Jumanne, 4 Novemba 2025

JAJI MKUU WA MAHAKAMA YA TANZANIA AMUAPISHA MHE.DKT. SAMIA NA MAKAMU WAKE

·       Rais Samia asisitiza amani, umoja na mshikamano kwa Watanzania

·       Azitaka Kamati za Ulinzi na Usalama nchini kurejesha amani na utulivu ili maisha ya Watanzania yaendelee kama kawaida

·       Marais wa Burundi na Zambia nao wawasihi Watanzania kudumisha sifa ya amani ya Tanzania

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amemuapisha Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Awamu ya Sita ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  katika kipindi cha pili.

Kadhalika, Mhe. Masaju amemuapisha Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi kuwa Makamu wa Rais wa Serikali ya Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hafla ya uapisho ilifanyika tarehe 03 Novemba, 2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma na kushuhudiwa na wageni mbalimbali akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Marais na Viongozi kutoka Nchi mbalimbali za Afrika akiwemo Rais wa Burundi, Rais wa Zambia, Rais wa Msumbiji, Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Somalia na kadhalika.

Wengine waliohudhuria hafla hiyo ni Mabalozi kutoka Nchi mbalimbali, Viongozi wa Serikali, Bunge, Mahakama, Viongozi wa Dini na Wananchi kwa ujumla.

Akizungumza mara baada ya uapisho, Mhe. Dkt. Samia aliwasihi Watanzania kuendelea kulinda itikadi ya umoja, amani na mshikamano ambapo alisema, “ndugu zangu wote tunaoitakia mema Nchi hii ‘Tanzania’ tumesikitishwa na vitendo vya uvunjifu wa amani, upotefu wa maisha na uharibifu wa mali za umma na mali za watu binafsi kwenye baadhi ya maeneo hapa nchini hasa kwenye Majiji na Miji, kilichotokea hakiendani na taswira na sifa za Kitanzania na sio Utanzania.”

Rais Samia alisema, Vyombo vya Ulinzi na Usalama nchini vinaendelea kufuatilia na kuchunguza kwa undani zaidi kilichotokea na kuirudisha nchi katika hali iliyozoeleka kwa haraka.

Aidha, Mhe. Dkt. Samia alizitaka Kamati ya Kitaifa ya Ulinzi na Usalama na Kamati za Mikoa na Wilaya kuhakikisha kuanzia jana tarehe (03 Novemba, 2025) maisha ya wananchi yanarejea katika hali ya kawaida mara moja.

“Amesema hapa Rais wa Zambia na Rais wa Burundi, machafuko ndani ya nchi si mema hayana thamani na sifa eidha kwa yeyote yule, kwahiyo ndugu zangu niwaombe sana, tuzingatia umoja, amani na utulivu wa nchi yetu,” alisisitiza Rais Samia.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Samia alitoa onyo kwa wote waliochochea uvunjifu wa amani, ambapo alisema, “nitumie fursa hii kutoa onyo kama mama kwa wale wote waliochochea uvunjifu wa amani na nawataka watambue kuwa, vurugu na uvunjifu wa amani huishia kupimana nguvu na uwezo wa kujihami ila mazungumzo huzaa mshikamano sasa tuchague lenye manufaa kwetu kwani usalama wa Taifa lolote hulindwa na wote kwa nguvu zote na gharama zozote.”

Katika hatua nyingine, Rais Samia aliwashukuru Watanzania kwa kumpigia kura zilizompa ushindi na kuahidi kuwa, yeye, Makamu wa Rais pamoja na Wabunge na Madiwani waliochaguliwa watalitumikia Taifa la Tanzania kwa maarifa na nguvu zao zote ili kuleta maendeleo katika Taifa hilo.

“Nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuturuzuku uhai na kutuwezesha kushiriki sherehe hizi za kihistoria kwa Taifa letu, pili niwashukuru Watanzania wote kwa imani yao kwa Chama cha Mapinduzi (CCM) na kwa mapenzi makubwa na kutupa mimi na Makamu wa Rais fursa hii adhimu ya kuwatumikia,” alisema Rais Samia.

Aidha, Mhe. Dkt. Samia aliipongeza Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) kwa kuratibu na kusimamia mchakato mzima wa uchaguzi kwa ufanisi usiotiliwa shaka.

Kadhalika, Rais Samia alikipongeza Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa namna walivyoendesha kampeni zao.

“Katika uchaguzi huu tulikuwa wagombea 17 kutoka Vyama mbalimbali nchini tukiwania nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda kuwashukuru sana wagombea wenzangu 16 ambao kwa hakika wameonesha ukomavu wa kidemokrasia kwa kuendesha kampeni ambazo tulishindana kwa hoja na kuonesha kuwa siasa sio vita,” alisema Rais Samia.

Aliongeza kwa kuwasisitiza Watanzania kuendelea kudumisha umoja, upendo na mshikamano sambamba na kuheshimu sheria za nchi.

“Ndugu wananchi sifa moja ya mwanadamu ni kutokukamilika, aliyekamilika kabisa kabisa bila kasoro yoyote ni Mwenyezi Mungu peke yake, ndio maana katika shughuli au harakati za wanadamu tunaunganishwa na mawasiliano, mazungumzo na maelewano au kwa maneno mengine tunaungwanishwa na suluhu ya mambo katika jamii zetu,” alisisitiza Mhe. Dkt. Samia.

Alisema, Serikali ya awamu ya sita itaendelea na falsafa yake ya kuzingatia (four Rs’) ikiwemo maridhiano na kuwataka wananchi kuchagua upendo badala ya chuki, umoja badala ya mgawanyiko, huruma badala ya hasira, hekima badala ya kiburi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais wa Jamhuri ya Burundi, Mhe.  Evariste Ndayishimiye amempongeza Rais Samia kwa ushindi alioupata, kumtakia heri sambamba na kuwasihi Watanzania kuendelea kudumisha amani, umoja na mshikamano.

Kwa upande wake Rais wa Zambia akizungumza katika hafla ya Uapisho, Mhe. Hakainde Hichilema naye amempongeza Rais Samia kwa ushindi aliopata na kutoa rai kwa Watanzania kuendelea kudumisha na kuilinda amani waliyonayo kwa muda mrefu.

“Sisi sote tunatakiwa kufanya kazi bila kuchoka kulinda amani na usalama wa nchi zetu ili kuleta maendeleo, tuchague kufanya mazungumzo ya amani ili kushughulikia changamoto ya aina yoyote inayoikabili nchi,” alisisitiza Rais Hichilema.

Kadhalika, Mhe. Hichilema ameahidi kuwa, Zambia itaendelea kushirikiana kwa karibu na Tanzania katika sekta mbalimbali ili kuendelea kukuza Uchumi wa nchi hizo mbili.

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliibuka Mshindi wa Kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupata asilimia 97.66 katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani uliofanyika nchini tarehe 29 Oktoba, 2025.  



Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akimuapisha Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kipindi cha pili cha Awamu ya Sita. Hafla ya Uapisho ya Rais na Makamu wa Rais wa Tanzania ilifanyika  tarehe 03 Novemba, 2025  katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akila kiapo kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kipindi cha pili cha Awamu ya Sita ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hafla ya uapisho ilifanyika tarehe 03 Novemba, 2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akimuapisha Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa tayari kwa ajili ya kukagua Gwaride maalum mara baada ya kuapishwa kushika nafasi hiyo tarehe 03 Novemba, 2025 
katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.
Rais Samia akikagua gwaride maalum la Vikosi vya Jeshi la Ulinzi na Usalama lililoandaliwa maalum wakati wa hafla ya uapisho wa Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wa Rais wa Tanzania tarehe 03 Novemba, 2025 
katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (wa kwanza mbele) akisindikizwa na sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Jaji Mkuu wa Zanzibar kuelekea kwenye jukwaa la Uapisho lililoandaliwa kwa ajili ya uapisho wa Rais na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 03 Novemba, 2025
katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) pamoja na wageni mbalimbali wakiimba Wimbo wa Taifa la Tanzania wakati wa hafla ya uapisho wa Rais na Makamu wa Rais wa Tanzania tarehe 03 Novemba, 2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia Taifa mara baada ya kula kiapo cha kushika nafasi hiyo tarehe 03 Novemba, 2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Rais wa Burundi, Mhe. Evariste Ndayishimiye akizungumza jambo wakati wa sherehe za uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wa Rais wa Tanzania tarehe 
03 Novemba, 2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Rais wa Zambia, 
Mhe. Hakainde Hichilema
  akizungumza jambo wakati wa sherehe za uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wa Rais wa Tanzania tarehe 03 Novemba, 2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

Picha mbalimbali za matukio ya Uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi tarehe 03 Novemba,    2025 katika Uwanja wa Chamwino Ikulu jijini Dodoma.                                         


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni