Jumanne, 14 Aprili 2026

WASHIRIKI WA MAFUNZO KIGOMA WAPITISHWA KWENYE SHERIA, KANUNI NA MIONGOZO YA USULUHISHI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile amewapitisha washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi kuhusu sheria, kanuni na miongozo ya usuluhishi inayotoa mwelekeo wa utatuzi na  utambuzi wa kiini cha mgogoro inayofikishwa Mahakamani.

Mhe. Rwizile ametoa mada hiyo leo tarehe 14 Aprili, 2026 mkoani Kigoma kwa washiriki 16 wa mafunzo ya  usuluhishi wa migogoro yanayoendelea Mahakama Kuu Kigoma. 

“Tunazo sheria, kanuni na miongozo ya usuluhishi inayotoa welekeo wa utatuzi na utambuzi wa kiini cha mgogoro inayofikishwa Mahakamani, hata hivyo zipo hatua nne muhimu za usuluhishi zikifuatwa na kuzingatiwa na msuluhishi yeyote basi mgogoro uliopo mbele ya msuluhishi utaleta matokeo mazuri,” amesema Jaji Rwizile.

Ameongeza kuwa, ni muhimu kwa Msuluhishi kuwa na ufahamu mkubwa wa kanuni za usuluhishi ili kufikia makubaliano ya usuluhisi wa mgogoro, na kwamba wasifungwe na uelewa mbalimbali unaotokana na kanuni, sheria na miongozo mingine inayotumika katika usuluhishi wa migogoro kutoka nchi mbalimbali duniani bali wajielekeze kwenye utatuzi wa mgogoro husika.

Kwa upande wake Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa amewasilisha mada juu ya utambuzi wa kiini cha mgogoro, ikiwa ni kuwasikiliza walengwa wa mgogoro, nini wanahitaji kila mmoja katika mgogoro huo, kisha kuwapa nafasi kila mdau kuweza kutoa mawazo ya kile anachohitaji katika kusuluhisha mgogoro huo, kuwapatia kila mmoja kile ambacho ataridhika nacho ili kumaliza migogoro iliyopo mahakamani.

Aidha, alifafanua mbinu mbalimbali wanazopaswa kutumia wasuluhishi hao ili kuendelea kuwa bora katika usuluhishi, hasa kutengeneza mazingira rafiki kwa walengwa wa mgogoro, mpangilio wa kuketi katika chumba cha usuluhishi, utoaji wa taarifa juu ya kila kitu kitakachofanyika katika usuluhishi, kuwaeleza malengo ya usuluhishi huo na jukumu lao la msingi katika usuluhishi, kuwatambua wadau wenye mgogoro husika bila upendeleo wala ubaguzi ikiwa ni sambamba na matarajio yao kupitia usuluhishi huo, kuwapa muda sawa wa kuzungumza, kujieleza na uwazi usio na mashaka.

Leo ni siku ya pili ya mafunzo kwa washiriki hao, wakiendelea kunolewa kwa ufasaha ili waje kuwa Wasuluhishi maridadi wa kutatua migogoro iliyopo hapa nchini.

Washiriki wa mafunzo hayo ni Mahakimu wa Kanda za Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.



Sehemu ya washiriki wa mafunzo  ya Usuluhishi wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikiwasilishwa na moja ya Mkufunzi wa mafunzo ya usuluhishi leo tarehe 14, Aprili 2026 Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akiwasilisha mada leo tarehe 14 Aprili, 2026 katika Mafunzo ya Usuluhishi yanayoendelea kufanyika Mahakama Kuu Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akisisitiza jambo wakati akiwasilisha mada kwa washiriki wa Mafunzo ya Usuluhishi leo tarehe 14 Aprili, 2026.

Washiriki wa mafunzo wakitoa mfano halisi wa jinsi Msuluhishi na Mdau wanaweza kukaa na kuzungumza juu ya jambo fulani linalohitaji usuluhishi.


Moja ya picha inayotumika na wakufunzi katika chumba cha kutolea mafunzo ya usuluhishi Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

JAJI MKUU AKUTANA NA RAIS MSTAAFU WA JAMHURI YA MALAWI

Na WAANDISHI WETU-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, leo tarehe 14 Aprili, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Malawi na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Dkt. Lazarus Chakwera, kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
















MAHAKAMA DODOMA YAANZA MAADHIMISHO YA WIKI YA USULUHISHI

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu, Dodoma

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, imeanza rasmi maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi yanayoendelea kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili, 2026, sambamba na Kanda nyingine nchini.

Maadhimisho hayo yanaenda sambamba na kaulimbiu isemayo, “Kutumia Njia Mbadala ya Utatuzi wa Migogoro kama Mbinu Inayopendelewa ya Kutatua Migogoro nchini Tanzania.”

Katika kipindi hiki, uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, ukiongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt.Juliana Masabo, umejipanga kuhakikisha Wananchi wanapata huduma kwa urahisi zaidi kwa kupokea na kusajili migogoro mbalimbali ikiwemo ya ardhi, ndoa na madai ya kawaida. Migogoro hiyo inapatiwa ufumbuzi kupitia Wasuluhishi waliobobea katika mbinu za usuluhishi.

Kwa upande mwingine, dawati maalumu la huduma limeanzishwa katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma kwa ajili ya kupokea malalamiko na kutoa mwongozo kwa Wananchi, huku mazingira maalumu yakiandaliwa ili kuhakikisha usuluhishi unafanyika kwa ufanisi na faragha.

Katika kuifikia jamii kwa upana zaidi, Mahakama pia imeendesha kampeni ya utoaji elimu kwa umma kupitia vyombo vya habari, ikiwemo Radio Mwangaza na Radio Family FM, ambapo Wananchi wameelimishwa juu ya umuhimu wa kuchagua usuluhishi kama njia ya haraka, nafuu na yenye tija katika kutatua migogoro.

Wananchi waliojitokeza kushiriki maadhimisho hayo wamepata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu dhana ya usuluhishi, kuuliza maswali na kupata majibu ya kitaalamu kuhusu masuala ya kisheria yanayohusu utatuzi wa migogoro nje ya mfumo wa kawaida wa Mahakama.

Kwa ujumla, Wiki ya Usuluhishi siyo tu jukwaa la kutoa elimu, bali ni fursa muhimu kwa jamii kubadili mtazamo kuhusu namna bora ya kushughulikia migogoro yao. Kupitia njia ya usuluhishi, Wananchi wanahimizwa kuchagua amani, maelewano na suluhisho la haraka badala ya migogoro mirefu inayoweza kuleta madhara kwa pande zote.

Mahakama ina matarajio kuwa Wananchi wataendelea kujitokeza kwa wingi kutumia fursa hii adhimu, siyo tu wakati wa maadhimisho haya, bali hata baada yake, kwa lengo la kujenga jamii yenye mshikamano, haki na ustawi wa kudumu.

Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiwa katika picha ya pamoja pamoja na Viongozi wa Dodoma baada ya kutembelea dawati maalumu lililowekwa kwa ajili ya Maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.  Katikati ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Kirefu, anaefuatia kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe Abraham Mwampashi, anaefuatia wa kwanza kulia kwake Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe Mustafa Ismail, wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo, wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, wa tatu kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Agatha Chugulu na wa nne kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitili.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe. Judith Baligenge akiwa katika studio za Radio Mwangaza iliyopo Jijini Dodoma akitoa elimu kuhusu usuluhishi.

 Wakili wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Mwita Mohere, akiwa katika studio za Radio Mwangaza iliyopo Jijini Dodoma akitoa elimu kuhusu usuluhishi.


 

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kongwa, Mhe. Sarah Mwalilino (wa kwanza kulia) akiwa ameambatana na Wakili wa Serikali Mwandamizi Wizara ya Katiba na Sheria, Bi Zerafina Gotora wakiwa katika Studio za Family Fm zilizopo Ilazo Jijini Dodoma wakitoa elimu kuhusu usuluhishi.

 

Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (katikati) na kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Mhe. Zabibu Mpangule na kushoto kwake ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Dodoma, Mhe. Thurston Kombe, wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa Wiki ya usuluhishi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

JAJI MFAWIDHI TANGA AONGOZA KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na MUSSA MWINJUMA-Mahakama, Tanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Katarina Mteule, jana tarehe 13 Aprili, 2026 aliongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi lililofanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Tanga.

Kikao hicho kilihudhuriwa na wajumbe wawakilishi kutoka sehemu mbalimbali ndani ya Kanda pamoja na wajumbe wengine waalikwa, wakiwemo Majaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Messe Chaba na Mhe. Happiness Ndesamburo.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Mteule aliwashukuru wajumbe wote kwa kufika pamoja na changamoto za mvua na kuharibika kwa mindombinu ya barabara. Aidha alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwenye kikao na kila Wilaya kupata uwakilishi.

“Baraza hili lipo kwa mujibu wa sheria na ni maelekezo ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Baraza ni sauti na ni lazima Watumishi wapate eneo au vikao rasmi kama hivi ili kutoa maoni ,ushauri na hata mapendekezo ya namna gani Taasisi yao inaweza kuendeshwa ili kuleta tija na matokeo Chanya,” alisema.

Aidha, Jaji Mfawidhi alisisitiza umuhimu wa Baraza kuwa ni kikao mahsusi kinachotoa fursa kwa Watumishi kujenga hoja za kiutendaji, kujua sera na mipango kupitia taarifa mbalimbali zitakazowasilishwa.

“Nawasihi sana kutoa maoni yenu kwa uhuru na maoni ya mnaowawakilisha hapa; usitoe maoni yako binafsi ukaacha ya wale unaowawakilisha, na ni vyema baada ya kikao hiki twende tukawape mrejesho wale wenzetu ambao hawapo hapa, hii itatusaidia kujenga mshikamano ,” alisisistiza Jaji Mteule.

Akizungumza Katika Baraza hilo, Ofisa Kazi Mwandamizi kutoka Idara ya Kazi jijini Tanga, Bi Diana Chacha, aliwaasa wajumbe juu ya usiri wa taarifa za Baraza na taarifa binafsi ndani ya kikao.

“Usiri wa Baraza ni muhimu sana kwa taarifa za Taasisi na taarifa binafsi, usitoe siri za Baraza kwani kinachoamuliwa kinabaki kuwa maazimo ya kikao,” alisema.

Taarifa mbalimbai za mashauri na kiutendaji ziliwasilishwa na wajumbe walipata fursa ya kujua hali ya mashauri pamoja na mipango ya baadaye ya Kanda kwenye masuala ya miundombinu, maslahi, afya za Watumishi na michezo.

Akifunga kikao hicho, Mhe. Mteule aliwashukuru wajumbe kwa michango yao mizuri yenye kujenga, lakini alitoa rai juu ya kujenga utamaduni wa kusikiliza hotuba za Viongozi wa Taasisi. Alisema kuwa ndani ya hotuba hizo kuna majibu ya maswali mengi ambayo huwa wanajiuliza bila kupata majibu.

“Najua mambo ni mengi, lakini nawaomba Watumishi tujenge utamaduni wa kusikiliza hotuba za Viongozi wetu ili kujua maboresho mbalimbali yanayofanywa kwa maslahi yetu kama Taasisi,” alisema.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Katarina Mteule, akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi.

Wajumbe waalikwa, Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Messe Chaba na Mhe. Hapiness Ndesamburo.

Ofisa Kazi Mwandamizi kutoka Idara ya Kazi Tanga, Bi. Diana Chacha, akiwasilisha mada ndani ya kikao cha Baraza.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tanga, Bw. Jumanne Msuta akiwasilisha taarifa ya utendaji mbele ya wajumbe wa Baraza.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Tanga, Mhe. Hudi Majid Hudi, akiwasilisha taarifa ya mashauri mbele ya wajumbe wa Baraza.


Baadhi ya wajumbe wa kikao cha Baraza wakimsikilzia Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Katarina Mteule (hayupo pichani).

 Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

WADAU WAJENGEWA UWEZO KUEPUKA KUTONESHA MAJERAHA KWA WAATHIRIKA WA UKATILI WA KINGONO

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma.

Mahakimu, Waendesha Mashtaka na Maofisa Ustawi wa jamii jana tarehe 13 Aprili, 2026 walipatiwa mafunzo ya namna ya kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kingono kabla ya kesi, wakati wa kutoa ushahidi mahakamani na baada ya kesi.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Marlin Komba, akifungua mafunzo hayo yanayotolewa katika ukumbi wa Mahakama Kuu Kanda ya Musoma, alisema mafunzo haya ni mahsusi kwa ajili ajili ya kuwajengea uwezo washiriki katika kushughulikia mashauri ya ukatili wa kijinsia kwa kuzingatia athari mbalimbali wanazopata wahusika, hasa za kiakili na kihisia.

Aidha, Mhe. Komba alisisitiza umuhimu wa washiriki hao kutumia weledi, lugha zenye huruma na staha pamoja na mbinu rafiki katika shughulikia mashauri ya unyanyasaji ili kutowajengea waathirika woga au kumbukumbu mbaya kutokana na majeraha waliyokwisha yapata hapo awali.

Mafunzo hayo ya siku tatu yatagusa maeneo mbalimbali, ikiwemo ushirikiano baina ya Taasisi katika kuwasaidia mashahidi walioko katika mazingira magumu, uelewa wa athari za kiakili na kihisia kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia pamoja na mbinu rafiki na salama za kuuliza maswali ili kuhakikisha utu na hisia za waathirika zinalindwa kuwaondolea woga wanapokuwa wakitoa ushahidi mahakamani.

Washiriki wa mafunzo hayo wametoka Wilaya za Simiyu, Maswa, Meatu, Busega, Sengeti, Tarime, Bunda, Rorya, Bariadi na Itilima.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda yaMusoma, Mhe. Marlin Komba akifungua mafunzo hayo kwa Mahakimu, Waendasha Mashtaka, Maofisa Ustawi wa Jamii yaliyohusu uwezo kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika wa ukatili wa kingono.

Hakimu Mkazi na Mratibu wa mafunzo kutoka Chuo cha uongozi wa Mahakama (IJA), Mhe. Gloria Shuma, akiwakaribisha washiriki wakati wa ufunguzi wa mafunzo haya.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (aliyesimama), akitoa neno wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.

Mwezeshaji, Mhe, Venance Mlingi (aliyesimama mbele) akielezea na kusisitiza jambo wakati wa mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia kwa umakini mada mbalimbali zinazoendelea kutolewa na wawezeshaji.

Ofisa Ustawi wa Jamii, Bi. Consolata Makomelo (aliyesimama) akiwasilisha mada wakati wa mafunzo hayo.

Muwezeshaji katika mafunzo hayo, Mhe, Nabwike Mbaba (aliyesimama) akiwasilisha mada kuhusiana na atahari za ukatili wa kinsia na kingono.

Wawezeshaji pamoja na washiriki wa mafunzo wakimsikiliza Mwananchi ambaye ndio mara yake ya kwanza kuingia mahakamani, Bi. Elizabeth Roman (aliyesimama kizimbani) aliyeshiriki katika igizo fupi, akielezea uzoefu alioupata kupitia tukio hilo ikiwa ni sehemu ya tathmini ya kujua namna waathirika wa matukio ya ukatili wavyojisikia wakati wa uendeshaji wa mashauri hayo.


Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Marlin Komba (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (kushoto), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia), wakiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji wa mafunzo hayo, Mhe. Venance Mlingi (aliyesimama kushoto) na Mhe. Nabwike Mbaba (aliyesimama kulia).

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Marlin Komba (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (kushoto), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia), wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki wote wa mafunzo hayo.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Marlin Komba (katikati), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (kushoto), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Monica Ndyekobora (kulia), akiwapamoja na sekretariet ya mafunzo hayo, Mhe. Gloria Shuma (aliyesimama kulia) na Mhe. Prisca Mkeha (aliyesimama kushoto).

Habari hii imeharriwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Jumatatu, 13 Aprili 2026

MBEYA YAZIDI KUIMARISHA UTENDAJI KAZI KWA NJIA YA TEHAMA

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga amekutana na wasaidizi wa kumbukumbu wa Mahakama Mkoa wa Mbeya na kufanya nao mazungumzo kuhusu masuala muhimu ya kazi ikiwemo nidhamu, uadilifu, matumizi ya mfumo mpya wa kusajili mashauri pamoja na utunzaji wa vielelezo.

Ameyasema hayo wakati wa kikao kazi hicho kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Mbeya. Mhe Tiganga alisisitiza kuwa, maadili ya utumishi wa umma na nidhamu kazini ndiyo msingi wa kazi za Mahakama. Aliongeza kuwa, utunzaji sahihi wa nyaraka na vielelezo ni jambo la msingi katika kuhakikisha haki inatolewa kwa wananchi bila vikwazo.

“Ni vizuri kuusoma mfumo wa kusajili mashauri na kuufanyia kazi, lakini pia tuongeze nidhamu na maadili kazini. Tunapaswa kuhakikisha tunatunza kumbukumbu vizuri pamoja na vielelezo ili kutokwamisha zoezi zima la utoaji haki kwa wananchi.” alisema Mhe. Tiganga

Naye, Hakimu Mkazi Mkuu kutoka Kurungenzi ya usimamizi, ukaguzi, Maadili na ufuatiliaji wa huduma za kimahakama kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Mhe. Mohamed Siliti alipata fursa ya kuongea na watumishi hao kwa njia ya mtandao.

Akitoa elimu juu ya utunzaji wa kumbukumbu za Mahakama Mhe. Mohamed Siliti aliwaasa watunza kumbukumbu hao kutimiza wajibu wao na kuepuka kutumia lugha zisizo za staha na nzuri kwa wateja.

Kupitia kikao kazi hicho kiliweka maazimio na kukubaliana kufanya kazi kwa ushirikiano na weledi mkubwa huku wakizingatia maadili na nidhamu kufuatia kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Aziza Temu, Mtendaji wa Mahakama Bi Mavis Miti, Maafisa Utumishi pamoja na wasaidizi wa kumbukumbu Mahakama Mkoa wa Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (katikati) akiongoza kikao kazi hicho cha wasaidizi wa kumbukumbu na nyaraka (kulia) ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Bi. Marvis Miti.

Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akitolea ufafanuzi sehemu ya mambo yaliyojadiliwa kwenye kikao hicho.

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Mmoja wa wajumbe akizungumza jambo katika kikao hicho Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama Kuu Mbeya Bi. Isabela Osiah

Mmoja wa wajumbe akizungumza jambo katika kikao hicho Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya wilaya Mbeya Bi. Queen Mapunda.

Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho
Sehemu ya wajumbe katika kikao hicho

Sehemu ya Maafisa Utumishi Mahakama Mbeya walioshiriki kikao kazi hicho.