Jumatatu, 22 Juni 2026

JAJI KIONGOZI ATEMBELEA MAHAKAMA YA WILAYA NYASA, GEREZA LA MBINGA

  • Azungumza na Watumishi
  • Afurahishwa na nidhamu ya Wafungwa, Mahabusu

Na FAUSTINE KAPAMA na Noel Daud-Mahakama, Songea

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, leo tarehe 22 Juni, 2026, ametembelea Mahakama ya Wilaya Nyasa na Gereza la Wilaya ya Mbinga, na kuzungumza na Watumishi, Mahabusu na Wafungwa.

Akiwa katika Mahakama ya Wilaya, Mhe. Dkt.  Siyani amepokea taarifa ya utendaji wa Mahakama hiyo, iliyowasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Osmund Ngatunga.

Kabla ya kuzungumza na Watumishi, Jaji Kiongozi alipokea pia changamoto zao na kuzitolea ufafanuzi na majawabu, ikiwepo upatikanani wa miundombinu ya majengo ya Mahakama ya Wilaya na Mahakama za Mwanzo.

Akizungumza na Watumishi hao, Mhe. Dkt. Siyani aliwakumbusha kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa bidii na uaminifu Kadiri inavyowezekana na kuzingatia maadili, huku matendo yao yakiakisi salamu ya Mahakama kuhusu uadilifu, weledi na uwajibikaji.

“Katika zama zetu hizi, kufanya kazi kwa haki ni njia mojawapo ya kulinda miundo mbinu yetu. Watu wasiporidhika na hukumu zenu, ndiyo matukio ya ajabu ajabu wakati mwingine yanatokea,” Jaji Kiongozi amesema.

Mhe. Dkt. Siyani amewataka pia Watumishi hao kutoa huduma kwa Wananchi kwa ufanisi zaidi ili kuongeza imani kwa Mahakama na kushughulikia kero zao zinazoletwa mahakamani mapema ipasavyo, kwani Mahakama ina mchango katika kutunza amani na usalama nchini.

“Hakuna sababu kwa Wananchi kuwa na wasiwasi na Mahakama yetu. Shughulikieni kero za Wananchi. Wananchi wanaleta kero mahakamani kwa njia nyingi, wengine kwa Mkuu wa Wilaya. Mtu ana dai nakala ya hukumu, mtu ana mirathi yake anazungushwa. Kila mmoja wetu ana wajibu wa kusaidia Mtanzania,” amesema.

Katika taarifa yake, Mhe. Ngatunga alieleza kuwa hapakuwepo na mashauri yaliyobaki kwa mwaka 2025, yaliyofunguliwa Januari hadi Juni, 2026 yalikuwa 208 na mashauri ambayo yamesikilizwa na kumalizika ni 200, yanayoendelea n inane.

Akizungumzia mashauri ya mirathi, ameeleza kuwa kwa kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Juni, 2026, Mahakama za Mwanzo zimefungua, kusikiliza na kufunga mashauri 11, huku katika Mahakama ya Wilaya yamefunguliwa mashauri ya mirathi 11, yamesikilizwa tisa na mashauri mawili bado kusikilizwa.

“Mashauri yote hayajafungwa kwa sababu muda wake wa kufunga bado. Ili kuhakikisha wasimamizi wa mirathi wanatekeleza wajibu wao kwa kufuata sheria, baada ya kuteuliwa kwao, tunawapangia kila mwisho wa mwezi wafike mahakamani kuelekeza namna wanavyoedelea na ukusanyaji na kugawa mali za marahemu,” amesema.

Akiwa kwenye Gereza la Wilaya, Jaji Kiongozi alipokea taarifa kutoka kwa Mkuu wa Gereza, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza, Afande Benjamin Masika, ambaye alionesha hali ya Gereza, idadi ya Mahabusu na Wafungwa.

Afande Masika pia alimwelezea Mhe. Dkt.  Siyani miradi mbalimbali inayotekelezwa na Gereza hilo, ikiwemo ufugaji wa samaki na ujenzi wa zahanati.

Baada ya kupokea taarifa hiyo, Jaji Kiongozi amewapongeza Mahakama katika Wilaya ya Mbinga na Nyasa pamoja na upande wa Mashataka kwa kazi nzuri ya kutekeleza sheria, ikiwemo kutozalisha Mahabusu wanaotoka Mahakama za Mwanzo.

Mhe. Dkt. Siyani pia amepongeza ubunifu unaofanywa na Gereza hilo katika maeneo mbalimbali na kushauri kuruhusu ushirikiano na Wadau, jambo litakalosaidia kuchochea maendeleo na kuondoa changamoto zilizopo.

Baada ya mazungumzo hayo, Jaji Kiongozi alikagua miradi hiyo na mazingira ya Gereza na baadaye kuzungumza na Mahabusu na Magereza na kisha kupokea changamoto zao na kuzitolea ufafanuzi na ufumbuzi.

Mhe. Dkt. Siyani ameonesha kufurahishwa na ukweli na nidhamu ya hali ya juu iliyooneshwa na vijana hao wakati wa mazungumzo hayo.

Jaji Kiongozi ataendelea na ziara yake ya kimahakama mkoani Ruvuma kwa kutembelea Magereza mawili ya Mkwaya na Kitai, yote yakiwa katika Wilaya ya Mbinga.

Katika ziara hiyo, Jaji Kiongozi ameambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mhe. Asha Waziri.

Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela, Mahakimu Wakazi Wfawidhi wa Mahakama za Wilaya ya Nyasa na Mbinga Songea na Watumishi wengine wa Mahakama Songea.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisalimiana na mmoja wa Watumishi alipowasili kwenye Mahakama ya Wilaya Nyasa mkoani Ruvuma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisaini kitabu cha wageni kwenye ofisi ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nyasa.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele (aliyesimama) akitoa utambulisho wa wageni mbalimbali walioambatana na Jaji Kiongozi. Aliyekaa ni Mtendaji wa Mahakama Songea, Bw. Allan Mwela.

Sehemu ya ujumbe ulioomgozana na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, ukiwa kwenye kikao na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nyasa.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama Wilaya ya Nyasa (juu na chini) wakiwa kwenye kikao hicho.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, aizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nyasa (hawapo kwenye picha).

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati). Wengine kutoka kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Dkt. Emanuel Kawishe, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songea, Mhe. James Karayemaha, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nyasa, Mhe. Osmund Ngatunga na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akisalimiana na mmoja wa Maafisa Magereza baada ya kuwasili kwenye Gereza la Wilaya ya Mbinga.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akiwa kwenye picha ya pamoja baada ya ukaguzi wa Gereza la Wilaya ya Mbinga.

 

JAJI MKUU WA TANZANIA AJITAMBULISHA RASMI KWA RAIS WA ZANZIBAR

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ya leo tarehe 22 Juni, 2026 amemtembelea Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kujitambulisha kwake rasmi na kufanya naye mazungumzo mafupi.

Yafuatayo ni matukio katika picha-Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipomtembelea na kufanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi-Ikulu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akimsalimia na kumkaribisha Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipomtembelea Ikulu Zanzibar leo tarehe 22 Juni, 2026.



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akizungumza na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipomtembelea Ikulu Zanzibar leo tarehe 22 Juni, 2026.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na   Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 22 Juni, 2026 alipomtembelea Rais Mhe. Dkt. Mwinyi Ikulu ya Zanzibar.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akisisitiza jambo leo tarehe 22 Juni, 2026 alipokuwa akizungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (hayupo katika picha).

Picha ya pamoja. Kulia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi na kushoto ni Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju. 

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Zanzibar)

 

 

 

FROF. OLE GABRIEL AKABIDHI RASMI OFISI KWA MTENDAJI MKUU MPYA WA MAHAKAMA

Na. JAMES BUSANYA & INNOCENT KANSHA - Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel leo tarehe 22 Juni, 2026 amefanya makabidhiano rasmi ya Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, kwa Mtendaji Mkuu Mpya Dkt. John Antony Jingu.

Akizungumza katika hafla hiyo ya makabidhiano ya Ofisi yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Prof Ole Gabriel alisema anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumwezesha kufikia siku hiyo muhimu ya kukabidhi ofisi baada ya kuitumikia Mahakama kwa miaka mitano kama Mtendaji Mkuu. Alieleza kuwa anathamini fursa aliyopewa ya kutoa maneno machache kabla ya kukabidhi rasmi majukumu hayo kwa mrithi wake.

Prof. Ole Gabriel aliongeza kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kumteua kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita. Alisema kuwa katika kipindi chote cha utumishi wake katika nafasi hiyo, Serikali alimpa ushirikiano na msaada mkubwa uliowezesha utekelezaji wa majukumu mbalimbali na kufanikisha mageuzi mengi ndani ya Mahakama.

Aidha, alimshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, pamoja na viongozi wote wa Menejimenti ya Mahakama kwa ushirikiano mkubwa waliompatia katika kipindi chote cha utendaji wake. Pia aliwashukuru aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bw. Emmanuel Tutuba, na Katibu Mkuu wa sasa, Dkt. Natu El- Maamry Mwamba, kwa ushirikiano wao mkubwa katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Mahakama.

Akizungumzia safari yake ya utumishi wa umma, Prof. Ole Gabriel alisema alianza kazi tarehe 1 Julai, 1991, na kwamba hadi anastaafu anahitimisha safari ya miaka 35 ya kulitumikia taifa. Aliwashukuru waajiri wake wote aliowahi kufanya nao kazi tangu alipoanza utumishi akiwa kijana wa miaka 20.

Vilevile, Prof Ole Gabriel aliwapongeza viongozi mbalimbali waliomlea na kumjengea uwezo wa kiutendaji, akiwemo Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Prof. Ibrahim Hamis Juma na Jaji Kiongozi wa wakati huo, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi, ambao walimfundisha mambo mengi kuhusu uongozi na utendaji ndani ya mhimili wa Mahakama. Hakuwasahau wazazi wake pamoja na familia yake, hususan mke wake Devotha na watoto wake, kwa msaada na uvumilivu waliompatia katika safari yake ya kazi.

Aidha, Prof. Ole Gabriel alisema kuwa, kustaafu ni jambo jema, lakini kustaafu kwa heshima ni jambo lenye thamani zaidi. Alisema hotuba ya Mheshimiwa Rais wakati wa kumuapisha Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama Dkt. John Anthony Jingu ilikuwa zawadi kubwa kwake kuliko hata fedha, unaposifiwa na kuagwa vizuri, kuna faraja na manufaa makubwa sana ndani yake kwa kuwa ilionesha kuthamini mchango wake katika utumishi wa umma kitu ambacho kilimpa faraja na heshima kubwa.

Katika hotuba yake, alimpongeza Dkt. Anthony Jingu kwa kuteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania na kuelezea kuwa, uteuzi huo umetokana na uwezo, uzoefu na utumishi wake wa muda mrefu katika nafasi mbalimbali za uongozi. Alieleza kuwa Mahakama imepata kiongozi mwenye uwezo wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana na kuimarisha zaidi utendaji wa Taasisi.

“Mheshimiwa Rais ametuletea mtu ambaye ana uelewa mpana na maarifa ya kiuongozi. Hawa viongozi waliopo mbele yako hapa leo, pamoja na watumishi wengine wote wanaofuatilia hafla hii kwa njia ya mtandao, ndiyo Timu ya Ushindi timu nzuri sana na mahiri ambayo nimekuwa nikiitumia kwa saa 24 kukamilisha majukumu ya mhimili huu. Timu iliyopo ndani ya Mahakama ni timu imara na yenye uwezo mkubwa, ambayo imekuwa msingi wa mafanikio yaliyopatikana katika kipindi changu cha uongozi. Aliwahimiza viongozi na watumishi wote wa Mahakama kuendelea kumpa ushirikiano Mtendaji Mkuu huyo Mpya kama mlivyonipa mimi,” alisisitiza Prof. Ole Gabriel.

Akieleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha uongozi wake Prof Ole Gabriel, alisema Mahakama imepiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma za haki. Miongoni mwa mafanikio hayo ni kuanzishwa kwa huduma za Mahakama Inayotembea, kuimarishwa kwa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), kuboreshwa kwa mifumo ya utunzaji wa kumbukumbu, kuongezeka kwa kasi ya usikilizaji wa mashauri, pamoja na kuimarishwa kwa uwezo wa ukaguzi wa Mahakama na pia kusimamia miradi mikubwa ya ujenzi wa miundombinu na kuboresha taratibu za utendaji kazi, mafunzo na nidhamu kwa watumishi.

Vilevile, Prof. Ole Gabriel alisisitiza umuhimu wa kuendelea kudumisha umoja na mshikamano kati ya Maafisa Mahakama na wasio Maafisa Mahakama. Pia alieleza umuhimu wa ushirikiano kati ya mihimili mitatu ya dola, akibainisha kuwa ushirikiano kati ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Katibu wa Bunge na Katibu Mkuu Kiongozi ni muhimu kwa maendeleo ya nchi na ufanisi wa Taasisi za umma.

Akizungumzia mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Prof. Ole Gabriel alisema Mahakama imepata ongezeko kubwa la bajeti ya maendeleo na matumizi ya kawaida, alieleza kuwa, rasilimali watu zimeongezeka kutoka watumishi 5,725 hadi zaidi ya watumishi 7,000. Mahakimu 377 wameongezeka, Majaji wa Mahakama Kuu wameongezeka kutoka 70 hadi 137, huku Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiongezeka kutoka 16 hadi 46.

Kwa upande wa miundombinu, Prof. Ole Gabriel alisema, Mahakama imepata maendeleo makubwa katika ujenzi wa majengo na makazi ya Majaji. Alibainisha kuwa jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililopo jijini Dodoma ni miongoni mwa majengo makubwa zaidi ya Mahakama duniani likiwa linashika nafasi ya sita na la kwanza barani Afrika.

Miundombinu hiyo, inajumuisha vituo Jumuishi vya utoaji haki sita vimejengwa katika mikoa mbalimbali ikiwemo Dar es Salaam, Morogoro, Mwanza, Dodoma na Arusha. Aliongeza kuwa usimamizi mzuri wa miradi hiyo umewezesha kuokoa zaidi ya shilingi bilioni tatu za Serikali.

Vilevile, Prof. Ole Gabriel amesema kuwa, kwa upande wa maslahi ya watumishi posho mbalimbali za watumishi zimeongezwa wakiwemo madereva na waendesha ofisi zimeongezwa na kuendelea kulipwa kwa wakati bila kuchelewa. Alitoa pongezi kwa Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji waliohusika katika kuhakikisha stahili za watumishi wa kada zote zinashughulikiwa kwa wakati.

Aliwataka watumishi wote wa Mahakama kuendelea kuzingatia nidhamu, uwajibikaji na maadili ya kazi yaliyokuwa msingi wa mafanikio ya Taasisi hiyo. Pia alimkumbusha Mtendaji Mkuu wa Mahakama Mpya Dkt. Jingu umuhimu wa kuendelea kuwajali na kuwasaidia Majaji wastaafu wanapohitaji msaada.

Aidha, Prof. Ole Gabriel alimhakikishia Dkt. Anthony Jingu kuwa ataendelea kumpa ushirikiano na ushauri pale utakapohitajika kwa maslahi ya Mahakama na Taifa kwa ujumla. Alimtakia Mtendaji Mkuu mpya utekelezaji mwema wa majukumu yake na mafanikio katika kusimamia mipango ya kimkakati ya Mahakama.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa nasaa zake wakati wa hotuba yake ya makabidhiano ya Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 22 Juni, 2026 jijini Dodoma.
Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Antony Jingu (katikati) akikabidhiwa nyezo na vitendea kazi vitakavyo mwongoza katika majukumu yake na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) huku zoezi hilo likishudiwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (kushoto) mara baada ya makabidhiano rasmi ya Ofisi leo tarehe 22 Juni, 2026 jijini Dododma. 

Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Antony Jingu (katikati) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (kushoto) wakimkabidhi Ua maalum lililoandaliwa kama zawadi kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel mara baada ya makabidhiano rasmi ya Ofisi leo tarehe 22 Juni, 2026 jijini Dododma. 

Meza Kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Antony Jingu (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa menejimenti ya Mahakama na sehemu ya watumishi wa Mahakama Makao Makuu.
Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Antony Jingu (katikati) akitia saini Kitabu cha wageni alipowasili ofisini kwake mara baada ya makabidhiano rasmi ya Ofis leo tarehe 22 Juni, 2026 jijini Dododma, wengine ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel (akulia) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel (akushoto) akipeana mikono kama ishara ya kuagana na Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Antony Jingu leo tarehe 22 Juni, 2026 walipokuwa wakifanya makabidhiano rasmi ya Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mstaafu Prof. Elisante Ole Gabriel (akulia) akipeana mikono na Mtendaji Mkuu Mpya wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Antony Jingu leo tarehe 22 Juni, 2026 walipokuwa wakifanya makabidhiano rasmi ya Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania. 

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)