Na
ARAPHA RUSHEKE- Mahakama Kuu Dodoma.
Mahakama Kuu ya Tanzania,
Masjala Ndogo ya Dodoma imeingia katika awamu mpya ya uongozi jana tarehe 18 Juni,
2026, baada ya Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Joachim Tiganga, kukabidhiwa ofisi na
mtangulizi wake, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama
ya Rufani.
Makabidhiano hayo yalijikita
katika kukabidhi majukumu ya kiutawala, nyaraka mbalimbali za ofisi, na taarifa
muhimu za utendaji kazi, zote zikiwa na lengo la kuhakikisha mwendelezo wa
utoaji wa huduma za kimahakama na usimamizi wa shughuli za Mahakama katika
Masjala Ndogo hiyo.
Akizungumza katika
hafla hiyo ya makabidhiano, Mhe. Dkt. Masabo alimpongeza Jaji Tiganga kwa
kukabidhiwa majukumu hayo na kumtakia mafanikio katika utekelezaji wake.
“Nitumie fursa hii
kumpongeza Mhe. Tiganga, tunaungana nawe kumshkuru mwenyezi Mungu kwa kibali
ambacho amekupatia ili uje uhudumu hapa uwatumikie watu wake. Namshukuru pia Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, kwa imani kubwa ambayo ameionesha kwako
na kuona ni muda sahihi kuweza kufanya kazi katika kituo hiki cha Dodoma,”
alisema.
Naye Mhe Tiganga
aliwashukuru Viongozi na Watumishi wote wa Mahakama Kuu Dodoma kwa mapokezi
mazuri aliyoyapata na alisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano uliopo ili
kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa Wananchi.
Makabidhiano hayo
yanaashiria mwanzo wa awamu mpya ya uongozi katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma,
huku yakisisitiza dhamira ya kuendeleza ufanisi, uwazi na ubora katika utoaji
wa huduma za Mahakama kwa Wananchi kwa kuzingatia salamu ya Mahakama isemayo
Uadilifu,Weredi na Uwajibikaji.
Jaji
wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (wa kwanza kulia)
akikabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga,
wakati wa hafla ya makabidhiano iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu
Dodoma Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).

Watumishi
wa Mahakama Kuu Dodoma wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa kumpokea Jaji Mfawidhi
mpya mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Mahakama Kuu Masjala ndogo
Dodoma.

Meza
Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (aliyepo
katikati waliokaa), kulia kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe.
Joachim Tiganga na kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Biswalo
Mganga, ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Mahakama Kuu Dodoma
waliohudhuria hafla hiyo ya makabidhiano.

Meza
Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (aliyepo
katikati waliokaa), kulia kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe.
Joachim Tiganga na kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Biswalo
Mganga, ikiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma
waliohudhuria hafla hiyo ya makabidhiano.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (aliyepo
katikati) na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe.
Joachim Tiganga (kulia) wakisaini nyaraka za makabidhiano. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Biswalo
Mganga, anayeshughudia zoezi hilo.

Baadhi
ya watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma waliohudhuria hafla hiyo ya makabidhiano.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.