Jumapili, 9 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS MPIRA WA MIGUU MLIMA WA MOTO

 · Maji yashindwa kuupanda na kutiririshwa nje mashindano SHIMIWI

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Wimbo usemao Mungu akipenda tutaonana tena baadaye leo tarehe 9 Octoba, 2022 ulitawala katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Galanos mara baada ya Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume kuyakausha Maji kwenye mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.

Mahakama Sports iliichapa Timu ya Maji mabao 5:3 kwa mikwaju ya matuta baada ya timu zote mbili kushindwa kufungana katika muda wa kawaida. Hatua hiyo imeiwezesha Mahakama Sports kutinga katika hatua ya robo fainali.

Mchezo huo ambao umechezwa majira ya saa nane mchana ulianza kwa kasi huku timu zote mbili zikishambuliana kwa zamu. Maji ndiyo waliokuwa wa kwanza kulisakama lango la Mahakama, lakini beki yao ilikuwa makini na kuzuia hatari zote zilizokuwa zinaelekezwa upande wao.

Baada ya dakika chache, wachezaji wa Mahakama walitulia na kuanza kucheza pasi fupi fupi na kufanikiwa kumiriki mpira muda wote. Hatua hiyo iliamsha shangwe za mashabiki wa Mahakama Sports ambao waliishangilia timu yao muda wote wa mchezo huo.

Mahakama ilitengeneza nafasi nyingi za kuweza kujipatia mabao, lakini wachezaji walishindwa kutumia nafasi hizo katika vipindi vyote viwili. Kulikuwepo na zomea zomea na kejeli za kimichezo za hapa na pale kutoka pande zote mbili, lakini kandanda safi lililoonyeshwa na Mahakama Sports liliwanyamazisha mashabiki wa timu pinzani.

Hadi mwamuzi anapuliza kipenga kuashiria kumalizika kwa mpambamo huo timu zote zilikuwa zimetoshana nguvu sawa. Baada ya mikwaju ya matuta kuamriwa kupigwa, Mahakama Sports ndiyo iliyooanza kuukwamisha mpira kambani.

Katika upigaji huo, Mahakama Sports ilipata mikwaju yote mitano na Maji wakaambulia mitatu baada ya Mdaka Mabomu wa Mahakama, Hassan Aufi kupangua mkwaju mmoja na kuwafanya timu hiyo pinzani kuondoshwa kwenye mashindano hayo.

Mwalimu wa Timu hiyo Spear Mbwembwe alishindwa kuzungumza chochote baada ya kumalizika kwa mchezo huo kutokana na furaha kubwa aliyokuwa nayo. Katibu Mkuu wa Mahakama Sports Robert Tende alisema vijana wake wameau Jitu jingine kwenye mashindano hayo.

"Timu ya Maji ndiyo iliyokuwa inaogopwa kwenye mchezo huu. Tumewahukumu kifungo cha mwaka mmoja kutokushiriki kwenye mashindano haya. Jalada la kesi hii limefungwa, tuonane mwakani," Katibu huyo alitamba.

Kabla ya kufikia hatua hiyo, Mahakama Sports Mpira wa Miguu ilishiriki kwenye mechi za makundi na ilianza kwa kukutana na Timu ya Utumishi na kuisanua mabao mawili kwa nunge na baadaye ikakutana na Hazina katika mechi ya pili na kupoteza kwa taaaabu kwa mabao mawili kwa moja.

Katika mechi yake ya tatu, Mahakama ilimenyana na Ukaguzi na kuwafumua kwa bao moja kwa yai na baadaye ilifanya mauaji kwa kuishindilia timu ya Maendeleo ya Jamii kwa mabao sita kwa moja.

Wachezaji wa Mpira wa Miguu walioiwakilisha Mahakama katika michezo hiyo walikuwa Fahamu Kibona; Iman Patson; Gisbert Chentro; Akida Mzee; Emmanuel Mwamole; Selemani Magawa; Frank Obadia; Gabriel Tabana; Martin Mpanduzi; Mwinjuma Bwanga, Shamte Seif, Hassan Aufi; Nassoro Mwampamba; Kelvin Rutalemwa; Shabiru Hood; David Mnubi; Beatus Simwanza na Timoth Mwakisambwe.

Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa Shaibu Kanyochole.

Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza tarehe 1 Octoba, 2022 na kufunguliwa rasmi tarehe 5 Octoba, 2022 yanafanyika katika viwanja tofauti tofauti ikiwemo Viwanja vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana kwa kuhusisha michezo kadhaa.

Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume ikiwa katika picha ya pamoja kabla ya kumenyana na Timu ya Maji.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume wakilisakama lango la Timu ya Maji wakati wa mchezo huo.
Mwalimu wa Timu ya Mahakama Spear Mbwembwe akiongea na wachezaji wakati wa mapumziko.
Mlinda Mlango wa Timu ya Maji akiokota mpira ndani ya kamba.
Mdaka Mabomu wa Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume, Hassan Aufi akiokoa moja ya mikwaju ya matuta kutoka kwa mchezaji wa Timu ya Maji.
Mdaka Mabomu wa Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume, Hassan Aufi akiwa amebebwa juu juu na mmoja wa mashabiki baada ya kuokoa mkwaju mmoja wa matuta baada ya mchezo huo kumalizika
Sehemu ya mashabiki wa Timu ya Mahakama Sports (juu na chini) wakishangilia ushindi baada ya kuibandua Timu ya Maji kwenye mashindano.


Sehemu nyingine ya mashabiki wa Timu ya Mahakama Sports (juu na chini) wakishangilia ushindi baada ya kuibandua Timu ya Maji kwenye mashindano.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni