Ijumaa, 11 Julai 2025

ASHANTI GOLD YAKABIDHI NYUMBA YA KUTUNZIA VIELELEZO MAHAKAMA KUU GEITA

Na. DOTTO NKAJA-Mahakakama, Geita

Kampuni ya Uchimbaji Madini Mkoa wa Geita (Ashanti Geita Gold Mine Limited) hivi karibuni ilikabidhi nyumba ya kisasa ya kutunzia vielelezo katika Mahakama Kuu Geita kama sehemu ya kurejesha huduma kwa jamii.

Kitendo hicho pia ni kutambua mchango mkubwa unaotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Geita, hasa katika utoaji haki kwa wakati na kupunguza malalamiko katika jamii.

Mradi huo uliokabidhiwa kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina ulijengwa na kampuni hiyo katika mwaka wa fedha (2024/2025) baada ya Mahakama kukabiliwa na ufinyu wa nafasi ya kutunzia vielelezo.

Makamu Rais wa kampuni hiyo barani Afrika, Bw. Simon Shayo, ambaye aliambatana na Meneja Mwandamizi eneo la Mahusiano ya Jamii, Bw. Gilbert Mwulia, Mkuu wa Kitengo cha Wanasheria, Bw. David Nzaligo na Maofisa wengine ndiye aliyekabidhi nyumba hiyo kwa Jaji Mfawidhi.

Wakati akikabidhi nyumba hiyo yenye vyumba vitatu, Makamu Rais huyo alisema kuwa msaada wa ujenzi wa nyumba hiyo ni sehemu ya majukumu ya Kampuni yao kurejesha wanachokipata kwa jamiii.

Alisema pia kuwa hawatoishia kujenga nyumba hiyo bali wataendelea kuwezesha kama uhitaji utajitokeza kwa sababu Kampuni yake inatambua mchango wa Mahakama katika kutatua changamoto za utoaji haki mkoani Geita.

Naye Wakili Mwandamizi wa Sheria wa Kampuni hiyo alieleza kuwa moja ya thamani kubwa katika kampuni yao ni jamii kunufaika kupitia wanachokizalisha, hivyo wameona ni vyema wajenge nyumba ya kuhifadhia vielelezo kwa sababu mchakatoa mzima wa utaoji haki unahitaji pia utunzaji salama wa nyaraka.

Jaji Mfawidhi aliwashukuru kwa jambo kubwa walilolifanya na kueleza kuwa jengo hilo litasaidia kutatua tatizo la sehemu ya kutunzia vielelezo. Aliongeza kuwa nyumba hiyo itatumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA   kuhifadhi vielelezo ili kwenda na dhima ya Kanda ya Geita ya matumizi sahihi ya TEHAMA na kuacha matumizi ya karatasi.

Tukio hilo la kukabidhi nyumba lilishuhudiwa na Jaji wa Mahakama Kuu kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Fredrick Lukuna Viongozi wengine.

Makamu wa Rais wa Kampuni ya Geita Gold Mine Barani Afrika, Bw. Simon Shayo akikabidhi funguo ya nyumba ya kuhifadhia vielelezo kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina akizungumuza na Viongozi wa Kampuni la Uchimaji Madini Mkoa wa Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina akitoa shukrani kwa niaba ya watumishi wote wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita kwa wawakilishi kutoka Kampuni hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni