Alhamisi, 19 Machi 2026

NCHI WANACHAMA UMOJA WA MATAIFA WAKUTANA KUJADILI HALI YA WANAWAKE DUNIANI

  •  Mkutano Wa Hali Ya Wanawake Duniani (CSW 70) Wafunguliwa Rasmi Jijini New York
  • Waziri Gwajima atoa Taarifa Ya Tanzania
  • Wanachama wa TAWJA nao washiriki katika mkutano huo

Na WMJJWM, New York-Marekani

Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa zimekutana jijini New York nchini Marekani kwa lengo la kujadili hali ya wanawake katika nchi hizo.

Mkutano huo ni wa 70 kuhusu Hali ya Wanawake Duniani unaoongozwa na Kaulimbiu isemayo "Kuhakikisha na Kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa Wanawake na Wasichana wote, ikiwa ni pamoja na kukuza mifumo ya kisheria nyenye usawa na jumuishi, kuondoa sheria, sera, na desturi za kibaguzi na kushughulikia vikwazo vya kimuundo", (Ensuring and Strengthening access to justice for all Women and Girls, including by promoting inclusive and equitable legal system, eliminating discriminatory laws, policies, and practices and addressing structural barriers”).

Mkutano huo ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  António Guterres tarehe 09 Machi, 2026 na kumalizika leo tarehe 19 Machi, 2026.

Miongoni mwa washiriki waliohudhuria katika Mkutano huo ni pamoja na sehemu ya Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho, Mhe. Barke Sehel.

Mkutano huo umejadili masuala mbalimbali ya upatikanaji wa haki na huduma kwa Wanawake ikiwemo haki ya upatikanaji wa Ardhi, haki kwa upatikanaji wa Elimu, haki ya kujua masuala ya sheria na upatikanaji wa haki za kisheria, kushiriki katika masuala ya uongozi na siasa, haki ya kumilili na upatikanaji wa huduma bora za Afya.

Siku ya kwanza ya mkutano huo, Tanzania iliongozwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Felister Mdemu, Wataalamu kutoka Wizara hiyo, Wizara nyingine za Kisekta, Taasisi za Serikali na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.

Aidha taarifa ya Nchi katika Mkutano huo ilitolewa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima.

Madhumuni ya mkutano huo yalikuwa kutafakari juu ya kuimarisha sauti ya Afrika katika CSW, kupokea taarifa kuhusu mazungumzo na kubadilishana maoni kuhusu ugombea wa Afrika kuwa mwenyeji wa mzunguko wa kwanza wa kikanda wakati wa CSW74 utakaofanyika mwaka wa 2030.

Aidha, katika mkutano huo masuala mbalimbali yalijadiliwa ikiwa ni pamoja na Mkataba wa Wanawake wa Afrika wa Kukomesha Unyanyasaji Dhidi ya Wanawake, masuala mbalimbali yanayohitaji kushughulikiwa kimkakati Afrika na kuja na sauti moja na mengine.

Katika mkutano huo iliamuliwa kuwa ili kuimarisha msimamo wa pamoja, Ofisi ya CSW inapaswa kujumuisha wawakilishi na wanachama kutoka Afrika katika hatua zote, kitaifa na kimataifa, ⁠Afrika inapaswa kusimama imara juu ya yale ambayo yamefikiwa kutoka kwa jukwaa la Beijing na inapaswa kutumika kama sehemu ya marejeo.

Iliamriwa pia kuwe na ushirikiano thabiti na mawasiliano ya Kimkakati yanayoungwa mkono na data yanapaswa kutumika kufuatilia maendeleo yaliyopatikana kufikia sasa.

Wana-TAWJA (Tanzania Women Judges Association) walishiriki katika side event ya MOCLA iliyokuwa na kichwa cha habari: "Kuimarisha Upatikanaji wa Haki kwa Wanawake na Wasichana. Huduma za Misaada ya Kisheria katika Kukabiliana na Ukatili wa Kijinsia na Kuwawezesha Wanawake".

Katika side event hiyo, Mhe. Barke Sehel Jr., Mwenyekiti wa TAWJA, ndio aliyefungua, na ilifungwa na Mhe. Sauda Mjasiri (Rtd J).

Matukio katika picha Mkutano wa Mkutano Wa Hali Ya Wanawake Duniani (CSW 70) na ushiriki wa Wana Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) katika Jiji la New York nchini Marekani.


Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (wa pili kushoto) pamoja na Wanachama wengine wa Chama hicho wakiwa kwenye Mkutano Wa Hali Ya Wanawake Duniani (CSW 70) jijini New York nchini Marekani.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima akiwasilisha mada katika mkutano huo.









Jaji Mkuu wa Mahakama ya Kenya na Rais wa Mahakama ya Juu ya Kenya, Mhe. Martha Koome (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sauda Mjasiri katika Mkutano wa Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.


Juu ni picha mbalimbali za Wana TAWJA na wanachama wengine walioshiriki Mkutano wa CSW katika Jiji la New York nchini Marekani wakiwa katika picha ya pamoja na 
Waziri  wa Wanawake, jinsia na maendeleo ya jamii, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni