Jumatatu, 20 Aprili 2026

MAHAKAMA GEITA YAPOKEA UGENI KUTOKA DIVISHENI YA BIASHARA, MASJALA NDOGO SINGIDA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, imeendelea kujipambanua katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), baada ya kupokea ugeni kutoka Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara ya Dar es Salaam pamoja na Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida.

Lengo la ziara hizo lilikuwa ni kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya TEHAMA katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.

Ugeni wa kwanza uliwasili tarehe 16 Aprili, 2026 ukitokea Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, ukiwa na wajumbe wanane ukiongozwa na Naibu Msajili, Mhe. Suzan Kihawa, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Anatory Kagaruki.

Ugeni wa pili ulitoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, ukiwa na Watumishi tisa, wakiongozwa na Naibu Msajili, Mhe. Evodia Kyaruzi, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Filbert Matotay.

Katika ziara hiyo, kulifanyika mafunzo yaliyofunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, ambaye aliwakaribisha wageni na kuwashukuru kwa kuchagua Geita kama Kituo cha kujifunza.

Alieleza kuwa ziara hiyo ni fursa muhimu ya kubadilishana mawazo na uzoefu kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama kwa kutumia TEHAMA.

Jaji Mhina alibainisha kuwa mafanikio ya Mahakama Kuu Geita yametokana na misingi madhubuti iliyowekwa tangu kuanzishwa kwake, ikiwemo maelekezo ya Viongozi wakuu wa Mahakama, yaliyosisitiza umuhimu wa kuifanya Mahakama kuwa ya kisasa kidijitali.

Aliongeza kuwa matumizi ya TEHAMA yameongeza uwazi, yamepunguza gharama za uendeshaji, yamerahisisha upatikanaji wa taarifa na kuboresha mifumo ya ukaguzi wa shughuli za Mahakama.

Aidha, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa mafanikio hayo yanatokana na mambo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara wa mifumo, usimamizi thabiti wa Watumishi, ufuatiliaji wa karibu wa utendaji kazi, utoaji wa motisha, pamoja na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa Watumishi bila kujali kada zao.

Mafunzo hayo yalihusisha jumla ya mada tano zilizowasilishwa na Watumishi mbalimbali wa Mahakama, kwa lengo la kupeana uzoefu na kuboresha utendaji wa kazi.

Mada hizo zilitolewa na Naibu Msajili, Mhe. Fredrick Lukuna, Mtendaji wa Mahakama Bi. Masalu Kisasila, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, pamoja na Mtunza Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Geita, Bi. Winfirda Ng’humbu.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mhe. Lukuna, alisisitiza kuwa mafanikio ya Taasisi yoyote yanategemea mshikamano wa pamoja miongoni mwa Watumishi wake.

Alieleza kuwa ni muhimu kuwa na malengo ya pamoja, kushirikiana kikamilifu katika utekelezaji wa majukumu, kukubali makosa na kujifunza kutokana nayo, pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa vitendea kazi vya kutosha.

Aidha, alihimiza utambuzi wa mapema wa changamoto zinazoweza kujitokeza ili zisikwamishe utekelezaji wa malengo yaliyowekwa.

Kwa upande wa mada ya utawala na matumizi ya TEHAMA, Mtendaji wa Mahakama Geita alieleza kuwa wamefanikiwa kuendesha shughuli nyingi za kiutawala bila matumizi ya karatasi.

Alifafanua kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano wa Watumishi wote pamoja na utayari wao wa kuendana na dira ya uongozi wa Mahakama Kuu Geita ya kuimarisha matumizi ya TEHAMA.

Akizungumza kwa niaba ya wageni, Mhe. Kihawa alitoa shukrani kwa mapokezi mazuri pamoja na mafunzo waliyoyapata, akieleza kuwa uzoefu huo utasaidia kuboresha utendaji katika Mahakama zao.

Naye Mhe. Kyaruzi alieleza kuridhishwa na mafunzo hayo na kuahidi kutumia maarifa hayo kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika Masjala zao.

Wageni walipata fursa ya kujionea kwa karibu namna Mahakama Kuu ya Geita ilivyofanikiwa kufikia hatua ya matumizi kamili ya TEHAMA katika utoaji wa huduma zake.

Kupitia uzoefu huo, wageni hao waliondoka wakiwa na matarajio na dhamira ya kutekeleza maboresho makubwa zaidi katika maeneo yao ya kazi, wakilenga kuiga na kuendeleza mifumo waliyoishuhudia.

Lengo kuu ni kuhakikisha kuwa wanakuwa sehemu ya mabadiliko chanya yatakayochochea utoaji wa huduma za haki kwa Wananchi kwa ufanisi zaidi, uwazi ulioboreshwa na kwa wakati muafaka.

Kwa mtazamo wa jumla, ziara hizi zimekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA ndani ya Mahakama za Tanzania.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina akifungua mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akitoa ufafanuzi juu ya ushirikiano biana ya Viongozi na Watumishi unavyoleta mafanikio katika kuongeza ufanisi wa matimizi ya Tekinolojia ya Habari na mawasiliano (TEHAMA).

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Suzan Kihawa akitoa shukrani wakati wa ziara waliyoifanya Mahakama Kuu Geita.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi akieleza jinsi Geita ilivyowavutia kwenye matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, akielezea namna utawala Mahakama Geita ulivyoachana na matumizi ya karatasi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Mujuni Muchunguzi, akieleza jinsi Mahakama za Wilaya wanavyotumia mifumo katika Mahakama za Wilaya.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, akieleza jinsi Mahakama za Mwanzo zilivyoachana na matumizi ya karatasi kwa kubuni Mfumo wa Mahakama za Mwanzo.

Picha ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara.


 Picha ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na Mahakama Kuu Singida.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKAMA SONGEA YAZINDUA MAJENGO MATATU YA MAHAKAMA ZA MWANZO

Na NOEL SYLIVESTER – Mahakama, Songea

Mahakama ya Tanzania katika Mkoa wa Ruvuma, tarehe 17 Aprili, 2026 imezindua Mahakama za Mwanzo tatu kwenye Wilaya mbalimbali baada ya ujenzi wake kukamilika.

Uzinduzi huo uliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, ambao ulifanyika kwa pamoja katika Viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Lilondo katika Wilaya ya Songea.

Mahakama nyingine zilizozinduliwa ni Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga iliyopo katika Wilaya ya Namtumbo na Mahakama ya Mwanzo Nalasi iliyopo Wilaya ya Tunduru.

Uzinduzi wa Mahakama hizo unalenga kurahisisha upatikanaji wa haki kwa Wananchi, kupunguza umbali wa kufuata huduma za kimahakama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa wakati na garama nafuu.

Katika hafla hiyo, Jaji Mfawidhi aliongelea dhima ya Mahakama katika kutoa haki kwa wakati unaostahili bila kuchelewesha huduma hizo za msingi kwa Wananchi.

Vilevile, Mhe. Karayemaha aliwaasa Watumishi na Wananchi wa maeneo hayo  kuhakikisha wanayatunza majengo hayo na miundombinu yake ili yaweze kudumu kwa muda mrefu.

“Kuanzishwa kwa Mahakama hizi kutasaidia kupunguza msongamano wa mashauri na kuharakisha utoaji wa haki. Hatua hii ni sehemu ya juhudi za Mahakama na Serikali ya Tanzania kuhakikisha kila Mwananchi anapata haki kwa wakati na kwa ghalama nafuu,”alisema.

Kwa upande wake, mgeni maalumu katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Kapenjama Ndile, aliwaasa Wananchi kushirikiana na Watumishi wa Mahakama kwa ajili ya kulinda msingi wa amani na kudumisha ustawi wa utoaji haki kwa Wananchi.

“Mahakama ni mali ya Wananchi, hivyo ni wajibu wetu sote kushirikiana na kuyatunza majengo ya Mahakama zetu pamoja na miundombinu yake kwa ujumla,” alisema Mhe. Ndile.

Katika taarifa yake, Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, alitoa ufafanuzi kuhusu majengo hayo ambayo yamezinduliwa na gharama zilizotumika mpaka kukamilika kwa ujenzi wa majengo hayo yote matatu.

Alibainisha kuwa Mahakama ya Mwanzo Lilondo mpaka kukamilika kwake imetumia 985,625,739/=. Mahakama ya Mwanzo Likuyusekamaganga imegharimu 961,400,162/= na Mahakama ya Mwanzo Nalasi imegharimu 1,007,033,928.18/=, hivyo kufanya  jumla ya 2,954,059,829.18/=

Hafla hiyo pia ilihudhuliwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Songea, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Songea, Mbinga, Nyasa, Namtumbo na Tunduru, pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha akihutubia katika hafra ya uzinduzi wa Mahakama za Mwanzo tatu baada ya ujenzi wake kukamilika.

Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Kapenjama Ndile, akihutubia katika hafla hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, akisoma taarifa ya ujenzi wa Mahakama hizo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha (wa tatu kutoka kushoto) akikata utepe kuashiria kuzinduliwa wa Mahakama hizo.

Sehemu ya Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama waliohudhulia hafla hiyo.

Kikundi cha Ngoma za Asili kikitumbuiza wakati wa halfa hiyo.

Sehemu ya Wananchi wa Lilondo wakishuhudia uzinduzi wa Mahakama hizo.

Sehemu ya Wanafunzi waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Serikali waliohudhuria katika hafla hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKIMU WAPATIWA MAFUNZO KUHUSU TARATIBU UCHUKUAJI MAELEZO YA UNGAMO

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Mahakama Dodoma tarehe 17 Aprili, 2026 iliendesha mafunzo ya taratibu za uchukuaji wa maelezo ya ungamo, yakihusisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutoka Dodoma na Singida.

Mafunzo hayo yaliyoendeshwa kwa mfumo mseto, yalifanyika katika ukumbi wa Mahakama uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Baadhi ya washiriki walihudhuria ana kwa ana ukumbini, huku wengine wakishiriki kwa njia ya mtandao kupitia kiunganishi maalumu. Hatua hiyo iliwezesha ushiriki mpana zaidi wa Mahakimu, wakiwemo wale ambao hawakuweza kufika eneo la mafunzo.

Akifungua mafunzo hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, alisisitiza umuhimu wa Mahakimu kuzingatia kikamilifu taratibu za kisheria katika uchukuaji wa maelezo ya ungamo ili kulinda haki na kuhakikisha ushahidi unaokubalika mahakamani.

“Ubora wa uamuzi wa Mahakama huanza na ubora wa ushahidi unaowasilishwa, ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa maelezo ya ungamo yanachukuliwa kwa kuzingatia kikamilifu sheria, miongozo na kanuni zilizowekwa,” alisema Dkt. Masabo.

Katika hotuba yake, aliwashukuru kwa dhati wawezeshaji wa mafunzo hayo kwa kujitoa kwao, hususan wale waliowezesha mafunzo kwa njia ya mtandao, akiwemo Naibu Msajili na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Huduma za Mahakama, Ukaguzi, Mrejesho kwa Umma na Maadili, Mhe. Maira Kasonde, pamoja na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mombo, ambaye pia ni mwezeshaji wa mafunzo hayo.

Aidha, alitambua na kushukuru ushiriki wa Viongozi wa juu wa Mahakama waliohudhuria kwa njia ya mtandao, akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayubu Mwenda, ambaye alifuatilia mafunzo hayo kama sehemu ya kuimarisha utoaji haki katika maeneo yao.

Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea Mahakimu uelewa wa kina kuhusu taratibu sahihi za kisheria katika uchukuaji wa maelezo ya ungamo, pamoja na kuwapa mbinu bora za vitendo zitakazosaidia kuepuka makosa ya kiutaratibu yanayoweza kuathiri ushahidi na uamuzi wa Mahakama.

Kupitia mafunzo hayo, Mahakimu wamekumbushwa umuhimu wa kufuata miongozo ya sheria katika kila hatua ya uchukuaji wa maelezo ya ungamo, ikiwemo kuhakikisha mtuhumiwa anafahamishwa haki zake, kurekodi maelezo kwa usahihi, na kuthibitisha uhalali wa maelezo hayo kwa mujibu wa sheria.

Mafunzo hayo yameacha alama muhimu kwa washiriki, yakiwakumbusha wajibu wao mkubwa katika kulinda haki za Wananchi kupitia uzingatiaji sahihi wa sheria na taratibu.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya mifumo ya utoaji haki na changamoto zinazoendelea kujitokeza, utoaji wa mafunzo hayo kwa njia ya ana kwa ana pamoja na mtandao unaonesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha Mahakimu wanakuwa na uelewa wa kisasa unaokidhi mahitaji ya wakati.

Hatua hiyo si tu inalenga kuboresha utendaji kazi wa Mahakimu, bali pia inalenga kuimarisha imani ya jamii kwa Mhimili wa Mahakama, ambapo haki haitolewi tu bali inaonekana ikitendeka kwa uwazi, weledi na uadilifu.

Akimhitimisha mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule, amewashukuru washiriki kwa ushiriki wao mzuri, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yatachangia kuleta mabadiliko chanya katika utoaji wa haki na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masab,o akisoma hotuba ya ufunguzi wa mafunzo ya taratibu za uchukuaji wa maelezo ya ungamo (Extra-Judicial Statements) kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo Dodoma.

 

Meza kuu ikiongoza na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo Dodoma Mjini waliohudhuria mafunzo hayo. Kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule na kushoto kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe Thurstone Kombe.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Jumapili, 19 Aprili 2026

BARAZA ELIMU YA SHERIA LAKAGUA MAZINGIRA UTOAJI ELIMU YA SHERIA VYUO VIKUU

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Dar es Salaam na REHEMA AWET-Mahakama, Mwanza

Baraza la Elimu ya Sheria nchini, chini ya Mwenyekiti, ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, hivi karibuni lilifanya ziara maalum, kukagua Vyuo Vikuu vitatu, kama sehemu ya juhudi za kuimarisha ubora wa elimu ya sheria nchini.

Wajumbe wa Baraza hilo walifanya ukaguzi katika Chuo cha Kimataifa Kampala, Chuo Kikuu Huria Tanzania na Chuo cha St. Augustine Mwanza.

Ziara hiyo ni sehemu ya mpango mpana wa Baraza la Elimu ya Sheria wa kutembelea na kukagua mazingira ya vyuo mbalimbali nchini ili kuhakikisha elimu ya sheria inatolewa kwa viwango vinavyokubalika na vinavyoendana na mahitaji ya jamii

Akizungumza wakati wa ziara hizo, Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria alisema kuwa lengo kuu ni kukagua na kuboresha mifumo ya ufundishaji, mitaala, pamoja na miundombinu inayotumika kufundishia sheria ili kuhakikisha wahitimu wanakidhi viwango vinavyotakiwa kitaifa na kimataifa.

Alisema kuwa Baraza la Elimu ya Sheria lina jukumu la kusimamia na kudhibiti ubora wa elimu hiyo nchini, hivyo ziara kama hizo ni muhimu katika kubaini changamoto na kuweka mikakati ya kuzitatua kwa kushirikiana na Taasisi husika.

Wakuu wa vyuo hivyo walipongeza ziara hiyo, wakieleza ni fursa muhimu kwao ya kubadilishana mawazo na kupokea ushauri utakaosaidia kuboresha utoaji wa elimu ya sheria.

Katika ziara hizo, Baraza pia lilipata nafasi ya kukutana na Wanafunzi wa kitivo cha sheria vyuoni hapo na kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili, pamoja na kupokea mapendekezo yao ya namna ya kuboresha mazingira bora ya kujifunzia ili kuweza kupatikana wanasheria bora.

Baraza pia lilipata wasaa wa kutembelea baadhi ya maeneo katika vyuo vikuu hivyo, ikiwemo Moot Court, Maktaba, Mabweni ya Wanavyuo, Ofisi za Viongozi pamoja na Walimu.

Aidha, Baraza hilo lilifanya mazungumzo na uongozi wa vyuo hivyo na kupokea taarifa ili kuona namna wanavyoweza kuboresha mitaala ili kuendana na soko la ajira.

Pamoja na hayo, Mwenyekiti wa Baraza alishauri namna bora ambayo inaweza kusaidia uhusiano mzuri kati ya vyuo hivyo, Mahakama na Taasisi mbalimbali za elimu katika kuandaa Wanafunzi bora na wenye tija katika soko la ajira.

Mapokezi ya Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini katika Chuo Kikuu cha Kimataifa Kampala.

Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria pamoja na Wanafunzi wa Chuo Kikuu Kampala.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani (katikati), Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kimataifa Kampala, Prof. Honoratha Mushi (tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini.

Mapokezi ya Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini katika Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria pamoja na Uongozi wa Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini akitembelea Maktaba ya Chuo Kikuu cha St. Augustine.

Mwenyekiti wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini, Mhe. Dkt Mustapher Mohamed Siyani (katikati), Mkuu wa Chuo cha St. Augustine, Padre. Prof. Juvenalis Asantemungu (tatu kushoto) pamoja na Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Sheria nchini.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

 

Jumamosi, 18 Aprili 2026

ENDELEENI KUWA WANYENYEKEVU HATA BAADA YA MAFANIKIO: JAJI MKUU

Na WAANDISHI WETU, Mahakama -Serengeti Mara

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. George Masaju, amewataka waumini wa Kanisa la Waadventista Wa Sabato na Watanzania wote kwa ujumla kuendelea kuwa wanyenyekevu hata baada ya kubarikiwa na kupata mafanikio, hivyo wanapaswa kuendeleza uhusiano wao mzuri na Mungu.

Mhe. Masaju ameyasema hayo akiwa Mgeni Maalum katika Hafla ya Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wa Sabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati, iliyofanyika leo tarehe 18 Aprili, 2026 katika Kijiji cha Musati Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.

“Ninayo furaha kubwa sana leo kukutana nanyi, jambo hili ni kubwa wengi wetu Mungu anapotubariki tunakuwa na kiburi kwahiyo hatua hii inaonesha jinsi ambavyo Mhe. Dkt. Nyansaho alivyo mnyenyekevu,”amesema Jaji Mkuu. 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Mhe. Masaju ametoa pongezi kwa waumini wa kanisa hilo pamoja na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho, ambao kwa dhati wameshiriki katika ujenzi wa kanisa hilo sambamba na kuendesha zoezi la kuchangia ujenzi wa shule na zahanati kijijini hapo.

Aidha, Jaji Mkuu amesisitiza kuhusu umuhimu wa kufanya kazi na kuwataka watu wafanye kazi kwa bidii wakijishughulisha na shughuli halali kama kilimo, uvuvi na ufugaji huku wakiilinda amani kwa sababu amani ikitoweka watu hawataweza kufanya shughuli nyingine za kiuchumi na kijamii.

Ameongeza kuwa uwepo wa kanisa hilo utasaidia katika kujenga jamii yenye umoja na amani kwani maovu yatakemewa jambo litakalohakikisha uwepo wa amani, usalama, ulinzi wa maadili pamoja na ulinzi wa mila na desturi za Kitanzania.

Kanisa hilo ambalo limezinduliwa na Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Hamis Ulega (MB) ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika hafla hiyo. 

Ujenzi wa Kanisa hilo umegharimu kiasi cha shilingi za kitanzania milioni 500.

Aidha katika Hafla hiyo, imeendeshwa harambee maalum ya kuchangia ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati ambapo Jaji Mkuu ameshiriki pia kuchangia katika zoezi hilo. 

Pamoja na Jaji Mkuu hafla hiyo ilihudhuriwa na Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Hamis Ulega (MB), aliyekuwa Mgeni Rasmi, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Jacob John Mkunda, Wakuu wa Mikoa ya Mara na Tabora, Wakuu wa Wilaya za mkoani Mara, baadhi ya Wabunge wa Mkoa wa Mara, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wilaya, Madiwani, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mara, Viongozi mbalimbali na Wananchi kwa ujumla ambao mwenyeji wao alikuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho. 

Mgeni Rasmi Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega (MB) (wa nne kushoto) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara. Kushoto kwake ni Mgeni Maalum Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, mwenye shati jeupe ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho pamoja na Viongozi wengine walioshiriki katika hafla hiyo.

Zoezi la uzinduzi wa Kanisa likiendelea.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.




Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akipokelewa katika viwanja vya Kanisa jipya ya Waadventista Wasabato alipowasili kushiriki katika Hafla ya Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.  











 Matukio mbalimbali katika picha Hafla ya Ufunguzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Musati Central na Harambee ya Ujenzi wa Shule pamoja na Zahanati leo tarehe 18 Aprili, 2026 Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara. 


MAHAKAMA DAR ES SALAAM YAOKOA ZAIDI YA MILIONI 60 KUTOKA KATIKA MATUMIZI YA KARATASI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam imefanya tathmini ya matumizi ya karatasi na matumizi ya kieletroniki na kubaini kuwa, imefanikiwa kuokoa zaidi ya Shilingi Milioni 64.

Hayo yamebainishwa jana tarehe 17 Aprili, 2026 katika Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Hatua hiyo ni moja ya Yatokananyo ya kikao kilichofanyika tarehe 18 Julai, 2025 ambapo moja ya maazimio ilikuwa ni kutathmini gharama zilizokuwa zinatumika kununua karatasi, wino pamoja na kalamu kabla ya Mahakama kuachana na matumizi ya karatasi (paperless) na kutumia njia ya mtandao.

Akitoa mchanganuo Mahakama Kuu pekee, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti amesema Mahakama hiyo imefanikiwa kuokoa shilingi 21,418,724/= kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2024/2025.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam imeokoa shilingi 21,496,555/= ikijumlisha na Mahakama zake zote za Wilaya yaani Ilala, Temeke na Kigamboni.

Kwa upande wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Bw. Manoti amesema imefanikiwa kuokoa shilingi 16,653,508 pamoja na Mahakama zake za Wilaya yaani Kinondoni na Ubungo.

Ameongeza kuwa, Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani imeokoa kiasi cha shilingi 9,200,000/= pamoja na Mahakama zake za Wilaya yaani Kibaha, Bagamoyo, Kisarawe, Mkuranga, Rufiji, Kibiti na Mafia.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amewapongeza Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Kanda hiyo na kueleza kuwa, amepokea pia pongezi kutoka Gereza la Mahabusu Segerea kwa utendaji kazi mzuri wa Kanda hiyo na kueleza kuwa, pongezi hizo sio zake ni za Wafawidhi maana wao ndio wana mashauri hayo na wamejitahidi kuyaondoa. Pamoja na pongezi hizo amewataka kukaa kwa amani.

Aidha, Mhe. Maghimbi amewatahadharisha wajumbe hao kuwa kuna viashiria vya mlundikano wa mashauri kukaribia hivyo, amewaomba kujitahidi kuyafanyia kazi mashauri hayo ili kuondokana na mlundikano ambao umekuwepo kipindi cha nyuma lakini kwa juhudi na mshikamano walifanikiwa kuyaondoa kabisa hivyo yasije kurudi tena. 

“Mwanzo wa mwaka waanze ndio wakati wa kupanga mikakati jinsi gani umeyazuia, unayachukua hayo yenye viashiria unayafanyi kazi vikao vya kuyasukuma ili mmalizane nayo,” alisema Jaji Maghimbi.

Katika jitihada za kuhakikisha huduma za Mahakama zinasogezwa karibu na wananchi, Jaji Mfawidhi huyo amewataka Wafawidhi kupitia Uongozi wa Serikali za vijiji kuomba kupatiwa viwanja vya kujenga Mahakama za Mwanzo kwa Kata zilizopo katika maeneo yao. Baadhi ya Wilaya ambazo tayari zimeshapata viwanja. Mhe. Maghimbi amewataka kufuatilia hati za maeneo hayo.

Sambamba na kikao hicho wajumbe wamepata fursa ya kujifunza kuhusu Mfuko wa Wekeza Maisha (UTT AMIS) na kujua faida zinazopatikana kupitia mfuko huo.

Miongoni mwa maazimio ya kikao hicho ni pamoja na kuandaa  ya uandishi wa muhtasari  wa vikao, Dira ya Taifa ya 2050 na huduma kwa wateja kwa Maofisa Mahakama Kanda ya Dar es Salaam, Kanda kuandaa mafunzo maalum kwa Maofisa  wa Mahakama  kwa ajili ya kuwajengea uwezo katika kusikiliza mashauri na uandishi wa hukumu, Mahakimu Wafawidhi kuwajulisha Mahakimu walio chini yao pamoja na Watendaji juu ya umuhimu wa  takwa la kisheria la kufungua akaunti maalum ya Mirathi, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, Maofisa Utumishi na Maofisa Tawala kufuatilia upatikanaji wa viwanja na hati kwa ajili ya Kata ambazo hazina Mahakama za Mwanzo.

Wajumbe wa Kikao cha Menejimenti cha Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam  wakifuatilia kikao hicho kilichofanyika jana tarehe 17 Aprili, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni.

Baadhi wa wajumbe wa kikao cha Menejimenti wakifuatilia somo kwa meneja masoko wa mfuko wa uwekeza wa Pamoja (UTT) Bi. Paskazia Charles (hayupo pichani).


Meneja Masoko wa Mfuko wa Wekeza Maisha (UTT) Bi. Pakazia Charles  akiwapa somo wajumbe wa Kikao cha Menejimeneti cha Mahakama Kanda ya Dar es Salaam.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikao cha Menejimenti, Mhe. Salma Maghimbi (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Livin Lyakinana (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu kanda ya Dart es Salaam, Bw. Sumera Manoti wakiwa katika kikao hicho.

Meza kuu wakiwa na katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam. Kutoka kushoto waliosimama ni Mhe. Aziza Mbadjo, Mhe. Hussein Mushi na  Mhe. Franco Kiswaga. 

 Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Kada mbalimbali wa Makhakama Kanda ya Dar es Salaam ambao ni wajumbe wa Kikao cha Menejimenti.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Mara)