Jumanne, 5 Mei 2026

JAJI NONGWA AHITIMISHA MICHEZO NJOMBE KWA WANA MAHAKAMA SPORTS

·        Mahakama Sports yashinda Makombe manne Njombe mashindano ya michezo Mei Mosi

·       Asisitiza umuhimu wa Michezo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa amewasisitiza Wanamichezo wa Mahakama Sports na Watumishi wengine Mahakama juu ya umuhimu wa Michezo na kusema kuwa ina faida nyingi ikiwemo kulinda afya ya mwili, pia ni ajira, vilevile huleta furaha pamoja na ushirikiano.

 

Mhe. Nongwa aliyasema hayo hivi karibuni alipohudhuria hafla ya usiku ya kuhitimisha michezo Mkoani Njombe iliyofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya ‘Agreement’ mkoani Njombe.

 

Katika hafla hiyo, alikuwepo pia Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Martine Mushi, Makamu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Maria Mayalla na Wanamichezo wa Mahakama Sports.

 

Naye, Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Donald Tende aliwasilisha taarifa aliyoisoma mbele ya Mhe. Nongwa pamoja na Wanamichezo ambapo alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwalinda na kuwajaalia afya njema na kuwakinga na maradhi na majeraha mbalimbali wakati wote wa mashindano.

 

“Pili, naushukuru Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kutupatia ruhusa na uwezeshaji wa rasilimali fedha wa kutuwezesha kushiriki kikamilifu katika mashindano ya Mei Mosi, 2026,” alisema Bw. Tende.

 

Vilevile, aliwashukuru Wachezaji wa Mahakama Sports walioshiriki mazoezi na mashindano kwa kujituma na kujitoa kwao katika kipindi chote kwa manufaa ya Timu ya Mahakama ya Tanzania.

 

Katibu huyo wa Mahakama Sports aliendelea kusema kuwa, “Wafanyakazi wanaoshiriki michezo ni kundi mojawapo la wafanyakazi wanaotegemewa na Taifa kiuchumi, kijamii na huduma mbalimbali kwa umma.” 

Bw. Tende aliongeza kuwa, Timu ya Michezo ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ilishiriki kikamilifu katika Mashindano ya Mei mosi yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe kuanzia tarehe 13 Aprili, 2026 hadi 01 Mei, 2026.

Alisema kuwa, Mashindano hayo yalifunguliwa rasmi tarehe 20 Aprili, 2022 na Mgeni Rasmi aliyekuwa Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo.

 Mashindano ya Mei Mosi yamelenga kusherehesha Sikukuu ya Wafanyakazi ili kuboresha mahusiano baina ya watumishi wa umma,  kutoka Wizara, Mashirika, Taasisi na Idara mbalimbali za Serikali, pamoja na jamii lengo likiwa ni kuboresha na kulinda afya za watumishi na kuimarisha nguvu kazi katika utumishi wa umma. 

Bw. Tende alibainisha kupitia taarifa yake kuwa katika michezo hiyo jumla ya Wizara, Idara, Taasisi za Umma, Mashirika ya Umma 61   walishiriki mashindano hayo ikiwemo Mahakama ya Tanzania.

Alieleza kuwa, Timu ya Mahakama ilijumuisha washiriki 84 na Timu ya ‘Mahakama Sports Club’ ilishiriki jumla ya michezo saba ambapo  iliweza kunyakua jumla ya Makombe manne ambayo ni Kamba mshindi wa tatu, Karata mshindi wa kwanza, Baiskeli mshindi wa pili na Mchezo wa Bao ni mshindi wa pili.

Wanamichezo wa Mahakama Sports ni watumishi kutoka katika Mahakama mbalimbali zilizopo nchini Tanzania ambapo wanamichezo hao wamejikita katika michezo  kama vile Mpira wa Miguu, Netiboli, Kamba Wanawake, Kamba Wanaume, Riadha, Kurusha Tufe, Drafti Karata, Baiskeli na Bao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wana Mahakama Sports. Wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, wa pili kushoto ni  Mwenyekiti wa Michezo Mahakama Sports, Mhe. Martine Mushi, wa kwanza kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Mhe. Maria Mayalla na wa kwanza kushoto ni Katibu wa Michezo Mahakama Sports, Bw. Robert  Tende. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa (aliyesimama) akizungumza na Wana Mahakama Sports kuhusu umuhimu wa michezo na kutoa hongera kwa wana michezo hao. Kushoto ni Mwenyekiti wa Michezo wa Mahakama Sports Mhe. Martine Mushi.

Katibu wa Mahakama Sports Club,  Bw. Robert  Tende akisoma taarifa ya michezo tangu walipoanza mpaka walipomaliza na mashindano ya michezo ya Mei Mosi, 2026.



Sehemu ya wageni waalikwa na wanamichezo waliohudhuria kwenye hafla hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

 

 

 

 

 

 

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni