Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe
Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Mkoa
Songwe wamefanya kikao cha kutathmini utendaji kazi pamoja na kukuza malezi ya
kitaaluma, kubadilishana uzoefu na kuwakaribisha wananchama wapya, kikao kazi
hicho kilifanyika katika ukumbi wa Simple Palace uliopo mji wa Vwawa wilayani
Mbozi.
Katika kikao hicho, Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe
Mhe. Magreth Kannonyele alimkaribisha Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo
ya Songwe Mhe. Gabriel Pascal Malata ambaye alitambulishwa kama mlezi wa Chama
cha TMJA Mkoa wa Songwe kwani Katiba ya TMJA inamtambua Jaji Mfawidhi kama
mlezi wa matawi yote yaliyo chini ya Masjala husika.
Sambamba na hilo, Mwenyekiti huyo alimkaribisha Jaji
wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha,
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde pamoja
na wanachama wengine wapya TMJA Mkoa wa Songwe.
Akiwasilisha taarifa ya Chama ya mwaka 2025/2026 Naibu
Katibu wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Ian Mnyigumba alisema Chama kilifanikiwa
kufanya safari za kitalii katika maporomoko ya Kalambo Mkoa wa Rukwa na Beach
ya Kasanga na baada ya safari hizo walifanikiwa kuchagua viongozi wa TMJA Mkoa
wa Songwe.
Aidha, Chama kilifanikiwa kutoa elimu kwa shule za Msingi
na Sekondari zikiwemo, Shule ya Msingi Nungwi iliyopo Wilaya ya Mbozi na Shule
ya Sekondari Tunduma iliyopo Halmashauri ya Mji wa Tunduma.
Vilevile, wanachama wa TMJA Mkoa Songwe walishiriki
kutoa Elimu ya usuluhishi wakati wa wiki ya suluhishi katika maeneo mbalimbali ya
Mkoa wa Songwe.
Mnamo Juni, 2025 TMJA Mkoa wa Songwe walishiriki
mafunzo ya utafiti wa Sheria “Legal
Research” chini ya
aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe.
Joachim Charles Tiganga, sambamba na hayo wanachama walifanikiwa kufanya
bonanza la michezo mbali mbali ikiwemo drafti na karata.
Vilevile, Chama cha TMJA Mkoa wa Songwe kilifanya
matendo ya huruma ikiwa ni pamoja na kutembelea Hospitali ya Halmashauri ya Mji
wa Tunduma na kutoa misaada mbali mbali kwa wagonjwa, Pia waliweza kutoa
misaada kwa mahabusu na wafungwa katika baadhi ya magereza yaliyopo Mkoa wa
Songwe.
Kuhusu ada ya uanachama Naibu Katibu Mhe. Ian
Mnyigumba alisema kuwa, michango hiyo hutumika kuendesha Chama cha TMJA Mkoa wa
Songwe ikiwa ni pamoja na kufarijiana pale mwanachama anapougua, anapofiwa,
anapouguliwa na kupongezana katika nyakati za furaha, aliendelea kusema kuwa
ada ya uanachama hutumika pia kama mtaji wa kuendesha miradi mbalimbali ya
Chama kama vile kutengeneza T-shirt, Kofia na Vikombe.
Mhe. Mnyigumba alisisitiza kuwa, wateja wakubwa wa
miradi hiyo yote ni wanachama wa TJMA Mkoa wa Songwe, pia alihimiza wanachama
kuendelea kununua bidhaa zinazotokana na miradi hiyo ili kukuza mfuko wa chama
hicho.
Aidha, kuhusu idadi ya wanachama Mhe. Mnyigumba
alisema kuwa, TMJA Mkoa wa Songwe ina jumla ya wanachama 32 wakiwemo Majaji
wawili, Naibu Msajili na Mahakimu wa ngazi mbali mbali.
Katibu wa chama TMJA Songwe alimuomba mlezi wa chama
hicho awasaidie katika kuhimiza wanachama kulipa ada zao kwa wakati kwasababu
ada ya uanachama ndio mapato pekee na pia ni mtaji wa kuendesha miradi mbalimbali
ya Chama.
Akielezea kuhusu mafanikio ya ubunifu wa miradi wa chama
cha TMJA Mkoa wa Songwe walifanikiwa kupata tuzo ya ubunifu bora wa miradi
kutoka TJMA Taifa kwenye mkutano uliofanyika Dodoma mwezi Junuari, 2025.
Akiwasilisha taarifa ya fedha na miradi mweka hazina
wa chama TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Martha Malima alisema kuwa, ada za uanachama
ziliwezesha miradi ya T-shirt, Kofia, Vikombe na Badge vyote vikiwa na nembo za
TMJA.
Mhazini wa Chama alisoma gharama na faida walizozipata
kutokana na miradi hiyo, pia alitaja
bidhaa zilizosalia na wanachama kwa pamoja walikubaliana kuzitoa baadhi ya
bidhaa kama zawadi kwa mlezi wa Chama ambaye ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu
Masijala Ndogo ya Songwe, Mhe. Gabriel Pascal Malata, Jaji wa Mahakama Kuu
Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu
Masijala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde.
Mhe. Martha Malima mhazini wa Chama TMJA Mkoa wa
Songwe alikabidhi tuzo ya ubunifu bora wa miradi waliyoipata mwezi Januari, 2025 kwa mlezi wa chama
TMJA Songwe.
Kwa upande mwingine wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe
kupitia kikao hicho waliridhia kufanya marekebisho ya katiba kutokana na
mapungufu waliyoyabaini kwenye katiba iliyopo. Wanachama walimchagua Mhe. Raymond
Kaswaga kama mjumbe wa kamati ya maboresho ya katiba ya chama cha TMJA Mkoa wa
Songwe na kila Wilaya ilichagua mjumbe mmoja ili kukusanya maoni ya katiba mpya.
Wajumbe kwa pamoja walikubaliana kuwa, mapendekezo
hayo yatawasilishwa meza kuu mwezi Agosti 2026, wajumbe wataamua kama wameyakubali
mabadiliko hayo ili mabadiliko ya katiba yaweze kwenda sanjari na hali ya sasa.
Mwenyekiti wa TMJA Mhe. Magreth Kannonyele na Mhe.
Abubakar Mrisha aliwashauri wajumbe waliochaguliwa kuisoma vyema na kuielewa
vizuri katiba iliyopo kabla ya kuanza zoezi la ukusanyaji wa maoni.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Songwe
Mhe. Gabriel Malata alitoa elimu kuhusu Applicability of Electronic Evidence in
Primary Court, aliwasisitiza wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe kuendana na
teknolojia kwasababu Mahakama Kuu ya Tanzania imeruhusu electronic evidence
kutumika mahakamani, ambapo kwa mara ya kwanza Commercial Court ilikubali
matumizi ya electronic evidence na sasa imeruhusiwa pia kutumika katika
Mahakama za Mwanzo.
“Sisi kama kama Mahakimu na Majaji tunalazimika kusoma
na kuielewa vilivyo sheria ya kimtandao Electronic Transaction Act ya 2015 ili
itusaidie katika kufanya maamuzi sahihi ya mashauri ya aina hiyo,” alisisitiza
Mhe. Malata.
Mhe. Malata aliwashauri wanachama wa TMJA Mkoa wa
Songwe watambue kuwa, kwa sasa Songwe imepewa mamlaka kamili hivyo ni wajibu wa
kila mmoja kutimiza majukumu yake ipasavyo.
Kwa upande wa Chama, Mhe. Malata alisisitiza kuwa,
kila mwanachama ana wajibu wa kutekeleza majukumu ya chama ikiwa ni pamoja na
kulipa ada za uanachama kwa wakati, kushiriki kikamilifu shughuli zote za chama
na kununua bidhaa za chama ili kuboresha mfuko wa chama.
Wanachama wa TMJA Mkoa wa Songwe, Mwenyekiti wa TMJA
Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kanonyele (katikati), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu
ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (wa pili kushoto), Jaji wa Mkuu
wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha ( wa pili kulia)
wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kikao hicho.
.jpg)
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala
Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (kushoto) na Jaji Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha wakiteta jambo wakiwa kwenye kikao cha
TMJA Mkoa wa Songwe.
Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele (kushoto) mara baada ya kukabidhi tuzo ya ubunifu bora wa miradi kwa mlezi wa TMJA Mkoa wa Songwe
ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe
Mhe. Gabriel Malata.
Sehemu ya wanachama waliohudhuria kikao cha TMJA Mkoa
wa Songwe.
Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele akipeana mkono na Jaji wa Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe
Mhe. Abubakar Mrisha wakati wa kumkabidhi zawadi.
Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele (kushoto) akimkabidhi zawadi Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya
Songwe Mhe. Joyce Minde (kulia).
Mwenyekiti wa TMJA Mkoa wa Songwe Mhe. Magreth Kannonyele
(aliyesimama) akifafanua jambo kwenye kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe.
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe
Mhe. Francis Kishenyi akiwa katika kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe akifuatilia mawasilisho.
Viongozi wa TMJA Mkoa wa Songwe wakiongozwa na
Mwenyekiti Mhe. Magreth Kannonyele (wa pili kushoto), Makamu Mwenyekiti Mhe.
Machumu G. Pamba (katikati), Mhazini wa Chama Mhe. Martha Malima (wa pili kulia), Mwakilishi TMJA Taifa Mhe. Linah Okello (wa kwanza kulia), na Kaimu Katibu wa
chama Mhe. Ian Mnyigumba (wa kwanza kushoto)wakiwa kwenye kikao cha TMJA Mkoa wa Songwe.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)