Na. INNOCENT KANSHA & JAMES BUSANYA - Mahakama
Watumishi wa Mahakama ya
Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma leo tarehe Mosi Mei, 2026 wameungana na
wafanyakazi wa Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi kuadhimisha Siku ya
wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) katika Kiwanja cha michezo cha Jamhuri jijini
Dodoma.
Maadhimisho hayo yalianza
kwa Taasisi mbalimbali kushiriki kwenye maandamano huku wakiwa wamebeba Mabango
yenye kaulimbiu ya maadhimisho hayo isemayo “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara
kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050” matembezi
hayo yaliyoanzia kwenye viwanja vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
kuhitimishwa kiwanjani Jamhuri na kupokelewa na Mgeni Rasmi ambaye alikuwa Mkuu
wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule.
Akizungumza katika
maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, mgeni rasmi ambaye alikuwa Mkuu wa
Mkoa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amelishukuru Shirikisho la Vyama vya
wafanyakazi TUCTA kwa kumualika kushiriki katika kilele cha maadhimisho hayo,
huku akimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa juhudi zake za kuhimiza uwajibikaji na bidii kazini miongoni mwa
wafanyakazi.
Serikali imeendelea
kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha mazingira ya kazi kwa wafanyakazi nchini
ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kufikia malengo ya
maendeleo ya Dira ya Taifa ifikapo mwaka 2050.
Mhe. Senyamule amesema kuwa,
katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, Serikali imefanikiwa kutatua
changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi, huku ikiendelea kuboresha
miundombinu muhimu ya kurahisisha mfanyakazi kutoa huduma bora kwa jamii kama
vile upatikanaji wa umeme, ujenzi wa miundombinu ya majengo pamoja na
kuimarisha mawasiliano ya simu na intaneti.
“Serikali inaendelea
kuweka mazingira bora ya kazi ili kuwasaidia wafanyakazi kufanya kazi kwa
urahisi na ufanisi zaidi ili kuongeza tabasamu kwa wananchi,” alisema Mkuu wa
Mkoa huyo.
Aidha, alitoa wito kwa
wafanyakazi kushirikiana na Serikali kwa kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia
maadili ya utumishi wa umma, huku akisisitiza umuhimu wa Sekta binafsi kufuata
taratibu na sheria zilizowekwa ili kuboresha maslahi ya wafanyakazi.
Mhe. Senyamule akigusia
maelekezo ya Rais Samia amesema kuwa, alielekeza kuwapa tabasamu wananchi nanyi
Viongozi muwape tabasamu watumishi ili wafanyaka wawape tabasamu wananchi
wanaowahudumia kuendelea kuimarisha ustawi wa wananchi kwa kuhakikisha huduma
bora zinatolewa kwa usawa na kuepuka rushwa.
Aidha, Mhe. Senyamule
amesema kwamba, Mkoa wa Dodoma umetajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayonufaika
na uwekezaji wa Serikali hususan Vyuo vya elimu ya Juu. Mkuu wa Mkoa ametoa
wito kwa wafanyazi kujiendeleza kielimu kutokana na fursa hiyo.
Katika hatua nyingine,
wafanyakazi wametakiwa kuepuka vitendo vya rushwa na badala yake kuzingatia
uadilifu katika utoaji wa huduma kwa wananchi. Pia wamehimizwa kutenga siku
maalum za kusikiliza kero za wananchi ili kuboresha huduma.
Mkuu wa Mkoa huyo aliwatakia
wafanyakazi wote mkoani Dodoma maadhimisho mema ya Siku ya Wafanyakazi Duniani na
kuwataka kuendelea kushirikiana kwa ngazi zote kitaasisi katika kujenga Taifa
lenye maendeleo na ustawi.
Kwa
upande wake, Katibu wa Shirikisho la Vyama vya wafanyakazi Mkoa wa Dodoma Bw.
Albert Stanslaus akisoma risala ya wafanyakazi mbele ya
Mgeni rasmi amesema kuwa, licha ya juhudi za Serikali kuboresha maslahi ya
wafanyakazi nchini, bado kuna changamoto zinazoikumba Sekta ya ajira ambazo
zimeendelea kujitokeza, hususan katika sekta binafsi, ambapo wafanyakazi
wanalalamikia ukiukwaji wa haki zao za msingi.
Risala hiyo ya
wafanyakazi imebainisha mambo mbalimbali yaliyotajwa na wadau kwamba licha ya
hatua stahiki zilizochukuliwa na Serikali kutatua changamoto za wafanyakazi
lakini bado kuna matatizo yanayohitaji ufumbuzi wa haraka.
Bw. Stanslaus ameongeza
kuwa, kupitia risala hiyo wafanyakazi wanakumbwa na ucheleweshaji wa malipo ya
malimbikizo mbalimbali kama vile likizo, kupanda madaraja, huku wengine wakidai
kutokuwa na mikataba rasmi ya ajira, hali inayowafanya kukosa uhakika wa ajira
zao. Aidha, ilibainika kuwa kuna waajiri wanaolipa mishahara midogo isiyokidhi
viwango vinavyokubalika kisheria.
Changamoto nyingine
iliyotajwa ni kutowasilishwa kwa michango ya wafanyakazi kwenye mifuko ya
hifadhi ya jamii kwa wakati, jambo linalosababisha usumbufu mkubwa wanapohitaji
mafao yao pindi wanapostaafu au wanapopata matatizo.
Pamoja na hayo, washiriki
wa maadhimisho hayo walitoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa jitihada zake katika kuboresha mazingira ya kazi, ikiwa ni pamoja na
kupandisha mishahara kwa mwaka 2025, kupandisha watumishi madaraja na kulipa
madeni ya muda mrefu ya wafanyakazi.
Kupitia risala hiyo Katibu
huyo alisisitiza kuwa juhudi zaidi zinahitajika ili kuhakikisha haki za
wafanyakazi zinalindwa kikamilifu, hasa kwa kuimarisha usimamizi wa sheria za
kazi na kuwawajibisha waajiri wanaokiuka taratibu.

















