Jumamosi, 26 Aprili 2025

SERIKALI MTANDAO, MAHAKAMA KUSHIRIKIANA

Na MWANAIDI MSEKWA na NAOMI KITONKA- Mahakama, Dar es Salaam.

Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) imeahidi kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili kuimarisha na kuboresha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji huduma mbalimbali za kimahakama ikiwemo usikilizaji wa mashauri.

Ahadi hiyo imetolewa jana tarehe 25 Aprili, 2025 na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Bw. Benedict Benny Ndomba alipokuwa anawasilisha mada kuhusu matumizi ya TEHAMA katika usikilizaji wa mashauri kwenye Mkutano wa Mwaka wa Mahakama ya Rufani uliokuwa unafanyika kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano Julius Nyerere jijini Dar-es-Salaam.

Akizungumza katika wasilisho lake, Bw. Ndomba alisema, “Kila Taifa, sekta na Taasisi ulimwenguni zinalenga mkazo wa matumizi ya TEHAMA ili kuboresha utendaji kazi na kuwahudumia Wadau kwa urahisi na ufanisi.

Aliongeza kwa kusema TEHAMA ina uwezo wa kuleta mapinduzi chanya kwenye utendaji kazi wa Taasisi, ikiwemo ngazi zote za Mahakama kama ilivyo kwa Taasisi nyingine.

Alieleza kuwa Mahakama iwe tayari kukubali mabadiliko yanayoletwa na teknolojia ikiwemo kuendelea kuboresha taratibu zake za utendaji kazi (Business Process re-engineering) na kujifunza namna ya kuendana nayo kama njia bora zaidi ya kukamilisha majukumu ya kimahakama.

Vilevile katika Mkutano huo, Majaji wa Mahakama ya Rufani na wajumbe wengine wote walipata elimu ya jinsi ya kufurahi pale wanapostaafu kutoka kwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi, ambaye alisisitiza umuhimu wa kujali afya pamoja na malezi ya familia yenye tija ili kupunguza migogoro na mawazo kabla na baada ya kustaafu.

Aidha, Dkt. Shilingi alitoa zawadi kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na kwa Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert baada ya wasilisho lake.

Mkutano huo ulihitimishwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na ulihudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani, Msajili Mkuu, Mtendaji Mkuu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Wakurugenzi, Wasaidizi wa Sheria na watumishi wa kada mbalimbali za Mahakama.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi katika Mkutano huo.

Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi Katika Mkutano huo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Serikali Mtandao (eGA), Bw. Benedict Benny Ndomba akitoa mada kwenye mkutano huo.

Wajumbe wa Mkutano wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Serikali Mtandao (eGA), Bw. Benedict Benny Ndomba (hayupo pichani) kwenye mkutano huo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Ijumaa, 25 Aprili 2025

JAJI MKUU ATANGAZA KUUNDA KAMATI KUHUISHA TARATIBU ZA UENDESHAJI MASHAURI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Mkutano wa mwaka wa mapitio ya shughuli za Mahakama ya Rufani 2024 uiliokuwa unafanyika kwenye Ukumbi wa Kimataifa Mikutano wa Julius Nyerere jijini hapa kimehitimishwa leo tarehe 25 Aprili, 2025 na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha Mkutano huo, Mhe. Prof. Juma ametangaza kuunda Kamati ya Kuhuisha Taratibu za Uendeshaji wa Mashauri katika Mahakama ya Rufani -Business process Re-engineering-ili kuboresha utendaji kazi katika utoaji haki kwa Wananchi.

Ameagiza mwenendo wa kikao hicho utayarishwe mapema ili kama kuna mambo ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi yafanyiwe kwa haraka zaidi.

‘Kitu kimoja ambacho naenda kukifanya ni kuwa na Kamati ya Business Process Re-engineering ili ianze kazi mara moja na kutupa taarifa kwa muda mfupi ili tujue tunaweza kufanya nini,’ Jaji Mkuu amesema.

Kabla ya kuhitimisha Mkutano huo, Wajumbe walipitishwa kwenye mada mbalimbali, ikiwemo matumizi ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA-katika usikilizaji wa mashauri iliyowasilishwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Mhandisi Benedict Ndomba na Mkurugenzi wa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Kaleghe Enock.

Katika wasilisho lao, wataalam hao waliwaeleza wajumbe wa Mkutano kuwa matumizi ya TEHAMA katika sekta na Taasisi mbalimbali hayaepukiki ili kuboresha   huduma kwa urahisi na ufanisi zaidi.

Mada nyingine ilihusu maandalizi ya kustaafu katika utumishi na uongozi iliyowasilishwa na Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi pamoja na ile inayohusu namna ya kuthibiti msongo wa mawazo iliyowasilishwa na Bi. Zuhura Muro.

Katika mada yake, Dkt Mashillingi amewakumbusha Majaji hao kuwa kustaafu ni fursa ya kuanza maisha mapya yenye utulivu na furaha, hivyo maandalizi mazuri, yanaweza kuwa na mchango mkubwa katika jamii na kufurahia maisha.

‘Panga maisha yako: aina gani ya maisha ungependa uishi? Punguza msongo wa mawazo, usitumie akiba yako kwa mambo ya siasa. Samehe na kusahau: huu siyo muda wa kuwaza wale waliokukosea, waliokudhulumu,’ amesema.

Wakati wa Mkutano huo, wajumbe walipokea na kujadili taarifa mbalimbali zinazohusu mashauri katika Mahakama ya Rufani pamoja na masuala mbalimbali ya kiutumishi, ikiwa ni pamoja na ikama, bajeti, stahiki za Majaji, mabadiliko ya sheria kwenye stahiki za Majaji pamoja na mafunzo kwa watumishi wa Mahakama ya Rufani.

Kadhalika, wajumbe walijadili masuala mbalimbali katika Mahakama ya Rufani na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla, ambayo yanalenga kuboresha utendaji wa kazi ya utoaji haki.

Mkutano huo ulihudhuriwa na Majaji wote wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mtandaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Naibu Wasajili, Watendaji na watumishi mbalimbali wa Mahakaka hiyo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati wa kuhitimisha Mkutano wa Mwaka wa Mahakama ya Rufani Tanzania.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania-juu na chini-ikiwa kwenye Mkutano huo.


Sehemu nyingine ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Watumishi wengine wa Mahakama-juu na chini-ikiwa kwenye Mkutano huo.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Mhandisi Benedict Ndomba akiwasilisha mada kwenye Mkutano huo.

Mkurugenzi wa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Kaleghe Enock akiwasilisha mada kwenye Mkutano huo.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi akiwasilisha mada kwenye Mkutano huo. Picha chini ni Mtaalam wa Saikolojia, Bi. Zuhura Muro.



Alhamisi, 24 Aprili 2025

MAHAKAMA YA RUFANI NA KASI YA UONDOSHWAJI MASHAURI YA MLUNDIKANO

Na MWANAIDI MSEKWA na NAOMI KITONKA- Mahakama, Dar es Salaam.

  • Kiwango uondoshaji mashauri kimepanda mwaka 2024.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamisi Juma leo tarehe 24 Aprili 2025 ameongoza kikao kazi cha tathmini ya shughuli za Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2024.

Kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano Julius Kambarage Nyerere, Dar-es Salaam kiliambatana na uwasilishaji wa Taarifa ya Mashauri kwa kipindi cha Januari hadi Disemba 2024 iliyowasilishwa na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert pamoja na taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya kiutawala na kiutumishi kwa mwaka 2024/2025 iliyowasilishwa na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Victor Kategere.

Akiongea katika taarifa hiyo, Mhe. Herbert alisema takwimu zinaonyesha idadi ya mashauri yanayoondolewa ni kubwa katika kipindi cha mwaka mmoja kulinganisha na kipindi kilichopita cha mwaka 2023, japokuwa mzigo wa mashauri umeongezeka kwa mwaka 2024.

Alisema pia kuwa Mahakama ya Rufani imeendelea kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao kwenye vikao vya majopo, maombi ya faragha, usomaji wa maamuzi na usikilizaji wa maombi ya madai ya gharama za kesi (taxations).

Kadhalika, Mahakama imeendelea kupandisha kwa wakati maamuzi yote yanayopaswa katika tovuti ya TanzLII na kuanzia mwezi Februari mwaka 2025 Mahakama ya Rufani imeanza rasmi matumizi ya mfumo wa eCMS kuanzia kufungua shauri hadi kusomwa hukumu.

Pia taarifa iliyowasilishwa na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani iligusia maeneo muhimu ya vipaumbele vilivyowekwa na Mahakama hiyo, yakiwemo mkakati wa kuharakisha utatuzi wa mashauri ya kawaida, uendeshaji wa vikao vya Mahakama (Session), matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano -TEHAMA Pamoja na kuongeza ushirikiano na wadau wa haki jinai.

“Pamoja na mafanikio haya, Mahakama ya Rufani imedhamiria kuharakisha utatuzi wa mashauri ya kawaida na mkakati wa kumaliza mashauri ya muda mrefu, kuboresha mifumo na matumizi ya TEHAMA, kuimarisha uwezo katika ukaguzi na usimamizi wa shughuli za Mahakama, kuendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama, kuongeza ushirikiano na wadau wa haki jinai pamoja na kuimarisha maendeleo ya rasilimali watu ikijumuisha mafunzo na nidhamu ya watumishi wetu,” aliongeza Bw. Kategere.

Aidha, alihitimisha kwa kusisitiza kuwa Mahakama ya Rufani itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kushirikiana na wadau wa ndani na nje ili kuhakikisha haki inaendelea kutolewa kwa wakati. Aidha, ili kuwafikia wananchi kwa wakati, Mahakama itaendelea kuimarisha na kuboresha matumizi ya TEHAMA katika huduma mbalimbali zitolewazo na Mahakama.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi, Msajili Mkuu, Mtendaji Mkuu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Wakurugenzi, Wasaidizi wa Sheria na Watumishi wa kada mbalimbali za Mahakama.

Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert akitoa wasilisho katika kikao kazi cha tathmini ya shughuli za Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2024 kilichofanyika leo tarehe 24 Aprili 2025.

Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Victor F. Kategere akitoa wasilisho katika kikao kazi cha Tathmini ya shughuli za Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2024 kilichofanyika leo tarehe 24 Aprili 2025.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzani,a Mhe. Prof. Ibrahim Hamisi Juma akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na picha mbili chini.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Jaji wa Mahakama Kuu na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wanaohudumu katika Mahakama ya Rufani.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Menejimenti wa Mahakama ya Tanzania.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JAJI MKUU ATAKA MKAKATI MADHUBUTI KUKABILI ONGEZEKO LA MASHAURI MAHAKAMA YA RUFANI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ametoa wito kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania kubuni mbinu mpya zitakazosaidia kukabiliana na ongezeko la mashauri kutoka Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya.

Mhe. Prof. Juma ametoa wito huo leo tarehe 24 Aprili, 2025 alipokuwa anafungua Mkutano wa Mwaka 2024 unaofanyika kwa siku mbili kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, kujadili masuala mbalimbali katika Mahakama ya Rufani na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.

‘Hiki ni kikao cha kupanga mikakati juu wajibu wetu katika kukabiliana na ongezeko la mashauri baada ya kukamilika ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tisa na Mahakama za Mahakimu 60 zinazoendelea kujengwa…

‘…Katika kikao hiki tutakaribisha majadilino yatakayotusaidia kuendelea kubaini maeneo muhimu ambayo bado yanaleta changamoto katika utekelezaji wa majukumu yetu na kutafuta mbinu za kuondokana na changamoto hizo.’ Jaji Mkuu amesema.

Amebainisha kuwa takwimu zinaonyesha idadi ya mashauri yanayofunguliwa Mahakama ya Rufani kwa mwaka imeendelea kuongezeka na kwamba Mkuu wa Idara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA- amefanya makisio ya mzigo ambao Majaji 39 wataubeba kuanzia mwaka 2026 hadi 2030.

Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa kila Jaji wa Mahakama ya Rufani amekadiriwa uwezo wa kushughulikia rufaa 99 kwa mwaka, hivyo uwezo wa Majaji wa Mahakama ya Rufani 39 ni kushughulikia rufaa 3,861 kwa mwaka.

Amesema kuwa makisio ya ongezeko la rufani kuanzia 2026 hadi 2030 yatakuwa mashauri 10,434 kwa mwaka 2026, mashauri 11,248 mwaka 2027, mwaka 2028 mashauri 12,061, mwaka 2029 mashauri 12,875 na mwaka 2030 ni mashauri 13,690, huku kila mwaka Majaji hao wakiwa na wastani wa kushughulikia mashauri 3,861.

‘Hatuwezi kukabiliana na wingi na ongezeko la mashauri yanayotiririka kupitia ngazi na vituo mbalimbali hadi kuishia katika Mahakama ya Rufani kwa kutegemea tu mpangilio wa kisheria, kanuni na idadi ya Majaji wa Rufani na Majopo yaliyopo,’ Jaji Mkuu amesema.

Amebainisha kuwa Mkutano huo wa Majaji wa Rufani, uwe mwanzo wa kujiwekea mikakati ya kuziangalia sheria, kanuni na kuzichakata upya taratibu za Mahakama ya Rufani na zile za Mahakama za ngazi za chini ili kumudu ongezeko kubwa la mashauri.

Akizungumzia mlundikano wa mashauri, Jaji Mkuu amebainisha kuwa mwaka 2024, Mahakama ya Rufani ilikuwa na mashauri ya mlundikano 1,273, sawa na asilimia 21 ya mashauri yake na kuchangia asilimia 74 ya mlundikano wa mashauri ulioko mahakamani katika ngazi zote, huku ngazi zingine za Mahakama zikiweza kudhibiti changamoto hiyo.

Ameeleza pia kuwa kati ya Januari na Desemba 2024, wakati Mahakama ya Rufani ilikuwa na asilimia 21 ya mashauri ya mlundikano, Mahakama Kuu haikuwa na tatizo hilo kwani mwaka 2024, mlundikano ulikuwa ni asilimia 2 tu, Mahakama za Hakimu Mkazi ulikuwa asilimia 6 pekee na Mahakama za Wilaya zilikuwa asilimia 1 na Mahakama za Mwanzo hazikuwa na mlundikano mwaka 2024.

‘Kwa ulinganifu wa ngazi zote za Mahakama, hali yetu Mahakama ya Rufani sio nzuri katika mlundikano, tunachangia asilimia 74 ya mzigo wa mlundikano katika ngazi zote za Mahakama ya Tanzania,’ Mhe. Prof. Juma amesema.

Jaji Mkuu amesisitiza matumizi ya TEHAMA katika utoaji huduma za kimahakama kwani ni njia bora ya kupambana na changamoto hiyo na amewapongeza Majaji wote kwa kuanza utekelezaji wa jambo hilo.

‘Tunaomba tusirudi nyumba, tuendelee kusikiliza mashauri yote kwa njia ya mfumo na tuendelea kubaini changamoto na kuziwasilisha kwa wajenzi wa mfumo ili tuendelee kuboresha zaidi mfumo na kurahisisha utendaji kazi,’amesema.

Ametumia fursa hiyo kuwapongeza Majaji na Watumishi wote wa Mahakama ya Rufani kwa kuendelea na jitihada za kuamua mashauri kwa mafanikio makubwa, licha ya changamoto mbalimbali mnazokabiliana nazo.

Wakati wa Mkutano huo, wajumbe watapokea na kujadili taarifa mbalimbali zinazohusu mashauri katika Mahakama ya Rufani pamoja na masuala mbalimbali ya kiutumishi, ikiwa ni pamoja na ikama, bajeti, stahiki za Majaji, mabadiliko ya sheria kwenye stahiki za Majaji pamoja na mafunzo kwa watumishi wa Mahakama ya Rufani.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-juu na chini-akizungumza wakati anafungua Mkutano wa Mwaka wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 24 Aprili, 2025 jijini Dar es Salaam.

Amidi wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Augustine Mwarija akimkaribisha Jaji Mkuu wa Tanzania kufungua Mkutano huo. Picha chini ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert akitoa maelezo ya awali kuhusu Mkutano huo.

Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na chini-wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa Mkutano huo.

Sehemu nyingine ya Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na picha mbili chini-wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa Mkutano huo.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani-wa kwanza kulia-pamoja na Viongozi wengine waandamizi wa Mahakama ya Tanzania-juu na chini-wakiwa kwenye Mkutano huo.

Naibu Wasajili na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya Rufani-juu na chini-wakifuatilia hoja mbalimbali kwenye Mkutano huo.

Sehemu nyingine ya Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya Rufani pamoja na Watumishi katika Mahakama hiyo-juu na chini-wakifuatilia hoja mbalimbali kwenye Mkutano huo.


Sehemu nyingine ya tatu ya Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya Rufani pamoja na Watumishi katika Mahakama hiyo-juu na chini-wakifuatilia hoja mbalimbali kwenye Mkutano huo.



JAJI DKT. MLYAMBINA AHAIDI MAHAKAMA YA KAZI KUENDELEZA USHIRIKIANO NA OSHA

Na ARAPHA RUSHEKE- Mahakama, Dodoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina jana tarehe 23 Aprili, 2025 ameongoza Kikao kazi cha watumishi wa Mahakama ya Tanzania kutoka sehemu mbalimbali wakiwemo waheshimiwa Majaji Wafawidhi, Majaji, Naibu wasajili, Mahakimu, Wasaidizi wa sheria wa Majaji, watendaji wa Mahakama na viongozi mbalimbali wataasisi za kiserikali zinazofanya kazi katika mnyororo wa Mahakama kazi.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) uliopo tambukareli jijini Dodoma

Akizungumza wakati wa neno la utangulizi wa Kikao hicho, Mhe. Dkt. Mlyambina alieleza kuwa Mafunzo haya ni sehemu ya mwendelezo wa ushirikiano mwema kati ya Mahakama na OSHA ushirikiano ulioanza kuimarika tangu kufanyika kwa mafunzo ya awali yaliyohusisha Watumishi wenye ulemavu kutoka taasisi mbalimbali za Serikali na Kanda tofauti za Mahakama.

“Awamu hii ya pili, tunajivunia kuwahusisha viongozi wa Mahakama, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, Ofisi ya kamishina wa Kazi, CMA pamoja na viongozi kutoka OSHA, jambo ambalo linadhihirisha dhamira ya dhati ya Muhimili wa Mahakama na Serikali katika kuboresha mazingira ya kazi na huduma kwa wananchi. Ushirikiano huu ni utekelezaji wa Nguzo ya Tatu ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya mwaka 2020/2021– 2024/2025, inayolenga kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama pamoja na ushirikishwaji wa wadau katika shughuli za Mahakama,” Jaji Mfawidhi huyo alisema.

Aliendelea kubainisha kuwa katika dunia ya sasa inayobadilika kwa kasi, maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yameleta mapinduzi makubwa katika sekta mbalimbali, ikiwemo Sekta ya Haki-Kazi. Matumizi ya Akili Unde (Artificial Intelligence – AI) ni nyenzo muhimu ya kuongeza tija, kupunguza gharama za uendeshaji, na kuharakisha utoaji wa maamuzi kwa wakati. Ni kwa msingi huo, kauli mbiu ya mafunzo haya inasema: "Nafasi ya Akili Unde (Artificial Intelligence –AI) Mahali pa Kazi (Mapinduzi na Fursa)." Kauli mbiu hii si tu inasisitiza umuhimu wa teknolojia, bali pia inatufungua macho kuhusu nafasi ya AI katika kuongeza ufanisi wa utendaji kazi, kuhakikisha usalama wa watumishi, na kupunguza hatari kazini.

Katika salamu zake za ukaribisho Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, vijana, Ajira na Wenye ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete ameushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kundeleza ushirikiano mzuri na muhimili huo katika kutambua umuhimu wa usalama mahala pakazi kupelekea kukubali watumishi kushiriki mafunzo hayo ambayo yatawasaidi na kuwajengea uelewa washiriki katika masuala ya usalama na afya waweze kutekeleza maşukumu yao yake kila siku kwa kuzingatia kanuni bora na kujilinda dhidi ya viatarishi vya magonjwa na ajali mahala pa kazi.

Naye, Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi Hadija Mwenda aliwasihi washiriki wa mafunzo hayo kutumia fursa hiyo kujifunza vitu vingi na kwaweredi mkubwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina akitoa neno la ukaribisho wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usalama mahala pa kazi kwa watumishi wa mahakama na taasisi za mnyororo wa Mahakama Kazi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, vijana, Ajira na Wenye ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete akitoa neno wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo.

Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi Hadija Mwenda aliwasihi washiriki wa mafunzo hayo kutumia fursa hiyo kuwashukuru washiriki hao
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania Dkt.Mustapher Mohamed Siyani ikiwa katika picha ya pamoja na wadau kutoka OSHA waliohudhuria mafunzo hayo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha- Mahakama)







Jumatano, 23 Aprili 2025

JAJI KIONGOZI AFUNGUA KONGAMANO LA WADAU WA MAHAKAMA KAZI

Na INNOCENT KANSHA - Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani leo tarehe 23 Aprili, 2025 amefungua Kongamano la mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi.  

Kongamano la mafunzo hayo yanayofanyika jijini Dodoma katika Ukumbi wa Mikutano wa jengo la OSHA limebeba Kauli mbiu maalum kwa ajili ya kutafakari na kubadilishana uzoefu juu ya “Nafasi ya Akili Unde (Artificial Intelligence - AI) Mahali pa Kazi (Mapinduzi na Fursa)”

“Kwa kuwa nyinyi ni wadau wa utoaji haki na huduma katika sekta mbalimbali, mafunzo haya ni muhimu sana kwenu. Matumizi ya akili unde yamedhihirika kuleta mafaniko na ufanisi katika sekta mbalimbali duniani. Tanzania sio kisiwa na hivyo hatuwezi kubaki nyuma. Ni lazima nchi yetu iendane na mabadiliko chanya ya kiteknolojia na utendaji yanayotokea kote ulimwenguni. Mafunzo haya yanatoa fursa ya kupiga hatua muhimu katika safari ya uboreshaji wa mifumo na utendaji kazi wetu,”. amesisitiza Jaji Kiongozi Mhe. Dkt. Siyani.

Jaji Siyani amendelea kwa kusema, akili unde ni matokeo ya kuongezeka kwa utafiti na kukua kwa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kiasi cha kuwezesha kutengenezwa kwa mifumo yenye utambuzi wa mambo mfano wa binadamu. Viwango vya usahihi vinavyozidi kuongezeka kadri ya mifumo hiyo inavyotumiwa na muda mfupi ambao mifumo hiyo inatumia kutekeleza kazi mbalimbali, vinaongeza hamasa na kuonyesha umuhimu wa matumizi yake. 

Mhe. Dkt. Siyani ameongeza kuwa, matumizi ya akili unde yanazaa fursa na changamoto mbalimbali kupitia mafunzo washiriki watapata nafasi ya kupitia faida na hasara za matumizi ya akili unde. Faida za matumizi ya akili unde ni nyingi na kama nilivyotangulia kusema ni pamoja na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi, kurahisha tatifi mbalimbali, kutafsiri lugha, kupunguza makosa ya kibinadamu, pamoja na kuokoa muda na gharama.

“Aidha, akili unde inaweza kuwapa wafanyakazi muda zaidi wa kufikiria mambo yenye tija kubwa zaidi kwa taasisi na kutunza kumbukumbu muhimu kazini, mambo yanayoweza kukuza ugunduzi na ushindani,” amesema Mhe. Dkt. Siyani.

Aidha, Jaji Kiongozi ameongeza kuwa, akili unde haikuja na faida pekee bali pia, inazo changamoto zake. Moja ya changamoto hizo ni hofu ya watu kudhani kuwa watapoteza kazi zao ikiwa akili unde itaachwa kuendelea kukua na kufanya kazi ambazo kimsingi zinafanywa na binadamu. Hofu nyingine ni kupotea kwa usiri na uwezekano wa taarifa muhimu kudukuliwa.

“Ni muhimu kujua kuwa katika dunia yetu ya sasa matumizi ya akili unde hayakwepeki. Iko haja ya kujadili na kuhakikisha kwamba kila mmoja anajiongezea thamani kama mfanyakazi ili kufikia viwango na kufanya kazi ambazo haziwezi kufanywa na akili unde, lakini pia kuhakikisha kuwa mifumo yetu imewekewa ulinzi wa kutosha kudhibiti matumizi mabaya ya akili unde kwa ajili ya udukuzi wa taarifa,” amesema Jaji Siyani.

 

Vilevile, Mhe. Dkt. Siyani amesema kwamba, uzoefu watakaoupata washiriki wa mafunzo hayo, utawapa jukumu la kuhakikisha kuwa matumizi ya akili unde yanawasaidia kuboresha utendaji kazi kama mtu mmoja mmoja na ufanisi wa taasisi. Ni matumaini ya Mahakama na taasisi zingine zinazoshiriki mafunzo ya akili unde yatawapa pia ujuzi wa kukabiliana na changamoto zitokanazo na maendeleo ya teknolojia katika utendaji kazi.

 

Aidha, Jaji Kiongozi akatoa rai kwa washiriki wa mafunzo kutumia nafasi ya mafunzo hayo ipasavyo kubadilishana uzoefu, kujielimisha, na kutoa maoni ya namna ya kuboresha utendaji wa kazi, lakini pia sheria na sera zinazosimamia matumizi ya akili unde pamoja na usalama na afya kwa watumishi kwa ajili ya kulinda maslahi ya wafanyakazi.

 

Akihitimisha hotuba yake ya ufunguzi wa mafunzo Mhe. Dkt. Siyani  ameushukuru uongozi wa OSHA kwa kutambua uhitaji wa mafunzo hayo kwa watumishi wa umma na kukubali kuwezesha kufanyika kwake kwa mara ya pili jijini Dodoma.

 

“Ni rai yangu kuwa ushirikiano huu baina ya OSHA kama mdau wa Mahakama uendelezwe ili kuwapa watumishi wa umma wakiwemo wale wa Mahakama fursa ya kupata elimu na kubadilishana uzoefu kupitia mijadala mbalimbali itakayoongeza tija kazini...

 

Aliwashukuru wafanyakazi wa Mahakama na wa Taasisi nyingine za umma kwa kutenga muda na kuja kushiriki mafunzo haya muhimu. Ni matarajio yangu kuwa baada ya mafunzo haya, washiriki watarejea katika maeneo yao ya kazi wakiwa na maarifa mapya yatakayowasaidia kuongeza tija, kuboresha utoaji wa haki na huduma bora kwa wananchi,” ameongeza Jaji Siyani.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akifungua Kongamano la mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi leo tarehe 23 Aprili, 2025 jijini Dodoma katika Ukumbi wa jengo la OSHA.  


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akifungua Kongamano la mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi leo tarehe 23 Aprili, 2025 jijini Dodoma katika Ukumbi wa jengo la OSHA.  


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisalimiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete alipowasili kufungua Kongamano la mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi, kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina.
 
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisalimiana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, kulia kwake ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete alipowasili kufungua Kongamano la mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani aliyekaa katikati akikagua nyaraka wakati wa hafla hiyo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani aliyeketi katikati akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wanaoshiriki mafunzo hayo. 
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani aliyeketi katikati akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi kutoka Taasisi za Kazi na usuluhishi na uamuzi wanaoshiriki mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani aliyeketi katikati akiwa kwenye picha ya pamoja na Naibu Wasajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania wanaoshiriki mafunzo hayo.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akipokea Tuzo maalum kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete wakati wa hafla hiyo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akionyesha Tuzo maalum aliyopokea kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete wakati wa hafla hiyo.


Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya Usalama Mahala pa Kazi kati ya Mahakama Kuu ya Tanzania – Divisheni ya Kazi, Taasisi ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) pamoja taasisi za kiserikali ambazo ni wadau wa Mahakama Kazi. 

(Picha kutoka Mahakama ya Tanzania)