Jumanne, 3 Februari 2026

JAJI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA RAIS WA MAHAKAMA YA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 03 Februari, 2026 ametembelewa na kufanya mazungumzo na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera.

Akizungumzia kuhusu lengo la kumtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Kayobera amesema lengo mojawapo ni kumsalimia na kumpongeza kwa kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania tangu Juni, 2025.

Aidha, Rais huyo wa EACJ amesema kuwa, anafurahishwa na ushirikiano ambao Mahakama hiyo inapata kutoka Serikali ya Tanzania na Mahakama kwa ujumla na kukiri kuwa, mazingira yaliyopo ya amani yanawawezesha kutekeleza majukumu yao kwa amani na utulivu.

Kadhalika, Mhe. Kayobera amemueleza Jaji Mkuu kwamba, katika kuhakikisha kuwa, Mahakama hiyo inaendelea kufanya kazi ipasavyo na kwa diplomasia, tangu alipoingia katika Mahakama hiyo mwaka 2021 aliweka Falsafa tatu muhimu ikiwa ni pamoja na Kufanya kazi kama Timu moja (Teamwork) ambapo amesema kuwa, Mahakama ni Taasisi ya pamoja na si ya mtu mmoja, hivyo ushirikiano wa Majaji na wadau wengine ni muhimu na huchochea ufanisi, uwajibikaji na utoaji haki kwa wakati.

Ametaja Falsafa nyingine kuwa ni Kutekeleza majukumu kwa nia njema (Good Faith) na kwamba tafsiri na utekelezaji wa Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ufanyike kwa uaminifu ili kuepuka mbinu za kukwepa haki kwa ujanja wa kisheria.

Rais huyo wa Mahakama ya Jumuiya Afrika Mashariki ameongeza kuwa, Falsafa nyingine anayotumia ni Mahakama kutekeleza mamlaka yake kwa hekima na busara (Judicial Diplomacy) lengo likiwa ni kudumisha mahusiano mazuri na Taasisi za Jumuiya na Nchi Wanachama, Kutoa maamuzi yenye nguvu kisheria lakini kwa lugha na mtazamo unaojenga ujumuishaji, si kuvunja wala kuyumbisha uhuru wa Mahakama, bali kusawazisha haki na uhai wa Jumuiya.

Kwa upande wake Jaji Mkuu amemuhakikishia Rais huyo wa EACJ kuwa, Mahakama ya Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano wa dhati katika utendaji kazi wake na kujenga mahusiano mazuri ya Mahakama hiyo na Mahakama ya Tanzania.

Mhe. Masaju ameonesha na kukiri kufurahishwa na ujio wa Mhe. Kayobera aliyeambatana na Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara, Msaidizi wa Rais wa  Jumuiya ya Afrika Mashariki, Wakili Nina Sokoine na Afisa Masjala Mkuu wa Mahakama hiyo, Bw. Mennas Mafwere na kuwaeleza kuwa wasisite kufanya mawasiliano wakati wowote wanapopata changamoto.

Kadhalika Jaji Mkuu ameikaribisha Mahakama hiyo kuja Mahakama ya Tanzania kufanyia vikao vyake kama ambavyo imefanya na kuendelea kufanya katika baadhi ya Nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Masharti.


Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera (kulia) akisaini kitabu cha wageni leo tarehe 03 Februari, 2026 alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju na katikati ni Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara.



Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Yohane Masara akisaini kitabu cha wageni leo tarehe 03 Februari, 2026 alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mazungumzo yakiendelea. Wa kwanza kushoto ni 
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju , wa kwanza kulia ni Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera, wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Yohane Masara na wa pili kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wakifuatilia mazungumzo kati ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe.George Masaju na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Mhe. Nestor Kayobera yaliyofanyika ofisini kwa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. Kutoka kushoto ni Msaidizi wa Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ), Wakili Nina Sokoine, anayefuata ni Afisa Masjala Mkuu wa Mahakama hiyo, Bw. Mennas Mafwere, Naibu Msajili wa Mahakama na Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi na Katibu Msaidizi wa Jaji Mkuu, Mhe. Clarence Mhoja.



‘MAHAKAMA INATOA MCHANGO KATIKA KUIMARISHA UCHUMI NCHINI’

Na EMMANUEL OGUDA, Mahakama-Shinyanga

Mahakama ya Tanzania imekuwa na inaendelea kushiriki katika kutoa mchango mkubwa katika kuimarisha uchumi wa Nchi kupitia usikilizwaji wa mashauri ya kimkakati yanayohusu kodi, benki, ardhi na uwekezaji ambapo kwa upande wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga ilisikiliza na kumaliza mashauri 84 kati ya 92 yaliyokuwepo katika Mahakama hiyo.

Hayo yalibainishwa tarehe 02 Februari, 2026 na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. John Kahyoza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ambayo kwa Kanda hiyo yaliadhimishwa katika viwanja vya Mahakama Kuu Shinyanga.

“Kwa upande wa Mahakama Kuu Kanda Shinyanga, tulikuwa na mashauri ya aina hiyo 92, yaliyoanza kusikilizwa kuanzia mwezi Oktoba hadi Desemba, 2025, tulikuwa tumesikiliza mashauri 84 na kubakiwa na mashauri nane tu hivyo kufanya Kanda yetu kutoa mchango katika maendeleo ya Taifa kwa kukwamua fedha zilizokuwa zimekwama Mahakamani kutokana na uwepo wa mashauri ya kikodi na uwekezaji,’’ alisema Mhe.Kahyoza.

Aidha, Jaji Kahyoza alisema kuwa, Mahakama itaendelea kutoa mchango katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuwa na Taifa lenye ustawi wa Haki hivyo, mchango wa Mahakama katika kufanikisha adhma hiyo unahitajika ili Taifa liwe na uchumi imara zaidi, jumuishi na shindani, uwezo wa watu wake pamoja na uhifadhi wa mazingira.

“Tunatarajia kufikia mwaka 2050, tutaendelea kuwa na Taifa lenye kuheshimu Utawala Bora, Taifa lenye amani, usalama na tulivu na Mahakama lazima tutimize lengo letu la utoaji wa haki mapema ipasavyo na kwa watu wote kuchochea maendeleo ya Taifa na kupunguza gharama na muda wa kutatua migogoro,’’ Jaji Mfawidhi huyo.

Naye Wakili wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Shinyanga, Bw. Lameck Merumbe alisema kuwa, ustawi wa Taifa lolote Duniani ni matokeo ya Mihimili yote mitatu kwa maana ya Serikali, Bunge na Mahakama kushirikiana pamoja, kwa upande wa Mahakama ina jukumu la kikatiba la kutafsiri sheria hivyo kuweka mazingira wezeshi ya kisheria na utekelezaji bora wa Sera za kitaifa.

Aidha, Bw. Merumbe alibainisha kuwa, Mahakama huru inahakikisha usawa, haki na maendeleo ya nchi kwakuwa Mahakama ni kichocheo cha ukuaji wa uchumi ambapo Mhimili huo huhakikisha Mikataba ya kibiashara inatekelezwa hivyo kusaidia Wawekezaji kuwa na Imani na uwekezaji wao sambamba na uwepo wa mifumo thabiti ya utatuzi wa migogoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mkoa wa Shinyanga, Wakili Shaban Mvungi alisema kuwa, Taifa linapokuwa na mfumo mzuri wa utoaji haki nchini, ustawi wa kiuchumi, kijamii na kisiasa huimarika, Mahakama ina jukumu la kulinda haki za msingi za wananchi kwa kutoa maamuzi huru bila upendeleo pamoja na kujenga mazingira rafiki kwa wawekezaji sambamba na kukuza shughuli za kiuchumi.

Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa upande wa Shinyanga yalihudhuriwa na wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo Watumishi wa Mahakama, wanafunzi kutoka shule mbalimbali pamoja na wananchi.

  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. John Kahyoza akisisiza jambo wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Shinyanga.

    
Wakili wa Serikali Mfawidhi Mkoa wa Shinyanga, Bw. Lameck Merumbe akiwasilisha salamu kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Shinyanga.

   Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mkoa wa Shinyanga, Wakili Shaban Mvungi akiwasilisha salamu za Chama hicho wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini iliyoadhimishwa tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Shinyanga.

  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga Mhe. John Kahyoza akikagua Gwaride maalum lililoandaliwa kuashiria kuanza kwa mwaka mpya wa Mahakama, 2026.

    Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. John Kahyoza akiwa tayari kwa ukaguzi wa Gwaride maalum kuashiria uzinduzi wa Mahakama mpya wa shughuli za Kimahakama kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika tarehe 02 Februari, 2026. Waliosimama nyuma ni Majaji, Mawakili na sehemu ya Wadau wengine wa Mahakama Kanda ya Shinyanga.

      Kikundi cha Burudani cha Sungusungu kutoka Kata ya Mwamalili kikitoa burudani wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Shinyanga.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Kanda ya Shinyanga wakiwa katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026 Mahakama Kuu Shinyanga.

    Picha ya pamoja kati ya mgeni rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. John Kahyoza meza Kuu  na watumishi wa Mahakama wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

JAJI MFAWIDHI MAHAKAMA KUU KANDA YA TABORA AONGOZA MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA NCHINI

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi ameongoza sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Tabora tukio ambalo limeashiria mwanzo rasmi wa shughuli za Mahakama kwa mwaka huu, 2026. 

Maadhimisho hayo yalianza kwa Viongozi wa Dini mbalimbali kufanya sala maalum, wakiombea amani na Mahakama kutekeleza vizuri jukumu la utoaji wa haki nchini.

Akihutubia wananchi, Wadau wa Sheria na Watumishi wa Mahakama waliojitokeza kwa wingi, Jaji Mfawidhi alisema Mahakama itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia misingi ya sheria, haki na utu wa mwanadamu ili kuendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya Taifa.

Kwa kutambua ukweli kuwa Mahakama ina nafasi kubwa katika kuchochea ustawi na maendeleo ya Taifa, tutahakikisha Mahakama inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia misingi ya sheria, haki na utu wa mwanadamu,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Upendo Wella ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya Tabora aliipongeza Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kwa kuimarisha ushirikiano na wadau wake muhimu katika mnyororo wa utoaji haki na hivyo kufanya jukumu zima la utoaji haki kufanyika kwa ufanisi mkubwa.

Mhe. Wella ameahidi kwamba, Serikali itaendelea kushirikiana na Mhimili wa Mahakama katika kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.

“Mahakama katika Kanda ya Tabora imeendelea kuimarisha ushirikiano na wadau wake muhimu katika mnyororo mzima wa utoaji haki na hivyo kufanya jukumu zima la utoaji haki kufanyika kwa ufanisi mkubwa. Napenda kuwaahidi kwamba, Serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa Mahakama kama ambavyo imeendelea kutoa ili kuhakikisha Mahakama inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi,” alisisitiza Mwakilishi huyo wa Mkuu wa Mkoa wa Tabora.

Naye Wakili wa Serikali wa Mkoa wa Tabora kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  Carson Nkya akihutubia katika hafla hiyo, alieleza kuwa Kaulimbiu ya mwaka huu inaonesha Mahakama inachangia ustawi na maendeleo ya Taifa kwa kuchochea ukuaji wa uchumi na uwekezaji, kulinda Utawala wa Sheria na amani ya kijamii, kuimarisha uwajibikaji na uwazi pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wote na kulinda haki za msingi za binadamu.

“Mahakama inatoa mchango mkubwa katika ustawi na maendeleo ya Taifa kwa kuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi na uwekezaji kupitia utekelezaji wa kisheria wa mikataba, ulinzi wa haki za mali na utatuzi wa migogoro kwa wakati. Mahakama inahakikisha utawala wa sheria na utulivu wa kijamii kwa kusimamia mgawanyo wa madaraka, kudhibiti matumizi mabaya ya madaraka ya Serikali, kulinda haki za msingi za binadamu na kudumisha amani katika jamii. Aidha, Mahakama inakuza uwajibikaji na kuzuia rushwa kwa kuhakikisha uwazi na utii wa sheria katika utekelezaji wa sera na maamuzi ya Serikali," alisema Wakili Nkya.

Aliongeza kuwa, Mahakama inawezesha maendeleo ya binadamu na jamii kwa kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wote, ikiwemo makundi yaliyo katika mazingira magumu pamoja na kutekeleza misingi ya kimataifa ya haki za binadamu na biashara, hivyo kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika Mkoa wa Tabora,  Wakili Kelvin Kayaga alitambua na kupongeza jitihada kubwa zinazofanywa na Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kwa kufanya kazi kwa kiwango cha juu cha taaluma, weledi na nidhamu ya kazi.

Ni vema tukatambua na kupongeza jitihada kubwa zinazofanywa na Mahakama Kuu - Kanda ya Tabora, Kanda yetu imeendelea kuonesha kiwango cha juu cha taaluma, weledi na nidhamu ya kazi.” alisema Wakili Kayaga.

Maadhimisho hayo yalipambwa na burudani mbalimbali ikiwemo Kikundi cha JKT Msange, Kikundi cha Ngoma za Asili cha Uaridi na Igizo lililoandaliwa na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Tabora.

Baada ya shughuli za Maadhimisho kukamilika, shauri la kwanza la mwaka wa Mahakama lilisikilizwa ikiwa ni ishara rasmi ya kuanza kwa shughuli za kimahakama kwa mwaka huu.

Maadhimisho ya Siku ya Sheria hufanyika kila mwaka nchini na hutumika kama jukwaa la kutafakari mchango wa Mahakama katika kujenga jamii yenye haki, amani na utawala wa sheria.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi akihutubia wananchi katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi  akikagua Gwaride la Heshima lililoandaliwa kuashiria kufunguliwa kwa rasmi kwa shughuli za Mahakama.

Watumishi wa Mahakama Tabora wakisakata rumba wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini tarehe 02 Februari, 2026.


Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa, Mhe. Upendo Wella ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria tarehe 02 Februari, 2026.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

MAHAKAMA KUU KANDA YA SIMIYU YAADHIMISHA SIKU YA SHERIA NCHINI, 2026

 ·       Jaji Mfawidhi asisitiza mwisho wa matumizi ya karatasi katika uendeshaji wa mashauri

Na NAUMI SHEKILINDI, Mahakama-Simiyu

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Simiyu, Mhe Wilbert Chuma amewaongoza watumishi wa Kanda hiyo na WanaSimiyu katika kuadhimisha Siku ya Sheria nchini 2026.

Mhe. Chuma ambaye alikuwa Mgeni rasmi katika sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria mkoani humo aliambatana na Mgeni Maalum Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha KATIKA sherehe hizo zilizofanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu.

Akizungumzia kuhusu Kauli Mbiu ya Siku ya sheria nchini, 2026 isemayo; ‘Mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa’ Jaji Mfawidhi alisema kuwa, Kauli Mbiu hiyo ina dhamira ya kutambulisha kwa umma nafasi ya Mahakama katika kuleta maendeleo na ustawi wa Taifa na kudhihirisha kuwa haki na maendeleo havitengani.

Mhe. Chuma alisisitiza kuwa, haki inapopatikana kwa wananchi kwa uwazi na kwa kufuata misingi ya sheria hujenga imani kwa Taasisi za Haki na kuweka mazingira bora ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Aidha, Mhe. Chuma alizungumzia juu ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuepukana na matumizi ya karatasi na kusema kuwa, “huduma za Mahakama kwa njia ya mtandao zimeimarishwa, hatua iliyosaidia kusogeza haki karibu zaidi na wananchi bila gharama kubwa za usafiri.”

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha alisisitiza watumishi wa Mahakama kuwa na uadilifu, weledi na uwajibikaji ili kuweza kutoa haki kwa wananchi.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Simiyu, Mhe. Elimo Massawe aliongoza wadau kwa ajili ya kwenda kusikiliza shauri la jinai la kwanza kusikilizwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu.

 

Hotuba nyingine zilitolewa na Viongozi kutoka Ofisi ya Mwendesha Mashtaka na Ofisi ya Mawakili wa Kujitegemea wote wakisisitiza kwamba Mahakama ndio nguzo ya maendeleo na maendeleo ndio azma ya Serikali ili kuleta ustawi na haki kwa jamii, vilevile walieleza kuwa, ustawi wa maendeleo ni matokeo ya Mihimili yote mitatu yaani Mahakama, Serikali Kuu na Bunge.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na watumishi pamoja na wadau kutoka Taasisi mbalimbali wakiwemo Wadau kutoka Ofisi ya Mwendesha Mashtaka, Mawakili wa Kujitegemea,Taasisi ya Kuzui ana Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), PSSSF, NHIF, TRA, Polisi, Uhamiaji na wananchi kwa ujumla.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Simiyu, Mhe.Wilbert Chuma akihutubia watumishi na wadau waliohudhuria sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026.

   Sehemu ya Wadau wa Mahakama waliohudhuria sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini wakiwa katika viwanja vya Mahakama Kuu Simiyu.

Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert Chuma (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na 
watumishi wa Mahakama Kuu Simiyu. Wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Elimo Massawe, wa kwanza kulia ni Mkuu wa Mashtaka Mkoa wa Simiyu, Mhe. Kainunula, wa pili kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha pamoja na wa kwanza kushoto ni Wakili wa Kujitegemea, Wakili Sabini.

Kwaya ya Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu wakitumbuiza mbele ya Mgeni Rasmi wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
   Gwaride tayari kwa ajili ya kukaguliuwa na Jaji Mfawidhi Mhe. Wilbert Chuma kuashiria ufunguzi wa mwaka mpya wa Kimahakama kwa mwaka 2026.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

'HALI YA MASHAURI YA MKOA NJOMBE YAENDELEA KUPUNGUA SANA'

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe na Mgeni Rasmi wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini mkoani humo, Mhe. Liadi Chamshama amesema hali ya mashauri imepungua kwa asilimia 85 ukilinganisha na miaka ya nyuma hali iliyotokana na kujiwekea Mpango Mkakati wa kuyamaliza mashauri kwa wakati kuanzia Mahakama za Mwanzo.

Mhe. Chamshama alibainisha hayo katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026 wakati  akizungumza na wageni waalikwa pamoja na wadau wa Mahakama walioshiriki katika sherehe hizo.

Mhe.Chamshama aligusia Dira ya Mahakama isemayo; 'Haki Sawa kwa Wote Mapema Ipasavyo,' na kusema kuwa, “Mahakama ikiwa ni mojawapo ya Mhimili wa Dola imekuwa ikitoa haki kwa wote bila kujali hali ya mtu kijamii au kiuchumi, kutochelewesha haki bila sababu ya msingi, kutenda haki bila kufungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi hivyo kutoa haki kwa wakati ili kuiwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shunghuli za kiuchumi kwa lengo la kujiongezea kipato cha mtu mmoja mmoja  na Taifa kwa ujumla kwa kufanya hivyo, Mahakama ina mchango mkubwa wa kukuza ustawi na maendeleo ya Taifa kiujumla.” 

Kwa upande wake Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe,  Bw. Richard Mbambe akizungumza wakati wa Maadhimisho hayo, aliwakaribisha wananchi na wadau wa Mahakama waliofika katika viwanja vya Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi jombe huku akiwajuza juu ya Kauli Mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu 2026 isemayo; 'Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa'.

Naye, Wakili wa Serikali, Mhe. Elise James alieleza kuwa, Mahakama ni Uti wa Mgongo wa Taifa kwa kuwa Dunia yote kwa sasa ipo katika vita vya Kiuchumi wa Kijiografia na ya kisiasa  kwa kuwa, kila Nchi  inachukua hatua za makusudi kutumia nguvu ya kisiasa au kiuchumi ama rasilimali za asili kama vile  hali ya hewa ya eneo kuhusiana na nchi nyingine katika kukuza na kuendeleza uchumi na kuleta maendeleo ya Taifa lake.

"Vilevile kumekuwepo na ushaidi wa kufunguliwa kwa miradi mikubwa hapa nchini katika sekta mbalimbali ikiwemo uchukuzi, ujenzi, nishati, madini na huduma za jamii na kadhalika hii ni ishara kuwa Serikali yetu kwa kushirikiana na Mhimili wa Mahakama na Bunge ni kuweka mazingira rafiki ya kuanzisha uwekezaji na hivyo kukuza uchumi na maendeleo ya Nchi yetu," alisema Wakili James.

Katika hatua nyingine, Kiongozi  wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mkoa wa Njombe, Bw. Innocent Kibadu alizungumzia kuhusu Kaulimbiu ya mwaka huu katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini isemayo, 'Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa.'

Aliendelea kusema kuwa, "hakuna maendeleo ya kweli bila ulinzi wa haki, Utawala wa Sheria na Misingi ya Utawala Bora na Mahakama ni moja ya Mhimili kati ya Mihimili mitatu ya Dola ambayo imeundwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhimili huu unatupa mwelekeo wa haki, uaminivu na utulivu wa Taifa pamoja na kuwepo na maslahi ya wananchi pasipo kuwepo upendeleo na kuleta matumaini kwa wananchi katika ustawi wa kiuchumi na maendeleo ya Taifa kiujumla."

Naye Mgeni Mahsusi Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Njombe,     Mhe. Joseph Rutashubilwa aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Njombe alisema kuwa, Serikali ya awamu hii imeweza kutambua mchango mkubwa unaoendelea kutolewa na Mahakama na kuendelea kusisitiza utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia falsafa ya kazi na utu kwa Mahakama na wadau wote wa Mahakama wana nafasi ya msingi ya kuhakikisha haki inatendeka kwa wakati na kwa  uwazi.

Mhe. Rutashubilwa aliwaeleza wananchi kuwa, kwa  kuzingatia utu wa mwananchi, Mkoa wa Njombe unathamini na kutambua  Mhimili wa Mahakama na Taasisi zote za Haki Jinai kwa kuwa na ushirikiano na mshikamano kwani ni  nguzo muhimu. Pamoja na hayo aliwataka wananchi wote watumie fursa ya Siku ya Sheria kujifunza masuala ya Kisheria.


Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama akihutubia mbele ya wananchi (hawapo katika picha) wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini. Nyuma yake ni kulia ni Mgeni Mahsusi Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Njombe, Mhe. Joseph Rutashubirwa pamoja na Viongozi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Njombe.

Sehemu ya Mahakimu, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitengemea, Watumishi na wananchi wakisikiliza hotuba zilizotolewa na Viongozi wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.



Mgeni rasmi ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe.Liadi Chamshama (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe. Matilda Kayombo (kulia), kushoto ni Mgeni Mahsusi Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Njombe, Mhe.Joseph Rutashubirwa wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini tarehe 02 Februari, 2026.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Bw. Richard Mbambe akizungumza wakati Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini mkoani humo.


Kiongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mkoa wa Njombe, Wakili 
Innocent Kibadu akihutubia mbele ya wananchi (ambao hawapo katika picha) jana tarehe 02 Februari, 2026 wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.

Mgeni Mahsusi Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Njombe, Mhe. Joseph Rutashubirwa  Mhe. Joseph Rutashubirwa akihutubia mbele ya wananchi (hawapo katika picha) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini tarehe 02 Februari, 2026.

Kwaya ya Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Njombe wakiburudisha kwa kuimba nyimbo maalum waliyoitunga inayohusu Haki na Utawala Bora.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma) 

 

JAJI MANYANDA ATOA RAI KWA WANANCHI KUSHIRIKI KATIKA UJENZI WA MAHAKAMA

Na.  Fredrick Mahava-Mahakama, Sumbawanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda ameongoza watumishi na wadau wa Mahakama kusherehekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini katika viwanja vya Mahakama Kuu Sumbawanga ikiwa ni ishara ya kuanza kwa mwaka mpya wa shughuli za kimahakama.

Akizungumza katika hafla hiyo jana tarehe 02 Februari, 2026, Mhe. Manyanda alitoa rai kwa wananchi Mkoa wa Rukwa kwa kushirikiana na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kushiriki katika ujenzi wa Mahakama hasa Mahakama za Mwanzo  kama Muze, Ilemba, Kate, WampembeKipande  ambazo hazina majengo ya Mahakama na zinaendesha shughuli zake kwenye ofisi za Kata na Maghala ya kijiji.

Mhe. Manyanda alisema Kauli mbiu  ya mwaka 2026 inasema “Mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa” inatukumbusha na kutuonyesha kuwa, ili Taifa liweze kusonga mbele kimaendeleo, Mahakama pia inayo nafasi ya kushiriki katika kuhakikisha hilo linafanikiwa na hivyo taifa linahitaji kuwa na Mahakama iliyo imara, huru na yenye kusimamia haki kwa mujibu wa mamlaka iliyopewa na Katiba.

Vilevile, Mhe. Manyanda amehimiza matumizi ya usuluhishi katika ngazi mbalimbali kwa lengo la kutatua migogoro mapema zaidi na kwa njia ambayo haithiri mahusiano ya wadaawa na hivyo kusaidia kujenga jamii yenye amani na kusisitiza juu ya matumizi ya mifumo mbalimbali kuanzia ngazi ya familia hadi Mahakama kuhakikisha kuwa migogoro inayoweza kutatuliwa kwa usuluhishi itatuliwe kwa njia hiyo.

Kwa upande wake, Mwanasheria Mkuu wa serikali, Bw. Mjahidi B. Kamugisha alisema kuwa, Mahakama kama mlezi wa Katiba, Mlinzi wa haki za binadamu na utawala wa sheria ni nguzo muhimu katika kukuza na kuendeleza ustawi na maendeleo ya Taifa. Mahakama iliyo huru na yenye kuheshimika na kuaminika huhakikisha utekelezaji thabiti wa mikataba, ulindaji wa haki za mali na kudhibiti matumizi  mabaya ya madaraka ili kukuza imani ya wawekezaji hivyo kuwezesha ukuaji imara na endelevu wa uchumi wa Taifa.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashitaka na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali zitaendelea kushirikiana na Mahakama katika kuhakikisha watu wote wanapata huduma kwa weledi ubora, uadilifu ili kiu ya kila anayekimbilia haki ikatimiekwa wakati.

 Kwa upande wake, Wakili kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Bi, Tunu Mahundi alisema kuwa, kwa sasa TLS inahudumia wananchi mbalimbali wanaohitaji huduma za Msaada wa Kisheria kwa wenye uhitaji na kuhakikisha wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za mawakili wanapata haki bila vikwazo katika ofisi zake zilizopo kwenye chapter 21 Tanzania nzima.

Vilevilie, aliipongeza Mahakama kwa kuendelea kuboresha Mifumo ya TEHAMA ambayo imewawezesha Mawakili kuweza kufanya shughuli zao mahali popote kwa kupitia mfumo wa e-Filing na Virtual court na pia TLS itaendelea kushiriki katika matukio mbalimbali yanayohusu utoaji elimu ya sheria kama vile wiki ya sheria, maonyesho ya sabasaba na kampeni ya msaada wa kisheria (Samia legal Aids)

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Bw. Makongoro Nyerere aliwashukuru na kuwapongeza Viongozi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga kwa Maandalizi mazuri ya Siku ya Sheria nchini na kuipongeza Mahakama kwa kuwa mstari wa mbele katika kutimiza Dira ya maendeleo ya Taifa na kuhimiza umuhimu wa wananchi kujitokeza kujenga Mahakama ili kusogeza huduma kwa Wananchi

Wadau waliohudhuria Maadhimisho ya kilele cha Siku ya Sheria nchini ni pamoja na Watumishi wa Kanda ya Sumbawanga, Mawakili wa Serikali, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Rukwa, Viongozi wa Dini, Wakuu wa Taasisi za Umma, TAKUKURU, Madalali wa Mahakama na Wasambaza Nyaraka za Mahakama na wananchi kutoka sehemu mbalimbali ya Mkoa wa Rukwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda akiwahutubia wadau wa Mahakama na wananchi mbalimbali waoshiriki katika kilele cha maadhimisho ya siku ya sheria nchini jana tarehe 2 Februari, 2026.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda akikagua gwaride maalum la uzinduzi wa siku ya sheria nchini.

Mwakilishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mkoa wa Rukwa Bw Mjahidi B. Kamugisha akitoa hotuba yake ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 mbele ya Wananchi na wadau waliohudhuria katika viwanja vya Mahakama Kuu Sumbawanga.

Mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Bi.Tunu Mahundi  akisoma hotuba  yake ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 mbele ya Wananchi na wadau waliohudhuria katika viwanja vya Mahakama Kuu Sumbawanga.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick K. Manyanda (Katikati), Mkuu wa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe, Makongoro Nyerere (Kushoto) na Katibu Tawala na Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya Mhe, Masinga (kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu 

Wakuu wa Taasisi mbalimbali, Viongozi wa Dini wakisiliza hotuba kutoka kwa Jaji mfawidhi, TLS na Mwakilishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

(Habari Hii Imehariri na Innocent Kansha - Mahakama)


 

MAHAKAMA KATAVI YAPONGEZWA KWA KUBORESHA MIUNDO MBINU YA UTOAJI HAKI

Na. Ally A. Ramadhani – Mahakama Katavi

Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mhe. Bi Jamila Yusufu Kimaro jana tarehe 2 Februari, 2026 alikuwa Mgeni Maalumu akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Hoza Mlindoko na kuhutubia katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini na kuipongeza Mahakama kwa kuanzisha miradi mbalimbali ya ujenzi na miundo mbinu ya Mahakama inayoendelea Mkoani Katavi.

Mhe. Bi. Kimaro aliitaja miradi mbalimbali inyoendelea mkoani Katavimfano, Vituo vya Mahakama za Mwanzo kama vile Mamba, Sibwesa, Ugalla na Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi ambavyo kwa wastani ujenzi unaendelea kukamilika.

Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya ya Mpanda alisema “kukamilika kwa miradi yote ya ujenzi wa Mahakama inayoendelea mkoani Katavi itasaidia kwa kiwango kikubwa hasa kwa upande wa gharama za wananchi kutumia umbali mrefu kutoka eneo moja kwenda jingine akitolea mfano; kutoka Katavi kwenda Sumbawanga kwa ajili ya kusikiliza mashauri yao yanayoendelea Mahakama Kuu, pia kupunguza mashauri ya mlundikano (Backlog) pamoja na muda wa kumaliza mashauri kupungua”.

Kwa upande wake, Wakili wa kujitegemea Bw. Lutende Masinde akihutubia kwa niaba ya Mwenyekiti wa chama cha Mawakili Tanganyika Mkoa wa Katavi Bi. Sekela Amulike aliongeza kuwa, “Kutokana na kauli mbiu ya mwaka huu inayosema Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa, Mahakama inawajibu wa kulinda Haki na Wajibu kwa wananchi, hii itasaidia kutatua migogoro miongoni mwa wananchi, hivyo kuongeza uzalishaji kwa Taifa,” aliongeza Bw. Masinde.

Kama ilivyo Moja ya nguzo katika Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ni utoaji haki kwa wakati. Mahakama inatekeleza mpango huo kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mhe. Bi Jamila Yusufu Kimaro, ambaye ni Mgeni Maalum kwenye Maadhimisho ya siku ya Sheria nchini 2026 alipokuwa akiwahutubia wananchi na wadau mbalimbali wa Mahakama mkoani Katavi.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama mkoani Katavi wakitoa burudani kwenye Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini

Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi Mhe. Gway K. Sumaye na Mgeni Rasmi wa Sherehe za Maadhimishi ya Siku ya Sheria nchini akitoa hotuba ya siku hiyo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)