·Baada ya Mahakama kuwabamiza Ikulu
·Kamba Wanawake yatisha, RAS Manyara wakimbia
Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Usemi usemao usicheze na Mahakama utaumia
umejidhihirisha leo tarehe 4 Octoba, 2022 katika mashindano ya Shirikisho la
Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa
baada ya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume
kuwabamiza bila huruma Ikulu.
Mchezo huo uliovutia washiriki wa mashindano hayo
karibia wote kutoka taasisi mbalimbali za Serikali ulichezwa majira ya saa moja
asubuhi katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagala, huku zomea zomea kutoka
kwa mashabiki wa pande zote mbili ikichagiza mchezo huo.
Ikulu waliingia uwanjani kwa kujiamini na kuikejeli
Mahakama kuwa safari hii haichomoi, huku wakihamasishana kwa kuimba "Ilete
Mahakama, ilete Mahakama,” ili kuumaliza mchezo huo dakika za awali. Kitendo
hicho kiliibua shangilia shangilia za hapa na pale uwanjani hapo.
Hata hivyo, wachezaji wa Mahakama walibaki kimya na
watulivu huku wakiwasoma wapinzani wao jinsi watakavyoanza mpambano huo. Mchezo
ulipooanza Ikulu wakadaka kamba kwa kasi na kuwatikisa Mahakama kwa sekunde
kadhaa. Lakini walijikuta wakigonga mwamba baada ya Mahakama kuwaonyesha 'mtu
kazi' na kuwagalagaza vibaya.
Tukio hilo lilisababisha kibao kugeuka na uwanja mzima
ukalipuka kwa furaha baada ya kukamilika kwa hatua ya kwanza ambapo Ikulu
walionekana kuchanganyikiwa na wakaanza kulaumiana kwa kushindwa kutimiza ndoto
yao ya mchana waliyoota.
Baadaye ikaanza minong'ono ya hapa na pale kutoka kwa
mashabiki huku wakiisifia Mahakama. "Hawa jamaa wameshindikana, lakini
ngoja tusubiri hatua ya pili tuone itakuwaje," alisikika shabiki mmoja
akisema.
Hatua hiyo ya pili ilianza kwa kupokelewa na wimbo
kutoka kwa wanamichezo mbalimbali waliokuwa wakiimba, " walete Ikulu, walete
ikulu, walete Ikulu" na Mahakama haikuwa na cha kufanya zaidi ya kutembeza
kuchapo cha mbwa koko na kuwakamua kisawasawa Ikulu ambao walijikuta wakilamba
nyasi bila wao kutegemea.
Ikulu waliondoka katika Viwanja hivyo wakiwa vichwa
chini, huku wakisindikizwa kwa wimbo maarufu kutoka kwa mashabiki wa Mahakama,
"hawaamini macho yao, hawaamini macho yao, hawaamini macho yao."
Alisikika shabiki mmoja akiuliza, "Mlisema leo Mahakama haichomoi, kwani ilikuwa
imechomeka wapi?"
Baada ya mchezo wa Kamba Wanaume kumalizika, Kamba Wanawake
ilifuata ambapo Mahakama ilipangwa kumenyana na RAS Manyara. Ilipofika wakati
wa mchezo huo Mahakama Sports walitinga katika uwanja kibabe.
Hatua hiyo iliyowatisha wapinzani wao na kuondoka
mmoja mmoja na kutokomea kabisa kusikojulikana, hivyo Mahakama Sports
ikajizolea pointi zote tatu za mchezo huo baada ya RAS Manyara kuitwa mara tatu
na waammuzi na kushindwa kutokea uwanjani.
Akiongea baada ya mchezo huo, Katibu Mkuu wa Mahakama
Sports Robert Tende alisema hajafurahishwa na tabia ya wapinzani wao katika
mashindano hayo ya kuwakimbia kwani walishaahidi kutoa dozi kwa kila mmoja
anayostahili.
"Kama ulivyoona mjomba, Ikulu wamepata dozi yao
saaafi kabisa na haki waliyokuwa wanaitaka wameipata na imetendeka, kila mtu
ameona. Tunataka na wengine waje tuwape haki yao. Hii ndiyo kazi ya Mahakama,
hatujazoea kufanya mambo mengine sisi," alisema.
Katika mchezo wa leo, Kamba wanaume iliwakilishwa na
Leonard Kazimzuri, Yuda Mgalla, Patrick Mundwe, Denis Kipeta, Joseph Chokela,
Mjuni Denis, Mussa Komba, Mochiwa Marko, Abdul Mumini na Mushi Martin, Magesa
Phabian, Emmanuel Datsan, Robert Oguda, Rajab Mwaliko, Fidelis Choka na Exavery
Kasembe.
Kwa upande wa Kamba Wanawake wachezaji walikuwa
Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Merino Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca
Mwakabuba, Salma Mwamende, Safina Mkumbo, Maria Mayala, Zawadi Amir, Namweta
Mcharo, Valeria Ntyangili, Anne Hebron, Lucy Mbwaga na Rose Mwalongo.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile.
Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza jana tarehe 1
Octoba, 2022 yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassimu Majaliwa kesho tarehe 5 Octoba, 2022. Kauli
mbiu ya mashindano ya SHIMIWI 2022 ni “Michezo hupunguza magonjwa yasiyo
ambukiza na kuongeza tija mahala pa kazi.”
Mashindano hayo ambayo yanashirikisha michezo
mbalimbali yatafanyika katika viwanja tofauti tofauti nane ambavyo ni Viwanja
vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule
ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni