Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) imeanza
kukusanya makombe katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara
za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa baada ya mkimbiza upepo wake
hatari, Atugonza Justa kufanya vizuri kwenye mchezo wa riadha mita 3,000 na kuwatimulia vumbi wapinzani wake.
Mwanariadha huyo wa Mahakama alishika nafasi ya kwanza
kwenye mchezo huo uliofanyika majira ya asubuhi leo tarehe 8 Octoba, 2022 katika
Viwanja vya Shule ya Ufundi Tanga na kuwaacha kwa mbali wapinzani wake kutoka
katika taasisi mbalimbali zinazoshiriki katika mashindano hayo.
Kufuatia hatua hiyo, Mchezaji huyo wa Mahakama Sports anakuwa
mshindi katika riadha mita 3,000 na kumfanya asubiri kukabidhiwa medali ya
dhahabu na kikombe cha mshindi wa kwanza kwenye mchezo huo kwenye kilele cha
mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika tarehe 15 Octoba, 2022.
Mbali na mchezo huo, Mahakama Sports pia ilishiriki
katika mbio za mita 400 kwa Wanawake ambapo mchezaji wake Upendo Mapunda
alifanikiwa kushikia nafasi ya tatu kwenye mechi ya makundi, hivyo kutinga
katika hatua ya fainali.
Kadhalika, wafukuza upepo wa Mahakama, Atugonza Justa,
Upendo Mapunda, Zamoyoni Komba na Filomena Haule walishiriki kwenye mchezo wa
kupokezana vijiti na kushika nafasi ya tatu kwenye hatua ya makundi, hatua
iliyowawezesha kufika fainali katika mchezo huo.
Kadhalika, wanamichezo wa Mahakama Sports, Gisbert Chentro,
Frank Obadia, Martin Mpanduzi na John Masunga nao walishiriki katika mchezo huo
wa kupokezana vijiti na kufanikiwa kukamata nafasi ya pili, hivyo kutinga
katika fainali. Fainali zote hizo zinategemewa kufanyika leo tarehe 9 Octoba, 2022.
Mahakama Sports ambayo imeambatana na viongozi
mbalimbali ipo jijini Tanga kushiriki katika mashindano ya SHIMIWI yaliyoanza
tarehe 1 Octoba, 2022 na kufunguliwa rasmi tarehe 5 Octoba, 2022 na Waziri wa
Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Jenista
Mhagama.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa
Shaibu Kanyochole.
Mwamba Atugonza Justa, mshindi wa riadha mita 3,000.
Mwana Mahakama Sports Upendo Mapunda akijiandaa kuchomoka alipokuwa anashiriki mbio za mita 400. Upendo aliibuka mshindi wa tatu kwenye mechi za makundi na kutinga fainali.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni