Jumanne, 4 Oktoba 2022

MAHAKAMA YAONGEZA WIGO UTOAJI TAARIFA KWA WANANCHI KUHUSU MIRATHI

Na Tiganya Vincent-Mahakama ya Tanzania

Mahakama ya Tanzania imeanzisha namba maalum kwa ajili ya upokeaji wa taarifa na utoaji wa elimu sahihi kwa wananchi ili kupunguza na kuondoa migogoro inayotokana na masuala ya mirathi.

Akizungumza leo tarehe 04 Oktoba, 2022 ofisini kwake jijini Dar es Salaam, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema Mahakama imeamua kuongeza mifumo ya utoaji wa taarifa na elimu kwa wananchi katika eneo la mirathi baada ya kuona watu wengi wanakosa haki zao kwa sababu ya kutokuwa na elimu na taarifa sahihi.

Amesema taarifa na elimu hiyo inatolewa saa 24 mwaka mzima kupitia namba maalum ya 0739 502 401 na barua pepe ambayo ni ccamirathi@judiciary.go.tz ambapo wananchi wapata fursa ya kuuliza maswali na kufuatilia masuala ya mirathi.

Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa, huduma hiyo imeanzishwa kupitia Kituo cha Mrejesho wa Taarifa (Call Center) cha Mahakama ili kuwawezesha wananchi kupata taarifa kwa haraka na uongozi wa Mahakama kupata mrejesho wa jinsi wateja wanavyohudumiwa katika eneo la mirathi.

“Masuala ya mirathi yanawasumbua wananchi wengi wakiwemo wanawake wanapata shida sana na ndio maana kupitia Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Juma tumeamua kuja na mfumo utakaosaidia kutoa taarifa na elimu sahihi ya jinsi ya kushughulikia masuala ya mirathi. Mfumo huu utasaidia kuondoa vishoka na baadhi ya watu wachache ambao sio waaminifu wanaodhulumu haki za wananchi kwa sababu ya kutokuwa na elimu sahihi,” amesisitiza.

Aliongeza wananchi wanayo fursa pia ya kupata elimu kuhusu masuala ya mirathi kupitia barua pepe na namba hiyo wakati wowote.

“Tunawaomba wananchi waweze kuitumia namba hiyo na barua pepe hiyo kutoa taarifa sahihi ili tuweze kuwahuduma kwa wakati na wawe na muda wa kutosha katika kutekeleza shughuli nyingine za maendeleo,” amesema.

Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa, uanzishwaji wa huduma hii ni mwendelezo wa Mahakama katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wa uboreshaji wa huduma za Mahakama ikiwemo utawala bora, uwazi na tija katika mnyororo wa utoaji haki kwa wananchi.

Amesema, huduma hii ina lengo la kuondoa vishoka na watu wengine ambao sio waaminifu ambayo wamekuwa wakiwaumiza wananchi wanaofuatilia masuala ya mirathi ambao hawana taarifa na elimu sahihi kuhusu jinsi ya kufuatilia masuala ya mirathi.

Huu ni mfumo wa pili kuwa ndani ya Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Center) cha Mahakama ya Tanzania ikitanguliwa na ule wa kutoa maoni na malalamiko kupitia namba 0752 500 400.

 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na Waandishi wa Habari leo tarehe 04 Oktoba, 2022 ofisini kwake jijini Dar es Salaam, kuhusu uanzishwaji wa namba maalum ya utoaji wa huduma elimu na taarifa  za ufuatiliaji wa masuala ya mirathi ya 0739 502 401.


Waandishi wa Habari kutoka vyombo vya habari mbalimbali wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) wakati akizungumza leo tarehe 04 Oktoba , 2022 ofisini kwake jijini Dar es Salaam ,kuhusu uanzishwaji wa namba maalum ya utoaji wa huduma elimu na taarifa  za ufuatiliaji wa masuala ya mirathi  ya 0739 502 401.

 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akizungumza leo tarehe 4 Oktoba , 2022 na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam ,kuhusu uanzishwaji wa namba maalum ya utoaji wa huduma elimu na taarifa  za ufuatiliaji wa masuala ya mirathi ya 0739 502 401.

 (Picha na Castilia Mwanossa, SAUT)

 

 


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni