Jumatano, 8 Mei 2019

MAHAKAMA YAUNGANISHA MFUMO WA JSDS NA MFUMO WA MAPATO WA SERIKALI


Na Dennis Buyekwa-Mahakama
Mahakama ya Tanzania  imeunganisha mfumo wake wa kusajili na kuratibu mashauri (JSDS ll) na mfumo wa serikali wa ukusanyaji wa Mapato (GePG) ili kurahisisha ukusanyaji wa mapato na kuondokana na changamoto zinazotokana na ukusanyaji na utunzanji wa mapato ya serikali.

Katika hatua za kuhakikisha mfumo huu unafanya kazi yake ipasavyo, Mahakama ya Tanzania imeandaa mafunzo ya siku mbili kwa Wahasibu na Makarani wake yaliyoanza jana katika  kituo cha Mafunzo na Habari  kilichopo ndani ya viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam.

Akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji Bw. Mathias Mwangu alisema mafunzo hayo yanawahusisha Wahasibu na Makarani wa Mahakama wenye uelewa wa namna mfumo wa JSDS ll unavyofanya kazi na yanaendeshwa na Mahakama kwa kutumia maafisa Tehama wake ambao ndio waratibu na wasimamizi wa Mfumo huo.

Alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwaandaa Wahasibu na Makarani kufanya kazi ya kuratibu vyema makusanyo yote yanayokusanywa baina ya Mahakama ya Tanzania na Serikali.

Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji alisema mfumo huo pia utaongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za Mahakama kwa kuwa sasa utawapunguzia mzigo Makarani wa kukutana na wadaawa moja kwa moja na badala yake Shughuli zote zitafanyika kupitia mfumo huo na watumishi sasa wataweza kufuatilia malipo yote kupitia mfumo huo wa kielektroniki.

Alizitaja faida za kutumia mfumo huo katika ukusanyaji wa maduhuli kuwa ni , pamoja na kusaidia kukusanya mapato yanayotokana na huduma zinazotolewa na Mahakama ili kusaidia Serikali kuboresha huduma mbalimbali kwa wananchi wake.
“Mfumo huu umekuja kama muarobaini wa kuzuia upotevu wa mapato ya serikali kiholela", alisema Bwn. Mwangu na kuongeza kuwa ukusanyaji mzuri wa mapato utaisaidia Serikali kutekeleza mipango yake ya maendeleo.

Kuhusu utaratibu wa kutoa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji alisema Mahakama imeyagawa mafunzo hayo katika kanda kuu nne (4) ambapo kutakuwa na vituo vya Dar es Salaam ambacho kina jumuisha washiriki kutoka katika mikoa ya Morogoro, Pwani, Tanga, Lindi na Mtwara.

Vituo vingine ni Mbeya, Mwanza na Dodoma ambapo pia wanatarajia kuendesha mafunzo kama hayo katika siku za usoni kulingana na namna ratiba za uendeshaji wa mafunzo hayo.

Naye mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka katika kitengo cha Tehama cha Mahakama Bwn. Athumani Juma ameeleza kuwa kupitia mfumo huu wa kielektroniki Mawakili pamoja na wadaawa wataweza kufanya malipo kwa wakati kitendo kitakachowasaidia kusajili kesi zao kwa urahisi na haraka Zaidi.

Alisema mfumo huo utarahisisha ukusanyaji wa mapato ndani ya Mahakama, utaokoa muda na gharama na pia utasaidia kufanya malipo mahakamani ikiwa ni pamoja na kuimarisha ulinzi katika kutunza taarifa za kimahakama.

Mfumo wa kielekitroniki wa kusajili na kuratibu mashauri (JSDS ll) ulianzishwa kwa lengo la kurahisisha zoezi zima la usajili wa kesi mbalimbali, lakini kutokana na uhitaji wa kuboresha huduma za kimahakama, Mahakama imeona ni vyema kuboresha huduma kwa kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato hatua itakayosaidia kutoa huduma bora na haki sawa kwa wote.

 Watumishi wa Mahakama wakiwemo Wahasibu na Makarani wakiwa kwenye mafunzo kuhusu ukusanyaji wa mapato baada ya kuunganishwa kwa mfumo wa  kusajili na kuratibu mashauri (JSDS ll) wa Mahakama ya Tanzania na mfumo wa  serikali wa ukusanyaji wa Mapato (GePG) yanayofanyika katika kituo cha Mafunzo na Habari  kilichopo ndani ya viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam.
 Mhasibu wa Mahakama ya Tanzania Bibi Annastela Natai akizungumza wakati wa mafunzo ya Wahasibu na Makarani wa Mahakama kuhusu ukusanyaji wa mapato baada ya kuunganishwa kwa mfumo wa  kusajili na kuratibu mashauri (JSDS ll) wa Mahakama ya Tanzania na mfumo wa  serikali wa ukusanyaji wa Mapato (GePG) yanayofanyika katika kituo cha Mafunzo na Habari  kilichopo ndani ya viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam.
 Afisa Tehama wa Mahakama, Samwel Mshote akitoa mada wakati wa mafunzo ya Wahasibu na Makarani wa Mahakama kuhusu ukusanyaji wa mapato baada ya kuunganishwa kwa mfumo wa  kusajili na kuratibu mashauri (JSDS ll) wa Mahakama ya Tanzania na mfumo wa  serikali wa ukusanyaji wa Mapato (GePG) yanayofanyika katika kituo cha Mafunzo na Habari  kilichopo ndani ya viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam.
 Afisa Tehama wa Mahakama, Athuman Juma akitoa mada wakati wa mafunzo ya Wahasibu na Makarani wa Mahakama kuhusu ukusanyaji wa mapato baada ya kuunganishwa kwa mfumo wa  kusajili na kuratibu mashauri (JSDS ll) wa Mahakama ya Tanzania na mfumo wa  serikali wa ukusanyaji wa Mapato (GePG) yanayofanyika katika kituo cha Mafunzo na Habari  kilichopo ndani ya viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam.

 Mmoja wa Watumishi wa Mahakama wanaohudhuria mafunzo akichangia mada wakati wa mafunzo hayo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni