Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Mwanza
Timu za Mpira wa Miguu, Netiboli na Kamba zimefuzu kuingia 16 bora katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) yanayofanyika katika viwanja mbalimbali jijini Mwanza.
Akizungumza leo tarehe 06 Septemba, 2025 jijini Dodoma, Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Tende amesema hatua ya makundi imeisha katika timu za Kamba, Netiboli na Mpira wa Miguu ambapo Kamba wanawake na wanaume wanaongoza katika makundi yao. Kwa upande wa netboli na mpira wa miguu wameshika nafasi ya pili katika makundi.
Katika mchezo wa Kamba wanawake walikuwa kundi A ambapo kulikuwa na Timu ya Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Mkoa wa Kagera, Mahakama, Katiba na Sheria na Hazina ambapo Mahakama ilifanikiwa kuwavuta kwa mivuto yote miwili hivyo kusababisha kuingia 16 bora kwa pointi sita.
Katika Mchezo wa Kamba wanaume walikuwa kwenye kundi B ambapo kulikuwa na Timu kutoka Mahakama, Viwanda, Kilimo na Maji ambapo Mahakama Sports ilifanikiwa kuivuta Timu kutoka Viwanda na Kilimo kwa mivuto miwili lakini Timu ya Maji walifanikiwa kuwavuta mvuto mmoja na mvuto mmoja walitoka sare na kusababisha kuingia 16 bora kwa pointi tano.
Kwa upande wa Mpira wa Miguu Timu ya Mahakama ilikuwa kundi E pamoja na Timu ya Madini, OSHA, Kilimo, Mahakama na Wakili Mkuu ambapo Timu ya Mahakama ilimfunga Wakili Mkuu bao moja kwa nunge, bao hilo lilifungwa na Mchezaji mchachali wa Mahakama Sports, Bw. Martine Mpanduzi baada ya mpira wa kona kuchongwa na mchezaji Seif Shamte na hivyo kufanikiwa kushinda katika mechi hiyo.
Na katika Mechi ya Mahakama na Timu kutoka Wizara ya Madini Mahakama ilishinda kwa bao mbili kwa moja ambapo bao la kwanza lilifungwa na Seif Shamte na la pili lilifungwa na Martine Mpanduzi kwa usaidizi wa Seif Shamte na kusababisha ushindi kwa mara nyingine katika mchezo wa mwisho wa kundi hilo, Mahakama ilicheza na timu ya OSHA na kufungwa bao moja kwa nunge na hivyo kusababisha kupata pointi tisa na kuingia katika 16 bora.
Aidha, Timu ya Netiboli ya Mahakama iliyokuwa katika kundi F lililojumuisha timu kutoka Uwekezaji, Timu kutoka Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Katavi, Ukaguzi, Mahakama na Timu kutoka GST na kufungwa na Uwekezaji kwa magoli 32 kwa 24 na baada ya hapo Mahakama iliwafunga GST magoli 41-11, uwekezaji magoli 33-11 na RAS Katavi magoli 43-11 na hivyo kufanikiwa kutinga 16 bora wakiwa na pointi sita.
Katika hatua hiyo, ya makundi Timu za Netiboli na Mpira wa Miguu wamepoteza mechi moja moja na kushinda mechi zingine zote.
Akizungumza baada ya timu hizo kushinda na kuingia 16 bora, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Club, Bw. Wilson Dede amesema amefurahi na kushukuru timu zake kufikia hatua hiyo huku akisema kuwa, matokeo hayo yametokea kutokana na nidhamu ya wachezaji na ushirikiano mkubwa baina ya wachezaji lakini pia mazoezi.
Bw. Dede ameongeza kwamba, wamejiandaa kwa hatua nyingine ya mtoano
ambapo maandalizi yanaendelea vizuri na ana matumaini ya kufika mbali katika
mashindano hayo.
Mfungaji wa Timu ya Netiboli (GS) wa Mahakama Sports, Bi. Tatu Mawazo akifunga goli wakati wakicheza na Timu ya RAS Katavi leo tarehe 06 Septemba, 2025 jijini Mwanza.
Kikosi cha netiboli kikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi kabla ya mechi yao dhidi ya Ofisi ya Katibu Tawala (RAS) Katavi.
Kikosi cha Mahakama Sports Mpira wa Miguu kabla ya kuvaana na Timu ya OSHA.
Timu ya Kamba wanawake wakiwa katika picha ya pamoja na Kocha wa Kamba Rajab Mwariko (wa kwanza kulia) na na Naibu Katibu wa Mahakama Sports, Bi. Theodosia Mwangoka.
Timu ya Kamba wanaume Mahakama Sports wakiwa katika picha ya pamoja.
Katibu wa Mahakama Sports, Bw. Robert Tende akizungumza wakati wa mahojiano.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)