Ijumaa, 1 Aprili 2022

MAHAKAMA YA JUU NI MUHIMU TANZANIA: JAJI WARIOBA

 Na Faustine Kapama– Mahakama

Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba jana tarehe 31 Machi, 2022 alitembelea ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kushauri Serikali kuanzisha Mahakama ya Juu (Supreme Court), ambayo ni muhimu kuwepo hapa nchini.

Akizungumza na viongozi wa Mahakama katika eneo la mradi wa ujenzi huo walioongozwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Jaji Warioba alionesha kuridhishwa na mpangilio wa jengo hilo ambao unaonesha uwepo wa sehemu iliyotengwa kwa ajili ya Supreme Court.

“Nimefurahi kuona majengo haya ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania ambayo yanaonesha sehemu kwa ajili ya Supreme Court. Mahakama hii ni muhimu, ni vema kama tutaianzisha hapa nchini kwetu,” alisema Jaji Warioba. Jengo hilo la Makao Makuu ya Mahakama ni kubwa na la kisasa kuliko yote ya Mahakama yaliyopo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Kazi za ujenzi katika mradi huo wenye gharama ya billioni 129.7 za Kitanzania unaosimamiwa na Kampuni ya CRJE ya Kichina zilianza Julai 2020 na zinategemewa kumalizika ifikapo tarehe 29 Desemba, 2022.

Kabla ya kutembelea ujenzi huo, Mhe. Warioba ambaye amehudumu katika nafasi mbalimbali serikalini kabla ya kustaafu alitembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma na kuonesha kufurahishwa na mabadiliko makubwa yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania katika utoaji wa haki kwa wananchi.

Baada ya kuingia ndani ya jengo hilo, Jaji Warioba hakuweza kuficha hisia zake baada ya kuona uzuri na uimara wa jengo hilo ambapo alionesha kuridhika na thamani ya fedha iliyotumika katika ujenzi huo.

Alikuwa na maswali kadhaa ambapo alitaka kujua kama kuna baadhi ya Mahakimu ambao bado wanatembelea kituo zaidi ya kimoja na kama Mahakama bado ina ajili Mahakimu wenye Diploma kuhudumu katika Mahakama za Mwanzo.

Katika majibu yake, Mhe. Chuma alimfahamisha Jaji Warioba kuwa kwa sasa kuna mabadiliko makubwa ambayo yamefanyika katika sekta ya sheria, ikiwemo Mahakimu wenye Shahada ya Kwanza ya Sheria na Mawakili wa Kujitegemea kuhudumu katika Mahakama za Mwanzo.

Alibainisha mabadiliko mengine kama matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), uwepo wa mfumo wa kusajili mashauri kwa njia ya mtandao (JSDS2), tovuti ya Mahakama ya Tanzania inayochapisha uamuzi wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu, Sheria na Kanuni (TanzLii) na mfumo wa kielektoniki wa kusajili na kuwatambua Mawakili nchini(e-wakili).

Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba akiwasili katika eneo la ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jinini Dodoma.





Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba (wa pili kushoto) akipokea maelezo kutoka kwa msimamizi wa ujenzi huo (wa kwanza kushoto).

Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba (wa kwanza kushoto) akitambulishwa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma (picha ya juu na chini) kwa baadhi ya viongozi, wakimwemo Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania mara baada ya kuwasili katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma (wa pili kushoto) akimweleza jambo Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba (picha ya juu na chini) mara baada ya utambulisho.


Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha (wa kwanza kulia) akimweleza jambo Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba mara baada ya utambulisho.

Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Leonard Magacha (wa kwanza kulia) akimweleza jambo Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba alipoingia ndani ya jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma.
Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba akizungumza na sehemu ya viongozi wa Mahakama ya Tanzania ndani ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma.
Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba akiwa katika picha ya pamoja na viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania baada ya kutembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma. 
(Picha na Arafa Rusheke-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni