Jumapili, 9 Oktoba 2022

TARURA, RAS SIMIYU WAKIRI MAKOSA MAHAKAMANI

·Wasalimu amri Mahakama Kamba Wanaume, Wanawake wakielekea robo fainali

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Wanawake imetinga katika hatua ya robo fainali baada ya kutembeza kichapo kikali kwa wapinzani wao, TARURA na RAS Simiyu katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.

Ulikuwa mchezo wa Kamba Wanawake ulioanza kuchezwa majira ya saa nne asubuhi katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagala ambapo vijana wa Mahakama hawakutaka kuleta utani na mtu na kuwakamata kisawasawa wapinzani wao ambao hawakupata nafasi yoyote ya kupumua.

RAS Simiyu walijaribu kujitutumua kwa sekunde kadhaa lakini wakaamua kukiri makosa mahakamani na kujikuta maji waliyokuwa wanataka kuyaoga yameshafika shingoni na kukubali yaishe kwenye mzunguko wa kwanza.

Kipindi cha pili hakikuwa na ugumu wowote kwa Mahakama kwa jinsi walivyokuwa wamejipanga kuumaliza mchezo huo bila kupoteza muda. Hadi mchezo unamalizika RAS Simiyu wakaondoka uwanjani wakiwa vichwa chini, huku wakiiacha Mahakama Sports ikisherekea ushindi walioupata.

Baada ya mechi hiyo, Kamba Wanaume ilifuata ambapo Mahakama Sports waliparurana na TARURA ambao hawakutoa upinzani wowote kwa wababe wa mchezo huo. Wapinzani hao wa Mahakama walijuta kujitokeza katika mchezo huo baada ya kupoteana katika mzunguko wa kwanza.

Kama ilivyokuwa kwa dada zao, Mahakama Sports Kamba wanaume walitembeza kichapo kitakatifu katika mzunguko wa pili baada ya wapinzani wao nao kukiri makosa ya kushindana na Mahakama, hivyo kuahidi Mungu akipenda watajaribu tena baadaye.

Kufuatia matokeo hayo, Mahakama Sports Kamba Wanaume itakutana na Uchukuzi kwenye robo fainali. Uchukuzi waliwango’oa kwenye mashidano hayo timu ya Maji huku Mahakama Sports Wanawake ikikabiliana vilivyo na RAS Iringa ambao waliwatoa upepo Haki.

Akizungumza baada ya mechi hizo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza vijana wake kwa kutoa salamu kwa wapinzani kuwa hawana utani na mtu. Amesema mapambano bado yanaendelea na watapambana mpaka mwisho kwani kilichowaleta Tanga kinajulikana.

"Sisi hatuna papara na mtu kama walivyo wengine ambao wanakuja uwanjani na mikwara ya hapa na pale, sijui wanamtisha nani. Ninawashangaa sana, unakuta mtu anapita na mikwara kututisha, hivi wanaijua Mahakama hawa, nawaonea hurumia sana hawa," alisema.

Kabla ya kuingia kwenye 16 bora, Mahakama Sports ilikutana na timu zingine nne katika hatua ya makundi. Kwa upande wa Wanaume, mechi ya kwanza Mahakama ilikutana na Haki ambayo ilikamuliwa kisawaswa katika hatua zote. Mechi ya pili Mahakama iliwabana mbavu Ikulu na baadaye wakaikaribisha RAS Singida ambao nao wakakumbana na kichapo kikali kabla ya kuwanyonyoa RAS Dodoma.

Mahakama Sports Kamba Wanawake ilimaliza mechi zake za makundi kwa kushinda zote na kufanya iongoze kwenye kundi hilo. Ilicheza mechi yake ya kwanza ya makundi na RAS Singida ambapo ilitoa kichapo kikali.

Mechi yake ya pili ilikutana na Maji ambayo yalikamuliwa kisawasawa kwa mizunguko yote miwili na katika mechi ya tatu ilipangiwa na RAS Manyara ambao waliingia mitini baada ya kuogopa kupokea dozi iliyokuwa imeandaliwa kwa ajili yao. Mahakama Sports ilikutana na Viwanda na kuisambaratisha vikali katika mechi yake ya nne.

Wachezaji wa Kamba Wanawake ni Zahara Abdallah, Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Melina Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca Mwakabuba, Salma Mwamende, Sarafina Mkumbo, Mariam Mayala, Zawadi Amir, Namweta Mcharo, Valeria Ntyangili, Anna Hebron, Lucy Mbwaga, Rose Mwalongo na Tumaini Kizito.

Katika mchezo wa Kamba Wanaume, Mahakama Sports inawakilishwa na Leonard Kazimzuri, Yuda Mgalla, Patrick Mundwe, Denis Kipeta, Joseph Chokela, Mjuni Denis, Komba Mussa, Mochiwa Marko, Abdul Mumini, Mushi Martin, Magesa Phabian, Emmanuel Datsan, Robert Oguda, Rajab Mwaliko, Fidelis Choka na Exavery Kasembe.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Wanawake ikiwa katika picha ya pamoja kabla ya kupambana na TARURA na RAS Simiyu.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake ikijiandaa kukabiliana na RAS Simiyu (hawapo katika picha).
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume ikijiandaa kuparurana na TARURA (hawapo katika picha).
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake (juu) ikitembeza kichapo kwa RAS Simiyu (chini) ambao walipoteana baada ya mchezo.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume (juu) wakiwagalagaza TARURA (chini).

Magwiji wa mchezo wa Kamba (juu na picha mbili chini) wakipasha misuri kabla ya kuanza kwa mchezo huo kukabiliana na TARURA na RAS Simiyu.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni