· Jaji Nongwa awasihi Maofisa Utumishi kujali Maslahi ya Watumishi
Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe
Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kuu
Kanda ya Njombe limefanya kikao chake huku Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo, Mhe. Victoria
Nongwa akiwaasa Maofisa Utumishi kujali maslahi ya watumishi walio chini yao
hasa katika stahiki zao zinazohusu malimbikizo ya mishahara pamoja na posho
wanazodai.
Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi
Mahakama Njombe kilifanyika tarehe 01 Aprili, 2026 ambapo Mhe. Nongwa alikuwa
Mwenyekiti na kuhudhuriwa na wajumbe kutoka Mkoa na Wilaya za Makete, Ludewa, Wanging’ombe
lilikutana kwa ajili ya kujadiliana masuala mbalimbali ya
kiutumishi pamoja na maslahi ya Wafanyakazi.
Jaji Nongwa alifungua kikao hicho kwa
kusoma ajenda mbalimbali pamoja na kufanya uchaguzi wa viongozi mbalimbali
waliopendekezwa na wajumbe wa Baraza hilo ambao walipigiwa kura huku Msimamizi wa Uchaguzi
akiwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano.
Baada ya uchaguzi alipatikana Katibu wa
Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Njombe, Mhe. Isack Mlowe na Naibu Katibu wa
Baraza Kanda ya Njombe, Bi. Tumaini Jembe pamoja na Mjumbe wa Baraza Kuu Taifa,
Bw. Juma Nyenzi.
Wakati kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi
la kinaendelea zilitolewa hoja mbalimbali zilizoibuka za watumishi ambazo zilihusu
stahiki za wafanyakazi huku hoja nyingine zikijibiwa papo kwa hapo na hoja
nyingine zikichukuliwa kwa ajili ya kwenda kuziwasilisha kwenye Baraza Kuu la Taifa
la Mahakama ya Tanzania.
Mhe. Nongwa pamoja na Mtendaji wa
Mahakama Kuu Njombe, Bw. Richard Mbambe akiwa Katibu wa mpito wa Baraza la Wafanyakazi
walihimiza Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) ambacho kiliwakilishwa na Kaimu Katibu
wa TUGHE Mkoa wa Njombe, Bi. Zenaida Sanjo kutoa elimu kwa watumishi waliopo
Mahakama za Mkoa wa Njombe na Mahakama za Wilaya Kanda hiyo juu ya umuhimu wa
kujiunga na chama hicho.
Bi. Sanjo alitoa neno la
shukrani kwa kushiriki katika mkutano huo na kutoa ahadi juu ya kuwapa elimu
watumishi wote juu ya umuhimu wa kujiunga na TUGHE.
Aidha katika mkutano huo, lilifanyika
zoezi kuchagua Mfanyakazi Bora wa Kanda ambapo lilifanyika kwa kushindanishwa kwa
watumishi wawili waliokuwa na sifa za ufanyakazi bora wote kwa pamoja wakiwa na
Vyeo vya Mwandishi Mwendesha Ofisi ambao walipigiwa kura kwa mara nyingine na hatimaye
mtumishi mmoja Bi. Deodatha Mhagama alipita kwa kupata kura nyingi.
Kabla ya kufungwa kwa kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Njombe viongozi mbalimbali waliohudhuria walitoa neno la shukrani.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe na Mwenyekiti wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akizungumza na wajumbe wa kikao hicho waliohudhuria (hawapo katika picha). Kulia ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Njombe, Mhe. Isack Mlowe na kushoto ni Naibu Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Njombe, Bi. Tumaini Jembe.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano (kulia) akisimamia zoezi la kuesabu kura za wajumbe waliopiga kura (hawapo katika picha). Katikati ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Ludewa Mjini, Mhe. Pius Ngosi Piusi na kushoto Mtunza Kumbukumbu wa Mahakama ya Mwanzo Makambako, Bi. Aneth Mfikwa.
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Tawi la Mahakama Mkoa wa Njombe, Bi. Happy Merere (kulia) akiwa na Afisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Njombe, Bi. Lusia Mpepo ambao ni Sekretarieti ya Mahakama Kuu Kanda ya Njombe wakisikiliza kwa umakini hoja mbalimbali za kiutumishi zilizokuwa zikitolewa kwenye kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kanda ya Njombe.
Kutoka upande wa kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe. Matilda Kayombo, katikati ni Mtunza Kumbukumbu wa Mahakama ya Mwanzo Makambako, Bi. Aneth Mfikwa na kushoto Kaimu Katibu wa TUGHE Mkoa wa Njombe, Bi. Zenaida Sanjo wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda hiyo.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


































