Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira
wa Miguu Wanaume na Netiboli leo tarehe 4 Octoba, 2022 zimetakata katika
mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI)
yanayofanyika jijini hapa baada ya kufanya vizuri kwenye michezo waliyocheza.
Timu ya Mpira wa Miguu iliwapapasa Timu ya Ukaguzi kwa
bao moja kwa nunge, huku Netiboli ikiwatoa jasho Timu ya Ujenzi baada ya kutoshana
nguvu kwa kila timu kutupia vikapu 20.
Ilikuwa mechi ya Netiboli iliyoanza kuchezwa majira ya
saa tisa alasiri katika Viwanja vya Polisi Chumbageni ambapo kila timu
ilionyesha kumkamia mwenzake. Ujenzi walianza mchezo kwa kasi na kutupia tupia kwenye lango la Mahakama.
Hata hivyo, Mahakama ikaja juu baada ya dakika chache
na kuanza kulisakama lango la wapinzani wao huku wakijaza kapu la magori kila
baada ya dakika. Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika, Ujenzi walikuwa wameitangulia
Mahakama kwa kikapu kimoja tu.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo Mahakama
ilifungulia msululu wa vikapu na kuweza kuwafunika wapinzani wao, ambao nao
walikuwa wakijibu kila kichapo walichokuwa wanakipokea. Hadi mchezo
unamalizika, kila timu ilikuwa imeshatupia vikapu 20:20.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Mwalimu wa Timu
Mtumwa Sululu aliwapongeza vijana wake kwa kupambana na kujituma muda wote kama
alivyowaelekeza, hivyo kupata matokeo mazuri katika mchezo huo.
“Hawa wenzetu walidhani Mahakama ni mdebwedo,
tumewaonyesha kazi na wanabahati sana. Walikuwa wanapumulia mashine hawa, niliwaona
viongozi wao muda wote walikuwa wanaomba mechi iishe, tulishawakamata
kisawasawa. Mchezo huu umeisha, tunajipanga kwa mechi nyingine,” alisema.
Baada ya mechi hiyo kumalizika, mzuka ukahamia kwenye
viwanja vya Shule ya Sekondari ya Galanosi ambapo Mahakama Sports Mpira wa
Miguu Wanaume ilikuwa ikipepetana na Ukaguzi.
Mchezo huo ulianza majira ya saa kumi jioni kwa kasi,
huku Mahakama ikilishambulia lango la wapinzani wao kama nyuki. Juhudi hizo
zilizaa matunda katika dakika ya kumi tu ya mchezo ambapo kiungo mkabaji Selemani
Magawa alikukwamisha mpira wavuni na kuuandikia timu yake bao la kuongoza.
Baada ya kupachikwa bao hilo, timu zote zilishambuliana
kwa zamu na kulikuwepo na kosa kosa za magori za hapa na pale. Hadi timu zinaenda
mapumziko, ubao wa matangazo ulikuwa unasoma mabao 1:0 kwa Mahakama na Ukaguzi,
mtawaliwa.
Timu zote mbili zilifanya mabadiliko ya wachezaji
kadhaa katika kipindi cha pili huku zikiwa zinashambuliana kwa zamu. Gori hilo
la Mahakama lilidumu hadi mwisho wa mchezo na kuiwezesha timu hiyo kujizolea
pointi zote tatu muhimu katika mashindano hayo.
Akiongea baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama
Sports Wilson Dede amesema Mahakama Sports haitapoa hata siku moja mpaka
ushindi upatikane. “Tumesema tangu mwanzo kuwa tutakuwa tunatoa dozi ya kutwa
mara tatu. Nadhani umesikia kilichotokea leo asubuhi pale viwanja vya Usagala,
mchana Polisi Chumbageni tumewatoa kamasi watu, hapa napo tumewafumua kwa bao moja,
hiyo siyo dozi! Hizi ni mvua za rasharasha tu, masika yanakuna,” alisema.
Mwalimu wa Timu Spear Mbwembwe amewapongeza vijana
wake kwa ushindi huo na kwa kazi nzuri waliyoifanya. Amewataka wachezaji wake kujipanga
vilivyo kwenye mechi inayofuata. “Jamani, bado hatujamaliza. Najua tunakamiwa
sana, lakini sisi mwendo wetu ni ule ule wa kutoa dozi takatifu kama hizi
tulizotoa leo. Tutaendelea na dozi hizi mpaka mwisho wa mashindano,” alisema.
Wachezaji walioiwakilisha Mahakama katika mchezo wa
Netiboli walikuwa Filomena Haule, Upendo Matunda, Nyange Simola, Veronica
Kajobi, Diane's Akanganyila, Shani Ally, Tarita Kayuni. Wachezaji wa akiba
walikuwa Marikia Nondo, Margaret Kanyaga, Agnes Kilian,Jackline Paul, Adeudata
Mkonkosha.
Kwa upande wa Mpira wa Miguu, wachezaji wa Mahakama
walikuwa Fahamu Kibona; Iman Patson; Gisbert Chentro; Akida Mzee; Emmanuel
Mwamole; Selemani Magawa; Frank Obadia; Gabriel Tabana; Martin Mpanduzi;
Mwinjuma Bwanga, Shamte Seif, Hassan Aufi; Nassoro Mwampamba; Kelvin Rutalemwa;
Shabiru Hood na Beatus Simwanza.
Wakati huo huo, Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa
Mahakama ya Tanzania, Bw. Erasmus Uiso, ambaye pia ndiye mlezi wa Mahakama
Sports leo amekutana na wanamichezo wote wa Mahakama wanaoshiriki katika
mashindano ya SHIMIWI na kuwapongeza kwa kazi nzuri wanayofanya, hususani
ushindi wanaoupata kwenye michezo mbalimbali.
“Taarifa zenu ninazo, Mwenyekiti wenu amenipa taarifa
ya kile kinachoendekea, niwapongeze sana kwa kazi nzuri mnayofanya na mimi nawatakia
kila heri ili mpate ushindi kwenye michezo yote,” alisema.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa
Shaibu Kanyochole.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni