Ijumaa, 29 Julai 2022

TUMIENI ADHABU MBADALA ISIYOSHANGAZA JAMII: JAJI MLACHA

Na Festo Sanga-Mahakama, Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha amewasihi wadau wa haki jinai kutotumia adhabu mbadala katika mazingira ambayo jamii itawashangaa kwa vile matumizi ya adhabu ya aina hiyo sio matakwa ya mtu binafsi wala taasisi fulani bali ni matakwa ya kisheria.

Mhe. Mlacha alitoa wito huo wakati akifungua mafunzo ya siku mbili yaliyoanza tarehe 29 Julai 2022 yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Ndani- Idara ya Huduma za Uangalizi Mkoa wa Kigoma yakiwashirikisha wadau wa haki jinai kutoka Mahakama, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Huduma za Uangalizi, Polisi, Magereza na Ustawi wa Jamii.

“Adhabu mbadala haitakiwi kutolewa kiholela kwani inaweza kuharibu jamii. Adhabu ya  miaka chini ya mitatu sio kigezo pekee, zingatieni aina ya kosa lililotendeka, jamii ina mtazamo gani na tabia za mhusika,” Jaji Mfawidhi huyo alisisitiza.

Aliongeza kuwa Utekelezaji wa adhabu mbadala utawaepusha wahalifu wa makosa madogo kuiga tabia mbaya ya wahalifu sugu waliopo gerezani na pia utapungunguza msongamano na gharama za kutunza wafungwa gerezani.

Aidha, Mhe. Mlacha alibainisha kuwa utaratibu huo utatoa fursa kwa wahalifu wa makosa madogo kuwa karibu na familia zao na kutekeleza wajibu wao wa kifamilia na kijamii na utaiwezesha jamii kushiriki katika urekebishaji wa wahalifu na kunufaika moja kwa moja na shughuli wanazozifanya na pia kuwezesha utengamanisho wa wafungwa na jamii (re-integration of offenders into the community).

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Huduma za Uangalizi,  Bw. Charles Nsanze alisema kuwa mafunzo hayo  yatakuwa chachu ya kutoa msukumo mpya wa utekelezaji na usimamizi wa adhabu mbadala katika Mkoa wa Kigoma kwa kusaidia kujenga uelewa wa pamoja juu ya utekelezaji wake na taratibu za kisheria katika utoaji wa adhabu hiyo ambayo ni moja ya mikakati ya kujenga ushirikiano miongoni mwa wadau wa Haki Jinai kutekeleza majukumu yao ya kila siku ya kuwahudumia wananchi.

Mafunzo hayo yanalenga kutekeleza maelekezo ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ambayo amekuwa akiyatoa  kwa nyakati tofauti  akihimiza matumizi ya adhabu mbadala kwa wahalifu wasio hatarishi kwa usalama wa raia na mali zao, huku akiwataka wadau kutekeleza adhabu hiyo kwa wahalifu wote waliotimiza vigezo vya kisheria.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha akitoa hotuba katika mafunzo ya Utekelezaji wa Adhabu Mbadala kwa wadau wa haki jinai leo tarehe 29 Julai, 2022.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza kwa makini Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (hayupo katika picha).
Mshiriki wa mafunzo ambaye ni Mhe Rajabu Fakihi Mtuli kutoka  Mahakama ya Mwanzo Kasulu Mjini akiuliza swali.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na meza kuu na washiriki wa mafunzo hayo. Viongozi wengine ni Naibu Msajili,  Mhe. Gadiel Mariki (wa pili kulia) na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Huduma za Uangalizi  Bw Charles Nsanze (wa tatu kushoto).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha akiongea na waandishi wa Habari mara baada ya ufunguzi wa mafunzo ya siku mbili yanayohusu adhabu mbadala kwa wadau wa Haki jinai mkoa wa Kigoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni