Alhamisi, 14 Aprili 2022

JAJI MFAWIDHI SHINYANGA AKUNWA NA KIKOSI KAZI CHA KUMALIZA MASHAURI YA MLUNDIKANO

 Na Emmanuel Oguda-Mahakama, Shinyanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma jana tarehe 13 Aprili, 2022 ametembelea kikosi kazi maalum cha kumaliza mlundikano kinachosikiliza mashauri katika Mahakama ya Wilaya Maswa mkoani Simiyu na kupongeza jitihada zinazoendelea kufanywa.

Mhe. Matuma ameridhishwa na utendaji kazi wa kikosi hicho pamoja na mikakati iliyowekwa ya kuhakikisha mashauri ya mlundikano yanamalizika ndani ya siku 14 kama ilivyopangwa toka yalipooanza kusikilizwa tarehe 11 Aprili, 2022.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo ameridhishwa na hatua ya wadau wa Mahakama kuendelea kushirikiana na kikosi kazi hicho ili kumaliza mashauri ya mlundikano katika Wilaya hiyo.

Amesisitiza kuwa malengo ya Kanda ya Shinyanga ni kumaliza kabisa mashauri ya muda mrefu na kutoruhusu mlundikano kulingana na mikakati mbalimbali iliyowekwa katika kuzuia hali hiyo isijitokeze tena.

 Kwa upande wao, wananchi wa Wilaya Maswa wamepongeza jitihada za Mahakama kwa kuamua kuleta Mahakimu toka maeneo mengine kwa lengo la kuondoa mashauri ya muda mrefu. Wamesema jitihada hizo ziendelee pia katika maeneo mengine ili wananchi wapate haki zao kwa wakati.

‘’Kesi yangu ina miaka mitatu hadi sasa, lakini imeanza kusikilizwa na nimeambiwa itamalizika ndani ya siku 14, ninaipongeza sana Mahakama kwa hatua hii, sasa nina amani kwa vile shauri langu litamalizika ndani ya muda mfupi,’’ alisema mwananchi mmoja.

Jumla ya Mashauri kumi ya mlundikano yanaendelea kusikilizwa na yanatarajiwa kukamilika ndani ya siku 14 toka siku ya kuanza kusikilizwa. Itakumbukwa kikosi kazi hiki cha Mahakimu Wakazi kimemaliza kusikiliza mashauri ya mlundikano katika Mahakama za Hakimu Mkazi Simiyu na Wilaya Bariadi na kuhamia katika Mahakama ya Wilaya ya Maswa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athuman Matuma (katikati) akiongea na Mahakimu wanaounda kikosi kazi maalum cha kumaliza mashauri ya mlundikano wakati alipotembelea kikosi kazi hicho katika Mahakama ya Wilaya Maswa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athuman Matuma (aliyenyosha mkono wa kushoto katika picha ya juu na chini) akiongea na wananchi waliofika kusikiliza mashauri yao Wilaya ya Maswa wakati alipotembelea kikosi kazi maalum cha kumaliza mashauri ya muda mrefu.


Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga  Mhe. Athuman Matuma (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja  na Mahakimu wanaounda kikosi kazi maalum cha kumaliza mlundikano wa mashauri wakati alipotembelea kikosi kazi hicho Wilaya ya Maswa. Kutoka kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Maswa, Mhe. Christian Lugumira, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Meatu, Mhe. Mohamed Siliti na Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya Maswa, Mhe. Enos Misana.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni