- Ataka kila Mdau wa Uhifadhi kuwajibika ipasavyo kwenye eneo lake
Na MARY GWERA, Mahakama-Arusha
Wadau wa uhifadhi wa Wanyamapori nchini
wametakiwa kuweka mikakati thabiti itakayowawezesha kuwajibika na kusimamia
ipasavyo Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori ili kukabiliana na changamoto
mbalimbali zinazoikabili Sekta ya Uhifadhi wa maliasilia ikiwemo Mazingira na
Wanyamapori.
Akizungumza jana tarehe 09 Septemba, 2025
jijini Arusha wakati akifungua Mafunzo baina ya Shirika la Hifadhi za Taifa
Tanzania (TANAPA) na Wadau wa Haki Jinai, Mgeni Rasmi ambaye ni Jaji Mkuu wa
Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju alisema licha ya kuwepo kwa sheria
hiyo bado kumekuwa na changamoto kadhaa katika eneo la uhifadhi wa maliasili.
Mhe. Masaju alisema pamoja na kusimamia
Sheria kuna miongozo mingine ya kusimamia uhifadhi ikiwemo Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Sera ya Uhifadhi, Matamko ya Wakuu wa Taifa ikiwa ni
pamoja na Tamko la Hayati Mwalimu Nyerere la mwaka 1961 kuhusu uhifadhi ambapo alinukuu
tamko hilo kuwa, “uhai wa wanyamapori (Wanyama na Mimea) ni jambo linalotuhusu
sana sote katika Afrika, viumbe hawa wa porini wakiwa katika mapori wanamoishi
sio muhimu tu kwa ajili ya kuwavutia ni sehemu ya mustakabali wa maisha yetu ya
baadaye, kwa kukubali dhamana ya wanyamapori wetu tunatamka kwa dhati kwamba tutafanya
kila tuwezalo kuhakikisha kwamba tunafanya kila tuwezalo kuhakikisha kwamba
wajukuu wa watoto wetu wataweza kufurahia urithi huu mkubwa na wa thamani
adimu.......”
Kadhalika, Jaji Mkuu aliwataka Wadau hao wa
uhifadhi kusoma na kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambapo ukurasa wa
41 wa Dira hiyo unasisitiza juu ya uhifadhi wa mazingira kuwa ni muhimu katika
kufikia malengo...., vilevile amesema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
inatoa haki na wajibu huku akinukuu Ibara ya 27 ya Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania (1977) inasema kwamba kila mtu ana wajibu wa kulinda
maliasilia ya Jamhuri ya Muungano, mali ya mamlaka ya nchi na mali yoyote
inayomilikiwa kwa pamoja na wananchi na pia kuiheshimu mali ya mtu mwingine, vilevile
watu wote watatakiwa na sheria kutunza vizuri mali ya mamlaka ya nchi na ya
pamoja, kupiga vita aina zote za uharibifu na ubadhilifu na kuendesha uchumi wa
Taifa kwa umakini kama watu ambao ndio waamuzi wa hali ya baadaye ya Taifa
lao......
Mhe. Masaju aliongeza pia kwa kurejea Ibara
ya 25 (i) a-b ya Katiba ambayo inasema kila mmoja anatakiwa kuwajibika na
kwamba kazi pekee ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii ndilo chimbuko la
ustawi wa wananchi na kipimo cha utu na kila mtu anao wajibu wa kushiriki kwa
kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji mali na kutimiza nidhamu
ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji mali ya binafsi na yale
malengo ya pamoja yanayotakiwa au yaliyowekwa na sheria.
“Tujiulize, nidhamu ya kazi yetu ni nini sisi
tuliopo kwenye Vyombo vya utoaji maamuzi, tuliopo mahakamani nidhamu yetu ya kazi ni
nini, waliopo kwenye uhifadhi nidhamu yao ya kazi ni ipi na malengo yao
yaliyowekwa kwa mujibu wa sheria. Haya mambo lazima tuyazingatie,” alisisitiza
Jaji Mkuu.
Alisema kwamba, Kipaumbele cha tatu cha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ni Uwajibikaji kwa watumishi wa umma, huku akisisitiza uwajibikaji wa kila Mdau wa uhifadhi ambapo alishauri kuwa, kuna haja ya kutungwa kwa Sheria ya Uwajibikaji ili suala la uwajibikaji liweze kuchukuliwa kwa uzito wa kipekee na kusimamiwa ipasavyo.
“Sisi hapa hatung’ang’anii huu uhifadhi kwa sababu ya kudumisha uhai wetu tu kwa maana ya ‘ecology’ lakini pia ni kwa sababu ya manufaa ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni,” alisisitiza Mhe. Masaju.
Mhe. Masaju alisema kuwa, kumekuwa na changamoto kadhaa zinazoikabili sekta ya uhifadhi ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa ujangili na biashara haramu ya nyara na mazao ya misitu ambapo matukio ya ujangili wa wanyamapori na biashara haramu ya meno ya tembo yamekuwa yakiongezeka,” alieleza Jaji Mkuu.
Aliongeza kuwa,
changamoto nyingine ni kuongezeka kwa matumizi ya silaha za kivita kwenye matukio ya ujangili, kutokuwepo kwa vikao kazi vya kitaaluma kati ya Majaji, Mahakimu,
Mawakili wa Serikali na Wadau wengine wa Uhifadhi ikiwa ni pamoja na TANAPA na Idara
ya Misitu, jambo ambalo linafifisha mahusiano baina wadau wote.
“Changamoto nyingine ni kutozingatia umuhimu wa
urithi wa Taifa kwenye Uchumi wa nchi wakati wa kushughulikia migogoro ya maliasili,
ugumu wa kupata Shahidi binafsi unaotokana
na mazingira ya maeneo ambayo ujangili
unatokea, kuongezeka kwa uingizaji mifugo katika maeneo ya Hifadhi
kunakosababisha wanyamapori watoke
na kuingia katika maeneo ya jamii na kusababisha uharibifu wa mazao pamoja na kujeruhi ama
kusababisha maafa kwa jamii,” alisema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju aliongeza kuwa, kumekuwa na migogoro kati ya wanyamapori na binadamu ambayo inatokana na Uingizaji mifugo katika maeneo ya hifadhi na kufungwa kwa mapito ya wanyamapori.
Mhe. Masaju aliwasihi wadau hao kila mmoja katika nafasi yake kuwajibika ipasavyo katika usimamizi wa Sheria na miongozo mbalimbali ili kuondoa changamoto hizo zinazoikabili sekta hiyo muhimu ambayo inachangia kwa asilimia kubwa kuongeza kipato cha nchi na maendeleo kwa ujumla.
Kadhalika, Jaji Mkuu alionesha kusikitishwa na kukemea tabia ya baadhi ya wadau wakishirikiana na watu wa nchi za nje kuhujumu maliasili za nchi, “Polisi wakishirikiana na watu wa uhifadhi wamekamata watu mara nyingi wengine sio raia wa Tanzania wakisafirisha pembe za ndovu, wengine wakisafirisha faru na kadhalika.”
Aidha, Mhe. Masaju amekemea vitendo vya baadhi ya maafisa wanyapori kuruhusu kuingiza mifugo kwenye hifadhi na baadaye wanaikamata na kuiuza/kutaifisha mifugo hiyo ikiwemo ng'ombe za wafugaji hao na baadaye kugawana.
Aidha, Jaji Mkuu alisema pia kwa muda mrefu
zimekuwa zikitumika njia za kawaida katika kutunza mazingira ikiwamo wanyama
pori, hivyo ametoa wito kwa wadau hao
kuangalia matumizi ya akili Unde (AI) ili kuongezea uwezo njia za zamani zilizokuwa
zinatumika.
“Ninaamini kwenye kikao hiki na mijadala
itaonyesha namna matumizi ya akili unde yanavyoweza kuleta mapinduzi katika uhifadhi wa wanyamapori kwa kuwezesha ufuatiliaji na ugunduzi wa haraka wa vitisho kama vile ujangili na uchanganuzi wa kutabiri mabadiliko ya mazingira na athari za mfumo ikolojia. Zana zinazoendeshwa na AI, kama vile ndege zisizo na rubani zenye utambuzi wa picha na uchanganuzi wa data ya satelaiti, naamini uhifadhi utakuwa wa ufanisi zaidi kuliko mbinu za zamani pekee. Matumizi ya Akili Unde yatasaidia pia kuzuia ujangili,” alieleza Mhe. Masaju.
Aliongeza kuwa, kikao hicho kimeandaliwa kwa lengo la kuboresha utekelezaji wa Sheria zinazolenga kuhifadhi mazingira na kipekee sheria ya wanyamapori na kusisitiza kwamba, ushiriki wa Mahakama katika kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa wanyamapori ni muhimu na haupaswi kupuuzwa.
Aidha, Jaji Mkuu alitoa rai kwamba, wakati
mwingine wadau wengine muhimu kama Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira, Wizara ya
Ardhi, Wakala wa Misitu Tanzania wahusishwe katika mafunzo hayo kwa kuwa nao ni
sehemu muhimu katika uhifadhi.
Akitoa neno la ukaribisho kwa niaba ya
Kamishna Mkuu wa TANAPA wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo hayo naye Naibu
Kamishna Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara, Bw. Misana Mwishawa alisema kuwa,
ni jukumu la kila mdau kuhakikisha kwamba uhai wa wanyapori unaendelea kuwepo
hadi vizazi vijavyo.
“Mafunzo haya ni jitihada za kuhakikisha
kuwa, maliasili zetu zinaendelea kuhifadhiwa, uhifadhi ni kitu endelevu hivyo
ni wajibu wa kila mmoja wetu kushiriki,” alisema Kamishna Mwishawa.
Aliongeza kuwa, kikao hicho kinaonesha bayana
kuwa ni utekelezaji kwa vitendo kuhusu uhifadhi wa Rasilimali za Taifa.
Mafunzo hayo yenye kauli mbiu isemayo “Kuongeza ushirikiano kati ya Mahakama na teknolojia katika kupambana na uhalifu wa wanyamapori nchini Tanzania” yameandaliwa na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA)
kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania kwa lengo likiwa ni kuboresha utekelezaji wa Sheria
zinazolenga kuhifadhi
mazingira yetu na kipekee sheria ya wanyamapori.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni