Na. Stephen Kapiga-Mahakama Mwanza.
Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Stanley Kamana tarehe 25 Novemba, 2023 alifungua rasmi maadhimisho ya siku 16 ya kupinga ukatili wa kijinsia katika sherehe zilizofanyika katika Kata ya Igoma jijini Mwanza.
Akifungua maadhimisho hayo, Mhe. Kamana aliwasihi wananchi wote kuwa mstari wa mbele katika vita ya kupinga ukatili wa kijinsia kwa maendeleo ya uchumi na ustawi wa jamii ya watanzania wote hasa kwa kuhakikisha kuwa vitendo vyote vya unyanyasi wa kijinsia vinatolewa taarifa kwa wakati ili wanyanyasaji waweze kuchukukuliwa hatua.
“Kwetu sisi wote ambao tunasimamia utekelezaji wa sheria ni vizuri tukatoa kipaumbele katika kusimamia mashauri yanayohusu unyanyasaji wa kijinsia. Hii inaanzia kwa wenye jukumu la kutoa taarifa, kuchunguza, kukamata na kutoa ushahidi. Muda mwingine inapotekea taarifa imechelewa kutolewa hili linaweza kuharibu hata hatua za ushahidi na hivyo kupelekea kesi hizi za unyanyasi wa kijinsia kuharibika”, alisema Mhe. Jaji Kamana.
Akifafanua zaidi juu ya vyanzo vya unyanyasaji wa kijinsia hasa kwa wanawake, Mhe. Kamana alisema ni kutokana na hali ngumu ya kiuchumi kwa wanawake inasababisha matukio mengi na hivvo kujikuta wakinaswa katika mitego ya wanyanysaji wa kijinsia.
“Wakina mama wengi wamekuwa wahanga wa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kutokana na kukosa nguvu ya kiuchumi na hivyo kupelekea wanawake wengi kuwa tegemezi na kunyanyaswa kijinsia. Napenda kutoa wito kwa wadau mbalimbali kuweka wepesi kwa wanawake kuweza kupata mikopo yenye marejesho rafiki ili kuwaepusha na ile mikopo ya kausha damu, mikopo umiza, na mikopo ya mtoto wa shetani” alisisitiza Mhe. Kamana.
Mhe. Kamana alieleza kuwa, kwa sasa unyanyasi wa kinjisia unakua kwa kasi sana kwa watoto wa kiume na hivyo kuwaweka katika hatari kubwa sana kwa watoto hao katika unyanyasaji wa kijinsia na hili mara nyingi hufanywa na watu wa karibu na hivyo kuufikia hatua katika jamii kuona ni bora kuwa na mtoto wa kike kuliko wa kiume ambao wapo kwenye hatari kubwa sana.
Aidha, Mhe. Kamana aliwasihi wananchi kuchukua hatua kwa kukataa kushiriki katika unyanyasaji wa kijinsia hasa kwa njia ya mtandao ambayo imekuwa ikikua kwa kasi hapa nchi kwa watu kukimbilia kuona “connection” zinazotumwa katika mitandao na hivo kuwaacha na maumivu makubwa waathirika wa matukio hayo na wengine kuufikia hatua ya kukatisha uhai wao.
“kwa
sasa watu wamekuwa wapo tayari kulipa pesa zao ili mradi tu kuona clip za video
zilizorekodiwa za watu mashuhuri
wakinyanyasika kijinsia bila kujua kuwa na wao wanashiriki katika
kueneza unyanyasi huo na hivo kuacha maumivu makubwa kwa wahanga wa matukio
hayo ya unyanyasi kijinsia kwa njia ya mitandao”, alisema Mhe. Kamana
Katika
hatua nyingine, asasi zinazojishughulisha na upingaji wa unyanyasaji wa
kijinsia uliziomba Mahakama kuweza kuweka kipaumbele kwa kuyasikiliza kwa
haraka mashauri yanayohusu unyanyasaji wa kinjisia na hivo kuondoka ile nafasi
ya wahusika kuweza kuharibu ushahidi au kushawishi kuyamaliza mambo nyumbani na
hivo kuendelea kukuza tatizo la unyanyasi wa kijinsia nchini.
Kaimu Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Kamana Stanley akitoa
hotuba ya ufunguzi wa siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia maadhimisho
yalifanyika tarehe 25 Novemba, 2023 katika viwanja vya Igoma Stendi ya Magu.
Kaimu Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Mhe. Kamana Stanley Kamana (aliyevaa kofia) akiwa kwenye picha ya pamoja kwenye meza kuu na wageni wengine wakati wa ufunguzi
wa siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia nchini maadhimisho yaliyofungliwa
tarehe 25 disemba 2023 katika viwanja vya Igoma Stendi ya Magu. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya mwanza Mhe. Lilian Itemba (wa pili kulia), kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. Monica Ndyekobora na Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa mwanza Bi. Janeth Mathias.
Kaimu Jaji
Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Mwanza Mhe. Kamana Stanley (wa nane kutoka kulia) akiwa
katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali walioshirikini maadhimisho ya
ufunguzi wa siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia maadhimisho yaliyofanyika katika
viwanja vya Igoma stendi ya Magu.
Sehemu ya
wanachama wa chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) walioshika
bango walioshiriki katika ufunguzi wa maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili
wakijinsia zilizofanyika katika viwanja vya igoma stendi ya Magu.
Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni