Na. Fredrick Mahava-Mahakama, Sumbawanga
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya
Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda ameongoza watumishi na wadau wa Mahakama
kusherehekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini katika viwanja vya
Mahakama Kuu Sumbawanga ikiwa ni ishara ya kuanza
kwa mwaka mpya wa shughuli za kimahakama.
Akizungumza katika hafla hiyo jana tarehe 02 Februari, 2026,
Mhe. Manyanda alitoa rai kwa wananchi Mkoa wa Rukwa kwa kushirikiana na Tawala
za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kushiriki katika ujenzi wa Mahakama
hasa Mahakama za Mwanzo kama Muze, Ilemba,
Kate, WampembeKipande ambazo hazina majengo
ya Mahakama na zinaendesha shughuli zake kwenye ofisi za Kata na Maghala ya
kijiji.
Mhe.
Manyanda alisema Kauli mbiu ya mwaka
2026 inasema “Mchango
wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa” inatukumbusha
na kutuonyesha kuwa, ili Taifa liweze kusonga mbele kimaendeleo, Mahakama pia
inayo nafasi ya kushiriki katika kuhakikisha hilo linafanikiwa na hivyo taifa linahitaji
kuwa na Mahakama iliyo imara, huru na yenye kusimamia haki kwa mujibu wa
mamlaka iliyopewa na Katiba.
Vilevile,
Mhe. Manyanda amehimiza matumizi ya usuluhishi katika ngazi mbalimbali kwa
lengo la kutatua migogoro mapema zaidi na kwa njia ambayo haithiri mahusiano ya
wadaawa na hivyo kusaidia kujenga jamii yenye amani na kusisitiza juu ya
matumizi ya mifumo mbalimbali kuanzia ngazi ya familia hadi Mahakama
kuhakikisha kuwa migogoro inayoweza kutatuliwa kwa usuluhishi itatuliwe kwa
njia hiyo.
Kwa upande wake, Mwanasheria Mkuu wa
serikali, Bw. Mjahidi B. Kamugisha alisema kuwa, Mahakama kama mlezi wa Katiba,
Mlinzi wa haki za binadamu na utawala wa sheria ni nguzo muhimu katika kukuza
na kuendeleza ustawi na maendeleo ya Taifa. Mahakama iliyo huru na yenye kuheshimika
na kuaminika huhakikisha utekelezaji thabiti wa mikataba, ulindaji wa haki za
mali na kudhibiti matumizi mabaya ya
madaraka ili kukuza imani ya wawekezaji hivyo kuwezesha ukuaji imara na
endelevu wa uchumi wa Taifa.
Aliongeza kuwa Ofisi ya Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashitaka na Ofisi ya Wakili Mkuu wa
Serikali zitaendelea kushirikiana na Mahakama katika kuhakikisha watu wote
wanapata huduma kwa weledi ubora, uadilifu ili kiu ya kila anayekimbilia haki
ikatimiekwa wakati.
Kwa
upande wake, Wakili kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Bi, Tunu
Mahundi alisema kuwa, kwa sasa TLS inahudumia
wananchi mbalimbali wanaohitaji huduma za Msaada wa Kisheria kwa wenye uhitaji na kuhakikisha
wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za mawakili wanapata haki bila
vikwazo katika ofisi zake zilizopo kwenye chapter 21 Tanzania nzima.
Vilevilie,
aliipongeza Mahakama kwa kuendelea kuboresha Mifumo ya TEHAMA ambayo
imewawezesha Mawakili kuweza kufanya shughuli zao mahali popote kwa kupitia mfumo
wa e-Filing na Virtual court na pia TLS itaendelea kushiriki katika matukio
mbalimbali yanayohusu utoaji elimu ya sheria kama vile wiki ya sheria,
maonyesho ya sabasaba na kampeni ya msaada wa kisheria (Samia legal Aids)
Naye,
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Bw. Makongoro Nyerere aliwashukuru na kuwapongeza
Viongozi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga kwa Maandalizi mazuri ya Siku ya
Sheria nchini na kuipongeza Mahakama kwa kuwa mstari wa mbele katika kutimiza
Dira ya maendeleo ya Taifa na kuhimiza umuhimu wa wananchi kujitokeza kujenga
Mahakama ili kusogeza huduma kwa Wananchi
Wadau waliohudhuria Maadhimisho ya kilele cha Siku ya Sheria nchini ni pamoja na Watumishi wa Kanda ya Sumbawanga, Mawakili wa Serikali, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Rukwa, Viongozi wa Dini, Wakuu wa Taasisi za Umma, TAKUKURU, Madalali wa Mahakama na Wasambaza Nyaraka za Mahakama na wananchi kutoka sehemu mbalimbali ya Mkoa wa Rukwa.
Mwakilishi wa Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mkoa wa Rukwa Bw Mjahidi B. Kamugisha akitoa
hotuba yake ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 mbele ya Wananchi na wadau
waliohudhuria katika viwanja vya Mahakama Kuu Sumbawanga.
Mwakilishi wa Chama cha
Wanasheria Tanganyika (TLS) Bi.Tunu Mahundi akisoma hotuba
yake ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 mbele ya Wananchi na wadau
waliohudhuria katika viwanja vya Mahakama Kuu Sumbawanga.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick K. Manyanda (Katikati), Mkuu wa Mkuu wa
Mkoa wa Rukwa Mhe, Makongoro Nyerere (Kushoto) na Katibu Tawala na Mwakilishi
wa Mkuu wa Wilaya Mhe, Masinga (kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na
Mahakimu
(Habari Hii Imehariri na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni