· Asisitiza pia uwajibikaji katika kazi
· Atoa rai kwa Majaji, Watendaji kusimamia maadili ya watumishi walio chini yao
Na MARY GWERA, Mahakama-
Dodoma
Jaji Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Majaji na Viongozi wa Mahakama nchini
kuanza maandalizi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 kwa
kufuata miongozo iliyowekwa ya utekelezaji wa dira hiyo.
Akizungumza jana tarehe 03
Septemba, 2025 wakati akifunga Kikao Kazi cha siku tatu cha Majaji Wafawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania kilichofanyika kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Masaju alisema kuwa, eneo la Utawala
bora na Haki ni kipaumbele cha kwanza kilichoainishwa katika Dira hiyo
hivyo, ni muhimu kwa Mahakama kushiriki katika utekelezaji wake ili kuboresha eneo
la utoaji haki.
“Niwaombe tufanye
maandalizi sasa kwa ajili ya utekelezaji wa Dira hii kwa mujibu wa mwongozo
tuliowekewa na hii dira imeweka pia mpango wa utekelezaji,” alisema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju alisema huku
akirejea ukurasa wa 63 wa Dira hiyo ambao unasema, “ili kuhakikisha kuwa Dira
2050 inatekelezwa kwa ufanisi, Serikali imeweka mfumo imara wa usimamizi
unaozingatia malengo yake mahsusi, mfumo huu umekusudia kuhimiza uwajibikaji,
ukihitaji uongozi mahiri na ulio makini katika ufuatiliaji, aidha mfumo
unahimiza matumizi ya mbinu zitakazotoa matokeo yanayopimika.”
Aliwahimiza viongozi hao
kwa kuwaeleza kuwa, ambao bado hawajasoma Dira hiyo, kuisoma ili kuielewa
ipasavyo na kuanza utekelezaji wake. Akisisitiza kuwa, Dira hiyo inasisitiza kwamba,
msingi wa mkakati huo ni mabadiliko makubwa ya kifikra ambayo yanalenga kwenye
vitendo zaidi kuliko maneno na matokeo badala ya ahadi.
Akirejea Dira hiyo, Jaji
Mkuu alisema, “Uongozi, Taasisi pamoja na watendaji na wadau wote wanapaswa
kuwajibika kutimiza malengo la dira kwa ufanisi......”
Kadhalika, Jaji Mkuu aliwakumbusha Majaji hao kuendelea kuishi viapo vyao na kusimamia haki ipasavyo kwa kuzingatia Katiba na Sheria za Nchi.
"Tutambue tunalo jukumu kubwa, kwanza Ibara ya 4 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 107A na Ibara ya 107B, sote tunazifahamu lakini kubwa hapa sisi Mahakama ya Tanzania tumepewa jukumu ya kuwa mamlaka yenye kauli ya mwisho katika utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na katika hizi Ibara nilizozisoma hapa zimeweka na kanuni na mwongozo ukiacha yale maadili mengine ya utumishi wa Mahakama, niwaombe tuendelee kuzingatia haya," alisisitiza Mhe. Masaju.
Jaji Mkuu aliendelea kuwasisitiza Majaji na Mahakimu kutekeleza jukumu la utoaji haki ipasavyo kwani ni kazi ambayo wamekasimiwa na Mungu na inatambulika hata kwenye Vitabu Vitakatifu vya Mungu ikiwemo Biblia na Quran, na kuwasihi kusoma Biblia kwenye Kitabu vya ‘Kumbukumbu la Torati 4:2, 6, Kutoka 18:21-22 na 2 Mambo ya Nyakati 19: 6-7.
Aidha, Mhe. Masaju
aliwataka pia Majaji hao kudumisha umakini katika utekelezaji wa majukumu ili Mhimili
wa Mahakama ya Tanzania uwe moja ya Mhimili wenye hadhi duniani.
Katika hatua nyingine,
Jaji Mkuu alitoa rai kwa Majaji, Mahakimu, watumishi wa Mahakama na wananchi wote
kwa ujumla kuwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Uzoefu wangu ni kana kwamba wengi serikalini
tumekuwa tukidhani kwamba mambo ya Taifa hili yanamuhusu Rais wa nchi wa hii peke
yake na Viongozi kama Mawaziri na viongozi wengine Wakuu wa Mihimili na Watendaji
Wakuu katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na kwetu sasa mahakamani
tunafikiri kwamba mambo haya yanamuhusu Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi, Mtendaji Mkuu,
Msajili Mkuu, Msajili wa Mahakama ya Rufani na hata Msajili wa Mahakama na
wengine sisi sote hatuwajibiki,” alisema Mhe. Masaju.
Aliongeza kuwa, wengine
wanadhani kwamba suala la uwajibikaji linawahusu makao makuu ya Mahakama ya
Tanzania peke yake lakini wengine hatuhusiki na wakati fulani hata ambao wanahusika
kwenye ngazi ya kanda wanadhani kwamba yanawahusu wao peke yao.
“Wakishatambua wajibu huo,
kila mmoja atajiona ni mhusika kuanzia kiongozi wa juu kabisa mpaka mwananchi
wa kawaida tukiwemo na sisi viongozi,” alisisitiza Mhe. Masaju.
Kadhalika, Jaji Mkuu alisema
kuwa, ili kuboresha uwajibikaji ni muhimu watumishi wa Mahakama kuzingatia na
kusimamia haki kwa kuhakikisha haki inatendeka, uadilifu, uwezo wa kumudu
majukumu ipasavyo, kujiongeza, kuwa na ubunifu na kuwa na uzalendo wa nchi.
“Majaji Wafawidhi wasimamieni
watumishi waliopo chini yenu kwa kutoa ushauri, kuwalea na inapobidi kutoa
adhabu wanapokwenda kinyume na maadili,” alisisitiza Mhe. Masaju.
Katika kikao hicho
ambacho kilihudhuriwa pia na baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mtendaji Mkuu, Msajili Mkuu na Wajumbe wa
Menejimenti ya Mahakama kwa pamoja walipata fursa ya kubadilishana uzoefu
katika utendaji kazi, kushirikishana kuhusu mafanikio na changamoto.
Kikao hicho kimetoka na maazimio kadhaa baadhi yake ni kuwa na ushirikishwaji wa viongozi katika miradi ya ujenzi katika hatua zote, kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi (mediation), haki za watumishi za kisheria zilipwe mapema ipasavyo na kikamilifu, ufanisi wa mifumo ya kielektroniki ya usikilizaji mashauri (TTS na e-CMS) ufanyiwe tathmini na kuboreshwa ili iwe rafiki zaidi kwa watumiaji na mengine.
Washiriki wa Kikao Kazi cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakifuatilia kilichokuwa kikijiri katika kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 03 Septemba, 2025.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni