Jumatatu, 10 Oktoba 2022

BUNDI ATUA MASHINDANO YA SHIMIWI TANGA

·Mahakama Sports yahujumiwa kila kona baada ya kuonekana tishio

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Katika hali isiyokuwa ya kawaida, mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa leo tarehe10 Octoba, 2022 yameingia doa kutokana na dosari lukuki, ikiwemo viongozi kuruhusu baadhi ya timu kuchezesha mamluki.

Dosari zilianza kujionyesha mapema asubuhi wakati wa mchezo wa kamba kwa lengo la kuihujumu Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume iliyokuwa inashiriki mchezo huo. Katika mchezo huo, Mahakama Sports ilikuwa imenyane na Uchukuzi kwa kufuata kanuni za mashindano, lakini ilichezeshwa kibabe huku viongozi wa SHIMIWI wakiruhusu Uchukuzi kuchezesha wachezaji ambao siyo watumishi.

Kwa kwa mujibu wa kanuni za mashindano, kila timu inatakiwa kuleta wachezaji wenye vitambulisho ambavyo vinaonyesha picha ya mshiriki, namba yake ya cheki, tarehe ya ajira, kituo chake cha kazi na kitambulisho hicho kisainiwe na afisa wa michezo wa Idara au Wizara yake.

Wakati ulipowadia wa kuchezwa mchezo huo katika Viwanja vya Shule ya Ufundi Tanga, mmoja wa wachezaji wa Uchukuzi hakuwa na kitambukisho na baadhi ya vitambulisho vya wachezaji wengine havikuwa na kumbukumbu muhimu, ikiwemo namba za cheki za watumishi hao.

Lakini cha kushangaza, mwamuzi wa mchezo huo ambaye inasadikiwa ni mtumishi wa Uchukuzi pamoja na baadhi ya viongozi wa SHIMIWI wakaamuru mchezo huo ufanyike, kitendo kilichoifanya Timu ya Mahakama kucheza chini ya mgomo na kupoteza mpambano huo.

Viongozi wa Mahakama wameamua kuchukua hatua, ikiwemo kukata rufaa ambayo kuna figisufigisu zinaendelea za kutosikiliza rufaa hiyo kwa wakati ili kuibeba timu ya Uchukuzi.

Baada ya mchezo huo, figisufigisu zilihamia katika Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Popatlal majira ya jioni ambapo Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu ilikuwa icheze na timu ya RAS Simiyu, lakini cha kushangaza Timu ya Uchukuzi ilivamia uwanja huo na kusababisha mchezo huo uahirishwa katika mazingira ya kutatanisha bila ya viongozi wa SHIMIWI kuchukua hatua.

Figisu zingine zenye nia ya kuihujumu Timu ya Mahakama zilijitokeza wakati wa mchezo wa riadha ambapo Mahakama ilishiriki katika mbio za kupokezana vijiti. Lakini cha kushangaza Timu hiyo ya Mahakama iliondolewa kwenye mashindano hayo katika mazingira ya kutatanisha. Mahakama Sports iliingia katika mchezo wa robo fainali ya mchezo huo baada ya kushika nafasi ya tatu kwenye makundi.

Janja janja nyingine ilijitokeza wakati mchezaji wa Mahakama mbio za wazee alishika nafasi ya tatu, lakini waamuzi wakachomeka jina na mtu mwingine na mtumishi huyo kupewa nafasi ya nne, hivyo kukosa medali aliyokuwa amestahili kuipata.

Mahakama Sports ipo Tanga kushiriki katika michezo mbalimbali inayoendeshwa na SHIMIWI, ikiwemo Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Riadha, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, bao, pamoja na michezo mingine mingi ya ndani.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Riadha.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni