Na MWANAIDI MSEKWA na NAOMI KITONKA- Mahakama, Dar es Salaam.
Mamlaka
ya Serikali Mtandao (eGA) imeahidi
kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili
kuimarisha na kuboresha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
(TEHAMA) katika utoaji huduma mbalimbali za kimahakama
ikiwemo usikilizaji wa mashauri.
Ahadi
hiyo imetolewa jana
tarehe 25 Aprili,
2025 na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Bw. Benedict
Benny Ndomba alipokuwa anawasilisha mada kuhusu matumizi
ya TEHAMA katika usikilizaji wa mashauri kwenye Mkutano wa Mwaka wa Mahakama ya Rufani uliokuwa
unafanyika kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano Julius Nyerere jijini
Dar-es-Salaam.
Akizungumza
katika wasilisho lake,
Bw. Ndomba alisema, “Kila Taifa,
sekta na Taasisi
ulimwenguni zinalenga mkazo wa matumizi ya TEHAMA ili kuboresha utendaji kazi
na kuwahudumia Wadau
kwa urahisi na ufanisi.”
Aliongeza kwa kusema TEHAMA ina uwezo wa kuleta mapinduzi chanya kwenye
utendaji kazi wa Taasisi, ikiwemo ngazi zote za Mahakama kama ilivyo kwa Taasisi
nyingine.
Alieleza kuwa Mahakama iwe tayari kukubali mabadiliko
yanayoletwa na teknolojia ikiwemo kuendelea kuboresha taratibu zake za utendaji
kazi (Business Process re-engineering) na kujifunza namna ya kuendana nayo kama
njia bora zaidi ya kukamilisha majukumu ya kimahakama.
Vilevile
katika Mkutano huo, Majaji
wa Mahakama ya Rufani na wajumbe wengine wote walipata elimu ya jinsi ya
kufurahi pale wanapostaafu kutoka kwa Mhadhiri
Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi, ambaye alisisitiza umuhimu wa
kujali afya pamoja na malezi ya familia yenye tija ili kupunguza migogoro na
mawazo kabla na baada ya kustaafu.
Aidha,
Dkt. Shilingi alitoa zawadi kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis
Juma na kwa Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert baada ya wasilisho lake.
Mkutano huo ulihitimishwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na ulihudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani, Msajili Mkuu, Mtendaji Mkuu, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Wakurugenzi, Wasaidizi wa Sheria na watumishi wa kada mbalimbali za Mahakama.
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akipokea zawadi ya kitabu
kutoka kwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi katika Mkutano huo.
Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe, Dkt. Venance Shilingi Katika Mkutano huo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Serikali Mtandao (eGA), Bw. Benedict Benny Ndomba akitoa mada kwenye mkutano huo.
Wajumbe wa Mkutano wakisikiliza kwa makini wasilisho kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Serikali Mtandao (eGA), Bw. Benedict Benny Ndomba (hayupo pichani) kwenye mkutano huo.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma