitaifa ambazo zinaweza kusaidia katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Amesema miongoni mwa nyenzo hizo ni pamoja na maandiko ya kitaaluma kama kitabu kilichoandikwa na Kosana Beker kinachojadili Gender and Diversity in the Judiciary, ambacho kinaeleza kwa kina umuhimu wa kuzingatia masuala ya kijinsia na utofauti katika mfumo wa utoaji haki.

Kwa mujibu wa Jaji Kerefu, uwepo wa vitendea kazi hivyo unaonesha wazi kuwa, kuna uwanja mpana wa kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa ipasavyo na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.

Hata hivyo, ameeleza kuwa, pamoja na uwepo wa misingi hiyo imara ya kisheria na kitaaluma bado kuna changamoto zinazotokana na baadhi ya mila, desturi na tamaduni katika jamii ambazo wakati mwingine zimekuwa zikikwamisha juhudi za kuimarisha usawa wa kijinsia.

Amesema baadhi ya mila na desturi hizo zimejikita katika mfumo dume, hali ambayo wakati mwingine imekuwa ikiweka vikwazo kwa watoa haki katika kuhakikisha misingi ya usawa wa kijinsia kama ilivyoainishwa katika mikataba ya kimataifa, Katiba ya nchi na sheria mbalimbali zinazozingatia masuala ya kijinsia zinatekelezwa kikamilifu.

Aidha, amesema licha ya maendeleo yaliyopatikana katika kuimarisha haki za wanawake, bado kuna changamoto mbalimbali zinazoendelea kujitokeza katika jamii ikiwemo ongezeko la mashauri ya ubakaji, unyanyasaji wa kingono, ukatili wa majumbani pamoja na ndoa za utotoni.

Ameongeza kuwa, hata katika masuala ya umiliki wa mali na mirathi bado kuna changamoto zinazowakabili wanawake katika jamii, huku baadhi ya sheria zilizopo zikionekana kutokidhi kikamilifu matakwa ya usawa wa kijinsia.

Ametolea mfano wa ‘Customary Law Declaration Order’ ya mwaka 1963 pamoja na baadhi ya vipengele vya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ambavyo bado vinaibua mjadala kutokana na kuwepo kwa vipengele vinavyohusishwa na ruhusa ya ndoa za utotoni.

Kwa upande mwingine, washiriki wa mada hiyo walieleza kuwa, changamoto hizo zinapaswa kuwa chachu kwa wadau wa sekta ya sheria, hususan majaji na Mahakimu wanawake, kuendelea kutumia elimu yao ya sheria pamoja na misingi iliyowekwa kuhakikisha vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinatokomezwa.

Vilevile ilielezwa kuwa mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia yanahitaji ushirikiano mpana wa taasisi mbalimbali, ikiwemo Mahakama, Serikali, Wadau wa maendeleo pamoja na jamii kwa ujumla.

Akizungumzia uwakilishi wa wanawake katika Sekta ya Mahakama duniani, Mhe. Kerefu alieleza kuwa baadhi ya nchi zimepiga hatua kubwa katika kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi za kimahakama, akitolea mfano wa Italia ambapo wanawake wanawakilisha zaidi ya asilimia 52.9 ya Majaji.

Hata hivyo, alisema bado kuna nchi ambazo uwakilishi wa wanawake katika Mahakama uko chini, akitolea mfano wa Iraq yenye takribani asilimia 7.6 na Nepal yenye asilimia 3.8.

Kwa upande wa Tanzania, washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa, kumekuwa na mafanikio makubwa katika kuongeza uwakilishi wa wanawake katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

Imeelezwa kuwa Mahakama ya Rufani tangu ilipoanzishwa mwaka 1979 ilianza na Majaji watano wote wakiwa wanaume, lakini kwa sasa idadi hiyo imeongezeka na kufikia Majaji 37, ambapo wanaume ni 25 na wanawake ni 12, idadi inayozidi asilimia 30 ya uwakilishi wa wanawake.

Aidha, katika Mahakama Kuu kuna jumla ya Majaji 104 ambapo wanaume ni 65 na wanawake 39, wakati Mahakama za Hakimu Mkazi zina jumla ya Mahakimu 1,434 ambapo wanaume ni 746 na wanawake 688 sawa na takribani asilimia 48.

Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo, kuna Mahakimu 189 ambapo wanaume ni 111 na wanawake 78 sawa na asilimia 41.

Kwa upande wa Zanzibar, Mahakama Kuu ina jumla ya majaji 14 ambapo wanaume ni tisa na wanawake watano sawa na asilimia 35, huku katika ngazi ya mahakimu kukiwa na jumla ya Mahakimu 66 ambapo wanawake ni 23 na wanaume 43.

Washiriki wa kongamano hilo walieleza kuwa takwimu hizo zinaonesha wazi juhudi za Serikali katika kuhakikisha wanawake wanapata nafasi katika ngazi mbalimbali za uongozi ndani ya Mhimili wa Mahakama.

Hata hivyo, walisisitiza kuwa pamoja na ongezeko hilo la uwakilishi wa wanawake, bado kuna umuhimu wa kuhakikisha kuwa nafasi hizo zinatumika ipasavyo kuimarisha utoaji wa haki na kuchangia kikamilifu katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Rehema Kerefu (wa kwanza kulia) akiongoza mada isemayo, “Nafasi ya Mwanamke kama Kiongozi katika Kuleta Mabadiliko kwenye Jamii kupitia Utoaji wa Haki unaozingatia Masuala ya Kijinsia," wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake ambayo huadhimishwa tarehe 10 Machi kila mwaka.


Baadhi ya washiriki wa Kongamano maalum la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Majaji na Mahakimu Wanawake ambalo limefanyika  leo tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa New Generation jijini Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)