Jumatatu, 9 Februari 2026

MAJAJI, MAHAKIMU TABORA WAPATIWA MAFUNZO YA TEHAMA

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora imeendesha mafunzo maalum kwa Majaji na Mahakimu yanayolenga kuimarisha uelewa wa dhana na taratibu za kupokelewa kwa ushahidi wa kielektroniki pamoja Maadili na Mienendo (Nidhamu) ya Kimahakama.

Mafunzo hayo yaliendeshwa hivi karibuni na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Juma Mambi aliyewasilisha mada kuhusu ushahidi wa kielektroniki, pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert Martin Chuma aliyefundisha kuhusu maadili na nidhamu ya kimahakama kwa njia ya mtandao.

Akitoa mada yake, Mhe. Dkt. Mambi alieleza kwa kina dhana ya ushahidi wa kielektroniki, aina zake na masharti ya kisheria yanayozingatiwa ili ushahidi huo upokelewe mahakamani. Alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria husika, taratibu, pamoja na misingi ya uhalisia, uaminifu na uadilifu wa ushahidi huo.

“Katika zama hizi za teknolojia, Mahakama haziwezi kukwepa ushahidi wa kielektroniki. Hata hivyo, ni wajibu wa Mahakama kuhakikisha kuwa, ushahidi huo umepatikana na kuhifadhiwa kwa njia halali na kwamba haujabadilishwa,” alisema  Jaji Dkt. Mambi.

Aliongeza kuwa Mahakimu na Majaji wanapaswa kuwa makini katika kupima uzito wa ushahidi wa aina hiyo, hususan ujumbe wa simu, barua pepe, rekodi za miamala ya kielektroniki na vielelezo vinavyotokana na mitandao ya kijamii.

Kwa upande wake,  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert Martin Chuma alipowasilisha mada ya Maadili na Mienendo ya Kimahakama kwa njia ya Mtandao, alisisitiza kuwa maadili ni nguzo kuu ya uaminifu wa Mhimili wa Mahakama akieleza kuwa, huo ni wajibu wa kikatiba kisheria, kitaaluma na kimaadili akitolea mifano mbalimbali ya ibara za katiba, vifungu vya sheria na kanuni za maadili.

“Heshima na imani ya wananchi kwa Mahakama inaanzia kwenye mienendo yetu sisi Majaji na Mahakimu. Nidhamu ya kimahakama ni wajibu wa kikatiba, kisheria na kitaaluma,” alieleza.

Alifafanua kuhusu misingi ya uhuru wa kimahakama kwa kufanya kazi bila kupendelea, huba, hofu wala chuki na kuzingatia uadilifu, kujiepusha na mgongano wa maslahi pamoja na wajibu wa kuilinda hadhi ya Mahakama ndani na nje ya mazingira ya kazi.

Mafunzo hayo yaliwashirikisha Majaji wa Kanda hiyo wakiwemo Mhe. Dkt. Zainabu Mango na Mhe. Frank Mirindo pamoja na Naibu Msajili, Mahakimu Wakazi Wafawidhi na Mahakimu wa ngazi mbalimbali kutoka katika Kanda husika.

Washiriki walipata fursa ya kuuliza maswali, kubadilishana uzoefu, na kujadili changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa sheria na maadili ya kimahakama katika mazingira ya sasa yanayokua kwa kasi ya matumizi ya teknolojia.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Juma Mambi akiwasilisha mada kuhusu halali wa kupokelewa kwa ushahidi wa kielektroniki kwa Majaji na Mahakimu wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora yaliyotolewa hivi karibuni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi-Mahakama ya Hakimu Mkazi Tabora, 
Mhe. Gabriel Patrick Ngaeje akieleza wasifu wa 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Simiyu, Mhe. Wilbert  Martin Chuma ambaye alifundisha kwa njia ya mtandao kuhusu Maadili na Mienendo ya Kimahakama wakati wa mafunzo.

Mahakimu wa ngazi mbalimbali wakifuatilia mada kwa umakini ili kuimarisha utoaji wa haki.

Washiriki wa mafunzo
wakifurahia mada jambo wakati wa mafunzo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, 
Mhe. Pamela Mazengo  akizungumza wakati wa mafunzo hayo.


Hakimu Mkazi, Mhe. Felix Ginene (aliyesimama) akichangia mada wakati wa Mafunzo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni