Jumatatu, 10 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS KAMBA HAISHIKIKI

·Kamba Wanawake watangulia nusu fainali

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake leo tarehe 10 Octoba, 2022 imeizamisha RAS Iringa na kufanikiwa kuingia hatua ya nusu fainali katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.

Mchezo huo mzuri wa robo fainali uliofanyika majira ya saa moja asubuhi katika Viwanja vya Tanga Technical School ulianza kwa timu zote kutunishiana misuri, huku RAS Iringa wakijaribu kuwakazia wapinzani wao.

Hata hivyo, Mahakama Sports walisimama imara na kuwaondoa kwenye mchezo baada ya kuwakata pumzi na kufanikiwa kupata ushindi katika mzunguko wa kwanza. Katika mzunguko wa pili, Mahakama Sports hawakuwa na mzaha na mtu na haikuwachukua muda kumaliza mchezo huo kwa kuwaminya kisawasawa RAS Iringa.

Kufuatia matokeo hayo, Mahakama Sports Kamba Wanawake itakutana na Waziri Mkuu Sera kwenye nusu fainali. Timu ya Waziri Mkuu Sera wamefika katika hatua hiyo baada ya kuwatoa kwenye mashidano hayo timu ya Tamisemi.

Kabla ya kuingia kwenye nusu fainali, Mahakama Sports ilishiriki katika 16 bora na kushinda mechi zake zote.  Ilicheza mechi yake ya kwanza ya makundi na RAS Singida ambapo ilitoa kichapo kikali.

Mechi yake ya pili ilikutana na Maji ambayo yalikamuliwa kisawasawa kwa mizunguko yote miwili na katika mechi ya tatu ilipangiwa na RAS Manyara ambao waliingia mitini baada ya kuogopa kupokea dozi iliyokuwa imeandaliwa kwa ajili yao. Mahakama Sports ilikutana na Viwanda na kuisambaratisha vikali katika mechi yake ya nne.

Wachezaji wa Kamba Wanawake ni Zahara Abdallah, Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Melina Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca Mwakabuba, Salma Mwamende, Sarafina Mkumbo, Mariam Mayala, Zawadi Amir, Namweta Mcharo, Valeria Ntyangili, Anna Hebron, Lucy Mbwaga, Rose Mwalongo na Tumaini Kizito.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake kabla ya mchezo (picha na maktaba).
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake ikijiandaa kukamuana na RAS Iringa.
Timu ya Kamba Iringa ikijiandaa kupambana.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake (juu) ikiwakamua RAS Iringa (chini), ambao baadhi yao wanaonekana kuzidiwa na kuamua kuvuta kamba wakiwa wamekaa chini.

Majabari ya Mchezo wa Kamba Wanawake yakitoka uwanjani baada ya kuwashikisha adamu RAS Iringa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni