Ijumaa, 3 Aprili 2026

 MAHAKAMA YA TANZANIA YANG’ARA KIMATAIFA KATIKA UTAALAMU WA MATUMIZI YA AKILI UNDE

  •  Wasilisho la Jaji Dkt. Adam Mambi lawavutia wengi

Na Mwandishi-Mahakama

Mahakama ya Tanzania imeng’ara Kimataifa katika utaalamu wa matumizi ya Akili unde (Artificial Inteligence) na ushahidi wa teknoljia unaotokana na Akili unde baada ya Wasilisho lililofanywa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora Mhe. Dkt. Adam Mambi kuvutia wengi.

Jaji Mambi aliwasilisha Mada kuhusu matumizi ya akili unde na namna kupokea na kuchambua Ushahidi wa kielektroniki unaozalishwa na akili unde mahakamani wakati wa Mafunzo ya Matumizi ya Akili unde kwenye utoaji wa haki mahakamani  yaliyofanyika hivi karibuni jijini Victoria Falls nchini Zimbabwe.

Aidha, Jaji Mambi ambaye pia ni Mtaalam wa Sheria za Tehama, Usalama Mtandaoni na Akili unde alialikwa kutoa mada kwenye Mafunzo ya Matumizi ya Akili Unde katika utoaji wa haki mahakamani ya Majaji, Mahakimu na Wanasheria wa Zimbabwe ambayo pia yaliwahusisha wanasheria wa nchi za Afrika kusini, Ethiopia na Kazakhstan.

.  Akitoa Mada hiyo kwa Majaji na Mahakimu zaidi ya 120 katika Mafunzo hayo, Jaji Mambi aliwafundisha aina mbalimbali za ushahidi unaotokana na matumizi ya akiliunde na changamoto watakazokutana nazo katika kupokea na kuchambua ushahidi unaotengenezwa au unaoboreshwa kwa kutumia akiliunde.

Akitoa mifano ya kesi kutoka nchi Mbali Mbali, Mheshimiwa Dkt. Mambi pia aliwaeleza  juu ya masharti na misingi ya kisheria inayohusu upokeaji na uchambuzi wa ushahidi wa kielektroniki akilinganisha na ushahidi unaozalishwa na akiliunde kama vile sauti, picha, video, Ushahidi uliotengenzwa kwa kutumia akili unde pamoja na changamoto zake.

Katika mada hiyo, Jaji Mambi pia alielezea juu ya nafasi ya Akiliunde katika kusuluhisha migogoro nje ya Mahakama (ADR) na katika tasnia ya Miliki bunifu (Intellectual Property). Aidha, Washiriki hao pia walijifunza aina mabalimbali za Ushahidi wa kielektroniki unaotokana na Akiliunde na namna ya kubaini taarifa za kutungwa au ushahidi wa kutengenezwa kwa kutumia teknolojia  feki (Deepfake).

Jaji Mfawidhi huyo pia walifundisha namna ya kutumia Akiliunde kubaini kesi za uwongo zinazoweza kuwasilishwa na mawakili wanaotumia akiliunde pasipo kujiridhisha huku akitoa mifano ya kesi mbalimbali toka nchi mbalimbali duniani.

Katika mafunzo hayo, Mhe. Dkt. Mambi pia aliwafundisha washiriki juu ya nafasi ya Mahakama katika kutafsiri Sheria na sera zinazogusa akili unde pamoja na kuweka misingi endelevu wakati wa kutoa maamuzi yao. Aidha, washiriki walijifunza kwa vitendo namna ya kutumia zana za akiliunde (AI Tools) katika kufanya utafiti, Kuchambua kesi na kuandaa maamuzi.

Mada nyingine zilizowasilishwa kwenye mafunzo hayo ni pamoja na Maadaili ya Taaluma (Professional Ethics) katika matumizi ya akili unde, taarifa za faragaha (Data Protection), Usalama mtandaoni (Cyber Security) na Miliki bunifu (Intellectual Property) katika tasnia ya Akili Unde.

Akifunga mafunzo hayo, Jaji Mkuu wa Zimbabwe Mhe. Luke Malaba alimshukuru Jaji Mambiambaye ni mbobezi wa kimataifa katika masuala ya akiliunde na TEHAMA kwa mafunzo mazuri aliyotoa yatakayowasaidia Majaji na Mahakimu wa Zimbabwe katika kurahisisha kazi zao za utoaji wa haki.

Aidha Malaba pia alimshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania kwa kumruhusu Jaji Mambi Kwenda kutoa mafunzo Zimbabwe na kuahidi kuimarisha ushirikiano zaidi na Mahakama ya Tanzania. Alisema kuwa Majaji wanahitaji mafunzo kwa vitendo katika maeneo ya tekonolijia zinazoibuka kwa kasi kama akili unde.

Kwa upande wao, washiriki wa mafunzo hayo waliishukukuru Mahakama ya Zimbabwe kwa kualika mtaalamu Sheria za Mitandao na Akiliunde aliyetoa mafunzo ya aina yake kwa vitendo zaidi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora Mhe. Dkt. Adam Mambi akitoa Mada kwenye Mafunzo ya Matumizi ya Akili Unde katika utoaji wa haki mahakamani hivi karibuni katika mji wa Victoria Falls nchini Zimbabwe. Jaji Mambi pia ni mtaalamu wa Sheria za Tehama, Usalama mtandaoni na Akili Unde.   

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora Mhe. Dkt. Adam Mambi akijibu hoja mbalimbali za wajumbe mara baada ya kuwasilisha Mada kwenye Mafunzo ya Matumizi ya Akili Unde katika utoaji wa haki mahakamani hivi karibuni katika mji wa Victoria Falls nchini Zimbabwe.   

Sehemu ya Washiriki wa Mafunzo ya Matumizi ya Akili Unde katika utoaji wa haki mahakamani wakiwa kwenye Mafunzo hayo mjini Victoria Falls nchini Zimbabwe. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni