Ijumaa, 12 Julai 2024

WANAFUNZI SHULE YA MSINGI MATSAPA WATEMBELEA MAHAKAMA KUU DAR ES SALAAM

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Wanafunzi 54 wa Darasa la Saba katika Shule ya Msingi Matsapa iliyopo Wilaya ya Ubungo inayofundisha kwa lugha ya Kiingeleza leo tarehe 12 Julai, 2024 wametembelea Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam kujifunza mambo mbalimbali ya kisheria na utoaji haki.

Wakiwa wemeongozana na Walimu sita, Wanafunzi hao waliwasili katika jengo la Mahakama hiyo majira ya saa 3.00 asubuhi na kupokelewa na Afisa Utumishi, Bi. Winnie Shirima na kupelekwa kwenye Ukumbi wa Chumba cha Habari NMB.

Baada ya mapumziko mafupi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi alikutana na Wanafunzi hao na kuwapa maelezo kadhaa kuhusu Mahakama ya Tanzania, kama moja ya Mihimili inayounda Dola hapa nchini, kabla ya kuanza ziara yao.

Maeneo waliyotaka kujua ili kuwawezesha Wanafunzi hao kujifunza na kupata umahiri katika uhalisia baada ya nadharia ya darasani ni muundo wa Mahakama ya Tanzania, aina mbalimbali za mashauri na Mahakama zenye mamlaka ya kuyasikiliza na Viongozi wanaohusika na usikilizaji wa mashauri mbalimbali kulingana na uzito.

Akizungumza na Wanafunzi hao, Mhe. Maghimbi aliwaeleza jinsi Mahakama ilivyoanzishwa kwa mujibu wa Katiba, ngazi za Mahakama zilizopo kuanzia Mahakama za Mwanzo hadi Mahakama ya Rufani na namna mwananchi anavyopata haki kwa njia ya kusikiliza, rufaa, marejeo na mapitio.

Jaji Mfawidhi alieleza kuwa Mahakama hutekeleza majukumu yake kwa uhuru bila kuingiliwa na Mihimili mingine ya Dola kama Serikali na Bunge na kwamba uhuru huo unapenya hata ndani ya Mahakama yenyewe kwa Majaji na Mahakimu kuamua mashauri bila kupokea maelekezo kwa mtu yoyote.

Kadhalika, Mhe. Maghimbi aliwaeleza Wanafunzi hao kuwa kwa sasa Mahakama inaendesha shughuli zake kwa njia ya mtandao na kwamba usajili wa mashauri yote unafanyika kwa njia ya mtandao, hivyo akawahimiza kujikita kwenye teknolojia wakati wa masomo yao ili wasije wakaachwa na utandawazi.

Amewaeleza pia kuwa Viongozi wa Mahakama, kama Jaji Mkuu, Majaji, Mtendaji Mkuu, Msajili Mkuu, Msajili wa Mahakama ya Rufani na Msajili wa Mahakama Kuu huteuliwa na Rais na kwamba Mahakimu huajiriwa kama watumishi wengine baada ya kupita kwenye mchakato wa ajira.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (juu na chini) akisisitiza jambo alipokuwa anazungumza na Wanafunzi wawa Darasa la Saba katika  Shule ya Msingi Matsapa (hawapo kwenye picha) ambao leo tarehe 12 Julai, 2024 wametembelea Mahakama Kuu kujifunza mambo mbalimbali ya kisheria.Wengine katika picha ya chini ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbajo (kushoto) na Hakimu Mkazi na Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Juliana Nankoma.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbajo alitoa maelezo ya utangulizi kabla ya Jaji Mfawidhi kuzungumza na Wanafunzi hao (picha chini).


Sehemu ya Wanafunzi wa Shule ya Msingi Matsapa  Darasa la Saba (juu na chini) wakimsikiliza Jaji Mfawidhi.


Sehemu nyingine ya Wanafunzi wa Shule ya Msingi Matsapa Darasa la Saba (juu na chini) wakimsikiliza Jaji Mfawidhi.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwa katika picha ya pamoja na Wanafunzi wa Shule ya Msingi Matsapa Darasa la Saba (juu wakike na chini wa kiume).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwa katika picha ya pamoja na Wanafunzi wote wa Darasa la Saba katika Shule ya Msingi Matsapa.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwa na Walimu walioambatana na Wanafunzi wa Darasa la Saba katika Shule ya Msingi Matsapa.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni