Ijumaa, 1 Mei 2026

SERIKALI ITAENDELEA KUBORESHA MASLAHI, MAZINGIRA YA KAZI KWA WAFANYAKAZI; MHE. SENYAMULE

Na. INNOCENT KANSHA & JAMES BUSANYA - Mahakama

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma leo tarehe Mosi Mei, 2026 wameungana na wafanyakazi wa Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi kuadhimisha Siku ya wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) katika Kiwanja cha michezo cha Jamhuri jijini Dodoma.

Maadhimisho hayo yalianza kwa Taasisi mbalimbali kushiriki kwenye maandamano huku wakiwa wamebeba Mabango yenye kaulimbiu ya maadhimisho hayo isemayo “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050” matembezi hayo yaliyoanzia kwenye viwanja vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuhitimishwa kiwanjani Jamhuri na kupokelewa na Mgeni Rasmi ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, mgeni rasmi ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amelishukuru Shirikisho la Vyama vya wafanyakazi TUCTA kwa kumualika kushiriki katika kilele cha maadhimisho hayo, huku akimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuhimiza uwajibikaji na bidii kazini miongoni mwa wafanyakazi.

Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha mazingira ya kazi kwa wafanyakazi nchini ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kufikia malengo ya maendeleo ya Dira ya Taifa ifikapo mwaka 2050.

Mhe. Senyamule amesema kuwa, katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, Serikali imefanikiwa kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi, huku ikiendelea kuboresha miundombinu muhimu ya kurahisisha mfanyakazi kutoa huduma bora kwa jamii kama vile upatikanaji wa umeme, ujenzi wa miundombinu ya majengo pamoja na kuimarisha mawasiliano ya simu na intaneti.

“Serikali inaendelea kuweka mazingira bora ya kazi ili kuwasaidia wafanyakazi kufanya kazi kwa urahisi na ufanisi zaidi ili kuongeza tabasamu kwa wananchi,” alisema Mkuu wa Mkoa huyo.

Aidha, alitoa wito kwa wafanyakazi kushirikiana na Serikali kwa kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, huku akisisitiza umuhimu wa Sekta binafsi kufuata taratibu na sheria zilizowekwa ili kuboresha maslahi ya wafanyakazi.

Mhe. Senyamule akigusia maelekezo ya Rais Samia amesema kuwa, alielekeza kuwapa tabasamu wananchi nanyi Viongozi muwape tabasamu watumishi ili wafanyaka wawape tabasamu wananchi wanaowahudumia kuendelea kuimarisha ustawi wa wananchi kwa kuhakikisha huduma bora zinatolewa kwa usawa na kuepuka rushwa.

Aidha, Mhe. Senyamule amesema kwamba, Mkoa wa Dodoma umetajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayonufaika na uwekezaji wa Serikali hususan Vyuo vya elimu ya Juu. Mkuu wa Mkoa ametoa wito kwa wafanyazi kujiendeleza kielimu kutokana na fursa hiyo.

Katika hatua nyingine, wafanyakazi wametakiwa kuepuka vitendo vya rushwa na badala yake kuzingatia uadilifu katika utoaji wa huduma kwa wananchi. Pia wamehimizwa kutenga siku maalum za kusikiliza kero za wananchi ili kuboresha huduma.

Mkuu wa Mkoa huyo aliwatakia wafanyakazi wote mkoani Dodoma maadhimisho mema ya Siku ya Wafanyakazi Duniani na kuwataka kuendelea kushirikiana kwa ngazi zote kitaasisi katika kujenga Taifa lenye maendeleo na ustawi.

Kwa upande wake, Katibu wa Shirikisho la Vyama vya wafanyakazi Mkoa wa Dodoma Bw. Albert Stanslaus akisoma risala ya wafanyakazi mbele ya Mgeni rasmi amesema kuwa, licha ya juhudi za Serikali kuboresha maslahi ya wafanyakazi nchini, bado kuna changamoto zinazoikumba Sekta ya ajira ambazo zimeendelea kujitokeza, hususan katika sekta binafsi, ambapo wafanyakazi wanalalamikia ukiukwaji wa haki zao za msingi.

Risala hiyo ya wafanyakazi imebainisha mambo mbalimbali yaliyotajwa na wadau kwamba licha ya hatua stahiki zilizochukuliwa na Serikali kutatua changamoto za wafanyakazi lakini bado kuna matatizo yanayohitaji ufumbuzi wa haraka.

Bw. Stanslaus ameongeza kuwa, kupitia risala hiyo wafanyakazi wanakumbwa na ucheleweshaji wa malipo ya malimbikizo mbalimbali kama vile likizo, kupanda madaraja, huku wengine wakidai kutokuwa na mikataba rasmi ya ajira, hali inayowafanya kukosa uhakika wa ajira zao. Aidha, ilibainika kuwa kuna waajiri wanaolipa mishahara midogo isiyokidhi viwango vinavyokubalika kisheria.

Changamoto nyingine iliyotajwa ni kutowasilishwa kwa michango ya wafanyakazi kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii kwa wakati, jambo linalosababisha usumbufu mkubwa wanapohitaji mafao yao pindi wanapostaafu au wanapopata matatizo.

Pamoja na hayo, washiriki wa maadhimisho hayo walitoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake katika kuboresha mazingira ya kazi, ikiwa ni pamoja na kupandisha mishahara kwa mwaka 2025, kupandisha watumishi madaraja na kulipa madeni ya muda mrefu ya wafanyakazi.

Kupitia risala hiyo Katibu huyo alisisitiza kuwa juhudi zaidi zinahitajika ili kuhakikisha haki za wafanyakazi zinalindwa kikamilifu, hasa kwa kuimarisha usimamizi wa sheria za kazi na kuwawajibisha waajiri wanaokiuka taratibu.


Mkuu wa Mkoa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule akihutubia alaiki ya wafanyakazi wa Taasisi mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi katika Siku ya Maadhimisho ya Wafanyakazi Duniani leo tarehe Mei, Mosi, 2026 katika kiwanja cha michezo cha Jamhuri jijini Dodoma.




Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa tayari kwa ajili ya matembezi ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani leo tarehe Mosi Mei, 2026 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa tayari kwa ajili ya matembezi ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani leo tarehe Mosi Mei, 2026 katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma.
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanashiriki matembezi na Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi ikiwa ni ishara ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanashiriki matembezi na Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi ikiwa ni ishara ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani.
Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanashiriki matembezi na Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi ikiwa ni ishara ya kuadhimisha Siku ya Wanyakazi Duniani
Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kuhitimisha matembezi 

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Makao Makuu jijini Dodoma wakiwa wanapita mbele ya Mgeni Rasmi kwa mbwembwe na bashasha wakati wanaingia uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

 

 

MSIWE CHANZO CHA MAFARAKANO NA CHUKI KWA JAMII; JAJI SALMA MAGHIMBI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Msata

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amewataka watumishi wa Mahakama Mkoa wa Pwani kutokuwa chanzo cha mafarakano na chuki kwa jamii.

Mhe. Maghimbi ameyasema hayo jana tarehe 30 Aprili, 2026 alipokuwa akifungua jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata lililopo Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani.

Akizungumza wakati akitoa hotuba yake Jaji Maghimbi amesema jengo hilo ni nyumba ya haki na kuleta amani kwenye jamii hivyo watumishi wasiwe chanzo cha mafarakano na chuki kwenye jamii.

“Tumekabidhiwa kwa Mwenyezi Mungu sisi na jengo, hivyo; tujue anatuangalia na kutuonya tabia na matendo yetu mema na mabaya yatawekwa kwenye mizani, tutende yaliyo mema na yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu,” alisema Jaji Mfawidhi huyo.

Katika hotuba yake, Mhe. Maghimbi ameeleza kuwa, katika Wilaya ya Bagamoyo kuna Mahakama za Mwanzo saba ikiwemo Mahakama ya Mwanzo Msoga- Lugoba ambayo siku za hivi karibuni jengo lake lote liliungua kwa moto, hivyo upelelezi unaenddelea kubaini chanzo cha moto huo.

Kupitia ufunguzi wa jengo hilo pia, Mhe. Maghimbi amewaarifu na kuwatangazia wananchi wote  kuwa, huduma za Mahakama ya Wilaya Bagamoyo zilizokuwa zikisogezwa na kutolewa katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Lugoba/Msoga zitaanza kutolewa katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata.

