Jumamosi, 6 Septemba 2025

TIMU ZA MAHAKAMA SPORTS ZATINGA 16 BORA MASHINDANO YA SHIMIWI

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Mwanza

Timu za Mpira wa Miguu, Netiboli na Kamba zimefuzu kuingia 16 bora katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) yanayofanyika katika viwanja mbalimbali jijini Mwanza.

Akizungumza leo tarehe 06 Septemba, 2025 jijini Dodoma, Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Tende amesema hatua ya makundi imeisha katika timu za Kamba, Netiboli na Mpira wa Miguu ambapo Kamba wanawake na wanaume wanaongoza katika makundi yao. Kwa upande wa netboli na mpira wa miguu wameshika nafasi ya pili katika makundi. 

Katika mchezo wa Kamba wanawake walikuwa kundi A ambapo kulikuwa na Timu ya Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Mkoa wa Kagera, Mahakama, Katiba na Sheria na Hazina ambapo Mahakama ilifanikiwa kuwavuta kwa mivuto yote miwili hivyo kusababisha kuingia 16 bora  kwa pointi sita.

Katika Mchezo wa Kamba wanaume walikuwa kwenye kundi B ambapo kulikuwa na Timu kutoka Mahakama, Viwanda, Kilimo na Maji ambapo Mahakama Sports ilifanikiwa kuivuta Timu kutoka Viwanda na Kilimo kwa mivuto miwili lakini Timu ya Maji walifanikiwa kuwavuta mvuto mmoja na mvuto mmoja walitoka sare na kusababisha kuingia 16 bora kwa pointi tano.

Kwa upande wa Mpira wa Miguu Timu ya Mahakama ilikuwa kundi E pamoja na Timu ya Madini, OSHA, Kilimo, Mahakama na Wakili Mkuu ambapo Timu ya Mahakama ilimfunga Wakili Mkuu bao moja kwa nunge, bao hilo lilifungwa na Mchezaji mchachali wa Mahakama Sports, Bw. Martine Mpanduzi baada ya mpira wa kona kuchongwa na mchezaji Seif Shamte na hivyo kufanikiwa kushinda katika mechi hiyo.

Na katika Mechi ya Mahakama na Timu kutoka Wizara ya Madini Mahakama ilishinda kwa bao mbili kwa moja ambapo bao la kwanza lilifungwa na Seif Shamte na la pili lilifungwa na Martine Mpanduzi kwa usaidizi wa Seif Shamte na kusababisha ushindi kwa mara nyingine katika mchezo wa mwisho wa kundi hilo, Mahakama ilicheza na timu ya OSHA na kufungwa bao moja kwa nunge na hivyo kusababisha kupata pointi tisa na kuingia katika 16 bora.

Aidha, Timu ya Netiboli ya Mahakama iliyokuwa katika kundi F lililojumuisha timu kutoka Uwekezaji, Timu kutoka Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Katavi, Ukaguzi, Mahakama na Timu kutoka GST na kufungwa na Uwekezaji kwa magoli 32 kwa 24 na baada ya hapo Mahakama iliwafunga GST magoli 41-11, uwekezaji magoli 33-11 na RAS Katavi magoli 43-11 na hivyo kufanikiwa kutinga 16 bora wakiwa na pointi sita.

Katika hatua hiyo, ya makundi Timu za Netiboli na Mpira wa Miguu wamepoteza mechi moja moja na kushinda mechi zingine zote.

Akizungumza baada ya timu hizo kushinda na kuingia 16 bora, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Club, Bw. Wilson Dede amesema amefurahi na kushukuru timu zake kufikia hatua hiyo huku akisema kuwa, matokeo hayo yametokea kutokana na nidhamu ya wachezaji na ushirikiano mkubwa baina ya wachezaji lakini pia mazoezi. 

Bw. Dede ameongeza kwamba, wamejiandaa kwa hatua nyingine ya mtoano ambapo maandalizi yanaendelea vizuri na ana matumaini ya kufika mbali katika mashindano hayo.

Mfungaji wa Timu ya Netiboli (GS) wa Mahakama Sports, Bi. Tatu Mawazo akifunga goli wakati wakicheza na Timu ya RAS Katavi leo tarehe 06 Septemba, 2025 jijini Mwanza.

Kikosi cha netiboli kikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi kabla ya mechi yao dhidi ya Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Katavi.

Kikosi cha Mahakama Sports Mpira wa Miguu kabla ya kuvaana na Timu ya OSHA.

Timu ya Kamba wanawake wakiwa katika picha ya pamoja na Kocha wa Kamba Rajab Mwariko (wa kwanza kulia) na na Naibu Katibu wa Mahakama Sports, Bi. Theodosia Mwangoka.

Timu ya Kamba wanaume Mahakama Sports wakiwa katika picha ya pamoja.

Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Tende akizungumza wakati wa mahojiano.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

MWAJABU BWIRE WA MAHAKAMA SPORTS ANG'ARA MBIO ZA BAISKELI SHIMIWI MWANZA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Mwanza

Mwendesha baiskeli machachali wa Timu ya Mahakama ya Tanzania-Mahakama Sports, Bi Mwajabu Bwire ameibuka kidedea kwenye mchezo wa mbio za baiskeli wanawake  katika mashindao ya Michezo ya 39 ya Shirikisho la Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) yanayofanyika jijini Mwanza.

Akizungumza baada ya mashindano hayo leo tarehe 06 Septemba, 2025, Bi. Mwajabu amesema alianza kushiriki mashindano hayo SHIMIWI mwaka jana Morogoro na kushika nafasi ya nne kutokana na kutokuwa na vifaa vya mchezo huo lakini mwaka huu Mahakama imemuwezesha vitendea kazi na mazoezi mazuri ndio yamechangia kuleta matokeo hayo.

"Nasikia furaha sana kwa kupata nafasi ya kwanza na kumshinda bingwa mtetezi wa mchezo huu mwaka jana vifaa vilikuwa hakuna ndio maana sikuweza kufanikiwa," amesema Mwanamichezo huyo.

Bi. Mwajabu Bwire ameshinda mbio hizo za Kilometa 30 akitumia saa moja na dakika nane, kwa upande wa wanaume Mahakama imeshika nafasi ya nne baada ya Mwakilishi Gerald Robert kufanikiwa kupata nafasi hiyo. 

Amesema pia, alianzia namba nne akaja mbili na leo hii amekuwa mshindi namba moja. Amechukua fursa hiyo kuwashukuru Wana Mahakama Sports kwa kumtia moyo katika mbio hizo na hatimaye kufika katika nafasi hiyo.

Aidha, hii ni mara ya kwanza kwa Mahakama kutoa mwakilishi upande wa wanaume katika mbio hizo za Baiskeli. Akizungumza na Mwandishi wa Habari hii, Mwakilishi huyo amesema amepata matokeo hayo kutokana na maandalizi hafifu ya mchezo huo na kifaa cha mashindano hayo kutokuwa na viwango bora.

"Ukiangalia mshindi namba moja, mbili na tatu baiskeli zao zilikuwa na viwango tofauti na ya kwangu," amesema Bw. Robert akiongeza kuwa, anajiandaa kwa mwakani akipata vifaa vizuri na mazoezi mazuri atafika nafasi nzuri zaidi.

Naye Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Bw. Wilson Dede amesema kwa upande wa wanaume, imekuwa mara ya kwanza kushiriki na mshiriki aliyefanya mazoezi ya mbio hizo alipata ajali akiwa mazoezini na kusababisha majeraha na Daktari kushauri kutoshiriki kutokana na hali yake kutoimarika kiasi cha kuingia katika mashindano hayo kwakuwa Mahakama ina watu wana vipaji vingi, Mwanariadha Gerald Robert aliomba kuingia katika mashindano hayo na kushika nafasi ya nne, ambapo amekiri kuwa ameshika nafasi hiyo kwakuwa hakuwa na maandalizi mazuri na kutokuwa na vifaa vya mchezo huo.

Kadhalika, amesema hii ni mara ya pili kwa Mahakama Sports kutoa washiriki katika mbio za baiskeli katika mashindano hayo na mara ya kwanza mshiriki Bi. Mwajabu Bwire alishika nafasi ya nne.

Mashindano hayo ya mbio za baiskeli yalianzia makaburi ya Mv Bukoba Igoma mpaka Isangijo na kurudi wakati mbio za baiskeli wanaume kilometa 50 yameanzia makaburi ya Mv Bukoba mpaka Nyangune na kurudi.

Mwanamichezo kutoka Timu ya Mahakama ya Tanzania- Mahakama Sports, Bi. Mwajabu Bwire akijiandaa kuanza mashindano ya mbio za baiskeli katika eneo la  Makaburi ya Mv Bukoba Igoma jijini Mwanza leo tarehe 06 Septemba, 2025.

Mwendesha Baiskeli wa Mahakama Sports, Bw. Gerald Robert akiwa katika kinyanganyiro cha ushindi wakati wa mashindano ya mchezo wa mbio za baiskeli.

 

 Mshindi namba moja wa Mbio za Baiskeli -Mashindano ya 39 ya SHIMIWI, Bi. Mwajabu Bwire (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Maafisa Utumishi wa Mahakama ya Tanzania. Kushoto ni Bw. Nkrumah Katagira na na kulia ni Bw. Peter Machalo.

Upozaji koo baada ya ushindi ukiendelea.....

Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Bw. Wilson Dede (kulia) katika picha ya pamoja na Afisa Utumishi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Peter Machalo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Alhamisi, 4 Septemba 2025

BENKI YA DUNIA YAPONGEZA KASI YA UJENZI WA JENGO LA IJC KATAVI

Na. Ally Ally Ramadhani – Mahakama, Katavi

Kiongozi wa Msafara wa Benki ya Dunia Bi. Christine Owuor, amepongeza kasi ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Katavi.

Ameyasema hayo jana tarehe 03 Septemba, 2025 wakati wa ziara ya hiyo iliyokuwa na lengo la kukagua mradi wa ujenzi jengo hilo la kisasa la Mahakama ya Tanzania ya litakalo tumika kutoa haki kwa wananchi wa Mkoa huo.

Akitoa taarifa ya  maendeleo ya mradi wa ujenzi wa jengo la hilo mkoani hapo Mhandisi  Victor Vedasto ambaye ni mwakilishi wa Mkandarasi kampuni ya AZHAR Construction Co. Ltd, alisema mradi huo umefikia asilimia 76.1 za utekelezaji wake na kuongeza kuwa tayari kazi za umaliziaji wa jengo zinaendelea.

Aidha, Mhandisi huyo aliongeza kuwa, mradi huo unahusisha sehemu tatu ambazo ni jengo Kuu, eneo la nje (uzio, mgahawa, chumba cha ulinzi) pamoja na Manzari (Landscaping).

Vilevile, akieleza kuhusu mradi huo, Mhandisi na mtaalam wa manunuzi Bw. Fedrick Nkya kutoka Benki ya Dunia alishauri kuzingatia uwepo wa mfumo wa mifereji ya kupitisha maji nje ya jengo ili kuzuia maji kuingia eneo la jengo hasa kipindi cha mvua za masika.

Naye, Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Angelo Rumisha akiwa kwenye ziara ya Benki ya Dunia ya kukagua  mradi wa ujenzi wa jengo hilo la Mahakama, alisema jengo hilo linalojengwa na Kampuni ya AZHAR Construction Co. Ltd. linatarajiwa kukamilika Mwezi Novemba, 2025.

Jaji Rumisha aliongeza kuwa, ”tumepokea pongezi hili linatupa nguvu ya kuendelea kuongeza kasi kwa kushirikiana na timu nzima ili ifikapo mwezi Novemba 2025 mradi wetu uwe umekamilika kama tulivyo kubaliana na kampuni inayojenga jengo letu la IJC – Katavi”.

Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama aliongeza kuwa, nguzo ya pili ya Mpango Mkakakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania inasisitiza Utoaji Haki kwa wakati. Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huu kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hiyo.

Kiongozi wa msafara wa Benki ya Dunia Bi. Christine Owuor, (wa kwanza mbele) akikagua ujenzi wa IJC KATAVI.

Mhandisi Victor Vedasto, akitoa maelezo kuhusu maendeleo ya mradi wa ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Katavi kwa kiongozi wa msafara wa Benki ya Dunia Bi. Christine Owuor.


Msanifu Linda Kasilima, mshauri wa mradi kutoka kampuni ya Crystal Consultant akielezea maendeleo ya Mradi wa ujenzi IJC KATAVI kwa timu ya msafara wa Benki ya Dunia.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho Mhe. Dkt. Angelo Rumisha akitoa maelezo kwa kiongozi wa Msafara wa Benki ya Dunia wakati wa ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa IJC Katavi.


 

JAJI MKUU AWAAGIZA MAJAJI, WATENDAJI WA MAHAKAMA KUANZA UTEKELEZAJI WA DIRA, 2050

·       Asisitiza pia uwajibikaji katika kazi

·       Atoa rai kwa Majaji, Watendaji kusimamia maadili ya watumishi walio chini yao

Na MARY GWERA, Mahakama- Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Majaji na Viongozi wa Mahakama nchini kuanza maandalizi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 kwa kufuata miongozo iliyowekwa ya utekelezaji wa dira hiyo.

Akizungumza jana tarehe 03 Septemba, 2025 wakati akifunga Kikao Kazi cha siku tatu cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kilichofanyika kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Masaju alisema kuwa, eneo la Utawala bora na Haki ni kipaumbele cha kwanza kilichoainishwa katika Dira hiyo hivyo, ni muhimu kwa Mahakama kushiriki katika utekelezaji wake ili kuboresha eneo la utoaji haki.

“Niwaombe tufanye maandalizi sasa kwa ajili ya utekelezaji wa Dira hii kwa mujibu wa mwongozo tuliowekewa na hii dira imeweka pia mpango wa utekelezaji,” alisema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alisema huku akirejea ukurasa wa 63 wa Dira hiyo ambao unasema, “ili kuhakikisha kuwa Dira 2050 inatekelezwa kwa ufanisi, Serikali imeweka mfumo imara wa usimamizi unaozingatia malengo yake mahsusi, mfumo huu umekusudia kuhimiza uwajibikaji, ukihitaji uongozi mahiri na ulio makini katika ufuatiliaji, aidha mfumo unahimiza matumizi ya mbinu zitakazotoa matokeo yanayopimika.”  

Aliwahimiza viongozi hao kwa kuwaeleza kuwa, ambao bado hawajasoma Dira hiyo, kuisoma ili kuielewa ipasavyo na kuanza utekelezaji wake. Akisisitiza kuwa, Dira hiyo inasisitiza kwamba, msingi wa mkakati huo ni mabadiliko makubwa ya kifikra ambayo yanalenga kwenye vitendo zaidi kuliko maneno na matokeo badala ya ahadi.

Akirejea Dira hiyo, Jaji Mkuu alisema, “Uongozi, Taasisi pamoja na watendaji na wadau wote wanapaswa kuwajibika kutimiza malengo la dira kwa ufanisi......”

Kadhalika, Jaji Mkuu aliwakumbusha Majaji hao kuendelea kuishi viapo vyao na kusimamia haki ipasavyo kwa kuzingatia Katiba na Sheria  za Nchi.

"Tutambue tunalo jukumu kubwa, kwanza Ibara ya 4 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 107A na Ibara ya 107B, sote tunazifahamu  lakini kubwa hapa sisi Mahakama ya Tanzania tumepewa jukumu ya kuwa mamlaka yenye kauli ya mwisho katika utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na katika hizi Ibara nilizozisoma hapa zimeweka na kanuni na mwongozo ukiacha yale maadili mengine ya utumishi wa Mahakama, niwaombe tuendelee kuzingatia haya," alisisitiza Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu aliendelea kuwasisitiza Majaji na Mahakimu kutekeleza jukumu la utoaji haki ipasavyo kwani ni kazi ambayo wamekasimiwa na Mungu na inatambulika hata kwenye Vitabu Vitakatifu vya Mungu ikiwemo Biblia na Quran, na kuwasihi kusoma Biblia kwenye Kitabu vya ‘Kumbukumbu la Torati 4:2, 6, Kutoka 18:21-22 na 2 Mambo ya Nyakati 19: 6-7.

Aidha, Mhe. Masaju aliwataka pia Majaji hao kudumisha umakini katika utekelezaji wa majukumu ili Mhimili wa Mahakama ya Tanzania uwe moja ya Mhimili wenye hadhi duniani.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu alitoa rai kwa Majaji, Mahakimu, watumishi wa Mahakama na wananchi wote kwa ujumla kuwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Uzoefu wangu ni kana kwamba wengi serikalini tumekuwa tukidhani kwamba mambo ya Taifa hili yanamuhusu Rais wa nchi wa hii peke yake na Viongozi kama Mawaziri na viongozi wengine Wakuu wa Mihimili na Watendaji Wakuu katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na kwetu sasa mahakamani tunafikiri kwamba mambo haya yanamuhusu Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi, Mtendaji Mkuu, Msajili Mkuu, Msajili wa Mahakama ya Rufani na hata Msajili wa Mahakama na wengine sisi sote hatuwajibiki,” alisema Mhe. Masaju.

Aliongeza kuwa, wengine wanadhani kwamba suala la uwajibikaji linawahusu makao makuu ya Mahakama ya Tanzania peke yake lakini wengine hatuhusiki na wakati fulani hata ambao wanahusika kwenye ngazi ya kanda wanadhani kwamba yanawahusu wao peke yao.

“Wakishatambua wajibu huo, kila mmoja atajiona ni mhusika kuanzia kiongozi wa juu kabisa mpaka mwananchi wa kawaida tukiwemo na sisi viongozi,” alisisitiza Mhe. Masaju.

Kadhalika, Jaji Mkuu alisema kuwa, ili kuboresha uwajibikaji ni muhimu watumishi wa Mahakama kuzingatia na kusimamia haki kwa kuhakikisha haki inatendeka, uadilifu, uwezo wa kumudu majukumu ipasavyo, kujiongeza, kuwa na ubunifu na kuwa na uzalendo wa nchi.

“Majaji Wafawidhi wasimamieni watumishi waliopo chini yenu kwa kutoa ushauri, kuwalea na inapobidi kutoa adhabu wanapokwenda kinyume na maadili,” alisisitiza Mhe. Masaju.

Katika kikao hicho ambacho kilihudhuriwa pia na baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mtendaji Mkuu, Msajili Mkuu na Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama kwa pamoja walipata fursa ya kubadilishana uzoefu katika utendaji kazi, kushirikishana kuhusu mafanikio na changamoto.

Kikao hicho kimetoka na maazimio kadhaa baadhi yake ni kuwa na ushirikishwaji wa viongozi katika miradi ya ujenzi katika hatua zote, kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi (mediation), haki za watumishi za kisheria zilipwe mapema ipasavyo na kikamilifu, ufanisi wa mifumo ya kielektroniki ya usikilizaji mashauri (TTS na e-CMS) ufanyiwe tathmini na kuboreshwa ili iwe rafiki zaidi kwa watumiaji na mengine.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Majaji Wafawidhi na Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania (hawapo katika picha) wakati akifunga Kikao Kazi cha siku tatu cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania  jana tarehe 03 Septemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.




Washiriki wa Kikao Kazi cha Majaji Wafawidhi wakiwa katika kikao hicho jana tarehe 03 Septemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.





    Washiriki wa Kikao Kazi cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakifuatilia kilichokuwa kikijiri katika kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 03 Septemba, 2025.

 

Jumatano, 3 Septemba 2025

MAHAKAMA SPORTS YAANZA KIBABE MASHINDANO YA SHIMIWI JIJINI MWANZA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Mwanza

Timu za Kamba (wanaume na wanawake), Mpira wa Pete na Mpira wa Miguu zimeanza vema michuano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) inayoendelea kwenye viwanja mbalimbali jijini Mwanza.

Katika michezo ya siku ya kwanza wanawake walivutana na Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Kagera na kutoka na ushindi wa bao mbili (2) kwa 0 katika mchezo huo wa vuta nikuvute Mahakama wanawake walifanikiwa kuvuta mivuto yote miwili na kupata ushindi.

Na katika siku ya pili Mahakama walivutana dhidi ya Timu ya Wizara Katiba na Sheria na kufanikiwa kuwavuta mivuto yote miwili hivyo kuondoka na ushindi.

Akizungumza baada ya mechi hiyo jana tarehe 02 Septemba, 2025, Nahodha Msaidizi wa Timu ya Kamba Wanawake, Bi. Eva Mapunda alisema siri ya ushindi huo ni mazoezi na ndio maana wanapata matokeo mazuri.

Aidha, Nahodha huyo amemuahidi Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuwa, watarudi na ushindi mnono na vikombe, kutokana na malezi mazuri wanayoyapata kambini hapo.

Kwa upande wa mchezo wa kamba wanaume ambapo siku ya kwanza walivutana na timu kutoka Viwanda na kufanikiwa kuwavuta mivuto yote miwili kama karatasi na kujichukulia pointi mbili  lakini katika mchezo wa pili baada ya kuona viwanda walivyovutwa kama karatasi Timu ya Kilimo waliingia mitini na kutokutokea uwanjani na hivyo kusababisha ushindi.

Katika michezo hiyo ya kamba kwa wanawake na wanaume iliyofanyika katika viwanja vya Furahisha jiji Mwanza timu za Mahakama wameshinda mechi zote mbili katika hatua hii ya makundi.

Nayo Timu ya Mpira wa Pete ya Mahakama imefanikiwa kushinda katika mchezo wake wa kwanza kwa kuifunga Timu ya GST magoli 41 kwa 11 katika mchezo uliofanyika katika viwanja vya CCM Kirumba, Nahodha wa timu hiyo, Akanganyila Theophil alisema wapinzani hao walikuwa wa kawaida na hivyo kusababisha ushindi huo kupatikana na kuongeza kuwa wamejiandaa vizuri kwa mechi ijayo ambapo wanatarajia ushindi mnono.

Katika mtanange uliofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mabatini B kati ya Timu ya Mahakama na Kilimo, kilimo walichokikimbia asubuhi kwenye kamba wanaume wamekutana nacho kwenye mpira wa miguu kwa kuchabangwa bao mbili kwa nunge, magoli hayo yalifungwa dakika ya 17 na ya 26 ya kipindi cha pili. Magoli hayo yote yalifungwa na mchezaji Muhamadi Ghafuru.

Kocha wa Timu ya Mpira wa Miguu, Spear Dunia Mbwembwe alisema ushindi huo uliopatikana ni salamu za shukrani kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel kwa kuwezesha timu kuishi vizuri kupata malazi mazuri, chakula na mavazi kwa kupindi chote tangu wamefika kambini hapo na hivyo Kocha huyo kuahidi kurudi na  vikombe.

Mashindano ya SHIMIWI yalianza tarehe 01 Septemba, 2025 na yanatarajiwa kufunguliwa rasmi tarehe 06 Septemba 2025. Mahakama ya Tanzania imepeleka jumla ya timu tisa ambazo ni Timu za Mpira wa Miguu, Mpira wa Pete, Kamba (wanawake na wanaume), Riadha, Baiskeli, Tufe, Karata na Bao.

Kikosi cha Timu ya Mpira wa Miguu cha Mahakama kabla ya mtanange.


Timu wa kamba wanawake baada ya mechi dhidi ya Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Kagera.

Timu ya Kamba Wanaume baada ya mechi dhidi ya Viwanda.

Kikosi cha Timu ya Mpira wa Pete kabla ya mechi kuanza.

Mfungaji wa Timu ya Mahakama akifunga goli.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Jumanne, 2 Septemba 2025

NAIBU MSAJILI MAHAKAMA ARUSHA ASISITIZA USHIRIKIANO NA JESHI LA POLISI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi amesema kuwa ushirikiano baina ya Mahakama na Jeshi la Polisi ni muhimu ili kuhakikisha mashauri ya jinai yanayoletwa mahakamani yanasikilizwa mapema ipasavyo kuepuka kuchelewesha haki za watu pamoja na kuzuia mlundikano wa mashauri usio wa lazima.

Mhe. Msumi aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akifungua Mafunzo ya Kubadilishana Uzoefu Kuhusu Utaratibu wa Ufunguaji na Uendeshaji wa Mashauri ya Jinai katika Mahakama za Mwanzo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) jijini Arusha.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Naibu Msajili alieleza kuwa, mafunzo hayo yalilenga kuongeza uelewa, kuimarisha weledi na kukuza ushirikiano kati ya Mahakama na Jeshi la Polisi lengo likiwa ni kuhakikisha mashauri ya jinai yanashughulikiwa kwa haraka, ufanisi na kwa mujibu wa sheria.

“Nawaomba washiriki kutumia kikamilifu fursa hii ya mafunzo kwa kuuliza maswali, kujadili changamoto na kubadilishana mbinu bora zinazoweza kusaidia kuboresha huduma za utoaji haki katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo,” alisisitiza Mhe. Msumi.

Akiwasilisha mada, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Themi, Mhe. Julieth Mbise alieleza kuwa, zipo changamoto nyingi zinazokwamisha uendeshaji wa haki jinai, ikiwemo kasoro katika hati za mashtaka, ucheleweshaji wa vielelezo, kutokuwepo kwa walalamikaji mahakamani na kutofuatwa kwa taratibu za upelelezi.

Mhe. Mbise alisisitiza kwamba, ushirikiano madhubuti kati ya Mahakama na Polisi ni muhimu ili kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati na kuimarisha imani ya wananchi kwa vyombo vya utoaji haki.

Naye Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Arusha, ASP Mahita Omary alizungumzia changamoto zinazolikabili Jeshi la Polisi katika kushughulikia mashauri kuwa, ni pamoja na watuhumiwa kujidhamini, adhabu ndogo zinazotolewa na Mahakama pamoja na Mahakama kuahirisha mashauri bila kujali kwamba mashahidi wameletwa kwa ajili ya shauri husika kusikilizwa.

Akizungumzia kuhusu suala la watuhumiwa kujidhamini wenyewe katika Mahakama za Mwanzo, ASP Mahita alisema kuwa, pamoja na kwamba dhamana ni haki ya mtuhumiwa kwa makosa yenye dhamana, Mahakama imekuwa ikitoa dhamana bila kuwa na taarifa za kina za mtuhumiwa na mdhamini wake, hali ambayo husababisha mtuhumiwa kutorudi mahakamani na Mahakama kulazimika kutoa tena hati ya kukamatwa mtuhumiwa huyo kwa Jeshi la Polisi.

Akitoa neno la kufunga mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Arusha, Mhe. Sheila Manento aliwahimiza washiriki kuzingatia uadilifu na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao, akibainisha kuwa hakuna haki bila uaminifu.

Aliwataka pia washiriki kuendeleza kujifunza kila mara ili kuendana na mabadiliko ya dunia ya sasa na kuwapongeza waandaaji wa mafunzo hayo kwa maandalizi bora na kuwashukuru washiriki wote kwa nidhamu na ushirikiano waliouonesha.

Kikao hicho kililenga kujadili changamoto, kueleza athari zake katika upatikanaji wa haki na kutoa mapendekezo ya uboreshaji, ikiwemo kuongeza ushirikiano kati ya Mahakama na Jeshi la Polisi, mafunzo endelevu kwa askari na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kutoa taarifa kwa walalamikaji.

Mafunzo haya yaliandaliwa na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Mwanzo katika Wilaya ya Arusha, ambazo ni Mahakama ya Mwanzo Themi, Arusha Mjini na Terat na kuratibiwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Arusha.

Wajumbe mbalimbali walihudhuria mafunzo hayo wakiwemo Mahakimu Wakazi wote wa Mahakama za Mwanzo katika Wilaya ya Arusha pamoja na wawakilishi kutoka Jeshi la Polisi.


Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi(aliyesimama) akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo baina ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi, mafunzo hayo yalifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC). Kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento na kushoto ni Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Arusha, ASP Mahita Omary.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Mhe. Sheila Manento akizungumza wakati wa mafunzo kati ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi, mafunzo hayo yalifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Themi, Mhe. Julieth Mbise akiwasilisha mada wakati wa mafunzo baina ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).

Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Arusha, ASP Mahita Omary akichangia jambo wakati wa mafunzo baina ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi, mafunzo hayo yalifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha tarehe 29 Agosti, 2025.

Mkuu wa Kituo Msaidizi, Inspekta Hassan Ibrahim akiwasilisha taarifa ya Jeshi la Polisi wakati 
 wa mafunzo baina ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).

Washiriki wa mafunzo baina ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi wakiwa katika picha ya pamoja. Mafunzo hayo yalifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 



 

 

 

Jumatatu, 1 Septemba 2025

JAJI MANYANDA ASISITIZA KUTUNZA VITENDEA KAZI VYA TEHAMA

Na Fredrick Mahava- Mahakama, Sumbawanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe, Fredrick Manyanda amewataka watumishi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga kutumia na kutunza vitendea kazi vya TEHAMA vilivyopo ili kuendana na kasi ya ukuaji wa teknolojia.

Mhe. Manyanda aliyasema hayo tarehe hivi karibuni wakati wa kikao cha watumishi kilichofanyika katika ukumbi uliopo Mahakama Kuu Sumbawanga alipokuwa akifungua kikao hicho cha siku moja.

“Tuwe na utamaduni wa kuwa na vikao vya mara kwa mara kwani vikao vinasaidia kutatua changamoto zetu kwa umoja, pia tuwe wabunifu, tujiongeze pale tunapokuwa na changamoto na tufanye kazi kwa bidi.

Aidha, Mwenyekiti wa Kikao hicho Mhe. Manyanda aliongeza kuwa, katika zama za teknolojia ni vizuri vitendea kazi vya TEHAMA viendane na Mifumo ya TEHAMA iliyopo mahakamani hivyo ni wajibu wa kila mtumishi kutumia na kutunza vitendea kazi hivyo.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe. Joseph Luambano alihimiza kila mtumishi kutimiza wajibu wake kwa kuzingatia miongozo na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na viongozi.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Bw. Machumu E. Essaba alisema Mahakama inaendelea kutatua changamoto mbalimbali za watumishi ikiwemo kulipa shahiki mbalimbali za watumishi kama vile nauli za likizo na pia kuwapeleka watumishi wa Kada mbalimbali kuhudhulia semina, mafuzo na makongamano mbalimbali yanayotekea ili kuwajengea uwezo.

Kikao hicho kilihudhuriwa na watumishi kutoka Mahakama Kuu Sumbawanga, Mahakama ya Hakimu Mkazi Rukwa na Mahakama ya Wilaya Sumbawanga.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Manyanda akiongoza kikao hicho cha watumishi

Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Mhe. Joseph Luambano akizungumza wakati wa kikao cha watumishi

Msaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Sumbawanga Bw Ipyana Mwambebule akizungumza wakati wa kikao
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Sumbawanga Mhe, Lilian Ndelwa akizungumza wakati wa kikao

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Bw. Machumu E.Essaba akifafanua jambo wakati wa kikao cha watumishi




Ijumaa, 29 Agosti 2025

SHUGHULIKIENI IPASAVYO MASHAURI YA UCHAGUZI KUREJESHA IMANI YA UMMA KWA MAHAKAMA; JAJI KIONGOZI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ametoa rai kwa Majaji wa Mahakama Kuu nchini kuwa, namna watakavyotimiza wajibu wao ipasavyo katika utatuzi wa migogoro ya mashauri yanayotokana na uchaguzi inaweza kuwa fursa mojawapo ya kurejesha imani ya umma kwa Mahakama.

Akitoa neno fupi la utangulizi wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi yanayotolewa kwa Majaji wa Mahakama Kuu jana tarehe 28 Agosti, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Dkt. Siyani alisema kuwa, katika jamii kuna baadhi ya watu hawana imani na taasisi mbalimbali za Umma ikiwemo Mahakama, ambapo malalamiko mengi yanahusishwa na huduma zinazotolewa.

“Sote tunafahamu tarehe 29 Oktoba, 2025 kutakuwa na uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, hivyo tunapojiandaa kupokea na kusikiliza mashauri ya uchaguzi ni lazima kujua kuwa mashauri ya uchaguzi ni moja kati ya maeneo oevu kwa malalamiko, kwahiyo hatuna budi kutimiza wajibu wetu katika namna itakayohakikisha haki inapatikana lakini tunajenga imani ya Mahakama kwa umma, hili nadhani ni jambo la msingi sana," alisema Jaji Kiongozi.

Alisisitiza kwamba, Mahakama ndio Chombo pekee chenye kauli ya mwisho kwenye utoaji haki kwa mujibu wa Ibara ya 107 A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa msingi huo Mahakama inayo wajibu wa kupokea, kusikiliza na kutoa maamuzi kwenye migogoro inayotokana na uchaguzi.

“Katika kutimiza wajibu huo, yapo masharti ya kikatiba yanayopaswa kuzingatiwa na Mahakama ikiwemo kutenda haki bila kujali hali ya kijamii, nafasi ya mtu kiuchumi kwa pande zote,ni kuhakikisha kuwa, usikilizwaji na uamuzi wa mashauri ya uchaguzi unakuwa ni wa haki, haraka kadri inavyopaswa na pia kutochelewesha haki bila sababu ya msingi na zaidi kutofungwa na masharti ya kiufundi ambayo yanaweza kukwamisha utoaji haki,” alisema Mhe. Dkt. Siyani.

Akizungumzia kuhusu mafunzo hayo muhimu, Jaji Kiongozi alisema kuwa, “mimi naamini mafunzo haya yamepangwa kwa wakati muafaka, ambapo sote kama ambavyo tunavyofahamu Taifa letu linaelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani.”

Alisema kwamba, uchaguzi ni mchakato unaohusisha ushindani baina ya watu kutoka kwenye vyama tofauti tofauti vya kisiasa, migororo inayotokana na ushindani huo imekuwa ikisababisha mashauri hayo kuwa na mvuto wa aina yake kwa umma, ni kwa msingi huo matarajio ya wananchi kwa Mahakama huwa ni makubwa.

Aliongeza kuwa, mafunzo hayo yamelenga kubadilishana uzoefu juu ya namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, Majaji wa Mahakama Kuu, Naibu Wasajili na Mahakimu Wafawidhi wa ngazi zote na hivyo kujengeana uwezo wa jinsi ya kushughulikia mashauri ya aina hiyo.

Mhe. Dkt. Siyani alisema kuwa, mafunzo hayo ni fursa muhimu kwa Majaji ambao waliteuliwa baada ya chaguzi zilizopita kujua changamoto zinazojitokeza katika uendeshaji wa mashauri yanayotokana na chaguzi hizo, kufahamu kwa kina sheria za sasa za uchaguzi na usimamizi wa mashauri hayo.

“Ni matumaini yangu kuwa, mafunzo haya yatawawezesha kuwa na viwango vya juu vya weledi, uwajibikaji na maadili zaidi katika kutimiza majukumu yenu, niwasihi Majaji kuwa tayari kupokea na kubadilishana uzoefu kwenye mada zitakazojadiliwa ili matokeo yaliyokusudiwa yaweze kufikiwa,” alisema Mhe. Dkt. Siyani.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akitoa neno wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama Kuu jana tarehe 28 Agosti, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Sehemu ya Majaji Wafawidhi pamoja na Majaji wengine wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa katika mafunzo hayo yanayofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)