Ijumaa, 24 Oktoba 2025

MAHAKAMA MOROROGO YAWEKA MIKAKATI MBADALA KUHUSU UFUNGAJI MIRATHI

Na AYSHER JUMA-Mahakama, Morogoro

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro, imeweka mikakati mbadala ya kushughulikia changamoto ya kutofungwa kwa mashauri ya mirathi kwa wakati.

Mikakati hiyo imewasilishwa katika kikao cha menejimenti kilichoongozwa na Kaimu Mwenyekiti wa kikao, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga.

Kikao hicho kilifanyika tarehe 22 Oktoba, 2025 katika ukumbi namba mbili wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC), Morogoro.

Kikao hicho kililenga kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mashauri na hali ya kiutawala katika Mahakama zote ndani ya Kanda ya Morogoro.

Katika uchambuzi wa mashauri mbalimbali, mashauri ya mirathi yalibainika kuwa mengi hayajafungwa kutokana na sababu mbalimbali kama vifo vya wasimamizi wa mirathi, matatizo ya kiafya, migogoro ya kifamilia, kesi kuingia kwenye mchakato wa rufaa na zaidi ya yote, ukosefu wa uelewa wa kisheria juu ya hatua ya mwisho ya kufunga mirathi.

Kutokana na changamoto hizo, kikao kiliazimia kuanzisha kampeni maalum iitwayo “Oparesheni Funga Mirathi” ambayo inalenga kuwafikia wananchi kupitia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii, Viongozi wa mitaa, Viongozi wa kimila, pamoja na kuwasiliana na warithi au wasimamizi wa mirathi kupitia simu ili kuhamasisha na kurahisisha hatua ya kufunga mashauri husika.

Akisoma taarifa ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Hakimu Mfawidhi wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo alieleza kuwa baadhi ya mikakati iliyowekwa katika robo ya tatu ya mwaka 2025 imetekelezwa kwa mafanikio makubwa.

Alisema utekelezaji wa adhabu mbadala umechangia kwa kiasi kikubwa kupungua kwa idadi ya wafungwa, pia  mahabusu kwa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya na kutokuwa na Mahabusu  wa Mahakama za Mwanzo, hivyo kufanya maelekezo ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju kutekelezeka kwa asilimia 100.

Mbali na mikakati ya kuondoa changamoto ya ufungaji mirathi, Kanda ya Morogoro kupitia kikao hicho kimeazimia kuingia na baki sifuri kwa Mahakama zote za Mwanzo na  baki single digit  kwa Mahakama za Wilaya.

Kwa upande wa maendeleo ya kiutawala, taarifa kutoka kwa Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Morogoro, Bw. Ahmed Ng’eni ilieleza hali ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA], majengo mapya ya Mahakama, viwanja vya Mahakama na uboreshaji wa miundombinu.

Alisema kuwa Mahakama mpya zinaendelea kujengwa katika maeneo ya Bwakila, Minepa, Ngoheranga, Kilosa na Magubika, ambapo baadhi ya miradi hiyo inafadhiliwa na Benki ya Dunia, na mingine ni sehemu ya mipango ya ndani ya Mahakama ya Tanzania, hususan kutumia fedha kutoka serikalini.

Kikao hicho kilihudhuriwa na wajumbe mbalimbali wakiwemo Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya zote, Maofisa Utumishi kutoka Wilaya mbalimbali, Mkaguzi wa Ndani, Maofisa TEHAMA na Wahasibu wa Mahakama. 

Wajumbe hao walielezea kuunga mkono kampeni ya “Oparesheni Funga Mirathi” na kuahidi kutoa ushirikiano ili kuhakikisha kuwa mashauri yote yaliyosalia yanafungwa kwa wakati na kwa mujibu wa sheria.



Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga akiongoza kikao hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Bw. Ahmed Ng’eni  akisoma taarifa ya hali ya utekelezaji wa miradi mbalimbali.


Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo akisoma taarifa ya  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro.

Sehemu ya wajumbe walio hudhuria kikao hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAHAKAMA MOSHI, ARUSHA NA MANYARA ZAUSIMAMISHA MJI WA MOSHI KWA BONANZA LA MICHEZO

  •  Mahakama Kuu Kanda ya Moshi yaibuka kidedea katika Bonanza hilo
  • Mamia ya wananchi wajitokeza viwanja vya ‘Moshi Club’ kushuhudia mtanange baina ya timu kutoka Moshi, Arusha na Manyara
  • Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Mongella asisitiza Michezo kuwa kipaumbele kwa watumishi wa Mahakama katika kukabiliana na Magonjwa yasioambukiza
  •  Michezo kuwa nyenzo ya ushirikiano kwa watumishi kwa Kanda ya Moshi, Arusha na Manyara

Na PAUL PASCAL, Mahakama-Moshi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella amewataka watumishi wa Mahakama kuwa na utamaduni wa kukutana mara kwa mara na kufanya mazoezi na kushiriki kwenye michezo mbalimbali itakayowahusisha watumishi wa kada zote ili kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza pamoja na kuimarisha afya zao.

Mhe. Dkt. Mongella aliyasema hayo 18 Oktoba 2025 katika Uwanja wa Moshi (Moshi Club) wakati wa uzinduzi wa Bonanza maalum kwa watumishi wa Mahakama wa Kanda za Moshi, Arusha na Manyara ambapo alisema, lengo ni kuwakutanisha watumishi wote pamoja kufahamiana na kukumbushana wajibu wa kutekeleza majukumu yao ya kila siku. 

"Watumishi waliofika hapa ni sisi wenyeji Moshi na wageni wetu kutoka Kanda ya Arusha na Manyara lengo ni kufahamiana, kukosoana, kukumbushana na kufurahi, kwa kuwa michezo ni afya. Pia inafuta madaraja baina ya watumishi na Viongozi na kuweka uwanja wa kusikiliza changamoto, maoni na ushauri kutoka kwa watumishi wa vituo vyote, bonanza hili lina sura ya Siku ya Familia ya Watumishi wa Mahakama japo sisi tumeegemea kwenye mazoezi na michezo zaidi,” alisema Jaji Mfawidhi huyo. 

Mhe. Dkt. Mongella aliwataka watumishi wote kuwa na ratiba ya michezo katika vituo vyao ambapo alisema, “kwa sisi wa Mahakama Kuu Moshi tunafanya mazoezi kila siku ya Jumanne na Alhamisi kuanzia saa 10:30 Jioni, vema wote tukaiga utamaduni huu kwa maslahi ya afya zetu.”

Kwa upande wake Mgeni Rasmi katika Bonanza hilo ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Manyara, Mhe. Ilvin Mugeta aliwahimiza watumishi kushirikiana katika maeneo ya kazi.

“Tukitaka kufanikiwa katika kufikia malengo yetu, suala la ushirikiano ni lazima liwepo kati yetu tutumie michezo na mazoezi kama nyenzo ya kujenga ushirikiano baina yetu na kukiwa na ushirikiano baina ya watumishi ni dhahiri tunakwenda kutimiza majukumu yetu yote kwa urahisi turejee methali isemayo, ‘umoja ni nguvu utengano ni udhaifu,” alisema Mhe. Mugeta.

Alisema, pasipokuwa na ushirikiano baina ya vituo hivyo vinakwenda kuanguka, hivyo aliwasisitiza watumishi hao kushirikiana katika maisha ya kazini, maisha ya baada ya kazi na jamii zinazowazunguka.

Katika Bonanza hilo, Mahakama Kuu Kanda ya Moshi iliibuka mshindi wa jumla kwa kufanikiwa kukusanya jumla ya medali 27 kati ya 38 zilizokuwa zikishindaniwa katika bonanza hilo. Washindi wote katika Bonanza hilo walipatiwa zawadi za makombe na medali.

Mahakama Kuu Kanda ya Moshi iliandaa na kufanya Bonanza la michezo lililokusanya washiriki na watazamaji wapatao 1,200 wakishuhudia na kushiriki michezo ya Riadha mita 1,200 kwa wanaume mita 1000 na kwa wanawake mita 100 kwa viongozi, mpira wa miguu wanaume, mpira wa pete wanawake, kukimbia na yai, mchezo wa karata, bao, drafti, ‘pool table’, kukimbia na gunia, mashindani ya kula tikiti, mashindani ya kufukuza kuku pamoja na kuimba muziki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Manyara, Mhe. Ilvin Mugeta (Mgeni rasmi katika bonanza) akipiga penati katika viwanja vya Moshi Club tarehe 18 Oktoba, 2025 wakati wa ufunguzi wa Bonanza la Michezo lililowashirikisha watumishi wa Mahakama Kanda ya Moshi, Arusha na Manyara.


Wacheza bao, Timu ya Mahakama Kuu Moshi wakichuana vikali na wapinzani wao kutoka Timu ya Mahakama Kuu Manyara ambapo Mahakama Kuu Moshi iliibuka Mshindi wa kwanza katika mchezo huo.

Wacheza 'pool table' Timu ya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha wakichuana vikali na wapinzani wao kutoka Timu ya Mahakama Kuu Moshi ambapo Mahakama Kuu Arusha waliibuka Mshindi wa kwanza katika mchezo huo.

Mshindi wa mbio Mita 1,500 wanaume, Bw. Godlisten Mwingereza (aliyebebwa) akishangilia pamoja na mashabiki wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi baada ya kuibuka mshindi katika mbio hizo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Lillian Mongella (kulia) akipokea tuzo ya Mshindi wa jumla kutoka kwa Mkuu wa Mashtaka Mkoa wa Kilimanjaro, Bi. Esther Mfuse baada ya Mahakama Kuu Moshi kuibuka mshindi wa jumla katika mashindano hayo kwa kupata medali 27 kati ya 38.

Wachezaji wa Mbio za Magunia Timu ya Mahakama Kuu Moshi wakichuana vikali na wapinzani wao kutoka Timu ya Mahakama Kuu Manyara na Arusha ambapo Mahakama Kuu Moshi iliibuka Mshindi wa kwanza katika mchezo huo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 


MAJAJI NA MAHAKIMU WANAWAKE MNA WAJIBU WA KULETA USAWA KATIKA JAMII; JAJI MKUU

 ·       Awasisitiza Majaji, Mahakimu Wanawake kusimamia maadili ya jamii

·       Asisitiza usawa kati ya Mwanamke na Mwanaume

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amesema Majaji na Mahakimu Wanawake nchini wana wajibu mkubwa wa kusimamia haki za binadamu, maadili ya jamii na usawa wa kijinsia ili kuleta ustawi katika jamii.

Akizungumza jana tarehe 23 Oktoba, 2025 wakati akifungua Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kwenye ukumbi wa Mikutnao wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Masaju alisema kupitia mafunzo hayo ni muhimu wakaweka mikakati thabiti itakayowezesha kufikia ustawi katika jamii.

“Ninachoona ni kwamba ninyi TAWJA mnajitambua, wajibu wenu leo ni kuja na mikakati ambayo itawezesha kutatua hizi changamoto ambazo zimekuwa zinajitokeza kwenye haya masuala yanayowahusu na hasa haki za binadamu wote ambao humo wanajumuishwa Wanawake na Wanaume wakiwa wa umri mbalimbali, wengine watu wazima, wengine wazee na wengine Watoto kwa mfano kuna changamoto hii ya makosa unyanyasaji wa kijinsia,” alisema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alibainisha kuwa, kumekuwa na makosa ya unyanyasaji wa kijinsia na wakati fulani kumekuwa na tafsiri ambayo sio sahihi kwamba jinsia inawahusu Wanawake tu, lakini ni pamoja na wanaume, na hata wanaume kwa wakati au namna fulani nao wananyanyaswa na wa jinsia tofauti.

“Ninatambua kwamba tatizo la unyanyasaji wa wanawake pengine ni wa kiwango kikubwa kuliko ukilinganishwa na unyanyasaji wa wanaume, lakini na wanaume wananyanyaswa isipokuwa tu wanavumilia, jamii yetu imeweka mfumo ambao mwanaume hapaswi kuonekana kama ni dhaifu vile lakini wanavumilia tu na wakati fulani wanapoteza maisha mapema na wakishapotea ndio tunawatambua umuhimu wao, mimi nawashauri muendelee kuwajali wakiwa hai, nawahakikishia kila mmoja anamuhitaji mwenzake, mwanaume anamuhitaji sana mwanamke na mwanamke anamuhitaji sana mwanaume,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju aliongeza kwa kusisitiza kuhusu usawa wa kijinsia ambapo amesema hata Nembo ya Taifa ya Tanzania nayo imeonesha umuhimu kwa kuwa ina Bibi na Bwana, “Mimi si mtaalamu sana wa masuala ya nembo za Taifa japo najua nembo za taifa za Mataifa yote Duniani lakini Tanzania ni ya pekee, Nembo ya Taifa letu inamtambua Mwanaume na Mwanamke na usawa unaanzia pale kama binadamu na wote wanapewa uhuru wa rasilimali za Nchi, hawa ndio wananchi wanaounda Taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama inavyoelezwa kwenye Ibara ya 1 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasema (i) Tanzania ni Nchi moja nayo ni Jamhuri ya Muungano na Ibara ya 2 (1) inaeleza; Eneo la Jamhuri ya Muungano ni eneo lote la Tanzania Bara na eneo lote la Tanzania Zanzibar na pamoja na sehemu yake ya Bahari ambayo Tanzania inapakana nayo.”

Alisema kupitia Nembo hiyo, kila mmoja anaonekana akiwa ameshika Pembe ya Ndovu ambayo ndio utajiri urithi wa Taifa la Tanzania na kiwango cha pembe walichoshika ni sawa kwa hazitofautiani kwa urefu ama ufupi, juu ya nembo hiyo pia kuna Taifa la Tanzania ambao ndio wanamiliki rasilimali za Taifa na nyingine zilizomo kwenye nembo hiyo....

Jaji Mkuu alisema, misingi ya umoja kati ya umoja Mwanaume na Mwanamke ilishawekwa tangu Taifa lipate uhuru na ndio ilipokuja kauli ya ‘Uhuru na Umoja’ hivyo, Mwanaume na Mwanamke wanaounda Taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwa wanaheshimiana, watakuwa huru na wamoja, na kila mmoja amepewa fursa ya kufaidi matunda ya uhuru na rasilimali za nchi na stahili zake nyingine zote.

“Sasa wajibu wetu sisi TAWJA ni kutambua changamoto zinazofanya tusifikie hayo malengo ambayo yapo tangu kuasisiwa na kwa Taifa hili na yamesisitizwa pia katika Katiba Ibara ya 7, 8, 9, 11 lakini pia Ibara ya 22; Ibara ya 22 na 24 zinasema; kila mtu anayo haki ya kufanya kazi; hivyo; mtaendelea kutambua changamoto zipi zinazofanya kwa mfano wanawake wakose hizo fursa,” alisisitiza Mhe. Masaju.

Aliongeza kwamba, Ibara (2) inasema; ‘kila raia anastahili fursa na haki sawa kwa masharti ya usawa ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyo chini ya mamlaka ya Nchi; “hivyo nyie kama Viongozi mtajifunza ni namna gani mtaweza kuimarisha fursa ya ku ‘access’ hivi vitu maana havitakuja kwa upendeleo,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alisema, Majaji na Mahakimu hao wao kama Wanasheria wanaofahamu Katiba na Sheria mbalimbali wana nafasi kubwa ya kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika kuimarisha usawa na heshima ya kijinsia katika Taifa.

“Ibara ya 24 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu kumilika mali inasema; ‘kila mtu anayo haki ya kumiliki mali na haki ya hifadhi ya mali yake aliyo nayo kwa mujibu wa sheria’,” alisema Jaji Mkuu huku akiongeza kuwa hata mwanamke ana haki ya kumiliki mali kama vile Ardhi na kadhalika.

Aidha, Mhe. Masaju alibainisha kwamba, Ibara ya 7 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema, ‘Bila kujali masharti ya Ibara (2) ya Ibara hiyo, Serikali, vyombo vyake vyote na watu wote au mamlaka yoyote yenye kutekeleza mamlaka ya utawala, Madaraka ya kutunga sheria au Madaraka ya Utoaji haki watakuwa na jukumu na wajibu wa kuzingatia, kutia maanani na kutekeleza masharti yote ya sura hiyo, na Ibara ya 8 inasema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii...’

Mhe. Masaju amekihakikishia Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kuwaunga mkono jitihada zinazofanywa na Chama hicho katika kuleta usawa wa kijinsia.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) (hawapo katika picha) wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya Wanachama na Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya na Makamu Mwenyekeiti wa Chama hicho, Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akisalimiana na Majaji Wastaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambao pia ni Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025. Kulia ni Mhe. Dkt. Atuganile Ngwalla na katikati ni Mhe. Joaquine De-Mello.












 

 

BILA AMANI HAKUNA USTAWI WA WANANCHI: JAJI MKUU

  •  Wanawake kama viongozi timizeni wajibu wa kulinda amani, usawa katika jamii
  •  Asema kila Mtanzania ana haki ya kutambulika kwa jinsia yake

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa bila amani hakuwezi kuwa na ustawi wa wananchi jambo ambalo litasababisha jamii kushindwa kutekeleza shughuli zake za kila siku mfano kilimo na uvuvi.

Mhe. Masaju aliyasema hayo jana 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma,wakati alipokuwa akifungua Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) huku akiwataka Majaji na Mahakimu kama wanawake kama viongozi kutimiza wajibu wao wa kulinda amani hasa wanawake wanaofanya kazi katika Mahakama kudumisha Utawala wa Sheria.

“Hivyo bila kuwepo amani, hakuwezi kuwa na ustawi wa wananchi huwezi kwenda shambani, huwezi kwenda kulima, huwezi kwenda kuvua, huwezi kufunga ndoa, huwezi kwenda kwenye ibada huwezi kufanya hata na mambo ya uongozi, huwezi kufanya kazi, utafanyaje kazi wakati hakuna amani kwa hiyo wajibu wa wanawake katika kazi zenu na kama viongozi ni kusisitiza haya na hasa nyinyi wa Mahakamani ambao mna jukumu kubwa sana la kudumisha utawala wa sheria,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alisema kuwa, amani ndio nguzo muhimu ya ustawi wa jamii na kuwataka wanawake ambao ni viongozi kusisisitiza kuhusu amani katika kutekeleza majukumu yao na hasa Mahakama ambayo ina jukumu kubwa la kudumisha utawala wa sheria.

Aidha, Jaji Mkuu, alizungumzia msingi wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwenye utawala, amani, utulivu na usalama pamoja na vipengele vyake vikuu vinne ikiwa ni pamoja na Utawala Bora na Haki, Serikali za mitaa imara zenye ufanisi pamoja na vingine ambavyo vina mchango mkubwa katika kutunza na kuendeleza usalama na ustawi wa Taifa.

Akizungumza kuhusu suala la Utawala wa Sheria, Mhe. Masaju alisema kuwa, “Utawala wa Sheria uliwekwa kwa sababu gani ni kutaka kushamirisha na kuhakikisha kwamba kunakuwa na ustawi wa wananchi ili watu waweze kufanya shughuli zao za kisiasa, kiuchumi na kijamii kwa amani na wakiwa huru lakini sizungumzii utawala wa sheria ambao sisi tumeutaja katika Ibara ya 26 katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.”

Katika upande mwingine, Jaji Mkuu alieleza kuwa Serikali na Vyombo vyote vya Umma vinatoa haki sawa kwa raia wote bila kujali rangi, kabila au dini ya mtu kama inavyotambulika katika Ibara ya 12 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba binadamu wote huzaliwa huru na wote ni sawa.

“Vyombo vyote vya umma vinatoa nafasi iliyo sawa kwa raia wote wake kwa waume bila kujali rangi kabila, dini au hali ya mtu, kwa kuangalia mtu unasema huyu wa dini fulani, sasa hiyo ni changamoto, kwa aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uovu au upendeleo vinaondolewa nchini, kwamba matumizi ya utajiri wa Taifa yanatilia mkazo maendeleo ya wananchi na hasa zaidi yalielekezwa kwenye jitihada za kuondoa umasikini, ujinga na maradhi,” alisema Mhe. Masaju.

Aliongeza kuwa, kila Mtanzania ana haki ya kutambulika kwa jinsia yake, na kuthaminiwa kupewa haki kama ilivyotajwa katika Ibara ya 12 (2) kwamba kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.

“Mimi naamini tunapaswa kutambua na kuthamini hizi jinsia zetu kwa jinsi wanavyozaliwa anayezaliwa mwanaume ataitwa mwanaume, anayezaliwa mwanamke ataitwa mwanamke, vinginevyo tutashindwa kupata haki iliyotajwa katika Ibara ya 12 kwa sababu binadamu wote tumezaliwa huru na wote ni sawa,” alisema Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju aliwasisitiza pia TAWJA kusimamia uhuru wao wa kufanya maamuzi na kwamba wawe huru kufanya kazi kwa kuzingatia Katiba na Sheria bila kuburuzwa na mtu yoyote ili kuendelea kujenga jamii yenye ustawi amani na usawa.


 Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakifuatilia hotuba ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA)  iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya Wanachama na Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya na Makamu Mwenyekeiti wa Chama hicho, Mhe. Victoria Nongwa.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

TAWJA KUIMARISHA UONGOZI, HAKI ZA KIJINSIA KWA WARATIBU KIKANDA

      Yafanya mafunzo yazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050

      Yadhamiria kuimarisha haki, usawa wa kijinsia nchini

Na HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma

Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba 2025 kimeanza kufanya mafunzo maalum kwa Waratibu wa Kikanda wa chama hicho, ambayo yamelenga kuimarisha uongozi, usimamizi na uwajibikaji katika kulinda haki za kijinsia na za binadamu.

Mafunzo hayo yalifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, ambapo mgeni rasmi alikuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa TAWJA ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Barke Sehel, alisema kuwa kufanyika kwa mafunzo hayo kuongeza uwezo wa Waratibu wa Mkoa katika uratibu, mawasiliano, na utekelezaji wa programu za kikanda.

“Tunatarajia kuwa kupitia waratibu hawa, TAWJA itaimarika na kuwa kinara katika ulinzi wa haki za binadamu na usawa wa kijinsia nchini,” alisema Mhe. Sehel.

Aliwataka washiriki wa mafunzo hayo kutumia fursa hiyo kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuboresha ushiriki wa wanawake katika uongozi, si tu ndani ya Mahakama bali pia katika jamii kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Mhe. Sehel, TAWJA imejikita katika kupambana na unyanyasaji wa kijinsia kwa kutoa elimu, kuhamasisha jamii na kushirikiana na Taasisi mbalimbali ili kuhakikisha haki za wanawake na watoto zinalindwa.

Aliongeza kuwa, takwimu zinaonyesha mashauri ya unyanyasaji wa kijinsia bado ni changamoto nchini, jambo linalohitaji juhudi endelevu za wadau wote katika kutoa elimu na kufungua mashauri kwa wakati.

Mhe. Sehel alitumia nafasi hiyo kumshukuru Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwa kukubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi na kwa kuonyesha utayari wa kuunga mkono juhudi za chama katika kukuza nafasi ya mwanamke ndani ya mfumo wa Mahakama na jamii kwa ujumla.

Mafunzo hayo ya siku mbili yamefadhiliwa na Mahakama ya Tanzania kupitia ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama, hatua inayodhihirisha ushirikiano mkubwa unaolenga kutimiza Ibara ya 9 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayosisitiza heshima ya utu, usawa wa binadamu na haki sawa kwa wote bila ubaguzi.

Mada mbalimbali zitawasilishwa kwenye mafunzo hayo ya siku mbili, ikiwemo Dhamira na Vipaumbele vya Kimkakati vya TAWJA, Uimarishaji wa Uanachama na Ushiriki wa Kikanda, Haki za Kijinsia na Uongozi, Ufuatiliaji na Tathmini, pamoja na Uhamasishaji wa Rasilimali na Uendelevu. Mada hizo zinalenga kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025/2050 inayohimiza utawala bora, amani, usalama, na fursa sawa kwa wote.


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzani (TAWJA),  Mhe. Barke Sehel akitoa neno la utangulizi mbele ya Mgeni Rasmi Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo maalum kwa Waratibu wa Kikanda wa chama hicho jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mwenyekiti wa TAWJA, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya na Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Mhe. Victoria Nongwa.


Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakifuatilia kinachojiri wakati wa hafla ya ufunguzi 
wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Alhamisi, 23 Oktoba 2025

TANZANIA’S PRINCIPAL JUDGE DR. MUSTAPHER SIYANI SHARES JUDICIAL INSIGHTS AT 2025 WIPO INTELLECTUAL PROPERTY JUDGES FORUM

By UPENDO NGITIRI-Judiciary of Tanzania, Switzerland

The World Intellectual Property Organization (WIPO) held the 2025 WIPO Intellectual Property Judges Forum on 14th and 15th October 2025 at its headquarters in Geneva, Switzerland.

The forum brought together over 500 judges from various jurisdictions across the globe, providing a platform for sharing experiences, exchanging expertise, and fostering cross-border judicial dialogue on pressing intellectual property issues.

Hon. Dr. Mustapher Siyani, Principal Judge of the High Court of Tanzania and a newly elected member of the WIPO Advisory Board of Judges, was among distinguished esteemed   jurists invited to share judicial experiences from their respective jurisdictions at the forum.

The discussions at the forum covered a wide range of topics, including judicial protection of well-known marks, digital and cross-border evidence, industrial designs, pharmaceutical patents, copyright and related rights, personality rights, calculation of damages in civil proceedings, and criminal enforcement. Each session was presented by a panel of eminent jurists carefully selected by WIPO.

Hon. Dr. Siyani, who served as a panellist in Session 7, delivered a compelling presentation on Tanzania’s judicial approach on calculation of damages in intellectual property disputes. He observed that while damages are recognized as a legal remedy under Tanzanian law, there is no codified formula for their calculation. Drawing on Tanzanian jurisprudence, he deliberated the notable case of Tanzania-China Friendship Textile Company Limited v. Nida Textile Mills (T) Ltd., Civil Case No. 106 of 2020 where the Court awarded general damages for copyright infringement but declined to award specific damages due to lack of evidence directly linking the claimed specific damages and the infringement. The Court also denied the claim for the infringer’s profits, as it was not properly pleaded and proven.

 

Hon. Dr. Siyani underscored that general and specific damages are the two primary categories of damages awarded in IP disputes in Tanzania. He emphasized that, although there is no fixed formula in calculation of damages, courts have developed a flexible, case-by-case approach guided by judicial precedents. He further clarified that specific damages must be specifically pleaded and strictly proven, while general damages require proof of ownership and infringement and are awarded at the court’s discretion.  However, he noted that reliance on judicial discretion can lead to inconsistency and unpredictability, even when different judges are presented with the same facts. To mitigate this, he remarked that statutory damages,which establish defined ranges for awards in IP disputes,could serve as an effective means of ensuring fairness, consistency, and predictability. Currently, Tanzanian law does not provide for such damages.

In the same session, Hon. Justice Dedar Singh Gill of the Supreme Court of Singapore shared Singapore’s approach in assessing damages under the Trademark Act, which allows for statutory damages in infringement cases. He described that damages are assessed within a defined range after considering factors such as the flagrancy of the infringement, losses suffered by the claimant, benefits gained by the defendant, and the need for deterrence.

He also outlined the Canadian method used to quantify damages in counterfeit goods cases, where damages are assessed per incident of infringement and vary depending on the nature of the infringer. Canadian law specifies different amounts payable in situations such as when the defendant operates from temporary facilities (flea markets), conventional retail premises (stores), or as a manufacturer, importer, or distributor of counterfeit goods.

 

Hon. Justice Dr. Nehad Alhusban of the Supreme Court of Jordan also shared Jordan’s approach on calculation of damages in IP disputes under its Copyright Protection Law, where material damages are determined based on two essential elements: actual losses and loss of profits.

Other distinguished jurists who contributed in Session 7 included Judge Woo Sungyop, Presiding Judge of the IP High Court of Korea, and Judge Jean Gayet, Presiding Judge of the Third Section, Court of Paris, France.

Beyond the rich judicial dialogue, Ms. Eun-Joo Min, Director of the WIPO Judicial Institute, presented an overview of WIPO’s work with Judiciaries. Ms. Eun- Joo Min highlighted various activities undertaken by WIPO Judicial Institute in collaboration with the judiciaries across the globe. She  acknowledged   the Judiciary of Tanzania for its exemplary collaboration with WIPO, highlighting several key achievements attained  under the longstanding  strong partnership .The  Achievement highlighted  in the forum  includes development of customized judicial training materials, participation of  great  number of Tanzanian judicial officers in judicial capacity-building programs such as the General Distance Learning Course for Judges, Judicial Colloquiums held in Tanzania, and the WIPO Annual Judges Forum, publication of Tanzanian judicial decisions on WIPO Lex, adoption of WIPO’s online mediation tools, and appointment of Hon. Dr. Siyani, Principal Judge of the High Court of Tanzania to the WIPO Advisory Board of Judges.

During the second day of the forum, WIPO officially announced the newly elected WIPO Advisory Board of Judges. The Advisory Board provides practical and technical advice to WIPO on matters related to the judicial administration of intellectual property worldwide. The Principal Judge of the High Court of Tanzania and other nine eminent Jurist appointed to join the board was announced to be the member of the WIPO Advisory Board of Judges. His appointment marks an important milestone, highlighting Tanzania’s growing role in global judicial cooperation.

The 2025 WIPO Judges Forum, which ended on 15th October 2025, has reinforced the Judiciary of Tanzania’s position as an active and respected voice in the global IP community. Through the meaningful contributions of the Principal Judge at the forum, as well as the participation of Tanzanian judges in the forum, the Judiciary has consistently demonstrated its commitment to advancing knowledge, consistency, and cooperation in the adjudication of intellectual property disputes. This involvement reflects Tanzania’s dedication to shaping the national landscape of intellectual property rights while strengthening its role in international judicial dialogue.

Judges of the Court of Appeal and High Court of Tanzania who participated  the forum virtually included   Hon. Zephrine Galeba, JA; Hon. Dr. Paul F. Kihwelo,JA ; Hon. Issa Maige, JA ;Hon. Gerson Mdemu, JA ; Hon. Prof. Ubena John,JA ;  Hon. Rose Ibrahim,J ;  Hon. Salma Magimbi , J Hon. Isaya Arufani,J ; Hon. Dr. Adam Mambi, J;  Hon. Ilvin Mugeta,J ;Hon. Dr. Yose Mlaymbina,J Hon. Stephen Magoiga,J; Hon. Thadeo Mwenempazi,J;  Hon.  Butamo Philiph, J; Hon. Fahamu Mtulya, J;Hon. Dr. Juliana Masabo,J; Hon. Dr. Lilian Mongela,J; Hon. Revocati Mteule,J; Hon. Messeka Chaba, J; Hon. Frank Mahimbali, J; Hon. Safina Simfukwe, J; Hon. Nyigulila Mwaseba, Hon. John Nkwabi,J; Hon.  Awamu Mbagwa, J; Hon. Dr. Theodora Mweneghoha,J; Hon. Dr. Fatma Khalfan,J; Hon. Suleiman Hassan J; Hon. Musa Pomo, J; Hon. Wilbert Chuma, J; Hon. Sarah Mwaipopo, J; Hon. Dr. Emanuel Kawishe,J; Hon. Abdallah Gonzi, J; Hon. Irene Musokwa, J; and Hon. Hadija Kinyaka,J.

After the Conclusion of the Judges forum, the WIPO Advisory Board of Judges held its inaugural meeting on 16th October 2025 at WIPO Headquarters. Hon. Dr.  Siyani, Principal Judge of the High Court of Tanzania, attended the meeting along with nine other appointed eminent Board members. His leadership at WIPO is testament of the Judiciary of Tanzania’s firm commitment to international cooperation on intellectual property and his dedication in protection of justice.

Concurrently with the Advisory Board meeting, the Judiciary of Tanzania and WIPO convened special meetings, held each year at WIPO Head quarters after the Judges Forum. These meetings were attended by the Chief Registrar of the Judiciary of Tanzania, the focal person for collaboration between WIPO and the Judiciary of Tanzania, and senior officials from the WIPO Judicial Institute, WIPO Arbitration and Mediation Center, and WIPO Academy. The discussions focused on key issues concerning the ongoing collaboration and activities to be undertaken in 2026 as part of implementation of the Memorandum of Understanding (MoU) executed in 2021.

 

       Hon. Dr. Mustapher , Siyani , Principal Judge of the High Court of Tanzania

Panelists  during  Session on Calculation of Damages.

Participants from various Jurisdictions at the opening ceremony of the WIPO  Annual Judges Forum.

The third from left is WIPO Assistant Director General,  Dr. Marco Aleman,  centre is Principal Judge of the High Court  of Tanzania and Member of   WIPO Advisory Board of Judges, Hon. Dr. Mustapher Siyani, the second from left is Judge of High Court of Zanzibar, Hon.  Haji Suleiman Khamis,  the  first from right is Chief Registrar of the Judiciary of Tanzania, Hon. Eva Nkya, the second from right is Director of WIPO Judicial Institute,  Ms. Eu- Joo Min, the third from right is Legal Officer , WIPO Judicial Institute  Ms.  Ines Ferdinandez and the first from left is Deputy Registrar and Focal Person for the Collaboration between WIPO and the Judiciary of Tanzania, Hon.Upendo Ngitiri.