Aidha, Mhe. Maghimbi amesema kujengwa kwa jengo hilo la Mahakama ya Mwanzo Msata siyo kwa bahati mbaya bali ni utekelezaji wa programu ya maboresho inayofanywa na Mahakama ya Tanzania kupitia Mpango Mkakati wake ulioanza awamu ya kwanza mwaka 2015 hadi 2016 na awamu ya pili 2020 hadi 2025.

“Mpango Mkakati huu wa Mahakama unaongozwa na nguzo tatu za Utawala bora, uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali, upatikanaji wa haki kwa wakati na uimarishaji wa imani ya wananchi kwa Mahakama pamoja na ushirikishwaji wa wadau katika shughuli za Mahakama,” ameeleza Jaji Maghimbi.

Mhe. Maghimbi amesema Mahakama hiyo itahudumia wananchi wa maeneo ya Kata za Mbwewe, Kibindu, Msata, Mandesa na Kimange. Kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2022 ujenzi huo umeboresha huduma za Mahakama kwa wakazi zaidi ya 92,890 wanaoishi katika Kata hizo tano.

Kadhalika amewakumbusha wananchi kuwa, haki ndio msingi wa ustawi wa Taifa kwa kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kuongeza kwamba, ili shughuli yoyote ya kiuchumi iweze kufanyika  kwa ufanisi, inahitaji mazingira ya amani, utulivu, utawala bora, utawala wa sheria na mfumo rafiki wa utatuzi wa migogoro inapotokea. Kwa mantiki hiyo haki huinua Taifa.

Amesema pia kujenga jengo kama hilo ni jambo adhimu, lakini pia kulitumia jengo hilo katika kutoa huduma bora na zinazomlenga mwananchi ni jambo lingine.

Ametumia fursa hiyo, kuwajulisha kuwa, maboresho ya huduma za Mahakama hayajalenga tu majengo bali pia yamelenga kubadili mitazamo ya watumishi wa Mahakama katika kutoa huduma za haki kwa mtazamo wa zamani wa Mahakama inayotisha na sasa kutoa huduma za kimahakama zinazomlenga Mwananchi.

Katika hotuba yake amesema programu ya maboresho ya Mahakama imeleta utamaduni mpya wa utoaji huduma wenye mitazamo ya utoaji haki kwa haraka, weledi, uwazi, ufanisi na unaomjali mwananchi (Citizen Centric Justice Delivery) ili mwananchi atumie muda wake mwingi kwenye uzalishaji wa mal ibadala ya kupoteza muda katika kutatua migogoro Mahakamani.

Amesema katika kuyafikia hayo watajipima kwenye Dira ya Mahaklama ya Tanzania isemayo “Utoaji Haki kwa Wote Mapema ipasavyo.’

Jaji Mfawidhi ametoa maelekezo muhimu kwa watumishi wa Mahakama kulilinda na kulitunza jengo hilo ili lidumu kwa muda mrefu na utunzaji huo uende sambamba na upandaji miti, jengo litumike katika kutoa huduma bora zinazoendana na utekelezaji wa maboresho yanayozingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo.

Ameongeza kuwa, Kituo hicho kinapaswa kuongezewa watumishi ili kiendane na kasi ya kuwahudumia wananchi pamoja na vitendea kazi vingine ikiwemo vifaa vya TEHAMA sambamba na kuimarisha weledi, uadilifu, uwazi, umoja na maelewano baina ya watumishi na wateja.

Kadhalika, Mhe. Maghimbi amewataka Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea kuhakikisha hawatakuwa kikwazo katika utoaji huduma za Mahakama hiyo kwa kuchelewesha haki bila sababu ya msingi ili kusaidia Mahakama kutoa huduma bora, kulinda na kutunza heshima na uhuru wa Mahakama.

Vilevile, Jaji Mfawidhi huyo ametoa rai kwa Viongozi wa Serikali  kusaidia kutoa huduma bora kwa kuweka mazingira wezeshi ua ulinzi na usalama katika jengo la Mahakama, kuisaidia Mahakama kupata maeneo mengine ya kujenga Mahakama mpya hususan katika Kata ambazo hazina Mahakama, kuwafikishia taarifa wananchi wa Kata zingine kuhusu kuanza kwa huduma za Mahakama ya Mwanzo Msata ili waitumie.

Kwa upande wa wananchi, Mhe. Maghimbi amewaomba kufikisha mahakamani migogoro yote inayohitaji kushughulikiwa  na Mahakama sambamba na kusaidia ulinzi wa jengo  hilo na mali za Mahakama ili zitumike kwa manufaa ya umma wa Watanzania.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo ametoa mwelekeo wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ya kuwa shughuli za utoaji haki za Kanda hiyo inasimamia Mikoa miwili ya Dar es salaam na Pwani na inasimamaia Mahakama za Hakimu Mkazi nne na Mahakama za Wilaya 12 na Mahakama za Mwanzo 54.

Pamoja na uzinduzi huo, mwezi uliopita Mhe. Maghimbi alizindua Mahakama mpya ya Wilaya ya Kigamboni inayoketi Somangila  iliyopo Mkoa wa Dar es Salaam, majengo mapya matatu ya Mahakama za Mwanzo ambazo ni Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Temeke inayoketi Mbagala, Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Mkuranga inayoketi Kimanzichana na Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Kibiti inayoketi Bungu. 

Amesema pia iko safari ya kufikisha huduma za Mahakama Mkoa wa Pwani na Mahakama za Mwanzo katika Kata za Talawanda, Pera, Vigwaza, Ubena Zomozi, Kimange, Mbwewe, Kibindu, Mandera, Mkange, Makurunge, Fukayosi, Mapinga, Yombo, Kiromo, Zinga, Nianjema, Kisutu, Lugoba na Magomeni. 

Naye Mhandisi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhandisi Francis Deogratius Upendo akitoa taarifa ya Mradi wa Mahakama ya Mwanzo Msata amesema, usanifu wa mradi wa Mahakama ya Mwanzo Msata umezingatia mazingira bora ya kufanyia kazi katika ofisi mbalimbali, urahisi wa kufikika na miundombinu wezeshi kwa makundi maalum.

Pia matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma na uendeshaji wa shughuli za Mahakama, ulinzi na usalama kwa watumiaji wa jengo pamoja na muonekano na taswira pekee ya Mahakama.

Akitoa salamu za Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya hiyo, Bi. Jesca  Samson amesema Mkuu huyo ametuma salamu za pongezi kwa Mhimili wa Mahakama kwa kuboresha maeneo ya kutolea haki wananchi wa Msata wamefurahi sana.

Baada ya ufunguzi wa Jengo la Mahakama hiyo, Jaji Mfawidhi Maghimbi pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Dar es Salaam, Mhe. Hamidu Mwanga, Mtendaji wa Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Sumera Manoti, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Pwani, Bw. Nestor Mujunangoma, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bagamoyo, Mhe. Yasinta Kingwala walipata wasaa wa kupanda miti katika eneo la Mahakama hiyo.

  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam akihutubia watumishi wa Mahakama, Wadau kutoka Taasisi mbalimbali na wananchi walioshiriki katika sherehe za uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata-Bagamoyo iliyofanyika jana tarehe 30 Aprili, 2026.


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (katikati). wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Hamidu Mwanga, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mhakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Livin Lyakinana na wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Jesca  Samson.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Livin Lyakinana akitoa utambulisho wa wageni waliohudhuria Sherehe ya Ufunguzi wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Bagamoyo inayoketi Msata.

Mhandisi wa Majengo wa Mahakama Kuu, Bw. Francis Deogratius Upendo akitoa taarifa ya mradi huo wakati wa hafla ya uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata lililopo Wilaya ya Bagamoyo.

Kikundi cha Hamasa cha Watumishi wa Mahakama Pwani wakitumbuiza wakati wa sherehe hizo.

Kwaya ya Mahakama ya Tanzania (Ng’aring’ari Quir one) wakiimba katika sherehe za ufunguzi wa Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya ya Bagamoyo inayoketi Msata. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi akikata utepe kuashiria ufunguzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata.


Jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata lililozinduliwa.

Kikundi cha Ngoma cha Tosuba kutoka Bagamoyo wakitumbuiza katika sherehe ya uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Msata-Bagamoyo.

Meza kuu katika picha ya pamoja na baadhi ya wananchi waliohudhuria sherehe za ufunguzi wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo Msata.


Meza kuu aktika picha ya pamoja na Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama Dar es Salaam na Pwani. Katikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu divisheni ya Biashara Mhe. Cyprian Mkeha, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Hamidu Mwanga, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili wa Mhakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Livin Lyakinana na wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Jesca  Samson.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



 

  


 

 


 



Alhamisi, 30 Aprili 2026

MSAJILI MKUU ASISITIZA WATUMISHI KUILINDA HADHI YA MAHAKAMA

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, amewaasa Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Musoma kuilinda hadhi ya Mahakama kupitia utendaji wao wa kazi na hata katika maisha nje ya kazi.

Mhe. Nkya alitoa wito huo jana tarehe 29 Aprili, 2026 alipofanya kikao kazi na Watumishi hao pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma.

Awali akifungua kikao kazi hicho, Mhe Nkya alisema yuko Musoma kwa siku tatu kwa ajili ya ufuatiliaji na tathmini ya shughuli mbalimbali za kimahakama ambazo zimefanyika katika baadhi ya Mahakama za Masjala Ndogo Musoma.

Vilevile kupitia kikao hicho, Mhe. Nkya aliwasisitiza Watumishi kupenda kujisomea ili kujiongezea maarifa ya vitu tofauti vitakavyoboresha utendaji wao wa kazi, afya na maisha kwa ujumla.

Kupitia kikao kazi hicho, Watumishi mbalimbali walipata nafasi ya kuwasilisha hoja, changamoto na mapendekezo ya maboresho mbalimbali ili kuboresha mazingira ya kazi, maslahi na huduma kwa mteja.

Aidha, pamoja na ufuatiliaji na tathmini ya shughuli mbalimbali za kimahakama Mhe. Nkya alikabidhi vifaa vya kazi ambavyo ni kompyuta mpakato kwa Majaji wa Mahakama Kuu Musoma.

Katika ziara hiyo, Msajili Mkuu ametembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mahakama ya Wilaya Musoma, Mahakama ya Wilaya Butiama, Mahakama za Mwanzo Musoma Mjini, Mukendo na Kukirango na kote alikopita ameongea na Watumishi wa maeneo hayo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyesimama) akiwasalimia watumishi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakati wa kikao kazi hicho.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Omary Kingwele (aliyesimama) akimkaribisha Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Mkurugenzi wa Ufuatiliaji, Ukaguzi na Mrejesho wa Huduma za Mahakama, Mhe. Maira Kasonde (wa pili kushoto) akichangia jambo wakati wa kikao kazi na watumishi wa Mahakama Musoma.

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakifuatilia kwa makini kikao kazi cha Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu Musoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma wakimsikiliza kwa makini Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya (aliyeketi mbele katikati) wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao kazi na Watumishi wa Mahakama Musoma.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Marlin Komba (kushoto) akipokea kompyuta mpakato kutoka kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kulia) alipokuwa katika ziara ya Mahakama Musoma.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Geita.

 

 

 

 

 

 

Jumanne, 28 Aprili 2026

WAJUMBE BARAZA LA WAFANYAKAZI KIGOMA KUWAJIBIKA IPASAVYO

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kutumia kikao hicho kama jukwaa muhimu la majadiliano ya wazi ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji wa waatumishi katika masuala ya kiutumishi.

Mhe. Rwizile aliyasema hayo hivi karibuni kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma wakati akiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Kigoma kilicholenga kujadili ustawi wa Watumishi, tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyopita na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Jaji Rwizile alisisitiza umuhimu wa Baraza kama chombo cha kushauri na kuimarisha mahusiano kazini kwa kuzingatia mkataba mpya unaolenga kuboresha maslahi ya mwajiri na watumishi wake.

Jaji Mfawidhi huyo alieleza kuwa, “Baraza hili lipo kisheria na mkataba mpya umejikita katika kujenga Taasisi yetu kwa pamoja, hivyo mawazo yenu ni msingi wa maboresho tunayoyahitaji katika usimamizi wa shughuli za usimamizi wa usikilizwaji mashauri katika Mahakama zetu.”

Hata hivyo, aliwajulisha wajumbe kuwa, kupitia kikao hicho kulikuwa na ajenda ya uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza kwa mujibu wa mkataba mpya wa Baraza la Wafanyakazi, hivyo aliwashukuru na kuwaaga Viongozi wa Baraza waliopita amba oni Mhe.  Victor Kagina, aliyekuwa Katibu na Bi. Naomi Chawe aliyekuwa Katibu Msaidizi wa Baraza hilo.

Zoezi la uchaguzi liliongozwa na Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro ambaye alisisitiza taratibu za uchaguzi kuwa wazi na shirikishi kwa wajumbe wote kwa  mujibu wa Mkataba.  

Baada ya zoezi la kupiga kura kukamilia, Msaidizi wa Kumbukumbu, Bw. Julius Manyanya alichaguliwa kuwa Katibu mpya wa Baraza hilo na  Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Mburalina Maira aliteuliwa kuwa Katibu Msaidizi na Bi. Naomi Chawe alichaguliwa kuwa Mwakilishi TUGHE Baraza la Wafanyakazi Taifa.

Katika tathmini ya utekelezaji wa maazimio ya kikao kilichopita, Baraza liliridhishwa kubaini kuwepo kwa hatua kadhaa zenye tija zinazoonesha juhudi za uongozi katika kuboresha ustawi wa watumishi na ufanisi wa utendaji kazi.

Aidha, Watumishi waliibua hoja ya kuchelewa kupandishwa madaraja, hususan kwa wale walio kwenye ajira za muda mrefu. Katika mjadala, ilisisitizwa kuwa, watumishi wanapaswa pia kujitahidi kujiendeleza kielimu ili kukidhi vigezo.

Wajumbe wa Baraza hilo wamesisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2025/2026, huku wakichukua hatua za haraka na za kimkakati kushughulikia mara tu changamoto zilizobainika ili kutatuliwa.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akitoa neno la ufunguzi wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kigoma kilichofanyika hivi karibuni.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala  Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (kulia) akimkabidhi Mkataba wa Baraza la Wafanyakazi Katibu wa Baraza mpya, Bw. Julius Manyanya mara baada ya kuibuka mshindi katika nafasi hiyo kwa kupata kura nyingi za kishindo kutoka kwa wajumbe.


Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Mahakama Kigoma wakifuatilia kwa makini mjadala ulikuwa ukiendelea wakati wa kikao cha Baraza hilo.


Ofisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanznaia Masjala Ndogo ya Kigoma, Bw. Festo Sanga akiwasilisha taarifa ya utendaji wa shughuli za kimahakama kwa mwaka 2025/2026.

Ofisa Kazi, Bw. Frank Kimaro akitoa ufafanuzi juu ya utaratibu wa uchaguzi wa Viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi wa  Mahakama Kigoma.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

MASHAURI 48 YA MAHAKAMA YA RUFANI KUSIKILIZWA MASJALA NDOGO MBEYA

Na. MWINGA MPOLI – Mahakama, Mbeya

Mashauri ya Rufaa 48 ya Ardhi, Kazi na Ndoa yanatarajiwa kumalizika katika kikao cha Uendeshaji wa Mashauri (session) katika Masjala Ndogo ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania mkoani Mbeya.

Kikao hicho kinachoendeshwa na Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, kikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye ambaye ameambatana na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Eliezer M. Feleshi na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Deo J. Nangela, wakisaidiwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Daudi P. Kinywafu pamoja na watumishi wengine wa Mahakama ya Rufani.

Akiongea katika kikao cha mapokezi, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Mkuye aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya unaongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim C. Tiganga kwa maandalizi na mapokezi mazuri. Alifafanua kuwa, ushirikiano kutoka kwa wadau na wahusika, utawezesha umalizaji wa mashauri hayo kama ilivyopangwa.

“Tunawashukuru sana kwa mapokezi na maandalizi mazuri ya kikao hiki kwa hakika tumefarijika sana na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu tunaamini kuwa mashauri haya yote tutayasikiliza bila kikwazo chochote,” alisema Mhe. Mkuye.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga ameahidi kutoa ushirikiano kwa kipindi chote ambacho Waheshimiwa hao watakuwepo Masjala Ndogo ya Mbeya kuendesha usikilizaji wa mashauri hayo ya Mahakama ya Rufani.

Kikao cha usikilizaji wa Mashauri hayo kimeanza jana tarehe 27 Aprili, 2026 na kinatarajiwa kuhitimishwa tarehe 22 Mei, 2026.

Mwenyekiti wa jopo la Majaji ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye akisaini katika kitabu cha wageni mara tu baada ya kuwasili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakiwa pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya wakisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili Masjala Ndogo Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho kwa waheshimiwa Majaji hao mara baada ya kuwapokea.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Daudi kinywafu (wa pili kushoto kushoto), Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya Mhe. Aziza Temu (kulia), Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya Mhe. Judith lyimo (wa kwanza kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti wakishiriki mapokezi hayo.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.

Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Rehema K. Mkuye wakisalimiana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Pamoja na watumishi mbalimbali.



WANACHAMA TMJA TAWI LA RUKWA WAFANYA KIKAO KAZI, MAFUNZO

Na. SHARIFU MOKIWA -Mahakama, Sumbawanga 

Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (Tanzania Magistrates and Judges Association (TMJA) Tawi la Rukwa walikutana hivi karibuni na kufanya kikao maalumu kilicholenga kuimalisha ushirikiano wa kitaaluma, kujadili maendeleo ya chama ili kujenga mshikamano miongoni mwa wanachama. Kikao hicho kilifanyika katika ufukwe wa Kasanga ziwa Tanganyika.

Akizungumza wakati wa kufungua kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda alisisitiza umuhimu wa umoja, ushirikiano na ushiriki wa wanachama katika kuimalisha utendaji wa Chama pamoja na utoaji wa haki kwa jamii.

Wakati wa kikao hicho Baraza Tendaji la TMJA Tawi la Rukwa lilipokea taarifa mbali mbali ikiwemo tarifa ya uimarishaji wa Tawi, taarifa ya mwakilishi wa TMJA pamoja na taarifa ya Mhazini wa Tawi ambapo wanachama walipata nafasi ya kujadili maendeleo yaliyofikiwa pamoja na changamoto zinazokikabili Chama.

Aidha, majadiliano mbali mbali yalifanyika na maazimio muhimu kutolewa kwa lengo la kuimalisha Tawi na kuboresha ushirikiano wa wanachama katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Wanachama pia walipata mafunzo maalum kuhusu program ya Mentorship yaliyotolewa na Mhe. Manyanda, mafunzo hayo yalilenga kuongeza uelewa wa kitaaluma, kurejesha utendaji wa kazi pamoja na kujenga mazingira bora ya ushauri na uongozi ndani ya Taasisi.

Vilevile, baada ya kikao na mafunzo wanachama waliendelea na shughuli za utalii katika eneo la Kasanga, hatua iliyosaidia kuongeza ukaribu kujenga mahusiano bora ya kikazi pamoja na kuweka kumbukumbu nzuri za pamoja.

Kikao hicho kilihudhuliwa na   na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Pamela Mazengo pamoja na Mahakimu wa ngazi mbali mbali.

Picha ya pamoja ya Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Rukwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Frederick Kapela Mayanda akifungua kikao cha TMJA Tawi la Rukwa.

Wanachama wa TMJA Tawi la Rukwa wakiwa kwenye kikao wakifatilia na kusikiliza kwa makini taarifa zilizokuwa zikiwasilishwa.

Mwakilishi wa TMJA Tawi la Rukwa Mhe. David Mbembela (aliyesimama) wa Baraza la TMJA Taifa akiwasilisha taarifa wakati wa kikao

Sehemu ya Wanachama wakiwa katika Fukwe za ziwa Tanganyika ikiwa ni sehemu ya Utalii.

Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Rukwa (kulia) akimpa mkono wa shukrani wakati wa kumuaga Mhe. Elisha Daudi Mwasomola (kushoto) ambaye amehamishiwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Njombe.

Picha ya pamoja ya Wanachama wapya na waliohamia (TMJA) Tawi la Rukwa.                             


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Masjala ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Thadeo Mwenempazi (kulia) wakikata keki iliyoandaliwa na Chama cha (TMJA )Tawi la Rukwa.