Alhamisi, 7 Februari 2019

MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA DODOMA: WADAU WATAKIWA KUTEKELEZA WAJIBU WAO KURAHISISHA UPATIKANAJI WA HAKI


Na Lydia Churi- Mahakama, Dodoma
Watumishi wa Mahakama, wadau pamoja na wananchi wametakiwa kila moja kutekeleza wajibu wake katika mchakato uzima wa upatikanaji wa haki ili kesi ziweze kumalizika kwa wakati Mahakamani.

Akizungumza kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa Mahakama Kuu kanda ya Dodoma, Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo Mhe. Ignas Kitusi alisema kesi kutokumalizika kwa wakati Mahakamani hakutokani na Mahakama pekee bali wakati mwingine huchangiwa na wadau wa mahakama wakiwemo wananchi.

“Mawakili mnapaswa kujiuliza pale mnaposhindwa kesi Mahakamani kwa sababu za kisheria, je mnawaeleza wateja wenu ukweli kuwa mmeshindwa kutokana na makosa yenu au mnawaambia maneno yanayoharibu sifa ya Jaji?” alisema Jaji Kitusi na kuongeza kuwa Mawakili nao wana mchango katika kufanya kesi zisimalizike kwa wakati. 

Kuhusu wananchi kwa upande wao, Jaji Kitusi alisema wanao mchango mkubwa katika kukwamisha kesi kusonga mbele pale wanaposhindwa kufika Mahakamani kutoa ushahidi katika kesi mbalimbali. Aliwataka wananchi wanaotoa ushahidi Mahakamani kufanya hivyo kwa kusema ukweli na kuwa na hofu ya Mungu. 

Jaji Kitusi pia alitoa wito kwa wananchi kuamini vyombo vya Sheria na pia kuwaamini Majaji na Mahakimu wanapoendesha kesi zao ili haki zao zipatikane kwa wakati. Alisema kitendo cha Mwananchi kutomwamini Jaji au Hakimu kinachangia kuchelewesha upatikanaji wa haki. 

Aidha, Jaji Mfawidhi aliwataka wakuu wa Mikoa na wilaya nchini kuwashauri wananchi wanaopeleka malalamiko kwenye ofisi za viongozi hao kuwashauri kutumia mfumo uliopo kisheria wa kukata rufaa na si kulalamika ili kurahisisha upatikanaji wa haki.

Alitoa wito kwa jeshi la Polisi nchini kuwaongezea uwezo askari wake wa upelelezi ili kesi ziendeshwe kwa kutotegemea maelezo ya ungamo ya watuhumiwa kwa kuwa kwa kutumia maelezo hayo huifanya kesi kuwa na ugumu inapofika mahakamani.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Dkt. Binilith Mahenge aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa Kauli mbiu ya mwaka huu ambayo alisema iko wazi kuhusu suala la upatikanaji wa haki. Alisema upatikanaji wa haki kwa wakati  hutegemea Mahakama, wadau na wananchi.

Alisema changamoto ya upatikanaji wa haki kwa wakati iko kwa Watumishi wa Mahakama, Majaji na Mahakimu pamoja na wananchi kwa kuwa kila mmoja ana changamoto zake katika mchakato wa upatikanaji wa haki.

Naye Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Samwel Malecela aliitaka Mahakama kutenda haki ili kudumisha Amani ya nchi. Aliwataka viongozi wa Mahakama kutekeleza wajibu wao kwa kufuata haki na utawala bora. 

Maadhimisho ya wiki ya sheria yalifanyika kitaifa katika jiji la Dodoma kuanzia Januari 31 na kufikiwa kilele chake ambacho ni siku ya Sheria nchini Februari 6, 2019. Maadhimisho haya yamefanyika nchini kotye katika ngazi ya Mahakama za wilaya na Mikoa.

 Brass Bendi ya Jeshi la Polisi ikiongoza Maandamano ya kuadhimisha Siku ya Sheria nchini katika kanda ya Dodoma ya Mahakama Kuu ya Tanzania. 


Majaji wakiongoza Maandamano ya kuadhimisha siku ya Sheria Nchini Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Ddodoma jana. Katikati ni Jaji  wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Dodoma Mhe. Ignas Kitusi. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu kanda ya Dodoma Mhe. Latifa Mansoor na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma Mhe. George Masaju.
Wanafunzi wa vyuo na shule za Sekondari pia walishiriki kwenye Maandamano ya kuadhimisha siku ya Sheria Nchini Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Ddodoma jana.
Majaji wakiwa tayari kuanza shughuli za Maadhimisho mara baada ya Maandamano ya kuadhimisha siku ya Sheria Nchini Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Ddodoma jana. Katikati ni Jaji  wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Dodoma Mhe. Ignas Kitusi. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu kanda ya Dodoma Mhe. Latifa Mansoor na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma Mhe. George Masaju.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Dkt. Binilith Mahenge (katikati) akiongoza wageni mbalimbali walioalikwa kuhudhuria hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome.
 Jaji  wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Dodoma Mhe. Ignas Kitusi akijiandaa kukagua Gwaride la Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
 Jaji  wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Dodoma Mhe. Ignas Kitusi akikagua Gwaride la Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
 Kikundi cha Ngoma ya Asili ya kabila la Wagogo wakitumbuiza wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
 Baadhi ya Mahakimu, watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania pamoja na wadau wakiwa kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
Baadhi ya Wanafunzi wakiwa kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.

 Jaji  wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Dodoma Mhe. Ignas Kitusi akizungumza wakati wa sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samwel John Malecela (wa kwanza kulia) alikuwa ni miongoni mwa wazee wa jiji la Dodoma walioalikwa kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni