Na Stephen Kapiga –Mahakama, Mwanza
Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Mwanza leo tarehe 28 Julai, 2022 imefanya kikao cha kusukuma
mashauri kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kujadili mikakati ya pamoja ili
kuharakisha utoaji wa haki kwa wananchi.
Kikao hicho kilichoongozwa
na Jaji Mfawidhi wa Mahakama kutoka Kanda hiyo, Mhe. John Kahyoza kilianza kwa
kupokea taarifa ya utendaji kutoka kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe.
Chiganga Mashauri ambaye alionyesha kuwa kasi ya ufunguaji wa mashauri kwa upande
wa Mahakama Kuu imepanda kwa wastani wa mashauri 60 kwa kila mwezi.
“Kasi hii inaendana na usikilizaji
na umalizaji wa mashauri kwa wakati. Nawapongeza Majaji kwa kushirikiana na Ofisi
ya Taifa ya Mashtaka na ile ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa kwa ushirikiano mzuri
katika kasi ya usikilizaji wa mashauri, hivyo kuwezesha kiwango cha mashauri ya
mlundikano kushuka kwa asilimia 5 mpaka sasa ukilinganisha na mwezi Machi
tulivokutana hapa,” alisema.
Kuhusu uendeshaji wa
mashauri kwa njia ya TEHAMA, Naibu Msajili huyo alibainisha kuwa kwa kipindi
cha Machi hadi Julai 2022, jumla ya mashauri 44 ya jinai yameendeshwa kwa njia
ya mfumo wa video conference na hivyo kuokoa muda kwa wadaawa na pia gharama za
uendeshaji kwa Mahakama.
Akizungumza katika
Kikao hicho ambacho pia kilihudhuriwa na Majaji wote wa Mahakama Kuu, Kanda ya
Mwanza, Mahakimu Wafawidhi wote wa Mahakama za Mkoa na Wilaya kutoka Mwanza na
Geita, Polisi, Magereza, Ustawi wa Jamii, Mawakili wa Serikali na kutoka Chama
cha Mawakili Tanganyika (TLS), Jaji Mfawidhi huyo aliwasihi Magereza kuenda na kasi
ya Mahakama katika matumizi ya TEHAMA kwa vile teknolojia hiyo kwa sasa
haikwepeki.
“Ndugu zangu wa Magereza,
kwa sasa matumizi ya TEHAMA kwa upande wa Mahakama hayakwepeki. Nawaomba na kuwasisistiza
sana mtumie TEHAMA haswa katika ufunguaji wa rufaa za wafungwa, kwani hii itasaidia
kuepuka kuchelewesha rufaa hizo na pia hata usahihi wa taarifa na utunzaji wake
ni wa uhakika kwa vile kila taarifa inakuwa imehifadhiwa katika mfumo,”
alisema.
Aidha, Mwenyekiti wa Kikao
aliwataka Mkoa wa Geita kuweka mkakati bora baina ya polisi na waendesha
mashtaka ili kusukuma kwa haraka mashauri ya mauaji ambayo kwa kiwango kikubwa
yapo katika Mkoa huo, hivyo kupelekea mlundikano. Kadhalika aliwataka Mahakimu
katika Mahakama za chini kuwa na mfumo bora wa kuondokana na mashauri ya mlundikano.
“Siyo Geita tu
nawaambia haya hata nyie ambao kwa sasa hamna mashauri ya aina hii, ni vizuri
mkawa na namna bora ya kufanya uchambuzi na kuzuia mlundikano kwa kuyatambua
mapema mashauri ambayo huenda yataingia katika hatua hiyo. Pia ni vizuri kwa
hayo machache yalipo kuyaendesha kwa njia ya vikao ili kusafisha kabisa mlundikano
mlionao,” alisema.
Kauli hiyo iliungwa
mkono na Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Mwanza ambaye aliwaomba wale wote wenye mlundikano
kuwasiliana na ofisi yake ili waweze kuwashirikisha waendesha mashtaka kupanga
namna bora ya kushirikiana katika kuondoa mashauri hayo mahakamani, huku
waendesha mashtaka hao wakiomba uwepo wa ratiba nzuri ya Mahakimu kwani wao
wapo tayari kushirikiana na Mahakama katika mkakati huo.
Kwa upande wake, Afisa
Ustawi wa Jamii, Bw. Magnus Rwekaza ameipongeza Mahakama kwa kuzingatia
matumizi ya adhabu mbadala kwani kwa sasa inasaidia kupunguza msongamano katika
Magereza, hivyo akawasihi Mahakimu ambao bado hawajaanza kutumia utaratibu huo kufanya
hivyo kwa vile utasaidia wote wakiwa kama wadau wa haki jinai.
Akizungumzia upande wa Mawakili,
Mwenyekiti huyo aliwasisitiza kuanza kutumia fomu maalumu ya maelezo ya shaidi kwani
itasaidia katika usikilizaji kwa haraka zaidi na kuondoa zile mbwembwe za
kuhoji mashahidi ambao zimekuwa zikichukua muda mrefu wa Mahakama. Amesema
matumizi ya fomu hiyo pia itasaidia kuchuja mashahidi na kubaki na wale ambao
ni muhimu katika mashauri yatakayokuwa yanaletwa mahakamani, hivyo kuchochea
kumalizika kwa haraka.
Aidha, Mhe. Kahyoza
aliwasihi wale wote wanaoleta mashauri ya mirathi kuwasilisha cheti halisi cha
kifo wakati wa ufunguaji, huku akionya shauri hilo halitafunguliwa bila kuwepo
wa nyaraka hiyo muhimu au wosia halisi. Amesema hatua hiyo itaepusha wale wenye
tabia ya kufungua mirathi zaidi ya Mahakama moja pale wanapoona wanaelekea
kushindwa katika Mahakama zingine na pia kuondoa mgongano wa uwepo wa mashauri
mengi ya marehemu mmoja.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza akiwa katika kikao cha wadau wa Mahakama cha kusukuma mashauri kilichofanyika leo tarehe 28 Julai, 2022.
Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Mwanza, Bw. Steven Kitale (kushoto) akizungumza jambo na Wakili Amri Linus baada ya kikao cha wadau wa Mahakama cha kusukuma mashauri.
Sehemu ya wajumbe wakiwa katika majadiliano mbalimbali nje ya ukumbi baada ya kumaliza kikao cha kusukuma mshauri Mahakama Kuu Mwanza.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni